Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MCHANGO WANGU KATIKA UTUME WA BWANA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Ijumaa, Septemba 20, 2026 
Juma la 24 la Mwaka


1 Kor 15: 12-20
Zab 16: 1, 6-8, 15
Lk 8: 1-3


MCHANGO WANGU KATIKA UTUME WA BWANA!

Luka anatuambia kuhusu kazi kubwa waliofanya idadi kubwa ya wanawake katika kutegemeza utume wa Bwana wetu na Wafuasi. Pamoja na tofauti zao kati ya wanawake, lakini inaonekana wote walikuwa na kitu cha pamoja kwamba: Yesu amewaponya kimiujiza kwasababu ambayo hakuna jibu sahihi kutoka kwa Mwanadamu. Katika hali ya kufikirika, kundi lililo fuatana na Yesu lilitoa ushahidi na kumtambulisha Yesu kama Kristo Masiha. Wanawake hawa hawakuwa watu wasiojitambua waliofuata tu, walikuwa watu waliokuwa hai katika kutangaza Injili ya Ufalme wa Mungu. Wakati Yesu alivyo watuma wale kumi na wawili (Lk 9: 1-6) na wale sabini na mbili (Lk 10: 1-12). Aliwaambia wasichukue chochote. Hii ni kwasababu walikuwa wafanye utume kwa wale waliowafuata, ambao kati yao waliishi miongoni mwao. Tunapaswa tuwe tunafanya walichofanya wanawake hawa. Walimpenda Yesu sana, walimtumikia yeye na wafuasi wake kwa vile walivyokuwa navyo. 

Je unadhani Yesu alihitaji msaada wao? Hapana. je, alihitaji chakula chao? Hapana. Kama Yesu angependa angeweza kuchukua tu kipande cha mkate katika mkoba, na pale watakapo hisi njaa yeye na wafuasi wake Yesu angeiongeza hata kuwa kikapu kilicho jaa. Kwanini hakufanya hivyo? Hii ni kwasababu kama kuna kitu anachopenda Yesu zaidi kuliko kuwalisha watu, ni wakati watu wanampa yeye kwasababu wanampenda. Hahitaji yote hayo, bali anapenda kupokea. Inampa furaha kubwa tukimpenda. Yesu hajapungukiwa chochote, tukimpenda na kumtumikia ni faida kwetu sisi kwamba tunampendeza Bwana, nasi tunajipatia Baraka kwa ajili ya roho zetu. Tunajua kwamba sala zetu hazi muongezei Mungu kitu, ila za faa kwa ajili ya wokovu wetu. Tumtumikie Mungu kwa uchaji katika wema na kweli ili tujipatie utakatifu wa roho zetu.

Sala: Bwana, nijalie moyo wa ukarimu. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA IJUMAA, SEPTEMBA 18, 2026





MASOMO YA MISA 
IJUMAA, SEPTEMBA 18, 2026
JUMA LA 24 LA MWAKA


SOMO 1
1Kor. 15:12 – 20

Ikiwa Kristo anahubiriwa ya kwamba amefufuka katika wafu, mbona baadhi yenu husema kwamba hakuna kiyama ya wafu? Lakini kama hakuna kiyama ya wafu, Kristo naye hakufufuka; tena kama Kristo hakufufuka, basi, kuhubiri kwenu ni bure na Imani yetu ni bure. Naam, na sisi tumeonekana kuwa mashahidi wa uongo wa Mungu; kwa maana tulimshuhudia Mungu ya kuwa alimfufua Kristo, ambaye hakumfufua, ikiwa wafu hawafufuliwi. Maana kama wafu hawafufuliwi, Kristo naye hakufufuka. Na kama Kristo hakufufuka, Imani yenu ni bure; mngalimo katika dhambi zenu. Na hapo wao nao waliolala katika Kristo wamepotea. Kama katika maisha haya tu tumemtumaini Kristo, sisi tu maskini kuliko watu wote. Lakini sasa Kristo amefufuka katika wafu, limbuko lao waliolala.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 17:1, 6 – 8, 15

(K) Nishibishwe, Ee Bwana, kwa sura yako.

