Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MASOMO YA MISA, APRILI 26, 2026



MASOMO YA MISA, APRILI 26, 2026
DOMINIKA YA 4 YA PASAKA
JUMAPILI YA MCHUNGAJI MWEMA


MWANZO:
Zab. 33:5–6
Nchi imejaa fadhili za Bwana. Kwa neno la Bwana mbingu zilifanyika, aleluya.


SOMO 1
Mdo 2:14, 36– 41

Siku ya Pentekoste Petro akasimama pamoja na wale kumi na mmoja, akapaza sauti yake, akawaambia,

Basi nyumba yote ya Israeli na wajue yakini ya kwamba Mungu amemfanya Yesu huyo mliyesulibisha kuwa Bwana na Kristo.

Walipoyasikia haya wakachomwa mioyo yao, wakamwambia Petro na mitume wengine, Tutendeje, ndugu zetu? Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Krito, mpate kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu. Kwa kuwa ahadi hii ni kwa ajili yenu, na kwa watoto wenu, na kwa watu wote walio mbali, na kwa wote watakaoitwa na Bwana Mungu wetu wamjie. Akawashuhudia kwa maneno mengine mengi sana na kuwaonya, akisema, Jiokoeni na kizazi hiki chenye ukaidi. Nao waliolipokea neno lake wakabatizwa; na siku ile wakaongezeka watu wapata elfu tatu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 23:1 – 6 (K) 1

(K) Bwana ndiye mchungaji wangu, sitapungukiwa na kitu.

Bwana ndiye mchungaji wangu,
Sitapungukiwa na kitu.
Katika malisho ya majani mabichi hunilaza,
Kando ya maji ya utulivu huniongoza. (K)

Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza
Katika njia za haki kwa ajili ya jina lake.
Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti,
Sitaogopa mabaya;
Kwa maana Wewe upo pamoja nami,
Gongo lako na fimbo yako vyanifariji. (K)

Waandaa meza mbele yangu,
Machoni pa watesi wangu.
Umenipaka mafuta kichwani pangu,
Na kikombe changu kinafurika. (K)

Hakika wema na fadhili zitanifuata
Siku zote za maisha yangu;
Nami nitakaa nyumbani mwa Bwana milele. (K)



SOMO 2
1Pet. 2:20– 25

Kustahimili, mtendapo mema na kupata mateso, huu ndio wema hasa mbele za Mungu. Kwa sababu ndio mlioitiwa; maana Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia kielelezo, mfuate nyayo zake.

Yeye hakutenda dhambi, wala hila haikuonekana kinywani mwake. Yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogopfya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki. Yeye mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti; ili, tukiwa wafu kwa mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki; na kwa kupigwa kwake mliponywa. Kwa maana mlikuwa mnapotea kama kondoo; lakini sasa mmemrudia Mchungaji na Mwangalizi war oho zenu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



SHANGILIO
Yn. 10:14

Aleluya, aleluya,
Mimi ndimi mchungaji mwema; nao walio wangu nawajua; nao walio wangu wanijua mimi.
Aleluya.



INJILI
Yn. 10:1 – 10

Yesu aliwaambia Wayahudi, Amin, amin, nawaambieni, Yeye asiyeingia mlangoni katika zizi la kondoo, lakini akwea penginepo, huyo ni mwivi naye ni mnyang’anyi. Aingiaye mlangoni ni mchungaji wa kondoo. Bawabu humfungulia huyo, na kondoo humsikia sauti yake; naye huwaita kondoo wake kwa majina yao, na kuwapeleka nje. Naye awatoapo kondoo humfuata, kwa maana waijua sauti yake. Mgeni hawatamfuata kabisa, bali watamkimbia; kwa maana hawazijui sauti za wageni.

Mithali hiyo Yesu aliwaambia; lakini wao hawakuelewa na mambo hayo aliyowaambia.

