Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

KATIKA KUVUA SAMAKI NA KUVUA WATU!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Alhamisi, Septemba, 3 2026, 
Juma la 22 la Mwaka wa Kanisa

1Kor 3: 18-23; 
Zab 23: 1-6; 
Lk 5: 1-11

KATIKA KUVUA SAMAKI NA KUVUA WATU! 

Katika Injili, tunamuona Petro na wenzake walikuwa na bahati mbaya kwamba hawakupata samaki usiku uliopita. Yesu anamwambia tena Petro achukue jarife baharini kwa mara nyingine na atupe nyavu ili kuvua samaki. Petro anajibu kwamba “tumefanya kazi ya kuchosa usiku kucha tusipate kitu, lakini kwa neno lako nitazishusha nyavu kwa mara nyingine”. Kiasi cha samaki wengi waliovua kiliwashangaza sana. Ilimshtua Petro, alihisi uwepo wa utukufu wa Mungu. Alianguka magotini pa Yesu kwa kujitambua kutoka ndani kutostahiili kwake, “ondoka kwangu” alisema, “kwakuwa mimi ni mtu mwenye dhambi”. Kumbukumbu ya tukio hili haikuisha katika maisha ya Petro katika kumfuasa Yesu, ilileta msukumu wa ndani na imani kubwa ndani yake juu ya Yesu. Petro aliandaliwa kwani alikuwa afanye jambo kubwa kwaajili ya Yesu “Usiogope, tangu sasa utakuwa ukivua watu.” Yesu anatuita nasi leo, pengine mpaka sasa hatujafanya kitu kwaajili ya faida ya roho zetu. Pengine tumejaribu kushusha neti, kwakuishi maisha yetu bila Yesu na mwisho hatujapata kitu, pengine tumetegemea nguvu zetu wenyewe na mwishowe tumeishia bila chochote. Pengine kwa maisha yetu tumeshindwa kuwavua watu waje kwa Yesu kwasababu ya maisha yetu ya ubinafsi. 

Licha ya yote haya Yesu leo anatupa tena nafasi nyingine tutupe tena nyavu zetu, tumrudie tena yeye, kama tulizoea kuishi maisha bila neno lake basi tuanze leo kuliishi tena, tutavua samaki wengi zaidi, tutafanikiwa sana maisha yetu kama Yesu atatawala nasi daima. Kwa maisha yetu tutakuwa kivutio cha kuwaleta wengi kwa Yesu. Maisha yetu yakitawaliwa na Yesu wengi watavutwa nasi na kwa pamoja tutakuwa wavuvi wawatu tunaowaleta watu kwa Yesu ili kwa pamoja tumtumikie yeye. 

Sala: Asante Yesu, nimejikabidhi kwako naomba nisikuache kamwe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 3, 2026



MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 3, 2026
ALHAMISI, JUMA LA 22 LA MWAKA


SOMO 1
1Kor. 3:18 – 23

Mtu asijidanganye mwenyewe; kama mtu akijiona kuwa mwenye hekima miongoni mwenu katika dunia hii, na awe mpumbavu, ii apate kuwa mwenye hekima. Maana hekima ya dunia hii ni upuzi mbele za Mungu. Kwa maana imeandikwa, yeye ndiye awanasaye wenye hekima katika hila yao. Na tena, Bwana anayafahamu mawazo ya wenye hekima ya kwamba ni Paulo, au Apolo, au Kefa; au dunia, au uzima, au mauti; au vile vilivyopo sasa, au vile vitakavyokuwapo; vyote ni vyenu; nanyi ni wa Kristo, na Kristo ni wa Mungu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 24:1 – 6 (K) 1

(K) Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana.

Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana,
Dunia na wote wakaao ndani yake.
Maana ameiweka misingi yake juu ya bahari,
Na juu ya mito ya maji aliithibitisha. (K)

Ni nani atakayepanda katika mlima wa Bwana?
Ni nani atakayesimama katika patakatifu pake?
Mtu aliye na mikono safi na moyo mweupe,
Asiyeiinua nafsi yake kwa ubatili,
Wala hakuapa kwa hila. (K)

Atapokea Baraka kwa Bwana,
Na haki kwa Mungu wa wokovu wake.
Hiki ndicho kizazi cha wamtafutao,
Wakutafutao uso wako, Ee Mungu wa Yakobo. (K)


SHAGILIO
1Thes. 2:13

Aleluya, aleluya,
Lipokeeni neno la Mungu, siyo kama neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu.
Aleluya.


