Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

KUFUNGUA MIOYO YETU KWA YESU



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatano, Septemba 16, 2026, 
Juma la 24 la Mwaka 

1 Kor 12:31 – 13:13; 
Zab 32: 2-5, 12, 22; 
Lk 7: 31-35.


KUFUNGUA MIOYO YETU KWA YESU

“Nitakifananisha na nini kizazi hiki?” Kama Yesu angeuliza swali hili hili leo katika kizazi hiki. Angetuweka wapi? Je sisi tutakuwa kama wale watoto ambao wakiwekewa muziki hawachezi hata kukiwa na maombolezo hawaombolezi? Somo la leo linatualika tuweze kuwa katika mstari mmoja na wito wa Mungu, tujitafakari wenyewe na kazi zetu ili tuweze kuwa kweli watoto wa Ufalme wa Mungu. 

Paulo katika Barua yake anatuelekeza juu ya “ni kwa jinsi gani tunapaswa kuwa katika nyumba ya Mungu”. Anawakumbusha waumini kwamba wao ni watu katika nyumba ya Mungu aliye hai, iliyodhihirishwa na Yesu, na kutangazwa na ulimwengu. Anaonesha aina Fulani ya kanuni ya Imani ambayo ilikuwa ni ishara ya Wakristo wa Mwanzo.  Kanuni hii inaonesha aina Fulani ya sifa za Yesu na matendo yake na mpango wa Mungu kwa mwanadamu kwa njia ya Yesu. 

Katika somo la Injili, Mafarisayo wanajiona wenyewe kuwa wema wanafananishwa na wale watoto wasiopenda kufanya chochote. Kama ilivyo vigumu kwa mmoja kuingia nyumba ambayo mlango wake umefungwa na madirisha kufungwa. Yesu hakuweza kuingia katika mioyo ya Mafarisayo kwasababu wameifunga na wameamua kutokuamini. Yesu na Yohane Mbatizaji walikataliwa na Mafarisayo. Injili inamalizikia kwakusema maneno haya: “Aliye na masikio na asikie” yakitutaka tuwe wasikivu na kusikiliza sauti au wito wa Yesu.  

Watoto waliokaa sokoni inatoa picha ya watu ambao muda wote wapo na mambo yao, hawana muda wa kutafakari kuhusu nafsi yao.Wanajishughulisha na biashara zao, kuwa na simu muda wote, au kukesha kwenye komputa. Maisha yetu yamejazwa na uharibifu wa kila aina. Tunajishughulisha na mambo mengi na kusahau lile la muhimu. Hali hii inatufunga sisi na kushindwa kujitambua wenyewe. 
Tutafakari leo kama maisha yetu yamekuwa ya utulivu ya kutufanya tumtambue Yesu. Je, nimekuwa msikivu kwa nafsi yangu? Je, nipo tayari kumrushusu Mungu afanye kazi katika maisha yangu? Kama sio basi fanya jitihada ya kumfuata Yesu na kustahilishwa katika ufalme Mungu. 

Sala: Bwana, ninakuomba ufungue moyo wangu. Ninakuomba nisikie sauti yako ikiniita. Yesu, nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 16, 2026




MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 16, 2026
JUMATANO, JUMA LA 24 LA MWAKA


SOMO 1
1Kor. 12:31--13:13

Takeni sana karama zilizo kuu. Hata hivyo nawaonyesha njia iliyo bora. Nijaposema kwa lugha za wanadamu na za malaika, kama sina upendo, nimekuwa shaba iliayo na upatu uvumao. Tena nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, si kitu mimi. Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu.

Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu; upendo hautakabari; haujivuni; haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni uchungu; hauhesabu mabaya; haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli; huvumilia yote; huamini yote; hutumaini yote; hustahimili yote.

Upendo haupungui neno wakati wowote; bali ukiwapo unabii utabatilika; zikiwapo lugha, zitakoma, yakiwapo maarifua, yatabatilika. Kwa maana tunafahamu kwa sehemu; na tunafanya unabii kwa sehemu; lakini ijapo ile iliyo kamili, iliyo kwa sehemu itabatilika. Nilipokuwa mtoto mchanga, nalisema kama mtoto mchanga, nalifahamu kama mtoto mchanga, nalifikiri kama mtoto mchanga; tokea hapo nilipokuwa mtu mzima, nimeyabatilisha mambo ya kitoto. Maana wakati wa sasa tunaona kwa kioo kwa jinsi ya fumbo; wakati ule tutaona uso kwa uso; wakati wa sasa nafahamu kwa sehemu; wakati wa sasa nafahamu kwa sehemu; wakati ule nitajua sana kama mimi nami ninavyojuliwa sana.

