Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

YESU ANATOSHA KABISA



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Pasaka
Jumanne, Aprili 21, 2026
Juma la 3 la Pasaka

Mdo 7:51-8:1;
Zab 31:3-4,6-8,17,21 (K. 6);
Yn 6:30-35.


YESU ANATOSHA KABISA

Leo, Yesu anatumia njaa na kiu kutufundisha kwamba tunapaswa kuwa na njaa na kiu ya kiroho. Kuna njia moja tu ya kutuliza na kumaliza kiu hii… ni kwa njia yake tu. 

Mara nyingi tunapatwa na njaa na kiu. Tunakula na kunywa, lakini baada ya masaa kadhaa tunahisi tena njaa na kiu. Huu mzunguko hatuwezi kuukwepa. Miili yetu daima inadai chakula na kinywaji. Hii ni sawa pia katika maisha ya kiroho. Hatuwezi kusali mara moja na kusema basi inatosha na kumaliza kiu ya kiroho milele. Hatuwezi tu kusema namwamini Yesu mara moja na kubaki tu. Hii ni kwasababu sala na muunganiko na Yesu ni kitu ambacho kinapaswa kuchukua nafasi kila siku.

Ekaristi, “mkate wa uzima” unaridhisha kiu yetu na njaa yetu. Ekarisi ni zawadi ambayo tunapaswa kuitamani na kuipokea daima. Ukweli kwamba tunapaswa kuhudhuria misa na kupokea Ekaristi kila wakati ni ukweli kwamba maisha yetu ya Kikristo yanapaswa kufanywa mapya kila siku. 

Kumpenda Yesu na kumfuata yeye ni uamuzi ambao haupaswi tu kufanywa upaya kila siku, bali kufanywa upya kila wakati. Unapaswa kufanywa upya kama unavyo sikia njaa ya kimwili na kiu. Yesu ni mkate wa uzima wa Kiroho na kinywaji cha kweli cha kiroho. Yeye yupo kwa ajili yako. Muache yeye akamilishe hamu ya maisha. 

Sala: Bwana, ninakutamani wewe. Natamani umalize kiu yangu. Nisaidie nikugeukie wewe katika kila kitu. Nisaidie daima nitambue kuwa wewe ni yule ambaye namuhitaji na unatosha. Yesu, nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, APRILI 21, 2026



MASOMO YA MISA, APRILI 21, 2026
JUMA LA 3 LA PASAKA, JUMANNE

SOMO 1
Mdo. 7:51-8:1

Stefano aliwaambia Wakuu wa Makuhani: Enyi wenye shingo gumu, msiotahiriwa mioyo wala masikio, sikuzote mnampinga Roho Mtakatifu; kama baba zenu walivyofanya, na ninyi ni vivyo hivyo. Ni yupi katika manabii ambaye baba zenu hawakumwudhi? Nao waliwaua wale waliotabiri habari za kuja kwake yule Mwenye Haki; ambaye ninyi sasa mmekuwa wasaliti wake, mkamwua; ninyi mlioipokea torati agizo la malaika msiishike.

Basi waliposikia maneno haya, wakachomwa mioyo, wakamsagia meno.

Lakini yeye akijaa Roho Mtakatifu, akakaza macho yake, akitazama mbinguni, akauona utukufu wa Mungu, na Yesu akisimama upande wa mkono wa kuume wa Mungu. Akasema, Tazama, naona mbingu zimefunguka, na Mwana wa Adamu amesimama mkono wa kuume wa Mungu. Wakapiga kelele kwa sauti kuu, wakaziba masikio yao, wakamrukia kwa nia moja, wakamtoa nje ya mji, wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi wakaweka nguo zao miguuni pa kijana mmoja aliyeitwa Sauli. Wakampiga kw amawe Stefano, naye akiomba, akisema Bwana Yesu, pokea roho yangu. Akapiga magoti, akalia kwa sauti kuu, Bwana, usiwahesabie dhambi hii. Akiisha kusema haya akalala. Na Sauli alikuwa akiona vema kwa kuuawa kwake.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 31:2-3, 5, 7, 16, 20 (K) 5

(K) Mikononi mwako naiweka roho yangu, ee Bwana.

Uwe kwangu mwamba wa nguvu,
Nyumba yenye maboma ya kunionkoa.
Ndiwe genge langu na ngome yangu;
Kwa ajili ya jina lako uniongoze, unichunge. (K)

Mikononi mwako naiweka roho yangu; 
Umenikomboa, Ee Bwana, Mungu wa kweli.
Bali mimi namtumaini Bwana.
Na nishangilie, nizifurahie fadhili zako. (K)

Umwangaze mtumishi wako,
Kwa nuru ya uso wako;
Uniokoe kwa ajili ya fadhili zako.
Utawaficha katika hema
Na mashindano ya ndimi. (K)


SHANGILIO
Yn. 10:14

Aleluya, aleluya, 
Mimi ndimi mchungaji mwema,
nao walio wangu nawajua,
nao walio wangu wanijua mimi.
Aleluya.


