Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

KUTOKA MAJIVU MPAKA KWENYE UTUKUFU!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Kwaresima 
Jumatano, Februari 18, 2026, 

Jumatano ya majivu (Siku ya kufunga na kujinyima) 

Yoel 2: 2-18; 
Zab 51: 3-17; 
2 Kor 5:20 – 6:2
Mt 6: 1-6, 16-18


KUTOKA MAJIVU MPAKA KWENYE UTUKUFU!

Leo tumeanza kipindi cha neema cha Kwaresima, na tunaitwa kusali, kutolea sadaka na matendo ya huruma. Tukiwa tunatafakari kipindi hichi, tukiangalia mbele katika kuadhimisha mateso, kifo na ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo. Maisha ya toba na kuongoka ndio maada kuu ya Kwaresima. 

Katika somo la kwanza ujumbe wa wongovu umetengenezwa na maneno haya “mrudieni Mungu kwa mioyo yenu yote” (Yoel 2:12). Kwa Yoeli, kuongoka ni njia ya kurudi nyuma. Wale wote waliojiweka katika njia isio sawa wanaitwa kurudi nyuma. Katika somo la pili Paulo anaongelea kuhusu upatanisho. Anasema “tunaomba Mungu awapatanishe” upatanisho na Mungu unapatikana kwa kuishi ujumbe unaoletwa kwetu na wajumbe wa Mungu-wajumbe waneno lake (Warumi 10:14, 17).

Katika somo la Injili Yesu anaongelea mara saba tuzo ambalo wanalipokea wale wanaotenda kadiri ya mafundisho yake. Injili mara nyingi inaelezea kuhusu ‘tuzo’ walilowekewa wenye haki na ‘adhabu’ kwa walio waovu. Tuzo analo liongelea Yesu, sio kuwa na sehemu nzuri ya juu mbinguni bali , kuongezeka mapendo, hali ya muunganiko wa ndani, na hali ya kufanana na uso wa Baba wa mbinguni. ‘Tuzo’ ni furaha ya upendo wa hali ya juu, kama Mungu anavyofanya, ni hali ya “kuwepo katika ufalme wake”. Kukuwa katika hali hii ya juu, katika mwanzo wa kwaresima Yesu anatualika tufanye mambo matatu: kutolea sadaka, sala na kufunga. Hizi zinajenga nguzo tatu za kiroho za Wayahudi, na yeye anaziweka tena lakini katika hali yake ya kipekee. 

Sadaka: katika kipindi cha Yesu, baadhi ya watu walikuwa wana jukumu la kukusanya na kugawa sadaka kwa maskini, yatima, wajane na wasio jiweza. Wakati wa Sabato, kulikuwa na tabia ya kuwasifia wale waliotoa nyingi na walitangazwa mbele ya mikusanyiko. Kwa Yesu, kutoa sadaka sio kuweka hela kidogo, bali kuwa na haki, ni kutambua kuwa vitu vyote vya dunia sio vyetu ni vya Mungu. Kil aliyechukuwa zaidi anapaswa kurudisha kwa wale wasio nacho. Mt. Ambrose, aliwaambia matajiri “kumbuka kwamba, hamuwapi maskini kilicho chenu; bali mnawapa tu kile kilicho mali yao” 

Sala: wakati wa kipindi cha Yesu kulikuwa na aina mbili za sala: sala ya pamoja na sala binafsi. Sala za pamoja, zilifanywa hekaluni, katika masinagogi na katika mitaa, mara mbili kwa siku. Yesu hakatazi matendo haya. Yeye anaelekeza macho yake zaidi kwenye sala ya binafsi, ambayo inafanywa na mtu mwenyewe, milango imefungwa katika hali ya muunganiko wa ndani na Baba “anaye ona vyote”. Sala hii sio marudio ya fomula mbali mbali, bali ni mazungumzo na Mungu, nikumwomba asikilize mapenzi yetu na kutimiza ndoto zetu, lakini pia kuishi mapenzi yake na kupokea kutoka kwake majukumu aliotupangia ya kujenga ufalme wake. Sala, kwanza kabla ya yote ni kusikiliza, kufungua mioyo yetu na kukaribisha mipango ya Mungu na bila kukiuka matazamio yake. 

Kufunga: katika kipindi cha Yesu, waliamini kwamba kufunga kwa kweli ilileta baraka kubwa sana: ilisaidia kuacha dhambi, na kumfanya Bwana aone huruma, kuepuka adhabu yake, na kukinga na mabaya yote. Kufunga kwa Mkristo haihitaji kutambulika. Wanaosha nyuso zao na kuonekana wenye furaha, ana furaha kwasababu kwa kujinyima kwake anamuona maskini akifurahia kutumia ulichompa. Kufunga kuliko kubalika na Mungu ni “kuvunja  aina zote za ukosefu wa haki….funga kwa kushirikisha mkate wako na wale walio na njaa, walete katika nyumba yako wasio na nyumbani, wavalishe wale walio uchi” (Isa 58:6-7). “kuweni wakarimu kati yenu …msiweke maovu juu ya mwingine ndani ya moyo yenu” (Zek 7:5-10).

