Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

YESU YUPO PAMOJA NASI KUTUOKOA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila Jumapili
Jumapili, Juni 21, 2026
Dominika ya 12 ya Mwaka


Yer 20: 10-13; 
Zab 68: 8-10, 14, 17, 33-35; 
Rom 5: 12-15; 
Mt 10: 26-33.


YESU YUPO PAMOJA NASI KUTUOKOA!

Kabla ya kuingia katika barabara kuu ukitokea mitaani, lazima kuwa makini na mwangalifu kwa kuangalia pia alama zilizo wekwa. Ni vizuri kuangalia kama tunafuata gari jingine au kuna mtu barabarani. Hivyo hivyo, wafuasi wa Yesu wanapaswa kuwa makini katika kutembea kinyume na mapigo ya dunia. Kama wakichagua njia ya kujikatalia, kuwapenda watu, kusamehe, uaminifu, wata waona watu wakitembea mwelekeo mwingine. Na watatambua kuwa na kuchukua tahadhari kwamba haijalishi nakuwa mwaminifu namna ghani, migongano haikwepeki. Watakuwa tu watu wakuteseka, kuonekana kama waliopoteza mwelekeo, wavunjifu wa sheria zinazo kubalika na wote. Hili pia laweza kuwafanya wakristo kujisikia kwamba wamechagua njia isiyo sahihi.

Katika somo la kwanza tunakutana na Yeremia aliyeishi katika kipindi katika historia ya mwenendo usio kuwa mzuri wa watu wake. Jeshi la Nebukadneza limeizunguka Yerusalemu na kuichukua mateka. Mfalme na majeshi yake wamefanya maamuzi yasio kuwa sahihi ya kuleta maangamizi. Badala ya viongozi wa dini kutambua yanayo wapata watu, wanamsifia Mfalme na jeshi lake. Katika hali hii ngumu, Yeremia kijana mdogo, mwenye aibu, na mtu wa amani anaitwa na Mungu kufanya utume hatarishi juu ya “Mfalme wa Yuda na viongozi wake, makuhani wake na watu wote katika nchi”. Ana imarishwa na Bwana kwa maneno haya “watapigana nawe lakini hawata kushinda, kwani nipo nawe kukuokoa” (Yer 1:17-19). Yeremia anakutana na upinzani. Maadui wa Yeremia hawaja jifunga tu katika makundi bala wanamtafuta ili wamtundike na kumuua. Yeremia anaona utume wake umeshindwa, anajisikia kukataliwa na watu wake na watu wote. Anakata tamaa, na kujiuliza kama kweli wito wake pengine haukuwa wa kweli. Anaeleza hisia zake kwa Mungu. Sala yake alioifanya kwa mkazo, lakini katika uaminifu, inaleta matokeo kwake ya ukweli wa uamini fu wa Mungu. Ujasiri wake na matumaini yake yana amka tena. Anatangaza: “Yahweh Bwana wa majeshi yupo nami” (mstari. 11). Ana ujasiri na uhakika kwamba Mungu, Mungu atamshindia, anafanya ukweli utawale na kumfanya mwenye kutetea haki kungara.

Katika somo la pili kutoka barua kwa Warumi, Paulo anamlinganisha Adamu na Yesu: analinganisha matokeo ya dhambi ya mtu wa kwanza na matokeo ya ukombozi ulioletwa na Kristo. Tangu awali mwanadamu alitenda dhambi, kwa kufuata mfano wa Adamu aliyekosa utii na kwenda kinyume na mapenzi ya Mungu, lakini, Yesu alifanya kinyume chake. Yeye ni mtii kwa Baba, ametimiza mapenzi yake mpaka kufa. Matokeo ya dhambi ya Adamu ni kifo. Neema inayo patika kwa utii wa Kristo, ni mkuu sana. Kwa njia ya Kristo, Mungu amewapa uhai wote.

