Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

VISHAWISHI-NAFASI YA KUKUWA!



“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Jumapili, Februari 22, 2026
Jumapili ya 1 ya Kwaresima

Mwa 2:7-9; 3:1-7; 
Zab 51:3-6, 12-14, 17; 
Rum 5: 12-19;
Mt 4: 1-11.


VISHAWISHI-NAFASI YA KUKUWA! 


Kushawishiwa , maana yake ni kuvutwa kwenye kitu kisichoruhusiwa. Injili ya Leo inatuambia Yesu alijaribiwa “Kristo kuhani Mkuu, alijaribiwa kwa kila namna kama tulivyo lakini hakutenda dhambi” (Ebr 4:15). Biblia inatualika tutazame vishawishi kama nafasi ya kujipima uchaguzi wetu, nafasi ya kukuwa. Uchaguzi upo kati ya kukubali mpango wa Mungu au kuukataa. Adamu aliamua kuchagua njia isiofaa/hukumu yake mwenyewe; Kristo daima alirejea neno la Mungu daima. Adamu alinyoosha mkono wake juu ya tunda la kifo; Yesu amekuwa chanzo cha uhai. 

Kitabu cha Mwanzo kinamuonesha mwanadamu akiwa katika bustani ya Edeni, ambapo katikati yake kulikuwa na mti wa “uhai” na “maarifa” mema na mabaya. Ni kwa ajili ya Mungu na unawakilisha vizuizi viwili ambavyo havipaswi kuvukwa. Kwanza unawakilisha alama ya Mungu, mtoa uhai, na asiyeweza kufa. Mwanadamu kunyoosha mkono juu ya mti huu ni sawa na kukataa hali yake ya kibinadamu. Pia mti ni wa maarifa ya mema na mabaya. Kunyoosha mkono juu ya mti huu ni kutaka kuwa mkuu wa maamuzi yako na matendo yako mwenyewe. Ni jambo kubwa la kutaka kujianzilishia ukuu-kuanza kumpinga Mungu au kukataa maneno yake ya Kibaba ambayo ni maneno ya maadili mema ya kuchagua. Wakati mwanadamu anasahau kwamba yeye ni kiumbe aliyeumbwa na kujaribu kujifanya Mungu, mjuaji wa mema na mabaya anajimaliza mwenyewe. Ni wazi kwamba anaanza kuita “ubaya kuwa ni wema na kuita wema ni ubaya: kubadili giza kuwa mwanga na mwanga kuwa giza, vitu vichungu na kusema vitamu, au kusema vitamu kuwa vichungu” (Isa 5:20). 

Nyoka anaingia katikati na anawaalika Adamu na Eva kula tunda lililokatazwa. Kitabu cha Hekima kinanyambulisha kuwa ni muovu. (Hek 2:23-24). Kinatufanye tushangae ni muovu yupi anaye shawishi na kudanganya. Nyoka ni mnyama , mwerevu kuliko wanyama wote aliyeumbwa na Mungu. Ni kilele cha kazi ya Mungu aliofanya. Ndio, nyoka si mwingine isipokuwa mwanadamu mwenyewe ambaye, kwa kufikia kilele cha majivuno yake, anatambua mwisho wa uwezo wake. Anajitengenezea maadili yake mwenyewe, akijifanya kutenda mambo katika hali ya kipekee. Nyoka anawakilisha hali yetu ya kupenda mapenzi yetu yawe zaidi ya mapenzi ya Mungu, kujiona wenyewe kuwa Mungu. Ndio sehemu hii ya mwanadamu inatufanya tutende pasipo Mungu. Maneno ya nyoka si kitu kingine zaidi ya mawazo yetu ya ndani ambayo ndipo dhambi inapo anzia. Kitu kingine ni dhambi. Dhambi inazaliwa kwa kutafuta vitu vizuri na vya furaha. Uharibifu ni kwamba, kutokumwamini Mungu, mwanadamu anachagua sehemu mbaya, kupoteza lengo na kujiangamiza mwenyewe. Baada ya dhambi hawaukubali ukweli. Wanajaribu kujificha na kujisikia kukata majani na kujifunika wenyewe. 