Ee Bwana, usikie haki, ukisikilize kilio changu, 
Utege sikio lako kwa maombi yangu,
Yasiyotoka katika midomo ya hila. (K)

Ee Mungu, nimekuita kwa maana utaitika,
Utege sikio lako ulisikie neno langu.
Dhihirisha fadhili zako za ajabu,
Wewe uwaokoaye wanaokukimbilia;
Kwa mkono wako wa kuume
Uwaokoe nao wanaowaondokea. (K)

Unilinde kama mboni ya jicho,
Unifiche chini ya uvuli wa mbawa zako;
Bali mimi nikutazame uso wako katika haki,
Niamkapo nishibishwe kwa sura yako. (K)


SHANGILIO
Efe. 1:17, 18

Aleluya, aleluya,
Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, 
awape roho ya hekima mjue tumaini la mwito wake.
Aleluya.


INJILI
Lk. 8:1–3

Yesu alikuwa akizunguka-zunguka katika miji na vijiji akihubiri na kuitangaza habari njema ya ufalme wa Mungu; na wale Thenashara walikuwa pamoja naye, na wanawake kadha wa kadha ambao walikuwa na pepo wabaya na magonjwa wakaponywa; nao ni Mariamu aitwaye Magdalene aliyetokwa na pepo saba, na Yohana mkewe Kuza, wakili wake Herode, na Susana, na wengine wengi, waliokuwa wakimhudumia kwa mali zao.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUOMBA HURUMA



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Alhamisi, Septemba 17, 2026,
Juma la 24 la Mwaka

1Kor 15:1-11
Zab 117: 1-2, 15-17, 28;
Lk7: 36-50.

KUOMBA HURUMA

Karibuni sana ndugu zangu wapendwa kwa adhimisho la Misa Takatifu tena asubuhi ya leo. Bado tunaendelea kuongozwa na tafakari ya neno la Mungu toka katika kitabu cha waraka wa kwanza wa mtume Paulo kwa Wakorintho. Na bado anaendelea kujibu maswali na changamoto zilizoikumba ile jumuiya. Na leo anazungumzia changamoto juu ya suala la ufufuko. Wakristo wa Korintho waliishi kati ya wanafalsafa waliowakejeli juu ya suala la ufufuko baada ya wafu. Walikuwako wanafalsafa kama akina Epicureans waliosisitizia juu ya kuponda mali na anasa. Wakati huu falsafa hii ilikuwa imeshika kasi sana na hawakuamini ufufuko.

Wakristo walimtegemea Kristo aje kwa haraka ili basi awafufue wale wakristo waliokuwa wakifariki kabla ya Kristo kuja ili basi wale wanafalsafa wapate kuoneshwa kwamba walichokifundisha sio sahihi. Lakini basi Yesu hakufika kwa haraka vile walivyokuwa wakihisi na hivyo basi wakauliza je, kwa nini? Wanafalsafa hawa waliwakejeli sana wakristo na imani yao juu ya ufufuko kwa kuwaambia kwamba ni uzushi.

Lakini basi Paulo anajibu suala hili na kwa kuanza kusema kwamba kwanza suala la ufufuko ni la kweli kabisa na si la uzushi kama wanafalsafa hawa wanavyodai. Anaanza hoja yake kwa kumtaja Yesu-yeye alishuhudiwa na watu tena kati yetu akifa msalabani kabisa, akafa na akazikwa-lakini pia alishuhudiwa na baadhi yetu akiwa amefufuka tena ikiwapo mimi-sasa anawauliza-ninyi mnasemaje kuhusu hili? Ni uzushi tena? Anawaambia jamani bakini katika imani yenu-msidanganywe na hawa watu; mtumaini Kristo.

Ndivyo inavyotokea na kwetu ndugu zangu. Bado tunadanganywa na falsafa mbalimbali na kuziungamia. Tumedanganywa na mitandao mbalimbali na kupotezea muda huko kana kwamba kila kitu kisemwacho nayo ni sahihi. Tunajisikia hofu kubwa pale tunaposafiri bila simu kuliko pale tusafiripo bila hata rozari mfukoni. Tunakuwa tayari kuacha rozari au hata biblia kuliko simu-lengo ni kwamba simu itatulinda, itatuburudisha kwa kutupatia habari mbalimbali za kwenye mitandao. Tuna hofu yakukosa habari kuliko kukosa kanisani.

