Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

HARUFU NZURI YA UPENDO!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Kwaresima
Jumatatu, Machi 30, 2026
Juma Kuu

Isa 42: 1-7; 
Zab 27: 1-3, 13-14; 
Yn 12: 1-11.


HARUFU NZURI YA UPENDO!

Upendo haujui mipaka. Leo, Maria anafanya kitu ambacho ni upendo pekee waweza kufanya. Alichukua kitu cha thamani kubwa kabisa alichokuwa nacho, alichukuwa mafuta na kumpaka Yesu miguu. Kitendo cha Maria kilisukumwa na kitu kimoja tu, tena kimoja tu, Upendo wake kwa Yesu na shukrani kwa huruma ya Mungu. Ilikuwa pia muhimu tena kwamba, Maria alimpangusa Yesu miguu kwa nywele zake, wakati nywele zuri zilizo wekwa vizuri huonyesha utu wa mwanamke kipindi hicho.

Kawaida mwanamke alijisikia fahari kwa nywele zake, ambazo zilichukuliwa kama kivutio, na kama mmoja nywele zake hazikuwa vizuri au kuharibika basi alionekana kama asiye na bahati, au anakosa thamani. Kwakutumia nywele zake kupangusa miguu ya Yesu, Maria alionyesha hali yake ya kujishusha na utayari wake wa kumtumikia Kristo. Maria ni mkarimu na ni mfano wa mfuasi mwema. Anafanya kitu ambacho Yesu angefanya baadae……kuwaosha miguu wafuasi wake.

Yesu hakuwa mbinafsi kwa upendo wake kwetu sisi. Kwa kukubali kupakwa mafuta na Maria Yesu anatukumbusha kitu ambacho tunapaswa kutenda. Tunapaswa kumwabudu, kumheshimu na kumfanya kuwa kiini cha maisha yetu. Tunapaswa kunyenyekea mbele zake na kumtumikia. Si kwasababu yeye anataka tufanye vile tu, bali sisi tunapaswa tufanya vile. Kumheshimu kwa unyenyekevu na upendo ndicho tunacho hitaji kufanya kwasababu ya utakatifu wetu na furaha yetu. Yesu alitambua hili, hivyo anamsifu Maria kwa upendo huu. Kitendo hichi kinatukumbusha sisi pia kufanya vile vile. Kinataka tumtazame Yesu na kumfanya kiini cha kumtukuza na Upendo. Inatualika kuweka kila kazi yetu kwa Yesu (ambayo inawakilishwa na yale Marahamu, mshahara wa siku 300). Hakuna kitu ambacho ni cha gharama sana kwa Yesu. Hakuna chenye thamani kubwa kama Kumwabudu Yesu. 

Injili inaeleza kwamba, nyumba yote ilijazwa harufu nzuri ya marashi aliopakwa Yesu. Alichofanya Maria kinaleta harufu nzuri ya furaha kila mahali, ni kama siku chache zijazo tutakapo muona Yesu akituonesha upendo wake wa hali ya juu kwa kutoa kilicho chema kabisa alichokuwa nacho, ambacho ni kutoa damu yake kwaajili yetu na kutupa Roho wake Mtakatifu. Tunapata mfano wa upendo ndani ya Maria na ndani ya Yesu, tuombe pia maisha yetu yatoe harufu nzuri ya upendo wa Yesu. 

Sala: Bwana, ninaomba nifuate mfano wa huyu mwanamke mtakatifu, maria. Bwana mpendwa, hakuna kitu kwenye maisha chenye thamani kama wewe na majitoleo yangu kwako. Ninaomba unitue kwako Ee Yesu, ninyenyekeshe mbele ya utukufu wako nisaidie niweze kupenda na kukuabudu kwa moyo wangu wote. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MACHI 30, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 30, 2026
JUMATATU YA JUMA KUU

SOMO
Isa. 42:1-7

Tazama mtumishi wangu nimtegemezaye; mteule wangu, ambaye nafsi yangu imependezwa naye; nimetia roho yangu juu yake; naye atawatolea mataifa hukumu.

Hatalia, wala hatapaza sauti yake, wala kuifanya isikiwe katika njia kuu. Mwanzi uliopondeka hatauvunja, wala utambi utokao moshi hatauzima; atatokeza hukumu kwa kweli.

Hatazimia, wala hatakata tamaa, hata atakapoweka hukumu duniani; na visiwa vitaingojea sheria yake.

Mungu Bwana anena, yeye aliyeziumba mbingu, na kuzitanda; yeye aliyeitandaza nchi na mazao yake; yeye awapaye pumzi watu walio juu yake; yeye awapaye roho wao waendao ndani yake.

Mimi, Bwana nimekuita katika haki, nami nitakushika mkono, na kukulinda, na kukutoa uwe agano la watu, na nuru ya mataifa; kuyafunua macho ya vipofu, kuwatoa gerezani waliofungwa, kuwatoa wale walioketi gizani katika nyumba ya kufungwa.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 27:1-3, 13-14 (K) 1

(K) Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu.

Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu,
Nimwogope nani?
Bwana ni ngome ya uzima wangu,
Nimhofu nani? (K)

Watenda mabaya waliponikaribia,
Wanile nyama yangu,
Watesi wangu na adui zangu,
Walijikwaa wakaanguka. (K)

Jeshi lijapojipanga kupigana nami,
Moyo wangu hautaogopa.
Vita vijaponitokea,
Hata japo nitatumaini. (K)

Naamini ya kuwa nitauona wema wa Bwana
Katika nchi ya walio hai.
Umngoje Bwana, uwe hodari,
Upige moyo konde, naam, umngoje Bwana. (K)


SANGILIO
Eze. 18:31

Tupilieni mbali nanyi makossa yenu yote mliyoyakosa, asema Bwana, jifanyieni moyo mpya na roho mpya.


INJILI
Yn. 12:1-11

Siku sita kabla ya Pasaka, Yesu alifika Bethania, alipokuwapo Lazaro, yeye ambaye Yesu alimfufua katika wafu. Basi wakamwandalia karamu huko; naye Martha akatumika; na Lazaro alikuwa mmojawapo wa wale walioketi chakulani pamoja naye. 

Basi Mariamu akatwaa ratli ya marhamu ya nardo safi yenye thamani nyingi, akampaka Yesu miguu, akamfuta miguu kwa nywele zake. Nayo nyumba pia ikajaa harufu ya marhamu.

Basi Yuda Iskariote, mmojawapo wa wanafunzi wake, ambaye ndiye atakaye kumsaliti, akasema, Mbona marhamu hii haikuuzwa kwa dinari mia tatu, wakapewa maskini? Naye aliyasema hayo, si kwa kuwahurumia maskini; bali kwa kuwa ni mwivi, naye ndiye aliyeshika mfuko, akavichukua vilivyotiwa humo.