INJILI
Yn. 6:30-35

Siku ile, Wayahudi walimwambia Yesu: Unafanya ishara gani basi, ili tuione tukakuamini? Unatenda kazi gani? Baba zetu waliila mana jangwani, kama vile ilivyoandikwa, Aliwapa chakula cha mbinguni ili wale.

Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Siye Musa aliyewapa chakula kile cha mbinguni, bali Baba yangu anawapa ninyi chakula cha kweli kitokacho mbinguni. Kwa maana chakula cha Mungu ni kile kishukacho kutoka mbinguni na kuupa ulimwengu uzima.
Basi wakamwambia, Bwana, sikuzote utupe chakula hiki. Yesu akawaambia, Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo 


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUKUTANA NA MCHUNGAJI MWEMA ANAYETAKATISHA ROHO ZETU




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Pasaka
JUMATATU, JUMA LA 3 LA PASAKA
Aprili 20, 2026

KUKUTANA NA MCHUNGAJI MWEMA ANAYETAKATISHA ROHO ZETU

Shangwe za Pasaka zinaendelea kutupa msingi hasa tunapo ingia katika juma la tatu la Pasaka. Mchungaji mwema amefufuka. Yeye ambaye alitoa maisha yake kwa ajili ya kondoo wake, amefufuka. Yeye ambaye anatupenda na kulinda kundi lake hakuweza kufungwa na kifo. Kilicho cha muhimu anaendelea kuwa mchungaji wetu mwema.

Shemasi Stefano alifanya kazi muhimu sana katika kanisa la mwanzo. Maisha yake ya kujitoa kabisa kwa Yesu, utayari wake wa kufa kwa ajili yake, Stefano anakuwa mfano kwa Wafiadini wote waliokuja baadae, na hata kwa wakristo wote wa nyakati zote. Leo tutasikia yupo katika kujaribiwa na kesho tutasikia kuuwawa kwake. “Wana heri ambao maisha yao hayana hatia”.

Mafundisho ya Yesu leo ni muhimu sana katika kuelewa kwetu juu ya asili ya Ekaristi na jinsi anavyotaka sisi tuijongee. Kundi lile ambalo lililishwa kwa mikate na samaki wawili sasa wapo katika kumtafuta. Kumtafuta Yesu ni muhimu sana, lakini cha muhimu yule mtafutaji lazima atambue nia yake mathubuti. Yesu anawambia, “hakika nawaambia hamnitafuti mimi kwasababu mliona miujiza, lakini kwasababu mlikula mikate na kushiba”.

Kumtafuta huku hakukuwa kwasababu ya upendo kwake, bali kufaidika naye. Sisi mara nyingi tunamtafuta Yesu kwa faida zetu, pengine kwasababu ya gari, nyumba, mchumba mwema, kuponywa kutoka katika magonjwa. Yesu aliwaonya watu wasitafute vitu viharibikavyo bali vya milele (Yesu mwenyewe). Tatizo ni hili sisi kama lile kundi, hatumtafuti Yesu zaidi ya chakula na mahitaji ya kimwili, hatumtambui kwamba yeye anafanya mioyo yetu safi kwa chakula cha milele anachotupa.

Yesu anaendelea kuwa mchungaji wetu mwema sasa. Anafanya hivi kwakutufundisha ni kitu gani tunachohitaji hasa kwa ajili ya maisha yetu, ambacho ni Ekaristi. Ni sakramenti kubwa kuliko zote, ambayo tunapaswa kuwa tumejiandaa, ili tuweze kukutana na Yesu mfufuka.

Sala: Mungu Baba yetu mwanga wako wa ukweli unatuangaza kwenye njia za Yesu Kristo. Bwana tunakuomba utuimarishe kwa sakramenti hii ya Ekaristi, ili tuweze kupata Amani, upendo, na kumjali Yesu Mchungaji wetu mwema.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, APRILI 20 2026





MASOMO YA MISA, APRILI 20  2026
JUMA LA 3 LA PASAKA, JUMATATU


SOMO 1
Mdo. 6:8-15

Stefano, akijaa neema na uwezo, alikuwa akifanya maajabu na ishara kubwa katika watu. Lakini baadhi ya watu wa sinagogi lililoitwa sinagogi la Mahuru, na la Wakirene, na la Waiskanderia, na la wale wa Kilikia na Asia, wakaondoka na kujadiliana na Stefano; lakini hawakuweza kushindana na hiyo hekima na huyo Roho aliyesema naye. Hata wakashawishi watu waliosema, tumemsikia mtu huyu akinena maneno ya kumtukana Musa na Mungu.