Kwenye somo la kwanza tunakutana na Yesu akimpinga mfarisayo aliyepinga yeye kupakwa mafuta na mama mmoja. Haya ni matendo aliyoyashindwa yule mfarisayo lakini akayaweza yule mama. Yule mama alionesha heshima kwa Yesu kuliko huyu mfarisayo. Mfarisayo aliona wivu kana kwamba yule mama alikuwa akijipatia sifa zaidi kuliko yeye. Hata majibu yake anayomueleza Yesu chanzo chake ni wivu. Anataka Yesu asitendewe uzuri kwa sababu ya wivu wake. Hata na sisi tupo hivihivi ndugu zangu. Wengi wetu tuna wivu; hatutaki wengine watendewe wema na sisi hatuko tayari kuwatendea. Tukiona wengine wakiutenda tunakasirika, ati tunataka wasifaidi? Tukiona wengine wakitendewa wema yabidi tufurahi zaidi. Kama huwezi kuutenda wema, mwingine ataweza.
------------------------
Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 17, 2026



MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 17, 2026
ALHAMISI, JUMA LA 24 LA MWAKA


SOMO 1
1Kor. 15:1 – 11

Ndugu zangu, nawaarifu ile injili niliyowahubiri; ambayo ndiyo mliyoipokea, na katika hiyo mnasimama, na kwa hiyo mnaokolewa; ikiwa mnayashika sana maneno niliyowahubiri; isipokuwa mliamini bure. Kwa maana naliwatolea ninyi hapo mwanzao yale niliyoyapokea mimi mwenyewe, ya kuwa Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu, kama yanenavyo maandiko; nay a kuwa alizikwa; nay a kuwa alifufuka siku ya tatu, kama yanenavyo maandiko; nay a kuwa alimtokea Kefa; tena na wale Thenashara; baadaye aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano pamoja; katika hao wengi wanaishi hata sasa, ila baadhi yao wamelala; baadaye akamtokea Yakobo; tena na mitume wote; na mwisho wa watu wote, alinitokea mimi, kama ni mtu aliyezaliwa si kwa wakati wake. Maana mimi ni mdogo katika mitume, nisiyestahili kuitwa mtume, kwa sababu naliliudhi kanisa la Mungu. Lakini kwa neema ya Mungu nimekuwa hivi nilivyo; na neema yake iliyo kwangu ilikuwa si bure, bali nalizidi sana kufanya kazi kupita wao wote; wala si mimi, bali ni neema ya Mungu pamoja nami. Basi, kama ni mimi, kama ni wale, ndivyo tuhubirivyo, na ndivyo mlivyoamini.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 118:1 – 2, 15 – 17, 28

(K) Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema.

Aleluya.
Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema,
Kwa maana fadhili zake ni za milele.
Israeli na aseme sasa,
Ya kwamba fadhili zake ni za milele. (K)

Mkono wa kuume wa Bwana umetukuzwa;
Mkono wa kuume wa Bwana hutenda makuu.
Sitakufa bali nitaishi,
Nami nitayasimulia matendo ya Bwana. (K)

Ndiwe Mungu wangu, nami nitakushukuru,
Ndiwe Mungu wangu, nami nitakutukuza. (K)


SHANGILIO
Kol. 3:16, 17

Aleluya, aleluya,
Neno la Kristo likae kwa wingi ndani yenu katika hekima yote, Mkimshukuru Mungu Baba kwa Yeye.
Aleluya.


