Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MBEGU NI NENO LA MUNGU




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
JANUARI 28, 2026

JUMA LA 3 LA MWAKA WA KANISA

Kumbukumbu ya Mt. Tomas Aquinas

2 Sam 2:4-17
Zab 89:3-4.26-29,
Mk 4:1-20

MBEGU NI NENO LA MUNGU

“lakini waliopanda katika udongo mzuri ni wale waliosikia neno la Mungu na kulikubali na kuliacha lizae matunda”. 

Katika Injili ya Marko ambayo ni fupi kati ya Injili nne, huwa inatazama kazi za Yesu zaidi kuliko mahubiri yake, tunapaswa kuchukulia kwa makini mafundisho ambayo anayachukua Marko katika Injili yake. Tunaweza kuchukulia mifano aliochagua Marko kama iliyo ya muhimu kabisa. 

Injili ya leo ina sehemu tatu muhimu. Sehemu ya kwanza naya mwisho inaelezea Yesu akitoa mfano na kuuelezea. Katikati Yesu anaelezea kwanini yeye anahubiri kwa mifano. Karibia sura nne za injili ya Marko zimebeba mifano, na Injili ya leo ya Marko imebeba mistari 20 ya sura ya nne. Hivyo mfano wa leo ni wa muhimu kweli kweli. 

Mpanzi ni Mungu Baba. Anayesia neno lake kwa kila mtu, hata kule kuko onekana kuwa kama ujinga kwasababu ya kusia mbegu zake hata katika mioyo migumu ya watu, hiki ni kipimo cha upendo wake kwa kila mtu. Anawapatia watu wake neno hata wale walio na mioyo migumu kama mwamba au jiwe, hata wale waliosongwa na ulimwengu, hata wale ambao machoni mwa mwanadamu hawafai. Changamoto hapa ni kwamba tunapaswa kulima na kutifua udongo wa mioyo yetu ili neno la Mungu liote na kuweka mizizi. Na pia tunapaswa kulipalilia linapo anza kukuwa kwa kufweka miiba (malimwengu yanayo tusonga), ili neno liweze kuzaa matunda mema na kuwafikia wote. 

Neno hili likizaa matunda watu watachuma matunda ya neema na kumshukuru Mungu kwa ajili ya zawadi ya mazao ya neno lake. Mmoja akilipokea neno la Mungu akampenda Mungu na jirani, hata jirani watampa Mungu shukrani kwasababu ya neno lililo ingia ndani ya nafsi ya huyo mtu kiasi cha kuzaa matunda yakawafikia wengine. 

Sala: Ee Mungu ninakuomba Neno la Mwanao lizame ndani ya moyo wangu lizae matunda ya upendo, Amani, furaha na utulivu wa kuungana nawe na pia niweze kuwaleta wengine kwako kutokana na matunda yake. Yesu nakutumaini .Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JANUARI 28, 2026



MASOMO YA MISA, JANUARI 28, 2026
JUMATANO, JUMA LA 3 LA MWAKA

KUMBUKUMBU YA MT. TOMAS AQUINUS


SOMO 1
2 Sam. 7:4:17

Neno la Bwana lilimfikia Nathani kusema, Enenda, ukamwambie mtumishi wangu, Daudi, Bwana asema hivi, Je! Wewe utanijengea nyumba, nikae ndani yake? Kwa maana mimi sikukaa ndani ya nyumba, tangu siku ile niliyowatoa wana wa Israeli katika Misri, hata leo, lakini nimekaa katika hema na maskani. Mahali mwote nilimokwenda na wana wa Israeli wote, je! Nimesema neno lolote na mtu yeyote wa waamuzi wa Israeli, niliyemwagiza kuwalisha watu wangu Israeli, niliyemwagiza kuwalisha watu wangu Israeli, nikisema, Mbona hamkunijengea nyumba ya mierezi?

Basi, sasa, mwambie mtumishi wangu, Daudi, maneno haya, Bwana wa majeshi asema hivi, Nalikutwaa katika zizi la kondoo, katika kuwaandama kondoo, ili uwe mkuu juu ya watu wangu, juu ya Israeli; nami nimekuwa pamoja nawe kila ulikokwenda, na kuwakatilia mbali adui zako wote mbele yako; nami nitakufanyia jina kuu, kama jina la wakuu walioko duniani. Tena nitawaagizia mahali watu wangu Israeli, nami nitawapanda, wapate kukaa mahali pao wenyewe, wasiondolewe tena; wala wana wa uovu hawatawatesa tena, kama hapo kwanza; naam, kama vilivyokuwa tangu siku ile nilipowaamuru waamuzi, wawe juu ya watu wangu Israeli; nami nitakustarehesha mbele ya adui zako wote.