Katika mwanzo wa kwaresima tunakumbushwa kwamba Kwaresima inaanza na majivu na kuishia na moto, moto wa pasaka wa ufufuko na moto wa Roho Mtakatifu wakati wa Pentekoste, uhakika wa jinsi tutakavyo kuwa. Yesu amezamisha uwepo wetu ambao ni vumbi na majivu katika damu yake, na kutuwezesha kufufuka katika maisha mapya. Roho Mtakatifu anatufanya viumbe vipya. 
Sala: Bwana, ninaomba kwaresima hii iwe yenye matunda katika maisha yangu. Ninaomba kiwe kipindi cha neema cha kukumbatia yote unayotaka niyafanye ndani yangu. Yesu, nakuamini wewe. Amina 


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 18, 2026


MASOMO YA MISA, FEBRUARI 18, 2026
KIPINDI CHA KWARESIMA
JUMATANO YA MAJIVU


SOMO 1
Yoe. 2:12-18

Lakini hata sasa, asema Bwana, nirudieni mimi kwa mioyo yenu yote, na kwa kufunga, na kwa kulia, na kwa kuombolea; rarueni mioyo yenu, wala si mavazi yenu, mkamrudie Bwana, Mungu wenu; kwa maana yeye ndiye mwenye neema, amejaa huruma; si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema, naye hughairi mabaya. N’nani ajuaye kwamba hatarudi na kugeuka, na kutuachia Baraka nyuma yake, naam, sadaka ya unga, na sadaka ya kinywaji, kwa Bwana, Mungu wenu?

Pigeni tarumbeta katika Sayuni, takaseni saumu, kusanyeni kusanyiko kuu; kusanyeni watu, litakaseni kusanyiko, kusanyeni wazee, kusanyeni watoto, na hao wanyonyao maziwa; bwana arusi na toke chumbani mwake, na bibi arusi katika hema yake.

Hao makuhani, wahudumu wa Bwana, na walie kati ya patakatifu na madhabahu, na waseme, Uwaachilie watu wako, Ee Bwana, wala usiutoe urithi wako upate aibu, hata mataifa watawale juu yao; kwani waseme kati ya watu, Yuko wapi Mungu wao?

Hapo ndipo Bwana alipoona wivu kwa ajili ya nchi yake, akawahurumia watu wake.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 51:1-4, 10-12, 15 (K) 1

(K) Uturehemu, Ee Bwana, kwa kuwa tumetenda dhambi.

Ee Mungu, nirehemu, 
Sawasawa na fadhili zako.
Kiasi cha wingi wa rehema zako,
Uyafute makosa yangu.
Unioshe kabisa na uovu wangu,
Unitakase dhambi zangu. (K)

Maana nimejua mimi makosa yangu,
Na dhambi yangu I mbele yangu daima.
Nimekutenda dhambi Wewe peke yako,
Na kufanya maovu mbele za macho yako. (K)

Ee Mungu, uniumbie moyo safi, 
Uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu
Usinitenge na uso wako,
Wala roho yako mtakatifu usiniondolee. (K)

Unirudishie furaha ya wokovu wako;
Unitegemeze kwa roho ya wepesi.
Ee Bwana, uifumbue midomo yangu,
Na kinywa change kitazinena sifa zako. (K)


SOMO 2
2 Kor. 5:20 – 6:2

Ndugu zangu, basi tu wajumbe kwa ajili ya Kristo, kana kwamba Mungu anasihi kwa vinywa vyetu; twawaomba ninyi kwa ajili ya Kristo mpatanishwe na Mungu. Yeye asiyejua dhambi alimfanya kuwa dhambi kwa ajili yetu, ili sisi tupate kuwa haki ya Mungu katika Yeye.

Nasi tukitenda kazi pamoja naye twawasihi msiipokee neema ya Mungu bure. Kwa maana asema, Wakati uliokubalika nalikusikia, Siku ya wokovu nilikusaidia; tazama, wakati uliokubalika ndio sasa; tazama, siku ya wokovu ndiyo sasa.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


SHANGILIO
Zab. 95:8

Msifanye migumu mioyo yenu; msikie sauti ya Bwana.


INJILI
Mt. 6:1-6, 16-18

Angalieni msifanye wema wenu machoni pa watu, kusudi mtazamwe na wao; kwa maana mkifanya kama hayo, hampatai thawabu kwa Baba yenu aliye mbinguni. Basi wewe utoapo sadaka, usipige panda mbele yako, kama wanafiki wafanyavyo katika masinagogi na njiani, ili watukuzwe na watu. Amini, nawaambieni, Wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe utoapo sadaka, hata mkono wako wa kushoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume; sadaka yako iwe kwa siri; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.

Tena msalipo, msiwe kama wanafiki; kwa maana wao wapenda kusali hali wamesimama katika masinagogi na katika pembe za njia, ili waonekane na watu. Amini, nawaambia, Wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani, na ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.

Tena mfungapo, msiwe kama wanafiki wenye uso wa kukunjamana; maana hujiumbua nyuso zao, ili waonekane na watu kuwa nafunga, Amin, nawaambia, Wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe ufungapo, jipake mafuta kichwani, unawe uso; ili usionekane na watu kuwa unafunga, ila na Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

CHACHU ULIMWENGUNI!


