Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

NJAA KWA AJILI YA MUNGU!




“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Ijumaa, Februari 20, 2026
Ijumaa baada ya Jumatano ya majivu

Isa 58: 1-9;
Zab 51: 3-6, 18-19;
Mk 9: 14-15.

NJAA KWA AJILI YA MUNGU!


“Muda utafika wakati Bwana harusi ataondolewa kwao, ndipo watafunga” (Mt 9:15). Tunaitwa wote kuwa na njaa kwa ajili ya Mungu na ufalme wake. Kufunga kunatusaidia. Yesu analinganisha ujio wa Ufalme wa Mungu ambao aliutangaza na kuuanzisha, na sherehe ya harusi ya Wayahudi. Kufunga wakati wa harusi ingekuwa ajabu kabisa. Kutakuwa na muda wa kufunga baada ya Yesu kuondoka kati ya Wafuasi wake, na kuwaachia wanafunzi wake kazi ya kuukamilisha ufalme wake. Tupo katika kipindi cha kwaresima. Kama Yesu alivyoenda jangwani kufunga na kusali alivyo anza kazi yake ya kutangaza na kuusimika Ufalme wa Mungu, pia tunapaswa kumwomba Mungu neema ya pekee kwa kufunga na kusali tukiwa tunaendelea na kazi ya kuutangaza Ufalme wa Mungu duniani.

Isaya anatueleza mambo muhimu ya kufunga. Kufunga ina hali ya wima na hali ya mlalo (Wima –kwa ajili ya Mungu, mlalo-kwenda kwa wanadamu). Kwanza kabisa, ni kazi ya mtu binafsi, kwa ajili ya mapendo ya Mungu. Tunatoa sadaka si kwasababu ya ukosefu wa chakula, bali tunatoa sadaka kwa vile tunavyo vipenda, ili tuweze kukuwa kwa mapendo kumwelekea Mungu. Pili, hakuna mfungo ulio na matunda mazuri isipokuwa kwa ajili kujali jirani. Tusipo punguza makali ya wale walio wagonjwa, walio na njaa, waliotengwa, tusipokuwa sauti ya wajane, sauti ya Yatima, mfungo wetu hautakuwa na sauti mbele za Mungu. Hivyo, angalao tujifunze kazi moja ya matendo ya huruma, kwa kuwashirikisha yote tunayo jinyima na wale wahitaji. Kwa kufunga chakula tunajifunza ni kwa jinsi ghani njaa inavyouma, na hivyo kuwa na huruma daima kwa wale ambao tunasikia kwamba wana njaa. Hatufungi ili kujilimbikizia kwa baadae bali ili tuwasaidie kile tulichofunga, na isiwe tu baada ya kuwasaidia inakuwa mwisho, bali kwasababu tutakuwa tumejifunza ni kwajinsi ghani njaa inauma, itufanye tuwafikirie daima wale wanao kosa chakula kila wakati. Siku za Ijumaa wakati wa kwaresima ni siku ambazo Kanisa pia linatuhimiza kufanya kitubio. Kitu muhimu katika ijumaa za kipindi cha Kwaresima inapaswa kuwa siku ya majitoleo.

Sala: Bwana, ninachagua siku hii, ili niweze kuwa wamoja pamoja na wewe, katika mateso. Ninaomba majitoleo na matendo yangu ya kujikatalia ninayo kutolea, yawe chanzo cha muunganiko wa ndani pamoja na wewe. Yesu nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, IJUMAA, FEBRUARI 20, 2026




MASOMO YA MISA, IJUMAA, FEBRUARI 20, 2026
IJUMAA BAADA YA MAJIVU


SOMO 1
Isa. 58:1-9

Bwana Mungu asema hivi: Piga kelele, usiache paza sauti yako kama tarumbeta; uwahubiri watu wangu kosa lao, na nyumba ya Yakobo dhambi zao.

Walakini wakinitafuta kila siku; hupenda kujua njia zangu; kama vile taifa waliotenda haki, wasioacha sheria ya Mungu wao, hutaka kwangu amri za haki; hufurahi kumkaribia Mungu. Husema, Mbona tumefunga, lakini huoni? Mbona tumejitaabisha nafsi zetu, lakini huangalii? Fahamuni, siku ya kufunga kwenu mnatafuta anasa zenu wenyewe, na kuwalemea wote watendao kazi kwenu.

