Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

KUWA MWEMA!




“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya kwaresima
Ijumaa, Februari 27, 2026
Juma la 1 la Kwaresima


Eze 18:21-28;
Zab 130: 1-8;
Mt 5:20-26.


KUWA MWEMA!


Leo, Nabii Ezekieli anaweka mbele yetu matarajio ya Mungu kwetu sisi. Anatoa sura ya Mungu akiwa amejawa na huruma kwa wale wote ambao hutubu dhambi zao. Hata hivyo anamuonesha Mungu akiwa hakimu wa haki aliye mwema asiye pendezwa na mabaya. Mungu hataki mtu aliye katika pande mbili (anayechanganya mema na mabaya kwa wakati mmoja), yeye anatazama kila mmoja wetu katika nafsi nzima.

Katika Injili Yesu anaongelea kuhusu Ufalme wa Mbinguni. Kuingia katika Ufalme wa mbinguni unapaswa kuwa lengo la Maisha yetu. Ni mara nyingi tunashindwa kuliona hili katika maisha. Tunashindwa kufungua macho yetu kuelekea Mbinguni kama lengo letu la kwanza la kuwa hapa duniani. Ni rahisi kunaswa na kuridhika na hali za kila siku kama viburudisho, pesa, mafanikio, na mengineyo.

Yesu anatupa njia ya pekee ya kufuata katika ujumbe huu wa Injili, jinsi ya kupata lengo la maisha-ufalme wa Mbinguni. Njia anayo ionesha ni haki. Haki maana yake ni kuwa mwaminifu, sio mdanganyifu. Mafarisayo walijifanya kwa kujionesha kuwa walikuwa watakatifu na wafuasi wazuri wa mapenzi ya Mungu. Lakini hawakuwa wazuri katika hilo. Wanaweza kuwa wazuri katika hali ya kutenda na huenda wanaweza kuwa wamewavutia watu, lakini hawakuweza kumdanganya Yesu. Yesu aliweza kuona udanganyifu wao na kujificha kwao kusiko kwakweli na akaona kile kilicho jificha. Yesu aliweza kuona haki yao ni kwa ajili tu ya kujionesha wenyewe kwa watu.

Kama tunataka kufanya Mbingu kuwa lengo letu, tunapaswa kujitahidi kuwa watakatifu. Na waaminifu. Tunapaswa kumtafuta Kristo katika hali ya kweli na uaminifu katika vitu vidogo vya maisha. Tunapaswa kuacha uaminifu huo uweze kungaa kwa kuonesha katika kweli kile kilichopo katika hali ya ndani. Kuwa wenye haki katika hali ya kweli, ni kwamba tunamtafuta Yesu katika hali ya haki na kumfanya Mungu kuwa lengo la maisha yetu.
Sala: Bwana, naomba unifanye mwenye haki. Nisaidie niweze kuwa mwaminifu kwa yote ninayofanya na yote ninayo tafuta katika maisha. Nisaidie mimi nikupende wewe kila wakati na siku zote. Yesu, nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 27, 2026



MASOMO YA MISA, FEBRUARI 27, 2026
IJUMAA, JUMA LA 1 LA KWARESIMA


SOMO 1
Eze. 18:21-28

Bwana asema hivi: Mtu mbaya akighairi, na kuacha dhambi zake zote alizozitenda, na kuzishika amri zangu zote, na kutenda yaliyo halali na haki hakika ataishi, hatakufa. Dhambi zake zote alizozitenda hazitakumbukwa juu yake hata mojawapo katika haki yake aliyoitenda ataishi. Je! Mimi ninafurahia kufa kwake mtu mwovu? Asema Bwana Mungu; si afadhali kwamba aghairi, na kuiacha njia yake, akaishi?

Bali mwenye haki atakapoghairi, na kuiacha haki yake, na kutenda uovu, na kufanya machukizo yote kama yale afanyayo mtu mwovu, je! Ataishi? Katika matendo yake yote ya haki aliyoyatenda halitakumbukwa hata mojawapo. Katika kosa lile alilolikosa, na katika dhambi yake aliyoitenda, atakufa. Lakini ninyi mwasema, Njia ya Bwana si sawa. Sikilizeni sasa, Enyi nyumba ya Israeli; Je! Njia yangu siyo iliyo sawa? Njia zenu sizo zisizo sawa? Mwenye haki atakapoghairi, na kuiacha haki yake, na kutenda uovu, atakufa katika uovu huo; katika uovu wake alioutenda atakufa. Tena, mtu mwovu atakapoghairi, na kuuacha uovu wake alioutenda, na kutenda yaliyo halali na haki ataponya roho yake, nayo itakuwa hai. Kwa sababu atafakari, na kughairi, na kuyaacha makosa yake yote aliyoyatenda, hakika ataishi, hatakufa.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 130 (K) 3

(K) Bwana kama Wewe ungehesabu maovu,
Ee Bwana, nani angesimama?

