Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

KUKUTANA NA YESU MFUFUKA KATIKA MAISHA YETU!




“KUFUFUKA NA KRISTO”
Tafakari ya Pasaka
Jumapili, Aprili 19, 2026 
Juma la 3 la Pasaka

Mdo 2: 14, 22-33;
Zab 15: 1-2, 5, 7-11;
1 Pet 1: 17-21;
Lk 24: 13-35.


KUKUTANA NA YESU MFUFUKA KATIKA MAISHA YETU!

Katika Asia ndogo, mwaka 80-90 AD, karibia mashuhuda wote wa Yesu mfufuka walikuwa wamesha toweka. Wakristo (wa kizazi cha tatu) wanajiuliza wenyewe: je, inawezekana sisi kukutana na Bwana? Inawezekanaje, kutoa ushuhuda kwamba yupo hai wakati sisi hatukumuona kwa macho, hatukumshika kwa mikono yetu, na wala hatukukaa mezani pamoja naye? Je sisi tunaongozwa tu kuamini kile walicho amini na kutuambia sisi? Wakristo wana tamani kumuona Yesu.

Injili ya Luka kuhusu habari ya Emaus huenda ilikuwa ndio uvuvio wa majibu na matarajio ya Wakristo hawa. Mmoja wa wawafuasi aliitwa Cleopa (mtu ambaye alijulikana sana wakati wa Kanisa la mwanzo, kwasababu alikuwa ndugu wa Yosefu, Yosefu “Baba” mlishi wa Yesu) na mwingine hajatajwa jina. Luka anaweza kuwa amefanya hivyo, kumwalika msomaji kuwa mfuasi wa pili. Mwaliko ni wito wa kutembea na Cleopa katika njia ya kumtambua Yesu mfufuka, ili kukusanyika pale ambapo wawili wamekusanyika kwa jina lake. 

Hawa wafuasi wawili wana huzuni kwasababu wameona maanguko ya mtarajio yao. Walimtazamia Masiha wa utukufu, mkuu na mfalme lakini wamejikuta wakipoteza. Marabi walifundisha kwamba, Masiha ataishi na kuongoza kwa muda wa miaka elfu moja, na tazama sasa Yesu amekufa. Walikata tamaa na kujikuta wakiona ukweli kwamba ulimwengu uliotangazwa na Yesu haukutimia. Bila Imani ya ufufuko, walioshindwa wameshindwa, maisha mwisho wake kifo, na maisha hayana maana. 

Hawa wafuasi wawili wa Emausi hawakuwa na shaka kwamba mawazo yao kuhusu Masiha yalikuwa sio sahihi. Walikuwa wamefungwa katika tamaduni na mapokeo. Walikuwa wamejifungia na kushindwa kufahamu mapya ya Mungu. Yesu hamwachi mtu ambaye anaamua kuchagua mwenyewe kwenda katika njia ya huzuni. Yeye huwa anakuwa pembeni na kuwa msindikizaji. Kutokea kwa Yesu kwa wanafunzi wake inashangaza sana. Yesu “anawafafanulia yote yaliosemwa kuhusu yeye katika Maandiko Matakatifu”. Kwa njia hiyo hawa wafuasi walitambua kwamba huyu mtu ana uelewa na hekima ya hali ya juu, na hivyo walimwalika akae pamoja nao. Yesu alikaa nao na kula nao chakula mezani nyumbani kwao. Walivyokuwa mezani “alichukua mkate, na kuubariki na kuumega na kuwapa vipande”. Macho yao yalifunguliwa na kumtambua Yesu mfufuka. Wale wafuasi baada ya kumtambua Yesu, walikimbia na kwenda kuwapasha habari na kutangaza kwamba “Bwana amefufuka kweli kweli”.

Habari ya wafuasi wa Emausi inarudiwa kila siku katika Liturjia ya Ekaristi (Misa Takatifu). Inaanza kwa kuingia kwa padre, alafu Liturjia ya neno la Mungu na homilia, na mwishowe, “kuumega mkate”. Ni katika wakati wa Ekaristi takatifu macho yetu yanafumbuliwa tunatambua kwamba Yesu mfufuka yupo kati yetu. Bila neno hatuwezi kuja kumtambua Bwana, hatuwezi kumtambua Yesu katika Ekaristi Takatifu. Wakati misa inaisha tunamaliza na wimbo wa mwisho na hatimaye tunaondoka na furaha, kwenda kushirikisha furaha ya Yesu mfufuka. 

