Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

UPENDO UNAOTESEKA



“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Ijumaa, Machi 6, 2026
Juma la 2 la Kwaresima

Mwa 37:3-4, 12-13, 17-28;
Zab 105:16-21;
Mt 21:33-43, 45-46


UPENDO UNAOTESEKA


Katika njia nyingi, Yusufu alikuwa mwaminifu, alikuwa akilindwa katika upendo na kutendewa vyema na Baba yake. Lakini kutokuwa na hatia kulimweka mashakani mara pale alipowaambia ndugu zake kuhusu ndoto yake, na alipowaonyesha kanzu nzuri Baba yake aliyokuwa amempa. Baadaye, ingawa ndugu zake walimpiga na kumuuza utumwani, Yusufu hakuacha kuziishi amri za Mungu. Hata alipokuwa ameshtakiwa kwa uongo na kufungwa gerezani kwamba alijaribu kumwingilia mke wa bwana wake kwa nguvu, yeye aliendelea kuwa imara mbele ya Mungu. Wakati akiwa gerezani, uwezo wake wa kutafsiri ndoto ulimfikia Farao ambaye hatimaye alimweka huru na kumweka awe mkuu baada yake. Kama Yusufu alivyoamini kwamba, Mungu atamletea mema, Mungu alifanya hivyo kwa ajili yake na kuutenga uovu. Nasi pia, tusikubali kamwe kumuacha Mungu tunapokabiliana na magumu siku zote katika maisha yetu. Tumgeukia Mungu Baba yetu na kumwomba atupiganie.

Katika hali zote za kuchukiwa na kukataliwa kwa karne zote, kuna mmoja tu aliyesimama imara kuliko wengine wote. Kukataliwa kwa Mwana wa Mungu. Yesu hakuwa na kitu kingine isipokuwa upendo kamili moyoni mwake. Alipenda ubora wa kila aliyekutana naye. Na alikuwa tayari kumpa upendo yeyote aliyekuwa tayari kuupokea. Ingawaje wengi waliupokea lakini pia wengi waliukataa. Ni vizuri kutambua kuwa kukataliwa kwa Yesu kuliacha maumivu ya ndani na mateso. Ni wazi kwamba mateso ya Msalabani ndio yaliokuwa ya hali ya juu kabisa. Lakini kidonda alichohisi moyoni mwake kwa kukataliwa kilisababisha mateso makubwa. Kuteseka namna hii ilikuwa ni kitendo cha upendo, sio kitendo cha udhaifu. Yesu hakuteseka ndani kwasababu ya majivuno au kwasababu ya ubinafsi wake. Bali moyo wake uliumia kwasababu alipenda kutoka ndani. Na pale upendo huo ulipo kataliwa, ulimjaza yeye huzuni kuu (Mt 5:4).

Jaribu kufikiria kama Yesu ange amua kukata tamaa. Jaribu kufikiria, kama kipindi cha kukamatwa kwake Yesu angeita malaika kama jeshi kutoka mbinguni kumwokoa. Ingekuwaje kama angefanya kitendo hichi cha kufikirika “watu hawa hawastahili!”. Matokeo yake yangekuwa tusinge pokea zawadi ya ukombozi wa milele kwa njia ya mateso, kifo na ufufuko. Mateso yasinge badilika kwenda kwenye upendo.

Yesu alijibu kwa mapendo kamili pale alipolia kwa sauti kuu “Baba, wasamehe, hawajui watendalo.” Kitendo hiki cha upendo katikati ya mateso yake na kukataliwa kwake kilimfanya awe “jiwe kuu la msingi” la Kanisa, na hivyo kuwa jiwe kuu la maisha mapya! Tunaitwa kuiga mapendo haya na kushiriki sio tu kwakusamehe, bali pia kutoa mapendo matakatifu ya huruma. Tukifanya hivyo, sisi pia tunakuwa jiwe la msingi la upendo na neema kwa wote wanao hitaji zaidi.