Wakawataharakisha watu na wazee na waandishi; wakamwendea, wakamkamata, wakampeleka mbele ya baraza. Wakasimamisha mashahidi wa uongo waliosema, Mtu huyu haachi kusema maneno ya kufuru juu ya mahali hapa patakatifu na juu ya torati; maana tumemsikia akisema kwamba Yesu huyo Mnazareti atapaharibu mahli hapa, na kuzibadili desturi tulizopewa na Musa.

Watu wote walioketi katika ile baraza wakamkazia macho yao, wakamwona uso wake kuwa kama uso wa malaika.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 119: 23-24, 26-27, 29-30 (K)

(K) Heri walio kamili njia zao.

Wakuu nao waliketi wakaninena,
Lakini mtumishi wako atazitafakari amri zako.
Shuhuda zako ndizo furaha yangu,
Na washauri wangu. (K)

Nalizisimulia njia zangu ukanijibu,
Unifundisha amri zako.
Unifahamishe njia ya mausia yako,
Nami nitayatafakari maajabu yako. (K)

Uniondolee njia ya uongo,
Unineemesha kwa sheria yako.
Nimeichagua njia ya uaminifu,
Na kuziweka hukumu zako mbele yangu. (K)


SHANGILIO
Lk. 24:25-26

Aleluya, aleluya,
Ilimpasa Kristu kupata mateso haya, na kuingia katika utukufu wake.
Aleluya.

INJILI
Yn. 6:22-29

Siku ya pili yake mkutano waliosimama ng’ambo ya bahari waliona ya kuwa hakuna mashua nyingine huko ila moja; tena ya kuwa Yesu hakuingia katika mashua ile pamoja na wanafunzi wake, bali wanafunzi wake walikwenda peke yao. Walakini zikaja mashua nyingine kutoka Tiberia mpaka karibu na mahali pale walipokula mikate, wakati Bwana aliposhukuru. Basi mkutano, walipoona ya kuwa Yesu hayuko huko wala wanafunzi wake, waliingia mashuani wenyewe, wakaenda Kapernaumu wakimtafuta Yesu. Hata walipomwona ng’ambo ya bahari, walimwambia, Rabi, wewe umekuja lini hapa?

Yesu akawajibu, akasema, Amin, amin, nawaambieni, Ninyi mnanitafuta, si kwa sababu mliona ishara, bali kwa sababu mlikula ile mikate mkashiba. Msikitendee kazi chakula chenye kuharibika, bali chakula kidumucho hata uzima wa milele; ambacho Mwana wa Adamu atawapa, kwa sababu huyo ndiye aliyetiwa muhuri na Baba, yaani, Mungu. Basi wakamwambia, Tufanyeje ili tupate kuzitenda kazi za Mungu? Yesu akajibu, akawaambia, Hii ndiyo kazi ya Mungu, mmwamini yeye aliyetumwa na yeye.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com


KUKUTANA NA YESU MFUFUKA KATIKA MAISHA YETU!




“KUFUFUKA NA KRISTO”
Tafakari ya Pasaka
Jumapili, Aprili 19, 2026 
Juma la 3 la Pasaka

Mdo 2: 14, 22-33;
Zab 15: 1-2, 5, 7-11;
1 Pet 1: 17-21;
Lk 24: 13-35.


KUKUTANA NA YESU MFUFUKA KATIKA MAISHA YETU!

Katika Asia ndogo, mwaka 80-90 AD, karibia mashuhuda wote wa Yesu mfufuka walikuwa wamesha toweka. Wakristo (wa kizazi cha tatu) wanajiuliza wenyewe: je, inawezekana sisi kukutana na Bwana? Inawezekanaje, kutoa ushuhuda kwamba yupo hai wakati sisi hatukumuona kwa macho, hatukumshika kwa mikono yetu, na wala hatukukaa mezani pamoja naye? Je sisi tunaongozwa tu kuamini kile walicho amini na kutuambia sisi? Wakristo wana tamani kumuona Yesu.

Injili ya Luka kuhusu habari ya Emaus huenda ilikuwa ndio uvuvio wa majibu na matarajio ya Wakristo hawa. Mmoja wa wawafuasi aliitwa Cleopa (mtu ambaye alijulikana sana wakati wa Kanisa la mwanzo, kwasababu alikuwa ndugu wa Yosefu, Yosefu “Baba” mlishi wa Yesu) na mwingine hajatajwa jina. Luka anaweza kuwa amefanya hivyo, kumwalika msomaji kuwa mfuasi wa pili. Mwaliko ni wito wa kutembea na Cleopa katika njia ya kumtambua Yesu mfufuka, ili kukusanyika pale ambapo wawili wamekusanyika kwa jina lake. 

