Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

NJIA AMBAYO KILA MKRISTO ANAPASWA KUSHIKILIA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatano, Mei, 27, 2026
Tafakari ya kila siku 
Juma la 8 la Mwaka wa Kanisa

1Pet 1: 18-25; 
Zab 147: 12-15, 19-20; 
Mk 10:32-45

NJIA AMBAYO KILA MKRISTO ANAPASWA KUSHIKILIA!


“Walikuwa njiani wakielekea Yerusalemu.” Yesu ndiye njia, na njia yake inamleta Yerusalemu, kubeba msalaba wake, kwakukubali kuachia maisha yake kwa upendo wa Baba nakutupenda sisi, akituongoza kwenye ushindi wa mwisho. Wote wanaopenda kuwa wafuasi wake wanapaswa wawe tayari kutembea katika njia hiyo pamoja naye. Wafuasi bado hawajafikia hali hii ya ufuasi. Wakati Yesu akisonga mbele kiaminifu kuelekea Yerusalemu, wafuasi wake wanaonekana kubaki nyuma kidogo. Walikuwa katika hali ya kutoelewa na wote walio wafuata walikuwa katika hali ya woga. Kwajinsi walivyofikiri wao walidhani Yesu hayupo katika mawazo yao. Kwenda Yerusalemu kipindi hiki, ilikuwa nikujitakia matatizo, tena makubwa. Yerusalemu palikuwa ni Sehemu ya mwisho kabisa kwenda.

Yesu kwa upole kabisa anawapa somo jingine, kuhusu nini maana halisi ya kuwa mkubwa katika hali ya ufalme wake. Katika dunia kuwa “mkubwa” ni kuwa na nguvu juu ya wengine, kutawala, kuwa na uwezo wakuwafanya watu wakubaliane na kile unachopenda, kuwatumia watu ili ufikie lengo lako. Lakini katika ulimwengu wa Yesu, ukubwa nikujiweka chini kwaajili ya kuwahudumia wengine, ndugu zetu, majirani, na zaidi sana wale waliowahitaji. Na watu wote kuwatumikia bila kuharibu utu wao. Mamlaka sio kuamrisha, bali kujitoa. Baada ya miaka zaidi ya 2000 ya Ukristo bado ni jambo kubwa sana kwetu kujifunza hili “Mwana wa mtu hakuja kutumikiwa bali kutumikia”. 

Sala; Bwana, badilisha mioyo yetu ya ubinafsi iwe mioyo ya kuwahudumia wengine. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MEI 27, 2026



MASOMO YA MISA, MEI 27, 2026
JUMATANO, JUMA LA 8 LA MWAKA

SOMO 1 
1 Pet. 1 :18-25

Nanyi mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa damu ya thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya Kristo. Naye amejulikana kweli tangu zamani, kabla haijawekwa misingi ya dunia; lakini alifunuliwa mwisho wa zamani kwa ajili yenu; ambao kwa yeye mmekuwa wenye kumwamini Mungu, aliyemfufua katika wafu akampa utukufu; hataimani yenu na tumaini lenu liwe kwa Mungu.

Mkiisha kujitakasa roho zenu kwa kuitii kweli, hata kuufikilia upendano wa ndugu usio na unafiki, basi jitahidini kupendana kwa moyo. Kwa kuwa mmezaliwa mara ya pili; si kwa mbegu iharibikayo, bali kwa ile isiyoharibika; kwa neno la Mungu ienye uzima, lidumulo hata milele. Maana, Mwili wote ni kama majani, Na fahari yake yote ni kama ua la majani. Majani hukauka na ua lake huanguka; Bali Neno la Bwana hudumu hata milele. Na neno hilo ni neno lile jema lililohubiriwa kwenu.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 147 :12-15,19-20

(K) Msifu Bwana, ee Yerusalemu. au: Aleluya.

Msifu Bwana, Ee Yerusalemu;
Msifu Mungu wako, Ee Sayuni.
Maana ameyakaza mapingo ya malango yako,
Amewabariki wanao ndani yako. (K)

Ndiye afanyaye amani mipakani mwako,
Akushibishaye kwa unono wa ngano.
Huipeleka amri yake juu ya nchi,
Neno lake lapiga mbio sana. (K)

Humhubiri Yakobo neno lake,
Na Israeli amri zake na hukumu zake.
Hakulitendea taifa lo lote mambo kama hayo,
Wala hukumu zake hawakuzijua.
Aleluya. (K)


SHANGILIO 
Yn. 14:5

Aleluya, aleluya, 
Bwana anasema: mimi ndimi njia, na ukweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi. 
Aleluya.