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumanne, Februari 17, 2026, 
Juma la 6 la Mwaka wa Kanisa

Yak 1:12-18
Zab 94:12-15.18-19;
Mk 8: 14-21.


CHACHU ULIMWENGUNI!


Kila anaye andaa mkate anatambua jinsi ya chachu kidogo (Amira) inavyo fanya kazi ndani ya donge la unga. Ukiweka kidogo tu ina umusha unga wote. Na yote hii inatokana tu na hii chachu kidogo tu. Kwahiyo ni nini hii chachu ya Mafarisayo na Herode? Ni maneno mabaya, maovu tena yenye makosa wanayo eneza. Kwa Mafarisayo, inaweza kuwa ni kushindwa kumwelewa Yesu alivyokuwa akifanya na kusema. Waliweza hata kubadilisha maneno yake kidogo tu na kuelezea kwa wengine katika maana tofauti. Hii ni mbaya sana na ilikuwa na madhara kwa kila mtu kwa wakati ule na baadae. Kidogo kidogo mbegu hiyo ndogo ya wasi wasi ingekuwa na kuenea kwa wengine. 

Tunawaza kufikiria juu ya yote hayo, tukafahamu pia watu wanaofanya hivyo kwa wakati wetu. Lakini tunaweza kukosea kama hatujaanza kujiangalia sisi wenyewe kwanza. Je, ninafanya haya wakati mwingine? Je, nimejikuta nikipindisha ukweli kwa kutengeneza maneno ambayo huleta maana tofauti na jinsi mtu alivyosema? Je, ninawaongoza wengine kwa maneno ya uongo wakati naufahamu ukweli? Tunapaswa tuangalie maneno yetu na kutambua uzito uliopo katika maneno hayo. Maneno machache yaweza kuleta madhara makubwa kwa kipindi kikubwa. Ni vizuri kuwa na hali ya kupenda ukweli kwani kujaribu kupindisha ukweli huleta madhara makubwa daima. 

Lakini pia sio hilo tu tunalopaswa kufanya. Tunapaswa kutambua pia neno dogo la upendo tunalosema limejaa utajiri mwingi ambao huweza kuleta mema na neema kwa muda wote. Pengine ni tabasamu tu dogo tunalo onesha au kitendo cha ukarimu ambacho tunadhani kinajiondokea tu bila kutambulika. Hili tabasamu dogo na ukarimu mdogo ni chachu ya Injili. Inaleta tofauti na kuleta chachu njema pia. Tutafakari juu ya mambo madogo tunayofanya katika maisha yetu. Tutambue kuwa labda iwe dhambi ndogo inaleta madhara makubwa , au kiwe kitendo kidogo cha upendo kinaleta Baraka kubwa mwishoni. 
Sala: Bwana, nisaidie niweze kuwa mwaminifu na nisaidie niweze kutamua ni chachu ghani ninayo ileta katika maisha ya kila siku. Nisaidie niweze kujitenga na mabaya na unijaze mema. Nisaidie niweze kuwa chachu njema katika yote ninayo sema nakutenda kila siku. Yesu nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 17, 2026



MASOMO YA MISA, FEBRUARI 17, 2026
JUMANNE, JUMA LA 6 LA MWAKA WA KANISA


SOMO 1
Yak. 1:12-18

Heri mtu astahimiliye majaribu; kwa sababu akiisha kukubaliwa ataipokea taji ya uzima, Bwana aliyowaahidia wampendao.

Mtu ajaribiwapo, asiseme, Ninajaribiwa na Mungu; maana Mungu hawezi kujaribiwa na maovu, mmoja hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe huku akivutwa na kudanganywa. Halafu ile tamaa ikiisha kuchukua mimba huzaa dhambi, na ile dhambi ikiisha kukomaa huzaa mauti.

Ndugu zangu wapenzi, msidanganyike. Kila kutoa kuliko kwema, na kila kitolewacho kilicho kamili, hutoka juu, hushuka kwa Baba wa mianga; kwake hakuna kubadilika, wala kivuli cha kugeukageuka. Kwa kupenda kwake mwenyewe alituzaa sisi kwa neno la kweli, tuwe kama limbuko la viumbe vyake.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 94:12-15, 18-19 (K) 12

(K) Ee Bwana, heri mtu yule uliyemfundisha.

Ee Bwana, heri mtu yule 
umwadhibuye na kumfundisha,
Kwa sheria yako;
Mpate kumstarehesha siku ya mabaya. (K)

Kwa kuwa Bwana hatawatupa watu wake,
Wala hutauacha urithi wake,
Maana hukumu itairejea haki,
Na wote walio wanyofu wa moyo wataifuata. (K)

Niliposema, mguu wangu unateleza;
Ee Bwana, fadhili zako zilinitegemeza.
Katika wingi wa mawazo ya moyoni mwangu,
Faraja zako zaifurahisha roho yangu. (K)


SHANGILIO
Yn. 14:23

Aleluya, aleluya,
Mtu akinipenda, atalishika neno langu, 
na baba yangu atampenda, nasi tutakuja kwake.
Aleluya.


