Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

KUKIMBILIA KWA YESU



Jumatatu, Februari 9 2026
Juma la 5 la Mwaka

1 Fal8: 1-7.9-13;
Zab 132: 6-10,
Mk 6: 53-56.

KUKIMBILIA KWA YESU

Karibuni ndugu zangu kwa adhimisho la Misa Takatifu asubuhi ya leo. Leo neno la Bwana katika asubuhi ya leo tunaanza kwa kuliangalia somo la kwanza. Leo tunakutana na mfalme Solomoni ndio kamalizia kumjengea Bwana hekalu na leo analipeleka sanduku la Agano ndani ya lile hakalu-kwenye sehemu iitwayo patakatifu pa patakatifu. Na Bwana mara moja anafurahia kukaa ndani ya lile hekalu. Utukufu wake unatanda ndani ya hekalu la Bwana-na kipindi chote hiki Israeli yote ilibarikiwa ardhi ilikuwa na chakula cha kutosha, watu wakawa katika furaha kubwa tu. Bwana alikubali kukaa ndani ya hekalu na kuwabariki watu. Lakini mambo yalibadilika watu walipoanza kutenda dhambi wakiongozwa na mfalme Sulemani. Waliingia katika dhambi za kuitolea dhabihu miungu mingine. Nakwambia Mungu alikasirika. Ile nchi ikalaaniwa, ikawa haizaagi tena hata mazao vizuri, Bwana akawakimbia, mambo yakaanza kuwa magumu, njaa tu, hakuna kitu, na walipoendelea kutenda dhambi Zaidi, Bwana alikimbia kabisa ndani ya lile hakalu na ndipo alipokuja mfalme Nebuchadnezer kuliteketeza hakalu. Ndivyo ilivyo ndugu yangu, Bwana anastahili heshima, apewe haki yake. Ukiwa mtii kwake anakuja na kusafiri nawe katika hali zote, ziwe za shida au raha. Lakini ukikosa utii, anakukimbia.

Katika Injili tunakutana na Yesu akiwaponya watu mbalimbali. Watu wanakwenda kwa Yesu, wanamkimbilia, wanapatiwa ufumbuzi wa magonjwa yao nao wanafurahi. Nasi ndugu zangu siku hizi tunaye Yesu, yupo nasi katika sakramenti. Kwa sakramenti zake, Yesu hutuponya-hiki ni kitu kilichoahidiwa na Yesu. Lakini nasi tuna changamoto kama ilivyowakuta wale watu wa nyakati za sulemani. Kweli Bwana alikubali kukaa kule hekaluni na waliona kwa macho. Lakini wakamkimbiza kwa dhambi. Vile vile na sisi. Bwana hukaa katika sakramenti lakini tukiwa watu wa dhambi na kuzikufuru sakramenti zake, basi tutaishia kukumbwa na hiki kilichowakumba wana wa Israeli. Bwana atatukimbia ndani ya hizo sakramenti. Utazitumia lakini uponyaji hauji kwa sababu ya kukosa heshima na Imani. Tuwe na Imani leo. Ni muhimu. Kabla ya kupokea sakramenti au kuja kanisani au ukiwa katika sala, tuliza mawazo. Sali kwa Imani.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 9, 2026



MASOMO YA MISA, FEBRUARI 9, 2026
JUMATATU YA MWAKA 


SOMO 1
1Fal 8:1-7,9-13

Sulemani alipowakusanya wazee wa Israeli, na wakuu wote wa kabila, wakuu wa mbari za mababa wa wana wa Israeli, wamwendee mfalme Sulemani huko Yerusalemu, ili walipandishe sanduku la agano la Bwana kutoka mji wa Daudi, yaani, Sayuni. Wakakutana mbele ya mfalme Sulemani watu wote wa Israeli wakati wa sikukuu, katika mwezi wa Ethanimu, ndio mwezi wa saba. Wazee wote wa Israeli wakaja, nao makuhani wakajitwika sanduku. Wakalipandisha sanduku la Bwana, na ile hema ya kukutania, na vyombo vitakatifu vyote vilivyokuwa katika ile Hema; vitu hivyo makuhani na Walawi wakavipandisha. Mfalme Sulemani, na mkutano wote wa Israeli waliokutanika kwake, walikuwako pamoja naye mbele ya sanduku, wakichinja sadaka kondoo na ng'ombe, wasioweza kuhesabiwa wala kufahamiwa idadi yao kwa kuwa wengi. Makuhani wakalileta sanduku la agano la Bwana hata mahali pake, katika chumba cha ndani cha ile nyumba, patakatifu pa patakatifu, naam, chini ya mbawa za makerubi. Kwa maana makerubi yalinyosha mbawa zao, juu ya mahali pa sanduku, makerubi yakalifunika lile sanduku na miti yake kwa juu.Hamkuwa na kitu ndani ya sanduku, ila zile mbao mbili za mawe ambazo Musa aliziweka ndani huko Horebu, Bwana alipofanya agano na wana wa Israeli, hapo walipotoka katika nchi ya Misri. Ikawa, makuhani walipotoka katika patakatifu, nyumba ya Bwana ikajaa wingu; hata makuhani hawakuweza kusimama ili kufanya huduma yao, kwa sababu ya wingu lile; kwa kuwa nyumba ya Bwana ilikuwa imejaa utukufu wa Bwana. Ndipo Sulemani akanena, Bwana alisema ya kwamba atakaa katika giza nene. Hakika nimekujengea nyumba ya kukaa, iwe mahali pa makao yako milele.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab 132:6-10

