Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

WAHUJAJI WA KUELEKEA MBINGUNI!



“KUFUFUKA NA KRISTO”
Tafakari ya Pasaka
Jumapili, Mei 17, 2026 
Juma la 7 la Pasaka
Sherehe ya kupaa Bwana wetu Yesu Kristo Mbinguni

Mdo 1:1-11
Zab 47: 1-2, 5-6, 7-8, (K)
Ef 1:17-23
Mt 28:16-20


WAHUJAJI WA KUELEKEA MBINGUNI!

Leo Kanisa lina sheherekea sherehe ya Kupaa Bwana wetu Yesu Kristo Mbinguni. Sherehe hii inadhihirisha Umungu wa Kristo, na unasherekewa na wakristo wote. Sherehe hii inadhihirisha kile ambacho tunakiri katika nasadiki “Akapaa mbinguni, ameketi mkono wa kuume wa Baba”. 
Maandiko yanatuambia kwamba Enok na Elia hawakufa, lakini walipelekwa mbinguni. Kanisa pia linatuambia kuwa Bikira Maria alipalizwa mbinguni mwili na roho. Yesu alikuwa Mungu na mwanadamu. Imani yetu ya umwilishi inatuambia kwamba alikuja duniani akapata mwili ili kuwakomboa wanadamu. Yesu sasa anakamilisha utume wake duniani na sasa anapaa mbinguni katika kiti chake cha utukufu milele yote. Kupaa ni mwisho na pia ni mwanzo. Kupaa ni mwisho wa utume wake lakini pia ni mwanzo wa utume wa Roho Mtakatifu. Ni kuvuka katika ngazi nyingine katika mpango kamili wa Baba. 

Mitume huenda walikuwa na hofu na kushangazwa. Yesu alikuwa pamoja nao, alikufa na kufufuka na kuwatokea mara nyingi, na sasa anapaa mbele ya macho yao. Yesu alikuwa ameshawaambia kuwa Msaidizi atakuja na kuwaongoza katika ukweli wote. Mitume watakuwa walitoka katika hofu na kuwa na furaha, kutoka katika huzuni na kuelewa, na kuwa tena na furaha. Pengine ndivyo wengine tunavyo yakuta maisha yetu. Furaha na uchungu, masikitiko na wakati mwingine furaha, nk. Kila tukio hufunua kitu kipya, kitu chenye kutoa changamoto au kuleta utukufu au huzuni. Habari njema ni kwamba mpango wa Baba hujifunua katika ukamilifu wote. Kwa sherehe hii, Yesu anaanza kuelekeza utume wake kwa kuanzisha ufalme wa Mungu kutoka Mbinguni. Ukuu wake ni utawala kama wa kiti cha dereva akielekeza maisha yetu. Kutoka mbinguni Yesu sasa ameanza kushuka katika maisha yetu, akitimiza utume wake kwa njia ya mitume na njia yetu wote. Kupaa haina maana kwamba Yesu ameondoka, bali, ina maana kwamba Yesu yupo sasa kwa kila mmoja wetu anaye mkaribisha na kujikabidhi katika utume wake. Kutoka mbinguni Yesu anauwezo wa kujifunua kwa wote. Yupo tayari kuishi ndani mwetu na kutukaribisha tuishi ndani yake. Ni mwanzo mpya wa Kanisa. Wanacho paswa kufanya sasa Mitume ni kumsubiri Roho Mtakatifu kuwashukia.

Somo la kwanza linaelezea nyakati za mwisho za Yesu mfufuka akiwa na wanafunzi wake hapa duniani. Baada ya ufufuko,Yesu alibaki kwa siku arobaini akiwatokea wanafunzi wake na kuwaongoza. Alikuwa amesahafungua akili zao Kuhusu ujumbe uliomhusu yeye kutoka katika Agano la Kale, lakini kulikuwa bado mambo mengine walio paswa kujifunza zaidi kabla hawaja anza utume wao. Yesu kipindi hicho aliwafundisha mambo mengi kwa ajili ya utume huu maalum. 

Katika somo la Pili Mt. Paulo anaelezea nguvu ya Mungu ya kumfufua Yesu kutoka wafu na kumfanya aketi mkono wake wa kuume, ambapo yeye you juu ya utawala wa vyote, mamlaka na nguvu na tawala. Yesu mfufuka ni Mfalme kweli wa Ulimwengu wote. 

