Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

ISHARA YA UTUKUFU YA JUA LA HAKI !



“MBEGU ZA UZIMA”
Tafakari ya Jumapili
Jumatano, Juni 24, 2026. 
Juma la 12 la Mwaka wa Kanisa

Sherehe ya kuzaliwa kwa Mt.Yohane Mbatizaji 

Is 49: 1-6; 
Zab 138: 1-3, 13-15; 
Mdo13: 22-26; 
Lk 1: 57-66, 80


ISHARA YA UTUKUFU YA JUA LA HAKI !

Kwa kawaida Kanisa halisheherekei sikukuu za kuzaliwa za watakatifu. Lakini kuna sikukuu nyingine za pekee ambazo ni kuzaliwa Bwana wetu Yesu Kristo-na sherehe za kuzaliwa Bikira Maria naya kuzawaliwa kwa Yohane Mbatizaji. Hii ni kwasababu Maria, tangu kuumbwa kwake kwanza alikingiwa dhambi ya asili. Yohane Mbatizaji alitakaswa kutoka dhambi ya asili akiwa tumboni mwa mama yake. Leo inajulikana kama “Noeli ndogo” kwasababu Yohane alimtangulia Yesu na alimbatiza Kristo. Maisha ya Yohane Mbatizaji yalijazwa na jambo moja-kumuonesha Yesu kwa watu na kuandaa ujio wa Ufalme wa Mungu. Maandiko matakatifu yanatuambia kwamba Yohane Mbatizaji alijazwa na Roho Mtakatifu hata angali tumboni mwa mama yake (Lk 1: 15, 41) na Kristo mwenyewe ambaye Bikira Maria alipata mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu. Moto wa Roho Mtakatifu ulimjaza Yohane na akawa mtangulizi wa Masiha. Yohane alivunja ukimya wa manabii wa karne zilizopita alipoanza kuongelea kuhusu Neno wa Mungu kwa watu wa Israeli. Akiwa katikati ya watu waliopoteza matumaini yao kuhusu Mungu, sasa anaiamsha tena Imani yao, kuwatahadharisha kuhusu usafi wa mioyo yao, kuamsha tena ndani yao mapenzi mema ya kumtambua na kumkubali Masiha anayekuja. Watu walikimbilia jangwani kwenda kumsikiliza na kubatizwa.

Yohane aliitwa kutoka tumboni mwa mama yake kuwa mjumbe wa ufalme wa Mungu. Kwa njia hiyo hiyo Yesu naye anatualika sisi tuliowafuasi wake na tuliobatizwa kwa jina lake, tuweze kuwa manabii- tuwe watu wanaotangaza kwa maneno na matendo ujumbe wa haki na huruma. Tangu ubatizo wetu (Kuzaliwa katika maisha ya Kimungu) sisi kama Yohane, tuna utume wakufanya kutoka katika mpango wa Baba yetu. Sio tuu kumfuata Yesu, bali kutangaza siku ya ukombozi tunayo tumaini ndani ya kristo kwamba itatimilizwa.

Tutafakari leo, hasa katika zile hali ambazo hatukuwa waaminifu kwa Mungu katika maisha yetu. Mungu atatupokea tena na kubadilisha maisha yetu. Mungu anatusubiri na huruma yake haina kikomo. Turuhusu huruma yake ijaze mioyo yetu ili iweze kupokea daima uzuri wa Mungu. Nasi pia kama Yohane, alivyo itwa kuwa mjumbe wa Ufalme wa Mungu, Yesu anampa kila mbatizwa Roho wake kutangaza kwa maneno na matendo ufalme wa haki na huruma. 

Watu wameishia kujidharau na kukataa maisha yao na sasa wanaishi maisha ya wengine. Ishi kuendana na mpango wa Mungu aliouweka katika maisha yako. Watu wengi wamekataa maisha yao ambayo wanapaswa kuyaishi na wameishia kuishi maisha ya wengine. Wewe ni wa thamani sana kwa jinsi ulivyo na Mungu anakupenda kwa jinsi ulivyo. 

Katika maisha ya Yohane Mbatizaji tunaona unyenyekevu wa hali ya juu. Hakujisifu kwa kitu ambacho hakihusiani na yeye. Hata kwa wale ambao walikuwa wakichanganyikiwa kuhusu Masiha na yeye mwenyewe alisema “mimi sie Masiha” (Yn 1:20). Aliendelea hata nakusema kwamba Masiha ni mkubwa kuliko yeye, hivyo anapaswa yeye abatizwe na Masiha sio yeye ammbatize Masiha. (Mat. 3:14). Tunaitwa daima kutafakari juu ya unyenyekevu daima katika maisha yetu. Kilicho muhimu sana katika hili nikufahamu nafasi zetu na kuzikubali na bila kujaribu kuwa mtu mwingine ambaye sio mimi. 

Ukweli ulikuwa ni kilele cha utume wa Yohane Mbatizaji. Tunatambau kwamba yeye alikuja ili aushuhudie ukweli. Bila shaka ukweli wenyewe ni Yesu (Mat. 14:1-12). Maisha yetu yanapaswa yapambwe na ukweli daima. Ukweli unapaswa kusemwa daima kwasababu unamuinua na kumtukuza Mungu. 