Basi Yesu aliwaambia tena, Amin, amin, nawaambieni, Mimi ndimi mlango wa kondoo. Wote walionitangulia ni wevi na wanyang’anyi; lakini kondoo hawakuwasikia. Mimi ndimi mlango; mtu akiingia kwa mimi, ataokoka; ataingia na kutoka, naye atapata malisho. Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo..


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

UNA MANENO YA UZIMA WA MILELE!



“KUFUFUKA NA KRISTO”
Tafakari ya Pasaka
Jumamosi, Aprili 25, 2026
Juma la 3 la Pasaka

Mdo 9: 31-42;
Zab 116: 12-17;
Yn 6: 60-69.


UNA MANENO YA UZIMA WA MILELE!


Yohane anataka kutuonesha kwamba Yesu ndiye anayetulisha chakula cha uzima wa Kimungu, kwakutupa sisi maisha yake mwenyewe na mwili wake. Kula mkate na samaki aliowapa Yesu ilikuwa rahisi lakini kusikiliza maneno yake ilikuwa vigumu, baada ya haya Injili inasema wazi kwamba wafuasi wengi walimwacha na wengine waliacha kuambatana naye. Lakini wakati Yesu alipowauliza wale kumi na wawili, kama na wao wanataka kuondoka pia, Petro alijibu, “Bwana tuende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele” Ndio, Petro anatambua japo kuwa si kwahakika sana kipindi hicho, kwamba “Roho ndiyo itiayo uzima, mwili haufai kitu”

Swali hili la Yesu kwa Mitume wake ni muhimu sana. Kwa kuwauliza wao moja kwa moja, Yesu anawapa uhuru kamili wa kuchagua. Hawashinikizi kukubali au kuamini alichokuwa amefundisha mara. Hili lilikuwa muhimu kwa sababu kwa kiasi ambacho Yesu anatoa cha kuachia yote ni mwaliko wa kuwa na uhuru kamili, kwa upande wa mitume, kwa mafundisho yake ya utukufu juu ya Ekaristi. Wapo huru kabisa kukubali au kukataa. Ni uhuru huu utawafanya wazame katika Imani yao juu ya Yesu.

Tutafakari leo, juu ya kujikabidhi kwetu kwa Yesu. Tupo huru kabisa kumfuata yeye au kumkataa. Yesu hapendi tumchague na kumfuata nusu nusu. Maneno ya Yesu yana nguvu, yana changamoto na yanahitaji sadaka. Anataka tumwamini yeye na kumfuata kwa moyo wote na kujikabidhi kweli. Ni Yesu mwenyewe mwenye maneno ya uzima wa milele na tunapaswa tukubali maneno yake na kuamini kwa nguvu zetu zote.

Ni neno la Mungu kweli linalo tutakasa na kutuburudisha. Linatupa uzima; kwahiyo kinachotupa uzima ni Neno la Mungu, kwani maneno anayosema Yesu ni roho tena ni uzima. Jumuiya ya Wakristo kama tunavyosikia katika Somo la kwanza leo, walijenga msingi wao juu ya uzima huu walioupokea kutoka kwa Yesu na faraja ya Roho Mtakatifu. Sisi tuna uhai na uzima, ila uzima wetu na maisha yetu tuyaweke ndani ya Bwana wa uzima Yesu Kristo mwenyewe. Ni maneno haya yenye uzima ya Yesu yalioweza kumrudishia uzima Dorcasi kama tunavyosikia katika somo la kwanza.

Sala: Bwana Yesu, ni wewe pekee ninaye kuchagua kukuamini na kukufuata. Nisaidie nikumbatie yote uliyo fundisha na nisaidie kukuchagua kwa uhuru katika maisha yangu ya kila siku. Yesu nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, APRILI 25, 2026




MASOMO YA MISA, APRILI 25, 2026
JUMAMOSI, JUMA LA 3 LA PASAKA


SOMO 1
Mdo. 9:31-42

Kanisa lilipata raha katika Uyahudi wote na Galilaya na Samaria, likajengwa, likiendelea na kuongoezeka katika kicho cha Bwana, na faraja ya Roho Mtakatifu.