Ee Bwana, toka vilindini nimekulilia.
Bwana, uisikie sauti yangu.
Masikio yako na yaisikize
Sauti ya dua zangu. (K)

Bwana, kama Wewe ungehesabu maovu,
Ee Bwana, nani angesimama?
Lakini kwako kuna msamaha,
Ili Wewe uogopwe. (K)

Nimemgnoja Bwana, roho yangu imengoja,
Na neno lake nimelitumainia.
Nafsi yangu inamngoja Bwana,
Kuliko walinzi waingojavyo asubuhi,
Naam, walinzi waingojao asubuhi. (K)

Ee Israeli, umtarajie Bwana;
Maana kwa Bwana kuna fadhili,
Na kwake kuna ukombozi mwingi.
Yeye atamkomboa Israeli na maovu yake yote. (K)


SHANGILIO
Yoe. 2:12-13

Hata sasa, nirudieni mimi kwa mioyo yenu yote, Asema Bwana, kwa maana mimi ndiye mwenye neema, Nimejaa huruma.

I
NJILI
Mt. 5:20-26

Siku ile Yesu aliwaambia wafuasi wake: Maana nawaambia ya kwamba, Haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo, hamtaingia kwamwe katika ufalme wa mbinguni.

Mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, Usiue; na mtu akiua, itampasa hukumu. Bali mimi nawaambieni, Kila amwoneaye ndugu yake hasira itampasa hukumu; na mtu akimfyolea ndugu yake, itampasa baraza; na mtu akimwapiza, itampasa jehanam ya moto.

Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako. Patana na mshitaki wako upesi, wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani. Amin, nakuambia, Hutoki humo kamwe hata uishe kulipa senti ya mwisho.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

OMBENI NANYI MTAPEWA!





“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Alhamisi, Februari 25, 2026.
Juma la 1 la Kwaresima

Est 4:17, 23-25;
Zab 138:1-3, 7-8
Mt: 7:7-12


OMBENI NANYI MTAPEWA!


Mara baada ya kuwafundisha Wanafunzi wake kusali, leo Yesu anawaambia: “ombeni nanyi mtapokea …” Baba yetu wa Mbinguni anatupatia kwa neema zake yale yote tunayo muomba hata kwa jinsi tusio tegemea, na kwa wote wanaojua na kutegemea upendo wake, husali kwa hakika. Sala inatokana na upendo wetu kwa Mungu na upendo wake kwetu sisi. Hili linatusaidia kushirikisha upendo wake kwa wengine, kwani Mungu amemimina upendo wake ndani ya Roho zetu kwa njia ya Roho Mtakatifu. (Warumi 5: 5). 

Yesu ana hakika kabisa kwamba tutakapo omba tutapokea, tutakapo tafuta, tutapata, na tutakapo bisha hodi, tutafunguliwa mlango. Mara nyingi tunaweza kuomba na kuomba, lakini tunaona sala zetu hazijibiwi, katika hali ya jinsi tulivyo ziomba. Hili linaleta swali “sasa nisalije na nisali kwa ajili ya nini?”. Lakini kila sala au ombi tunalosema linapaswa liwe kwa ajili ya mapenzi ya Mungu yafanyike, hakuna zaidi, wala hakuna chakupunguza. Ni kwa ajili tu ya mapenzi yake kamili yatimie.

Tutafakari leo, jinsi tunavyosali. Tubadili sala zetu ili ziwe zinatafuta mambo mazuri ambayo Mungu anataka kuyaweka kwetu. Itakuwa ngumu mara ya kwanza kuachana na mapenzi yetu na mawazo yetu, lakini mwishoni tutabarikiwa na mambo mengi mazuri kutoka kwa Mungu. 

Sala: Bwana, ninasali mapenzi yako yatimizwe katika kila kitu. Ninatamani kukabidhi kwako, na kuamini mpango wako mkamilifu. Nisaidie Bwana kuachana na mawazo yangu peke yangu na kutafuta ya kwako daima. Yesu, nakuamini wewe. Amina. 