Basi yesu alisema, Mwache aiweke kwa siku za maziko yangu. Kwa maana maskini mnao sikuzote pamoja nanyi; bali mimi hamnami sikuzote.

Basi watu wengi katika Wayahudi walipata kujua ya kuwa yeye yuko huko; nao wakaja, si kwa ajili yake Yesu tu, ila wamwone na Lazaro, ambaye Yesu alimfufua katika wafu. Nao wakuu wa makuhani wakafanya shauri la kumwua Lazaro naye; maana kwa ajili yake wengi katika Wayahudi walijitenga, wakamwamini Yesu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MUNGU WANGU, MUNGU WANGU, MBONA UMENIACHA!


KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Jumapili, Machi 29, 2026
Juma Kuu

JUMAPILI YA MATAWI

Mt 21:1-11 (Kutangaza ujio wa Bwana, Baraka ya matawi)

Isa 50: 4-7;
Zab 22: 8-9, 17-20, 23-24;
Fil  2: 6-11;
Mt 26:14 - 27:66.


MUNGU WANGU, MUNGU WANGU, MBONA UMENIACHA!


Leo ni jumapili ya matawi au jumapili ya mateso. Kipindi cha kwaresima tulicho kianza Jumatano ya Majivu, kinapata nguvu kwa liturjia ya juma hili na kilele chake kwa jumapili ya Pasaka. Kuanzia leo, liturjia zitakuwa zimejazwa na ishara na alama mbali mbali: matawi, kuoshwa miguu, nk. Tusikubali ibada hizi zipite machoni mwetu kama tu ishara ya nje pekee bali tuzichukue kama nafasi ya kuchunguza Imani yangu, ukweli na uhusiano wangu na Mungu.

Jumapili ya matawi inaonesha shangwe juu ya Yesu akiwa anaingia Yerusalem. Liturjia ya leo tunakumbwa na hisia mbili tofauti. Tunaanza lirtujia yetu kwa utukufu na shangwe kuenzi jinsi Yesu alivyo ingia Yerusalemu kwa shangwe kwa kuimba ‘hosanna, hosanna juu mbinguni’. Watu walifurahi kumuona Yesu alivyo ingia Yerusalemu kwa shangwe, lakini hali hii inapotea taratibu baada ya kuanza kuingia kwa undani katika masomo yetu hali inabadilika na kuwa ya kustua na huzuni. Injili inaishia na kutundikwa kwa Yesu msalabani na Yesu analia kwa sauti kuu nakusema “Mungu wangu mungu wangu, mbona umeniacha” na baada ya hayo Yesu anatoa pumzi yake ya mwisho na kukata roho. Kwa muda huu watu wote hupiga magoni kwa ukimya kutafakari kifo cha Yesu. Ni kwa jinsi ghani mambo yanaweza kubadilika kwa muda mfupi? Ni nini kilitokea kwa watu ambao walikuwa wakishangilia na kumsifu alivyokuwa anaingia Yerusalemu? Waliruhusuje, mtu huyu aingie katika mateso ya msalaba na kufa?

Jibu la ndani na la kweli kabisa kwa swali hili ni kwamba Baba aliruhusu haya yatendeke. Baba aliruhusu wamkane na kuruhusu asulubiwe. Yesu alikuwa na uwezo wakuonesha nguvu zake za Kimungu na kukataa kukumbatia mateso ya msalaba. Lakini hakufanya hivyo. Bali aliingia katika mateso na kukataliwa. Na wala hakufanya kwa kujutia au akilalamika. Aliyafanya kwa mapezi yake na kuyachagua kwa mapenzi yake.

Leo somo la kwanza linaeleza kwa undani kwamba, Yesu ni “Mtumishi wa Bwana anayeteseka”. Alijifunza kutii kwa njia ya mateso na kwa ajili ya utii wake, Mungu alimkweza juu kabisa. Alikuwa mtii hata kufa! Kila mkristo anatakiwa kupata nguvu kutoka katika njia ya Kristo. “Niliwapa mgongo wangu walio nipiga” somo la kwanza linasema. Hali ileile ambayo Yesu, mtumishi wa Mungu aliyeteseka ikatusaidia sisi wote. Hakurudisha kisasi, hakulalamika, wala kulaumu au kujionea huruma. Yesu aliyaangalia mateso na uchungu kama njia ya kuonesha upendo wake kwa Baba na upendo wake kwetu.

Mateso ya Yesu, yanatuonesha hisia, tabia na mtazamo wa watu. Kwa wakati mmoja walikuwa wamebeba matawi mikononi, wakitandaza nguo zao, wakiimba hosanna mfalme na siku chache baadae wanakuja kupiga tena kelele, ‘asulubiwe’ kwa Pilato. Kwanini, Mungu Baba aliruhusu haya? Kwa nini Yesu alichagua mateso na kifo? Kwasababu ndani ya hekima kamilifu ya Baba, mateso na kifo yalikuwa kwa lengo kubwa. Mungu aliamua kuaibisha hekima ya ulimwengu huu kwa kutumia mateso na kifo kama njia kamili ya kupata utakatifu. Kwa tendo hili, alibadilisha uovu mkubwa kuwa wema mkubwa. Msalaba unaninginia katikati mbele ya makanisa yetu na nyumbani kwetu, kuonesha kwamba hakuna hata uovu uwe mkubwa kiasi ghani unaoweza kushinda nguvu, hekima na upendo wa Mungu. Mungu ana nguvu kuliko kifo chenyewe na Mungu ana ushindi wa mwisho hata baada ya yote kuonekana yamepotea. Juma hili litupe matumaini ya Kimungu mara nyingi tunaweza kusukumwa kukata tamaa na mbaya zaidi tunaweza kushawishika kukata tamaa kabisa. Hakuna ugumu, hakuna msalaba unaweza kutushinda kama tutabaki waaminifu kwa Yesu Kristo tukimruhusu yeye abadilishe maisha yetu kwa utukufu aliokumbatia msalabani.

Ilikuwa ni watu kama Maria, Mama yake, mtume mwaminifu kama Yohane na wengine wachache walioweza kusimama pembeni nje ya kundi na kusimama karibu na Yesu. Katika mwanga wa simulizi la mateso ya Yesu na matukio mengine katika maisha ya Yesu ambayo yatasikika katika juma hili, tunapaswa kujitambua wenyewe. Je, mimi ni Mkristo wa makundi tu au Mkristo tu tukiwa wengi? Je mi ni Mkristo tu pale ninapo pata pato Fulani au sifa Fulani? Je, mimi ni muoga kusimamia ukweli?

