Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

KUTEMBEA KATIKATI YA MITEGO!

 

“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Tafakari ya kila siku
Jumanne, Juni 2, 2026,
Juma la 9 la Mwaka


2 Pet 3: 12-15,17-18
Zab 90:2-4,10,14,16; ;
Mk 12: 13-17.


KUTEMBEA KATIKATI YA MITEGO!



Mafarisayo na Maherodi walijaribu kumtega Yesu katika maongezi yake. Walijaribu kutumia akili yao ili kumfanya Yesu aongee maneno ya kumpinga Kaisari na hivyo kupata kisingizio cha ugomvi na utawala wa Kirumi. Lakini chakushangaza walichokuwa wakisema kuhusu Yesu kilikuwa cha kweli na ilikuwa fadhila kubwa.

Walisema mambo mawili ambayo yalionesha unyenyekevu wa Yesu na uaminifu wake: “twajua ya kuwa wewe u mtu wa kweli,” na “wala hujali cheo cha mtu; kwa maana hutazami sura za watu; lakini katika kweli waifundisha njia ya Mungu”. Yesu haingii katika mtego wao na anafanya kwa hekima kubwa na kumalizana nao.

Tukitafakari juu ya fadhila hizi mbili, tunatambua kuwa maisha yetu ni mara chache sana yanakuwa namna hiyo. Kwanza kabisa, sisi tuna hangaika sana na maneno ya wengine. Ni vizuri kusikiliza wengine na kuwasiliana nao katika hali ya utambuzi. Mawazo ya wengine yanaweza kuwa chanzo cha kugeukia maisha mazuri. Lakini wakati mwingine tunaruhusu wengine watupeleke kwenye dhambi kwasababu ya hofu na woga. Wakati mwingine mawazo mabaya na ushauri mbaya unaongoza maisha yetu. Yesu hakuingia katika mawazo mabaya ya wengine wala hakuruhusu kupelekwa na kutenda kunyume.

Pili, Yesu hakuruhusu “cheo” cha mtu kumpelekesha. Cheo cha mtu wala madaraka havi mfanyi mtu kuwa mkweli zaidi kuliko wengine. Kilicho cha muhimu ni uaminifu na ukweli wa kila mtu. Yesu alizitenda fadhila hizi kiaminifu.

Tutafakari pia sisi kama maneno haya yanaweza kusemwa yakitulenga sisi. Tukazane kuishi maisha ya unyenyenyekevu na kweli na hivyo tutavuka vikwazo na mitego iliyotegwa katika njia yetu ya maisha.

Sala: Bwana, ninataka kuwa mtu mwaminifu. Ninataka kusikiliza mawaidha mazuri ya wengine lakini sio mawazo yakunipeleka kwenye dhambi. Nisaidie niweze kukutafuta wewe na ukweli wako katika kila kitu. Yesu, nakuamini wewe. Amina.

------------------------
Copyright ©2013-2026 ©FurKat, FurahayaKikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUMANNE, JUNI 2, 2026

 

MASOMO YA MISA, JUMANNE, JUNI 2, 2026
JUMA LA 9 LA MWAKA


SOMO 1
Mdo 11:21-26, 13:1-3

Watu wengi waliamini, wakamwelekea Bwana. Habari hizo za watu hao zikafika masikioni mwa kanisa lililokuwako katika Yerusalemu; wakamtuma Baranaba, aende hata Antiokia. Naye, alipokwisha kufika na kuiona neema ya Mungu akafurahi, akawasihi wote wawaambatane na Bwana kwa kusudi la moyo. Maana alikuwa mtu mwema amejaa Roho Mtakatifu na Imani; watu wengi wakaongezeka upande wa Bwana.

Kasha akatoka akaenda Tarso kumtafuta Sauli; hata alipokwisha kumwona akamleta Antiokia. Ikawa kwa muda wa mwaka mzima wakakusanyika pamoja na kanisa na kuwafundisha watu wengi. Na wanafunzi waliitwa Wakristo kwanza hapo Antiokia.