Sala: Bwana, nisaidie niweze kuona dhambi zangu za zamani si katika hali ya kupoteza tumaini bali kama sababu ya kurudi kwako kwa uaminifu mkubwa. Bila kujali nimeanguka mara ngapi, nisaidie niweze kunyanyuka na kuimba tena sifa zako. Yesu nakuamini wewe. Mt. Yohane mbatizaji mhubiri wa ukweli usiye kuwa na woga, utuombee. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JUNI 24, 2026



MASOMO YA MISA, JUNI 24, 2026
JUMATANO YA 12 YA MWAKA


SHEREHE YA KUZALIWA YOHANE MBATIZAJI


SOMO 1
Isa. 49:1 – 6

Nisikilizeni, enyi visiwa; tegeni masikio yenu, enyi kabila za watu mlio mbali sana; Bwana ameniita tangu tumboni; toka tumbo la mama yangu amenitaja jina langu.

Naye anifanya kinywa changu kuwa kama upanga mkali; katika kivuli cha mkono wake amenisitiri; naye amenifanya kuwa mshale uliosuguliwa; katika podo lake amenificha.

Akaniambia; Wewe u mtumishi wangu, Israeli, ambaye katika wewe nitatukuzwa. Lakini nikasema, Nimejitaabisha bure, nimetumia nguvu zangu bure bila faida; lakini hakika hukumu yangu ina Bwana, na thawabu yangu ina Mungu wangu.

Na sasa Bwana asema hivi, yeye aliyeniumba tangu tumboni niwe mtumishi wake, ili nimletee Yakobo tena, na Israeli wakusanyike mbele zake tena; (maana mimi nimepata heshima mbele ay macho ya Bwana, na mungu wangu amekuwa nguvu zangu); naam, asema hivi, Ni neno dogo sana wewe kuwa mtumishi wangu ili kuziinua kabila za Yakobo, na kuwarejeza watu wa Israeli waliohifandhiwa; zaidi ya hayo nitakutoa uwe nuru ya mataifa, upate kuwa wokovu wangu hata miisho ya dunia.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 139:1 – 3, 13 – 15 (K) 14

(K) Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa.

Ee Bwana umenichunguza na kunijua.
Wewe wajua kuketi kwangu na kuondoka kwangu;
Umelifahamu wazo alngu toke mbali.
Umepepeta kwenda kwangu na kulala kwangu,
Umeelewa na njia zangu zote. (K)

Maana Wewe ndiwe uliyeniumba mtima wangu,
Uliniunga tumboni mwa mama yangu.
Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa
Kwa jinsi ya ajabu ya kutisha.
Matendo yako ni ya ajabu. (K)

Na nafsi yangu yajua sansa,
Mifupa yangu haikusitirika kwako,
Nilipoumbwa kwa siri,
Nilipoungwa kwa ustadi pande za chini za nchi. (K)


SOMO 2
Mdo. 13:22 – 26

Paulo alisema, Mungu alimwinua Daudi awe mfalme wao ambaye alimshuhudia, akisema, Nimemwona Daudi, mwana wa Yesu, mtu anayeupendeza moyo wangu, atakayefanya mapenzi yangu yote. Katika uzao wake mtu huyo Mungu amewaletea Israeli habari za ubatizo wa toba, kabla ya kuja kwake. Naye Yohane alipokuwa akimaliza mwendo wake alinena, Mwanaidhani mimi kuwa nani? Mimi siye. Lakini , angalieni, anakuja mmoja nyuma yangu ambaye mimi sistahili kumlegezea viatu vya miguu yake.

Ndugu zangu, wana wa ukoo wa Ibrahimu, na hao miongoni mwenu wanaomcha Mungu, kwetu sisi neno la wokovu huu limepelekwa.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


SHANGILIO
Lk. 1:76

Aleluya, aleluya,
Nawe, mtoto, utaitwa nabii wake aliye juu. Utatangulia mbele za uso wa Bwana, umtengenezee njia zake.
Aleluya.


INJILI
Lk. 1:57 – 66, 80

Ikawa, siku za kuzaa kwake Elisabeti zilipotimia, alizaa mtoto mwanamume. Wakasikia jirani zake na jamaa zake ya kwamba Bwana amemwongezea rehema zake, wakafurahi pamoja naye.
Ikawa siku ya nane wakaja kutahiri mtoto; wakataka kumpa jina la babaye, Zakaria. Mama akajibu akasema, La, sivyo; bali ataitwa Yohane, wakamwambia, Hapana mtu katika jamaa zako aitwaye jina hilo. Wakamwashiria babaye wajue atakavyo kumwita. Akataka kibao, akaandika ya kwamba, Jina lake ni Yohane. Wakastaajabu wote. Papo hapo kinywa chake kikafunguliwa na ulimi wake pia, akaanza kunena akimsifu Mungu. Wakaingiwa na hofu wote waliokuwa wakikaa karibu nao; na mambo hayo yote yakatangazwa katika nchi yote ya milima na milima ya Uyahudi. Na wote walioyasikia wakayaweka mioyoni mwao, wakisema, Mtoto huyu atakauwa wa namna gani? Kwa sababu mkono wa Bwana ulikuwa pamoja naye.

Yule mtoto akakua, akaongezeka nguvu rohoni, akakaa jangwani hata siku ya kutokea kwake kwa Israeli.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUNI 23, 2026


  


MASOMO YA MISA, JUNI 23, 2026
JUMANNE, JUMA LA 12 LA MWAKA


SOMO 1

2 Fal. 19 : 9-11, 14-21, 31-36

 

Senakeribu alituma wajumbe kwa Hezekia mara ya pili, kusema, Mwambieni Hezekia, mfalme wa Yuda, maneno haya, mkisema, Asikudanganye Mungu wako unayemtumaini, akisema, Yerusalemu hautatiwa katika mikono ya mfalme wa Ashuru. Tazama, umesikia ni mambo gani wafalme wa Ashuru waliyozitenda nchi zote, kwa kuziangamiza kabisa; je! utaokoka wewe?

