Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

KWARESIMA: MUDA WA KUMFAHAMU YESU!



“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Jumapili, Machi 1, 2026.
Dominika ya 2 ya Kwaresima

Mwa 1:1-4;
Zab 33:4-5, 18-22;
2 Tim 1:8-10;
Mt 17: 1-9.



KWARESIMA: MUDA WA KUMFAHAMU YESU!



Juma la kwanza la Kwaresima linatuandaa, kufanya matendo ya kwaresima, kusali, kufunga na kutoa sadaka. Inakuwa ni hatua kwetu kutengeneza hali nzuri ya kuingia katika kipindi hichi kwa undani. Jumapili iliopita ilituandaa kuhusu majaribu, na umuhimu wa kusafisha dhambi zetu rohoni mwetu. Yesu alituanyesha njia ya kumshinda shetani na dunia na pia vishawishi vya miili yetu, alipokuwa jangwani. Leo anajifunua kwa njia ya Kugeuka sura kutualika wote kwenye utukufu alio nao na Baba yake. Kwa njia ya kungara sura tunaalikwa kwenye ufufuko wa miili, wakati tutakapo kuwa huru kuhusu dhambi. Kama mwili wa Yesu ulivyokuwa katika utukufu, ndivyo miili ya watakatifu itangaa. “Utukufu ulionipa mimi nimewapa wao” (Yn 17:22).

Uhusiano unakuwa kadiri ya muda. Tunawafahamu watu zaidi kadiri ya muda unavyo sogea. Mitume pia lazima na wao waliendelea kumfahamu Yesu kadiri ya muda ulivyokuwa ukisogea. Uhusiano wao ulianza alivyo waita hapo awali. Waliishi naye na kumsikiliza na kushuhudia miujiza na uponyaji mbali mbali. Uelewa wao lazima utakuwa ulikuwa kadiri ya muda, mpaka Petro akafikia kiwango cha kusema “Wewe ni Masiha Mwana wa Mungu aliye hai”. Lakini Petro alimpinga alivyosikia habari ya kifo chake, na Yesu alitambua kuwa Wafuasi wake hawajamfahamu vizuri bado. Walimwelewa vibaya kuwa kama Masiha wa kidunia atakaye iongoza dunia daima. Ndio, maana baada ya siku sita hivi Yesu awaliwachagua Petro, Yohane na Yakobo kwenda mlima na kushuhudia kungara kwake kwa sura inayoelezewa leo katika Injili.

Kungara sura kwa Yesu kunatokea wakiwa juu ya milima. Mlimani palijulikna kama sehemu ya kukutana na Mungu. Wakati Yesu anageuka sura mavazi yake yalingaa sana na uso wake ulingara. Taswira hii alioionyesha Yesu ni hali ya utukufu ambayo itakuja baada ya maisha ya ulimwengu huu. Musa na Elia ambao katika tamaduni ya Wayahudi waliwakilisha mambo mawili muhimu ya Wayahudi. Sheria na Manabii. Musa na Elia walikuwa ni watu ambao walipata kuwasiliana na Mungu wakiwa katika milima. Na waliwaongoza watu wa Israeli kumrudia Mungu.

Kwa kuangalia hali hii ya kugusa na kuogopesha, Petro anaomba kujengwe vibanda vitatu kimoja cha Yesu, kimoja cha Elia na kimoja cha Musa. Petro alipenda hii hali iendelee kuwapo. Mungu anaingia kati na kumfunua mwanae (Mwana wa Mungu) kwa wafuasi “Huyu ndiye Mwanangu mpendwa…” Mitume wanaogopa na wanainamisha nyuso zao. Walivyo nyanyuka walikuta kila kitu kikiwa katika hali yakawaida. Tukio hili ni lazima lilikuwa ni la nguvu sana kuliko tukio lolote lile ambalo mitume hawa watatu waliweza kulishuhudia. Katika tukio hili la kungara sura, Umungu wa Yesu ulifunuliwa kwao. Waliweza kufahamu Yesu ni nani na kwanini Yesu alikuwa akiongelea kuhusu kifo na ufufuko . wafuasi waliweza kuja kumfahamu Yesu vizuri zaidi wakati wa Karamu ya mwisho, mateso yake alivyokuwa pale Getsemane, mateso yake, kifo na kufufuka. Muda wote waliokuwa na Yesu waliweza kuja kumfahamu Yesu na kutambua nini maana ya kuwa wafuasi. Nasi ni hivyo hivyo.

