Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MASOMO YA MISA JUNI 5, 2026

 



MASOMO YA MISA JUNI 5, 2026
ALHAMISI, JUMA LA 9 LA MWAKA

KUMBUKUMBU YA MTAKATIFU BONIFASI, ASKOFU NE MFIADINI

SOMO 1 
2 Tim. 3 :10-17

Wewe umeyafuata mafundisho yangu, na mwenendo wangu, na makusudi yangu, na imani, na uvumilivu, na upendo, na saburi; tena na adha zangu na mateso, mambo yaliyonipata katika Antiokia, katika Ikonio, na katika Listra, kila namna ya adha niliyoistahimili; naye Bwana aliniokoa katika hayo yote. Naam, na wote wapendao kuishi maisha ya utauwa katika Kristo Yesu wataudhiwa. Lakini watu wabaya na wadanganyaji wataendelea, na kuzidi kuwa waovu, wakidanganya na kudanganyika.

Bali wewe ukae katika mambo yale uliyofundishwa na kuhakikishwa, kwa maana unajua ni akina nani ambao ulijifunza kwao; na ya kuwa tangu utoto umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu. Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, Iafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 119 : 157, 160-161, 165-166, 168 (K) 165

(K) Wana amani nyingi waipendao sheria yako.

Wanaonifuatia na watesi wangu ni wengi, 
lakini sikujiepusha na shuhuda zako.
Jumla ya neno lako ni kweli,
na kila hukumu ya haki yako ni ya milele. (K)

Wakuu wameniudhi bure,
ila moyo wangu unayahofia maneno yako.
Wana amani nyingi waipendao sheria yako, 
wala hawana la kuwakwaza. (K)

Ee Bwana, nimeungojea wokovu wako, 
na maagizo yako nimeyatenda.
Nimeyashika mauasi yako na shuhuda zako, 
maana njia zangu zote zi mbele zako. (K)


SHANGILIO 
Zab. 111 :7, 8

Aleluya, aleluya, Maagizo yako yote, ee Bwana, ni amini, yamethibitika milele na milele. Aleluya.


INJILI 
Mk. 12:35-37

Yesu alipokuwa akifundisha katika hekalu, alijibu, akasema, Husemaje waandishi ya kwamba Kristo ni Mwana wa Daudi? Daudi mwenyewe alisema, kwa uweza wa Roho Mtakatifu. Bwana alimwambia Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, hata niwawekapo adui zako kuwa chini ya miguu yako. Daudi mwenyewe asema ni Bwana; basi amekuwaje mwanawe? Na mkutano mkubwa walikuwa wakimsikiliza kwa furaha.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com. 

UPENDO WA AGAPE

 

“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Alhamisi, Juni, 4, 2026, 
Tafakari ya kila siku
Juma la 9 la Mwaka wa Kanisa

2 Tim 2: 8-15; 
Zab 25: 4-5, 8-10, 14; 
Mk 12: 28-34


UPENDO WA AGAPE!

Kwakusoma Injili tunaweza kufanya muktasari wa nafsi ya Yesu kwa neno moja tu, nalo ni UPENDO. Yesu anatuambia kwamba sheria zote zinaweza kufupishwa katika sheria mbili tuu. Ya kwanza kabisa ambayo ni muhimu sana ni upendo kwa Mungu usio na kikwazo chochote, ya pili ni matokea ya hiyo ya kwanza, kwasababu wakati mwanadamu anapendwa, Mungu anapendwa, kwasababu mwanadamu ameumwa kwa sura na mfano wa Mungu

Upendo ulimsukuma Yesu aweze kuwanyanyua wanyonge, kuwasaida waliotengwa, kuponya walioumizwa, kuwafanya huru wafungwa na akatoa maisha yake msalabani ili kutukomboa sisi kutoka utumwa wa dhambi. Upendo wa Mungu hauna masharti. Yesu kwa maneno na matendo yake anatuhimiza kutimiza na kutenda “UPENDO huu” kwaajili ya ukombozi wetu na ukombozi wa ulimwengu mzima. Na hiki ndicho kitambulisho chetu kama Wakristo wanaomfuata Yesu kwa uaminifu. Kwa namna hiyo tutakuwa wakristu wa kweli “kama Kristo”. Pengine tujiulize swali lingine ambalo hatujazoea sana kujiuliza, tunajua Mungu anatupenda wote bila ubaguzi. Je, ninampenda mwenzangu/jirani yangu kama Mungu anavyompenda?

