Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

WAPENDE MAADUI



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Alhamisi, Septemba 10,  2026, 
Juma la 23 la Mwaka

1Kor 8: 1-7, 11-13; 
Zab 139: 1-3, 13-14, 23-24; 
Lk 6: 27-38


WAPENDE MAADUI 

Yesu aliwaambia wafuasi wake: “kwenu sikieni wapendeni maadui zenu, watendeeni mema wanao wachukia, wabarikini wanao walaani, waombeeni wanao watenda vibaya.” - Luka 6:27-28

Maneno haya ni marahisi sana kuyasema kuliko kuyatenda. Wakati watu wamekutendea vibaya kwa kukutenda vibaya unachopaswa kufanya ni kuwapenda na kuwaombea. Na Yesu anasema kwa uhakika kwamba hichi ndicho tulichoitwa kufanya. 

Katikati ya mateso na vita inayofanywa juu yetu ni rahisi kuumia. Na huku kuumia kunaweza kutufanya tupatwe na hasira na kutaka kurudisha kisasi na hata chuki. Kama tutakubali kuingia katika kishawishi hichi tutakuwa sisi wenyewe tumeamua kujiumiza. Ukweli ni kwamba kuwachukia wale waliotuumiza hufanya mambo yawe mbaya zaidi. 

Lakini tutakuwa waongo kusema ukweli kuhusu nguvu inayotusukuma kutoka ndani mwetu hasa pale tunapokosewa na inavyokuwa vigumu kutimiza maneno ya Yesu ya kurudisha kwa upendo. Ili kuwa waaminifu ni vizuri tukubali ukweli huu kwanza. Nguvu hii huondoka ndani pale tunapojaribu kushika upendo licha ya hasira na hisia tulizo nazo. 

Hisia hizi zinatujulisha kwamba Mungu anahitaji mengi zaidi kutoka kwetu na sio kuongozwa na hisia hizi. Kuwa na hasira au chuki sio kitu cha kufurahisha. Ukweli ni kwamba kinaweza kuwa ni kitendo cha mateso makubwa, lakini haipaswi kuwa hivyo. Kama tumeeelewa ujumbe huu wa Yesu njia yake ni njia nzuri ya kukwepa mateso haya. Tutatambua kwamba kulipiza kisasa hufanya kidonda kiwe kikubwa zaidi na zaidi. Tukijifunza kupenda pale mahali ambapo tumetendewa vibaya tunatambua kwamba upendo katika hali hii huwa na nguvu sana. Ni upendo ndio unaoenda zaidi ya hisia. Upendo huu tumepewa kama zawadi kutoka kwa Mungu. Ni upendo na ukarimu ndio unatufanya tuwe na furaha ya kweli..

Tafakari leo juu ya kidonda chochote kile unachokibeba ndani mwako. Tambua kwamba vidonda hivi vinaweza kuwa sababu ya utakatifu wako na furaha yako kama utamruhusu Mungu akubadilishe na kuanza kuwatendea kwa upendo wale waliokutenda mabaya. 

Sala: Bwana, ninatambua kwamba nimeitwa niwapende maadui wangu. Ninatambua kwamba nimeitwa niwapende wale wote walionitenda mabaya. Nisaidie niweze kukabidhi kwako hisia zote za chuki au hasira naomba uvibadilishe kwa upendo wa kweli. Yesu nakuamini wewe. Amina


.Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 10, 2026



MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 10, 2026
ALHAMISI, JUMA LA 23 LA MWAKA

SOMO 1
1Kor. 8:1-7, 11-13

Twajua ya kuwa sisi sote tuna ujuzi. Ujuzi huleta majivuno, bali upendo hujenga. Mtu akidhani ya kuwa anajua neno, hajui neno lolote bado, kama impasavyo kujua. Lakini mtu akimpenda Mungu, huyo amejulikana naye. Basi kwa habari ya kuvila vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu; twajua ya kuwa sanamu si kitu katika ulimwengu, nay a kuwa hakuna Mungu ila mmoja tu. Kwa maana ijapokuwa wako waitwao miungu, ama mbinguni ama duniani, kama vile walivyoko miungu mingi na mabwana wengi; lakini kwetu sisi Mungu ni mmoja tu, aliye Baba, ambaye vitu vyote vimetoka kwake, nasi tunaishi kwake; yuko na Bwana mmoja Yesu Kristo, ambaye kwake vitu vyote vimekuwapo, na sisi kwa yeye huyo.

