Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

TAZAMA NINATENDA TENDO JIPYA


Tafakari ya Ukarimu
Jumatatu, Machi 23, 2026
Juma la 5 la Kwaresima

Dan 13:1-9,15-17,19-30,33-62; 
Zab 23: 1-6; 
Yn 8: 1-11


TAZAMA NINATENDA TENDO JIPYA


Katika injili, tunamkuta akinamama mmoja aliyesukumwa mbele ya Yesu. “Amefumaniwa alipokuwa akizini. Mwanaume yeye ametoweka lakini mwana mke huyo amekamatwa. Mafarisayo wamemleta mbeie yaYesu. Macho yao yana mhukumu sawasawa na maneno yao. Ha Yesu hamwangalii hata. Asiwe anamw aibisha, Yesu anatazama chini naye anawazungumzia kwanza wenye kumshtaki. Kitambo tu nao wameondoka kwa sababu wanaona kwamba hata wao wenyewe wangeweza kushtakiwa.

Yesu alifanya nini kwa ajili ya mwanamke huyo. Je, alisema kwamba alilo tenda si jambo baya? Je, alisema kwamba kwa vyo vyote si vibaya sana kulala na mtu asiye mumewe? Hata. Ha alimsaidia aende mbele. Asahau mambo ya zamani na kutazama siku za usoni

“Hakuna aliyekuhumu kuwa na hatia?
Wala mimi sikuhukumu.
Enenda zako; wala usitende dhambi tena.”

Yesu anasahau na kusamehe mambo yake ya zamani. Ndivyo Mungu alivyo Ndivyo alivyokuwa amefanya kwa ajili ya Taifa lake —taifa Ia Israeli - kabla ya Yesu kuja ulimwenguni petu. Mungu anawaita: “Wateule wangu”. Hata ikiwa taifa lake wamekuwa wanamkosea uaminifu mara nyingi sana. Hata ikiwa mara nyingi mno wamekwenda mbali naye wala hawakutii amri zake, Mungu anawaambia waya sahau mambo ya zamani na kuona “tendojipya”analowafanyia. Anawasamehe tena na kuwaokoa.

Ndivyo Mungu wetu alivyo: Mungu anayeangalia mambo yetu ya zamani ili kuyasamehe ikiwatunayasikitikia hayo tuliyotenda. Ndiye Mungu mwenye kuele keza macho na mioyo yetu kwa siku za usoni. kwa hayo anayotuandalia Yeye

Ndio hasa ujumbe wa injili - Habari Njema ambayo sote twahitaji kuisikia. Mungu hataki kutuona tunasukuma makosa yetu ya zamani na kushindwa kwetu kama mzigo mzito. Mungu haoni furaha kutuona tunatembea tukiwa na nyuso zenye huzuni na mioyo mizito kwa ajili ya mzigo wa dhambi zetu za zamani.

Makumbukumbu mabaya, masikitiko, na hall mbaya mno ya kujisikia kuwa hawawezi kuyafuta kabisa mambo ya zamani. Mambo hayo yote yawalemeza watu. Wanajisikia wamepondwa na mzigo wa namna hii. Wangependa kuwekwa huru kutoka kwa mzigo huo, ila upo nao siku zote, mchana na usiku.

Lakini yupo Mmoja awezaye kutuweka huru kutoka kwa mziço wetu Mzigo wa dhambi na hatia. Mzigo wa makumbukumbu mabaya na masikitiko. Mungu ndiye atakaye kufanya hivi. Mwanaye Yesu amekuja kwetu kwa kusudi hilo hasa. Anangoja tu tuwe tunamgeukia. Pengine, hata ndiye Mwenyewe anayetugeukia akituomba tuukubali msaada wake.

Kama ilivyomtokea mwanamke yule aliyegunduliwa katika kuzini. Aliachwa na mpenzi wake. Sasa wenye kumshtaki wameondoka naye yupo peke yake mbele ya Yesu akiogopa Yesu alimsamehe mwanamke naye alimwachia Yesu mambo yake ya zamani

Sisi vile vile mara nyingi twajisikia tumeachwa tu peke yetu na kuogopa Lakini sisi pia twaweza kusamehewa. Na tukiwa tumesamehewa, Mungu anatu omba tumwachie mambo yetu ya zamani. Lililo Ia maana hasa siyo hayo tuli yosema na kutenda. Lililo a maana ndiyo afanyayo Mungu na hayo atakayotuwe zesha kufanya na sisi wakati ujao

Tukimruhusu Mungu ayashughulikie mambo yetu ya zamani, hapotutajisikia kama Wayahudi. Katika Zaburi ya leo, tumewasikia wakisema: “Bwana alipoture jeza, tulikuwa kama waotao ndoto. Ndipo kinywa chetu kilipojaa kicheko.” Jambo tile tile laweza kututokea sisi, ikiwa tutamruhusu Mungu atufanye tuwe wapya kwa msamaha wake.