Sala: Bwana; nisaidie niweze kuwa Mkristo wa kweli kwa kuishi na kutimiza Upendo usio na masharti wala kikomo. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA JUNI 4, 2026


MASOMO YA MISA JUNI 4, 2026

ALHAMISI, JUMA LA 9 LA MWAKA

SOMO 1
2Tim. 2:8-15

Mkumbuke Yesu Kristo, aliyefufuka katika wafu, wa uzao wa Daudi kama inenavyo injili yangu. Nami katika hiyo nimeteswa hata kufungwa kama mtenda mabaya; lakini neno la Mungu halifungwi. Kwa ajili ya hilo nastahimili mambo yote, kwa ajili ya wateule, ili wao nao waupate wokovu ule ulio katika Kristo Yesu, pamoja na utukufu wa milele. Ni neno la kuaminiwa.

Kwa maana, kama tukifa pamoja naye, tutaishi pamoja naye pia; kama tukistahimili, tutamiliki pamoja naye; kama tukimkana yeye, yeye naye atatukana sisi; kama sisi hatuamini, yeye hudumu wa kuaminiwa. Kwa maana hawezi kujikana mwenyewe.

Uwakumbushe mambo hayo, ukiwaonya machoni pa Mungu, wasiwe na mashindano ya maneno ambayo hayana faida, bali huwaharibu wasikiao. Jitahidi kujionyesha kuwa umekubaliwa na Mungu, mtenda kazi asiye na sababu ya kutahayari, ukitumia kwa halali neno la kweli.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI

(K) Ee Bwana, unijulishe njia zako.

Ee Bwana, unijulishe njia zako,
Unifundishe mapito yako,
Uniongoze katika kweli yako,
Na kunifundisha. (K)

Maana Wewe ndiwe Mungu wa wokovu wangu,
Nakungoja Wewe mchana kutwa.
Bwana yu mwema, mwenye adili,
Kwa hiyo atawafundisha wenye dhambi njia.
Wenye upole atawaongoza katika hukumu,
Wenye upole atawafundisha njia yake. (K)

Njia zote za Bwana ni fadhili na kweli,
Kwao walishikao agano lake na shuhuda zake.
Siri ya Bwana iko kwao wamchao,
Naye atawajulisha agano lake. (K)

SHANGILIO
Yn. 8:12

Aleluya, aleluya,
Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, asema, Bwana, yeye anifuataye hatakwenda gizani kamwe, bali atakuwa na nuru ya uzima.
Aleluya.

INJILI
Mk. 12: 28-34

Mmoja wa waandishi alifika kwa Yesu akamwuliza, Katika amri zote ni ipi iliyo ya kwanza? Yesu akamjibu, Ya kwanza ndiyo hii, Sikia, Israeli, Bwana Mungu wetu ni Bwana mmoja. nawe mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote, na kwa nguvu zako zote. Na ya pili ndiyo hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Hakuna amri nyingine iliyo kuu kuliko hizi.

Yule mwandishi akamwambia, Hakika, Mwalimu, umesema vema ya kwamba Mungu ni mmoja, wala hakuna mwingine ila yeye; na kumpenda yeye kwa moyo wote, na kwa ufahamu wote, na kwa nguvu zote, na kumpenda jirani kama nafsi yako, kwafaa kuliko sadaka nzima za kuteketezwa na dhabihu zote pia. Naye Yesu, alipoona kwamba amejibu kwa busara, alimwambia, Wewe hu mbali na ufalme wa Mungu. Wala hakuthubutu mtu kumsaili neno tena tokea hapo.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MIMI NI UFUFUO NA UZIMA!

 

“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatano, Juni, 3, 2026, 
Tafakari ya kila siku
Juma la 9 la Mwaka wa Kanisa


2 Tim 1: 1-3, 6-12; 
Zab 122: 1-2; 
Mk 12: 18-27.


MIMI NI UFUFUO NA UZIMA!


Somo la kwanza la leo linatuonesha jinsi ghani Mtume Paulo alivyo elewa kwamba Injili inaweza kuhubiriwa kwa mataifa yote tu, kwa nguvu ya Yesu mfufuka. Kwa kujikita kwenye faida yetu, au vipaji vyetu au nguvu zetu wenyewe maisha yatakuwa kama balbu ya umeme isiokuwa na umeme. Hitaji la sasa nikumtumikia Bwana wetu kwa moyo safi tukijikita katika ahadi zake za uzima wa milele alizo tuachia Yesu mwenyewe. 