INJILI
Lk. 5:1 – 11

Makutano walipomsonga Yesu wakilisikiliza neno la Mungu, yeye alikuwa amesimama kando ya ziwa la Genesareti, akaona vyombo viwili vimekaa kando ya ziwa, lakini wavuvi wametoka, wanaosha nyavu zao. Akaingia katika chombo kimoja, ndicho chake Simoni, akamtaka akipeleke kidogo na pwani. Akaketi, akawafundisha makutano ali chomboni.

Hata alipokwisha kunena, alimwambia Simoni, Tweka mpaka kilindini, mkashushe nyavu zenu mvue samaki. Simony akajibu akamwambia, Bwana mkubwa, tumefanya kazi ya kuchosha usiku kucha, tusipate kitu; lakini kwa neno lako nitazishusha nyavu. Basi, walipofanya hivyo walipata samaki wengi mno, nyavu zao zikaanza kukatika; wakawapungia mikono washirika wao waliokuwa katika chombo cha pili, waje kuwasaidia; wakaja, wakavijaza vyombo vyote viwili, hata vikataka kuzama.

Simoni Petro alipona hayo, alianguka magotini pa yesu, akisema, Ondoka kwangu, kwa kuwa mimi ni mtu mwenye dhambi, Bwana. Maana alishikwa na ushangao, yeye na wote waliokuwa pamoja naye, kwa sababu ya wingi wa samaki walaioupata; na kadhalika Yakobo na Yohane, wana wa Zebedayo, waliokuwa washirika wa Simoni. Yesu akamwambia Simoni, Usiogope, tangu sasa utakuwa ukivua watu. Hata walipokwisha kuviegesha pwani vyombo vyao, wakaacha vyote wakamfuata.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

NGUVU YA MAMLAKA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatano, Septemba 2, 2026, 
Juma la 22 la Mwaka wa Kanisa

1 Kor 3: 1-9 
Zab 32: 12-15, 20-21 
Lk 4: 38-44

NGUVU YA MAMLAKA!

Katika Injili ya leo, tunaona Yesu akimponya mkwewe Simoni. Mara nyingi Yesu aliponya kwa kugusa bali pia alikuwa na neno la mamlaka la kuponya kwa kuamuru. Msisitizo unaoneshwa kwenye Injili, ugonjwa ndio unao amriwa, kama Yesu alivyo amuru mawimbi ya bahari ya Galilaya kwa mamlaka, “hali ikawa shwari” na Amani ikawapo (Mk 4: 39), na mawimbi yakatulia. Je, hili linawezekana kwa mfuasi wa Yesu katika nyakati hizi!. Ukweli ni kwamba amri ya kuamuru inatoka katika mamlaka sio katika nguvu. Kwahiyo tunapaswa kuwa wafuasi tuliojazwa na mamlaka sio nguvu. Hili linawezekana tu, namanisha tu kwa kukutana na Yesu nakumvaa yeye sio kwakuwa na elimu ya Yesu tu. Ni katika kufikia kiwango cha kusema kama Paulo kuishi kwangu sio mimi bali Kristo anaishi ndani yangu. Twaweza kufanya yote kama tutaunganika na Yesu kweli kweli, si katika kuwa na elimu kuhusu maandiko na kushindwa kuyaruhusu yakufanye uunganike na Yesu. Kwa njia nyingine tumvae Kristo.

Kama tunavyosikia katika somo la kwanza, tumruhusu Mungu akuze maisha yetu, tumuache Kristo afanye mabadiliko ndani yetu. Sisi ni shamba la Mungu tumruhusu Mungu akuze zawadi mbali mbali mioyoni mwetu ili tuweze kuzaa matunda yenye kumpendeza. Tushirikiane na Mungu ili zawadi anazo kuza ndani yetu ziweze kumrudishia sifa na utukufu.

Sala: Bwana, tufanye washiriki wa mamlaka yako. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 2, 2026



MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 2, 2026
JUMATANO , JUMA LA 22 LA MWAKA

SOMO 1
1 Kor. 3:1 – 9

Ndugu zangu, mimi siwezi kusema nanyi kama na watu wenye tabia ya rohoni, bali kama na watu wenye tabia ya mwilini, kama na watoto wachanga katika Kristo. Naliwanywesha maziwa, sikuwalisha chakula; kwa kuwa mlikuwa hamjakiweza. Naam, hata sasa hamkiwezi, kwa maana hata sasa ninyi ni watu wa tabia ya mwilini. Maana, ikiwa kwenu kuna husuda na fitina, je! Si watu wa tabia ya mwilini ninyi; tena mnaenenda kwa jinsi ya kibinadamu? Maana hapo mtu mmoja asemapo, Mimi ni wa Paulo; na mwingine, Mimi ni wa Apolo, je! Ninyi si wanadamu?