(K) Ee Bwana,uinuke, uende kwenye raha yako

Tazama, tulisikia habari zake katika Efrata,
Katika konde la Yearimu tuliiona.
Na tuingie katika maskani yake,
Tusujudu penye kiti cha kuwekea miguu yake.

Ee Bwana, uinuke, uende kwenye raha yako,
Wewe na sanduku la nguvu zako.
Makuhani wako na wavikwe haki,
Watauwa wako na washangilie.
Kwa ajili ya Daudi, mtumishi wako,
Usiurudishe nyuma uso wa masihi
(K) Ee Bwana,uinuke, uende kwenye raha yako.


SOMO 2
1 Kor. 15:1-11

Ndugu zangu, nawaarifu ile injili niliyowahubiri; ambayo ndiyo mliyoipokea, na katika hiyo mnasimama, na kwa hiyo mnaokolewa; ikiwa mnayashika sana maneno niliyowahubiri; isipokuwa mliamini bure. Kwa maana naliwatolea ninyi hapa mwanzo yale niliyoyapokea mimi mwenyewe, ya kuwa Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu, kama yanenavyo maandiko; na ya kuwa alizikwa; na ya kuwa alifufuka siku ya tatu, kama yanenavyo maandiko; na ya kuwa alimtokea Kefa; tena na wale Thenashara; baadaye aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano pamoja; katika hao wengi wanaishi hata sasa, ila baadhi yao wamelala; baadaye akamtokea Yakobo; tena na mitume wote; na mwisho wa watu wote, alinitokea mimi, kama ni mtu aliyezaliwa si kwa wakati wake. Maana mimi ni mdogo katika mitume, nisiyestahili kuitwa mtume, kwa sababu naliliudhi Kanisa la Mungu. Lakini kwa neema ya Mungu nimekuwa hivi nilivyo; na neema yake iliyo kwangu ilikuwa si bure, bali nalizidi sana kufanya kazi kupita wao wote; wala si mimi, bali ni neema ya Mungu pamoja nami. Basi, kama ni mimi, kama ni wale, ndivyo tuhubirivyo, na ndivyo mlivyoamini.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


SHANGILIO
Mt. 8:17

Aleluya, aleluya,
Aliutwaa udahifu wetu na kuyachukua magonjwa yetu.
Aleluya.


INJILI
Mk 6:53-56

Yesu na wanafunzi wake walipokwisha kuvuka, walifika nchi ya Genesareti, wakatia nanga. Nao wakiisha kutoka mashuani, mara watu walimtambua, wakaenda mbio, wakizunguka nchi ile yote, wakaanza kuwachukua vitandani walio hawawezi, kwenda kila mahali waliposikia kwamba yupo. Na kila alikokwenda, akiingia vijijini, au mijini, au mashambani, wakawaweka wagonjwa sokoni, wakamsihi waguse ngaa pindo la vazi lake; nao wote waliomgusa wakapona.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.
 
Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

CHUMVI NA MWANGA WA DUNIA!



“MBEGU ZA UZIMA”
Tafakari ya kila Jumapili
Jumapili, Februari 8, 2026 
Dominika ya 5 ya Mwaka A wa Kanisa

Isa 58:7-10; 
Zab 112: 4-9; 
1Kor 2: 1-5; 
Mt 5:13-16


CHUMVI NA MWANGA WA DUNIA!

