Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

KONDOO NA MBWA MWITU!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Ijumaa, Julai, 10, 2026
Tafakari ya kila siku
Juma la 14 la Mwaka wa Kanisa

Hos 14: 2-10; 
Zab 50: 3-4, 8-9, 12-14, 17; 
Mt 10: 16-23


KONDOO NA MBWA MWITU!

“Mti unaozaa matunda mazuri hupigwa mawe mengi”; vile vile Mkristo anayeshika kiaminifu tunu za Injili anapata mateso mengi. Katika Injili ya leo Yesu anatupa maelekezo nini cha kufanya wakati wa mambo kama hayo yanapotokea kwetu. “Nina watuma kama kondoo kati ya mbwa mwitu”. Yesu anatuita kondoo kwasababu hatutumii fujo wala vita, bali tunatumia ujumbe wa upendo, msamaha, Amani na haki kama silaha ya kuwatibia maadui na watesi wetu. Tunu hizi za kiroho mara nyingi kwao zinakuwa sumu na wanakuwa na hasira zaidi nakutaka kutuangamiza, lakini Yesu anatuambia ndio njia sahihi kabisa yenye tabia za Kimungu. 

Pili, “Muwe na busara kama nyoka wenye upole kama njiwa”. Tunapaswa kuwa wabunifu na wenye kuzaa matunda mema kawasababu tutakukumbana na mambo ya ulimwengu bila hivyo tunaweza kutekwa na kuanza kuwa kama wa ulimwengu pia. 

Tatu, “msiwe na wasiwasi mtasema nini au mtasema namna ghani”. Roho Mtakatifu aliyewashukia Mitume siku ile ya Pentekoste na kuwajaza nguvu wakatao ushuhuda juu ya Kristo atawaimarisha na ninyi pia. Sisi pia tumempokea Roho Mtakatifu kwa ubatizo wetu, atatuongoza na ataongea ndani mwetu wakati tunavyo ulizwa maswali na mamlaka ya ulimwengu huu, kama tuta shirikiana naye. Kwa nguvu zetu wenyewe bila msaada wake tutashindwa.

Neno la Kristo linatutia nguvu na kututia moyo katika hali ya vitisho na misukosuko yahusuyo Imani yetu. Kama Wafuasi wa Yesu mmoja wetu anaweza kupatwa na changamoto katika maisha, labda kuhukumiwa bila hatia, kuvunjika kwa familia, au kuonewa na kutengwa na jamii na mengine mengi. Katika nyakati hizi mmoja hapaswi kuwa kama mbwa mwitu (hasira, kulaumu na kulaani) , bali anapaswa kuwa kama kondoo akiendelea kuzishika tunu za Injili na kutoa ushuhuda wa Yesu kwa ujasiri na hekima. Yote yakiwa yametimilika katika mapendo ya Kristo, lengo la maisha yetu litakuwa limetimilika na tutapata tuzo katika maisha ya umilele. 

Sala: Bwana wangu, nifanye mimi nitambue njia yako na uniongoze katika njia hiyo ili niweze kufuata kiaminifu neno lako na kuwa shuhuda wako. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JULAI 10, 2026