Basi Apolo ni nani? Na Paulo ni nani? Ni wahudumu ambao kwao mliamini; na kila mtu kama Bwana alivyompa. Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu. Hivyo, apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye. Basi yeye apandaye, nay eye atiaye maji ni wamoja, lakini kila mtu atapata thawabu yake mwenyewe sawasawa na taabu yake mwenyewe. Maana sisi tu wafanya kazi pamoja na Mungu; ninyi ni shamba la Mungu, ni jingo la Mungu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 33:12 – 15, 20 – 21 (K) 12

(K) Heri taifa ambalo Bwana ni Mungu wao,
watu aliowachagua kuwa urithi wake.

Heri taifa ambalo Bwana ni Mungu wao,
Watu aliowachagua kuwa urithi wake.
Toka mbinguni Bwana huchungulia,
Huwatazama wanadamu wote pia. (K)

Toka mahali pake aketipo
Huwaangalia wote wakaao duniani.
Yeye aiumbaye mioyo yao wote
Huzifikiri kazi zao zote. (K)

Nafsi zetu zinamngoja Bwana;
Yeye ndiye msaada wetu na ngao yetu.
Maana mioyo yenu itamfurahia,
Kwa kuwa tumelitumainia jina lake takatifu. (K)


SHANGILIO
Yak. 1:21

Aleluya, aleluya,
Pokeeni kwa upole neno la Mungu lililopandwa ndani, liwezalo kuziokoa roho zenu.
Aleluya.


INJILI
Lk. 4:38 – 44

Yesu alitoka katika sinagogi, akaingia katika nyumba ya Simoni. Naye mkwewe Simoni, mamaye mwomba kwa ajili yake. Akasimama karibu naye, akikemea ile hma, ikamwacha; mara hiyo akaondoka, akawatumikia.

Na jua lilipokuwa likichwa, wote waliokuwa na wagonjwa wenye maradhi mbalimbali waliwaleta kwake, akaweka mikono yake juu ya kila mmoja akawaponya. Pepo nao waliwatoka watu wengi, wakipiga kelel na kusema, Wewe u Mwana wa Mungu. Akawakemea, asiwaache kunena, kwa sababu walimjua kuwa ndiye Kristo.

Hata kulipokucha alitoka akaenda mahali pasipokuwa na watu; makutano wakawa wakimtafutatafuta, wakafika kwake, wakataka kumzuia asiondoke kwao. Akawaambia, Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu katika miji mingine pia; maana kwa sababu hiyo nalitumwa. Basi, alikuwa akihubiri katika masinagogi ya Galilaya.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

VITA VYA KIROHO!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumanne, Septemba 1, 2026, 
Juma la 22 la mwaka wa Kanisa

1 Kor 2: 10-16 
Zab 144: 8-14
Lk 4: 31-37

VITA VYA KIROHO!

Leo katika somo la kwanza, Mt. Paulo anaongelea kuhusu Roho wa Mungu na roho wa ulimwengu, vita vya kila wakati katika mioyo yetu, tukivutwa huku na huku. Injili inamuonesha Yesu akitoa pepo, akiamuru “pepo mchafu” atoke ndani ya mtu. Watu wa Kapernaumu huenda walijua mtu yule alikuwa na pepo mchafu, lakini hawakujua nini, au nani, huyo pepo. Hawakuweza kulitambua kwa jina au kufahamu. Lakini Yesu aliweza. Umoja wake na Baba unampa utambuzi ambao wengine hawana. Mt. Inyasi wa Loyola anatumia neno la “utambuzi wa roho” kwa mpangilio uliojikita kwenye Imani kwa nia ya kutambua na kuelewa, nini kinaendelea ndani ya mioyo yetu na nini mapenzi ya Mungu kwa ajili yetu. Tuombe neema ya kutambua machafuko ndani ya mioyo yetu na kuisikiliza sauti ya Mungu. 

