Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

AMRI KUU



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Ijumaa, Agosti 21, 2026 
Juma la 20 la Mwaka 


Eze 37: 1-14; 
Zab 107: 2-9; 
Mt 22: 34-40


AMRI KUU


Injili ya leo inatualika tutafakari njia iliyo kuu ambayo kila mfuasi wa Kristo inapaswa kuwa msingi wake. Upendo kwa Mungu na upendo kwa jirani. Kwanza kabisa upendo kwa Mungu ni kushuhudia na kukiri upendo wa Mungu kwetu sisi. Sisi ni dhaifu sana na tunashindwa kumpenda Mungu kama inavyotupasa. Lakini ndani ya Yesu tunahisi upendo wa Mungu kwetu. Kwahiyo, kuhisi upendo wa Mungu, licha ya upweke wa mtu mwenyewe inamfanya mtu ampende Mungu kama matokeo ya kuhisi upendo huo. Huu ndio mwanzo wa kumpenda Mungu. Wakati mtoto anavyohisi upendo wa Mama, hafanyi kitu kinyume na Mama. Hii ndio maana ya kumpenda Mungu. Tukihisi upendo wa Mungu hatutafanya mambo kinyume na Mungu, hatujiingiza kwenye dhambi, bali tutafanya yote yenye kumpendeza. 

Inamfurahisha Mungu tukiwapenda wengine. Kwahiyo, wakati mtu anampenda Mungu, anaanza kumpenda jirani pia. Je, ni muda ghani upendo wangu juu ya jirani unapokuwa kamilifu? Tunapowapenda ndugu zetu tunakuwa tunatamani na wao kila wakati wawe washiriki kwenye uzima wa milele. Tunakuwa tunatamani na kuomba kwamba waishi maisha yao yote katika neema. Kwahiyo wanakuwa washiriki wa uzima wa milele zawadi tuliopewa na Yesu. Tunakumbuka alichosema Yesu ‘mlicho watendea wadogo hawa mme mtendea yeye’. Tutoke njee ya nafsi zetu, tuweze kukutana na watu waliowahitaji, tuwasaidie kadiri ya uwezo wetu. Huu ndio upendo kwa jirani zetu. 

Sala: Bwana nisaidiye niweze kukupenda wewe ili niweze kuwapenda wengine. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA IJUMAA, AGOSTI 21, 2026




MASOMO YA MISA, IJUMAA, AGOSTI 21, 2026
JUMA LA 20 LA MWAKA


SOMO 1
Eze. 37:1 – 14

Mkono wa Bwana ulikuwa juu yangu, naye akanichukua nje katika roho ya Bwana, akaniweka chini, katikati ya bonde; nalo limejaa mifupa; akanipitisha karibu nayo pande zote; na tazama, palikuwa na mifupa mingi katika ule uwanda! Nayo, tazama, ilikuwa mikavu sana.

Akaniambia, Mwanadamu, je! Mifupa hii yaweza kuishi? Nami nikajibu, Ee Bwana Mungu, wajua wewe. Akaniambia tena, Toa unabii juu ya mifupa hii, uiambie, Enyi mifupa mikavu, lisikieni neno la Bwana. Bwana Mungu aiambia mifupa hii maneno haya; Tazama, nitatia pumzi ndani yenu, nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana.

Basi nikatoa unabii kama nilivyoamriwa; hata nilipokuwa nikitoa unabii, palikuwa na mshindo mkuu; na tazama, teteme3ko la nchi, na ile mifupa ikasogeleana, mfupa kwa mfupa mwenziwe. Nikatazama, kumbe! Kulikuwa na mishipa juu yake, nyama ikatokea juu yake, ngozi ikaifunika juu yake, lakini haikuwamo pumzi ndani yake. Ndipo akaniambia, Tabiri, utabirie upepo, mwanadamu, ukauambie upepo, Bwana Mungu asema hivi; Njoo, kutoka pande za pepo nne, Ee pumzi, ukawapuzie hawa waliouawa, wapate kuishi. Basi nikatabiri kama alivyoiamuru; pumzi ikawaingia, wakaishi, wakasimama kwa miguu yao, jeshi kubwa mno.

