Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MPENDE ADUI YAKO!




ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumanne, Juni 16, 2026,
Juma la 11 la Mwaka


MPENDE ADUI YAKO!


Katika Injili ya Leo Yesu anatupa changamoto kwa kutupa kazi ngumu, anawaambia wafuasi wake “wapendeni adui zenu na waombeeni wanao wadhulumu”. Kwa njia hii anatualika sisi tuwe kama yeye, kuwa sura yake kwakuwaombea wote, kuwapenda wote kama yeye alivyofanya. “kwani Mungu huwapa watu wote jua lake, wazuri na wabaya, mvua ya Mungu huwanyeshea walio na haki na wasio na haki”.

Injili inataka kutuonesha sisi kwamba, Mungu anafunuliwa kila wakati na kwakupitia watu wengi. Ni jukumu letu binafsi na kama jumuiya kuwa tayari, kuwa wazi ili kumuona Mungu tunapokutana na hali mbali mbali za Kimungu katika maisha yetu. Mungu wetu ni Mungu wa nafsi. Kila mara sura yake hubadilika ndani yetu na kutufanya sisi tuwe watimilifu.

Tutafakari juu ya wale wote ambao tunapata wakati mgumu kuwapenda. Anaweza kuwa ndugu wa familia, mmoja wa wafanyakazi wenzako, jirani yako au mmoja ya mtu ambaye mlikosana zamani na humjapatana. Ukishamtambua huyo mtu, jiulize kama unamuombea, ulisha Sali kumuombea? Je ulisha tumia muda Fulani kusali na kumwombea? Unasali ili Mungu awamiminie huruma yake na neema yake? Inaweza kuwa vigumu kuonesha upendo na huruma kwao, lakini sio vigumu kusali kwa ajili yao. Kusali kwa ajili ya walio tuumiza ni ufunguo wa kumruhusu Mungu alete mapendo ya kweli na hali ya kuwajali katika mioyo yetu. Ni sehemu ya kumruhusu Mungu abadili hisia zetu juu yao ili tusiwe tena na chuki juu yao na kuwachukia. Jiweke katika hali ya kusali na kumuombea mtu ambae unamchukia sana. Sala hii haina maana itabadili jambo hili kwa usiku mmoja, lakini kama utajikita katika sala ya namna hii kila siku, taratibu Mungu atabadilisha hali yako ya Moyo na kukuondolea mzigo wa hasira na maumivu ulio umizwa ambayo yanaweza kukuweka mbali na upendo wake ambao anataka uwe nao kwa watu wake.

Sala: Bwana, nina Sali kwa ajili ya mtu ambaye unapenda mimi nimwombee. Nisaidie niweze kuwapenda watu wote na zaidi sana kuwapenda wale ambao naona vigumu kuwapenda. Badilisha hisia na mtazamo wangu juu yao na nisaidie niweze kuwa huru kutoka katika kila aina ya hasira. Bwana, naomba unisaidie nikutane na wewe ili niweze kuwa kama wewe. Yesu, nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JUNI 16, 2026




MASOMO YA MISA, JUNI 16, 2026
JUMANNE, JUMA LA 11 LA MWAKA


SOMO 1
1 Fal. 21:17-29

Neno la Bwana likamjia Eliya Mtishbi, kusema, Ondoka, ushuke, ukutane na Ahabu mfalme wa Israeli, akaaye katika Samaria; yuko katika shamba la mizabibu la Nabothi, ndiko alikoshukuia ili alitamalaki. Ukamwambie, ukisema, Bwan aasema hivi, Je! Umeua, ukatamalaki? Nawe utamwambia, kusema, Bwana asema hivi, mahali pale mbwa walipoiramba damu ya Nabothi, mbwa watairamba na damu yako, naam, damu yako.

Ahabu akamwambia Eliya, Je! Umenipata, ewe adui yangu? Akamwambia, Nimekupata, kwa sababu umejiuza utende yaliyo mabaya machoni pa Bwana. Angalia, nitaleta mabaya juu yako; nami nitakuangamiza kabisa, nitamkatia Ahabu kila mume, aliyefungwa na aliyeachwa katika Israeli.

Kisha nitaifanya nyumba yako iwe kama nyumba ya Yeroboamu mwana wa Nebari, na kama nyumba ya Baasha mwana wa Ahiya, kwa ajili ya chukizo ulilonichukiza, hata kunighadhibisha, ukawakosesha Israeli. Tena Bwana alinena habari za Yezebeli, akisema, Mbwa watamla Yezebeli katika kiwanja cha Yezreeli. Mtu wa nyumba ya Ahabu afanye mjini, mbwa watamla, na yeye afaye mashamba ndege wa angani watamla.