INJILI
Lk. 7:36 – 50

Mtu mmoja katika Mafarisayo alimwalika Yesu ale chakula kwake; akaingia katika nyumba yake yule Farisayo, akaketi chakulani. Na tazama, mwanamke mmoja wa mji ule, aliyekuwa mwenye dhambi, alipopata habari ya kuwa ameketi chakulani katika nyumba ya yule Farisayo, alileta chupa ya marimari yenye marhamu. Akasimama nyuma karibu na miguu yake, akilia, akaanza kumdondoshea machozi yake, na kuipangusa kwa nywele za kichwa chake, akiibusu-busu miguu yake na kuipaka yale marhamu. Basi, yule Farisayo aliyemwalika alipoona vile, alisema moyoni mwake, Mtu huyu kama angekuwa nabii, angemtambua mwanamke huyu amgusaye, ni nani, naye ni wa namna gani, ya kwamba ni mwenye dhambi. Yesu akajibu akamwambia, Simoni, nina neno nitakalo kukuambia. Akasema, Mwalimu, nena. Akasema, Mtu mmoja mkopeshaji alikuwa na wadeni wawili; mmoja amwia dinari mia tano, na wa pili hamsini. Nao walipokuwa hawana cha kumlipa, aliwasamehe wote wawili. Katika hao wawili ni yupi atakayempenda zaidi? Simony akajibu akasema, Nadhani ni yule ambaye alimsamehe nyingi. Akamwambia, Umeamua haki. Akamgeukia yule mwanamke, akamwambia Simoni, Wamwona mwanamke huyu? Niliingia nyumbani kwako, hukunipa maji kwa miguu yangu; bali huyu amenidondoshea machozi miguu yangu; na hakuacha kunibusu sana miguu yangu. Hukunipa kichwa change mafuta; bali huyu amenipaka miguu yangu marhamu. Kwa ajili ya hayo nakuambia, Amesamehewa dhambi zake ambazo ni nyingi, kwa kuwa amependa sana; lakini asamehewaye kidogo, huyo hupenda kidogo. Kisha alimwambia mwanamke, Umesamehewa dhambi zako. Ndipo wale walioketi chakulani pamoja naye walianza kusema mioyoni mwao, Ni nani huyu hata asamehe dhambi? Akamwambia yule mwanamke, Imani yako imekuokoa, enenda zako kwa amani.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

KUFUNGUA MIOYO YETU KWA YESU



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatano, Septemba 16, 2026, 
Juma la 24 la Mwaka 

1 Kor 12:31 – 13:13; 
Zab 32: 2-5, 12, 22; 
Lk 7: 31-35.


KUFUNGUA MIOYO YETU KWA YESU

“Nitakifananisha na nini kizazi hiki?” Kama Yesu angeuliza swali hili hili leo katika kizazi hiki. Angetuweka wapi? Je sisi tutakuwa kama wale watoto ambao wakiwekewa muziki hawachezi hata kukiwa na maombolezo hawaombolezi? Somo la leo linatualika tuweze kuwa katika mstari mmoja na wito wa Mungu, tujitafakari wenyewe na kazi zetu ili tuweze kuwa kweli watoto wa Ufalme wa Mungu. 

Paulo katika Barua yake anatuelekeza juu ya “ni kwa jinsi gani tunapaswa kuwa katika nyumba ya Mungu”. Anawakumbusha waumini kwamba wao ni watu katika nyumba ya Mungu aliye hai, iliyodhihirishwa na Yesu, na kutangazwa na ulimwengu. Anaonesha aina Fulani ya kanuni ya Imani ambayo ilikuwa ni ishara ya Wakristo wa Mwanzo.  Kanuni hii inaonesha aina Fulani ya sifa za Yesu na matendo yake na mpango wa Mungu kwa mwanadamu kwa njia ya Yesu. 

Katika somo la Injili, Mafarisayo wanajiona wenyewe kuwa wema wanafananishwa na wale watoto wasiopenda kufanya chochote. Kama ilivyo vigumu kwa mmoja kuingia nyumba ambayo mlango wake umefungwa na madirisha kufungwa. Yesu hakuweza kuingia katika mioyo ya Mafarisayo kwasababu wameifunga na wameamua kutokuamini. Yesu na Yohane Mbatizaji walikataliwa na Mafarisayo. Injili inamalizikia kwakusema maneno haya: “Aliye na masikio na asikie” yakitutaka tuwe wasikivu na kusikiliza sauti au wito wa Yesu.  

