Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MATUNDA YENYE KUWAVUTA WATU




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Ijumaa, Mei, 29, 2026 
Juma la 8 la mwaka wa Kanisa

1 Pet 4: 7-13; 
Zab 95: 10-13; 
Mk 11: 11-26


MATUNDA YENYE KUWAVUTA WATU

Yesu alivyo ulaani mtini baada ya kuuona hauna matunda, kitendo hiki kinaweza kuonekana cha ajabu kidogo na cha kutisha. Yesu alijua kabisa ilikuwa sio kipindi cha matunda ya mti ule. Mt. Bede katika maelezo yake akiongelea kuhusu muujiza huu wa Yesu, anatuambia kwamba, muujiza huu wa Yesu ulikuwa na lengo maalumu. Yesu alikuja kati ya watu wake, Wayahudi, akiwa na njaa yakutaka matunda ya utakatifu, wao hawakuupokea ujumbe wake na matunda ya kazi yake. Lakini yote aliyo yakuta ni msisitizo wakushika dini, matendo ya njee yasioendani na kilicho ndani, na katika hali hii wamekuwa kama majani ya miti bila matunda. Wakati alivyo ingia Hekaluni alikuta wamepageuza kuwa pango la biashara. Kitu ambacho kilimfanya hata halitakase kwakutumia nguvu. “Kwahio wewe” anasema Mt. Bede kwakumalizia, “unapaswa ujilinde usiwe kama mti usio zaa matunda, jitoe kwa Yesu, aliyejifanya mwenyewe maskini, anategemea uwe tunda la utakatifu” 

Fadhili zinaongeza furaha ya maisha ya sala na sala inapaswa ionekane katika matendo ya fadhila. Sala ya kweli inapaswa utuongoze taratibu katika mabadiliko ya kweli ya maisha yetu, tukikua katika fadhila na madiliko ya ndani. Vinginevyo tutakuwa kama Wayahudi, mtini uliyo na majani pekee usio zaa matunda.

Sala: Bwana nijaliye neema, ili kwa maisha yangu niweze kutoa matunda mema. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MEI 29, 2026

 



MASOMO YA MISA, MEI 29, 2026
IJUMAA, JUMA LA 8 LA MWAKA

SOMO 1 
1 Pet. 4:7-13

Mwisho wa mambo yote umekaribia; basi iweni na akili, mkeshe katika sala. Zaidi ya yote iweni na juhudi, mkeshe katika sala. Zaidi ya yote iweni na juhudi nyingi katika kupendana; kwa sababu upendano husitiri wingi wa dhambi. Mkaribishane ninyi kwa ninyi, pasipo kunung’unika; kila mmoja kwa kadiri alivyoipokea karama, itumieni kwa kuhudumiana; kama mawakili wema wa neema mbalimbali za Mungu. Mtu akisema, na aseme kama mausia ya Mungu; mtu akihudumu, na ahudumu kwa nguvu anazojaliwa na Mungu; ili Mungu atukuzwe katika mambo yote kwa Yesu Kristo. Utukufu na uweza una yeye hata milele na milele. Amina.

Wapenzi, msione kuwa ni ajabu ule msiba ulio katik yenu, unaowapata kama moto ili kuwajaribu, kana kwamba ni kitu kigeni kiwapatacho. Lakini kama mnavyoyashiriki mateso ya Kristo, furahini; ili na katika ufunuo wa utukufu wake mfurahi kwa shangwe.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 149:1-6,9 (K) 4

(K) Bwana awaridhia watu wake. au: Aleluva.

Mwimbieni Bwana wimbo mpya,
Sifa zake katika kusanyiko la watauwa.
Israeli na amfurahie Yeye aliyemfanya,
Wana wa Sayuni na wamshangilie mfalme wao. (K)

Na walisifu jina lake kwa kucheza,
Kwa matari na kinubi wamwimbie.
Kwa kuwa Bwana awaridhia watu wake, 
Huwapamba wenye upole kwa wokovu. (K)

Watauwa na waushangilie utukufu,
Waimbe kwa sauti kuu vitandani mwao.
Sifa kuu za Mungu na ziwe vinywani mwao,
Hiyo ndiyo heshima ya watauwa wake wote. (K)


SHANGILIO 
Lk. 8 :15

Aleluya, aleluya, 
Wanabarikiwa wale ambao kwa unyofu na wema wa mioyo yao, hulisikia neno la Mungu na kulishika. 
Aleluya.