Tazama, ninyi mwafunga mpate kushindana na kugombana, na kupiga kwa ngumi ya uvou. Hamfungi siku hii ya leo hata kuiskizisha sauti yenu juu. Je! Kufunga namna hii ni saumu niliyoichagua mimi? Je! Si siku ya mtu kujitaabisha nafsi yake? Ni kuinama kichwa kama unyasi, na kutanda nguo za magunia na majivu chini yake?

Je! Utasema ni siku ya kufunga, na ya kukubaliwa na Bwana. Je! Saumu niliyoichagua, siyo ya namna hii? Kufungua vifungo vya uovu, kuzilegeza kamba za nira, kuwaacha huru walioonewa, na kwamba mvunje kila nira? Je! Siyo kuwagawia wenye njaa chakula chako, na kuwaleta maskini waliotupwa nje nyumbani kwako? Umwonapo mtu aliye uchi, umvike nguo; wala usijifiche na mtu mwenye damu moja nawe?

Ndipo nuru yako itakapopambazuka kama asubuhi, na afya ayko itatokea mara; na haki yako itakutangulia; utukufu wa Bwana utakufuata nyuma ukulinde. Ndipo utaita, na Bwana ataitika; atalia, naye atasema, Mimi hapa.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 51:3-4, 5-6a, 18-19 (K) 17

(K) Moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu, hutadharau.

Maana nimejua mimi makosa yangu,
Na dhambi yangu I mbele yangu daima.
Nimekutenda dhambi Wewe peke yako.
Na kufanya maovu mbele za macho yako. (K)

Tazama, mimi naliumbwa katika hali ya uovu;
Mama yangu alinichukua mimba hatiani.
Tazama, wapendezwa na kweli iliyo moyoni;
Nawe utanijulisha hekima kwa siri. (K)

Uitendee mema Sayuni kwa radhi yako,
Uzijenge kuta za Yerusalemu.
Ndipo utakapopendezwa na dhabihu za haki;
Na sadaka za kuteketezwa, na kafara. (K)


SHANGILIO
Ez. 18:31

Tupilieni mbali nanyi makosa yenu yote mliyoyakosa; Jifanyieni moyo mpya na roho mpya.


INJILI
Mt. 9:14:15

Siku ile: Yesu alipofika ng’ambo, katika nchi ya Wagerasi, wanafunzi wake Yohane wakamwendea, wakasema, Kwa nini sisi na Mafarisayo twafunga, bali wanafunzi wako hawafungi? Yesu akawaambia, Walioalikwa arusini wawezaje kuomboleza, muda bwana arusi akiwapo pamoja nao? Lakini siku zitakuja watakapoondolewa bwana arusi; ndipo watakapofunga.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUIPATA ROHO KWA KUPOTEZA ULIMWENGU!



“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya kwaresima
Alhamisi, Februari 19, 2026
Alhamisi baada ya Jumatano ya majivu

Kum 30: 15-20;
Za 1: 1-4, 6;
Lk 9: 22-25


KUIPATA ROHO KWA KUPOTEZA ULIMWENGU!


Somo la kwanza kutoka katika kumbukumbu la Torati linatufundisha kushika Amri za Mungu kwa kumpenda Mungu, kwa kumtii na kutembea katika njia zake. Kama tutafanya hivyo, tutapokea ahadi zake, ambazo ni uhai na mafanikio. Kwa upande mwingine yule ambaye hamtafuti Mungu anakuwa amechagua kifo na uovu.

Injili inaongelea kuhusu kuchukuwa misalaba yetu na kumfuata Yesu kila siku. Luka anasisitiza “KILA SIKU”, kuonesha umuhimu wakujikita kila siku na kukumbutia misalaba inayopitia katika njia zetu kwa uaminifu na mapendo. Kukumbatia kile ambacho kinaleta uchungu, kisicholipa, kilicho chukiwa na ulimwengu sio rahisi. Hili ndilo alilolifanya Yesu kwa njia ya mateso yake, na kifo juu ya msalaba kwa ajili yetu, akashinda kwa ajili ya wokovu wetu.

Kuchagua maisha ya Imani na ukombozi wa roho zetu inatupasa kuacha mengi ulimwenguni humu. Tunapaswa kuishi katika hali ambayo inatuweka tayari “kuachia yote” hata kama yalikuwa kwa ajili ya faida yetu au kwa ajili ya ukombozi wa wengine. Hili ni ngumu kulifanya na linahitaji mapendo makubwa kwa Mungu. Inatakiwa tuwe tumeridhia wenyewe kutoka ndani, kiasi kwamba kuona utakatifu ni zaidi ya kitu kingine chochote. Usisite kumfanya Mungu kuwa kiini na lengo la maisha yako. Kipindi cha kwaresima ni kipindi muhimu sana cha kuingia ndani na kutazama mitazamo yako na tamaa yako na lengo la maisha yako katika hali ya juu kabisa. Mchague Mungu awe zaidi ya yote na wala hutajutia kufanya kufanya hivyo.