Sala: Bwana, ninapojaribiwa mpaka kukaribia kukata tamaa, naomba unipe matumaini. Nisaidie niweze kuona uwepo wako katika kila kitu, hata katika vitu ambavyo vinanisumbua mimi. Ninaomba juma hili kuu, libadilishe nyakati zangu za giza na mapungufu ninapo jikabidhi kwako, Mungu wangu. Yesu, nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MACHI 29, 2026




MASOMO YA MISA, MACHI 29, 2026
DOMINIKA YA MATAWI

SOMO 1
Isa. 50:4 – 7

Bwana Mungu amenipa ulimi wa hao wafundishwao, nipate kujua jinsi ya kumtegemeza kwa maneno yeye aliyechoka, huniamsha asubuhi baada ya asubuhi; huniamsha, sikio langu lipate kusikia kama watu wafundishwao. Bwana Mungu amenizibua sikio langu, wala sikuwa mkaidi, wala sikurudi nyuma. Naliwatolea wapigao mgongo wangu, na wang’oao ndevu mashavu yangu; sikuficha uso wangu usipate fedheha na kutemewa mate. Maana Bwana Mungu atanisaidia; kwa sababu hiyo sikutahayari, kwa sababu hiyo nimekaza uso wangu kama gumegume, nami najua ya kuwa sitaona haya.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 22:7 – 8; 16 – 17a; 18 – 19; 22 – 23 (K)22:1

(K) Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?

Wote wanionao hunicheka sana
Hinifyonya, wakitikisa vichwa vyao;
Husema: Umtegemee Bwana; na amponye;
Na amwokoe sasa, maana apendezwa naye. (K)

Kwa maana mbwa wamenizunguka;
Kusanyiko la waovu wamenisonga;
Yamenizua mikono na miguu.
Naweza kuihesabu mifupa yangu yote. (K)

Wanagawanya nguo zangu,
Na vazi langu wanalipigia kura.
Nawe, Bwana, usiwe mbali,
Ee Mungu wangu, fanya haraka kunisaidia. (K)

Nitalihubiri jina lako kwa ndugu zangu,
Katikati ya kusanyiko nitakusifu.
Ninyi mnaomcha Bwana msifuni
Enyi nyote mlio wazao wa Yakobo, mtukuzeni. (K)



SOMO 2
Flp. 2:6 – 11

Ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa Yesu Kristo ni Bwana, kwa utukufu wa Mungu Baba.



SHANGILIO
Flp. 2:8 – 9

Kristu alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina.