Hawa wafuasi wawili wana huzuni kwasababu wameona maanguko ya mtarajio yao. Walimtazamia Masiha wa utukufu, mkuu na mfalme lakini wamejikuta wakipoteza. Marabi walifundisha kwamba, Masiha ataishi na kuongoza kwa muda wa miaka elfu moja, na tazama sasa Yesu amekufa. Walikata tamaa na kujikuta wakiona ukweli kwamba ulimwengu uliotangazwa na Yesu haukutimia. Bila Imani ya ufufuko, walioshindwa wameshindwa, maisha mwisho wake kifo, na maisha hayana maana. 

Hawa wafuasi wawili wa Emausi hawakuwa na shaka kwamba mawazo yao kuhusu Masiha yalikuwa sio sahihi. Walikuwa wamefungwa katika tamaduni na mapokeo. Walikuwa wamejifungia na kushindwa kufahamu mapya ya Mungu. Yesu hamwachi mtu ambaye anaamua kuchagua mwenyewe kwenda katika njia ya huzuni. Yeye huwa anakuwa pembeni na kuwa msindikizaji. Kutokea kwa Yesu kwa wanafunzi wake inashangaza sana. Yesu “anawafafanulia yote yaliosemwa kuhusu yeye katika Maandiko Matakatifu”. Kwa njia hiyo hawa wafuasi walitambua kwamba huyu mtu ana uelewa na hekima ya hali ya juu, na hivyo walimwalika akae pamoja nao. Yesu alikaa nao na kula nao chakula mezani nyumbani kwao. Walivyokuwa mezani “alichukua mkate, na kuubariki na kuumega na kuwapa vipande”. Macho yao yalifunguliwa na kumtambua Yesu mfufuka. Wale wafuasi baada ya kumtambua Yesu, walikimbia na kwenda kuwapasha habari na kutangaza kwamba “Bwana amefufuka kweli kweli”.

Habari ya wafuasi wa Emausi inarudiwa kila siku katika Liturjia ya Ekaristi (Misa Takatifu). Inaanza kwa kuingia kwa padre, alafu Liturjia ya neno la Mungu na homilia, na mwishowe, “kuumega mkate”. Ni katika wakati wa Ekaristi takatifu macho yetu yanafumbuliwa tunatambua kwamba Yesu mfufuka yupo kati yetu. Bila neno hatuwezi kuja kumtambua Bwana, hatuwezi kumtambua Yesu katika Ekaristi Takatifu. Wakati misa inaisha tunamaliza na wimbo wa mwisho na hatimaye tunaondoka na furaha, kwenda kushirikisha furaha ya Yesu mfufuka. 

Misa takatifu ni safari yetu ya Emmaus. Tunapaswa kujikita wenyewe katika kumuona Yesu, na kumtambua na kumwabudu. Tunapaswa kutambua uwepo wa Yesu mfufuka kati yetu. Yupo nasi hapa sasa, anatupenda sisi, anaongea na sisi, na anatuita tumpende yeye. Mtafute na msikilize sauti yake. Tutashangaa ni kwa jinsi ghani Bwana mfufuka atakavyo tufanya tutembee naye katika Maandiko Matakatifu, na kujifunua mwenyewe na kuleta furaha katika huzuni yetu na katika mioyo yetu iliokata tamaa. 

Sala: Bwana, ninakushukuru kwa kunipenda mimi sana kiasi kwamba upo na mimi daima. Nipe macho ya Imani niweze kukutana nawe katika Maandiko Matakatifu na kukuona wewe ukiwa ndani ya Ekaristi Takatifu. Ninaomba niweze kutambua uwepo wako katika mambo ya kawaida yanayo tokea katika maisha yangu. Ninakupenda Bwana wangu. Yesu, nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, APRILI 19, 2026



MASOMO YA MISA, APRILI 19, 2026
DOMINIKA YA 3 YA PASAKA

SOMO 1
Mdo. 2:14, 22 – 28

Petro akasimama pamoja na wale kumi na mmoja, akapaza sauti yake, akawaambia, Enyi watu wa Uyahudi, na ninyi nyote mkaao Yerusalemu, lijueni jambo hili, mkasikilize maneno yangu.

Yesu wa Nazareti, mtu aliyedhihirishwa kwenu na Mungu kwa miujiza na ajabu na ishara, ambazo Mungu alizifanya kwa mkono wake kati yenu, kama ninyi wenyewe mnavyojua; mtu huyu alipotolewa kwa shauri la Mungu lililokusudiwa, na kwa kujua kwake tangu zamani, ninyi mkasulibisha kwa mikono ya watu wabaya, mkamwua; ambaye Mungu alimfufua, akaufungua uchungu wa mauti, kwa sababu haikuwezekana ashikwe nao. Maana Daudi ataja habari zake.

Nalimwona Bwana mbele yangu sikuzote, Kwa kuwa yuko upande wa mkono wangu wa kuume, nisitikisike.

