Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MASOMO YA MISA JUMAPILI, AGOSTI 2, 2026




MASOMO YA MISA 
JUMAPILI, AGOSTI 2, 2026
DOMINIKA YA 18 YA MWAKA



SOMO 1
ISA 55:1-3

Haya, kila aonaye kiu, njoni majini, 
Naye asiye na fedha; njoni, nunueni mle; 
Naam, njoni, nunueni divai na maziwa, 
Bila fedha na bila thamani.
Kwani kutoa fedha kwa ajili ya kitu ambacho si chakula? 
Na mapato yenu kwa kitu kisichoshibisha? 
Nisikilizeni kwa bidii, mle kilicho chema, 
Na kujifurahisha nafsi zenu kwa unono.
Tegeni masikio yenu, na kunijia; 
Sikieni, na nafsi zenu zitaishi; 
Nami nitafanya nanyi agano la milele, 
Naam, rehema za Daudi zilizo imara.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 145:8-9,15-18

(K) Bwana waufumbua mkono wako, Wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.


BWANA ana fadhili, ni mwingi wa huruma, 
Si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema,
BWANA ni mwema kwa watu wote, 
Na rehema zake zi juu ya kazi zake zote. (K)

Macho ya watu wote yakuelekea Wewe, 
Nawe huwapa chakula chao wakati wake.
Waufumbua mkono wako, 
Wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake. (K)

BWANA ni mwenye haki katika njia zake zote, 
Na mwenye fadhili juu ya kazi zake zote.
BWANA yu karibu na wote wamwitao, 
Wote wamwitao kwa uaminifu. (K)


SOMO 2
RUMI  8:35,37-39

Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! Ni dhiki au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga?

Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda.

Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


SHANGILIO
Mt. 4:4

Aleluya, aleluya,
Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.
Aleluya.


INJILI
MT 14:13-21

Naye Yesu aliposikia; hayo, aliondoka huko katika chombo, akaenda mahali pasipo watu, faraghani. Na makutano waliposikia, walimfuata kwa miguu kutoka mijini mwao.

Yesu akatoka, akaona mkutano mkuu, akawahurumia, akawaponya wagonjwa wao.

Hata kulipokuwa jioni, wanafunzi wake walimwendea, wakasema, Mahali hapa ni nyika tupu, na saa imekwisha pita; uwaage makutano, waende zao vijijini, wakajinunulie vyakula.

Yesu akawaambia, Hawana haja kwenda zao, wapeni ninyi vyakula.
Wakamwambia, Hamna kitu hapa ila mikate mitano na samaki wawili.

Akasema, Nileteeni hapa.

Akawaagiza makutano waketi katika majani; akaitwaa ile mikate mitano na wale samaki wawili, akatazama juu mbinguni, akabariki, akaimega ile mikate, akawapa wanafunzi, wanafunzi wakawapa makutano.

Wakala wote wakashiba; wakayaokota masazo ya vipande vya mikate, vikapu kumi na viwili, vimejaa.

Nao waliokula walikuwa wanaume wapata elfu tano, bila wanawake na watoto.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo

Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com. 

UCHAGUZI SAHIHI!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumamosi, Agosti 1, 2026
Tafakari ya kila siku
Juma la 17 la Mwaka wa Kanisa


Yer 26: 11-16, 24; 
Zab 69: 14-15, 29-30, 32-33; 
Mt 14: 1-12


UCHAGUZI SAHIHI!

Masomo ya leo yanahusu mateso ya watumishi wa Mungu. Yeremia aliteseka, huku Yohane anauwawa kwasababu ambazo zina uoga ndani yake. Tuangalie tabia za Herode na Herodia ambao wanahusika na kifo cha Yohane Mbatizaji. Herode alikuwa mtu wa ulimwengu. Aliishi pia kwa hofu na woga. Pengine Herode alikuwa na vingi vya kunywa katika siku yake ya kuzaliwa mpaka akatoa ahadi ambayo hakufikiri sana, ambayo mke wake Herodia alipata nafasi wa kutimiza nia yake ovu. Herode anafanya kitu bila kufikiri ili kumfurahisha mke wake. Mtu wa majivuno, Herode anaamuru Yohane akatwe kichwa na akapewa mkewe. Ni ajabu Herodia hata dhamiri yake haikuwa na wasi wasi katika kutenda uovu wake kwa kumshauri mwanaye aombe jambo baya. 