Maisha mapya - Juma hililija uchukue muda na uone jambo gani maishani mwako ni zito kubebwa. Ujiulize kwa nini unasukuma mzigo huo. Halafu, umgeukie Bwana na umwachie jambo lo lote lenye kukulemeza tangu zamani.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MACHI 23, 2026


MASOMO YA MISA, MACHI 23, 2026
JUMATATU, JUMA LA 5 LA KWARESIMA


SOMO 1
Dan.13:41-62

Palikuwa na mtu mmoja jina lake Yoakimu, akikaa Babeli, naye ameoa mke jina lake Susana binti Helkia, mwanamke mzuri sana na mcha Mungu. Wazee wake nao walikuwa wenye haki, pia wamemfundisha binti yao sawasawa na Torati ya Musa. Basi Yoakimu alikuwa mwungwana tajiri, na karibu na nyumba yake alikuwa na bustani nzuri; hivyo Wayahudi humwendea, maana alikuwa ni mwenye heshima kupita wengineo wote. Mwaka ule ule wakaamriwa wawili miongoni mwa wazee wa watu ili kuamua, watu wa namna ile ambao Bwana aliwanena, ya kama ufisadi ulitoka Babeli kwa wazee waamuzi waliohesabiwa kuwa wanatawala watu. Hao walikuwa wakienda mara nyingi kuzuru kwenye nyumba yake Yoakimu; na wote wenye mashtaka yoyote desturi yao wakawajia huko. Basi watu walipoondoka kwenda zao panapo saa sita, Susana huingia katika bustani ya mumewe ili kutembea. Nao wale wazee humwona kila siku anakwenda kutembea; hata wakawaka tamaa kwa sababu yake. Ndipo walipozipotosha nia zao, wakayageuza upande macho yao wasiweze kutazama mbinguni wala kukumbuka hukumu za haki. Ikawa walipongoja wakati wa kufaa, yeye aliingia bustanini kama ilivyokuwa desturi yake pamoja na wajakazi wawili, naye alitaka kuoga kwa sababu kulikuwa na joto. Wala hapakuwa na mtu yeyote isipokuwa wale wazee wawili, ambao wamejificha wakimvizia. Basi akawaambia wajakazi wake, Nileteeni mafuta na sabuni, mkaifunge milango ya bustani ili nioge . Mara wale wajakazi walipokwishas kutoka, wale wazee wawili waliondoka wakamwendea mbio, wakasema, Tazama, milango ya bustani imefungwa asiweze kutuona mtu yeyote nasi tunakupenda sana; haya! Basi, utukubali na ulale nasi. La! Hutaki tutakushuhudia ya kuwa hapa palikuwapo na kijana pamoja nawe, ndiyo sababu uliwaruhusu wajakazi wako. Basi Susana aliugua akasema, Nimesongwa pande zote, maana nikilitenda hilo ni mauti yangu; nisipolitenda siwezi kuokoka mikononi mwenu. Ni afadhali niangukie katika mikono yenu na kukataa, kuliko kutenda dhambi machoni pa Mungu. Mara Susana akapiga kelele kwa sauti kuu; nao wale wazee wawili wakampigia kelele pia. Kisha mmoja wao akakimbia, akaifungua milango ya bustani. Hivyo watumishi wa nyumbani waliposikia kelele bustanini, wao waliingia kwa kasi kwa mlango wa nyuma ili waone ni nini iliyompata. Lakini wale wazee waliisimulia hadith yao nao watumishi wakaona aibu kabisa, kwa maana Susana hakuchongelewa habari ya namna hiyo wakati wowote.

Ikawa kesho yake watu walipokusanyika kwa Yoakimu mumewe, wale wazee wawili wakaja nao, wamejaa kusudi lao ovu juu ya Susana la kumfisha. Wakasema mbele ya watu, "Mwiteni Susana binti Helkia, mkewe Yoakim, aje hapa". Basi akaenda kuitwa; naye akaja pamoja na baba yake na mama yake, na watoto wake, na jamaa zake wote. Naye huyo Susana alikuwa mwanamke mwenye adabu, mzuri wa uso; basi hao watu wabaya waliamuru afunuliwe uso, maana alifunikwa utaji, ili washibe uzuri wake. Kwa hiyo rafiki zake na wote waliomtazama wakasikitika. Ndipo wale wazee wawili waliposimama katikati ya watu, wakaweka mikono yao juu ya kichwa chake. Naye akatoka machozi, akatazama juu mbinguni, kwa maana moyo wake ulimtumaini Mungu. Wale wazee wakasema, Sisi tulipokuwa tukitembea bustanini peke yetu, huyu aliingia pamoja na wajakazi wawili, wakaifunga milango ya bustani, naye mara akawaruhusu wajakazi. Kisha kukatokea kijana, ambaye amejificha humo, akamwendea akalala naye. Walakini sisi tungaliko pembeni mwa bustani, tuliona ubaya huo, tukamwendea mbio. Hata tukiwa tumewaona pamoja, yule kijana hatukuweza kumkamata, maana alikuwa mwenye nguvu kuliko sisi, akifungua milango akaepuka. Bali huyu tulimkamata, tukauliza yule kijana yu nani, asikubali kutuambia. Hayo basi, tunashuhudu. Basi waliohudhuria wakawasadiki, wakiwa wazee wa watu na waamuzi; hivyo wakahukumu auawe. Mara Susana akalia kwa sauti kuu, akasema, Ee Mungu wa milele, Wewe wajua yaliyositirika, wajua mambo yote yasijekuwako, Wewe wajua ya kwamba wananishuhudia uongo, na tazama, imenipasa kufa; walakini sikufanya mambo kama hayo, ambayo watu hawa wameyabuni juu yangu kwa ukorofi.

Naye Bwana akaisikia sauti yake. Kwa hiyo, alipochukuliwa huyo kwenda kuuawa, Mungu alimchocheleza roho kijana mmoja, jina lake Danieli; naye akapaza sauti akasema, Mimi simo; mimi sina hatia kwa habari ya damu yake mwanamke huyu. Mara wote wakamgeukia, wakasema, Maneno hayo uyasemayo, maana yake nini? Akasimama katikati, akasema, Enyi bani Israeli, mmekuwa wapumbavu, hata kumhukumu binti Israeli bila kuhoji wala kupata hakika ya kweli? Rudini hukumuni; mradi hao wanamshuhudia uongo.