Sala: Bwana, nisaidie mimi niweze kuwa jiwe la pembeni. Nisaidie mimi sio nisamehe tu kila mara ninapokosewa bali pia nitoe upendo na huruma kwao. Wewe ni Mungu na mfano kamili wa upendo huu. Ninaomba nishiriki katika upendo huu, nikilia kwa sauti kuu pamoja nawe “Baba wasamehe, hawajui watendalo”. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MACHI 6, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 6, 2026
IJUMAA, JUMA LA 2 LA KWARESIMA


SOMO 1
Mwa. 37:3-4, 12-13, 17-28

Israeli akampenda Yusufu kuliko wanawe wote, maana ni mwana wa uzee wake, akamfanyia kanzu ndefu. Ndugu zake wakaona ya kuwa baba yao anampenda kuliko ndugu zake wote, wakamchukia, na hawakuweza kusema naye kwa amani.

Ndugu zake wakaenda kuchunga kondoo za baba yao huko Shekemu. Israeli akamwambia Yusufu, Je! Ndugu zako hawachungi kondoo katika Shekemu? Njoo, nikutume kwao.

Basi Yusufu akawafuata ndugu zake akawakuta huko Dothani. Wakamwona toka mbali, na kabla hajawakaribia, wakafanya shuri juu yake ili wamwue. Wakasemezana wao kwa wao, Tazama, yule bwana wa ndoto anakuja. Haya, twende, tukamwue na kumtupa katika birika mojawapo, nasi tutasema, Mnyama mkali amemla; kisha tutaona zitakuwaje ndoto zake. Reubeni akasikia akamwokoa katika mikono yao, akasema, Tusimwue. Reubeni akawaambia, Msimwage damu; mtupeni katika birika iliyopo nyikani, wala msimguse; ili apate kumwokoa katika mikono yao, akamrudishe kwa baba yake. Ikawa Yusufu alipofika kwa ndugu zake, wakamvua Yusufu kanzu yake, kanzu ile ndefu aliyoivaa, wakamtwaa wakamtupa katika birika; na hiyo birika ilikuwa tupu, hamna maji. Nao wakakaa kitako kula chakula.

Wakainua macho yao, wakaona, msafara wa Waishmaeli wanakuja wakitoka Gileadi na ngamia zao, wakichukua ubani na zeri na manemane, wakisafiri kuvichukua mpaka Misri. Yuda akawaambia ndugu zake, Kwafaa nini kumwua ndugu yetu, na kuificha damu yake? haya, na tumwuze kwa hawa Waishmaeli, wala mikono yenu isimdhuru, maana yeye ni ndugu yetu, na damu yetu. Ndugu zake wakakubali.

Wakapita wafanyabiashara Wamidiani; basi wakamtoa Yusufu, wakampandisha kumtoa katika birika wakamwuza Yusufu kwa Waishmaeli kwa vipande vya fedha ishirini; nao wakamchukua Yusufu mpaka Misri.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 105:16-21 (K) 5

(K) Zikumbukeni ajabu zake Bwana alizozifanya.

Akaiita njaa iijilie nchi,
Akakiharibu chakula chote walichokitegemea.
Alimpeleka mtu mbele yao,
Yusufu utumwani. (K)

Walimwumiza miguu yake kwa pingu,
Akatiwa katika minyororo ya chuma.
Hata wakati wa kuwadia neno lake,
Ahadi ya Bwana ilimjaribu. (K)

Mfalme alituma watu akamfungua,
Mkuu wa watu akamwachia.
Akamweka kuwa bwana wa nyumba yake,
Na mwenye amri juu ya mali zake zote. (K)



SHANGILIO
Yn. 3:16

Jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe wa pekee; Kila mtu amwaminiye huwa na uzima wa milele.