Kisha akaniambia, Mwanadamu, mifupa hii ni nyumba yote ya Israeli; tazama, wao husema, Mifupa yetu imekauka, matumaini yetu yametupotea; tumekatiliwa mbali kabisa. Basi tabiri, uwaambie Bwana Mungu asema hivi; Tazama, nitafunua makaburi yenu, na kuwapandisha kutoka katika makaburi yenu, enyi watu wangu, nami nitawaingizeni katika nchi ya Israeli. Nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, nitakapoyafunua makaburi yenu, na kuwatoa ninyi katika makaburi yenu, enyi watu wangu. Nami nitatia roho yangu ndani yenu, nanyi mtaishi, nami nitawawekeni katika nchi yenu, nanyi mtajua ya kuwa mimi, Bwana, nimesema hayo, na kuyatimiza asema Bwana.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 107:1 – 9 (K) 1

(K) Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema, kwa maana fadhili zake ni za milele.

Waseme hivi waliokombolewa na Bwana,
Wale waliowakomboa na mkono wa mtesi.
Akawakusanya kutoka nchi zote,
Mashariki na magharibi, kaskazini na kusini. (K)

Walitanga-tanga jangwani katika njia ya nyika;
Hawakuona mji wa kukaa.
Waliona njaa, waliona na kiu,
Nafsi yao ilikuwa ikizimia ndani yao. (K)

Wakamlilia Bwana katika dhiki zao,
Akawaponya na shida zao.
Akawaongoza kwa njia ya kunyoka,
Wapate kwenda mpaka mji wa kukaa.(K)

Na wamshukuru Bwana kwa fadhili zake,
Na maajabu yake kwa wanadamu.
Maana hushibisha nafsi yenye shauku,
Na nafsi yenye njaa huijaza mema. (K)


SHANGILIO
Zab. 111:7, 8

Aleluya, aleluya,
Maagizo yako yote, ee Bwana, 
ni amini, yamethibitika milele na milele.
Aleluya.


INJILI
Mt. 22:34 – 40

Mafarisayo waliposikia ya kwamba amewafumba kinywa wale Masadukayo, walifanya shauri pamoja. Mmoja wao, mwana-sheria, akamwuliza, akimjaribu; Mwalimu, katika torati ni amri ipi iliyo kuu? Akamwambia, Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote. Hii ndiyo amri kuu, tena ni ya kwanza. Na ya pili yafanana nayo, ni hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Katika amri hizi mbili hutegemea torati yote na manabii.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

SHEREHE YA HARUSI!


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Alhamisi, Agosti 20, 2026, 
Juma la 20 la Mwaka 

Eze 36:23-28; 
Zab 50:12-15, 18-19; 
Mt 22:1-14


SHEREHE YA HARUSI!

Inafarijisha sana, kufikiri mbinguni kama sehemu ya sherehe ya harusi/karamuni. Itakuwa Yesu aliipenda sherehe ya harusi na akaona ni kielelezo/mfano mzuri wa kutueleza sisi alicho tuandalia Mungu. 

Katika somo la injili, mfalme anashangazwa kwamba ameandaa sherehe kubwa ya harusi ya mtoto wake lakini wageni walioalikwa hawana muda wakuhudhuria karamu hiyo. Kuna mambo mengi katika mfano huu. Kwa hakika cha kwanza ni kuhusu kualikwa. Mungu anatualika na hatulazimishi anatupa uhuru. Tunaweza kukubali au kukataa. Tupo huru. Inavyoonekana alivyotendewa yule asiyevaa vazi la harusi inaweza kushangaza kidogo. Tuliangalie hili kwa ukaribu zaidi. Wakati mfalme anavyomtambua “alikaa kimya!” iko wazi kutoka kwenye somo kwamba huyu mtu hakuwa na vazi la harusi kitendo cha kukosa kuwa makini na heshima kwa mfalme. Si kwamba huyu mgeni alishindwa kuwa na vazi

Sisi tumealikwa kwenye urafiki na Mungu. Tumepewa neema ya utakaso kama zawadi, lakini ni zawadi inayohitaji kujishughulisha. Tunapaswa tuishi ujumbe wa Ukristo unaoweza kutulazimu kubadili mitizamo yetu, tabia na aina ya maisha. Huyu mtu aliyeelezwa kwenye injili hakuwa na lakusema. Hakuwa amejiandaa kuingia katika karamu. 

Mfano wa karamu unaoendana sambamba na mfano huu ni Ekaristi Takatifu- zawadi ambayo ni ya hali ya juu kabisa ambayo hatuwezi kujitetea kuwa haki yetu, zawadi tusio stahili. Je, tunamaanisha kweli maneno tunayo sema kabla ya komunyo; Ee Bwana sistahili uingie kwangu lakini sema neno tu na roho yangu itapona? Kwahiyo leo, tunaomba mfano huu, ututikise mioyo yetu nakututoa katika uvivu na hali ya kuridhika na hali yetu. Tusimchukulie Mungu kwa mizaha! Tumpende Mungu kweli tuwe tayari kutoa sadaka yote yanayotufanya tujifariji binafsi na kushindwa kujiweka tayari kwa karamu na hapo kiaminifu tuweze kusema kwa ujasiri “Kufanya mapenzi yako, Ee Mungu, ndio furaha yangu”.

