Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

Mt. YOSEFU: MTU WA NDOTO NA MTU WA KAZI!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kwaresima 
Alhamisi, Machi 19, 2026
Juma la 5 la Kwaresima

Sherehe ya Mt. Yosefu, Mume wa Bikira Maria. 

2Sam 7:4-5,12-14,16; 
Zab 89:2-5,27,29; 
Rum 4:13,16-18,22; 
Mt 1:16,18-21,24 au Lk 2:41-51


Mt. YOSEFU: MTU WA NDOTO NA MTU WA KAZI! 

“Wakati Yosefu alivyo amka, alifanya kama malaika alivyo mwambia” (Mt 1:24). Haya maneno ya mwisho ya Injili ya leo, yanatupa muktasari mzima wa sherehe ya leo, ya Mt. Yosefu mume wa Bikira Maria. Maandiko yanatuambia kuwa Yosefu alikuwa mwana wa Yakobo na mume wa Maria na pia ni Mseremala kutoka Nazareth. Baada ya kumposa Maria, baada ya kutambua Bikira Maria ana mimba kabla hawajaanza kuishi pamoja, Yosefu akiwa ni mtu mwaminifu katika sheria, anaacha kumwaibisha Maria na ana azimu kumwacha kwa siri. Mungu aliongea naye kwenye ndoto na akatii. Malaika wa Bwana alimtokea katika ndoto na akafunua mpango wa Mungu kwa mwanadamu, na akamchukua Maria nyumbani kama mke wake.

Cha kuvutia, ni kwamba Yosefu hajaongea neno lolote katika maandiko (Injili). Bali ni mtu wa vitendo tu: anafanya alicho ambiwa na Malaika, anamchukua Maria kama mke wake na anaenda Bethlehemu: anatafuta sehemu ya kujihifadhi usiku, na anachukua familia yake Misri. Ingawaje sio matu wa maneno, lakini kwa hakika ni mtu wa matendo. Mungu alikuwa na mpango na Yosefu, na alikuwa tayari kuyafanya mapenzi ya Mungu. Alikuwa ni mtu ambaye alikuwa akiyafuata mapenzi ya Mungu. Shauku ya maisha ya baadae, na vipingamizi vya nje havikumzuia kuacha kuyatimiza mapenzi ya Mungu. Kwasababu alikuwa mwamini fu kutimiza mapenzi ya Mungu, Mungu alikuwa naye katika maisha yake yote.
Somo la kwanza kutoka katika kitabu cha Samueli na pia wimbo wa katikati unatumbia kwamba Mfalme Daudi aliahidiwa kuwa mtoto wake ataishi milele. Daudi hakubaki mpaka kuiona ahadi hii ikitimia. Katika somo la pili, Paulo anawaeleza Warumi kuhusu Abraham, mtu mwingine mwenye haki ambaye hakuishi mpaka kuona matunda ya kazi yake. Alifanya mapenzi ya Mungu, lakini hakuona kutimia kwa ahadi ya Mungu kwake. Ingawaje hayakutimizwa kwa kipindi chake alitumaini na kuamini na Imani yake ilimpa kibali kwa Mungu. Katika somo la Injili tunamuona Yosefu mwenye Imani kwa Bwana. Alitembea katika majaribu mbali mbali kwa Imani. Aliamka kutoka katika ndoto na anakaanza kuweka kwenye matendo. Nini tunaweza kujifunza kutoka kwa Yosefu. 

Utii kwa Mungu zaidi kuliko mwanadamu: sheria ilimwambia Yosefu kumwacha Maria na kumwacha aadhibiwe. Lakini hakusikiliza mawazo yake mwenyewe au kilichosemwa na sheria na watu. Yeye kwa nafsi yake anafuata mapenzi ya Mungu. Yosefu alikuwa mtu shujaa katika kumtii Mungu licha ya msukumo wa tamaduni. Je, jamii au Imani yangu inaleta mchango katika maamuzi yangu?

Wito ni muhimu kuliko kazi zetu: kwa Yosefu mpango wa Mungu maishani mwake ulikuwa muhimu zaidi kuliko mambo yake ya kijamii, kazi na familia. Yosefu yeye alikuwa Baba mume kabla yakuwa mseremala. Mungu wake, na familia yake ilikuwa muhimu zaidi kuliko kazi yake. Wito wake ulipita kazi zake. Je, familia yangu inakuwa muhimu zaidi kuliko kazi yangu? Familia inapaswa kuwa ya kwanza. 

Mlinzi wa nyumba yake: Yosefu alikuwa mtu wa kuwa karibu na mke wake na kulinda familia yake. Anaitwa pia mlishi na mlinzi wa kanisa Katoliki. Watu walio mfano wa Yosefu ndio tunaokosa siku hizi. Watoto wetu wana achwa na kuingia kwenye hatari kama, mitandao, picha chafu, ulevi nk. Je, ni kwa jinsi ghani tulivyo walinzi wa familia zetu? 

Mtu wa vitendo: Yosefu alikuwa mfanyakazi, na Mseremala. Hakuwa tu mtu wa ndoto, alikuwa mtu mchapa kazi, aliyepata chakula chake kwa uaminifu. Yosefu ni mfano kwetu kwa watu wanaopata chakula chao kwa kufanya kazi kihalali. 

Yosefu ni mlinzi na mlishi wa Kanisa Katoliki, mlinzi na mlishi wa kanisa katika hatua za mwanzo, wakati kanisa lilipokuwa, Yesu, Maria na Yosefu. Tunafanya vizuri kumuiga Mt. Yosefu na kumuomba atuombee kama akina Baba wa familia walishi na walinzi. Mt. Yosefu utuombee.. 