INJILI 
Mk. 11:11-26

Yesu aliingia Yerusalemu hata ndani ya hekalu; na alipokwisha kutazama yote pande zote, kwa kuwa ni wakati wa jioni, akatoka, akaenda Bethania pamoja na wale Thenashara.

Hata asubuhi yake walipotoka Bethania aliona njaa. Akaona kwa mbali mtini wenye majani, akaenda ili labda aone kitu juu yake; na alipouiikilia hakuona kitu ila majani; maana si wakati wa tini. Akajibu, akauambia, Tangu leo hata milele mtu asile matunda kwako. Wanafunzi wake wakasikia.

Wakafika Yerusalemu, naye akaingia ndani ya hekalu, akaanza kuwafukuza wale waliokuwa wakiuza na kununua ndani ya hekalu, akazipindua meza na wabadili fedha, na viti vyao wauzao njiwa; wala hakuacha mtu achukue chombo kati ya hekalu. Akafundisha, akasema, Je! haikuandikwa, Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote? Bali ninyi mmeifanya kuwa pango la wanyang’anyi. Wakuu wa makuhani na waandishi wakapata habari wakatafuta jinsi ya kumwangamiza; maana walimwogopa, kwa sababu mkutano wote walishangaa kwa mafundisho yake. Na kulipokuwa jioni alitoka mjini.

Na asubuhi walipokuwa wakipita, waliuona ule mtini umenyauka toka shinani. Petro akakumbuka habari yake, akamwambia, Rabi, tazama, mtini ulioulaani umenyauka. Yesu akajibu, akawaambia, Mwaminini Mungu. Amin, nawaambia, Ye yote atakayeuambia mlima huu, Ng’oka ukatupwe baharini, wala asione shaka moyoni mwake, ila aamini kwamba hayo asemayo yametukia, yatakuwa yake. Kwa sababu hiyo nawaambia, Yo yote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu.

Nanyi, kila msimamapo na kusali, sameheni, ntkiwa na neno juu ya mtu; ili na Baba yenu aliye mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu. Lakini kama ninyi hamsamehe, wala Baba yenu aliye mbinguni hatawasamehe ninyi makosa yenu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

KUONA TENA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Alhamisi, Mei, 28, 2026,
Juma la 8 la Mwaka


1Pet 2: 2-5, 9-12; 
Zab 100:2-5; 
Mk 10:46-52.


KUONA TENA!

Leo, wakati Yesu akiuacha mji, akiwa anafuatana na wafuasi wake na umati mkubwa wa watu, kulikuwa na kipofu mmoja muombaji anayeitwa Batimayo mwana wa Timayo, akiwa amekaa pembeni ya barabara. Wakati kipofu huyu alivyosikia sauti za umati kama ilivyokawaida alitaka kujua nikitu ghani kinaendelea na anaambiwa kuwa ni Yesu Mnazareti anapita katika njia ile, mara moja baada ya kusikia hilo anapaaza sauti yake “Yesu Mwana wa Daudi unirehemu”. Ni aina ya sala tunayoiita sasa “Sala ya Yesu”. Sala tunayopaswa kuisali kila mara; ni sala ambayo tunaweza kuisali kwa uaminifu wakati tunapokubali kwamba sisi tunahitaji msaada wa Yesu na kuongozwa naye, na wakati tunapotambua nakukubali kwamba tupo mbali sana na kile alichotuitia Yesu tukiishi.