Kwa hiyo moyo wangu ukapendezewa, ulimi wangu ukafurahi; Tena mwili wangu nao utakaa katika matumaini. Kwa maana hutaiacha roho yangu katika kuzimu; Wala hutamtoa Mtakatifu wako aone uharibifu. Umenijulisha njia za uzima; Utanijaza furaha kwa uso wako.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 16:1 – 2, 5, 7 – 11 (K) 11

(K) Utanijulisha njia ya uzima.

Mungu unihifadhi mimi,
Kwa maana nakukimbilia Wewe.
Nimemwambia Bwana, Ndiwe Bwana wangu;
Bwana ndiye fungu la posho langu, na la kikombe changu;
Wewe unaishika kura yangu. (K)

Nitamhimidi Bwana aliyenipa shauri,
Naam, mtima wangu umenifundisha usiku.
Nimemweka Bwana mbele yangu daima,
Kwa kuwa yako kuumeni kwangu, sitaondoshwa. (K)

Kwa hiyo moyo wangu unafurahi,
Nao utukufu wangu unashangilia,
Naam, mwili wangu nao utakaa kwa kutumaini.
Maana hutaiachaia kuzimu nafsi yangu.
Wala hutamtoa mtakatifu wako aone uharibifu. (K)

Utanijulisha njia ya uzima;
Mbele za uso wako ziko furaha tele;
Na katika mkono wako wa kuume mna mema ya milele. (K)



SOMO 2
1Pet. 1:17 – 21

Ikiwa mnamwita Baba, yeye ahukumuye kila mtu pasipo upendeleo, kwa kadiri ya kazi yake enendeni kwa hofu katika wakati wenu wa kukaa hapa kama wageni. Nanyi mfahamu kwamba mlikombolewa kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa damu ya thamani, kama ya mwanakondoo asiye na ila, asiye na waa, ya Kristo. Naye amejulikana kweli tangu zamani, kabla haijawekwa misingi ya dunia; lakini alifunuliwa mwisho wa zamani kwa ajili yenu; ambao kwa yeye mmekuwa wenye kumwamini Mungu, aliyemfufua katika wafu akampa utukufu; hata Imani yenu na tumaini lenu liwe kwa Mungu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



SHANGILIO
Lk. 24:32

Aleluya, aleluya,
Bwana Yesu, utufunulie maandiko; uwashe mioyo yetu unaposema nasi. Aleluya.



INJILI
Lk. 24:13 – 35

Siku ile watu wawili miongoni mwa wafuasi wa Yesu walikuwa wakienda kijiji kimoja, jina lake Emau, kilichokuwa mbali na Yerusalemu kama mwendo wa saa mbili. nao walikuwa wakizungumza wao kwa wao habari za mambo hayo yote yaliyotukia. Ikawa katika kuzungumza na kuulizana kwao, Yesu mwenyewe alikaribia, akaandamana nao. Macho yao yakafumbwa wasimtambue. Akawaambia, Ni maneno gani haya mnayosemezana hivi mnapotembea? Wakasimama wamekunja nyuso zao.

Akajibu mmoja wao, jina lake Kleopa, akamwambia, Je! Wewe peke yako u mgeni katika Yerusalemu, hata huyajui yaliyotukia humo siku hizi? Akawauliza, Mambo gani? Wakamwambia, Mambo ya Yesu wa Nazareti, aliyekuwa mtu nabii, mwenye uwezo katika kutenda na kunena mbele za Mungu na watu wote; tena jinsi wakuu wa makuhani na wakubwa wetu walivyomtia katika hukumu ya kufa, wakamsulibisha. Nasi tulikuwa tukitumaini ya kuwa yeye ndiye atakayewakomboa Israeli. Zaidi ya hayo yote, leo ni siku ya tatu tangu yalipotendeka mambo hayo; tena, wanawake kadha wa kadha wa kwetu walitushitusha, waliokwenda kaburini asubuhi na mapema, wasiuone mwili wake; wakaja wakasema ya kwamba wametokewa na malaika waliosema kwamba yu hai. Na wengine waliokuwa pamoja nasi walikwenda kaburini wakaona vivyo hivyo kama wale wanawake walivyosema, ila yeye hawakumwona.

Akawaambia, Enyi msiofahamu, wenye mioyo mizito ya kuamini yote waliyoyasema manabii! Je! Haikumpasa Kristo kupata mateso haya na kuingia katika utukufu wake? Akaanza kutoka Musa na manabii wote, akawaeleza katika maandiko yote mambo yaliyomhusu yeye mwenyewe.

Wakakikaribia kile kijiji walichokuwa wakienda, naye alifanya kama anataka kuendelea mbele. Wakamshawishi wakisema, Kaa pamoja nasi, kwa kuwa kumekuchwa, na mchana unakwisha. Akaingia ndani kukaa nao. Ikawa alipokuwa ameketi nao chakulani, alitwaa mkate, akaubariki, akaumega, akawapa. Yakafumbuliwa macho yao, wakamtambua; kisha akatoweka mbele yao. Wakaambiana, Je! Mioyo yetu haikuwaka ndani yetu hapo alipokuwa akisema nasi njiani, na kutufunulia maandiko?