Sala: Bwana, tunakuomba tuwe watu wakuiga maisha ya Mt. Yosefu ili tuweze kuwa tayari kutimiza mapenzi yako bila kuwa na wasi wasi. Yesu nakumini wewe. Amina 


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MACHI 19, 2026




MASOMO YA MISA, MACHI 19, 2026
ALHAMISI JUMA LA 4 LA KWARESIMA

SHEREHE YA MT. YOSEFU, MUME WAKE BIKIRA MARIA

SOMO 1
2Sam 7:4-5, 12-14

Ikawa usiku uo huo, neno la Bwana likamfikia Nathani kusema, Enenda, ukamwambie mtumishi wangu, Daudi, Bwana asema hivi, Je! Wewe utanijengea nyumba, nikae ndani yake? Nawe siku zako zitakapotimia, ukalala na baba zako, nitainua mzao wako nyuma yako, atakayetoka viunoni mwako, nami nitaufanya imara ufalme wake. Yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa jina langu, nacho kiti cha enzi cha ufalme wake nitakifanya imara milele. Mimi nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwanangu; akitenda maovu nitamwadhibu kwa fimbo ya binadamu na kwa mapigo ya wanadamu; Na nyumba yako, na ufalme wako, vitathibitishwa milele mbele yako. Nacho kiti chako kitafanywa imara milele. 

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu



WIMBO WA KATIKATI
Zab 89:1-4, 26, 28

(K) Wazao wako watadumu milele.

 Fadhili za Bwana nitaziimba milele; 
Kwa kinywa changu nitavijulisha vizazi vyote uaminifu wako. 
Maana nimesema, Fadhili zitajengwa milele; 
Katika mbingu utauthibitisha uaminifu wako. (K)

Nimefanya agano na mteule wangu, 
Nimemuapia Daudi, mtumishi wangu. 
Wazao wako nitawafanya imara milele, 
Nitakijenga kiti chako cha enzi hata milele. (K)

Yeye ataniita, Wewe baba yangu, 
Mungu wangu na mwamba wa wokovu wangu. 
Hata milele nitamwekea fadhili zangu, 
Na agano langu litafanyika amini kwake. (K)



SOMO 2
Rum 4:13, 16-18, 22

Kwa maana ahadi ile ya kwamba atakuwa mrithi wa ulimwengu alipewa Ibrahimu na uzao wake, si kwa sheria bali kwa haki aliyohesabiwa kwa imani.Kwa hiyo ilitoka katika imani, iwe kwa njia ya neema, ili kwamba ile ahadi iwe imara kwa wazao wote; si kwa wale wa torati tu, ila na kwa wale wa imani ya Ibrahimu; aliye baba yetu sisi sote; (kama ilivyoandikwa, Nimekuweka kuwa baba wa mataifa mengi); mbele zake yeye aliyemwamini, yaani Mungu, mwenye kuwahuisha wafu, ayatajaye yale yasiyokuwako kana kwamba yamekuwako. Naye aliamini kwa kutarajia yasiyoweza kutarajiwa, ili apate kuwa baba wa mataifa mengi, kama ilivyonenwa, Ndivyo utakavyokuwa uzao wako. Kwa hiyo ilihesabiwa kwake kuwa ni haki. 

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu



INJILI
Mt 1:16, 18-21, 24

Yakobo akamzaa Yusufu mumewe Mariamu aliyemzaa YESU aitwaye Kristo.Kuzaliwa kwake Yesu Kristo kulikuwa hivi. Mariamu mama yake alipokuwa ameposwa na Yusufu, kabla hawajakaribiana, alionekana ana mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu. Naye Yusufu, mumewe, kwa vile alivyokuwa mtu wa haki, asitake kumwaibisha, aliazimu kumwacha kwa siri. Basi alipokuwa akifikiri hayo, tazama, malaika wa Bwana alimtokea katika ndoto, akisema, Yusufu, mwana wa Daudi, usihofu kumchukua Mariamu mkeo, maana mimba yake ni kwa uweza wa Roho Mtakatifu. Naye atazaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, maana, yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao. Naye Yusufu alipoamka katika usingizi, alifanya kama malaika wa Bwana alivyomwagiza; akamchukua mkewe.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Krist0


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

FURAHI KATIKA MAPENZI YA MUNGU!


 “KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Jumatano, Machi 18, 2026 
Juma la 4 la Kwaresima

Isa 49: 8-15;
Zab 145: 8-9, 13-14, 17-18;
Yn 5:17-30


FURAHI KATIKA MAPENZI YA MUNGU!


Kama mtoto wa Yosefu mseremala, alijifunza ni nini baba yake alipenda. Muda baada ya muda alikuja kuelewa zaidi, jinsi ya kunyoosha au kukata vipande viwili na kuviunganisha. Alianza kuona kazi iliomalizika ya baba yake, kuona meza au kiti alicho tengeneza baba yake. Na mwisho pengine aliweza kutengeneza kama baba yake na kumfanya baba yake afurahi. Leo katika Injili Yesu anaongea na Baba yake wa Mbinguni katika hali ya mfanano kama hiyo. Anasema na kufanya yale malengo ya Baba yake. Kwasababu ameyaweka malengo yote moyoni mwake. Anatambua kabisa katika hali zote ni kwa ajili ya ukombozi. 

Kwa upande wetu, tunaweza kuchukua uelewa wa umoja huu wa Baba na Mwana, somo la utukufu jinsi ya kuingia katika umoja huu na Mungu. Pili, tunapaswa kuamini tunacho elewa, na tukichague kwa ajili ya maisha yetu. Changamoto ni kwamba kuna sauti nyingi zinazo tuita na kushindana na maamuzi yetu. Tukiwa tunachagua kati ya hizo, kuchagua tu ile ambayo Mungu anatufunulia, tunakuwa tunavutwa moja kwa moja kwa mapenzi ya Mungu na kuyafanya. Kwa njia hii sisi nasi tunakuwa wamoja na Mungu. 

