Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

WATETEA IMANI!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumanne, Julai, 7, 2026 
Tafakari ya kila siku
Juma la 14 la Mwaka wa Kanisa


Hos 8: 4-7, 11-13; 
Zab 115: 3-10; 
Mt 9: 32-38


WATETEA IMANI!

Tukijaribu kufikiria kuhusu mpangilio na muunganiko ulivyo katika Kanisa Katoliki, tukijaribu kurudi tangu mwanzo wa kipindi cha mitume, mafundisho yake, msimamo wake, tamaduni zake zinazoletea faraja, sakramenti mbali mbali, umoja wa mafundisho yake, uongozi wa asili ya mitume, mpangilio wake katika kazi ya watakatifu na mashahidi, liki neemeshwa na naombezi ya Mama wa Bwana wetu Yesu Kristo, tukitizama pia umoja wa uwepo wa Mkombozi wetu juu ya Altare, tunajisikia Kanisa hili, Moja, Takatifu, Katoliki la Mitume limetupatia mpangilo mzuri sana na kuwa jua linalo angaza kuondoa giza. 

Ni hakika, tangu mwanzoni kabisa Kanisa limepingana kwa hali zote na mafundisho ya uongo yaliojaribu kuharibu ujumbe halisi wa mapokeo ya Mitume. Kanisa limebaki aminifu na litaendelea kubaki aminifu kwa kiini cha mafundisho ya Imani juu ya Kristo. 

Sisi pia mara nyingi tumekutana na watu wengi wanaotuuliza maswali kuhusu Imani yetu, na zaidi sana kuhusu kumhesimu Bikira Maria na kumuomba atuombee na pia kuhusu watakatifu au kuhusu sakramenti na zaidi sana sakramenti ya Kitubio na mengine mengi. Huwa tunakabiliano nao vipi? Leo Injili inatufundisha jinsi ya kukabiliana na hali hizo katika maisha yetu. 

Injili inatuambia kwamba, mara nyingi Yesu aliwaonea huruma wale wasiokuwa na msaada, walioteseka na wale waliotengwa. Watu mashuhuri hawakupenda Yesu awape nafasi ya kwanza wadhambi na kula pamoja nao. Lakini Yesu hakuwasikiliza walivyo mlaumu. Kama Yesu tunapaswa kuwa imara tunapotaka kuyumbishwa juu ya Imani yetu na tunu za Injili. Kanisa Katoliki sio Kanisa la Biblia tu, lina Mapokeo Matakatifu (mafundisho ya mitume na mababa wa Kanisa, Mafundisho ya Mababa watakatifu n.k), bahati mbaya au kwakutotaka kuyafahamu wengi wanao uliza maswali haya, hawayajui na zaidi sana hawapo tayari kujifunza kwasababu kwao kama kitu hakijaandikwa kwenye Biblia sio kitu kizuri. Kanisa Katoliki chanzo cha mafundisho yake yamejikita katika Maandiko Matakatifu na Mapokeo Matakatifu (Sacred Tradions), kwahiyo Kanisa Katoliki sio dini ya Biblia tu. Tunapaswa kuwa Makini kuhusu Imani yetu, tusiyumbishwe , tushikilie imara kile tunacho amini, mafundisho yalio asili ya Imani yetu. 

Najaribu kufikiria hivi wale wanaokataa mapokeo, je mapokeo sio matokeo pia ya kusoma Biblia? Hivi wao wanapofafanua Biblia, je, maneno wanayo tumia kufafanua yameandikwa kwenye Biblia? Maneno wanayohubiri Mtu akiyaandika na baadae akaja kuwafundisha watu  je sio mapokeo ambayo yametokana na mtu kusoma Biblia? Ukikataa Mapokeo maana yake umekataa pia watu wasifafanue Biblia kwani, utakavyo fafanua lazima utatumia maneno yako kueleza na ni hakika yatakuwa hayajaandikwa kwenye Biblia. Ni ngumu sana kukataa Mapokeo. Ukikataa mapokeo uwe tayari kuwaambia watu kwamba nikusoma Biblia tu na hakuna kuhubiri kwani mahubiri hayajaandikwa neno kwa neno kwenye Biblia. Tulinde Imani yetu daima.