Katika somo la Injili Yesu anatuambia ni wale tuu wanao elewa maandiko matakatifu na nguvu ya Mungu wataamini katika ufufuo wa wafu. Hili lilikuwa jibu kwa swali lililoulizwa na Masadukayo. Yesu anawajibu kwamba mambo ya ndoa ni mambo ya dunia hii. Baada ya kufa tunakuwa kama malaika wa mbinguni. Yesu kwa njia ya ufufuko wake ameyashinda mauti na kutupatia uzima wa milele. Yeye ni Bwana wa uzima. Maisha yetu yapaswa yamwelekee yeye zaidi, tukitazamia lililo kubwa zaidi kuliko maisha yetu ya dunia, tukijua uzima wa milele ndio lengo letu baada ya maisha haya. Tusifungwe na malimwengu tushindwe kumuona Mungu baada ya maisha haya. Kwa mfano wa mfiadini Mt.Yustino tujifunze kutoa maisha yetu kwa Kristo mfufuka ili tuweze kupata lile taji lisilofifia (uzima wa milele).

Sala. Bwana Yesu, hatuweze kuwa Wakristo wenye kuzaa matunda mema kama tutajitenga nawe. Tunaomba utusaidie tuweze kupata kitambulisho chetu, kuishi kwetu na maisha yetu kutoka kwako. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA JUNI 3, 2026



MASOMO YA MISA JUNI 3, 2026
JUMATANO, JUMA LA 9 LA MWAKA

KUMBUKUMBU YA WATAKATIFU KAROLI LWANGA NA WENZAKE, WAFIDIANI

SOMO 1
2Tim. 1:1-3, 6-12

Paulo, mtume wa Kristo Yesu, kwa mapenzi ya Mungu; kwa ajili ya ahadi ya uzima ulio katika Kristo Yesu; kwa Timotheo, mwanangu mpendwa. Neema na iwe kwako, na rehema, na amani, zitokazo kwa Mungu Baba na kwa Kristo Yesu Bwana wetu.

Namshukuru Mungu, nimwabuduye kwa dhamiri safi tangu zamani za wazee wangu, kama vile nikukumbukavyo wewe daima, katika kuomba kwangu usiku na mchana.

Kwa sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono yangu. Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi. Basi usiuonee haya ushuhuda wa Bwana wetu, wala usinionee haya mimi mfungwa wake, bali uvumilie mabaya pamoja nami kwa ajili ya Injili, kwa kadiri ya nguvu ya Mungu; ambaye alituokoa akatuita kwa mwito mtakatifu, si kwa kadiri ya matendo yetu sisi, bali kwa kadiri ya makusudi yake yeye na neema yake. Neema hiyo tulipewa katika Kristo Yesu tangu milele, na sasa inadhihirishwa kwa kufunuliwa kwake Mwokozi wetu Kristo Yesu; aliyebatili mauti, na kuufunua uzima na kutokuharibika, kwa ile Injili; ambayo kwa ajili ya hiyo naliwekwa niwe mhubiri na mtume na mwalimu.

Kwa sababu hiyo nimepatikana na mateso haya, wala sitahari; kwa maana namjua yeye niliyemwamini, na kusadiki ya kwamba aweza kukilinda kile nilichokiweka amana kwake hata siku ile.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI
Zab. 123:1-2 (K) 1

(K) Nimekuinulia macho yangu, ee Bwana.

Nimekuinulia macho yangu,
Wewe uketiye mbinguni.
Kama vile macho ya watumishi
Kwa mkono wa bwana zao. (K)

Kama macho ya mjakazi
Kwa mkono wa bibi yake;
Hivyo macho yetu humwelekea Bwana, Mungu wetu.
Hata atakapoturehemu. (K)

SHANGILIO
Lk. 8:15

Aleluya, aleluya.
Wanabarikiwa wale ambao kwa unyofu na wema wa mioyo yao hulisikia neno la Mungu, na kulishika.
Aleluya.