Katika Injili ya Mathayo iliyo andikwa kipindi cha Mfalme Domitian wa Kirumi, aliye amuru kuabudiwa kama Mungu. Wakristo hawakuweza kumpa mfalme sifa za Mungu. Kwa njia hiyo, matatizo yalianza, kupigwa, kutengwa, mali zao kuchukuliwa yalianza juu yao. Walio wengi hawakuweza kuvumilia unyanyasaji wa namna hii. Walikuwa katika hali ngumu ya kufanya uamuzi. Hivyo, ili kuwafariji wakristo wa jamii yake, Mathayo ana andika maneno hayo ya Yesu, ya kihistoria, ambayo aliyaweka katika Injili, maneno ya Yesu kuhusu kupatwa na magumu na mateso kwa wafuasi wake. Kwa Wakristo mateso sio ajali; haya kwepeki: “wale wote wanaotaka kumtumikia Mungu kwa njia ya Kristo, watateseka”. (2 Tim 3:12).


Katika Injili ya Leo, Yesu anasisitiza mara tatu “msiogope!” na kila wakati ameongeza motisha ili kuonesha msisitizo wa ujumbe wake. Yesu ana tuhakikishia kwamba licha ya magumu na mateso, Injili itaenea ulimwenguni na kuubadilisha. Yesu anatuita pia tutafakari: ni madhara ghani adui wa Injili anaweza kuleta? Kusingiziwa, kuhukumiwa bila haki, kupigwa, kuchukua mali, kuuwawa! Ndio, lakini hamna zaidi! Hakuna vita vyenye uwezo wakuweza kuchukua thamani ya uzima: uzima aliotoa Mungu hakuna anaye weza kuuchukua. Lakini kuna mtu-Yesu anaendelea-ambaye anapaswa kuogopwa. Ni “yule ambaye ana nguvu ya kuangamiza mwili na roho kwa pamoja”. Hali hii sio hali ya nje, bali niuovu ambao tangu kuzaliwa, tunauchukua ndani mwetu. Hii ni msukumo mbaya unao tuongoza kwenye njia tofauti na njia ya Kristo. Hivyo tunapaswa pia kujiogopa sisi wenyewe na hofu yetu. Yesu anatuita kutegemea nguvu ya Mungu. Anatupa uhakika kwamba Mungu atatambua uzuri wetu kama tutakuwa jasiri na kubaki waaminifu.

Sala: Baba wa Mbinguni, ninakushukuru kwa upendo wako katika maisha yangu. Ninakushukuru kwa kuniita mimi na kunibadili ili niweze pia kubadili ulimwengu. Nisaidie mimi nitegemee upendo wako na kujikabidhi kwako. Katika nyakati za mateso, kuwa nguvu yangu na tumaini. Ninawaombea pia wakristo wote wanao onewa ulimwenguni, ili waweze kuvumilia mpaka mwisho. Yesu nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUNI 21, 2026



MASOMO YA MISA, JUNI 21, 2026
JUMAPILI YA 12 YA MWAKA



SOMO 1
Yer. 20 : 10-13

Nimesikia mashutumu ya watu wengi; hofu ziko pande zote. Rafiki zangu wote wanaonivizia nisite, husema, Mshitaki, nasi tutamshitaki; huenda akahahadaika; nasi tutamshinda, tutajilipiza kisasi kwake. Lakini Bwana yu pamoja nami, mfano wa shujaa mwenye kutisha; kwa hiyo hao wanaonionea watajikwaa, wala hawatashinda; watatahayarika sana. Kwa sababu hawakutenda kwa akili, wataona aibu ya milele, ambayo haitasahauliwa kamwe. Lakini Ee Bwana wa majeshi, wewe wawajaribu wenye haki, waona viuno na mioyo. nijalie kuona kisasi chako juu yao; kwa maana nimekufunulia wewe neno langu.

Mwimbieni Bwana; msifuni Bwana; 
Kwa maana ameiponya roho ya mhitaji 
Katika mikono ya watu watendao maovu.


Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 69 : 7-9, 13,16, 32-34 (K) 13

(K) Kwa wingi wa fadhili zako unijibu.