Maelezo ya yule kipofu ni maneno ambayo yanamfaa kila mmoja wetu anayemtambua Yesu. Sisi bila Yesu, ni vipofu, hatuwezi kuona vizuri ingawaje tunaweza kujiona wenye akili na maarifa mengi, tuliyosoma sana. Sisi ni waombaji. Tunaweza kumfuata Yesu kweli kama tutatambua kwamba, hata tuwe na akili ya namna ghani, maadili ya namna ghana au mali nyingi kiasi ghani, sisi kwa hakika ni masikini. Yule kipofu alikuwa amekaa kando ya barabara, sio barabarani. Na hii ndio maana halisi ya anaye kaa kando ya barabara, kwamba ni mwombani na kipofu kweli. Barabara au njia kwenye habari iliopo kwenye Injili ni ishara inayoonesha kwamba Kristo ni njia. Aliye na ukweli na uzima wote. Kwahiyo mwishoni mwa ujumbe wa Injili, baada ya yule kipofu kukutana na Yesu sasa anaweza kuona tena, yeye sio muombaji tena, na anafuatana na Yesu barabarani, njiani. Nasi tuliokutana na Yesu katika ubatizo, tutembee katika njia yake. 

Sala: Yesu Mpendwa, naomba niweze kuona vyema katika wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.



Copyright ©2013-2025 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MEI 28, 2026




MASOMO YA MISA, MEI 28, 2026
ALHAMISI, JUMA LA 8 LA MWAKA


SOMO 1 
1 Pet. 2:2-5,9-12

Kama watoto wachanga waliozaliwa sasa yatamanini maziwa ya akili yasiyoghoshiwa, ili kwa hayo mpate kuukulia wokovu; ikiwa mmeonja ya kwamba Bwana ni mwenye fadhili.

Mmwendee yeye, jiwe lililo hai, lililokataliwa na wanadamu, bali kwa Mungu ni teule, lenye heshima. Ninyi nanyi, kama mawe yaliyo hai, mmejengwa mwe nyumba ya Roho, ukuhani mtakatifu, mtoe dhabihu za roho, zinazokubaliwa na Mungu, kwa njia ya Yesu Kristo. Ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu; ninyi mliokuwa kwanza si taifa, bali sasa ni taifa la Mungu; mliokuwa hamkupata rehema, bali sasa mmepata rehema.

Wapenzi, nawasihi kama wapitaji na wasafiri. ziepukeni tamaa za mwili zipiganazo na roho. Mwe na mwenendo mzuri kati ya Mataifa, ili, iwapo huwasingizia kuwa watenda mabaya, wayatazamapo matendo yenu mazuri, wamtukuze Mungu siku ya kujiliwa.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 100 :2-5 (K) 2

(K) Njoni mbele za Bwana kwa kuimba kwa furaha

Mtumikieni Bwana kwa furaha;
Njoni mbele zake kwa kuimba. (K)

Jueni kwamba Bwana ndiyc Mungu;
Ndiye aliyetuumba na sisi tu watu wake;
Tu watu wake, na kondoo wa malisho yake. (K)

Ingieni malangoni mwake kwa kushukuru;
Nyuani mwake kwa kusifu;
Mshukuruni, lihimidini jina lake. (K)

Kwa kuwa Bwana ndiye mwema;
Rehema zake ni za milele;
Na uaminifu wake vizazi na vizazi. (K)


SHANGILIO 
Yn. 14 21

Aleluya, aleluya, Mtu akinipenda, atalishika neno langu, na Baba yangu atampenda, na sisi tutakuja kwake. Aleluya.


INJILI 
Mk. 10:46-52

Walifika Yeriko; Yesu alipokuwa akishika njia kutoka Yeriko, pamoja na wanafunzi wake, na mkutano mkubwa, mwana wa Timayo, Bartimayo, yule mwombaji kipofu, alikuwa ameketi kando ya njia. Naye aliposikia ya kwamba ni Yesu Mnazareti, alianza kupaza sauti yake, na kusema, Mwana wa Daudi, Yesu, unirehemu. Na wengi wakamkemea ili anyamaze, lakini alizidi kupaza sauti, Mwana wa Daudi, unirehemu.