Katika somo la Injili, Bwana kwa mamlaka yote aliyopewa na Baba yake, Yesu ana waamuru wanafunzi wake waende ulimwenguni kote kuwafanya watu wote kuwa wafuasi wake. Anawaita wawe mashahidi wake. Shihidi ni yule anaye shuhudia kile alicho sikia na kuona (Mdo 4: 19-20). Sisi pia tupo kama Wanafunzi wake tunaitwa kumshuhudia na katika mateso, kifo, na kufufuka na kutubu dhambi katika jina la Yesu. Njia pekee ya kushika ukweli wa Yesu mfufuka ni kuwa mashahidi wake popote pale tulipo. 

Wafuasi walitazama juu wakati Yesu alivyokuwa akipaa mbinguni. Sisi nasi tunapaswa kutazama juu, kujikumbusha kwamba maisha yetu hapa duniani ni utume, safari ambayo inakamilika huko mbinguni. Yesu anatuita sisi tupae kwa kwenda katika maisha mengine. Yesu yupo nasi mpaka ukamilifu wa Dahari. Tukaribie sasa kiti cha Mungu cha neema kwa ujasiri, ili tuweze kupokea huruma na kupata neema ya kutusaidia wakati wa taabu (Heb 4:16). Sherehe hii itusaidie tuweze kuishi maisha yetu ya ukristo , kama Enok, Elia na Bikira Maria waliofurahia zawadi ya neema za Mungu. 

Sala: Bwana, katika kila kitu nisaidie kusema “ndio” kwa mpango wako. Ninakuomba nikushuhudie wewe kwa marafiki zangu na jirani zangu kwa njia ya maneno na matendo. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MEI 17, 2026



MASOMO YA MISA, MEI 17, 2026
DOMINIKA YA 7 YA PASAKA
SHEREHE YA KUPAA BWANA


MWANZO:
Mdo. 1:11

Enyi watu wa Galilaya, mbona mmesimama mkitazama mbinguni? Atakuja vivyo hivyo mlivyomwona akienda zake mbinguni, Aleluya.


SOMO 1
Mdo. 1:1-11

Kitabu kile cha kwanza nalikiandika, Theofilo, katika habari ya mambo yote aliyoanza Yesu kufanya na kufundisha, hata siku ile alipochukuliwa juu, alipokuwa amekwisha kuwaagiza kwa Roho Mtakatifu wale mitume aliowachagua; wale aliowadhihirishia nafsi yake, kwa dalili nyingi, baada ya kuteswa kwake, ya kwamba yu hai, akiwatokea muda wa siku arobaini, na kuyanena mambo yaliyouhusu ufalme wa Mungu. Hata alipokuwa amekutana nao aliwaagiza wasitoke Yerusalemu, bali waingoje ahadi ya Baba, ambayo mlisikia habari zake kwangu; ya kwamba Yohane alibatiza kwa maji, bali ninyi mtabatizwa katika Roho Mtakatifu baada ya siku hizi chache.

Basi walipokutanika, wakamwuliza, wakisema, Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme? Akawaambia, Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe. Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.

Akiisha kusema hayo, walipokuwa wakitazama, akainuliwa, wingu likampokea kutoka machoni pao. Walipokuwa wakikaza macho mbinguni, yeye alipokuwa akienda zake, tazama, watu wawili wakasimama karibu nao, wenye nguo nyeupe, wakasema, Enyi watu wa Galilaya, mbona mmesimama mkitazama mbinguni? Huyu Yesu aliyechukuliwa kutoka kwenu kwenda juu mbinguni, atakuja jinsi iyo hiyo mlivyomwona akienda zake mbinguni.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 47 : 1-2, 5-6, 7-8, (K) 5

(K) Mungu amepaa kwa kelele za shangwe, Bwana kwa sauti ya baragumu. au: Aleluya

Enyi watu wote, pigeni makofi,
Mpigieni Mungu kelele kwa sauti ya shangwe,
Kwa kuwa Bwana Aliye juu, mwenye kuogofya,
Ndiye mfalme mkuu juu ya dunia yote. (K)

Mungu amepaa kwa kelele za shangwe,
Bwana kwa sauti ya baragumu.
Mwimbieni Mungu, naam, imbeni;
Mwimbieni mfalme wetu, naam, imbeni. (K)

Maana Mungu ndiye mfalme wa dunia yote,
Imbeni kwa akili.
Mungu awamiliki mataifa,
Mungu ameketi katika kiti chake kitakatifu. (K)



SOMO 2
Efe 1 : 17-23

Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa utukufu, awape ninyi roho ya hekima na ya ufunuo katika kumjua yeye; macho ya mioyo yenu yatiwe nuru, mjue tumaini la mwito wake jinsi lilivyo; na utajiri wa utukufu wa urithi wake katika watakatifu jinsi ulivyo; na ubora wa ukuu wa uweza wake ndani yetu tuaminio jinsi ulivyo; kwa kadiri ya utendaji wa nguvu za uweza wake; aliotenda katika Kristo alipomfufua katika wafu, akamweka mkono wake wa kuume katika ulimwengu wa roho; juu sana kuliko ufalme wote, na mamlaka, na nguvu, na usultani, na kila jina litajwalo, wala si ulimwenguni humu tu, bali katika ule ujao pia; akavitia vitu vyote chini ya miguu yake, akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwa ajili ya kanisa; ambalo ndilo mwili wake, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


SHANGILIO
Mt. 28:19-20

Aleluya, aleluya,
Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, na tazama, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote.
Aleluya.