Basi, sasa inadumu imani, tumaini, upendo, haya matatu; na katika hayo lililo kuu ni upendo.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 33:2-5, 12, 22 (K) 12

(K) Heri taifa ambalo Bwana ni Mungu wao.

Mshukuruni Bwana kwa kinubi,
Kwa kinanda cha nyuzi kumi mwimbieni sifa.
Mwimbieni wimbo mpya,
Pigeni kwa ustadi kwa sauti ya shangwe. (K)

Kwa kuwa neno la Bwana lina adili,
Na kazi yake yote huitenda kwa uaminfu.
Huzipenda haki na hukumu,
Nchi imejaa fadhili za Bwana. (K)

Heri taifa ambalo Bwana ni Mungu wao,
Watu aliowachagua kuwa urithi wake.
Ee Bwana, fadhili zako zikae nasi,
Kama vile tulivyokungoja Wewe. (K)



SHANGILIO
Efe. 1:17, 18

Aleluya, aleluya,
Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, awape roho ya hekima mjue tumaini la mwito wake.
Aleluya.



INJILI
Lk. 7:31-35

Yesu aliwaambia makutano: Niwafananishe na nini watu wa kizazi hiki? Nao wamefanana na nini? Wamefanana na watoto walioketi sokoni na kuitana, wakisema, Tuliwapigia filimbi wala hamkucheza; tuliomboleza, wala hamkulia.

Kwa kuwa Yohane Mbatizaji alikuja, hali mkate wala hanywi divai, nanyi mwasema, Ana pepo. Mwana wa Adamu amekuja, anakula na kunywa; nanyi mwasema, Tazama, mlafi huyu, na mnywaji wa divai, rafiki wao watoza ushuru na wenye dhambi. Na hekima imejulikana huwa ina haki kwa watoto wake wote.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

KUTESEKA KWA AMANI NA FURAHA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Jumanne, Septemba 15, 2026 
Juma la 24 la Mwaka


Kumbukumbu ya Bikira Maria Mtakatifu wa Mateso

Ebr 5: 7-9; au 1Kor 15:1-11
Zab 30: 2-6, 15-16, 20; 
Yn 19: 25-27, 35 au Lk 2: 33-35


KUTESEKA KWA AMANI NA FURAHA!


Leo tunakumbuka mateso ya Mama yetu Bikira Maria. Mateso ya Maria yalikuwa ya ndani. Bikira Maria alikuwa mwanadamu kamili kwasababu hakutenda dhambi na kati ya watu waliompendeza Mungu katika hali ya ukamilifu wote ni Bikira Maria licha ya Mwanae, lakini kwa ajili ya hili hatuwezi kusema hakuwa na hisia ya kuhisi mambo ya duniani. Kwasababu ya ukamilifu wake, alipenda kwa mapendo ya ndani kuliko sisi. Kwasababu ya upendo huu, alihisi uchungu wa kumpoteza mwanae kuliko sisi. Mateso ya Maria tofauti na yetu yalikuwa kamili. Mateso yetu mara nyingi yamechanganyika na udhaifu wetu. Maria hakuhuzunika kwasababu atamkosa Mwanae ampe msaada. Aliteseka kwasababu aliona mateso ya yule anaye mpenda, na akahisi mateso yale kama Mwanae alivyohisi. Tunaweza kuhisi pia ni kwa jinsi ghani Yesu alivyojisikia alivyomuona Mamaye katika huzuni. Ni hakika ilimsababishia mateso pia, lakini ilikuwa pia ni hali ya kuonesha ukaribu wao. Ulimwengu mzima unaweza kuwa umekuwa wa ukatili na hali zote, lakini uso wa Mama yake ulikuwa ni sehemu pekee alioweza kuelekezea macho yake, akiona sura na mfano aliouweka wakati anatuumba sisi.

Huzuni ya mama haikuwa ni huzuni bila matumaini. Alijua kwa matumani fulani kwamba Mwanae atafufuka kutoka wafu. Tumaini lake halikumzuia kuhisi uchungu na wala halikumzuia kutazamia ufufuko wake. Maria ni Mama yetu. Kama ilivyo kwa Mama mwema, anatufundisha sisi. Tunapaswa tutuoe muda wetu tukiwa naye katika mti wa Msalaba, tukimuomba atufundishe jinsi ya kuhisi nasi mateso yetu katika maisha. Tusisite kumkimbilia atuombee tunapokumbana na adha na mateso katika maisha, yeye awe faraja na msaada wetu kwani atakuwa nasi, akisimama nasi na kuteseka nasi, akiyaweka yote chini ya Msalaba wa Mwanae kwa niaba yetu.