Yesu akasimama akasema, Mwiteni. Wakamwita yule kipofu, wakamwambia, Jipe moyo; inuka, anakuita. Akatupa vazi lake, akaruka, akamwendea Yesu. Yesu akamjibu, akamwambia, Wataka nikufanyie nini? Yule kipofu akamwambia, Mwalimu wangu, nataka nipate kuona. Yesu akamwambia. Enenda zako, imani yako imekuponya. Mara akapata kuona; akamfuata njiani.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

NJIA AMBAYO KILA MKRISTO ANAPASWA KUSHIKILIA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatano, Mei, 27, 2026
Tafakari ya kila siku 
Juma la 8 la Mwaka wa Kanisa

1Pet 1: 18-25; 
Zab 147: 12-15, 19-20; 
Mk 10:32-45

NJIA AMBAYO KILA MKRISTO ANAPASWA KUSHIKILIA!


“Walikuwa njiani wakielekea Yerusalemu.” Yesu ndiye njia, na njia yake inamleta Yerusalemu, kubeba msalaba wake, kwakukubali kuachia maisha yake kwa upendo wa Baba nakutupenda sisi, akituongoza kwenye ushindi wa mwisho. Wote wanaopenda kuwa wafuasi wake wanapaswa wawe tayari kutembea katika njia hiyo pamoja naye. Wafuasi bado hawajafikia hali hii ya ufuasi. Wakati Yesu akisonga mbele kiaminifu kuelekea Yerusalemu, wafuasi wake wanaonekana kubaki nyuma kidogo. Walikuwa katika hali ya kutoelewa na wote walio wafuata walikuwa katika hali ya woga. Kwajinsi walivyofikiri wao walidhani Yesu hayupo katika mawazo yao. Kwenda Yerusalemu kipindi hiki, ilikuwa nikujitakia matatizo, tena makubwa. Yerusalemu palikuwa ni Sehemu ya mwisho kabisa kwenda.

Yesu kwa upole kabisa anawapa somo jingine, kuhusu nini maana halisi ya kuwa mkubwa katika hali ya ufalme wake. Katika dunia kuwa “mkubwa” ni kuwa na nguvu juu ya wengine, kutawala, kuwa na uwezo wakuwafanya watu wakubaliane na kile unachopenda, kuwatumia watu ili ufikie lengo lako. Lakini katika ulimwengu wa Yesu, ukubwa nikujiweka chini kwaajili ya kuwahudumia wengine, ndugu zetu, majirani, na zaidi sana wale waliowahitaji. Na watu wote kuwatumikia bila kuharibu utu wao. Mamlaka sio kuamrisha, bali kujitoa. Baada ya miaka zaidi ya 2000 ya Ukristo bado ni jambo kubwa sana kwetu kujifunza hili “Mwana wa mtu hakuja kutumikiwa bali kutumikia”. 

Sala; Bwana, badilisha mioyo yetu ya ubinafsi iwe mioyo ya kuwahudumia wengine. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MEI 27, 2026



MASOMO YA MISA, MEI 27, 2026
JUMATANO, JUMA LA 8 LA MWAKA

SOMO 1 
1 Pet. 1 :18-25

Nanyi mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa damu ya thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya Kristo. Naye amejulikana kweli tangu zamani, kabla haijawekwa misingi ya dunia; lakini alifunuliwa mwisho wa zamani kwa ajili yenu; ambao kwa yeye mmekuwa wenye kumwamini Mungu, aliyemfufua katika wafu akampa utukufu; hataimani yenu na tumaini lenu liwe kwa Mungu.

Mkiisha kujitakasa roho zenu kwa kuitii kweli, hata kuufikilia upendano wa ndugu usio na unafiki, basi jitahidini kupendana kwa moyo. Kwa kuwa mmezaliwa mara ya pili; si kwa mbegu iharibikayo, bali kwa ile isiyoharibika; kwa neno la Mungu ienye uzima, lidumulo hata milele. Maana, Mwili wote ni kama majani, Na fahari yake yote ni kama ua la majani. Majani hukauka na ua lake huanguka; Bali Neno la Bwana hudumu hata milele. Na neno hilo ni neno lile jema lililohubiriwa kwenu.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 147 :12-15,19-20

(K) Msifu Bwana, ee Yerusalemu. au: Aleluya.

