Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MUNGU ALIYE NA MSIMAMO NA MWENYE HURUMA





ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumapili, Juni 14, 2026
Juma la 11 la Mwaka


Kut. 19:2-6; 
Rum. 5:6-11; 
Mt. 9:36-10:8


MUNGU ALIYE NA MSIMAMO NA MWENYE HURUMA

Kwenye Injili ya Jumapili hii, Yesu alipowaoona umati wa watu aliwaonea huruma. Walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji au kiongozi. Jumapili hii pia twaadhimisha ukumbusho wa mababa wote. Basi nawatakieni mababa wote heri na mafanikio mema kwa siku kuu yao na tunawaombea wote, walio karibu na wale walio mbali, pamoja na kuwakumbuka wale waliotuacha. Kwa njia ya pekee tuwaombee akina baba kwenye parokia zetu. Nitaanza mahubiri haya kwa hadhithi moja. Kwenye familia mmoja kulikuwa na mtoto mvulana aliyekuwa aliyekuwa na tabia ya kutotii amri za kinyumbani. Basi siku moja baba yule akamwita mtoto wake akamwambia: wakati utakayevunja amri tena nitakufungia nje kwenye ghala. Punde si punde, yule mtoto akavunja amri tena. Ndipo babaye akampeleka mtoto ghalani na kumfungia mle. Baada ya kufanya hivyo baba akahuzunika asile au kunywa chochote. Ndipo mama akamwambia, mimi naelewa vile unavyofikiria. Nakusihi usimtoe mtoto kutoka ghanani, kwa sababu ukimtoa ataendelea kutotii amri zako. Hatakuheshimu kamwe. Baba alifikiria kuelewa kwamba mama amesema hakika. Mwishowe yule baba akamwonea mwanae huruma, na badala ya kumfungulia akachukua blanketi na mikate ya chapati na akaenda kule ghalani kulala naye usiku huo.

Masomo ya Jumapili hii hasa yatufumbulia Mungu aliye kama yule baba kwenye hadithi kwa ajili ya msimamo wake na pia huruma wake.Kwenye Somo la Kwanza, Mungu Musa anatangaza ujumber wa Mungu kwa Waisraeli. “Ikiwa mtasikiliza sauti yangu na kufuata agano langu mtakuwa watu wangu wa maana sana.” Mungu ana msimamo, na anatuita tumsikilize na kuzijali ahadi tulioweka naye wakati wa Ubatizo wetu. Mungu angetaka tuseme ukweli, tuwaheshimu wazazi wetu na tuhudhurie Misa Jumapili. Lakini badala ya kumsikiliza Mungu tunasikiliza sauti zingine. Wakati tuangukapo Mungu hutuonyesha kwamba anamsimamo, kwa sababu angetaku kuturudisha kwenye njia ya kweli na katika neema yake. Mtk Paulo kwenye Somo la Pili anatuonyesha kwamba wakati tulikuwa bado katika maasi yetu na Mungu, Mungu alituma Mwanae kutukomboa. Kama vile tunasikia kwenye Injili, Yesu aliona umati wa watu wakiwa na ulegevu wa kimwili na wa kiroho. Walikuwa kama kondoo bila mchungaji na bila kujua jinsi wangejipatia chakula cha kiroho. Tungesema kwamba barani Afrika twajikuta katika hali kama ile ya wakati wa Yesu. Hivi leo twaendelea kuvunja amri za Mungu na kutoitii Kanisa kama yule mtoto kwenye hadithi. Lakini Mungu katika Mwanae Yesu anatuonyesha msimamo wake na pia ana huruma. Anakuja kwetu kama yule baba alifanya kutuonyesha huruma wake na kutualika turudi katika neema yake. 

Ujumbe: 
1) Mungu ana msimamo na huruma kama yule baba kwenye hadithi; 
2) Mungu huzingatia tuisikilize sauti yake na sio sauti zingine; 
3) Wakati tulio katika maasi, Mungu hutuma Mwanae kama mchungaji kuturudisha katika neema yake.



Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUNI 14, 2026




MASOMO YA MISA, JUNI 14, 2026
JUMAPILI, JUMA LA 11 LA MWAKA


SOMO 1 
Kut. 19 :2-6

Waisraeli walipokuwa wameondoka Refidimu na kufika jangwa la Sinai, wakatua katika lile jangwa; wakapiga kambi huko wakiukabili mlima. Musa akapanda kwa Mungu, na Bwana akamwita toka mlima ule, akisema, Utawaambia nyumba ya Yakobo, na kuwaarifu wana wa Israeli, maneno haya: Mmeona jinsi nilivyowatendea Wamisri, na jinsi nilivyowachukua ninyi juu ya mbawa za tai, nikawaleta ninyi kwangu mimi. Sasa basi ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli, na kulishika agano langu, hapo ndipo mtakapokuwa tunu kwangu kuliko makabila yote ya watu; maana dunia yote pia ni mali yangu, nanyi mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani, na taifa takatifu.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 100 :2-3, 5 (K) 3

(K) Tu watu wake, na kondoo wa malisho yake.

Mtumikieni Bwana kwa furaha;
Njoni mbele zake kwa kuimba. (K)

Jueni kwamba Bwana ndiye Mungu;
Ndiye aliyetuumba na sisi tu watu wake;
Tu watu wake, na kondoo wa malisho yake. (K)

Kwa kuwa Bwana ndiye mwema;
Rehema zake ni za milele;
Na uaminifu wake vizazi na vizazi. (K)


SOMO 2 
Rum. 5 : 6-11

Wapendwa, hapo tulipokuwa hatuna nguvu, wakati ulipotimia, Kristo alikufa kwa ajili ya waovu. Kwa kuwa ni shida mtu kufa kwa ajili ya mtu mwenye haki; lakini yawezekana mtu kuthubutu kufa kwa ajili ya mtu aliye mwema. Bali Mungu aonyesha pendo lake veye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi. Basi zaidi sana tukiisha kuhesabiwa haki katika damu yake, tutaokolewa na ghadhabu kwa yeye. Kwa maana ikiwa tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kwa mauti ya Mwana wake, zaidi sana baada ya kupatanishwa tutaokolewa katika uzima wake. Wala si hivyo tu, ila pia twajifurahisha katika Mungu kwa Bwana wetu Yesu Kristo, am have kwa yeye sasa tumeupokea huo upatanisho.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


SHANG1LIO 
Yn. 15 :15

Aleluya, aleluya, Ninyi nimewaita rafiki, kwa kuwa yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu.
Aleluya.


INJILI 
Mt. 9:36-10:8

Yesu alipowaona makutano, aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji. Ndipo alipowaambia wanafunzi wake, Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache. Basi mwombeni Bwana wa mavuno, apeleke watenda kazi katika mavuno yake. Akawaita wanafunzi wake kumi na wawili, akawapa amri juu ya pepo wachafu, wawatoe, na kupoza

magonjwa yote na udhaifu wa kila aina. Na majina ya hao mitume kumi na wawili ni haya; Wa kwanza Simoni aliyeitwa Petro, na Andrea nduguye; Yakobo wa Zebedayo, na Yohane nduguye; Filipo, na Bartholomayo; Tomaso, na Mathayo mtoza ushuru; Yakobo wa Alfayo, na Thadayo; Simoni Mkananayo, na Yuda Iskariote, naye ndiye mwenye kumsaliti. Hao Thenashara Yesu aliwatuma, akawaagiza, akisema, Katika njia ya Mataifa msiende, wala katika mji wo wote wa Wasamaria msiingie. Afadhali shikeni njia kuwaendea kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli. Na katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme wa mbinguni umekaribia. Pozeni wagonjwa, fufueni wafu, takaseni wenye ukoma, toeni pepo; mmepata bure, toeni bure.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MOYO ULIYO SAFI!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Ijumaa, Juni 13, 2026
Juma la 10 la Mwaka wa Kanisa

1Fal 19: 9, 11-16; 
Zab. 16:1-2, 5, 7-10; 
Mt 2: 41-51


MOYO ULIYO SAFI!

Tukiangalia katika somo la Injili ya leo tunaweza kushangazwa na maneno makali ya Yesu. “ngoa jicho lako” au “ukate mkono wako na kuutupa mbali”. Yesu alitumia lugha hii kali ili aweze kuweka mbele ya wafuasi lengho moja katika maisha ambalo ni maisha safi ya sadaka- hii ikiwa ni muunganiko wa matakwa yetu na Mungu. Kama Daktari anavyoweza kuondoa mguu au sehemu ya mwili kwamanufaa ya mwili mzima, nasi pia tunapaswa tuwe tayari kuachana na kile kinachoweza kutufanya tutende dhambi, na ambacho kwa njia yeyote kitatuletea kifo cha roho zetu. Yesu pia anatuonya sisi pia tuwe na jukumu kubwa la kutokuwa kikwazo au kisababishi cha kuwafanya wengine watende dhambi, au kuwaangusha, tusiwe kipingamizi au tusitoe mfano mbaya ambao utawaongoza wengine kwenye dhambi. 