Basi watu wote walirejea kwa haraka, nao wale wazee wakamwambia, Njoo uketi kati yetu, utujulishe habari hiyo, endapo Mungu amekupa wewe heshima yam zee. Hapo Danieli aliwaambia, Watu hawa wawili watengwe, nami nitawahoji. Basi wakiisha kutengwa, akamwita mmoja wao akamwambia, Ewe uliyepata kuwa mzee katika uovu, sasa dhambi zako zimekukalia, ulizozitenda zamani kwa kuhukumu isivyo haki, kumpatiliza asiye na hatia na kumwachilia mwovu; lakini Bwana asema, Asiye na hatia, mwenye haki, usimwue. Haya! Basi, wewe ulimwona kwa macho; useme; Chini ya mti gani ulipowaona wakikaa pamoja? Naye akajibu, Chini ya msandarusi. Danieli akasema, Hakika umesema uongo juu ya kichwa chako mwenyewe; maana sas hivi malaika wa Mungu amepokea hukumu ya Mungu, akukate vipande viwili. akamtenga huyo tena, akaamuru kumleta yule mwingine, akamwambia, Ewe mzao wa Kanaani, wala si wa Yuda, uzuri umekudanganya, na tamaa imeupotosha moyo wako. Hivyo ndivyo ulivyowafanyia binti za Israeli, na kwa hofu walitembea nawe; bali huyu binti Yuda hakuweza kuustahimili uovu wako. Haya! Basi, nawe useme; Chini ya mti gani ulipowaona wakikaa pamoja? Naye akajibu, Chini ya mkwaju. Danieli akamwambia, Hakika wewe nawe umesema uongo juu ya kichwa chako mwenyewe; maana malaika wa Mungu yu tayari, anakungoja mwenye upanga, akukate vipande viwili; ili awaangamize nyote wawili.

Mara hiyo makusanyiko yote wakapaza sauti kwa nguvu, wakamhimidi Mungu awaokoaye wamtumainio. Wakawaondokea wale wazee wawili, kwa maana Danieli ameuhakikisha ushuhuda wao wa uongo hata vinywani mwao wenyewe. Wakawatenda kwa Torati ya Musa kama vile walivyokusudia kwa ukorofi kumfanyia jirani yao; wakawaua; na mwenye damu isiyo na hatia aliokolewa siku ile.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 23 (K) 4

(K) Nijapopita katika bonde la uvuli wa mauti, Sitaogopa mabaya; Kwa maana Wewe upo pamoja nami.

Bwana ndiye mchungaji wangu,
Sitapungukiwa na kitu.
Katika malisho ya majani mabichi hunilaza,
Kando ya maji ya utulivu huniongoza. (K)

Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza,
Katika njia za haki kwa ajili ya jina lake.
Naam, nijapopita kati aya bonde la uvuli wa mauti
Sitaogopa mabaya; kwa maana Wewe upo pamoja nami,
Gongo lako na fimbo yako vyanifariji. (K)

Waandaa meza mbele yangu,
Machoni pa watesi wangu.
Umenipaka mafuta kichwani pangu,
Na kikombe change kinafurika. (K)

Hakika wema na fadhili zinanifuata,
Siku zote za maisha yangu,
Nami nitakaa nyumbani mwa Bwana milele. (K)



SHANGILIO
Yn. 6:64, 69

Maneno yako, Ee Bwana, ni roho, tena ni uzima, Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.



INJILI
Yn. 8:1-11

Yesu akaenda mpaka mlima wa Mizeituni. Hata asubuhi kulipokucha akaingia tena hekaluni, na watu wote wakamwendea; naye akaketi, akawa akiwafundisha.

Waandishi na Mafarisayo wakamletea mwanamke aliyefumaniwa katika uzinzi, wakamweka katikati. Wakamwambia, Mwalimu, mwanamke huyu amefumaniwa alipokuwa akizini. Basi katiak torati, Musa alituamuru kuwapiga kwa mawe wanawake namna hii; nawe wasemaje? Nao wakasema neno hili wakimjaribu, ili wapate sababu ya kumshitaki.

Lakini Yesu akainama, akaandika kwa kidole chake katika nchi. Nao walipozidi kumhoji, alijiinua, akawaambia, Yeye asiye na dhambi miongoni mwenu na awe wa kwanza wa kumtupia jiwe. Akainama tena, akaandika kwa kidole chake katika nchi. Nao waliposikia, wakashitakiwa na dhamiri zao, wakatoka mmoja mmoja, wakianzia tangu wazee hata wa mwisho wao; akabaki Yesu peke yake, na yule mwanamke amesimama katikati.

Yesu akajiinua asimwone mtu ila yule mwanamke, akamwambia, Mwanamke, wako wapi wale washitaki wako? Hakuna aliyekuhukumu kuwa na hatia? Akamwambia, Hakuna, Bwana. Yesu akamwambia, Wala mimi sikuhukumu. Enenda zako; wala usitende dhambi tena.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

WATU WA UFUFUKO



“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Jumapili, Machi 22, 2026
Juma la 5 la Kwaresima

Eze 37: 12-14;
Zab 130: 1-8;
Rum 8: 8-11;
Yn 11: 1-45.