INJILI
Mk. 8:14 – 21

Wafuasi wake Yesu walisahau kuchukua mikate, wala chomboni hawana ila mkate mmoja tu. Akawaagiza, akasema, Angalieni, jihadharini na chachu ya Mafarisayo na chachu ya Herode. Wakabishana wao kwa wao, kwa kuwa hawana mikate.

Naye Yesu akatambua, akawaambia, Mbona mnabishana kwa sababu hamna mikate? Hamfahamu bado, wala hamjaelewa? Je! Mioyo yenu ni mizito? Mna macho, hamwoni; mna masikio, hamsikii? Wala hamkumbuki? Nilipoivunja ile mikate mitano na kuwapa wale elfu tano, mlichukua vikapu vingapi vimejaa vipande? Wakamwambia, Kumi na viwili. Na ile saba kuwapa wale elfu nne, mlichukua makanda mangapi yamejaa vipande? Wakamwambia, Saba. Akawaambia, Hamjafahamu bado?

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MIUJIZA KUTOKA MBINGUNI!



ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatatu, Februari 16, 2026
Juma la 6 la Mwaka wa Kanisa
 
Yak 1:1-11;
Zab 119: 67-68.71.75-76;
Mk 8: 11-13

 
MIUJIZA KUTOKA MBINGUNI!

 
Karibuni ndugu zangu kwa adhimisho la Misa Takatifu asubuhi ya leo. Leo neno la Bwana katika asubuhi ya leo tunaanza kwa kuliangalia somo la kwanza toka katika kitabu cha Yakobo. Hiki ni kitabu kilichoandikwa kutoa muongozo kwa jamii ya Wakristo wa mwanzo hasa juu ya fundisho la kuhusu neema na matendo ya sheria kwa kanisa ambalo lilikuwa katika hatua zake za uchanga na lilikuwa likisumbuliwa na madhulumu toka kwa maadui wa nje na pia lilikuwa likijitahidi kuyapatia msingi mafundisho yake makuu.

Katika sehemu tunayoisikia leo, Yakobo anatambua mateso ya hawa Wakristo na majaribu waliyokuwa wanayapata na pia juu ya changamoto kama za umaskini walizokuwa wanazipata. Wakristo hawa walikuwa wakiishi kama jumuiya ndogo kati ya wengi waliokuwa wapagani. Changamoto waliyoipata Wakristo ni kwamba walitengwa kwa sababu ya dini yao. Hawakupata wa kuwapatia ajira, walinyanganywa ardhi yao na walikosa wa kuwatetea. Hivyo, walikumbwa na jaribu la kutaka kuacha dini yao ili nao wapate ajira. Hivyo, Yakobo anawaandikia akisema kwamba hayo ni majaribu tu. Wasikubali yawafanye wakate tamaa. Yasiwafanye waache ukristo ili waajiriwe, wavumilie, ni majaribu tu, ni mapito tu, yote haya yanamwisho wake. Yanakujaga maishani na kupita tu lakini hadi yapite lazima uwe imara ili yasikusombe. Wawe na hekima kutambua kwamba vitu vya dunia na utajiri wake vinakwisha.

Ndugu zangu, fundisho hili la Yakobo ni la uhalisia mkubwa kwa sababu hadi leo changamoto hasa za umaskini ni sababu ya watu kukubali kumtumikia shetani. Tupo tayari kufanya matendo ya ushetani kwa sababu tunaogopa umaskini. Tunaona mali zikiisha, matajiri wakubwa wanakwenda na kuwaachia wengine mali zao ambao hata hawakuwasaidia kufanya kazi au hata mali zao zinaishia kuibwa na wengine tu ambao hata hawakuwasaidia kufanya kazi. Hayo yote tunaona. Lakini umwambie mtu ati awe na hekima asitegemee pesa-weee? Hakuelewi. Nitakusikiliza sasa hivi lakini baada ya dakika tano nikiona changamoto kidogo tu ya fedha basi nitakuwa tayari kufanya hata tendo la uovu.

Yakobo anasisitiza leo tuwe na hekima. Yanayotokea kwa wenzetu, jinsi mali zinavyoshindwa kumfikisha mtu popote yatufanye tuwe na hekima zaidi.

Katika somo la injili tumesikia Yesu akikataa kutoa ishara kwa mafarisayo kwa sababu alijua kwamba walikuwa wanamjaribu na kumchezea chezea tu na hata angeitoa wasingeweza kumwamini. Ni hivyo hivyo na kwetu sisi ndugu zangu. Yesu anatoa ishara kila siku. Yanayotokea kwa mwenzako ni ishara tu. Wapo wengi walioshindwa kuvumilia majaribu yaletwayo na changamoto mbalimbali kama umaskini. Wakaishia kutumia njia za uovu kama wizi, kudhulumu mali za wengine, kudhulumu mirathi ya mayatima, kugushi vyeti na kuiba mali za watu lakini sasa wako wapi? Mali imewafikisha wapi?. Iwe ishara kwetu-ya kuijenga Imani yetu. Tusipoyaona haya kama ishara ya kujenga Imani yetu, basi tusitegemee ya ziada. Haya ndio ya mwisho.
 
Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 16, 2026


 

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 16, 2026
JUMATATU YA JUMA LA 6 LA MWAKA

SOMO 1
Yak. 1:1-11

Yakobo, mtumwa wa Mungu, na Bwana Yesu Kristo, kwa kabila kumi na mbili waliotawanyika; salamu.Ndugu zangu, hesmbali; mkifahamu ya kuwa kujaribiwa kwa imani yenu huleta saburi. Saburi na iwe na kazi kamilifu, mpate kuwa wakamilifu na watimilifu bila kupungukiwa na neno.Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote k
abuni ya kuwa ni furaha tupu, mkiangukia katika majaribu mbaliwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa. Ila na aombe kwa imani, pasipo shaka yoyote; maana mwenye shaka ni kama wimbi la bahari lillilochukuliwa na upepo, na kupeperushwa huku na huku. Maana mtu kama yule asidhani ya kuwa atapokea kitu kwa Bwana. Mtu wa nia mbili husitasita katika njia zake zote. Lakini ndugu asiye na cheo na afurahi kwa kuwa ametukuzwa; bali tajiri kwa kuwa ameshushwa; kwa maana kama ua la majani atatoweka. Maana jua huchomoza kwa hari, huyakausha majani; ua lake huanguka, uzuri wa umbo lake hupotea; vivyo hivyo naye tajiri atanyauka katika njia zake.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 119:67, 68, 71, 72, 75, 76 (K) 77

(K) Rehema zako, ee Bwana, zinijie nipate kuishi.

Kabla sijateswa mimi nalipotea,
Lakini sasa nimelitii neno lako.
Wewe U mwema na mtenda mema,
Unifundishe amri zako. (K)

Ilikuwa vema kwangu kuwa naliteswa,
Nipate kujifunza amri zako.
Sheria ya kinywa chako ni njema kwangu,
Kuliko maelfu ya dhahabu na fedha. (K)

Najua ya kuwa hukumu zako ni za haki,
Ee Bwana, na kwa uaminifu umenitesa.
Nakuomba, fadhili zako ziwe faraja kwangu,
Sawasawa na ahadi yako kwa mtumishi wako. (K)


SHANGILIO
Yn. 14:6

Aleluya, aleluya,
Bwana asema: Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.
Aleluya.
 
 
INJILI
Mk. 8:11 – 13

Walitokea Mafarisayo, wakaanza kuhojiana na Yesu; wakitafuta kwake ishara itokayo mbinguni; wakimjaribu. Akaugua rohoni mwake, akasema, Mbona kizazi hiki chatafuta ishara? Amin, nawaambieni, Hakitapewa ishara kizazi hiki. Akawaacha akapanda tena chomboni, akaenda zake hata ng’ambo.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.
 
Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUSHIKA SHERIA!



“MBEGU ZA UZIMA”
Tafakari ya kila Jumapili
Jumapili, Februari 15, 2026
Dominika ya 6 ya Mwaka A wa Kanisa

YbS 15:16-21;
Zab 118:1-2, 4-5, 17-18, 33-34;
1Kor 2:6-10;
Mt 5:17-37


KUSHIKA SHERIA!


Mungu anatuita sio katika maisha ya maadili tu, lakini katika hali ya kuishi ya juu zaidi. Tunatembea kuelekea ukamilifu kwa kujitahidi daima kuchagua kufanya mazuri. Katika hali ya asili sisi sio wakamilifu, lakini Mungu anatuita tutafakari jinsi tunavyo ishi na kutambua ni kipi kimeenda vibaya na kipi kimeenda vizuri. Kwa kutafakari maisha yetu kwa kupitia njia ya Imani maisha yetu yanakuwa katika hekima. Yesu anatufundisha dini ambayo itatufanya ikuwa ndani yetu na kuwa sehemu ya maisha yetu.

Somo la kwanza linatualika tufanye kila jitihada ya kufanya uchaguzi sahihi katika maisha. Yoshua bin Sira anatangaza kwamba amri za Mungu zina nguvu ya kuokoa. Musa aliwaambia watu alivyokuwa karibu na mto Yordani kwamba anawapa nafasi yakuamua: maisha na mafanikio, kifo na maangamizi. Uchaguzi ulikuwa wao kuamua. Yoshua bin Sira sasa anawaambia watu, akisisitiza ujumbe ule wa Musa kwamba Mungu ameweka mbele yao moto na maji, maisha na kifo, mema na mabaya. Wanatusukuma nasi tufanye uchaguzi sahihi kwa kusema kwamba macho ya Mungu huwaelekea wale wenye kutenda mema. Ni ujumbe mzito kwetu kwamba hatuwezi kufuta mawazo yetu na matendo yetu kutoka kwa Mungu.