INJILI
Mt. 28:16-20

Wale wanafunzi kumi na mmoja walikwenda Galilaya mpaka mlima ule aliowaagiza Yesu. Nao walipomwona, walimsujudia; lakini baadhi yao waliona shaka. Yesu akaja kwao, akasema nao, akawambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, hata ukamilifu wa dahari.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUELEWA NENO LA MUNGU!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Pasaka
Jumamosi, Mei 16, 2026
Juma la 6 la Pasaka

Mdo 18: 23-28
Zab 47: 2-3, 8-10 (k. 8);
Yn 16: 23-28.


KUELEWA NENO LA MUNGU!

Katika somo la kwanza kutoka katika kitabu cha matendo ya Mitume, kina muongelea mtu mmoja ambaye anaitwa Apollo ambaye ni mfano kwa wakristo wote. Alifahamu maandiko na alikuwa na ujasiri wa kuhubiri habari njema. Alifanya watu wengi wabadilishe maisha yao na kuongoka, kwa kutangaza Neno la Mungu. Sio wote walio na uweze wa kufafanua Neno la Mungu. Tunahitaji msaada wa Mungu na uongozi wa Roho Mtakatifu. Ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo umefungua milango ya neema. Tunaweza kuomba kwa Mungu kwa jina la Kristo na nguvu ya Roho Mtakatifu. 

Maandiko Matakatifu, na hasa mafundisho ya Kristo yapo katika lugha ambayo imefunikwa kiasi kikubwa, ambayo sio wote waweza kuelewa. Kwahiyo kwanini Yesu anaongea katika lugha ambayo imefunikwa au kufichwa na asiongee kwa wazi wazi moja kwa moja? Jibu linahusika na sisi ukosefu wetu wa kutokuwa wazi katika ukweli. Kama tunakuwa wazi katika ukweli, na kuwa tayari kukumbatia ukweli bila kujali ni namna ghani, Yesu angeongea nasi na sisi kuitika mara moja. Lakini sivyo ilivyo. Ufunguo wa kuelewa haya ni kuelewa na kutambua elimu ya mapenzi ya Mungu na utayari wa kutimiza mapenzi hayo. Mara nyingi sisi tunataka Yesu atuambie mapenzi yake, tufikirie juu yake, na kuangalia, alafu sisi tunakuja na majibu yetu wenyewe. Lakini kama tunataka Yesu aongee nasi wazi wazi, tunapaswa kusema ndio kwa Yesu hata bila kutambua anataka tufanye nini. Utayari wa kukubali mapenzi yake ni mwanzo wa kuelewa mapenzi yake. 

Mfano kamili wa hili ni Mama yetu Bikira Maria. Kabala ya Malaika kuja kwake yeye alikuwa akiyashika mapenzi ya Mungu. na Malaika alipofika na kumwelezea nini kitacho tokea, yeye aliuliza uelewa zaidi. Na kweli alipata kuelewa zaidi kwa kupata jibu kwa swali lake. Lakini sababu moja ya malaika, kama mjumbe wa Mungu, aliongea wazi wazi kwasababu alishafahamu wazi moyo wa Maria kuwa unamtegemea Mungu bila kujali kutatokea nini. 

Je, unataka Mungu aongee nawe katika hali ya uwazi? Je, unataka kuelewa Neno la Mungu? kama ndivyo, sema ndio kwa kile ambacho Mungu anapenda wewe utende daima. Kwa kujenga hali hii ya kusema ndio kwa mapenzi ya Mungu, itamfanya Mungu kukufungulia mlango mara moja kuelewa yale yote anayotaka uyatende katika kutimiza mapenzi yake. 