MASOMO YA MISA, JULAI 10, 2026
IJUMAA , JUMA LA 14 LA MWAKA

SOMO 1
Hos. 14: 2 – 9

Bwana anasema: Chukueni maneno pamoja nanyi, mkamrudie Bwana; mkamwambie, Ondoa maovu yote, uyatakabali yaliyo mema; na hivyo ndivyo tutakavyotoa sadaka za midomo yetu kana kwamba ni ng’ombe. Ashuru hatatuokoa; hatutapanda farasi; wala hatutaiambia tena kazi ya mikono yetu, Ninyi ndinyi miungu yetu; maana kwako wewe wasio na baba hupata rehema. Mimi nitawaponya kurudi nyuma kwao; nitawapenda kwa ukunjufu wa moyo; kwa maana hasira yangu imemwacha. Nitakuwa kama umande kwa Israeli; naye atachanua maua kama nyiroro, na kuieneza mizizi yake kama Lebanoni.
Matawi yake yatatandaa, na uzuri wake utakuwa kama uzuri wa mzeituni, na harufu yake kama Lebanoni. Na wao wakaao chini ya uvuli wake watarejea; watafufuka kama ngano, na kuchanua maua kama mzabibu; harufu yake itakuwa kama harufu ya divai ya Lebanoni.
Efraimu atasema, Mimi nina nini tena na sanamu? Mimi nimeitika, name nitamwangalia. Mimi ni kama mberoshi wenye majani mabichi. Kwangu mimi yamepatikana matunda yako.
Ni nani aliey na hekima, naye atayafahamu mambo haya? Ni nani aliey na busara, naye atayajua? Kwa maana njia za Bwana zimenyoka, nao wenye haki watakwenda katika njia hizo; bali waasio wataanguka ndani yake.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI
Zab. 51: 1 – 2, 6 – 7, 10 – 11, 15 (K) 15

(K) Ulimi wangu utaiimba haki yako.

Ee Mungu, unirehemu,
Sawasawa na fadhili zako. 
Kiasi cha wingi wa rehema zako,
Uyafute makosa yangu.
Unioshe kabisa na uovu wangu,
Unitakase dhambi zangu. (K) 

Tazama, wapendezwa na kweli iliyo moyoni,
Nawe utanijulisha hekima kwa siri,
Unisafishe kwa hisopo name nitakuwa safi,
Unioshe, name nitakuwa mweupe kuliko theluji. (K)

Ee Mungu, uniumbie moyo safi,
Uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu.
Usinitenge na uso wako,
Wala roho yako mtakatifu usiniondolee. (K)

Ee Bwana, uifumbue midomo yangu,
Na kinywa change kitazinena sifa zako. (K)

SHANGILIO
1 Pet. 1:25

Aleluya, aleluya,
Neno la Bwana hudumu hata milele, na neno hilo ni neno lile jema lililohubiriwa kwenu. 
Aleluya.

INJILI
Mt. 10: 16 – 23

Yesu aliwaambia mitume wake: Angalieni, mimi nawatuma kama kondoo kati ya mbwa mwitu; basi iweni na busara kama nyoka, na kuwa watu wapole kama hua.
Jihadharini na wanadamu; kwa maana watawapeleka mabarazani, na katika masinagogi yao watawapiga; nanyi mtachukuliwa mbele ya maliwali na wafalme kwa ajili yangu, kuwa ushuhuda kwao na kwa mataifa. Lakini hapo watakapowapeleka, msifikirifikiri jinsi mtakavyosema; maana mtapewa saa ile mtakayosema. Kwa kuwa si ninyi msemao, bali ni Roho wa Baba yenu ndani yenu.
Na ndugu atamsaliti nduguye ili auawe, na baba atamsaliti mwana, na wana watawainukia wazazi wao, na kuwafisha. Nanyi mtakuwa mkichukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu; lakini mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka. Lakini watakapowafukuza katika mji huu, kimbilieni mwingine; kwa maana ni kweli nawaambia, Hamtaimaliza miji ya Israeli, hata ajapo Mwana wa Adamu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

UWEZO KATIKA UTUME!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Alhamisi, Julai 9, 2026, 
Tafakari ya kila siku
Juma la 14 la Mwaka wa Kanisa


Hos 11:1-4, 8-9; 
Zab 79:2-3, 15-16; 
Mt 10:7-15


UWEZO KATIKA UTUME!


Yesu mwana wa Mungu, alitumwa Ulimwenguni kwa Upendo wa Baba, alitangaza Ufalme wa Mungu ndani ya ufalme wa mwanadamu, ili watoke kutoka katika utawala wa yule mwovu. Akitutaka wadhambi kama mimi na wewe, tuache dhambi tushirikiane naye katika kuokoa ulimwengu kutoka katika giza la kifo na mauti, aliwachagua wafuasi kumi na wawili akawaita mitume mwazoni kabisa mwa utume wake. Kwa hawa aliwapa mafundisho maalumu kwaajili ya utume wao, akawapa uwezo wakutoa pepo, kufufua wafu na kuponya magonjwa mbali mbali.