Misa takatifu ni safari yetu ya Emmaus. Tunapaswa kujikita wenyewe katika kumuona Yesu, na kumtambua na kumwabudu. Tunapaswa kutambua uwepo wa Yesu mfufuka kati yetu. Yupo nasi hapa sasa, anatupenda sisi, anaongea na sisi, na anatuita tumpende yeye. Mtafute na msikilize sauti yake. Tutashangaa ni kwa jinsi ghani Bwana mfufuka atakavyo tufanya tutembee naye katika Maandiko Matakatifu, na kujifunua mwenyewe na kuleta furaha katika huzuni yetu na katika mioyo yetu iliokata tamaa. 

Sala: Bwana, ninakushukuru kwa kunipenda mimi sana kiasi kwamba upo na mimi daima. Nipe macho ya Imani niweze kukutana nawe katika Maandiko Matakatifu na kukuona wewe ukiwa ndani ya Ekaristi Takatifu. Ninaomba niweze kutambua uwepo wako katika mambo ya kawaida yanayo tokea katika maisha yangu. Ninakupenda Bwana wangu. Yesu, nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, APRILI 19, 2026



MASOMO YA MISA, APRILI 19, 2026
DOMINIKA YA 3 YA PASAKA

SOMO 1
Mdo. 2:14, 22 – 28

Petro akasimama pamoja na wale kumi na mmoja, akapaza sauti yake, akawaambia, Enyi watu wa Uyahudi, na ninyi nyote mkaao Yerusalemu, lijueni jambo hili, mkasikilize maneno yangu.

Yesu wa Nazareti, mtu aliyedhihirishwa kwenu na Mungu kwa miujiza na ajabu na ishara, ambazo Mungu alizifanya kwa mkono wake kati yenu, kama ninyi wenyewe mnavyojua; mtu huyu alipotolewa kwa shauri la Mungu lililokusudiwa, na kwa kujua kwake tangu zamani, ninyi mkasulibisha kwa mikono ya watu wabaya, mkamwua; ambaye Mungu alimfufua, akaufungua uchungu wa mauti, kwa sababu haikuwezekana ashikwe nao. Maana Daudi ataja habari zake.

Nalimwona Bwana mbele yangu sikuzote, Kwa kuwa yuko upande wa mkono wangu wa kuume, nisitikisike.

Kwa hiyo moyo wangu ukapendezewa, ulimi wangu ukafurahi; Tena mwili wangu nao utakaa katika matumaini. Kwa maana hutaiacha roho yangu katika kuzimu; Wala hutamtoa Mtakatifu wako aone uharibifu. Umenijulisha njia za uzima; Utanijaza furaha kwa uso wako.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 16:1 – 2, 5, 7 – 11 (K) 11

(K) Utanijulisha njia ya uzima.

Mungu unihifadhi mimi,
Kwa maana nakukimbilia Wewe.
Nimemwambia Bwana, Ndiwe Bwana wangu;
Bwana ndiye fungu la posho langu, na la kikombe changu;
Wewe unaishika kura yangu. (K)

Nitamhimidi Bwana aliyenipa shauri,
Naam, mtima wangu umenifundisha usiku.
Nimemweka Bwana mbele yangu daima,
Kwa kuwa yako kuumeni kwangu, sitaondoshwa. (K)

Kwa hiyo moyo wangu unafurahi,
Nao utukufu wangu unashangilia,
Naam, mwili wangu nao utakaa kwa kutumaini.
Maana hutaiachaia kuzimu nafsi yangu.
Wala hutamtoa mtakatifu wako aone uharibifu. (K)

Utanijulisha njia ya uzima;
Mbele za uso wako ziko furaha tele;
Na katika mkono wako wa kuume mna mema ya milele. (K)



SOMO 2
1Pet. 1:17 – 21

Ikiwa mnamwita Baba, yeye ahukumuye kila mtu pasipo upendeleo, kwa kadiri ya kazi yake enendeni kwa hofu katika wakati wenu wa kukaa hapa kama wageni. Nanyi mfahamu kwamba mlikombolewa kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa damu ya thamani, kama ya mwanakondoo asiye na ila, asiye na waa, ya Kristo. Naye amejulikana kweli tangu zamani, kabla haijawekwa misingi ya dunia; lakini alifunuliwa mwisho wa zamani kwa ajili yenu; ambao kwa yeye mmekuwa wenye kumwamini Mungu, aliyemfufua katika wafu akampa utukufu; hata Imani yenu na tumaini lenu liwe kwa Mungu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



SHANGILIO
Lk. 24:32

Aleluya, aleluya,
Bwana Yesu, utufunulie maandiko; uwashe mioyo yetu unaposema nasi. Aleluya.