INJILI
Mt. 26: 14 – 27: 66

Wakati huo mmoja wa wale Thenashara, jina lake Yuda Iskariote, aliwaendea wakuu wa makuhani, akasema, Ni nini mtakachonipa, nami nitamsaliti kwenu? Wakampimia vipande thelathini vya fedha. Tokea wakati huo akawa akitafuta nafasi apate kumsaliti. Hata siku ya kwanza ya mikate isiyotiwa chachu, wanafunzi wake wakamwendea Yesu, wakamwambia, Ni wapi utakapo tukuandalie uile Pasaka? Akasema, Enendeni mjini kwa mtu fulani, mkamwambie, Mwalimu asema, Majira yangu ni karibu; kwako nitafanya Pasaka pamoja na wanafunzi wangu. Wanafunzi wakafanya kama Yesu alivyowaagiza, wakaiandaa Pasaka. Basi kulipokuwa jioni aliketi chakulani pamoja na wale Thenashara. Nao walipokuwa wakila, alisema, Amin, nawaambia, Mmoja wenu atanisaliti. Wakahuzunika sana, wakaanza kumwuliza mmoja mmoja, Ni mimi, Bwana? Akajibu akasema, Yeye aliyetia mkono wake pamoja nami katika kombe, ndiye atakayenisaliti. Mwana wa Adamu aenda zake, kama alivyoandikiwa; lakini ole wake mtu yule ambaye amsaliti Mwana wa Adamu! Ingekuwa heri kwake mtu yule kama asingalizaliwa. Yuda, yule mwenye kumsaliti, akajibu, akasema, Ni mimi, Rabi? Akamwambia, Wewe umesema. Nao walipokuwa wakila Yesu alitwaa mkate, akabariki, akaumega, akawapa wanafunzi wake, akasema, Twaeni, mle; huu ndio mwili wangu Akakitwaa kikombe, akashukuru, akawapa, akisema, Nyweni nyote katika hiki; kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi. Lakini nawaambieni, Sitakunywa kabisa tangu sasa uzao huu wa mzabibu, hata siku ile nitakapokunywa mpya pamoja nanyi katika ufalme wa Baba yangu. Nao walipokwisha kuimba, wakatoka nje kwenda mlima wa Mizeituni. Ndipo Yesu akawaambia, Ninyi nyote mtachukizwa kwa ajili yangu usiku huu kwa kuwa imeandikwa, Nitampiga mchungaji, na kondoo wa kundi watatawanyika. Lakini baada ya kufufuka kwangu, nitawatangulia kwenda Galilaya. Petro akajibu, akamwambia, Wajapochukizwa wote kwa ajili yako, mimi sitachukizwa kamwe. Yesu akamwambia, Amin, nakuambia wewe, usiku huu kabla ya kuwika jogoo, utanikana mara tatu. Petro akamwambia, Ijaponipasa kufa nawe, sitakukana kamwe. Na wanafunzi wote wakasema vivyo hivyo. Kisha Yesu akaenda pamoja nao mpaka bustani iitwayo Gethsemane, akawaambia wanafunzi wake, Ketini hapa, hata niende kule nikaombe. Akamchukua Petro na wale wana wawili wa Zebedayo, akaanza kuhuzunika na kusononeka. Ndipo akawaambia, Roho yangu ina huzuni nyingi kiasi cha kufa; kaeni hapa, mkeshe pamoja nami. Akaendelea mbele kidogo, akaanguka kifulifuli, akaomba, akisema, Baba yangu, ikiwezekana, kikombe hiki kiniepuke; walakini si kama nitakavyo mimi, bali kama utakavyo wewe. Akawajia wale wanafunzi, akawakuta wamelala, akamwambia Petro, Je! Hamkuweza kukesha pamoja nami hata saa moja? Kesheni, mwombe, msije mkaingia majaribuni; roho i radhi, lakini mwili ni dhaifu. Akaenda tena mara ya pili, akaomba, akisema, Baba yangu, ikiwa haiwezekani kikombe hiki kiniepuke nisipokunywa, mapenzi yako yatimizwe. Akaja tena, akawakuta wamelala; maana macho yao yamekuwa mazito. Akawaacha tena, akaenda, akaomba mara ya tatu, akisema maneno yale yale. Kisha akawajia wanafunzi wake, akawaambia, Laleni sasa, mpumzike tazama, saa imekaribia, na Mwana wa Adamu anatiwa katika mikono ya wenye dhambi. Ondokeni, twende zetuni! Tazama, yule anayenisaliti amekaribia. Basi alipokuwa katika kusema, tazama, Yuda, mmoja wa wale Thenashara akaja, na pamoja naye kundi kubwa wenye panga na marungu, wametoka kwa wakuu wa makuhani na wazee wa watu. Na yule mwenye kumsaliti alikuwa amewapa ishara, akisema, Nitakayembusu, huyo ndiye; mkamateni. Mara akamwendea Yesu, akasema, Salamu, Rabi, akambusu. Yesu akamwambia, Rafiki, fanya ulilolijia. Wakaenda, wakanyosha mikono yao wakamkamata Yesu. Na tazama, mmoja wao waliokuwa pamoja na Yesu akanyosha mkono wake, akaufuta upanga wake, akampiga mtumwa wa Kuhani Mkuu, akamkata sikio. Ndipo Yesu akamwambia, Rudisha upanga wako mahali pake, maana wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga. Ama wadhani ya kuwa mimi siwezi kumsihi Baba yangu, naye ataniletea sasa hivi zaidi ya majeshi kumi na mawili ya malaika? Yatatimizwaje basi maandiko, ya kwamba hivyo ndivyo vilivyopasa kujiri? Saa ile Yesu akawaambia makutano, Je, mmetoka kama kumkamata mnyang'anyi, wenye panga na marungu, ili kunishika? Kila siku naliketi hekaluni nikifundisha, msinikamate. Lakini haya yote yamekuwa, ili maandiko ya manabii yatimizwe. Ndipo wanafunzi wote wakamwacha, wakakimbia. Nao waliomkamata Yesu wakampeleka kwa Kayafa, Kuhani Mkuu, walikokuwa wamekutanika waandishi na wazee. Na Petro akamfuata kwa mbali mpaka behewa ya Kuhani Mkuu, akaingia ndani, akaketi pamoja na watumishi, auone mwisho. Basi wakuu wa makuhani na baraza yote wakatafuta ushuhuda wa uongo juu ya Yesu, wapate kumwua; wasiuone wangawa walitokea mashahidi wa uongo wengi. Hata baadaye wawili wakatokea, wakasema, Huyu alisema, Naweza kulivunja hekalu la Mungu, na kulijenga kwa siku tatu. Kisha Kuhani Mkuu akasimama akamwambia, Hujibu neno? Hawa wanakushuhudia nini? Lakini, Yesu akanyamaza. Kuhani Mkuu akamwambia, Nakuapisha kwa Mungu aliye hai, utuambie kama wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu. Yesu akamwambia, Wewe umesema; lakini nawaambieni, Tangu sasa mtamwona Mwana wa Adamu ameketi mkono wa kuume wa nguvu, akija juu ya mawingu ya mbinguni. Ndipo Kuhani Mkuu akararua mavazi yake, akisema, Amekufuru; mna haja gani tena ya mashahidi? Tazameni, sasa mmesikia hiyo kufuru yake; mwaonaje ninyi? Wakajibu, wakasema, Imempasa kuuawa. Ndipo wakamtemea mate ya uso, wakampiga makonde; wengine wakampiga makofi, wakisema, Ewe Kristo, tufumbulie; ni nani aliyekupiga? Na Petro alikuwa ameketi nje behewani; kijakazi mmoja akamwendea, akasema, Wewe nawe ulikuwapo pamoja na Yesu wa Galilaya. Akakana mbele ya wote, akisema, Sijui usemalo. Naye alipotoka nje hata ukumbini, mwanamke mwingine alimwona, akawaambia watu waliokuwako huko, Huyu alikuwapo pamoja na Yesu Mnazareti. Akakana tena kwa kiapo, Simjui mtu huyu. Punde kidogo, wale waliohudhuria wakamwendea, wakamwambia Petro, Hakika wewe nawe u mmoja wao; kwa sababu hata usemi wako wakutambulisha. Ndipo akaanza kulaani na kuapa akisema, Simjui mtu huyu. Na mara akawika jogoo. Petro akalikumbuka lile neno la Yesu alilolisema, Kabla ya kuwika jogoo, utanikana mara tatu. Akatoka nje, akalia kwa majonzi. Na ilipokuwa asubuhi, wakuu wa makuhani wote na wazee wa watu wakafanya shauri juu ya Yesu, wapate kumwua; wakamfunga, wakamchukua, wakampeleka kwa Pilato aliyekuwa liwali. Kisha Yuda, yule mwenye kumsaliti, alipoona ya kuwa amekwisha kuhukumiwa, alijuta, akawarudishia