WATU WA UFUFUKO


Giza, na ukimya, vilifunika kifo kadiri ya tamadunii za Wayahudi. Ni vigumu kupata maelezo kuhusu kutoharibika kwa roho au ufufuko wa wafu katika Agano la Kale. Ayubu alisema “kuna matumaini kwa mti; kama ukikatwa unaweza kuchipua tena, machipukizi mapya yatatokea tena. Lakini mwanadamu anavyokatwa, huanguka chini na huvuta pumzi yake ya mwisho-atakuwa wapi? Maji ya bahari yanaweza kutoweka, mito kukauka, lakini yule anayelala chini hawezi kuamka tena; mbingu zitaisha kabla hajaamka, kabla hajaamka usingizini.” (Ayubu 14:7-12). Biblia ilihifadhi kumbukumbu ya jinsi jambo lilivyokuwa gumu ili kutukumbusha ni kwa jinsi ghani giza lilitisha katika kaburi, kabla ya ufufuko na mwanga wa Pasaka duniani. Lakini pia mzaburi analeta matumaini. “Nijapopita katika giza la mauti, sintaogopa mbaya, kwani wewe Bwana wa uhai utakuwa pamoja nami”

“Kifo” kinaonekana kutisha kwa watu wengi, lakini ni wazi kwamba hakuna kitu tulicho na uhakika nacho katika maisha zaidi ya kifo. Wengi wetu tunazungukwa na hofu, baada ya kifo kuna nini? Wafuasi hawakuwa na tofauti. Hali yote inayo wazunguka inaonekana kutisha, na kwa upande mwingine Yesu anatabiri kuwa kifo chake kipo karibu na kwa upande mwingine wanawaogopa Wayahudi amabao walitaka kumpiga Yesu mawe mpaka afe. Kwa kipindi hichi tunaona jibu laTomasi lilivyo na mashaka “twende na sisi tukafe pamoja naye”. Ni hakika kwamba hofu ya kifo iliwakumba wafuasi. Yesu kwa kumfufua Lazaro kutoka wafu anataka kuwafunulia mitume na watu wengine kwamba yeye ni nani “YEYE NI UFUFUO NA UZIMA”.

Kifo ni nini?
Katika Injili ya leo, Yesu anakwepa kutumia neno ‘kufa’ badala yake anatumia ‘kupumzika’ akionesha kifo cha Lazaro. Kifo kilionekana kuwa ni kitu hasi na pia mwisho wa kitu. Lakini Yesu kwa kutumia neno “kupumzika’ anataka kuwaambia wafuasi kwamba kifo sio mwisho wa kila kitu, bali njia ya kupitia kutoka hali moja kwenda hali nyingine ya maisha. Kifo ni njia ya kupitia kutoka maisha haya ya duniani kuelekea maisha ya milele, njia ambayo imefunguliwa kwa ufufuko wa Yesu.

Ufufuko ni nini?
Wayahudi waliamini kwamba ni Mungu mwenyewe anaweza kurudisha uhai. Yesu anatumia kifo cha Lazaro kuonesha kweli yeye ni mwana wa Mungu, kwa kumfufua kutoka wafu. Lazaro ambaye alikuwa amekufa kwa siku nne, sasa anakuwa hai. Lazaro aliyekuwa amekufa sasa anatembea kutoka kaburini. Wayahudi waliamini kuhusu ufufuo wa wafu lakini ilikuwa mpaka dunia itakapopita. Na hapa wanaona kitu ambacho kina washangaza, mtu ambaye alikuwa amekufa kwa siku nne, anakuwa hai tena. Walio shuhudia waliamini kabisa Yesu sio nabii wa kawaida wala mwalimu wa kawaida bali Mungu mwenyewe. Yesu anaendelea kuonesha kwamba ufufuko sio tukio baada ya kifo, bali linaanza duniani kwa kuishi ukiwa umeunganika na Yesu.

Katika somo la kwanza katika kitabu cha nabii Ezekieli, anatangaza tukio ambalo Mungu anaenda kulitenda, muujiza wa ajabu. Mungu analeta uhai katika mifupa iliokauka. Mungu atafunua makaburi ambayo walikuwa wamefungwa, atawafanya watoke katika makaburi yao na kuwaongoza tena katika Nchi yao. Roho wa Mungu aliingia kila mahali na maisha yakaanza. Yalianza wakati wa mwanzo wa dunia, wakati Mungu anamuumba mwanadamu kutoka mavumbini, alimpulizia pumzi ya uhai na mwanadamu akaishi (Mwa 2:7). Hakuna kinacho shindikana kwa Roho wa Mungu. Anaweza kuleta maisha pia hata katika mifupa iliyo kauka kabisa.

Katika somo la pili, Paulo anatuambia, Yesu akiwa mtu kama sisi, alikufa. Lakini alifufuka. Yesu ana Roho kamili wa Mungu, ni kwamba ana ndani yake uhai wa Kimungu ambao hauwezi kufa. Yesu alikuwa na uhai huu wa Kimungu ndani yake. Roho wa Mungu alimfufua, na kumtambulisha katika utukufu wa Baba. Wale walio batizwa katika roho wake, katika maisha yake, hawafi tena. Maisha yetu katika ulimwengu huu yataisha, yatafika mwisho, lakini haitakuwa mwisho wa kila kitu. Roho aliye mfufua Yesu atatufua na kuipatia uzima wa milele miili Yetu inayo kufa.

