Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

SI HAKI YAKO, BALI NI NEEMA!


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumapili, Septemba 20,  2026,
Juma la 25 la Mwaka


Isa 55: 6-9; 
Zab 144: 2-3,8-9,17-18; 
Phil 1: 20-24, 27; 
Mt 20: 1-16

SI HAKI YAKO, BALI NI NEEMA!

Liturjia ya leo inatupa hali ya kivutio kizuri sana kuhusu Mungu. Inautambia kwamba Mungu hayupo katika hali ya ubaya au ugumu kama sisi tunavyo fikiri. Yeye ni mkarimu, mwenye huruma, na mwenye kusamehe. Yeye ni mkarimu na mwingi wa huruma, hakasiriki upesi ni mwingi wa mapendo.

Sisi mara nyingi tunamtazama Mungu katika hali ya ubinadamu. Tunamfanya awe katika hali ya udogo na fikra kama za kwetu. Lakini katika somo la kwanza kutoka kitabu cha nabii Isaya, Mungu anasema “njia zangu sio njia zenu”. Waisraeli walipokuwa utumwani huko Babiloni waliteseka sana. Kwa machozi wazee wa Waisraeli waliwaelezea kizazi kilicho zaliwa huku utumwani kwa machozi jinsi hekalu lao la Yerusalemu lilivyo bomolewa, wakiwaonesha ni kwa jinsi ghani Mungu alivyo waacha. Wakimuonesha Mungu kama Mungu anaye lipa kisasi, anaye wakirimia wanaotenda mema na kuwa adhibu walio wabaya. Katika hali hii, Isaya anasema na kuwapa maneno mengine tofauti na fikra zao; njia za Mungu sio kama za wanadamu. Nabii anawaambia wabadilishe mtazamo wao kuhusu Mungu. Badili njia zote mbaya ambazo mwanadamu anaonesha kwamba Mungu anazo. “mawazo yangu sio sawa na mawazo yenu, njia zenu si sawa na njia zangu. Kama vile mbingu zilivyo mbali na nchi, ndivyo njia zangu zilivyo mbali na mawazo yenu”.

Somo la pili linabeba mistari aliyo andika Paulo akiwa gerezani kwa ajili ya watu wa Filipi. Anafikiria huhusu kifo chake lakini anakumbuka kuhusu muunganiko kamili na Kristo. Katika mistari hii anafunua hali nzuri ya moyo wake. “kwangu kuishi ni Kristo, na kufa ni faida” ni muunganiko wa hisia zake na Imani yake.

Somo la Injili linabeba simulizi kuhusu ukarimu wa Mungu, ukarimu ambao unapanda juu zaidi ya ukarimu wetu wa kibinadamu. Huu ni mfano wa ajabu kabisa . mfano huu unawafanya wasikilizaji kukasirika. Ni nini maana ya mtu kujituma na kutimiza majukumu yake yote wakati mwishoni tunakuja kulipwa sawa na wengine? Ya nini kujishughulisha siku nzima wakati wengine wanakuja saa kumi na moja jioni na kupokea mshahara sawa na wewe uliye anza saa moja asubuhi?

Ni vizuri kutambua kwamba wale waliokuwaja saa kumi na moja hawakuwa watu walio lala tu bali walikuwa watu ambao walikuwa wakitafuta kazi katika hali zote, na wala hakuwa watu wakukwepa kazi. Walikuwa katika hali ya kweli kutaka kufanya kazi. Ni kwamba hawakupata tu mtu wa kuwaajiri. Kipindi hicho sehemu ya soko ilikuwa ndio sehemu ya kutafutia ajira. Watu walienda pale, wakisubiri mtu aje na kuwaajiri. Kama mtu alihitaji watu wa kuajiri alienda tu sokoni na kupata watu, lakini ilipofika saa kumi na moja hakuna mwajiri hata mmoja aliye waajiri, lakini walikuwa tayari kufanya kazi.

Sasa kila mtu alifahamu ni nani Yesu anamuongelea katika Injili. Wale watu wa saa kumi na moja walikuwa ni wadhambi na Wayunani. Wale ambao walikuwa wakifanya kazi mchana kutwa walikuwa Waisraeli. Na shamba lilikuwa ni ufalme wa Mungu. Aliye waajiri ni Mungu. Yesu alikuwa anasema kwamba Mungu amewapa ufalme wake wadhambi na Wayunani sawa sawa na Waisraeli. Katika hali halisi Wayahudi walipinga sana. Hawakudhani kwamba ni haki, walidhani kwamba wanahitaji mshahara maalumu kwani walikuwa wakifanya kazi muda wote wamekuwa na Mungu katika maisha yao. Lakini Yesu anabadili mtazamo wao waliokuwa nao tangu kuzaliwa.