wakuu wa makuhani na wazee vile vipande thelathini vya fedha, akasema, Nalikosa nilipoisaliti damu isiyo na hatia. Wakasema, Basi, haya yatupasani sisi? Yaangalie haya wewe mwenyewe. Akavitupa vile vipande vya fedha katika hekalu, akaondoka; akaenda, akajinyonga. Wakuu wa makuhani wakavitwaa vile vipande vya fedha, wakasema, Si halali kuviweka katika sanduku ya sadaka, kwa kuwa ni kima cha damu. Wakafanya shauri, wakavitumia kwa kununua konde la mfinyanzi liwe mahali pa kuzika wageni. Kwa hiyo konde lile huitwa konde la damu hata leo. Ndipo likatimia neno lililonenwa na nabii Yeremia, akisema, Wakavitwaa vipande thelathini vya fedha, kima chake aliyetiwa kima, ambaye baadhi ya Waisraeli walimtia kima; wakavitumia kwa kununua konde la mfinyanzi, kama Bwana alivyoniagiza. Naye Yesu akasimama mbele ya liwali; liwali akamwuliza, akasema, Wewe ndiwe mfalme wa Wayahudi? Yesu akamwambia, Wewe wasema. Lakini aliposhitakiwa na wakuu wa makuhani na wazee, hakujibu hata neno. Ndipo Pilato akamwambia, Husikii ni mambo mangapi wanayokushuhudia? Asimjibu hata neno moja, hata liwali akastaajabu sana. Basi wakati wa siku kuu, liwali desturi yake huwafungulia mkutano mfungwa mmoja waliyemtaka. Basi palikuwa na mfungwa mashuhuri siku zile, aitwaye Baraba. Basi walipokutanika, Pilato akawaambia, Mnataka niwafungulie yupi? Yule Baraba, au Yesu aitwaye Kristo? Kwa maana alijua ya kuwa wamemtoa kwa husuda. Na alipokuwa ameketi juu ya kiti cha hukumu, mkewe alimpelekea mjumbe, kumwambia, Usiwe na neno na yule mwenye haki; kwa sababu nimeteswa mengi leo katika ndoto kwa ajili yake. Nao wakuu wa makuhani na wazee wakawashawishi makutano ili wamtake Baraba, na kumwangamiza Yesu. Basi liwali akajibu, akawaambia, Mnataka niwafungulie yupi katika hawa wawili? Wakasema, Baraba. Pilato akawaambia, Basi, nimtendeje Yesu aitwaye Kristo? Wakasema wote, Asulibiwe. Akasema, Kwani? Ni ubaya gani alioutenda? Wakazidi sana kupiga kelele, wakisema, Na asulibiwe. Basi Pilato alipoona ya kuwa hafai lo lote, bali ghasia inazidi tu, akatwaa maji, akanawa mikono yake mbele ya mkutano, akasema, Mimi sina hatia katika damu ya mtu huyu mwenye haki; yaangalieni haya ninyi wenyewe. Watu wote wakajibu wakasema, Damu yake na iwe juu yetu, na juu ya watoto wetu. Ndipo akawafungulia Baraba; na baada ya kumpiga Yesu mijeledi, akamtoa ili asulibiwe. Ndipo askari wa liwali wakamchukua Yesu ndani ya Praitorio, wakamkusanyikia kikosi kizima. Wakamvua nguo, wakamvika vazi jekundu. Wakasokota taji ya miiba, wakaiweka juu ya kichwa chake, na mwanzi katika mkono wake wa kuume; wakapiga magoti mbele yake, wakamdhihaki, wakisema, Salamu, Mfalme wa Wayahudi! Kisha wakamtemea mate, wakautwaa ule mwanzi, wakampiga-piga kichwani. Walipokwisha kumdhihaki, wakalivua lile vazi, wakamvika mavazi yake, wakamchukua kumsulibisha. Hata walipokuwa wakitoka, wakamwona mtu Mkirene, jina lake Simoni; huyu wakamshurutisha auchukue msalaba wake. Na walipofika mahali paitwapo Golgotha, yaani, Fuvu la kichwa, wakampa kunywa divai iliyochanganyika na nyongo; lakini yeye alipoionja hakutaka kunywa. Walipokwisha kumsulibisha, waligawa mavazi yake, wakipiga kura; [ili litimie neno lililonenwa na nabii, Waligawa nguo zangu kati yao, na juu ya vazi langu walipiga kura.] Wakaketi, wakamlinda huko. Wakaweka juu ya kichwa chake mashitaka yake, yaliyoandikwa HUYU NI YESU, MFALME WA WAYAHUDI. Wakati uo huo wanyang'anyi wawili wakasulibiwa pamoja naye, mmoja mkono wake wa kuume, na mmoja mkono wake wa kushoto. Nao waliokuwa wakipita njiani wakamtukana, wakitikisa-tikisa vichwa vyao, wakisema, Ewe mwenye kulivunja hekalu na kulijenga kwa siku tatu, jiokoe nafsi yako; ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, shuka msalabani. Kadhalika na wale wakuu wa makuhani wakamdhihaki pamoja na waandishi na wazee, wakisema, Aliokoa wengine, hawezi kujiokoa mwenyewe. Yeye ni mfalme wa Israeli; na ashuke sasa msalabani, nasi tutamwamini. Amemtegemea Mungu; na amwokoe sasa, kama anamtaka; kwa maana alisema, Mimi ni Mwana wa Mungu. Pia wale wanyang'anyi waliosulibiwa pamoja naye walimshutumu vile vile. Basi tangu saa sita palikuwa na giza juu ya nchi yote hata saa tisa. Na kama saa tisa, Yesu akapaza sauti yake kwa nguvu akisema, Eloi, Eloi, lama sabakthani? Yaani, Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha? Na baadhi yao waliohudhuria, waliposikia, walisema, Huyu anamwita Eliya. Mara mmoja wao akaenda mbio, akatwaa sifongo, akaijaza siki, akaitia juu ya mwanzi, akamnywesha. Wale wengine wakasema, Acha; na tuone kama Eliya anakuja kumwokoa. Naye Yesu akiisha kupaza sauti tena kwa nguvu, akaitoa roho yake. Na tazama, pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu hata chini; nchi ikatetemeka; miamba ikapasuka; makaburi yakafunuka; ikainuka miili mingi ya watakatifu waliolala; nao wakiisha kutoka makaburini mwao, baada ya kufufuka kwake, wakauingia mji mtakatifu, wakawatokea wengi. Basi yule akida, na hao waliokuwa pamoja naye wakimlinda Yesu, walipoliona tetemeko la nchi na mambo yaliyofanyika, wakaogopa sana, wakisema, Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu. Palikuwa na wanawake wengi pale wakitazama kwa mbali, hao ndio waliomfuata Yesu toka Galilaya, na kumtumikia. Miongoni mwao alikuwamo Mariamu Magdalene, na Mariamu mama yao Yakobo na Yusufu, na mama yao wana wa Zebedayo. Hata ilipokuwa jioni akafika mtu tajiri wa Arimathaya, jina lake Yusufu, naye mwenyewe alikuwa mwanafunzi wa Yesu; mtu huyu alimwendea Pilato akauomba mwili wa Yesu. Ndipo Pilato akaamuru apewe. Yusufu akautwaa mwili, akauzonga-zonga katika sanda ya kitani safi, akauweka katika kaburi lake jipya, alilokuwa amelichonga mwambani; akavingirisha jiwe kubwa mbele ya mlango wa kaburi, akaenda zake. Na pale walikuwapo Mariamu Magdalene, na Mariamu yule wa pili, wameketi kulielekea kaburi. Hata siku ya pili, ndiyo iliyo baada ya Maandalio, wakuu wa makuhani, na Mafarisayo wakamkusanyikia Pilato, wakasema, Bwana, tumekumbuka kwamba yule mjanja alisema, alipokuwa akali hai, Baada ya siku tatu nitafufuka. Basi amuru kwamba kaburi lilindwe salama hata siku ya tatu; wasije wanafunzi wake wakamwiba, na kuwaambia watu, Amefufuka katika wafu; na udanganyifu wa mwisho utapita ule wa kwanza. Pilato akawaambia, Mna askari; nendeni mkalilinde salama kadiri mjuavyo. Wakaenda, wakalilinda kaburi salama, kwa kulitia lile jiwe muhuri, pamoja na wale askari walinzi.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUJITAZAMA KIDOGO NA KUMTAZAMA YESU ZAIDI!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kwaresima
Jumamosi, Machi 28, 2026
Juma la 5 la Kwaresima