Ukristo sio dini ya mtu binafsi. Ukristo ni mwanga unaokusudiwa kubadili ulimwengu, na wala hamna shaka kuhusu hilo kwamba, kwa kiasi kikubwa, umefanya hivyo. Lakini, inaonekana kwamba baadhi ya wafuasi wanafanya kama vile kucheza mchezo wa “kujificha na kutafuta”. Hawaonyeshi Imani yao au hawaishi Imani yao inavyopaswa. Wakristu wengi wanajificha kwenye kundi. Wanaficha Imani yao kwa kutembea kwenye kundi, wanashirikiana na wengine kwenye mambo ambayo sio ya muumini wa kweli. Tunapo kumbatia dunia na vipimo vyake, bila kujitambua, tunajikuta tumenaswa na Ulimwengu. Tunapo ficha Imani yetu na kuishi, kama vile tu ulimwengu unavyo ishi, ulimwengu unatupepeta unavyopenda. 

Lakini pia, kama unaishi kama mwanga, ukaonyesha upendo wa Kimungu, kukubali mapenzi yake na neema zake, watu watavutwa kwako watakapo kuwa wanakumbana na giza kama vile vipepeo wanavyofuata mwanga usiku. Kuna sababu moja ya sisi kuwa mwanga na chumvi kwa wengine nani kwanjia hiyo watu waweze kuvutwa kwa Mungu kama Bwana wao. Umuhimu wetu wakuishi Injili katika hali ya juu kabisa ni ili kuwavuta watu na kuwaelekeza kwa Mungu ambaye anawapenda na ambaye ndiye furaha ya juu kabisa. Jukumu letu ni kuwaelekeza watu waishi katika Ulimwengu ambao Mungu anapenda sisi tuishi. Hili linawezekana kwa watu wote tena wa kawaida kabisa, hata wasio soma. Sio kitendo cha kuongeza akili bali kushirikishana uzoefu wetu wa kuwa na Mungu. Tukiishi kama chumvi na Mwanga, tunaleta furaha na kiburudisho, matumaini na muongozo kwa wote walio karibu yetu. Watu watatutafuta. 

Chumvi ni kitu cha pekee kabisa kinacho ongeza ladha kwenye chakula. Chumvi yenyewe tu bila chakula haileti ladha sana. Lakini inapo ongezwa kwenye chakula, vyakula mbali mbali, inaingia ndani na kuleta ladha nzuri. Tunakumbushwa kuwa sisi ni “ chumvi na mwanga”. Kama chumvi, hatujaitwa kujijengea umaarufu wetu wenyewe na kuwa wabinafsi. Hatuja umbwa kwa ajili yetu wenyewe. Ni jukumu letu kama Wakristu kuingia katika Ulimwengu wetu, na kuongeza ladha, kwa kuusaidia ubadilike kuwa ulimwengu wa neema na huruma, ulio jaa “ladha” ya Ufalme wa Mungu. Hili linafanywa kwa kujenga uhusiano mwema. Hili linafanywa kwa kugusa maisha ya watu na kuwavuta kwa Kristo. Upendo wa Mungu tunaoleta ulimwenguni, na katika maisha ya wote tunao kutana nao, yataonekana dhahiri kuwa ni chumvi inaingia katika chakula na kuleta ladha. 

Je, tunapotezaje ladha? Kwa maneno mengine, tunashindwaje kuwa “chumvi ya Ulimwengu?’ Tunafanya haya tunapo ingia ulimwenguni, na kushindwa kuishi maisha baada ya maisha yetu kukutana na watu mbali mbali na kushindwa kweli kugusa maisha yao.Wakati maisha yetu mbele ya wengine hayana chochote cha kuongeza au hayana ladha yoyote yakuongeza katika chakula, na hapo matendo yetu yanakuwa kama chumvi ilioisha ladha ambayo ni nzuri tu kwa kutupa na kukanywagwa na watu. Kama tunashindwa kuleta mabadiliko katika maisha ya wengine, tunakosa mwelekeo wa uhusiano na tunashindwa kuwa chumvi ya dunia.

Tutafakari juu ya hili jukumu tulilopewa na Kristo, wito tuliopewa wakuleta mabadiliko duniani katika maisha ya wengine. Watu wanapokuwa katika Imani na upendo kwasababu ya uwepo wako katika maisha yao, tunatimiza agizo la Kristo kwamba sisi ni chumvi na Mwanga wa Ulimwengu. Tujitahidi sisi wenyewe kuwa chumvi ya dunia ili ulimwengu wetu uweze kuwa sehemu nzuri ya kuishi, uliojazwa na ladha ya Ufalme wa Mungu. 

Sala: Bwana, ninajitoa mwenyewe kwa ajili ya huduma yako na kwa ajili ya utukufu wako. Ninakuomba unitumie mimi niweze kuubadili ulimwengu wetu kuwa sehemu takatifu ya kuishi na sehemu ambayo uzuri wako utatawala. Ninakushukuru kwa upendeleo wa kutumiwa nawe na ninaomba unitumie upendavyo katika kuwa mwanga na chumvi ulimwenguni. Yesu, nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 8, 2026



MASOMO YA MISA, FEBRUARI 8, 2026
DOMINIKA YA 5 YA MWAKA A WA KANISA


MWANZO:
Zab. 95:6 – 7
Njoni, tuabudu, tusujudu, tupige magoti mbele za Bwana aliyetuumba; kwa maana ndiye Mungu wetu.