Tena Bwana anakuambia ya kwamba Bwana atakujengea nyumba. Nawe siku zako zitakapotimia, ukalala na baba zako, nitainua mzao wako nyuma yako, atakayetoka viunoni mwako, nami nitaufanya imara ufalme wake. Yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa jina langu, nacho kiti cha enzi cha ufalme wake nitakifanya imara milele. Mimi nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwanangu, akitenda maovu nitamwadhibu kwa fimbo ya binadamu na kwa mapigo ya wanadamu; lakini fadhili zangu hazitamwondoa mbele yako. Na nyumba yako, na ufalme wako, vitathibitishwa milele mbele yako. Nacho kiti chako kitafanywa imara milele.

Kwa maneno hayo yote, na kwa maono hayo yote, na kwa maono hayo yote, ndivyo Nathani alivyonena na Daudi.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 89:3-4, 26-29 (K) 28

(K) Hata milele nitamwekea fadhili zangu.

Nimefanya agano na mteule wangu, 
Nimemwapia Daudi mtumishi wangu.
Wazao wako nitawafanya imara milele,
Nitakijenga kiti chako cha enzi hata milele. (K)

Yeye ataniita: Wewe Baba yangu,
Mungu wangu na mwamba wa wokovu wangu.
Nami nitamjalia kuwa mzaliwa wangu wa kwanza,
Kuwa juu sana kuliko wafalme wa dunia. (K)

Hata milele nitamwekea fadhili zangu,
Na agano langu litafanyika amini kwake.
Wazao wake nao nitawadumisha milele.
Na kiti chake cha enzi kama siku za mbingu. (K)


SHANGILIO

Aleluya, aleluya,
Mbegu ni neno la Mungu, anayepanda ni Kristo; atakayemkuta, ataishi milele.
Aleluya.


INJILI
Mk. 4:1-20

Yesu alianza kufundisha tena kando ya bahari. Wakamkusanyikia mkutano mkubwa mno, hata yeye akapanda chomboni, akakaa baharini; mkutano wote ulikuwako juu ya nchi kavu kando ya bahari. Akawafundisha mambo mengi kwa mifano, akawaambia katika mafundisho yake, Sikilizeni; Tazama, mpanzi alitoka kwenda kupanda; ikawa alipokuwa akipanda, mbegu nyingine ilianguka kando ya njia, wakaja ndege wakaila. Nyingine ikaanguka penye mwamba, pasipokuwa na udongo mwingi; mara ikaota kwa kuwa na udongo haba; hata jua lilipozuka iliungua, na kwa kuwa haina mizizi ikanyauka. Nyingine ikaanguka penye miiba; ile miiba ikamea, ikaisonga, isizae matunda. Nyingine zikaanguka penye udongo ulio mzuri, zikazaa matunda, zikimea na kukua, na kuzaa, moja thelathini, moja sitini, na moja mia. Akasema, Aliye na masikio ya kusikia, na asikie.

Naye alipokuwa peke yake, wale watu waliomzunguka, na wale Thenashara, walimwuliza habari za ile mifano. Akawaambia, Ninyi mmejaliwa kuijua siri ya ufalme wa Mungu, bali kwa wale walio nje yote hufanywa kwa mifano, Ili wakitazama watazame, wasione, na wakisikia wasikie, wasielewe; wasije wakaongoka, na kusamehewa.
Akawaambia, Hamjui mfano huu? Basi mifano yote mtaitambuaje? Mpanzi huyo hulipanda neno. Hawa ndio walio kando ya njia, lipandwapo neno; nao, wakiisha kusikia, mara huja Shetani, akaliondoa lile neno lililopandwa mioyoni mwao. Kadhalika na hawa ndio wapandwao penye miamba, ambao kwamba wakiisha kulisikia lile neno, mara hulipokea kwa furaha; ila hawana mizizi ndani yao, bali hudumu muda mchache; kisha ikitokea dhiki au udhia kwa ajili ya lile neno, mara hujikwaa. Na hawa ndio wale wapandwao penye miiba, ni watu walisikiao lile neno, na shughuli za dunia, na udanganyifu wa mali, na tamaa za mambo mengine zikiingia, hulisonga lile neno, likawa halizai. Na hawa ndio waliopandwa penye udongo ulio mzuri; ni watu walisikialo lile neno na kulipokea, na kuzaa matunda, mmoja thelathini, mmoja sitini, na mmoja mia.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

FAMILIA YA MUNGU!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Januari 27, 2026
JUMA LA 3 LA MWAKA

2 Sam 6:12-15.17-19
Zab 24:7-10
Mk 3: 31-35


FAMILIA YA MUNGU!


Yesu aliongea mambo mengi yanayo stusha katika utume wake. Katika Injili ya leo kuna aina Fulani ya ukimya unatawala katika umati wa watu wakati Yesu alivyo ongelea kuhusu familia yake. Wengi waliomsikiliza kidogo walidhani Yesu alimkosea heshima Mama yake na ndugu zake. Lakini je ni kweli? Je, unadhani Mama yake alilichukulia hivi? Kwa hakika sio hivyo.