INJILI
Mk. 12:18-27

Masadukayo, watu wasemao ya kwamba hakuna kiyama, walimwendea Yesu, wakamwuliza na kusema, Mwalimu, Musa alituandikia ya kwamba ndugu ya mtu akifa, akamwacha mkewe wala hana mtoto, ndugu yake amtwae yule mkewe akampatie ndugu yake mzao. Basi kulikuwa na ndugu saba; wa kwanza akatwaa mke, akafa, asiache mzao. Wa pili naye akamtwaa akafa, wala yeye hakuacha mzao. Na wa tatu kadhalika; hata na wote saba, wasiache mzao. Mwisho wa wote yule mwanamke akafa naye. Basi, katika kiyama atakuwa mke wa yupi katika hao? Maana wote saba walikuwa naye.

Yesu akajibu, akawaambia, Je! hampotei kwa sababu hii, kwa kuwa hamyajui maandiko wala uweza wa Mungu? Kwa maana watakapofufuka katika wafu, hawaoi wala hawaolewi, bali huwa kama malaika walioko mbinguni. Na kwa habari ya wafu ya kwamba wafufuliwa, hamjasoma katika kitabu cha Musa, Sura ya Kijiti, jinsi Mungu alivyomwambia, akisema, Mimi ni Mungu wa Ibrahi- mu, na Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo? Yeye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai. Hivyo mwapotea sana.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com. 

KUTEMBEA KATIKATI YA MITEGO!

 

“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Tafakari ya kila siku
Jumanne, Juni 2, 2026,
Juma la 9 la Mwaka


2 Pet 3: 12-15,17-18
Zab 90:2-4,10,14,16; ;
Mk 12: 13-17.


KUTEMBEA KATIKATI YA MITEGO!



Mafarisayo na Maherodi walijaribu kumtega Yesu katika maongezi yake. Walijaribu kutumia akili yao ili kumfanya Yesu aongee maneno ya kumpinga Kaisari na hivyo kupata kisingizio cha ugomvi na utawala wa Kirumi. Lakini chakushangaza walichokuwa wakisema kuhusu Yesu kilikuwa cha kweli na ilikuwa fadhila kubwa.

Walisema mambo mawili ambayo yalionesha unyenyekevu wa Yesu na uaminifu wake: “twajua ya kuwa wewe u mtu wa kweli,” na “wala hujali cheo cha mtu; kwa maana hutazami sura za watu; lakini katika kweli waifundisha njia ya Mungu”. Yesu haingii katika mtego wao na anafanya kwa hekima kubwa na kumalizana nao.

Tukitafakari juu ya fadhila hizi mbili, tunatambua kuwa maisha yetu ni mara chache sana yanakuwa namna hiyo. Kwanza kabisa, sisi tuna hangaika sana na maneno ya wengine. Ni vizuri kusikiliza wengine na kuwasiliana nao katika hali ya utambuzi. Mawazo ya wengine yanaweza kuwa chanzo cha kugeukia maisha mazuri. Lakini wakati mwingine tunaruhusu wengine watupeleke kwenye dhambi kwasababu ya hofu na woga. Wakati mwingine mawazo mabaya na ushauri mbaya unaongoza maisha yetu. Yesu hakuingia katika mawazo mabaya ya wengine wala hakuruhusu kupelekwa na kutenda kunyume.

Pili, Yesu hakuruhusu “cheo” cha mtu kumpelekesha. Cheo cha mtu wala madaraka havi mfanyi mtu kuwa mkweli zaidi kuliko wengine. Kilicho cha muhimu ni uaminifu na ukweli wa kila mtu. Yesu alizitenda fadhila hizi kiaminifu.

Tutafakari pia sisi kama maneno haya yanaweza kusemwa yakitulenga sisi. Tukazane kuishi maisha ya unyenyenyekevu na kweli na hivyo tutavuka vikwazo na mitego iliyotegwa katika njia yetu ya maisha.

Sala: Bwana, ninataka kuwa mtu mwaminifu. Ninataka kusikiliza mawaidha mazuri ya wengine lakini sio mawazo yakunipeleka kwenye dhambi. Nisaidie niweze kukutafuta wewe na ukweli wako katika kila kitu. Yesu, nakuamini wewe. Amina.