SOMO 1
Isa. 58:7 – 10

Je! Siyo kuwagawia wenye njaa chakula chako, na kuwaleta maskini waliotupwa nje nyumbani kwako? Umwonapo mtu aliye uchi, umvike nguo; wala usijifiche na mtu mwenye damu moja nawe? Ndipo nuru yako itakapopambazuka kama asubuhi, na afya yako itatokea mara; na haki yako itakutangulia; utukufu wa Bwana utakufuata nyuma ukulinde. Ndipo utaita, na Bwana ataitika; utalia, naye atasema, Mimi hapa. Kama ukiiondoa nira; isiwepo kati yako, wala kunyosha kidole, wala kunena maovu; na kama ukimkunjulia mtu mwenye njaa nafsi yako, na kuishibisha nafsi iliyoteswa; ndipo nuru yako itakapopambazuka gizani; na kiwi chako kitakuwa kama adhuhuri.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 112:4 – 9 (K) 4

(K) Nuru huwazukia wenye adili gizani.

Nuru huwazukia wenye adili gizani;
Ana fadhili na huruma na haki.
Heri atendaye fadhili na kukopesha;
Atengenezaye mambo yake kwa haki. (K)

Kwa maana hataondoshwa kamwe;
Mwenye haki atakumbukwa milele.
Hataogopa habari mbaya;
Moyo wake u imara ukimtumaini Bwana. (K)

Moyo wake umethibitika hataogopa,
Hata awaone watesi wake wameshindwa.
Amekirimu na kuwapa maskini,
Haki yake yakaa milele,
Pembe yake itatukuzwa kwa utukufu. (K)



SOMO 2
1Kor. 2:1 – 5

Ndugu zangu, mimi nilipopkuja kwenu, sikuja niwahubiri siri ya Mungu kwa ufasaha wa maneno, wala kwa hekima. Maana naliazimu nisijue neno lolote kwenu ila Yesu Kristo, naye amesulibiwa. Nami nalikuwako kwenu katika hali ya udhaifu na hofu na matetemeko mengi. Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu, ili Imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



SHANGILIO
Mdo. 16:14

Aleluya, aleluya,
Mwanamke mmoja, jina lake Lidia, mwenye kuuza rangi ya zambarau, mwenyeji wa Thiatira, mcha Mungu, akatusikiliza, ambaye moyo wake ulifunguliwa na Bwana, ayatunze maneno yaliyonenwa na Paulo.
Aleluya.



INJILI
Mt. 5:13 – 16

Yesu aliwaambia wafuasi wake: Ninyi ni chumvi ya dunia; lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena kabisa, ila kutupwa nje na kukanyagwa na watu. Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu yam lima. Wala watu hawawashi taa na kuiweka chini ya pishi, bali juu ya kiango; nayo yawaangaza wote waliomo nyumbani. Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

YESU MWENYE HURUMA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Februari 7, 2026
JUMA LA 4 LA MWAKA

1 Fal 3:4-13
Zab 119:9-14 (K)
Mk 6: 14-29.


YESU MWENYE HURUMA!

Yesu ni kiongozi bora mwenye huruma kwa wanyonge katika jamii, mwenye huruma pia kuelekea mahitaji ya binadamu. Baada ya Wanafunzi kurudi kutoka utume kuhubiri, Yesu anapendekeza wapumzike. Lakini yeye mwenyewe, akiacha mahitaji yake kama kupumzika, chakula, nk, alianza kuwahudumia watu, kwa sababu walikuwa na uhitaji mkubwa zaidi. Binadamu kwa kawaida tena mara nying anajifikiria yeye kwanza,( binafsi); na anatimiza mahitaji yake kwanza. Lakini Yesu ni mfano halisi wa kutokuwa na ubinafsi.

Jibu la Yesu linaonesha moyo wenye huruma. Anasukumwa na huruma kwa ajili yao na anaendelea kuwafundisha mambo mengi. Haya yanatokea kwasababu ya sababu nyingi. Kwanza, kwa sababu ya hamu kubwa ya ndani ya watu kuhusu yeye. Walivutwa kwa Yesu, kumsikiliza na kujifunza kwake. Pili, ni kwasababu Yesu alikuwa na hamu kubwa ya kuwa na watu wake. Alitamani kushirikisha moyo wake na wao na kuwachunga kama mchungaji, kuwaongoza kwenye ukweli aliokuja kuufunua. Yesu alikuwa Mchungaji wa kweli aliye wapenda kondoo wake na kuwakaribisha daima. 