Pili, Yesu anatufundisha kwamba kuwa safi ni pamoja nakuwa tayari kukabili kila hali katika maisha katika hali ambayo inatimiza sheria ya Mungu, si tu katika matendo ya njee bali naya ndani pia. Yesu anasema tamaa mbaya hutoka moyoni. Ndio maana dhambi yakukosa uaminifu ni lazima itibiwe kwanza kutoka ndani ya moyo, sehemu ambayo si ya hisia tuu, bali utashi, maamuzi, mawazo, na malengo pia. Ni lazima tutambue lengho la Amri za Mungu na tuamue kutoka moyoni kumfuata Mungu. 

Sala: Baba wa Mbinguni, nitakase mimi, ili niweze kufanana na Kristo mwanao kwa maisha yangu. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JUNI 13, 2026




MASOMO YA MISA, JUNI 13, 2026
JUMAMOSI, JUMA LA 10 LA MWAKA

SOMO 1
1Fal 19:19-21

Eliya aliondoka huko, akamkuta Elisha mwana wa Shafati, aliyekuwa akilima, mwenye jozi za ng’ombe kumi na mbili mbele yake, nay eye mwenyewe alikuwa pamoja na lile la kumi na mbili. Eliya akapita karibu naye, akatupa vazi lake juu yake. Naye akawaacha ng’ombe, akamfuata Eliya mbio, akasema, Nipe ruhusa, nakuomba, nimbusu baba yangu na mama yangu, kisha mimi nitakufuata. Akamwambia, Enenda urudi; ni nini niliyokutendea. Akarudi akiacha kumfuata, akatwaa lile jozi la ng’ombe, akawachinja, akatokosa nyama zao kwa ile miti ya ng’ombe, akawapa watu, wakala. Kisha akainuka, akamfuata Eliya, akamhudumia.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 16:1-2, 5, 7-10 (K) 5

(K) Bwana ndiye fungu la posho langu, na la kikombe changu.

Mungu, unihifadhi mimi,
Kwa maana nakukimbilia Wewe.
Nimemwambia Bwana, Ndiwe Bwana wangu;
Sina wema ila utokao kwako. (K)

Nitamhimidi Bwana aliyenipa shauri,
Naam, mtima wangu umenifundisha usiku.
Nimemweka Bwana mbele yangu daima,
Kwa kuwa yuko kuumeni kwangu, sitaondoshwa. (K)

Kwa hiyo moyo wangu unafurahi,
Na utukufu wangu unashangilia,
Naam mwili wangu nao utakaa kwa kutumaini.
Maana hutakuachia kuzimu nafsi yangu,
Wala hutamtoa mtakatifu wako aone uharibifu. (K)


SHANGILIO
Lk 2:19

Aleluya, aleluya
Abarikiwe Bikira Mariamu aliyeyaweka maneno hayo yote, akiyafikiri moyoni mwake.
Aleluya


INJILI
Lk 2: 41-51

Wazee wake huenda Yerusalemu kila mwaka, wakati wa sikukuu ya Pasaka. Na alipopata umri wake miaka kumi na miwili, walipanda kama ilivyokuwa desturi ya sikukuu; na walipokwisha kuzitimiza siku, wakati wa kurudi kwao, yule mtoto Yesu alibaki nyuma huko Yerusalemu, na wazee wake walikuwa hawana habari. Nao wakadhani ya kuwa yumo katika msafara; wakaenenda mwendo wa kutwa, wakawa wakimtafuta katika jamaa zao na wenzao; na walipomkosa, wakarejea Yerusalemu, huku wakimtafuta. Ikawa baada ya siku tatu wakamwona hekaluni, ameketi katikati ya waalimu, akiwasikiliza na kuwauliza maswali. Nao wote waliomsikia walistaajabia fahamu zake na majibu yake. Na walipomwona walishangaa, na mama yake akamwambia, Mwanangu, mbona umetutenda hivi? Tazama, baba yako na mimi tulikuwa tukikutafuta kwa huzuni. Akawaambia, Kwani kunitafuta? Hamkujua ya kuwa imenipasa kuwamo katika nyumba ya Baba yangu? Nao hawakuelewa na neno hilo alilowaambia. Akashuka pamoja nao mpaka Nazareti, naye alikuwa akiwatii; na mamaye aliyaweka hayo yote moyoni mwake.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MOYO UNAO WAKA MAPENDO!