Kwa ajili yako nimestahimili laumu,
Fedheha imenifunika uso wangu.
Nimekuwa mgeni kwa ndugu zangu,
Na msikwao kwa wana wa mama yangu.
Maana wivu wa nyumba yako umenila,
Na laumu yao wanaokulaumu zimenipata. (K)

Nami maombi yangu nakuomba Wewe, Bwana, 
Wakati ukupendezao; Ee Mungu,
Kwa wingi wa fadhili zako unijibu,
Katika kweli ya wokovu wako.
Ee Bwana, unijibu, maana fadhili zako ni njema,
Kwa kadiri ya rehema zako unielekee. (K)

Walioonewa watakapoona watafurahi;
Enyi mmtafutao Mungu, mioyo yetu ihuishwe.
Kwa kuwa Bwana huwasikia wahitaji,
Wala hawadharau wafunga wake.
Mbingu na nchi zimsifu
Bahari na vyote viendavyo ndani yake. (K)



SOMO 2
Rum. 5:12-15

Kama kwa mtu mmoja dhambi iliingia uli mwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi; maana kabla ya sheria dhambi ilikuwamo ulimwenguni, lakini dhambi haihesabiwi isipokuwapo sheria; walakini mauti ilitawala tangu Adamu mpaka Musa, nayo iliwatawala hata wao wasiofanya dhambi ifananayo na kosa la Adamu, alive mfano wake yeye atakayekuja. Lakini karama ile haikuwa kama lile kosa; kwa maana ikiwa kwa kukosa kwake yule mmoja wengi walikufa, zaidi sana neema ya Mungu, na kipawa kilicho katika neema yake mwanadamu mmoja Yesu Kristo kimezidi kwa ajili ya wale wengi.


Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.




SHANG1LIO
Mdo. 16:14

Aleluya, aleluya,
Fungua mioyo yetu, ee Bwana, 
Ili tuyatunze maneno ya Mwanao.
Aleluya.



INJILI
Mt. 10:26-33

Yesu aliwaambia mitume wake: Msiwaogope, kwa maana hakuna neno lililositirika, ambalo halitafunuliwa; wala lililofichwa, ambalo halitajulikana. Niwaambialo ninyi katika giza, lisemeni katika nuru; na msikialo kwa siri, lihubirini juu ya nyumba. Msiwaogope wauuao mwili, wasiweze kuiua na roho; afadhali mwogopeni yule awezaye kuangamiza mwili na roho pia katika jehanum, Je! mashomoro wawili hawauzwi kwa senti moja? Wala hata mmoja haanguki chini asipojua Baba yenu; lakini ninyi, hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope basi; bora nyinyi kuliko mashomoro wengi. Basi, kila mtu atakayenikiri mbele ya watu, nami nitamkiri mbele za Baba yangu aliye mbinguni. Bali mtu ye yote atakayenikana mbele ya watu, nami nitamkana mbele za Baba yangu aliye mbinguni.


Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

BWANA WANGU NINANI- MUNGU AU PESA?




ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumamosi, Juni, 20, 2026,
Juma la 11 la Mwaka


2 Nya 24: 17-25;
Zab 88: 4-5, 29-34;
Mt 6: 24-34


BWANA WANGU NINANI- MUNGU AU PESA?


“Moyo uliogawanyika ni moyo wa huzuni.”  Wote tunajua hili kwasababu ni moyo ulio na wasi wasi na usiojiweza. Leo tunasikia Yesu akituambia hatuwezi kutumikia mabwana wawili. Hatuwezi kujitoa kwa Mungu moja kwa moja kama tumetekwa na pesa. Kwanini? Kwasababu vyote vinahitaji kujikita na kujitoa. Mungu anahitaji majitoleo ya kweli si kwaajili yake bali kwaajili yetu wenyewe. Hatuwezi kuwa na furaha kabisa au furaha ya kweli bila Mungu. Na ni Mungu mwenyewe anaweza kurudhisha tamaa ya moyo wa Mwanadamu.

Hakuna mtu anaeweza kuwatumikia mabwana wawili kwa muda mrefu. Kwasababu wakati Mabwana wote wawili wakiwa wanatembea pamoja, anaweza kuwafuata nyuma yao lakini watakapo amua mmoja kwenda uelekeo wake na huyu wake, lazima achague ni yupi wakumfuata. Haijalishi ni mara ngapi watu wamemuasi Mungu na kufuata au kuabudu mali na pesa, Mungu haachi kamwe kuwapigania warudi kwake. Tujikumbushe maneno haya ya Mungu “Sitawaacha kamwe wala kuwakataa ninyi” (Kumb 31: 6). Somo la kweli katika historia ya Mwanadamu ni kwamba-Hakuna mtu anayeweza kuwatumikia mabwana wawili katika hali ya kweli. Mkristo kwa kweli hawezi kutenda haki ya Mungu kwakujiingiza kabisa katika mali na anasa za ulimwengu huu.