 

Basi Hezekia akaupokea waraka katika mikono ya wale wajumbe, akausoma; kisha Hezekia akapanda, akaingia katika nyumba ya Bwana, akaukunjua mbele za Bwana. Naye Hezekia akaomba mbele za Bwana, akasema, Ee Bwana, Mungu wa Israeli, ukaaye juu ya makerubi, wewe, naam, wewe peke yako, ndiwe Mungu wa falme zote za dunia; wewe ndiwe uliyeziumba mbingu na nchi. Tega sikio lako, Ee Bwana, usikie; fumbua macho yako, Ee Bwana, uone; uyasikie maneno ya Senakeribu, ambayo amemtuma mtu aje nayo ili kumtukana Mungu aliye hai.

 

Ni kweli, Bwana, wafalme wa Ashuru wamewaharibu mataifa na nchi zao, na kuitupa miungu yao motoni; kwa maana haikuwa miungu, bali ni kazi ya mikono ya wanadamu; ilikuwa miti na mawe tu, ndiyo sababu wakaiharibu. Basi sasa, Ee Bwana, Mungu wetu, utuokoe na mkono wake, nakusihi, ili kwamba falme zote za dunia zipate kujua ya kuwa wewe ndiwe Bwana Mungu, wewe peke yako.

 

Ndiyo Isaya. mwana wa Amozi, akapeleka ujumbe kwa Hezekia, akisema, “Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Kwa kuwa umeniomba juu ya Senake- ribu, mfalme wa Ashuru, mimi nimekusikia. Tamko alilolitamka Bwana katika habari zake ndilo hili, Bikira, binti Sayuni, amekudharau, na kukudhihaki sana; binti Yerusalemu ametikisa kichwa chake juu yako. Maana mabaki yatatoka katika Yerusalemu, na, wao watakaookoka katika mlima wa Sayuni; wivu wa Bwana utatimiza jambo hilo.

 

Basi Bwana asema hivi katika habari za mfalme wa Ashuru, Yeye hatauingia mji huu, wala hatapiga mshale hapa, wala hatakuja mbele yake kwa ngao, wala hatajenga boma juu yake.Njia  ile ile aliyojia, kwa njia iyo hiyo atarudi zake, wala hataingia ndani ya ya mji huu, asema Bwana. Maana nitaulinda mji huu, niuokoe, kwa ajili yangu mwenyewe, na kwa ajili ya Daudi, mtumishi wangu.

 

Ikawa usiku uo huo malaika wa Bwana alitoka. akakiingia kituo cha Waashuri, akawapiga watu mia na themanini na tano elfu. Na watu walipoondoka asubuhi na mapema, kumbe! hao walikuwa maiti wote pia. Basi Senakeribu mfalme wa Ashuru akaondoka, akaenda zake, akarudi akakaa Ninawi.


Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.

 

 

WIMBO WA KATIKATI

Zab. 48 :1-3,9-10 (K) 8

 

(K) Mungu ataufanya imara hata milele.

 

Bwana ndiye aliye mkuu,

Na mwenye kusifiwa sana

Katika mji wa Mungu wetu,

Katika mlima wake mtakatifu. (K)

 

Mlima Sayuni pande za kaskazini,

Mji wa Mfalme mkuu.

Mungu katika majumba yake

Amejijulisha kuwa ngome. (K)

 

Tumezitafakari fadhili zako, Ee Mungu,

Katikati ya hekalu lako,

Ndivyo na sifa yako hata miisho ya dunia.

Mkono wako wa kuume umejaa haki. (K)


 

 

SHANGILIO

Zab. 130:5

 

Aleluya, aleluya, Roho yangu inamngoja Bwana, na neno lake nimelituaminia. Aleluya.


 

 

INJILI 

Mt. 7:6,12-15


Yesu aliwaambia wanafunzi wake; Msiwape mbwa kilicho kitakatifu, wala msitupe lulu zenu mbele ya nguruwe, wasije wakazikanyaga chini ya miguu yao, wakageuka na kuwararua. Basi yoyote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeeni vivyo hivya hiyo” maana hiyo ndiyo torati na manabii. Ingieni kwa kupitia mlango uliyo mwembamba, maana, mlango ni mpana, na njia ni pana iendayo upotevuni, nao ni wengi waingiao kwa mlango huo. Bali mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani, nao waionao ni wachache. 

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by FurahayaKikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

NJIA NYEMBAMBA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumanne, Juni 23, 2026 
Juma la 12 la Mwaka

2 Fal. 19 : 9-11, 14-21, 31-36
Zab. 48 :1-3,9-10 (K) 8
Mt 7: 6, 12-14


NJIA NYEMBAMBA!


Katika Injili ya leo Bwana wetu anatuambia, “tuingie kupitia mlango mwembamba, maana mlango mpana, na njia ni pana iendayo upotevuni, nao ni wengi waingiao kwa mlango huo” (Mt 7:13). Tukiangalia maisha yetu kwa ujumla, si kitu zaidi ya msururu wa matokeo ya chaguzi zetu. Kuna wakati tumehuzunikana sana kwa kufanya uchaguzi mbaya na pia kuna wakati tumefurahi sana kwa kufanya uchaguzi au uamuzi sahihi.