Bali ujuzi huu haumo ndani ya watu wote; ila wengine kwa kuizoelea ile sanamu hata sasa hula kana kwamba ni kitu kilichotolewa sadaka kwa sanamu; na dhamiri zao, kwa kuwa dhaifu, hunajisika. Na yule aliye dhaifu aangamizwa kwa ujuzi wako, naye ni ndugu ambaye Kristo alikufa kwa ajili yake. Hivyo, mkiwatenda dhambi ndugu zenu na kuitia jeraha dhambiri iliyo dhaifu, mnamtenda dhambi Kristo. Kwa hiyo, chakula kikimkwaza ndugu yangu, hakika sitakula nyama hata milele, nisije nikamkwaza ndugu yangu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 139:1-3, 13-14, 23-24 (K) 24

(K) Uniongoze, Bwana, katika njia ya milele.

Ee Bwana umenichunguza na kunijua.
Wewe wajua kuketi kwangu na kuondoka kwangu;
Umelifahamu wazo langu tokea mbali.
Umepepeta kwenda kwangu na kulala kwangu,
Umeelewa na njia zangu zote. (K)

Maana Wewe ndiwe uliyeniumba mtima wangu,
Uliniunga tumboni mwa mama yangu.
Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa
Kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. (K)

Ee Mungu, unichunguze, uujue moyo wangu,
Unijaribu, uyajue mawazo yangu;
Uone kama iko njia iletayo majuto ndani yangu,
Ukaniongoze katika njia ya milele. (K)


SHANGILIO
Zab. 147:12,15

Aleluya, aleluya,
Msifu Bwana, Ee Yerusalemu, huipeleka amri yake juu ya nchi.
Aleluya.


INJILI
Lk. 6:27-38

Yesu aliwaambia wafuasi wake: Nawaambia ninyi mnaosikia, Wapendeni adui zenu, watendeeni mema wale ambao wawachukia ninyi, wabarikieni wale ambao wawalaani ninyi, waombeeni wale ambao wawaonea ninyi. Akupigaye shavu moja, mgeuzie la pili, naye akunyang’anyaye joho yako, usimzuilie na kanzu. Mpe kila akuombaye, na akunyang’anyaye vitu vyako, usitake akurudishie. Na kama mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni vivyo hivyo.

Maana mkiwapenda wale wawapendao ninyi, mwaonyesha fadhili gani? Kwa kuwa hata wenye dhambi huwapenda wale wawapendao. Nanyi mkiwatendea mema wale wawatendao mema, mwaonyesha fadhili gani? Hata wenye dhambi hufanya vivyo hivyo. Na mkiwakopesha watu huku mkitumaini kupata kitu kwao, mwaonyesha fadhili gani? Hata wenye dhambi huwakopesha wenye dhambi, ili warudishiwe vile vile.

Bali wapendeni adui zenu, tendeni mema, na kukopesha msitumaini kupata malipo, na thawabu yenu itakuwa nyingi; nanyi mtakuwa wana wa Aliye juu, kwa kuwa yeye ni mwema kwa wasiomshukuru, na waovu.

Basi, iweni na huruma, kama Baba yenu alivyo na huruma. Msihukumu, nanyi hamtahukumiwa; msilaumu, nanyi hamtalaumiwa; achilieni, nanyi mtaachiliwa. Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwasukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

KIU YA KUTAKA FURAHA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatano, Septemba 9, 2026
Juma la 23 la Mwaka


1 Kor 7: 25-31; 
Ps 44: 11-12, 14-17; 
Lk 6: 20-26


KIU YA KUTAKA FURAHA!

Kila moyo wa mwanadamu umeumbwa kwa ajili ya furaha. Mungu mwenyewe, katika Utatu Mtakatifu, ndiye Furaha Kuu, ndiye Furaha yote. Masomo yetu ya leo yanatuambia kwamba maskini wapo katika hali salama zaidi kuliko matajiri. Moyo wa Mwanadamu, na uzuri wake na uwezo wake wakupata utakatifu, unachafuliwa, unazimwa na kuharibiwa kwa kuwa mtumwa wa mali na anasa. Tamaa isiyo na mpangilio ya fedha, nyumba, ardhi na vitu vimechafua furaha ya watu wengi na pia furaha ya familia mbali mbali. 

Leo Injili inaongelea pia kitu kingine kinachochafua roho nyingi: tamaa ya anasa na kusifiwa (kijenga jina). “Ole wenu ninyi watu wote watakapo wasifu, kwakuwa baba zao waliwatenda manabii wa uongo mambo kama hayo” (Lk 6: 26). “heri yenu ninyi watu watakapo wachukia, na kuwatenga, na kuwashutumu, na kulitupa nje jina lenu kama neno ovu, kwa ajili ya Mwana wa Adamu. Furahini na kuruka-ruka, kwakuwa, tazama, thawabu yenu ni kubwa mbinguni, maana, baba zao waliwatenda manabii vivyo hivyo.” (Lk 6: 22-23). 