Wakaondoka saa ile ile, wakarejea Yerusalemu, wakawakuta wale kumi na mmoja wamekutanika, wao na wale waliokuwa pamoja nao, wakisema, Bwana amefufuka kweli kweli, naye amemtokea Simoni, nao waliwapa habari ya mambo yale ya njiani, na jinsi alivyotambulikana nao katika kuumega mkate.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUTULIZA DHORUBA ZETU!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Pasaka
Jumamosi, Aprili 18, 2026 
Juma la 2 la Pasaka


Mdo 6:1-7
Zab 33:1-2,4-5,18-19,22
Yn 6:16-21


KUTULIZA DHORUBA ZETU!

Katika Injili ya leo Yesu anatembea juu ya maji na anawaambia mitume wake “Jipeni moyo ni mimi. Msiogope”. Injili ya leo inatutia nguvu na kutuambia tusiogope tunapo kutana na dhoruba na mawimbi ya maisha. Hatupaswi kuogopa tupo na Yesu. 

Kuwa katikati ya bahari wakati wa giza inaogopesha sana. Kila upande unaoneakana kuwa sawa na huwezi kuona nchi kavu. Tunajisikia kama vile hatujazungukwa na kitu. Mitume wametoka, na wapo baharini wakati wa giza. Watakuwa wamejisikia kama vile wamepotea katikati na hamna kitu. Lakini katikati ya hali hii, Yesu anawajia akiwa anatembea juu ya maji. Na kuwaambia “jipeni moyo ni mimi. Msiogope”. 

Tunaona katika maisha haya ya mitume mfanano wa maisha ya kila siku ya wengi wetu. Wengi twaweza kujisikia kwamba hatuja zungukwa na mtu na hatuna msaidizi, tupo wenyewe na tunapotea. Injili inatufunulia kwamba Yesu anakuja kwetu haijalishi tupo sehemu ghani au tumejikuta katika hali ghani. Yeye hatusubiri sisi tuende kumtafuta, bali anakuja na kuingia katika maisha yetu, alimradi tunamtambua na kumkaribisha. 

Pengine maisha yetu yamejazwa na kazi nyingi, lakini tunajisikia wa pweke. Pengine maisha yetu ni yale ambayo hatuna watu wengi wanaotupenda na tunajikuta tupo wenyewe na kutengwa. Au pengine tunajifanya kuvaa sura ya kuonesha kwamba nina kila kitu lakini ndani mwangu nina hangaika. Katika hali yeyote ile ambayo unaweza kujikuta Yesu anataka kuja kwetu na kutufariji. Msikilize akisema “jipe moyo ni mimi. Usiogope”. Hali katika maisha inaweza kuwa inatisha na kutupa mashaka na woga. Lakini tutakapo ruhusu kumwelekea Yesu, hofu inapotea. Tutambua ndani mwetu kwamba Yesu yupo na mambo yataenda vizuri kwasababu yeye anaongoza kila kitu. Mwache aingie katika mashua ya moyo wako na umwache aongoze. Anakuja kwako na anasubiri jibu lako. 

Sala: Bwana, ni mara nyingi nimeshindwa kushuhudia uwepo wako wa Kimungu katika maisha yangu. Ni mara nyingi nimeshindwa kukuona ukija katika maisha yangu. Nisaidie niweze kutambua kuwa kila mara upo. Niweke huru kutoka katika hali mbali mbali za maisha, na nipe ujasiri wa kukukaribisha wewe katika maisha yangu. Yesu nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, APRILI 18, 2026



MASOMO YA MISA, APRILI 18, 2026
JUMA LA PILI LA PASAKA, JUMAMOSI

SOMO 1
Mdo 6:1-7

Hata siku zile wanafunzi walipokuwa wakiongezeka hesabu yao, palikuwa na manung'uniko ya Wayahudi wa Kiyunani juu ya Waebrania kwa sababu wajane wao walisahauliwa katika huduma ya kila siku. Wale Thenashara wakawaita jamii ya wanafunzi, wakasema, Haipendezi sisi kuliacha neno la Mungu na kuhudumu mezani. Basi ndugu, chagueni watu saba miongoni mwenu, walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho, na hekima, ili tuwaweke juu ya jambo hili; na sisi tutadumu katika kuomba na kulihudumia lile Neno. Neno hili likapendeza machoni pa mkutano wote; wakamchagua Stefano, mtu aliyejaa imani na Roho Mtakatifu, na Filipo, na Prokoro, na Nikanori, na Timoni, na Parmena, na Nikolao mwongofu wa Antiokia; ambao wakawaweka mbele ya mitume, na walipokwisha kuomba wakaweka mikono yao juu yao. Neno la Mungu likaenea; na hesabu ya wanafunzi ikazidi sana katika Yerusalemu; jamii kubwa ya makuhani wakaitii ile Imani.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab 33:1-2, 4-5, 18-19

(K)Ee Bwana, fadhili zako zikae nasi, Kama vile tulivyokungoja Wewe.