Lakini hapakuwa na mtu kama Ahabu, aliyejiuza atende maovu machoni pa Bwana, ambaye Yezebeli mkewe alimchochea. Akachukiza mno, kwa kuzifuata sanamu sawasawa na yote waliyoyafanya Waamori, Bwana aliowafukuza mbele ya wana wa Israeli.

Ikawa, Ahabu alipoyasikia maneno hayo, akayararua mavazi yake, akavaa magunia mwilini mwake, akafunga, akajilaza juu ya magunia, akaenda kwa upole. Neno la Bwana likaja kwa Eliya Mtishbi, kusema, Huoni jinsi Ahabu alivyojidhili mbele yangu? Basi kwa sababu amejidhili mbele yangu, sitayaleta yale mabaya katik asiku zake; ila katika siku za mwanawe nitayaleta mabaya hayo juu ya nyumba yake.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 51:1-4, 9, 15 (K) 1


(K) Ee Mungu uturehemu uyafute makosa yetu.

Ee Mungu unirehemu, sawasawa na fadhili zako.
Kiasi cha wingi wa rehema zako,
Uyafute makosa yangu.
Unioshe kabisa na uovu wangu,
Unitakase dhambi zangu. (K)

Maana nimejua mimi makosa yangu,
Na dhambi yangu i mbele yangu daima.
Nimekutenda dhambi Wewe peke yako. (K)

Usitiri uso wako usitazame dhambi zangu,
Uzifute hatia zangu zote.
Ee Bwana, uifumbue midomo yangu,
Na kinywa hcangu kitazinena sifa zako. (K)


SHANGILIO
Yak. 1:21

Aleluya, aleluya.
Pokeeni kwa upole neno la mungu lililopandwa ndani, liwezalo kuiokoa roho zenu.
Aleluya.


INJILI
Mt. 5:43 – 48

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, pendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi; ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki. Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyk, mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru; je! Nao hawafanyi yayo hayo? Tena mkiwaamkia ndugu zenu tu, mnatenda tendo gani la ziada? Hata watu wa mataifa, je! Nao hawafanyi kama hayo? Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUUSHINDA UOVU KWA WEMA!




ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatatu, Juni 15, 2026.
Juma la 11 la Mwaka


KUUSHINDA UOVU KWA WEMA!

Injili ya leo inaelezea jinsi ya kupita kutoka kwenye haki ya zamani ya Mafarisayo (Mt 5: 20) kwenda kwenye haki mpya ya Ufalme wa Mungu ambayo inapaswa izidi zaidi na kupita haki ya Mafarisayo. (Mt 5: 20). Inaelezea ni jinsi gani ya kupanda mlima na kwenda kwenye zile heri nane, ambapo Yesu alitangaza sheria mpya ya Upendo. Kilele chake kinaelezewa katika mstari mmoja tuu, “kuweni wakamilifu kama Baba yenu wa Mbinguni alivyo mkamilifu” (Mt 5: 48)

Kisasi kinadai “jicho kwa jicho, jino kwa jino”. Yesu anafundisha tukitendewa ovu turudishe wema, tukifanya kinyume chake uovu utaibuka na kutawala na hatutajua nini cha kufanya zaidi. Kuwa waaminifu kwa mafundisho ya Yesu, Paulo anaandika kwenye barua yake kwa Warumi “usilipe ovu kwa ovu, badala yake nuiya kuwatendea watu wote mema”. (Rum 12: 17-21). Njia nzuri ya kukabiliana na uovu, nikumwachia Mungu atawale mwenyewe!

Pengine tujiulize sisi wenyewe, hivi nilisha wakwa na hasira kubwa ndani mwangu na nikatamani kulipa kisasi cha “jicho kwa jicho, jino kwa jino”? Nilifanya nini ili kukishinda? Je, maisha katika familia zetu, jumuiya zetu za kitawa, au popote ninapokaa, yanalijenga kanisa na sisi wenyewe katika hali ya upendo ambao Yesu anaeleza leo katika Injili? Je mimi sio mwanzilishi wa fujo na migogoro katika jumuiya au familia yangu? Je, furaha yangu inapatakana pale ninapo waona ndugu au jamaa hawana Amani? Je, ninafurahi ninapoona wenzangu wanafurahi? Au ninatafuta mbinu za kuzima Amani na furaha yao? Je, umekuwa chanzo chakuleta mashindano pale pasipo hitaji mashindo, nakuvuruga upendo na Amani iliyokuwepo? Haya ni maswali ambayo sisi wenyewe tunaweza tusitambue kama tumeyatenda katika hali zetu za maisha kama tutayaangalia kwa haraka haraka bila kutafakari na kujitafiti. Amani inaletwa na sisi wenyewe katika mazingira yetu, Amani na upendo iwe ndio wimbo wa matendo yetu katika maisha yetu. Kujikubali na kuwapokea wengine kwa furaha bila kisasi ni kujenga ufalme wa Mungu kati yetu.