Sala: Bwana nisaidiye niweze kulinda Imani yangu. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JULAI 7, 2026




MASOMO YA MISA, JULAI 7, 2026
JUMANNE , JUMA LA 14 LA MWAKA


SOMO 1
Hos. 8:4 – 7, 11 – 13

Bwana asema hivi: Wamesimamisha wafalme, lakini si kwa shauri langu; wamejifanyia wakuu, lakini nalikuwa sina habari; kwa fedha yao na dhahabu yao wamejifanyizia sanamu, kusudi wakatiliwe mbali. Amemtupa ndama yako, Ee Samaria; hasira yangu imewaka juu yao; siku ngapi zitapita kabla ya hao kupata hali isiyo na hatia? Maana katika Israeli kimetokea hata na kitu hiki; fundi ndiye aliyekifanya, nacho si mungu kamwe; naam, ndama ya Samaria itavunjiaka vipande vipande. Kwa maana wao hupanda upepo, nao watavuna tufani; nafaka haina bua; machipuko yake hayatoi masuke; hata ikiwa yatoa, wageni watayameza. 

Kwa kuwa Efraimu ameongeza madhabahu kwa dhambi, madhabahu zimekuwa dhambi kwake. Nijapomwandikia sharia yangu katika amri elfu kumi, zimehesabiwa kuwa ni kitu kigeni. Kwa habari za dhabihu za matoleo yangu, hutoa dhabihu ya nyama na kuila; lakini Bwana hawakubali; sasa ataukumbuka uovu wao, na kuwapatiliza dhambi zao; watarudi kwenda Misri.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 115:3 – 10 (K) 9

(K) Enyi Israeli, mtumainini Bwana.

Mungu wetu yuko mbinguni,
Alitakalo lote amelitenda.
Sanamu zao ni fedha na dhahabu,
Kazi ya mikono ya wanadamu. (K)

Zina vinywa lakini hazisemi,
Zina macho lakini hazioni,
Zina masikio lakini hazisikii,
Zina pua lakini hazisikii harufu. (K)

Mikono lakini hazishiki, miguu lakini haziendi,
Wala hazitoi sauti kwa koo zake.
Wazifanyao watafanana nazo,
Kila mmoja anayezitumainia. (K)

Enyi Israeli, mtumaini Bwana;
Yeye ni msaada wao na ngao yao;
Enyi mlango wa Haruni, mtumainini Bwana;
Yeye ni msaada wao na ngao yao. (K)


SHANGILIO
Efe. 1:7, 18

Aleluya, aleluya,
Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, awape roho ya hekima mjue tumaini la mwito wake.
Aleluya.


INJILI
Mt. 9:32 – 39

Walimletea Yesu mtu bubu mwenye pepo. Na pepo alipotolewa, yule bubu alinena, makutano wakastaajabu, wakasema, Haijaonekana hivi katika Israeli wakati wowote. Lakini Mafarisayo wakasema, Kwa nguvu za mkuu wa pepo atoa pepo.
Naye Yesu alikuwa akizunguka katika miji yote na vijiji, akifundisha katika masinagogi yao, na kuihubiri habari njema ya ufalme, na kuponya magonjwa yote na udhaifu wa kila aina.
Na laipowaona makutano, aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji. Ndipo alipowaambia wanafunzi wake, Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache. Basi mwombeni Bwana wa mavuno, apelike watenda kazi katika mavuno yake.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

UPONYAJI WA IMANI!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatatu, Julai, 6, 2026, 
Tafakari ya kila siku
Juma la 14 la Mwaka wa Kanisa

Hos 2: 16-18, 21-22; 
Zab 144: 2-9; 
Mt 9: 18-26


UPONYAJI WA IMANI!


Leo katika Injili, tunaona matukio mawili ya miujiza wa kuponya. Hawa ni watu walio muhitaji Yesu ili waponywe. Tunakutana na watu wengi wanao ulizia kuhusu upendo wa Mungu na kwanini Mungu hawaponyi? Kuna wengine pia wanajiuliza pia kuhusu Imani yao wenyewe wanajisikia kama wangekuwa na Imani kubwa zaidi kwa Mungu ungekuta Mungu amesha waponya. 