Uovu wa kujaribu kugawanya uaminifu wetu unajikita katika kushindwa kwetu kutumainia Upendo wa Mungu Baba yetu. Tunajaribu kutafuta ulinzi wa maisha yetu katika mali na utajiri wetu. Tunafanya kila liwezekanalo kulinda heshima yetu katika mali, tunadhani tukipungukiwa tutadharauliwa na watu, kwahiyo siku zote tunajaribu kujilinda kuweka mambo yetu vizuri bila kujali kama na muumiza mwanadamu mwenzangu. Tunawatumikisha wengine wanateseka bila maji au chakula, ali mradi nimepata faida na utajiri wangu ubaki pale pale. Tunaogopa kuwasaidia wengine kwasababu tunadhani tutapungukiwa. Roho na akili yetu haina Amani usiku kucha kwasababu natafuta jinsi ya kutegemeza utajiri wangu, tumekamatwa sana na mali mpaka tunasahau nafsi ya Mungu katika maisha yetu. Tunakimbilia kwenye biashara kiasi chakushindwa hata kufanya ishara ya msalaba ili Mungu abariki mipango yetu. Mungu ni namba moja, mengine yote ni sifuri, tujitahidi kuitanguliza hii numba moja ili hizi sifuri zinazofuata nyuma yake zifanye yote yawe mengi, lakini ukitanguliza sifuri badala ya moja nadhani unajua utapata nini.

Kwa ufupi maisha yetu yatawaliwe na Mungu, chochote kamwe kisichukue nafasi ya Mungu. Mungu anapenda maadili yetu na thamani ya yote tulionayo yajengwe katika msingi wake yeye mwenyewe na hapo yataleta furaha na Amani kwetu. Mungu anajua mahitaji yetu hata kabla hatuja mwomba na anawapa wote kwa upendo wanao mtumainia.

Sala: Bwana naomba usinifanye maskini wala usinifanye tajiri mno, nishibishe kwa chakula ninacho hitaji nisije nikashiba mno nikakutukana nikasema “Mungu ni nani kwani?” au nisiwe maskini mno nikaiba nikalikashifu jina lako Mungu. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JUNI 20, 2026





MASOMO YA MISA, JUNI 20, 2026
JUMAMOSI, JUMA LA 11 LA MWAKA



SOMO 1
Nya. 24:17 – 25

Baada ya kufa kwake Yehoyada, wakuu wa Yuda wakamwendea mfalme, wakamsujudia. Naye mfalme akawasikiliza maneno yao. Wakaiacha nyumba ya Bwana, mungu wa baba zao; wakatumikia maashera na sanamu; ghadhabu ikawajia Yuda na Yerusalemu kwa sababu ya hiyo hatia yao. Hata hivyo akawapelekea manabii, ili kuwarudisha kwa Bwana; nao wakawashuhudia; lakini hawakukubali kuwasikiliza.

Na roho ya Mungu ikamjia Zekaria, mwana wa Yehoyada, kuhani; naye akasimama juu ya watu, akawaambia, Mungu asema hivi, Kwani ninyi kuzihalifu amri za Bwana, hata msiweze kufanikiwa? Kwa kuwa mmemwacha Bwana, yeye naye amewaacha ninyi. Basi, wakafanya shauri juu yake, wakampiga kwa mawe kwa amri ya mfalme, katika ua wa nyumba ya Bwana. Basi hivyo mfalme Yoashi hakuukumbuka wema, ambao Yehoyada, baba yake, alimfanyia, bali alimwua mwanawe. Naye alipokufa, alisema, Bwana na ayaangalie haya, akayatakie kisasi.

Ikawa mwisho wa mwaka, wakakwea juu yake jeshi la Washami; wakafika Yuda na Yerusalemu, wakawaangamiza wakuu wa watu wote miongoni mwa watu, wakamletea mfalme wa Dameski nyara zao zote. Maana wakaja jeshi la Washami watu haba; Bwana akatia mikononi mwao jeshi kubwa mno, kwa sababu wamemwacha Bwana, Mungu wa baba zao.