Kama Yesu, sisi wote tunataka kufanya mapenzi ya Mungu. Lakini ili kuwa wenye mafanikio katika kazi zetu tunapaswa kutambua picha yote. Mara nyingi tunachoka tukijaribu kuchagua vitu vidogo, kwamba sijui Mungu atapenda nibaki katika familia yangu jioni hii au niende kwenye mkutano parokiani. Ni wazi Yesu anajali kila kitu katika maisha yetu, lakini tutajikuta ni rahisi kufanya uchaguzi sahihi wakati tukiwa na uelewa mkubwa juu ya nini Baba anatengeneza na ni kwa jinsi ghani anatualika kila mmoja wetu kuingia katika malengo yake makubwa. 

Sala: Baba wa Mbinguni, ninakushukuru kwa zawadi ya Yesu Mwanao na ninakushukuru kwa umoja mlionao. Nivute katika utukufu uliopo katika kuyafanya mapenzi yako. Nifanye mmoja wako, uendelee kuwa Baba yangu daima. Baba wa Mbinguni, Yesu Mwana wa Mungu, nakuamini wewe. Amina .

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MACHI 18, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 18, 2026
JUMATANO, JUMA LA 4 LA KWARESIMA


SOMO 1
Isa. 49:8-15

Bwana asema hivi, Wakati uliokubalika nimekujibu, na siku ya wokovu nimekusaidia; nami nitakuhifadhi, nitakutoa uwe agano la watu hawa, ili kuiinua nchi hii, na kuwarithisha urithi uliokuwa ukiwa; kuwaambia waliofungwa, Haya, tokeni; na hao walio katika giza, Jionyesheni.

Watajilisha katika njia, na juu ya majabali watapata malisho. Hawataona njaa, wala hawataona kiu; hari haitawapiga, wala jua; kwa maana yeye aliyewarehemu atawatangulia, naam, karibu na chemchemi za maji atawaongoza. Nami nitafanya milima yangu yote kuwa njia, na njia kuu zangu zitatukuzwa zote.

Tazama, hawa watakuja kutoka mbali; na tazama, hawa kutoka kaskazini, na kutoka magharibi, na hawa kutoka nchi ya sinimu. Imbeni, enyi mbingu; ufurahi, Ee nchi; pazeni sauti ya kuimba, enyi milima; kwa kuwa Bwana amewafariji watu wake, naye atawahurumia watu wake walioteswa.

Bali Sayuni alisema, Yehova ameniacha, Bwana amenisahau. Je! Mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata asimhurumie mwana wa tumbo lake? Naam, hawa waweza kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 145:8-9, 13-14, 17-18 (K)

(K) Bwana ana fadhili, ni mwingi wa huruma.

Bwana ana fadhili, ni mwingi wa huruma,
Si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema.
Bwana ni mwema kwa watu wote,
Na rehema zake zi juu ya kazi zake zote. (K)

Ufalme wako ni ufalme wa zamani zote,
Ni mamlaka yako ni ya vizazi vyote.
Bwana huwategemeza wote waangukao,
Huwainua wote walioinama chini. (K)

Bwana ni mwenye haki katika njia zake zote,
Na mwenye fadhili juu ya kazi zake zote.
Bwana yu karibu na wote wamwitao,
Wote wamwitao kwa uaminifu. (K)



SHANGILIO
Mt. 4:4

Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.



INJILI
Yn. 5:17-30

Yesu aliwajibu Wayahudi: Baba yangu anatenda kazi hata sasa, nami ninatenda kazi. Basi kwa sababu hiyo Wayahudi walizidi kutaka kumwua, kwa kuwa hakuivunja sabato tu, bali pamoja na hayo alimwita Mungu Baba yake, akijifanya sawa na Mungu.

Basi Yesu akajibu, akawaambia, Amin, amin, nawaambia, Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe ila lile ambalo amwona Baba analitenda; kwa maana yote ayatendayo yeye, ndiyo ayatendayo Mwana vile vile. Kwa kuwa Baba ampenda Mwana, naye humwonyesha yote ayatendayo mwenyewe; hata na kazi kubwa zaidi kuliko hizi atamwonyesha ili ninyi mpate kustaajabu. Maana kama Baba awafufuavyo wafu na kuwahuisha, vivyo hivyo na Mwana ahuisha wale awatakao. Tena Baba hamhukumu mtu yeyote, bali amempa Mwana hukumu yote, ili watu wote wamheshimu Mwana kama vile wanavyomheshimu Baba. Asiyemheshimu Mwana hamheshimu Baba aliyempeleka.

Amin, amin, nawaambia, yeye alisikiaye neno langu na kumwamini yeye aliyenipeleka yuna uzima wa milele; wala haingii hukumuni, bali amepita kutoka mautini kuingia uzimani. Amin, amin, nawaambia, Saa inakuja, na sasa ipo, wafu watakapoisikia sauti ya Mwana wa Mungu, na wale waisikiao watakuwa hai.

Maana kam avile Baba alivyo na uzima nafsini mwake, vivyo hivyo alimpa na Mwana kuwa na uzima nafsini mwake. Naye akampa amri ya kufanya hukumu kwa sababu ni Mwana wa Adamu. Msistaajabie maneno hayo; kwa maana sasa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu. Mimi siwezi kufanya neno mwenyewe; kama nisikiavyo ndivyo nihukumuvyo na hukumu yangu ni ya haki, kwa sababu siyatafuti mapenzi yangu mimi, bali mapenzi yake aliyenipeleka.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

INUKA!


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Kwaresima
Jumanne, Machi 17, 2026 
Juma la 4 la Kwaresima

Ez 47: 1-9, 12;
Zab 46: 2-3, 5-6, 8-9; 
Yn 5: 1-16.

INUKA!