INJILI 
Mk. 10:32-45

Walikuwako njiani, huku wakipanda kwenda Yerusalemu; na Yesu alikuwa akiwatangulia; wakashangaa, nao katika kufuata wakaogopa. Akawatwaa tena wale Thenashara, akaanza kuwaambia habari za mambo yatakayompata, akisema, Angalieni, tunapanda kwenda Yerusalemu; na Mwana wa Adamu atatiwa mikononi mwa wakuu wa makuhani na waandishi, nao watamhukumu afe, watamtia mikononi mwa Mataifa, nao watamdhihaki, na kumtemea mate, na kumpiga mijeledi, na kumwua; na baada ya siku tatu atafufuka.

Na Yakobo na Yohane, wana wa Zebedayo, wakamwendea, wakamwambia, Mwalimu, twataka utufanyie lo lote tutakalokuomba. Akawaambia, Mwataka niwafanyie nini? Wakamwambia, Utujalie sisi tuketi, mmoja mkono wako wa kuume, na mmoja mkono wako wa kushoto, katika utukufu wako. Yesu akawaambia, Hamjui mnaloliomba. Mwaweza kunywea kikombe ninyweacho mimi, au kubatizwa ubatizo nibatizwao mimi? Wakamwambia, Twaweza. Yesu akawaambia, Kikombe ninyweacho mimi mtakinywea, na ubatizo nibatizwao mimi mtabatizwa; lakini habari ya kuketi mkono wangu wa kuume au mkono wangu wa kushoto si langu kuwapa, ila wao watapewa waliowekewa tayari.

Hata wale kumi waliposikia wakaanza kuwakasirikia Yakobo na Yohane. Yesu akawaita,  akawaambia, Mwajua ya kuwa wale wanaohesabiwa kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha. Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu anayetaka kuwa mkubwa kwenu, atakuwa mtumishi wenu, na mtu anayetaka kuwa wa kwanza wenu, atakuwa mtumwa wa wote. Kwa maana Mwana wa Adamu naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo. 

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUMFUATA YESU BILA MASHARTI!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumanne, Mei 26, 2026, 
Juma la 8 la mwaka wa Kanisa

KUMBUKUMBU YA MTAKATIFU FILIPO NERI

1 Pet 1: 10-16;
Zab 98: 1-4;
Mk 10: 28-31


KUMFUATA YESU BILA MASHARTI!

Baadhi wameitwa kuacha mengi na kumfuata Yesu. Baadhi ya hawa wameitwa kuishi maisha ya kitawa (wakike na wakiume). Wanaacha yote ya ulimwengu na kufuata mwaliko wa Yesu wa kumfuata katika hali ya pekee. Sisi wote lakini tumeitwa “kuacha yote” na kumfuata Yesu katika hali zetu za kipekee. Kwa kuacha yote, tunaitwa kukabidhi yote, uhuru wetu na kutumikia kwa kadiri ya mpango mtakatifu wa Kristo. Hili linaweza likachukua hali mbali mbali lakini mwishoni, linahitaji daima kuacha yote.

Habari njema ni kwamba ‘kuacha yote’ si zaidi ya kuacha mitazamo yetu mibaya ya maisha na kuchagua mapenzi ya Mungu. Maisha alio tuandalia ni mazuri kuliko hata chochote tunachoweza kufikiri. Kwa kusema “hapana” kwa mapenzi yetu na kufanya vitu kwa njia zetu, ni wazi tunasema “Ndio” kufanya vitu kwa ukamilifu wa Kimungu. Hata iwe ni wito ghani wa pekee katika maisha yako, ni vizuri kukumbatia mapenzi ya Mungu. 

Tutafakari ni namna ghani mimi na wewe tupo tayari kusema “ndio” kwa Yesu bila kujali anatutaka nini. Je, upo tayari kusema ndio hata kwa kile ambacho hajakufunulia bado? Sema “ndio” leo kwa maisha yako ya baadae na Mungu atakujaza Baraka katika njia hiyo. 

Sala: Bwana, haijalishi ni nini umeniitia kufanya katika maisha, jibu langu ni “ndio”. Ninataka kukutumikia kwa moyo wote. Nisaidie niweze kuishi wito huo kwa ukarimu na mapendo. Yesu, nakuamini wewe. Amina!