Sala: Bwana, nisaidie niweze kuiga huruma yako na hali yako ya kusamehe. Nisaidie niweze kuwasamehe wale walio niumiza mimi na nisaidie niweze kuwapenda. Yesu, nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JUNI 15, 2026




MASOMO YA MISA, JUNI 15, 2026
JUMATATU, JUMA LA 11 LA MWAKA

SOMO 1
1 Fal. 21:1-16

Nabothi Myezreeli alikuwa na shamba la mizabibu katika Yezreeli, karibu na nyumba ya kifalme ya Ahabu mfalme wa Samaria. Ahabu akasema na Nabothi, akamwambia, Nipe shamba lako la mizabibu nilifanye shamba la mboga, maana ni karibu na nyumba yangu; nami nitakupa badala yake shamba la mizabibu lililo zuri zaidi; au ukipenda, nitakupa fedha sawasawa na thamani yake. Nabothi akamwambia Ahabu, Bwana apishe mbali nikupe urithi wa baba zangu.

Basi Ahabu akaenda nyumbani kwake, ana moyo mzito, tena amekasirika, kwa sababu ya neno lile aliloambiwa na Nabothi Myezreeli, akisema, Sitakupa urithi wa baba zangu. Akajilaza kitandani pake, akageuza uso wake, akakataa kula. Lakini Yezebeli mkewe akamwendea, akamwambia, Kwa nini roho yako ina huzuni hata usile chakula? Akamwambia, Kwa sababu nimesema na Nabothi Myezreeli, nikamwambia, Unipe shamba lako la mizabibu kwa fedha, au, ukipenda, nitakupa shamba la mizabibu lingine badala yake. Akajibu, Sitakupa shamba langu la mizabibu.

Yezebeli mkewe akamwambia, Je! Sasa wewe unaumiliki ufalme wa Israeli? Ondoka, ule chakula, moyo wako ufurahi; mimi nitakupa shamba la mizabibu la Nabothi Myezreeli.

Basi, akaandika nyaraka kwa jina la Ahabu, akazitia muhuri yake, akazipeleka zile nyaraka kwa wazee, na kwa watu wenye nguvu waliokuwa katika mji wake, waliokaa pamoja na Nabothi. Akaandika katika zile nyaraka, akasema, Pigeni mbiu ya watu kufunga, mkaweke Nabothi juu mbele ya watu; mkainue watu wawili, watu wasiofaa, ili wamshitaki, na kumshuhudia, kunena, Umemtukana Mungu na mfalme. Kisha mchukueni nje, mkampige kwa mawe, ili afe.

Wale wazee wa mji wake, na walio wenye nguvu waliokaa mjini mwake, wakafanya kama Yezebeli alivyowaagiza, kama ailivyoandikwa katika nyaraka alizowapelekea. Wakapiga mbiu ya watu kufunga, wakamweka Nabothi juu mbele ya watu. Na hao watu wawili, watu wasiofaa, wakaingia, wakaketi mbele yake; wale watu wasiofaa wakamshuhudia Nabothi mbele ya watu, wakasema, Nabothi amemtukana Mungu na mfalme. Ndipo wakamchukua nje ya mji, wakampiga kwa mawe hata akafa.

Wakampelekea Yezebeli habari, wakasema, Nabothi amepigwa kwa mawe, amekufa. Ikawa Yezebeli aliposikia ya kwamba Nabothi amepigwa kwa mawe na kufa, Yezebeli akamwambia Ahabu, Inuka, ulitamalaki shamba la mizabibu la Nabothi Myezreeli, alilokataa kukupa kwa fedha, maana Nabothi hako hai, lakini amekufa. Ikawa Ahabu aliposikia ya kwamba Nabothi amekufa, akaondoka, alitelemkie shamba la mizabibu la Nabothi Myezreeli, ili alitamalaki.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 5:2-3, 5-7 (K) 2

(K) Uisikie sauti ya kilio changu, ee Bwana.