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 25, 2026





MASOMO YA MISA, FEBRUARI 25, 2026
ALHAMISI, JUMA LA  1 LA KWARESIMA


SOMO 1
Est. 4:17

Malkia Esta naye alimkimbilia Bwana, akishikwa na uchungu wa mauti. Akazivua nguo zake za fahari akavaa nguo za huzuni, na kilio, na badala ya manukato mazuri alijitia majivu na samadi kichwani; akajinyenyekesha mwili wake, hata mahali pa mapambo ya furaha alijifunika kwa nywele zake zilizofumuliwa. Akamwomba Bwana wa Israeli, akisema:

Bwana wangu, Wewe peke yako u Mfalme wetu. Unisaidie mimi niliye mkiwa, wala sina msaidizi wmingine ila Wewe; maana hatari yangu imo mkononi mwangu.

Tangu nilipozaliwa katika kabila ya jamaa yangu, nimesikia ya kuwa Wewe, Bwana, ulimchagua Israeli katika mataifa yote, na baba zetu katika jamaa zao, kuwa urithi wa daima, ukawatimilizia yote uliyoyaahidi.

Utukumbuke, Ee Bwana; ujifunue wakati wa taabu yetu; unipe moyo thabiti, Ee Mfalme wa miungu na Bwana wa milki zote. Unitie kinywani mwangu maneno ya kufaa mbele ya samba, ukaugeuza moyo wake apate kumchukia yule anayepigana nasi, ili akomeshwe pamoja na wote wenye nia moja naye. Lakini utuokoe sisi kwa mkono wako; unisaidie mimi niliye peke yangu, bila msaidizi mwingine ila Wewe, Bwana.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 138:1-3, 8-9 (K) 1

(K) Siku ile niliyokuita uliniitikia, Ukanifariji nafsi kwa kunitia nguvu.

Nitakushukuru kwa moyo wangu wote,
Mbele ya miungu nitakuimbia zaburi.
Nitasujudu nikilikabili hekalu lako takatifu,
Nitalishukuru jina lako. (K)

Kwa ajili ya fadhili zako na uaminifu wako,
Kwa amana umeikuza ahadi yako,
Kuliko jina lako lote.
Siku ile niliyokuita uliniitikia,
Ukanifariji nafsi kwa kunitia nguvu. (K)

Na mkono wako wa kuume utaniokoa.
Bwana atanitimilizia mambo yangu;
Ee Bwana, fadhili zako ni za milele;
Usiziache kazi za mikono yako. (K)


SHANGILIO
Eze. 33:11

Sikufurahii kufa kwake mtu mwovu, asema Bwana, Bali aiache njia yake mbaya, akaishi.


INJILI
Mt. 7:7-12

Siku ile Yesu aliwaambia wafuasi wake: Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa; kwa maana kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa. Au kuna mtu yupi kwenu, ambaye, mwanawe akiomwomba mkate, atampa jiwe? Atampa jiwe? Au akiomba samaki, atampa nyoka? Basi ikiwa ninyi, mlio waovu, mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Si zaidi sana Baba yenu aliye mbinguni atawapa mema wao wamwombao?

Basi yoyote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hivyo ndiyo torati na manabii.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com


KUMKUBALI YESU NA UPENDO WAKE!





“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Jumatano, Februari 25, 2026
Juma la 1 la Mwaka

Jon 3:1-10;
Ps 51:3-4,12-13,18-19;
Lk 11:29-32


KUMKUBALI YESU NA UPENDO WAKE!


Katika masomo ya leo tunamwona Yona akipeleka Neno la Mungu kwa watu wa Ninawi, na anapo anza kuingia katika mji, anaanza kutangaza kwake kuharibiwa kwa mji huo na watu wanasikia . Mfalme anasikia na kutangaza kufunga, watu wavae magunia wajipake majivu na kutubu. Mfalme mwenyewe ana anza kuvaa magunia, kuacha kiti chake cha enzi na kukaa katika majivu. Hivyo Mungu anawaonea huruma watu wa Ninawi na ana sitisha mpango wa kuuharibu mji huo. Muujiza huu sio Mungu kuacha kuuanga miza mji wa Ninawi bali ni namna watu walivyo mgeukia Mungu. Walipokea neno la Mungu na wakaliweka katika matendo.

Katika Injili, tunaona watu ambao wanahitaji ishara ya ajabu ili waweze kusikiliza maneno ya Yesu. Yesu anashangazwa na anawaambia, Malkia wa Sheba alikuja kutoka mbali kumsikia Sulemani na Ninawi walitubu baada ya kumsikia Yona, wao wapo na mtu mkubwa zaidi kuliko Yona na Sulemani lakini wanashindwa kumtambua. Wapo na mwana wa Mungu lakini kwasababu ya mioyo yao migumu wanashindwa kumtambua Yesu nakuongoka.