Sala: Ee Mungu, ninakushukuru kwa kunialika kwenye karamu yako ya Mbinguni. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA ALHAMISI, AGOSTI 20, 2026



MASOMO YA MISA 
ALHAMISI, AGOSTI 20, 2026
JUMA LA 20 LA MWAKA


SOMO 1
Eze. 36:23 – 28

Neno la Bwana linifikia hivi: Nitalitakasa jina langu kuu, lililotiwa unajisi katika mataifa, mlilolitia unajisi kati yao; nao mataifa watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, asema Bwana Mungu, nitakapotakaswa kati yenu mbele ya macho yao. Maana nitawatwaa kati ya mataifa, nami nitawakusanya na kuwatoa katika nchi zote, na kuwarudisha katika nchi yenu wenyewe. Nami nitawanyunyizia maji safi, nayi mtakuwa safi; nitawatakaseni na uchafu wenu wote, na vinyago vyenu vyote.

Nami nitawapa ninyi moyo mpya, nami nitatia roho mpya ndani yenu, nami nitatoa moyo wa jiwe uliomo ndani ya mwili wenu, nami nitawapa moyo wa nyama. Nami nitatia rohoyangu ndani yenu, na kuwaendesha katika sheria zangu, nanyi mtazishika hukumu zangu, na kuzitenda. Nayi mtakaa katika nchi ile niliyowapa baba zenu, nanyi mtakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wenu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 51:10: - 13, 16 – 17 (K) Eze. 36:25

(K) Nitawanyunyizia maji safi, Nanyi mtakuwa safi, nitawatakaseni na uchafu wenu wote.

Ee Mungu, uniumbie moyo safi,
Uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu.
Usinitenge na uso wako,
Wala roho yako mtakatifu usiniondolee. (K)

Unirudishie furaha ya wokovu wako;
Unitegemeze kwa roho ya wepesi.
Nitawafundisha wakosaji njia zako,
Na wenye dhambi watarejea kwako. (K)

Maana hupendezwi na dhabihu, au ningeitoa,
Wewe huridhii sadaka ya kuteketezwa.
Dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika;
Moyo uliovunjika na kupondeka,
Ee Mungu, hutaudharau. (K)



SHANGILIO
Zab. 19:8

Aleluya, aleluya,
Amri ya Bwana ni safi, huyatia macho nuru.
Aleluya.



INJILI
Mt. 22:1 – 14

Yesu aliwaambia makuhani na makutano kwa mithali, akisema, Ufalme wa mbinguni umefanana na mfalme mmoja aliyemfanyia mwanawe arusi. Akawatuma watumwa waake wawaite walioalikwa kuja arusini; nao wakakataa kuja. Akatuma tena watumwa wengine, akisema, Waambieni wale walioalikwa, Tazameni, nimeandaa karamu yangu, ng’ombe zangu na vinono vimekwisha kuchinjwa, na vyote vimekuwa tayari, njoni arusi. Lakini hawakujali, wakaenda zao, mmoja shambani kwake, mmoja kwenye biashara yake; nao waliosalia wakawakamata watumwa wake, wakawatenda jeuri, na kuwaua. Basi yule mfalme akaghadhibika; akapeleka majeshi yake, akawaangamiza wauaji wale, akauteketeza mji wao.

Kisha akawaambia watumwa wake, Arusi i tayari, lakin wale walioalikwa hawakustahili. Basi enendeni hata njia panda za barabara, na wote mwaonao waiteni arusini. Watumwa wale wakatoka wakaenda njia kuu, wakakusanya wote waliowaona, waovu kwa wema; arusi ikajaa wageni.

Lakini alipoingia yule mfalme ili kuwatazama wageni wake, akaona mle mtu mmoja asiyevaa vazi la arusi. Akamwambia, Rafiki, uliingiaje humu nawe huna vazi la arusi? Naye akatekewa. Mfalme akawaambia watumishi, Mfungeni mikono na miguu, mchukueni mkamtupe katika giza la nje; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno. Kwa maana waitwao ni wengi, bali wateule ni wachache.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUWA MUWAJIBIKAJI!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatano, Agosti 19, 2026, 
Juma la 20 la Mwaka 


Eze 34:1-11; 
Zab 22:1-6; 
Mt 20:1-16


KUWA MUWAJIBIKAJI!