Mpigieni Bwana vigelegele, enyi wenye haki, 
Kusifu kunawapasa wanyofu wa moyo. 
Mshukuruni Bwana kwa kinubi, 
Kwa kinanda cha nyuzi kumi mwimbieni sifa. (K)

Kwa kuwa neno la Bwana lina adili, 
Na kazi yake yote huitenda kwa uaminifu. 
Huzipenda haki na hukumu, 
Nchi imejaa fadhili za Bwana. (K)

Tazama, jicho la Bwana li kwao wamchao, 
Wazingojeao fadhili zake. 
Yeye huwaponya nafsi zao na mauti, 
Na kuwahuisha wakati wa njaa. (K) 



SHANGILIO
Yn. 10:27

Aleluya, aleluya,
Kondoo wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua, nao wanifuata.
Aleluya.



INJILI
Yn 6:16-21

Hata ilipokuwa jioni wanafunzi wake wakatelemka baharini wakapanda chomboni, wakaanza kuivuka bahari kwenda Kapernaumu. Nako kumekwisha kuwa giza, wala Yesu hajawafikia. Na bahari ikaanza kuchafuka kwa kuvuma upepo mkuu. Basi wakavuta makasia kadiri ya maili tatu nne, wakamwona Yesu anakwenda juu ya bahari na kukikaribia chombo; wakaogopa. Naye akawaambia, Ni mimi, msiogope. Basi wakataka kumpokea chomboni; na mara hiyo chombo kikaifikilia nchi waliyokuwa wakiiendea.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo. 


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUFAULU KATIKA JARIBIO LA IMANI!


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Pasaka
Ijumaa, Aprili 17, 2026
Juma la 2 la Pasaka

Mdo 5:34-42
Zab 27: 1,4,13-14
Yn 6:1-15


KUFAULU KATIKA JARIBIO LA IMANI!

Mungu daima anatambua anachopenda kufanya. Daima yeye ana mpango mkamilifu wa maisha yetu. Leo katika Injili, Yesu anafanya muujiza wa kuwalisha watu kwa mkate na samaki. Yesu alitambua kwamba ataongeza mkate na samaki ili kuwalisha watu zaidi ya elfu tano. Lakini kabla ya kufanya hili, anamjaribu Philipo. Hivyo hivyo Yesu anatujaribu wakati mwingine. Je, hafanyi hivyo? 

Majaribio haya sio kwamba Yesu anapenda kutuuliza tu au kufanya mchezo Fulani na sisi. Bali, anatupa nafasi ya kudhihirisha imani yetu kwake. Jaribio lililopo kwenye Injili lilikuwa ni kumfanya Philipo atumie Imani zaidi kuliko kufikiri kwa kawaida pekee. Philipo aliitwa ili kudhihirisha imani kwamba Mwana wa Mungu yupo pamoja nao pale. Lakini alishindwa jaribio. Alinyoosha mkono kwa ile hali ya kutokuwezekana. Lakini katika hali nyingine ni kama Andrea alikuja kuokoa. Anasema kuna kijana hapa ana mkate na visamaki vichache. Lakini yeye pia alikuwa na Imani kidogo, aliongeza kusema “lakini vya faa nini kwa umati huu mkubwa namna hii?”. 

Chembe hii dogo ya imani ya Andrea, ilitosha kwa Yesu kuamuru watu waketi makundi makundi na hivyo kufanya ule muujiza. Inaonekana kwamba Andrea alikuwa na ufahamu kidogo kwamba ilikuwa muhimu kutaja visamaki hivi na mkate. Yesu anavichukua kutoka katika mikono ya Andrea na kuwajali watu. 

Mara nyingi tunajikuta katika hali ngumu na hatujui tufanye nini. Tunapaswa kujitahidi kuwa na imani kidogo ili Yesu aweze kuwa na kitu cha kutenda katika maisha yetu. Tunaweza tusiwe na ufahamu wa nini anaenda kufanya, lakini ni lazima kuwa na ufahamu hata kidogo kwamba Mungu ndiye anaye tuongoza sisi. Kama tutaweza hata kukuza Imani hii kidogo sisi pia tutashinda majaribio. 