Leo Yesu anaongelea kuhusu uchaguzi kati ya njia rahisi na njia iliyongumu. Tuna shawishika kuchagua njia pana na iliyo rahisi na kukwepa njia nyembamba. Lakini katika maisha ya kiuzoefu ya mwanadamu yanatuambia kwamba hakuna njia iliorahisi inayopelekea mafanikio mazuri ya maisha ya mwanadamu. Ukuu/mafanikio mara nyingi ni matokeo ya kazi ngumu. Njia inayoelekea kwenye Ufalme wa Mungu ni nyembamba. Ina mambo yake, inatuhitaji tujitoe, kujikatalia na sadaka.

Kutenda dhambi ni rahisi na inaonekana kuwa kawaida kwa mwanadamu, lakini kubaki bila dhambi ni ngumu kwasababu inatutaka kupingana na matamanio yetu. Inatutaka tujikatalie. Na Injili ya Leo inatuambia kwamba ni wachache sana wanaochagua njia nyembamba, walio wengi wanachagua njia iliopana na iliyo rahisi. Ni wachache sana wanao ipokea Injili na kuishi kadiri ya ujumbe wake. Tuombe neema ya Mungu itusaidie tuweze kuchagua njia nyembamba yakutuchukua kwenye ufalme wa Mungu, inatugarimu sisi wakati mwingine kwenda kinyume na matakwa ya wengi, unaweza kuchukiwa nakutopendwa lakini kwakuujua ukweli wa Yesu katika Injili, ishi kadiri yake.

Sala: Bwana, nioneshe njia nyembamba inayo niongoza kwako. Nisaidie niwatendee wengine yale ambayo natamani wanitendee. Nisaidie nitumie upendo ulio ndani yangu kuhusu mimi mwenyewe niweze kuutumia kuwapenda wengine. Katika kujitoa kwangu, nisaidie niweze kupata ukamilifu katika majitoleo hayo. Yesu, nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

USIHUKUMU!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatatu, Juni, 22, 2026
Tafakari ya kila siku, 
Juma la 12 la mwaka wa Kanisa


2 Fal 17: 5-8, 13-15, 18; 
Zab 59: 3-5, 12-13; 
Mt 7: 1-5


USIHUKUMU!

Katika Injili ya leo Yesu anatuambia tusiwahukumu wengine. Kwanini tusiwahukumu wengine? Kwanza kabisa, washiriki wa ufalme wa Mungu wanapaswa kuachia hukumu kwa hakimu wa mwisho (Mungu). Kama Bwana wao wanapaswa wajiingize katika kuponya nakuyafanya yote upya. Kurekebishana kindugu sio kuhukumu, lakini pia namna ya kurekebisha inapaswa kuwa na roho nzuri. Msukumo daima uwe kumpenda jirani yangu kama nafsi yangu. 

Pili, hatuwezi kujua nafsi ya mtu asilimia mia moja. Ni vigumu na huenda haiwezekani kwa mwanadamu kuwa mwema kabisa katika kuhukumu mtu. Hakuna mwanadamu aliye mkamilifu kabisa anayeweza kumuhumu mwanadamu mwingine. Ni bora kuangalia makosa yetu wenyewe na kuachia mapungufu ya wengine kwa Mungu. Tusitangaze dhambi za wengine kwani sio kazi yetu, tutambue na sisi pia tungeweza kuanguka au kokosea kama wao. Tuwasaidie wenzetu pale wanapo anguka ili warudi tena kwa Baba yetu wote mwenye huruma. Sisi wote ni wakosefu tunahitaji neema ya Mungu. Kuna usemi unaosema “Tunacho ona kwa wengine ni kidogo sana kulinganisha na kile tusicho kiona”. Tuishi kindugu tukichukuliana katika madhaifu yetu, na tunapokosea tujue hakuna cha ziada zaidi ya kutubu na kumrudia Mungu. Kunyoosheana kidole sio kazi yetu. Mungu angehesabu maovu yetu hakuna mwanadamu angeweza kujidai au kutamba kuwa mwema. Tusihukumu turekebishane kindugu na kwa upendo, tukishikana mikono wote tupelekana Mbinguni kwa Mungu Baba yetu wote.

Sala: Bwana mwenye huruma, nisaidie mimi niweze kutengeneza mwenendo wangu kwanza, kabla ya mimi kujitoa kuwarekebisha wengine. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JUNI 22, 2026




MASOMO YA MISA, JUNI 22, 2026
JUMATATU, JUMA LA 12 LA MWAKA

SOMO 1
2 Fal. 17:5 – 8, 13 – 15, 18

Mfalme wa Ashuru akakwea katikati ya nchi yote, akaenda Samaria, akauhusuru miaka mitatu. Katika mwaka wa kenda wa Hoshea, huyo mfalme wa Ashuru akautwaa Samaria, akawahamisha Israeli mpaka Ashuru, akawaweka katika Hala na Habori, karibu na mto wa Gozani, na katika miji ya Wamedi.

Yalitukia hayo kwa sababu wana wa Israeli walikuwa wametenda dhambi juu ya Bwana, Mungu wao, aliyewaleta kutoka katika nchi ya Misri watoke chini ya mkono wa Farao mfalme wa Misri, wakawaacha miungu mingine. Wakaziendea sheria za mataifa, ambao Bwana aliwafukuza mbele ya wana wa Israeli, na sheria za wafalme wa Israeli walizozifanya. 