Injili ya Mathayo kwa asili iliandikwa kwa ajili ya Wayahudi Wakristu, inaweza kuonekana kama maneno ya kufariji kwao. Mathayo daima amekuwa akirejea Agano la Kale kuwaonesha kuwa maisha ya Yesu hajaja kuvunja sheria za zamani za Wayahudi bali ni mwendelezo wa yote ambayo yalitabiriwa na manabii hapo zamani. Maisha na mafundisho ya Yesu hayapaswi kuonekana kama ni dini mpya, maisha ya Yesu ni maisha ya asili ya habari ya Ukombozi. Anawahakikishia wasomaji wake kwamba Yesu hakuja kutengua Sheria bali amekuja kuikamilisha. Kwa hiyo, sheria bado ina nafasi yake na hivyo haitatupwa mbali hadi pale itakapo timiza jukumu lake. Kwasababu kwa Yesu, maana halisi ya sheria inaweza kufupishwa kwa neno moja “heshima”. Heshima kwa Mungu, kwa jina lake, kwa siku yake, heshima kwa wazazi, heshima kwa uhai, utu, heshima kwa ukweli na heshima kwa jina la mtu na hatimaye heshima kwa nafsi. Kwa maneno mengine sheria yote inahitimishwa kwa ‘heshima kwa Mungu’ na ‘heshima kwa nafsi” na jirani. Kwasababu heshima hii haijalimbikizwa katika visheria vidogo na miiko bali imejibeba katika amri ya mapendo: Upendo kwa Mungu na upendo kwa jirani. Yesu hakutambulisha sheria mpya bali alitambulisha njia mpya yakufikiria na kuelewa sheria. Hakutengua sheria wala kubadili bali alienda mbele zaidi ya kile kinacho hitaji. Kwasababu kwa Yesu, hali ya nje tu ya kushika sheria haitoshi. Kuwa mfuasi wa Yesu ni vizuri kutambua sheria iliojengwa katika mapendo. Kushika sheria bila mapendo ni sawa na kuwa na mwili bila roho. Ndio maana anawaambia wafuasi wake kwamba fadhila zao zisipo zidi zile za Mafarisayo na Waandishi, hawataingia katika Ufalme wa Mungu.

Ili kuwafanya wafuasi wake waelewe mafundisho yake, Yesu aliwapa mifano sita mizito na katika injili ya leo tuna minne, tuna kuhusu: hasira, uasherati, talaka na kiapo. Anasema wazi kwamba haitoshi tu kushika ambacho sheria inatuambia bila kutenda fadhila zinazo ambatana nazo. Kwa Yesu, hakuwezi kuwa na utengano kati ya uhusiano wetu na Mungu na watu. Mkristo anapaswa kumpata Mungu kwa watu wote na katika uumbaji.

Sala: Bwana, nifanye niwe safi moyoni. Nifanye niweze kuwa mtu mwaminifu na mwenye kujali utu. Ninaomba ukweli ulio uweka ndani ya moyo wangu uweze kuwa msingi wa matendo yangu na maneno yangu. Ninaomba niongee nikiwa na dhamiri safi kila wakati nikiongea ulichonipa niongee. Yesu, nakumini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 15, 2026



MASOMO YA MISA, FEBRUARI 15, 2026
DOMINIKA YA 6 YA MWAKA A


WIMBO WA MWANZO:
Zab. 31:2 – 4
Uwe kwangu mwamba wa nguvu, nyumba yenye maboma ya kuniokoa. Ndiwe genge langu na ngome yangu; kwa ajili ya jina lako uniongoze, unichunge.



SOMO 1
YbS. 15:15 – 20

Ukipenda utazishika amri zake, na kutenda amini ni shauri lako. Ameweka mbele yako moto na maji; utanyosha mkono wako uchaguavyo. Mbele ya mwanadamu upo uzima na muti, naye atapewa apendavyo. Mradi hekima ya Bwana yatosha, Mkuu mwenye uweza hutazama vyote. Macho yake ni juu yao wamchao, naye atapeleleza kila kazi ya watu. Hakumwamuru mtu yeyote awe asi, wala kumruhusu atende dhambi.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 118:1 – 2, 4 – 5, 17 – 18, 33 – 34 (K) 1

(K) Heri waendao katika sheria ya Bwana.

Heri walio kamili njia zao,
Waendao katika sheria ya Bwana.
Heri wazitiio shuhuda zake,
Wamtafutao kwa moyo wote. (K)

Wewe umetuamuru mausia yako,
Ili sisi tuyatii sana.
Ningependa njia zangu ziwe thabiti,
Nizitii amri zako. (K)

Umtendee mtumishi wako ukarimu,
Nipate kuishi, nami italitii neno lako.
Unifumbue macho yangu niyatazame
Maajabu yatokayo katika sheria yako. (K)

Ee Bwana, unifundishe njia ya amri zako,
Nami nitaishika hata mwisho.
Unifahamishe nami nitaishika sheria yako,
Naam, nitaitii kwa moyo wangu wote. (K)



SOMO 2
1Kor. 2:6 – 10

Iko hekima tusemayo kati ya wakamilifu; ila si hekima ya dunia hii, wala ya hao wanaoitawala dunia hii, wanaobatilika; bali twanena hekima ya Mungu katika siri, ile hekima iliyofichwa, ambayo Mungu aliiazimu tangu milele, kwa utukufu wetu; ambayo wenye kuitawala dunia hii hawaijui hata mmoja; maana kama wangaliijua, wasingalimsulibisha Bwana wa utukufu; lakini, kama ilivyoandikwa, Mambo ambayo jicho halikuyaona wala sikio halikuyasikia, (Wala hayakuingia katika moyo wa mwanadamu).

Mambo ambayo Mungu aliwaandalia wampendao. Lakini Mungu ametufunulia sisi kwa Roho. Maana Roho huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu.