Katika somo la kwanza tunasikia kuhusu kuitwa kwa Abrahamu. Abrahamu anajibu wito wa kwanza kabisa wa Mungu. Na ni baada ya muda tu alikuja kumfahamu Mungu vizuri na utume wake kwa ajili yake. Hivyo, tunavyopata muda wa kuwa na Mungu zaidi ndivyo tunavyozidi kuendelea kumfahamu zaidi, na kadiri tunayo endelea kumfahamu Mungu, ndivyo tunavyo fahamu mpango wake kwetu.

Kwaresima ni kipindi cha kutafakari na kukaribisha neema ya Mungu katika maisha yetu. Sio muda tu wakuachia vitu, bali pia ni muda wakupokea zawadi kubwa kutoka kwa Mungu. Mungu hajatusahau sisi watoto wake ila ni sisi tuliomsahau yeye na kukimbia uso wake. Leo, upendo unafunuliwa kwetu kwa njia ya Yesu. Yesu kwa njia ya ufufuko anatufanya sisi kuwa sehemu ya mpango wa Mungu tangu milele, kuwa watakatifu na kupendwa na Mungu kwa kuwa daima mbele zake. Ufufuko unaleta kwetu mwanga katika maisha yetu kama wa kungara sura kwa Yesu, kiasi kwamba hakuna giza linalo baki.

Maandiko matakatifu yanatuonesha njia ya kwenda katika muelekeo huu. Kwanza kabisa, kuwa na muda wa kusali kama Yesu. Pili ni kumfahamu Yesu, na hili linafanyika kwa kutafakari Maandiko Matakatifu, Mungu aliwaambia wafuasi kwamba “Msikilizeni yeye” pia Neno la Mungu linafunua nafsi ya Yesu kwetu sisi kila siku. Tatu, tuwe tumeungana katika jumuiya zetu. Kama mitume watatu walivyo pata kumshuhudia Yesu, na kushiriki katika mwanga uliofunuliwa na Mungu. Hili linawezekana daima tunavyo shiriki katika Ekaristi Takatifu, tunaitwa wote kuunganika katika kungara kwa Yesu katika Ekaristi takatifu. Na mwisho kabisa, kushiriki katika mahusiano mazuri na wenzetu. Mitume hawakuweza kushirikisha walio yaona muda ule, bali walishirikisha baada ya ufufuko wakati wamesha elewa maana kamili ya kungara kwake sura, walishirikisha wengine kwa kuhubiri habari Njema. Sisi pia tunaitwa kutangaza kungara kwa sura kwa Yesu kwa kuwatangazia wale wote waliotengwa. Tunaitwa kutambua matendo ya roho na matendo ya nje ya huruma: kuwalisha maskini, kuwapa maji walio na kiu, kuwavisha wasio na nguo, kuwakaribisha wasio na makao, kuwaponya wagonjwa, kutembelea wafungwa, kuwazika wafu, , kuwasaidia walio na mashaka, kuwaelekeza walio wajinga, kuwa elekeza wadhambi warudi, kuwafariji wenye matatizo, kuwasamehe walio tukosea, kuchukuliana kwa huruma wale wote wanao tuumiza na kuwaombea walio wazima na wafu.

Sala: Bwana, ninaomba nifarijike kwa utukufu wako na ukweli wako. Ninaomba nikumbuke utukufu huu ninapo tembea katika changamoto mbali mbali katika maisha. Utatembea mbele yangu na kunitangulia nikikuamini wewe. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MACHI 1, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 1, 2026
JUMAPILI YA 2 YA KWARESIMA



SOMO 1
Mwa. 12:1 – 4a

Bwana akamwambia Abramu, Toka wewe katika nchi yako, na jamaa zako, na nyumba ya baba yako, uende mpaka nchi nitakayokuonyesha; nami nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa, na kukubariki, na kulitukuza jina lako; nawe uwe Baraka; nami nitawabariki wakubarikio, naye akulaaniye nitamlaani; na katika wewe jamaa zote za dunia watabarikiwa.

Basi Abramu akaenda, kama Bwana alivyomwamuru.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 33:4 – 5, 18 – 20, 22 (K) 22

(K) Ee Bwana, fadhili zako zikae nasi,
Kama vile tulivyokungoja Wewe.