Sala: Baba Mungu, ninakuomba wewe “Roho ya utambuzi” ili niweze kukua daima na kusikiliza sauti ya Roho wako kwa haraka na kwa ufasaha kila wakati. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 1, 2026



MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 1, 2026
JUMANNE, JUMA LA 22 LA MWAKA

SOMO 1
1 Kor. 2:10 – 16

Roho huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu. Maana ni nani katika binadamu ayajuaye mambo ya binadamu ila roho ya binadamu ayajuaye mambo ya binadamu ila roho ya binadamu iliyo ndani yake? Vivyo hivyo na mambo ya Mungu hakuna ayafahamuye ila Roho wa Mungu. Lakini sisi hatukuipokea roho ya dunia, bali Roho atokaye kwa Mungu, makusudi tupate kuyajua tuliyokirimiwa na Mungu. Nayo twayanena, si kwa maneno yanayofundishwa kwa hekima ya kibinadamu, bali yanayofundishwa na Roho, tukiyafasiri mambo ya rohoni kwa maneno ya rohoni.

Basi mwanadamu wa tabia ya asili hayapokei mambo ya Roho wa Mungu; maana kwake huyo ni upuzi, wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana kwa jinsi ya rohoni. Lakini mtu wa rohoni kuyatambua yote, wala yeye hatambuliwi na mtu. Maana, ni nani aliyeifahamu nia ya Bwana, amwelimishe? Lakini sisi tunayo nia ya Kristo.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 145:8 – 14 (K) 17

(K) Bwana ni mwenye haki katika njia zake zote.

Bwana ana fadhili, ni mwingi wa huruma,
Si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema,
Bwana ni mwema kwa watu wote,
Na rehema zake zi juu ya kazi zake zote. (K)

Ee Bwana, kazi zako zote zitakushukuru,
Na wacha Mungu wako watakuhimidi.
Wataunena utukufu wa ufalme wako,
Na kuuhadithia uweza wako.
Ili kuwajulisha watu matendo yake makuu,
Na utukufu wa fahari ya ufalme wake. (K)

Ufalme wako ni ufalme wa zamani zote,
Na mamlaka yako ni ya vizazi vyote.
Bwana huwategemeza wote waangukao,
Huwainua wote walioinama chini. (K)


SHANGILIO
Ebr. 4:12

Aleluya, aleluya,
Neno la Mungu li hai tena li na nguvu, li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo.
Aleluya.


INJILI
Lk. 4:31 – 37

Yesu alishuka mpaka Kapernaumu, mji wa Galilaya, akawa akiwafundisha siku ya sabato; wakashangaa mno kwa mafundisho yake, kwa kuwa neno lake lilikuwa na uwezo.

Na ndani ya sinagogi mlikuwa na mtu mwenye roho ya pepo mchafu, akalia kwa sauti kuu, akisema, Acha! Tuna nini nawe, Yesu wa Nazareti? Umekuja kutuangamiza? Nakujua u nani, Mtakatifu wa Mungu. Yesu akamkemea, akisema, Fumba kinywa, mtoke. Ndipo yule pepo akamwangusha katikati, akamtoka asimdhuru neno. Mshangao ukawashika wote, wakasemezana wakisema, Ni neno gani hili, maana awaamuru pepo wachafu kwa uwezo na nguvu, nao hutoka. Habari zake zikaenea kila mahali katika nchi ile.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

KRISTO ANAONGEA NASI KWA NJIA YA FAMILIA NA MARAFIKI ZETU!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatatu, Agosti 31, 2026.
Juma la 22 la Mwaka


1 Kor 2: 10-16; 
Zab 119:97-102
Lk 4:16-30

KRISTO ANAONGEA NASI KWA NJIA YA FAMILIA NA MARAFIKI ZETU! 

Kwa ujumla tukitazama maisha yetu, inaweza kuwa vigumu kuongelea mambo ya kiroho, Biblia na Yesu na familia zetu, ndugu na marafiki tukilinganisha na kuongea na watu tusio wajua. Inaweza ikawa tena ngumu zaidi kwa sisi wenyewe kushindwa kuona jambo lolote zuri la kiroho tunalo weza kujifunza kutoka kwa wenzetu. Inaweza kuwa tunaogopa kuchekwa au kukataliwa.

Leo Yesu anasoma sehemu ya maandiko katika chuo cha nabii Isaya, hekaluni, mbele ya ndugu zake. Yesu anaendelea kusema “hakuna nabii anaye kubalika nyumbani kwake mwenyewe”. Jamaa zake walimsikiliza na walivutwa sana, lakini wakaanza kuhitimisha mara moja kwamba huyu hana kitu, si mwana wa seremala? Mwishoni wanashikwa na hasira na wanamtoa Yesu nje wakitaka kumua. 