Sala: Bwana, tunapoingia katika kipindi hiki cha kwaresima, nipe neema niweze kutazama juu ya malengo yangu. Nisaidie niweze kuchagua kile kilicho cha muhimu kabisa na kiini cha maisha yangu. Nisaidie nikuchague wewe zaidi ya yote katika maisha yangu ili unisaidie kuendana na mapenzi yako matakatifu. Yesu, nakuamini wewe.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 19, 2026





MASOMO YA MISA, FEBRUARI 19, 2026
ALHAMISI BAADA YA MAJIVU


SOMO 1
Kum. 30:15-20

Musa aliwaambia watu akisema: Aangalia, nimekuwekea leo mbele yako uzima na mema, na mauti na mabaya; kwa hivi nikuagizavyo leo kumpenda Bwana, Mungu wako, kuenenda katika njia zake, na kushika maagizo yake, na amri zake, na hukumu zake, upate kuwa hai na kuongezeka; Bwana, Mungu wako, apate kukubarikia katika nchi uingiayo kuimiliki. Lakini moyo wako ukikengeuka, usipotaka kusikiza, lakini ukavutwa kando kwenda kuabudu miungu mingine, na kuitumikia; nawahubiri hivi leo hakika mtaangamia; hamtazifanya siku zenu kuwa nyingi juu ya nchi, uivukiayo Yoradani, uingie kuimiliki. Nazishuhudiza mbingu na nchi juu yenu hivi leo, kuwa nimekuwekea mbele yako uzima na mauti Baraka na laana; basi chagua uzima, ili uwe hai, wewe na uzao wako; kupenda Bwana, Mungu wako, kuitii sauti yake, na kushikamana naye; kwani hiyo ndiyo uzima wako, na wingi wa siku zako; upate kukaa katika nchi Bwana aliyowaapia baba zako, Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo, kuwa atawapa.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 1:1-4, 6 (K) Zab. 39:5

(K) Heri mtu aliyemfanya Bwana kuwa tumaini lake.

Heri mtu yule asiyekwenda
Katika shauri la wasio haki;
Wala hakusimama katika njia ya wakosaji;
Wala hakuketi barazani pa wenye mizaha.
Bali sheria ya Bwana ndiyo impendezayo,
Na sheria yake huitafakari mchana na usiku. (K)

Naye atakuwa kama mti ulipopandwa
Kandokando ya vijito vya maji,
Uzaao matunda yake kwa majira yake,
Wala jani lake halinyauki;
Na kila alitendalo litafanikiwa. (K)

Sivyo walivyo wasio haki;
Hao ni kama makapi yapeperushayo na upepo.
Kwa kuwa Bwana anaijua njia ya wenye haki,
Bali njia ya wasio haki itapotea. (K)



SHANGILIO
Zab. 130:5

Nimemgnoja Bwana, roho yangu imengoja, na neno lake nimelitumaini. Nafsi yangu inamngoja Bwana, kuliko walinzi waingojavyo asubuhi, naam, walinzi waingojao asubuhi.



INJILI
Lk. 9:22-25

Siku ile: Yesu aliwaambia wafuasi wake kwamba imempasa Mwana wa Adamu kupata mateso mengi na kukataliwa na wazee na wakuu wa makuhani na waandishi, na kuuawa na siku ya tatu kufufuka.

Akawaambia wote, Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake kila siku, anifuate. Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu ndiye atakayeisalimisha. Kwa kuwa yamfaa nini mtu kuupata ulimwengu wote, kama akijiangamiza, na kujipoteza mwenyewe?

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUTOKA MAJIVU MPAKA KWENYE UTUKUFU!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Kwaresima 
Jumatano, Februari 18, 2026, 

Jumatano ya majivu (Siku ya kufunga na kujinyima) 

Yoel 2: 2-18; 
Zab 51: 3-17; 
2 Kor 5:20 – 6:2
Mt 6: 1-6, 16-18


KUTOKA MAJIVU MPAKA KWENYE UTUKUFU!

Leo tumeanza kipindi cha neema cha Kwaresima, na tunaitwa kusali, kutolea sadaka na matendo ya huruma. Tukiwa tunatafakari kipindi hichi, tukiangalia mbele katika kuadhimisha mateso, kifo na ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo. Maisha ya toba na kuongoka ndio maada kuu ya Kwaresima. 