Hata Petro alipokuwa akizunguka-zunguka pande zote akawatelemkia na watakatifu waliokaa Lida. Akamwona mtu mmoja huko, jina lake Ainea, mtu huyo amelala kitandani miaka minane; maana alikuwa amepooza. Petro akamwambia. Ainea, Yesu Kriso akuponya; ondoka, ujitandikie. Mara akaondoka. Na watu waliokaa Lida na Sharani wakamwona, wakamgeukia Bwana.

Na mwanafunzi mmoja alikuwako Yafa, jina lake Tabitha, tafsiri yake ni Dorkasi (yaani paa); mwanamke huyu alikuwa amejaa matendo mema na sadaka alizozitoa. Ikawa siku zile akaugua, akafa; hata walipokwisha kumwosha, wakamweka orofani. Na kwa kuwa mji wa Lida ulikuwa karibu na Yafa, nao wanafunzi wamesikia ya kwamba Petro yuko huko, wakatuma watu wawili kwake, kumsihi na kusema, Usikawie kuja kwetu.

Petro akaondoka akafuatana nao. Alipofika, wakampeleka juu orofani wajane wote wakasimama karibu naye, wakilia na kumwonyesha zile kanzu na nguo alizozishona Dorkasi wakati ule alipokuwa pamoja nao. Petro akawatoa nje wote, akapiga maogi, akaomba, kisha akaelekea yule maiti, akanena, Tabitha, ondoka. Naye akafumbua macho yake, na alipomwona Petro akajiinua, akaketi. Akampa mkono, akamwinua, hata akiisha kuwaita wale watakatifu na wajane akamweka mbele yao, hali yu hai. Ikajulikana katika mji mzima wa Yafa; watu wengi wakamwamini Bwana.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 116:12-17 (K) 12

(K) Nimrudishie Bwana nini kwa ukarimu wake wote alionitendea?

Nimrudishie Bwana nini
Kwa ukarimu wake wote alionitendea?
Nitakipokea kikombe cha wokovu;
Na kulitangaza jina la Bwana. (K)

Nitaziondoa nadhiri zangu kwa Bwana,
Naam, mbele ya watu wake wote.
Ina thamani machoni pa Bwana
Mauti ya wacha Mungu wake. (K)

Ee Bwana, hakika mimi ni mtumishi wako,
Mtumishi wako, mwana na mjakazi wako,
Umenifungua vifungo vyangu.
Nitakutolea dhabihu ya kushukuru;
Na kulitangaza jina la Bwana. (K)



SHANGILIO
Kol. 3:1

Aleluya, aleluya,
Mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu, Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu.
Aleluya.



INJILI
Yn. 6:60:69

Siku ile, watu wengi miongoni mwa wanafunzi wake waliposikia maneno ya Yesu juu ya mkate wa uzima, walisema: Neno hili ni gumu, ni nani awezaye kulisikia? Naye Yesu akafahamu nafsini mwake ya kuwa wanafunzi wake wanalinung’unukia neno hilo, akawaambia, Je! Neno hili linawakwaza? Itakuwaje basi, mmwonapo Mwana wa Adamu akipaa huko alikokuwako kwanza? Roho ndiyo itiayo uzima, mwili haufai kitu; maneno hayo niliyowaambia ni roho, tena ni uzima.

Lakini kuna wengine miongoni mwenu wasiomini. Kwa maana Yesu alijua tangu mwanzo ni nani wasioamini, naye ni nani atakayemsaliti. Akasema, kwa sababu hiyo nimewaambia ya kwamba hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa amejaliwa na Baba yangu. Kwa ajili ya hayo wengi miongoni mwa wanafunzi wake wakarejea nyuma wasiandamane naye tena.