Hivyo wakamfanyia Yoashi hukumu. Hata walipoondoka kwake, (nao walimwacha ameshikwa sana na maradhi) watumishi wake mwenyewe wakamfanyia fitina kwa ajili ya damu ya mwana wa Yehoyada kuhani, wakamwua kitandani pake, akafa; wakamzika mjini mwa Daudi, lakini hawakumzika katika makaburi ya wafalme.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 89: 3- 4, 28 – 33 (K) 28


(K) Nitamwekea fadhili zangu milele.

Nimefanya agano na mteule wangu,
Nimemwapa Daudi, mtumishi wangu.
Wazao wako nitawafanya imara milele,
Nitakijenga kiti chako cha enzi hata milele. (K)

Hata milele nitamwekea fadhili zangu,
Na agano langu litafanyika amini kwake.
Wazao wake nao nitawadumisha milele,
Na kiti chake cha enzi kama siku za mbingu. (K)

Wanawe wakiiacha sheria yangu,
Wasiende katika hukumu zangu,
Wakizihalifu amri zangu,
Wasiyashike maagizo yangu. (K)

Basi, nitawarudi makosa yao kwa fimbo,
Na uovu wao kwa mapigo.
Lakini fadhili zangu sitamwondolea yeye,
Wala sitafanya uaminifu wangu kuwa uongo. (K)



SHANGILIO
Zab. 119: 135

Aleluya, aleluya,
Umwangazie mtumishi wako uso wako, na kunifundisha amri zako.
Aleluya.


INJILI
Mt. 6: 24 – 34


Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Hkuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili, kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali.

Kwa sababu hiyo nawaambieni, Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini. Maisha je! Si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi? Waangalieni ndege wa angani, ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao. Ninyi je! Si bora kupita hao? Ni yupi kwenu ambaye akijisumbua aweza kujiongoeza kimo chake hata mkono mmoja? Na mavazi, ya nini kuyasumbukia? Fikirini maua ya mashamba, jinsi yameavyo; hayafanyi kazi, wala hayasonkoti; nami nawaambia, ya kwamba hata Sulemani katika fahari yake yote hakuvikwa vizuri kama mojawapo la hayo.

Basi, ikiwa Mungu huyavika hivi majani ya kondeni, yaliyopo leo, na kesho hutupwa kalibuni, je! Hatazidi sana kuwavika ninyi, enyi wa imani haba? Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? Au Tunywe nini? Au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.

Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.


Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MTUMAINI KRISTO KWANI ATAKUOKOA





ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Ijumaa, Juni, 19, 2026,
Juma la 11 la Mwaka

2 Fal 11: 1-4, 9-18, 20;
Zab 131: 11-14,17-18;
Mt 6: 19-23


MTUMAINI KRISTO KWANI ATAKUOKOA


Biblia ina ujumbe ndani yake ambazo kwa haraka haraka unaona hazipaswi kukaa katika Biblia Takatifu. Somo la kwanza ni moja wapo ya ujumbe hizo ambazo zinaongelewa kuhusu vita, umwagaji wa damu, shutuma, kukataliwa. Kwahiyo ni vizuri kuelewa nini uhusiano ujumbe huu. Vita kati ya falme na falme au shutuma na kukataliana ndani ya familia za kifalme yalikuwa mambo yaliojiri katika siasa za kipindi cha Agano la Kale. Biblia ni Historia ya moja wapo ya falme hizi-Israeli. Ingawaje, historia hii ilichukua umuhimu zaidi katika historia ya Waisraeli lakini matukio haya yanaelezewa katika mwanga wa mpango wa Mungu juu ya watu wake. Kwahiyo, kushinda au kuanguka kwa wana Waisraeli katika vita ni alama ya uaminifu wao au kutokuwa waaminifu kwa Mungu. Ushindi katika vita ni alama ya uaminifu kwa Mungu, na kushindwa katika vita ni kukosa uaminifu Kwa Mungu. Kwahiyo waandishi wa Biblia walipenda kuelezea ujumbe huu kwakutumia ishara hizo.