Watoto waliokaa sokoni inatoa picha ya watu ambao muda wote wapo na mambo yao, hawana muda wa kutafakari kuhusu nafsi yao.Wanajishughulisha na biashara zao, kuwa na simu muda wote, au kukesha kwenye komputa. Maisha yetu yamejazwa na uharibifu wa kila aina. Tunajishughulisha na mambo mengi na kusahau lile la muhimu. Hali hii inatufunga sisi na kushindwa kujitambua wenyewe. 
Tutafakari leo kama maisha yetu yamekuwa ya utulivu ya kutufanya tumtambue Yesu. Je, nimekuwa msikivu kwa nafsi yangu? Je, nipo tayari kumrushusu Mungu afanye kazi katika maisha yangu? Kama sio basi fanya jitihada ya kumfuata Yesu na kustahilishwa katika ufalme Mungu. 

Sala: Bwana, ninakuomba ufungue moyo wangu. Ninakuomba nisikie sauti yako ikiniita. Yesu, nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 16, 2026




MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 16, 2026
JUMATANO, JUMA LA 24 LA MWAKA


SOMO 1
1Kor. 12:31--13:13

Takeni sana karama zilizo kuu. Hata hivyo nawaonyesha njia iliyo bora. Nijaposema kwa lugha za wanadamu na za malaika, kama sina upendo, nimekuwa shaba iliayo na upatu uvumao. Tena nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, si kitu mimi. Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu.

Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu; upendo hautakabari; haujivuni; haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni uchungu; hauhesabu mabaya; haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli; huvumilia yote; huamini yote; hutumaini yote; hustahimili yote.

Upendo haupungui neno wakati wowote; bali ukiwapo unabii utabatilika; zikiwapo lugha, zitakoma, yakiwapo maarifua, yatabatilika. Kwa maana tunafahamu kwa sehemu; na tunafanya unabii kwa sehemu; lakini ijapo ile iliyo kamili, iliyo kwa sehemu itabatilika. Nilipokuwa mtoto mchanga, nalisema kama mtoto mchanga, nalifahamu kama mtoto mchanga, nalifikiri kama mtoto mchanga; tokea hapo nilipokuwa mtu mzima, nimeyabatilisha mambo ya kitoto. Maana wakati wa sasa tunaona kwa kioo kwa jinsi ya fumbo; wakati ule tutaona uso kwa uso; wakati wa sasa nafahamu kwa sehemu; wakati wa sasa nafahamu kwa sehemu; wakati ule nitajua sana kama mimi nami ninavyojuliwa sana.

Basi, sasa inadumu imani, tumaini, upendo, haya matatu; na katika hayo lililo kuu ni upendo.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 33:2-5, 12, 22 (K) 12

(K) Heri taifa ambalo Bwana ni Mungu wao.

Mshukuruni Bwana kwa kinubi,
Kwa kinanda cha nyuzi kumi mwimbieni sifa.
Mwimbieni wimbo mpya,
Pigeni kwa ustadi kwa sauti ya shangwe. (K)

Kwa kuwa neno la Bwana lina adili,
Na kazi yake yote huitenda kwa uaminfu.
Huzipenda haki na hukumu,
Nchi imejaa fadhili za Bwana. (K)

Heri taifa ambalo Bwana ni Mungu wao,
Watu aliowachagua kuwa urithi wake.
Ee Bwana, fadhili zako zikae nasi,
Kama vile tulivyokungoja Wewe. (K)



SHANGILIO
Efe. 1:17, 18

Aleluya, aleluya,
Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, awape roho ya hekima mjue tumaini la mwito wake.
Aleluya.



INJILI
Lk. 7:31-35

Yesu aliwaambia makutano: Niwafananishe na nini watu wa kizazi hiki? Nao wamefanana na nini? Wamefanana na watoto walioketi sokoni na kuitana, wakisema, Tuliwapigia filimbi wala hamkucheza; tuliomboleza, wala hamkulia.