INJILI
Mt. 21:33-43; 45-46

Yesu aliwaambia wakuu wa makuhani na wazee wa watu, Sikilizeni mfano mwingine. Kulikuwa na mtu mwenye nyumba, naye alipanda shamba la mizabibu, akalizungusha ugo, akachimba shimo la shinikizo ndani yake, akajenga mnara, akapangisha wakulima, akasafiri. Wakati wa matunda ulipokuwa karibu, akawatuma watumwa wake kwa wale wakulima, wapokee matunda yake. Wale wakulima wakawakamata watumwa wake, huyu wakampiga, na huyu wakamwua, na huyu wakampiga kwa mawe. Akawatuma tena watumwa wengine wengi kuliko wa kwanza, wakawatenda vile vile.
Mwishowe akamtuma mwanawe kwao, akisema, Watamstahi mwanangu. Lakini wale wakulima walipomwona yule mwana, wakasemezana wao kwa wao, Huyu ni mrithi; haya na tumwue, tuutwae urithi wake. Wakamkamata, wakamtupa nje ya shamba la mizabibu, wakamwua. Basi atakapokuja yule bwana wa shamba la mizabibu, atawatendaje wale wakulima? Wakamwambia, Ataangamiza vibaya wale wabaya; na shamba la mizabibu atawapangisha wakulima wengine, watakaomlipa matunda kwa wakati wake.

Yesu akawaambia, Hamkupata kusoma katika maandiko, Jiwe walilolikataa waashi, hilo limekuwa jiwe kuu la pembeni; neno hili limetoka kwa Bwana, nalo ni ajabu machoni petu? Kwa sababu hiyo nawaambia, Ufalme wa Mungu utaondolewa kwenu, nao watapewa taifa, linguine lenye kuzaa matunda yake.

Wakuu wa makuhani na Mafarisayo, waliposikia mifano yake, walitambua ya kuwa anawanenea wao. Nao walipotafuta kumkamata waliogopa makutano, kwa maana wao walimwona kuwa nabii.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

UPENDO WA MUNGU KWA MASKINI



“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Alhamisi, 5 Machi 2026
Juma la 2 la Kwaresima

Yer 17:5-10;
Zab 1:1-4, 6;
Lk 16:19-31


UPENDO WA MUNGU KWA MASKINI


Katika mfano wa Injili ya Leo tuna mtu mmoja ambaye ametajwa kwa jina, Lazaro. Mfano wa tajiri na Lazaro ni mfano ambao unabaki kuwa maarufu. Ni Lazaro tu anayetambulika katika hali hii? Kwanini Lazaro? Inawezekana ni kwasababu ya nafasi walio nayo maskini machoni pa Mungu. Mfano huu unatuonyesha ni kwa jinsi ghani Mungu anavyo chukizwa na ukosefu wa haki wa kuwafanya wana wake kuwa waombaji na kuwafanya kula makombo yanayotoka katika viti vya jirani zao walio na Mafanikio. Yesu anatuita kutoka moyoni mwake kwa ajili ya maskini. Anatuita tumuone kila mmoja hata wale maskini kabisa na walio katika hali ya mwisho kabisa, na kuwahudumia katika hali ya utu na heshima wanayostahili kama wanadamu wenzetu na watoto wa Mungu.

Kama ilikuwa ni kuchagua ungechagua nini? Kuwa tajiri na kuponda maisha kila siku, ukivaa mavazi ya kitani, kuwa na kila kitu unachopenda ulimwenguni? Au kuwa maskini uliye mwombaji, uliyefunika vidonda vyako, kuishi katika njia ya milango, ukihisi njaa?. Ni swali rahisi sana kujibu katika hali ya kawaida. Maisha ya utajiri na mafanikio yanavutia katika hali ya kwanza kabisa. Lakini swala ni kwamba hayapaswa kuchukuliwa katika hali ya kawaida, tunapaswa kuzama ndani kabisa na kulinganisha watu hawa wawili na matokeo ya maisha yao ya ndani ya roho yao ya milele.

Kwa maskini alivyokufa, “alichukuliwa na malaika katika kifua cha Abraham”. Na kwa tajiri, maandiko yanasema kwamba “alikufa na kuzikwa” na kwenda kwenye “ulimwengu mwingine ambapo alikuwa akiteseka” Sasa ni yupi unayependa kuchagua? Lengo la mfano huu ni rahisi kabisa, tukiwa hapa duniani tunapaswa kutubu, kuacha dhambi, kusikiliza Maandiko Matakatifu, kuamini na kuweka mioyo yetu kuelekea lengo letu la utajiri wa mbinguni.