Leo nabii Ezekieli anatupa alama nzuri ya picha ya jinsi ya kuzaliwa upya na kuwa mpya.! Kama mfereji mdogo unaotoka katika hekalu na kuwa mto Mkubwa, ardhi kavu ya Israeli itasitawi kwa miti yenye matunda. Katika nchi ambayo daima iliteseka kwa ukame na kwa kukosa maji, sasa itasitawi, jambo hili lilikuwa la matumiani makubwa. Wakristo wa mwanzo waliamini kwa njia ya Yesu hili lilitimia. Yeye ni hekalu hai la Mungu. Yeye ni chemchemi ya maji ya uzima. Ambapo kutoka kwake miito mikubwa humwaga maji, ambapo kwa ubatizo unafanya upya ulimwengu na kuichipusha. Kanisa limeona kutoka kwa Ezekeli alama ya ubatizo. Kama vile maji ya mto huleta ukuwaji wa vitu na mengi hufanywa upya, ndivyo maji ya ubatizo yanatuletea kuzaliwa upya rohoni na kufanya yote upya tena.

Katika Injili, Yesu anamponya mgonjwa aliye pooza. Kupooza kwa mwili ni alama inayowakilisha matokeo ya dhambi. Tukitenda dhambi tunakuwa “tumepooza” sisi wenyewe. Dhambi ina matokeo katika maisha yetu na matokeo ambayo ni hakika kabisa ni kwamba tunabaki tumeanguka na tunashindwa kutembea katika njia za Mungu. Dhambi za mauti hasa, zinatufanya tukose nguvu ya kupenda na kuishi huru. Inatuacha katika mtego tukiwa tunashindwa kujali maisha yetu ya kiroho au ya wengine katika hali yeyote. Ni vizuri kuona matokeo ya dhambi. Hata dhambi ndogo inatuathiri uwezo wetu, inatukosesha nguvu, na kutuacha tukiwa vilema kwa njia moja au nyingine.

Tunapaswa kujiona wenyewe katika habari hii. Yesu hakumponya huyu mgonjwa kwa faida yake mwenyewe tu. Anamponya akitaka kutuambia kwamba anatuona katika udhaifu wetu tukiwa tunapatwa na matokeo ya dhambi zetu, anatuangalia na kutuita tuinuke tena na kutembea naye. Angalia dhambi yako, mruhusu Yesu aione, na msikilize akiongea maneno ya uponyaji na uhuru. Yesu anatupatia uponyaji kwa njia ya Sakramenti ya Kitubio, hasa wakati huu wa Kwaresima. Nenda kaungame na gundua uponyaji wa Yesu. Kitubio ni jibu la uhuru unao tungoja sisi, kutufanya upya na kuwa na Baraka, neema na maisha ya mtu aliye jaa mema.

Sala: Bwana, naomba unisamehe dhambi zangu. Ninatamani kuzifahamu nakuona matokeo yake. Ninajua unatamani daima kuniweka huru kutoka katika mizigo hii na kuiponya kutoka katika chanzo chake. Bwana, nipe nguvu niweze kuziungama dhambi zangu kwako, hasa katika sakramenti ya Kitubio. Yesu nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MACHI 17, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 17, 2026, 
JUMANNE: JUMA LA 4 LA KWARESIMA


SOMO 1
Eze. 47:1-9, 12

Malaika alinileta mpaka lango la nyumba; na tazama, maji yalitoka chini ya kizingiti cha nyumba, kwa njia ya mashariki, maana upande wa mbele wa nyumba ulielekea upande wa mashariki; nayo maji yakashuka toka chini ya upande wa kuume wa nyumba, upande wa kusini wa madhabahu. Ndipo akanileta nje kwa njia ya lango upande wa kaskazini, akanizungusha kwa njia ya nje mpaka lango la nje, kwa njia yake iliyoelekea mashariki; na tazama, maji yalitoka upande wa kuume. Na alipotoka mtu yule, mwenye uzi wa kupimia mkononi mwake, kwenda masharikini, akapima dhiraa elfu, akanivusha maji yale; maji yakafika mpka viweko vya miguu.
Kisha akapima dhiraa elfu, akanivusha maji yale, maji yakafika mpaka magoti. Kisha akapima dhiraa elfu, akanivusha, maji yakafika mpaka viuno. Kisha akapima dhiraa elfu, yakawa mto nisioweza kuuvuka; maana maji yamezidi, maji ya kuogelea, mto usiovukika. Akaniambia, Mwanadamu, je! Umeona haya? Kisha akanichukua, akanirudisha mpaka ukingo wa mto.

Basi nikiisha kurudi, tazama, kando ya ukingo wa mto ilikuwapo miti mingi sana, upande huu na upande huu. Ndipo akaniambia, Maji haya yanatoka kwenda pande za nchi ya mashariki, nayo yanashuka mpaka Araba, na kuingia katika bahari; maji yatokezwayo yataingia baharini, na maji yake yataponyeka. Tena itakuwa, kila kiumbe hai kisonganamacho, kila mahali itakapofika mito hiyo, kitaishi; kutakuwapo wingi mkubwa wa samaki, kwa sababu maji haya yamefika huko; maana maji yale yataponyeka, na kila kitu kitaishi popote utakapofikilia mto huo.

Na karibu na mto, juu ya ukingo wake, upande huu na upande huu, utamea kila mti wa chakula, ambao majani yake hayatanyauka, wala matunda yake hayatatindika kamwe; utatoa matunda mapya kila mwezi, kwa sababu maji yake yanatoka mahali patakatifu; na matunda yake yatakuwa ni chakula; na majani yake yatakuwa ni dawa.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 46:1-2, 4-5, 7-8 (K) 7

(K) Bwana wa majeshi yu pamoja nasi, Mungu wa Yakobo ni ngome yetu.

Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu,
Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso.
Kwa hiyo hatutaogopa ijapobadilika nchi,
Ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. (K)

Kuna mto, vijito vyake vyaufurahisha mji wa Mungu,
Patakatifu pa maskani zake Aliye juu.
Mungu yu katikati yake hautatetemeshwa; 
Mungu atausaidia asubuhi na mapema. (K)

Bwana wa majeshi yu pamoja nasi,
Mungu wa Yakobo ni ngome yetu.
Njoni myatazame matendo ya Bwana,
Jinsi alivyofanya ukiwa katika nchi. (K)


SHANGILIO
Amo. 5:14

Tafuteni mema, wala si mabaya, mpate kuishi, hivyo Bwana, atakuwa pamoja nanyi.