Sala: Bwana, ninachagua mapenzi yako leo na daima. Sichagui kitu kingine ni mapenzi yako tu. Ninavyosema ndio kwako, nisaidie niweze kukuwa katika hali ya uwazi wako unaopenda. Yesu, ninakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MEI 16, 2026



MASOMO YA MISA, MEI 16, 2026
JUMA LA 6 LA PASAKA, JUMAMOSI

SOMO 1 
Mdo. 18:23-28

Paulo, akiisha kukaa Antiokia siku kadha wa kadha aliondoka, akapita kati ya nchi ya Galatia na Frigia, mji kwa mji, akiwathibitisha wanafunzi. Basi Myahudi mmoja, jina lake Apolo, mzaliwa wa Iskanderia, mtu wa elimu, akafika Efeso; naye alikuwa hodari katika maandiko. Mtu huyo alikuwa amefundishwa njia ya Bwana; na kwa kuwa roho yake ilikuwa ikimwaka, alianza kunena na kufundisha kwa usahihi habari za Yesu; naye alijua ubatizo wa Yohane tu. Akaanza kunena kwa ujasiri katika sinagogi; hata Prisila na Akila walipomsikia wakamchukua kwao, wakamweleza njia ya Bwana kwa usahihi zaidi.

Na alipotaka kuvuka bahari aende mpaka Akaya, ndugu wakamhimiza, wakawaandikia wale wanafunzi wamkaribishe; naye alipofika akawasaidia sana wale waliokwisha kuamini kwa neema ya Mungu. Kwa maana aliwashinda Wayahudi kabisa kabisa mbele ya watu wote, akionyesha kwa maneno ya maandiko ya kuwa Yesu ni Kristo.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 47: 1-2, 7-9 (K) 7

(K) Mungu ndiye mfalme wa dunia yote. 
Au: Aleluya.

Enyi watu wote, pigeni makofi,
Mpigieni Mungu kelele kwa sauti ya shangwe, 
Kwa kuwa Bwana Aliye juu, mwenye kuogofya, 
Ndiye mfalme mkuu juu ya dunia yote. (K)

Maana Mungu ndiye mfalme wa dunia yote, 
Imbeni kwa akili.
Mungu awamiliki mataifa,
Mungu ameketi katika kiti chake kitakatifu. (K)

Wakuu wa watu wamekusanyika,
Wawe watu wa Mungu wa Ibrahimu.
Maana ngao za dunia zina Mungu,
Ametukuka sana. (K)


SHANGILIO 
Yn. 10:27

Aleluya, aleluya, 
Kondoo wangu waisikia sauti yangu, nami nawajua, nao wanifuata. 
Aleluya.


INJILI 
Yn. 16:23-28

Siku ile, Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Amin, amin, nawaambia, Mkimwomba Baba neno lo lote atawapa kwa jina langu. Hata sasa hamkuomba neno kwa jina langu; ombeni, nanyi mtapata; furaha yenu iwe timilifu. Hayo nimesema nanyi kwa mithali; saa yaja ambayo sitasema nanyi tena kwa mithali; lakini nitawapa waziwazi habari ya Baba. Na siku ile mtaomba kwa jina langu; wala siwaambii ya kwamba mimi nitawaombea kwa Baba; kwa maana Baba mwenyewe awapenda kwa kuwa ninyi mmenipenda mimi, na kusadiki ya kwamba mimi nalitoka kwa Baba. Nalitoka kwa Baba, nami nimekuja hapa ulimwenguni; tena nauacha ulimwengu; na kwenda kwa Baba.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo. 


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

FURAHA NA TUMAINI LA UFUFUKO!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Pasaka
Ijumaa, Mei, 15, 2026 
Juma la 6 la Pasaka


Mdo 18: 9-18;
Zab 47: 2-7 (K. 8);
Yn 16: 20-23.


FURAHA NA TUMAINI LA UFUFUKO!

Kila tukio katika maisha yetu linaleta matokeo fulani katika maisha yetu. Wakati matokeo yakiwa mazuri tunakuwa na furaha. Na wakati tukiwa tunazamia mazuri yatokee hilo tunaita kuwa tumaini. Kama matokeo ni mabaya tunakuwa na huzuni na tunakuwa na hofu na mashaka. Hali hizi zinabadilika kadiri ya hisia zetu, na hayabakii kuwa yale yale. Injili inayaweka yote haya katika mfano wa kuzaliwa kwa mtoto. Kunakuwepo na maumivu, hofu lakini furaha huja baadae. Tunapaswa kuwenda zaidi ya haya tunayo yaona ulimwenguni ili tuweze kwenda kufuhia furaha ya ufalme wa Mungu. Kama Yesu alivyokufa juu ya vitu vyote ili afufuke katika utukufu wa Mungu, hivyo hivyo nasi tunapaswa tufe juu ya mambo yanayoleta furaha ya muda na kwa kufanya hivi lazima tuhizi uchungu wa kuacha baadhi ya mambo ili tuweze kufufuka ndani Yake. Maisha yanakuwa kwa kuyatoa, lakini yanaharibika kwa kujitenga na kujifariji binafsi.