Sala: Mama wa Upendo, Mama wa Mateso na Mama wa huruma, utuombee sisi. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA JUMANNE, SEPTEMBA 15, 2026


MASOMO YA MISA 
JUMANNE, SEPTEMBA 15, 2026
JUMA LA 24 LA MWAKA


KUMBUKUMBU YA BIKIRA MARIA MTAKATIFU WA MATESO


SOMO 1
Ebr. 5:7 – 9

Kristo, siku hizo za mwili wake, alimtolea yule, awezaye kumwokoa na kumtoa katika mauti, maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi, akasikilizwa wa jinsi alivyokuwa mcha Mungu; na, ingawa ni Mwana, alijifunza kutii kwa mates ohayo yaliyompata; naye alipokwisha kukamilishwa, akawa sababu ya wokovu wa milele kwa watu wote wanaomtii.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 31:1 – 5, 14 – 15, 19 (K) 16

(K) Uniokoe, Ee Bwana, kwa ajili ya fadhili yako.

Nimekukimbilia Wewe, Bwana,
Nisiaibike mbele kwa haki yako uniponye.
Unitegee sikio lako, uniokoe hima. (K)

Uwe kwangu mwamba wa nguvu,
Nyumba yenye maboma ya kuniokoa,
Ndiwe genge langu na ngome yangu,
Kwa ajili ya jina lako uniongoze, unichunge. (K)

Utanitoa katika wavu walionitegea kwa siri,
Maana wewe ndiwe ngome yangu.
Mikononi mwako naiweka roho yangu,
Umenikomboa, Ee Bwana, Mungu wa kweli. (K)

Lakini mimi nakutumaini Wewe, Bwana,
Nimesema, Wewe ndiwe Mungu wangu.
Nyakati zangu zimo mikononi mwako;
Uniponye na adui zangu, nao wanaonifuatia. (K)

Jinsi zilivyo nyingi fadhili zako
Ulizowawekea wakuchao;
Ulizowatendea wakukimbiliao
Mbele ya wanadamu! (K)


SHANGILIO

Aleluya, aleluya,
Bikira Maria anafurahi yeye ameshinda na kupata nishani ya ushahidi pasipo kufa, alipokuwa chini ya msalaba wa Bwana.
Aleluya.


INJILI
Yn. 19:25 – 27

Penye msalaba wake Yesu walikuwa wamesimama mamaye, na umbu la mamaye, Mariamu wa Klopa, na Mariamu Magdalene. Basi Yesu alipomwona mama yake, na yule mwanafunzi aliyempenda amesimama karibu, alimwambia mama yake, Mama, tazama, mwanao. Kisha akamwambia yule mwanafunzi, Tazama, mama yako. Na tangu saa ile mwanafunzi yule akamchukua nyumbani mwake.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Au

INJILI
Lk. 2:33 – 35

Babaye na mamaye wa Yesu walikuwa wakiyastaajabia hayo yaliyonenwa juu yake. Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa. Nawe mwenyewe, upanga ukaingia moyoni mwako, ili yafunuliwe mawazo ya mioyo mingi.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MSALABA WA KRISTO NI TUMAINI NA UKOMBOZI WETU!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatatu, Septemba 14, 2026, 
Juma la 24 la Mwaka wa Kanisa

Sikukuu ya Kutukuka kwa Msalaba Mtakatifu

Hes 21: 4-9 
Zab 77: 1-2, 34-38
Fil 2: 6-11
Yn 3: 13-17


MSALABA WA KRISTO NI TUMAINI NA UKOMBOZI WETU!


Msalaba ni ishara ya Mkristo. Kila Mkristo, mtoto na hata mtakatifu mkubwa kabisa, wanafanya ishara ya Msalaba, kutoa ushuhuda wa nguvu yake na umuhimu wake. Yesu alitoa maisha yake Msalabani na hapo akakomboa ubinadamu. Kwa njia hii hamna tena alama ya mateso na aibu, bali ukombozi. Msalaba ni njia ya kwenda kwenye utukufu, kwahiyo ni changamoto kwa kila Mkristo. Kama Mtakatifu Paulo anavyosema “Tunamuhubiri Yesu Msulubiwa, kwa Wayahudi ni kikwazo na kwa Wayunani ni upuuzi, bali kwao waitwao, Wayahudi kwa Wayunani ni Kristo, Nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu” (1 Kor 1: 23-24). 