Ukarimu ni kitu pekee kilicho hitajika kwani kilifanya watu wote kupokea sawa. Iliondoa hali yao ya kujiona wema na kwamba wanahitaji ukarimu maalumu. Walidhani kwamba Mungu anapendelea. Wakidhani kwamba Mungu atawapa zaidi kwasababu ya kazi ngumu waliofanya. Yesu anaweka mtazamo mpya kwamba Mungu ni mkarimu kwa watu wote. Yesu anamuonesha Mungu kama Baba mwenye huruma. Yeye ni Baba yetu wa Mbinguni, sisi ni watoto wake. Ni wazi kwamba Baba anapaswa kuwa mkarimu kama anahitaji jina hili katika uhalisia wake. Mfano huu unonesha hali halisi kwamba Mungu ni mkarimu. Ukarimu wake upo kwa ajili ya watu wote, hata kwa wadhambi na Wayunani. Hatupaswi kumfikiria Mungu kuwa yupo kama sisi. “mawazo yangu sio sawa na mawazo yenu”, asema Bwana.

Kwa wakristo tunachopaswa kutazama sio taji au malipo, bali furaha ya kumtumikia Mungu. Sio tu kitu kizuri kufanya kazi katika shamba la Mungu, bali ni thamani kubwa, badala ya kubaki katika soko siku nzima, bila maana hali ya maisha. Kama Mungu anawaonea huruma wale ambao siku nzima wamekuwa wakitazamia kuajiriwa na kuwachukuwa na kuwapa thamani ile ile kama sisi na kuwakirimia sawa na sisi, kwanini kukasirika? Hili linatufundisha kitu. Kama tunakasirika basi tujue kwamba kuna kitu kinapungua katika maisha yetu ya kumtumikia Mungu. Kuna ubinafsi ndani mwetu, au pengine hatufanyi kazi kwa ajili ya Bwana bali tunafanya kwa ajili yetu. Au pengine, huenda hatujaacha ile tabia ya kujiona wenyewe kuwa wema na kujipa utukufu kwasababu tunatenda matendo mema.

Njia nzuri ambayo tunaweza kufanya na kuwavutia wote ni kufanya kila kitu kwa upendo. Ingawaje sio rahisi, lakini hili ndilo linalo kirimu katika hali ya ukubwa kabisa. Ni katika moyo huu tunaweza kufanya katika hali njema na haki. Kama moyo wangu haupo kwenye kazi basi mimi sina tufauti na mtumwa. Lakini kama moyo wangu upo ndani yake, inakuwa ni furaha na ninaweka jitihada yangu yote ndani ya kazi. Kufanya kazi kwa mikono tu, bila kuwa na moyo haina tofauti na mtu ambaye hana mikono. Hivyo tuvae upendo na tutambue Mungu ni mkarimu kwa watu wote na anapenda watu wote waonje huruma na ukarimu wake, Mungu hafurahii muovu kupotea bali aache njia yake na kuonja ukarimu na huruma yake. Mwenzako anavyorudi kutoka kwenye dhambi furahi na mtukuze Mungu, usinune na kuanza kutafuta njia ya kumrudisha kwenye dhambi.

Sala: Bwana, nisaidie mimi niweze kuongeza bidi katika kuishi maisha yangu ya Imani. Nisaidie mimi niweze kusikia sauti yako na wito wako wakunialika nifanye kazi katika shamba lako la neema. Ninakushukuru wewe kwasababu ya ukarimu wako na huruma yako unayotupatia kama zawadi kwetu. Yesu nakumini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUMAPILI, SEPTEMBA 20, 2026



MASOMO YA MISA, JUMAPILI, SEPTEMBA 20, 2026
JUMA LA 25 LA MWAKA 
________

MWANZO
YbS 36:15.16

Bwana asema: Mimi ni wokovu wa watu. Wakinililia katika taabu yoyote nitawasikiliza, nami nitakuwa Bwana wao milele.
________

SOMO I
Isa. 55:6 – 9

Mtafuteni Bwana, maadamu anapatikana, Mwiteni, maadamu yu karibu; Mtu mbaya na aache njia yake, Na mtu asiye haki aache njia yake, Na mtu asiye haki aache mawazo yake; na amrudie Bwana. Naye atamrehemu; Na arejee kwa Mungu wetu, Naye atamsamehe kabisa.

Maana mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu; asema Bwana. Kwa maana kwa vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu
________

WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 145:2-3, 8-9, 17-18 (K) 18

(K) Bwana yu karibu na wote wamwitao.

Kila siku nitakuhimidi,
Nitalisifu jina lako milele na milele.
Bwana ndiye mkuu mwenye kusifiwa sana,
Wala ukuu wake hautambulikani. (K)

Bwana ana fadhili ni mwingi wa huruma,
Si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema.
Bwana ni mwema kwa watu wote;
Na rehema zake zi juu ya kazi zake zote. (K)

Bwana ni mwenye haki katika njia zake zote,
Na mwenye fadhili juu ya kazi zake zote.
Bwana yu karibu na wote wamwitao,
Wote wamwitao kwa uaminifu. (K)
________

SOMO 2 
Flp. 1:20-24, 27

Kristu ataadhimishwa katika mwili wangu; ikiwa kwa maisha yangu, au ikiwa kwa mauti yangu. Kwa maana kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida. Ila ikiwa kuishi katika mwili, kwangu mimi ni matunda ya kazi; basi nitakalolichagua silitambui.