------------------------
Copyright ©2013-2026 ©FurKat, FurahayaKikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUMANNE, JUNI 2, 2026

 

MASOMO YA MISA, JUMANNE, JUNI 2, 2026
JUMA LA 9 LA MWAKA


SOMO 1
Mdo 11:21-26, 13:1-3

Watu wengi waliamini, wakamwelekea Bwana. Habari hizo za watu hao zikafika masikioni mwa kanisa lililokuwako katika Yerusalemu; wakamtuma Baranaba, aende hata Antiokia. Naye, alipokwisha kufika na kuiona neema ya Mungu akafurahi, akawasihi wote wawaambatane na Bwana kwa kusudi la moyo. Maana alikuwa mtu mwema amejaa Roho Mtakatifu na Imani; watu wengi wakaongezeka upande wa Bwana.

Kasha akatoka akaenda Tarso kumtafuta Sauli; hata alipokwisha kumwona akamleta Antiokia. Ikawa kwa muda wa mwaka mzima wakakusanyika pamoja na kanisa na kuwafundisha watu wengi. Na wanafunzi waliitwa Wakristo kwanza hapo Antiokia.

  Na huko Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli. Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi niliyowaitia. Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 98:1-6 (K) 2

(K) Bwana ameufunua wokovu wake machoni pa mataifa.

Mwimbieni Bwana wimbo mpya,
Kwa maana ametenda mambo ya ajabu.
Mkono wa kuume wake mwenyewe,
Mkono wake mtakatifu umemtendea wokovu. (K)

Bwana ameufunua wokovu wake,
Machoni pa mataifa ameidhihirisha haki yake.
Amezikumbuka rehema zake,
Na uaminifu wake kwa nyumba ya Israeli. (K)

Miisho yote ya dunia imeuona
Wokovu wa Mungu wetu.
Mshangilieni Bwana, nchi yote,
Inueni sauti, imbeni kwa furaha, imbeni zaburi. (K)

Mwimbieni Bwana zaburi kwa kinubi,
Kwa kinubi na sauti ya zaburi.
Kwa panda na sauti ya baragumu.
Shangilieni mbele za Mfalme, Bwana. (K)


SHANGILIO
Aleluya, aleluya,
Ee Mungu, tunakusifu, tunakukiri kuwa Bwana.
Jamii tukufu ya mitume inakusifu.
Aleluya.


INJILI
Mt 5:13-16

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Ninyi ni chumvi ya dunia; lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena kabisa, ila kutupwa nje na kukanyagwa na watu. Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima. Wala watu hawawashi taa na kuiweka chini ya pishi, bali juu ya kiango; nayo yawaangaza wote waliomo nyumbani. Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2024, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MUNGU ANAYETUJALI (MWEMA)!

 

“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatatu, Juni 1, 2026,
Juma la 9 la Mwaka wa Kanisa

2 Pet 1: 2-7;
Zab 90: 1-2, 14-16;
Mk 12: 1-12

MUNGU ANAYETUJALI (MWEMA)!

Fumbo tulilo nalo leo kwa tafakari yetu ni kuhusu muonekano wa uzuri na wema wa Mungu. Jinsi Mungu anavyotenda na jinsi mwanadamu anavyofikiri ni vitu viwili tofauti kabisa kiasi ambacho mwanadamu anajiandaa akidhani atashambuliwa. Wema haujajikita katika kutoa mengi tu, bali kutoa hata kidogo kwa wakati. Mungu alimtoa mwanaye kwawakati kwaajili yetu. Alitupa yote kwa wakati. Yesu aliongea na kutenda katika hali ambayo watu kwakuona anayosema nakutenda, wakatambua Mungu ni wa namna ghani.

Kwa maneno mwengine, Yesu hakuongea tuu kuhusu Mungu na kuonyesha muelekeo wa kwenda kwake, bali alionesha uwepo wa Mungu na Mungu akaonekana akiwa kati ya watu wake. Kama sio yeye, Mungu kwetu angekuwa ni kama kitu tuu cha kutumaini nakutafuta. Lakini kwa njia yake Mungu yupo kati yetu (Ekaristi Takatifu). Kabla ya Yesu, hakuna aliyejua sifa za Ufalme wa Mungu ulivyo, yeye ndiye aliyetupa mifano akielezea jinsi Ufalme wa Mungu ulivyo, na akatuambia yeye amekuja kuutangaza, upo kati yetu, nabado utatimilizwa katika maisha ya umilele. Kwahiyo tukiishi vizuri na wengine tunaishi Ufalme wake tukiwa hapa duniani.