INJILI
Lk. 24:13 – 35

Siku ile watu wawili miongoni mwa wafuasi wa Yesu walikuwa wakienda kijiji kimoja, jina lake Emau, kilichokuwa mbali na Yerusalemu kama mwendo wa saa mbili. nao walikuwa wakizungumza wao kwa wao habari za mambo hayo yote yaliyotukia. Ikawa katika kuzungumza na kuulizana kwao, Yesu mwenyewe alikaribia, akaandamana nao. Macho yao yakafumbwa wasimtambue. Akawaambia, Ni maneno gani haya mnayosemezana hivi mnapotembea? Wakasimama wamekunja nyuso zao.

Akajibu mmoja wao, jina lake Kleopa, akamwambia, Je! Wewe peke yako u mgeni katika Yerusalemu, hata huyajui yaliyotukia humo siku hizi? Akawauliza, Mambo gani? Wakamwambia, Mambo ya Yesu wa Nazareti, aliyekuwa mtu nabii, mwenye uwezo katika kutenda na kunena mbele za Mungu na watu wote; tena jinsi wakuu wa makuhani na wakubwa wetu walivyomtia katika hukumu ya kufa, wakamsulibisha. Nasi tulikuwa tukitumaini ya kuwa yeye ndiye atakayewakomboa Israeli. Zaidi ya hayo yote, leo ni siku ya tatu tangu yalipotendeka mambo hayo; tena, wanawake kadha wa kadha wa kwetu walitushitusha, waliokwenda kaburini asubuhi na mapema, wasiuone mwili wake; wakaja wakasema ya kwamba wametokewa na malaika waliosema kwamba yu hai. Na wengine waliokuwa pamoja nasi walikwenda kaburini wakaona vivyo hivyo kama wale wanawake walivyosema, ila yeye hawakumwona.

Akawaambia, Enyi msiofahamu, wenye mioyo mizito ya kuamini yote waliyoyasema manabii! Je! Haikumpasa Kristo kupata mateso haya na kuingia katika utukufu wake? Akaanza kutoka Musa na manabii wote, akawaeleza katika maandiko yote mambo yaliyomhusu yeye mwenyewe.

Wakakikaribia kile kijiji walichokuwa wakienda, naye alifanya kama anataka kuendelea mbele. Wakamshawishi wakisema, Kaa pamoja nasi, kwa kuwa kumekuchwa, na mchana unakwisha. Akaingia ndani kukaa nao. Ikawa alipokuwa ameketi nao chakulani, alitwaa mkate, akaubariki, akaumega, akawapa. Yakafumbuliwa macho yao, wakamtambua; kisha akatoweka mbele yao. Wakaambiana, Je! Mioyo yetu haikuwaka ndani yetu hapo alipokuwa akisema nasi njiani, na kutufunulia maandiko?

Wakaondoka saa ile ile, wakarejea Yerusalemu, wakawakuta wale kumi na mmoja wamekutanika, wao na wale waliokuwa pamoja nao, wakisema, Bwana amefufuka kweli kweli, naye amemtokea Simoni, nao waliwapa habari ya mambo yale ya njiani, na jinsi alivyotambulikana nao katika kuumega mkate.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUTULIZA DHORUBA ZETU!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Pasaka
Jumamosi, Aprili 18, 2026 
Juma la 2 la Pasaka


Mdo 6:1-7
Zab 33:1-2,4-5,18-19,22
Yn 6:16-21


KUTULIZA DHORUBA ZETU!

Katika Injili ya leo Yesu anatembea juu ya maji na anawaambia mitume wake “Jipeni moyo ni mimi. Msiogope”. Injili ya leo inatutia nguvu na kutuambia tusiogope tunapo kutana na dhoruba na mawimbi ya maisha. Hatupaswi kuogopa tupo na Yesu. 

Kuwa katikati ya bahari wakati wa giza inaogopesha sana. Kila upande unaoneakana kuwa sawa na huwezi kuona nchi kavu. Tunajisikia kama vile hatujazungukwa na kitu. Mitume wametoka, na wapo baharini wakati wa giza. Watakuwa wamejisikia kama vile wamepotea katikati na hamna kitu. Lakini katikati ya hali hii, Yesu anawajia akiwa anatembea juu ya maji. Na kuwaambia “jipeni moyo ni mimi. Msiogope”. 

Tunaona katika maisha haya ya mitume mfanano wa maisha ya kila siku ya wengi wetu. Wengi twaweza kujisikia kwamba hatuja zungukwa na mtu na hatuna msaidizi, tupo wenyewe na tunapotea. Injili inatufunulia kwamba Yesu anakuja kwetu haijalishi tupo sehemu ghani au tumejikuta katika hali ghani. Yeye hatusubiri sisi tuende kumtafuta, bali anakuja na kuingia katika maisha yetu, alimradi tunamtambua na kumkaribisha. 