Pamoja na hayo Bwana aliwashuhudia Israeli, na Yuda, kwa kinywa cha kila nabii, na cha kila mwonaji, akisema, Geukeni, na kuziacha njia zenu sawasawa na ile sheria yote niliyowaamuru baba zenu, nikawapelekea kwa kinywa cha manabii watumishi wangu. Walakini hawakutaka kusikia, bali walifanya shingo zao kuwa nguvu, kama shingo za baba zao, wasiomwamini Bwana, Mungu wao. Wakazikataa sheria zake, na agano lake, alilolifanya na baba zao; na shuhuda zake alizowashuhudia; wakafuata ubatili, wakawa ubatili, nao wakaandamana na mataifa waliowazunguka, ambao Bwana alikuwa amewaagiza, wasitende kwa mfano wao. Kwa hiyo Bwana akawaghadhibikia Israeli sana, akawahamisha mbali na uso wake; wala hapana aliyesalia ila kabila ya Yuda peke yake.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 60:1 – 3, 10 – 11 (K) 5

(K) Uokoe kwa mkono wako wa kuume, Ee Bwana, utuitikie.

Ee Mungu, umetutupa na kututawanya,
Umekuwa na hasira, uturudishe tena. (K)

Umeitetemesha nchi na kuipasua,
Upaponye palipobomoka, maana inatikisika.
Umewaonyesha watu wako mazito,
Na kutunywesha mvinyo ya kutuyumbisha. (K)

Ee Mungu, si Wewe uliyetutupa?
Wala, Ee Mungu, hutoki na majeshi yetu?
Utuletee msaada juu ya mtesi,
Maana wokovu wa binadamu haufai. (K)


SHANGILIO
Zab. 119:28, 33

Aleluya, aleluya,
Unitie nguvu sawasawa na neno lako, ee Bwana, unifundishe njia ya amri zako.
Aleluya.


INJILI
Mk. 7:1 – 5

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Msihukumu msije mkahukumiwa ninyi. Kwa kuwa hukumu mhukumuyo, ndiyo mtakayohukumiwa; na kipimo kile mpimiacho, ndicho mtakachopimiwa. Basi, mbona wakitazama kibanzi kilicho ndani ya jicho la ndugu yako, na boriti iliyo ndani ya jicho lako mwenyewe huiangalii? Au utamwambiaje nduguyo, Niache nikitoe kibanzi katika jicho lako; na kumbe! Mna boriti ndani ya jicho lako mwenyewe? Mnafiki wewe, itoe kwanza ile boriti katika jicho lako mwenyewe; ndipo utakapoona vema kukitoa kile kibanzi katika jicho la ndugu yako.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

YESU YUPO PAMOJA NASI KUTUOKOA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila Jumapili
Jumapili, Juni 21, 2026
Dominika ya 12 ya Mwaka


Yer 20: 10-13; 
Zab 68: 8-10, 14, 17, 33-35; 
Rom 5: 12-15; 
Mt 10: 26-33.


YESU YUPO PAMOJA NASI KUTUOKOA!

Kabla ya kuingia katika barabara kuu ukitokea mitaani, lazima kuwa makini na mwangalifu kwa kuangalia pia alama zilizo wekwa. Ni vizuri kuangalia kama tunafuata gari jingine au kuna mtu barabarani. Hivyo hivyo, wafuasi wa Yesu wanapaswa kuwa makini katika kutembea kinyume na mapigo ya dunia. Kama wakichagua njia ya kujikatalia, kuwapenda watu, kusamehe, uaminifu, wata waona watu wakitembea mwelekeo mwingine. Na watatambua kuwa na kuchukua tahadhari kwamba haijalishi nakuwa mwaminifu namna ghani, migongano haikwepeki. Watakuwa tu watu wakuteseka, kuonekana kama waliopoteza mwelekeo, wavunjifu wa sheria zinazo kubalika na wote. Hili pia laweza kuwafanya wakristo kujisikia kwamba wamechagua njia isiyo sahihi.

Katika somo la kwanza tunakutana na Yeremia aliyeishi katika kipindi katika historia ya mwenendo usio kuwa mzuri wa watu wake. Jeshi la Nebukadneza limeizunguka Yerusalemu na kuichukua mateka. Mfalme na majeshi yake wamefanya maamuzi yasio kuwa sahihi ya kuleta maangamizi. Badala ya viongozi wa dini kutambua yanayo wapata watu, wanamsifia Mfalme na jeshi lake. Katika hali hii ngumu, Yeremia kijana mdogo, mwenye aibu, na mtu wa amani anaitwa na Mungu kufanya utume hatarishi juu ya “Mfalme wa Yuda na viongozi wake, makuhani wake na watu wote katika nchi”. Ana imarishwa na Bwana kwa maneno haya “watapigana nawe lakini hawata kushinda, kwani nipo nawe kukuokoa” (Yer 1:17-19). Yeremia anakutana na upinzani. Maadui wa Yeremia hawaja jifunga tu katika makundi bala wanamtafuta ili wamtundike na kumuua. Yeremia anaona utume wake umeshindwa, anajisikia kukataliwa na watu wake na watu wote. Anakata tamaa, na kujiuliza kama kweli wito wake pengine haukuwa wa kweli. Anaeleza hisia zake kwa Mungu. Sala yake alioifanya kwa mkazo, lakini katika uaminifu, inaleta matokeo kwake ya ukweli wa uamini fu wa Mungu. Ujasiri wake na matumaini yake yana amka tena. Anatangaza: “Yahweh Bwana wa majeshi yupo nami” (mstari. 11). Ana ujasiri na uhakika kwamba Mungu, Mungu atamshindia, anafanya ukweli utawale na kumfanya mwenye kutetea haki kungara.