Hili linaonesha kwamba Mama yake zaidi ya wote, ndiye aliye yashika maneno ya Mungu zaidi kuliko wote, na kwamba Mama yake alimtii Mungu na kufanya mapenzi ya Mungu katika ukamilifu wote. Ndugu zake walikuwa muhimu. Lakini Mama yake alikuwa zaidi, kwasababu alitimiza yote kwa utii mkamilifu katika kutii mapenzi ya Mungu. Kwahiyo, kwa utii mkamilifu kwa Mungu, Maria alikuwa mama mkamilifu wa Mwana wa Mungu. 

Mara nyingine ujumbe wa Yesu hawakuuelewa. Kwanini hivi? Kwasababu Yesu alijua ni kwa jinsi ghani ya kuwasilisha ujumbe wake na upokelewe vizuri. Alijua ujumbe wake unaweza tu kupokelewa na wale wote waliofungua mioyo yao na kwa Imani. Na alitambua wote walio fungua mioyo yao kwa Imani wataelewa au kutafakari juu ya ujumbe wake mpaka utakapo ingia ndani kabisa. Ujumbe wa Yesu hauwezi kuchukuliwa nakufanyiwa midahalo kama vile ni somo la falsafa. Maria alisikiliza maneno hayo ya Yesu kwa Imani kamili alielewa na alijazwa na furaha. Ilikuwa ni kwasababu ya “NDIO” yake kamili kwa Mungu iliyo mwezesha kuelewa yote aliosema Yesu. Na pia hili lilimsaidia Maria kustahili jina takatifu “Mama” zaidi ya kuwa na uhusiano wa damu. Uhusiano wake wa damu hauna mashaka na nimuhimu, lakini la muhimu zaidi ni muunganiko wake wa kiroho ni muhimu zaidi. 

Sisi wote tunaitwa tujiunge kwa undani katika familia hii ya Yesu. Tunaitwa kwenye familia yake kwa njia ya utii wetu wa kutii mapenzi ya Mungu. Tunaitwa tuwe wasikivu, kusikiliza, kuelewa na kutenda yote anayotuambia Yesu. Tuseme “Ndio” kwa Bwana wetu leo, na kuruhusu “Ndio” hiyo iwe ndio msingi wa kujiunga na familia hii ya Mungu. 

Sala: Bwana, nisaidie mimi daima niweze kukusikiliza kwa moyo uliofunguka. Nisaidie niweze kutafakari juu ya maneno yako kwa Imani. Kwa tendo hili la Imani, nisaidie mimi niweze kukuwa katika muunganiko nawe na kuingia katika familia yako ya Kimungu. Yesu nakuamini wewe. Amina 

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JANUARI 27, 2026



MASOMO YA MISA, JANUARI 27, 2026
JUMANNE, JUMA LA 3 LA MWAKA 

SOMO 1
2Sam. 6:12–15, 17-19

Daudi alienda, akalileta sanduku la Mungu, toka nyumb ya Obed-edomu mpaka mji wa Daudi, kwa shangwe. Hata ikawa, watu waliolichukua sanduku la Bwana walipokwisha kwenda hatua sita, akachinja ngómbe na kikono. Daudi akacheza mbele za Bwana kwa nguvu zake zote; na Daudi na nyumba yote ya Israeli wakalileta sanduku la Bwana kwa shangwe, na kwa sauti ya tarumbeta.

Wakaliingiza sanduku la Bwana, na kuliweka mahali pake, katikati ya hema aliyoipiga Daudi kwa ajili yake; naye Daudi akatoa sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani mbele za Bwana. Kisha Daudi alipokwisha kutoa sadaka ya kuteketezwa na sadaka za amani akawabarikia watu kwa jina la Bwana wa majeshi. Akawagawia watu wote, makutano wote wa Israeli, wanaume kwa wanawake, kila mtu mkate wa ngano, na kipande cha nyama, na mkate wa zabibu. Basi watu wote wakaenda zao, kila mtu nyumbani kwake.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 24:7-10 (K) 8

(K) Ni nani mfalme mtukufu? 

Ndiye Bwana, Mfalme wa utukufu.
Inueni vichwa vyenu, enyi malango,
Inukeni, enyi malango ya milele,
Mfalme mtukufu apate kuingia. (K)

Ni nani mfalme wa utukufu?
Bwana mwenye nguvu hodari,
Bwana hodari wa vita. (K)

Inueni vichwa vyenu, enyi malango,
Naam, viinueni, enyi malango ya milele,
Mfalme wa utukufu apate kuingia. (K)

Ni nani huyu Mfalme wa utukufu?
Bwana wa majeshi, 
Yeye ndiye mfalme wa utukufu. (K)


SHANGILIO
Mt. 11:25

Aleluya, aleluya,
Utukuzwe Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga.
Aleluya.


