Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

NDOA-AGANO LA UPENDO!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Ijumaa, Agosti 14, 2026, 
Tafakari ya kila siku
Juma la 19 la mwaka wa Kanisa

Ez 16: 1-15, 60, 63; 
Is 12: 2-6; 
Mt 19: 3-12


NDOA-AGANO LA UPENDO!


Katika somo la Injili leo tunaona tafakari na ukweli kuhusu ndoa na maisha ya kitawa. Yesu anaeleza kuhusu kifungo cha ndoa. Mtu yeyote asitenganishe- mtu anayeongelewa hapa ni mwanamume sio mtu mwingine wa tatu kama hakimu hivi. Katika ndoa za Wayahudi ilikuwa ni mkataba, ambao mwanamume alikuwa na uwezo wakuuvunja (Kumb 24:1). Mafarisayo waliichukua sheria hii kama sheria nzuri, bali Yesu katika Injili anaielewa kama sheria iliowekwa kwa wale waliokuwa na mioyo migumu. Anawaeleza akiwarudisha kabisa mwanzoni mwa mpango wa Mungu kuhusu ndoa aliokuwa nao tangu kuumbwa kwa Ulimwengu, “Kwahiyo Mwanamume atamuacha Baba yake na Mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja’” (Mwanzo 2:24) 

Siku hizi uelewa kuhusu ndoa, talaka na maisha ya usafi wa moyo unapata maana mbali mbali. Kizazi cha sasa imewawia vigumu kuelewa kwamba ndoa ni kifungo na Agano la maisha yote. Wakati watu wanapofikiria hivyo wanaona haifai na haiwezekani na wanamua kupeana talaka kama njia rahisi tu. Kuishi katika mahusiano bila ndoa inawavutia vijana wa leo zaidi kuliko kufunga ndoa kwani wanaona ni rahisi zaidi kuachana kama maisha hayaendi. Watu wanaishi uchumba sugu miaka baada ya miaka hata wengine wamefariki wakiwa katika hali hiyo. Leo tunaalikwa tusikie ujumbe wa Yesu ambao ni changamoto kwetu. Hakuna maisha ya majaribio katika ndoa, ndoa ni agano kati ya mume na mke, na linafanyika kwa uhuru kamili wa mke na mume bila shuruti, baada ya maamuzi yao hufanya agano hilo hadharani na kuamua kuishi pamoja siku zote za maisha yao. Tofauti na hilo sio ndoa ni maisha ya dhambi na kuigiza. 

Sala: Mungu Baba yetu, tunaomba ulichokiunganisha wewe Mwanadamu asikitenganishe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, AGOSTI 14, 2026



MASOMO YA MISA, AGOSTI 14, 2026
IJUMAA, JUMA LA 19 LA MWAKA


SOMO 1
Eze. 16:59 – 63

Bwana Mungu asema hivi; Nitakutenda vile vile kama ulivyotenda, uliyekidharau kiapo kwa kulivunja agano. Walakini nitalikumbuka agano langu nililolifanya pamoja nawe, katika siku za ujana wako, nami nitaweka imara agano la milele pamoja nawe. Hapo ndipo utakapozikumbuka njia zako, na kutahayarika, hapo utakapowakaribisha maumbu yako, walio wakubwa wako na wadogo wako; nami nitakupa hao wawe binti zako, lakini si kwa agano lako. Nami nitaweka imara agano langu nawe; nawe utajua ya kuwa mimi ndimi Bwana; upate kukumbuka, na kufadhaika, usifumbue kinywa chako tena, kwa sababu ya aiba yako; hapo nitakapokusamehe yote uliyoyatenda, asema Bwana Mungu.

Neno la Bwana... Tumshukuru Bwana.


WIMBO WA KATIKATI
Isa. 12:2 - 6 (K) 1

(K) Hasira yako imegeukia mbali, nawe unanifariji moyo.