Basi Yesu akawambia wale Thenashara, Je! Ninyi nanyi mwataka kuondoka? Basi Simoni Petro akamjibu, Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele. Nasi tumesadiki, tena tumejua, ya kuwa wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MAISHA YETU YANATOKA KWA KRISTO!

 


“KUFUFUKA NA KRISTO”
Tafakari ya Pasaka
Ijumaa, Aprili 24, 2026
Juma la 3 la Pasaka

Mdo 9:1-20;
Zab 117:1-2 (K. Mk 16:15);
Yn  6:52-59.


MAISHA YETU YANATOKA KWA KRISTO!


Mt. Paulo ambaye tunamsikia katika somo la kwanza la leo alikuwa mtu mwenye Elimu ya juu/ busara aliyesoma chini ya mwalimu mkuu Gamaliel. Uongofu wake wa ghafla ulitokea  barabarani akielekea Dameski. Paulo ambaye alikuwa na mambo mengi, lakini akikosa jambo muhimu zaidi ambalo alilipata kupitia ndani ya tukio hili la wongofu. Alimpata Yesu Kristo. Baada ya uzoefu huo Paulo anatangaza, "Kwangu mimi, kuishi ni Kristo"; kama nilivyo, maisha ni Yesu Kristo" au "Naweza kufanya  yote katika Yeye anitiaye nguvu." "Naishi sasa si kwa maisha yangu mwenyewe bali kwa maisha ya Kristo anayeishi ndani yangu."

Mara baada ya Paulo kukutana na Yesu, maisha yake hayakubaki kamwe jinsi yalivyo kuwa mwanzo. Alibadilika kabisa. Alikuwa kiumbe kipya katika Kristo. Nasi pia tunampokea Kristo katika Ekaristi Takatifu. Ni kwa kiasi gani Ekaristi inabadilisha maisha yetu? Ni kwa kiasi gani najitoa mwenyewe kwa Kristo pale anapojitoa mwenyewe kwangu?

Katika somo la Injili, Yesu anasema “msipo ula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake hamna uzima ndani yenu”. Wengi wao walichukizwa na kuanza kuuliza uliza juu ya maneno yake. Inavutia kwamba wakati Yesu anapokutana na maneno makali ya wengine, anajibu tena kwa ujasiri mkubwa zaidi na uwazi zaidi. Hili linamuonesha kuwa mtu wa ujasiri mkubwa, mwenye nguvu na kuelewa. Unafunua pia kwetu sisi ujasiri ambao sisi tunapaswa kuwa nao katika ulimwengu huu. Ulimwengu tunaoishi ni ulimwengu unao kataa ukweli. Unakataa ukweli wa maadili, lakini pia unapinga ukweli wa ndani wa kiroho pia. Ukweli huu wa ndani ni kama uwepo wa uzuri wa Ekaristi Takatifu, umuhimu wa sala za kila siku, unyenyekevu, na kumtegemea Mungu, kuweka mapenzi ya Mungu mbele kuliko kitu chochote nk. Tunapaswa kutambua kuwa kila mara tunapo sogea karibu zaidi na Mungu, ndivyo tunavyozidi kujikabidhi kwake zaidi, na tutakapo hubiri ukweli wa Mungu ndivyo tunavyo upa ulimwengu shinikizo uache kutuiba kutoka kwa Mungu.

Sasa tufanye nini? Tunajifunza kutoka katika ujasiri na nguvu ya Yesu. Tunapojikuta sisi wenyewe tukiwa katika changamoto au tunapo hisi kana kwamba Imani yetu inashambuliwa, ndivyo tunavyo takiwa tuzame ndani zaidi na kuwa waaminifu zaidi na zaidi. Hili litatufanya tuwe na nguvu zaidi na kufanya vishawishi vinayokuja kuwa nafasi ya neema! Chagua kuiga ujasiri na ushupavu wa Bwana wetu na utakuwa chombo chenye kuonekana cha neema na huruma.