INJILI
Yn. 5:1-3, 5-16

Baada ya hayo palikuwa na sikukuu ya Wayahudi; naye Yesu akakwea kwenda Yerusalemu. Na huko Yerusalemu penye mlango wa kondoo pana birika, iitwayo kwa Kiebrania Betzatha, nayo ina matao matano. Ndani ya hayo jamii kubwa ya wagonjwa walikuwa wamelala, vipofu, viwete, nao waliopooza.

Na hapa palikuwa na mtu, ambaye amekuwa hawezi muda wa miaka thelathini na minane. Yesu alipomwona huyu amelala, naye akijua ya kuwa amekuwa hali hiyo siku nyingi, alimwambia, Wataka kuwa mzima? Yule mgonjwa akamjibu, Bwana, mimi sina mtu wa kunitia birikani, maji yanapotibuliwa; ila wakati ninapokuja mimi, mtu mwingine hushuka mbele yangu. Yesu akamwambia, Simama, jitwike godoro lako, uende. Mara yule mtu akawa mzima, akajitwika godoro lake, akaenda.

Nayo ilikuwa ni sabato siku hiyo. Kwa sababu hiyo Wayahudi wakamwambia yule aliyeponywa, Leo ni sabato, wala si halali kwako kujitwika godoro. Akawajibu, Yeye aliyenifanya kuwa mzima ndiye aliyeniambia, Jitwike godoro lako, uende. Basi wakamwuliza, Yule aliyekuambia, Jitwike uende, ni nani? Lakini yule mtu aliyeponywa hakumjua ni nani; maan aYesu alikuwa amejitenga, kwa sababu palikuwa na watu wengi mahali pale.

Baada ya hayo Yesu akamkuta ndani ya hekalu, akamwambia, Angalia, umekuwa mzima; usitende dhambi tena, lisije likakupata jambo lililo baya zaidi. Yule akaenda zake, akawapasha habari Wayahudi ya kwamba ni Yesu aliyemfanya kuwa mzima. Kwa sababu hiyo Wayahudi wakamwudhi Yesu, kwa kuwa alitenda hayo siku ya sabato.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

IMANI KWA YESU



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Kwaresima
Jumatatu, Machi 16, 2026.
Juma la 4 la Kwaresima

Isa 65: 17-21;
Zab 29: 2, 4-6, 11-13;
Yn 4: 43-54.


IMANI KWA YESU

Leo, tunamwona Jemedari anamwomba Yesu kwa ajili ya uhai wa mtoto wake. Anaweka Imani kamili kabisa kwa Yesu. Anadhihirisha Imani yake kwa Yesu. Wakati Yesu alivyosema “waweza kwenda, mtoto wako yu mzima” bila hata kupoteza dakika moja huyu Jemedari anaondoka. Hili linaonesha Imani yake kamili kwa Yesu. Baada ya Yesu kusema mtoto wa huyu Jemedari alipona. Huyu jemedari anashuhudia muujiza. Anapokea kadiri ya Imani yake.

Kitu cha kuvutia cha kugundua katika Injili hii ni utofauti wa maneno ya Yesu. Kwanza kabisa, inaonekana kama Yesu amekasirika aliposema, “bila watu kuona ishara na miujiza, hamuamini”. Lakini mara moja anamponya kijana wa jemedari kwa kumwambia, “Mwanao atakuwa mzima”. Je, kwanini kuna utufatui katika maeneno haya ya Yesu na matendo yake? Yesu anatambua kwamba watu wengi wana Imani dhaifu. Antambua pia ishara na miujiza inasaidia watu wakati mwingine waweze kuamini. Lakini kilele cha malengo ya Yesu haikuwa kwa sababu ya kuponya mwili.

Leo hii dunia imetawaliwa na ugonjwa wa kimwili, kisaikologia na kiroho. Watu wanaenda kutoka sehemu moja hadi nyingine kwenda kutafuta msaada. Lakini je, tunaenda kwa Yesu yeye ambaye ni mponyaji wa Kimungu, ambaye haponyi tu mwili bali roho pia? Je, tuna Imani kama huyu jemedari?

Sala: Bwana, tafadhali ongeza Imani yangu. Ninakuomba nikuone wewe ukitenda katika maisha yangu, na nisaidie niweze kutambua upendo wako mkamilifu kwa kila kitu. Ninapo kuona wewe ukitenda katika maisha yangu, nisaidie niweze kuutambua kwa hakika kabisa, upendo wakomkamilifu. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JUMATATU, MACHI 16, 2026



MASOMO YA MISA, JUMATATU, MACHI 16, 2026
JUMA LA 4 LA KWARESIMA


SOMO 1
Isa. 65:17-21

Bwana asema: Tazama, mimi naumba mbingu mpya na nchi mpya, na mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni. Lakini furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo; maana, tazama, naumba Yerusalemu uwe shangwe, na watu wake wawe furaha.

Nami nitaufurahia Yerusalemu, nitawaonea shangwe watu wangu; sauti ya kulia haitasikiwa ndani yake tena, wala sauti ya kuomboleza. Hatakuwapo tena mtoto wa siku chache, wala mzee asiyetimia siku zake; kwa maana mtoto atakufa mwenye umri wa miaka mia; bali mtenda dhambi mwenye umri wa miaka mia atalaaniwa. Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 30:1, 3-5, 10-12 (K) 1

(K) Nitakutukuza, ee Bwana, kwa maana umeniinua.