Je, ni ujumbe ghani tunapata kutoka somo hili la kwanza? Malkia Athalia kwakukosa uaminifu alichukua ufalme wa Yuda kwakuharibu familia zote za kifalme. Lakini hata hivyo Mungu alimlinda na kumuokoa mtoto mmoja wa kwanza wa Mfalme aliyeuwawa, ambaye alikuja kuwa alama ya matumaini. Ujumbe ni kwamba walio waovu hawataongoza siku zote, siku moja Mungu lazima atamleta mkombozi. Kwahiyo, mtumainie Mungu naye atakuokoa. Kwa upande mwingine, ujumbe huu pia unaeleza tena maana nyingine muhimu. Unatoa pia ujumbe na taswira ya baadae ambayo Mungu ataileta ya ukombozi kupitia mwanaye Yesu Kristo. Kama vile Mungu alivyowaokoa watu wake kutoka kwa kiongozi mbaya, vivyo hivyo Mungu atawaokoa watu wake kutoka katika utawala wa muovu-dhambi. Kwahiyo kwa kumuokoa mtoto Yoashi kutoka katika mikono ya Athalia, inatukumbusha kuhusu mtoto mwingine pia aliyeokolewa kutoka kwa mikono ya Herodi, ambaye alikuwa na kuongezeka katika hekima na kuwakomboa wanadamu wote-ambaye ni Yesu Kristo.

Sala: Bwana, haijalishi nimeteseka namna ghani, au ni mateso ya namna ghani, naomba nisipoteze tumaini langu kwako juu ya neema yako Ee Bwana Mkombozi wangu. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JUNI 19, 2026




MASOMO YA MISA, JUNI 19, 2026
IJUMAA, JUMA LA 11 LA MWAKA


SOMO 1
2 Fal. 11:1-4, 9-18, 20

Athalia, mama yake Ahazia, alipoona ya kuwa mwanawe amekufa, akainuka, akawaharibu wazao wote wa kifalme. Ila Yehosheba, binti wa mfalme Yehoramu, umbu lake Ahazia, akamtwaa Yoashi mwana wa Ahazia, akamwiba miongoni mwa hao wana wa mfalme waliouawa, yeye na mlezi wake, na kuwatia katika chumba cha kulala; wakamficha usoni pa Athalia, basi kwa hiyo hakuuawa. Alikuwako pamoja naye, amefichwa nyumbani mwa Bwana, miaka sita. Naye Athalia akaitawala nchi.

Hata mwaka wa saba Yehoyada akatujma, na kuwaleta wakuu wa mamia, wa Wakari, na wa walinzi, akawaleta kwake ndani ya nyumba ya Bwana; akapatana nao, akawaapisha nyumbani mwa Bwana, akawaonyesha huyo mwana wa mfalme.

Nao wakuu wa mamia wakafanya sawasawa na yote aliyowaamuru Yehoyada kuhani; wakawatwaa kila mtu watu wake, hao watakaoingia sabato, nao watakaotoka sabato, wakaja kwa Yehoyada kuhani. Naye yule kuhani akawapa wakuu wa mamia mikuki na ngao zilizokuwa za mfalme Daudi, zilizokuwamo nyumbani mwa Bwana. Walinzi wakasimama, kila mtu na silaha zake mkononi, kutoka pembe ya kuume ya nyumba mpaka pembe ya kushoto ya nyumba mpaka pembe ya kushoto ya nyumba, kando ya madhabahu na nyumba, wakimzunguka mfalme pande zote. Ndipo akamleta nje mwana wa mfalme, akamvika taji, na kumpa ushuhuda; wakamfanya mfalme, wakamtia mafuta; wakapiga makofi, wakasema, Mfalme na aishi.

Na Athalia alipoisikia sauti ya walinzi na ya watu, aliingia kwa watu nyumbani kwa Bwana; akatazama, na tazama, mfalme amesimama karibu na nguzo kama ilivyokuwa desturi, nao wakuu na wapiga baragumu karibu na mfalme; na watu wote wa nchi wakafurahi, wakapiga baragumu. Ndipo Athalia akararua mavazi yake, akalia, Fitina! Fitina! Naye Yehoyada kuhani akawaamuru wakuu wa mamia, majemadari wa jeshi, akawaambia, Mtoeni kati ya safu; nay yeyote amfuataye mwueni kwa upanga. Kwani kuhani akasema, Asiuawe nyumbani mwa Bwana. Basi wakampisha njia; akaenda kwa njia ya kuingia kwa farasi nyumbani mwa mfalme; akauawa huko.