Tazama, Mungu ndiye wokovu wangu;
Nitatumaini wala sitaogopa;
Maana Bwana Yehova ni nguvu zangu
Na wimbo wangu;
Naye amekuwa wokovu wangu. (K)

Basi, kwa furaha mtateka maji 
Katika visima vya wokovu.
Na katika siku hiyo mtasema,
Mshukuruni Bwana, liitieni jina lake;
Yatangazeni matendo yake kati ya mataifa,
Litajeni jina lake kuwa limetukuka. (K)

Mwimbieni Bwana; kwa kuwa ametenda makuu;
Na yajulikane haya katika dunia yote.
Paza sauti, piga kelele, mwenyeji wa Sayuni;
Maana Mtakatifu wa Israeli ni mkuu kati yako. (K)


SHANGILIO
Ebr. 4:12

Aleluya, aleluya,
Kwa kupenda kwake mwenyewe, Baba alituzaa sisi kwa neno la kweli, tuwe kama limbuko la viumbe vyake.
Aleluya.


INJILI
Mt. 19:3 – 12

Mafarisayo walimwendea Yesu wakamjaribu, wakimwambia, Je! Ni halali mtu kumwacha mkewe kwa kila sababu? Akajibu, akawaambia, Hamkusoma ya kwamba yeye aliyewaumba mwanzo, aliumba mtu mume na mtu mke, akasema, Kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja? Hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe.

Wakamwambia, Jinsi gani basi Musa aliamuru kumpa hati ya talaka, na kumwacha? Akawaambia, Musa, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu, aliwapa ruhusa kuwaacha wake zenu; lakini tangu mwanzo haikuwa hivi. Nami nawambia ninyi, Kila mtu atakayemwacha mkewe, isipokuwa ni kwa sababu ya uasherati, akaoa mwingine, azini; naye amwoaye yule aliyeachwa azini.

Wanafunzi wake wakamwambia, Mambo ya mtu na mkewe yakiwa hivyo, haifai kuoa. Lakini yeye akawaambia, Si wote wawezao kulipokea neno hili, ila wale waliojaliwa. Maana wako matowashi waliozaliwa hali hiyo toka matumobni mwa mama zao; tena wak omatowashi waliofanywa na watu kuwa matowashi; tena wako matowashi waliojifanya kuwa matowashi kwa ajili ya ufalme wa mbinguni. Awezaye kulipokea neno hili, na alipokee.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MSAMAHA KATIKA MAISHA YA MKRISTO!


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Alhamisi, Agosti 13, 2026, 
Juma la 19 la Mwaka


Eze 12: 1-12; 
Zab 77: 56-59, 61-62; 
Mt 18: 21-19:1


MSAMAHA KATIKA MAISHA YA MKRISTO!

Inasemwa kwamba kukosea ni ubinadamu lakini kusamehe ni Umungu. Kwa njia hii kusamehe imekuwa changamoto kwa mwanadamu. Katika Injili, jibu la Yesu lipo tofauti na mawazo aliyokuwa akiwaza Petro, kwamba kusamehe hakuna kikomo. Inapaswa kuendelea na kuwa hali halisi katika maisha ya mtu. 

Msamaha hautufanyi dhaifu, wajinga, kudhalilika, au wasio na thamani. Bali unatualika katika hali ya juu kabisa ya kuishi. Kwanza kabisa maisha ya Bwana yalikuwa maisha ya msamaha. Aliwasamehe wafuasi wake na adui zake. Zaidi sana, anatusamehe sisi na wale waliotukosea. Kwahiyo, huwa tunamuomba kila tusalipo sala ya Baba yetu, “atusamehe dhambi zetu kama tunavyo wasamehe waliotukosea”. Ulimwengu hauwezi kusitawi kama tutatafuta tu haki. Hamna Amani kama hamna haki kadhalika hamna haki kama hamna msamaha.

Ya pili, msamaha si sawa na kusahau; bali msamaha ni sawa na utakatifu. Msamaha hauwezekani bila neema ya Mungu. Naweza tu kuwasamehe adui zangu kama kuna neema ya Mungu ndani mwangu-maisha binafsi ya kuhisi msamaha wa Mungu ndani mwangu, na ile hamu ya kuwasamehe walionikosea. Kwahiyo, ninaposamehe sisahau kile alichofanya Mungu kwangu. 