Katika somo la pili, Paulo najaribu kuonesha kwamba Adamu ni wazi anajukumu la maovu yote. Anatumia ulinganishaji, kati ya Adamu na Kristo kuelezea kazi ya ukombozi alioitimiza Yesu. Adamu alitaka kuwa bwana wa mema na mabaya, na badala yake akapata kifo kama mshahara wake. Kristo, kinyume na Adamu, alitambua utegemezi wake na Mungu. Alikuwa daima mwaminifu kwa Baba, akawa Bwana wa uhai. Wote wanaomfuata na kuiga utii wake kwa Baba watafanywa wenye haki. 

Katika somo la Injili, “Yesu alikaa jangwani kwa siku arobaini na alijaribiwa na shetani” (Mk 1:12-13). Kwa kutumia lugha ya Biblia na lugha ya picha, alimaanisha maisha yote ya Yesu yalikuwa kati yake na huku shetani akimjaribu. Majibu ya Yesu kwa shetani yanawakilisha matukio matatu ya wana Waisraeli katika kitabu cha kutoka: manunguniko ya chakula na zawadi ya manna (Kut 16), kugoma kwasababu ya maji (Kut 17), kuabudu ndama wa shaba (kut 32) hivyo Yesu anayaishi tena maisha ya watu wake. Yeye anapatwa na majaribu yale yale, lakini anayashinda. Ni wale tu, wanaothamini maisha yao katika mwanga wa neno la Mungu wanaoweza kutoa ushuhuda wa kweli Ulimwenguni. 

Vishawishi vipo. Ni matokeo ya maanguko ya wanadamu wa kwanza. Yanatoka katika udhaifu wetu lakini pia kutoka katika yule muovu. Yesu hakukubali kuanguka katika vishawishi alivyokuwa jangwani na wala hakuanguka katika kishawishi katika maisha yake yote. Aliyashinda na kuteseka kwa ajili ya hayo. Hili linatuambia kwamba anaweza kuwa kiongozi wetu na mfano wetu wa kuiga wakati tukiwa katikati ya vishawishi kila mara na kila siku. Wakati mwingine tunaweza kujisikia wa pweke tuliotengwa katika jangwa la dhambi zetu. Tunaweza kujisikia kama vile mnyama mkali wa tamaa zetu unatushinda. Tunaweza kujisikia yule muovu anatunyemelea. Sawa, Yesu alipatwa na haya pia. Aliruhusu kupitia haya kwa kushiriki ubinadamu wetu. Kwa njia hii ni Yesu anayeweza kukutana nasi katika jangwa letu. Yupo tayari anatusubiri, akitutafuta, akituita sisi. Ni huyu alieyeshinda vishawishi vya muovu jangwani, ndiye atakaye tuongoza kuepuka. Kwahiyo, kama jangwa lako ni mahangaiko ya maisha sasa, au ni majaribu mbali mbali, Yesu anataka kukutana nawe akuongoze katika njia iliyo njema. Alimshinda yule wa jangwani na jinsi alivyokuwa, hivyo anauwezo wakushinda jangwa lolote lile katika maisha yako.

Sala: Bwana, ninakubali upendo wako mkamilifu kwangu. Nina amini kwamba unanipenda mimi kiasi kwamba nitaweza kuvumilia mateso, kuelewa mateso yote. Ninakuomba nikutane nawe katika jangwa la maisha yangu. Ninakuomba nikuruhusu wewe uniongoza katika sehemu tulivu na yenye maji. Yesu nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 22, 2026



MASOMO YA MISA, FEBRUARI 22, 2026
DOMINIKA YA 1 YA KWARESIMA



SOMO 1
Mwa. 2:7 – 9, 3:1 – 7

Bwana Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai. Bwana Mungu akampanda bustani upande wa mashariki wa Edeni, akamweka ndani yake huyo mtu aliyemfanya. Bwana Mungu akachipusha katika ardhi kila mti unaotamanika kwa macho na kufaa kwa kuliwa; na mti wa uzima katikati ya bustani, na mti wa ujuzi wa mema na mabaya.