SHANGILIO
Yn. 14:6

Aleluya, aleluya.
Mimi ndimi Njia, na Ukweli, na Uzima, asema Bwana; Mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.
Aleluya.



INJILI
Mt. 5:17:37

Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza. Kwa maana, amin, nawaambia, Mpaka mbingu na nchi zitakapoondoka, yodi moja wala nukata moja ya torati haitaondoka, hata yote yatimie. Basi mtu yeyote atakayevunja amri moja katika hizi zilizo ndogo, na kuwafundisha watu hivyo, ataitwa mdogo kabisa katika ufalme wa mbinguni; bali mtu atakayezitenda na kuzifundisha, huyo ataitwa mkubwa katika ufalme wa mbinguni.

Mwaana nawaaambia ya kwamba, Haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni. Mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, Usiue; na mtu akiua itampasa hukumu. Bali mimi nawaambieni, kila amwonaye ndugu yake hasira itampasa hukumu; na mtu akimfyolea ndugu yake, itampasa baraza; na mtu akimwapiza, itampasa jehanum ya moto. Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, ukapatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako. Patina na mshitaki wako upesi wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije akakupeleka kwa kadhi na kadhi akakupeleka  kwa askari, akatupwa gerezani. Amin, nakuambia, Hutoki humo kamwe hata uishe kulipa senti ya mwisho.
Mmesikia kwamba imenenwa, Usizini; lakini mimi nawaambia, Kila mtu atazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni mwake. Jicho lako la kuume likikukosesha, ling’oe ulitupe mbali nawe; kwa maana yakufaa kiungo chako kimoja kipotee wala mwili wako mzima usitupwe katika jehanum. Na mkono wako wa kuume ukikukosesha, ukate uutupe mbali nawe; kwa maana yakufaa kiungo chako kimoja kipotee, wala mwili wako mzima usitupwe katika jehanum. Imenenwa pia, Mtu akimwacha mkewe, na ampe hati ya talaka; lakini mimi nawaambia, Kila mtu amwachaye mkewe, isipokuwa kwa habari ya uasherati, amfanya kuwa mzinzi; na mtu akimwoa yule aliyeachwa, azini. Tena mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, Usizuru, ila mtimizie Bwana nyapo zako; lakini mimi nawaambia, Usiape kabisa; hata kwa mbingu, kwa maana ndicho kiti cha enzi cha Mungu; wala kwa nchi, kwa maana ndiyo pa kuwekea miguu yake; wala kwa Yerusalemu, kwa maana ndio mji Mfalme mkuu. Wala usiape kwa kichwa chako, maana huwezi kufanya unywele mmoja kuwa mweupe au mweusi. Bali maneno yenu yawe Ndiyo, ndiyo; Siyo, siyo; kwa kuwa yazidiyo hayo yatoka kwa yule mwovu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

JE UNA NJAA YA MUNGU?



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumamosi, Februari 14, 2026, 
Juma la 5 la Mwaka wa Kanisa

Kumbukumbu ya Mt. Skolastika Bikira 

1Fal 12:26-32;13:33-34
Zab 106:6-7.19-22
Mk 8: 1-10.


JE UNA NJAA YA MUNGU?


Sehemu ya Injili inaweza kuonekana katika hali mbali mbali inayo funua huruma ya Yesu. Kulikuwa na mkusanyiko mkubwa ulio wahusianisha Wayahudi pia Wayunani, waume na wake pamoja na watoto. Na wote walikuwa na kitu kimoja tu muhimu. Walikuwa na njaa. Walikuwa na njaa ya mafundisho ya Yesu-ni kitu kipi kingine kinacho weza kuwaweka pamoja namna ile kwa siku tatu? Na kwasababu ya njaa yao ya kiroho, walihisi pia njaa ya kimwili. Je, ulishawahi kuwa na njaa ya Mungu? Ulishawahi kuhisi kutaka kuwa na Mungu zaidi ya kutaka kukaa mahali na kupata mambo mengine ya maisha? 

Umati walikuwa wamevutwa sana na Yesu kiasi kwamba walikaa siku tatu wakiwa naye, wakimsikiliza wakiwa katika jangwa pamoja na kwamba hawakuwa na chakula. Walimchagua Yesu zaidi ya chakula na faraja ya nyumbani kwao. Inaonesha ni kwa jinsi ghani walivyokuwa wamevutwa naye. Hakuna kitu kingine kilichokuwa na thamani, walitaka tu wawe na Yesu. Ujumbe huu pia unaonesha jinsi Yesu alivyo onesha kujali watu. Moyo wake ulijazwa na huruma juu yao. Alifurahi pia kwa uwepo wao lakini pia alijali pia kuhusu usalama wao wa mwili hata kuliko wao wenyewe. Yesu, baada ya kutambua tatizo la watu kuwa bila chakula kwa muda mrefu anawaalika pia Mitume wake watambue tatizo hilo. Pengine, Yesu alitaka mitume waweze kuwa na upendo na kujali watu katika mioyo yao. Pengine, ilikuwa ni wakati ambapo alikuwa akiwajaribu na kuwafundisha wawe wakiwaza kuhusu mahitaji ya watu. Yesu alitaka mioyo yao isukumwe na “huruma kwa ule umati” kama yeye alivyokuwa.  