Ninasongwa katikati ya mambo mawili; ninatamani kwenda zangu nikae na Kristo; maana ni vizuri Zaidi sana; bali kudumu katika mwili kwahitajiwa Zaidi kwa ajili yenu. Lakini mwenendo wenu na uwe kama inavyoipasa Injili ya Kristo.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu
________

SHANGILIO
Yn. 1:12, 14

Aleluya, aleluya,
Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; 
Wote waliompokea aliwapa uwezo wa 
kufanyika watoto wa Mungu.
Aleluya.
________

INJILI 
Mt. 20:1-16

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Ufalme wa mbinguni umefanana na mtu mwenye nyumba, aliyetoka alfajiri kwenda kuajiri wakulima awapeleke katika shamba lake la mizabibu. Naye alipokwisha kupatana na wakulima kuwapa kutwa dinari, aliwapeleka katika shamba lake la mizabibu. Akatoka mnamo saa tatu, akaona wengine wamesimama sokoni wasiokuwa na kazi; na hao nao akawaambia, Enendeni nanyi katika shamba langu la mizabibu, na iliyo haki nitawapa. Wakaenda. Akatoka tena mnamo saa sita na saa kenda, akafanya vile vile. Hata kama saa kumi na moja akatoka, akakuta wengine wamesimama, akawaambia, Mbona mmesimama hapa mchana kutwa bila kazi? Wakamwambia, Kwa sababu hakuna mtu aliyetuajiri. Akawaambia, enendeni nanyi katika shamba la mizabibu. Kulipokuchwa, yule bwana wa shamba akamwambia, enendeni nanyi katika shamba la mizabibu. Kulipokuchwa, yule bwana wa shamba akamwambia msimamizi wake, Waite wakulima, uwalipe ujira wao, ukianzia wa mwisho hata wa kwanza. Na walipokuja wale wa saa kumi na moja, walipokea kila mtu dinari. Na wale wa kwanza walipokuja, walidhani kwamba watapokea Zaidi; na hao pia wakapokea kila mtu dinari. Basi wakiisha kuipokea, wakamnung’unikia mwenye nyumba, wakisema, Hao wa mwisho wametenda kazi saa moja tu, nawe umewasawazisha na sisi tuliostahimili taabu na hari za mchana kutwa. Naye akamjibu mmoja wao, akamwambia, Rafiki, sikudhulumu; hukupatana nami kwa dinari? Chukua iliyo yako, uende zako; napenda kumpa huyu wa mwisho sawa na wewe. Si halali yangu kutumia vilivyo vyangu kama nipendavyo? Au jicho lako limekuwa ovu kwa sababu ya mimi kuwa mwema? Vivyo hivyo wa mwisho watakuwa wa kwanza, na wa kwanza watakuwa wa mwisho.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo
________

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

UFUFUKO: LENGO LA MAISHA YETU!


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumamosi, Septemba 19, 2026 
Juma la 24 la Mwaka


1 Kor 15: 35-37, 42-49 
Zab 55: 10-14
Lk 8: 4-15


UFUFUKO: LENGO LA MAISHA YETU!

Katika somo la kwanza Mt. Paulo anaelezea kuhusu tatizo la kutoamini ukweli wa ufufuko. Mtakatifu Paulo anaeleza wazi wazi kwamba ufufuko wa wafu ni ukweli halisi ambao imani yetu imejikita. “Kama hamna ufufuko wa wafu” anasema, “Yesu hakufufuka… na Imani yenu ni bure” (1 Kor 15: 13-14). Tunafufuliwa na mwili wa utukufu, ambao ni tofauti na mwili tunao uona. Mwili tunao uona unaisha na ni dhaifu, mwili wa utukufu hauharibiki kamwe, wenye nguvu na uliofufuliwa kwa utukufu. Hili ndilo tunalo amini kama Wakristo, tunalolitazamia kuwa na kuishi kwalo. 

Mungu amemuumba kila mtu ili aweze kuingia katika utukufu wa ufufuko ‘ili awe naye milele katika maisha ya umilele Mbinguni’. Lakini pia Injili inaelezea mfano wa jinsi wengi wetu kama mbegu tunashindwa kulipata lengo hili. Ufufuko ni zawadi, sio haki, na utapewa kwa wale walio kama mbegu zilizo anguka kwenye udongo mzuri, wanaozishika kweli amri za Bwana, “kwa unyofu na wema wa mioyo yao hulisikia neno, na kulishika; kisha huzaa matunda kwa kuvumilia.” Ni juu yetu kukubali au kukataa wema huu mkuu wa Mungu kwetu. Tutumie uhuru wetu vizuri tuweze kuchangua kuwa mbegu zuri na tulio ota katika udogo wenye rutuba. Maisha yetu yawe yanamtumainia Yesu kila siku, lakini tunapaswa kumwagilia kwa sala, kusoma neno lake, kuishi vyema na ndugu zetu, uvumilivu katika changamoto za maisha, kwa njia hiyo tutasitawa na kumea na kuzaa matunda mema daima. Na mwishowe tutazaliwa upya katika ufalme wa Mungu (ufufuko) baada ya maisha yetu hapa duniani.