Basi nyoka alikuwa mwerevu kuliko wanyama wote wa mwitu aliowafanya Bwana Mungu. Akamwambia mwanamke, Ati! Hivi ndivyo alivyosema Mungu, Msile matunda ya miti yote ya bustani?
Mwanamke akamwambia nyoka, Matunda ya miti ya bustanini twaweza kula; lakini matunda ya mti ulio katikati ya bustani Mungu amesema, Msiyale wala msiyaguse, msije mkafa.

Nyoka akamwambia mwanamke, Hakika hamtakufa, kwa maana Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.

Mwanamke alipoona ya kuwa ule mti wafaa kwa chakula, wapendeza macho, nao ni mti wa kutamanika kwa maarifa, basi alitwaa katika matunda yake akala, akampa na mumewe, naye akala. Wakafumbuliwa macho wote wawili wakajijua kuwa wa uchi, wakashona majani ya mtini, wakajifanyia nguo.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 51:1 – 4, 10 – 12, 15

(K) Uturehemu, ee Bwana, kwa kuwa tumetenda dhambi.

Ee Mungu unirehemu,
Sawasawa na fadhili zako.
Kiasi cha wingi wa rehema zako,
Uyafute makosa yangu.
Unioshe kabisa na uovu wangu,
Unitakase dhambi zangu. (K)

Maana nimejua mimi makosa yangu,
Na dhambi yangu I mbele yangu daima.
Nimekutenda dhambi Wewe peke yako,
Na kufanya maovu mbele ya macho yako. (K)

Ee Mungu, uniumbie moyo safi,
Uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu.
Usinitenge na uso wako,
Wala roho yako mtakatifu usiniondolee. (K)

Unirudishie furaha ya wokovu wako;
Unitegemeze kwa roho ya wepesi.
Ee Bwana, uifumbue midomo yangu,
Na kinywa changu kitazinena sifa zako. (K)



SOMO 2
Rum. 5:12 – 19

Kama kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.

Maana kabla ya sheria dhambi ilikuwamo ulimwenguni, lakini dhambi haihesabiwi isipokuwapo sheria; walakini mauti ilitawala tangu Adamu mpka Musa, nayo iliwatawala hata wao wasiofanya dhambi ifananayo na kosa la Adamu, aliye mfano wake yeye atakayekuja. Lakini karama ile haikuwa kama lile kosa; kwa maana ikiwa kwa kukosa kwake yule mmoja wengi walikufa, zaidi sana neema ya Mungu, na kipawa kilicho katika neema yake mwanadamu mmoja Yesu Kristo kimezidi kwa ajili ya wale wengi. Wala kadiri ya yule mtu mmoja aliyefanya dhambi si kadiri ya kile kipawa; kwa maana hukumu ilikuja kwa njia ya mtu mmoja ikaleta adhabu; bali karama ya neema ilikuja kwa ajili ya makosa mengi, ikaleta kuhesabiwa haki.

Kwa maana ikiwa kwa kusa mtu mmoja mauti ilitawala kwa sababu ya yule mmoja, zaidi sana wao wapokeao wingi wa neema, na kile kipawa cha haki, watatawala katika uzima kwa yule mmoja, Yesu Kristo. Basi tena, kama kwa kosa moja watu wote walihukumiwa adhabu, kadhalika kwa tendo moja la haki watu wote walihesabiwa haki yenye uzima. Kwa sababu kama kwa kuasi kwake mtu mmoja watu wengi waliingizwa katika hali ya wenye dhambi, kadhalika kwa kutii kwake mmoja watu wengi wameingizwa katika hali ya wenye haki.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



SHANGILIO
Mt. 4:4

Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.