  Na huko Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli. Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi niliyowaitia. Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 98:1-6 (K) 2

(K) Bwana ameufunua wokovu wake machoni pa mataifa.

Mwimbieni Bwana wimbo mpya,
Kwa maana ametenda mambo ya ajabu.
Mkono wa kuume wake mwenyewe,
Mkono wake mtakatifu umemtendea wokovu. (K)

Bwana ameufunua wokovu wake,
Machoni pa mataifa ameidhihirisha haki yake.
Amezikumbuka rehema zake,
Na uaminifu wake kwa nyumba ya Israeli. (K)

Miisho yote ya dunia imeuona
Wokovu wa Mungu wetu.
Mshangilieni Bwana, nchi yote,
Inueni sauti, imbeni kwa furaha, imbeni zaburi. (K)

Mwimbieni Bwana zaburi kwa kinubi,
Kwa kinubi na sauti ya zaburi.
Kwa panda na sauti ya baragumu.
Shangilieni mbele za Mfalme, Bwana. (K)


SHANGILIO
Aleluya, aleluya,
Ee Mungu, tunakusifu, tunakukiri kuwa Bwana.
Jamii tukufu ya mitume inakusifu.
Aleluya.


INJILI
Mt 5:13-16

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Ninyi ni chumvi ya dunia; lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena kabisa, ila kutupwa nje na kukanyagwa na watu. Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima. Wala watu hawawashi taa na kuiweka chini ya pishi, bali juu ya kiango; nayo yawaangaza wote waliomo nyumbani. Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2024, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MUNGU ANAYETUJALI (MWEMA)!

 

“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatatu, Juni 1, 2026,
Juma la 9 la Mwaka wa Kanisa

2 Pet 1: 2-7;
Zab 90: 1-2, 14-16;
Mk 12: 1-12

MUNGU ANAYETUJALI (MWEMA)!

Fumbo tulilo nalo leo kwa tafakari yetu ni kuhusu muonekano wa uzuri na wema wa Mungu. Jinsi Mungu anavyotenda na jinsi mwanadamu anavyofikiri ni vitu viwili tofauti kabisa kiasi ambacho mwanadamu anajiandaa akidhani atashambuliwa. Wema haujajikita katika kutoa mengi tu, bali kutoa hata kidogo kwa wakati. Mungu alimtoa mwanaye kwawakati kwaajili yetu. Alitupa yote kwa wakati. Yesu aliongea na kutenda katika hali ambayo watu kwakuona anayosema nakutenda, wakatambua Mungu ni wa namna ghani.

Kwa maneno mwengine, Yesu hakuongea tuu kuhusu Mungu na kuonyesha muelekeo wa kwenda kwake, bali alionesha uwepo wa Mungu na Mungu akaonekana akiwa kati ya watu wake. Kama sio yeye, Mungu kwetu angekuwa ni kama kitu tuu cha kutumaini nakutafuta. Lakini kwa njia yake Mungu yupo kati yetu (Ekaristi Takatifu). Kabla ya Yesu, hakuna aliyejua sifa za Ufalme wa Mungu ulivyo, yeye ndiye aliyetupa mifano akielezea jinsi Ufalme wa Mungu ulivyo, na akatuambia yeye amekuja kuutangaza, upo kati yetu, nabado utatimilizwa katika maisha ya umilele. Kwahiyo tukiishi vizuri na wengine tunaishi Ufalme wake tukiwa hapa duniani.

Yesu, hakutaka chochote kwaajili yake binafsi, bali kila kitu alichokuwa nacho na kutenda, alifanya kwaajili yawengine. Kila mmoja wetu ni wa Yesu, chombo cha upendo wa Mungu, na chombo chakupokea wema wa Mungu. Leo tujiulize kama tumekuwa wazi kwa wema na upendo huu wa Mungu.