Yesu anataka kutuambia kwamba watu wakweli wanaomfuata watapata mateso mengi, haitakuwa rahisi njia ya Yesu, mtu anapaswa kusema ukweli hata pale inapo hatarisha maisha yake, kama vile manabii wa ukweli walivyoteseka zamani. Sifa za nabii wa ukweli ni kwamba hakuambii kile ambacho unachotaka kusikia bali anasema ukweli kwasababu ni ukweli. Manabii wengi walipoteza maisha yao kwasababu waliitwa na wafalme ili kutoa unabii juu ya jambo Fulani, lakini wao kwa ujasiri walisema ukweli hata kumrekebisha mfalme na hapo maisha yao yakawa hatarini. Mfalme alitegemea kusikia akisifiwa tu, lakini manabii wa kweli walisema ukweli, huu ndio wito anaotuambia Yesu. Tusiwe kama nmanabii wa uongo wanaopenda kuongea tu kile ambacho watu wanapenda kusikia bali tuseme ukweli kwasababu ni jambo la kweli. 

Sala: “Umetuumba kwa ajili yako mwenyewe, ee Bwana! Na roho zetu hazitatulia mpaka zitakapo tulia kwako.” (Mt. Agustino)  Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA JUMATANO, SEPTEMBA 9, 2026



MASOMO YA MISA 
JUMATANO, SEPTEMBA 9, 2026
JUMA LA 23 LA MWAKA


SOMO 1
1Kor. 7:25 – 31

Kwa habari za wanawali sina amri ya Bwana, lakini natoa shauri langu, mimi niliyejaliwa kwa rehema za Bwana kuwa mwaminifu. Basi, naona hili kuwa jema, kwa ajili ya shida iliyopo, kwamba ni vema mtu akae kama alivyo. Je! Umefungwa kwa mke? Usitake kufunguliwa. Umefunguliwa? Usitafute mke. Lakini, kama ukioa, huna hatia; wala mwanamwamli akiolewa, hana hatia; lakini watu kama hao watakuwa na dhiki katika mwili; name nataka kuwazuilia hayo.

Lakini, ndugu, nasema hivi, muda ubakio si mwingi; basi tokea sasa wale walio na wake na wawe kama hawana; na wale waliao kama hawalii; na wale wafurahio kama hawafurahi; na wale wanunuao, kama hawana kitu. Na wale wautumiao ulimwengu huu, kama hawautumii sana; kwa maana mambo ya ulimwengu huu yanapita.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 45:10 – 11, 13 – 16 (K) 10

(K) Sikia, binti, utazame, utege sikio lako.

Sikia, binti, utazame, utege sikio lako, 
Uwasahau watu wako na nyumba ya baba yako.
Naye mfalme atautamani uzuri wako,
Maana ndiye bwana wako, nawe umsujudie. (K)

Binti mfalme yumo ndani ana fahari tupu, 
Mavazi yake ni nyuzi za dhahabu.
Atapelekwa kwa mfalme
Wanawali wenzake wanaomfuata. (K)

Watapelekwa kwa furaha na shangwe,
Na kuingia katika nyumba ya mfalme.
Badala ya baba zako watakuwapo watoto wako, 
Utawafanya kuwa wakuu katika nchi zote. (K)


SHANGILIO
Zab. 119:105

Aleluya, aleluya,
Neno lako ni taa ya miguu yangu, 
na mwanga wa njia yangu.
Aleluya.


INJILI
Lk. 6:20 – 26

Yesu aliinua macho yake akawatazama wanafunzi wake, akasema,
Heri ninny imlio maskini, kwa sababu ufalme wa Mungu ni wenu.
Heri ninyi mlio na njaa sasa, kwa sababu mtashiba.
Heri ninny mliao sasa, kwa sababu mtacheka.

Heri ninyi watu watakapowachukia na kuwatenga, na kuwashutumu, na kulitupa nje jina lenu kama neno ovu, kwa ajili ya Mwana wa Adamu.

Furahiwani siku ile na kuruka-ruka, kwa kuwa, tazama, thawabu yenu ni kubwa mbinguni; maana, baba zao waliwatenda manabii vivyo hivyo.

Lakini, ole wenu ninyi mlio na mali, kwa kuwa faraja yenu mmekwisha kuipata.

Ole wenu ninyi ambao mmeshiba sasa, kwa kuwa mtaona njaa.
Ole wenu ninyi mnaocheka sasa, kwa kuwa mtaomboleza na kulia.
Ole wenu ninyi watu wote watakapowasifu, kwa kuwa baba zao waliwatenda manabii wa uongo mambo kama hayo.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MUNGU ANA MPANGO NASI!


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatatu, Septemba 8, 2026 
Juma la 23 la Mwaka


Sikukuu ya Kuzaliwa Bikira Maria Mtakatifu

Mik 5: 1-4 au Rum 8: 28-30; 
Zab 12: 6; 
Mt 1: 1-16, 18-23


MUNGU ANA MPANGO NASI!