INJILI
Mt. 4:1 – 11

Kisha Yesu alipandishwa na Roho nyikani, ili ajaribiwe na Ibilisi. Akafunga siku arobaini mchana na usiku, mwisho akaona njaa. Mjaribu akamjia akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, amuru kwamba mawe haya yawe mikate. Naye akajibu akasema, Imeandikwa, Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa ila neno litokalo katika kinywa cha Mungu. Kisha Ibilisi akamchukua mpaka mji mtakatifu, akamweka juu ya kinara cha hekalu, akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu jitupe chini; kwa maana imeandikwa, Atakuagizia malaika zake; na mikononi mwao watakuchukua; Usije ukajikwaa mguu wako katika jiwe.

Yesu akamwambia, Tena imeandikwa, Usimjaribu Bwana Mungu wako. Kisha Ibilisi akamchukua mpaka mlima mrefu mno, akamwonyesha milki zote za ulimwengu, na fahari yake, akamwambia, Haya yote nitakupa, ukianguka kunisujudia. Ndipo Yesu alipomwambia, Nenda zako, Shetani; kwa maana imeandikwa, Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake. Kisha Ibilisi akamwacha; na tazama, wakaja malaika wakamtumikia.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUMTEMBELEA DAKTARI YA MIOYO YETU!



“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Jumamosi, Februari 21, 2026
Jumamosi baada ya Jumatano ya majivu

Isa 58: 9-14;
Zab 86: 1-6;
Lk 5: 27-32


KUMTEMBELEA DAKTARI YA MIOYO YETU!


Roho ya kweli ya Kwaresima ni, kufunga, kutoa sadaka na sala, yote haya yamejengwa juu ya kwenda kinyume na matamanio yetu, na kutamani kuwa na Mungu katika Ufalme wake. Hii haina maana kwamba mmoja anapaswa kuacha kwa muda wa siku 40 ili awasaidie maskini wakati wa Kwaresima tu. Tunapaswa kuelewa nafasi mbali mbali zinazokuja katika maisha yetu ya kila siku. Ni muda pia wa kuacha dhambi na kupokea uponyaji kutoka kwa mganga mtakatifu.

Yesu aliwahitaji wadhambi. Yeye ni mkombozi, na mkombozi aliwahitaji wadhambi ili awakomboe! Kuja kwa Yesu tukiwa na mizigo ya dhambi zetu, inampa furaha katika moyo wake. Anafurahi kwasababu anatimiza ule utume aliotumwa na Baba yake, akionesha kuruma yake kama Mkombozi pekee. Muacha akupe huruma yake! Unafanya hivi kwa kuja kwake katika hali yako ya dhambi na kujinyenyekesha mbele kama asiestahili huruma yake, na ambaye unastahili tu hukumu. Kuja kwa Yesu inamfanya yeye aweze kuonesha huruma yake kutoka katika chemchemi ya huruma yake.

Angalia katika hali ya kwamba Yesu ni Mganga Mtakatifu anayekusubiri ili aweze kutimiza wajibu wake wa kuponya. Anakuhitaji wewe ukubali dhambi zako na kuwa wazi kwa uponyaji wake. Kwa kufanya hivyo, unaruhusu mlango wa huruma yake ufunguke na kumimina baraka kwako na katika kipindi chetu.
               
Sala: Mpendwa Mkombozi na Mganga Mtakatifu, ninakushukuru kwa kuja kutukomboa na kutuponya. Ninakushukuru kwa tamaa yako ya kuonesha huruma yako katika maisha yangu. Naomba uninyenyekeshe niweze kuwa wazi kwa uponyaji wako. Yesu nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 21, 2026





MASOMO YA MISA, FEBRUARI 21, 2026
JUMAMOSI BAADA YA MAJIVU


SOMO 1
Isa. 58:9-14

Bwana asema hivi: Kama ukiiondoa nira; isiwepo kati yako, wala kunyosha kidole, wala kunena maovu; na kama ukimkunjulia mtu mwenye njaa nafsi yako, na kuishibisha nafsi iliyoteswa; ndipo nuru yako itakapopambazuka gizani; na kiwi chako kitakuwa kama adhuhuri.