Sala: Nisaidie Bwana, niweze kuutambua wema wako ili niweze kuwa mwema. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUNI 1, 2026

 


MASOMO YA MISA, JUNI 1, 2026
JUMATATU YA 9 YA MWAKA
KUMBUKUMBU YA MTAKATIFU JUSTIN

SOMO 1
2Pet. 1:2-7
Neema na iwe kwenu na amani iongezwe katika kumjua Mungu na Yesu Bwana wetu.
Kwa kuwa uweza wake wa Uungu umetukirimia vitu vyote vipasavyo uzima na utauwa, kwa kumjua yeye aliyetuita kwa utukufu wake na wema wake mwenyewe. Tena kwa hayo ametukirimia ahadi kubwa mno, za thamani, ili kwamba kwa hizo mpate kuwa washirika wa tabia ya Uungu, mkiokolewa na uharibifu uliomo duniani kwa sababu ya tamaa. Naam, na kwa sababu iyo hiyo mkijitahidi sana kwa upande wenu, katika imani yenu tieni na wema, na katika wema wenu maarifa, na katika maarifa yenu kiasi, na katika kiasi chenu saburi, na katika sabauri yenu utauwa, na katika utauwa wenu upendano wa ndugu, na ktika upendano wa ndugu, upendo.
Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI
Zab. 91:1-2, 14-16, (K) 2
(K) Mungu wangu ninakutumaini.
Aketiye mahali pa siri pake Aliye juu
Atakaa katika uvuli wake Mwenyezi.
Nitasema, Bwana ndiye kimbilio langu na ngome yangu,
Mungu wangu nitakayemtumaini. (K)
(K) Mungu wangu ninakutumaini.
Mwana-simba na joka utawaseta kwa miguu.
Kwa kuwa amekaza kunipenda
Nitamwokoa; na kumweka palipo juu, kw akuwa amenijua jina langu.
Ataniita nami nitamwitikia. (K)
Nitakuwa pamoja naye taabuni,
Nitamwokoa na kumtukuza;
Kwa siku nyingi nitamshibisha,
Nami nitamwonyesha wokovu wangu. (K)

SHANGILIO
Zab. 130:5
Aleluya, aleluya.
Roho yangu inamngoja Bwana, na neno lake nimelitumainia.
Aleluya.

INJILI
Mk. 12:1-12
Yesu alisema na Mafarisayo kwa mifano; Mtu mmoja alipanda shamba la mizabibu, akazungusha ugo, akachimba shimo la shinikizo, akajenga mnara, akapangisha wakulima, akasafiri. Hata kwa wakati wake akatuma, mtumwa kwa wale wakulima, ili apokee kwa wakulima katika matunda ya mizabibu. Wakamtwaa, wakampiga, wakamtoa nje, hana kitu. Akatuma tena kwao mtumwa mwingine, na huyo wakamtia jeraha -za kichwa, wakamfanyia jeuri. Akamtuma mwingine, huyo wakamwua; na wengine wengi, hawa wakiwapiga na hawa wakiwaua. Basi alikuwa na mmoja bado, mwana mpendwa wake; huyu naye akamtuma kwao mwisho, akisema, Watamstahi mwanangu. Lakini wale wakulima wakasemezana, Huyu ni mrithi; haya, na tumwue, na urithi utakuwa wetu. Wakamkamata, wakamwua, wakamtupa nje ya shamba la mizabibu. basi atafanyaje yule bwana wa shamba la mizabibu? Atakuja na kuwaangamiza wale wakulima, na lile shamba la mizabibu atawapa wengine. Hata andiko hili hamjalisoma, Jiwe walilolikataa waashi, hilo limekuwa jiwe kuu la pembeni. Neno hili limetoka kwa Bwana, nalo ni ajabu machoni petu? Nao wakatafuta kumkamata, wakaogopa mkutano; maana walitambua ya kwamba ule mfano amewanenea wao. Wakamwacha wakaenda zao.
Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MUNGU KATIKA UTATU

 



“MBEGU ZA UZIMA”
Tafakari ya kila Jumapili
Jumapili, Mei 31, 2026 
Sherehe ya Utatu Mtakatifu

Kut. 34 : 4-6, 8-9;
Dan. 3:52-56. (K) 52;
2 Kor. 13 :11-14;
Yn. 3:16-18.