Neno la Mungu linaongea nasi kuhusu kuwajibika, na kwanamna ya pekee, majukumu yaliowekwa juu yetu na Mungu. Katika somo la kwanza, Mungu anawakumbusha viongozi wa wana Waisraeli kuwa wao ni wawajibikaji wa matatizo na mateso ya watu. Walichaguliwa kuongoza watu, kuendana na amri zake. Lakini, wanawaongoza katika kuvunja uhusiano wao na Mungu kwakuharibu taratibu za kidini, nakuwachanganya kati yao ili waweze kujinufaisha binafsi kifedha na kisiasa. Na hili lime sababisha uharibifu na kupelekwa uhamishoni. Ezekiel anawaeleza kuhusu kushindwa kwao kuwa wachugaji wema wa watu.

Sisi wote pia, katika hali Fulani, tumewekwa kuwa wachungaji au wahudumu juu ya wengine. Kama Padre, Mtawa, Wazazi, Walimu, viongozi wa serikali, tunapaswa kutimiza majukumu yetu yakuwahudumia watu waliowekwa chini yetu au wanao tutegemea. Somo la kwanza linatueleza kwamba watu hawa hawapo chini yetu ili kuwahujumu au kuwaonea bali ni watu wa Mungu waliowekwa chini yetu na Mungu ili tuwahudumie. Hii inamaana kwamba sisi tupo na tutabaki kuwa wawajibikaji wa Mungu.

Somo la Injili ni juu ya mfano wa wafanyakazi wa shamba la mizabibu walio ajiriwa nakufanya kazi kwa masaa tofauti bali wanapewa mshahara sawa. Kitu kimoja cha kweli ambacho mfano huu unatufunulia ni kwamba, kwakuangalia majukumu yetu aliotupa Mungu, Mungu haangalii umefanya kazi muda mrefu kiasi ghani, bali anaangalia ni kwa jinsi ghani tumetenda kazi kwa uaminifu na kwa majitoleo. Hatimaye, hata kama tuna kazi ndefu na majukumu marefu katika maisha kama ya wazazi au kama ya mwalimu anayefundisha wanafunzi kwa kipindi kifupi, tunapaswa kuwa sawa katika kuitenda hiyo kazi kiaminifu na kwa majitoleo. Na majitoleo yetu ya kujitoa kwetu kutakuwa kwa hali ya juu na hapo tutaambiwa-“njooni kwangu mliobarikiwa na Baba yangu, muurithi ufalme mliotayarishiwa kabla ya kuumbwa misingi ya ulimwengu” (Mt 25:34).

Sala: Bwana, nakuomba unisaidie niweze kuwa mchungaji mwema wa kundi lililowekwa chini yangu, niweze kutimiza majukumu yaliowekwa chini yangu. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA JUMATANO, AGOSTI 19, 2026




MASOMO YA MISA 
JUMATANO, AGOSTI 19, 2026
JUMA LA 20 LA MWAKA


SOMO 1
Eze. 34:1 – 11

Neno la Bwana likanijia, kusema, Mwanadamu, toa unabii juu ya wachungaji wa Israeli, toa unabii, uwaambie, naam, hao wachungaji, Bwana Mungu asema hivi; Ole wao wachungaji wa Israeli, wanaojilisha wenyewe; je! Haiwapasi wachungaji kuwalisha kondoo? Mnawala walionona, mnajivika manyoya, mnawachinja walionona; lakini hamwalishi kondoo. Wagonjwa hamkuwatia nguvu, wala hamkuwaponya wenye maradhi, wala hamkuwafunga waliovunjika, wala hamkuwarudisha waliofukuzwa, wala hamkuwatafuta waliopotea; bali kwa nguvu na kwa ukali mmewatawala. Nao wakatawanyika, kwa sababu hapakuwa na mchungaji; wakawa chakula cha wanyama-mwitu, wakatawanyika. Kondoo zangu walitanga-tanga katika milima yote, na juu ya kila kilima kirefu; naam, kondoo zangu walitawanyika juu ya uso wote wa dunia; wala hapakuwa na mtu aliyewaulizia, wala kuwatafuta.