Injili inomuonesha Yesu kama daktari mkuu, akiwaponya wenye ukoma, waliopooza, vipofu na viziwi, na hata kuwafufua wafu. Yesu, sasa anawashirikisha mitume wake nguvu hizi, ambao watakuwa mawakili wa kutangaza ufalme wa Mungu. Kama ilivyo katika elimu, mafunzo ya kijeshi, au mafunzo yeyote., inawapa watu ujuzi wa maisha, pia mitume wa Yesu walihiitaji mafundisho ili waweze kuwa na kiwango cha kutangaza Ufalme wa Mungu. Ufukara ulipaswa kuwa silaha yao dhidi ya hekima ya ulimwengu, na Amani ilipaswa kuwa matunda ya hekima yao. Walipaswa wamtegemee Mungu na pia kwa msaada wa waliowapa watu. Hii ni jinsi ghani Yesu alivyojua vizuri pesa ni chanzo cha maovu mengi. 

Ni kwa jinsi ghani wakati mwingine Kanisa limedhoofishwa katika utume wake kwasababu ya kuwa dhaifu katika pesa, pengine utajiri na tamaa. Uwezo wa Kanisa unakuja kwa ufukara wake na misaada ambapo unyenyekevu wa kweli ndio msingi wake. Chanzo kingine cha uwezo wa utume ni Amani ya ndani na utulivu unaotoka katika dhamira iliyo safi na yenye unyenyekevu wa kweli. Mtume wa kweli anabaki mtulivu pale anapo kubaliwa au kukataliwa. 

Sala: Roho Mtakatifu, tunaomba utufanye Wakristo wapya, na zaidi sana watumishi wako makleri waweze kuwa mitume wa kweli siku zote. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JULAI 9, 2026






MASOMO YA MISA, JULAI 9, 2026
ALHAMISI, JUMA LA 14 LA MWAKA


SOMO 1
Hos. 11:1, 3 -4, 8 – 9

Bwana anasema: Israeli alipokuwa mtoto, nalikuwa nikimpenda, nikamwita mwanangu atoke Misrei. Lakini nalimfundisha Efraimu kwenda kwa miguu; naliwachukua mikononi mwangu; hawakujua ya kuwa naliwaponya. Naliwavuta kwa Kamba za kibinadamu, kwa mafungo ya upendo; name nalikuwa kwao kama hao waondoao kongwa tayari mwao, nikaandika chakula mbele yao.

Niwezeje kukuacha, Efraimu? Niwezeje kukuponya, Israeli? Niwezeje kukufanya kama Adma? Niwezeje kukuweka kama Seboimu? Moyo wangu umegeuka ndani yangu, huruma zangu zimewaka pamoja. Sitatumia ukali wa hasira yangu, sitarudi kumwangamiza Efraimu; kwa maana mimi ni Mungu, si mwanadamu mimi; mimi ndiye aliye Mtakatifu katikati yenu; wala sitaingia ndani ya mji.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 80: 1 – 2, 14 – 15 (K) 3

(K) Uangazishe uso wako, Ee Bwana, nasi tutaokoka.

Wewe uchungaye Israeli, usikie,
Wewe umwongozaye Yusufu kama kundi;
Wewe uketiye juu ya makerubi, utoe nuru.
Uziamshe nguvu zako.
Uje, utuokoe. (K)

Ee Mungu wa majeshi, tunakusihi, urudi,
Utazame toka juu uone, uujilie mzabibu huu.
Na mche ule ulioupanda
Kwa mkono wako wa kuume;
Na tawi lile ulilolifanya
Kuwa imara kwa nafsi yako. (K)


SHANGILIO
Yak. 1:18

Aleluya, aleluya,
Kwa kupenda kwake mwenyewe, Baba alituzaa sisi kwa neno la kweli, tuwe kama limbuko la viumbe vyake.
Aleluya.