Sala: Bwana, ninaomba unipe ujasiri wa nguvu zako . Ninaomba unipe mwangaza katika utume wangu na unisaidie kukutumikia kiaminifu katika kila kitu. Ninaomba nisiwe muoga ninapo kutana na changamoto za maisha bali nitazame hamu yangu ya kukutumikia kwa moyo wangu wote. Yesu nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, APRILI 24, 2026





MASOMO YA MISA, APRILI 24, 2026
IJUMAA, JUMA LA 3 LA PASAKA


SOMO 1
Mdo. 9:1-20

Siku zile, Sauli, akizidi kutisha na kuwaza kuwaua wanafunzi wa Bwana, akamwendea Kuhani Mkuu, akataka ampe barua za kwenda Dameski zilizoandikwa kwa masinagogi, ili akiona watu wa Njia hii, waume kwa wake, awafunge na kuwaleta Yerusalemu.

Hapo alipokuwa akisafiri, ikawa anakaribia Dameski; ghafula ikamwangaza kote kote nuru kutoka mbinguni. Akaanguka chini, akasikia sauti ikimwambia, Sauli, Sauli, mbona waniudhi? Akasema, U nani wewe, Bwana? Naye akasema, Mimi ndimi Yesu unayeniudhi wewe. Lakini simama, uingie mjini, nawe utaambiwa yakupasayo kutenda. Na wale watu waliosafiri pamoja naye wakasimama kimya, wakiisikia sauti, wasione mtu. Sauli akainuka katika nchi, na macho yake yalipofumbuka, hakuona kitu; wakamshika mkono wakamleta mpaka Dameski. Akawa siku tatu haoni; hali, wala hanywi.

Basi palipokuwapo Dameski mwanafunzi jina lake Anania. Bwana akamwambia katika maono, Anania. Akasema, Mimi hapa, Bwana. Bwana akamwambia, Simama, enenda zako katika njia iitwayo Nyofu, ukaulize katika nyumba ya Yuda mtu aitwaye Sauli, wa Tarso; maana, angalia, anaomba; naye amemwona mtu, jina lake Anania, akiingia, na kumwekea mikono juu yake, apate kuona tena.

Lakini Anania akajibu, Bwana, nimesikia habari za mtu huyu kwa watu wengi, mabaya mengi aliyowatenda watakatifu wako Yerusalemu; hata hapa ana amri itokayo kwa wakuu wa makuhani awafunge wote wakuitiao Jina lako. Lakini Bwana akamwambia, Nenda tu; kwa maan ahuyu ni chombo kiteule kwangu, alichukue Jina langu mbele ya Mataifa, na wafalme, na wana wa Israeli. Maana nitamwonyesha yalivyo mengi yatakayompasa kuteswa kwa ajili ya Jina langu. Anania akaenda zake, akaingia mle nyumbani, akamwekea mikono akisema, Ndugu, Sauli, Bwana amenituma, Yesu yeye aliyekutokea katika njia uliyoijia, upate kuona tena, ukajazwe Roho Mtakatifu. Mara vikaanguka machoni pake vitu kama magamba, akapata kuona, akasimama, akabatizwa, akala chakula, na kupata nguvu.

Akawa huko siku kadha wa kadha pamoja na wanafunzi walioko Dameski. Mara akamhubiri Yesu katika masinagogi, kwamba yeye ni Mwana wa Mungu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 117 (K) Mk. 16:15

(K) Enendeni ulimwenguni mwote,
mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe.

Enyi mataifa yote, msifuni Bwana,
Enyi watu wote, mhimidini. (K)

Maana fadhili zake kwetu sisi ni kuu,
Na uaminifu wa Bwana ni wa milele. (K)



SHANGILIO
Rum. 6:9

Aleluya, aleluya,
Kristo akiisha kufufuka katika wafu hafi tena, wala mauti haimtawali tena. Aleluya.



INJILI
Yn. 6:52-59

Siku ile, Wayahudi walishindana wao kwa wao wakisema, Awezaje mtu huyu kutupa sisi mwili wake ili tuule?