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MEI 26, 2026




MASOMO YA MISA, MEI 26, 2026
JUMANNE YA 8 YA MWAKA

KUMBUKUMBU YA MTAKATIFU FILIPO NERI

SOMO 1 
1 Pet l : 10-16

Katika habari ya wokovu huo manabii walitafuta-tafuta na kuchunguza-chunguza, ambao walitabiri habari za neema itakayowafikia ninyi. Wakatafuta ni wakati upi, na wakati wa namna gani ulioonywa na Roho wa Kristo aliyekuwa ndani yao, ambaye alitanerulia kuyashuhudia mateso yatakayompata Kristo, na utukufu utakaokuwako baada ya hayo. Wakafunuliwa ya kuwa si kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili yenu walihudumu katika mambo hayo, ambayo sasa yamehubiriwa kwenu na wale waliowahubiri ninyi Injili kwa Roho Mtakatifu aliyetumwa kutoka mbinguni. Mambo hayo malaika wanatamani kuyachungulia. Kwa hiyo vifungeni viuno vya nia zenu, na kuwa na kiasi; mkiitumainia kwa utimilifu ile neema mtakayoletewa katika ufunuo wake Yesu Kristo. Kama watoto wa kutii msijifananishe na tamaa zenu za kwanza, za ujinga wenu; bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu. 


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 98 :1-4

(K) Bwana ameufunua wokovu wake.

Mwimbieni Bwana wimbo mpya,
Kwa maana ametenda mambo ya ajabu.
Mkono wa kuume wake mwenyewe,
Mkono wake mtakatifu umemtendea wokovu.

Bwana ameufunua wokovu wake,
Machoni pa mataifa ameidhihirisha haki yake.
Amezikumbuka rehema zake,
Na uaminifu wake kwa nyumba ya Israeli.

Miisho yote ya dunia imeuona
Wokovu wa Mungu wetu.
Mshangilieni Bwana, nchi yote,
Inueni sauti, imbeni kwa furaha, imbeni zaburi.


SHANGILIO 
Yn. 8 :12

Aleluya, aleluya,
Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, asema Bwana, yeye anifuataye hatakwenda gizani kamwe, bali atakuwa na nuru ya uzima.
Aleluya.


INJILI 
Mk. 10:28-31

Petro alimwambia Yesu, Tazama, sisi tumeacha vyote tukakufuata wewe. Yesu akasema, Amin, nawaambieni, Hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume, au ndugu wake, au mama, au baba, au watoto, au mashamba, kwa ajili yangu, na kwa ajili ya Injili, ila atapewa mara mia sasa wakati huu, nyumba, na ndugu waume, na ndugu wake, na. mama, na watoto na mashamba, pamoja na udhia; na katika ulimwengu ujao uzima wa milele. Lakini wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho; na wa mwisho watakuwa wa kwanza.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MAMA WA KANISA



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatatu, Mei, 25, 2026 
Juma la 8 la Mwaka .

Kumbukumbu ya Bikira Maria Mama wa Kanisa

Mwa 3:9-15,20; 
Zab 87; 
Yn 19:25-34


MAMA WA KANISA


Sherehe ya Bikira Maria Mama wa Kanisa kuanzia mwaka 2018 inaadhimishwa Jumatatu baada ya Sherehe ya Pentekoste na mwaka huu ni tarehe 20 Mei 2024. Mabadiliko haya yanapaswa kuwa tayari yamekwisha kuingizwa kwenye Kalenda za maadhimisho ya Liturujia ya Kanisa na kufanyiwa kazi tangu sasa! Ibada hii kwa Bikira Maria, itawasaidia waamini kukumbuka kwamba, maisha ya Kikristo yanafumbatwa katika Fumbo la Msalaba linaloadhimishwa katika Ekaristi Takatifu, Kanisa linapomtolea pia sifa na heshima Bikira Maria, Mama wa Mkombozi, aliyesadaka maisha yake kwa ajili ya kushiriki kikamilifu katika kazi ya ukombozi!

Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican katika Tamko lao kuhusu Fumbo la Kanisa wanafafanua kwa kina na mapana nafasi ya Bikira Maria, Mama wa Mungu katika Fumbo la Kristo na la Kanisa: tangu Agano la Kale, Fumbo la Umwilisho, Bikira Maria katika maisha ya hadharani ya Kristo Yesu, Bikira Maria baada ya Kristo Yesu kupaa mbinguni. Wanaendelea kufafanua dhamana na nafasi ya Bikira Maria katika maisha na utume wa Kanisa kama mshiriki mwaminifu wa kazi ya ukombozi, mwombezi kwa ajili ya wokovu, Bikira Maria kama mfano wa utimilifu wa Kanisa katika maisha na utakatifu wake na kwamba, Bikira Maria ni ishara na matumaini thabiti na faraja kwa taifa la Mungu linalosafiri huku Bondeni kwenye machozi!

Kwa hakika, Mapokeo ya maadhimisho ya Fumbo la maisha ya Kristo ambayo kamwe hayawezi kumtenga Bikira Maria, Mama wa Kristo na Kanisa. Bikira Maria anatambulikana kuwa ni Mama wa Wakristo ambao wamezaliwa kwake kwa njia ya fadhila ya upendo na kwamba, Bikira Maria ni Mama wa Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa kama wanavyofundisha Mtakatifu Agostino, Askofu na Mwalimu wa Kanisa pamoja na Mtakatifu Leo Mkuu. Umama wa Kristo na Kanisa ulidhihirishwa pale chini ya Msalaba, Bikira Maria alipopokea upendo wa dhati kutoka kwa Mwanaye mpendwa na Yohane kwa niaba ya wengine wote, wakawa ni wafuasi na mitume wa upendo kwa ajili ya Mama yake.