Sala: Bwana, nisaidie niweze kuwa na Imani kamili ya mpango wako ambao unapenda kuufanya katika maisha yangu. Nisaidie niweze kufahamu kwamba wewe unaongoza na kuyalinda maisha yangu hata pale ninapo ona maisha yanayumba. Katika hali hizo, ninaomba Imani ninayo onesha iwe zawadi kwako ili uweze kuitumia kwa utukufu wako. Yesu, nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, APRILI 17, 2026


MASOMO YA MISA, APRILI 17, 2026
JUMA LA PILI LA PASAKA, IJUMAA

SOMO 1
Mdo 5:34-42

Lakini mtu mmoja, Farisayo, jina lake Gamalieli, mwalimu wa torati, mwenye kuheshimiwa na watu wote, akasimama katika baraza, akaamuru mitume wawekwe nje kitambo kidogo, akawaambia, Enyi waume wa Israeli, jihadharini jinsi mtakavyowatenda watu hawa. Kwa sababu kabla ya siku hizi aliondoka Theuda, akijidai ya kuwa yeye ni mtu mkuu, watu wapata mia nne wakashikamana naye; naye aliuawa na wote waliomsadiki wakatawanyika wakawa si kitu. Baada ya mtu huyo aliondoka Yuda Mgalilaya, siku zile za kuandikiwa orodha, akawavuta watu kadha wa kadha nyuma yake, naye pia akapotea na wote waliomsadiki wakatawanyika. Basi sasa nawaambia, Jiepusheni na watu hawa, waacheni; kwa kuwa shauri hili au kazi hii ikiwa imetoka kwa binadamu, itavunjwa, lakini ikiwa imetoka kwa Mungu hamwezi kuivunja; msije mkaonekana kuwa mnapigana na Mungu. Wakakubali maneno yake; nao walipowaita mitume, wakawapiga, wakawaamuru wasinene kwa jina lake Yesu; kisha wakawaacha waende zao. Nao wakatoka katika ile baraza, wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya Jina hilo. Na kila siku, ndani ya hekalu na nyumbani mwao, hawakuacha kufundisha na kuhubiri habari njema za Yesu kwamba ni Kristo.

Neno la Bwana… Tumshukuru Bwana.


WIMBO WA KATIKATI
Zab 27:1, 4, 13-14

(K)Neno moja nimelitaka kwa Bwana,
Nikae nyumbani mwa Bwana.

Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, 
Nimwogope nani? 
Bwana ni ngome ya uzima wangu, 
Nimhofu nani? (K)

Neno Moja nimelitaka kwa Bwana, 
Nalo ndilo nitakalolitafuta,
Nikae nyumbani mwa Bwana 
Siku zote za maisha yangu, 
Niutazame uzuri wa Bwana, 
Na kutafakari hekaluni mwake. (K)

Naamini ya kuwa nitauona wema wa Bwana 
Katika nchi ya walio hai. 
Umngoje Bwana, uwe hodari, 
Upige moyo konde, naam, umngoje Bwana. (K)



SHANGILIO
Kol. 3:1

Aleluya, aleluya.
Mkiwa mmefufuliwa na Kristo, yatafuteni yaliyo juu, Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu.
Aleluya.


INJILI
Yn 6:1-15

Baada ya hayo Yesu alikwenda zake ng'ambo ya Bahari ya Galilaya, nayo ndiyo ya Tiberia. Na mkutano mkuu wakamfuata, kwa sababu waliziona ishara alizowafanyia wagonjwa. Naye Yesu akakwea mlimani, akaketi huko pamoja na wanafunzi wake. Na Pasaka, sikukuu ya Wayahudi, ilikuwa karibu. Basi Yesu alipoinua macho yake akaona mkutano mkuu wanakuja kwake, alimwambia Filipo, Tununue wapi mikate, ili hawa wapate kula? Na hilo alilinena ili kumjaribu; kwa maana alijua mwenyewe atakalotenda. Filipo akamjibu, Mikate ya dinari mia mbili haiwatoshi, kila mmoja apate kidogo tu. Wanafunzi wake mmojawapo, Andrea, nduguye Simoni Petro, akamwambia, Yupo hapa mtoto, yuna mikate mitano ya shayiri na samaki wawili, lakini hivi ni nini kwa watu wengi kama hawa? Yesu akasema, Waketisheni watu. Na mahali pale palikuwa na majani tele. Basi watu waume wakaketi, wapata elfu tano jumla yao. Basi Yesu akaitwaa ile mikate, akashukuru, akawagawia walioketi; na kadhalika katika wale samaki kwa kadiri walivyotaka. Nao waliposhiba, aliwaambia wanafunzi wake, Kusanyeni vipande vilivyobaki, kisipotee cho chote. Basi wakavikusanya, wakajaza vikapu kumi na viwili, vipande vya mikate mitano ya shayiri vilivyowabakia wale waliokula. Basi watu wale, walipoiona ishara aliyoifanya, walisema, Hakika huyu ni nabii yule ajaye ulimwenguni. Kisha Yesu, hali akitambua ya kuwa walitaka kuja kumshika ili wamfanye mfalme, akajitenga, akaenda tena mlimani yeye peke yake. 

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo
 

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.