Pengine sisi kama wazazi tunawashauri watoto wetu watende matendo ghani? Pengine wakituletea fedha au mali ambazo kwa hakika unatambua sio halali tunawashaurije, tunajaribu hata kuchunguza kapata wapi pengine kuendana nahali yake ilivyo? Je! pengine tumezoea kutenda maovu kiasi kwamba dhamiri zetu hazitushtaki tena? Lugha tunazotumia, hatuhalalishi lugha mbaya nakuchukulia tu hali ya kawaida? Je tunamkumbuka Mungu tunapofurahi au tunapopatwa na mateso au tunaamua tuu maamuzi yetu bila kujali amri za Mungu kama Herode? Je tunalinda uhai wa binadamu wenzetu? Tunatambua kwamba uhai wa kila mtu ni zawaidi ya pekee kwa Mungu? Je, tunawaua wenzetu kwakuwasema vibaya na kuharibu utu wao, kiasi kwamba wanashindwa kueleweka na jamii?

Ujumbe wetu leo ni kwamba tujiulize tunakabilianaje na maswala ya maadali tunayokumbana nayo. Je tunafikiria kuhusu uovu wetu na kujaribu kuwafanya wengine wafanye hayo hayo, tukiwaambia wafanye ni mazuri ili sisi wenyewe tufiche uovu wetu? Kitu chema kinatoka kwenye kitu chema. Huwezi kutenda dhambi utegemee neema. Tubadili mienendo yetu tuishi kadiri atakavyo Mungu. 

Sala: Ee Roho Mtakatifu angaza giza la moyo na akili yangu ili kila wakati niweze kuchagua lililo jema na unipe nguvu ya kuishi kadiri ya hilo jema. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, AGOSTI 1, 2026




MASOMO YA MISA, AGOSTI 1, 2026
JUMAMOSI , JUMA LA 17 LA MWAKA


SOMO 1
Yer. 26:11 – 16, 24

Makuhani, na manabii, waliwaambia wakuu na watu wote, wakisema, Mtu huyu amestahili kufa, kwa sababu ametabiri juu ya mji huu, kama mlivyosikia kwa masikio yenu. Ndipo Yeremia akawaambia wakuu wote na watu wote, akisema, Bwana ndiye aliyenituma kuitabiri juu ya nyumba hii, na juu ya mji huu, maneno hayo yote mliyoyasikia. Basi sisi, tengenezeni njia zenu, na matendo yenu, mkaisikilize sauti ya Bwana, Mungu wenu; naye Bwana atayaghairi mabaya aliyoyanena juu yenu. Lakini kwangu mimi, tazama, mimi nipo hapa mikononi mwenu; nitendeni myaonayo kuwa mema na haki mbele ya macho yenu. Lakini jueni yakini ya kuwa, mkiniua, mtajiletea juu yenu damu isiyo na hatia; itakuwa juu yenu, na juu ya mji huu, na juu ya wenyeji wake; kwa maana ni kweli Bwana amenituma kwenu, kuwaambieni yote mliyoyasikia.

Ndipo wakuu na watu wote wakawaambia makuhani, na manabii, wakisema, Mtu huyu hastahili kuuawa; kwa maana amesema nasi katika jina la Bwana, mungu wetu. Mkono wa Ahikamu, mwana wa Shafani, ulikuwa pamoja na Yeremia, wasimtie katika mikono ya watu auawe.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 69:14 – 15, 29 – 30, 32 – 33 (K) 14

(K) Kwa wingi wa fadhili zako unijibu, Ee Mungu.

Uniponye kwa kunitoa matopeni,
Wala usiniache nikazama.
Na niponywe nao wanaonichukia,
Na katika vilindi vya maji.
Mkondo usinigharikishe, wala vilindi visinimeze,
Wala shimo lisifumbe kinywa chake juu yangu. (K)

Nami niliye maskini na mtu wa huzuni.
Mungu, wokovu wako utaniinua.
Nitalisifu jina la Mungu kwa wimbo,
Nami nitamtukuza kwa shukrani. (K)

Walioonewa watakapoona watafurahi, 
Enyi mmtafutao Mungu, mioyo yenu ihuishwe.
Kwa kuwa Bwana huwasikia wahitaji,
Wala hawadharau wafunga wake. (K)


SHANGILIO
Zab. 119:18

Aleluya, aleluya,
Unifumbue macho yangu niyatazame maajabu yatokayo katika sheria yako.
Aleluya.


INJILI
Mt. 14:1 – 12

Mfalme Herode alisikia habari za Yesu, akawaambia watumishi wake, Huyo ndiye Yohane Mbatizaji; amefufuka katika wafu; na kwa hiyo nguvu hizo zinatenda kazi ndani yake.