Je, mateso yana maana kwamba upo mbali na Mungu? Au hauna neema ya Mungu? Ina maana kwamba Mungu amekuacha? Au ina maana kwamba unafanya kitu kibaya? Hakika sio hivyo, tunachopaswa kufanya nikuangalia maisha ya Yesu na tutatambua kwamba hili halipo hivyo. Alikuwa katika hali ya misuko suko na kupingwa na viongozi kila wakati lakini alijikita zaidi katika utume wa Baba yake. Alikuwa akisali kwa siku arobaini jangwani. Katika utume wake alikutana na vipingamizi vingi sana. Alitukanwa na kupingwa, kutokueleweka, kutemewa mate, na zaidi hata mpaka alivyokufa msalabani. 

Mama yetu Bikira Maria alipatwa na “uchungu kama upanga” ukampenya moyo wake. Alikuwa na upendo kamili kwa mtoto wake. Aliwaona wengi waliokuwa wakimpenda mwanae na wale wasiompenda mwanae. Aliwaona wale waliokuwa wakimsulubisha na kumbebesha msalaba. 

Lakini fikiria juu ya maisha yao. Wanafurahi sasa Mbinguni kama watakatifu, na Mama yetu kama Malkia wa mbinguni na watakatifu wote, na Yesu kama Mfalme wa Mbingu na Nchi. Wanaishi katika utukufu milele. Huzuni zao zimebadilika na kuwa furaha kamili. Kama unafikiri umetendewa vibaya au wamekuonea, furahi upo salama. Tambua kuwa unapo bakia mwaminifu na kutembea katika njia ya uaminifu ya Mungu aliokuwekea, mwisho ni kwamba utafurahia! Shikilia katika tumaini hilo na elekeza macho yako katika njia ya Mungu. Hakika utafanikiwa. 

Sala: Bwana, ninakabidhi mizigo yangu yote na uchungu wote kwako. Ninaunganisha na msalaba wako nikitumaini kuwa utakuwa nami katika yote katika njia yangu ya maisha. Ninaomba niweke moyo wangu katika lengo langu nikiwa na furaha katika upendo wako kamili. Yesu, nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MEI 15, 2026





MASOMO YA MISA, MEI 15, 2026
JUMA LA 6 LA PASAKA, IJUMAA

SOMO 1 
Mdo. 18: 9-18

Bwana alimwambia Paulo kwa maono usiku, Usiogope, bali nena, wala usinyamaze, kwa kuwa mimi ni pamoja nawe, wala hapana mtu atakayekushambulia ili kukudhuru; kwa maana mimi nina watu wengi katika mji huu. Akakaa huko muda wa mwaka mmoja na miezi sita akifundisha kati yao neno la Mungu.

Hata Galio alipokuwa liwali wa Akaya, Wayahudi wakamwinukia Paulo kwa nia moja, wakamleta mbele ya kiti cha hukumu, wakisema, Mtu huyu huwavuta watu ili wamwabudu Mungu kinyume cha sheria. Na Paulo alipotaka kufunua kinywa chake, Galio akawaambia Wayahudi, Kama lingekuwa jambo la dhuluma au la hila mbaya, enyi Wayahudi, ingekuwa haki mimi kuchukuliana nanyi; bali ikiwa ni hoja juu ya maneno na majina na sheria yenu, liangalieni ninyi wenyewe, maana mimi sitaki kuwa mwamuzi wa mambo hayo.

Akawafukuza waondoke mbele ya kiti cha hukumu. Nao wote wakamshika Sosthene, mkuu wa sinagogi, wakampiga mbele ya kiti cha hukumu. Wala Galio hakuyaona mambo hayo kuwa ni kitu. Baada ya hayo Paulo akazidi kukaa huko siku nyingi, kisha akaagana na ndugu akaabiri kwenda Shamu; na Prisila na Akila wakaenda pamoja naye, alipokwisha kunyoa kichwa chake huko Kenkrea; maana alikuwa ana nadhiri.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 47:1-6 (K) 7

(K) Mungu ndiye mfalme wa dunia yote. 
Au: Aleluya.

Enyi watu wote, pigeni makofi,
Mpigieni Mungu kelele kwa sauti ya shangwe,
Kwa kuwa Bwana Aliye juu, mwenye kuogofya, 
Ndiye mfalme mkuu juu ya dunia yote. (K)

Atawatiisha watu wa nchi chini yetu,
Na mataifa chini ya miguu yetu.
Atatuchagulia urithi wetu,
Fahari ya Yakobo ambaye alimpenda. (K)

Mungu amepaa kwa kelele za shangwe,
Bwana kwa sauti ya baragumu.
Mwimbieni Mungu, naam, imbeni;
Mwimbieni mfalme wetu, naam, imbeni. (K)


SHANGILIO 
Yn- 10:14

Aleluya, aleluya, 
Mimi ndimi mchungaji mwema, nao walio wangu nawajua, nao walio wangu wanijua mimi. 
Aleluya.