Kijana mmoja aliitwa Stefano wa umri wa miaka 18, alipata ajali ya gari na alipata hitilafu katika ubongo wake kiasi cha kushindwa pia kuongea vizuri. Na mwaka mmoja baadaye akadondoka kutoka kwenye paa la nyumba, akapooza kuanzia kwenye kiuno kushuka chini. Daktari akamwambia Stefano hutaweze kutembea tena. Lakini Stefano akamwambia Mungu ameniambia huu ni muda wake wakuniponya. Imani yake ilikuwa ya kweli na hakika, hakuwa na mashaka yeyote kwamba Mungu atamponya. Siku moja watu walikusanyika kumuombea, yeye alienda mbele kwakujivuta na kukaa mbele yao, wakamuombea na kusali sana lakini hali yake ikabaki vile vile. Baada ya hapo watu walimuhuzunikia sana kwa hali yake. Walishangaa sana kwamba alikuwa na Imani na walijiridhisha kwamba atapona lakini wakashangaa sasa Imani yake imekuwaje tena? Baada ya mkutano wao wakamkuta Stefano wakashngaa. Alikuwa hayupo vizuri lakini Imani yake ilikuwa haijayumbishwa. Kwa sauti ya huzuni Stefano alisema “haikuwa muda wangu wakupona lakini siku moja nitasimama na kukimbia”.

Hakika tuna muujiza hapa. Muujiza haukuwa katika miguu yake, bali ulikuwa muujiza wa roho yake. Mwanga wa Yesu ulikuwa ukingaa ndani ya roho yake. Na zaidi ya yote, uponyaji wa mwili ni kwa ajili ya muda mfupi. Bali uponyaji wa roho na Uponyaji wa Imani unadumu kwa ajili ya uzima wa milele. Tumuombe Mungu atusaidie kushughulika zaidi na uponyaji wa Imani yetu na maisha yetu ya kiroho ili tuweze kupata nafasi katika maisha ya milele.

Sala: Bwana naomba uniponye kiroho. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JULAI 6, 2026



MASOMO YA MISA, JULAI 6, 2026
JUMATATU, JUMA 14 LA MWAKA


SOMO 1
Hos. 2:14 – 16, 19 – 20

Bwana asema hivi: Angalia, mimi nitamshawishi, na kumleta nyikani, na kusema naye maneno ya kumtuliza moyo. Naye ataniitikia huko, kama siku zile za ujana wake, na kama siku ile alipopanda kutoka nchi ya Misri. Tena siku hiyo itakuwa, asema Bwana, utaniita Ishi, wala hutaniita tena, Baali. Name nitakuposa uwe wangu kwa milele; naam, nitakuposa kwa haki, na kwa hukumu, na kwa ufadhili, na kwa rehema. Name nitakuposa kwa uaminifu; nawe utamjua Bwana.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 145: 2 – 9 (K) 8

(K) Bwana ana fadhili ni mwingi wa huruma.

Kila siku nitakuhimidi, 
Nitalisifu jina lako milele na milele.
Bwana ndiye mkuu mwenye kusifiwa sana,
Wala ukuu wake hautambulikani. (K)

Kizazi kwa kizazi kitayasifu matendo yako,
Kitayatangaza matendo yako makuu.
Nitaifikiri fahari ya utukufu wa adhama yako,
Na matendo yako yote ya ajabu. (K)

Watu watayataja matendo yako ya kutisha,
Name nitausimulia ukuu wako.
Watalihubiri kumbukumbu la wema wako mkuu,
Wataiimba haki yako. (K)

Bwan ana fadhili, ni mwingi wa huruma,
Si mwepesi kwa hasira, ni mwingi wa rehema.
Bwana ni mwema kwa watu wote,
Na rehema zake zi juu ya kazi zake zote. (K)


SHANGILIO
Yn. 8:12 

Aleluya, aleluya,
Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, asema Bwana, yeye anifuataye hatakwenda gizani kamwe, bali atakuwa na nuru ya uzima.
Aleluya.


INJILI
Mt. 9:18 – 26

Yesu alipokuwa akiwaambia hayo, tazama, akaja jumbe mmoja, akamsujudia, akisema, Binti yangu sasa hivi amekufa; lakini njoo, uweke mkono wako juu yake, naye ataishi. Akaondoka Yesu, akamfuata, pamoja na wanafunzi wake.

Na tazama, mwanamke aliyekuwa na ugonjwa wa kutoka damu muda wa miaka kumi na miwili, alikuja kwa nyuma, akaugusa upindo wa vazi lake. Kwa maana alisema moyoni mwake, Nikigusa tu upindo wa vazi lake nitapona. Yesu akageuka, akamwona, akamwambia, Jipe moyo mkuu, binti yangu, Imani yako imekuponya. Yule mwanamke akapona tangu saa ile.