Kama Mwana wa Mungu alipata wakati mgumu wa kukubalika katika jamaa yake mwenyewe, itakuwa vigumu pia kushirikishana Injili na wale walio karibu yetu. Lakini kilicho cha muhimu inategemea tuna fanyaje au hatumuone Kristo katika wale walio karibu yetu? Je, sisi ni mmoja wapo wa wale wasiopenda au kukataa kumuona Kristo katika ndugu zetu wa familia na wa karibu? Je, tunakuwa watu wakuhukumu wale walio karibu yetu? 

Ukweli ni kwamba ni rahisi kwetu sisi kuona makosa ya wale walio karibu yetu kuliko kuona fadhila zao. Ni rahisi zaidi kuona dhambi zao kuliko kuona uwepo wa Kristo katika maisha yao. Lakini sio kazi yetu kunyoosha kidole juu ya dhambi zao. Ni jukumu letu kumuona Mungu ndani yao. Kila mtu aliye karibu yetu bila kuwa na shaka, ana uzuri ndani yake. Watakuwa na hali ya kumtafakari Mungu kama sisi tupo tayari kuliona kwao zaidi. Kazi yetu haipaswi kuliona hilo tu bali kulitafuta ndani yao. Na tunapo kuwa karibu zaidi kati yao ndivyo tunavyopaswa kuchunguza zaidi uwepo wa Mungu ndani ya maisha yao. 

Tafakari leo, kama upo tayarii kutaka kuona unabii wa sauti ya Kristo ulio ndani ya watu walio karibu yako. Je, upo tayari kuona, kumkubali na kumpenda yeye ndani yao? 

Sala: Bwana, ninakuomba nikuone wewe kwa wale wote waliokaribu yangu kila siku. Ninakuomba nikutafute wewe zaidi katika maisha yao. Na ninapo kupata wewe ndani yao, nikupende wewe ndani yao. Yesu, nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, AGOSTI 31, 2026



MASOMO YA MISA, AGOSTI 31, 2026
JUMATATU, JUMA LA 22 LA MWAKA

SOMO 1
1 Kor. 2:1 – 5

Ndugu zangu, mimi nilipokuja kwenu, sikuja niiwahubiri siri ya Mungu kwa ufasaha wa maneno, wala kwa hekima. Maana naliazimu nisijue neno lolote kwenu ila Yesu Kristo, naye amesulibiwa. Name nalikuwako kwenu katika hali ya udhaifu na hofu na matetemeko mengi. Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu, ili Imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 119:97 – 102 (K) 97

(K) Sheria yako, Ee Bwana, naipenda mno ajabu.

Sharia yako naipenda mno ajabu,
Ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa.
Maagizo yako hunitia hekima kuliko adui zangu,
Kwa maana ninayo siku zote. (K)

Ninazo akili kuliko wakufunzi wangu wote,
Maana shuhuda zako ndizo nizifikirizo.
Ninao ufahamu kuliko wazee,
Kwa kuwa nimeyashika mausia yako. (K)

Nimeiepusha miguu yangu na kila njia mbaya,
Ili nilitii neno lako.
Sikujiepusha na hukumu zako,
Maana Wewe mwenyewe umenifundisha. (K)


SHANGILIO
Kol. 3:16, 17

Aleluya, aleluya,
Neno la Kristo likae kwa wingi ndani yenu katika hekima yote; mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye.
Aleluya.


INJILI
Lk. 4:16 – 30

Yesu alienda Nazareti, hapo alipolelewa; na siku ya sabato akaingia katika sinagogi kama ilivyokuwa desturi yake, akasimama ilia some. Akapewa chuo cha nabii Isaya, akakifungua chuo, akatafuta mahali palipoandikwa, 

Roho wa Bwana yu juu yangu, kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, na vipofu kupata kuona tena, kuwaacha huru waliosetwa, na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa.

Akakifunga chuo, akamtudishia mtumishi, akaketi; na watu wote waliokuwamo katika sinagogi wakamkazia macho. Akaanza kuwaambia, Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu. Wakamshuhudia wote, wakiyastaajabia maneno ya neema yaliyotoka kinywani mwake.

Wakasema, Huyu siye mwana wa Yusufu? Akawaambia, Hapana shaka mtaniambia mithali hii, Tabibu, jiponye nafsi yako; mambo yote tuliyosikia kwamba yametendeka Kapernaumu, yatende hapa pia katika nchi yako mwenyewe. akasema, Amin, nawaambia ya kuwa, Hakuna nabii mwenye kukubalika nchi yake mwenyewe.