Basi Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho. Kwa maana mwili wangu ni chakula cha kweli, na damu yangu ni kinywaji cha kweli. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake. Kama vile Baba aliye hai alivyonituma mimi, nami ni hai kwa Baba; kadhalika naye mwenye kunila atakuwa hai kwa mimi. Hiki ndicho chakula kishukacho kutoka mbinguni; si kama mababa walivyokula, wakafa; bali akilaye chakula hicho ataishi milele.

Maneno hayo aliyasema katika sinagogi, alipokuwa akifundisha, huko Kapernaumu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

KUVUTWA KWA YESU!



“KUFUFUKA NA KRISTO”
Tafakari ya Pasaka
Alhamisi, Aprili 23, 2026
Juma la 3 la Mwaka

Mdo 8:26-40;
Zab 66:8-9,16-17,20 (K. 1);
Yn 6:44-51.


KUVUTWA KWA YESU!

Karl Rahner anasema, “kila ninapo ongea kuhusu mimi najikuta nikiongelea kuhusu Mungu, na kila ninapo ongelea kuhusu Mungu najikuta naongea kuhusu mimi”. Safari ya maisha yetu pia karibia ni kuvuta kila kitu na kila mtu kwangu. Katika ulimwengu huu ambao kila mtu yupo na shughuli zake ni rahisi sana kuruhusu sauti mbali mbali zituharibu. Ni rahisi kusikia kusukumwa huku na kule katika ulimwengu na mambo yake yote. Ulimwengu umekuwa mzuri sana ukiteka mipango yetu yote na kutupatia kuridhika kwa haraka lakini utatuacha bila kitu.

Lakini sauti ya Mungu na mwaliko wake ni tofauti. Unapatikana katika ukimya wa ndani. Lakini haina maana kwamba unapaswa kuwa katika monasteri ili kupata ukimya huu wa ndani. Unapatika katika uaminifu mkubwa katika sala kila siku, na tabia ya kurudi kwa Mungu kila wakati katika vitu vyote. Unapatikana tunapo jibu wito wa Mungu, na kuifuata, na kurudia tena kila mara. Hili linajenga tabia ya kuvutwa karibu, kusikia, na kuitika na kuvutwa karibu na kusikiliza na kuitika tena na tena.

Katika Injili ya leo, tunatambua kuwa tumeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, na tunavutwa daima kwa Mungu. Ndani kabisa mwa moyo wa Mwanadamu, ana mtamani Mungu. Ndio maana Yesu anasema wazi kwamba “hakuna ajaye kwangu asipovutwa na Baba yangu” (Yn 6: 44). Katika somo la kwanza tunamuona Ofisa wa Ethiopia wakati akisoma chuo cha nabii Isaya, anakutana na ukweli katika Maandiko Matakatifu kwa msaada wa Filipo, na baadae anamkubali Yesu kama Mkombozi na Bwana.

Tutenge muda tuvutwe kwa Yesu. Tenga muda mchache au zaidi kila siku wa ukimya. Funga macho na jisikilize. Msikilize Mungu akiongea na wewe. Wakati akikuvuta kwake itika kwa ukarimu. Huu ndio uchaguzi mzuri kabisa ambao waweza kufanya kila siku!

Sala: Bwana, naomba univute karibu ili niweze kutambua sauti yako. Ninapo kusikia ukiita, nisaidie niweze kukuitikia kwa ukarimu. Maisha yangu ni yako, Bwana mpendwa. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, APRILI 23, 2026