⁠⁠⁠⁠⁠“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Kila Siku
Ijumaa, Juni 12, 2026,
Juma la 10 la Mwaka wa Kanisa

Sherehe ya Moyo Mtakatifu wa Yesu

Kumb 7: 6-11;
Zab 103: 1-4;
1 Yn 4: 7-16;
Mt 11: 25-30


MOYO UNAO WAKA MAPENDO!


“Huu ni upendo si kwamba sisi tulimpenda Mungu kwanza bali yeye alitupenda sisi kwanza akamtuma mwanaye ulimwenguni kama sadaka kwaajili ya dhambi zetu” (1 Yn 4: 10). Sherehe ya Moyo Mtakatifu wa Yesu ni sherehe ya upendo wa ukombozi wa Mungu wetu. Mungu anayetupenda alimtoa mwanaye aje ulimwenguni kama sadaka kwaajili ya ukombozi wa Ulimwengu. Upendo huu unaoneshwa katika moyo wa mwana wa Mungu. Neno “moyo” linasimama kama upendo wa mtu. Na hivyo watu husema “Nakupenda kwa moyo wangu wote” na wakati tunapo sheherekea sikukuu ya Moyo Mtakatifu wa Yesu kanisa linatuhimiza kutafakari juu ya upendo wa Mungu, upendo uliofunuliwa ndani ya mwili wa Mwanaye Yesu Kristo.

Ni Mungu aliyewachagua wa Israeli kuwa watu wake. Aliwabariki na akawachagua kuwa watu wake kati ya mataifa mengi. Si kwasababu walikuwa na nguvu kuliko wengine lakini kwasababu ya upendo wake. Hili ndilo Musa alilowafundisha watu wa Israeli. Anawakumbusha juu ya upendo wa Mungu juu yao. Upendo wa Mungu kwa watu wake hauna mwisho na hauna masharti. Aliwapenda watu wake pamoja na mapungufu yao na makosa yao. Na hata hivyo ubinadamu uliponaswa na dhambi alimtoa mwanaye wa pekee kwajili yetu. Kwahiyo tunapaswa kuuzoea nakuupenda upendo huu ili tuweze kuuelewa zaidi na kuwa watu wakweli wanotamani kuwa na Mungu daima. Ili tuweze kumpenda kwa moyo wetu wote na akili yetu zote.

Kwahiyo katika sikuu hii ya moyo Mtakatifu wa Yesu, tunamshukuru Mungu kwa upendo wake mkubwa kwetu anaotuonesha kila siku. Tuupende na kuushi upendo huu ndani mwetu ili tuweze kuwashirikisha na wengine.

SALA: Moyo Mtakatifu wa Yesu, utuhurumie. Ninakushukuru Bwana wangu kwa kunipa yote hayo. Hakuficha kitu kwangu na unaendelea kunigawia maisha yako kwa ajili yangu na kwa ajili ya ulimwengu mzima. Ninaomba nipokee yote unayonipa bila kubakiza chochote kutoka kwako. Yesu, nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JUNI 12, 2026




MASOMO YA MISA, JUNI 12, 2026
IJUMAA, JUMA LA 10 LA MWAKA

SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU


SOMO 1
Kum. 7:6 - 11

Musa aliwaambia makutano: Kwa maana wewe u taifa takatifu kwa Bwana Mungu wako; Bwana, Mungu wako, amekuchagua kuwa watu wake hasa, zaidi ya mataifa yote walioko juu ya uso wa nchi.

Bwana hakuwapenda ninyi, wala hakuwachagua ninyi, kwa sababu mlikuwa wengi kuliko mataifa yote, maana mlikuwa wachache kuliko watu wote; bali kwa sababu Bwana anawapenda, na kwa sababu alitaka kuutimiza uapo wake aliowaapia baba zenu, ndiyo sababu Bwana akawatoa kwa mkono wa nguvu, akawakomboa katika nyumba ya utumwa katika mkono wa Farao, mfalme wa Misri.

Basi, jueni ya kuwa Bwana, Mungu wenu, ndiye Mungu; Mungu mwaminifu, ashikaye agano lake na rehema zake kwao wampendao, na kushika amri zake, hata vizazi elfu; naye huwalipa wamchukiao mbele ya uso wao, ili kuwangamiza. Hatakuwa mlegevu kwake yeye amchukiaye, atamlipa mbele ya uso wake. Basi zishike amri, na sheria, na hukumu ninazoamuru leo, uzitende.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 103:1 – 4, 6 – 8, 10 (K) 17

(K) Fadhili za Bwana zina wamchao, tangu milele hata milele.

Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana,
Naam, vyote vilivyo ndani yangu
Vilihimidi jina lake takatifu.
Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana,
Wala usizisahau fadhili zake zote. (K)

Akusamehe maovu yako yote,
Akuponya magonjwa yako yote,
Aukomboa uhai wako na kaburi,
Akutia taji ya fadhili na rehema. (K)

Bwana ndiye afanyaye mambo ya haki,
Na hukumu kwa wote wanaoonewa.
Alimjulisha Musa njia zake,
Wana wa Israeli matendo yake. (K)

Bwana amejaa huruma na neema,
Haoni hasira upesi, ni mwingi wa fadhili.
Hakututenda sawasawa na hatia zetu,
Wala hakutulipa kwa kadiri ya maovu yetu. (K)



SOMO 2
1Yoh. 4:7 – 16

Wapenzi na tupendane, kwa kuwa pendo latoka kwa Mungu, na kila apendaye amezaliwa na Mungu, naye anamjua Mungu. Yeye asiyependa, hakumjua Mungu, kwa maana Mungu ni upendo. Katika hili pendo la Mungu lilionekana kwetu, kwamba Mungu amemtuma Mwanawe pekee ulimwenguni, ili tupate uzima kwa yeye. Hili ndilo pendo, si kwamba sisi tulimpenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda sisi, akamtuma Mwanawe kuwa kipatanisho kwa dhambi zetu. Wapenzi, ikiwa Mungu alitupenda sisi hivi, imetupasa na sisi kupendana. Hakuna mtu aliyemwona Mungu wakati wowote. Tukipendana, Mungu hukaa ndani yetu, na pendo lake limekamilika ndani yetu. Katika hili tunafahamu ya kuwa tunakaa ndani yake, naye ndani yetu, kwa kuwa ametushirikisha Roho wake. Na sisi tumeona na kushuhudia ya kuwa Baba amemtuma Mwana kuwa Mwokozi wa ulimwengu. Kila akiriye ya kuwa Yesu ni Mwana wa Mungu, Mungu hukaa ndani yake, naye ndani ya Mungu. Nasi tumelifahamu pendo alilo nalo Mungu kwetu sisi, na kuliamini. Mungu ni upendo, naye akaaye katika pendo, hukaa ndani ya Mungu, na Mungu hukaa ndani yake.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



SHANGILIO
Mt. 11:29

Aleluya, aleluya,
Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu, kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo.
Aleluya.



INJILI
Mt. 11:25-30

Wakati ule Yesu alijibu, akasema, Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga. Naam, Baba, kwa kuwa ndiyvo ilivyopendeza mbele zako. Akasema, Nimekabidhiwa vyote na baba yangu; wala hakuna amjuaye Mwana, ila Baba; wala hakuna amjuaye Baba, ila Mwana na yeyote ambaye Mwana apenda kumfunulia.

Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

PEANENI MOYO!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Alhamisi, Juni 11, 2026 
Juma la 10 la Mwaka

Kumbukumbu ya Mt. Barnaba Mtume.


Mdo 11: 21-26, 13: 1-3; 
Zab 98: 1-6; 
Mt 5: 13-16


PEANENI MOYO!


Barnaba alikuwa mtu muhimu katika kanisa la mwanzo, ingawaje sio mmoja wa wale mitume kumi na mbili aliyokuwa nao Yesu katika karamu ya mwisho, yeye alipata cheo cha mtume. Uwepo wake unaonekana kuwa muhimu katika sura kumi na tano za mwanzo za kitabu cha Matendo ya mitume. Aliuza mali zake zote na akaleta yote kwa mitume (Mdo 4: 37). Alikuwa akijulikana kama Yosefu kutoka Cyprus, lakini mitume walimpa jina la Barnaba ( maana yake mwana wa kutia moyo), ukweli uliopo katika jina hii, aliwatia moyo watu wa Yerusalemu wa mpokee Saulo kwasababu sio tena mtesi wa kanisa baada ya kuongoka (Mdo 9: 27). Wakati idadi kumbwa ya Wasamaria ilipo ongoka nakupokea Ukristo katika Antokia ya Siria, Jumuiya ya Yerusalemu walimtuma kwenda Antokia kuhakikisha na kuangalia hali halisi. Barnaba aliijua neema ya Mungu alipoona na kuwatia moyo jumuiya hii mpya kwa maendeleo mazuri (Mdo 11: 19-26).