MUNGU KATIKA UTATU


Wakatoliki, duniani kote, sio kwamba wanaamini Mungu tu, bali wanaamini Mungu mmoja. Lakini Mungu wetu yupo katika Utatu- Utatu katika umoja na umoja katika Utatu. Kila mmoja ni Mungu kwa asili na wote ni Mungu mmoja. Sawa katika Nguvu, ni wa milele na wana utukufu. Fumbo hili kuu linaweza kuchukuliwa kama fumbo lililo kuu kabisa katika Biblia Takatifu. Wakristo tunaamini fumbo hili kuu ndani ya mamlaka ya Yesu Kristo na Agano Jipya. Ni moja wapo ya fumbo kubwa la ndani kabisa lililofunuliwa na lililopo juu kabisa kupita akili ya mwanadamu. Yesu mara nyingi ameongea kuhusu Mungu kama Baba yake. Sauti ya Baba ilisikika wakati wa ubatizo wa Yesu; “Huyu ni mwanangu mpendwa niliye pendezwa naye msikilizeni yeye”. Yesu alipo ngara sura, pia, sauti hiyo hiyo ilisikika ikisema maneno hayo hayo. Katika matukio yote uwepo wa wingu jeupe ilionyesha uwepo wa Roho Mtakatifu, ambaye Yesu aliwaahidia wakati alipokuwa akipaa kwenda kwa Baba, “nitawapa msaidizi Mwingine-Roho wa kweli anayetoka kwa Baba”. 

Yesu anatuambia kwamba, Mungu aliupenda sana ulimwengu mpaka akamtuma mwanaye ulimwenguni, ili wote watakao muamini wasipotee bali wawe na uzima wa milele (Yn 3:16). Anaelezea uhusiano wake ndani ya Mungu mmoja wa kweli na anawataka mitume na wafuasi watambue na wakubali kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu, na kwamba Mungu ni Baba yake, na kwamba Roho Mtakatifu alitumwa kwao na Baba na Mwana. Wakristo wa kwanza walisadiki ndani ya Utatu Mtakatifu bila kupinga. Baada ya kuamini, kinachofuata ni Upendo. “Kama mtu akinipenda mimi” Yesu anasema, “Baba yangu atampenda. Nasi tutakuja kwake nakufanya makao ndani yake.”

“…(Wana ndoa) matunda ya wana ndoa yanakuwa ishara ya kuelewa na kuelezea fumbo la Mungu mwenyewe, kwasababu kwa mtazamo wa Kikristo wa Utatu mtakatifu, Mungu anatafakariwa kama Baba, na Mwana na Roho Upendo. Utatu Mtakatifu ni umoja wa upendo, na familia ndiyo inayoishi kuonesha umoja huu. Mtakatifu Papa Yohane Paulo wa Pili, alitoa mwanga kwa hili alivyosema ‘Mungu wetu katika undani wake sio upweke bali ni familia, kwani ndani yake ana Ubaba, mwana na undani wa familia ambaye ni Upendo. upendo huo ndani ya familia ya Kimungu ni Roho Mtakatifu’”. (Baba Mtakatifu Fransisko katika Furaha ya upendo, Amoris Laetitia, 11)

Tutafakari leo juu ya sherehe hii ya Utatu Mtakatifu, ni mara ngapi nina enzi upendo huu wa Utatu Mtakatifu katika mahusiano yangu? Tujaribu kufanya jitihada tusonge mbele zaidi, katika mapendo yetu, na kumruhusu Mungu akupe matokeo mazuri ya tokanayo na upendo wako kwake na kwa jirani. 