Tajiri huyu angeweza kumuona Lazaro na kujali utu wake na thamani yake, yeye aliyekuwa amelala katika mlango wake, na kumuona kwa mapendo na huruma. Lakini hakufanya hivyo. Alikuwa amejikita sana juu ya nafsi yake. Dhambi zilimfunika macho akashindwa kumuona Lazaro. Tutafakari leo, kama unaona dhambi yeyote ndani yako inayo fanana na huyu tajiri katika maisha yako, ungama dhambi leo na kuziacha. Na kama umezoea kujikita katika ubinafsi, ukijiingiza katika anaasa za hali ya juu, kumbatia umaskini wa roho, na kujitahidi kuunganika na Mungu tu na baraka nyingi zinazokuja kwetu kwa kukumbatia yote yale aliyo yafunua kwetu.

Sala: Bwana, niweke huru kutoka katika hali isio faa. Nisaidie mimi niweze kubaki katika heshima ya kuwaheshimu watu wote, na kujitoa mwenyewe kuwahudumia. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MACHI 5, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 5, 2026
ALHAMISI JUMA LA 2 LA KWARESIMA

SOMO 1
Yer. 17:5-10

Bwana asema hivi: Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu, amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake, na moyoni mwake amemwacha Bwana. Maana atakuwa kama fukara nyikani, hataona yatakapotokea mema; bali atakaa jangwani palipo na ukame, katika nchi ya chumvi isiyokaliwa na watu.

Amebarikiwa mtu yule anayemtegemea Bwana, ambaye Bwana ni tumaini lake. Maana atakuwa kama mti uliopandwa kando ya maji, uenezao mizizi yake karibu na mto; hautaona hofu wakati wa hari ujapo, bali jani lake litakuwa bichi; wala hautahangaika mwaka wa uchache wa mvua, wala hautaacha kuzaa matunda.

Moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha; nani awezaye kuujua? Mimi, Bwana, nauchunguza moyo, navijaribu viuno, hata kumpa kila mtu kiasi cha njia zake, kiasi cha matunda ya matendo yake.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 1:1-4, 6 (K) 40:4

(K) Heri aliyemfanya Bwana kuwa tumaini lake.

Heri mtu yule asiyekwenda
Katika shauri la wasio haki;
Wala hakusimama katika njia ya wakosaji;
Wala hakuketi barazani pa wenye mizaha.
Bali sheria ya Bwana ndiyo impendezayo,
Na sheria yake huitafakari mchana na usiku. (K)

Naye atakuwa kama mti uliopandwa
Kandokando ya vijito vya maji,
Uzaao matunda yake kwa majira yake,
Wala jani lake halinyauki;
Na kila alitendalo litafanikiwa. (K)

Sivyo walivyo wasio haki;
Hao ni kama makapi yapeperushwayo na upepo.
Kw akuwa Bwana anaijua njia ya wenye haki,
Bali njia ya wasio haki itapotea. (K)



SHANGILIO

Nitaondoka, nitakwenda kwa baba yangu na kumwambia, Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako.



INJILI
Lk. 16:19-31

Yesu aliwaambia Mafarisayo: Palikuwa na mtu mmoja, tajiri, aliyevaa nguo za rangi ya zambarau na kitani safi, na kula sikuzote kwa anasa. Na maskini mmoja, jina lake Lazaro, huwekwa mlangoni pake, ana vidonda vingi, naye alikuwa akitamani kushibishwa kwa makombo yaliyoanguka katika meza ya yule tajiri; hata mbwa wakaja wakamramba vidonda vyake. Ikawa yule maskini alikufa, akachukuliwa na malaika mpaka kifuani kwa Ibrahimu. Yule tajiri naye akafa, akazikwa.

Basi, kule kuzimu aliyainua macho yake, alipokuwa katika mateso, akamwona Ibrahimu kwa mbali, na Lazaro kifuani mwake. Akalia, akasema, Ee baba Ibrahimu, nihurumie, umtume Lazaro achovye ncha ya kidole chake majini, auburudishe ulimi wangu; kwa sababu ninateswa katika moto huu. Ibrahimu akasema, Mwanangu, kumbuka ya kwamba wewe uliyapokea mambo mema yako katika maisha yako, na Lazaro vivyo alipata mabaya; na sasa yeye yupo hapa anafarijiwa, na wewe unaumizwa. Na zaidi ya hayo, kati yetu sisi na ninyi kumewekwa shimo kubwa, ili wale watakao kutoka huku kwenda kwenu wasiweze; wala watu wa kwenu wasivuke kuja kwetu.