Jumuiya ya Antokia waliwachagua Paulo na Barnaba kuwa watu wakwanza kwa safari ya kimisionari, kutoka kati ya “manabii na walimu” ili wafanye kazi ya Roho Mtakatifu (Mdo 13 na 14). Katika utume Barnaba alifuatana na Paulo mtu wa haki. Ingawaje baadae kulikuwa na mgongano kati yao. Waligawa jumuiya walizo zianzisha. Katika hili tunaona ubinadamu kama sisi katika nguvu na madhaifu. Tukijikita wenyewe katika kazi ya Mungu, Roho Mtakatifu atatutumia mpaka mwisho wa kilele cha nguvu zetu, licha ya madhaifu yetu.


Mt. Barnaba anatufundisha kitu katika maisha yetu kama wafuasi wa Kristo, tuwe na moyo wa kushirikisha yale aliyotujalia Mungu pasipo choyo. Tuwe tayari kuwatazama jirani zetu kwa yale aliotujalia Mungu. Barnaba aliuza yote aliokuwa nayo akaleta kwa Mitume ili jumuiya yote ya waumini iweze kufaidika kwa majitoleo yake. Katika jumuiya zetu ndogo ndogo wakati mwingine tunasali pamoja, tunacheka pamoja baada ya sala na kupanga mipango mbali mbali. Pengine tujiulize katika mipango yetu tunapata muda wa kuwajali maskini na wasio jiweza walio kati yetu? Na pengine tumesali nao? Au tunafurahi kucheka nao bila kujali wanaishi je? Na pengine mnapotofautiana katika mawazo mnatafuta njia sahihi ya kurudisha tena upendo kati yenu? Au mnaishi kwakununiana ili mradi nimekuja tuu jumuiya nimeonekana ili na wao waje kwangu kipindi kingine? Ndugu zangu, mipango yetu katika jumuiya zetu isimtenge mtu au kumuona mmoja kati yetu ni bora zaidi ya mwingine. Tufanye yote kwa umoja tukiwajali wale wasio nacho kama jumuiya ya kwanza ya Yerusalemu. Tuwe kama Barnaba tuwafariji wengine na kuona uzuri pia ndani ya wengine, tuwape moyo ili wasikate tamaa. Mungu amatupa vipaji tofauti tuviunganishe vyote kwa pamoja ili vikamilishane vijenge jumuiya yenye nguvu, mmoja asijione kuwa yeye ndio kila kitu. Tushirikiane kwa upendo tukichukuliana kwa furaha na Amani ili ufalme wa Mungu uwe kati yetu.


Sala: Nisaidie mimi Bwana, niwatie moyo na kushirikiana na wenzangu katika kujenga kanisa lako. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, ALHAMISI, JUNI 11, 2026



MASOMO YA MISA, 
ALHAMISI, JUNI 11, 2026
JUMA LA 10 LA MWAKA

KUMBUKUMBU YA MTUME BARNABA


SOMO 1
Mdo 11:21-26, 13:1-3

Watu wengi waliamini, wakamwelekea Bwana. Habari hizo za watu hao zikafika masikioni mwa kanisa lililokuwako katika Yerusalemu; wakamtuma Baranaba, aende hata Antiokia. Naye, alipokwisha kufika na kuiona neema ya Mungu akafurahi, akawasihi wote wawaambatane na Bwana kwa kusudi la moyo. Maana alikuwa mtu mwema amejaa Roho Mtakatifu na Imani; watu wengi wakaongezeka upande wa Bwana.

Kasha akatoka akaenda Tarso kumtafuta Sauli; hata alipokwisha kumwona akamleta Antiokia. Ikawa kwa muda wa mwaka mzima wakakusanyika pamoja na kanisa na kuwafundisha watu wengi. Na wanafunzi waliitwa Wakristo kwanza hapo Antiokia.

  Na huko Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli. Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi niliyowaitia. Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 98:1-6 (K) 2

(K) Bwana ameufunua wokovu wake machoni pa mataifa.