Bikira Maria aliendelea kuandamana na Kanisa katika sala wakati Mitume wakisubiria ujio wa Roho Mtakatifu. Kwa nyakati mbali mbali, waamini wamekuwa wakimheshimu na kumfanyia Ibada Bikira Maria kama: Mama wa Mitume, Mama wa waamini wa wale wote wanaozaliwa upya katika Kristo Yesu na Mama wa Kanisa kama wanavyofundisha Papa Benedikto XV pamoja na Papa Leo wa XIII. Mtakatifu Paulo VI kunako tarehe 21 Novemba 1964, Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican walipokuwa wanahitimisha Kikao cha tatu cha Mkutano huo, alitamka kwamba, Bikira Maria ni Mama wa Kanisa; yaani: ni Mama wa Wakristo wote na wachungaji wanaomkimbilia kama Mama.

Kumbe, Bikira Maria, Mama wa Kanisa anapaswa kuheshimiwa na Wakristo wote. Katika maadhimisho ya Mwaka wa Upatanisho1975, kuliadhimishwa Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya Bikira Maria, Mama wa Kanisa. Litania ya Bikira Maria wa Loreto ikaongeza heshima hii katika Litania. Majimbo mbali mbali wakaona kwamba, inafaa na kuomba Kiti Kitakatifu kuruhusu maadhimisho haya yaingizwe katika kalenda ya majimbo yao! Kutokana na kukua na hatimaye, kukomaa kwa Ibada ya Bikira Maria, Mama wa Kanisa, Baba Mtakatifu Francisko ameridhia tamko lililotolewa na Baraza la Kipapa la Ibada na Sakramenti za Kanisa kwamba, kuanzia sasa Sherehe ya Bikira Maria Mama wa Kanisa itakuwa inaadhimishwa Jumatatu baada ya Sherehe ya Pentekoste ya kila mwaka!

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MEI 25, 2026

 


MASOMO YA MISA, MEI 25, 2026
JUMATATU, JUMA LA 8 LA MWAKA

Kumbukumbu ya Bikira Maria Mama wa Kanisa


SOMO 1 
Mwa 3:9-15, 20

Baada ya Adamu kule tunda la ule mti, Bwana Mungu akamwita Adamu, akamwambia, Uko wapi? Akasema, Nalisikia sauti yako bustanini, nikaogopa kwa kuwa mimi ni uchi; nikajificha. Akasema, Ni nani aliyekuambia ya kuwa u uchi? Je! Umekula wewe matunda ya mti niliyokuagiza usiyale? Adamu akasema, Huyo mwanamke uliyenipa awe pamoja nami ndiye aliyenipa matunda ya mti huo, nikala. Bwana Mungu akamwambia mwanamke, Nini hili ulilolifanya? Mwanamke akasema, Nyoka alinidanganya, nikala. Bwana Mungu akamwambia nyoka, Kwa sababu umeyafanya hayo, umelaaniwa wewe kuliko wanyama wote, na kuliko hayawani wote walioko mwituni; kwa tumbo utakwenda, na mavumbi utakula siku zote za maisha yako; nami nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino. Adamu akamwita mkewe jina lake Hawa; kwa kuwa yeye ndiye aliye mama yao wote walio hai.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI 
Zab 87:1-7

(K) Enyi mataifa yote msifuni Bwana.

Msingi wake upo Juu ya milima mitakatifu.
Bwana ayapenda malango ya Sayuni
Kuliko maskani zote za Yakobo.
Umetajwa kwa mambo matukufu, Ee Mji wa Mungu.
(K) Enyi mataifa yote msifuni Bwana.

Nitataja Rahabu na Babeli Miongoni mwao wanaonijua.
Tazama Filisti, na Tiro, na Kushi; Huyu alizaliwa humo.
Naam, mintarafu Sayuni itasemwa,
Huyu na huyu alizaliwa humo.
Na Yeye Aliye juu Ataufanya imara.
(K) Enyi mataifa yote msifuni Bwana.

Bwana atahesabu, awaandikapo mataifa,
Huyu alizaliwa humo.
Waimbao na wachezao na waseme,
Visima vyangu vyote vimo mwako.
(K) Enyi mataifa yote msifuni Bwana.



SHANGILIO 
Zab. 147:12,15

Aleluya, aleluya,
Msifu Bwana, ee Yerusalemu, huipeleka amri yake juu ya nchi.
Aleluya.