Na mwisho kabisa, kusamehe sio ubinadamu, ni Ukristo. Leo, Yesu anatualika tufuate hatua alisowafundisha wafuasi wake: ongea na Baba kwanza, ungama sehemu yako, kabiliana na tatizo lenyewe sio kumshambulia mtu, ona huruma na wengine na kuwa muelewa, na baadae chukua hatua ya kuonana na aliyekukosea. Hakuna hatua rahisi katika msamaha. Yesu hakusema itakuwa rahisi katika kumfuata. Msamaha unatupa changamoto sisi wote. Lakini hiki ndicho kinacho tutambulisha sisi na Yesu. Tumuombe Yesu atupe neema yakuachia yote moyoni mwetu na kuwasamehe wote waliotukosea katika maisha yetu yote. Hata kama ni kosa kubwa kiasi ghani, tuachie yote ili Mungu aendelee kutusamehe na sisi na kutupatia Baraka zake.

Sala: Bwana nisaidie niweze kuwasamehe ndugu zangu wote. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA - AGOSTI 13, 2026



MASOMO YA MISA 
ALHAMISI, AGOSTI 13, 2026
JUMA LA 19 LA MWAKA


SOMO 1
Eze. 12:1 – 12

Neno la Bwana likanijia tena, kusema, Mwanadamu, wewe unakaa katika ya nyumba iliyoasi, watu ambao wana macho ya kuona, ila hawaoni, wana masikio ya kusikia, ila hawasikii; kwa maana ni nyumba iliyoasi. Basi, mwanadamu, funga tayari vyombo kwa uhamisho, ukahame wakati wa mchana mbele ya macho yao; nawe utahama toka mahali pako hapa mpka mahaoli pengine mbele ya macho yao; labda watafahamu, wajapokuwa ni nyumba iliyoasi. Nawe ukatoa vyombo vyako, wakati wa mchana, mbele ya macho yao, kana kwamba ni vyombo vya kuhamishwa; nawe mwenyewe utatoka, wakati wa jioni, mbele ya macho yao, kama watu watokavyo katika kuhamishwa. Toboa mahali ukutani mbele ya macho yao, kama watu watokavyo katika kuhamishwa. Toboa mahali ukutani mbele ya macho yao, ukachukue vitu kwa kuvipitisha pale. Mbele ya macho yao utajitwika begani pako, na kuvichukua nje gizani; utafunika uso wako, hata usiione nchi; kwa maana nimekuweka uwe ishara kwa nyumba ya Israeli.

Nikafanya vile vile kama nilivyoamriwa; nalitoa vyombo vyangu wakati wa mchana kana kwamba ni vyombo vya kuhamishwa, na wakati wa jioni nikautoboa ukuta kwa mkono wangu; nikavito agizani, nikavichukua begani, mbele ya macho yao.

Asubuhi neno la Bwana likanijia, kusema, Mwanadamu, nyumba ya Israeli, je! Nyumba ile iliyoasi, hawakukuambia, Unafanya nini wewe? Waambie Bwana Mungu asema hivi; Ufunuo huu wamhusu mkuu wa Yerusalemu, na nyumba yote ya Israeli walio kati ayo. Sema, Mimi ni ishara kwenu; kama mimi nilivyotenda, wao nao watatendwa vile vile; watahamishwa, watakwenda kufungwa. Naye mkuu aliye kati yao atachukua begani katika giza; naye atatoka kwenda zake; watatoboa mahali ukutani, wapate kuvichukua vyombo vyao nje; atafunika uso wake, kwa sababu hataiona nchi kwa macho yake.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 78:56 – 59, 61 – 62 (K) 7

(K) Usiyasahau matendo ya Mungu.

Walimjaribu Mungu Aliye juu wakamwasi.
Wala hawakuzishika shuhuda zake.
Bali walirudi nyuma, wakahaini kama baba zao;
Wakaepea kama upinde usiofaa. (K)

Wakamkasirisha kwa mahali pao pa juu,
Wakamtia wivu kwa sanamu zao,
Mungu akasikia, akaghadhibika,
Akamkataa Israeli kabisa. (K)

Akaziacha nguvu zake kutekwa,
Na fahari yake mkononi mwa mtesi.
Akawatoa watu wake wapigwe kwa upanga;
Akaughadhibikia urithi wake. (K)


SHANGILIO
Kol. 3:16, 17

Aleluya, aleluya,
Neno la Kristu likae kwa wingi ndani yenu katika hekima yote; mkimshukuru Mungu Baba kwa Yeye.