Msifu Bwana, Ee Yerusalemu;
Msifu Mungu wako, Ee Sayuni.
Maana ameyakaza mapingo ya malango yako,
Amewabariki wanao ndani yako. (K)

Ndiye afanyaye amani mipakani mwako,
Akushibishaye kwa unono wa ngano.
Huipeleka amri yake juu ya nchi,
Neno lake lapiga mbio sana. (K)

Humhubiri Yakobo neno lake,
Na Israeli amri zake na hukumu zake.
Hakulitendea taifa lo lote mambo kama hayo,
Wala hukumu zake hawakuzijua.
Aleluya. (K)


SHANGILIO 
Yn. 14:5

Aleluya, aleluya, 
Bwana anasema: mimi ndimi njia, na ukweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi. 
Aleluya.


INJILI 
Mk. 10:32-45

Walikuwako njiani, huku wakipanda kwenda Yerusalemu; na Yesu alikuwa akiwatangulia; wakashangaa, nao katika kufuata wakaogopa. Akawatwaa tena wale Thenashara, akaanza kuwaambia habari za mambo yatakayompata, akisema, Angalieni, tunapanda kwenda Yerusalemu; na Mwana wa Adamu atatiwa mikononi mwa wakuu wa makuhani na waandishi, nao watamhukumu afe, watamtia mikononi mwa Mataifa, nao watamdhihaki, na kumtemea mate, na kumpiga mijeledi, na kumwua; na baada ya siku tatu atafufuka.

Na Yakobo na Yohane, wana wa Zebedayo, wakamwendea, wakamwambia, Mwalimu, twataka utufanyie lo lote tutakalokuomba. Akawaambia, Mwataka niwafanyie nini? Wakamwambia, Utujalie sisi tuketi, mmoja mkono wako wa kuume, na mmoja mkono wako wa kushoto, katika utukufu wako. Yesu akawaambia, Hamjui mnaloliomba. Mwaweza kunywea kikombe ninyweacho mimi, au kubatizwa ubatizo nibatizwao mimi? Wakamwambia, Twaweza. Yesu akawaambia, Kikombe ninyweacho mimi mtakinywea, na ubatizo nibatizwao mimi mtabatizwa; lakini habari ya kuketi mkono wangu wa kuume au mkono wangu wa kushoto si langu kuwapa, ila wao watapewa waliowekewa tayari.

Hata wale kumi waliposikia wakaanza kuwakasirikia Yakobo na Yohane. Yesu akawaita,  akawaambia, Mwajua ya kuwa wale wanaohesabiwa kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha. Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu anayetaka kuwa mkubwa kwenu, atakuwa mtumishi wenu, na mtu anayetaka kuwa wa kwanza wenu, atakuwa mtumwa wa wote. Kwa maana Mwana wa Adamu naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo. 

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUMFUATA YESU BILA MASHARTI!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumanne, Mei 26, 2026, 
Juma la 8 la mwaka wa Kanisa

KUMBUKUMBU YA MTAKATIFU FILIPO NERI

1 Pet 1: 10-16;
Zab 98: 1-4;
Mk 10: 28-31


KUMFUATA YESU BILA MASHARTI!

Baadhi wameitwa kuacha mengi na kumfuata Yesu. Baadhi ya hawa wameitwa kuishi maisha ya kitawa (wakike na wakiume). Wanaacha yote ya ulimwengu na kufuata mwaliko wa Yesu wa kumfuata katika hali ya pekee. Sisi wote lakini tumeitwa “kuacha yote” na kumfuata Yesu katika hali zetu za kipekee. Kwa kuacha yote, tunaitwa kukabidhi yote, uhuru wetu na kutumikia kwa kadiri ya mpango mtakatifu wa Kristo. Hili linaweza likachukua hali mbali mbali lakini mwishoni, linahitaji daima kuacha yote.

Habari njema ni kwamba ‘kuacha yote’ si zaidi ya kuacha mitazamo yetu mibaya ya maisha na kuchagua mapenzi ya Mungu. Maisha alio tuandalia ni mazuri kuliko hata chochote tunachoweza kufikiri. Kwa kusema “hapana” kwa mapenzi yetu na kufanya vitu kwa njia zetu, ni wazi tunasema “Ndio” kufanya vitu kwa ukamilifu wa Kimungu. Hata iwe ni wito ghani wa pekee katika maisha yako, ni vizuri kukumbatia mapenzi ya Mungu. 