INJILI
Mt. 10: 7 – 15

Yesu aliwaambia mitume wake: Katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme wa mbinguni umekaribia. Pozeni wagonjwa, fufueni wafu, takasene wenye ukoma, toeni pepo; mmepata bure, toeni bure. Msichukue dhahabu, wala fedha wala mapesa mishipini mwenu; wala mkoba wa safari, wala kanzu mbili, wala viatu, wala fimbo; maana mtenda kazi astahili posho lake.

Na mji wowote au kijiji chochote mtakachoingia, tafuteni ni nani humo aliye mtu mwaminifu; make kwake hata mtakapotoka. Nanyi mkiingia katika nyumba isalimuni. Na nyumba ile ikistahili, Amani yenu na iifikilie; la, kwamba haistahili, Amani yenu na iwarudie ninyi. Na mtu asipowakaribisha wala kuyasikiliza maneno yenu, mtokapo katika nyumba ile, au mji ule, kung’uteni mavumbi ya miguuni mwenu. Amin, nawambia, Itakuwa rahisi nchi ya Sodoma na Gomora kustahimili adhabu ya siku ya hukumu, kuliko mji ule.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

KUWA MMISIONARI!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatano, Julai, 8, 2026
Tafakari ya kila siku
Juma la 14 la Mwaka wa Kanisa

Hos 10: 1-3, 7-8, 12; 
Zab 104: 2-7; 
Mt 10: 1-7


KUWA MMISIONARI!


Injili ya leo inaonyesha maelekezo kwa wafuasi wa Yesu jinsi ya kufanya kazi yao ya umisionari na mambo yanayoweza kuwapata. Inaanza kwanza na kuitwa kwa wafuasi kumi na mbili ambao hawa wanaitwa Mitume. Mfuasi (kwa kilatini discipulus- maana yake “kujifunza”) ni mtu anayefuata mwalimu ili kujifunza na kuweka mafundisho ya mwalimu wake katika maisha yake. Mtume (kwa Kigiriki Apostolos) ni yule anayetumwa kwa kazi ya kutangaza mafundisho ya mwalimu wake. 

Tunaitwa kuwa wafuasi na tunatarajiwa kuwa mitume, kwa moyo wote tuweze kuwashirikisha wengine Imani yetu. Ni rahisi kujiona wenyewe kama Wakatoliki wa ‘kawaida’, kama wafuasi tu, na kuwaona Mapadre na Watawa kama wao tu ndio wafanya kazi wa utume wa Kanisa. Hii itakuwa sio sahihi. Sisi wote tumeitwa kuwa wafuasi kwa njia ya ubatizo wetu na Kipaimara, pia tumeitwa kuwa mitume. 

Sisi tupo wapi katika kufanya utume wetu? Je, tuna ujasiri ndani yetu ili tuweze kufika sehemu za giza kabisa ambapo neno la Yesu halijafika bado? Au sisi ni dhaifu ndani yetu kiasi cha kushindwa hata kumshuhudia Yesu katika maeneo yetu tunayoishi? Yesu anawataka wamisionari wanaojitoa sio watu maalumu bali wafuasi wake wote wanaofanya mapenzi ya Baba yake. 

Sala: Bwana Yesu Kristo, umetuita sisi ili tutangaze Injili yako ya Matumaini na ukombozi hapa katika maeneo yetu na ulimwenguni kote. Tufundishe kuwa wamisionari waaminifu kwa maneno na matendo. Amina .