INJILI
Mk. 3:31-35

Wakaja mamaye na nduguze wa Yesu; wakasimama nje, wakatuma mtu kumwita. Na makutano walikuwa wameketi, wakimzunguka; wakamwambia, Tazama, mama yako na ndugu zako wako nje, wanakutafuta. Akawajibu, akisema, Mama yangu na ndugu zangu ni akina nani? Akawatazama wale walioketi wakimzunguka pande zote, akasema, Tazama, mama yangu na ndugu zangu! Kwa maana mtu yeyote atakayeyafanya mapenzi ya Mungu, huyo ndiye ndugu yangu, na umbu langu, na mama yangu.


Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

WAJUMBE WA AMANI


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatatu, Januari 26, 2026, 
Juma la 3 la Mwaka wa Kanisa

Kumbukumbu ya Watakatifu Timotheo na Tito(Maaskofu)

2 Tim 1: 1-8 au Tit 1: 1-5;
Zab 96: 1-3, 7-8, 10; 
Lk 10: 1-9.


WAJUMBE WA AMANI

Leo tunaangalia juu ya wazee wetu wa Imani na jinsi walivyo weka Injili katika matendo yao baada ya ufufuko wa Yesu. Hawa wanaume na wanawake ni wa kizazi cha pili: wafuasi wa wafuasi na walikuwa wakitumwa mara kwa mara wakiwa wawili wawili kuhubiri kwa uwepo wao. Kwa njia ya kutembelea na kusafiri inaonyesha kwamba ufalme wa haki na Amani ulikuwa tayari Ulimwenguni. 

Ujumbe kutoka katika barua kwa Timotheo, Paulo anaelezea mapendo yake makubwa kwa Timotheo, na wenzake katika utume, na hamu yake kubwa ya kumuona. Anamshukuru Mungu kwa Imani ya Timotheo alioonesha kwa mama yake Myahudi na bibi yake Loisi. Wakati huo huo anamkumbusha Timotheo kuhusu zawadi aliopokea wakati Paulo alivyo mwekea mikono juu yake. Zawadi anayosema Paulo, ilikuwa sio ya woga bali yenye nguvu, upendo na ujasiri na kuleta ujasiri wote wakuhubiri Injili hata wakati, wa kipindi cha Paulo, kuonewa na kuteswa. Katika somo la kuchagua la pili, kutoka katika barua ya Paulo kwa Tito, Paulo anawakumbusha wamisionari wenzake juu ya kazi ya mtume. Ni “kuwaleta wote ambao Mungu amewachagua kwenye Imani na akili ya kweli inayo ongoza kwenye dini ya kweli”. 

Katika somo la Injili linaongelea kuhusu maelekezo anayotoa Yesu kwa wale Wafuasi 72 anavyowatuma kwenda kwa utume kufanya kazi ile ile aliokuwa akifanya yeye mwenyewe. Maneno yake ya ufunguzi ni kweli kama ilivyokuwa katika kipindi cha Timotheo na Tito: “mavuno ni mengi lakini watenda kazi ni wachache; hivyo muombeni Bwana wa mavuno apelike wafanya kazi katika shamba lake.” Ujumbe wao ulipaswa kuwa wenye kuponya. Sio tuu uponyaji wa mwili tu, bali uponyaji wa kila aina unaofanya mahusiano na maisha ya watu yalete Amani. Kwa kufanya hivi walileta uwepo wa ufalme wa Mungu kwa watu walio watembelea. Ni upendo na uwezo wakuishi kwa pamoja kwa kujaliana na kusaidiana vinaonesha uwepo wa Ufalme wa Mungu katika maisha yetu. Haya ndio Timotheo na Tito walijitolea kufanya. Sisi-hata tungekuwa na cheo ghani katika jamii ya Kikristo-tunaitwa kufanya hayo hayo. 

Sala: Bwana, ninaomba niwe mjumbe wako wa Amani na uponyaji. Ninaomba nijifunze kutegemea nguvu zako na kuishi maisha nikijikabidhi katika utume wako. Yesu nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JANUARI 26, 2026



MASOMO YA MISA, JANUARI 26, 2026
JUMATATU, JUMA LA 3 LA MWAKA

KUMBUKUMBU YA WATAKATIFU TIMOTHEO NA TITO, MAASKOFU


SOMO 1
2 Tim. 1:1-8

Paulo, mtume wa Kristo Yesu, kwa mapenzi ya Mungu; kwa ajili ya ahadi ya uzima ulio katika Kristo Yesu; kwa Timotheo, mwanangu mpendwa. Neema na iwe kwako, na rehema, na amani, zitokazo kwa Mungu Baba na kwa Kristo Yesu Bwana wetu.