Katika historia ya Ukristo Msalaba aliofia Kristo na kwa njia hii akafufuka, umekuwa ni ishara wazi ya nguvu ya Mungu ya kuokoa. Mababa wa Kanisa wanalinganisha Msalaba wa Yesu na mti wa uzima katika bustani ya dunia, safina ya Noah, na kuni alizobeba Isaka katika mlima Moriah, na ile ngazi ya Yakobo, na ile Fimbo ya Musa, na yule nyoka ya Shaba. Haya yote katika hali ya juu yana husishwa na fumbo la ukombozi. Katika Ubatizo kila Mkristo amesulubiwa na Kristo, kufa na kufufuka na Kristo. Mtakatifu Leo Mkuu anasema, “Msalaba ni chanzo cha kila Baraka, chanzo cha mafanikio yote: kwa waamini unawapa nguvu kutoka katika udhaifu wake, utukufu kutoka katika aibu yake, na uzima kutoka katika kifo”.

Tafakari leo, juu ya msalaba wa Yesu Kristo. Chukua muda Fulani ukiutazama na kutafakari. Na ona jibu katika msalaba huo juu ya shughuli zako za kila siku. Yesu yupo karibu na wale wanaoteseka, na nguvu yake ipo kwa wale wote wanao mwamini ndani yake.

Sala: Bwana, nisaidie mimi niweze kutazama msalaba wako. Nisaidie niweze kuonja ushindi wa mwisho wa mateso yako. Ninaomba nikusanywe na kuponywa ninapo kutazama wewe. Yesu nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 14, 2026



MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 14, 2026
JUMATATU, JUMA LA 24 LA MWAKA

SIKUKUU YA KUTUKUKA KWA MSALABA


SOMO 1
Hes. 21:4 – 9

Siku zile jangwani, watu walimnung’unikia Mungu, na Musa, mbona mmetupandisha huku kutoka nchi ya Misri, ili tufe jangwani? Maana hapana chakula, wala hapana maji, na roho zetu zinakinai chakula hiki dhaifu. Bwana akatuma nyoka za moto kati ya watu, wakawauma, watu wengi wakafa. Watu wakamwendea Musa, wakasema, tumefanya dambi kwa sababu tumemnung’unukia Mungu, na wewe, utuombee kwa Bwana, atuondolee nyoka hawa. Basi, Musa akawaombea watu. Bwana akawaambia Musa, Jifanyie nyoka ya shaba, ukaiweke juu ya mti, na itakuwa kila mtu aliyeumwa, aitazamapo, ataishi. Musa akafanya nyoka ya shaba, akaiweka juu ya mti, hata ikiwa nyoka amemwuma mtu, alipoitazama ile nyoka ya shaba, akaishi.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 78:1 – 2, 34 – 38 (K) 7

(K) Msiyasahau matendo ya Mungu.

Enyi watu wangu, sikilizeni sheria yangu,
Tegeni masikio kwa maneno ya kinywa changu.
Na nifunue kinywa changu kwa mithali,
Niyatamke mafumbo ya kale. (K)

Alipowaua ndipo walipokuwa wakimtafuta;
Wakarudi wakamtaka Mungu kwa bidii.
Wakakumbuka kuwa Mungu ni mwamba wao,
Na Mungu Aliye juu ni mkombozi wako. (K)

Lakini walimdanganya kwa vinywa vyao, 
Wakamwambia uongo kwa ndimi zao.
Kwa maana mioyo yao haikuwa thabiti kwake,
Wala hawakuwa waaminifu katika agano lake. (K)

Lakini Yeye, kwa kuwa anayo rehema,
Husamehe uovu wala haangamizi.
Mara nyingi huipishia mbali ghadhabu yake,
Wala haiwashi hasira yake yote. (K)


SOMO 2
Fil. 2:6 – 11

Yesu Kristo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama wanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Kwa hiyo tena Mung alimwadhimisha mno, akamkirimia jina lile lipitalo kila jina, ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa Yesu Kristo ni Bwana, kwa utukufu wa Mungu Baba.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


SHANGILIO

Aleluya, aleluya,
Ee Kristu tunakuabudu na kukutukuza, kwa kuwa umeikomboa dunia kwa msalaba wako.
Aleluya.