Inapaswa iwe hivi pia kwetu sisi. Tunapaswa tutafute daima kuwa naye, kumpenda na kufuata amri zake. Tunapaswa kujitoa bila kuchoka kumtafuta bila kujali ni ugumu ghani tuna upata. Tuna jukumu, kwa upendo tumtafute na kumpata Bwana wetu. Na Yesu, atafanya jukumu lake la kutuchunga na kutuongoza kama mchungaji na kutufundisha mambo mengi. Ataruhusu moyo wake uongozwe na huruma juu yetu na kutuvuta karibu naye.

Kuna msichana mmoja, alikuwa anarudi kutoka shuleni, kwa miguu akiwa pamoja na wadogo zake wawili wakiume. Ghafla theluji ikaanguka ya kutisha. Wakaona kifo kipo mbele yao. Yule Msichana akatoa zile nguo zake mwenyewe za kuzuia baridi akawafunika kaka zake ndani ya nguo zile akawakumbatia, kuwalinda, kama vile alivyoweza, na mwili wake mwenyewe. Badaaye, wazazi wakatoka kwenda kuwatafuta watoto,wakawakuta wale wavulana hai na dada yao amekufa. Wenyeji wa kijiji kile wakajenga mnara wa kumbukumbu pale, wakaandika "Msukumo kwaajili ya kulinda uhai". Je! Imani yako kwa Yesu inakuongoza ufanye nini ? Leo Yesu anatukaribisha na kutuongoza tumuige yeye, je upo tayari?

Sala: Bwana, nakupenda wewe na ninatoa maisha yangu kwako. Ninakuomba unijaze daima na na moto wa kutaka kukutafuta kila siku. Ninakushukuru kwa huruma yako na uchungaji wa roho yangu. Ninaomba nijipumzishe karibu na moyo wako daima. Yesu nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 7, 2026



MASOMO YA MISA, FEBRUARI 7, 2026
JUMAMOSI YA WIKI YA 4 MWAKA

SOMO 1
1 Fal. 3:4-13

Mfalme Sulemani alienda Gibeoni, ilia toe dhabihu huko; kwa kuwa ndipo mahali pa juu palipo pakuu. Sulemani akatoa sadaka elfu za kuteketezwa juu ya madhabahu ile. Na huko Gibeoni Bwana akamtokea Sulemani katika ndoto ya usiku; Mungu akamwambia, Omba utakalo nikupe. Sulemani akasema, Umemfanyia mtumwa wako Daudi baba yangu fadhili kuu, kadiri alivyoenenda mbele zako katika kweli, na katika haki, na katika unyofu wa moyo pamoja nawe; nawe umemwekea na fadhili hii kubwa, maana umempa mwana wa kuketi kitini pake kama ilivyo leo.

Na sasa, Ee Bwana, Mungu wangu, umenitawaza niwe mfalme mimi mtumwa wako badala ya Daudi baba yangu; nami ni mtoto mdogo tu; sijui jinsi inipasavyo kutoka wala kuingia. Na mtumwa wako yu katikati ya watu wako uliowachagua, watu wengi wasioweza kuhesabiwa, wala kufahamiwa idadi yao, kwa kuwa ni wengi. Kwa hiyo nipe mimi mtumwa wako moyo wa adili niwahukumu watu wako, na kupambanua mema na mabaya; maana ni nani awezaye kuwahukumu hawa watu wako walio wengi?

Neno hili likawa jema machoni pa Bwana, ya kuwa Sulemani ameomba neno hili. Mungu akamwambia, Kwa kuwa umeomba neno hili, wala hukujitakia maisha ya siku nyingi; wala hukutaka utajiri kwa nafsi yako; wala hukutaka roho za adui zako; bali umejitakia akili za kujua kuhukumu; basi, tazama, nimefanya kama ulivyosema. Tazama, nimekupa moyo wa hekima na wa akili; hata kabla yako hapakuwa na mtu kama wewe. Na mambo yale usiyoyaomba nimekupa, mali na fahari, hata hapatakuwa na mtu katika wafalme kama wewe, siku zako zote.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 119:9-14 (K) 12

(K) Unifundishe amri zako, ee Bwana.

Jinsi gani kijana aisafishe njia yake?
Kwa kutii akilifuata neno lako.
Kwa moyo wangu wote nimekutafuta,
Usiniache nipotee mbali na maagizo yako. (K)

Moyoni mwangu nimeliweka neno lako,
Nisije nikakutenda dhambi.
Ee Bwana umehimidiwa,
Unifundishe amri zako. (K)

Kwa midomo yangu nimezisimulia
Hukumu zote za kinywa chako.
Nimeifurahia njia ya shuhuda zako
Kana kwamba ni mali mengi. (K)


SHANGILIO
Zab. 119:28, 33

Aleluya, aleluya,
Unitie nguvu sawasawa na neno lako,
Ee Bwana, unifundishe njia ya amri zako.
Aleluya.