INJILI
Yn 19:25-34

Penye msalaba wake Yesu walikuwa wamesimama mamaye, na umbu la mamaye, Mariamu wa Klopa, na Mariamu Magdalene. Basi Yesu alipomwona mama yake, na yule mwanafunzi aliyempenda amesimama karibu, alimwambia mama yake, Mama, tazama, mwanao. Kisha akamwambia yule mwanafunzi, Tazama, mama yako. Na tangu saa ile mwanafunzi yule akamchukua nyumbani kwake. Baada ya hayo Yesu, hali akijua ya kuwa yote yamekwisha kumalizika ili andiko litimizwe, akasema, Naona kiu. Kulikuwako huko chombo kimejaa siki; basi wakatia sifongo iliyojaa siki juu ya ufito wa hisopo, wakampelekea kinywani. Basi Yesu alipokwisha kuipokea ile siki, alisema, Imekwisha. Akainama kichwa, akaisalimu roho yake. Basi Wayahudi, kwa sababu ni Maandalio, miili isikae juu ya misalaba siku ya sabato, (maana sabato ile ilikuwa siku kubwa), walimwomba Pilato miguu yao ivunjwe, wakaondolewe. Basi askari wakaenda, wakamvunja miguu wa kwanza, na wa pili, aliyesulibiwa pamoja naye. Lakini walipomjia Yesu na kuona ya kuwa amekwisha kufa, hawakumvunja miguu; lakini askari mmojawapo alimchoma ubavu kwa mkuki; na mara ikatoka damu na maji.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo. 

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

WEKA ULIMWENGU KWENYE MOTO WA MAPENDO YA MUNGU



“MBEGU ZA UZIMA”
Tafakari ya Pasaka
Jumapili, Mei 24, 2026

Sherehe ya Pentekoste

Mdo 2: 1-11;
Zab, 104: 1, 24, 29-31, 34;
1 Kor 12:3-7, 12-13 au Rom 8:8-17 
Yn 20:19-23 au Yn 14:15-16, 23-26


WEKA ULIMWENGU KWENYE MOTO
WA MAPENDO YA MUNGU

‘Pentekoste’ ni neno la Kigiriki lenye maana ya “Hamsini”. Wakristo wanasherekea sherehe hii siku hamsini baada ya Pasaka (Mdo 2). Ikiwa ni tamaduni iliyotoka Agano la Kale, yenye maana ya “sikukuu ya mavuno” katika siku ya hamsini baada ya “Pasaka ya Wayahudi” (Kut. 23:16, Hes. 28:26-31, Kum. 16:19-21). Siku hii ilikuja kuwa muhimu kwa Wakristo kwasababu, majuma saba baada ya ufufuko wa Yesu, wakati wa sikukuu ya mavuno ya Wayahudi, Roho Mtakatifu aliwashukia wafuasi wa kwanza wa Yesu, akiwapa nguvu na uwezo wakumtangaza Kristo na kuwakusanya pamoja kama Kanisa. Kama Wayahudi walivyokuwa wakitoa matunda ya mazao yao ya kwanza, wakijiandaa kwa mvua kwa ajili ya mazao yajayo; wafuasi, mazao ya kwanza ya utume wa Kristo yaliyoiva, wanapokea mvua ya Roho Mtakatifu, Roho atakaye wafanya wakue na kuwa mazao na mbegu kwa ajili ya vizazi vijavyo. Katika Siku hii, umoja wa watu wa Mungu kama Kanisa, kwa nguvu ya Roho Mtakatifu ulianza.

Roho Mtakatifu alitumwa kama Yesu alivyo ahidi, ili kukamilisha kilele cha ufunuo wa upendo wa Mungu. Roho Mtakatifu hajiweki kwa Wayahudi peke yao, bali anafunua upendo wa Mungu usio na mipaka kwa watu wote, akileta Baraka, matunda katika nchi ambayo ilikuwa imelaaniwa kipindi cha Adamu na Eva. Lugha iliyoleta mtafaruku nakutoelewana katika mnara wa Babeli, inakuwa kiunganisho kikuu kwa njia ya Roho Mtakatifu. Ukosefu wa urafiki na umoja na Mungu uliopotea katika Edeni, Roho Mtakatifu anaurudisha tena kwa kuwa na Kanisa daima.

Pentekoste tunasheherekea kazi na uwepo wa Roho Mtakatifu ndani yetu kama waumini na Kanisa. Mungu amemimina juu yenu wote Roho Mtakatifu (Rom 8:1-11) na tunapaswa kuishi ndani ya uwepo wa nguvu ya Roho wa Mungu. Roho Mtakatifu anatusaidia kumkiri Yesu kwamba ni Bwana wetu (1 Kor 12:3), akituwezesha kumtumikia Mungu (1 Kor 12:4-11), akituunganisha pamoja kama Mwili wa Kristu (1 Kor 12:12-13), anatusaidia kusali (Rom 8:26), anatuombea ndani ya Mungu Baba (Rom 8:27). Roho Mtakatifu anatuongoza (Gal 5:25) na Roho Mtakatifu anatusaidia tuishi kama Yesu (Gal 5:22-23). 