Sala: Baba na Mwana na Roho Mtakatifu, nisaidie mimi niweze kuku fahamu wewe na kukupenda. Nisaidie niweze kuelewa upendo unaoshiriki na Mwanao. Kwa kuelewa upendo huo, nisaidie na mimi niweze kushirikisha upendo huo kwa wengine. Baba na Mwana na Roho Mtakatifu, nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUMAPILI MEI 31, 2026

 



MASOMO YA MISA, JUMAPILI MEI 31, 2026
SHEREHE YA UTATU MTAKATIFU

JUMAPILI BAADA YA PENTEKOSTE - MWAKA A


SOMO 1 
Kut. 34 : 4-6, 8-9

Musa aliinuka na mapema asubuhi, naye akakwea katika mlima wa Sinai, kama Bwana alivyomwamuru, akazichukua hizo mbao mbili za mawe mkononi mwake.

Bwana akashuka ndani ya lile wingu, akasimama pamoja naye huko, akalitangaza jina la Bwana. Bwana akapita mbele yake, akatangaza, Bwana, Bwana, Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; Musa akafanya haraka, akainamisha kichwa chake hata nchi, akasujudu. Akasema, Ikiwa sasa nimepata neema mbele zako, Bwana, nakuomba, Bwana, uende kati yetu maana ni watu wenye shingo ngumu; ukasamehe uovu wetu na dhambi yetu, ukatutwae tuwe urithi wako.


WIMBO WA KATIKATI 
Dan. 3:52-56. (K) 52

(K) Wastahili kusifiwa na kutukuzwa milele.

Umehimidiwa, Ee Bwana, Mungu wa baba zetu: 
Wastahili kusifiwa na kutukuzwa milele. 
Limehimidiwa jina lako takatifu, tukufu;
Wastahili kusifiwa na kutukuzwa milele. (K)

Umehimidiwa katika hekalu la fahari yako takatifu; 
Wastahili kusifiwa na kutukuzwa milele. 
Umehimidiwa juu ya kiti cha ufalme wako;
Wastahili kusifiwa na kutukuzwa milele. (K)

Umehimidiwa utazamaye vilindi, uketiye juu ya makerubi;
Wastahili kusifiwa na kutukuzwa milele.
Umehimidiwa katika anga la mbinguni 
Wastahili kusifiwa na kutukuzwa milele. (K)


SOMO 2 
2 Kor. 13 :11-14

Hatimaye, ndugu, kwaherini; mtimilike, mfariji- ke, nieni mamoja, mkae katika amani; na Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nanyi. Sali- mianeni kwa busu takatifu. Watakatifu wote wawasalimu. Neema ya Bwana Yesu Kristo, na pendo la Mungu. na ushirika wa Roho Mtakatifu ukae nanyi nyote.


SHANG1LIO 
Ufu. 1 :8

Aleluya, Aleluya, Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu, Mungu ambaye yupo, aliyekuwako, na atakayekuja. Aleluya.


INJILI 
Yn. 3:16-18

Yesu alimwambia Nikodemu: Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe wa pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhu- kumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu.



Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUMUONA MUNGU KATIKA MAISHA YETU!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumamosi, Mei 30, 2026, 
Juma la 8 la Mwaka wa Kanisa

Yud 17:20-25; 
Zab: 62: 2-6; 
Mk 11: 27-33


KUMUONA MUNGU KATIKA MAISHA YETU!

Yesu sasa yupo Yerusalemu. Katika Injili ya leo, wakati Yesu akiwa anatembea hekaluni, walimuendea viongozi na wazee Wawayahudi, Makuhani, walimu wa sheria na Wazee. “nikwa mamlaka ya nani unatenda haya?” walimuuliza Yesu. Hii ikimaanisha kwamba hafanyi katika hali ambayo inaonesha kujali mamlaka yao. Kama ilivyo ada kwa Yesu, anawauliza swali na wao. Aliuliza kama kazi ya Yohane Mbatizaji ilitoka kwa wanadamu au kwa Mungu.