Bikira Maria Mama yetu, alichukuliwa mimba kitakatifu, alizaliwa na kuishi bila dhambi, na sasa anatuombea ili hata mmoja wetu asipotee. Sisi, wanawe tunafurahi kusheherekea sikukuu yake ya kuzaliwa. Kuhusu sikukuu ya leo Mt. Andrea wa Crete anasema,"viumbe vyote vilivyo umbwa viimbe sifa na kucheza na kwa pamoja viungane kuadhimisha utukufu wa siku hii...kwani leo hekalu limejengwa kwa ajili ya Muumba wa ulimwengu". Maria alizaliwa kama hekalu la Muumba, na kwa njia ya utii wake akatimiza lengo lake ambalo alizaliwa kwa ajili yalo.

Kama Mungu alivyokuwa na mpango kwa Maria, kuzaliwa kwetu sio kwa bahati mbaya au makosa. Mungu ana mpango nasi. Kama Maria alivyotimiza lengo lake duniani, tunapaswa kutambua lengo letu katika maisha na kuwa waaminifu kwa lengo hilo. Tunapaswa kuheshimu maisha ya wengine pia, kwani Mungu naye ana mpango nao pia! Tuwaombee kwa namna ya pekee “ watoto wa kike” ambao siku hii pia ni maalumu kwa ajili yao pia

Sala: Bwana, kwa maombezi ya Bikira Maria Mama yetu, tufundishe kuheshimu kila mtu. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA SEPTEMBA 8, 2026


MASOMO YA MISA 
JUMATATU, SEPTEMBA 8, 2026
JUMA LA 23 LA MWAKA


SIKUKUU YA KUZALIWA BIKIRA MARIA MTAKATIFU

SOMO 1
Rum. 8:28 – 30

Twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake. Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi. Na wale aliowachagua tangu asili, hao akawaita; na wale aliowaita, hao akawahesabia haki; na wale aliowahesabia haki, hao akawatukuza.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 13:5 – 6 (K) Isa. 61:10

(K) Nitafurahi sana katika Bwana.

Nami nimezitumainia fadhili zako;
Moyo wangu na uufurahie wokovu wako. (K)

Naam, nimwimbie Bwana,
Kwa kuwa amenitendea kwa ukarimu. (K)



INJILI
Mt. 1:1 – 16, 18 – 23

Kitabu cha ukoo wa Yesu Kristo, mwana wa Daudi, mwana wa Ibrahimu.

Ibrahimu alimza Isaka; Isaka akamzaa Yakobo; Yakobo akamzaa Yuda na ndugu zake; Yuda akamzaa Peresi na zera kwa Tamari; Peresi akamzaa Esromu; Esromu akamzaa Aramu; Aramu akamzaa Aminadabu; Aminadabu akamzaa Nashoni; Nashoni akamzaa Salmoni; Salmoni akamzaa Boazi kwa Rahabu; Boazi akamzaa Obedi kwa Ruthu; Obedi akamzaa Yese; Yese akamzaa mfalme Daui. Daudi akamzaa Sulemani kwa yule mke wa Uria; Sulemani akamzaa Rehoboamu; Rehoboamu akamzaa Abiya; Abiya akamzaa Asa; Asa akamzaa Yehoshafati; Yehosahafati akamzaa Yoramu; Yoramu akamzaa Uzia; Uzia akamzaa Yothamu; Yothamu akamzaa Ahazi; Ahazi akamzaa Hezekia; Hezekia akamaza Yosia; Yosia akamzaa Yekonia na ndugu zake, wakati wa ule uhamisho wa Babeli. Na baada ya ule uhamisho wa Babeli, Yekonia akamzaa Shealtieli; Shealtieli akamzaa Zerubabeli; Zerubabeli akamzaa Abihudi; Abihudi akamzaa Eliakimu; Eliakimu akamzaa Azori; Azori akamzaa Sadoki; Sadoki akamzaa Akimu; Akimu akamzaa Eliudi; Eliudi akamzaa Eleazari; Eleazari akamzaa Matani; Matani akamzaa Yakobo; Yakobo akamzaa Yusufu mumewe Mariamu aliyemzaa Yesu aitwaye Kristo.

Kuzaliwa kwake Yesu Kristo kulikuwa hivi.