Maana Herode alikuwa amemkamata Yohane, akamfunga, akamtia gerezani, kwa ajili ya Herodia, mke wa Filipo nduguye. Kwa sababu Yohane alimwambia, Si halali kwako kuwa naye. Naye alipotaka kumwua, aliwaogopa watu, maana walimwona Yohane kuwa nabii. Hata ilipofika sikukuu ya kuzaliwa kwake Herode, binti Herodia alicheza mbele ya watu, akampendeza Heorode. Hata akaahidi kwa kiapo ya kwamba atampa lolote atakaloliomba. Naye, huku akichochewa na mamaye, akasema, nipe hapa katika kombe kichwa cha Yohane Mbatizaji.

Naye mfalme akasikitika; lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya wale walioketi chakulani pamoja naye, akaamuru apewe; akatuma mtu akamkata kichwa Yohane mle gerezani. Kichwa chake kikaletwa katika kombe, akapewa yule kijana; akakichukua kwa mamaye. Wanafunzi wake wakaenda, wakamchukua yule maiti, wakamzika; kisha wakaenda wakampasha Yesu habari.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

UDONGO WENYE RUTUBA ILI KUPOKEA BARAKA ZA MUNGU



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Ijumaa, Julai 31, 2026
Juma la 17 la Mwaka wa Kanisa

Yer 26: 1-9;
Zab 68: 5, 8-10, 14;
Mt. 13: 54-58.


UDONGO WENYE RUTUBA ILI KUPOKEA BARAKA ZA MUNGU


Yesu anaenda katika mji wa nyumbani kwake na kuhubiri habari njema lakini anakutana na upinzani wakutokukaribishwa kutoka kwa watu wake. Sio kwamba walikataa tu mafundisho yake na miujiza yake bali walitoa hukumu ambayo ni ya ajabu tena wakiangalia familia yake. “Je, huyu sio Mwana wa seremala? Mama yake sio Mariam”. Walimtazama kama mtu wa kawaida. Na hivyo wakazuia utukufu wa Mungu unaokuja kati yao. 

Ujumbe huu wa Injili unatufundisha kwamba tunapaswa kuwa tayari kujifunza kwa wengine, hasa wale wanaofahamu hata kama tunawafahamu familia yao au tunamfahamu. Kwani Mungu anaweza kutufundisha sisi kupitia kwa ndugu wa familia zetu. Kingine tunapaswa kuchelewa au kutokuhukumu mtu kwa kutazama historia ya familia yake au mambo yake ya zamani. Hakuna mtu ambaye anabaki kama alivyo daima. Tunapaswa kuwatazama watu kwa mtazamo mpya na mtazamo mpya. Tatu, kila wakati tunaposikia neno la Mungu likitangazwa kwetu, tunapaswa kusikiliza sio kwa kutazama mtu bali kutazama Roho Mtakatifu aneyeongea kupitia yeye. Nne, usikatishwe tamaa na watu kutokupokea neno la Mungu wala usikubali kuangushwa na mtu ambaye hataki kukufuata. Zaidi sana usiache kuwatendea mema wengine. 
Matendo matukufu ya Mungu hayakuweza kutendeka kule Nazareti kwasababu ya kukosa kwao Imani. Watu walikuwa na mioyo migumu wakashindwa kuruhusu mioyo na akili zao zipokee neno la Yesu. Kwa njia hii Yesu hakuweza kufanya miujiza mikuu maeneno ya nyumbani kwake. 

Je, unamruhusu Yesu akufanye uwe mpya siku kwa siku? Je, unamruhusu yeye atende mambo makuu katika maisha yako? Kama utakuwa na mashaka katika swali hili ni ishara kwamba Mungu anataka kufanya makuu katika maisha yako. 