Wakatambua mara moja kujibu Swahili la Yesu ingewaletea matatizo. Kwa udhaifu mkubwa wanajibu, “hatujui”. Jibu lisilo lakawaida kabisa tena lisiloridhisha na ajabu kabisa tena kutoka kwa viongozi wakubwa wa kiroho wa watu. Hapo Yesu akakataa kuwajibu swali lao walilokuwa wameuliza awali. Hali ya Yesu inafanana na ile ya Yohane Mbatizaji. Watu waliomsikia Yesu akiongea (“hakuna aliyewahi kuzungumza namna hii”) na kuona anavyoponya watu (“Mungu amewajia watu wake”), hawakuwa na wasiwasi wowote juu ya mamlaka yake. “Watu walishangazwa na mafundisho yake, kwani alifundisha kwa mamlaka sio kama Walimu wa sheria” (Mk 1:22). Swali la viongozi wa Wayahudi ilidhirisha kabisa udhaifu wao na upofu wao kwenye jambo ambalo lipo wazi lisiloweza kufichika machoni pa watu wote. 

Sisi pia tunaweza kuwa na upofu huo. Tunaweza tukakataa kuona uwepo wa kazi ya Mungu katika hali ambazo sisi wenyewe hatutaki kuona, katika watu ambao hatutaki kuwaona, au kuwadharau baadhi ya watu na kuwaona kama hawana chochote chakuweza kuniambia pengine kwasababu ya elimu yao au udhaifu wao. Lakini tutambue Mungu anaweza kumtumia mtu yeyote, jambo lolote, zuri au lisiloonekana zuri machoni petu, ili kuleta ujumbe wake. 

Sala: Nisaidiye Bwana, kukutafuta na kukupata na nitende yale yote unayotaka nitende katika Maisha yangu. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MEI 30, 2026




MASOMO YA MISA, MEI 30, 2026
JUMAMOSI, JUMA LA 8 LA MWAKA

SOMO 1
Yud. 1:17,20-25

Wapenzi, yakumbukeni maneno yaliyonenwa zamani na mitume wa Bwana wetu Yesu Kristo, Bali ninyi, wapenzi, mkijijenga juu ya imani yenu iliyo takatifu sana, na kuomba katika Roho Mtakatifu, jilindeni katika upendo wa Mungu, huku mkingojea rehema ya Bwana wetu Yesu Kristo, hata mpate uzima wa milele. Wahurumieni wengine walio na shaka, na wengine waokoeni kwa kuwanyakua katika moto; na wengine wahurumieni kwa hofu, mkilichukia hata vazi lililotiwa uchafu na mwili.

Yeye awezaye kuwalinda ninyi msijikwae, na kuwasimamisha mbele ya utukufu wake bila mawaa katika furaha kuu; Yeye aliye Mungu pekee, Mwokozi wetu kwa Yesu Kristo Bwana wetu; utukufu una yeye, na ukuu, na uwezo, na nguvu, tangu milele, na sasa, na hata milele. Amina.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 63:1-5 (K) 1

(K) Nafsi yangu inakuonea kiu, Ee Bwana.

Ee Mungu, Mungu wangu, nitakutafuta mapema,
Nafsi yangu inakuonea kiu,
Mwili wangu wakuonea shauku,
Katika nchi kame na uchovu, isiyo na maji. (K)

Ndivyo nilivyokutazama katika patakatifu,
Nizione nguvu zako na utukufu wako.
Maana fadhili zako ni njema kuliko uhai;
Midomo yangu itakusifu. (K)

Ndivyo nitakavyokubariki maadamu ni hai;
Kwa jina lako nitaiinua mikono yangu.
Nafsi yangu itakinai kama kushiba mafuta na vinono;
Kinywa changu kitakusifu kwa midomo ya furaha. (K)