Katika somo la kwanza ujumbe wa wongovu umetengenezwa na maneno haya “mrudieni Mungu kwa mioyo yenu yote” (Yoel 2:12). Kwa Yoeli, kuongoka ni njia ya kurudi nyuma. Wale wote waliojiweka katika njia isio sawa wanaitwa kurudi nyuma. Katika somo la pili Paulo anaongelea kuhusu upatanisho. Anasema “tunaomba Mungu awapatanishe” upatanisho na Mungu unapatikana kwa kuishi ujumbe unaoletwa kwetu na wajumbe wa Mungu-wajumbe waneno lake (Warumi 10:14, 17).

Katika somo la Injili Yesu anaongelea mara saba tuzo ambalo wanalipokea wale wanaotenda kadiri ya mafundisho yake. Injili mara nyingi inaelezea kuhusu ‘tuzo’ walilowekewa wenye haki na ‘adhabu’ kwa walio waovu. Tuzo analo liongelea Yesu, sio kuwa na sehemu nzuri ya juu mbinguni bali , kuongezeka mapendo, hali ya muunganiko wa ndani, na hali ya kufanana na uso wa Baba wa mbinguni. ‘Tuzo’ ni furaha ya upendo wa hali ya juu, kama Mungu anavyofanya, ni hali ya “kuwepo katika ufalme wake”. Kukuwa katika hali hii ya juu, katika mwanzo wa kwaresima Yesu anatualika tufanye mambo matatu: kutolea sadaka, sala na kufunga. Hizi zinajenga nguzo tatu za kiroho za Wayahudi, na yeye anaziweka tena lakini katika hali yake ya kipekee. 

Sadaka: katika kipindi cha Yesu, baadhi ya watu walikuwa wana jukumu la kukusanya na kugawa sadaka kwa maskini, yatima, wajane na wasio jiweza. Wakati wa Sabato, kulikuwa na tabia ya kuwasifia wale waliotoa nyingi na walitangazwa mbele ya mikusanyiko. Kwa Yesu, kutoa sadaka sio kuweka hela kidogo, bali kuwa na haki, ni kutambua kuwa vitu vyote vya dunia sio vyetu ni vya Mungu. Kil aliyechukuwa zaidi anapaswa kurudisha kwa wale wasio nacho. Mt. Ambrose, aliwaambia matajiri “kumbuka kwamba, hamuwapi maskini kilicho chenu; bali mnawapa tu kile kilicho mali yao” 

Sala: wakati wa kipindi cha Yesu kulikuwa na aina mbili za sala: sala ya pamoja na sala binafsi. Sala za pamoja, zilifanywa hekaluni, katika masinagogi na katika mitaa, mara mbili kwa siku. Yesu hakatazi matendo haya. Yeye anaelekeza macho yake zaidi kwenye sala ya binafsi, ambayo inafanywa na mtu mwenyewe, milango imefungwa katika hali ya muunganiko wa ndani na Baba “anaye ona vyote”. Sala hii sio marudio ya fomula mbali mbali, bali ni mazungumzo na Mungu, nikumwomba asikilize mapenzi yetu na kutimiza ndoto zetu, lakini pia kuishi mapenzi yake na kupokea kutoka kwake majukumu aliotupangia ya kujenga ufalme wake. Sala, kwanza kabla ya yote ni kusikiliza, kufungua mioyo yetu na kukaribisha mipango ya Mungu na bila kukiuka matazamio yake. 

Kufunga: katika kipindi cha Yesu, waliamini kwamba kufunga kwa kweli ilileta baraka kubwa sana: ilisaidia kuacha dhambi, na kumfanya Bwana aone huruma, kuepuka adhabu yake, na kukinga na mabaya yote. Kufunga kwa Mkristo haihitaji kutambulika. Wanaosha nyuso zao na kuonekana wenye furaha, ana furaha kwasababu kwa kujinyima kwake anamuona maskini akifurahia kutumia ulichompa. Kufunga kuliko kubalika na Mungu ni “kuvunja  aina zote za ukosefu wa haki….funga kwa kushirikisha mkate wako na wale walio na njaa, walete katika nyumba yako wasio na nyumbani, wavalishe wale walio uchi” (Isa 58:6-7). “kuweni wakarimu kati yenu …msiweke maovu juu ya mwingine ndani ya moyo yenu” (Zek 7:5-10).