INJILI
Mk. 6:30-34

Mitume walikusanyika mbele ya Yesu; wakampa habari za mambo yote waliyoyafanya, na mambo yote waliyoyafundisha. Akawaambia, Njoni ninyi peke yenu kwa faragha; mahali pasipokuwa na watu, mkapumzike kidogo. Kwa sababu walikuwako watu wengi, wakija, wakienda, hata haikuwako nafasi ya kula. Wakaenda zao faragha mashuani, mahali pasipokuwa na watu. Watu wakawaona wakienda zao, na wengi wakatambua, wakaenda huko mbio kwa miguu, toka miji yote, wakatangulia kufika. Naye aliposhuka mashuani, akaona mkutano mkuu, akawahurumia; kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji; akaanza kuwafundisha mambo mengi.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

CHAGUA KULINDA MAISHA!

 


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Tafakari ya kila siku

Ijumaa, Februari 6, 2026,

Juma la 4 la Mwaka wa Kanisa

 

YbS 47: 2-11

Zab 18: 31 47, 50, 51

Mk 6: 14-29.

 

CHAGUA KULINDA MAISHA!

Leo tunaona mwisho na unyong'onyevu wa mwenye haki na asiyeogopa nabii wa kweli Yohani Mbatizaji katika mikono ya mtawala dhalimu, aliye jazwa na tamaa, na picha ya utukufu dhalimu wa uongo wa hadhi na heshima! Herode alifanya makosa makubwa matatu, ambayo mtawala mwenye kuwajibika hapaswi kufanya hivyo. Kwanza, yeye alionesha mfano mbaya, kwa kumuoa mke wa nduguye. Pili, yeye alifanya ahadi ya bila kufikiri kwa yule msichana aliyecheza. Tatu, alihofu watu watasema nini na kujaribu kuokoa heshima yake ya uongo, aliamuru mauaji ya mtu mwenye haki asiye na hatiya. Yohane Mbatizaji.

Hakuna mtu mwenye haki ya kucheza na maisha ya mtu mwingine, iwe katika gereza au katika mitaa au akiwa tumboni. Na waliopo katika madaraka, wana wajibu wa kulinda maisha, na wanalazimika kufikiri mara mbili na kufanya hakika kwamba maisha hayapo hatarini.

Tutafakari leo, kuhusu hali zetu za kila siku za maisha. Je, unapatwa na hasira na kujifanya kuielekeza kwa wengine ambao hawastahili? Tutafakari juu ya tabia hizi na tuangalie kwa undani chanzo chake. Kama ukiona chanzo cha tabia hii ambayo sio nzuri pengine ni kwasababu ya dhambi yako mwenyewe ya maisha yako, tubu kwa hakika na kuimaliza ili Bwana wetu akuweke huru kutoka katika malipo yake.

Mara moja nyuki, ambaye mwenendo wake ulikuwa mzuri na kama asali anayofanya, alikwenda kwa Mungu na kumuomba mafanikio akisema. "Naomba ninapo muuma mtu afe hapo hapo." Mungu akashtuka. Mafanikio mara moja yakabadilishwa na kuwa laana. "Mungu akasema ni sawa. Lakini yule atakayeuma ndiye atakayekufa sio yule atakayeumwa” "Mungu anapenda maisha ya endelee, sio yaharibiwe. 

Sala: Bwana, natubu dhambi zangu zote. Ninasali ili niweze kuziona dhambi zangu kwa uaminifu kabisa na kwa kweli. Ninapo ona dhambi zangu, nisaidie niweze kuziungama niweze kuwa huru na sio aliye elemewa na mzigo wa dhambi. Bwana, ninaomba niyalinde maisha ya aina zote. Ninaomba nijitahidi kuwa mjumbe wa maisha. Yesu nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com 

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 6, 2026

 


MASOMO YA MISA, FEBRUARI 6, 2026

IJUMAA YA 4 MWAKA

KUMBUKUMBU YA WAT. PAULO MIKI NA WENZAKE (Shahidi)


SOMO 1

Ybs. 47:2-11


Kama mafuta yalivyotengwa na kafara ya amani, vivyo hivyo Daudi alitengwa na wana wa Israeli. Naye alicheza pamoja na samba kana kwamba ni wana-mbuzi, pia pamoja na dubu kana kwamba ni wana-kondoo wa kundi.