INJILI
Yn. 3:13 – 17

Yesu alimwambia Nikodemo: Hakuna mtu aliyepaa mbinguni, ila yeye aliyeshuka kutoka mbinguni, yaani, Mwana wa Adamu. Na kama vile Musa alivyomwinua yule nyoka jangwani, vivyo hivyo Mwana wa Adamu hana budi kuinuliwa; ili kila mtu aaminiye awe na uzima wa milele katika yeye. Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe wa pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

KUJENGA JUMUIYA YENYE KUWA NA TAHADHARI!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumapili, Septemba 13,  2026
Juma la 24 la Mwaka wa Kanisa


YbS 27:30-28:1-7
Zab. 103:1-4, 9-12
Rum. 14:7-9
Mt. 18:21-35


KILA MKRISTU NI LAZIMA AWE TAYARI KUSAMEHE WENGINE

Ndugu Zangu, tumesikia neno la Mungu, katika masomo yote matatu. Kama nilivyowadokeza katika utangulizi wangu, kwamba masomo yote, yanaongelea jambo lilio muhimu, katika maisha yetu ya kikristu. Nalo ni kuhusu msamaha. Katika Injili tumesikia, Yesu akiwahitaji wafuasi wake, kuishi maisha ya kusameheana, hivyo nasi wakristo, tunawajibika kuyaishi maisha haya. Kila mkristu ni lazima awe tayari kusamehe wengine, wakati wo wote na bila masharti ye yote. Je, sisi nasi tupo tayari kusamehe? Ni rahisi sana kwetu kuzungumzia kuhusu neno msamaha, lakini linapokufika wewe inakuwa vigumu sana kulitekeleza.

Hebu, tusikilize tukio hili linalowahusu wanawake wawili waliokuwa marafiki wakubwa. Japo nyumba zao zilikuwa siyo karibu sana, lakini mara nyingi walikuwa pamoja. Siku moja kulitokea kutokuelewana baina yao. Kwa sababu ya mambo Fulani-Fulani waliyoyajua wao. Na tangu siku hiyo, urafiki wao ukafikia kikomo na wakawa maadui wakubwa. Viongozi wengi wa dini, waliokuwa wakiufahamu urafiki wao kindani, hasa mapadre, walijitahidi kadiri ya uwezo wao kuwapatanisha, lakini hawakufanikiwa. Ikatokea kuwa wakati wa mgogoro wao huo mimi niliamishiwa maeneo waliyoishi. Kwa vile, niliwafahamu vizuri hawa akina mama, mimi nami niliamua kujaribu bahati yangu ya kuwapatanisha. Hivyo siku moja, nilienda nyumbani kwa mmoja wao, na kuanza kuzungumzia kuhusu neno msamaha. Hususani kwa rafiki yake. Nilimsisitiza kuhusu kusamehe na kusahau tofauti zilizopo baina yao, ili urafiki wao uweze kuendelea. Mnajua alinijibu nini? He! Niko tayari kuingia katika moto wa jehanamu, lakini siyo kumsamehe.

Hivyo tunaweza kuona katika tukio hili ni jinsi gani, mwanamama huyu, alivyokuwa na hasira, na kwamba yupo tayari kwenda jehanamu, lakini siyo kumsamehe mwenzake. Kama hivyo ndivyo tulivyo, tunawezaje kuisema, ile sala aliyotufundisha BY? Ambayo ni sala ya Baba Yetu. Katika sala hii tunasema “utusamehe makosa yetu, kama tunavyowasamehe na sisi wale waliotukosea”. Hii, ina maana kwamba, tunamwomba Mungu atusamehe makosa yetu kama vile, sisi tufanyavyo kwa wenzetu. Hamna shaka NZ, ni wazi kwamba inatuwia vigumu sana kuwasamehe wale waliotusababishia matatizo katika maisha yetu. Lakini swali linabaki, tunaweza kuendelea na kinyongo chetu mpaka lini?

Katika somo la kwanza, tumesikia jinsi hasira na kinyongo vinavyoumiza. Hivyo tunasisitizwa kuwasamehe jirani zetu. Na katika Injili, Yesu anatukumbusha kuhusu kusameheana hasa pale anapomwambia Petro, samehe siyo mara saba tu, bali mara saba sabini. Hivyo na sisi, tunatakiwa kuwasamehe majirani zetu zaidi ya mara saba. Ili tuweze kufanya hivyo tunahitaji kufanya nini?