Aleluya.


INJILI
Mt. 18:21 – 19:1

Petro alimwendea Yesu akamwambia, Bwana, ndugu yangu anikose mara ngapi nami nimsamehe? Hata mara saba? Yesu akamwambia, Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini.

Kwa sababu hii ufalme wa mbinguni umefanana na mfalme mmoja aliyetaka kufanya hesabu na watumwa wake. Alipoanza kuifanya, aliletewa mtu mmoja awiwaye talanta elfu kumi. Naye alipokosa cha kulipa, bwana wake akaamuru auzwe, yeye na mkewe na watoto wake, na vitu vyote alivyo navyo, ikalipowe ile deni. Basi yule mtumwa akaanguka, akamsujudia akisema, Bwana, nivumilie, nami nitakulipa yote pia. Bwana wa mtumwa yule akamhurumia, akamfungua, akamsamehe ile deni.

Mtumwa yule akatoka, akamwona mmoja wa waojli wake akaanguka miguuni pake, akamsihi, akisema, Nivumilie, nami nitakulipa yote pia. Lakini hakutaka, akaenda, akamtupa kifungoni, hata atakapoilipa ile deni.

Basi wajoli wake walipoyaona yaliyotendeka, walisikitika sana, wakaenda wakamweleza bwana wao yote yaliyotendeka. Ndipo bwana wake akamwita akamwambia, Ewe mtumwa mwovu, nalikusamehe wewe deni ile yote, uliponisihi; nawe, je! Haikukupasa kumrehemu mjoli wako, kama mimi nilivyokurehemu wewe? Bwana wake akaghadhibika, akampeleka kwa watesaji, hata atakapoilipa deni ile yote.

Ndivyo na Baba yangu wa mbinguni atakavyowatenda ninyi, msiposamehe kwa mioyo yenu kila mtu ndugu yake. Ikawa Yesu alipomaliza maneno hayo, akatoka Galilaya akafika mipaka ya Uyahudi, ng’ambo ya Yordani.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

UJASIRI WA KUPATANA




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatano, Agosti 12, 2026, 
Juma la 19 la Mwaka


Eze 9: 1-7, 10, 18-22
Zab. 113 : 1-6 (K) 4;
Mt 18:15-20


UJASIRI WA KUPATANA


Ni mara nyingi watu wanapotukosea au wakiishi katika dhambi inayo julikana na wote, huwa tunaingia katika kulaani na kuhukumu. Inakuwa ni rahisi kuwasema. Hili ni jambo la kukosa unyenyekevu na kuruma kwa upande wetu. Huruma na unyenyekevu vitatuongoza kupenda mapatano na kusamehe. Huruma na unyenyekevu vina tatufanya sisi tuone dhambi zao kama sehemu ya kuanza kumpenda zaidi na kumtafutia msamaha licha ya kuhukumu na kulaani.

Huwa unawachukuliaje wale watu waliokukosea, hasa wewe binafsi? Yesu anatutegemea sisi kuweza kumuokoa huyo mdhambi arudi. Unapaswa kutumia muda mwingi kumrudisha katika hali ya kweli. Anza kwa kuongea ninyi kwa ninyi. Jaribu kukaribisha watu wenye hekima na wenye kupenda kufurahi wanapo waona mkifurahi pamoja. Wapo watu wasiopenda kuona watu wakifurahi pamoja. Hata hivyo unapaswa kuwasaidia na wao warudi pamoja katika jumuiya. Jumuiya ya kanisa ina nguvu sana kwani walipo kusanyingika hata watu wawili kwa jina la Mungu, yeye yupo kati yao. Nia kuu ni kuwapeleka kwenye ukweli na kutatua mambo na kufanya mambo yaende tena katika uhusiano mwema. Una waacha tu pale ambapo umefanya kila jitihada lakini wao wakachagua dhambi na kukataa ukweli. Lakini pia kitendo hiki ni kitendo cha upendo kuwasaidia waweze kuona matokeo ya dhambi au maamuzi yao.