Naye Bwana atakuongoza daima, ataishibisha nafsi yako mahali pasipokuwa na maji, na kuitia nguvu mifupa yako; nawe utakuwa kama bustani iliyotiwa maji, na kama chemchemi ambayo maji yake hayapungui.

Na watu wako watapajenga mahali palipokuwa ukiwa; utaiinua misingi ya vizazi vingi; nawe utaitwa, Mwenye kutengeneza mahali palipobomoka; na, Mwenye kurejeza njia za kukalia.

Kama ukigeuza mguu wako usiihalifu sabato, usifanye anasa yako siku ya utakatifu wangu; ukiita sabato siku ya furaha, na siku takatifu ya Bwana yenye heshima; ukiitukuza, kwa kutokuzifanya njia zako mwenyewe, wala kuyatafuta yakupendezayo wala kusema maneno yako mwenyewe; ndipo utakapojifurahisha katika Bwana; nami nitakupandisha mahali pa nchi palipoinuka; nitakulisha urithi wa Yakobo baba yako; kwa maana kinywa cha Bwana kimenena hayo.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 86:1-2, 3-4, 5-6 (K) 11

(K) Ee Bwana, unifundishe njia yako;
Nitakwenda katika kweli yako.

Ee Bwana, utege sikio lako unijibu,
Maana mimi ni maskini na mhitaji,
Unihifadhi nafsi yangu,
Maana mimi ni mcha Mungu.
Wewe uliye Mungu wangu,
Umwokoe mtumishi wako anayekutumaini. (K)

Wewe, Bwana, unifadhili,
Maana nakulilia Wewe mchana kutwa.
Uifurahishe nafsi ya mtumishi wako,
Maana nafsi yangu nakuinulia Wewe, Bwana. (K)

Kwa maana Wewe, Bwana, U mwema,
Umekuwa tayari kusamehe,
Na mwingi wa fadhili,
Kw awatu wote wakuitao.
Ee Bwana, uyasikie maombi yangu;
Uisikilize sauti ya dua zangu. (K)



SHANGILIO
Eze. 33:11

Waambie, kama mimi niishivyo, asema Bwana Mungu, Sikufurahii kufa kwake mtu mwovu; Bali aghairi mtu mwovu, na kuiacha njia yake akaishi.



INJILI
Lk. 5:27-32

Siku ile: Yesu akaona mtoza ushuru, jina lake Lawi, ameketi forodhani, akamwambia, Nifuate. Akaacha vyote, akaondoka, akamfuata.

Na Lawi akamfanyia karamu kubwa nyumbani mwake; palikuwa na mkutano mkuu wa watoza ushuru na watu wengineo waliokuwa wameketi chakulani pamoja nao. Ikawa Mafarisayo na waandishi wao kuwanung’unukia wanafunzi wake, wakisema, Mbona mnakula na kunywa pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi? Yesu akajibu akawaambia, Wenye afya hawana haja na tabibu, isipokuwa walio hawawezi. Sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

NJAA KWA AJILI YA MUNGU!




“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Ijumaa, Februari 20, 2026
Ijumaa baada ya Jumatano ya majivu

Isa 58: 1-9;
Zab 51: 3-6, 18-19;
Mk 9: 14-15.

NJAA KWA AJILI YA MUNGU!


“Muda utafika wakati Bwana harusi ataondolewa kwao, ndipo watafunga” (Mt 9:15). Tunaitwa wote kuwa na njaa kwa ajili ya Mungu na ufalme wake. Kufunga kunatusaidia. Yesu analinganisha ujio wa Ufalme wa Mungu ambao aliutangaza na kuuanzisha, na sherehe ya harusi ya Wayahudi. Kufunga wakati wa harusi ingekuwa ajabu kabisa. Kutakuwa na muda wa kufunga baada ya Yesu kuondoka kati ya Wafuasi wake, na kuwaachia wanafunzi wake kazi ya kuukamilisha ufalme wake. Tupo katika kipindi cha kwaresima. Kama Yesu alivyoenda jangwani kufunga na kusali alivyo anza kazi yake ya kutangaza na kuusimika Ufalme wa Mungu, pia tunapaswa kumwomba Mungu neema ya pekee kwa kufunga na kusali tukiwa tunaendelea na kazi ya kuutangaza Ufalme wa Mungu duniani.