Basi, enyi wachungaji, lisikieni neno la Bwana; kama mimi niishivyo, asema Bwana Mungu, kwa sababu kondoo zangu wakawa chakula cha wanyama mwitu wote, kwa sababu hapakuwa na mchungaji, wala wachungaji wangu hawakutafuta kondoo zangu, bali wachungaji walijilisha wenyewe wala hawakuwalisha kondoo zangu; kwa sababu hiyo, enyi wachungaji, lisikieni neno la Bwana.

Bwana Mungu asema hivi; Tazama, mimi ni juu ya wachungaji; nami nitawataka kondoo zangu mikononi mwao, nami nitawaachisha hiyo kazi ya kuwalisha kondoo; nao wachungaji hawatajilisha wenyewe tena; nami nitawaokoa kondoo zangu vinywani mwao, wasiwe tena chakula chao.

Maana, Bwana Mungu asema hivi; Tazama, mimi mwenyewe, naam, mimi nitawatafuta kondoo zangu, na kuwaulizia.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 23:1 – 6 (K) 1

(K) Bwana ndiye mchungaji wangu, sitapungukiwa na kitu.

Bwana ndiye mchungaji wangu,
Sitapungukiwa na kitu.
Katika malisho ya majani mabichi hunilaza,
Kando ya maji ya utulivu huniongoza. (K)

Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza
Katika njia za haki kwa ajili ya jina lake.
Naam, nijapopita kati aya bonde la uvuli wa mauti,
Sitaogopa mabaya;
Kwa maana Wewe upo pamoja nami,
Gongo lako na fimbo yako vyanifariji. (K)

Waandaa meza mbele yangu,
Machoni pa watesi wangu.
Umenipaka mafuta kichwani pangu,
Na kikombe changu kinafurika. (K)

Hakika wema na fadhili zitanifuata
Siku zote za maisha yangu;
Nami nitakaa nyumbani mwa Bwana milele. (K)


SHANGILIO
Zab. 119:34

Aleluya, aleluya,
Unifahamishe nami nitaishika sheria yako, nitaitii kwa moyo wangu wote.
Aleluya.


INJILI
Mt. 20:1–16

Yesu aliwaambia wafuasi wake: Ufalme wa mbinguni umefanana na mtu mwenye nyumba, aliyetoka alfajiri kwenda kuajiri wakulima awapeleke katika shamba lake la mizabibu. Naye alipokwisha kupatana na wakulima kuwapa kutwa dinari, aliwapeleka katika shamba lake la mizabibu. Akatoka mnamo saa tatu, akaona wengine wamesimama sokoni wasiokuwa na kazi; na hao nao akawaambia, Enendeni nanyi katika shamba langu la mizabibu, na iliyo haki nitawapa. Wakaenda.

Akatoka tena mnamo saa sita na saa kenda, akafanya vile vile. Hata kama saa kumi na moja akatoka, akauta wengine wamesimama, akawaambia, Mbona mmesimama hapa mchana kutwa bila kazi? Wakamwambia, Kwa sababu hakuna mtu aliyetuajiri. Akawaambia enendeni nanyi katika shamba la mizabibu.

Kulipokuchwa, yule bwana wa shamba akamwambia masimamizi wake, Waite wakulima, uwalipe ujira wao, ukianzia wa mwisho hata wa kwanza. Na walipokuja wale wa saa kumi na moja, walipokea kila mtu dinari. Na wale wa kwanza walipokuja, walidhani kwamba watapokea zaidi; na hao pia wakapokea kila mtu dinari.

Basi wakiisha kuipokea, wakamnung’unukia mwenye nyuma, wakisema, Hao wa mwisho wametenda kazi saa moja tu, nawe umewasawazisha na sisi tuliostahimili taabu na hari za mchana kutwa. Naye akamjibu mmoja wao, akamwambia, Rafiki, sikudhulumu; hukupatana nami kwa dinari? Chukua iliyo yako, uende zako; napenda kumpa huyu wa mwisho sawa na wewe. Si halali yangu kutumia vilivyo vyangu kama nipendavyo? Au jicho lako limekuwa ovu kwa sababu ya mimi kuwa mwema Vivyo hivyo wa mwisho watakuwa wa kwanza, na wa kwanza watakuwa wa mwisho.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUACHA YOTE NA KUMFUATA KRISTO!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumanne, Agosti 18, 2026, 
Tafakari ya kila siku
Juma la 20 la Mwaka  Kanisa

Ez 28:1-10; 
Kumb 32:26-28, 30, 35-36; 
Mt 19:23- 30


KUACHA YOTE NA KUMFUATA KRISTO!