Baba Mtakatifu Fransisko anamuita Roho Mtakatifu “Upendo” unaokosekana ndani ya familia zetu na Ulimwenguni. Katika ujumbe wake ndani ya “Amoris Laetitia”, “Furaha ya Upendo” anamuonesha Roho Mtakatifu kama mfano halisi wa Familia za Kikristo na Kanisa. 

“Upendo ndani ya familia ya Kimungu, ni Roho Mtakatifu….tunaweza kutambua upendo wa Mungu ndani ya Roho Mtakatifu….kwa njia ya Kanisa, ndoa na familia zinapokea neema za Roho Mtakatifu kutoka kwa Kristo, ili tuweze kutoa ushuhuda wa Injili ya Upendo wa Mungu.”

Baba Mtakatifu anazialika familia zote za Kikristo “kila wakati kualika usaidizi wa Roho Mtakatifu anayetakatifuza umoja wenu, ili neema zake ziweze kutawala katika kila jambo mnalokutana nalo”. Pia anasema, bila Roho Mtakatifu umoja wa familia za Kikristo hauwezekani. “hakuna hata moja kati ya haya, litakalo wezekana bila kusali kwa Roho Mtakatifu ili amimine neema zake, nguvu zake na moto wa Roho, kutufanya wake, kutuongoza na kubadili mapendo yetu kwa kila hali”

Leo tunaitwa, tuweze kujali kazi ya Roho Mtakatifu katika maisha yetu binafsi, familia, jumuiya na Kanisa zima. Je sisi ni vyombo vya kazi ya Roho Mtakatifu? Je, tumekuwa wasikivu wakati Roho Mtakatifu anapotuongoza? Matunda ya Roho Mtakatifu (Upendo, furaha, Amani nk.) yanakuwa ndani mwangu? Sisi wote tunaishi ndani ya uwepo wa nguvu ya Roho Mtakatifu lakini katika viwango tofauti. Tunazuiwa na uoga wetu, dhambi zetu, Mapungufu yetu na uharibifu wetu wa kila siku unaotufanya tushindwe kuhisi uwepo wa zawadi ya Mungu ya Upendo ‘Roho Mtakatifu’. Pentekoste inatupa tena wakati wa kuhisi moto wa Roho Mtakatifu na kuuweka Ulimwengu kwenye moto wa upendo wa Mungu.

Sala: Nivuvie nguvu ya Roho Mtakatifu Bwana, ili mawazo yangu yaweze kuwa matakatifu. Nivuvie pia nguvu ya Roho Mtakatifu ili kazi yangu iweze kuwa takatifu. Gusa moyo wangu Roho Mtakatifu, niweze kupenda vile vitakatifu tu. Nipe ujasiri Roho Mtakatifu ili niweze kulinda kila kilicho kitakatifu. Nilinde Roho Mtakatifu, ili niweze kuwa Mtakatifu daima. Roho Mtakatifu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JUMAPILI, MEI 24, 2026



MASOMO YA MISA, JUMAPILI, MEI 24, 2026
SHEREHE YA PENTEKOSTE


SOMO 1 
Mdo. 2:1-11

Hata ilipotimia siku ya Pentekoste walikuwako wote mahali pamoja. Kukaja ghafula toka mbinguni uvumi kama uvumi wa upepo wa nguvu ukienda kasi, ukaijaza nyumba yote waliyokuwa wameketi. Kukawatokea ndimi zilizogawanyikana, kama ndimi za moto uliowakalia kila mmoja wao. Wote wakajazwa Roho Mtakatifu, wakaanza kusema kwa lugha nyingine, kama Roho alivyowajalia kutamka.

Na walikuwako Yerusalemu Wayahudi wakikaa, watu watauwa, watu wa kila taifa chini ya mbingu. Basi sauti hii iliposikiwa makutano walikutanika, wakashikwa na fadhaa, kwa kuwa kila mmoja aliwasikia wakisema kwa lugha yake mwenyewe. Wakashangaa wote, wakastaajabu wakiambiana, Tazama, hawa wote wasemao si Wagalilaya? Imekuwaje basi sisi kusikia kila mtu lugha yetu tuliyozaliwa nayo? Waparthi na Wamedi na Waelani, nao wakaao Mesopotamia, Uyahudi na Kapadokia, Ponto na Asia, Frigia na Pamfilia, Misri na pande za Libia karibu na Kirene, na wageni watokao Rumi, Wayahudi na waongofu, Wakrete na Waarabu; tunawasikia hawa wakisema kwa lugha zetu matendo makuu ya Mungu.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATI KATI 
Zab. 104:1, 24, 29-31, 34, (K) 30

(K) Waipeleka roho yako, Ee Bwana, Nawe waufanya upya uso wa nchi. au: Aleluya.

Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana,
Wewe, Bwana, Mungu wangu,
Umejifanya mkuu sana;
Ee Bwana, jinsi yalivyo mengi matendo yako!
Dunia imejaa mali zako. (K)

Waiondoa pumzi yao, wanakufa,
Na kuyarudia mavumbi yao,
Waipeleka roho yako, wanaumbwa,
Nawe waufanya upya uso wa nchi. (K)

Utukufu wa Bwana na udumu milele;
Bwana na ayafurahie matendo yake.
Kutafakari kwangu na kuwe kutamu kwake;
Mimi nitamfurahia Bwana. (K)


SOMO 2 
1 Kor. 12 :3-7, 12-13

Hawezi mtu kusema, Yesu ni Bwana, isipokuwa katika Roho Mtakatifu. Basi pana tofauti za karama; bali Roho ni yeye yule. Tena pana tofauti za huduma, na Bwana ni yeye yule. Kisha pana tofauti za kutenda kazi, bali Mungu ni yeye yule azitendaye kazi zote katika wote. Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana.

Maana kama vile mwili ni mmoja, nao una viungo vingi, na viungo vyote vya mwili ule, navyo ni vingi, ni mwili mmoja; vivyo hivyo na Kristo. Kwa maana katika Roho mmoja sisi sote tulibatizwa kuwa mwili mmoja, kwamba tu Wayahudi, au kwamba tu Wayunani; ikiwa tu watumwa au ikiwa tu huru; nasi sote tulinyweshwa Roho mmoja.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


SHANGILIO

Aleluya, aleluya, Uje Roho Mtakatifu, uzienee nyoyo za waamini wako uwatie mapendo yako. Aleluya.


INJILI 
Yn. 20 :19-23

Ikawa jioni, siku ile ya kwanza ya juma, pale walipokuwapo wanafunzi, milango imefungwa kwa hofu ya Wayahudi; akaja Yesu, akasimama katikati, akawaambia, Amani iwe kwenu. Naye akiisha kusema hayo, akawaonyesha mikono yake na ubavu wake. Basi wale wanafunzi wakafurahi walipomwona Bwana.

Basi Yesu akawaambia tena, Amani iwe kwenu; kama Baba alivyonituma mimi, mimi nami nawapeleka ninyi. Naye akiisha kusema hayo, akawavuvia, akawaambia, Pokeeni Roho Mtakatifu. Wo wote mtakaowaondolea dhambi, wameondolewa; na wo wote mtakaowafungia dhambi, wamefungiwa.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUMFAHAMU YESU!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Pasaka
Jumamosi, Mei 23, 2026 
Juma la 7 la Pasaka


Mdo 28: 16-20, 30-31;
Zab 11: 4-5, 7 (R. 7);
Yn 21: 20-25


KUMFAHAMU YESU!

Jaribu kufikiria ni mitizamo aliokuwa nayo Mama Bikira Maria kuhusu Mwanae. Yeye kama Mama yake, atakuwa aliona mambo mengi na kuelewa nyakati nyingi za maisha yake ambazo nyingine hatuzifahamu. Yeye alikuwa akimtizama akikuwa mwaka baada ya mwaka. Alikuwa akimtizama akiongea na watu na kushirikiana na wengine. Atakuwa alitambau alikuwa akijiandaa kwa utume wake. Na atakuwa ameshuhudia nyakati nyingi za utume wake Mtakatifu na maisha yake yote ambayo hayaja andikwa katika Injili. 

Maneno ya mwisho ya Injili ya Yohane yanatupa hali Fulani ya kutafakari zaidi. Mambo yote tunayo fahamu kuhusu maisha ya Yesu, yanapatikana katika Injili, lakini inawezekanaje Injili hizi kuweza kuelezea maisha yote ya Yesu, kila kitu alichofanya? Ni hakika kwamba haziwezi. Kufanya hivyo kama Yohane alivyosema, “nadhani hata ulimwengu usingetosha kwa vile vitabu vitakavyoandikwa.”