Mariamu mama yake alipokuwa ameposwa na Yusufu kabla hawajakaribiana, alionekana ana mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu. Naye Yusufu, mumewe, kwa vile alivyokuwa mtu wa haki, asitake kumwaibisha, aliazimu kumwacha kwa siri. Basi alipokuwa akifikiri hayo, tazama, malaika wa Bwana alimtoke katika ndoto, akisema, Yusufu, mwana wa DAudi, usihofu kumchukua Mariamu mkeo, maana mbimba yake ni kwa uweza wa Roho Mtakatifu. Naye atazaa mwana, nawe utwamwita jina lake Yesu, maana, yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao. Hayo yote yamekuwa, ili litimie neno lililonenwa na Bwana kwa ujumbe wa nabii akisema, Tazama, bikira atachukua mimba, Naye atazaa mwana; Nao watamwita jina lake Imanueli; Yaani, Mungu pamoja nasi.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

WATU WASIO TIWA CHACHU!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatatu, Septemba 7, 2026. 
Juma la 23 la Mwaka


1 Kor 5: 1-8; 
Zab 5: 5-7, 12; 
Lk 6: 6-11


WATU WASIO TIWA CHACHU!


“Mahusiano hayawezi kufa hivi hivi bila sababu. Yanakufa kwacsababu ya ubinafsi na kukosa uelewa”. Kukiwa na upendo na uelewa uhusiano hauwezi kufa kamwe.  Katika Injili ya Leo tunamsikia Yesu akimponya mtu aliye na mkono ulio pooza akiwa katika Sinagogi siku ya Sabato. Katika hali ya kukosa uelewa, kuwa na ubinafsi, na umimi wa viongozi wa Wayahudi, Waandishi na Mafarisayo hawakuruhusu akili zao na mioyo yao kuelewa maneno na matendo ya Yesu. Walianza kumlaumu. Viongozi hawa walikuwa wanajali zaidi kushika sheria za Sabato zaidi ya kuleta nafuu kwa wanao teseka. Waliweza kuokoa mnyama aliyeanguka shimoni siku ya sababu zaidi ya kuonesha huruma kwa mwanadamu mwenzao.

Yesu alikuwa na haki ya kumuokoa yule mgonjwa sio tu kwa kumponya mkono wake lakini hata kumsamehe makosa yake na kumpa neema, Amani na furaha. Mt. Paulo anatuonya sisi tugeuze hali zetu, tuzirekebishe. Tuadhimishe uwepo wetu na Yesu, si kwakurudia chachu ya kale, chachu ya chuki na uovu bali tukiwa donge jipya lisilochachuka ambalo Paulo anasema ni weupe wa moyo na kweli. Tusiwe watu wasio eleweka katika maisha yetu ya ufuasi, tumgeukie Yesu kweli na tuweke lengo la kuacha maisha ya kale. Achana na kiburi, wivu, kushengenya wengine, kufurahia uovu, ubinafsi, uchoyo! Kwani hizi sio sifa za mfuasi wa Yesu. Tuombe neema ya Mungu ituongoze ili daima tuweze kufurahi jirani zetu wanapofanikiwa, tusiwazibie milango tusije tukawa kama mafarisayo na waandishi. 

Sala: Ee Bwana, tusaidie tuweze kusafisha chachu ya kale na kuiondoa, tunaomba utufanye donge jipya la uaminifu na kweli. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA JUMATATU, SEPTEMBA 7, 2026



MASOMO YA MISA 
JUMATATU, SEPTEMBA 7, 2026
JUMA LA 23 LA MWAKA


SOMO 1
1Kor. 5:1 – 8

Habari imeenea ya kuwa kwenu kuna zinaa, na zinaa ya namna isiyokuwako hata katika Mataifa, kwamba mtu awe na mke wa babaye. Nanyi mwajivuna, wala hamkusikitika, ili kwamba aondolewe miongoni mwenu huyo aliyetenda jambo hilo. Kwa maana kweli, nisipokuwapo kwa mwili, lakini nikiwapo kwa roho, mimi mwenyewe, nimekwisha kumhukumu yeye aliyetenda jambo hilo, kana kwamba nikiwapo. Katika jina la Bwana wetu Yesu, ninyi mkiwa mmekusanyika pamoja na roho yangu, pamoja na uweza wa Bwana wetu Yesu; kumtolea Shetani mtu huyo, ili mwili uadhibiwe, ili na roho iokolewe katika siku ya Bwana Yesu.

Kujisifu kwenu si kuzuri. Hamjui kwamba chachu kidogo hulichachusha donge zima? Basi, jisafisheni, mkatoe ile chachu ya kale, mpate kuwa donge jipya, kama vile mlivyo hamkutiwa chachu. Kwa maana Pasaka wetu amekwisha kutolewa kuwa sadaka, yaani, Kristo; basin a tuifanye karamu, si kwa chachu ya kale, wala kwa chachu ya uovu na ubaya, bali kwa yasiyochachika, ndio weupe wa moyo na kweli.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 5:4 – 6, 11 (K) 8

(K) Bwana, uniongoze kwa haki yako.