Katika mwanzo wa kwaresima tunakumbushwa kwamba Kwaresima inaanza na majivu na kuishia na moto, moto wa pasaka wa ufufuko na moto wa Roho Mtakatifu wakati wa Pentekoste, uhakika wa jinsi tutakavyo kuwa. Yesu amezamisha uwepo wetu ambao ni vumbi na majivu katika damu yake, na kutuwezesha kufufuka katika maisha mapya. Roho Mtakatifu anatufanya viumbe vipya. 
Sala: Bwana, ninaomba kwaresima hii iwe yenye matunda katika maisha yangu. Ninaomba kiwe kipindi cha neema cha kukumbatia yote unayotaka niyafanye ndani yangu. Yesu, nakuamini wewe. Amina 


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 18, 2026


MASOMO YA MISA, FEBRUARI 18, 2026
KIPINDI CHA KWARESIMA
JUMATANO YA MAJIVU


SOMO 1
Yoe. 2:12-18

Lakini hata sasa, asema Bwana, nirudieni mimi kwa mioyo yenu yote, na kwa kufunga, na kwa kulia, na kwa kuombolea; rarueni mioyo yenu, wala si mavazi yenu, mkamrudie Bwana, Mungu wenu; kwa maana yeye ndiye mwenye neema, amejaa huruma; si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema, naye hughairi mabaya. N’nani ajuaye kwamba hatarudi na kugeuka, na kutuachia Baraka nyuma yake, naam, sadaka ya unga, na sadaka ya kinywaji, kwa Bwana, Mungu wenu?

Pigeni tarumbeta katika Sayuni, takaseni saumu, kusanyeni kusanyiko kuu; kusanyeni watu, litakaseni kusanyiko, kusanyeni wazee, kusanyeni watoto, na hao wanyonyao maziwa; bwana arusi na toke chumbani mwake, na bibi arusi katika hema yake.

Hao makuhani, wahudumu wa Bwana, na walie kati ya patakatifu na madhabahu, na waseme, Uwaachilie watu wako, Ee Bwana, wala usiutoe urithi wako upate aibu, hata mataifa watawale juu yao; kwani waseme kati ya watu, Yuko wapi Mungu wao?

Hapo ndipo Bwana alipoona wivu kwa ajili ya nchi yake, akawahurumia watu wake.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 51:1-4, 10-12, 15 (K) 1

(K) Uturehemu, Ee Bwana, kwa kuwa tumetenda dhambi.

Ee Mungu, nirehemu, 
Sawasawa na fadhili zako.
Kiasi cha wingi wa rehema zako,
Uyafute makosa yangu.
Unioshe kabisa na uovu wangu,
Unitakase dhambi zangu. (K)

Maana nimejua mimi makosa yangu,
Na dhambi yangu I mbele yangu daima.
Nimekutenda dhambi Wewe peke yako,
Na kufanya maovu mbele za macho yako. (K)

Ee Mungu, uniumbie moyo safi, 
Uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu
Usinitenge na uso wako,
Wala roho yako mtakatifu usiniondolee. (K)

Unirudishie furaha ya wokovu wako;
Unitegemeze kwa roho ya wepesi.
Ee Bwana, uifumbue midomo yangu,
Na kinywa change kitazinena sifa zako. (K)


SOMO 2
2 Kor. 5:20 – 6:2

Ndugu zangu, basi tu wajumbe kwa ajili ya Kristo, kana kwamba Mungu anasihi kwa vinywa vyetu; twawaomba ninyi kwa ajili ya Kristo mpatanishwe na Mungu. Yeye asiyejua dhambi alimfanya kuwa dhambi kwa ajili yetu, ili sisi tupate kuwa haki ya Mungu katika Yeye.

Nasi tukitenda kazi pamoja naye twawasihi msiipokee neema ya Mungu bure. Kwa maana asema, Wakati uliokubalika nalikusikia, Siku ya wokovu nilikusaidia; tazama, wakati uliokubalika ndio sasa; tazama, siku ya wokovu ndiyo sasa.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


SHANGILIO
Zab. 95:8

Msifanye migumu mioyo yenu; msikie sauti ya Bwana.


INJILI
Mt. 6:1-6, 16-18

Angalieni msifanye wema wenu machoni pa watu, kusudi mtazamwe na wao; kwa maana mkifanya kama hayo, hampatai thawabu kwa Baba yenu aliye mbinguni. Basi wewe utoapo sadaka, usipige panda mbele yako, kama wanafiki wafanyavyo katika masinagogi na njiani, ili watukuzwe na watu. Amini, nawaambieni, Wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe utoapo sadaka, hata mkono wako wa kushoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume; sadaka yako iwe kwa siri; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.