Kwa kuwa Yohane Mbatizaji alikuja, hali mkate wala hanywi divai, nanyi mwasema, Ana pepo. Mwana wa Adamu amekuja, anakula na kunywa; nanyi mwasema, Tazama, mlafi huyu, na mnywaji wa divai, rafiki wao watoza ushuru na wenye dhambi. Na hekima imejulikana huwa ina haki kwa watoto wake wote.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

KUTESEKA KWA AMANI NA FURAHA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Jumanne, Septemba 15, 2026 
Juma la 24 la Mwaka


Kumbukumbu ya Bikira Maria Mtakatifu wa Mateso

Ebr 5: 7-9; au 1Kor 15:1-11
Zab 30: 2-6, 15-16, 20; 
Yn 19: 25-27, 35 au Lk 2: 33-35


KUTESEKA KWA AMANI NA FURAHA!


Leo tunakumbuka mateso ya Mama yetu Bikira Maria. Mateso ya Maria yalikuwa ya ndani. Bikira Maria alikuwa mwanadamu kamili kwasababu hakutenda dhambi na kati ya watu waliompendeza Mungu katika hali ya ukamilifu wote ni Bikira Maria licha ya Mwanae, lakini kwa ajili ya hili hatuwezi kusema hakuwa na hisia ya kuhisi mambo ya duniani. Kwasababu ya ukamilifu wake, alipenda kwa mapendo ya ndani kuliko sisi. Kwasababu ya upendo huu, alihisi uchungu wa kumpoteza mwanae kuliko sisi. Mateso ya Maria tofauti na yetu yalikuwa kamili. Mateso yetu mara nyingi yamechanganyika na udhaifu wetu. Maria hakuhuzunika kwasababu atamkosa Mwanae ampe msaada. Aliteseka kwasababu aliona mateso ya yule anaye mpenda, na akahisi mateso yale kama Mwanae alivyohisi. Tunaweza kuhisi pia ni kwa jinsi ghani Yesu alivyojisikia alivyomuona Mamaye katika huzuni. Ni hakika ilimsababishia mateso pia, lakini ilikuwa pia ni hali ya kuonesha ukaribu wao. Ulimwengu mzima unaweza kuwa umekuwa wa ukatili na hali zote, lakini uso wa Mama yake ulikuwa ni sehemu pekee alioweza kuelekezea macho yake, akiona sura na mfano aliouweka wakati anatuumba sisi.

Huzuni ya mama haikuwa ni huzuni bila matumaini. Alijua kwa matumani fulani kwamba Mwanae atafufuka kutoka wafu. Tumaini lake halikumzuia kuhisi uchungu na wala halikumzuia kutazamia ufufuko wake. Maria ni Mama yetu. Kama ilivyo kwa Mama mwema, anatufundisha sisi. Tunapaswa tutuoe muda wetu tukiwa naye katika mti wa Msalaba, tukimuomba atufundishe jinsi ya kuhisi nasi mateso yetu katika maisha. Tusisite kumkimbilia atuombee tunapokumbana na adha na mateso katika maisha, yeye awe faraja na msaada wetu kwani atakuwa nasi, akisimama nasi na kuteseka nasi, akiyaweka yote chini ya Msalaba wa Mwanae kwa niaba yetu.


Sala: Mama wa Upendo, Mama wa Mateso na Mama wa huruma, utuombee sisi. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA JUMANNE, SEPTEMBA 15, 2026


MASOMO YA MISA 
JUMANNE, SEPTEMBA 15, 2026
JUMA LA 24 LA MWAKA


KUMBUKUMBU YA BIKIRA MARIA MTAKATIFU WA MATESO


SOMO 1
Ebr. 5:7 – 9

Kristo, siku hizo za mwili wake, alimtolea yule, awezaye kumwokoa na kumtoa katika mauti, maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi, akasikilizwa wa jinsi alivyokuwa mcha Mungu; na, ingawa ni Mwana, alijifunza kutii kwa mates ohayo yaliyompata; naye alipokwisha kukamilishwa, akawa sababu ya wokovu wa milele kwa watu wote wanaomtii.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 31:1 – 5, 14 – 15, 19 (K) 16

(K) Uniokoe, Ee Bwana, kwa ajili ya fadhili yako.