Kwa kuwa neno la Bwana lina adili,
Na kazi yake yote huitenda kwa uaminifu.
Huzipenda haki na hukumu,
Nchi imejaa fadhili za Bwana. (K)

Tazama, jicho la Bwana li kwao wamchao,
Wazingojeao fadhili zake.
Yeye huwaponya nafsi zao na mauti,
Na kuwahuisha wakati wa njaa. (K)

Nafsi zetu zinamngoja Bwana;
Yeye ndiye msaada wetu na ngao yetu.
Ee Bwana, fadhili zako zikae nasi,
Kama vile tulivyokungoja Wewe. (K)



SOMO 2
2Tim. 1:8b – 10

Uvumilie mabaya pamoja nami kwa ajili ya Injili, kwa kadiri ya nguvu ya Mungu; ambaye alituokoa akatuita kwa mwito mtakatifu, si kwa kadiri ya matendo yetu sisi, bali kwa kadiri ya makusudi yake yeye na neema yake. Neema hiyo tulipewa katika Kristo Yesu tangu milele, na sasa inadhihirishwa kwa kufunuliwa kwake Mwokozi wetu Kristo Yesu; aliyebatili mauti, na kuufunua uzima na kutokuharibika, kwa ile Injili.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



SHANGILIO
Mt. 17:5

Sauti ya Baba ilitoka katika wingu jeupe: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, msikieni yeye.”



INJILI
Mt. 17:1 – 9

Yesu akawatwaa Petro, na Yakobo, na Yohane nduguye, akawaleta juu yam lima mrefu faraghani; akageuka sura yake mbele yao; uso wake ukang’aa kama jua, mavazi yake yakawa meupe kama nuru. Na tazama, wakatokewa na Musa na Eliya, wakizungumza naye.

Petro akajibu akamwambia Yesu, Bwana, ni vizuri sisi kuwapo hapa; ukitaka, nitafanya hapa vibanda vitatu, kimoja chako wewe, na kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya.

Alipokuwa katika kusema, tazama, wingu jeupe likawatia uvuli; na tazama, sauti ikatoka katika lile wingu, ikasema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye; msikieni yeye. Na wale wanafunzi waliposikia, walianguka kifulifuli, wakaogopa sana.

Yesu akaja, akawagusa, akasema, Inukeni, wala msiogope. Wakainua macho mlimani, Yesu aliwaagiza, akasema, Msimwambie mtu yeyote habari ya maono hayo, hata Mwana wa Adamu atakapofufuka katika wafu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUTAMANI KUWA MKAMILIFU!





“KWARESIMA YA UKARIMU”
Jumamosi, Februari 28, 2026,
Juma la 1 la Kwaresima


Kumb 26: 16-19;
Zab 119: 1-2, 4-5, 7-8;
Mt 5: 43-48



KUTAMANI KUWA MKAMILIFU!


Liturujia ya leo inalenga katika Sheria ya Mungu, ambayo Mungu ametupa kwa njia ya Musa ili kuifuata kwa moyo na nafsi nzima. Katika Injili, tunaona Yesu, analeta upendo wenye athari kubwa, zaidi kuliko wowote ule ambao waliutenda kabla. Kumpenda kila mtu, bila kuwa na fikra au sababu yeyote ile, bila kujali kama wao wanatupenda sisi au la, bila kufikiria wanatuwazia mabaya au mazuri?

Yesu wakati alipokuwa dunia hii, alikabiliwa na upinzani sana, kutoka kwa mamlaka ya kidini, kutoka kwenye mamlaka ya kisiasa, kutoka mji wake mwenyewe, kutoka kwa baadhi ya wanafunzi wake mwenyewe. Hata hivyo, yeye amewapenda daima wote. Ujumbe wake wa huruma au wa kubadilika mara zote ulijawa na upendo mkuu. Hata juu ya Msalaba, aliwatazama kwa huruma watesi wake. Upendo kwa Mungu na kwa jirani huenda pamoja, na hauwezi kutenganishwa. Mt. Yohane anaweka wazi kwamba, “Mtu akisema, “Nampenda Mungu,” naye anamchukia ndugu yake, ni mwongo (1Yoh 4:20). 

Leo tunapewa changamoto na upendo huu wa Yesu Kristo. Tumekuwa mara nyingi sana watu ambao tunabagua wengine, juu ya rangi, dini, jinsia, kabila, juu ya tabaka, utaifa, juu ya hadhi ya jamii, utamaduni, elimu, kiasi cha mali ulicho nacho nk, Je, tunaweza kuamua kumwiga Yesu kuanzia sasa na kuendelea? Je, tunaweza kuwapenda wale wote ambao wametuumiza katika maisha yetu? Wale wanaotutesa kwasababu ya utamaduni wetu, dini yetu,au mawazo yetu? Yesu alishinda haya yote kwa upendo wake, Je, sisi twaweza kufanya hivyo tushinde kwa njia ya upendo?