Sala: Bwana, nashukuru kwa zawadi ya ufufuko. Naomba unifanye nistahili kuupokea. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA JUMAMOSI, SEPTEMBA 19, 2026



MASOMO YA MISA 
JUMAMOSI, SEPTEMBA 19, 2026
JUMA LA 24 LA MWAKA


SOMO 1
1Kor. 15:35 – 37, 42 – 49

Labda mtu atasema, Wafufuliwaje wafu? Nao huja kwa mwili gani? Ewe mpumbavu! Uipandayo haihuiki, isipokufa; nayo uipandayo, huupandi mwili ule utakaokuwa, ila chembe tupu, ikiwa ni ya ngano au nyingineyo. Kadhalika na kiyama ya wafu. Hupandwa katika uharibifu; hufufuliwa katika kutokuharibika; hupandwa katika aibu; hufufuliwa katika fahari; hupandwa katika udhaifu; hufuliwa katika nguvu; hupandwa mwili wa asili; hufufuliwa mwili war oho. Ikiwa uko mwili wa asili, na war oho pia uko. Ndivyo ilivyoandikwa, mtu wa kwanza, Adamu, akawa nafsi iliyo hai; Adamu wa mwisho ni roho yenye kuhuisha. Lakini hautangulii ule wa roho, bali ule wa asili; baadaye huja ule wa roho. Mtu wa kwanza atoka katika nchi, ni wa udongo. Mtu wa pili atoka mbinguni. Kama alivyo yeye wa udongo, ndivyo walivyo walio wa udongo; na kama alivyo yeye wa mbinguni, ndivyo walivyo walio wa mbinguni. Na kama tulivyoichukua sura yake yule wa udongo, kadhalika tutaichukua sura yake yeye aliye wa mbinguni.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 56:9 – 13

(K) Nienende mbele za Mungu katika nuru ya walio hai.

Ndipo adui zangu watarudi nyuma siku ile niitapo.
Neno hili najua kuwa Mungu yu upande wangu. (K)

Kwa msaada wa Mungu nitalisifu neno lake.
Kwa msaada wa Bwana nitalisifu neno lake.
Nimemtumaini Mungu, sitaogopa
Mwanadamu atanitenda nini? (K)

Ee Mungu, nadhiri zako zi juu yangu;
Nitakutolea dhabihu za kushukuru.
Maana umeniponya nafsi yangu na mauti;
Je! Hukuizuia miguu yangu isianguke?
Ili nienende mbele za Mungu
Katika nuru ya walio hai. (K)


SHANGILIO
2Tim. 1:10

Aleluya, aleluya,
Mwokozi wetu Yesu Kristo alibatili mauti, 
na kuufunua uzima na kutokuharibika kwa Injili.
Aleluya.


INJILI 
Lk. 8:4 – 15

Mkutano mkuu ulipokutanika, na wale waliotoka kila mji wakimjia, Yesu alisema kwa mfano: Mpanzi alitoka kwenda kupanda mbegu zake; naye alipokuwa akizipanda, nyingine zilianguka karibu na njia, zikakanyagwa, ndege wa angani wakazila. Nyingine zikaanguka penye mwamba; zilipoanza kumea zikakauka kwa kukosa rutuba. Nyingine zikaanguka kati ya miiba, na miiba ikamea pamoja nazo ikazisonga. Nyingine zikaanguka penye udongo mzuri; zikamea, zikazaa moja kwa mia. Alipokuwa akinena hayo alipaza sauti akisema, Mwenye masikio ya kusikilia, na asikie. Wanafunzi wake wakamwuliza, Maana yake nini mfano huo? Akasema, Ninyi mmepewa kuzijua siri za ufalme wa Mungu; bali wengine kwa mifano, ili wakiona wasione, na wakisikia wasielewe. Na huo mfano, maana yake ni hii; Mbegu ni neno la Mungu. Wale wa karibu na njia ndio wasikiaopo hulipokea lile neno kwa furaha; nao hawana mizizi, huamini kitambo kidogo, na wakati wa kujaribiwa hujitenga. Na zilipoanguka penye miiba ni wale waliosikia, na katika kuenenda kwao husongwa na shughuli na mali, na anasa za maisha haya, wasiivishe lolote. Na zile penye udongo mzuri, ndio wale ambao kwa unyofu na wema wa mioyo yao hulisikia neno, na kulishika; kisha huzaa matunda kwa kuvumilia.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MCHANGO WANGU KATIKA UTUME WA BWANA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Ijumaa, Septemba 20, 2026 
Juma la 24 la Mwaka


1 Kor 15: 12-20
Zab 16: 1, 6-8, 15
Lk 8: 1-3


MCHANGO WANGU KATIKA UTUME WA BWANA!