Ee Bwana, nitakutukuza kwa maana umeniinua,
Wala hukuwafurahisha adui zangu juu yangu.
Umeniinua nafsi yangu,
Ee Bwana, kutoka kuzimu.
Umenihuisha na kunitoa
Miongoni mwao washukao shimoni. (K)

Mwimbieni Bwana zaburi,
Enyi watauwa wake.
Na kufanya shukrani.
Kwa kumbukumbu la utakatifu wake.
Maana ghadhabu zake ni za kitambo kidogo,
Katika radhi yake mna uhai.
Huenda kilio huja kukaa usiku,
Lakini asubuhi huwa furaha. (K)

Ee Bwana, usikie, unirehemu,
Bwana, uwe msaidizi wangu.
Uligeuza matanga yangu kuwa machezo;
Ulinivua gunia, ukanivika furaha.
Ee Bwana, mungu wangu,
Nitakushukuru milele. (K)



SHANGILIO
Eze. 33:11

Sikufurahii kufa kwake mtu mwovu, 
asema Bwana, bali aiache njia yake mbaya, akaishi.



INJILI
Yn. 4:43-54

Baada ya siku mbili hizo Yesu aliondoka huko, akaenda Galilaya. Kwa maana Yesu mwenyewe alishuhudia ya kwamba nabii hapati heshima katika nchi yake mwenyewe. Basi alipofika Galilaya, Wagalilaya walimpokea; kwa kuwa wameyaona mambo yote aliyoyatenda huko Yerusalemu wakati wa sikukuu; maana hao nao waliiendea sikukuu.

Basi alifika tena Kana ya Galilaya, hapo alipoyafanya yale maji kuwa divai. Na palikuwa na diwani mmoja ambaye mwanawe hawezi huko Kapernaumu. Huyo aliposikia ya kwamba Yesu amekuja kutoka Uyahudi mpaka Galilaya, alimwendea, akamsihi ashuke na kumponya mwanawe; kwa maana alikuwa kufani. Basi Yesu akamwambia, Msipoona ishara na maajabu hamtaamini kabisa? Yule diwani akamwambia, Bwana, ushuke asijakufa mtoto wangu. Yesu akamwambia, Enenda; mwanao yu hai. Mtu yule akalisadiki lile neno aliloambiwa na Yesu, naye akashika njia. Hata alipokuwa akishuka, watumwa wake walimlaki, wakisema ya kwamba mtoto wake yu hai. Basi akawauliza habari ya saa alipoanza kuwa hajambo; nao wakamwambia, jana, saa saba, homa ilimwacha. Basi babaye akafahamu ya kuwa ni saa ile ile alipoambiwa na Yesu, Mwanao yu hai. Akaamini yeye na wote wa nyumbani mwake.

Hiyo ni ishara ya pili aliyoifanya Yesu, alipokuwa ametoka Uyahudi kufika Galilaya.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

--KUPONYWA KWA UPOFU--

 


“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Jumapili, Machi 15, 2026.
Dominika ya 4 ya Kwaresima

1Sam 16: 1, 6-7,10-13;
Zab 23: 1-6;
Ef 5: 8-14;
Yn 9: 1-41.


KUPONYWA KWA UPOFU


Kulikuwa na kijana mmoja alyezaliza kipofu katika kijiji kimoja. Kila siku jioni alikuwa akichukua taa ili kuvuka msitu mmoja wenye giza kuelekea nyumbani kwake. Mtu mmoja mpita njia alikutana na huyu kipofu akamuuliza swali “je, wewe si kipofu; sasa inakuwaje umebeba taa?’ Yule kipofu akajibu akasema hii taa ni kwa ajili yenu ili msije mkagongana na mimi.

Katika maisha, macho yenye afya hayawezi kuona yote. Tunaweza kuona vitu vingine tunapokuwa na wengine. Elimu ya kisayansi ambayo inaweza kutusaidia kuchunguza na kujaribu yale yote yanayo shikika, na kutufanya tuwe na hali ya kutaka kujua zaidi, kufurahia na kuamini yote yanayo onekana kwa macho, kugundulika kwa kutumia milango ya fahamu, na kuangalia na vyombo vya maabara na kusema ni kweli. Kuna upofu mwingine pia ambao umejikita katika mizani ya ulimwengu,: pesa, mafanikio, kazi, mapenzi, afya na ugonjwa, ujana na uzee n.k. lakini uwezo wa kuamini kuona vizuri unafunga ndani na macho ya kiroho yanayo tusaidia kuzama katika mafumbo ya Mungu, maana ya maisha na kifo, na kilele cha historia ya mwanandamu.

“Mwanga wa kweli unao mwangaza kila mtu umekuja ulimwenguni” (Yn 1:9). Yesu alikuja kufukuza giza letu, kuangaza usiku wetu, kukaa katika “watoto wa mwanga na watoto wa mchana” (1 Thes 5:5). Tunaitwa kuangalia katika upofu wetu wa roho. Tunaitwa kuushinda kwa kufungua macho yetu ya kiroho.

Katika somo la kwanza tunamwona Mfalme Sauli anashindwa kumtii Mungu. Anakiuka amri za Mungu, Sauli alimhifadhi Mfalme wa Ameleki na kujipatia vingi kwasababu ya vita. Ndipo Mungu akamkataa Sauli akamtuma Samueli kwenda katika mji wa Bethlehemu kumchagua Mfalme atakaye muonesha. Samueli anaenda katika nyumba ya Yese na baada ya kumuona mtoto wa kwanza wa Yese ambaye alikuwa na nguvu, mzuri, na mrefu. Samueli alidhani huyu ndiye aliyechaguliwa na Bwana, na hapo anasikia sauti kwamba “Mungu haangalii kama Mwanadamu anavyo angalia; mwanadamu hutazama sura ya nje bali Mungu huangalia unyofu wa moyo”. Samueli anaoneshwa Daudi na anamchagua, akiwa ni mtoto wa mwisho wa Yese ambaye alikuwa akichunga kondoo. Wanadamu wana mambo mengi katika akili, ambayo hayawa saidii kufikia hitimisho.