Kwanza kabisa, ni lazima tusali. Tumwombe Mungu atupe neema ya kuweza kusamehe na pia kusahau. Halafu mwombee na yule aliyekugadhabisha. Wakati Yesu anapotutia moyo wa kuwapenda adui zetu, huwa anatupa pia neema za kutenda hayo. Pili, hebu tujaribu kutafakari ni mara ngapi, Mungu ametusamehe sisi. Yeye ametusamehe mara nyingi zaidi kuliko anavyopenda, sisi kuwasamehe wenzetu. Mungu ni mwenye kusamehe, ni mwenye upendo na ni mwenye huruma kwa wale wote wanaokiuka maagizo yake. Sasa tujiulize ni kwa muda gani, sisi tutaendeleza hasira yetu kwa jirani zetu? Tatu, tujaribu kubadilisha msimamo wetu. Tujaribu kuangalia wale waliotukosea katika muonekano tofauti. Siyo kama adui zetu, bali kama wanadamu na kama tulivyo sisi. Sisi sote tuna vipaji vinavyofanana kama vile, kupenda na kutokupenda, hobi tofauti, muhono tofauti kuhusu mazuri na mabaya na mbaya zaidi tunawaumiza wenzetu, maneno na matendo yetu. Hivyo, pia jirani zetu kama tulivyo, sisi nao pia wanatuumiza kama sisi tunavyoumiza wengine. Ndiyo maana basi, sisi nasi tunahitaji kupata msamaha kutoka kwa wenzetu, kama wao wanaohitaji kutoka kwetu. Kwa hiyo ni jukumu letu kuwasamehe wale waliotukosea.

Yesu alipokuwa pale msalabani aliwaombea watesi wake, “Baba, uwasamehe, kwa kuwa hawajui watendalo” (Lk 23/34). Yesu aliwaona hawa kuwa ni watoto wa Baba ambao wamepotea njia. Kwa hiyo, ni lazima na sisi tuanze kuwaona adui zetu kama vile Yesu alivyowaona watesi wake, na anavyotuona sisi leo hii. Anza leo kutekeleza haya. Omba neema ya kusamehe wengine, na kukumbuka huruma ya Yesu kwetu. Na muone jirani yako au mtesi wako kama ulivyo wewe. Hapo ndipo tutaweza kusamehe na kusahau kama atufanyiavyo Baba yetu wa mbinguni. Katika misa ya leo tumwombe Mungu atupe neema hii ili tuweze kuwa kielelezo bora cha ukristo wetu popote pale tutakapo kuwa.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUMAPILI, SEPTEMBA 13, 2026



MASOMO YA MISA, JUMAPILI, SEPTEMBA 13, 2026
JUMA LA 24 LA MWAKA 
________

MWANZO
YbS 36:15.16

Ee Bwana, uwape amani wakungojao, ili watu wawasadiki manabii wako; usikilize sala ya mtumwa wako, na ya taifa lako Israeli.
________

SOMO I
YbS 27:30-28:1-7

Hasira na ghadhabu, haya pia ni machukuzo na aliye mwenye dhambi yatampata. Mwenye kujilipiza kisasi ataona kisasi kutoka kwa Bwana; hakika Yeye atamfungia dhambi zake. Umsamehe jirani yako dhara alilokufanyia, hivyo nawe utasamehewa dhambi zako wakati utakaposali. Mwanadamu humkasirikia mwanadamu, je! atatafuta kuponywa na Bwana? Hamrehemu mwanadamu aliye mwenzake, je! atalalamika kwa ajili ya dhambi zake mwenyewe? Aliye mwili na damu tu huilisha hasira yake, je! ni nani atakayempatanisha yeye kwa makosa yake? Basi kumbuka mwisho wako, uuache uadui; kumbuka uozi na mauti , ujiepushe na kutenda dhambi. Kumbuka zile amri, usikasirike na jirani yako; nawe ulikumbuke agano lake Aliye juu, umwachilie ujinga wake.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu
________

WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 103:1-4, 9-12

(K) Bwana amejaa huruma na neema, 
si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa fadhili.

Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana,
Naam, vyote vilivyo ndani yangu
Vilihimidi jina lake takatifu.
Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana,
Wala usizisahau fadhili zake zote. (K)

Ndiye anayekusamehe maovu yako yote,
Akuponya magonjwa yako yote.
Akomboa uhai wako na kaburi,
Akutia taji ya fadhili na rehema. (K)

Yeye hatateta siku zote,
Wala hatashika hasira yake milele.
Hatutendei kadiri ya hatia zetu,
Wala halipi kwa kadiri ya maovu yetu. (K)

Maana vile mbingu zilivyoinuka juu ya nchi,
Kadiri ile ile rehema zake ni kuu kwa wamchao.
Kama mashariki ilivyo mbali ma magharibi,
Ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi. (K)
________

SOMO 2 
Rum. 14:7-9

Hakuna mtu miongoni mwetu aishiye kwa nafsi yake, wala hakuna afaye kwa nafsi yake. Kwa maana kama tukiishi, twaishi kwa Bwana, au kama tukifa, twafa kwa Bwana. Basi kama tukiishi au kama tukifa, tu mali ya Bwana. Maana Kristo alikufa akawa hai tena kwa sababu hii, awamiliki waliokufa na walio hai pia.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu
________

SHANGILIO
Yn. 13:34

Aleluya, aleluya,
Amri mpya nawapa, asema Bwana, 
mpendane, kama vile nilivyowapenda ninyi.
Aleluya.
________

INJILI 
Mt. 18:21-35

Petro alimwendea Yesu akamwambia, Bwana ndugu yangu anikose mara ngapi nami nimsamehe? hata mara saba? Yesu akamwambia, Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini.