Yesu alipofika nyumbani kwa yule jumbe, aliona wapiga filimbi, na makutano wakifanya maombolezo, akawaambia, Ondokeni; kwa maana kijana hakufa, amelala tu. Wakamcheka sana. Lakini makutano walipoondoshwa, aliingia, akamshika mkono; yule kijana akasimama. Zikaenea habari hizi katika nchi ile yote.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MUNGU ANAJIFUNUA MWENYEWE KWA MASKINI



"ASALI ITOKAYO MWAMBANI"
Tafakari ya Kila siku
Jumapili, Julai 5, 2026
Dominika ya 14 ya Mwaka

Zak 9:9-10; 
Zab 4:1-2, 8-11, 13-14;
Rom 8:9, 11-13; 
Mt 11: 25-30.


MUNGU ANAJIFUNUA MWENYEWE KWA MASKINI

Jamii ya Wayahudi daima waliongea kuhusu ni nani aliye mkubwa, ambaye anastahili heshima kubwa. Kwa Mungu wa Israeli, ambaye hapinduliwi na miungu ya magharibi, Wagiriki na wa Misri, “ukuu” huu haukukwepeka kwake. Kwa sababu hii Solomon alitangaza na kusema “Yahweh ni mkuu kuliko miungu yote”. (Kut 18:11) na Musa aliwa hakikishia wa Israeli kwamba “Yahweh ni Mungu wa miungu na Bwana wa mabwana. Yeye ni Mungu mkuu na wakutisha sana” (Kumb 10:17). Kwa karne iliopita kabla ya Kristo, ujumbe kuhusu ukuu wa Mungu ulienea sana. Alikuwa, Mungu aliye juu, mkuu (Est 8:12). Lakini tazama Kristo anatokea na hali yake, maskini, asiye na kitu, asiye na jeshi la kumlinda, mwenye mama mdogo anaye mjali. Kuanzia hapo ule ukuu ukashushwa. Uwepo wa mwanadamu ni kutafuta uso wa Mungu. Ni yule mtu tu aliye mnyenyekevu anaweza kuuona uso wa Mungu. Masomo yetu yote matatu yanatufunulia kwamba Mungu hujifunua kwa maskni.

Katika somo la kwanza nabii Zakaria anamtangaza Masiha ambaye ni maskini na myenyekevu. Ilikuwa ni muda ambao Israeli hawakuwa tena huru kama taifa, walikuwa wakikandamizwa na kuonewa na mataifa mengine. Watu wa Mungu walikuwa wanategemea kumpata Masiha ambaye atawakomboa kutoka katika utumwa na utawala wa mataifa hayo. Lakini Zakaria anabadilisha mawazo ya utawala wa Kifalme. Mfalme sio yule ambaye anatumikiwa bali yule anaye waweka watu na kuwajali. Wanyonge hawapaswi kujikabidhi kwake, bali yeye hujikabidhi kwa wanyonge ili aweze kuwahudumia. Nguvu zake ndizo watu wanazo ona kuwa ni dhaifu. Yesu anatatimiza unabii huu katika ukamilifu wote pale anapo ingia Yerusalem akiwa amepanda juu ya mwana punda. Kwa ishara hii anaonesha kwamba yeye ni Amani-Mfalme mpendwa aliye tangazwa na nabii Zakaria.

Katika somo la pili Mt. Paulo anaandika kwa Warumi akionesha hali ambayo mtu anapaswa kuwa nayo ili aweze kumpokea Roho wa Mungu. Anasema kwamba Roho huyu anaweza kupokelewa tu na wanyenyekevu na wale maskini wa roho. Mitume wanaeleze hali mpya ambayo wana wabatizwa wamejiingiza. Wanapaswa kufanya kazi ambazo zinaendana na maisha ya Mungu, kwa matokeo ya Roho Mtakatifu. Kama mtu “atachagua kuishi kwa njia ya mwili amechagua kifo”.

Somo la Injili limeanza na Yesu akishangilia: “Baba, Bwana wa mbingu na Nchi, ninakusifu kwani umewaficha mambo haya wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga.” Ukitazama wafuasi wa Yesu ni wavuvi wa Galilaya, watoza ushuru, watu wa kawaida, wadhambi, wale wote waliotengwa na jamii. Hawa ndio wale watu waliompokea Masiha na sio wale walio jiona wenye ufahamu mkubwa. Ilikuwa vigumu sana kwa Mafarisayo na waandishi kumkubali Yesu kuwa ni Masiha. Kwanza walimkejeli na kutaka kumtupilia mbali. Ilikuwa ni Maskini waliomkaribisha Yesu na kula pamoja naye na kumsikiliza. Walikuwa na akili kama za watoto wadogo kuweza kupokea hekima ya Mungu na sio hekima ya watu wa ulimwengu. Waliteseka kwa kiu ya haki, wakimsubiri Mungu awainue juu na kuwajaza furaha.