Yesu, hakutaka chochote kwaajili yake binafsi, bali kila kitu alichokuwa nacho na kutenda, alifanya kwaajili yawengine. Kila mmoja wetu ni wa Yesu, chombo cha upendo wa Mungu, na chombo chakupokea wema wa Mungu. Leo tujiulize kama tumekuwa wazi kwa wema na upendo huu wa Mungu.

Sala: Nisaidie Bwana, niweze kuutambua wema wako ili niweze kuwa mwema. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUNI 1, 2026

 


MASOMO YA MISA, JUNI 1, 2026
JUMATATU YA 9 YA MWAKA
KUMBUKUMBU YA MTAKATIFU JUSTIN

SOMO 1
2Pet. 1:2-7
Neema na iwe kwenu na amani iongezwe katika kumjua Mungu na Yesu Bwana wetu.
Kwa kuwa uweza wake wa Uungu umetukirimia vitu vyote vipasavyo uzima na utauwa, kwa kumjua yeye aliyetuita kwa utukufu wake na wema wake mwenyewe. Tena kwa hayo ametukirimia ahadi kubwa mno, za thamani, ili kwamba kwa hizo mpate kuwa washirika wa tabia ya Uungu, mkiokolewa na uharibifu uliomo duniani kwa sababu ya tamaa. Naam, na kwa sababu iyo hiyo mkijitahidi sana kwa upande wenu, katika imani yenu tieni na wema, na katika wema wenu maarifa, na katika maarifa yenu kiasi, na katika kiasi chenu saburi, na katika sabauri yenu utauwa, na katika utauwa wenu upendano wa ndugu, na ktika upendano wa ndugu, upendo.
Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI
Zab. 91:1-2, 14-16, (K) 2
(K) Mungu wangu ninakutumaini.
Aketiye mahali pa siri pake Aliye juu
Atakaa katika uvuli wake Mwenyezi.
Nitasema, Bwana ndiye kimbilio langu na ngome yangu,
Mungu wangu nitakayemtumaini. (K)
(K) Mungu wangu ninakutumaini.
Mwana-simba na joka utawaseta kwa miguu.
Kwa kuwa amekaza kunipenda
Nitamwokoa; na kumweka palipo juu, kw akuwa amenijua jina langu.
Ataniita nami nitamwitikia. (K)
Nitakuwa pamoja naye taabuni,
Nitamwokoa na kumtukuza;
Kwa siku nyingi nitamshibisha,
Nami nitamwonyesha wokovu wangu. (K)

SHANGILIO
Zab. 130:5
Aleluya, aleluya.
Roho yangu inamngoja Bwana, na neno lake nimelitumainia.
Aleluya.

INJILI
Mk. 12:1-12
Yesu alisema na Mafarisayo kwa mifano; Mtu mmoja alipanda shamba la mizabibu, akazungusha ugo, akachimba shimo la shinikizo, akajenga mnara, akapangisha wakulima, akasafiri. Hata kwa wakati wake akatuma, mtumwa kwa wale wakulima, ili apokee kwa wakulima katika matunda ya mizabibu. Wakamtwaa, wakampiga, wakamtoa nje, hana kitu. Akatuma tena kwao mtumwa mwingine, na huyo wakamtia jeraha -za kichwa, wakamfanyia jeuri. Akamtuma mwingine, huyo wakamwua; na wengine wengi, hawa wakiwapiga na hawa wakiwaua. Basi alikuwa na mmoja bado, mwana mpendwa wake; huyu naye akamtuma kwao mwisho, akisema, Watamstahi mwanangu. Lakini wale wakulima wakasemezana, Huyu ni mrithi; haya, na tumwue, na urithi utakuwa wetu. Wakamkamata, wakamwua, wakamtupa nje ya shamba la mizabibu. basi atafanyaje yule bwana wa shamba la mizabibu? Atakuja na kuwaangamiza wale wakulima, na lile shamba la mizabibu atawapa wengine. Hata andiko hili hamjalisoma, Jiwe walilolikataa waashi, hilo limekuwa jiwe kuu la pembeni. Neno hili limetoka kwa Bwana, nalo ni ajabu machoni petu? Nao wakatafuta kumkamata, wakaogopa mkutano; maana walitambua ya kwamba ule mfano amewanenea wao. Wakamwacha wakaenda zao.
Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MUNGU KATIKA UTATU

 



“MBEGU ZA UZIMA”
Tafakari ya kila Jumapili
Jumapili, Mei 31, 2026 
Sherehe ya Utatu Mtakatifu

Kut. 34 : 4-6, 8-9;
Dan. 3:52-56. (K) 52;
2 Kor. 13 :11-14;
Yn. 3:16-18.