Mkristo haamini katika kifo na ufufuko kama kitu ambacho kitatokea mwisho wa dunia. Ana amini kwamba mtu aliyekombolewa na Yesu hafi. Yesu alitangaza kwa Martha kwamba “kila anaye niamini mimi hatakufa kamwe”(Mtari wa 26). Pasaka inakaribia ni majuma mawili tu yajayo, na waliyo wengi tunatazama ufuko kama tukio litakalo tokea baadae. Tunashindwa kuishi kama watu wa ufufuko. Kwaresima inaonekana kama maombolezo, kujinyima, toba, lakini kwa hakika kwaresima ni kipindi cha kujifunza jinsi ya kuishi maisha ya ufufuko. Yesu amekuja kutukomboa sisi, sio tu baada ya kifo chetu bali pia tukiwa hai. Tukiwa na matumaini na tukiishi Imani katika ufufuko tuishi kama watu wa ufufuko kuanzia leo. Na yeye aliyempa Lazaro uhai kwa hakika atatupa sisi uhai, uhai tele.

Sala: Bwana, wewe ni ufufuo na uzima. Nisaidie niondokane a muonekano wangu mbaya kuhusu uzima na kifo. Ninaomba nikuwe katika Imani ya roho wa uzima aliye ndani mwangu. Ninakuomba niweze kutambua Uzima wa Kimungu ndani mwangu. Ninaomba nitoke katika hofu zangu, na kwenda katika maisha ya ufufuo. Yesu, nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MACHI 22, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 22, 2026
DOMINIKA YA 5 YA KWARESIMA

MWANZO:
Zab. 43:1 – 2

Ee Bwana, unihukumu, unitetee kwa taifa lisilo haki, uniokoe na mtu wa hila asiye haki. Kwa kuwa wewe ndiwe Mungu uliye nguvu zangu.


SOMO 1
Eze. 37:12 – 14

Bwana Mungu asema hivi; Tazama, nitafunua makaburi yenu, na kuwapandisha kutoka katika makaburi yenu, enyi watu wangu, nami nitawaingizeni katika nchi ya Israeli. Nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, nitakapoyafunua makaburi yenu, na kuwatoa ninyi katika makaburi yenu, enyi watu wangu. Nami nitatia roho yangu ndani yenu, nanyi mtaishi, nami nitawawekeni katika nchi yenu, nanyi mtajua ya kuwa mimi, Bwana, nimesema hayo, na kuyatimiza asema Bwana, nimesema hayo, na kuyatimiza asema Bwana.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 130 (K) 7

(K) Kwa Bwana kuna fadhili, na kwake kuna ukombozi mwingi.

Ee Bwana, toka vilindini nimekulilia,
Bwana, uisikie sauti yangu.
Masikio yako na yaisikilize
Sauti ya dua zangu. (K)

Bwana, kama Wewe ungehesabu maovu,
Ee Bwana, nani angesimama?
Lakini kwako kuna msamaha,
Ili Wewe uogopwe. (K)

Nimemngoja Bwana, roho yangu imengoja,
Na neno lake nimelitumainia.
Nafsi yangu inamngoja Bwana,
Kuliko walinzi waingojavyo asubuhi,
Naam, walinzi waingojao asubuhi.
Ee Israeli, umtarajie Bwana. (K)

Maana kwa Bwana kuna fadhili,
Na kwake kuna ukombozi mwingi.
Yeye atamkomboa Israeli
Na maovu yake yote. (K)


SOMO 2
Rum. 8:8 – 11

Wale waufuatao mwili hawawezi kumpendeza Mungu. Lakini ikiwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu, ninyi hamwufuati mwili; bali mwaifuata roho.

Lakini mtu awaye yote asipokuwa na Roho wa Kristo, huyo si wake. Na Kristo akiwa ndani yenu, mwili wenu umekufa kwa sababu ya dhambi; bali roho yenu I hai, kwa sababu ya haki. Lakini, ikiwa Roho wake yeye aliyemfufua Yesu katika wafu anakaa ndani yenu, yeye aliyemfufua Kristo Yesu katika wafu ataihuisha na miili yenu iliyo katika hali ya kufa, kwa Roho wake anayekaa ndani yenu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


SHANGILIO
Yn. 11:25, 26

Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima, asema Bwana; Yeye aniaminiye mimi, hatakufa kabisa hata milele.


INJILI
Yn. 11:1 – 45

Basi mtu mmoja alikuwa hawezi, Lazaro wa Bethania, mwenyeji wa mji wa Mariamu na Martha, dada yake. Ndiye Mariamu yule aliyempaka Bwana marhamu, akamfuta miguu kwa nywele zake, ambaye Lazaro nduguye alikuwa hawezi.

Basi wale waumbu wakatuma ujumbe kwake wakesema, Bwana, yeye umpendaye hawezi. Naye Yesu aliposikia, alisema, Ugonjwa huu si wa mauti, bali ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu, ili Mwana wa Mungu atukuzwe kwa huo. Naye Yesu alimpenda Martha na umbu lake na Lazaro. Basi aliposikia ya kwamba hawezi, alikaa bado siku mbili pale pale alipokuwapo. Kisha, baada ya hayo, akawaambia wanafunzi wake, Twendeni Uyahudi tena.

Wale wanafunzi wakamwambia, Rabi, juzijuzi tu Wayahudi walikuwa wakitafuta kukupiga kwa mawe, nawe unakwenda huko tena? Yesu akajibu, Je! Saa za mchana si kumi na mbili? mtu akienda mchana hajikwai; kwa sababu aiona nuru ya ulimwengu huu. Basi akienda usiku hujikwaa; kwa sababu nuru haimo ndani yake.