Luka anatuambia kuhusu kazi kubwa waliofanya idadi kubwa ya wanawake katika kutegemeza utume wa Bwana wetu na Wafuasi. Pamoja na tofauti zao kati ya wanawake, lakini inaonekana wote walikuwa na kitu cha pamoja kwamba: Yesu amewaponya kimiujiza kwasababu ambayo hakuna jibu sahihi kutoka kwa Mwanadamu. Katika hali ya kufikirika, kundi lililo fuatana na Yesu lilitoa ushahidi na kumtambulisha Yesu kama Kristo Masiha. Wanawake hawa hawakuwa watu wasiojitambua waliofuata tu, walikuwa watu waliokuwa hai katika kutangaza Injili ya Ufalme wa Mungu. Wakati Yesu alivyo watuma wale kumi na wawili (Lk 9: 1-6) na wale sabini na mbili (Lk 10: 1-12). Aliwaambia wasichukue chochote. Hii ni kwasababu walikuwa wafanye utume kwa wale waliowafuata, ambao kati yao waliishi miongoni mwao. Tunapaswa tuwe tunafanya walichofanya wanawake hawa. Walimpenda Yesu sana, walimtumikia yeye na wafuasi wake kwa vile walivyokuwa navyo. 

Je unadhani Yesu alihitaji msaada wao? Hapana. je, alihitaji chakula chao? Hapana. Kama Yesu angependa angeweza kuchukua tu kipande cha mkate katika mkoba, na pale watakapo hisi njaa yeye na wafuasi wake Yesu angeiongeza hata kuwa kikapu kilicho jaa. Kwanini hakufanya hivyo? Hii ni kwasababu kama kuna kitu anachopenda Yesu zaidi kuliko kuwalisha watu, ni wakati watu wanampa yeye kwasababu wanampenda. Hahitaji yote hayo, bali anapenda kupokea. Inampa furaha kubwa tukimpenda. Yesu hajapungukiwa chochote, tukimpenda na kumtumikia ni faida kwetu sisi kwamba tunampendeza Bwana, nasi tunajipatia Baraka kwa ajili ya roho zetu. Tunajua kwamba sala zetu hazi muongezei Mungu kitu, ila za faa kwa ajili ya wokovu wetu. Tumtumikie Mungu kwa uchaji katika wema na kweli ili tujipatie utakatifu wa roho zetu.

Sala: Bwana, nijalie moyo wa ukarimu. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA IJUMAA, SEPTEMBA 18, 2026





MASOMO YA MISA 
IJUMAA, SEPTEMBA 18, 2026
JUMA LA 24 LA MWAKA


SOMO 1
1Kor. 15:12 – 20

Ikiwa Kristo anahubiriwa ya kwamba amefufuka katika wafu, mbona baadhi yenu husema kwamba hakuna kiyama ya wafu? Lakini kama hakuna kiyama ya wafu, Kristo naye hakufufuka; tena kama Kristo hakufufuka, basi, kuhubiri kwenu ni bure na Imani yetu ni bure. Naam, na sisi tumeonekana kuwa mashahidi wa uongo wa Mungu; kwa maana tulimshuhudia Mungu ya kuwa alimfufua Kristo, ambaye hakumfufua, ikiwa wafu hawafufuliwi. Maana kama wafu hawafufuliwi, Kristo naye hakufufuka. Na kama Kristo hakufufuka, Imani yenu ni bure; mngalimo katika dhambi zenu. Na hapo wao nao waliolala katika Kristo wamepotea. Kama katika maisha haya tu tumemtumaini Kristo, sisi tu maskini kuliko watu wote. Lakini sasa Kristo amefufuka katika wafu, limbuko lao waliolala.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 17:1, 6 – 8, 15

(K) Nishibishwe, Ee Bwana, kwa sura yako.

Ee Bwana, usikie haki, ukisikilize kilio changu, 
Utege sikio lako kwa maombi yangu,
Yasiyotoka katika midomo ya hila. (K)

Ee Mungu, nimekuita kwa maana utaitika,
Utege sikio lako ulisikie neno langu.
Dhihirisha fadhili zako za ajabu,
Wewe uwaokoaye wanaokukimbilia;
Kwa mkono wako wa kuume
Uwaokoe nao wanaowaondokea. (K)

Unilinde kama mboni ya jicho,
Unifiche chini ya uvuli wa mbawa zako;
Bali mimi nikutazame uso wako katika haki,
Niamkapo nishibishwe kwa sura yako. (K)


SHANGILIO
Efe. 1:17, 18

Aleluya, aleluya,
Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, 
awape roho ya hekima mjue tumaini la mwito wake.
Aleluya.


INJILI
Lk. 8:1–3

Yesu alikuwa akizunguka-zunguka katika miji na vijiji akihubiri na kuitangaza habari njema ya ufalme wa Mungu; na wale Thenashara walikuwa pamoja naye, na wanawake kadha wa kadha ambao walikuwa na pepo wabaya na magonjwa wakaponywa; nao ni Mariamu aitwaye Magdalene aliyetokwa na pepo saba, na Yohana mkewe Kuza, wakili wake Herode, na Susana, na wengine wengi, waliokuwa wakimhudumia kwa mali zao.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUOMBA HURUMA



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Alhamisi, Septemba 17, 2026,
Juma la 24 la Mwaka

1Kor 15:1-11
Zab 117: 1-2, 15-17, 28;
Lk7: 36-50.