Unawachukia wote watendao ubatili.
Utawaharibu wasemao uongo;
Bwana humzira mwuaji na mwenye hila. (K)

Maana huwi Mungu apendezwaye na ubaya;
Mtu mwovu hatakaa kwako;
Wajivunao hawatasimama mbele za macho yako. (K)

Nao wote wanaokukimbilia watafurahi;
Watapiga daima kelele za furaha.
Kwa kuwa Wewe unawahifadhi,
Walipendao jina lako watakufurahia. (K)


SHANGILIO
Zab. 19:8

Aleluya, aleluya,
Amri ya Bwana ni safi, 
huyatia macho nuru. 
Alelluya.


INJILI
Lk. 6:6 – 1

Ilikuwa siku ya sabato nyingine Yesu aliingia katika sinagogi akafundisha; na mlikuwamo mtu ambaye mkono wake wa kuume umepooza. Na waandishi na Mafarisayo walikuwa wakimvizia, ili waone kwamba ataponya siku ya sabato; kusudi wapate neno la kumshitakia. Lakini yeye atakayatambua mawazo yao, akamwambia yule mwenye mkono uliopooza, Ondoka, simama katikati; akaondoka akasimama.

Ndipo Yesu akawaambia, Nawauliza ninyi, Je! Ni halali siku ya sabato kutenda mema, au kutenda mabaya; kuponya roho au kuangamiza? Akawakazia macho wote pande zote, akamwambia yule mtu, Nyosha mkono wako. Akaunyosha; mkono wake ukawa mzima tena. Wakajawa na uchungu, wakashauriana wao kwa wao wamtendeje Yesu.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUJENGA JUMUIYA YENYE KUWA NA TAHADHARI!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila Jumapili
Jumapili, Septemba 6, 2026

Dominika ya 23 ya Mwaka

Ez 33: 7-9;
Zab 94: 1-2, 6-9;
Rom 13: 8-10;
Mt 18: 15-20


KUJENGA JUMUIYA YENYE KUWA NA TAHADHARI!

Wakati watu wameshakutana na ugumu fulani, wanakuwa wanatoa kiashirio kwa wengine kwamba muelekeo sio mzuri, viashirio vyao mara nyingi wengi hawa vitilii maanani. Lakini katika hali ya kweli, wengi hupenda kuwatazama wengine wakiwa katika njia isio faa. Mara nyingi wanawachukia, kuwatania na kuwaona wajinga. Mungu analinganisha kazi ya nabii Ezekieli na ya mlinzi. Alikuwa apewe onyo kutoka kwa Mungu naye alipeleke onyo hilo kwa kila mtu. Kazi ya Kanisa na ya kila mkristo ni sawa sawa. Ni kuwaongoza watu kwa ujumbe wa neno la Mungu. Siku hizi tunatumia teknolojia yenye nguvu kuwapa watu ishara ya hatari ya kujisahau kushika neno la Mungu. Tunachofanya leo na teknolojia kilifanyika katika Biblia, ambapo waliwaweka walinzi katika sehemu Fulani ili aweze kutoa ishara ya hatari wakati aduia anataka kukaribia.

"Mtu mmoja alikuwa akishanga shangaa aliokota ufunguo bondeni karibu na mlima mkubwa. Ulikuwa ni ufunguo wa ajabu, ufunguo ambao ulikuwa na uwezo wakufungua kila aina ya nyumba yenye hazina ulimwenguni. Kwa ufunguo huu alikusanya dhahabu na almasi kutoka katika sehemu mbali mbali alizopenda duniani. Akiwa njiani akirudi alisikia sauti ikimwambia kutoka chini ya mlima: “kabla haujatoka nje, hakikisha hausahau kitu muhimu kuliko vyote. Gafla mlango ukafunga moja kwa moja. Alikuwa amesahau kuchukua ufunguo.”

Mwanadamu daima anatafuta kupata ufunguo wa furaha, Amani na kujitosheleza. Sisi wote tunatafuta ufunguo wa urafiki, kueleweka, kuwa na jina na uzuri, na kuwa na kazi nzuri yenye kuvutia na faraja. Wengine wanatafuta furaha kwa fedha, madaraka nk. Lakini hivi vyote vinatufunga na kujikuta tunapotelea huko. Vinatufunga kiasi ambacho tunasahau kitu muhimu ziadi nacho ni ufunguo wa maisha. Maisha ya Ukristo yanatufundisha kwamba dunia hii itapita, hiki ndicho tunacho paswa kuzingatia kwa macho yetu na kutazama “maisha ya umilele”. Hii inamaana kwamba maisha yetu hapa duniani yana lengo zaidi ya lengo la kawaida. Furaha tulio nayo hapa sio kitu, ni kivuli tu cha furaha halisi ambayo tutakuwa nayo huko mbinguni. Lakini ufunguo wa furaha ya maisha haya uko wapi?