INJILI
Yn. 16:20-23

Siku ile Yesu aliwaambia wanafunzi wake; Amin, amin, nawaambia, Ninyi mtalia na kuomboleza, bali ulimwengu utafurahi; ninyi mtahuzunishwa, lakini huzuni yenu itageuka kuwa furaha. Mwanamke azaapo, yuna huzuni kwa kuwa saa yake imefika, lakini akiisha kuzaa mwana, haikumbuki tena ile dhiki, kwa sababu ya furaha ya kuzaliwa mtu ulimwenguni. Basi ninyi hivi sasa mna huzuni; lakini mimi nitawaona tena; na mioyo yenu itafurahi, na furaha yenu hakuna awaondoleaye. Tena siku ile hamtaniuliza neno lo lote. Amin, amin, nawaambia, Mkimwomba Baba neno lo lote atawapa kwa jina langu.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo. 

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

VYOMBO VYA UPENDO!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Alhamisi, Mei, 14, 2026, 
Juma la 6 la Pasaka

Sikukuu ya Mtakatifu Matia, Mtume

Mdo 1: 15-17, 20-26;
Zab,113: 1-8 (k.8);
Yn 15: 9-17.


VYOMBO VYA UPENDO!

“Hakuna upendo uliyo mkuu kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwaajli ya rafiki zake”. Upendo wa Yesu ni wa pekee na unajifunua kwa majitoleo yake pale msalabani. Upendo wa Yesu ni sadaka na hauna masharti. Yuda hakuutambua upendo huo, lakini sisi tunaitwa kuutambua kama wafuasi wa Kristo.

Kuwa mfuasi wa Kristo kuna mambo matatu yanayo jitokeza katika Injili ya leo, kwanza kabisa, kila Mkristu ana wito wa pekee wakupendana na mwezake. Na pili kila Mkristu ana wajibu wakumfuata Kristo na kutembea katika njia yake ya utakatifu na upendo. Na mwisho kabisa kila Mkristo anapaswa kujiunga na Mungu daima kwa njia ya sala. 

Tumuombe mtakatifu Matia mtume tunae muadhimisha leo atuombee kwa Mungu tuweze kuyashika hayo kama yeye alivyofanikiwa kuyashika kama mtume wa Kristo aliyechukuwa ile nafasi ya Yuda Iskariote.

Sala: Yesu, naomba unisaidie mimi niweze kuwa chombo cha upendo kama mtakatifu Matia mtume. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MEI 14, 2026




MASOMO YA MISA, MEI 14, 2026
ALHAMISI YA 6 YA PASAKA
SIKUKUU YA MT. MATHIA, MTUME


SOMO 1
Mdo. 1:15-17, 20-26

Siku zile Petro alisimama kati ya ndugu zake (jumala ya majina ilipata mia na ishirini), akasema, Ndugu, ilipasa andiko litimizwe, alilolinena Roho Mtakatifu zamani kwa kinywa cha Daudi. katika habari za Yuda aliyewaongoza wao waliomkamata Yesu, kwa sababu alikuwa amehesabiwa pamoja na sisi, akapata sehemu ya huduma hii. Kwa maana imeandikwa katika chuo cha Zaburi, Kikao chake na kiwe ukiwa,

Wala asiwepo mtu mwenye kukaa humo; tena, Usimamizi wake autwae mwingine. Basi katika watu waliofuatana nasi wakati wote Bwana Yesu alipokuwa akiingia na kutoka kwetu, kuanza tangu ubatizo wa Yohane, hata siku ile alipochukuliwa kwetu kwenda juu, inapasa mmoja wao awe shahidi wa kufufuka kwake pamoja nasi.

Wakaweka wawili, Yusufu, aitwaye Barsaba, aliyekuwa na jina la pili Yusto, na Mathiya. Kisha wakaomba, wakasema, Wewe, Bwana, ujuaye mioyo ya watu wote, tuonyeshe ni nani uliyemchagua katika hawa wawili, ashike mahali katika huduma hii na utume huu, alioukosa Yuda, aende zake mahali pake mwenyewe. Wakawapigia kura; kura ikamwangukia Mathiya; naye akahesabiwa kuwa pamoja na mitume kumi na mmoja.


W1MBO WA KATI KATI 
Zab. 113:1-8 (K) 8

(K) Amketishe pamoja na wakuu, pamoja na wakuu wa watu wake. au: Aleluya.