Isaya anatueleza mambo muhimu ya kufunga. Kufunga ina hali ya wima na hali ya mlalo (Wima –kwa ajili ya Mungu, mlalo-kwenda kwa wanadamu). Kwanza kabisa, ni kazi ya mtu binafsi, kwa ajili ya mapendo ya Mungu. Tunatoa sadaka si kwasababu ya ukosefu wa chakula, bali tunatoa sadaka kwa vile tunavyo vipenda, ili tuweze kukuwa kwa mapendo kumwelekea Mungu. Pili, hakuna mfungo ulio na matunda mazuri isipokuwa kwa ajili kujali jirani. Tusipo punguza makali ya wale walio wagonjwa, walio na njaa, waliotengwa, tusipokuwa sauti ya wajane, sauti ya Yatima, mfungo wetu hautakuwa na sauti mbele za Mungu. Hivyo, angalao tujifunze kazi moja ya matendo ya huruma, kwa kuwashirikisha yote tunayo jinyima na wale wahitaji. Kwa kufunga chakula tunajifunza ni kwa jinsi ghani njaa inavyouma, na hivyo kuwa na huruma daima kwa wale ambao tunasikia kwamba wana njaa. Hatufungi ili kujilimbikizia kwa baadae bali ili tuwasaidie kile tulichofunga, na isiwe tu baada ya kuwasaidia inakuwa mwisho, bali kwasababu tutakuwa tumejifunza ni kwajinsi ghani njaa inauma, itufanye tuwafikirie daima wale wanao kosa chakula kila wakati. Siku za Ijumaa wakati wa kwaresima ni siku ambazo Kanisa pia linatuhimiza kufanya kitubio. Kitu muhimu katika ijumaa za kipindi cha Kwaresima inapaswa kuwa siku ya majitoleo.

Sala: Bwana, ninachagua siku hii, ili niweze kuwa wamoja pamoja na wewe, katika mateso. Ninaomba majitoleo na matendo yangu ya kujikatalia ninayo kutolea, yawe chanzo cha muunganiko wa ndani pamoja na wewe. Yesu nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, IJUMAA, FEBRUARI 20, 2026




MASOMO YA MISA, IJUMAA, FEBRUARI 20, 2026
IJUMAA BAADA YA MAJIVU


SOMO 1
Isa. 58:1-9

Bwana Mungu asema hivi: Piga kelele, usiache paza sauti yako kama tarumbeta; uwahubiri watu wangu kosa lao, na nyumba ya Yakobo dhambi zao.

Walakini wakinitafuta kila siku; hupenda kujua njia zangu; kama vile taifa waliotenda haki, wasioacha sheria ya Mungu wao, hutaka kwangu amri za haki; hufurahi kumkaribia Mungu. Husema, Mbona tumefunga, lakini huoni? Mbona tumejitaabisha nafsi zetu, lakini huangalii? Fahamuni, siku ya kufunga kwenu mnatafuta anasa zenu wenyewe, na kuwalemea wote watendao kazi kwenu.

Tazama, ninyi mwafunga mpate kushindana na kugombana, na kupiga kwa ngumi ya uvou. Hamfungi siku hii ya leo hata kuiskizisha sauti yenu juu. Je! Kufunga namna hii ni saumu niliyoichagua mimi? Je! Si siku ya mtu kujitaabisha nafsi yake? Ni kuinama kichwa kama unyasi, na kutanda nguo za magunia na majivu chini yake?