MUNGU KATIKA UTATU


Wakatoliki, duniani kote, sio kwamba wanaamini Mungu tu, bali wanaamini Mungu mmoja. Lakini Mungu wetu yupo katika Utatu- Utatu katika umoja na umoja katika Utatu. Kila mmoja ni Mungu kwa asili na wote ni Mungu mmoja. Sawa katika Nguvu, ni wa milele na wana utukufu. Fumbo hili kuu linaweza kuchukuliwa kama fumbo lililo kuu kabisa katika Biblia Takatifu. Wakristo tunaamini fumbo hili kuu ndani ya mamlaka ya Yesu Kristo na Agano Jipya. Ni moja wapo ya fumbo kubwa la ndani kabisa lililofunuliwa na lililopo juu kabisa kupita akili ya mwanadamu. Yesu mara nyingi ameongea kuhusu Mungu kama Baba yake. Sauti ya Baba ilisikika wakati wa ubatizo wa Yesu; “Huyu ni mwanangu mpendwa niliye pendezwa naye msikilizeni yeye”. Yesu alipo ngara sura, pia, sauti hiyo hiyo ilisikika ikisema maneno hayo hayo. Katika matukio yote uwepo wa wingu jeupe ilionyesha uwepo wa Roho Mtakatifu, ambaye Yesu aliwaahidia wakati alipokuwa akipaa kwenda kwa Baba, “nitawapa msaidizi Mwingine-Roho wa kweli anayetoka kwa Baba”. 

Yesu anatuambia kwamba, Mungu aliupenda sana ulimwengu mpaka akamtuma mwanaye ulimwenguni, ili wote watakao muamini wasipotee bali wawe na uzima wa milele (Yn 3:16). Anaelezea uhusiano wake ndani ya Mungu mmoja wa kweli na anawataka mitume na wafuasi watambue na wakubali kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu, na kwamba Mungu ni Baba yake, na kwamba Roho Mtakatifu alitumwa kwao na Baba na Mwana. Wakristo wa kwanza walisadiki ndani ya Utatu Mtakatifu bila kupinga. Baada ya kuamini, kinachofuata ni Upendo. “Kama mtu akinipenda mimi” Yesu anasema, “Baba yangu atampenda. Nasi tutakuja kwake nakufanya makao ndani yake.”

“…(Wana ndoa) matunda ya wana ndoa yanakuwa ishara ya kuelewa na kuelezea fumbo la Mungu mwenyewe, kwasababu kwa mtazamo wa Kikristo wa Utatu mtakatifu, Mungu anatafakariwa kama Baba, na Mwana na Roho Upendo. Utatu Mtakatifu ni umoja wa upendo, na familia ndiyo inayoishi kuonesha umoja huu. Mtakatifu Papa Yohane Paulo wa Pili, alitoa mwanga kwa hili alivyosema ‘Mungu wetu katika undani wake sio upweke bali ni familia, kwani ndani yake ana Ubaba, mwana na undani wa familia ambaye ni Upendo. upendo huo ndani ya familia ya Kimungu ni Roho Mtakatifu’”. (Baba Mtakatifu Fransisko katika Furaha ya upendo, Amoris Laetitia, 11)

Tutafakari leo juu ya sherehe hii ya Utatu Mtakatifu, ni mara ngapi nina enzi upendo huu wa Utatu Mtakatifu katika mahusiano yangu? Tujaribu kufanya jitihada tusonge mbele zaidi, katika mapendo yetu, na kumruhusu Mungu akupe matokeo mazuri ya tokanayo na upendo wako kwake na kwa jirani. 

Sala: Baba na Mwana na Roho Mtakatifu, nisaidie mimi niweze kuku fahamu wewe na kukupenda. Nisaidie niweze kuelewa upendo unaoshiriki na Mwanao. Kwa kuelewa upendo huo, nisaidie na mimi niweze kushirikisha upendo huo kwa wengine. Baba na Mwana na Roho Mtakatifu, nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.