Sala: Bwana, ninakuomba moyo wangu uwe na rutuba kwa ajili ya kazi yako kuu. Ninaomba moyo wangu ufanywe upya nawe, maneno yako na uwepo wako katika maisha yangu. Njia katika maisha yangu na unifanye upya chombo cha neema yako. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JULAI 31, 2026



MASOMO YA MISA, JULAI 31, 2026
IJUMAA, JUMA LA 17 LA MWAKA


SOMO 1
Yer 26:1–9

Mwanzo wa kumiliki kwake Yehoyakimu, mwana wa Yosia, mfalme wa Yuda, neno hili lilitoka kwa Bwana, kusema, Bwana asema hivi, Simama katika uwanja wa nyumba ya Bwana, useme na miji yote ya Yuda, wajao ili kuabudu katika nyumba ya Bwana; sema nao maneno yote ninayokuamuru kuwaambia, usizuie hata neno moja. Labda watasikia, na kughairi na kuacha kila mtu njia yake mbaya; ili niyaghairi mabaya niliyokusudia kuwatenda, kwa sababu ya uovu wa matendo yao. Nawe utawaambia, Bwana sema hivi, kama hamtaki kunisikia, kwenda katika sheria yangu, niliyoiweka mbele yenu, kuyasikiliza maneno ya watumishi wangu, manabii, ninaowatuma kwenu, naam, nikiondoka mapema na kuwatuma; lakini ninyi hamkuwasikiliza; basi, nitafanya nyumba hii kuwa kama Shilo, na mji huu nitaufanya kuwa laana kwa taifa zote za dunia. Na makuhani, na manabii, na watu wote, wakamsikia Yeremia, hapo aliposema maneno haya katika nyumba ya Bwana. Ikawa, Yeremia alipokuwa amekwisha kusema maneno yote Bwana aliyomwamuru kuwaambia watu wote, ndipo hao makuhani, na manabii, na watu wote, wakamkamata, wakisema, Bila shaka utakufa. Kwa nini umetabiri kwa jina la Bwana, ukisema, Nyumba hii itakuwa kama Shilo, na mji huu utakuwa ukiwa, hautakaliwa na mtu? Watu wote wakamkusanyikia Yeremia katika nyumba ya Bwana.


Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab 69:4, 7–9, 13

(K) Kwa wingi wa fadhili zako, unijibu, Ee Bwana.

Wanaonichukia bure ni wengi
Kuliko nywele za kichwa changu.
Watakao kunikatilia mbali wamekuwa hodari,
Adui zangu kwa sababu isiyo kweli.
Hata mimi nalilipishwa kwa nguvu
Vitu nisivyovichukua.


Maana kwa ajili yako nimestahimili laumu,
Fedheha imenifunika uso wangu.
Nimekuwa mgeni kwa ndugu zangu,
Na msikwao kwa wana wa mama yangu.
Maana wivu wa nyumba yako umenila,
Na laumu zao wanaokulaumu zimenipata.

Nami maombi yangu nakuomba Wewe, Bwana,
Wakati ukupendezao; Ee Mungu,
Kwa wingi wa fadhili zako unijibu,
Katika kweli ya wokovu wako.


SHANGILIO
1 Sam 3:9, Yn. 6:68

Aleluya, aleluya,
Nena, Bwana, kwa kuwa mtumishi wako anasikia: wewe unayo maneno ya uzima wa milele.
Aleluya


INJILI
Mt 13:54-58

Yesu alipofika nchi yake, akawafundisha katika sinagogi lao, hata wakashangaa, wakasema, Huyu amepata wapi hekima hii na miujiza hii? Huyu si mwana wa seremala? Mamaye si yeye aitwaye Mariamu? Na nduguze si Yakobo, na Yusufu, na Simoni, na Yuda? Na maumbu yake wote hawapo hapa petu? Basi huyu amepata wapi haya yote? Wakachukizwa naye. Yesu akawaambia, Nabii hakosi kupata heshima, isipokuwa katika nchi yake, na nyumbani mwake mwenyewe. Wala hakufanya miujiza mingi huko, kwa sababu ya kutokuamini kwao.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MFINYANZI MTAKATIFU!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Alhamisi, Julai 30, 2026 
Juma la 17 la Mwaka


Yer 18: 1-6; 
Zab 145: 2-6; 
Mt 13: 47-53


MFINYANZI MTAKATIFU!

Katika lirtujia ya neno la Mungu leo, mwalimu mwenye hekima anatumia mifano miwili kutoka katika uhalisia wa maisha yetu ya kila siku ili kutufundisha kitu cha hali ya juu. Anatumia, udongo, chungu na mfinyanzi na mfano wa neti inayotumiwa na mvuvi kuvulia samaki. Wakati la kwanza likitueleza kuna maovu duniani, mabaya, mapungufu na dhambi ambayo Mungu atahukumu siku moja, na lingine linatuambia kwamba mpango wa Mungu ni kutusafisha nakututakasa kutoka katika maovu yote na kutufinyanga na kutubadili siku kwa siku ili tufanane naye. Ni Neema ya Kimungu ambayo Mungu anaiweka ndani mwetu ambayo itatutakasa na kutubadili. 