Uisikie sauti ya kilio changu,
Ee Mfalme wangu na Mungu wangu,
Kwa maana Wewe ndiwe nikuombaye.
Bwana, asubuhi utaisikia sauti yangu,
Asubuhi nitakupangia dua yangu na kutazamia. (K)

Wajivunao hawatasimama mbele za macho yako;
Unawachukia wote watendao ubatili.
Utawaharibu wasemao uongo;
Bwana humzira mwuaji na mwenye hila. (K)

Bali mimi, kwa wingi wa fadhili zako,
Na kusujudu kwa kicho,
Nikielekea hekalu lako takatifu. (K)



SHANGILIO
Kol. 3:16, 17

Aleluya, aleluya,
Neno la Kristu likae kwa wingi ndani yenu katika hekima yote;
Mkimshukuru Mungu Baba kwa Yeye.
Aleluya.



INJILI
Mt. 5:38 – 42

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Mmesikia kwamba imenenwa Jicho kwa jicho, na jino kwa jino; lakini mimi nawaambia, Msishindane na mtu mwovu; lakini mtu akupigaye shavu la kuume, mgeuzie na la pili. Na mtu atakaye kukushitaki na kuitwaa kanzu yako, mwachie na joho pia. Na mtu atakayekulazimisha mwendo wa maili moja, nenda naye mbili. Akuombaye, mpe; naye atakaye kukopa kwako, usimpe kisogo.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MUNGU ALIYE NA MSIMAMO NA MWENYE HURUMA





ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumapili, Juni 14, 2026
Juma la 11 la Mwaka


Kut. 19:2-6; 
Rum. 5:6-11; 
Mt. 9:36-10:8


MUNGU ALIYE NA MSIMAMO NA MWENYE HURUMA

Kwenye Injili ya Jumapili hii, Yesu alipowaoona umati wa watu aliwaonea huruma. Walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji au kiongozi. Jumapili hii pia twaadhimisha ukumbusho wa mababa wote. Basi nawatakieni mababa wote heri na mafanikio mema kwa siku kuu yao na tunawaombea wote, walio karibu na wale walio mbali, pamoja na kuwakumbuka wale waliotuacha. Kwa njia ya pekee tuwaombee akina baba kwenye parokia zetu. Nitaanza mahubiri haya kwa hadhithi moja. Kwenye familia mmoja kulikuwa na mtoto mvulana aliyekuwa aliyekuwa na tabia ya kutotii amri za kinyumbani. Basi siku moja baba yule akamwita mtoto wake akamwambia: wakati utakayevunja amri tena nitakufungia nje kwenye ghala. Punde si punde, yule mtoto akavunja amri tena. Ndipo babaye akampeleka mtoto ghalani na kumfungia mle. Baada ya kufanya hivyo baba akahuzunika asile au kunywa chochote. Ndipo mama akamwambia, mimi naelewa vile unavyofikiria. Nakusihi usimtoe mtoto kutoka ghanani, kwa sababu ukimtoa ataendelea kutotii amri zako. Hatakuheshimu kamwe. Baba alifikiria kuelewa kwamba mama amesema hakika. Mwishowe yule baba akamwonea mwanae huruma, na badala ya kumfungulia akachukua blanketi na mikate ya chapati na akaenda kule ghalani kulala naye usiku huo.

Masomo ya Jumapili hii hasa yatufumbulia Mungu aliye kama yule baba kwenye hadithi kwa ajili ya msimamo wake na pia huruma wake.Kwenye Somo la Kwanza, Mungu Musa anatangaza ujumber wa Mungu kwa Waisraeli. “Ikiwa mtasikiliza sauti yangu na kufuata agano langu mtakuwa watu wangu wa maana sana.” Mungu ana msimamo, na anatuita tumsikilize na kuzijali ahadi tulioweka naye wakati wa Ubatizo wetu. Mungu angetaka tuseme ukweli, tuwaheshimu wazazi wetu na tuhudhurie Misa Jumapili. Lakini badala ya kumsikiliza Mungu tunasikiliza sauti zingine. Wakati tuangukapo Mungu hutuonyesha kwamba anamsimamo, kwa sababu angetaku kuturudisha kwenye njia ya kweli na katika neema yake. Mtk Paulo kwenye Somo la Pili anatuonyesha kwamba wakati tulikuwa bado katika maasi yetu na Mungu, Mungu alituma Mwanae kutukomboa. Kama vile tunasikia kwenye Injili, Yesu aliona umati wa watu wakiwa na ulegevu wa kimwili na wa kiroho. Walikuwa kama kondoo bila mchungaji na bila kujua jinsi wangejipatia chakula cha kiroho. Tungesema kwamba barani Afrika twajikuta katika hali kama ile ya wakati wa Yesu. Hivi leo twaendelea kuvunja amri za Mungu na kutoitii Kanisa kama yule mtoto kwenye hadithi. Lakini Mungu katika Mwanae Yesu anatuonyesha msimamo wake na pia ana huruma. Anakuja kwetu kama yule baba alifanya kutuonyesha huruma wake na kutualika turudi katika neema yake. 