Pengine maisha yetu yamejazwa na kazi nyingi, lakini tunajisikia wa pweke. Pengine maisha yetu ni yale ambayo hatuna watu wengi wanaotupenda na tunajikuta tupo wenyewe na kutengwa. Au pengine tunajifanya kuvaa sura ya kuonesha kwamba nina kila kitu lakini ndani mwangu nina hangaika. Katika hali yeyote ile ambayo unaweza kujikuta Yesu anataka kuja kwetu na kutufariji. Msikilize akisema “jipe moyo ni mimi. Usiogope”. Hali katika maisha inaweza kuwa inatisha na kutupa mashaka na woga. Lakini tutakapo ruhusu kumwelekea Yesu, hofu inapotea. Tutambua ndani mwetu kwamba Yesu yupo na mambo yataenda vizuri kwasababu yeye anaongoza kila kitu. Mwache aingie katika mashua ya moyo wako na umwache aongoze. Anakuja kwako na anasubiri jibu lako. 

Sala: Bwana, ni mara nyingi nimeshindwa kushuhudia uwepo wako wa Kimungu katika maisha yangu. Ni mara nyingi nimeshindwa kukuona ukija katika maisha yangu. Nisaidie niweze kutambua kuwa kila mara upo. Niweke huru kutoka katika hali mbali mbali za maisha, na nipe ujasiri wa kukukaribisha wewe katika maisha yangu. Yesu nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, APRILI 18, 2026



MASOMO YA MISA, APRILI 18, 2026
JUMA LA PILI LA PASAKA, JUMAMOSI

SOMO 1
Mdo 6:1-7

Hata siku zile wanafunzi walipokuwa wakiongezeka hesabu yao, palikuwa na manung'uniko ya Wayahudi wa Kiyunani juu ya Waebrania kwa sababu wajane wao walisahauliwa katika huduma ya kila siku. Wale Thenashara wakawaita jamii ya wanafunzi, wakasema, Haipendezi sisi kuliacha neno la Mungu na kuhudumu mezani. Basi ndugu, chagueni watu saba miongoni mwenu, walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho, na hekima, ili tuwaweke juu ya jambo hili; na sisi tutadumu katika kuomba na kulihudumia lile Neno. Neno hili likapendeza machoni pa mkutano wote; wakamchagua Stefano, mtu aliyejaa imani na Roho Mtakatifu, na Filipo, na Prokoro, na Nikanori, na Timoni, na Parmena, na Nikolao mwongofu wa Antiokia; ambao wakawaweka mbele ya mitume, na walipokwisha kuomba wakaweka mikono yao juu yao. Neno la Mungu likaenea; na hesabu ya wanafunzi ikazidi sana katika Yerusalemu; jamii kubwa ya makuhani wakaitii ile Imani.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab 33:1-2, 4-5, 18-19

(K)Ee Bwana, fadhili zako zikae nasi, Kama vile tulivyokungoja Wewe.

Mpigieni Bwana vigelegele, enyi wenye haki, 
Kusifu kunawapasa wanyofu wa moyo. 
Mshukuruni Bwana kwa kinubi, 
Kwa kinanda cha nyuzi kumi mwimbieni sifa. (K)

Kwa kuwa neno la Bwana lina adili, 
Na kazi yake yote huitenda kwa uaminifu. 
Huzipenda haki na hukumu, 
Nchi imejaa fadhili za Bwana. (K)

Tazama, jicho la Bwana li kwao wamchao, 
Wazingojeao fadhili zake. 
Yeye huwaponya nafsi zao na mauti, 
Na kuwahuisha wakati wa njaa. (K) 



SHANGILIO
Yn. 10:27

Aleluya, aleluya,
Kondoo wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua, nao wanifuata.
Aleluya.



INJILI
Yn 6:16-21

Hata ilipokuwa jioni wanafunzi wake wakatelemka baharini wakapanda chomboni, wakaanza kuivuka bahari kwenda Kapernaumu. Nako kumekwisha kuwa giza, wala Yesu hajawafikia. Na bahari ikaanza kuchafuka kwa kuvuma upepo mkuu. Basi wakavuta makasia kadiri ya maili tatu nne, wakamwona Yesu anakwenda juu ya bahari na kukikaribia chombo; wakaogopa. Naye akawaambia, Ni mimi, msiogope. Basi wakataka kumpokea chomboni; na mara hiyo chombo kikaifikilia nchi waliyokuwa wakiiendea.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo. 


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUFAULU KATIKA JARIBIO LA IMANI!


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Pasaka
Ijumaa, Aprili 17, 2026
Juma la 2 la Pasaka

Mdo 5:34-42
Zab 27: 1,4,13-14
Yn 6:1-15


KUFAULU KATIKA JARIBIO LA IMANI!