Katika somo la pili kutoka barua kwa Warumi, Paulo anamlinganisha Adamu na Yesu: analinganisha matokeo ya dhambi ya mtu wa kwanza na matokeo ya ukombozi ulioletwa na Kristo. Tangu awali mwanadamu alitenda dhambi, kwa kufuata mfano wa Adamu aliyekosa utii na kwenda kinyume na mapenzi ya Mungu, lakini, Yesu alifanya kinyume chake. Yeye ni mtii kwa Baba, ametimiza mapenzi yake mpaka kufa. Matokeo ya dhambi ya Adamu ni kifo. Neema inayo patika kwa utii wa Kristo, ni mkuu sana. Kwa njia ya Kristo, Mungu amewapa uhai wote.

Katika Injili ya Mathayo iliyo andikwa kipindi cha Mfalme Domitian wa Kirumi, aliye amuru kuabudiwa kama Mungu. Wakristo hawakuweza kumpa mfalme sifa za Mungu. Kwa njia hiyo, matatizo yalianza, kupigwa, kutengwa, mali zao kuchukuliwa yalianza juu yao. Walio wengi hawakuweza kuvumilia unyanyasaji wa namna hii. Walikuwa katika hali ngumu ya kufanya uamuzi. Hivyo, ili kuwafariji wakristo wa jamii yake, Mathayo ana andika maneno hayo ya Yesu, ya kihistoria, ambayo aliyaweka katika Injili, maneno ya Yesu kuhusu kupatwa na magumu na mateso kwa wafuasi wake. Kwa Wakristo mateso sio ajali; haya kwepeki: “wale wote wanaotaka kumtumikia Mungu kwa njia ya Kristo, watateseka”. (2 Tim 3:12).


Katika Injili ya Leo, Yesu anasisitiza mara tatu “msiogope!” na kila wakati ameongeza motisha ili kuonesha msisitizo wa ujumbe wake. Yesu ana tuhakikishia kwamba licha ya magumu na mateso, Injili itaenea ulimwenguni na kuubadilisha. Yesu anatuita pia tutafakari: ni madhara ghani adui wa Injili anaweza kuleta? Kusingiziwa, kuhukumiwa bila haki, kupigwa, kuchukua mali, kuuwawa! Ndio, lakini hamna zaidi! Hakuna vita vyenye uwezo wakuweza kuchukua thamani ya uzima: uzima aliotoa Mungu hakuna anaye weza kuuchukua. Lakini kuna mtu-Yesu anaendelea-ambaye anapaswa kuogopwa. Ni “yule ambaye ana nguvu ya kuangamiza mwili na roho kwa pamoja”. Hali hii sio hali ya nje, bali niuovu ambao tangu kuzaliwa, tunauchukua ndani mwetu. Hii ni msukumo mbaya unao tuongoza kwenye njia tofauti na njia ya Kristo. Hivyo tunapaswa pia kujiogopa sisi wenyewe na hofu yetu. Yesu anatuita kutegemea nguvu ya Mungu. Anatupa uhakika kwamba Mungu atatambua uzuri wetu kama tutakuwa jasiri na kubaki waaminifu.

Sala: Baba wa Mbinguni, ninakushukuru kwa upendo wako katika maisha yangu. Ninakushukuru kwa kuniita mimi na kunibadili ili niweze pia kubadili ulimwengu. Nisaidie mimi nitegemee upendo wako na kujikabidhi kwako. Katika nyakati za mateso, kuwa nguvu yangu na tumaini. Ninawaombea pia wakristo wote wanao onewa ulimwenguni, ili waweze kuvumilia mpaka mwisho. Yesu nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUNI 21, 2026



MASOMO YA MISA, JUNI 21, 2026
JUMAPILI YA 12 YA MWAKA



SOMO 1
Yer. 20 : 10-13

Nimesikia mashutumu ya watu wengi; hofu ziko pande zote. Rafiki zangu wote wanaonivizia nisite, husema, Mshitaki, nasi tutamshitaki; huenda akahahadaika; nasi tutamshinda, tutajilipiza kisasi kwake. Lakini Bwana yu pamoja nami, mfano wa shujaa mwenye kutisha; kwa hiyo hao wanaonionea watajikwaa, wala hawatashinda; watatahayarika sana. Kwa sababu hawakutenda kwa akili, wataona aibu ya milele, ambayo haitasahauliwa kamwe. Lakini Ee Bwana wa majeshi, wewe wawajaribu wenye haki, waona viuno na mioyo. nijalie kuona kisasi chako juu yao; kwa maana nimekufunulia wewe neno langu.

Mwimbieni Bwana; msifuni Bwana; 
Kwa maana ameiponya roho ya mhitaji 
Katika mikono ya watu watendao maovu.


Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 69 : 7-9, 13,16, 32-34 (K) 13

(K) Kwa wingi wa fadhili zako unijibu.