Ukweli wa ndani wa watu wa Israeli ilikuwa kwamba Mungu ni rafiki wa wenye haki tu na wema. Lakini Yesu alienda kuwa toa wale ambao tumewatupa mbali. Aliwatazama wale ambao hakuna mtu wa kuwatazama, wanao onekana wadhambi wa mwisho na wasiofaa (Mt 11:19) na makahaba (Mt 21:31) kwani aliwapenda sana aweze kuwaokoa. Kwani Yesu anasema “hakuna amjuae Mwana ila Baba na wala hamna amjuae Baba ila Mwana na yeyote ambaye Mwana apenda kumfunulia”. Neno “kumjua” katika Biblia halimanishi mlikutana au kuwasilana na mtu muda Fulani, ila “kuwa na uzoefu kamili kabisa kuhusu huyo mtu”. Linatumika pia kuonesha kuwa na uhusiano wa ndani kati ya mke na muwe (rej. Lk 1:34). Akili kamili kuhusu Baba inawezekana tu kwa njia ya Mwana. Lakini anaweza kumfumbulia yeyote ampendae kadiri ya mapenzi yake. Ni nani atastahili kupokea ufunuo huu? Wale wadogo kwa hakika. Waandishi na Marabi walijifunza kila nyanja zote za sheria walijiona wao ndio wenye elimu yote kuhusu Mungu. Walibaki wakisema kwamba wana uwezo wakutambua lililo jema. Walijionesha wenyewe kuwa kama mwanga kwa wale walio katika giza, kama walimu kwa wale wajinga, na mabwana wa wale walio wadogo (Rum 2:18-20). Jinsi walivyo jiweka na kujiona wenye hekima na akili ndivyo walivyo jifungia hekima ya Mungu na utambuzi juu yao. 

Mafarisayo na waadishi walikuwa wametengeza dini ya hali ya ajabu, kutengeneza sheria ambazo haikuwezekana kuziishi. “Waliwatwisha watu mizigo ambayo wao wenyewe hawakuigusa kwa vidole vyao” (Lk 11:46). Kwa njia hiyo maskini hawakujisikia tu wanyonge bali walijiona hawafai mbele ya Mungu na hata katika ulimwengu ujao. Kwa maskini na wale walio tengwa Yesu alitangaza uhuru na kuweka dini ya kweli. Aliwaambia wapokee sheria yake ambayo ni laini ambayo inaweza kufupishwa kwa neno la Upendo. Nira yake laini. Kwanza kabisa nira ni yake, si kwasababu anaiweka tu, bali yeye ameiishi kwanza. Nira yake ni tamu kwasababu ni kwa wale tu wanaweza kumpokea wanaweza kufurahia hekima yake na Amani. Mwisho, anatualika tujifunze kutoka kwake, kwani “mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo”. Yesu anajionesha kama mpole na mnyenyekevu. Haya ni maneno ambayo tunayapata kutoka katika zile heri. Hayaoneshi woga, bali yanaonesha unyenyekevu kwa wale wote wanaoteseka kwa ajili yake lakini hawajibu kwa tukano.

Sehemu ya Injili ya leo ni sababu ya tafakari binafsi na tafakari ya jumuiya. Kuishi kwa uyenyekevu ili Mungu aweze kujifunua kwetu kwa ukweli ambao anatamani kutufunulia. Tafuta kukuwa katika unyenyekevu ili Mungu aendelee kujifunua kwako. Kazana daima kuwa mtoto wa Mungu na utakuwa mwenye hekima zaidi na zaidi kuliko jinsi ambavyo ungeweza kuwa kwa nafsi yako mwenyewe.

Sala: Bwana mpendwa, nisaidie mimi niweze kuwa mnyenyekevu na kuwa na Imani ndani yako, na kwa njia ya Imani hii, niweze kufahamu mafumbo matakatifu unayo penda kunifunulia mimi. Nipe hekima na akili Bwana wangu, zaidi ya kile ambacho ningeweza kupata kwa nafsi yangu mwenyewe. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUMAPILI, JULAI 5, 2026



MASOMO YA MISA, JUMAPILI, JULAI 5, 2026
DOMINIKA YA 14 YA MWAKA


SOMO 1
Zek. 9:9-10

Furahi sana, Ee binti Sayuni; Piga kelele, Ee binti Yerusalemu; Ni mwenye haki, naye ana wokovu; Ni mnyenyekevu, amepanda punda, Naam, mwana-punda, mtoto wa punda.