Kwa sababu hii ufalme wa mbinguni umefanana na mfalme mmoja aliyetaka kufanya hesabu na watumwa wake. Alipoanza kuifanya, aliletewa mtu mmoja awiwaye talanta elfu kumi. Naye alipokosa cha kulipa, bwana wake akaamuru auzwe, yeye na mkewe na watoto wake, na vitu vyote alivyo navyo, akalipwe ile deni. Basi yule mtumwa akaanguka, akamsujudia akisema, Bwana, nivumilie, nami nitakulipa yote pia. Bwana wa mtumwa yule akamhurumia, akamfungua, akamsamehe ile deni. Mtumwa yule akatoka, akamwona mmoja wa wajoli wake, aliyemwia dinari mia; akamkamata, akamshika koo, akisema, Nilipe uwiwacho. Basi mjoli wake akaanguka miguuni pake, akamsihi, akisema, Nivumilie, nami nitakulipa yote pia. Lakini hakutaka, akaenda, akamtupa kifungoni, hata atakapoilipa deni. Basi wajoli wake walipoyaona yaliyotendeka, walisikitika sana, wakaenda wakamweleza bwana wao yote yaliyotendeka. Ndipo bwana wake akamwita, akamwambia, Ewe mtumwa mwovu, nalikusamehe wewe deni ile yote, uliponisihi; nawe, je! haikukupasa kumrehemu mjoli wako, kama mimi nilivyokurehemu wewe? Bwana wake akaghadhibika, akampeleka kwa watesaji, hata atakapoilipa deni ile yote. Ndiyo na Baba yangu wa mbinguni atakavyowatenda ninyi, msiposamehe kwa mioyo yenu kila mtu ndugu yake.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo
________

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MATUNDA MAZURI NA MSINGI MZURI!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumamosi, Septemba 12, 2026 
Juma la 23 la Mwaka

Kumbukumbu ya jumamosi ya Bikira Maria Mtakatifu

1 Kor 10: 14-22
Zab 115: 12-13, 17-18
Lk 6: 43-49


MATUNDA MAZURI NA MSINGI MZURI!

Yesu mara nyingi alitoa mfano kutoka katika mazingira ya asili na kuelezea thamani za Ufalme wa Mungu. Katika Injili ya leo tuna mifano ya tini na zabibu. Mtini ilikuwa ni alama ya rutuba, mafanikio na Amani. Zabibu zinatoa divai, alama ya furaha. Yesu anatumia mifano hii na anawaeleza wafuasi wake kwamba mti unajulikana kwa matunda yake. Ni katika hali hiyo hiyo pia mtu anatoa matunda mazuri au mabaya kulingana na mbegu iliyosiwa moyoni mwake. Na zaidi sana inategemea sana tabia ya mtu katika kuzaa matunda mema au mabaya. Wanaoishi na Roho wa Mungu wanazalisha matunda mema kama, furaha, Amani, uvumilivu, kujali, huruma, uaminifu, upole na kuweza kujizuia na kujiongoza (rej. Wagalatia 5: 22- 23). 

Wale waliyo waaminifu kwa Munguwanajua nguvu zao zipo mikononi mwa Mungu na sio kwao binafsi bali zipo kwa Mungu anayewapa neema tele za kuishi kama wafuasi wake wa kweli. Je nimatunda ghani unayozalisha ili kudhihirisha ulipozamisha mizizi yako? Kwa Mungu au mwili / Dunia?