Tutafakari ni namna ghani mimi na wewe tupo tayari kusema “ndio” kwa Yesu bila kujali anatutaka nini. Je, upo tayari kusema ndio hata kwa kile ambacho hajakufunulia bado? Sema “ndio” leo kwa maisha yako ya baadae na Mungu atakujaza Baraka katika njia hiyo. 

Sala: Bwana, haijalishi ni nini umeniitia kufanya katika maisha, jibu langu ni “ndio”. Ninataka kukutumikia kwa moyo wote. Nisaidie niweze kuishi wito huo kwa ukarimu na mapendo. Yesu, nakuamini wewe. Amina!

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MEI 26, 2026




MASOMO YA MISA, MEI 26, 2026
JUMANNE YA 8 YA MWAKA

KUMBUKUMBU YA MTAKATIFU FILIPO NERI

SOMO 1 
1 Pet l : 10-16

Katika habari ya wokovu huo manabii walitafuta-tafuta na kuchunguza-chunguza, ambao walitabiri habari za neema itakayowafikia ninyi. Wakatafuta ni wakati upi, na wakati wa namna gani ulioonywa na Roho wa Kristo aliyekuwa ndani yao, ambaye alitanerulia kuyashuhudia mateso yatakayompata Kristo, na utukufu utakaokuwako baada ya hayo. Wakafunuliwa ya kuwa si kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili yenu walihudumu katika mambo hayo, ambayo sasa yamehubiriwa kwenu na wale waliowahubiri ninyi Injili kwa Roho Mtakatifu aliyetumwa kutoka mbinguni. Mambo hayo malaika wanatamani kuyachungulia. Kwa hiyo vifungeni viuno vya nia zenu, na kuwa na kiasi; mkiitumainia kwa utimilifu ile neema mtakayoletewa katika ufunuo wake Yesu Kristo. Kama watoto wa kutii msijifananishe na tamaa zenu za kwanza, za ujinga wenu; bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu. 


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 98 :1-4

(K) Bwana ameufunua wokovu wake.

Mwimbieni Bwana wimbo mpya,
Kwa maana ametenda mambo ya ajabu.
Mkono wa kuume wake mwenyewe,
Mkono wake mtakatifu umemtendea wokovu.

Bwana ameufunua wokovu wake,
Machoni pa mataifa ameidhihirisha haki yake.
Amezikumbuka rehema zake,
Na uaminifu wake kwa nyumba ya Israeli.

Miisho yote ya dunia imeuona
Wokovu wa Mungu wetu.
Mshangilieni Bwana, nchi yote,
Inueni sauti, imbeni kwa furaha, imbeni zaburi.


SHANGILIO 
Yn. 8 :12

Aleluya, aleluya,
Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, asema Bwana, yeye anifuataye hatakwenda gizani kamwe, bali atakuwa na nuru ya uzima.
Aleluya.


INJILI 
Mk. 10:28-31

Petro alimwambia Yesu, Tazama, sisi tumeacha vyote tukakufuata wewe. Yesu akasema, Amin, nawaambieni, Hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume, au ndugu wake, au mama, au baba, au watoto, au mashamba, kwa ajili yangu, na kwa ajili ya Injili, ila atapewa mara mia sasa wakati huu, nyumba, na ndugu waume, na ndugu wake, na. mama, na watoto na mashamba, pamoja na udhia; na katika ulimwengu ujao uzima wa milele. Lakini wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho; na wa mwisho watakuwa wa kwanza.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MAMA WA KANISA



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatatu, Mei, 25, 2026 
Juma la 8 la Mwaka .