Aliyasema hayo; kisha, baada ya hayo, akawaambia, Rafiki yetu, Lazaro, amelala; lakini ninakwenda nipate kumwamsha. Basi wale wanafunzi wakamwambia, Bwana, ikiwa amelala, atapona. Lakini Yesu alikuwa amenena habari ya mauti yake; nao walidhani aya kuwa ananena habari ya kulala usingizi. Basi hapo Yesu akawaambia waziwazi, Lazro amekufa. Nami nafurahi kwa ajili yenu kwamba sikuwapo huko, ili mpate kuamini; lakini na twendeni kwake. Basi Tomaso, aitwaye Pacha, akawaambia wanafunzi wenziwe, Twendeni na sisi ili tufe pamoja naye.

Basi Yesu alipofika, alimkuta amekwisha kuwamo kaburini yapata siku nne. Na Bethania ilikuwa karibu na Yerusalemu, kadiri ya maili mbili hivi; na watu wengi katika Wayahudi walikuwa wamekuja kwa Martha na Mariamu, ili kuwafariji kwa habari ya ndugu yao.

Basi Martha aliposikia kwamba Yesu anakuja, alikwenda kumlaki; na Mariamu alikuwa akikaa nyumbani. Basi Martha akamwambia Yesu, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa. Lakini hata sasa najua ya kuwa yoyote utakayomwomba Mungu, Mungu atakupa. Yesu akamwambia, Ndugu yako atafufuka. Martha akamwambia, Najua ya kuwa atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho. Yesu akamwambia, Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je! Unayasadiki hayo? Akamwambia, Naam, Bwana, mimi nimesadiki ya kwamba wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu, yule ajaye ulimwenguni.

Naye alipokwisha kusema hayo, alikwenda zake; akamwita umbu lake Mariamu faraghani, akisema, Mwalimu yupo anakuita. Naye aliposikia, aliondoka upesi, akamwendea. Na Yesu alikuwa hajafika ndani ya kijiji; lakini alikuwa akalipo pale pale alipomlaki Martha. Basi wale Wayahudi waliokuwapo na Mariamu nyumbani, wakimfariji, walipomwona jinsi alivyoondoka upesi na kutoka, walimfuata; huku wakidhania ya kuwa anakwenda kaburini ili alie huko.

Basi Mariamu alipofika pale alipokuwapo Yesu, na kumwona, alianguka miguuni pake, akamwambia, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa. Basi Yesu alipomwona Analia, na wale Wayahudi waliofuatana naye wanalia, aliugua rohoni, akafadhaika roho yake, akasema, Mmemweka wapi? Wakamwambia, Bwana, njoo utazame. Yesu akalia machozi. Basi Wayahudi wakasema, Angalieni jinsi alivyompenda. Bali wengine wao wakasema, Je! Huyu aliyemfumbua macho yule kipofu, hawezi kumfanya na huyu asife? Basi Yesu hali akiugua tena nafsini mwake, akafika kwenye kaburi. Nalo lilikuwa ni pango, na jiwe. Martha, dada yake yule aliyefariki, akamwambia, Bwana, ananuka sasa; maana amekuwa maiti siku nne. Yesu akamwambia, Mimi sikukuambia ya kwamba ukiamini utauona utukufu wa Mungu? Basi wakaliondoa lile jiwe. Yesu akainua macho yake juu, akasema, Baba nakushukuru kwa kuwa umenisikia. Nami nalijua ya kuwa wewe wanisikia sikuzote; lakini kwa ajili ya mkutano huu wanaohudhuria nalisema haya, ili wapate kusadiki kwamba ndiwe uliyenituma.

Naye akiisha kusema hayo, akalia kwa sauti kuu, Lazaro, njoo huku nje. Akatoka nje yule aliyekufa, amefungwa sanda miguuni na mikononi, na uso wake amefungwa leso. Naye Yesu akawaambia Mfungueni, mkamwache aende zake.

Basi wengi katika Wayahudi waliokuja kwa Mariamu, na kuyaona yale aliyoyafanya, wakamwamini.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUMSIKILIZA YESU



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Kwaresima
Jumamosi, Machi 21, 2026, 
Juma la 4 la Kwaresima

Yer 11: 18-20;
Zab 7: 2-3, 9-12;
Yn 7: 40-53.


KUMSIKILIZA YESU

Ni vigumu kutokuitika unapokutana na ujumbe wa Yesu. Baadhi ya watu waliamini kuwa Yeye ni nabii, wengine kwamba ni Masiha, na hivyo walikuwa wameshawishika huenda ni mmoja wapo kati ya hao. Lakini muonekano wa wakuu unashangaza. Walienda kumkamata lakini wakarudi mikono mitupu, kwasababu hawakuwahi kumsikia yeyote akiongea kama yeye. Mafariyo na Waandishi wanaonekana kutopendezwa. Muonekano wa Nikodemu unaonekana kuwa ni wa woga. Moyo wake ulimwambia amlinde Yesu, lakini akili yake ilimwambia asije akajihatarishia maisha. 

Wakati Yesu anafundisha kuna kitu kilichokuwa kikiwakilishwa zaidi ya maneno yake. Maneno yake yana nguvu ya kufanya mambo upya, lakini ilikuwa ni kwa jinsi yake ya kuongea. Ni vigumu kuelezea, lakini ni hakika kwamba alivyo ongea, aliwasilisha pia nguvu, utulivu, hali ya kuguswa na kukubali na pia uwepo wake. Aliwakilisha uwepo wake wa Kimungu bila dosari. Watu walitambua tu huyu mtu, Yesu , ni tofauti na wengine wote, na kujikuta wakisikiliza kila neno lake. 