Akasema, Basi, baba, nakuomba, umtume nyumbani kwa baba yangu, kwa kuwaninao ndugu watano, ili awashuhudie, wasije wao piawakafika mahali hapa pa mateso. Ibrahimu akasema, Wanao Musa na manabii; na wawasikilize wao. Akasema, La, baba Ibrahimu, lakini kama akiwaendea atokaye kwa wafu, watatubu. Akamwambia wasipowasikia Musa na manabii, hawatashawishwa hata mtu akifufuka katika wafu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

JE, TWAWEZA KUKINYWEA KIKOMBE CHA YESU?



“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Jumatano, Machi 4, 2026
Juma la 2 la Kwaresima

Yer 18:18-20;
Zab 31:5-6,14-16;
Mt 20:17-28.


JE, TWAWEZA KUKINYWEA KIKOMBE CHA YESU?


Ni rahisi kuwa na nia nzuri, lakini hiyo inatosha? Mama mpendwa anamwambia Yesu aagize kwamba wanawe, mmoja aketi upande wake wa kulia na mwingine upande wa kushoto katika Ufalme wake. Lakini, ni vizuri kutambua kwamba hakujua alichokuwa akiomba. Yesu alikuwa akienda Yerusalemu sehemu ambayo atapata utukufu wake kwa njia ya mateso msalabani. Ni katika hali hii Yesu anawauliza Yakobo na Yohane kama wanaweza kunywea kikombe hiki. Walikuwa wamealikwa na Yesu kutolea maisha yao kwa sadaka kwa ajili ya upendo kwa wengine. Walipaswa kuacha woga wote na kusema “NDIO” kwa misalaba yao wakati wakumtumikia Kristo na utume wake.

Kumfuata Yesu sio kitu ambacho tunapaswa kufuata nusu nusu. Kama tunataka kuwa wafuasi wa kweli wa Yesu, tunapaswa kukinywea kikombe cha damu yake takatifu ndani kabisa katika mioyo yetu na kujazwa na zawadi ili tuweze kujitoa wenyewe hata kufikia kiwango cha kujitoa kabisa sadaka. Tunapaswa kuwa tayari kutokuwa na kitu au kushikilia vitu, hata kama ikiwa ni sadaka kubwa. Tunaitwa wote kuwa wafiadini wa kiroho. Hii ina maana kwamba tunapaswa kujikabidhi wenyewe kwa Kristo na mapenzi yake na hii ina maana kwamba tutakuwa tumekufa wenyewe kutoka katika ubinafsi wetu.

“Je, twaweza kukinywea kikombe ambacho Yesu alikinywea?” je, upendo wako kwa Mungu na jirani waweza kuwa mkamilifu kiasi kwamba unakuwa mfiadini katika maana halisi ya neno lenyewe? Jitambue na sema “Ndio”  na kunywa katika kikombe cha damu yake Takatifu na kila siku toa maisha yako kwa sadaka kamili. Unastahili na unaweza!

Sala: Bwana, ninaomba upendo wangu kwako na kwa wengine uongezeke kiasi kwamba sishikilii kitu kingine nyuma yangu. Ninakuomba zawadi ya damu yako Takatifu iwe nguvu katika safari hii ili niweze kuiga sadaka yako kamili ya upendo. Yesu nakumini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MACHI 4, 2026


MASOMO YA MISA, MACHI 4, 2026
JUMATANO, JUMA LA 2 LA KWARESIMA


SOMO 1
Yer. 18-18-20

Waliposema, Njoni na tufanye mashauri juu ya Yeremia; maana sheria haitampotea kuhani, wala shauri halitampotea mwenye hekima, wala neno halitampotea nabii. Njoni, na tumpige kwa ndimi zetu, wala tusiyaangalie maneno yake yoyote.