Na gari la vita nitaliondoa liwe mbali na Efraimu, na farasi awe mbali na Yerusalemu, na upinde wa vita utaondolewa mbali; naye atawahubiri mataifa yote habari za Amani; na mamlaka yake yatakuwa toka bahari hata bahari, na toka Mto hata miisho ya dunia.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 145:1-2, 8-11, 14, 17 (K) 1

(K) Nitalihimidi jina lako milele na milele.

Ee Mungu wangu, Mfalme, nitakutukuza,
Nitalihimidi jina lako milele na milele.
Kila siku nitakuhimidi,
Nitalisifu jina lako milele na milele. (K)

Bwana ana fadhili, ni mwingi wa huruma,
Si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema.
Bwana ni mwema kwa watu wote,
Na rehema zake zi juu ya kazi zake zote. (K)

Ee Bwana, kazi zako zote zitakushukuru,
Na wacha Mungu wako watakuhimidi.
Wataunena utukufu wa ufalme wako. (K)

Bwana ni mwenye haki katika njia zake zote,
Na mwenye fadhili juu ya kazi zako zote.
Bwana huwategemeza wote waangukao,
Huwainua wote walioinama chini. (K)


SOMO 2
Rum. 8:9, 11-13

Roho wa Mungu anakaa ndani yenu, ninyi hamwufuati mwili; bali mwaifuata roho. Lakini mtu awaye yote asipokuwa na Roho wa Kristo, huyo si wake. Lakini, ikiwa Roho wake yeye aliyemfufua Yesu katika wafu anakaa ndani yenu, yeye aliyemfufua Kristo Yesu katika wafu ataihuisha na miili yenu iliyo katika hali ya kufa, kwa Roho wake anayekaa ndani yenu. Basi, kama ni hivyo, ndugu, tu wadeni, si wa mwili tuishi kwa kufuata mambo ya mwili; kwa maana kama mkiishi kwa kufuata mambo ya mwili, mwataka kufa; bali kama mkiyafisha matendo ya mwili kwa Roho, mtaishi.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


SHANGILIO
1Sam. 3:9; Yn. 6:68
Aleluya, aleluya,
Nena, Bwana, kwa kuwa mtumishi wako anasikia; 
Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.
Aleluya.


INJILI
Mt. 11:25 – 30

Wakati ule Yesu alijibu, akasema, Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga. Naam, Baba, kuwa kwa ndivyo ilivyopendeza mbele zako. Akasema, Nimekabidhiwa vyote na baba yangu; wala hakuna amjuaye Mwana, ila Baba; wala hakuna amjuaye Baba, ila Mwana, na yeyote ambaye Mwana apenda kumfunulia.

Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.

Neno la Bwana........Sifa kwako Ee Kristo


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

YESU, DIRA YA FURAHA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumamosi, Julai 4, 2026 
Tafakari ya kila siku
Juma la 13 la Mwaka wa Kanisa


Amo 9:11-15; 
Zab 84:9-14; 
Mt 9:14-17

YESU, DIRA YA FURAHA!

Dira ni kifaa kinachotumika na watu kama wanajeshi, nahodha nk. Masomo ya leo ni kama dira, yana tufunulia Umungu wa kweli ndani ya Yesu. Kama dira inavyo muongoza nahodha ili kufika mwisho wa safari yake. Pia Yesu ni dira yetu anatuongoza ili tufike kwenye furaha ya milele. Lakini furaha hii haipatikani hivi hivi, ni lazima kupitia mawimbi mbali mbali kama nahodha anapopitia njia mbali mbali na sehemu asioijua ili kufikia lengo lake, Yesu ni nahodha pekee aliyekuwa na hakika ya ushindi wake, mateso, kifo na ufufuko. Hata njia yetu itakuwa hivyo hivyo. Pili maisha yetu ni kama kioo kinacho tuonesha jinsi tulivyo. Lakini tunapomchukua Yesu, kama divai mpya na mawazo mapya na mtazamo mpya wa ukweli, yeye anakuwa kioo chetu cha kumulika maisha yetu nakutambua ukweli halisi ya kuwa tunapaswa kuwa tofauti zaidi na jinsi tulivyo sasa. Maisha ya zamani tuliyo jijengea yenye sheria ngumu na tena nyingine zenye ubinafsi na chovu au mambo mengine yanayopingana na upendo wa Yesu yanapaswa yaondolewe na kuwa kiumbe kipya na kuweka mambo mapya yaliosimikwa katika upendo wa Yesu.