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JULAI 8, 2026





MASOMO YA MISA, JULAI 8, 2026
JUMATANO, JUMA LA 14 LA MWAKA WA KANISA


SOMO 1
Hos. 10:1 – 3, 7 – 8, 12

Bwana asema hivi: Israeli ni mzabibu, utoao matunda yake; kwa kadiri ya wingi wa matunda yake; kwa kadiri iyo hiyo ameongeza madhabahu zake; kwa kadiri ya wema wan chi yake, kwa kadiri hiyo hiyo wamefanya nguzo nzuri. Moyo wao umegawanyika; sasa wataonekana kuwa na hatia; yeye atazipiga madhabahu zao, ataziharibu nguzo zao. Yakini sasa watasema, Hatunamfalme; kwa maana hatumchi Bwana; na mfalme huyu je! Aweza kututendea nini? Katika habari za Samaria, mfalme wake amekatiliwa mbali, kama povu usoni pa maji. Israeli, pataharibika; mwiba na mbigili itamea juu ya madhabahu zake; nao wataiambia milima, Tusitirini; na vilima, tuangukeni. Jipandieni katika haki, vuneni kwa fadhili; uchimbueni udongo wa mashamba yenu; kwa maana wakati umewadia wa kumtafuta Bwana, hata atakapokuja na kuwanyeshea haki.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 105:2 – 7 (K) 4

(K) Siku zote mtafuteni uso wake Bwana.

Mwimbieni, mwimbieni kwa zaburi,
Zitafakarini ajabu zake zote.
Jisifuni kwa jina lake takatifu,
Na ufurahi moyo wao wamtafutao Bwana. (K)

Mtakeni Bwana na nguvu zake,
Utafuteni uso wake sikuzote.
Zikumbukeni ajabu zake alizozifanya.
Miujiza yake na hukumu za kinywa chake. (K)

Enyi wazao wa Ibrahimu, mtumishi wake; 
Enyi wana wa Yakobo, wateule wake.
Yeye, Bwana, ndiye Mungu wetu;
Duniani mwote mna hukumu zake. (K)


SHANGILIO
2 Tim. 1:10

Aleluya, aleluya,
Mwokozi wetu Yesu Kristo alibatili mauti, na kuufunua uzima na kutokuharibika kwa Injili.
Aleluya.


INJILI
Mt. 10:1 – 7

Yesu aliwaita wanafunzi wake kumi na wawili, akawapa amri juu ya pepo wachafu, wawatoe, na kupoza magonjwa yote na udhaifu wa kila aina. Na majina ya hao mitume kumi na wawili ni haya; Wa kwanza Simoni aliyeitwa Petro, na Andrea nduguye; Yakobo wa Zebedayo, na Yohane nduguye; Filipo, na Bartholomayo; Tomaso, na Mathayo mtoza ushuru; Yakobo wa Alfayo, na Thadayo; Simoni Mkananayo, na Yuda Iskariote, naye ndiye mwenye kumsaliti. Hao Thenashara Yesu aliwatuma, akawaagiza, akisema.

Katika njia ya Mataifa msiende, wala katika mji wowote wa Wasamaria msiingie. Afadhali shikeni njia kuwaendea kodnoo waliopotea wa nyumba ya Israeli. Na katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme wa mbinguni umekaribia.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026.

WATETEA IMANI!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumanne, Julai, 7, 2026 
Tafakari ya kila siku
Juma la 14 la Mwaka wa Kanisa


Hos 8: 4-7, 11-13; 
Zab 115: 3-10; 
Mt 9: 32-38


WATETEA IMANI!

Tukijaribu kufikiria kuhusu mpangilio na muunganiko ulivyo katika Kanisa Katoliki, tukijaribu kurudi tangu mwanzo wa kipindi cha mitume, mafundisho yake, msimamo wake, tamaduni zake zinazoletea faraja, sakramenti mbali mbali, umoja wa mafundisho yake, uongozi wa asili ya mitume, mpangilio wake katika kazi ya watakatifu na mashahidi, liki neemeshwa na naombezi ya Mama wa Bwana wetu Yesu Kristo, tukitizama pia umoja wa uwepo wa Mkombozi wetu juu ya Altare, tunajisikia Kanisa hili, Moja, Takatifu, Katoliki la Mitume limetupatia mpangilo mzuri sana na kuwa jua linalo angaza kuondoa giza. 

Ni hakika, tangu mwanzoni kabisa Kanisa limepingana kwa hali zote na mafundisho ya uongo yaliojaribu kuharibu ujumbe halisi wa mapokeo ya Mitume. Kanisa limebaki aminifu na litaendelea kubaki aminifu kwa kiini cha mafundisho ya Imani juu ya Kristo. 