Niangalie, Ee Bwana, ukasikilize sauti ya wanaoshindana nami. Je! Mabaya yalipwe badala ya mema? Maana wameichimbia nafsi yangu shimo. Kumbuka jinsi nilivyosimama mbele zako, ili nisema mema kwa ajili yao, nikaigeuze ghadhabu yako isiwapate.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 31:4-5, 13-15 (K) 16

(K) Uniokoe kwa ajili ya fadhili zako, Ee Bwana.

Utanitoa katika wavu walionitegea kwa siri,
Maana Wewe ndiwe ngome yangu.
Mikononi mwako naiweka roho yangu;
Umenikomboa, Ee Bwana, Mungu wa kweli. (K)

Maana nimesikia masingizio ya wengi;
Hofu ziko pande zote.
Waliposhauriana juu yangu,
Walifanya hila wauondoe uhai wangu. (K)

Lakini mimi nakutumaini Wewe, Bwana,
Nimesema, Wewe ndiwe Mungu wangu.
Nyakati zangu zimo mikononi mwako;
Uniponye na adui zangu, nao wanaonifuatia. (K)



SHANGILIO
Lk. 8:15

Heri wale walishikao neno la Mungu katika moyo wao mwema na unyofu, na wazaao matunda katika uvumilivu.



INJILI
Mt. 20:17-28

Yesu alipokuwa akipanda kwenda Yerusalemu aliwachukua wale wanafunzi kumi na wawili faraghani; na njiani akawaambia, Angalieni, tunapanda kwenda Yerusalemu; na Mwana wa Adamu atatiwa mikononi mwa wakuu wa makuhani na waandishi nao watamhukumu afe; kisha watampeleka kwa Mataifa wapate kumdhihaki, na kumpiga mijeledi na kumsulibisha; na siku ya tatu atafufuka.

Ndipo mama yao wana wa Zebedayo akamwendea pamoja na wanawe, akamsujudia, na kumwomba neno. Akamwambia, Wataka nini? Akamwambia, agiza kwamba hawa wanangu wawili waketi mmoja mkono wako wa kuume, na mmoja mkono wako wa kushoto, katika ufalme wako. Yesu akajibu akasema, Hamjui mnaloliomba. Je! Mwaweza kunywea kikombe nitakachonywea mimi? Wakamwambia, Twaweza. Akawaambia, Hakika mtakinywa kikombe change; lakini kuketi mkono wangu wa kuume na mkono wangu wa kushoto, sina amri kuwapa, bali watapewa waliowekewa tayari na Baba yangu.

Na wale kumi waliposikia, waliwakasirikia wale ndugu wawili. Lakini Yesu akawaita, akasema, Mwajua ya kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha. Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu yeyote anayetaka kuwa mkubwa kwenu, na awe mtumishi wenu; na mtu yeyote anayetaka kuwa wa kwanza kwenu na awe mtumwa wenu; kama vile Mwana wa Adamu asivyokuja kutumikiwa, bali kutumikia na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

UNYENYEKEVU MBEGU YA KIMUNGU!




“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Machi 3, 2026
Juma la 2 la Kwaresima

Isa 1:10, 16-20;
Zab 50:8-9,16-17,21,23;
Mt 23:1-12


UNYENYEKEVU MBEGU YA KIMUNGU!


Leo nabii Isaya anawaambia wana Waisraeli wafanye uchaguzi. Wajioneshe wenyewe na waache kutenda maovu. Kwaresima ni kipindi cha neema kubwa, ni muda ambao tunapaswa kutafakari ni wapi tulipo kosea na kujaribu kurekebisha. Kama nimechukua fedha isio halali niangalie jinsi ya kurudisha. Kama nilikuwa mtu wa kuapa, niache na kubadilika. Katika hali yeyote, napaswa kufanya kitu. Naweza kuhitaji sakramenti ya kitubio au kutafuta upatanisho na mtu ambaye nilimuumiza au aliyeniumiza.