Kumbukumbu ya Bikira Maria Mama wa Kanisa

Mwa 3:9-15,20; 
Zab 87; 
Yn 19:25-34


MAMA WA KANISA


Sherehe ya Bikira Maria Mama wa Kanisa kuanzia mwaka 2018 inaadhimishwa Jumatatu baada ya Sherehe ya Pentekoste na mwaka huu ni tarehe 20 Mei 2024. Mabadiliko haya yanapaswa kuwa tayari yamekwisha kuingizwa kwenye Kalenda za maadhimisho ya Liturujia ya Kanisa na kufanyiwa kazi tangu sasa! Ibada hii kwa Bikira Maria, itawasaidia waamini kukumbuka kwamba, maisha ya Kikristo yanafumbatwa katika Fumbo la Msalaba linaloadhimishwa katika Ekaristi Takatifu, Kanisa linapomtolea pia sifa na heshima Bikira Maria, Mama wa Mkombozi, aliyesadaka maisha yake kwa ajili ya kushiriki kikamilifu katika kazi ya ukombozi!

Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican katika Tamko lao kuhusu Fumbo la Kanisa wanafafanua kwa kina na mapana nafasi ya Bikira Maria, Mama wa Mungu katika Fumbo la Kristo na la Kanisa: tangu Agano la Kale, Fumbo la Umwilisho, Bikira Maria katika maisha ya hadharani ya Kristo Yesu, Bikira Maria baada ya Kristo Yesu kupaa mbinguni. Wanaendelea kufafanua dhamana na nafasi ya Bikira Maria katika maisha na utume wa Kanisa kama mshiriki mwaminifu wa kazi ya ukombozi, mwombezi kwa ajili ya wokovu, Bikira Maria kama mfano wa utimilifu wa Kanisa katika maisha na utakatifu wake na kwamba, Bikira Maria ni ishara na matumaini thabiti na faraja kwa taifa la Mungu linalosafiri huku Bondeni kwenye machozi!

Kwa hakika, Mapokeo ya maadhimisho ya Fumbo la maisha ya Kristo ambayo kamwe hayawezi kumtenga Bikira Maria, Mama wa Kristo na Kanisa. Bikira Maria anatambulikana kuwa ni Mama wa Wakristo ambao wamezaliwa kwake kwa njia ya fadhila ya upendo na kwamba, Bikira Maria ni Mama wa Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa kama wanavyofundisha Mtakatifu Agostino, Askofu na Mwalimu wa Kanisa pamoja na Mtakatifu Leo Mkuu. Umama wa Kristo na Kanisa ulidhihirishwa pale chini ya Msalaba, Bikira Maria alipopokea upendo wa dhati kutoka kwa Mwanaye mpendwa na Yohane kwa niaba ya wengine wote, wakawa ni wafuasi na mitume wa upendo kwa ajili ya Mama yake.

Bikira Maria aliendelea kuandamana na Kanisa katika sala wakati Mitume wakisubiria ujio wa Roho Mtakatifu. Kwa nyakati mbali mbali, waamini wamekuwa wakimheshimu na kumfanyia Ibada Bikira Maria kama: Mama wa Mitume, Mama wa waamini wa wale wote wanaozaliwa upya katika Kristo Yesu na Mama wa Kanisa kama wanavyofundisha Papa Benedikto XV pamoja na Papa Leo wa XIII. Mtakatifu Paulo VI kunako tarehe 21 Novemba 1964, Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican walipokuwa wanahitimisha Kikao cha tatu cha Mkutano huo, alitamka kwamba, Bikira Maria ni Mama wa Kanisa; yaani: ni Mama wa Wakristo wote na wachungaji wanaomkimbilia kama Mama.

Kumbe, Bikira Maria, Mama wa Kanisa anapaswa kuheshimiwa na Wakristo wote. Katika maadhimisho ya Mwaka wa Upatanisho1975, kuliadhimishwa Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya Bikira Maria, Mama wa Kanisa. Litania ya Bikira Maria wa Loreto ikaongeza heshima hii katika Litania. Majimbo mbali mbali wakaona kwamba, inafaa na kuomba Kiti Kitakatifu kuruhusu maadhimisho haya yaingizwe katika kalenda ya majimbo yao! Kutokana na kukua na hatimaye, kukomaa kwa Ibada ya Bikira Maria, Mama wa Kanisa, Baba Mtakatifu Francisko ameridhia tamko lililotolewa na Baraza la Kipapa la Ibada na Sakramenti za Kanisa kwamba, kuanzia sasa Sherehe ya Bikira Maria Mama wa Kanisa itakuwa inaadhimishwa Jumatatu baada ya Sherehe ya Pentekoste ya kila mwaka!