KUOMBA HURUMA

Karibuni sana ndugu zangu wapendwa kwa adhimisho la Misa Takatifu tena asubuhi ya leo. Bado tunaendelea kuongozwa na tafakari ya neno la Mungu toka katika kitabu cha waraka wa kwanza wa mtume Paulo kwa Wakorintho. Na bado anaendelea kujibu maswali na changamoto zilizoikumba ile jumuiya. Na leo anazungumzia changamoto juu ya suala la ufufuko. Wakristo wa Korintho waliishi kati ya wanafalsafa waliowakejeli juu ya suala la ufufuko baada ya wafu. Walikuwako wanafalsafa kama akina Epicureans waliosisitizia juu ya kuponda mali na anasa. Wakati huu falsafa hii ilikuwa imeshika kasi sana na hawakuamini ufufuko.

Wakristo walimtegemea Kristo aje kwa haraka ili basi awafufue wale wakristo waliokuwa wakifariki kabla ya Kristo kuja ili basi wale wanafalsafa wapate kuoneshwa kwamba walichokifundisha sio sahihi. Lakini basi Yesu hakufika kwa haraka vile walivyokuwa wakihisi na hivyo basi wakauliza je, kwa nini? Wanafalsafa hawa waliwakejeli sana wakristo na imani yao juu ya ufufuko kwa kuwaambia kwamba ni uzushi.

Lakini basi Paulo anajibu suala hili na kwa kuanza kusema kwamba kwanza suala la ufufuko ni la kweli kabisa na si la uzushi kama wanafalsafa hawa wanavyodai. Anaanza hoja yake kwa kumtaja Yesu-yeye alishuhudiwa na watu tena kati yetu akifa msalabani kabisa, akafa na akazikwa-lakini pia alishuhudiwa na baadhi yetu akiwa amefufuka tena ikiwapo mimi-sasa anawauliza-ninyi mnasemaje kuhusu hili? Ni uzushi tena? Anawaambia jamani bakini katika imani yenu-msidanganywe na hawa watu; mtumaini Kristo.

Ndivyo inavyotokea na kwetu ndugu zangu. Bado tunadanganywa na falsafa mbalimbali na kuziungamia. Tumedanganywa na mitandao mbalimbali na kupotezea muda huko kana kwamba kila kitu kisemwacho nayo ni sahihi. Tunajisikia hofu kubwa pale tunaposafiri bila simu kuliko pale tusafiripo bila hata rozari mfukoni. Tunakuwa tayari kuacha rozari au hata biblia kuliko simu-lengo ni kwamba simu itatulinda, itatuburudisha kwa kutupatia habari mbalimbali za kwenye mitandao. Tuna hofu yakukosa habari kuliko kukosa kanisani.

Kwenye somo la kwanza tunakutana na Yesu akimpinga mfarisayo aliyepinga yeye kupakwa mafuta na mama mmoja. Haya ni matendo aliyoyashindwa yule mfarisayo lakini akayaweza yule mama. Yule mama alionesha heshima kwa Yesu kuliko huyu mfarisayo. Mfarisayo aliona wivu kana kwamba yule mama alikuwa akijipatia sifa zaidi kuliko yeye. Hata majibu yake anayomueleza Yesu chanzo chake ni wivu. Anataka Yesu asitendewe uzuri kwa sababu ya wivu wake. Hata na sisi tupo hivihivi ndugu zangu. Wengi wetu tuna wivu; hatutaki wengine watendewe wema na sisi hatuko tayari kuwatendea. Tukiona wengine wakiutenda tunakasirika, ati tunataka wasifaidi? Tukiona wengine wakitendewa wema yabidi tufurahi zaidi. Kama huwezi kuutenda wema, mwingine ataweza.
------------------------
Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 17, 2026



MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 17, 2026
ALHAMISI, JUMA LA 24 LA MWAKA


SOMO 1
1Kor. 15:1 – 11

Ndugu zangu, nawaarifu ile injili niliyowahubiri; ambayo ndiyo mliyoipokea, na katika hiyo mnasimama, na kwa hiyo mnaokolewa; ikiwa mnayashika sana maneno niliyowahubiri; isipokuwa mliamini bure. Kwa maana naliwatolea ninyi hapo mwanzao yale niliyoyapokea mimi mwenyewe, ya kuwa Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu, kama yanenavyo maandiko; nay a kuwa alizikwa; nay a kuwa alifufuka siku ya tatu, kama yanenavyo maandiko; nay a kuwa alimtokea Kefa; tena na wale Thenashara; baadaye aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano pamoja; katika hao wengi wanaishi hata sasa, ila baadhi yao wamelala; baadaye akamtokea Yakobo; tena na mitume wote; na mwisho wa watu wote, alinitokea mimi, kama ni mtu aliyezaliwa si kwa wakati wake. Maana mimi ni mdogo katika mitume, nisiyestahili kuitwa mtume, kwa sababu naliliudhi kanisa la Mungu. Lakini kwa neema ya Mungu nimekuwa hivi nilivyo; na neema yake iliyo kwangu ilikuwa si bure, bali nalizidi sana kufanya kazi kupita wao wote; wala si mimi, bali ni neema ya Mungu pamoja nami. Basi, kama ni mimi, kama ni wale, ndivyo tuhubirivyo, na ndivyo mlivyoamini.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 118:1 – 2, 15 – 17, 28

(K) Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema.