INJILI 
Mk. 11:27-33

Yesu na wanafunzi walifika Yerusalemu; alipokuwa akitembea hekaluni, walimwendea wakuu wa makuhani, na waandishi, na wazee, wakamwambia, Ni kwa mamlaka gani unatenda mambo haya? naye ni nani aliyekupa mamlaka hii uyatende haya? Yesu akawaambia, Nitawauliza neno moja, nanyi mnijibu, kisha nitawaambia ni kwa mamlaka gani nayatenda haya. Ubatizo wa Yohane ulitoka mbinguni, au kwa wanadamu? Nijibuni.

Wakasemezana wao kwa wao, wakisema, Kama tukisema, Ulitoka mbinguni, atasema, Mbona, basi, hamkumwamini? Ila tukisema, Ulitoka kwa wanadamu. Waliogopa watu; maana watu wote walimwona Yohane kuwa nabii halisi. Wakamjibu Yesu, wakasema, Hatujui. Yesu akawaambia, Wala mimi siwaambii ninyi ni kwa mamlaka gani nayatenda haya.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo. 

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MATUNDA YENYE KUWAVUTA WATU




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Ijumaa, Mei, 29, 2026 
Juma la 8 la mwaka wa Kanisa

1 Pet 4: 7-13; 
Zab 95: 10-13; 
Mk 11: 11-26


MATUNDA YENYE KUWAVUTA WATU

Yesu alivyo ulaani mtini baada ya kuuona hauna matunda, kitendo hiki kinaweza kuonekana cha ajabu kidogo na cha kutisha. Yesu alijua kabisa ilikuwa sio kipindi cha matunda ya mti ule. Mt. Bede katika maelezo yake akiongelea kuhusu muujiza huu wa Yesu, anatuambia kwamba, muujiza huu wa Yesu ulikuwa na lengo maalumu. Yesu alikuja kati ya watu wake, Wayahudi, akiwa na njaa yakutaka matunda ya utakatifu, wao hawakuupokea ujumbe wake na matunda ya kazi yake. Lakini yote aliyo yakuta ni msisitizo wakushika dini, matendo ya njee yasioendani na kilicho ndani, na katika hali hii wamekuwa kama majani ya miti bila matunda. Wakati alivyo ingia Hekaluni alikuta wamepageuza kuwa pango la biashara. Kitu ambacho kilimfanya hata halitakase kwakutumia nguvu. “Kwahio wewe” anasema Mt. Bede kwakumalizia, “unapaswa ujilinde usiwe kama mti usio zaa matunda, jitoe kwa Yesu, aliyejifanya mwenyewe maskini, anategemea uwe tunda la utakatifu” 

Fadhili zinaongeza furaha ya maisha ya sala na sala inapaswa ionekane katika matendo ya fadhila. Sala ya kweli inapaswa utuongoze taratibu katika mabadiliko ya kweli ya maisha yetu, tukikua katika fadhila na madiliko ya ndani. Vinginevyo tutakuwa kama Wayahudi, mtini uliyo na majani pekee usio zaa matunda.

Sala: Bwana nijaliye neema, ili kwa maisha yangu niweze kutoa matunda mema. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MEI 29, 2026

 



MASOMO YA MISA, MEI 29, 2026
IJUMAA, JUMA LA 8 LA MWAKA

SOMO 1 
1 Pet. 4:7-13

Mwisho wa mambo yote umekaribia; basi iweni na akili, mkeshe katika sala. Zaidi ya yote iweni na juhudi, mkeshe katika sala. Zaidi ya yote iweni na juhudi nyingi katika kupendana; kwa sababu upendano husitiri wingi wa dhambi. Mkaribishane ninyi kwa ninyi, pasipo kunung’unika; kila mmoja kwa kadiri alivyoipokea karama, itumieni kwa kuhudumiana; kama mawakili wema wa neema mbalimbali za Mungu. Mtu akisema, na aseme kama mausia ya Mungu; mtu akihudumu, na ahudumu kwa nguvu anazojaliwa na Mungu; ili Mungu atukuzwe katika mambo yote kwa Yesu Kristo. Utukufu na uweza una yeye hata milele na milele. Amina.