Kwahiyo kuna ulazima wa kubadili maisha yetu. Kwakumuweka Yesu kama kioo mbele yetu ili amulike maisha yetu. Hapo tutaona nafsi yetu ilivyo tofauti na nafsi ya Yesu ambaye sisi wote tumeitwa kuishi maisha yake. Maisha yangu yanapaswa yawe kama maisha ya Yesu, kama nashindwa kuishi kama Yesu alivyo basi napaswa kubadili mienendo yangu. Tutafute ukweli kuhusu nafsi zetu zaidi na tuondoe ile hali yakutaka kujua tuu ukweli kuhusu maisha yawengine na kuficha yetu. Tunapoteza muda mno kutaka kujua nafsi za wengine, tuanze na nafsi zetu na moja kwa moja mafanikio yataonekana na wengine. Tuombee neema ya Mungu ituongoze ili tuweze kubadili maisha yetu kwanza katika kweli ya Yesu kabla hatuja thubutu kuwarekebisha wengine.
Sala: Nitafurahi katika Bwana, nitamtukuza Mungu mwokozi wangu. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JULAI 4 2026



MASOMO YA MISA, JULAI 4, 2026
JUMAMOSI, JUMA LA 13 LA MWAKA
SOMO 1
Amo. 9:11 – 15

Bwana asema hivi: Siku hiyo nitaiinua tena maskani ya Daudi iliyoanguka, na kuziba mahali palipobomoka; nami nitayainua magofu yake, na kuyajenga kama siku za kale; wapate kuyamiliki mabaki ya Edomu, na mataifa yote yaitwayo kwa jina langu, asema Bwana, afanyaye hayo. Angalieni, siku zinakuja, asema Bwana, ambazo huyo alimaye atamfikilia avunaye, na yeye akanyagaye zabibu atamfikilia apandaye mbegu; nayo milima itadondoza divai tamu, na vilima vyote vitayeyuka. Nami nitawarejeza tena watu wangu Israeli waliohamishwa, nao wataijenga miji iliyoachwa maganjo, na kukaa ndani yake; nao watapanda mizabibu katika mashamba, na kunywa divai yake; nao watafanyiza bustani, na kula matunda yake. Nami nitawapanda katika nchi yao, wala hawatang’olewa tena watoke katika nchi yao niliyowapa, asema Bwana, Mungu wako.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 85:8, 10 – 13 (K) 8

(K) Bwana anawaambia watu wake amani.

Nisikie atakavyosema Mungu Bwana,
maana atawaambia watu wake amani.
Naam, na watauwa wake pia.
Bali wasiurudie upumbavu tena. (K) 

Fadhili na kweli zimekutana,
haki na amani zimebusiana.
Kweli imechipuka katika nchi,
haki imechungulia kutoka mbinguni. (K)

Naam, Bwana atatoa kilicho chema,
na nchi itatoa mazao yake.
Haki itakwenda mbele zake, 
nayo itazifanya hatua zake kuwa njia. (K)


SHANGILIO
Mt. 11:25

Aleluya, aleluya,
Nashukuru Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili ukawafunulia watoto wachanga.
Aleluya.


INJILI
Mt. 9:14 – 17

Wanafunzi wake Yohane walimwendea Yesu wakasema, Kwa nini sisi na Mafarisayo twafunga, bali wanafunzi wako hawafungi? Yesu akawaambia, walioalikwa arusini wawezaje kuomboleza, muda bwana arusi akiwapo pamoja nao? Lakini siku zitakuja watakapoondolewa bwana arusi; ndipo watakapofunga. Hakuna mtu atiaye kiraka cha nguo mpya katika vazi kuukuu; maana kile kilichotiwa huondoa kipande cha lile vazi, na pale palipotatuka huzidi. Wala watu hawatii divai mpya katika viriba vikuukuu; na kama wakitia, vile viriba hupasuka, divai ikamwagika, na viriba vikaharibika; bali hutia divai mpya katika viriba vipya, vikahifadhika vyote.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

KUTOA USHUHUDA KWA YESU MFUFUKA



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Ijumaa, Julai 3, 2026
Juma la 13 la Mwaka

Kumbukumbu ya Mt. Tomasi Mtume. 

Ef 2: 19-22; 
Zab 116: 1-2;
Yn 20: 24-29.

KUTOA USHUHUDA KWA YESU MFUFUKA!