Tena msalipo, msiwe kama wanafiki; kwa maana wao wapenda kusali hali wamesimama katika masinagogi na katika pembe za njia, ili waonekane na watu. Amini, nawaambia, Wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani, na ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.

Tena mfungapo, msiwe kama wanafiki wenye uso wa kukunjamana; maana hujiumbua nyuso zao, ili waonekane na watu kuwa nafunga, Amin, nawaambia, Wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe ufungapo, jipake mafuta kichwani, unawe uso; ili usionekane na watu kuwa unafunga, ila na Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

CHACHU ULIMWENGUNI!


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumanne, Februari 17, 2026, 
Juma la 6 la Mwaka wa Kanisa

Yak 1:12-18
Zab 94:12-15.18-19;
Mk 8: 14-21.


CHACHU ULIMWENGUNI!


Kila anaye andaa mkate anatambua jinsi ya chachu kidogo (Amira) inavyo fanya kazi ndani ya donge la unga. Ukiweka kidogo tu ina umusha unga wote. Na yote hii inatokana tu na hii chachu kidogo tu. Kwahiyo ni nini hii chachu ya Mafarisayo na Herode? Ni maneno mabaya, maovu tena yenye makosa wanayo eneza. Kwa Mafarisayo, inaweza kuwa ni kushindwa kumwelewa Yesu alivyokuwa akifanya na kusema. Waliweza hata kubadilisha maneno yake kidogo tu na kuelezea kwa wengine katika maana tofauti. Hii ni mbaya sana na ilikuwa na madhara kwa kila mtu kwa wakati ule na baadae. Kidogo kidogo mbegu hiyo ndogo ya wasi wasi ingekuwa na kuenea kwa wengine. 

Tunawaza kufikiria juu ya yote hayo, tukafahamu pia watu wanaofanya hivyo kwa wakati wetu. Lakini tunaweza kukosea kama hatujaanza kujiangalia sisi wenyewe kwanza. Je, ninafanya haya wakati mwingine? Je, nimejikuta nikipindisha ukweli kwa kutengeneza maneno ambayo huleta maana tofauti na jinsi mtu alivyosema? Je, ninawaongoza wengine kwa maneno ya uongo wakati naufahamu ukweli? Tunapaswa tuangalie maneno yetu na kutambua uzito uliopo katika maneno hayo. Maneno machache yaweza kuleta madhara makubwa kwa kipindi kikubwa. Ni vizuri kuwa na hali ya kupenda ukweli kwani kujaribu kupindisha ukweli huleta madhara makubwa daima. 

Lakini pia sio hilo tu tunalopaswa kufanya. Tunapaswa kutambua pia neno dogo la upendo tunalosema limejaa utajiri mwingi ambao huweza kuleta mema na neema kwa muda wote. Pengine ni tabasamu tu dogo tunalo onesha au kitendo cha ukarimu ambacho tunadhani kinajiondokea tu bila kutambulika. Hili tabasamu dogo na ukarimu mdogo ni chachu ya Injili. Inaleta tofauti na kuleta chachu njema pia. Tutafakari juu ya mambo madogo tunayofanya katika maisha yetu. Tutambue kuwa labda iwe dhambi ndogo inaleta madhara makubwa , au kiwe kitendo kidogo cha upendo kinaleta Baraka kubwa mwishoni. 
Sala: Bwana, nisaidie niweze kuwa mwaminifu na nisaidie niweze kutamua ni chachu ghani ninayo ileta katika maisha ya kila siku. Nisaidie niweze kujitenga na mabaya na unijaze mema. Nisaidie niweze kuwa chachu njema katika yote ninayo sema nakutenda kila siku. Yesu nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 17, 2026



MASOMO YA MISA, FEBRUARI 17, 2026
JUMANNE, JUMA LA 6 LA MWAKA WA KANISA


SOMO 1
Yak. 1:12-18

Heri mtu astahimiliye majaribu; kwa sababu akiisha kukubaliwa ataipokea taji ya uzima, Bwana aliyowaahidia wampendao.

Mtu ajaribiwapo, asiseme, Ninajaribiwa na Mungu; maana Mungu hawezi kujaribiwa na maovu, mmoja hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe huku akivutwa na kudanganywa. Halafu ile tamaa ikiisha kuchukua mimba huzaa dhambi, na ile dhambi ikiisha kukomaa huzaa mauti.