Kilele cha mwisho kabisa cha mwanadamu ni kujua, kupenda, kumtumikia Mungu na kufurahia maisha ya milele pamoja naye daima. Na Mungu anapenda kutushirikisha uzima huu wa milele. Ni zwadi kutoka kwa Mungu. Hatuwezi kupata uzima huu kwa nguvu za kibinadamu. Tungeachiwa sisi tu, ingekuwa vigumu sana kwetu sisi kuupata. Lakini kwa neema ya Mungu yote yanawezekana. Lakini, mali na utajiri vinaonekana viashiria vinavyo hatarisha kutokuupata ufalme huu wa milele. Katika ulimwengu huu wa sasa wenye mambo mengi inakuwa vigumu kwa wengine kukwepa hili. Ni jambo kubwa la kweli “kuacha yote” lakini kubwa zaidi “kumfuata Yesu”. 

Kumfuata Yesu ni kazi yetu.katika hili linabeba ukombozi wa mwanadamu, lakini hatuwezi kumfuata kristo kama hatutaacha yote yanayotufunga tushindwe kumfuata. Nabii Ezekiel katika somo la kwanza anatoa angalisho kwa mji wa Tiro na viongozi wake waliopata mafanikio makubwa na nguvu. Wamweka ulinzi wao na Imani yao katika utajiri na mali ambavyo vimegeuka kuwa miungu yao.

Lakini Petro anasema, “tumeacha yote” sio tuu vitu vya ulimwengu, lakini pia tamaa zinazopendwa na mioyo yetu. Wanaobaki wakiwa wameshikilia baadhi ya vitu, inakuwa hawajaacha yote. Kwa nini anatoa ujumbe mkali namna hiyo kwa matajiri? Kwanini Yesu anaongea sana kuhusu mali? Ni kwasababu mali inaweza kutufanya tusiwe huru au kutupa uhuru wa uongo. Wengine wameshindwa kumfuata Yesu kwasababu ina maana ya kuacha baadhi ya uhusiano, na wengine kama yule tajiri, ni kwasababu watapoteza nafasi yao ya heshima au njia zao za kupata mali. Wewe je? 
Sala: Bwana, naomba nikufanye wewe wa kwanza katika maisha yangu na nikuchague wewe kwa uhuru kamili hata kama kukufuata inagarimu.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, AGOSTI 18, 2026



MASOMO YA MISA, AGOSTI 18, 2026
JUMANNE, JUMA LA 20 LA MWAKA

SOMO 1
Eze. 28:1 – 10

Neno la Bwana likanijia tena, kusema, Mwanadamu, mwambie mkuu wa Tiro, Bwana mungu asema hivi; Kwa kuwa moyo wako umeinuka, nawe umesema, Mimi ni mungu, nami nimeketi katika kiti cha Mungu, kati ya bahari; lakini u mwanadamu wala si Mungu, ujapokuwa umeweka moyo wako kama moyo wa Mungu. Tazama, una hekima kuliko Danieli; hapana neno la siri watu wawezalo kukuficha; kwa hekima yako na kwa fahamu zako umejipatia utajiri, nawe umepata dhahabu na fedha katika hazina zako; kwa hekima yako nyingi, na kwa biashara yako, umeongeza utajiri wako, moyo wako umeinuka kwa sababu ya utajiri wako.

Basi, kwa hiyo, Bwana Mungu asema hivi; Kwa kuwa umeweka moyo wako kama moyo wa Mungu; basi, tazama, nitaleta wageni juu yako, watu wa mataifa wenye kutisha; nao watafuta panga zao juu ya uzuri wa hekima yako, nao watautia uchafu mwangaza wako. Watakushusha hata shimoni; nawe utazidi kusema mbele yake huyo akuuaye, Mimi ni Mungu? Lakini u mwanadamu, wala si Mungu, mkononi mwake akutiaye jeraha. Utakufa kifo cha hao wasiotahiriwa, kwa mikono ya wageni; kwa maana mimi nimenena neno hili, asema Bwana Mungu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Kum. 32:26 – 28, 30, 35 – 36 (K) 39

(K) Naua Mimi, nahuisha Mimi.