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MEI 25, 2026

 


MASOMO YA MISA, MEI 25, 2026
JUMATATU, JUMA LA 8 LA MWAKA

Kumbukumbu ya Bikira Maria Mama wa Kanisa


SOMO 1 
Mwa 3:9-15, 20

Baada ya Adamu kule tunda la ule mti, Bwana Mungu akamwita Adamu, akamwambia, Uko wapi? Akasema, Nalisikia sauti yako bustanini, nikaogopa kwa kuwa mimi ni uchi; nikajificha. Akasema, Ni nani aliyekuambia ya kuwa u uchi? Je! Umekula wewe matunda ya mti niliyokuagiza usiyale? Adamu akasema, Huyo mwanamke uliyenipa awe pamoja nami ndiye aliyenipa matunda ya mti huo, nikala. Bwana Mungu akamwambia mwanamke, Nini hili ulilolifanya? Mwanamke akasema, Nyoka alinidanganya, nikala. Bwana Mungu akamwambia nyoka, Kwa sababu umeyafanya hayo, umelaaniwa wewe kuliko wanyama wote, na kuliko hayawani wote walioko mwituni; kwa tumbo utakwenda, na mavumbi utakula siku zote za maisha yako; nami nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino. Adamu akamwita mkewe jina lake Hawa; kwa kuwa yeye ndiye aliye mama yao wote walio hai.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI 
Zab 87:1-7

(K) Enyi mataifa yote msifuni Bwana.

Msingi wake upo Juu ya milima mitakatifu.
Bwana ayapenda malango ya Sayuni
Kuliko maskani zote za Yakobo.
Umetajwa kwa mambo matukufu, Ee Mji wa Mungu.
(K) Enyi mataifa yote msifuni Bwana.

Nitataja Rahabu na Babeli Miongoni mwao wanaonijua.
Tazama Filisti, na Tiro, na Kushi; Huyu alizaliwa humo.
Naam, mintarafu Sayuni itasemwa,
Huyu na huyu alizaliwa humo.
Na Yeye Aliye juu Ataufanya imara.
(K) Enyi mataifa yote msifuni Bwana.

Bwana atahesabu, awaandikapo mataifa,
Huyu alizaliwa humo.
Waimbao na wachezao na waseme,
Visima vyangu vyote vimo mwako.
(K) Enyi mataifa yote msifuni Bwana.



SHANGILIO 
Zab. 147:12,15

Aleluya, aleluya,
Msifu Bwana, ee Yerusalemu, huipeleka amri yake juu ya nchi.
Aleluya.


INJILI
Yn 19:25-34

Penye msalaba wake Yesu walikuwa wamesimama mamaye, na umbu la mamaye, Mariamu wa Klopa, na Mariamu Magdalene. Basi Yesu alipomwona mama yake, na yule mwanafunzi aliyempenda amesimama karibu, alimwambia mama yake, Mama, tazama, mwanao. Kisha akamwambia yule mwanafunzi, Tazama, mama yako. Na tangu saa ile mwanafunzi yule akamchukua nyumbani kwake. Baada ya hayo Yesu, hali akijua ya kuwa yote yamekwisha kumalizika ili andiko litimizwe, akasema, Naona kiu. Kulikuwako huko chombo kimejaa siki; basi wakatia sifongo iliyojaa siki juu ya ufito wa hisopo, wakampelekea kinywani. Basi Yesu alipokwisha kuipokea ile siki, alisema, Imekwisha. Akainama kichwa, akaisalimu roho yake. Basi Wayahudi, kwa sababu ni Maandalio, miili isikae juu ya misalaba siku ya sabato, (maana sabato ile ilikuwa siku kubwa), walimwomba Pilato miguu yao ivunjwe, wakaondolewe. Basi askari wakaenda, wakamvunja miguu wa kwanza, na wa pili, aliyesulibiwa pamoja naye. Lakini walipomjia Yesu na kuona ya kuwa amekwisha kufa, hawakumvunja miguu; lakini askari mmojawapo alimchoma ubavu kwa mkuki; na mara ikatoka damu na maji.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo. 

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.