Nimekukimbilia Wewe, Bwana,
Nisiaibike mbele kwa haki yako uniponye.
Unitegee sikio lako, uniokoe hima. (K)

Uwe kwangu mwamba wa nguvu,
Nyumba yenye maboma ya kuniokoa,
Ndiwe genge langu na ngome yangu,
Kwa ajili ya jina lako uniongoze, unichunge. (K)

Utanitoa katika wavu walionitegea kwa siri,
Maana wewe ndiwe ngome yangu.
Mikononi mwako naiweka roho yangu,
Umenikomboa, Ee Bwana, Mungu wa kweli. (K)

Lakini mimi nakutumaini Wewe, Bwana,
Nimesema, Wewe ndiwe Mungu wangu.
Nyakati zangu zimo mikononi mwako;
Uniponye na adui zangu, nao wanaonifuatia. (K)

Jinsi zilivyo nyingi fadhili zako
Ulizowawekea wakuchao;
Ulizowatendea wakukimbiliao
Mbele ya wanadamu! (K)


SHANGILIO

Aleluya, aleluya,
Bikira Maria anafurahi yeye ameshinda na kupata nishani ya ushahidi pasipo kufa, alipokuwa chini ya msalaba wa Bwana.
Aleluya.


INJILI
Yn. 19:25 – 27

Penye msalaba wake Yesu walikuwa wamesimama mamaye, na umbu la mamaye, Mariamu wa Klopa, na Mariamu Magdalene. Basi Yesu alipomwona mama yake, na yule mwanafunzi aliyempenda amesimama karibu, alimwambia mama yake, Mama, tazama, mwanao. Kisha akamwambia yule mwanafunzi, Tazama, mama yako. Na tangu saa ile mwanafunzi yule akamchukua nyumbani mwake.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Au

INJILI
Lk. 2:33 – 35

Babaye na mamaye wa Yesu walikuwa wakiyastaajabia hayo yaliyonenwa juu yake. Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa. Nawe mwenyewe, upanga ukaingia moyoni mwako, ili yafunuliwe mawazo ya mioyo mingi.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MSALABA WA KRISTO NI TUMAINI NA UKOMBOZI WETU!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatatu, Septemba 14, 2026, 
Juma la 24 la Mwaka wa Kanisa

Sikukuu ya Kutukuka kwa Msalaba Mtakatifu

Hes 21: 4-9 
Zab 77: 1-2, 34-38
Fil 2: 6-11
Yn 3: 13-17


MSALABA WA KRISTO NI TUMAINI NA UKOMBOZI WETU!


Msalaba ni ishara ya Mkristo. Kila Mkristo, mtoto na hata mtakatifu mkubwa kabisa, wanafanya ishara ya Msalaba, kutoa ushuhuda wa nguvu yake na umuhimu wake. Yesu alitoa maisha yake Msalabani na hapo akakomboa ubinadamu. Kwa njia hii hamna tena alama ya mateso na aibu, bali ukombozi. Msalaba ni njia ya kwenda kwenye utukufu, kwahiyo ni changamoto kwa kila Mkristo. Kama Mtakatifu Paulo anavyosema “Tunamuhubiri Yesu Msulubiwa, kwa Wayahudi ni kikwazo na kwa Wayunani ni upuuzi, bali kwao waitwao, Wayahudi kwa Wayunani ni Kristo, Nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu” (1 Kor 1: 23-24). 

Katika historia ya Ukristo Msalaba aliofia Kristo na kwa njia hii akafufuka, umekuwa ni ishara wazi ya nguvu ya Mungu ya kuokoa. Mababa wa Kanisa wanalinganisha Msalaba wa Yesu na mti wa uzima katika bustani ya dunia, safina ya Noah, na kuni alizobeba Isaka katika mlima Moriah, na ile ngazi ya Yakobo, na ile Fimbo ya Musa, na yule nyoka ya Shaba. Haya yote katika hali ya juu yana husishwa na fumbo la ukombozi. Katika Ubatizo kila Mkristo amesulubiwa na Kristo, kufa na kufufuka na Kristo. Mtakatifu Leo Mkuu anasema, “Msalaba ni chanzo cha kila Baraka, chanzo cha mafanikio yote: kwa waamini unawapa nguvu kutoka katika udhaifu wake, utukufu kutoka katika aibu yake, na uzima kutoka katika kifo”.