Namshukuru Mungu, nimwabuduye kwa dhamiri safi tangu zamani za wazee wangu, kama vile nikukumbukavyo wewe daima, katika kuomba kwangu usiku na mchana. Nami natamani sana kukuona, nikiyakumbuka machozi yako, ili nijae furaha; nikiikumbuka Imani uliyo nayo isiyo na unafiki, ambayo ilikaa kwanza katika bibi yako Loisi, na katika mama yako Eunike, nami nasadiki wewe nawe unayo.

Kwa sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani yao kwa kuwekewa mikono yangu. Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu nay a upendo nay a moyo wa kiasi. Basi usiuonee haya ushuhuda wa Bwana wetu, wala usinionee haya mimi mfungwa wake, bali uvumilie mabaya pamoja nami kwa ajili ya Injili, kwa kadiri ya nguvu ya Mungu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 16:1-2, 5, 7-8, 11 (K) 5

(K) Bwana ndiye fungu la posho langu.

Mungu, unihifadhi mimi,
Kwa maana nakukimbilia Wewe.
Nimemwambia Bwana, 
Ndiwe Bwana wangu,
Sina wema ila utokao kwako. (K)

Nitamhimidi Bwana aliyenipa shauri,
Naam, mtima wangu umenifundisha usiku.
Nimemweka Bwana mbele yangu daima,
Kwa kuwa yako kuumeni kwangu, sitaondoshwa. (K)

Utanijulisha njia ya uzima,
Mbele za uso wako iko furaha tele,
Na katika mkono wako wa kuume
Mna mema ya milele (K)


SHANGILIO
Mt. 28:19-20

Aleluya, aleluya,
Enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, Bwana anasema. Mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari.
Aleluya.


INJILI
Lk. 10:1-9

Bwana aliweka wengine, sabini, akawatuma wawili wawili wamtangulie kwenda kila mji na kila mahali alipokusudia kwenda mwenyewe. Akawaambia, Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache; basi mwombeni Bwana wa mavuno apeleke watenda kazi katika mavuno yake. Enendeni; angalieni, nawatuma kama wana-kondoo kati ya mbwa-mwitu. Msichukue mfuko, wala mkoba, wala viatu; wala msimwamkie mtu njiani. Na nyumba yoyote mtakayoingia, semeni kwanza, Amani iwemo nyumbani humu; na akiwamo mwana wa amani, amani yenu itamkalia; la, hayumo, amani yenu itarudi kwenu. Basi, kaeni katika nyumba iyo hiyo, mkila na kunywa vya kwao; maana, mtenda kazi amestahili kupewa ujira wake. Msihame-hame kutoka nyumba hii kwenda nyumba hii. Na mji wowote mtakaouingia, wakiwakaribisha, vileni vyakula viwekwavyo mbele yenu; wapozeni wagonjwa waliomo, waambieni, Ufalme wa Mungu umewakaribia.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MWANGA KWA WALE WALIO GIZANI!



“MBEGU ZA UZIMA”
Tafakari ya kila Jumapili
Jumapili, Januari 25, 2026
Juma la 3 la Mwaka A wa Kanisa

Is 8:23 – 9:3;
Zab 27: 1, 4, 13-14;
1Kor 1: 10-13, 17;
Mt 4: 12-23.



MWANGA KWA WALE WALIO GIZANI!


Watu wenye nguvu sio wale wanao jionesha na kujigamba kuwa na nguvu mbele za watu, bali wale wanaoshinda katika vita hatujui chochote kuhusu wao. Leo tunatafakari kuhusu wito wetu wa kumfuata Yesu.

Katika somo la kwanza Isaya anawahakikishia watu wa Israeli kwamba sasa mambo yatakuwa shwari na mazuri. Analeta matumaini katika maisha yao kwamba wote wanaotembea katika giza wataona mwanga mkuu, na wote wanoishi katika huzuni watapata furaha kuu. Utabiri huu wa Isaya ni dhahiri umetimizwa kwa ujio wa Kristo. Yesu ni “Mwanga mkuu” ambao Isaya anaongelea. Kwahiyo Isaya anatabiri kuhusu habari hii ya kihistoria wakati Yesu akitokea ulimwenguni kwetu akihubiri Neno lake la Kimungu. Lakini hili neno la Isaya, kwetu lisiongelee tuu habari ya kihistoria ya utabiri wa ujio wa Kristo na utume wake, linapaswa lidhihirishe ukweli kwetu kwamba “Yesu ndiye mwanga mkuu” ambaye anangaa hata katika giza lolote lile ambayo tunakutana nalo katika maisha.