Je! Hakumwua jitu katika ujana wake, Akawaondolea watu lawama; Alipouinua mkono wake na jiwe la teo, Akayashusha majivuno ya Goliathi? Kwa maana alimwita Aliye juu; Na Yeye akaitia nguvu yamini yake; Ili amwue shujaa hodari wa vita; Ili aiinue pembe ya watu wake.

Kwa hiyo binti za watu wakamtukuza wakiimbiana, na kumheshimu alivyoua makumi elfu yake; naye alipokwisha kuivaa taji ya utukufu, alipigana na adui na kuwashinda pande zote; akajenga maboma yake kati ya Wafilisti, akaivunja pembe yao vipande vipande, hata siku hii ya leo.


Katika kila kazi yake

Daudi alimshukuru Mungu Aliye juu kwa maneno matukufu; na kwa moyo wake wote akampenda Mola wake, akamhimidi kila siku daima. Pia akaweka waimbaji mbele ya madhabahu, ili watoe sauti tamu katika kuimba kwao.


Akauongeza uzuri wa sikukuu, akaziratibisha nyakati katika ukamilifu; pindi walipolihimidi jina takatifu la Bwana, hata patakatifu pakavuma sauti tokea asubuhi na mapema. Naye Bwana akamwondolea dhambi zake, akaiinua pembe yake hata milele; akampa agano la ufalme, na kiti kitakatifu cha enzi katika Israeli.


Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI

Zab. 18:30, 46, 49-50 (K) 46


(K) Atukuzwe Mungu wa wokovu wangu.


Mungu njia yake ni kamilifu,

Ahadi ya Bwana imehakikishwa,

Yeye ndiye ngao yao wote wanaomkimbilia. (K)


Bwana ndiye aliye hai, na ahimidiwe mwamba wangu,

Na atukuzwe Mungu wa wokovu wangu.

Bwana, nitakushukuru kati ya mataifa.

Nami nitaliimbia jina lako. (K)


Ampa mfalme wake wokovu mkuu,

Amfanyia fadhili masihi wake,

Daudi na mzao wake hata milele. (K)


SHANGILIO

Lk. 8:15


Aleluya, aleluya,

Heri wale ambao kwa unyofu na wema wa moyo hulishika neno la Mungu, kasha huzaa matunda kwa kuvumilia.

Aleluya.


INJILI

Mk. 6:14-29


Mfalme Herode alisikia habari; kwa maana jina lake lilikuwa kutangaa, akasema, Yohane Mbatizaji amefufuka katika wafu, na kwa hiyo nguvu hizi zinatenda kazi ndani yake. Wengine walisema, Ni Eliya. Wengine walisema, Huyu ni nabii, au ni kama mmoja wa manabii. Lakini Herode aliposikia, alisema, Yohane mwenyewe alikuwa amefufuka.

Kwa maana Herode mwenyewe alikuwa ametuma watu, akamkamata Yohane, akamfunga gerezani, kwa ajili ya Herodia, mkewe Filipo ndugu yake; kwa kuwa amemwoa; kwa sababu Yohane alimwambia Herode, Si halali kwako kuwa na mke wa nduguyo. Naye yule Herodia akawa akimvizia, akataka kumwua, asipate. Maana Herode alimwogopa Yohane; akimjua kuwa ni mtu wa haki, mtakatifu, akamlinda; na alipokwisha kumsikiliza alifadhaika sana; naye alikuwa akimsikiliza kwa furaha.


Hata ilipotokea siku ya kufaa, na Herode, sikukuu ya kuzaliwa kwake, alipowafanyia karamu wakubwa wake, na majemadari, na watu wenye cheo wa Galilaya; ndipo binti yake yule Herodia alipoingia, akacheza, akampendeza Herode na wale walioketi pamoja naye karamuni. Mfalme akamwambia yule kijana, Niombe lolote utakalo nitakupa, hata nusu ya ufalme wangu. Basi akatoka, akamwuliza mamaye, Niombe nini? Naye akasema, Kichwa cha Yohane Mbatizaji. Mara akaingia kwa haraka mbele ya mfalme, akaomba akisema, Nataka unipe sasa hivi katika kombe kichwa cha Yohane Mbatizaji.


Mfalme akafanya huzuni sana, lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya hao walioketi karamuni, hakutaka kumkatalia. Mara mfalme akatuma askari, akaamuru kuleta kichwa chake. Basi, akaenda, akamkata kichwa mle gerezani, akakileta kichwa chake katika kombe, akampa yule kijana, naye yule kijana akampa mamaye.


Wanafunzi wake waliposikia habari, walikwenda, wakauchukua mwili wake, wakauzika kaburini.


Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

SAFARI ISIYO HITAJI MIZIGO




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Februari 5, 2026

JUMA LA 4 LA MWAKA 

2 Falm
Nya 29:10-12
Mk 6:7-13


SAFARI ISIYO HITAJI MIZIGO


Tunapo safari mara nyingi katika maisha yetu mara nyingi huwa tunabeba mizigo. Lakini mizigo mara nyingi inatufanya tusiwe wepesi sana katika kuendelea na safari yetu bila usumbufu. Ndio hivyo Yesu anawaonya mitume wake wasibebe mizigo wala kushikamana na vitu katatika safari yao ya utume. Kilicho cha muhimu ni kuwa waminifu kwa Mungu. Kutokufungamana na mali au malimwengu ambayo yatakufanya ushindwe kuhubiri neno lake vizuri.

Ndugu yangu jiulize ni jambo gani linalo kufunga ushindwe kuhubiri neno la Mungu vizuri? Je ni pesa? Au mali? Ni mzigo gani unao chelewesha safari yako ya kumtangaza Yesu? Jiulize na muombe Yesu akusaidie kuutua na kuanza safari Upya kwa maisha ya neema.

Sala: Bwana nakuomba unisaidie niweze kushika kiaminifu wito huu wa kutangaza neno lako kama Mkristo. Nisaidie nikushuhudie daima. Amina



Copyright ©2013-2024 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 5, 2026




MASOMO YA MISA, FEBRUARI 5, 2026
ALHAMISI YA JUMA LA 4 LA MWAKA

Kumbukumbu ya Mt Agatha


SOMO 1
1 Falm. 2:1-4, 10-12

Siku ya kufa kwake Daudi ilikaribia, akamwusia Sulemani mwanawe, akasema, Mimi naenda njia ya ulimwengu wote; basi uwe hodari, ujionyeshe kuwa mwanamume; uyashike mausia ya Bwana, Mungu wako, uende katika njia zake, uzishike sheria zake, na amri zake, na hukumu zake, na shuhuda zake, sawasawa na ilivyoandikwa katika torati ya Musa, upate kufanikiwa katika kila ufanyalo, na kila utazamako; ili Bwana afanye imara neno lake alilonena kwa habari yangu, akisema, Ikiwa watoto wako wataiangalia njia yao, wakenda mbele zangu kwa kweli, kwa moyo wao wote, na kwa roho yao yote, (akasema) hutakosa mtu katika kiti cha enzi cha Israeli.

Basi Daudi akalala na babaze, akazikwa mjini mwa Daudi. Na siku alizotawala Daudi juu ya Israeli zilikuwa miaka arobaini; huko Hebraoni alitawala miaka saba, na katika Yerusalemu akatawala miaka thelathini na mitatu. 

Basi Sulemani akaketi katika kiti cha enzi cha Daudi baba yake; na ufalme wake ukawa imara sana.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Nya. 29:10-12 (K) 12

(K) Nawe watawala juu ya vyote, Ee Bwana.

Uhimidiwe, ee Bwana, Mungu wa Israeli baba yetu milele na milele.
Ee Bwana, ukuu ni wako, na uweza, na utukufu,
Na kushinda, na enzi;
Maana vitu vyote vilivyo mbinguni
Na duniani ni vyako. (K)

Ufalme ni wako, Ee Bwana, nawe umetukuzwa,
U mkuu juu ya vitu vyote.
Utajiri na heshima hutoka kwako wewe. (K)

Nawe watawala juu ya vyote;
Na mkononi mwako mna uweza na nguvu;
Mkononi mwako mna kuwatukuza 
Na kuwawezesha wote. (K)


SHANGILIO
Mk. 1:15

Aleluya, aleluya,
Ufalme wa Mungu umekaribia, tubuni na kuiamini Injili.
Aleluya.


INJILI
Mk. 6:7-13

Siku ile Yesu aliwaita wale Thenashara, akaanza kuwatuma wawili wawili, akawapa amri juu ya pepo wachafu; akawakataza wasichukue kitu cha njiani isipokuwa fimbo tu; wala mkate, wala mkoba, wala pesa za bindoni; lakini wajifungie viatu, akasema, Msivae kanzu mbili. Akawaambia, Mahali popote mtakapoingia katika nyumba, kaeni humo hata mtakapotoka mahali pale. Na mahali popote wasipowakaribisha ninyi wala kuwasikia, mtokapo huko, yakung’uteni mavumbi yaliyo chini ya miguu yenu, kuwa ushuhuda kwao. Wakatoka, wakahubiri kwamba watu watubu. Wakatoa pepo wengi, wakapaka mafuta watu wengi waliokuwa wagonjwa, wakawapoza.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.