Tafakari leo, juu ya msalaba wa Yesu Kristo. Chukua muda Fulani ukiutazama na kutafakari. Na ona jibu katika msalaba huo juu ya shughuli zako za kila siku. Yesu yupo karibu na wale wanaoteseka, na nguvu yake ipo kwa wale wote wanao mwamini ndani yake.

Sala: Bwana, nisaidie mimi niweze kutazama msalaba wako. Nisaidie niweze kuonja ushindi wa mwisho wa mateso yako. Ninaomba nikusanywe na kuponywa ninapo kutazama wewe. Yesu nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 14, 2026



MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 14, 2026
JUMATATU, JUMA LA 24 LA MWAKA

SIKUKUU YA KUTUKUKA KWA MSALABA


SOMO 1
Hes. 21:4 – 9

Siku zile jangwani, watu walimnung’unikia Mungu, na Musa, mbona mmetupandisha huku kutoka nchi ya Misri, ili tufe jangwani? Maana hapana chakula, wala hapana maji, na roho zetu zinakinai chakula hiki dhaifu. Bwana akatuma nyoka za moto kati ya watu, wakawauma, watu wengi wakafa. Watu wakamwendea Musa, wakasema, tumefanya dambi kwa sababu tumemnung’unukia Mungu, na wewe, utuombee kwa Bwana, atuondolee nyoka hawa. Basi, Musa akawaombea watu. Bwana akawaambia Musa, Jifanyie nyoka ya shaba, ukaiweke juu ya mti, na itakuwa kila mtu aliyeumwa, aitazamapo, ataishi. Musa akafanya nyoka ya shaba, akaiweka juu ya mti, hata ikiwa nyoka amemwuma mtu, alipoitazama ile nyoka ya shaba, akaishi.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 78:1 – 2, 34 – 38 (K) 7

(K) Msiyasahau matendo ya Mungu.

Enyi watu wangu, sikilizeni sheria yangu,
Tegeni masikio kwa maneno ya kinywa changu.
Na nifunue kinywa changu kwa mithali,
Niyatamke mafumbo ya kale. (K)

Alipowaua ndipo walipokuwa wakimtafuta;
Wakarudi wakamtaka Mungu kwa bidii.
Wakakumbuka kuwa Mungu ni mwamba wao,
Na Mungu Aliye juu ni mkombozi wako. (K)

Lakini walimdanganya kwa vinywa vyao, 
Wakamwambia uongo kwa ndimi zao.
Kwa maana mioyo yao haikuwa thabiti kwake,
Wala hawakuwa waaminifu katika agano lake. (K)

Lakini Yeye, kwa kuwa anayo rehema,
Husamehe uovu wala haangamizi.
Mara nyingi huipishia mbali ghadhabu yake,
Wala haiwashi hasira yake yote. (K)


SOMO 2
Fil. 2:6 – 11

Yesu Kristo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama wanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Kwa hiyo tena Mung alimwadhimisha mno, akamkirimia jina lile lipitalo kila jina, ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa Yesu Kristo ni Bwana, kwa utukufu wa Mungu Baba.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


SHANGILIO

Aleluya, aleluya,
Ee Kristu tunakuabudu na kukutukuza, kwa kuwa umeikomboa dunia kwa msalaba wako.
Aleluya.


INJILI
Yn. 3:13 – 17

Yesu alimwambia Nikodemo: Hakuna mtu aliyepaa mbinguni, ila yeye aliyeshuka kutoka mbinguni, yaani, Mwana wa Adamu. Na kama vile Musa alivyomwinua yule nyoka jangwani, vivyo hivyo Mwana wa Adamu hana budi kuinuliwa; ili kila mtu aaminiye awe na uzima wa milele katika yeye. Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe wa pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com