Ndugu zangu wapenzi, msidanganyike. Kila kutoa kuliko kwema, na kila kitolewacho kilicho kamili, hutoka juu, hushuka kwa Baba wa mianga; kwake hakuna kubadilika, wala kivuli cha kugeukageuka. Kwa kupenda kwake mwenyewe alituzaa sisi kwa neno la kweli, tuwe kama limbuko la viumbe vyake.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 94:12-15, 18-19 (K) 12

(K) Ee Bwana, heri mtu yule uliyemfundisha.

Ee Bwana, heri mtu yule 
umwadhibuye na kumfundisha,
Kwa sheria yako;
Mpate kumstarehesha siku ya mabaya. (K)

Kwa kuwa Bwana hatawatupa watu wake,
Wala hutauacha urithi wake,
Maana hukumu itairejea haki,
Na wote walio wanyofu wa moyo wataifuata. (K)

Niliposema, mguu wangu unateleza;
Ee Bwana, fadhili zako zilinitegemeza.
Katika wingi wa mawazo ya moyoni mwangu,
Faraja zako zaifurahisha roho yangu. (K)


SHANGILIO
Yn. 14:23

Aleluya, aleluya,
Mtu akinipenda, atalishika neno langu, 
na baba yangu atampenda, nasi tutakuja kwake.
Aleluya.


INJILI
Mk. 8:14 – 21

Wafuasi wake Yesu walisahau kuchukua mikate, wala chomboni hawana ila mkate mmoja tu. Akawaagiza, akasema, Angalieni, jihadharini na chachu ya Mafarisayo na chachu ya Herode. Wakabishana wao kwa wao, kwa kuwa hawana mikate.

Naye Yesu akatambua, akawaambia, Mbona mnabishana kwa sababu hamna mikate? Hamfahamu bado, wala hamjaelewa? Je! Mioyo yenu ni mizito? Mna macho, hamwoni; mna masikio, hamsikii? Wala hamkumbuki? Nilipoivunja ile mikate mitano na kuwapa wale elfu tano, mlichukua vikapu vingapi vimejaa vipande? Wakamwambia, Kumi na viwili. Na ile saba kuwapa wale elfu nne, mlichukua makanda mangapi yamejaa vipande? Wakamwambia, Saba. Akawaambia, Hamjafahamu bado?

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MIUJIZA KUTOKA MBINGUNI!



ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatatu, Februari 16, 2026
Juma la 6 la Mwaka wa Kanisa
 
Yak 1:1-11;
Zab 119: 67-68.71.75-76;
Mk 8: 11-13

 
MIUJIZA KUTOKA MBINGUNI!

 
Karibuni ndugu zangu kwa adhimisho la Misa Takatifu asubuhi ya leo. Leo neno la Bwana katika asubuhi ya leo tunaanza kwa kuliangalia somo la kwanza toka katika kitabu cha Yakobo. Hiki ni kitabu kilichoandikwa kutoa muongozo kwa jamii ya Wakristo wa mwanzo hasa juu ya fundisho la kuhusu neema na matendo ya sheria kwa kanisa ambalo lilikuwa katika hatua zake za uchanga na lilikuwa likisumbuliwa na madhulumu toka kwa maadui wa nje na pia lilikuwa likijitahidi kuyapatia msingi mafundisho yake makuu.

Katika sehemu tunayoisikia leo, Yakobo anatambua mateso ya hawa Wakristo na majaribu waliyokuwa wanayapata na pia juu ya changamoto kama za umaskini walizokuwa wanazipata. Wakristo hawa walikuwa wakiishi kama jumuiya ndogo kati ya wengi waliokuwa wapagani. Changamoto waliyoipata Wakristo ni kwamba walitengwa kwa sababu ya dini yao. Hawakupata wa kuwapatia ajira, walinyanganywa ardhi yao na walikosa wa kuwatetea. Hivyo, walikumbwa na jaribu la kutaka kuacha dini yao ili nao wapate ajira. Hivyo, Yakobo anawaandikia akisema kwamba hayo ni majaribu tu. Wasikubali yawafanye wakate tamaa. Yasiwafanye waache ukristo ili waajiriwe, wavumilie, ni majaribu tu, ni mapito tu, yote haya yanamwisho wake. Yanakujaga maishani na kupita tu lakini hadi yapite lazima uwe imara ili yasikusombe. Wawe na hekima kutambua kwamba vitu vya dunia na utajiri wake vinakwisha.