Sisi pia mara nyingi tumekutana na watu wengi wanaotuuliza maswali kuhusu Imani yetu, na zaidi sana kuhusu kumhesimu Bikira Maria na kumuomba atuombee na pia kuhusu watakatifu au kuhusu sakramenti na zaidi sana sakramenti ya Kitubio na mengine mengi. Huwa tunakabiliano nao vipi? Leo Injili inatufundisha jinsi ya kukabiliana na hali hizo katika maisha yetu. 

Injili inatuambia kwamba, mara nyingi Yesu aliwaonea huruma wale wasiokuwa na msaada, walioteseka na wale waliotengwa. Watu mashuhuri hawakupenda Yesu awape nafasi ya kwanza wadhambi na kula pamoja nao. Lakini Yesu hakuwasikiliza walivyo mlaumu. Kama Yesu tunapaswa kuwa imara tunapotaka kuyumbishwa juu ya Imani yetu na tunu za Injili. Kanisa Katoliki sio Kanisa la Biblia tu, lina Mapokeo Matakatifu (mafundisho ya mitume na mababa wa Kanisa, Mafundisho ya Mababa watakatifu n.k), bahati mbaya au kwakutotaka kuyafahamu wengi wanao uliza maswali haya, hawayajui na zaidi sana hawapo tayari kujifunza kwasababu kwao kama kitu hakijaandikwa kwenye Biblia sio kitu kizuri. Kanisa Katoliki chanzo cha mafundisho yake yamejikita katika Maandiko Matakatifu na Mapokeo Matakatifu (Sacred Tradions), kwahiyo Kanisa Katoliki sio dini ya Biblia tu. Tunapaswa kuwa Makini kuhusu Imani yetu, tusiyumbishwe , tushikilie imara kile tunacho amini, mafundisho yalio asili ya Imani yetu. 

Najaribu kufikiria hivi wale wanaokataa mapokeo, je mapokeo sio matokeo pia ya kusoma Biblia? Hivi wao wanapofafanua Biblia, je, maneno wanayo tumia kufafanua yameandikwa kwenye Biblia? Maneno wanayohubiri Mtu akiyaandika na baadae akaja kuwafundisha watu  je sio mapokeo ambayo yametokana na mtu kusoma Biblia? Ukikataa Mapokeo maana yake umekataa pia watu wasifafanue Biblia kwani, utakavyo fafanua lazima utatumia maneno yako kueleza na ni hakika yatakuwa hayajaandikwa kwenye Biblia. Ni ngumu sana kukataa Mapokeo. Ukikataa mapokeo uwe tayari kuwaambia watu kwamba nikusoma Biblia tu na hakuna kuhubiri kwani mahubiri hayajaandikwa neno kwa neno kwenye Biblia. Tulinde Imani yetu daima.

Sala: Bwana nisaidiye niweze kulinda Imani yangu. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JULAI 7, 2026




MASOMO YA MISA, JULAI 7, 2026
JUMANNE , JUMA LA 14 LA MWAKA


SOMO 1
Hos. 8:4 – 7, 11 – 13

Bwana asema hivi: Wamesimamisha wafalme, lakini si kwa shauri langu; wamejifanyia wakuu, lakini nalikuwa sina habari; kwa fedha yao na dhahabu yao wamejifanyizia sanamu, kusudi wakatiliwe mbali. Amemtupa ndama yako, Ee Samaria; hasira yangu imewaka juu yao; siku ngapi zitapita kabla ya hao kupata hali isiyo na hatia? Maana katika Israeli kimetokea hata na kitu hiki; fundi ndiye aliyekifanya, nacho si mungu kamwe; naam, ndama ya Samaria itavunjiaka vipande vipande. Kwa maana wao hupanda upepo, nao watavuna tufani; nafaka haina bua; machipuko yake hayatoi masuke; hata ikiwa yatoa, wageni watayameza. 