Mungu ambaye ni Mfinyanzi Mtakatifu ametupa njia nyingi za sisi kujivika neema yake, Neno la Mungu, sakramenti ya Ekaristi na Kitubio, maisha ya sala, kufunga na kuomba toba, huruma na kufanya matendo ya huruma, kuvumilia kila wakati na kubeba misalaba yetu kila siku na mengine mengi. Yote haya yatatuongoza kwenye njia ya utakatifu na neema. Sasa tujivike neema ya Mungu isiyo na kikomo ambayo yeye mwenyewe kama Mfinyanzi Mtakatifu yupo tayari kutupatia ili kukua katika neema mpaka hapo tutakapo pata yote katika ukamilifu wote kwenye Ufalme wake.

Sala: Ee Bwana Yesu, nifiche katika madonda ya Moyo wako Mtakatifu. Niondoe katika hamu yangu ya kupenda kupendwa na kuheshimiwa. Nifanye mimi niwe mmoja nawe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JULAI 30, 2026




MASOMO YA MISA, JULAI 30, 2026
ALHAMISI, JUMA LA 17 LA MWAKA


SOMO 1
Yer. 18:1 – 6

Neno hili ndilo lilomjia Yeremia, kutoka kwa Bwana, kusema, Ondoka, ukashuke mpaka nyumba ya mfinyanzi, na huko nitakusikizisha maneno yangu. Basi nikashuka mpaka nyumba ya mfainyanzi, na tazama, alikuwa akifanya kazi yake kwa magurudumu. Na chombo kile, alichokuwa akikifinyanga, kilipoharibika mkononi mwake yule mfinyanzi, alikifanyiza tena kuwa chombo kingine, kama alivyoona vema yule mfinyanzi kukifanya.

Ndipo neno la Bwana likamjia, kusema, Ee nyumba ya Israeli, je! Siwezi mimi kuwatendea ninyi vile vile kama mfinyanzi huyu alivyotenda? Asema Bwana. Angalieni, kama udongo ulivyo katika mkono wa mfinyanzi, ndivyo mlivyo katika mkono wangu, Ee nyumba ya Israeli.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 146:1 – 5 (K) 5

(K) Heri ambaye Mungu wa Yakobo ni msaada wake.

Ee nafsi yangu umsifu Bwana,
Nitamsifu Bwana muda ninaoishi,
Nitamwimbia Mungu wangu ningali hai. (K)

Msiwatumainie wakuu,
Wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake.
Pumzi yake hutoka, huurudia udongo wake,
Siku hiyo mawazo yake yapotea. (K)

Heri ambaye Mungu wa Yakobo ni msaada wake,
Na tumaini lake ni kwa Bwana, Mungu wake.
Aliyezifanya mbingu na nchi,
Bahari na vitu vyote vilivyomo. (K)



SHANGILIO
1 Pet. 1:25

Aleluya, aleluya,
Neno la Bwana hudumu hata milele, na neno hilo ni neno jema lililohubiriwa kwenu.
Aleluya.



INJILI
Mt. 13:47 – 53

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Ufalme wa mbinguni umefanana na juya, lililotupwa baharini, likakusanya wa kila namna; hata lilipojaa, walilivuta pwani; wakaketi, wakakusanya walio wema vyomboni, bali walio wabaya wakawatupa. Ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia; malaika watatokea, watawatenga waovu mbali na wenye haki, na kuwatupa katika tanuru ya moto; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno.

Yesu aliwauliza, Mmeyafahamu hayo yote? Wakamwambia, Naam. Akawaambia, Kwa sababu hiyo, kila mwandishi mwenye elimu ya ufalme wa mbinguni amefanana na mtu mwenye nyumba atoaye katika hazina yake vitu vipya na vya kale.

Ikawa Yesu alipoimaliza mifano hiyo, alitoka akaenda zake.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

NGUVU YA YESU DHIDI YA MAUTI!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatano, Julai 29,  2026 
Juma la 17 la Mwaka

KUMBUKUMBU YA FAMILIA WA MARTA, MARIA NA LAZARO

Yer 13:1-11; 
Kum 32: 18-21; 
Yn 11: 19-27 or Lk 10: 38-42


NGUVU YA YESU DHIDI YA MAUTI!