Jaribu kutafakari leo, hivi ni nani unapaswa kusameheana naye? Pengine hujafanya tendo lolote kama vile kujishughulisha ili kuongea na muhusika kama hatua ya kwanza. Pengine unaogopa au umeamua kutupilia mbali. Omba kwa ajili ya neema, huruma , unyenyekevu ili uweze kuwakutia wote kwa jinsi Yesu anavyo penda.

Sala: Bwana, nisaidie mimi niweze kuondokana na maringo yeyote yale yanayo nifanya mimi niwe mbali na msamaha au kupatana. Nisaidie mimi niweze kusamehe hata wakati dhambi niliyo tendewa ni ndogo au kubwa. Ninaomba huruma ya moyo wako ijaze moyo wangu ili niweze kuwa na Amani. Yesu, nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.


MASOMO YA MISA JUMATANO, AGOSTI 12, 2026




MASOMO YA MISA 
JUMATANO, AGOSTI 12, 2026
JUMA LA 19 LA MWAKA


SOMO 1 
Eze 9: 1-7, 10, 18-22

Mungu alilia kwa sauti kuu masikioni mwangu, akisema, Waamuru wale wanaousimamia mji waka- ribie, kila mmoja na awe na kitu chake eha kuangamiza mkononi mwake. Na tazama, watu sita wakaja, wakitokea kwa njia ya lango la juu, lielekealo upande wa kaskazini, kila mmoja ana kitu chake cha kufisha mkononi mwake; na mtu mmoja kati yao amevaa bafta, naye ana kidau cha wino cha mwandishi kiunoni. Wakaingia, wakasimama karibu na madhabahu ya shaba. Na huo utukufu wa Bwana wa Israeli ulikuwa umepanda juu kutoka kwa kerubi, ambaye ulikuwa juu yake, mpaka kizingiti cha nyumba; akamwita mtu yule aliyekuwa amevaa bafta, mwenye kidau cha wino cha mwandishi kiunoni.

Bwana akamwambia, Pita kati ya mji, kati ya Yerusalemu, ukatie alama katika vipaji vya nyuso vya watu wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo vote yanayofanvika kati yake. Na hao wengine aliwaambia, nami nalisikia, Piteni kati ya mji nyuma yake, mkapige; jicho lenu lisiachilie, wala msione huruma; waueni kabisa, mzee, na kijana, na msichana, na watoto wachanga, na wanawake; lakini msimkaribie mtu ye vote mwenye hiyo alama; tena anzeni katika patakatifu pangu. Basi, wakaanza kwa wazee waliokuwa mbele ya nyumba. Akawaambia, Itieni nyumba unajisi, mkazijaze nyua mizoga ya hao waliouawa; haya, enendeni. Wakaenenda, wakapiga-piga katika mji.

Kisha huo utukufu wa Bwana ukatoka pale juu ya kizingiti cha nyumba, ukasimama juu ya makerubi. Nao makerubi wakainua mabawa yao, wa- kapaa juu kutoka katika dunia machoni pangu, hapo walipotoka nje, nayo magurudumu yakawa kando yao; wakasimama mahali pa kuingilia pa mlango wa upande wa mashariki wa nyumba ya Bwana; na utukufu wa Mungu wa Israeli ulikuwa juu yao. Huyu ndiye kiumbe hai niliyemwona, chini ya Mungu wa Israeli, karibu na mto Kebari; nikajua ya kuwa hao ni makerubi. Kila mmoja alikuwa na nyuso nne, na kila mmoja alikuwa na mabawa manne; na mifano ya mikono ya mwanadamu ilikuwa chini ya mabawa yao. Na mfano wa nyuso zao, ni nyuso zile zile nilizoziona karibu na mto Kebari; kuonekana kwao, na wao wenyewe; kila mmoja walikwenda mbele moja kwa moja.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 113 : 1-6 (K) 4

(K) Utukufu wa Bwana ni juu ya mbingu.