Kwa kuwa Efraimu ameongeza madhabahu kwa dhambi, madhabahu zimekuwa dhambi kwake. Nijapomwandikia sharia yangu katika amri elfu kumi, zimehesabiwa kuwa ni kitu kigeni. Kwa habari za dhabihu za matoleo yangu, hutoa dhabihu ya nyama na kuila; lakini Bwana hawakubali; sasa ataukumbuka uovu wao, na kuwapatiliza dhambi zao; watarudi kwenda Misri.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 115:3 – 10 (K) 9

(K) Enyi Israeli, mtumainini Bwana.

Mungu wetu yuko mbinguni,
Alitakalo lote amelitenda.
Sanamu zao ni fedha na dhahabu,
Kazi ya mikono ya wanadamu. (K)

Zina vinywa lakini hazisemi,
Zina macho lakini hazioni,
Zina masikio lakini hazisikii,
Zina pua lakini hazisikii harufu. (K)

Mikono lakini hazishiki, miguu lakini haziendi,
Wala hazitoi sauti kwa koo zake.
Wazifanyao watafanana nazo,
Kila mmoja anayezitumainia. (K)

Enyi Israeli, mtumaini Bwana;
Yeye ni msaada wao na ngao yao;
Enyi mlango wa Haruni, mtumainini Bwana;
Yeye ni msaada wao na ngao yao. (K)


SHANGILIO
Efe. 1:7, 18

Aleluya, aleluya,
Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, awape roho ya hekima mjue tumaini la mwito wake.
Aleluya.


INJILI
Mt. 9:32 – 39

Walimletea Yesu mtu bubu mwenye pepo. Na pepo alipotolewa, yule bubu alinena, makutano wakastaajabu, wakasema, Haijaonekana hivi katika Israeli wakati wowote. Lakini Mafarisayo wakasema, Kwa nguvu za mkuu wa pepo atoa pepo.
Naye Yesu alikuwa akizunguka katika miji yote na vijiji, akifundisha katika masinagogi yao, na kuihubiri habari njema ya ufalme, na kuponya magonjwa yote na udhaifu wa kila aina.
Na laipowaona makutano, aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji. Ndipo alipowaambia wanafunzi wake, Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache. Basi mwombeni Bwana wa mavuno, apelike watenda kazi katika mavuno yake.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

UPONYAJI WA IMANI!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatatu, Julai, 6, 2026, 
Tafakari ya kila siku
Juma la 14 la Mwaka wa Kanisa

Hos 2: 16-18, 21-22; 
Zab 144: 2-9; 
Mt 9: 18-26


UPONYAJI WA IMANI!


Leo katika Injili, tunaona matukio mawili ya miujiza wa kuponya. Hawa ni watu walio muhitaji Yesu ili waponywe. Tunakutana na watu wengi wanao ulizia kuhusu upendo wa Mungu na kwanini Mungu hawaponyi? Kuna wengine pia wanajiuliza pia kuhusu Imani yao wenyewe wanajisikia kama wangekuwa na Imani kubwa zaidi kwa Mungu ungekuta Mungu amesha waponya. 

Kijana mmoja aliitwa Stefano wa umri wa miaka 18, alipata ajali ya gari na alipata hitilafu katika ubongo wake kiasi cha kushindwa pia kuongea vizuri. Na mwaka mmoja baadaye akadondoka kutoka kwenye paa la nyumba, akapooza kuanzia kwenye kiuno kushuka chini. Daktari akamwambia Stefano hutaweze kutembea tena. Lakini Stefano akamwambia Mungu ameniambia huu ni muda wake wakuniponya. Imani yake ilikuwa ya kweli na hakika, hakuwa na mashaka yeyote kwamba Mungu atamponya. Siku moja watu walikusanyika kumuombea, yeye alienda mbele kwakujivuta na kukaa mbele yao, wakamuombea na kusali sana lakini hali yake ikabaki vile vile. Baada ya hapo watu walimuhuzunikia sana kwa hali yake. Walishangaa sana kwamba alikuwa na Imani na walijiridhisha kwamba atapona lakini wakashangaa sasa Imani yake imekuwaje tena? Baada ya mkutano wao wakamkuta Stefano wakashngaa. Alikuwa hayupo vizuri lakini Imani yake ilikuwa haijayumbishwa. Kwa sauti ya huzuni Stefano alisema “haikuwa muda wangu wakupona lakini siku moja nitasimama na kukimbia”.