Je! Utasema ni siku ya kufunga, na ya kukubaliwa na Bwana. Je! Saumu niliyoichagua, siyo ya namna hii? Kufungua vifungo vya uovu, kuzilegeza kamba za nira, kuwaacha huru walioonewa, na kwamba mvunje kila nira? Je! Siyo kuwagawia wenye njaa chakula chako, na kuwaleta maskini waliotupwa nje nyumbani kwako? Umwonapo mtu aliye uchi, umvike nguo; wala usijifiche na mtu mwenye damu moja nawe?

Ndipo nuru yako itakapopambazuka kama asubuhi, na afya ayko itatokea mara; na haki yako itakutangulia; utukufu wa Bwana utakufuata nyuma ukulinde. Ndipo utaita, na Bwana ataitika; atalia, naye atasema, Mimi hapa.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 51:3-4, 5-6a, 18-19 (K) 17

(K) Moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu, hutadharau.

Maana nimejua mimi makosa yangu,
Na dhambi yangu I mbele yangu daima.
Nimekutenda dhambi Wewe peke yako.
Na kufanya maovu mbele za macho yako. (K)

Tazama, mimi naliumbwa katika hali ya uovu;
Mama yangu alinichukua mimba hatiani.
Tazama, wapendezwa na kweli iliyo moyoni;
Nawe utanijulisha hekima kwa siri. (K)

Uitendee mema Sayuni kwa radhi yako,
Uzijenge kuta za Yerusalemu.
Ndipo utakapopendezwa na dhabihu za haki;
Na sadaka za kuteketezwa, na kafara. (K)


SHANGILIO
Ez. 18:31

Tupilieni mbali nanyi makosa yenu yote mliyoyakosa; Jifanyieni moyo mpya na roho mpya.


INJILI
Mt. 9:14:15

Siku ile: Yesu alipofika ng’ambo, katika nchi ya Wagerasi, wanafunzi wake Yohane wakamwendea, wakasema, Kwa nini sisi na Mafarisayo twafunga, bali wanafunzi wako hawafungi? Yesu akawaambia, Walioalikwa arusini wawezaje kuomboleza, muda bwana arusi akiwapo pamoja nao? Lakini siku zitakuja watakapoondolewa bwana arusi; ndipo watakapofunga.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUIPATA ROHO KWA KUPOTEZA ULIMWENGU!



“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya kwaresima
Alhamisi, Februari 19, 2026
Alhamisi baada ya Jumatano ya majivu

Kum 30: 15-20;
Za 1: 1-4, 6;
Lk 9: 22-25


KUIPATA ROHO KWA KUPOTEZA ULIMWENGU!


Somo la kwanza kutoka katika kumbukumbu la Torati linatufundisha kushika Amri za Mungu kwa kumpenda Mungu, kwa kumtii na kutembea katika njia zake. Kama tutafanya hivyo, tutapokea ahadi zake, ambazo ni uhai na mafanikio. Kwa upande mwingine yule ambaye hamtafuti Mungu anakuwa amechagua kifo na uovu.

Injili inaongelea kuhusu kuchukuwa misalaba yetu na kumfuata Yesu kila siku. Luka anasisitiza “KILA SIKU”, kuonesha umuhimu wakujikita kila siku na kukumbutia misalaba inayopitia katika njia zetu kwa uaminifu na mapendo. Kukumbatia kile ambacho kinaleta uchungu, kisicholipa, kilicho chukiwa na ulimwengu sio rahisi. Hili ndilo alilolifanya Yesu kwa njia ya mateso yake, na kifo juu ya msalaba kwa ajili yetu, akashinda kwa ajili ya wokovu wetu.

Kuchagua maisha ya Imani na ukombozi wa roho zetu inatupasa kuacha mengi ulimwenguni humu. Tunapaswa kuishi katika hali ambayo inatuweka tayari “kuachia yote” hata kama yalikuwa kwa ajili ya faida yetu au kwa ajili ya ukombozi wa wengine. Hili ni ngumu kulifanya na linahitaji mapendo makubwa kwa Mungu. Inatakiwa tuwe tumeridhia wenyewe kutoka ndani, kiasi kwamba kuona utakatifu ni zaidi ya kitu kingine chochote. Usisite kumfanya Mungu kuwa kiini na lengo la maisha yako. Kipindi cha kwaresima ni kipindi muhimu sana cha kuingia ndani na kutazama mitazamo yako na tamaa yako na lengo la maisha yako katika hali ya juu kabisa. Mchague Mungu awe zaidi ya yote na wala hutajutia kufanya kufanya hivyo.