Lakini, kwa hakika nawaambia, Palikuwa na wajane wengi katika nchi ya Israeli zamani za Eliya, wakati mbingu zilipofungwa miaka mitano na miezi sita, njaa kuu ikaingia nchi nzima; wala Eliya hakutumwa kwa mmojawapo, ila kwa mjane mmoja wa Sarepta katika nchi ya Sidoni. Tena, palikuwa na wenye ukoma wengi katika Israeli zamani za nabii Elisha, wala hapana aliyetakaswa ila Naamani, mtu wa Shamu.

Wakajaa ghadhabu wote waliokuwa katika sinagogi walipoyasikia hayo. Wakaondoka wakamtoa nje ya mji, wakampeleka mpaka ukingo wa kilima ambacho mji wao umejengwa juu yake, wapate kumtupa chini; lakini yeye alipita katikati yao, akaenda zake.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

YATOE MAISHA KAMA HUTAKI KUYAPOTEZA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumapili, Agosti 30, 2026 
Juma la 22 la Mwaka
___________________

Yer 20:7-9; 
Zab 62:2-6, 8-9; 
Rum 12;1-2; 
Mt 16:21-27
___________________

YATOE MAISHA KAMA HUTAKI KUYAPOTEZA!

“Mbegu ya ngano isipo anguka katika ardhi na kufa, inabaki kuwa hivyo hivyo, lakini ikifa, inazaa matunda zaidi” (Yn 12:24). Mungu alimwahidia Abrahamu mafanikio na kuwa na watoto kama nyota za Mbinguni, alimwambia pia amtoe sadaka mwanae wa pekee Isaka, ambaye ndiye aliyekuwa afanye ahadi yake itimie. Jaribio kama hili linaweza kukabiliwa na mtu mwenye kuamini kama Abraham. Leo Yesu ana ahidi kuwatambulisha wafuasi katika maisha “atakaye nifuata mimi atakuwa na nuru ya uzima…hataona kifo…hatakufa.” (Yn 8:12, 51-52)

“Mungu ni mwema kwa walio na haki, kwa watu walio na mioyo safi” (Zab 73:1). “Mwamini yeye na mruhusu yeye afanye kazi atakuwa sababu ya wewe kungaa kama jua”. (Zab 37:5-6). Mungu alimwita Yeremia “Nenda utume wowote nitakao kupa, na utasema chochote kile nitakacho kuamuru useme,” wakati alivyo kuwa na woga, akilalamika kwamba yeye ni mdogo na kwamba hafahamu kuongea, Bwana alimhakikishia: “usiogope..nitakuwa nawe kukulinda…watapigana nawe lakini hawatakushinda kwani nitakuwa nawe kukuokoa” (Yer 1:7-8, 19). Yeremia alikubali, watu hawakumuelewa, aliambiwa akae kimya na hata alipigwa na kufungwa gerezani. Katika hali hii Yeremia akapaza kilio chake kwa Mungu, ambapo kinasikika katika somo la kwanza “Yahweh, uliniita mimi nami nikaitika”. Nabii anafananisha wito wake kama vile mvulani anavyo mchumbia mwanamke kwa maneno mazuri, na baada ya kukubali maneno yake, na kutimiza haja ya moyo wake, anaachwa. Hivyo anajikuta akilaani kwanini alianguka kwenye upendo wa uongo. Katika hali hiyo ya taabu, Yeremia anajazwa na hasira kwa mpendwa wake na anasema “sintamfikiria tena Mungu na wala sintaongea tena juu ya jina la Mungu”. Lakini kwasababu alisha uonja upendo wa Mungu, Yeremia anashindwa kujinasua yeye ambaye alishaitika wito wake. Ndani ya moyo wake kuna waka moto ambao hawezi kuuzima. Pamoja na mateso anayopata na wakati mgumu alionayo hawezi kuacha utume wake.

Katika somo la pili Paulo anawaasa wakristo wasije wakashikamana na mtazamo wa “ulimwengu huu”, namna ya kuwaza na jinsi dunia inavyo dhani ni hekima kwa wote. Mkristo hapaswi kuwaza na kujiingiza kwenye maadili ambayo dunia inadhani ni sawa tu kwa wote. Mkristo anapaswa kutambua, kuwa mtulivu, na kuwa na akili ya upya muda wote, tabia ambayo inakubalika kwa Mungu hata kama watu hawaitaki au haionekani yenye maana kwa watu.