Injili ya leo inatuambia kwamba Yesu ndiye Mwanga mkuu unaongaa, unao ondoa giza na kuleta furaha, unaofungua maisha ya huzuni na kuleta furaha katika maisha. Jaribu kufikiria giza kubwa nene lililo lifunika dunia nzima. Jaribu kufikiria ukiwa katika jangwa usiku mkubwa na mawingu yamefunika kila kitu na hamna hata nyota hata moja. Jaribu kufikiria wakati mawingu yakiondoka wakati jua limeanza kuchomoza. Taratibu giza linaondoka na jua linatoa mwanga na kuangazia nchi yote. Hii sio taswira ya yaliotokea tu kwa kipindi alichokuja Yesu na kufanya utume wake tu, inatokea pia kila siku katika maisha yetu tunapolisikiliza Neno la Mungu kwa uaminifu, na kuliruhusu kupenya akili na mioyo yetu. Maneno ya Yesu yanapaswa kutujaza sisi na uwepo wa yeye mwenyewe, kwani yeye ni Mwanga mkuu wa ukweli.

Yesu alikuwa mtu aliyekuwa katika utume, utume wa kutangaza Ufalme wa Mungu kuwaokoa wanyonge na wadogo, ambao jamii iliwakataa. Utume wake wa wazi ni alama ya kuanza kuwakomboa wale waliopotea na kuleta mwanga na furaha katika maisha yao. Anahitaji watu washirikiane naye na kufanya naye kazi katika utume wake. Aliwachagua mitume wake wa kwanza, aliwaita wakati wakiwa wanajishughulisha na mambo yao, na mara moja walimfuata hata bila ya kufikiria kitu kingine. Wafuasi wake wa kwanza walikuwa watu wa kawaida wavuvi, wakitengeneza neti zao wakijiandaa kuvua samaki. Hawakuwa watu waliosoma au watu maarufu. Wanaonekana kama hawakidhi kufanya utume wa Yesu, lakini cha kushangaza upendo wa Mungu usio na kipimo umewabadilisha. Maisha yao yamepewa thamani na kuwa ya mafanikio na juu yao Kanisa limeanza.

Yesu aliwaangazia akili na mioyo yao na kuwapa nguvu ya kubeba mwanga ambao ni yeye mwenyewe na kuondoa giza lote na kuleta furaha ulimwenguni kwa ujumbe wa upendo wa Mungu. Yesu bado anahitaji wafuasi katika nyakati zetu zilizo vurugika, ambapo kila mtu anavutwa kwenda mwelekeo wake mwenyewe. Mungu anawatumia watu wasiopendwa. Anawapa nguvu na utukufu. Hivyo tuitikie na kujitoa kama mitume, walivyojitoa wenyewe kwa Mungu. Mungu anakuita kama ulivyo uweze kumtangaza na kumshuhudia kwa matendo na maneno yako. Haitaji ubadilike uwe kama mtu Fulani, bali anakuita kama ulivyo ukamshuhudie kila mahali ulipo.

Sala: Bwana, njoo ndani mwangu na ingia katika giza la akili yangu na moyo wangu. Njoo uondoe huzuni na uchungu ninao hisi leo. Naomba ulete mwangaza katika kuchanganikiwa na kuweka akili mpya ya mwanga wa uwepo wa upendo wako. Bwana, tusaidie tuweze kuitika na kufuata wito wako. Katika wito wangu kama Kasisi, Mtawa, mlei; ninaomba nijibu wito wako na kuleta mwanga wako kwa wote walio katika giza. Yesu nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JANUARI 25, 2026



MASOMO YA MISA, JANUARI 25, 2026
DOMINIKA YA 3 YA MWAKA A


WIMBO WA MWANZO:
Zab. 96:1, 6

Mwimbieni Bwana wimbo mpya, mwimbieni Bwana, nchi yote. Heshima na adhama ziko mbele zake, nguvu na uzuri zimo katika patakatifu pake.



SOMO 1
Isa. 9:1 – 4

Hapo kwanza aliingiza nchi ya Zabuloni na nchi ya Naftali katika hali ya kudharauliwa, lakini zamani za mwisho ameifanya kuwa tukufu, karibu na njia ya bahari; ng’ambo ya Yordani, Galilaya ya mataifa.

Watu wale waliokwenda katika giza wameona nuru kuu; wale waliokaa katika nchi ya uvuli wa mauti, nuru imewaangaza. Umeliongeza taifa, umezidisha furaha yao; Wanafurahi mbele zako, kama furaha ya wakati wa mavuno, kama watu wafurahivyo wagawanyapo nyara.

Kwa maana umeivunja nira ya mzigo wake, na gongo la bega lake, na fimbo yake yeye aliyemwonea, kama katika siku ya Midani.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 27:1, 4, 13-14 (K) 1

(K) Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu.

Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu,
Nimwogope nani?
Bwana ni ngome ya uzima wangu,
Nimhofu nani? (K)

Neno moja nimelitaka kwa Bwana,
Nalo ndilo nitakalolitafuta,
Nikae nyumbani mwa Bwana
Siku zote za maisha yangu.
Niutazame uzuri wa Bwana,
Na kutafakari hekaluni mwake. (K)

Naamini ya kuwa nitauona wema wa Bwana
Katika nchi ya walio hai.
Umngoje Bwana, uwe hodari,
Upige moyo konde, naam, umngoje Bwana. (K)



SOMO 2
1Kor. 1:10 – 13, 17

Basi ndugu, nawasihi, kwa jina la Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba nyote mnene mamoja; wala pasiwe kwenu faraka, bali mhitimu katika nia moja na shauri moja. Kwa maana, ndugu zangu, nimearifiwa habari zenu na wale walio wa nyumbani mwa Kloe, ya kwamba iko fitina kwenu. Basi, maana yangu ni hii, ya kwamba kila mtu wa kwenu husema, Mimi ni wa Paulo, na, Mimi ni wa Apolo, na, Mimi ni wa Kefa, na, Mimi ni wa Kristo. Je! Kristo amegawanyika? Je! Paulo alisulibiwa kwa ajili yenu? Au je! Mlibatizawa kwa jina la Paulo?

Maana Kristo hakunituma ili nibatize, bali niihubiri Habari Njema; wala si kwa hekima ya maneno, msalaba wa Kristu usije ukabatilika.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



SHANGILIO
Mt. 4:23

Aleluya, aleluya,
Kristo alihubiri Habari Njema ya ufalme, na kuponya ugonjwa na udhaifu wa kila namna katika watu.
Aleluya.



INJILI
Mt. 4:12 – 23

Basi Yesu aliposikia ya kwamba Yohane amefungwa, alikwenda zake mpka Galilaya; akatoka Nazareti, akaja akakaa Kapernaumu, mji ulioko pwani, mipakani mwa Zabuloni na Naftali: ili litimie neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, Nchi ya Zabuloni na nchi ya Naftali, Njia ya bahari, ng’ambo ya Yordani, Galilaya ya mataifa, Watu wale waliokaa katika giza wameona mwanga mkuu, Nao waliokaa katika nchi na uvuli wa mauti mwanga umewazukia.

Tokea wakati huo Yesu alianza kuhubiri, na kusema, Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.

Naye alipokuwa akitembea kando ya bahari ya Galilaya, aliona ndugu wawili, Simoni aitwaye Petro, na Andrea nduguye, wakitupa jarife baharini; kwa maana walikuwa wavuvi. Akawaambia, Nifuateni, nami nitawafanya kuwa wavuvi wa watu. Mara wakaziacha nyavu zao, wakamfuata. Akaendelea mbele, akaona ndugu wengine wawili, Yakobo wa Zebedayo, na Yohane nduguye, ambao walikuwamo chomboni pamoja na Zebedayo baba yao, wakizitengeneza nyavu zao; akawaita. Mara wakakiacha chombo na baba yao, wakamfuata.

Naye alikuwa akizunguka katika Galilaya yote, akifundisha katika masinagogi yao, na kuihubiri Habari Njema ya Ufalme, na kuponya ugonjwa na udhaifu wa kila namna katika watu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

VIPINGAMIZI KATIKA KUMFUATA YESU!


ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Januari 24, 2026

JUMA LA 2 LA MWAKA WA KANISA


KUMBUKUMBU YA MT. FRANSISKO WA SALES

 

2Sam. 1:1-4, 11-12, 17, 19, 23-27

Zab. 80:1-2, 4-6 (K) 3

Mk 3: 20-21

 

VIPINGAMIZI KATIKA KUMFUATA YESU!

 

Yesu ni Hekima ya Mungu na ni Mungu. Kila kitu alichofanya na kusema kilifunua upendo kamili wa Utatu Mtakatifu. Baadhi ya watu walimsikiliza kwa makini na kwa Imani na utukufu wa mshangao kwa maneno yake na matendo yake. Waliweza kuona Umungu wake ukingaa na kutambua kweli alikuwa Mwana wa Mungu, mkombozi wa Ulimwengu. Lakini walikuwepo wengine, hata wengine waliokuwa ndugu zake, waliodhani “hayupo vizuri kiakili”.

 

Kama haya yalisemwa kwa Yesu pamoja na ukamilifu wake, yatasemwa pia kwetu tunaofuata njia zake. Kumfuata Yesu na kutimiza mapenzi yake sio kila mara itawapendeza ndugu zetu. Yapo mambo mengi tunayoitwa na Injili kufanya na kusema, ambayo yatapingwa tu na ndugu au jirani zetu. Wakati haya yanatokea, tusishangae au kuogopa au kutu umiza. Tusipatwe na hasira wala kukata tamaa. Bali, tunapaswa kujiona wenyewe tukifuata katika njia za Kristo. Tunapaswa kufikiria pia kuhusu kusingiziwa kwake kwa uongo na kuhukumiwa kwa uongo na tusikubali tunayosikia kwa wenzetu yatuweke mbali na kufuata mapenzi ya Mungu.