Mungu daima anatambua anachopenda kufanya. Daima yeye ana mpango mkamilifu wa maisha yetu. Leo katika Injili, Yesu anafanya muujiza wa kuwalisha watu kwa mkate na samaki. Yesu alitambua kwamba ataongeza mkate na samaki ili kuwalisha watu zaidi ya elfu tano. Lakini kabla ya kufanya hili, anamjaribu Philipo. Hivyo hivyo Yesu anatujaribu wakati mwingine. Je, hafanyi hivyo? 

Majaribio haya sio kwamba Yesu anapenda kutuuliza tu au kufanya mchezo Fulani na sisi. Bali, anatupa nafasi ya kudhihirisha imani yetu kwake. Jaribio lililopo kwenye Injili lilikuwa ni kumfanya Philipo atumie Imani zaidi kuliko kufikiri kwa kawaida pekee. Philipo aliitwa ili kudhihirisha imani kwamba Mwana wa Mungu yupo pamoja nao pale. Lakini alishindwa jaribio. Alinyoosha mkono kwa ile hali ya kutokuwezekana. Lakini katika hali nyingine ni kama Andrea alikuja kuokoa. Anasema kuna kijana hapa ana mkate na visamaki vichache. Lakini yeye pia alikuwa na Imani kidogo, aliongeza kusema “lakini vya faa nini kwa umati huu mkubwa namna hii?”. 

Chembe hii dogo ya imani ya Andrea, ilitosha kwa Yesu kuamuru watu waketi makundi makundi na hivyo kufanya ule muujiza. Inaonekana kwamba Andrea alikuwa na ufahamu kidogo kwamba ilikuwa muhimu kutaja visamaki hivi na mkate. Yesu anavichukua kutoka katika mikono ya Andrea na kuwajali watu. 

Mara nyingi tunajikuta katika hali ngumu na hatujui tufanye nini. Tunapaswa kujitahidi kuwa na imani kidogo ili Yesu aweze kuwa na kitu cha kutenda katika maisha yetu. Tunaweza tusiwe na ufahamu wa nini anaenda kufanya, lakini ni lazima kuwa na ufahamu hata kidogo kwamba Mungu ndiye anaye tuongoza sisi. Kama tutaweza hata kukuza Imani hii kidogo sisi pia tutashinda majaribio. 

Sala: Bwana, nisaidie niweze kuwa na Imani kamili ya mpango wako ambao unapenda kuufanya katika maisha yangu. Nisaidie niweze kufahamu kwamba wewe unaongoza na kuyalinda maisha yangu hata pale ninapo ona maisha yanayumba. Katika hali hizo, ninaomba Imani ninayo onesha iwe zawadi kwako ili uweze kuitumia kwa utukufu wako. Yesu, nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, APRILI 17, 2026


MASOMO YA MISA, APRILI 17, 2026
JUMA LA PILI LA PASAKA, IJUMAA

SOMO 1
Mdo 5:34-42

Lakini mtu mmoja, Farisayo, jina lake Gamalieli, mwalimu wa torati, mwenye kuheshimiwa na watu wote, akasimama katika baraza, akaamuru mitume wawekwe nje kitambo kidogo, akawaambia, Enyi waume wa Israeli, jihadharini jinsi mtakavyowatenda watu hawa. Kwa sababu kabla ya siku hizi aliondoka Theuda, akijidai ya kuwa yeye ni mtu mkuu, watu wapata mia nne wakashikamana naye; naye aliuawa na wote waliomsadiki wakatawanyika wakawa si kitu. Baada ya mtu huyo aliondoka Yuda Mgalilaya, siku zile za kuandikiwa orodha, akawavuta watu kadha wa kadha nyuma yake, naye pia akapotea na wote waliomsadiki wakatawanyika. Basi sasa nawaambia, Jiepusheni na watu hawa, waacheni; kwa kuwa shauri hili au kazi hii ikiwa imetoka kwa binadamu, itavunjwa, lakini ikiwa imetoka kwa Mungu hamwezi kuivunja; msije mkaonekana kuwa mnapigana na Mungu. Wakakubali maneno yake; nao walipowaita mitume, wakawapiga, wakawaamuru wasinene kwa jina lake Yesu; kisha wakawaacha waende zao. Nao wakatoka katika ile baraza, wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya Jina hilo. Na kila siku, ndani ya hekalu na nyumbani mwao, hawakuacha kufundisha na kuhubiri habari njema za Yesu kwamba ni Kristo.

Neno la Bwana… Tumshukuru Bwana.


WIMBO WA KATIKATI
Zab 27:1, 4, 13-14

(K)Neno moja nimelitaka kwa Bwana,
Nikae nyumbani mwa Bwana.

Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, 
Nimwogope nani? 
Bwana ni ngome ya uzima wangu, 
Nimhofu nani? (K)

Neno Moja nimelitaka kwa Bwana, 
Nalo ndilo nitakalolitafuta,
Nikae nyumbani mwa Bwana 
Siku zote za maisha yangu, 
Niutazame uzuri wa Bwana, 
Na kutafakari hekaluni mwake. (K)

Naamini ya kuwa nitauona wema wa Bwana 
Katika nchi ya walio hai. 
Umngoje Bwana, uwe hodari, 
Upige moyo konde, naam, umngoje Bwana. (K)



SHANGILIO
Kol. 3:1

Aleluya, aleluya.
Mkiwa mmefufuliwa na Kristo, yatafuteni yaliyo juu, Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu.
Aleluya.


INJILI
Yn 6:1-15

Baada ya hayo Yesu alikwenda zake ng'ambo ya Bahari ya Galilaya, nayo ndiyo ya Tiberia. Na mkutano mkuu wakamfuata, kwa sababu waliziona ishara alizowafanyia wagonjwa. Naye Yesu akakwea mlimani, akaketi huko pamoja na wanafunzi wake. Na Pasaka, sikukuu ya Wayahudi, ilikuwa karibu. Basi Yesu alipoinua macho yake akaona mkutano mkuu wanakuja kwake, alimwambia Filipo, Tununue wapi mikate, ili hawa wapate kula? Na hilo alilinena ili kumjaribu; kwa maana alijua mwenyewe atakalotenda. Filipo akamjibu, Mikate ya dinari mia mbili haiwatoshi, kila mmoja apate kidogo tu. Wanafunzi wake mmojawapo, Andrea, nduguye Simoni Petro, akamwambia, Yupo hapa mtoto, yuna mikate mitano ya shayiri na samaki wawili, lakini hivi ni nini kwa watu wengi kama hawa? Yesu akasema, Waketisheni watu. Na mahali pale palikuwa na majani tele. Basi watu waume wakaketi, wapata elfu tano jumla yao. Basi Yesu akaitwaa ile mikate, akashukuru, akawagawia walioketi; na kadhalika katika wale samaki kwa kadiri walivyotaka. Nao waliposhiba, aliwaambia wanafunzi wake, Kusanyeni vipande vilivyobaki, kisipotee cho chote. Basi wakavikusanya, wakajaza vikapu kumi na viwili, vipande vya mikate mitano ya shayiri vilivyowabakia wale waliokula. Basi watu wale, walipoiona ishara aliyoifanya, walisema, Hakika huyu ni nabii yule ajaye ulimwenguni. Kisha Yesu, hali akitambua ya kuwa walitaka kuja kumshika ili wamfanye mfalme, akajitenga, akaenda tena mlimani yeye peke yake. 

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo
 

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUJAA NEEMAA: NI KUISHI KATIKA KILE MUNGU ALICHOKUPA!



“KUFUFUKA NA KRISTO”
Tafakari ya Pasaka
Alhamisi, Aprili 16, 2026
Juma la 2 la Pasaka

Mdo 5:27-33
Zab 33: 2, 9, 17-20
Yn 3:31-36


KUJAA NEEMAA: NI KUISHI KATIKA KILE MUNGU ALICHOKUPA!


Wakati lipo tokea janga linalotokana na asili, au vita vya kisiasa, na chakula ni vigumu kupata, watu hushikilia na kupangilia kile walicho nacho. Na wasipofanya hivyo wanaona wanaweza kukosa chakula na kufa kwa njaa. Hivi kama Roho Mtakatifu ange tuambiae “nitawasaidia kwa kiwango fulani tu. Na kama ukimaliza neema zako, basi utajitambua mwenyewe” Mmm!

Kwa neema kwetu, Mungu hutenda tofauti kabisa na sisi. Anatupatia na kutumiminia Roho Mtakatifu katika hali yote na kutupatia neema zote tunazo hitaji. Shida ni kwamba hatuzitumii zote, na badala yake tuna acha kuzitumia. Hii si kwamba hatumwamini Mungu ni mkarimu. Bali ni kwasababu tunaogopa kumruhusu Mungu amimine nguvu zake katika maisha yetu.

Tujaribu kufikiria hivi maisha yangu yatafananaje nitakapo mruhusu Mungu afanye chochote anachopenda katika maisha yangu. Hivi, maisha yetu ya kila siku yangekuwaje, mahusiano yetu, maneno yetu na wakati wetu ujao hautakuwa tofauti? Tunatambua kuwa ni haki kumkumbatia Mungu katika kila kitu. Lakini inapofikia sasa ni wakati wa kukitenda, tunakuwa na wasi wasi mwingi. Inaweza kuwa ni wasi wasi wakitu kisicho julikana. Au kunaweza kuwa hatutaki kubadilika. Vyovyote inavyoweza kuwa Mungu anatupa neema zake zisizo pimika kwa kutumiminia Roho wake. Ni juu yako kuchagua kuamua kumsikiliza na kumchagua au unajipimia na kuchagua mambo mengine. Kumchagua Mungu ni jambo kubwa kuliko kitu chohcote unacho weza kufanya katika maisha yako.