Ndugu zangu, fundisho hili la Yakobo ni la uhalisia mkubwa kwa sababu hadi leo changamoto hasa za umaskini ni sababu ya watu kukubali kumtumikia shetani. Tupo tayari kufanya matendo ya ushetani kwa sababu tunaogopa umaskini. Tunaona mali zikiisha, matajiri wakubwa wanakwenda na kuwaachia wengine mali zao ambao hata hawakuwasaidia kufanya kazi au hata mali zao zinaishia kuibwa na wengine tu ambao hata hawakuwasaidia kufanya kazi. Hayo yote tunaona. Lakini umwambie mtu ati awe na hekima asitegemee pesa-weee? Hakuelewi. Nitakusikiliza sasa hivi lakini baada ya dakika tano nikiona changamoto kidogo tu ya fedha basi nitakuwa tayari kufanya hata tendo la uovu.

Yakobo anasisitiza leo tuwe na hekima. Yanayotokea kwa wenzetu, jinsi mali zinavyoshindwa kumfikisha mtu popote yatufanye tuwe na hekima zaidi.

Katika somo la injili tumesikia Yesu akikataa kutoa ishara kwa mafarisayo kwa sababu alijua kwamba walikuwa wanamjaribu na kumchezea chezea tu na hata angeitoa wasingeweza kumwamini. Ni hivyo hivyo na kwetu sisi ndugu zangu. Yesu anatoa ishara kila siku. Yanayotokea kwa mwenzako ni ishara tu. Wapo wengi walioshindwa kuvumilia majaribu yaletwayo na changamoto mbalimbali kama umaskini. Wakaishia kutumia njia za uovu kama wizi, kudhulumu mali za wengine, kudhulumu mirathi ya mayatima, kugushi vyeti na kuiba mali za watu lakini sasa wako wapi? Mali imewafikisha wapi?. Iwe ishara kwetu-ya kuijenga Imani yetu. Tusipoyaona haya kama ishara ya kujenga Imani yetu, basi tusitegemee ya ziada. Haya ndio ya mwisho.
 
Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 16, 2026


 

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 16, 2026
JUMATATU YA JUMA LA 6 LA MWAKA

SOMO 1
Yak. 1:1-11

Yakobo, mtumwa wa Mungu, na Bwana Yesu Kristo, kwa kabila kumi na mbili waliotawanyika; salamu.Ndugu zangu, hesmbali; mkifahamu ya kuwa kujaribiwa kwa imani yenu huleta saburi. Saburi na iwe na kazi kamilifu, mpate kuwa wakamilifu na watimilifu bila kupungukiwa na neno.Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote k
abuni ya kuwa ni furaha tupu, mkiangukia katika majaribu mbaliwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa. Ila na aombe kwa imani, pasipo shaka yoyote; maana mwenye shaka ni kama wimbi la bahari lillilochukuliwa na upepo, na kupeperushwa huku na huku. Maana mtu kama yule asidhani ya kuwa atapokea kitu kwa Bwana. Mtu wa nia mbili husitasita katika njia zake zote. Lakini ndugu asiye na cheo na afurahi kwa kuwa ametukuzwa; bali tajiri kwa kuwa ameshushwa; kwa maana kama ua la majani atatoweka. Maana jua huchomoza kwa hari, huyakausha majani; ua lake huanguka, uzuri wa umbo lake hupotea; vivyo hivyo naye tajiri atanyauka katika njia zake.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 119:67, 68, 71, 72, 75, 76 (K) 77

(K) Rehema zako, ee Bwana, zinijie nipate kuishi.

Kabla sijateswa mimi nalipotea,
Lakini sasa nimelitii neno lako.
Wewe U mwema na mtenda mema,
Unifundishe amri zako. (K)

Ilikuwa vema kwangu kuwa naliteswa,
Nipate kujifunza amri zako.
Sheria ya kinywa chako ni njema kwangu,
Kuliko maelfu ya dhahabu na fedha. (K)

Najua ya kuwa hukumu zako ni za haki,
Ee Bwana, na kwa uaminifu umenitesa.
Nakuomba, fadhili zako ziwe faraja kwangu,
Sawasawa na ahadi yako kwa mtumishi wako. (K)


SHANGILIO
Yn. 14:6

Aleluya, aleluya,
Bwana asema: Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.
Aleluya.
 
 
INJILI
Mk. 8:11 – 13

Walitokea Mafarisayo, wakaanza kuhojiana na Yesu; wakitafuta kwake ishara itokayo mbinguni; wakimjaribu. Akaugua rohoni mwake, akasema, Mbona kizazi hiki chatafuta ishara? Amin, nawaambieni, Hakitapewa ishara kizazi hiki. Akawaacha akapanda tena chomboni, akaenda zake hata ng’ambo.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.
 
Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.