Ez 37: 21-28; 
Yer 31: 10-13; 
Yn 11: 45-56


KUJITAZAMA KIDOGO NA KUMTAZAMA YESU ZAIDI!

Katika Injili ya leo tunaona jinsi Kayafa kuhani mkuu anavyo fikiri. Maneno yake yanavutia katika hali kwamba ni ya huzuni lakini yanatoa unabii kwa wakati mmoja. Walitamani na wanaanza kupanga yeye na makuhani wengine pamoja na Mafarisayo jinsi ya kumkamata Yesu na kumuua. Lakini kinachotupa kitu ni jinsi ya msukumo wa Kayafa na wengine. 

Yesu alikuwa akipata umaarufu na walikuwa wakiogopa umaarufu wake utachochoea vitu kati ya Warumi. Na walikuwa na wivu kwamba Yesu amewavutia watu wengi sana. Na Kayafa anatoa mantiki iliojificha kwamba inapaswa mtu mmoja afe kwa ajili ya watu kuliko taifa zima liangamie. Kwa maneno mengine alifikiri kwamba kwasababu Yesu anapata umaarufu sana na kwasababu watu wengine walikuwa wakimsikiliza Yesu zaidi kuliko wao makuhani na mafariyo, ni kwamba “ni vizuri kuliondoa tatizo” ili mambo yaweze kuendelea kama yalivyo zoea. 

Hili linafunua ukweli kwamba Mafariyo walikuwa wakijali zaidi nafsi zao na umaarufu wao kuliko ukweli. Kama Mafarisayo na Makuhani walikuwa wanapenda ukweli, wangeona pia utukufu na mamlaka aliokuwa nayo na kumwamini yeye na kumfuata. Lakini hawakuweza kuacha majivuno yao na kukubali ukweli na kumfuata mtu mwingine badala ya nafsi zao. Hawakuweza kuachia mamlaka yao.

Hali hii pia tunaiona katika maisha yetu ya kila siku. Mara nyingi tunataka sisi tuwe kitovu cha kuangaliwa. Na mara nyingi tunavyo muona mtu mwingine akifanya vizuri au akipokea sifa tunapatwa na wivu mbaya. Na wivu wetu unageuka na kuwa chuki. Tuna enda mbali na Yesu pia. Tujaribu kufikiria muda tuliokuwa tukifanya kama Kayafa. Na tunapo ingia katika wiki kuu, tuelekeze macho yetu kwa Yesu kuliko kwa nafsi zetu. Tujikute sisi wenyewe chini ya mslaba wake siku ya Ijumaa kuu kwa mapendo na ujasiri, tukisimama karibu na tukimpenda katika njia zetu zote za maisha.

Sala: Bwana, ninaomba nikufuata wewe katika wiki kuu inayokuja. Ninakuomba niwe na upendo wa kukupenda wewe hata katika kukataliwa kwako na uchungu. Ninaomba unisaidie nitupilie mbali wivu na chuki na kukuona wewe katika mateso ya wengine na katika furaha yao. Yesu, nakuamini wewe. Amina



Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MACHI 28, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 28, 2026
JUMAMOSI JUMA LA 5 LA KWARESIMA

SOMO 1
Eze 37: 21-28

Bwana Mungu asema hivi: Tazama, nitawatwaa wana wa Israeli toka kati ya mataifa walikokwenda, nami nitawakusanya pande zote, na kuwaleta katika nchi yao wenyewe; nami nitawafanya kuwa taifa moja katika nchi hiyo, juu ya milima ya Israeli; na mfalme mmoja atakuwa mfalme wao wote; wala hawatakuwa tena mataifa mawili, wala hawatagawanyikana kuwa falme mbili tena, hata milele. Wala hawatajitia uchafu tena kwa vinyago vyao, wala kwa vitu vyao vichukizavyo, wala kwa makossa yao mojawapo; lakini nitawaokoa, na kuwatoa katika makao yao yote, ambayo wamefanya dhambi ndani yake, nami nitawatakasa; basi watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao. Na mtumishi wangu, Daudi, atakuwa mfalme juu yao, nao wote watakuwa na mchungaji mmoja; nao wataenenda katika hukumu zangu, na kuzishika amri zangu, na kuzitenda. Nao watakaa katika nchi niliyompa Yakobo, mtumishi wangu, walimokaa humo, wao na watoto wao, na watoto wa watoto wao, milele; na Daudi, mtumishi wangu, atakuwa mkuu wao milele; na Daudi, mtumishi wangu, atakuwa mkuu wao milele. Tena agano la milele pamoja nao; nami nitaweka na kati yao milele. Tena maskani yangu itakuwa pamoja nao; nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. Na mataifa watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, mimi niwatakasaye Israeli, patakatifu pangu patakapokuwa katikati yao milele. 

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI
Zab 31:10-13 (K) 10

(K) Bwana anatulinda kama mchungaji alindavyo kundi lake.

Lisikieni neno la Bwana, enyi mataifa,
Litangazeni visiwani mbali;
Mkasema: Aliyemtawanya Israeli atamkusanya,
Na kumlinda kama mchungaji alindavyo kundi lake.
Kwa maana Bwana amemweka huru Yakobo,
Amemkomboa mkononi mwake aliyekuwa hodari kuliko yeye. (K)

Watakuja na kuimba katika mlima Sayuni.
Wataukimbilia wema wa Bwana,
Nafaka, na divai, na mafuta,
Na wachanga wa kondoo na wa ng’ombe. (K)

Ndipo bikira atafurahi katika kucheza,
Na vijana na wazee pamoja;
Maana nitageuza masikitiko yao kuwa furaha,
Nami nitawafariji, na kuwafurahisha waache huzuni zao. (K)


SHANGILIO
Zab. 95:8, 9

Leo msifanye migumu mioyo yenu, lakini msikie sauti yake Bwana.


INJILI
Yn. 11:45-57

Wengi katika Wayahudi waliokuja kwa Maria, na kuyaona yale aliyoyafanya yesu, wakamwamini. Lakini wengine wakaenda zao kwa Mafarisayo wakawaambia aliyoyafanya.

Basi wakuu wa makuhani na Mafarisayo wakakusanya baraza, wakasema, Tunafanya nini? Maana mtu huyu afanya ishara nyingi. Tukimwacha hivi, watu wote watamwamini; na Warumi watakuja, watatuondolea mahali petu na taifa letu. Mtu mmoja miongoni mwao, Kayafa, aliyekuwa Kuhani Mkuu mwaka ule, akawaambia, Ninyi hamjui neno lolote; wala hamfikiri ya kwamba yafaa mtu mmoja afe kwa ajili ya watu, wala lisiangamie taifa zima. Na neno hilo yeye hakulisema kwa nafsi yake; bali kwa kuwa alikuwa Kuhani Mkuu mwaka ule, alitabiri ya kwamba Yesu atakaufa kwa ajili ya taifa hilo, wala si kwa ajili ya taifa hilo tu; lakini pamoja na hayo awakusanye watoto wa Mungu waliotawanyika, ili wawe wamoja. Basi tangu siku ile walifanya shauri la kumwua.