Sala: Bwana, ninataka wewe ufanye chochote unachopenda katika maisha yangu. Ninataka niingie kabisa ndani ya neema zako. Nisaidie niweze kusema “ndio” kwako bila kujali chochote kwa utukufu wa kusema “ndio” uliyo niitia. Yesu nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, APRILI 16, 2026

 


MASOMO YA MISA, APRILI 16, 2026

IJUMAA, JUMA LA 2 LA PASAKA


SOMO 1
Mdo 5:27-33

Walipowaleta, wakawaweka katika baraza. Kuhani Mkuu akawauliza, akisema, Je! Hatukuwaamuru ninyi kwa nguvu, msifundishe kwa jina hili? Nanyi, tazameni, mmeijaza Yerusalemu mafundisho yenu, na mnataka kuileta damu ya mtu yule juu yetu. Petro na mitume wakajibu, wakisema, Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu. Mungu wa baba zetu alimfufua Yesu, ambaye ninyi mlimwua mkimtundika katika mti. Mtu huyo Mungu amemtukuza kwa mkono wake wa kuume, awe Mkuu na Mwokozi, awape Waisraeli toba na msamaha wa dhambi. Na sisi tu mashahidi wa mambo haya, pamoja na Roho Mtakatifu ambaye Mungu amewapa wote wamtiio. Wao waliposikia wakachomwa mioyo yao; wakafanya shauri kuwaua.

Neno la Bwana… Tumshukuru Bwana.



WIMBO WA KATIKATI
Zab 34:1, 8, 15-19

(K)Maskini huyu aliita, Bwana akasikia.

Nitamhimidi Bwana kila wakati,
Sifa zake zi kinywani mwangu daima.
Onjeni mwone ya kuwa Bwana yu mwema;
Heri mtu yule anayemtumaini. (K)

Macho ya Bwana huwaelekea wenye haki,
Na masikio yake hukielekea kilio chao.
Uso wa Bwana ni juu ya watenda mabaya,
Aliondoe kumbukumbu lao duniani.
Walilia, naye Bwana akasikia,
Akawaponya na taabu zao zote(K)

Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo,
Na waliopondeka roho huwaokoa.
Mateso ya mwenye haki ni mengi,
Lakini Bwana humponya nayo yote(K)



SHANGILIO
Yn. 20:29

Aleluya, aleluya,
Umesadiki, Toma, kwa kuwa umeniona, wa heri wale wasioona, wakasadiki. Aleluya



INJILI
Yn 3:31-36

Yeye ajaye kutoka juu, huyo yu juu ya yote. Yeye aliye wa dunia, asili yake ni ya dunia, naye anena mambo ya duniani. Yeye ajaye kutoka mbinguni yu juu ya yote. Yale aliyoyaona na kuyasikia ndiyo anayoyashuhudia, wala hakuna anayeukubali ushuhuda wake. Yeye aliyeukubali ushuhuda wake ametia muhuri ya kwamba Mungu ni kweli. Kwa kuwa yeye aliyetumwa na Mungu huyanena maneno ya Mungu; kwa sababu hamtoi Roho kwa kipimo. Baba ampenda Mwana, naye amempa vyote mkononi mwake. Amwaminiye Mwana yuna uzima wa milele; asiyemwamini Mwana hataona uzima, bali ghadhabu ya Mungu inamkalia.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, APRILI 15, 2026



MASOMO YA MISA, APRILI 15, 2026
JUMATANO, JUMA LA 2 LA PASAKA


SOMO 1
Mdo 5:17-26

Akaondoka Kuhani Mkuu na wote waliokuwa pamoja naye, (hao ndio walio wa madhehebu ya Masadukayo), wamejaa wivu,wakawakamata mitume wakawaweka ndani ya gereza; lakini malaika wa Bwana akafungua milango ya gereza usiku, akawatoa, akasema, Enendeni mkasimame hekaluni mkawaambie watu maneno yote ya Uzima huu. Nao waliposikia wakaenda alfajiri hekaluni, wakaanza kufundisha. Akaja Kuhani Mkuu nao waliokuwa pamoja naye, wakawakutanisha watu wa baraza, na wazee wote wa wana wa Israeli, wakatuma watu gerezani ili wawalete. Hata watumishi walipofika hawakuwaona gerezani, wakarudi wakatoa habari, wakisema, Gereza tumeikuta imefungwa salama, nao walinzi wamesimama mbele ya mlango; lakini tulipoufungua hatukukuta mtu ndani. Basi jemadari wa hekalu na wakuu wa makuhani waliposikia haya, wakaingiwa na shaka kwa ajili yao, litakuwaje jambo hilo. Mtu mmoja akaja akawapasha habari ya kwamba, Watu wale mliowaweka gerezani wako ndani ya hekalu, wamesimama wakiwafundisha watu. Ndipo yule jemadari akaenda pamoja na watumishi, wakawaleta, lakini si kwa nguvu, kwa maana waliogopa watu wasije wakawapiga kwa mawe.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab 34:1-8

(K) Maskini huyu aliita, Bwana akasikia.