Katika somo la Injii Yesu ameamua kurarua matarajio ya wafuasi. Mawazo ya mitume yalikuwa ni kupata sehemu nzuri ya heshima kwasababu ya mawazo yaliyo kuwa yameshasemwa na vongozi wa Wayahudi, kuwa na Amani na ulimwengu mpya wenye haki. Waliamini kwamba mwisho wa ulimwengu ulikuwa karibu na mkuu wao alikuwa ni Kristo, Masiha anaye subiriwa “Mwana wa Daudi”. Tangu kungara sura, na kumpa Petro funguo, walimfuata Yesu ili waweze kushuhudia uhalisia wa ndoto zao za utukufu. 

Yesu akijua hali hii ya mtazamo mbaya kuhusu yeye, anaamua kubadilisha mitizamo yao. Anasema kwa wazi kwamba yeye hatembei kuuendea utukufu huo, bali kwenda Yerusalemu kuteswa, kuuwawa na siku ya tatu atafufuka. Mitume hawakuweza kulielewa hili., kwasababu walikuwa wameshajifunza kutoka kwa Marabi kwamba Masiha hawezi kufa, na kwamba waliowema watafufuka na kuingia katika utawala wa huyu Masiha atakaye kuja, na hivyo Petro anamjibu. Petro hataki kusimama katika barabara inayo ongoza katika kutofanikiwa. Anajaribu kumbadilisha Yesu abadilishe mtazamo wake.

Jibu la Yesu “rudi nyuma yangu shetani”. Petro hakuwa anatenda kosa dogo. Alikuwa anafuata njia inayo pingana na Bwana. Alikuwa akitenda kama zile tabia za shetani aliye jaribu kumshawishi Yesu aelekeze mawazo yake katika ufalme wa kidunia, na kuwa na mamlaka ya kuangamiza. Alimuongoza katika mlima mkubwa nakumuonesha falme zote kwa mara moja na utukufu wa ulimwengu na kumwambia “yote haya nitakupa, kama utapiga goti na kunisujudia mimi” lakini Yesu akajibu “nenda zako shetani” (Mt 4:8-10). Sasa kishawishi hiki hiki –katika hali ya juu pia na Petro-hawezi kuacha bali kujibu kwa ukali ule ule.

Katika Injili ya jumapili iliyopita, Simoni Petro alikuwa ameitwa na Yesu kwamba yeye ni jiwe linaloishi la kanisa lake kwasababu alikuwa amepokea ufunuo wa Baba yake, alipokea Imani na mpango wake na amekiri Imani juu ya Mwana wa Mungu aliye hai. Sasa anajikuta yeye mwenyewe akianguka kwani aliruhusu akili ya kibinadamu imtawale. Baada ya kumkemea Petro anawageukia pia na wengine na kuwaeleza wazi.

Mambo matatu muhimu katika kubadilika “Jikane mwenyewe uchukue msalaba wako unifuate”. Kwanza, kujikana mwenyewe maana yake kila mfuasi aache kujifikiria mwenyewe kwanza. Neno hili ni ni muhimu sana katika ulimwenu wetu wa ubinafsi na umimi. Hali ya kujali mambo binafsi zaidi yanazingatiwa hata katika jambo dogo la upendo kwa wengine. Mfuasi yeyote wa Kristo anaitwa kwanza kabisa kuacha mambo yeyote ya ubinafsi, hata kujipendelea mwenyewe kiroho bila kuwaombea wengine. Daima anapaswa kutenda mapenzi ya Mungu. 

Pili, “kuchukua msalaba” haina maana ya kuvumilia mateso kidogo au makubwa ya maisha kama sehemu ya kumfurahisha Mungu. Mkristo hatafuti mateso bali upendo. Msalaba ni ishara ya upendo na zawadi kuu. Kuubeba na kumfuata Kristo maana yake umeamua kufuata ile njia yake ya upendo kwa ajili ya wanadamu. Kutoa maisha kwa ajili ya wengine, kufariji, hata kifo na mateso kwa ajili ya kubaki katika kuishika injili yake. 

Na hatimaye, “Nifuate mimi” maana yake kushiriki’ kuchagua kumfuata, kwa mapendo na kukabidhi maisha yote kwa Mungu. Kutoa maisha yako kwa mapendo na kuwa naye.

Yesu anamalizia na sababu tatu za kuwasihi wafuasi wake wapokee hayo maelekezo: kwanza, anaye toa maisha yake kwa ajili ya mwingine hayapotezi bali anayapokea. Ni yule tuu mwenye ujasiri wa kupoteza mbegu ya uzima wa maisha yake, kutupwa ardhini, “kuilinda” “ataipokea”. Pili, maisha ya ulimwengu huu yanaisha mara moja. Ni ya kupita, ni hafifu, na sio vizuri kuyategemea kama vile ni ya milele. Tatu, ni zawadi ya mwisho, Mungu hataangalia majina au mangapi tumejitengenezea mbele za watu au kwa jina letu, bali ni kazi ngapi za mapendo zinazo toka katika majina yetu. Kwa njia hiyo utakatifu wetu haupimwi na sifa wanazo sema watu juu yetu bali kazi njema za mapendo na muonekano wetu mbele ya Mungu.