Sala: Bwana, tunapoingia katika kipindi hiki cha kwaresima, nipe neema niweze kutazama juu ya malengo yangu. Nisaidie niweze kuchagua kile kilicho cha muhimu kabisa na kiini cha maisha yangu. Nisaidie nikuchague wewe zaidi ya yote katika maisha yangu ili unisaidie kuendana na mapenzi yako matakatifu. Yesu, nakuamini wewe.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 19, 2026





MASOMO YA MISA, FEBRUARI 19, 2026
ALHAMISI BAADA YA MAJIVU


SOMO 1
Kum. 30:15-20

Musa aliwaambia watu akisema: Aangalia, nimekuwekea leo mbele yako uzima na mema, na mauti na mabaya; kwa hivi nikuagizavyo leo kumpenda Bwana, Mungu wako, kuenenda katika njia zake, na kushika maagizo yake, na amri zake, na hukumu zake, upate kuwa hai na kuongezeka; Bwana, Mungu wako, apate kukubarikia katika nchi uingiayo kuimiliki. Lakini moyo wako ukikengeuka, usipotaka kusikiza, lakini ukavutwa kando kwenda kuabudu miungu mingine, na kuitumikia; nawahubiri hivi leo hakika mtaangamia; hamtazifanya siku zenu kuwa nyingi juu ya nchi, uivukiayo Yoradani, uingie kuimiliki. Nazishuhudiza mbingu na nchi juu yenu hivi leo, kuwa nimekuwekea mbele yako uzima na mauti Baraka na laana; basi chagua uzima, ili uwe hai, wewe na uzao wako; kupenda Bwana, Mungu wako, kuitii sauti yake, na kushikamana naye; kwani hiyo ndiyo uzima wako, na wingi wa siku zako; upate kukaa katika nchi Bwana aliyowaapia baba zako, Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo, kuwa atawapa.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 1:1-4, 6 (K) Zab. 39:5

(K) Heri mtu aliyemfanya Bwana kuwa tumaini lake.

Heri mtu yule asiyekwenda
Katika shauri la wasio haki;
Wala hakusimama katika njia ya wakosaji;
Wala hakuketi barazani pa wenye mizaha.
Bali sheria ya Bwana ndiyo impendezayo,
Na sheria yake huitafakari mchana na usiku. (K)

Naye atakuwa kama mti ulipopandwa
Kandokando ya vijito vya maji,
Uzaao matunda yake kwa majira yake,
Wala jani lake halinyauki;
Na kila alitendalo litafanikiwa. (K)

Sivyo walivyo wasio haki;
Hao ni kama makapi yapeperushayo na upepo.
Kwa kuwa Bwana anaijua njia ya wenye haki,
Bali njia ya wasio haki itapotea. (K)



SHANGILIO
Zab. 130:5

Nimemgnoja Bwana, roho yangu imengoja, na neno lake nimelitumaini. Nafsi yangu inamngoja Bwana, kuliko walinzi waingojavyo asubuhi, naam, walinzi waingojao asubuhi.



INJILI
Lk. 9:22-25

Siku ile: Yesu aliwaambia wafuasi wake kwamba imempasa Mwana wa Adamu kupata mateso mengi na kukataliwa na wazee na wakuu wa makuhani na waandishi, na kuuawa na siku ya tatu kufufuka.

Akawaambia wote, Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake kila siku, anifuate. Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu ndiye atakayeisalimisha. Kwa kuwa yamfaa nini mtu kuupata ulimwengu wote, kama akijiangamiza, na kujipoteza mwenyewe?

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.