Ujumbe: 
1) Mungu ana msimamo na huruma kama yule baba kwenye hadithi; 
2) Mungu huzingatia tuisikilize sauti yake na sio sauti zingine; 
3) Wakati tulio katika maasi, Mungu hutuma Mwanae kama mchungaji kuturudisha katika neema yake.



Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUNI 14, 2026




MASOMO YA MISA, JUNI 14, 2026
JUMAPILI, JUMA LA 11 LA MWAKA


SOMO 1 
Kut. 19 :2-6

Waisraeli walipokuwa wameondoka Refidimu na kufika jangwa la Sinai, wakatua katika lile jangwa; wakapiga kambi huko wakiukabili mlima. Musa akapanda kwa Mungu, na Bwana akamwita toka mlima ule, akisema, Utawaambia nyumba ya Yakobo, na kuwaarifu wana wa Israeli, maneno haya: Mmeona jinsi nilivyowatendea Wamisri, na jinsi nilivyowachukua ninyi juu ya mbawa za tai, nikawaleta ninyi kwangu mimi. Sasa basi ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli, na kulishika agano langu, hapo ndipo mtakapokuwa tunu kwangu kuliko makabila yote ya watu; maana dunia yote pia ni mali yangu, nanyi mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani, na taifa takatifu.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 100 :2-3, 5 (K) 3

(K) Tu watu wake, na kondoo wa malisho yake.

Mtumikieni Bwana kwa furaha;
Njoni mbele zake kwa kuimba. (K)

Jueni kwamba Bwana ndiye Mungu;
Ndiye aliyetuumba na sisi tu watu wake;
Tu watu wake, na kondoo wa malisho yake. (K)

Kwa kuwa Bwana ndiye mwema;
Rehema zake ni za milele;
Na uaminifu wake vizazi na vizazi. (K)


SOMO 2 
Rum. 5 : 6-11

Wapendwa, hapo tulipokuwa hatuna nguvu, wakati ulipotimia, Kristo alikufa kwa ajili ya waovu. Kwa kuwa ni shida mtu kufa kwa ajili ya mtu mwenye haki; lakini yawezekana mtu kuthubutu kufa kwa ajili ya mtu aliye mwema. Bali Mungu aonyesha pendo lake veye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi. Basi zaidi sana tukiisha kuhesabiwa haki katika damu yake, tutaokolewa na ghadhabu kwa yeye. Kwa maana ikiwa tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kwa mauti ya Mwana wake, zaidi sana baada ya kupatanishwa tutaokolewa katika uzima wake. Wala si hivyo tu, ila pia twajifurahisha katika Mungu kwa Bwana wetu Yesu Kristo, am have kwa yeye sasa tumeupokea huo upatanisho.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


SHANG1LIO 
Yn. 15 :15

Aleluya, aleluya, Ninyi nimewaita rafiki, kwa kuwa yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu.
Aleluya.


INJILI 
Mt. 9:36-10:8

Yesu alipowaona makutano, aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji. Ndipo alipowaambia wanafunzi wake, Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache. Basi mwombeni Bwana wa mavuno, apeleke watenda kazi katika mavuno yake. Akawaita wanafunzi wake kumi na wawili, akawapa amri juu ya pepo wachafu, wawatoe, na kupoza

magonjwa yote na udhaifu wa kila aina. Na majina ya hao mitume kumi na wawili ni haya; Wa kwanza Simoni aliyeitwa Petro, na Andrea nduguye; Yakobo wa Zebedayo, na Yohane nduguye; Filipo, na Bartholomayo; Tomaso, na Mathayo mtoza ushuru; Yakobo wa Alfayo, na Thadayo; Simoni Mkananayo, na Yuda Iskariote, naye ndiye mwenye kumsaliti. Hao Thenashara Yesu aliwatuma, akawaagiza, akisema, Katika njia ya Mataifa msiende, wala katika mji wo wote wa Wasamaria msiingie. Afadhali shikeni njia kuwaendea kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli. Na katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme wa mbinguni umekaribia. Pozeni wagonjwa, fufueni wafu, takaseni wenye ukoma, toeni pepo; mmepata bure, toeni bure.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MOYO ULIYO SAFI!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Ijumaa, Juni 13, 2026
Juma la 10 la Mwaka wa Kanisa

1Fal 19: 9, 11-16; 
Zab. 16:1-2, 5, 7-10; 
Mt 2: 41-51


MOYO ULIYO SAFI!