Aleluya.
Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema,
Kwa maana fadhili zake ni za milele.
Israeli na aseme sasa,
Ya kwamba fadhili zake ni za milele. (K)

Mkono wa kuume wa Bwana umetukuzwa;
Mkono wa kuume wa Bwana hutenda makuu.
Sitakufa bali nitaishi,
Nami nitayasimulia matendo ya Bwana. (K)

Ndiwe Mungu wangu, nami nitakushukuru,
Ndiwe Mungu wangu, nami nitakutukuza. (K)


SHANGILIO
Kol. 3:16, 17

Aleluya, aleluya,
Neno la Kristo likae kwa wingi ndani yenu katika hekima yote, Mkimshukuru Mungu Baba kwa Yeye.
Aleluya.


INJILI
Lk. 7:36 – 50

Mtu mmoja katika Mafarisayo alimwalika Yesu ale chakula kwake; akaingia katika nyumba yake yule Farisayo, akaketi chakulani. Na tazama, mwanamke mmoja wa mji ule, aliyekuwa mwenye dhambi, alipopata habari ya kuwa ameketi chakulani katika nyumba ya yule Farisayo, alileta chupa ya marimari yenye marhamu. Akasimama nyuma karibu na miguu yake, akilia, akaanza kumdondoshea machozi yake, na kuipangusa kwa nywele za kichwa chake, akiibusu-busu miguu yake na kuipaka yale marhamu. Basi, yule Farisayo aliyemwalika alipoona vile, alisema moyoni mwake, Mtu huyu kama angekuwa nabii, angemtambua mwanamke huyu amgusaye, ni nani, naye ni wa namna gani, ya kwamba ni mwenye dhambi. Yesu akajibu akamwambia, Simoni, nina neno nitakalo kukuambia. Akasema, Mwalimu, nena. Akasema, Mtu mmoja mkopeshaji alikuwa na wadeni wawili; mmoja amwia dinari mia tano, na wa pili hamsini. Nao walipokuwa hawana cha kumlipa, aliwasamehe wote wawili. Katika hao wawili ni yupi atakayempenda zaidi? Simony akajibu akasema, Nadhani ni yule ambaye alimsamehe nyingi. Akamwambia, Umeamua haki. Akamgeukia yule mwanamke, akamwambia Simoni, Wamwona mwanamke huyu? Niliingia nyumbani kwako, hukunipa maji kwa miguu yangu; bali huyu amenidondoshea machozi miguu yangu; na hakuacha kunibusu sana miguu yangu. Hukunipa kichwa change mafuta; bali huyu amenipaka miguu yangu marhamu. Kwa ajili ya hayo nakuambia, Amesamehewa dhambi zake ambazo ni nyingi, kwa kuwa amependa sana; lakini asamehewaye kidogo, huyo hupenda kidogo. Kisha alimwambia mwanamke, Umesamehewa dhambi zako. Ndipo wale walioketi chakulani pamoja naye walianza kusema mioyoni mwao, Ni nani huyu hata asamehe dhambi? Akamwambia yule mwanamke, Imani yako imekuokoa, enenda zako kwa amani.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

KUFUNGUA MIOYO YETU KWA YESU



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatano, Septemba 16, 2026, 
Juma la 24 la Mwaka 

1 Kor 12:31 – 13:13; 
Zab 32: 2-5, 12, 22; 
Lk 7: 31-35.


KUFUNGUA MIOYO YETU KWA YESU

“Nitakifananisha na nini kizazi hiki?” Kama Yesu angeuliza swali hili hili leo katika kizazi hiki. Angetuweka wapi? Je sisi tutakuwa kama wale watoto ambao wakiwekewa muziki hawachezi hata kukiwa na maombolezo hawaombolezi? Somo la leo linatualika tuweze kuwa katika mstari mmoja na wito wa Mungu, tujitafakari wenyewe na kazi zetu ili tuweze kuwa kweli watoto wa Ufalme wa Mungu. 

Paulo katika Barua yake anatuelekeza juu ya “ni kwa jinsi gani tunapaswa kuwa katika nyumba ya Mungu”. Anawakumbusha waumini kwamba wao ni watu katika nyumba ya Mungu aliye hai, iliyodhihirishwa na Yesu, na kutangazwa na ulimwengu. Anaonesha aina Fulani ya kanuni ya Imani ambayo ilikuwa ni ishara ya Wakristo wa Mwanzo.  Kanuni hii inaonesha aina Fulani ya sifa za Yesu na matendo yake na mpango wa Mungu kwa mwanadamu kwa njia ya Yesu. 