Injili inatuonesha ni kwa jinsi ghani tunamfahamu Yesu kidogo sana. Inapaswa pia kufungua akili kwamba tunapaswa kumfahamu Yesu zaidi. Tunapaswa kutamani kumfahamu zaidi na zaidi. Na hii itatufunga tukazane kumtafuta Kristo zaidi na zaidi kwa ndani. Pia, ingawaje mambo mengine ya maisha ya Yesu hayaja andikwa, haina maana kwamba hatuwezi kumfahamu Yesu, tunaweza kumfahamu Yesu Mwenyewe kwa yale yote yaliyo katika maandiko Matakatifu. Hakika tutakutana naye. Tutakutana na Neno wa Mungu mwenyewe akiishi katika Maandiko na kukutana naye huku tunapewa yote tunayo hitaji. 

Tafakari leo, ni kwa jinsi ghani unamfahamu Yesu. Je, una muda wakusoma Maandiko Matakatifu na kuya tafakari? Je, unamtafuta kila siku na kutamani kumfahamu na kumpenda? Je, yeye yupo ndani yako na unajitahidi kujiweka mbele yake kila siku? Kama jibu ya moja wapo la maswali haya ni “HAPANA” basi hii ni siku nzuri ya kuanza tena kujituma katika kusoma maandiko Matakatifu, neno la Mungu. 

Sala: Bwana, ninaweza nisiwe nafahamu yote kuhusu maisha yako, lakini natamani kukufahamu. Ninatamani kukutana na wewe kila siku, kukupenda wewe na kukufahamu. Nisaidie nizame ndani zaidi katika uhusiano wangu na wewe. Yesu, nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MEI 23, 2026




MASOMO YA MISA, MEI 23, 2026
JUMAMOSI YA 7 YA PASAKA

SOMO 1
Mdo. 28 :16-20, 30-31

Tulipoingia Rumi Paulo alipewa ruhusa kukaa kwake mwenyewe pamoja na askari aliyemlinda.

Ikawa baada ya siku tatu akawaita wakuu wa Wayahudi wakutane; hata walipokutanika akawaambia, Ndugu zangu, ingawa sikufanya neno kinyume cha watu wetu wala neno lililopingamana na desturi za baba zetu, nalitiwa katika mikono ya Warumi, hali nimefungwa, tokea Yerusalemu. Na hao walipokwisha kuniuliza-uliza walitaka kunifungua, kwa maana hapakuwa na sababu yo yote kwangu ya kuuawa. Lakini Wayahudi walipotoa hoja juu ya shauri hili nalishurutishwa kutaka rufani kwa Kaisari. Si kwamba nalikuwa na neno la kuwashitaki watu wa taifa langu. Basi kwa ajili ya hayo, nimewaita mje kunitazama na kusema nami; kwa maana nimefungwa kwa mnyororo huu kwa ajili ya tumaini la Israeli.

Akakaa muda wa miaka miwlli mizima katika nyumba yake aliyokuwa ameipanga, akawakaribi sha watu wote waliokuwa wakimwendea, akihubiri habari za ufalme wa Mungu, na kuyafundisha mambo ya Bwana Yesu Kristo, kwa ujasiri mwingi, asikatazwe na mtu.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 11 :4-5, 7 (K) 7

(K) Wanyofu wa moyo wauona uso wake, Ee Bwana. au: Aleluya.

Bwana yu katika hekalu lake takatifu.
Bwana ambaye kiti chake kiko mbinguni,
Macho yake yanaangalia;
Kope zake zinawajaribu wanadamu. (K)

Bwana humjaribu mwenye haki;
Bali nafsi yake humchukia asiye haki,
Na mwenye kupenda udhalimu. (K)

Kwa kuwa Bwana ndiye mwenye haki,
Apenda matendo ya haki,
Wanyofu wa moyo watamwona uso wake. (K)


SHANGILIO 
Mt. 28 :19-20

Aleluya, aleluya, 
Enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi. Mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, Hata ukamilifu wa dahari. 
Aleluya.


INJILI 
Yn. 21:20-25

Petro aligeuka akamwona yule mwanafunzi aliyependwa na Yesu anafuata; (ndiye huyo aliyeegama kifuani pake wakati wa kula chakula cha jioni, akasema, Bwana, ni nani akusalitiye?). Basi Petro akamwona huyo, akamwambia Yesu, Bwana, na huyu je? Yesu akamwambia, Ikiwa nataka huyu akae hata nijapo, imekupasaje wewe? Wewe unifuate mimi.

Basi neno hilo lilienea katikati ya ndugu ya kwamba mwanafunzi yule hafi. Walakini Yesu hakumwambia ya kwamba hafi; bali, Ikiwa nataka huyu akae hata nijapo, imekupasaje wewe? Huyu ndiye yule mwanafunzi ayashuhudiaye haya, na aliyeyaandika haya; nasi twajua ya kuwa ushuhuda wake ni kweli. Kuna na mambo mengine mengi aliyoyafanya Yesu; ambayo yakiandikwa moja moja, nadhani hata ulimwengu usingetosha kwa vile vitabu vitakavyoandikwa.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo. 


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.