Aleluya.
Enyi watumishi wa Bwana, sifuni,
Lisifuni jina la Bwana.
Jina la Bwana lihimidiwe 
Tangu leo na hata milele. (K)

Toka maawio ya jua hata machweo yake 
Jina la Bwana husifiwa.
Bwana ni mkuu juu ya mataifa yote,
Na utukufu wake ni juu ya mbingu. (K)

Ni nani aliye mfano wa Bwana,
Mungu wetu aketiye juu;
Anyenyekeaye kutazama,
Mbinguni na duniani? (K)

Humwinua mnyonge kutoka mavumbini,
Na kumpandisha maskini kutoka jaani.
Amketishe pamoja na wakuu,
Pamoja na wakuu wa watu wake. (K)


SHANGILIO 
Yn. 15 :16

Aleluya, aleluya, Ni mimi niliyewachagua ninyi, nikawaweka mwende mkazae matunda, na matunda yenu yapate kukaa. Aleluya.


INJILI 
Yn. 15:9-17

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Kama vile Baba alivyonipenda mimi, nami nilivyowapenda ninyi, kaeni katika pendo langu. Mkizishika amri zangu, mtakaa katika pendo langu; kama vile mimi nilivyozishika amri za Baba yangu na kukaa katika pendo lake. Hayo nimewaambia, ili furaha yangu iwe ndani yenu, na furaha yenu itimizwe.

Amri yangu ndiyo hii, Mpendane, kama nilivyowapenda ninyi. Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake. Ninyi mmekuwa rafiki zangu, mkitenda niwaamuruyo. Siwaiti tena watumwa; kwa maana mtumwa hajui atendalo bwana wake; lakini ninyi nimewaita rafiki; kwa kuwa yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu. Si ninyi mlionichagua mimi, bali ni mimi niliyewachagua ninyi; nami nikawaweka mwende mkazae matunda; na matunda yenu yapate kukaa; ili kwamba lo lote mmwombalo Baba kwa jina langu awapeni. Haya nawaamuru ninyi, mpate kupendana.


Neno la Bwana.........sifa kwako Ee Kristo. 

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MUNGU ASIYE JULIKANA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Pasaka
Jumatano, Mei 13, 2026 
Juma la 6 la Pasaka

Mdo 17: 15, 22-18:1;
Zab 148: 1-2,11-14;
Yn 16:12-15.

MUNGU ASIYE JULIKANA!

Katika somo la kwanza, Mt. Paulo anawavuta watu wa Atheni katika utambuzi kuhusu altare zao walizojenga kwa “Mungu asiye julikana”. Anawaeleza kwamba amekuja kuwafunulia ukweli juu ya huyu Mungu asiye julikana wanaye mwabudu waweze kumtambua yeye ni nani. Wakati mwingine tunamtazamia Mungu ambaye tunataka kumuona au kumshika. Wakati mwingine tunajikuta tunakimbilia mara nyingi sehemu ambazo tunaona Mungu amechorwa katika picha ya kibinadamu. Lakini tunapaswa kutambua kwamba Mungu wetu ni Mungu aliyefichika (Is 45: 15). Amefichika katika ufahamu wetu. Katika wimbo wa kuabudu tunaimba ‘Yafichika machoni Imani yaona’, fahamu haiwezi kutambua fumbo hili bali Imani inatusaidia.

Katika Injili Yesu anatufunulia kuhusu Utatu Mtakatifu. “Roho atakayekuja atachukua kila kilicho changu” (Yn 16:14). “kila alicho nacho Baba ni changu” (Yn 16: 15). Hapa umoja wa Utatu Mtakatifu na asili ya nafsi tatu unafunuliwa.

Hii inamaana kwamba tunapaswa kuwa wazi katika maisha yetu juu ya nguvu na uwepo wa Roho Mtakatifu, yeye aliyebeba ukweli wote. Roho Mtakatifu anapaswa kuwa hai ndani mwetu, akifunua ukweli. Na tukiwa wazi kiakili na mioyo yetu kwa Roho Mtakatifu, tutakuwa watu wakutamani ukweli. Tutakuwa na hamu ya kuelewa vitu ambavyo vitafungua mioyo yetu. Tutakuwa na uwezo wakutazama mambo katika hali ya upya. 

Wewe ni wazi kiasi ghani katika uweli? Ni mara ngapi katika hali ya kweli unakumbatia yote ambayo Mungu ameyafunua kwako? Jifungue zaidi kwa Roho Mtakatifu na tafuta yote ambayo anayafunua kwako. 