Tukiangalia katika somo la Injili ya leo tunaweza kushangazwa na maneno makali ya Yesu. “ngoa jicho lako” au “ukate mkono wako na kuutupa mbali”. Yesu alitumia lugha hii kali ili aweze kuweka mbele ya wafuasi lengho moja katika maisha ambalo ni maisha safi ya sadaka- hii ikiwa ni muunganiko wa matakwa yetu na Mungu. Kama Daktari anavyoweza kuondoa mguu au sehemu ya mwili kwamanufaa ya mwili mzima, nasi pia tunapaswa tuwe tayari kuachana na kile kinachoweza kutufanya tutende dhambi, na ambacho kwa njia yeyote kitatuletea kifo cha roho zetu. Yesu pia anatuonya sisi pia tuwe na jukumu kubwa la kutokuwa kikwazo au kisababishi cha kuwafanya wengine watende dhambi, au kuwaangusha, tusiwe kipingamizi au tusitoe mfano mbaya ambao utawaongoza wengine kwenye dhambi. 

Pili, Yesu anatufundisha kwamba kuwa safi ni pamoja nakuwa tayari kukabili kila hali katika maisha katika hali ambayo inatimiza sheria ya Mungu, si tu katika matendo ya njee bali naya ndani pia. Yesu anasema tamaa mbaya hutoka moyoni. Ndio maana dhambi yakukosa uaminifu ni lazima itibiwe kwanza kutoka ndani ya moyo, sehemu ambayo si ya hisia tuu, bali utashi, maamuzi, mawazo, na malengo pia. Ni lazima tutambue lengho la Amri za Mungu na tuamue kutoka moyoni kumfuata Mungu. 

Sala: Baba wa Mbinguni, nitakase mimi, ili niweze kufanana na Kristo mwanao kwa maisha yangu. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JUNI 13, 2026




MASOMO YA MISA, JUNI 13, 2026
JUMAMOSI, JUMA LA 10 LA MWAKA

SOMO 1
1Fal 19:19-21

Eliya aliondoka huko, akamkuta Elisha mwana wa Shafati, aliyekuwa akilima, mwenye jozi za ng’ombe kumi na mbili mbele yake, nay eye mwenyewe alikuwa pamoja na lile la kumi na mbili. Eliya akapita karibu naye, akatupa vazi lake juu yake. Naye akawaacha ng’ombe, akamfuata Eliya mbio, akasema, Nipe ruhusa, nakuomba, nimbusu baba yangu na mama yangu, kisha mimi nitakufuata. Akamwambia, Enenda urudi; ni nini niliyokutendea. Akarudi akiacha kumfuata, akatwaa lile jozi la ng’ombe, akawachinja, akatokosa nyama zao kwa ile miti ya ng’ombe, akawapa watu, wakala. Kisha akainuka, akamfuata Eliya, akamhudumia.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 16:1-2, 5, 7-10 (K) 5

(K) Bwana ndiye fungu la posho langu, na la kikombe changu.

Mungu, unihifadhi mimi,
Kwa maana nakukimbilia Wewe.
Nimemwambia Bwana, Ndiwe Bwana wangu;
Sina wema ila utokao kwako. (K)

Nitamhimidi Bwana aliyenipa shauri,
Naam, mtima wangu umenifundisha usiku.
Nimemweka Bwana mbele yangu daima,
Kwa kuwa yuko kuumeni kwangu, sitaondoshwa. (K)

Kwa hiyo moyo wangu unafurahi,
Na utukufu wangu unashangilia,
Naam mwili wangu nao utakaa kwa kutumaini.
Maana hutakuachia kuzimu nafsi yangu,
Wala hutamtoa mtakatifu wako aone uharibifu. (K)


SHANGILIO
Lk 2:19

Aleluya, aleluya
Abarikiwe Bikira Mariamu aliyeyaweka maneno hayo yote, akiyafikiri moyoni mwake.
Aleluya