Kwa ajili yako nimestahimili laumu,
Fedheha imenifunika uso wangu.
Nimekuwa mgeni kwa ndugu zangu,
Na msikwao kwa wana wa mama yangu.
Maana wivu wa nyumba yako umenila,
Na laumu yao wanaokulaumu zimenipata. (K)

Nami maombi yangu nakuomba Wewe, Bwana, 
Wakati ukupendezao; Ee Mungu,
Kwa wingi wa fadhili zako unijibu,
Katika kweli ya wokovu wako.
Ee Bwana, unijibu, maana fadhili zako ni njema,
Kwa kadiri ya rehema zako unielekee. (K)

Walioonewa watakapoona watafurahi;
Enyi mmtafutao Mungu, mioyo yetu ihuishwe.
Kwa kuwa Bwana huwasikia wahitaji,
Wala hawadharau wafunga wake.
Mbingu na nchi zimsifu
Bahari na vyote viendavyo ndani yake. (K)



SOMO 2
Rum. 5:12-15

Kama kwa mtu mmoja dhambi iliingia uli mwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi; maana kabla ya sheria dhambi ilikuwamo ulimwenguni, lakini dhambi haihesabiwi isipokuwapo sheria; walakini mauti ilitawala tangu Adamu mpaka Musa, nayo iliwatawala hata wao wasiofanya dhambi ifananayo na kosa la Adamu, alive mfano wake yeye atakayekuja. Lakini karama ile haikuwa kama lile kosa; kwa maana ikiwa kwa kukosa kwake yule mmoja wengi walikufa, zaidi sana neema ya Mungu, na kipawa kilicho katika neema yake mwanadamu mmoja Yesu Kristo kimezidi kwa ajili ya wale wengi.


Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.




SHANG1LIO
Mdo. 16:14

Aleluya, aleluya,
Fungua mioyo yetu, ee Bwana, 
Ili tuyatunze maneno ya Mwanao.
Aleluya.



INJILI
Mt. 10:26-33

Yesu aliwaambia mitume wake: Msiwaogope, kwa maana hakuna neno lililositirika, ambalo halitafunuliwa; wala lililofichwa, ambalo halitajulikana. Niwaambialo ninyi katika giza, lisemeni katika nuru; na msikialo kwa siri, lihubirini juu ya nyumba. Msiwaogope wauuao mwili, wasiweze kuiua na roho; afadhali mwogopeni yule awezaye kuangamiza mwili na roho pia katika jehanum, Je! mashomoro wawili hawauzwi kwa senti moja? Wala hata mmoja haanguki chini asipojua Baba yenu; lakini ninyi, hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope basi; bora nyinyi kuliko mashomoro wengi. Basi, kila mtu atakayenikiri mbele ya watu, nami nitamkiri mbele za Baba yangu aliye mbinguni. Bali mtu ye yote atakayenikana mbele ya watu, nami nitamkana mbele za Baba yangu aliye mbinguni.


Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

BWANA WANGU NINANI- MUNGU AU PESA?




ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumamosi, Juni, 20, 2026,
Juma la 11 la Mwaka


2 Nya 24: 17-25;
Zab 88: 4-5, 29-34;
Mt 6: 24-34


BWANA WANGU NINANI- MUNGU AU PESA?


“Moyo uliogawanyika ni moyo wa huzuni.”  Wote tunajua hili kwasababu ni moyo ulio na wasi wasi na usiojiweza. Leo tunasikia Yesu akituambia hatuwezi kutumikia mabwana wawili. Hatuwezi kujitoa kwa Mungu moja kwa moja kama tumetekwa na pesa. Kwanini? Kwasababu vyote vinahitaji kujikita na kujitoa. Mungu anahitaji majitoleo ya kweli si kwaajili yake bali kwaajili yetu wenyewe. Hatuwezi kuwa na furaha kabisa au furaha ya kweli bila Mungu. Na ni Mungu mwenyewe anaweza kurudhisha tamaa ya moyo wa Mwanadamu.

Hakuna mtu anaeweza kuwatumikia mabwana wawili kwa muda mrefu. Kwasababu wakati Mabwana wote wawili wakiwa wanatembea pamoja, anaweza kuwafuata nyuma yao lakini watakapo amua mmoja kwenda uelekeo wake na huyu wake, lazima achague ni yupi wakumfuata. Haijalishi ni mara ngapi watu wamemuasi Mungu na kufuata au kuabudu mali na pesa, Mungu haachi kamwe kuwapigania warudi kwake. Tujikumbushe maneno haya ya Mungu “Sitawaacha kamwe wala kuwakataa ninyi” (Kumb 31: 6). Somo la kweli katika historia ya Mwanadamu ni kwamba-Hakuna mtu anayeweza kuwatumikia mabwana wawili katika hali ya kweli. Mkristo kwa kweli hawezi kutenda haki ya Mungu kwakujiingiza kabisa katika mali na anasa za ulimwengu huu.

Uovu wa kujaribu kugawanya uaminifu wetu unajikita katika kushindwa kwetu kutumainia Upendo wa Mungu Baba yetu. Tunajaribu kutafuta ulinzi wa maisha yetu katika mali na utajiri wetu. Tunafanya kila liwezekanalo kulinda heshima yetu katika mali, tunadhani tukipungukiwa tutadharauliwa na watu, kwahiyo siku zote tunajaribu kujilinda kuweka mambo yetu vizuri bila kujali kama na muumiza mwanadamu mwenzangu. Tunawatumikisha wengine wanateseka bila maji au chakula, ali mradi nimepata faida na utajiri wangu ubaki pale pale. Tunaogopa kuwasaidia wengine kwasababu tunadhani tutapungukiwa. Roho na akili yetu haina Amani usiku kucha kwasababu natafuta jinsi ya kutegemeza utajiri wangu, tumekamatwa sana na mali mpaka tunasahau nafsi ya Mungu katika maisha yetu. Tunakimbilia kwenye biashara kiasi chakushindwa hata kufanya ishara ya msalaba ili Mungu abariki mipango yetu. Mungu ni namba moja, mengine yote ni sifuri, tujitahidi kuitanguliza hii numba moja ili hizi sifuri zinazofuata nyuma yake zifanye yote yawe mengi, lakini ukitanguliza sifuri badala ya moja nadhani unajua utapata nini.