Katika somo la Injili ya leo Yesu anatuonesha picha nzuri ya jumuiya ya mapendo na yenye kujali. Inatuonesha ni kwa jinsi ghani tunaweza kuanzisha jumuiya ya kweli ya Kikristo na yenye kupendana.

1. Kama mtu akikukosa, tunapaswa tumwendee kwa upendo wa Kimungu na kumrudisha kundini. Tofauti kabisa na kumlaumu na kuanza kumlaumu, tunapaswa kumfuata kwa mapendo na kumsihi katika mapendo yetu. Injili inatushauri kuwa na mazungumzo ya moja kwa moja, kwa utulivu na katika hali ya upekee, katika hali ya kurekebishana kindugu, ili kuanzisha tena urafiki uliyo vunjika. Kama hili litashindikana inashauriwa kuchukuwa watu wenye hekima na kumfuata kumuonesha kwamba jumuiya nzima inakuhitaji kurudi kundini katika mapendo yote.

2. Yesu anasisitiza nguvu ya sala. Anasema “pale wawili au watatu walipokusanyika kwa ajili yangu, Baba atakuwa katikati yao”. Huu ni uhakika anaotoa Yesu kwamba wale wanaosali yeye atakuja katikati yao na kuwa kati yao na kushiriki katika sala yao. Wayahudi walikuwa na Imani kubwa katika sala za pamoja. Iliandikwa “wawili walipo kusanyika na wanajihusisha na kujifunza Torati, utukufu wa Mungu upo katikati yao” sala za jumuiya huweka magomvi mbali na kuleta umoja. Agano, jumuiya, ukarimu, msamaha hizi ni sifa za dini ya Kibiblia. Uzoefu wa haya yote vinafanya maisha yetu kuwa na furaha, na kuishi vizuri. Haya yote yanawezekana tu pale ambapo tuna upendo. Kwa mfano,

"Mfungwa mmoja alikuwa anarudi nyumbani, kutoka katika mahabusu ya mbali akiwa kwenye treni. Alikuwa akiona aibu kwa kufungwa kwake na alikuwa akidhani familia yake itakuwa imemsamehe. Kwa ishara ya kuonesha kwamba wamemsamehe, walipaswa wafunge riboni nyeupe kwenye mti ambao ulikuwa karibu na gari nyumbani kwake. Hivyo kama hataona riboni nyeupe kwenye mti, yeye atapitiliza na treni aelekee kokote atakapo kwenda. Wakati treni ilivyofika karibu na nyumbani, akawa na wasi wasi mkubwa kiasi ambacho hakuthubutu kutazama kupitia dirishani. Marafiki zake wakaamua kubadilisha nafasi wakisema tunafahamu tu ataangalia mti uliokaribu na gari. Ghafla akanyanyua kichwa bila kujua na tazama sio roboni moja iliyowekwa kwenye mti bali mti wote ulikuwa umejaa riboni"

Amani na mshikamano unawezekana tu, pale ambapo watu wanaishi kwa roho ya upendo na msamaha. Mungu ni upendo na penye upendo Mungu yupo. Upendo wa Mungu unabeba pia upendo kwa jirani. Upendo tunaweza kuupata tu tunapo amua kuishi na wenzetu, kwa mshikamano katika jumuiya. Hili halimuumizi mtu yeyote, bali linakamilisha kila kitu na kufanya maisha yafikie katika kilele cha hali ya juu.

Mungu ametufanya sisi tuwe walinzi wa dunia sasa. Tunapaswa kuwa walinzi, kutangaza kwa kila mmoja, jumuiya zetu, na ulimwengu wa ukweli katika Yesu Kristo. Tunaitwa kusimama pamoja, bila kuachana katika Imani bila kuogopa kuitwa tusio na maana au mafundisho potofu, bali tutangaze kwa jirani na jumuiya zetu, ili watu wafahamu katika kutokufahamu kwao, kumuamini Yesu, na kukuwa katika neema na utakatifu. Tunapaswa kuwasaidia wengine watambue makosa yao, hasa tukiwa na kazi kama ya wazazi kwa mtoto, mwalimu kwa wanafunzi, wazee na vijana.