Kisha, Yehoyada akafanya mapatano kati ya Bwana na mfalme na watu, ili wawe watu wa Bwana; tena kati ya mfalme na watu. Watu wote wa nchi wakaiendea nyumba ya Baali, wakaiangusha; madhabahu zake na sanamu zake wakazivunjavunja kabisa, na Matani kuhani wa Baali wakamwua mbele ya madhabahu.

Na Yehoyada kuhani akaweka maakida juu ya nyumba ya Bwana. Basi watu wote wa nchi wakafurahi, na mji ukatulia. Naye Athalia wakamwua kwa upanga karibu na nyumba ya mfalme.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 132: 11 – 14, 17 – 18 (K) 13

(K) Bwana ameichagua Sayuni, ameitamani akae ndani yake.

Bwana amemwapia Daudi neno la kweli,
Hatarudi nyuma akalihalifu,
Baadhi ya wazao wa mwili wako
Nitawaweka katika kiti chako cha enzi. (K)

Wanao wakiyashika maagano yangu,
Na shuhuda nitakazowafundisha;
Watoto wao nao wataketi
Katika kiti chako cha enzi milele. (K)

Kwa kuwa Bwana ameichagua Sayuni,
Ameitamani akae ndani yake.
Hapo ndipo mahali pangu pa raha milele,
Hapo nitakaa kwa maana nimepatamani. (K)

Hapo nitamchipushia Daudi pembe,
Na taa nimemtengenezea masihi wangu.
Adui zake nitawavika aibu,
Bali juu yake taji yake itasitawi. (K)



SHANGILIO
Zab. 119: 18

Aleluya, aleluya,
Unifumbue macho yangu niyatazame maajabu yatokayo katika sheria yako.
Aleluya.




INJILI
Mt. 6:19 – 23

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi huvunja na kuiba; bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala wevi hawavunji wala hawaibi; kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako.
Taa ya mwili ni jicho; basi jicho lako likiwa safi, mwili wako wote utakuwa na nuru. Lakini jicho lako likiwa bovu, mwili wako wote utakuwa na giza. Basi ile nuru iliyomo ndani yako ikiwa giza; si giza hilo!

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

BABA YETU!



ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Alhamisi, Juni 18, 2026
Juma la 11 la Mwaka

YbS 48: 1-14;
Zab 97: 1-7;
Mt 6: 7-15


BABA YETU!


Katika Injili ya leo hatuja alikwa tu kusali bali tunazamiwa kuwa watu wa kusali. Sala ya Bwana ni mwaliko sio tuu wa kusali bali kusali pamoja na wengine. Sala ya Bwana ilitolewa kwetu na Bwana wetu Yesu Kristo, kama njia ya kutufundisha kusali. Lakini, kusema sala hii haitoshi tu. Cha muhimu ni kuzama katika kila kipengele cha sala hii ili iweze kuwa mfano wa maombi yetu kwa Mungu na chombo cha maisha yetu yote kwake.

Sala ya Bwana haijaanza na ombi, bali ina anza na kitambulisho chetu kukubali kwamba sisi ni watoto wa Baba. Huu ni ufunguo wa sala ya Bwana ikisaliwa vizuri. Inafungua pia kila chimbuko la kila sala katika maisha ya Mkristu. Kila Mkristo anapaswa kumuona Mungu kuwa Baba yetu. Tunapaswa kujiona sisi kama watoto wa Mungu ili tuweze kumfuata kama watoto wake. Watoto wana ujasiri kwa wazazi wao bila kujali wanapendwa au la. Hiki kinapaswa kuwa chanzo cha sala zetu zote kila wakati. Tunapaswa kuanza na uelewa kwamba Mungu anatupenda bila kujali hali zetu. Kwa uelewa huu wa Mungu utatusaidia sisi tuwe na ujasiri wa kumuita yeye. Kumuita Mungu “Baba” kunaonesha Agano Jipya lililo anzishwa katika damu ya Yesu Kristu. Neema hii inaonesha pia umoja wetu wa pekee tulio nao katika Yesu Kristo kama Mwana wa Mungu. Kwa hiyo hatuja unganishwa kwa pamoja tu, bali tunawezeshwa pia kumwabudu Yesu kwa pamoja. Umimi huachwa na hivyo kuwa na undugu na umoja. Sisi ni wana wa familia zawadi ya utukufu wa Mungu.