Kwa hiyo Yesu hakutenda tena kwa wazi katikati ya Wayahudi; bali alitoka huko, akaenda mahali karibu na jangwa, mpaka mji uitwao Efraimu; akakaa huko pamoja na wanafunzi wake.

Na Pasaka ya Wayahudi ilikuwa karibu; na wengi wakakwea toka mashambani kwenda Yerusalemu kabla ya Pasaka, ili wajitakase. Basi wao wakamtafuta Yesu, wakasemezana hali wamesimama hekaluni, Mwaonaje? Haji kabisa sikukuu hii? Na wakuu wa makuhani na Mafarisayo walikuwa wametoa amri ya kwamba mtu akimjua alipo, alete habari, ili wapate kumkamata.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

IMANI ILIYO JARIBIWA


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Kwaresima
Ijumaa, Machi 27, 2026
Juma la 5 la Kwaresima

Yer 20: 10-13;
Zab 17: 2-7;
Yn 10: 31-42.


IMANI ILIYO JARIBIWA 

Lirtujia ya leo inampa changamoto kila mfuasi wa Kristo kuangalia uwiano wa maneno yake na matendo yake kama yanaendana. Katika masomo ya leo tunasikia nabii Yeremia akiwa katikati ya matatizo na Yesu akiwa katikati ya Wayahudi wakijianda kutaka kumpiga mawe. Nabii Yeremia aliongea kwa jina la Mungu na kwa niaba ya Mungu na sio kwa ajili yake mwenyewe. Maneno yake hayakupokelewa na wasikilizaji wake. Hili lilileta matatizo kwa Yeremia. Na kwa upande wa Yesu pia, maneno yake hawakuyapokea pia. 

Tukiwa tunakaribia juma kuu, na hasa ijumaa kuu, tunaona kwamba chuki inakuwa sana juu ya Yesu. Kumchukia Yesu na kufikia katika kitendo cha kutaka kumuua kwa mawe ni kitendo cha kutokufikiri. Taratibu taratibu wale waliokuwa wanamchukia Yesu chuki yao ilikuwa hata kufikia kilele cha siku ambayo Yesu anayatoa maisha yake kwa ajili yetu na kwa mapenzi makubwa kukabili kifo. Tukikutana na mabaya na uonevu tunapaswa kuwa kama Yesu alivyofanya. Tunapaswa tuyakabili bila woga. Aliyakabili katika ukweli na hakukubali uongo.

Ukweli wa mambo ni kwamba, kadiri tunavyosogea karibu zaidi na Mungu, ndivyo tunavyo shambuliwa zaidi na kuchukiwa zaidi. Kitu muhimu katika kuelekea utakatifu ni kwamba katikati ya madhulimu, mateso, magumu, na uchungu, tunapaswa kusimamia ukweli. Mara nyingi inashawishi kufikiria kwamba huenda tumefanya kitu kibaya wakati mambo hayaendi. Kitu kimoja ambacho Mungu anataka tutambue katika misalaba yetu, ni kuitakasa Imani yetu na kusimamia neno lake na ukweli. Huu ndio muda ulio muhimu kuliko muda mwingine wowote, ambapo tunatakiwa kusimama imara. Ni rahisi kusema tunamtumainia Mungu wakati maisha yakiwa yanaenda vizuri na inakuwa vigumu kumwamini wakati misalaba yetu inakuwa mizito. Kabili hofu yako na muombe Mungu akubadilishe katikati ya hayo matatizo. Ukifanya hivyo, utagundua kwamba mahangaiko makubwa katika maisha yanabadilika kuwa Baraka kubwa. 

Sala: Bwana, tunapokaribia kumbukumbu ya mateso na kifo chako, nisaidie niunganishe matatizo yangu na yako. Nisaidie kuona katika mahangaiko yangu ya kila siku, uwepo wako na nguvu yako. Nisaidie niweze kuona mpango ulionao kwa changamoto hizo. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MACHI 27, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 27, 2026 
IJUMAA JUMA LA 5 LA KWARESIMA

SOMO 1
Yer. 20:10-13

Nimesikia mashutumu ya watu wengi; hofu ziko pande zote. Rafiki zangu wote wanaonivizia nisite, husema, Mshitaki, nasi tutamshitaki; huenda akahadaika; nasi tutamshinda, tutajilipiza kisasi kwake.

Lakini Bwana yu pamoja nami, mfano wa shujaa mwenye kutisha; kwa hiyo hao wanaonionea watajikwaa, wala hawatashinda; watatahayarika sana. Kwa sababu hawakutenda kwa akili, wataona aibu ya milele, ambayo haitasahauliwa kamwe.

Lakini, Ee Bwana wa majeshi, wewe wawajaribu wenye haki, waona viuno na mioyo, nijalie kuona kisasi chako juu yao; kwa maana nimekufunulia wewe neno langu.

Mwimbieni Bwana; msifuni Bwana; kwa maana ameiponya roho ya mhitaji katika mikono ya watu watendao maovu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 18:1-6 (K) 6

(K) Katika shida yangu nalimwita Bwana, akaisikia sauti yangu.

Wewe, Bwana, nguvu zangu, nakupenda sana;
Bwana ni jabali langu, na boma langu, na mwokozi wangu,
Mungu wangu, mwamba wangu ninayemkimbilia,
Ngao yangu, na pembe ya wokovu wangu, na ngome yangu.
Nitamwita Bwana astahiliye kusifiwa,
Hivyo nitaokoka na adui zangu. (K)

Kamba za mauti zilinizunguka,
Mafuriko ya uovu yakanitia hofu.
Kamba za kuzimu zilinizunguka,
Mitego ya mauti ikanikabili. (K)

Katika shida yangu nalimwita Bwana, 
Na kumlalamikia Mungu wangu.
Akaisikia sauti yangu hekaluni mwake,
Kilio change kikaingia masikioni mwake. (K)


SHANGILIO

Mbegu ni neno la Mungu, mpanzi lakini ni Kristu, yeyote ampataye, ataishi milele. 


INJILI
Yn. 10:31-42

Wayahudi waliokota mawe ili wampige. Yesu akawajibu, Kazi njema nyingi nimewaonyesha zitokazo kwa Baba; kwa ajili ya kazi ipi katika hizo mnanipiga kwa mawe? Wayahudi wakamjibu, Kwa ajili ya kazi njema hatukupigi kwa mawe; bali kwa kukufuru, na kwa sababu wewe uliye mwanadamu wajifanya mwenyewe u Mungu.