Mwimbieni Bwana wimbo mpya,
Kwa maana ametenda mambo ya ajabu.
Mkono wa kuume wake mwenyewe,
Mkono wake mtakatifu umemtendea wokovu. (K)

Bwana ameufunua wokovu wake,
Machoni pa mataifa ameidhihirisha haki yake.
Amezikumbuka rehema zake,
Na uaminifu wake kwa nyumba ya Israeli. (K)

Miisho yote ya dunia imeuona
Wokovu wa Mungu wetu.
Mshangilieni Bwana, nchi yote,
Inueni sauti, imbeni kwa furaha, imbeni zaburi. (K)

Mwimbieni Bwana zaburi kwa kinubi,
Kwa kinubi na sauti ya zaburi.
Kwa panda na sauti ya baragumu.
Shangilieni mbele za Mfalme, Bwana. (K)


SHANGILIO
Aleluya, aleluya,
Ee Mungu, tunakusifu, tunakukiri kuwa Bwana.
Jamii tukufu ya mitume inakusifu.
Aleluya.


INJILI
Mt 5:13-16

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Ninyi ni chumvi ya dunia; lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena kabisa, ila kutupwa nje na kukanyagwa na watu. Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima. Wala watu hawawashi taa na kuiweka chini ya pishi, bali juu ya kiango; nayo yawaangaza wote waliomo nyumbani. Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

SHERIA YA UPENDO!


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatano, Juni, 10, 2026, 
Juma la 10 la Mwaka wa Kanisa

1Fal 18:20-39; 
Zab16: 1-2, 4-5, 8, 11; 
Mt 5:17-19.


SHERIA YA UPENDO!


Katika Injili ya leo, Yesu kwa hakika anawahakikishia wanaomsikiliza kwamba, “hakuja kutengua sheria na manabii. Nimekuja si kutengua bali kuikamilisha”. Yesu alikuja si kuifuta sheria bali aiinue katika hali ya juu ya ukamilifu. Mtazamo wa Yesu unatusaidia tuione sheria katika mwanga mpya. Maneno yake ni kwa ajili ya kufariji lakini pia yanaleta changamoto, akionesha njia inayoenda juu sana kuliko sheria mpaka kwenye sheria ya Upendo. Sheria isiyo na upendo haiwezi kulinda utu na maisha ya mwanadamu. Inamfanya mwanadamu awe kama aina fulani ya kitu kisicho na uhai. Yesu anatutaka tuwe na upendo zaidi. Pengine wakati mwingine tunasisitiza mno sheria kiasi cha kushindwa kuonesha upendo na msamaha kwa wengine.

Katika maisha yetu, tunapaswa kuwa tayari kusonga mbele tukiwa wabunifu wa njia mpya za kuweza kutufanya tuelewe na kuishi Imani yetu zaidi. Tamaduni zetu na mapokeo yetu ni mazuri na tusiyapoteze lakini pia tutumie hali hiyo hiyo katika kuelewa na kuangalia hitaji la sasa. 

Sala: Bwana Yesu, ifanye imani yetu iwe mpya kila siku katika mwanga wa sheria zetu na mapokeo yetu na katika njia ya sheria ya Upendo. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JUNI 10, 2026



MASOMO YA MISA, JUNI 10, 2026
JUMATANO, JUMA LA 10 LA MWAKA


SOMO 1
1 Fal. 18:20-39

Ahabu akapeleka watu kwa wana wa Israeli wote, akawakusanya manabii pamoja katika mlima wa Karmeli. Naye Eliya akawakaribia watu wote, akanena, Mtasitasita katikati ya mawazo mawili hata lini? Bwana akiwa ndiye Mungu, mfuateni; bali ikiwa Baali ni Mungu, haya! Mfuateni yeye. Wale watu hawakumjibu neno.

Ndipo Eliya akawaambia watu, Mimi nimesalia, mimi peke yangu, nabii wa Bwana; lakini manabii wa Baali ni watu mia nne na hamsini. Kwa hiyo na watutolee ng’ombe wawili; wao na wajichagulie ng’ombe mmoja, wamkatekate na kumweka juu ya kuni, wasitie moto chini; name nitamtengeza huyo ng’ombe wa pili, na kumweka juu ya kuni, wala sitatia moto chini. Nayi ombeni kwa jina la mungu wenu, name nitaomba kwa jina la Bwana; na Mungu yule ajibuye kwa moto, na awe ndiye Mungu. Watu wote wakajibu wakasema, Maneno haya ni mazuri.