Watu wakipindi cha Yesu walibarikiwa kwa kusikia neno la Mkombozi wa Ulimwengu. Je, na sisi pia?! Tuna Injili, mafundisho ya Kanisa, ushahidi wa Watakatifu wengi, uchungaji wa Baba Mtakatifu, Sakramenti na mengine mengi. tuna njia mbali mbali za kupata Injili katika Ulimwengu wa Teknologia lakini ni ajabu tunaweza kushindwa kusikia sauti ya Yesu. Tutafakari sisi wenyewe jinsi tunavyo itikia ujumbe wa Yesu. Anaongea na sisi mara nyingi kwa nguvu mbali mbali lakini tunashindwa kumsikia. Kushindwa kusikiliza, inapelekea tunashindwa kutubu.

Sala: Bwana, unaongea nami kwa njia mbali mbali. Unahubiri kwa njia ya Neno lako, Kanisa lako na katika maisha yangu ya sala. Ninakupenda wewe, Bwana wangu mpendwa, ninatubu dhambi zangu. Yesu nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 25, 2026




MASOMO YA MISA, FEBRUARI 25, 2026
JUMATANO, JUMA  LA 1 LA KWARESIMA


SOMO 1
Yon. 3:1-10

Neno la Bwana likamjia Yona mara ya pili, kusema, Ondoka, uende Ninawi, mji ule mkubwa, ukaihubiri habari nitakayokuamuru.

Basi Yona akaondoka, akaenda Ninawi, kama Bwana alivyonena. Basi Ninawi ulikiuwa mji mkubwa mno, ukubwa wake mwendo wa siku tatu, Yona akaanza kuuingia mji mwendo wa siku moja, akapaza sauti yake, akasema, Baada ya siku arobaini Ninawi utaangamizwa.

Basi watu wa Ninawi wakamsadiki Mungu; wakatangaza kufunga, wakajivika nguo za magunia, tangu yeye aliye mkubwa hata aliye mdogo. Habari ikamfikia mfalme wa Ninawi, naye akaondoka katika kiti chake cha enzi, akavua vazi lake, akajivika nguo za magunia, na kuketi katika majivu. Naye akapiga mbiu, akatangaza habari katika mji wa Ninawi, kwa amri ya mfalme na wakuu wake; kusema. Mwanadamu asionje kitu, wala mnyama wala makundi ya ng’ombe, wala makundi ya kondoo; wasile, wala wasinywe maji; bali na wafunikwe nguo za magunia, mwanadamu na mnyama pia, nao wakamlilie Mungu kwa nguvu, naam, na wageuke, kila mtu akaache njia yake mbaya, na udhalimu ulio mikononi mwake. Ni nani ajuaye kwamba Mungu hatageuka na kughairi, na kuiacha hasira yake kali, ili tusiangamizwe?

Mungu akaona matendo yao, ya kuwa wameiacha njia yao mbaya. Basi Mungu akalighairi neno lile baya, ambalo alisema atawatenda; asilitende.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 51:1-2, 10-11, 16-17 (K) 17

(K) Moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu, hutaudharau.

Ee Mungu, unirehemu,
Sawa na fadhili wako.
Kiasi cha wingi wa rehema zako,
Uyafute makosa yangu. (K)

Ee Mungu, uniumbie moyo safi,
Uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu.
Usinitenge na uso wako,
Wala roho yako mtakatifu usiniondolee. (K)

Maana hupendezwi na dhabihu, au ningeitoa,
Wewe huridhii sadaka ya kuteketezwa.
Dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika,
Moyo uliyovunjika na kupondeka. (K)


SHANGILIO
Eze. 18:31

Tupilieni mbali nanyi makosa yenu yote mliyoyakosea, Asema Bwana. Jifanyeni moyo mpya na roho mpya.



INJILI
Lk. 11:29-32

Makutano walipokuwa wakimkusanyikia, Yesu alianza kusema, Kizazi hiki ni kizazi kibaya; kinatafuta ishara, wala hakitapewa ishara, ila ishara ya Yona. Maana, kama vile Yona alivyokuwa ishara kwa Waninawi, ndivyo atakavyokuwa Mwana wa Adamu kwa kizazi hiki. Malkia wa Kusini ataondoka siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa na hatia; kwa sababu yeye alikuja kutoka nchi za dunia aisikie hekima ya Sulemani; na hapa pana mkubwa kuliko Sulemani. Watu wa Ninawi watasimama siku ya hukumu pamoja na kizazi hiki, nao watakihukumu kuwa na hatia; kwa sababu wao walitubu kwa mahubiri ya Yona, na hapa pana mkubwa kuliko Yona.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.