Nalisema, Ningewatawanyia mbali,
Ningekomesha kumbukumbu lao kati ya wanadamu;
Isipokuwa naliogopa makamio ya adui,
Adui zao wasije wakafikiri uongo. (K)

Wasije wakasema, Mkono wetu umetukuka,
Wala Bwana hakuyafanya haya yote.
Maana hawa ni taifa wasio shauri,
Wala fahamu hamna ndani yao. (K)

Mmoja angefukuzaje watu elfu,
Wawili wangekimbizaje elfu kumi,
Kama Mwamba wao asingaliwauza,
Kama Bwana asingaliwatoa? (K)

Mmoja angefukuzaje watu elfu,
Wawili wangekimbizaje elfu kumi,
Kama Mwamba wao asingaliwauza,
Kama Bwana asingaliwatoa? (K)

Maana siku ya msiba wao imekaribia,
Na mambo yatakayowapata yatafanya haraka.
Kwa kuwa Bwana atawaamua watu wake,
Atawahurumia watumwa wake. (K)


SHANGILIO
Zab. 25:4, 5

Aleluya, aleluya,
Ee Bwana, unijulishe njia zako, unifundishe mapito yako.
Aleluya.


INJILI
Mt. 19:23 – 30

Yesu aliwaambia wanafunzi wake, Amin, nawaambieni, ya kwamba itakuwa shida tajiri kuingia katika ufalme wa mbinguni. Nawaambia tena, Ni rahisi zaidi ngamia kupenya tundu la sindano, kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu. Wanafunzi waliposikia, walishangaa mno, wakisema, Ni nani basi awezaye kuokoka? Yesu akawakazia macho, akawaambia, Kwa wanadamu hilo haliwezekani; bali kwa Mungu yote yawezekana.

Ndipo Petro akajibu, akamwambia, Tazama, sisi tumeacha vyote tukakufuata; tutapata nini basi? Yesu akawaambia, Amin, nawaambia ya kwamba ninyi mlionifuata mimi, katika ulimwengu mpya, atakapoketi Mwana wa Adamu katika kiti cha utukufu wake, ninyi nanyi mtaketi katika viti kumi na viwili, mkiwahukumu kabila kumi na mbili za Israeli. Na kila mtu aliyeacha nyumba, au ndugu wa kiume au wa kike, au baba, au mama, au watoto, au mashamba, kwa ajili ya jina langu, atapokea mara mia, na kuurithi uzima wa milele.

Lakini wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho, na walio wa mwisho watakuwa wa kwanza.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

TUNAITWA KUWA MASKINI WA ROHO



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatatu, Agosti 17, 2026
Juma la 20 la Mwaka


Ez 24: 15-24
Lumb 32:18-21;
Mt 19: 16-22


TUNAITWA KUWA MASKINI WA ROHO 

Tunaishi katika ulimwengu ambao ni rahisi kuchukuliwa na mali au vitu na hivyo kupoteza muelekeo wetu na wa wengine. Sisi twaweza kuingia katika kujali mali kuwa ndio mwisho wa kila kitu. “kama unataka kuwa mkamilifu, uza vyote ulivyo navyo na uwape maskini, na utakuwa na hazina mbinguni. Alafu, njoo unifuate”. Wakati kijana huyu mdogo alivyo sikia hivyo alihuzunika sana kwani alikua na mali nyingi. 

Yesu anawaita baadhi ya watu katika hali ya kawaida wauze vyote walivyo navyo. Na wote wale wanao tambua wito huu na kujitoa katika kuacha kushikamana na mali, wanapata uhuru mkubwa. Wito wao ni alama ya ndani ya kila mmoja wetu, wito wa ndani ambao kila mmoja wetu amepewa. Lakini kwa wengine je, Bwana anawaitaje? Ni kwa kuwa maskini wa roho. Kwa kuwa “maskni wa roho” ni katika hali hiyo Bwana alikuwa anawaalika kuachilia yote ya malimwengu na kuacha kujifungamanisha nayo, kama hawa waliofanya katika hali ya vitendo. Tofati iliopo ni kwasababu wito wa mmoja ni wa ndani na wa njee, na wengine ni kwa ndani tu. Lakini inapaswa kuwa kamili. 

Umaskini wa roho ni kwamba tunatambua Baraka tunazozipata kwa kujinasua kwa kutokushikamana na mali za ulimwengu huu. Mali sio mbaya. Lakini ni rahisi kushikwa na vitu vya ulimwengu. Mara nyingi tunakuwa na vishawishi na kufikiri kwamba kadiri tunavyokuwa na mali nyingi ndivyo tunavyokuwa na raha zaidi. Lakini sio kweli, “aliye na vingi hatosheki”. 