Sala: Baba yetu, uliye Mbinguni jina lako litukuzwe, ufalme wako ufike utakalo lifanyike duniani kama mbinguni, utupe leo mkate wetu wa kila siku, utusamehe makosa yetu, kama tunavyo wasamehe na sisi waliotukosea usitutie katika kishawishi lakini utuopoe maovuni. Yesu nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JUNI 18, 2026




MASOMO YA MISA, JUNI 18, 2026
ALHAMISI, JUMA LA 11 LA MWAKA


SOMO 1
YbS. 48:1 – 14

Ndipo aliposimama Nabii Eliya, kama moto, hata na neno lake likawaka kama tanuru. Yeye alileta njaa juu yao, na kwa juhudi yake akawapunguzia hesabu yao; kwa neno la Bwana akazifunga mbingu, na mara tatu kutoka huko akatelemsha moto.

Jinsi ulivyotisha kwa miujiza yako! Aliye mfano wako ataona fahari. Aliyekufa ulimfufua katika mauti, Kutoka kuzimu, kwa neno la Bwana. Ukawashusha wafalme mpaka shimoni, na watu wateule vitandani mwao. Ukapaka mafuta wafalme kwa kisasi, na nabii ili akufuate nyuma yako. Ulisikia makaripio huko Sinai, na hukumu za kisasi huko Horebu. Ukachukuliwa juu katika kisulisuli, katika gari la farasi wa moto. Ukaandikiwa kuwa utaleta makemeo, ili kutuliza hasira siku ile ya Bwana; kugeuza moyo wa baba umwelekee mwana na kuhuisha kabila za Israeli.

Bila shaka wamebarikiwa wale waliokuona kwa macho wakafa; lakini wewe umezidi kubarikiwa, kwa maana unaishi.

Ndiyo huyo Eliya aliyefunikwa kwa kisulisuli; hata na Elisha naye akajazwa roho yake; akazidisha ishara maradufu, na yale yaliyotoka kinywani mwake yalikuwa ya ajabu. Siku zake zote huyu pia hakushawishwa kwa kumwogopa mwenye kutawala, wala hakutiishwa na mtu yeyote. Hakutokea neno lililokuwa gumu la kumshinda, hata na alipolala mautini mwili wake ulitoa unabii; kama alivyofanya miujiza katika maisha yake, kadhalika na mauti yake kazi zake zikawa za ajabu.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 97: 1 – 7 (K) 12

(K) Enyi wenye haki, mfurahieni Bwana.

Bwana ametamalaki, nchi na ishangilie,
Visiwa vingi na vifurahi.
Mawingu na giza vyamzunguka,
Haki na hukumu ndio msingi wa kiti chake. (K)

Moto hutangulia mbele zake,
Nao huwateketeza watesi wake pande zote.
Umeme wake uliangaza ulimwengu,
Nchi ikaona ikatetemeka. (K)

Milima iliyeyuka kama nta mbele za Bwana,
Mbele za Bwana wa dunia yote.
Mbingu zimetangaza haki yake,
Na watu wote wameuona utukufu wake. (K)

Na waaibishwe wote waabuduo sanamu,
Wajivunao kwa vitu visivyofaa;
Enyi miungu yote, msujuduni Yeye. (K)




SHANGILIO
1 Sam. 3:9

Aleluya, aleluya,
Nena Bwana, kwa kuwa mtumishi wako anasikia, Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.
Aleluya.



INJILI
Mt. 6:7-15

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke, kama watu wa mataifa; maana wao hudhani ya kuwa watasikiwa kwa sababu ya maneno yao kuwa mengi. Basi msifanane na hao; maana Baba yenu anajua mnayohitaji kabla ninyi hamjamwomba.

Basi ninyi salini hivi; Baba yetu uliyembinguni, jina lako litukuzwe, ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni. Utupe leo riziki yetu. Utusamehe deni zetu, kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu. Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu.
Kwa maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi. Bali msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.