Pengine tujaribu kujiuliza matendo yangu yanatoa ishara yeyote ya uwepo wa Kristo ndani yangu? Je matendo yangu yanaendana na Imani yangu? Au tunaishi tu na watu wanashindwa kufahamu sisi ni nani? Hatuwezi kujiita wafuasi wa Kristo wakati hatutendi kama Kristo au kama tunatenda tofauti na mapenzi ya Kristo. Matendo yetu na Imani yetu yaendane ili tuweze kuwa zabibu zinazo zaa zabibu na sio zabibu zinazo zaa mchongoma. Tuimarishe hazina njema ya mioyo yetu wenyewe ili iweze kutoa matunda mema kwa njia hii tutakuwa tumejenga msingi wetu katika Kristo na hivyo tutakuwa imara daima dhoruba ijapo tukitambua kwamba hata dhoruba iweje wa mwisho kutenda dhambi ni mimi mwenyewe, hakuna mtu anayemsaidia mtu kutenda dhambi, kwani dhambi huanzia ndani ya moyo wa mtu. Hata vingekuwepo vishawishi vya aina ghani, inabaki kwamba wa mwisho kutenda dhambi ni mtu mwenyewe. Tujenge mzingi mzuri ndani ya Yesu ili tuweze kungara kwa matunda mema.

Sala: Yesu nisaidiye niweze kuzaa matunda mema ya Imani, matumaini na upendo. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA JUMAMOSI, SEPTEMBA 12, 2026



MASOMO YA MISA 
JUMAMOSI, SEPTEMBA 12, 2026
JUMA LA 23 LA MWAKA


KUMBUKUMBU YA JUMAMOSI YA BIKIRA MARIA

SOMO 1
1Kor. 10:14 – 22

Wapenzi wangu, ikimbeni ibada ya sanamu. Nasema kama na watu wenye akili; lifikirini ninyi ninenalo. Kikombe kile cha Baraka tukibarikicho, je! Si ushirika wa damu ya Kristo? Mkate ule tuumegao, si ushirika wa mwili wa Kristo? Mkate ule tuumegao, si ushirika wa mwili wa Kristo? Kwa kuwa mkate ni mmoja, sisi tulio wengi tu mwili mmoja; kwa maana sisi sote twapokea sehemu ya ule mkate mmoja. Waangalieni hao waisraeli walivyokuwa kwa jinsi ya mwili; wale wazilao dhabihu, je! Hawana shirika na madhabahu?

Basi niseme nini? Ya kwamba kile kilicholewa sadaka kwa sanamu ni kitu? Au ya kwamba sanamu ni kitu? Sivyo, lakini vitu vile wavitoavyo sadaka wavitoa kwa mashetani, wala si kwa Mungu; nami sipendi ninyi kushirikiana na mashetani. Hamwezi kunywea kikombe cha Bwana na kikombe cha mashetani. Hamwezi kushirikiana katika meza ya Bwana na katika meza ya mashetani. Au twamtia Bwana wivu? Je! Tuna nguvu zaidi ya yeye?

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 116:12 – 13, 17 – 18 (K) 17

(K) Nitakutolea dhabihu ya kushukuru, Ee Bwana.

Nimrudishie Bwana nini
Kwa ukarimu wake wote alionitendea?
Nitakipokea kikombe cha wokovu;
Na kulitangaza jina la Bwana. (K)

Nitalitangaza jina la Bwana;
Nitaziondoa nadhiri zangu kwa Bwana,
Naam, mbele ya watu wake wote.
Katika nyua za nyumba ya Bwana,
Ndani yako, Ee Yerusalemu. (K)


SHANGILIO
Yn. 8:12

Aleluya, aleluya,
Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, 
asema Bwana, yeye anifuataye 
hatakwenda gizani kamwe, 
bali atakuwa na nuru ya uzima.
Aleluya.


INJILI
Lk. 6:43 – 49

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Hakuna mti mzuri uzaao matunda mabaya, wala mti mbaya uzaao matunda mazuri; kwa kuwa kila mti hutambulikana kwa matunda yake; maana, katika miiba hawachumi tini, wala katika michongoma hawachumi zabibu. Mtu mwema katika hazina njema ya moyo wake hutoa yaliyo mema, na mtu mwovu katika hazina mbovu ya moyo wake hutoa yaliyo maovu; kwa kuwa mtu, kinywa chake hunena yale yaujazayo moyo wake.

Na kwa nini mnaniita, Bwana, walakini hamtendi nisemayo?

Kila mtu ajaye kwangu, na kuyasikia maneno yangu na kuyatenda, nitawaonyesha mfano wake. Mfano wake ni mtu ajengaye nyumba, na kuchimba chini sana, na kuweka msingi juu ya mwamba; na kulipokuja gharika, mto uliishukia nyumba ile kwa nguvu, usiweze kuitikisa; kwa kuwa imejengwa vizuri. Lakini yule aliyesikia ila hakutenda, mfano wake ni mtu aliyejenga nyumba juu ya ardhi pasipokuwa na msingi, mto ukaishukia kwa nguvu, ikaanguka mara; na maangamizi yake nyumba yakawa makubwa.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.