Tuangalie pia leo: je, Yesu ni kiini cha maisha yako? Je, mioyo yetu inasukumwa na tamaa ya kutaka kuwa naye zaidi ya chochote kile? Je, tunatambua jinsi Yesu anavyo tujali? Je tupo tayari kuruhusu upendo na huruma anayo tupa Yesu, kuipeleka kwa wengine pia? Ni kwa jinsi hii tu twaweza kuitwa wafuasi wake.

Sala: Bwana, nisaidie niweze kuvutwa kwako kwa tamaa kubwa kabisa. Nisaidie niweze kukuona wewe kama kiini na chanzo cha yote ninayo tafuta. Ninaomba nikuchague wewe zaidi ya yote, nikikuamini wewe na kufahamu kwamba wewe ndiye utakaye ridhisha hamu ya moyo wangu. Nikiwa navutwa kwako nisaidie moyo wangu ujazwe na huruma nyingi kwa wote. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 14, 2026



MASOMO YA MISA, FEBRUARI 14, 2026
JUMAMOSI YA WIKI YA 5 YA MWAKA

KUMBUKUMBU YA WAT. CYRILI NA METHODIUS


SOMO 1
1Fal. 12:26-32; 13:33-34


Yeroboamu alisema moyoni mwake: Basi ufalme utairudia nyumba ya Daudi. Kama watu hawa wakipanda kwenda kutoa dhabihu katika nyumba ya Bwana huko Yerusalemu, ndipo mioyo ya watu hawa itamrudia bwana wao, yaani Rehoboamu, mfalme wa Yuda; nao wataniua mimi, na kumrudia Rehoboamu, mfalme wa Yuda.

Kwa hiyo mfalme akafanya shauri, akafanyiza ng’ombe wawili wa dhahabu, akawaambia watu, Ni vigumu kwenu kupanda kwenda Yerusalemu; tazama, hii ndiyo miungu yenu, enyi Israeli, iliyowapandisha kutoka nchi ya Misri. Akamweka mmoja katika Betheli, na wa pili akamweka katika Dani. Jambo hili likawa dhambi, maana watu walikwenda kuabudu mbele ya kila mmoja, hata huko Dani. Tena akafanya nyumba za mahali pa juu, akafanya na watu wowote, watu wasio wa wana wa Lawi, kuwa makuhani.

Yeroboamu akaamuru kushika sikukuu katika mwezi wa nane, siku ya kumi na tano ya mwezi, mfano wa sikukuu iliyokuwa katika Yuda, akapanda juu ili kuiendea madhabahu. Akafanya vivyo katiak Betheli akiwatolea dhabihu wale ng’ombe aliowafanya; akawaweka katika Betheli wale makuhani wa mahali pa juu alipokuwa amepafanya.

Baada ya hayo Yeroboamu hakuiacha njia yake mbovu, lakini akafanya tena makuhani wa mahali pa juu, wa watu wowote. Kila aliyetaka akamfanya wakfu, ili wawepo makuhani wa mahali pa juu. Jambo hilo likawa dhambi kwa nyumba ya Yeroboamu, hata kuiharibu, na kuifuta usoni pa nchi.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 106:6-7, 19-22 (K) 4


(K) Ee Bwana, unikumbuke mimi, kwa kibali uliyonayo kwa watu wako.


Tumetenda dhambi pamoja na baba zetu,
Tumetenda maovu, tumefanya ubaya.
Baba zetu katika Misri
Hawakufikiri matendo yako ya ajabu. (K)


Walifanya ndama huko Horebu,
Wakaisujudia sanamu ya kuyeyuka.
Wakaubadili utukufu wao
Kuwa mfano wa ng’ombe mla majani. (K)


Wakamsahau Mungu mwokozi wao,
Aliyetenda makuu katika Misri:
Matendo makuu katika nchi ya Hamu,
Mambo ya kutisha penye bahari ya Shamu. (K)



SHANGILIO
Mt. 4:4


Aleluya, aleluya,
Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.
Aleluya.



INJILI
Mk. 8:1 – 10


Katika siku zile, kwa vile ulivyokuwa mkuu tena ule mkutano, nao wamekosa kitu cha kula, Yesu aliwaita wanafunzi wake, akawaambia, Nawahurumia mkutano kwa sababu yapata siku tatu wamekaa nami, wala hawana kitu cha kula; nami nikiwaaga waende zao nyumbani kwao hali wanafunga, watazimia njiani; na baadhi yao wametoka mbali. Wanafunzi wake wakamjibu, Je! Ataweza wapi mtu kuwashibisha hawa mikate hapa nyikani? Akawauliza, Mnayo mikate mingapi? Wakasema, Saba.

Akawaagiza mkutano waketi chini; akaitwaa ile mikate saba, akashukuru, akaimega, akawapa wanafunzi wake waaandikie; wakawaaandikia mkutano. Walikuwa na visamaki vichache; akavibariki, akasema wawaandikie na hivyo pia. Wakala, wakashiba, wakakusanya mabaki ya vipande vya mikate makanda saba. Na watu waliokula wapata elfu nne. Akawaaga. Mara akapanda chomboni pamoja na wanafunzi wake, akaenda pande za Dalmanutha.


Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.