Sala: Bwana, ninataka kuwa mtakatifu. Ninataka kuwa mtakatifu kama wewe ulivyo mtakatifu. Nisaidie niishi kila wakati kwa ajili yako. Ninatoa muda wangu wote kwa ajili yako. Yesu, nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 28, 2026



MASOMO YA MISA, FEBRUARI 28, 2026
JUMAMOSI JUMA LA 1 LA KWARESIMA


SOMO 1
Kumb. 26:16-19

Musa aliwaambia watu: Leo hivi akuamuru Bwana, Mungu wako, kuzifanya amri hizi na hukumu; basi uzishike na kuzifanya kwa moyo wako wote na roho yako yote.

Umemwungama Bwana leo, kuwa ndiye Mungu wako, na kuwa yakupasa kutembea katika njia zake, na kushika amri zake na maagizo yake, na hukumu zake, na kusikiza sauti yake; naye Bwana amekuungama hivi leo kuwa taifa iliyotengwa iwe yake yeye, kama alivyokuahidi, na kuwa yakupasa kushika maagizo yake yote; na kuwa atakutukuza juu ya mataifa yote aliyoyafanya kwa sifa, na jina na heshima, nawe upate kuwa taifa takatifu kwa Bwana Mungu wako, kama alivyosema.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 119:1-2, 4-5, 7-8

(K) Heri walio kamili njia zao, Waendao katika sheria ya Bwana.

Heri walio kamili njia zao,
Waendao katika sheria ya Bwana.
Heri wazitiio shuhuda zake,
Wamtafutao kwa moyo wote. (K)

Wewe umetuamuru mausia yako,
Ili sisi tuyatii sana.
Ningependa njia zangu ziwe thabiti,
Nizitii amri zako. (K)

Nitakushukuru kwa unyofu wa moyo,
Nikiisha kujifunza hukumu za haki yako.
Nitazitii amri zako,
Usiniache kabisa. (K)


SHANGILIO
Amo. 5:14

Tafuteni mema, wala si mabaya, mpate kuishi, hivyo Bwana, atakuwa pamoja nanyi.


INJILI
Mt. 5:43-48

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako; lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi; ili mpate kuwa wana wa Baba yetu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki. Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyi, mwapata thawabu? Hata watoza ushuru; je! Nao hawafanyi yay ohayo? Tena mkiwaamkia ndugu zenu tu, mnatenda tendo gani la ziada? Hata watu wa mataifa, je! Nao hawafanyi kama hayo? Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

KUWA MWEMA!




“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya kwaresima
Ijumaa, Februari 27, 2026
Juma la 1 la Kwaresima


Eze 18:21-28;
Zab 130: 1-8;
Mt 5:20-26.


KUWA MWEMA!


Leo, Nabii Ezekieli anaweka mbele yetu matarajio ya Mungu kwetu sisi. Anatoa sura ya Mungu akiwa amejawa na huruma kwa wale wote ambao hutubu dhambi zao. Hata hivyo anamuonesha Mungu akiwa hakimu wa haki aliye mwema asiye pendezwa na mabaya. Mungu hataki mtu aliye katika pande mbili (anayechanganya mema na mabaya kwa wakati mmoja), yeye anatazama kila mmoja wetu katika nafsi nzima.

Katika Injili Yesu anaongelea kuhusu Ufalme wa Mbinguni. Kuingia katika Ufalme wa mbinguni unapaswa kuwa lengo la Maisha yetu. Ni mara nyingi tunashindwa kuliona hili katika maisha. Tunashindwa kufungua macho yetu kuelekea Mbinguni kama lengo letu la kwanza la kuwa hapa duniani. Ni rahisi kunaswa na kuridhika na hali za kila siku kama viburudisho, pesa, mafanikio, na mengineyo.

Yesu anatupa njia ya pekee ya kufuata katika ujumbe huu wa Injili, jinsi ya kupata lengo la maisha-ufalme wa Mbinguni. Njia anayo ionesha ni haki. Haki maana yake ni kuwa mwaminifu, sio mdanganyifu. Mafarisayo walijifanya kwa kujionesha kuwa walikuwa watakatifu na wafuasi wazuri wa mapenzi ya Mungu. Lakini hawakuwa wazuri katika hilo. Wanaweza kuwa wazuri katika hali ya kutenda na huenda wanaweza kuwa wamewavutia watu, lakini hawakuweza kumdanganya Yesu. Yesu aliweza kuona udanganyifu wao na kujificha kwao kusiko kwakweli na akaona kile kilicho jificha. Yesu aliweza kuona haki yao ni kwa ajili tu ya kujionesha wenyewe kwa watu.