“Upofu” ni kushindwa kuona mkono wa Mungu ukifanya kazi kati yetu. Tunakazana kutafuta miujiza ya Neema za Mungu zinazo onekana kwetu na kwa wengine. Kwahiyo kitu cha kwanza kabisa ambacho tunapaswa kufanya ndicho ambacho tunapata katika Injili ni kutambua upofu wetu. Ni lazima tukazane na kukubali kwamba tumeshindwa kumuona Mungu akiwa kazini akitenda kazi. Kukazana huku kutatusaidia kutambua na kutamani uponyaji wa kiroho. Kitu kizuri ni kwamba Yesu alimponya huyu mtu na kwamba atatuponya sisi pia. Kurudisha hali ya kuona ni rahisi sana kwa Yesu. Kwahiyo sala ya kwanza kabisa ambayo tunapaswa kuisali kutokana na ujumbe huu wa Injili “Bwana naomba niweze kuona” unyenyekevu wa kukiri upofu wetu utatusaidia Mungu aje kutenda kazi kwetu. Na kama hatutakiri kwa unyenyekevu upofu wetu, hatutakuwa katika nafasi ya kuomba uponyaji.

Alifanyaza tope kwa mate yake na kumpaka huyu kijana katika macho, kitendo hiki kina onesha kuwa ni ajabu. Lakini inaonesha kwamba Yesu anaweza kutumia kitu ambacho hatudhani kwa ajili ya kazi yake ya Kimungu. Ni mara nyingi tuna angalia kazi za Mungu katika hali ya juu kabisa. Lakini ni mara nyingi yupo nasi katika yale ya kawaida. Pengine tunaweza kushawishika kufikiri kwamba Mungu anafanya matendo yake kwa njia ya upendo au sadaka. Pengine tunaweza kushawishika kudhani kwamba Mungu hawezi kutumia mambo yetu ya kawaida kutenda miujiza yake. Lakini hili si kweli. Ni hakika kabisa maisha ya kawaida na vitu vya kawaida kabisa katika maisha ndipo Mungu alipo. Kwa hakika, kazi inapokuwa ya kwaida ndipo tukazane zaidi kuona Mungu akitenda kazi. Na tutakapo “muona” yeye akiwa katika mambo ya kawaida ya maisha, tunakuwa tumeponywa na upofu wetu wa roho.
               
Sala: Bwana, ninaomba nione. Nisaidie mimi niponywe na upofu wangu. Nisaidie mimi niweze kukuona katika kila kazi ya maisha yangu. Ninaomba unisaidie niweze kukuona katika matukio madogo ya kila siku katika maisha. Na ninapo kuona wewe ukiwa ndani, jaza Moyo wangu kwa shukrani kwa kuona huku. Yesu, nakuamini Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MACHI 15, 2026


MASOMO YA MISA, MACHI 15, 2026
DOMINIKA YA 4 YA KWARESIMA


MWANZO
Isa. 66:10 – 11

Furahi, Jerusalemu, mshangilieni ninyi nyote mmpendao; furahini, ninyi nyote mliao kwa ajili yake, mpate kunyonya, na kushibishwa kwa maziwa ya faraja zake.



SOMO 1
1Sam. 16:1, 6-7, 10-13

Bwana akamwambia Samweli, Ijaze pembe yako mafuta, uende, nami nitakupeleka kwa Yese, Mbethlehemi; maana nimejipatia mfalme katika wanawe.

Ikawa walipokuja, Samweli alimtazama Eliabu, akasema, Yakini masihi wa Bwana yupo hapa mbele zake. Lakini Bwana akamwambia Samweli, Usimtazame uso wake, wala urefu wa kimo chake; kwa maana mimi nimemkataa. Bwana haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali Bwana huutazama moyo.

Yese akawapitisha wanawe saba mbele ya Samweli, Samweli akamwambia Yese, Bwana hakuwachagua hawa. Kisha Samweli akamwambia Yese, Watoto wako wote wapo hapa? Naye akasema, Amesalia mdogo wao, na tazama, anawachunga kondoo. Basi Samweli akamwambia Yese, Tuma watu, wamlete; kwa sababu hatutaketi hata atakapokuja huku. Basi akatuma mtu, naye akamleta kwao. Naye alikuwa mwekundu, mwenye macho mazuri, na umbu lake lilikuwa la kupendeza. Bwana akasema, Ondoka, umtie mafuta; maana huyu ndiye.

Ndipo Samweli akaitwaa pembe yenye mafuta, akamtia mafuta kati ya ndugu zake; na roho ya Bwana ikamjilia Daudi kwa nguvu tangu siku ile.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
ZAB. 23 (K) 1

(K) Bwana ndiye mchungaji wangu, Sitapungukiwa na kitu.

Bwana ndiye mchungaji wangu,
Sitapungukiwa na kitu.
Katika malisho ya majani mabichi hunilaza,
Kando ya maji ya utulivu huniongoza. (K)

Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza
Katika njia za haki kwa ajili ya jina lake.
Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti,
Sitaogopa mabaya;
Kwa maana Wewe upo pamoja nami,
Gongo lako na fimbo yako vyanifariji. (K)

Waandaa meza mbele yangu,
Machoni pa watesi wangu.
Umenipaka mafuta kichwani pangu,
Na kikombe changu kinafurika. (K)

Hakika wema na fadhili zitanifuata
Siku zote za maisha yangu;
Nami nitakaa nyumbani mwa Bwana milele. (K)



SOMO 2
Efe. 5:8 – 14

Zamani ninyi mlikuwa giza, bali sasa mmekuwa nuru katika Bwana; enendeni kama watoto wa nuru; Kwa kuwa tunda la nuru ni katika wema wote na haki na kweli; mkihakiki ni nini impendezayo Bwana. Wala msishirikiane na matendo yasiyozaa ya giza, bali myakemee; kwa kuwa yanayotendeka kwao kwa siri, ni aibu hata kuyanena. Lakini yote yaliyokemewa hudhihirishwa na nuru; maana kila kilichodhihirika ni nuru. Hivyo husema, Amka wewe usinziaye, Ufufuke katika wafu, Na Kristo atakuangaza.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



SHANGILIO
Yn. 8:12

Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, asema Bwana, yeye anifuataye atakuwa na nuru ya uzima.