Kwa ufupi maisha yetu yatawaliwe na Mungu, chochote kamwe kisichukue nafasi ya Mungu. Mungu anapenda maadili yetu na thamani ya yote tulionayo yajengwe katika msingi wake yeye mwenyewe na hapo yataleta furaha na Amani kwetu. Mungu anajua mahitaji yetu hata kabla hatuja mwomba na anawapa wote kwa upendo wanao mtumainia.

Sala: Bwana naomba usinifanye maskini wala usinifanye tajiri mno, nishibishe kwa chakula ninacho hitaji nisije nikashiba mno nikakutukana nikasema “Mungu ni nani kwani?” au nisiwe maskini mno nikaiba nikalikashifu jina lako Mungu. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JUNI 20, 2026





MASOMO YA MISA, JUNI 20, 2026
JUMAMOSI, JUMA LA 11 LA MWAKA



SOMO 1
Nya. 24:17 – 25

Baada ya kufa kwake Yehoyada, wakuu wa Yuda wakamwendea mfalme, wakamsujudia. Naye mfalme akawasikiliza maneno yao. Wakaiacha nyumba ya Bwana, mungu wa baba zao; wakatumikia maashera na sanamu; ghadhabu ikawajia Yuda na Yerusalemu kwa sababu ya hiyo hatia yao. Hata hivyo akawapelekea manabii, ili kuwarudisha kwa Bwana; nao wakawashuhudia; lakini hawakukubali kuwasikiliza.

Na roho ya Mungu ikamjia Zekaria, mwana wa Yehoyada, kuhani; naye akasimama juu ya watu, akawaambia, Mungu asema hivi, Kwani ninyi kuzihalifu amri za Bwana, hata msiweze kufanikiwa? Kwa kuwa mmemwacha Bwana, yeye naye amewaacha ninyi. Basi, wakafanya shauri juu yake, wakampiga kwa mawe kwa amri ya mfalme, katika ua wa nyumba ya Bwana. Basi hivyo mfalme Yoashi hakuukumbuka wema, ambao Yehoyada, baba yake, alimfanyia, bali alimwua mwanawe. Naye alipokufa, alisema, Bwana na ayaangalie haya, akayatakie kisasi.

Ikawa mwisho wa mwaka, wakakwea juu yake jeshi la Washami; wakafika Yuda na Yerusalemu, wakawaangamiza wakuu wa watu wote miongoni mwa watu, wakamletea mfalme wa Dameski nyara zao zote. Maana wakaja jeshi la Washami watu haba; Bwana akatia mikononi mwao jeshi kubwa mno, kwa sababu wamemwacha Bwana, Mungu wa baba zao.

Hivyo wakamfanyia Yoashi hukumu. Hata walipoondoka kwake, (nao walimwacha ameshikwa sana na maradhi) watumishi wake mwenyewe wakamfanyia fitina kwa ajili ya damu ya mwana wa Yehoyada kuhani, wakamwua kitandani pake, akafa; wakamzika mjini mwa Daudi, lakini hawakumzika katika makaburi ya wafalme.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 89: 3- 4, 28 – 33 (K) 28


(K) Nitamwekea fadhili zangu milele.

Nimefanya agano na mteule wangu,
Nimemwapa Daudi, mtumishi wangu.
Wazao wako nitawafanya imara milele,
Nitakijenga kiti chako cha enzi hata milele. (K)

Hata milele nitamwekea fadhili zangu,
Na agano langu litafanyika amini kwake.
Wazao wake nao nitawadumisha milele,
Na kiti chake cha enzi kama siku za mbingu. (K)

Wanawe wakiiacha sheria yangu,
Wasiende katika hukumu zangu,
Wakizihalifu amri zangu,
Wasiyashike maagizo yangu. (K)

Basi, nitawarudi makosa yao kwa fimbo,
Na uovu wao kwa mapigo.
Lakini fadhili zangu sitamwondolea yeye,
Wala sitafanya uaminifu wangu kuwa uongo. (K)



SHANGILIO
Zab. 119: 135

Aleluya, aleluya,
Umwangazie mtumishi wako uso wako, na kunifundisha amri zako.
Aleluya.


INJILI
Mt. 6: 24 – 34


Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Hkuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili, kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali.

Kwa sababu hiyo nawaambieni, Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini. Maisha je! Si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi? Waangalieni ndege wa angani, ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao. Ninyi je! Si bora kupita hao? Ni yupi kwenu ambaye akijisumbua aweza kujiongoeza kimo chake hata mkono mmoja? Na mavazi, ya nini kuyasumbukia? Fikirini maua ya mashamba, jinsi yameavyo; hayafanyi kazi, wala hayasonkoti; nami nawaambia, ya kwamba hata Sulemani katika fahari yake yote hakuvikwa vizuri kama mojawapo la hayo.

Basi, ikiwa Mungu huyavika hivi majani ya kondeni, yaliyopo leo, na kesho hutupwa kalibuni, je! Hatazidi sana kuwavika ninyi, enyi wa imani haba? Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? Au Tunywe nini? Au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.

Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.


Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.