INJILI
Lk 2: 41-51

Wazee wake huenda Yerusalemu kila mwaka, wakati wa sikukuu ya Pasaka. Na alipopata umri wake miaka kumi na miwili, walipanda kama ilivyokuwa desturi ya sikukuu; na walipokwisha kuzitimiza siku, wakati wa kurudi kwao, yule mtoto Yesu alibaki nyuma huko Yerusalemu, na wazee wake walikuwa hawana habari. Nao wakadhani ya kuwa yumo katika msafara; wakaenenda mwendo wa kutwa, wakawa wakimtafuta katika jamaa zao na wenzao; na walipomkosa, wakarejea Yerusalemu, huku wakimtafuta. Ikawa baada ya siku tatu wakamwona hekaluni, ameketi katikati ya waalimu, akiwasikiliza na kuwauliza maswali. Nao wote waliomsikia walistaajabia fahamu zake na majibu yake. Na walipomwona walishangaa, na mama yake akamwambia, Mwanangu, mbona umetutenda hivi? Tazama, baba yako na mimi tulikuwa tukikutafuta kwa huzuni. Akawaambia, Kwani kunitafuta? Hamkujua ya kuwa imenipasa kuwamo katika nyumba ya Baba yangu? Nao hawakuelewa na neno hilo alilowaambia. Akashuka pamoja nao mpaka Nazareti, naye alikuwa akiwatii; na mamaye aliyaweka hayo yote moyoni mwake.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MOYO UNAO WAKA MAPENDO!



⁠⁠⁠⁠⁠“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Kila Siku
Ijumaa, Juni 12, 2026,
Juma la 10 la Mwaka wa Kanisa

Sherehe ya Moyo Mtakatifu wa Yesu

Kumb 7: 6-11;
Zab 103: 1-4;
1 Yn 4: 7-16;
Mt 11: 25-30


MOYO UNAO WAKA MAPENDO!


“Huu ni upendo si kwamba sisi tulimpenda Mungu kwanza bali yeye alitupenda sisi kwanza akamtuma mwanaye ulimwenguni kama sadaka kwaajili ya dhambi zetu” (1 Yn 4: 10). Sherehe ya Moyo Mtakatifu wa Yesu ni sherehe ya upendo wa ukombozi wa Mungu wetu. Mungu anayetupenda alimtoa mwanaye aje ulimwenguni kama sadaka kwaajili ya ukombozi wa Ulimwengu. Upendo huu unaoneshwa katika moyo wa mwana wa Mungu. Neno “moyo” linasimama kama upendo wa mtu. Na hivyo watu husema “Nakupenda kwa moyo wangu wote” na wakati tunapo sheherekea sikukuu ya Moyo Mtakatifu wa Yesu kanisa linatuhimiza kutafakari juu ya upendo wa Mungu, upendo uliofunuliwa ndani ya mwili wa Mwanaye Yesu Kristo.

Ni Mungu aliyewachagua wa Israeli kuwa watu wake. Aliwabariki na akawachagua kuwa watu wake kati ya mataifa mengi. Si kwasababu walikuwa na nguvu kuliko wengine lakini kwasababu ya upendo wake. Hili ndilo Musa alilowafundisha watu wa Israeli. Anawakumbusha juu ya upendo wa Mungu juu yao. Upendo wa Mungu kwa watu wake hauna mwisho na hauna masharti. Aliwapenda watu wake pamoja na mapungufu yao na makosa yao. Na hata hivyo ubinadamu uliponaswa na dhambi alimtoa mwanaye wa pekee kwajili yetu. Kwahiyo tunapaswa kuuzoea nakuupenda upendo huu ili tuweze kuuelewa zaidi na kuwa watu wakweli wanotamani kuwa na Mungu daima. Ili tuweze kumpenda kwa moyo wetu wote na akili yetu zote.

Kwahiyo katika sikuu hii ya moyo Mtakatifu wa Yesu, tunamshukuru Mungu kwa upendo wake mkubwa kwetu anaotuonesha kila siku. Tuupende na kuushi upendo huu ndani mwetu ili tuweze kuwashirikisha na wengine.