Yesu akawajibu, Je! Haikuandikwa katika torati yenu ya kwamba, Mimi nimesema, Ndinyi miungu? Ikiwa aliwaita miungu wale waliojiliwa na neno la Mungu; (na maandiko hayawezi kutanguka); je! Yeye ambaye Baba alimtakasa, akamtuma ulimwenguni, ninyi mnamwambia, Unakufuru; kwa sababu nalisema, Mimi ni Mwana wa Mungu? Kama sizitendi kazi za Baba yangu, msiniamini; lakini nikizitenda, ijapokuwa hamniamini mimi, ziaminini zile kazi; mpate kujua na kufahamu ya kuwa Baba yu ndani yangu, nami ni ndani ya Baba.

Wakatafuta tena kumkamata; lakini akatoka mikononi mwao.

Akaenda zake tena ng’ambo ya Yordani, mpaka mahali pale alipokuwapo Yohane akibatiza hapo kwanza, akakaa huko. Na watu wengi wakamwendea, wakasema, Yohane kweli hakufanya ishara yoyote, lakini yote aliyoyasema Yohane katika habari zake huyu yalikuwa kweli. Nao wengi wakamwamini huko.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo. 


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

AGANO LA UPENDO


“ASALI ITOKAYO MWMABANI”
Tafakari ya Kwaresima
Alhamisi, Machi 26, 2026
Juma la 5 la Kwaresima

Mwa17: 3-9;
Zab 104: 4-9; 
Yn 8: 51-59.


AGANO LA UPENDO!

Lirtujia na Neno la Mungu linatualika sisi kukumbuka Agano la Mungu nasi kwa njia ya Yesu. Somo la kwanza linaonesha ukarimu wa Mungu akifanya Agano na Abram, na kuingia katika historia ya Mwanadamu. Ukuu wa Abramu umejikita katika Imani yake na utii kwa Mungu. Bila hata kujua Abram ana anza safari kwenda nchi asio ifahamu. Kwa kumuita Abram Mungu alibadilisha maisha yake yote. Kwa mara ya kwanza katika historia ya Mwanadamu Mungu anabadilisha jina la mtu. Abram anaitwa Abrahamu. Ikiwa na maana kwamba Mungu anauwezo wa maisha yetu yote ya sasa na ya baadae. Agano la Mungu halifungwi tu kwa Abrahamu na familia yake tu. Kama mto unaotiririka daima limejaa ukarimu. Anacho taka Mungu kutoka kwetu ni kudumisha Agano hili daima. 

Katika somo la Injili, Yesu anawaita watu waheshimu Agano la Mungu. Kama watalishika Agano hili hawataona mauti. Kwani kifo ni matokeo ya dhambi. Kwasababu ya kutotii Mwanadamu alipoteza heri machoni pa Mungu lakini Agano la Mungu kwa njia ya Yesu ni kuirudisha tena ile neema iliyopotea.

Sala: Bwana, ninakuomba Moyo wako uweze kuchuja makosa yangu yote na kuruhusu mbegu ya ukweli kumea ndani ya akili na moyo wangu. Mungu wa Agano, tusaidie pia sisi tuweze kuwa waaminifu kwa maagano yetu nawe. Yesu, nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MACHI 26, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 26, 2026
ALHAMISI JUMA LA 5 LA KWARESIMA

SOMO 1
Mwa. 17:3-9

Abramu akaanguka kifudifudi. Mungu akamwambia, akasema, Mimi, agano langu nimefanya nawe, nawe utakuwa baba wa mataifa mengi, wala jina lako hutaitwa tena Abramu, lakini jina lako litakuwa Ibrahimu, kwani nimekuweka uwe baba wa mataifa mengi. Nitakufanya uwe na uzao mwingi sana, nami nitakufanya kuwa mataifa, na wafalme watatoka kwako. Agano langu nitalifanya imara katia ya mimi na wewe, na uzao wako baada yako, na vizazi vyao, kuwa agano la milele, kwamba nitakuwa Mungu kwako na kwa uzao wako baada yako, na vizazi vyao, kuwa agano la milele, kwamba nitakuwa Mungu kwako na kwa uzao wako baada yako, nami nitakupa wewe na uzao wako baada yako nchi hii unayoikaa ugeni, nchi yote ya Kanaani, kuwa milki ya milele; nami nitakuwa Mungu wao.

Mungu akamwambia Ibrahimu, Nawe ulishike agano langu, wewe na uzaqo wako kwa vizazi vyao baada yako.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 150: 4-9 (K) 8

(K) Analikumbuka agano lake milele.

Mtakeni Bwana na nguvu zake,
Utafuteni uso wake siku zote.
Zikumbukeni ajabu zake alizozifanya,
Miujiza yake na hukumu za kinywa chake. (K)

Enyi wazao wa Ibrahimu, mtumishi wake;
Enyi wana wa Yakobo, wateule wake.
Yeye, Bwana, ndiye Mungu wetu;
Duniani mwote mna hukumu zake. (K)

Analikumbuka agano lake milele;
Neno lile aliloviamuru vizazi elfu.
Agano alilofanya na Ibrahimu,
Na uapo wake kwa Isaka. (K)


SHANGILIO
2 Kor. 6:2

Tazama, wakati uliokubalika ndio sasa, tazama, siku ya wokovu ndiyo sasa.


INJILI
Yn. 8:51-59

Yesu aliwaambia Wayahudi: Amin, amin, nawaambia, Mtu akilishika neno langu, hataona mauti milele. Basi Wayahudi wakamwambia, Sasa tumeng’amua ya kuwa una pepo. Ibrahimu na manabii wamekufa; nawe wasema, Mtu akilishika neno langu, hataonja mauti milele. Wewe u mkuu kuliko baba yetu Ibrahimu, ambaye amekufa? Nao manabii wamekufa. Wajifanya u nani?

Yesu akajibu, nikijutukuza mwenyewe, utukufu wangu si kitu; anitukuzaye ni Baba yangu, ambaye ninyi mwanena kuwa ni Mungu wenu. Wala ninyi hamkumjua; lakini mimi namjua. Nikisema ya kwamba simjui, nitakuwa mwongo kama ninyi; lakini namjua, na neno lake nalishika. Ibrahimu, baba yenu, alishangilia kwa vile atakavyoiona siku yangu; naye akaiona, akafurahi.

Basi Wayahudi wakamwambia, Wewe hujapata bado miaka hamsini, nawe umemwona Ibrahimu? Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambia, Yeye Ibrahimu asijakuwako, mimi niko.

Basi wakaokota mawe ili wamtupie; lakini Yesu akajificha, akatoka hekaluni.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.