Nitamhimidi Bwana kila wakati,
Sifa zake zi kinywani mwangu daima.
Katika Bwana nafsi yangu itajisifu,
Wanyenyekevu wasikie wakafurahi. (K)

Mtukuzeni Bwana pamoja nami,
Na tuliadhimishe jina lake pamoja.
Nalimtafuta Bwana akanijibu,
Akaniponya na hofu zangu zote. (K)

Wakamwelekea macho wakatiwa nuru,
Wala nyuso zao hazitaona haya.
Maskini huyu aliita, Bwana akasikia,
Akamwokoa na taabu zake zote. (K)

Malaika wa Bwana hufanya kituo,
Akiwazungukia wamchao na kuwaokoa.
Onjeni mwone ya kuwa Bwana yu mwema;
Heri mtu yule anayemtumaini. (K)



SHANGILIO
Rum. 6:9

Aleluya, aleluya,
Kristo akiisha kufufuka, katika wafu hafi tena. Mauti haimtawali tena.
Aleluya.



INJILI
Yn 3:16-21

Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu. Na hii ndiyo hukumu; ya kuwa nuru imekuja ulimwenguni, na watu wakapenda giza kuliko nuru; kwa maana matendo yao yalikuwa maovu. Maana kila mtu atendaye mabaya huichukia nuru, wala haji kwenye nuru, matendo yake yasije yakakemewa. Bali yeye aitendaye kweli huja kwenye nuru, ili matendo yake yaonekane wazi ya kuwa yametendwa katika Mungu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUVUTWA KWENYE MWANGA!



“KUFUFUKA NA KRISTO”
Tafakari ya Pasaka
Jumatano, Aprili 15, 2026
Juma la 2 la Pasaka

Mdo 5:17-26
Zab 34:2-9
Yn 3:16-21


KUVUTWA KWENYE MWANGA!


Mungu Baba amemtuma Mwanae aje ulimwenguni kuwa mwanga wetu wote. Yeye ni Mwanga ambao unaondoa giza lote. Lakini Injili inasema kwamba “watu wamependa giza zaidi ya mwanga”. Wamechagua dhambi zao zaidi kuliko uhuru wa kutoka kwenye dhambi. Tv au magazeti huvutia watu zaidi wanapotoa habari za udhaifu wa watu, na watu hukimbilia hizi kwasababu ndicho chenye maana kwao. Kwasababu tunavutwa zaidi kupenda kusikia mambo ya giza kuliko ya mwanga.

Ni wazi kwamba sio kwa kila mtu. Walio wengi hawapendezwi na giza la ulimwengu pia na mambo ya kudhalilisha wengine. Lakini ukweli ni kwamba giza lipo mbele na tunapaswa kuwa makini kwasababu ya hali yetu yakuweza kuanguka. Tunapenda kwenda kwenye matope na kudhani tuna furaha.

Pasaka ni kipindi cha kuchunguza tunavutwa na nini zaidi. Je, tunajiruhusu sisi wenyewe kuvutwa kwenye mwanga? Je, tunavutwa na hali mbali mbali ambazo Mungu yupo karibu yetu hapa duniani? Lakini upo mvuto wa kutopenda mpangilio, nakuvutwa kwenye dhambi, mapambano ya ndani ambayo kila mtu yanamkuta. Pasaka ni kipindi cha kuwa makini na haya, kuya chunguza na kuyaona na kuamua kumchagua Yesu, kuanza kujenga maisha yetu ya fadhila kwa kuiga fadhila za maisha ya Yesu.

Kama wafuasi wa Yesu tunaitwa kuelekeza macho yetu kwake pekee. Tunapaswa kupenya giza kwa Imani na kuacha mambo yetu yavutwe kwa Yesu Kristo. Tujikite kwenye Mwanga katika kipindi hiki cha Pasaka. Tuache mwanga huu uongoze maisha yetu.

Sala: Nisaidie mimi niweze kuishi kwenye mwanga. Nisaidie niweze kuelekeza macho yangu kuelekea kwenye utukufu wa ufufuko wako. Ninaomba furaha hiyo iweze kuondoa uharibifu wa mabaya ndani mwangu. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2025 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.