Hakika tuna muujiza hapa. Muujiza haukuwa katika miguu yake, bali ulikuwa muujiza wa roho yake. Mwanga wa Yesu ulikuwa ukingaa ndani ya roho yake. Na zaidi ya yote, uponyaji wa mwili ni kwa ajili ya muda mfupi. Bali uponyaji wa roho na Uponyaji wa Imani unadumu kwa ajili ya uzima wa milele. Tumuombe Mungu atusaidie kushughulika zaidi na uponyaji wa Imani yetu na maisha yetu ya kiroho ili tuweze kupata nafasi katika maisha ya milele.

Sala: Bwana naomba uniponye kiroho. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JULAI 6, 2026



MASOMO YA MISA, JULAI 6, 2026
JUMATATU, JUMA 14 LA MWAKA


SOMO 1
Hos. 2:14 – 16, 19 – 20

Bwana asema hivi: Angalia, mimi nitamshawishi, na kumleta nyikani, na kusema naye maneno ya kumtuliza moyo. Naye ataniitikia huko, kama siku zile za ujana wake, na kama siku ile alipopanda kutoka nchi ya Misri. Tena siku hiyo itakuwa, asema Bwana, utaniita Ishi, wala hutaniita tena, Baali. Name nitakuposa uwe wangu kwa milele; naam, nitakuposa kwa haki, na kwa hukumu, na kwa ufadhili, na kwa rehema. Name nitakuposa kwa uaminifu; nawe utamjua Bwana.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 145: 2 – 9 (K) 8

(K) Bwana ana fadhili ni mwingi wa huruma.

Kila siku nitakuhimidi, 
Nitalisifu jina lako milele na milele.
Bwana ndiye mkuu mwenye kusifiwa sana,
Wala ukuu wake hautambulikani. (K)

Kizazi kwa kizazi kitayasifu matendo yako,
Kitayatangaza matendo yako makuu.
Nitaifikiri fahari ya utukufu wa adhama yako,
Na matendo yako yote ya ajabu. (K)

Watu watayataja matendo yako ya kutisha,
Name nitausimulia ukuu wako.
Watalihubiri kumbukumbu la wema wako mkuu,
Wataiimba haki yako. (K)

Bwan ana fadhili, ni mwingi wa huruma,
Si mwepesi kwa hasira, ni mwingi wa rehema.
Bwana ni mwema kwa watu wote,
Na rehema zake zi juu ya kazi zake zote. (K)


SHANGILIO
Yn. 8:12 

Aleluya, aleluya,
Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, asema Bwana, yeye anifuataye hatakwenda gizani kamwe, bali atakuwa na nuru ya uzima.
Aleluya.


INJILI
Mt. 9:18 – 26

Yesu alipokuwa akiwaambia hayo, tazama, akaja jumbe mmoja, akamsujudia, akisema, Binti yangu sasa hivi amekufa; lakini njoo, uweke mkono wako juu yake, naye ataishi. Akaondoka Yesu, akamfuata, pamoja na wanafunzi wake.

Na tazama, mwanamke aliyekuwa na ugonjwa wa kutoka damu muda wa miaka kumi na miwili, alikuja kwa nyuma, akaugusa upindo wa vazi lake. Kwa maana alisema moyoni mwake, Nikigusa tu upindo wa vazi lake nitapona. Yesu akageuka, akamwona, akamwambia, Jipe moyo mkuu, binti yangu, Imani yako imekuponya. Yule mwanamke akapona tangu saa ile.

Yesu alipofika nyumbani kwa yule jumbe, aliona wapiga filimbi, na makutano wakifanya maombolezo, akawaambia, Ondokeni; kwa maana kijana hakufa, amelala tu. Wakamcheka sana. Lakini makutano walipoondoshwa, aliingia, akamshika mkono; yule kijana akasimama. Zikaenea habari hizi katika nchi ile yote.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com