Sala: Bwana, nakupenda wewe. Ninakuomba nisiogope kujikana mwenyewe, kuchukua msalaba wangu, nakukufuata wewe. Ninakuomba nikuwe katika upendo na wewe, ili niweze kuishi maisha yangu kwa upendo wako. Ninakuomba matendo ya maisha yangu yalindwe na uhusiano wangu na wewe. Ninakuomba nifuate sadaka yako ya kujitoa bila kujibakiza, na kuwa sadaka kwa watu wote. Yesu, nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUMAPILI, AGOSTI 30, 2026


MASOMO YA MISA, 
JUMAPILI, AGOSTI 30, 2026
JUMA LA 22 LA MWAKA 
________

MWANZO
Zab. 86:3, 5

Ee Bwana, unifadhili maana nakulilia wewe mchana kutwa. Kwa maana wewe, Bwana, u mwema, umekuwa tayari kusamehe, na mwingi wa fadhili kwa watu wote wakuitao.
________

SOMO I
Jer. 20:7-9

Ee Bwana, umenihadaa, nami nimehadaika; wewe una nguvu kuliko mimi, ukashinda; nimekuwa kitu cha kuchekesha, mchana kutwa; kila mtu hunidhihaki. Maana kila ninenapo napiga kelele; nalia, Dhuluma na uharibifu! Kwa kuwa neno la Bwana limefanywa shutumu kwangu, na dhihaka, mchana kutwa. Nami nikisema, Sitamtaja wala sitasema tena kwa jina lake; ndipo moyoni mwangu kumekuwamo kama moto uwakao, uliofungwa ndani ya mifupa yangu, nami nimechoka kwa kustahimili, wala siwezi kujizuia.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu
________

WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 63:1-5, 7-8 (K) 1

(K) Ee Bwana, Mungu wangu, nafsi yangu inakuonea kiu.

Ee Mungu, Mungu wangu, nitakutafuta mapema,
Nafsi yangu inakuonea kiu.
Mwili wangu wakuonea shauku,
Katika nchi kame na chovu, isiyo na maji. (K)

Ndivyo nilivyokutazama katika patakatifu,
Nizione nguvu zako na utukufu wako.
Maana fadhili zako ni njema kuliko uhai,
Midomo yangu itakusifu. (K)

Ndivyo nitakavyokubariki maadamu ni hai,
Kwa jina lako nitaiinua mikono yangu.
Nafsi yangu itakinai kama kushiba mafuta na vinono,
Kinywa changu kitakusifu kwa midomo ya furaha. (K)

Maana Wewe umekuwa msaada wangu,
Na uvulini mwa mbawa zako nitashangilia.
Nafsi yangu imekuandama sana,
Mkono wako wa kuume unanitegemeza. (K)
________

SOMO 2 
Rum 12: 1-2

Basi ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana. Wala msifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu
________

SHANGILIO
Lk 21: 36

Aleluya, aleluya,
Kesheni kila wakati, ili mpate kuokoka, 
na kusimama mbele ya Mwana wa Adamu.
Aleluya
________

INJILI 
Mt 16:21-27

Tangu wakati huo Yesu alianza kuwaonya wanafunzi wake ya kwamba imempasa kwenda Yerusalemu, na kupata mateso mengi kwa wazee na wakuu wa makuhani, na waandishi, na kuuawa, na siku ya tatu kufufuka. Petro akamchukua, akaanza kumkemea, akisema. Hasha, Bwana, hayo hayatakupata. Akageuka, akamwambia Petro, nenda nyuma yangu, Shetani; u kikwazo kwangu; maana huyawazi yaliyo ya Mungu, bali ya wanadamu.

Wakati huo Yesu aliwaambia wanafunzi wake, Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake, anifuate. Kwa kuwa mtu atakaye kuiokoa nafsi yake, ataipoteza; na mtu atakayeipoteza nafsi yake kwa ajili yangu, ataiona. Kwani atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote, na kupata hasara ya nafsi yake? Au mtu atatoa nini badala ya nafsi yake? Kwa sababu Mwana wa Adamu atakuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika zake; ndipo atakapomlipa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo
________

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.