MASOMO YA MISA, JUNI 19, 2026
IJUMAA, JUMA LA 11 LA MWAKA
SOMO 1
2 Fal. 11:1-4, 9-18, 20
Athalia, mama yake Ahazia,
alipoona ya kuwa mwanawe amekufa, akainuka, akawaharibu wazao wote wa kifalme.
Ila Yehosheba, binti wa mfalme Yehoramu, umbu lake Ahazia, akamtwaa Yoashi
mwana wa Ahazia, akamwiba miongoni mwa hao wana wa mfalme waliouawa, yeye na
mlezi wake, na kuwatia katika chumba cha kulala; wakamficha usoni pa Athalia,
basi kwa hiyo hakuuawa. Alikuwako pamoja naye, amefichwa nyumbani mwa Bwana,
miaka sita. Naye Athalia akaitawala nchi.
Hata mwaka wa saba Yehoyada
akatujma, na kuwaleta wakuu wa mamia, wa Wakari, na wa walinzi, akawaleta kwake
ndani ya nyumba ya Bwana; akapatana nao, akawaapisha nyumbani mwa Bwana,
akawaonyesha huyo mwana wa mfalme.
Nao wakuu wa mamia wakafanya
sawasawa na yote aliyowaamuru Yehoyada kuhani; wakawatwaa kila mtu watu wake,
hao watakaoingia sabato, nao watakaotoka sabato, wakaja kwa Yehoyada kuhani.
Naye yule kuhani akawapa wakuu wa mamia mikuki na ngao zilizokuwa za mfalme
Daudi, zilizokuwamo nyumbani mwa Bwana. Walinzi wakasimama, kila mtu na silaha
zake mkononi, kutoka pembe ya kuume ya nyumba mpaka pembe ya kushoto ya nyumba
mpaka pembe ya kushoto ya nyumba, kando ya madhabahu na nyumba, wakimzunguka
mfalme pande zote. Ndipo akamleta nje mwana wa mfalme, akamvika taji, na kumpa
ushuhuda; wakamfanya mfalme, wakamtia mafuta; wakapiga makofi, wakasema, Mfalme
na aishi.
Na Athalia alipoisikia sauti ya
walinzi na ya watu, aliingia kwa watu nyumbani kwa Bwana; akatazama, na tazama,
mfalme amesimama karibu na nguzo kama ilivyokuwa desturi, nao wakuu na wapiga
baragumu karibu na mfalme; na watu wote wa nchi wakafurahi, wakapiga baragumu.
Ndipo Athalia akararua mavazi yake, akalia, Fitina! Fitina! Naye Yehoyada
kuhani akawaamuru wakuu wa mamia, majemadari wa jeshi, akawaambia, Mtoeni kati
ya safu; nay yeyote amfuataye mwueni kwa upanga. Kwani kuhani akasema, Asiuawe
nyumbani mwa Bwana. Basi wakampisha njia; akaenda kwa njia ya kuingia kwa
farasi nyumbani mwa mfalme; akauawa huko.
Kisha, Yehoyada akafanya
mapatano kati ya Bwana na mfalme na watu, ili wawe watu wa Bwana; tena kati ya
mfalme na watu. Watu wote wa nchi wakaiendea nyumba ya Baali, wakaiangusha;
madhabahu zake na sanamu zake wakazivunjavunja kabisa, na Matani kuhani wa
Baali wakamwua mbele ya madhabahu.
Na Yehoyada kuhani akaweka
maakida juu ya nyumba ya Bwana. Basi watu wote wa nchi wakafurahi, na mji
ukatulia. Naye Athalia wakamwua kwa upanga karibu na nyumba ya mfalme.
Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.
WIMBO WA KATIKATI
Zab. 132: 11 – 14, 17 – 18 (K) 13
(K) Bwana ameichagua Sayuni,
ameitamani akae ndani yake.
Bwana amemwapia Daudi neno la kweli,
Hatarudi nyuma akalihalifu,
Baadhi ya wazao wa mwili wako
Nitawaweka katika kiti chako
cha enzi. (K)
Wanao wakiyashika maagano
yangu,
Na shuhuda nitakazowafundisha;
Watoto wao nao wataketi
Katika kiti chako cha enzi
milele. (K)
Kwa kuwa Bwana ameichagua
Sayuni,
Ameitamani akae ndani yake.
Hapo ndipo mahali pangu pa raha
milele,
Hapo nitakaa kwa maana
nimepatamani. (K)
Hapo nitamchipushia Daudi
pembe,
Na taa nimemtengenezea masihi
wangu.
Adui zake nitawavika aibu,
Bali juu yake taji yake
itasitawi. (K)
SHANGILIO
Zab. 119: 18
Aleluya, aleluya,
Unifumbue macho yangu
niyatazame maajabu yatokayo katika sheria yako.
Aleluya.
INJILI
Mt. 6:19 – 23
Yesu aliwaambia wanafunzi wake:
Msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi huvunja na kuiba;
bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala
wevi hawavunji wala hawaibi; kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na
moyo wako.
Taa ya mwili ni jicho; basi
jicho lako likiwa safi, mwili wako wote utakuwa na nuru. Lakini jicho lako
likiwa bovu, mwili wako wote utakuwa na giza. Basi ile nuru iliyomo ndani yako
ikiwa giza; si giza hilo!
Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.
Copyright © 2026, "MASOMO
YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings
reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.