Sala: Roho Mtakatifu, ninaomba uje utawale maisha yangu. Nifundishe na kuniongoza katika ukweli wote. Roho Mtakatifu, Bwana Mtakatifu, Baba mwenyewe huruma, nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MEI 13, 2026


MASOMO YA MISA, MEI 13, 2026
JUMA LA 6 LA PASAKA, JUMATANO

SOMO 1 
Mdo. 17 :15, 22-18:1

Siku zile, wale waliomsindikiza Paulo wakampeleka mpaka Athene; nao wakiisha kupokea maagizo kuwapelekea Sila na Timotheo, ya kwamba wasikawie kumfuata, wakaenda zao. Paulo akasimama katikati ya Areopago, akasema, Enyi watu wa Athene, katika mambo yote naona ya kuwa ninyi ni watu wa kutafakari sana mambo ya dini. Kwa sababu nilipokuwa nikipita huko na huko na kuyaona mambo ya ibada yenu, naliona madhabahu iliyoandikwa maneno haya, kwa Mungu asiyejulikana.

Basi mimi nawahubirini habari zake yeye ambaye ninyi mnamwabudu bila kumjua. Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo, yeye, kwa kuwa ni Bwana wa mbingu na nchi, hakai katika hekalu zilizojengwa kwa mikono; wala hatumikiwi kwa mikono ya wanadamu kana kwamba anahitaji kitu cho chote; kwa maana ndiye anayewapa wote uzima na pumzi na vitu vyote. Naye alifanya kila taifa la wanadamu kutoka katika mmoja, wakae juu ya uso wa nchi yote, akiisha kuwawekea nyakati alizoziamuru tangu zamani, na mipaka ya makazi yao; ili wamtafute Mungu, ingawa ni kwa kupapasa-papasa, wakamwone, ijapokuwa hawi mbali na kila mmoja wetu. Kwa maana ndani yake yeye tunaishi, tunakwenda, na kuwa na uhai wetu. Kama vile mmoja wetu, mtunga mashairi alivyosema, Maana sisi sote tu wazao wake.

Basi, kwa kuwa sisi tu wazao wa Mungu, haitupasi kudhani ya kuwa Uungu ni mfano wa dhahabu au fedha au jiwe, vitu vilivyochongwa kwa ustadi na akili za wanadamu. Basi, zamani zile za ujinga Mungu alijifanya kama hazioni; bali sasa anawaagiza watu wote wa kila mahali watubu. Kwa maana ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu yule aliyemchagua; naye amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua katika wafu. Basi waliposikia habari za ufufuo wa wafu wengine walifanya dhihaka; wengine wakasema, Tutakusikiliza tena katika habari hiyo. Basi hivi Paulo akaondoka akawaacha. Baadhi ya watu wakashikamana naye, wakaamini; katika hao alikuwamo Dionisio, Mwareopago, na mwanamke mmoja jina lake Damari, na watu wengine pamoja na hao. Baada ya mambo hayo, Paulo akatoka Athene akafika Korintho.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 148:1-2, 11-14

(K) Utukufu wako unajaza mbingu na ulimwengu. 
Au: Aleluya.

Aleluya. 
Msifuni Bwana kutoka mbinguni;
Msifuni katika mahali palipo juu.
Msifuni. enyi malaika zake wote;
Msifuni, majeshi yake yote. (K)

Wafalme wa dunia, na watu wote,
Wakuu, na makadhi wote wa dunia.
Vijana waume, na wanawali,
Wazee, na watoto. (K)

Na walisifu jina la Bwana,
Maana jina lake peke yake limetukuka;
Adhama yake i juu ya nchi na mbingu. (K)

Naye amewainulia watu wake pembe,
Sifa za watauwa wake wote;
Wana wa Israeli, watu walio karibu naye. (K)


SHANGILIO 
Ufu. 1 : 5

Aleluya, aleluya, 
Ee Kristo, yu shahidi aliye mwaminifu, mzaliwa wa kwanza wa waliokufa, na mkuu wa wafalme wa dunia. 
Aleluya.

INJILI 
Yn. 16:12-15

Siku ile, Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Bado ningali ninayo mengi ya kuwaambia, lakini hamwezi kuyastahimili hivi sasa. Lakini yeye atakapokuja, huyo Roho wa kweli, atawaongoza awatie kwenye kweli yote; kwa maana hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini yote atakayoyasikia atayanena, na mambo yajayo atawapasha habari yake. Yeye atanitukuza mimi; kwa kuwa atatwaa katika yaliyo yangu na kuwapasha habari. Na yote aliyo nayo Baba ni yangu; kwa hiyo nalisema ya kwamba atatwaa katika yaliyo yangu, na kuwapasha habari.

Neno la Bwana... Sifa kwako ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.