Aleluya.
Enyi watumishi wa Bwana, sifuni,
Lisifuni jina la Bwana.
Jina la Bwana lihimidiwe Tangu leo na hata milele. (K)

Toka maawio ya jua hata machweo yake 
Jina la Bwana husifiwa.
Bwana ni mkuu juu ya mataifa yote,
Na utukufu wake ni juu ya mbingu. (K)

Ni nani alive mfano wa Bwana,
Mungu wetu aketiye juu;
Anyenyekeaye kutazama,
Mbinguni na duniani? (K)


SHANGILIO

Aleluya, aleluya,
Mbegu ni neno la Mungu, anayepanda ni Kristu, atakayemkuta, ataishi milele.
Aleluya.


INJILI 
Mt. 18: 15-20

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Ndugu yake akikukosa, enenda ukamwonye, wewe na yeye peke yenu: akikusikia, umepata nduguyo. La, kama hasikii, chukua pamoja nawe tena mtu mmoja an wawili. ili kwa vinywa vya mashahidi wawili a: watatu kila neno lithibitike. Na asipowasikiliza wao, liambie kanisa; na asipolisikiliza kanisa pia. na awe kwako kama mtu wa mataifa na mtoza ushuru.

Amin, nawaambieni, yo yote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni; na yo yote mtakayoyafungua duniani yatakuwa yamefunguliwa mbinguni.

Tena nawaambia, ya kwamba wawili wenu watakapopatana duniani katika jambo lo lote wata kaloliomba, watafanyiwa na Baba yangu alive mbinguni. Kwa kuwa walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo


Copyright © 2026 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

NINANI MKUBWA KATIKA UFALME WA MUNGU?




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumanne, Agosti 11, 2026,
Tafakari ya kila siku 
Juma la 19 la Mwaka  wa Kanisa

Ez 2:8 -3:4; 
Zab 119:14, 24, 72, 103, 111, 131; 
Mt 18: 1-5, 10, 12-14


NINANI MKUBWA KATIKA UFALME WA MUNGU?


Kuna video katika mitandao inayohusu Matt Woodrum, ambayo inabeba jina la “Kijana mlemavu awavutia wengi nyakati za mwisho”. Huyu kijana Matt ilikuwa vigumu kwake kutembea, lakini alishiriki katika mashindano ya kukimbia (katika mzunguko wa duara). Wakati mashindano yalipoanza wakimbiaji wote walimpita nakukimbia nakumaliza. Wakati akiwa nusu ya mzunguko wale wakimbiaji wengine walishamaliza mzunguko mwingine nakumpita. Na wakati hajamaliza mzunguko wa kwanza wote wakamaliza mizunguko yote. Lakini Matt hakuacha kuendelea kuzunguka, hata yule kiongozi wake alivyomwambia aache yeye hakuacha. Alisema anataka kumaliza. Hakujali ni sehemu ghani yeye alitaka kumaliza. Watu kwakuona moyo wake, wakamzunguka na kuanza kumpigia makofi nakusema “songa mbele, songa mbele Matt” Matt aliwafundisha wote somo. “Kushinda haimaanishi kumaliza kwa mwendo uliopangwa”

Katika somo la Injili tunaona wafuasi wa Yesu wakimuuliza; ‘ni nani aliyemkubwa katika Ufalme wa mbinguni?’ Matt, anatupa jibu, yule mdogo, mnyonge, anayeonewa, aliyekama mtoto, asiyejiweza………Wale waliojawa na elimu ya juu kabisa, matajiri na wenye mamlaka, wakialikwa kwenye sherehe kwanza wanaangalia ni nani atakuwepo ili kusimamia shughuli zake? Pia nitakuwa katika sehemu ghani kati ya waalikwa? Je nitapewa heshima ghani? Wakati kama mtoto, au mlemavu angealikwa kwa sherehe hiyo, angejisikia mwenye bahati sana kualikwa kwenye sherehe kama hiyo. Wanatambua kwakweli hawastahili kwa mwaliko huo, lakini wamealikwa na Bwana wa sherehe.