 

Sala: Bwana, ninatambua kuwa ulishindwa kueleweka na ukahukumiwa vibaya na watu wengine, wengine watu wa wakaribu kabisa. Nisaidie daima niweze kukubali pale ninaposhindwa kueleweka katika maisha hasa pale ninapo kufuata wewe katika maisha. Nisaidie nikutafute wewe na kufanya mapenzi yako licha ya vipingamizi kutoka kwa wengine. Yesu, nakuamini wewe. Amina.

 

-------------------------

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by FurahayaKikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JANUARI 24, 2026



MASOMO YA MISA, JANUARI 24, 2026

JUMAMOSI, JUMA LA 2 LA MWAKA


KUMBUKUMBU YA MT. FRANSISKO WA SALES

 

SOMO 1

2Sam. 1:1-4, 11-12, 17, 19, 23-27

 

Ikawa baada ya kufa kwake Sauli, hapo daudi aliporudi katika kuwaua Waamaleki, naye Daudi amekaa siku mbili katika Siklagi; hata siku ya tatu ikawa, tazama! Akaja mtu kutoka kambi ya Sauli, nguo zake zimeraruliwa, tena ana mavumbi kichwani mwake; basi, ikawa alipomfikia Daudi, akaanguka chini, akamsujudia. Daudi akamwambia, Umetoka wapi? Akamwambia, Nimeokoka katika kambi ya Israeli. Daudi akamwambia, Yalikwendaje? Tafadhali uniambie. Akajibu, Watu wamekimbia vitani, tena watu wengi wameanguka wamekufa; hata Sauli naye na Yonathani, mwanawe, wamekufa.

Ndipo Daudi akashika nguo zake akazirarua; na kadhalika watu wote waliokuwa pamoja naye; wakaomboleza, wakalia, wakafunga hata jioni, kwa ajili ya Sauli, na kwa ajili ya Yonathani mwanawe, na kwa ajili ya watu wa Bwana, na kwa ajili ya nyumba ya Israeli; kwa sababu wameanguka kwa upanga.

Basi Daudi akamwomboleza Sauli, na Yonathani, mwanawe, maombolezo haya,

Walio fahari yako, Ee Israeli juu ya mahali pako palipoinuka wameuawa; jinsi mashujaa walivyoanguka. Sauli na Jonathani walipendwa na kupendeza maishani wala mautini hawakutengwa; walikuwa wepesi kuliko tai.

Walikuwa hodari kuliko simba. Enyi binti za Israeli, mlilieni Huyo Sauli, ambaye aliwavika mavazi mekundu kwa anasa, Akazipamba nguo zenu dhahabu. Jinsi mashujaa walivyoanguka katikati ya vita! Ee Yonathani, wewe umeuawa juu ya mahali pako palipoinuka! Nimesikitika kwa ajili yako, Yonathani, ndugu yangu, ulikuwa ukinipendeza sana; upendo wako kwangu ulikuwa wa ajabu, unaopita upendo wa wanawake. Jinsi mashujaa walivyoanguka wakiwa na silaha za vita zilivyoangamia!

 

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

 


WIMBO WA KATIKATI

Zab. 80:1-2, 4-6 (K) 3

 

(K) Ee Mungu, uangazishe uso wako nasi tutaokoka.

 

Wewe uchungaye Israeli, usikie,

Wewe umwongozaye Yusufu kama kundi.

Wewe uketiye juu ya Makerubi, utoe nuru.

Mbele ya Efraimu, na Benyamini, na Manase,

Uziamshe nguvu zako,

Uje, utuokoe. (K)

 

Ee Bwana, Mungu wa majeshi,

Hata lini? Utayaghadhibikia maombi ya watu wako?

Umewalisha mkate wa machozi,

Umewanywesha machozi kwa kipimo kikuu.

Unatufanya sababu ya ugomvi kwa jirani zetu,

Na adui zetu wanacheka wao kwa wao. (K)

 


SHANGILIO

Mdo. 16:14

 

Aleluya, aleluya.

Ufungue Moyo wetu, ee Bwana, ili tuyatunze maneno ya Mwanao.

Aleluya.

 


INJILI

Mk. 3:20-21

 

Yesu aliingia nyumbani na mkutano wakakusanyika tena, hao wao wenyewe wasiweze hata kula mkate. Jamaa zake walipopata habari wakatoka kwenda kumkamata; maana walisema, Amerukwa na akili.

 

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

 

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.