Wapenzi, msione kuwa ni ajabu ule msiba ulio katik yenu, unaowapata kama moto ili kuwajaribu, kana kwamba ni kitu kigeni kiwapatacho. Lakini kama mnavyoyashiriki mateso ya Kristo, furahini; ili na katika ufunuo wa utukufu wake mfurahi kwa shangwe.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 149:1-6,9 (K) 4

(K) Bwana awaridhia watu wake. au: Aleluva.

Mwimbieni Bwana wimbo mpya,
Sifa zake katika kusanyiko la watauwa.
Israeli na amfurahie Yeye aliyemfanya,
Wana wa Sayuni na wamshangilie mfalme wao. (K)

Na walisifu jina lake kwa kucheza,
Kwa matari na kinubi wamwimbie.
Kwa kuwa Bwana awaridhia watu wake, 
Huwapamba wenye upole kwa wokovu. (K)

Watauwa na waushangilie utukufu,
Waimbe kwa sauti kuu vitandani mwao.
Sifa kuu za Mungu na ziwe vinywani mwao,
Hiyo ndiyo heshima ya watauwa wake wote. (K)


SHANGILIO 
Lk. 8 :15

Aleluya, aleluya, 
Wanabarikiwa wale ambao kwa unyofu na wema wa mioyo yao, hulisikia neno la Mungu na kulishika. 
Aleluya.


INJILI 
Mk. 11:11-26

Yesu aliingia Yerusalemu hata ndani ya hekalu; na alipokwisha kutazama yote pande zote, kwa kuwa ni wakati wa jioni, akatoka, akaenda Bethania pamoja na wale Thenashara.

Hata asubuhi yake walipotoka Bethania aliona njaa. Akaona kwa mbali mtini wenye majani, akaenda ili labda aone kitu juu yake; na alipouiikilia hakuona kitu ila majani; maana si wakati wa tini. Akajibu, akauambia, Tangu leo hata milele mtu asile matunda kwako. Wanafunzi wake wakasikia.

Wakafika Yerusalemu, naye akaingia ndani ya hekalu, akaanza kuwafukuza wale waliokuwa wakiuza na kununua ndani ya hekalu, akazipindua meza na wabadili fedha, na viti vyao wauzao njiwa; wala hakuacha mtu achukue chombo kati ya hekalu. Akafundisha, akasema, Je! haikuandikwa, Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote? Bali ninyi mmeifanya kuwa pango la wanyang’anyi. Wakuu wa makuhani na waandishi wakapata habari wakatafuta jinsi ya kumwangamiza; maana walimwogopa, kwa sababu mkutano wote walishangaa kwa mafundisho yake. Na kulipokuwa jioni alitoka mjini.

Na asubuhi walipokuwa wakipita, waliuona ule mtini umenyauka toka shinani. Petro akakumbuka habari yake, akamwambia, Rabi, tazama, mtini ulioulaani umenyauka. Yesu akajibu, akawaambia, Mwaminini Mungu. Amin, nawaambia, Ye yote atakayeuambia mlima huu, Ng’oka ukatupwe baharini, wala asione shaka moyoni mwake, ila aamini kwamba hayo asemayo yametukia, yatakuwa yake. Kwa sababu hiyo nawaambia, Yo yote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu.

Nanyi, kila msimamapo na kusali, sameheni, ntkiwa na neno juu ya mtu; ili na Baba yenu aliye mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu. Lakini kama ninyi hamsamehe, wala Baba yenu aliye mbinguni hatawasamehe ninyi makosa yenu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com