Katika somo la Injili, Mafarisayo wanajiona wenyewe kuwa wema wanafananishwa na wale watoto wasiopenda kufanya chochote. Kama ilivyo vigumu kwa mmoja kuingia nyumba ambayo mlango wake umefungwa na madirisha kufungwa. Yesu hakuweza kuingia katika mioyo ya Mafarisayo kwasababu wameifunga na wameamua kutokuamini. Yesu na Yohane Mbatizaji walikataliwa na Mafarisayo. Injili inamalizikia kwakusema maneno haya: “Aliye na masikio na asikie” yakitutaka tuwe wasikivu na kusikiliza sauti au wito wa Yesu.  

Watoto waliokaa sokoni inatoa picha ya watu ambao muda wote wapo na mambo yao, hawana muda wa kutafakari kuhusu nafsi yao.Wanajishughulisha na biashara zao, kuwa na simu muda wote, au kukesha kwenye komputa. Maisha yetu yamejazwa na uharibifu wa kila aina. Tunajishughulisha na mambo mengi na kusahau lile la muhimu. Hali hii inatufunga sisi na kushindwa kujitambua wenyewe. 
Tutafakari leo kama maisha yetu yamekuwa ya utulivu ya kutufanya tumtambue Yesu. Je, nimekuwa msikivu kwa nafsi yangu? Je, nipo tayari kumrushusu Mungu afanye kazi katika maisha yangu? Kama sio basi fanya jitihada ya kumfuata Yesu na kustahilishwa katika ufalme Mungu. 

Sala: Bwana, ninakuomba ufungue moyo wangu. Ninakuomba nisikie sauti yako ikiniita. Yesu, nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 16, 2026




MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 16, 2026
JUMATANO, JUMA LA 24 LA MWAKA


SOMO 1
1Kor. 12:31--13:13

Takeni sana karama zilizo kuu. Hata hivyo nawaonyesha njia iliyo bora. Nijaposema kwa lugha za wanadamu na za malaika, kama sina upendo, nimekuwa shaba iliayo na upatu uvumao. Tena nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, si kitu mimi. Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu.

Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu; upendo hautakabari; haujivuni; haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni uchungu; hauhesabu mabaya; haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli; huvumilia yote; huamini yote; hutumaini yote; hustahimili yote.

Upendo haupungui neno wakati wowote; bali ukiwapo unabii utabatilika; zikiwapo lugha, zitakoma, yakiwapo maarifua, yatabatilika. Kwa maana tunafahamu kwa sehemu; na tunafanya unabii kwa sehemu; lakini ijapo ile iliyo kamili, iliyo kwa sehemu itabatilika. Nilipokuwa mtoto mchanga, nalisema kama mtoto mchanga, nalifahamu kama mtoto mchanga, nalifikiri kama mtoto mchanga; tokea hapo nilipokuwa mtu mzima, nimeyabatilisha mambo ya kitoto. Maana wakati wa sasa tunaona kwa kioo kwa jinsi ya fumbo; wakati ule tutaona uso kwa uso; wakati wa sasa nafahamu kwa sehemu; wakati wa sasa nafahamu kwa sehemu; wakati ule nitajua sana kama mimi nami ninavyojuliwa sana.

Basi, sasa inadumu imani, tumaini, upendo, haya matatu; na katika hayo lililo kuu ni upendo.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 33:2-5, 12, 22 (K) 12

(K) Heri taifa ambalo Bwana ni Mungu wao.

Mshukuruni Bwana kwa kinubi,
Kwa kinanda cha nyuzi kumi mwimbieni sifa.
Mwimbieni wimbo mpya,
Pigeni kwa ustadi kwa sauti ya shangwe. (K)

Kwa kuwa neno la Bwana lina adili,
Na kazi yake yote huitenda kwa uaminfu.
Huzipenda haki na hukumu,
Nchi imejaa fadhili za Bwana. (K)

Heri taifa ambalo Bwana ni Mungu wao,
Watu aliowachagua kuwa urithi wake.
Ee Bwana, fadhili zako zikae nasi,
Kama vile tulivyokungoja Wewe. (K)



SHANGILIO
Efe. 1:17, 18

Aleluya, aleluya,
Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, awape roho ya hekima mjue tumaini la mwito wake.
Aleluya.



INJILI
Lk. 7:31-35

Yesu aliwaambia makutano: Niwafananishe na nini watu wa kizazi hiki? Nao wamefanana na nini? Wamefanana na watoto walioketi sokoni na kuitana, wakisema, Tuliwapigia filimbi wala hamkucheza; tuliomboleza, wala hamkulia.

Kwa kuwa Yohane Mbatizaji alikuja, hali mkate wala hanywi divai, nanyi mwasema, Ana pepo. Mwana wa Adamu amekuja, anakula na kunywa; nanyi mwasema, Tazama, mlafi huyu, na mnywaji wa divai, rafiki wao watoza ushuru na wenye dhambi. Na hekima imejulikana huwa ina haki kwa watoto wake wote.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com