SALA: Moyo Mtakatifu wa Yesu, utuhurumie. Ninakushukuru Bwana wangu kwa kunipa yote hayo. Hakuficha kitu kwangu na unaendelea kunigawia maisha yako kwa ajili yangu na kwa ajili ya ulimwengu mzima. Ninaomba nipokee yote unayonipa bila kubakiza chochote kutoka kwako. Yesu, nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JUNI 12, 2026




MASOMO YA MISA, JUNI 12, 2026
IJUMAA, JUMA LA 10 LA MWAKA

SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU


SOMO 1
Kum. 7:6 - 11

Musa aliwaambia makutano: Kwa maana wewe u taifa takatifu kwa Bwana Mungu wako; Bwana, Mungu wako, amekuchagua kuwa watu wake hasa, zaidi ya mataifa yote walioko juu ya uso wa nchi.

Bwana hakuwapenda ninyi, wala hakuwachagua ninyi, kwa sababu mlikuwa wengi kuliko mataifa yote, maana mlikuwa wachache kuliko watu wote; bali kwa sababu Bwana anawapenda, na kwa sababu alitaka kuutimiza uapo wake aliowaapia baba zenu, ndiyo sababu Bwana akawatoa kwa mkono wa nguvu, akawakomboa katika nyumba ya utumwa katika mkono wa Farao, mfalme wa Misri.

Basi, jueni ya kuwa Bwana, Mungu wenu, ndiye Mungu; Mungu mwaminifu, ashikaye agano lake na rehema zake kwao wampendao, na kushika amri zake, hata vizazi elfu; naye huwalipa wamchukiao mbele ya uso wao, ili kuwangamiza. Hatakuwa mlegevu kwake yeye amchukiaye, atamlipa mbele ya uso wake. Basi zishike amri, na sheria, na hukumu ninazoamuru leo, uzitende.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 103:1 – 4, 6 – 8, 10 (K) 17

(K) Fadhili za Bwana zina wamchao, tangu milele hata milele.

Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana,
Naam, vyote vilivyo ndani yangu
Vilihimidi jina lake takatifu.
Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana,
Wala usizisahau fadhili zake zote. (K)

Akusamehe maovu yako yote,
Akuponya magonjwa yako yote,
Aukomboa uhai wako na kaburi,
Akutia taji ya fadhili na rehema. (K)

Bwana ndiye afanyaye mambo ya haki,
Na hukumu kwa wote wanaoonewa.
Alimjulisha Musa njia zake,
Wana wa Israeli matendo yake. (K)

Bwana amejaa huruma na neema,
Haoni hasira upesi, ni mwingi wa fadhili.
Hakututenda sawasawa na hatia zetu,
Wala hakutulipa kwa kadiri ya maovu yetu. (K)



SOMO 2
1Yoh. 4:7 – 16

Wapenzi na tupendane, kwa kuwa pendo latoka kwa Mungu, na kila apendaye amezaliwa na Mungu, naye anamjua Mungu. Yeye asiyependa, hakumjua Mungu, kwa maana Mungu ni upendo. Katika hili pendo la Mungu lilionekana kwetu, kwamba Mungu amemtuma Mwanawe pekee ulimwenguni, ili tupate uzima kwa yeye. Hili ndilo pendo, si kwamba sisi tulimpenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda sisi, akamtuma Mwanawe kuwa kipatanisho kwa dhambi zetu. Wapenzi, ikiwa Mungu alitupenda sisi hivi, imetupasa na sisi kupendana. Hakuna mtu aliyemwona Mungu wakati wowote. Tukipendana, Mungu hukaa ndani yetu, na pendo lake limekamilika ndani yetu. Katika hili tunafahamu ya kuwa tunakaa ndani yake, naye ndani yetu, kwa kuwa ametushirikisha Roho wake. Na sisi tumeona na kushuhudia ya kuwa Baba amemtuma Mwana kuwa Mwokozi wa ulimwengu. Kila akiriye ya kuwa Yesu ni Mwana wa Mungu, Mungu hukaa ndani yake, naye ndani ya Mungu. Nasi tumelifahamu pendo alilo nalo Mungu kwetu sisi, na kuliamini. Mungu ni upendo, naye akaaye katika pendo, hukaa ndani ya Mungu, na Mungu hukaa ndani yake.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



SHANGILIO
Mt. 11:29

Aleluya, aleluya,
Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu, kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo.
Aleluya.



INJILI
Mt. 11:25-30

Wakati ule Yesu alijibu, akasema, Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga. Naam, Baba, kwa kuwa ndiyvo ilivyopendeza mbele zako. Akasema, Nimekabidhiwa vyote na baba yangu; wala hakuna amjuaye Mwana, ila Baba; wala hakuna amjuaye Baba, ila Mwana na yeyote ambaye Mwana apenda kumfunulia.

Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.