Eliya akawaambia manabii wa Baali, Jichagulieni ng’ombe mmoja, mkamtengeze kwanza; maana ninyi ndio wengi; mkaliitie jina la mungu wenu, wala msitie moto chini. Wakamtwaa yule ng’ombe waliyepewa, wakamtengeza, wakaliitia jina la Baali tangu asubuhi hata adhuhuri, wakisema, Ee Baali, utusikie. Lakini hapakuwa na sauti, wala aliyejibu. Nao wakaruka-ruka juu ya madhabahu waliyoifanya. Ikawa, wakati wa adhuhuri, Eliya akawafanyia dhihaka, akasema, Mwiteni kwa sauti kuu; maana ni mungu huyo; labda anazungumza, au ana shughuli, au anasafiri, au labda amelala, sharti aamshwe. Wakapiga kelele, wakajikatakata kwa visu na vyembe kama ilivyo desturi yao, hata damu ikawachuruzika. Ikawa, wakati wa adhuhuri ulipopita, walitabiri hata wakati wa kutoa dhabihu ya jioni; lakini hapakuwa na sauti, wala aliyejibu, wala aliangalia.

Kisha Eliya akawaambia watu wote, nikaribieni mimi. Watu wote wakamkaribia. Akaitengeneza madhabahu ya Bwana iliyovunjika. Eliya akatwaa mawe kumi na mawili, kwa hesabu ya kabila za wana wa Yakobo, aliyejiliwa na neno la Bwana na kuambiwa, Jina lako litakuwa Israeli. Naye akaijenga madhabahu kwa mawe hayo katika jina la Bwana; akafanya mfereji, kama wa vipimo viwili vya mbegu, ukiizunguka madhabahu. Kasha akazipanga zile kuni, akamkata yule ng’ombe vipande vipande, akaviweka, juu ya kuni. Akasema, Jazeni mapipa manne maji, mkayamwage juu ya sadaka ya kuteketezwa, juu ya kuni. Akasema, Jazeni mapipa mnne maji, mkayamwage juu ya sadaka ya kuteketezwa, na juu ya kuni. Akasema, Fanyeni mara ya pili. Wakafanya mara ya pili. Akasema, Fanyeni mara ya tatu. Wakafanya mara ya pili. Akasema, Fanyeni mara ya tatu. Wakafanya mara ya tatu. Yale maji yakaizunguka madhabahu; akaujaza mfereji maji.
Ikawa, wakati wa kutoa dhabihu ya jioni, Eliya nabii akakaribia, akasema, Ee Bwana, Mungu wa Ibrahimu, na wa Isaka, na wa Israeli, na ijulikane leo ya kuwa wewe ndiwe Mungu katika Israeli, nay a kuwa mimi ni mtumishi wako, nay a kuwa nimefanya mambo haya yote kwa neno lako. Unisikie, Ee Bwana, unisikie, ili watu hawa wajue ya kuwa wewe, Bwana, ndiwe Mungu, nay a kuwa wewe umewageuza moyo wakurudie.
Ndipo moto wa Bwana ukashuka, ukaiteketeza sadaka ya kuteketezwa, na kuni, na mawe, na mavumbi, ukayaramba yale maji yaliyokuwamo katika mfereji. Na watu wote walipoona, wakaanguka kifudifudi wakasema, Bwana ndiye Mungu, Bwana ndiye Mungu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 16:1-2, 4-5, 8-11 (K) 1

(K) Mungu, unihifadhi mimi, kwa maana nakukimbilia Wewe.

Mungu, unihifadhi mimi, 
Kwa maana nakukimbilia Wewe.
Nimemwambia Bwana, ndiwe Bwana wangu,
Sina wema ila utokao kwako. (K)

Huzuni zao zitaongezeka
Wambadilio mungu kwa mwingine;
Sitazimimina sadaka zao za damu,
Wala kuyataja majina yao midomoni mwangu. (K)

Bwana ndiye fungu la posho langu,
Na la kikombe changu;
Wewe unaishika kura yangu.
Nimemweka Bwana mbele yangu daima,
Kwa kuwa yako kuumeni kwangu sitaondoshwa. (K)

Utanijulisha njia ya uzima,
Mbele za uso wako ziko furaha tele.
Na katika mkono wako wa kuume,
Mna mema ya milele. (K)


SHANGILIO
Zab. 27:11

Aleluya, aleluya,
Ee Bwana, unifundishe njia yako, na kuniongoza katika njia iliyonyoka.
Aleluya.


INJILI
Mt. 5:17-19

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza. Kwa maana, amin, nawaambia, mpaka mbingu nan chi zitakapoondoka, yodi moja wala nukata moja ya torati haitaondoka, hata yote yatimie. Basi mtu yeyote atakayevunja amri moja katika hizi zilizo ndogo, na kuwafundisha watu hivyo, ataitwa mdogo kabisa katika ufalme wa mbinguni; bali mtu atakayezitenda na kuzifundisha, huyo ataitwa mkubwa katika ufalme wa mbinguni. 

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.