MASOMO YA MISA, APRILI 23, 2026
ALHAMISI, JUMA LA 3 LA PASAKA


SOMO 1
Mdo. 8:26-40

Malaika wa Bwana akasema na Filipo, akamwambia, Ondoka ukaende upande wa kusini hata njia ile itelemkayo kutoka Yerusalemu kwenda Gaza; nayo ni jangwa. Naye akaondoka, akaenda; mara akamwona mtu wa Kushi, towashi, mwenye mamlaka chini ya Kandake malkia wa Kushi, aliyewekwa juu ya hazina yake yote; naye alikuwa amekwenda Yerusalemu kuabudu, akawa akirejea, ameketi garini mwake akisoma chuo cha nabii Isaya. Roho akamwambia Filipo, Sogea karibu na gari hili, ukashikamane nalo. Basi Filipo akaenda mbio, akamsikia anasoma chuo cha nabii Isaya; akanena, Je! Yamekuelea haya unayosoma? Akasema, Nitawezaje kuelewa, mtu asiponiongoza? Akamsihi Filipo apande na kuketi pamoja naye. Na fungu la Maandiko alilokuwa akilisoma ni hili, Aliongozwa kwenda machinjoni kama kondoo, na kama vile mwana-kondoo alivyo kimya mbele yake amkataye manyoya, vivyo hivyo yeye naye hafunui kinywa chake. Katika kujidhili kwake hukumu yake iliondolewa. Ni nani atakayeeleza kizazi chake? Kwa maana uzima wake umeondolewa katika nchi.

Yule towashi akamjibu Filipo, akasema, Nakuomba, nabii huyu asema maneno haya kwa habari ya nani; ni habari zake mwenyewe au za mtu mwingine? Filipo akafunua kinywa chake, naye, akakianza kwa andiko lilo hilo, akamhubiri habari njema za Yesu.

Wakawa wakiendelea njiani, wakafika mahali penye maji; yule towashi akasema, Tazama, maji haya; ni nini kinachonizuia nisibatizwe? Akaamuru lile gari lisimame; wakatelemka wote wawili majini, Filipo na yule towashi; naye akambatiza. Kisha, walipopanda kutoka majini, Roho wa Bwana akamnyakua Filipo, yule towashi asimwone tena; basi alikwenda zake akifurahi.

Lakini Filipo akaonekana katika Azoto, na alipokuwa akipita akahubiri Injili katika miji yote, hata akafika Kaisaria.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 66:8-9, 16-17, 20 (K) 1

(K) Mpigie Mungu kelele za shangwe, nchi yote.

Enyi mataifa, mtukuzeni Mungu wetu,
Itangazeni sauti ya sifa zake;
Aliyeiweka nafsi yetu katika uhai,
Wala hakuuacha mguu wetu usogezwe. (K)

Njoni sikieni, ninyi nyote mnaomcha Mungu,
Nami nitayatangaza aliyonitendea roho yangu.
Nalimwita kwa kinywa changu,
Na sifa kuu zilikuwa chini ya ulinzi wangu. (K)

Na ahimidiwe Mungu asiyeyakataa maombi yangu;
Wala kuniondolea fadhili zake. (K)



SHANGILIO
Yn. 20: 29

Aleluya, aleluya,
Wewe Toma, umesadiki kwa kuwa umeniona, wa heri wale wasioona, wakasadiki.
Aleluya.



INJILI
Yn. 6:44-51

Yesu aliwaambia Wayahudi: Hakuna mtu awezaye kuja kwangu, asipovutwa na Baba aliyenipeleka; nami nitamfufua siku ya mwisho. Imeandikwa katika manabii, Na wote watakuwa wamefundishwa na Mungu. Basi kila aliyesikia na kujifunza kwa Baba huja kwangu.

Si kwamba mtu amemwona Baba, ila yeye atokaye kwa Mungu; huyo ndiye aliyemwona Baba. Amin, amin, nawaambia, Yeye aaminiye yuna uzima wa milele.

Mimi ndimi chakula cha uzima. Baba zenu waliila mana jangwani; wakafa. Hiki ni chakula kishukacho kutoka mbinguni; mtu akila chakula hiki, ataishi milele. Na chakula nitakachotoa mimi ni mwili wangu, kwa ajili ya uzima wa ulimwengu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com