Kama tunataka kufanya Mbingu kuwa lengo letu, tunapaswa kujitahidi kuwa watakatifu. Na waaminifu. Tunapaswa kumtafuta Kristo katika hali ya kweli na uaminifu katika vitu vidogo vya maisha. Tunapaswa kuacha uaminifu huo uweze kungaa kwa kuonesha katika kweli kile kilichopo katika hali ya ndani. Kuwa wenye haki katika hali ya kweli, ni kwamba tunamtafuta Yesu katika hali ya haki na kumfanya Mungu kuwa lengo la maisha yetu.
Sala: Bwana, naomba unifanye mwenye haki. Nisaidie niweze kuwa mwaminifu kwa yote ninayofanya na yote ninayo tafuta katika maisha. Nisaidie mimi nikupende wewe kila wakati na siku zote. Yesu, nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 27, 2026



MASOMO YA MISA, FEBRUARI 27, 2026
IJUMAA, JUMA LA 1 LA KWARESIMA


SOMO 1
Eze. 18:21-28

Bwana asema hivi: Mtu mbaya akighairi, na kuacha dhambi zake zote alizozitenda, na kuzishika amri zangu zote, na kutenda yaliyo halali na haki hakika ataishi, hatakufa. Dhambi zake zote alizozitenda hazitakumbukwa juu yake hata mojawapo katika haki yake aliyoitenda ataishi. Je! Mimi ninafurahia kufa kwake mtu mwovu? Asema Bwana Mungu; si afadhali kwamba aghairi, na kuiacha njia yake, akaishi?

Bali mwenye haki atakapoghairi, na kuiacha haki yake, na kutenda uovu, na kufanya machukizo yote kama yale afanyayo mtu mwovu, je! Ataishi? Katika matendo yake yote ya haki aliyoyatenda halitakumbukwa hata mojawapo. Katika kosa lile alilolikosa, na katika dhambi yake aliyoitenda, atakufa. Lakini ninyi mwasema, Njia ya Bwana si sawa. Sikilizeni sasa, Enyi nyumba ya Israeli; Je! Njia yangu siyo iliyo sawa? Njia zenu sizo zisizo sawa? Mwenye haki atakapoghairi, na kuiacha haki yake, na kutenda uovu, atakufa katika uovu huo; katika uovu wake alioutenda atakufa. Tena, mtu mwovu atakapoghairi, na kuuacha uovu wake alioutenda, na kutenda yaliyo halali na haki ataponya roho yake, nayo itakuwa hai. Kwa sababu atafakari, na kughairi, na kuyaacha makosa yake yote aliyoyatenda, hakika ataishi, hatakufa.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 130 (K) 3

(K) Bwana kama Wewe ungehesabu maovu,
Ee Bwana, nani angesimama?

Ee Bwana, toka vilindini nimekulilia.
Bwana, uisikie sauti yangu.
Masikio yako na yaisikize
Sauti ya dua zangu. (K)

Bwana, kama Wewe ungehesabu maovu,
Ee Bwana, nani angesimama?
Lakini kwako kuna msamaha,
Ili Wewe uogopwe. (K)

Nimemgnoja Bwana, roho yangu imengoja,
Na neno lake nimelitumainia.
Nafsi yangu inamngoja Bwana,
Kuliko walinzi waingojavyo asubuhi,
Naam, walinzi waingojao asubuhi. (K)

Ee Israeli, umtarajie Bwana;
Maana kwa Bwana kuna fadhili,
Na kwake kuna ukombozi mwingi.
Yeye atamkomboa Israeli na maovu yake yote. (K)


SHANGILIO
Yoe. 2:12-13

Hata sasa, nirudieni mimi kwa mioyo yenu yote, Asema Bwana, kwa maana mimi ndiye mwenye neema, Nimejaa huruma.

I
NJILI
Mt. 5:20-26

Siku ile Yesu aliwaambia wafuasi wake: Maana nawaambia ya kwamba, Haki yenu isipozidi hiyo haki ya waandishi na Mafarisayo, hamtaingia kwamwe katika ufalme wa mbinguni.

Mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, Usiue; na mtu akiua, itampasa hukumu. Bali mimi nawaambieni, Kila amwoneaye ndugu yake hasira itampasa hukumu; na mtu akimfyolea ndugu yake, itampasa baraza; na mtu akimwapiza, itampasa jehanam ya moto.

Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako. Patana na mshitaki wako upesi, wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani. Amin, nakuambia, Hutoki humo kamwe hata uishe kulipa senti ya mwisho.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com