Mungu anawasiliana nasi kwa namna hii. Yesu bado anaongea nasi. Tunapaswa tu kuwa wasikivu kwa neno lake. Tunapaswa kuwa wasikivu katika njia ambazo Mungu anaongea nasi katika hali ya wazi kabisa yenye kugusa mioyo yetu, na kwa mamlaka yake. Inaweza kuwa ni kitu mtu anasema, au matendo anayofanya mtu yakatugusa. Inaweza kuwa kitabu nilichosoma, au kitu ambacho nasikia katika maandiko. Katika hali yeyote inavyoweza kuwa, tunapaswa kusikiliza kwani ndipo tunapokutana na Yesu mwenyewe. Kujikita katika kufuata njia ya Mungu ni kujitahidi kutokusikiliza vipingamizi na shutuma unazoweza kupata katika kufuata sauti yake. Sauti yake inapaswa kushinda na kukuvuta katika kufanya yale yote anayopenda uyafanye. 

Sala: Bwana, ninaomba niwe msikivu kwa sauti yako isiyo na dosari na katika mamlaka unayo zungumza. Na ninapo kusikiliza, Bwana mpendwa, nisaidie niitike kwa Imani licha ya vipingamizi vya wengine. Yesu, nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MACHI 21, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 21, 2026
JUMAMOSI: JUMA LA 4 LA KWARESIMA


SOMO 1
Yer. 11:18-20

Bwana akanijulisha haya, nami nikayajua; ndipo uliponionyesha matendo yao. Lakini mimi nalikuwa kama mwana-kondoo mpole, achukuliwaye kwenda kuchinjwa; wala sikujua ya kuwa wamefanya mashauri kinyume changu, wakisema, Na tuuharibu mti pamoja na matunda yake, na tumkatilie mbali atoke katika nchi ya walio hai, ili jina lake lisikumbukwe tena.

Lakini, Ee Bwana wa majeshi, uhukumuye haki ujaribuye viuno na moyo, nijalie kuona kisasi chako juu yao; kwa maana nimekufunulia wewe neno langu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Bwana.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 7:1-2, 8-12 (K) 1

(K) Bwana, Mungu wangu, nimekukimbilia Wewe.

Bwana, Mungu wangu, nimekukimbilia Wewe,
Uniokoe na wote wanaonifuatia, uniponye.
Asije akaipapura nafsi yangu kama samba,
Akiivunja-vunja pasipokuwa na wa kuponya. (K)

Bwana, unihukumu mimi,
Kwa kadiri ya haki yangu,
Sawasawa na unyofu nilio nao.
Ubaya wao wasio haki na ukome,
Lakini umthibitishe mwenye haki. (K)

Ngao yangu ina Mungu,
Awaokoaye wanyofu wa moyo.
Mungu ni mwamuzi mwenye haki,
Naam, Mungu aghadhibikaye kila siku. (K)


SHANGILIO
Lk. 15:18

Nitaondoka, nitakwenda kwa baba yangu na kumwambia: Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako.


INJILI
Yn. 7:40-52

Wengine katika mkutano walipoyasikia maneno ya Yesu, walisema, Hakika huyu ndiye nabii yule. Wengine walisema, Huyu ndiye Kristo. Wengine wakasema, Je! Kristo atoka Galilaya? Andiko halikusema ya kwamba Kristo atoka katika uzao wa Daudi, na kutoka Bethlehemu, mji ule alioukaa Daudi? Basi kukaingia matengano katika mkutano kwa ajili yake. Baadhi yao wakataka kumkamata, alkini hakuna mtu aliyenyosha mikono yake ili kumshika.

Basi wale watumishi wakawaendea wakuu wa makuhani na Mafarisayo. Nao wakawaambia, Mbona hamkumleta? Wale watumishi wakajibu, Hajanena kamwe mtu yeyote kama huyu anavyonena. Basi Mafarisayo wakawajibu, Je! Ninyi nanyi mmedanganyika? Ni nani katika wakuu amwaminiye, au katika Mafarisayo? Lakini makutano hawa wasioifahamu torati wamelaaniwa.

Akawaambia Nikodemo, (naye ni yule aliyemwendea zamani, maana ni mmoja wao), Je! Torati yetu humhukumu mtu kabla ya kumsikia kwanza, na kujua atendavyo? Wakajibu, wakamwambia, Je! Wewe nawe umetoka Galilaya! Tafuta, ukaone ya kuwa kutoka Galilaya hakutokea nabii.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUWEKWA MAJARIBUNI



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Kwaresima
Ijumaa, Machi, 20, 2026, 
Juma la 4 la Kwaresima

Hek 2: 1, 12-22;
Zab 34: 17-21, 23;
Yn 7: 1-2, 10, 25-30.


KUWEKWA MAJARIBUNI

Kitabu cha Hekima kina kadiriwa kuandikwa miaka mia kabla ya kuja Kristo. Lakini cha kushangaza maelezo yake yanaonekana kuwa karibu sana katika kumwelezea Yesu. Somo la leo linaongelea kuhusu mtu ambaye anamjua Mungu na hata anajiita “Mtumishi wa Mungu” (Hek 2:3). Na kama Yesu, huyu mtu ana adui ambao wanamfuatilia ili kumtega katika maneno yake na hata kutaka kumua. (2:19-20).

Leo tunakumbushwa kwamba kutakuwa na upinzani daima juu ya Kristo na wale wanao mfuata. Katika somo la Injili, tunasoma, juu ya kushindwa kwa jaribio la kumkamata Yesu wakati wa sikukuu ya Tabernaklo kwasababu “saa yake bado” (Yn 7:30). Ni kweli, Yesu alisulubiwa na kufa, lakini kifo hakikuweza kumweka chini. Mungu alimfufua! Ndivyo hivyo sisi Mungu hataruhusu kitu tunacho vumilia kituangushe bila kutusaidia. Atatuimarisha. Atatupa neema. Atatuinua tena. 