Tutumie njia sawa ya kuwasaidia wengine watoke katika makosa yao bila ya kuwaumiza au kuwadhalilisha na kuwaachia makovu. Badala ya kuponya tukakuza kidonda zaidi. Katika vikao vyetu tuangalie njia njema ya kumsadia mtu na kumuonya badala ya kumwanika hadharani mbele ya watu wote, kama kuna njia nzuri ya mtu mmoja kumfuata kwa hekima utamsaidia zaidi, kuliko kumkosoa mtu mbele ya watu wengi au katika kikao, hili haliponyi kwani mmoja hujisikia amedhalilishwa na utu wake kudharauliwa. Mfano tusisubiri mpaka mtu afe ndio tupate muda wa kukaa pamoja tuje kumrekebisha mtu mbele ya kikao cha ukoo, badala yake tutumie njia mbadala ya kutuma mtu mwenye hekima amsaidie na kupatana kabla ya kukaa pamoja. Kutangaza dhambi ya mtu mbele ya kikao, daima haina lengo la kuleta upatanisho wa kweli badala yake humuachia mtu maumivu na kisasi moyoni. Hakuna hata mmoja wetu angependa dhambi yake itajwe mbele ya watu. Ndio maana sakramenti ya kitubio husaidia kweli. Tumuige Yesu aliyekuwa na huruma kwa wadhambi.

Sala: Bwana, upo nasi katika jumuiya yetu, tukishikana pamoja kwa mapendo, huruma na msamaha. Tunakuomba tuwe watu wakutafuta furaha, upendo na Amani. Tunakuomba tuwe tayari kusamehe na kupatana na kila mtu. Yesu, ninakuamini wewe. Amina

------------------------
Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUMAPILI, SEPTEMBA 6, 2026



MASOMO YA MISA,
JUMAPILI, SEPTEMBA 6, 2026
JUMA LA 23 LA MWAKA
________

MWANZO
Zab. 119:137, 124

Ee Bwana, wewe ndiwe mwenye haki, na hukumu zako ni za adili. Kama zilivyo rehema zako umtendee mtumishi wako.
________

SOMO I
Eze. 33:7-9

Basi wewe, mwanadamu, nimekuweka kuwa mlinzi kwa nyumba ya Israeli; basi ulisikie neno hili kinywani mwangu, ukawape maonyo yangu. Nimwambiapo mtu mbaya, Ewe mtu mbaya, hakika utakufa, nawe husemi neno la kumwonya mtu huyo, aiache njia yake, mtu mbaya huyo atakufa katika uovu wake, lakini damu yake nitaitaka mkononi mwako. Walakini ukimwonya mtu mbaya kwa sababu ya njia yake, kusudi aiache; wala yeye asiiache; atakufa huyo katika uovu wake, lakini wewe umejiokoa roho yako.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu
________

WIMBO WA KATIKATI
Zab. 95:1-2, 6-9 (K) 7-8

(K) Ingekuwa heri leo tusikie sauti yake!

Tusifanye migumu mioyo yetu.
Njoni tumwimbie Bwana,
Tumfanyie shangwe mwamba wa wokovu wetu.
Tuje mbele yake kwa shukrani,
Tumfanyie shangwe kwa zaburi. (K)

Njoni, tuabudu, tusujudu,
Tupige magoti mbele za Bwana aliyetuumba.
Kwa maana ndiye Mungu wetu,
Na sisi tu watu wa malisho yake,
Na kondoo za mkono wake. (K)

Ingekuwa heri leo msikie sauti yake!
Msifanye migumu mioyo yenu;
Kama vile huko Meriba;
Kama siku ile ya Masa jangwani,
Hapo waliponijaribu baba zetu;
Wakanipima, wakayaona matendo yangu. (K)
________

SOMO 2
Rum. 13:8-10

Msiwiwe na mtu chochote, isipokuwa kupendana; kwa maana ampendaye mwenzake ameitimiza sharia. Maana kule kusema, Usizini, Usiue, Usiibe, Usitamani, na ikiwapo amri nyingine yoyote, inajumlishwa katika neno hili, ya kwamba, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Pendo halimfanyii jirani neno baya, basi pendo ndilo utimilifu wa sheria.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu
________

SHANGILIO
Yn. 14:23

Aleluya, aleluya,
Mtu akinipenda, atalishika neno langu;
Na baba yangu atampenda; Nasi tutakuja kwake.
Aleluya.
________

INJILI
Mt. 18:15-20

Siku ile Yesu aliwaambia wafuasi wake: Ndugu yako akikukosa, enenda ukamwonye, wewe na yeye peke yenu; akikusikia, umempata nduguyo. La, kama hasikii, chukua pamoja nawe tena mtu mmoja au wawili, ili kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila neno lithibitike. Na asipowasikiliza wao, liambie kanisa; na asipolisikiliza kanisa pia, na awe kwako kama mtu wa mataifa na mtoza ushuru. Amin, nawaambieni, yoyote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni; na yoyote mtakayoyafungua duniani yatakuwa yamefunguliwa mbinguni.



Tena nawaambia, ya kwamba wawili wenu watakapopatana duniani katika jambo lolote watakaloliomba, watafanyiwa na Baba yangu aliye mbinguni. Kwa kuwa walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo
________

-------------------------
Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.