Yesu anatupa somo zuri sana katika Injili. Anatutaka sisi tuweze kutukuka! Anatutaka sisi tujulikane na wengine. Anataka mwanga wetu mzuri uangaze watu waweze kuuona na kwa mwanga huo waweze kufanya mabadiliko. Lakini anapenda hili lifanyike katika kweli sio katika hali ya kudanganya. Anataka ukweli wa “mimi” uangaze. Nao ni unyenyekevu. Unyenyekevu ni kuwa mnyofu na mwaminifu. Na wakati watu watakapo ona hali hii ndani yetu, watavutwa. Sio sana katika hali ya kidunia bali katika hali ya kibinadamu. Hawata tuangalia na kuwa na wivu bali, watatuangalia na kuona ukweli wenyewe na kuufurahia, kuutamani na kutaka kuuishi. Unyenyekevu unakusaidia ukweli kamili kuhusu wewe uweze kungaa. Na wewe ukiwa katika kweli unakuwa ndiye mtu mwingine ambaye wengine wanataka kukutana naye.

Sala: Bwana, naomba unifanye niwe mnyenyekevu. Nakuomba niweze kuwa mwaminifu na mkweli kwa jinsi nilivyo. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MACHI 3, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 3, 2026
JUMANNE, JUMA LA 2 LA KWARESIMA


SOMO 1
Isa. 1:10, 16-20

Lisikieni neno la Bwana, enyi waamuzi wa Sodoma; tegeni masikio msikie sheria ya Mungu wetu, enyi watu wa Gomora.

Jiosheni, jitakaseni; ondoeni uovu wa matendo yenu usiwe mbele za macho yangu; achene kutenda mabaya; jifunzeni kutenda mema; takeni hukumu na haki; wasaidieni walioonewa; mpatieni yatima haki yake; mteteeni mjane.

Haya, njoni, tusemezane, asema Bwana. Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji; zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa kama sufu.

Kama mkikubali na kutii mtakula mema ya nchi; bali kama mkikataa na kuasi mtaangamizwa kwa upanga; maana kinywa cha Bwana kimenena haya.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 50:8-9, 16-17, 21, 23 (K) 23

(K) Autengenezaye mwenendo wake,
Nitamwonyesha wokovu wangu.

Sitakukemea kwa ajili ya dhabihu zako,
Na kafara zako ziko mbele yangu daima.
Sitatwaa ng’ombe katika nyumba yako,
Wala beberu katika mazizi yako. (K)

Una nini wewe kuitangaza sheria yangu,
Na kuliweka agano langu kinywani mwako?
Maana wewe umechukia maonyo,
Na kuyatupa maneno yangu nyuma yako. (K)

Ndivyo ulivyofanya, nami nikanyamaza,
Ukadhani ya kuwa Mimi ni kama wewe,
Atoaye dhabihu za kushukuru, ndiye anayenitukuza.
Naye autengenezaye mwenyendo wake,
Nitamwonyesha wokovu wa Mungu. (K)



SHANGILIO
Mt. 4:17

Tubuni asema Bwana, kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.



INJILI
Mt. 23:1-12

Yesu aliwaambia makutano na wanafunzi wake, akasema, Waandishi na Mafarisayo wameketi katika kiti cha Musa; basi, yoyote watakayowaambia, myashike, na kuyatenda; lakini kwa mfano wa matendo yao, msitende; maana wao hunena lakini hawatendi. Wao hufunga mizigo mizito na kuwatwika watu mabegani mwao; wasitake wenyewe kuigusa kwa kidole chao. Tena matendo yao yote huyatenda ili kutazamwa na watu; kwa kuwa hupapanua hirizi zao, huongeza matamvua yao; hupenda viti vya mbele katika karamu, na kuketi mbele katika masinagogi, na kusalimiwa masokoni, na kuitwa na watu, Rabi.

Bali ninyi msiitwe Rabi, maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu. Wala msimwite mtu baba duniani; maana Baba yenu ni mmoja, aliye wa mbinguni. Wala msiitwe viongozi; maana kiongozi wenu ni mmoja, naye ndiye Kristo. Naye aliye mkubwa wenu atakuwa mtumishi wenu. Na yeyote atakayejikweza atadhiliwa; na yeyote atakayejidhili atakwezwa.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.