Wafuasi nao wameanguka kwenye mtego wakudhani kwamba wanastahili kwenye Ufalme wa Mungu. Kwamba ni haki yao kuwa pale, na kuwa katika nafasi ya juu kabisa. Wakati watoto hawajui hata kama watashiriki katika Ufalme huo. Wafuasi walikosa unyenyekevu, walipoteza maana ya maisha yao nakujisahau wao ni nani. Je, mimi na wewe tupo je? Je, unafikiri una haki ya kuwa katika Ufalme wa Mbinguni? Je, unasubiria sehemu ya juu kwasababu ya utume unaofanya kwaajili ya Mungu? Kama unataka kuingia katika Ufalme wa Mungu, kuwa na moyo mnyofu kama wa watoto. Tunapaswa kuwa na moyo mnyofu uliojaa unyenyekevu ili tuyapokee vyema mapenzi ya Mungu, kwa namna hii bila hata mastahili yetu, twajuaje kama Mungu hatatukaribisha kwake? Daima tuombee neema hiyo.

Sala: Bwana, fanya moyo wangu uwe mnyenyekevu na mnyoofu kama wako. Amina.



Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, AGOSTI 11, 2026





MASOMO YA MISA, AGOSTI 11, 2026
JUMANNE, JUMA LA 19 LA MWAKA

KUMBUKUMBU YA MTAKATIFU KLARA

SOMO 1
Eze. 2:8 – 3:4

Ezekieli aliisikia sauti, ikamwambia: Mwanadamu, sikia neno hili ninalokuambia; usiwe wewe mwenye kuasi kama nyumba ile yenye kuasi; funua kinywa chako, ule nikupacho. Nami nilipotazama, mkono ulinyoshwa kunielekea; na tazama, gombo la chuo lilikuwa ndani yake. Akalikunjua mbele yangu; nalo lilikuwa limeandikwa ndani na nje; ndani yake yalikuwa yameandikwa maombolezo, na vilio, na ole!

Akaniambia, Mwanadamu, kula uonacho; kula gombo hili, kisha enenda ukaseme na wana wa Israeli. Basi nikafunua kinywa changu, naye akanilisha lile gombo. Akaniambia, Mwanadamu, lisha tumbo lako, ulijaze tumbo lako kwa hili gombo nikupalo. Ndipo nikalila, nalo kinywani mwangu lilikuwa tamu, kama utamu wa asali.

Akaniambia, Mwanadamu, haya! Waendee wana wa Israeli, ukawaambie maneno yangu.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 119:14, 24, 72, 103, 111, 131 (K) 103

(K) Mausi yako ni matamu sana kwangu.

Nimeifurahia njia ya shuhuda zako,
Kana kwamba ni mali mengi.
Shuhuda zako nazo ndizo furaha yangu,
Na washauri wangu. (K)

Sheria ya kinywa chako ni njema kwangu,
Kuliko maelfu ya dhahabu na fedha.
Mausia yako ni matamu sana kwangu,
Kupita asali kinywani mwangu. (K)

Shuhuda zako nimezifanya urithi wa milele,
Maana ndizo changamko la moyo wangu.
Nalifunua kinywa changu nikakweta,
Maana naliyatamani maagizo yako. (K)



SHANGILIO
Yn. 17:17

Aleluya, aleluya,
Neno lako ndiyo kweli, Ee Bwana, ututakase kwa ile kweli. 
Aleluya.



INJILI
Mt. 18:1 – 5, 10 , 12, 14

Wanafunzi walimwendea Yesu wakisema, Ni nani basi aliye mkuu katika ufalme wa mbinguni? Akaita mtoto mmoja, akamweka katikati yao, akasema, Amin, nawaambia, Msipoongoka na kuwa kama vitoto, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni.

Basi, yeyote ajinyenyekeshaye mwenyewe kama mtoto huyu, huyo ndiye aliye mkuu katika ufalme wa mbinguni.

Na yeyote atakayempokea mtoto mmoja mfano wa huyu kwa jina langu, anipokea mimi.

Angalieni msidharau mmojawapo wadogo hawa; kwa maana nawaambia ya kwamba malaika zao mbinguni sikuzote huutazama uso wa Baba yangu aliye mbinguni.