Tafakari leo juu ya wito ulioitiwa wa kuishi huku Ulimwenguni bila kujifunganisha na mali. Mali na vitu vingine ni ishara tu ya njee ya kukusaidia kupata uzima wa milele katika malengo ya maisha. Na hili litakuwa na maana kwamba utapata unayo hitaji na kukwepa kuwa na vingi, na hasa kukwepa kujishika na malimwengu kutoka ndani. 

Sala: Bwana, ninatamani kuacha yote yanayo nifunga. Ninajitoa kwako kama sadaka ya kiroho. Pokea yote niliyonayo na nisaidie mimi niweze ku tumia katika hali ambayo wewe mwenyewe unatamani. Katika kuachilia huko niweze kuvumbua utajiri wa kweli ulioniwekea mimi. Yesu, nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, AGOSTI 17, 2026



MASOMO YA MISA, AGOSTI 17, 2026
JUMATATU, JUMA LA 20 LA MWAKA


SOMO 1
Eze. 24:15 – 24

Neno la Bwana linanijia tena, kusema, Mwanadamu, tazama, ninakuondolea kwa pigo moja tunu, mteule wa macho yako; walakini hutaomboleza wala kulia, wala yasichuruzike machozi yako. Ugua, lakini si kwa sauti ya kusikiwa; usifanye matanga kwa ajili yake yeye aliyekufa; jipige kilemba chako, ukavae viatu vyako, wala usiifunike midomo yako, wala usile chakula cha watu.

Basi nalisema na watu asubuhi; na jioni mke wangu akafa; nami nalifanya asubuhi kama nilivyoagizwa. Watu hao wakaniambia, Je! Hutaki kutuambia maana ya mambo haya kwetu, hata umefanya kama vile ufanyavyo.

Nikawaambia, Neno la Bwana, lilinijia, kusema, Uwaambie nyumba ya Israeli, Bwana Mungu asema hivi, Angalieni, nitapatia unajisi patakatifu pangu, fahari ya uwezo wenu, mahali pa kutamaniwa na macho yenu, ambapo roho zenu zinapahurumia; na wana wenu nab inti zenu, mliowaacha nyuma wataanguka kwa upanga. Nanyi mtafanya kama mimi nilivyofanya; hamtaifunika midomo yenu, wala kula chakula cha watu. Na vilemba vyenu vitakuwa juu ya vichwa vyenu, na viatu vyenu miguuni mwenu; hamtaomboleza wala kulia; lakini mtafifia katika maovu yenu, na kuugua kila mtu pamoja na mwenziwe. Basi ndivyo Ezekieli atakavyokuwa isahra kwenu; ninyi mtatenda sawasawa na yote aliyoyatenda yeye; litakapokuja jambo hili, ndipo mtakapojua ya kuwa mimi ndimi Bwana Mungu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Kum. 32:18 – 21 (K) 18

(K) Umemsahau Mungu aliyekuzaa.

Humkumbuki Mwamba aliyekuzaa, 
Mungu aliyekuzaa umemsahau.
Bwana akaona, akawachukia,
Kwa sababu ya kukasirishwa na wanawe nab inti zake. (K)

Akasema, Nitawaficha uso wangu, 
Nitaona mwisho wao utakuwaje;
Maana, ni kizazi cha ukaidi mwingi,
Watoto wasio Imani ndani yao. (K)

Wamenitia wivu kwa kisicho Mungu;
Wamenikasirisha kwa ubatili wao;
Nami nitawatia wivu kwa wasio watu,
Nami nitawakasirisha kwa taifa lipumbaalo. (K)


SHANGILIO
1Sam. 3:9, Yn. 6:68

Aleluya, aleluya,
Nena, Bwana, kwa kuwa mtumishi wako anasikia: Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.
Aleluya.


INJILI
Mt. 19:16 - 22

Mtu mmoja alimwendea Yesu akamwambia, Mwalimu, nitende jambo gani jema, ili nipate uzima wa milele? Akamwambia, Kwani kuniuliza habari ya wema? Aliye mwema ni mmoja. Lakini ukitaka kuingia katika uzima, zishike amri. Akamwambia, Zipi? Yesu akasema, Ni hivi, Usiue, Usizini, Usiibe, Usishuhudie uongo, Waheshimu baba yako na mama yako, na, Mpende jirani yako kama nafsi yako.

Yule kijana akamwambia, Haya yote nimeyashika; nimepungukiwa na nini tena? Yesu akamwambia, Ukitaka kuwa mkamilifu, enenda ukauze ulivyo navyo, uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha njoo unifuate. Yule kijana alipolisikia neno lile, akaenda zake kwa huzuni; kwa sababu alikuwa na mali nyingi.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com