INJILI
Yn. 9:1 – 41

Yesu alipokuwa akipita alimwona mtu, kipofu tangu kuzaliwa. Wanafunzi wake wakamwuliza wakisema, Rabi, ni yupi aliyetenda dhambi, mtu huyu au wazazi wake, hata azaliwe kipofu? Yesu akajibu, Huyu hakutenda dhambi, wala wazazi wake; bali kazi za Mungu zidhihirishwe ndani yake. Imetupasa kuzifanya kazi zake yeye aliyenipeleka maadamu ni mchana; usiku waja asipoweza mtu kufanya kazi. Muda nilipo ulimwenguni, mimi ni nuru ya ulimwengu.

Alipokwisha kusema hayo alitema mate chini, akafanya tope kwa yale mate. Akampaka kipofu tope za macho, akamwambia, Nenda kanawe katika birika ya Siloamu, (maana yake, Aliyetumwa). Basi akaenda na kunawa; akarudi anaona.

Basi jirani zake, na wale waliomwona zamani kuwa ni mwombaji, wakasema, Je! Huyu siye yule aliyekuwa akiketi na kuomba  wengine wakasema, Ndiye. Wengine wakasema, La; lakini amefanana naye. Yeye mwenyewe alisema, Mimi ndiye.

Basi wakamwambia, Macho yako yalifumbuliwaje? Yeye akajibu, Mtu yule aitwaye Yesu alifanya tope, akanipaka macho akaniambia, Nenda Siloamu ukanawe; basi nikaenda na kunawa, naikapata kuona. Wakamwambia Yuko wapi huyo? Akasema, Mimi sijui.

Basi wakampeleka kwa Mafarisayo yule aliyekuwa kipofu zamani. Nayo ilikuwa sabato, hapo Yesu alipofanya zile tope na kumfumbua macho. Basi Mafarisayo nao wakawmuliza tena jinasi gani alivyopata kuona. Akawaambia, Alinitia tope juu ya macho, nami nikanawa, na sasa naona. Basi baadhi ya Mafarisayo wakasema, Mtu huyo hakutoka kwa Mungu, kwa sababu haishiki sabato. Wengine wakasema, Awezaje mtu mwenye dhambi kufanya ishara kama hizo? Kukawa matengano kati yao. Basi wakamwambia yule kipofu mara ya pili, Wewe wasemaje katika habari zake kwa vile alivyokufumbua macho? Akasema, Ni nabii.

Basi Wayahudi hawakusadiki habari zake, ya kuwa alikuwa kipofu, kisha akapata kuona; hata walipowaita wazazi wake yule aliyepata kuona. Wakawauliza wakisema, Huyu ndiye mwana wenu, ambaye mnasema kwamba alizaliwa kipofu? Amepataje, basi, kuona sasa? Wazazi wake wakawajibu, wakasema, Tunajua ya kuwa huyu ndiye mwana wetu, tena ya kuwa alizaliwa kipofu; lakini jinsi aonavyo sasa hatujui; wala hatujui ni nani aliyemfumbua macho. Mwulizeni yeye mwenyewe; yeye ni mtu mzima; atajisemea mwenyewe. Wazazi wake waliyasema hayo kwa sababu waliwaogopa Wayahudi; kwa maana Wayaahudi walikuwa wamekwisha kuafikiana kwamba mtu akimkiri kuwa ni Kristo, atatengwa na sinagogi. Ndiyo sababu wale wazazi wake walisema, Ni mtu mzima, mwulizeni yeye.

Basi mara ya pili wakamwita yule mtu aliyekuwa kipofu, wakamwambia, Mpe Mungu utukufu. Sisi tunajua ya kuwa mtu huyo ni mwenye dhambi. Basi yule mtu akajibu, Kwamba yeye ni mwenye dhambi sijui. Najua neno moja, kuwa mimi nilikuwa kipofu na sasa naona. Basi wakamwambia, Alitutendea nini? Alikufumbua macho jinsi gani? Akawajibu, Nimekwisha kuwaambia, wala hamkusikia; mbona mnataka kusikia tena? Ninyi nanyi mnataka kuwa wanafunzi wake? Basi wakamshutumu, wakasema, Wewe u mwanafunzi wake yule; sisi tu wanafunzi wa Musa. Sisi tunajua ya kuwa Mungu alisema na Musa; bali yule hatujui atokako. Yule mtu akajibu, akawaambia, Hili ni ajabu! Kwamba ninyi hamjui atokako, naye alinifumbua macho! Twajua ya kuwa Mungu hawasikii wenye dhambi; bali mtu akiwa mcha Mungu, na kuyafanya mapenzi yake; humsikia huyo. Tokea hapo haijasikiwa ya kuwa mtu ameyafumbua macho ya kipofu, ambaye alizaliwa hali hiyo. Kama huyo asingalitoka kwa Mungu, asingeweza kutenda neno lolote.

Wakajibu, wakamwambia, Ama! Wewe ulizaliwa katika dhambi tupu, nawe unatufundisha sisi? Wakamtoa nje. Yesu akasikia kwamba wamemtoa nje; naye alipomwona alisema, Wewe wamwamini Mwana wa Mungu? Naye akajibu akasema, Ni nani, Bwana, nipate kumwamini? Yesu akamwambia, Umemwona, naye anayesema nawe ndiye. Akasema, Naamini, Bwana. Akamsujudia.

Yesu akasema, Mimi nimekuja ulimwenguni humu kwa hukumu, ili wao wasioona waone, nao wanaoona wawe vipofu. Baadhi ya Mafarisayo waliokuwapo pamoja naye wakasikia hayo, wakamwambia, Je! Sisi nasi tu vipofu? Yesu akamwambia, Kama mngekuwa vipofu, msingekuwa na dhambi; lakini sasa mwasema, Twaona; basi dhambi yenu inakaa.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo

Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.