Mwaonaje? Mtu akiwa na kondoo mia, mmoja akampotea, je! Hawaachi wale tisa na tisini, akaenda milimani, na kumtafuta yule aliyepotea? Vivyo hivyo haipendezwi mbele za Baba yenu aliye mbinguni kwamba mmoja wa wadogo hawa apotee.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MBEGU YA IMANI!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatatu, Agosti 10, 2026 
Juma la 19 la Mwaka wa Kanisa

Sikukuu ya Mt. Laurent, Shemasi na shahidi.

2 Kor 9: 6-10;
Zab 112: 1-2, 5-9 (K) 5;
Yn 12: 24-26.

MBEGU YA IMANI!

Yesu Kristo leo anafundisha kwa kutumia mfano wa mbegu ambao tutaelewa kwa haraka zaidi. Kwakuwa ili mbegu iweze kumea ni lazima ibadilike kutoka kwenye hali yake ya mwanzo, ipokee hewa, maji, mwanga na mazingira ambayo itairuhusu kukuwa. Kama itajiruhusu yenyewe kubadilika, hapo tutaona mizizi ikichomoza, baadae majani, alafu matawi, na baadae kuwa mti nakutoa matunda au mbegu zinazofanana na mbegu ya mwanzo iliyokufa. 

Katika historia ya Ukristo, tunaambiwa ni kwasababu ya damu ya mashahidi. Kanisa la mwanzo limekuwa na kumea katika hali hii hii kwa miaka elfu mbili iliyopita. Kwakifupi, “damu ya Mashahidi ni mbegu ya Kanisa.” Wafiadini (Mashahidi) ni wale waliouwawa kwasababu ya imani yao, na hiyo ilikuwa ni kulinda Imani yao ndani ya Yesu Kristo. Wote waliomwaga damu yao kama Mt. Laurent, wamekuwa kama mbegu iliokufa nakutoa matunda. Mashahidi walikufa wakijitahidi kutetea Imani yao ndani ya Bwana wetu Yesu Kristo, na kwa njia ya vifo vyao, watu wengi wamekuja kumuamini Kristo. Leo, Yesu anatualika kujitolea maisha yetu ili kuungama Imani yetu ndani ya Kristo. Tunapaswa kuzuia yote yasio katika mpango wa Mungu, ili tuzae matunda mema na tuweze kupokea uzima wa milele na kuwa naye daima.

Sala: Bwana, nakuomba niwe mbegu ya Imani. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, AGOSTI 10, 2026



MASOMO YA MISA, AGOSTI 10, 2026
JUMATATU , JUMA LA 19 LA MWAKA 

SIKUKUU YA MT. LAURENT

SOMO 1 
2Kor 9:6-10

Apandaye haba atavuna haba; apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu. Kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu. Na Mungu aweza kuwajaza kila neema kwa wingi, ili ninyi, mkiwa na riziki za kila namna sikuzote, mpate kuzidi sana katika kila tendo jema; kama ilivyoandikwa, Ametapanya, amewapa maskini, Haki yake yakaa milele.

Na yeye ampaye mbegu mwenye kupanda, na mkate uwe chakula, atawapa mbegu za kupanda na kuzizidisha, naye atavaongeza mazao ya haki yenu.

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 112: 1-2, 4, 9  (K) 5 

(K) Heri atendaye fadhali na kukopesha.

Heri mtu yule amchaye Bwana,
Apendezwaye sana na maagizo yake.
Wazao wake watakuwa hodari duniani;
Kizazi cha wenye adili kitabarikiwa. (K)

Nuru huwazukia wenye adili gizani;
Ana fadhili na huruma na haki. (K)

Amekirimu, na kuwapa maskini,
Haki yake yakaa milele,
Pembe yake itatukuzwa kwa utukufu. (K)


SHANGILIO
Yn 8: 12

Aleluya, aleluya,
Yeye anifuataye, asema Bwana, hatakwenda gizani kamwe, bali atakuwa na nuru ya uzima.
Aleluya.


INJILI 
Yn 12: 24-26

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi. Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele. Mtu akinitumikia, na anifuate; nami nilipo, ndipo na mtumishi wangu atakapokuwapo. Tena mtu akinitumikia, Baba atamheshimu.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com