Yesu anatuita sisi tuwe mabalozi wake. Anatutaka sisi tushirikishe habari njema kwa kila mtu tunae kutana naye. Huu ndio wito wa pekee, lakini pia kuna changamoto zake. Pengine juhudi zetu zitafanikiwa baada ya kupata upinzani mkubwa na majaribu makubwa, na hata changamoto nyingine ni za kusukumwa. Lakini tukibaki imara katika kushirikisha Injili kwa upendo na sio kwa kujiona wema wenyewe, kwa furaha na sio hasira, tutabarikiwa sana. Yesu atatuambia “vyema mtumwa mwema ingia katika furaha ya Bwana wako” (Mt 25:21). Hauhitaji kuwa mtu uliye bobea katika kuongea au kuwa mashuhuri katika kuongea. Wala haupaswi kuwa na nguvu labda nyingine. Tunapaswa kutambua tu Yesu anatupa nguvu na neema tunapo amua kumshuhudia. Na neema yake itatutunza kama ilivyo na nguvu ya kuwavuta watu kwake. 

Sala: Bwana, nakupenda. Nisaidie nikuone na kukupenda wewe katika jirani zangu. Nisaidie ninapo wekwa katika majaribu, na familia yangu, marafiki zangu, na wengine wanao nipinga kwasababu ya kukutangaza wewe na thamani ya Injili yako. Tufariji daima tunapo tangaza Injili yako. Tupe nguvu yako ya Kimungu. Yesu nakuamini wewe. Amina 

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MACHI 20, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 20, 2026
IJUMAA: JUMA LA 4 LA KWARESIMA

SOMO 1
Hek. 2:1, 12-22

Wasiomsadikia Mungu walisema hivi, huku wakimfikiri yasiyo kweli, Zaidi ya hayo na tumwotee mtu wa haki, maana hatuna haja naye, naye yu kinyume cha matendo yetu; atukaripia ya kama tumeiasi torati, na kutushitaki ya kama tumekosa adabu. Asema ya kwamba anamjua Mungu, na kujiita mtumishi wa Bwana. Ametuwia magombezi ya fikira zetu. Hata kumtazama twaona ni kugumu; maan amaisha yake si sawasawa na masiha ya wengine, na mwenendo wake ni wa kigeni. Tuanhesabiwa naye kuwa kama madini hafifu; anajitenga na njia zetu kama na uchafu. Wenye haki asema kuwa mwisho wao ni heri; hujivuna ya kwamba Mungu ndiye baba yake.

Haya na tuone kama maneno yake ni kweli; tufanye kujaribu yatakayompata wakati wa mwisho wake; mradi mwenye haki akiwa ni mwana wa Mungu, Yeye atamtegemeza na kumwokoa mikononi mwa adui zake. Na tumhakikishe kwa jeuri na maumivu, ili tujifunze upole wake na kuithibitisha saburi yake akidhulumiwa. Hata tumhukumu auawe mauti ya aibu, maana ataangaliwa sawasawa na maneno yake.

Ndivyo walivyosemezana, wakakosea kabisa. Kwa maana uovu wao uliwapofusha; hawakuzijua siri za Mungu; wala hawakuutarajia mshahara wa utakatifu, wala kudhani ya kwamba iko thawabu kwao wenye roho zisizo na hatia.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 34:16-20, 22 (K) 18

(K) Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo.

Uso wa Bwan ani juu ya watenda mabaya,
Aliondoe kumbukumbu lao duniani.
Walilia, naye Bwan akasikia,
Akawaponya na taabu zao zoe. (K)

Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo, 
Na waliopondeka roho huwaokoa.
Mateso ya mwenye haki ni mengi,
Lakini Bwana humponya nayo yote. (K)

Huihifadhi mifupa yake yote,
Haukuvunjika hata mmoja.
Bwana huzikombo a nafsi za watumishi wake,
Wala hawatahukumiwa wote wamkimbiliao. (K)


SHANGILIO
Lk. 8:15
Heri wale walishikao neno la Mungu katika moyo wao mwema na mnyofu, na wazaao matunda katika uvumilivu.


INJILI
Yn. 7:1-2, 25-30

Baada ya hayo Yesu alikuwa akitembea katika Galilaya; maana hakutaka kutembea katika Uyahudi, kwa sababu Wayahudi walikuw awakitafuta kumwua.

Na sikukuu ya Wayahudi, Sikukuu ya Vibanda, ilikuwa karibu. Hata ndugu zake walipokwisha kukwea kuiendea sikukuu, ndipo yeye naye laipokwea, si kwa wazi bali kana kwamba kwa siri.
Basi baadhi ya watu wa yerusalemu wakasema, Je! Huyu siye wanayemtafuta ili wamwue? Na kumbe! Anena waziwazi, wala hawamwambii neno! Yamkini hao wakuu tuna jua hakika ya kuwa huyu ndiye Kristo? Lakini huyu twamjua atokako; bali Kristo atakapokuja hakuna ajuaye atokako.

Basi Yesu akapaza sauti yake hekaluni, akifundisha na kusema, Mimi mnanijua, na huko nitokako mnakujua; wala sikuja kwa nafsi yangu; ila yeye aliyenipeleka ni wa kweli, msiyemjua ninyi. Mimi namjua, kwa kuwa nimetoka kwake, naye ndiye aliyenituma.

Basi wakatafuta kumkamata; lakini hakuna mtu aliyeunyosha mkono wake ili kumshika, kwa sababu saa yake ilikuwa haijaja bado.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.