Leo tuna sheherekea sikukuu ya Mt. Thomasi, Mtume. Thomas ni maarufu sana kwa maswali yake aliyeyaleta, na tunaweza kutulia kwasababu ya maneno ya kwanza aliyosema Yesu, wakati Tomasi akiwa na mashaka: “Amani iwe nanyi”. Yesu hakumwaibisha au kupatwa na hasira bali alimpa Amani. Yesu ambaye anatufahamu sisi katika ubinadamu wetu na ambaye anatufahamu undani wetu kabisa, anatupatia  sisi amani wakati tukiwa katika hofu na mashaka yetu. Wakati Thomasi anatoa ishara kwa ajili ya ombi lake la kuingia katika hali hiyo ya Imani au kuamini, haombi kitu kigeni zaidi ya ile Imani ambayo kila mfuasi alikuwa ameshapokea. Ni wazi kwamba yeye alitaka kupata naye muda wakushuhudia kama wengine walivyo fanya-kabla haja amini jambo hilo kubwa linalo shangaza. 

Lakini tukio haliishi hapa, kwa Yohane au kwa Bwana mfufuka mwenyewe anaendelea na kusema “je, una amini kwasababu umeniona? Wana heri wale wasio ona na kuamini”. Kwetu sisi maneno haya ni ya muhimu sana. Kwasababu hatukuona, sasa inakuwaje tuna amini? Tomasi hakuweza kuamini mpaka alipo ona. Petro hakuweza kaumini mpaka alivyo ona. Maria Magdalena hakuweza kuamini mpaka alivyo ona. Sasa tuta aminije wakati sisi hatujaona? Inawezekana kwasababu sisi tumesha barikiwa, “wamebarikiwa wale wasio ona lakini wana amini.”. Ni lazima tutambue na kukubali kwamba Imani yetu sio kutokana na juhudi zetu wenyewe au labda dini tunayo fuata bali ni “zawadi ya pekee kutoka kwa Mungu”. Mungu Baba ametupa kitu ambacho kina saidia Imani yetu kwa Bwana mfufuka iwezekane-hata pale ambapo hatuja muona Yesu mfufuka kwa macho yetu ya kibinadamu. 

Sala: Bwana, imarisha Imani yangu kama Tomasi alivyolia “Bwana wangu na Mungu wangu”. Yesu nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JULAI 3, 2026




MASOMO YA MISA, JULAI 3, 2026
IJUMAA, JUMA LA 13 LA MWAKA

SIKUKUU YA MTAKATIFU TOMA, MTUME


SOMO 1 
Efe. 2:19-22

Tangu sasa ninyi si wageni wala wapitaji, bali ninyi ni wenyeji pamoja na watakatifu, watu wa nyumbani mwake Mungu. Mmejengwa juu ya msingi wa mitume na manabii, naye Kristo Yesu mwenyewe ni jiwe kuu la pembeni. Katika yeye jengo lote linaungamanishwa vema na kukua hata liwe hekalu takatifu katika Bwana. Katika yeye ninyi nanyi mnajengwa pamoja kuwa maskani ya Mungu katika Roho.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 117 (K) Mk. 16:15 

(K) Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili.

Aleluya.
Enyi mataifa wote, mhimidini. 
enyi watu wote, mhimidini. (K)

Maana fadhili zake kwetu sisi ni kuu, 
na uaminifu wa Bwana ni wa milele. (K)


SHANGILIO 
Yn. 20 : 29

Aleluya, aleluya, 
Wewe, Tomaso, kwa kuwa umeniona, umesadiki, wa heri wale wasioona, wakasadiki. 
Aleluya.


INJILI 
Yn. 20 :24-29

Mmoja wa wale Thenashara, Tomaso, aitwaye Pacha, hakuwako pamoja nao alipokuja Yesu Basi wanafunzi wengine wakamwambia, Tumemwona Bwana. Akawaambia, Mimi nisipoziona mikononi mwake kovu za misumari, na kutia kidole changu katika mahali pa misumari, na kutia mkono wangu katika ubavu wake, mimi sisadiki hata kidogo. Basi, baada ya siku nane, wanafunzi wake walikuwamo ndani tena, na Tomaso pamoja nao. Akaja Yesu, na milango imefungwa, akasimama katikati, akasema, Amani iwe kwenu. Kisha akamwambia Tomaso, Lete hapa kidole chako, uitazame mikono yangu; ulete na mkono wako uutie ubavuni mwangu; wala usiwe asiyeamini, bali aaminiye. Tomaso akajibu, akamwambia, Bwana wangu na Mungu wangu! Yesu akamwambia, Wewe, kwa kuwa umeniona, umesadiki; wa heri wale wasioona, wakasadiki.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.