“Yesu aliwapenda, Martha, Maria na Lazaro” (Yn 11: 5). Maneno haya ya pekee katika Injili ya Yohane yanatueleza juu ya uhusiano wa pekee aliokuwa nao Yesu kati ya Martha, Maria na Lazaro. Inaonekana Yesu alikuwa mgeni wao mara nyingi katika familia hii huko Bethania, kijiji kidogo, maili mbili kutoka mji wa Yerusalemu. Tunasoma safari tatu za Yesu anazofanya ili kuwatembelea, katika Injili ya Luka 10:38-42, Yn 11: 1-53, Yn 12: 1-9. Sisi nasi tujenge Upendo kama huo na Yesu, mwana wa Mungu, tumjue Mungu. Tunaomba yeye asiwe tu mgeni wetu kila Mara katika maisha bali awe sehemu ya kiini cha familia zetu. 

Wakati Yesu alipowatembelea mara ya pili, Martha alikuwa akiomboleza na kulia juu ya kifo cha Lazaro kaka yake, na nyumba ikiwa imejawa pia na waombolezaji wengine. Lakini aliposikia Yesu amefika mahali pale, anasimama mara na kuwaacha wageni wengine na waombolezaji na anaenda kumuona Yesu. Hapa tunamuona Martha aliyebadilika. Pamoja na kwamba yupo katika hali ya majonzi na uchungu anaenda kumuona Yesu. Sasa anatambua lililo muhimu katika maisha. Katika mazungumzo yake anaanza moja kwa moja bila kuwa na wasi wasi kwamba anaamini juu ya nguvu ya Yesu, katika ufufuo wa wafu. Kwasababu ya hili analeta usemi uliomaarufu sana katika Injili ya Yohani. “MIMI (Yesu) ni ufufuo na uzima; aniaminiye mimi, hata kama anakufa ataishi na anayeishi na kuniamini hatakufa kamwe”. Baada ya hili, Martha analeta tena ungamo la Imani “ndio Bwana, ninaamini wewe ni Masiha , Mwana wa Mungu, ajaye ulimwenguni”. Na sasa Yesu anamfufua Lazaro. 

Kwa njia hii tunamuona Martha anavyoshirikiana na Neema ya Mungu katika maongezi yake na Yesu, sisi nasi tumpe Yesu nafasi aongee na sisi, sala zetu zisiwe ni sisi tu tunaongea na kueleza mambo yetu pekee, bali tumruhusu pia Mungu aongee nasi. Tumpe pia Mungu nafasi ajibu maombi yetu. Tuwe na muda wa kutafakari katika ukimya tumsikilize Mungu anataka kusema nini juu yangu? Tuwe na muda pia wa kumshukuru sio kuomba tuu, sala yetu iwe na nyanja mbali mbali. Tuwe na muda wa kumsifu, kumshukuru, kumuomba, kumsikiliza na pia kutafakari juu ya ukuu wake, na zaidi sana juu ya upendo aliotuonesha kupitia kwa Mwanaye Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwanjia yake watu wote wapo hai. 

Sala: Bwana, nina amini kwamba utanifufua siku ya mwisho, nizaliwe katika maisha ya umilele. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JULAI 29, 2026



MASOMO YA MISA, JULAI 29, 2026
JUMATANO, JUMA LA 17 LA MWAKA

KUMBUKUMBU YA FAMILIA WA MARTA, MARIA NA LAZARO


SOMO 1 
Yer. 13:1-11

Bwana aliniambia hivi, Enenda, ukajinunulie mshipi wa kitani, ukajivike viuno, wala usiutie majini. Basi nikanunua mshipi sawasawa na neno la Bwana, nikajivika viunoni. Nalo neno la Bwana likanijia mara ya pili, kusema, Twaa mshipi ule ulioununua, ulio viunoni mwako, kisha ondoka, enenda mpaka mto Frati, ukaufiche huko katika pango la jabali. Basi nikaenda, nikauficha karibu na mto Frati, kama Bwana alivyoniamuru.

Hata ikawa baada ya siku nyingi, Bwana akaniambia, Ondoka, enenda mpaka mto Frati, ukautwae ule mshipi, niliokuamuru kuuficha huko. Ndipo nikaenda mpaka mto Frati, nikachimba, nikautwaa ule mshipi katika mahali pale nilipouficha; na tazama, mshipi ulikuwa umeharibika, haukufaa tena kwa lo lote. Ndipo neno la Bwana likanijia, kusema, Bwana asema hivi, Jinsi iyo hiyo nitakiharibu kiburi cha Yuda, na kiburi kikuu cha Yerusalemu. Wata hawa waovu, wanaokataa kusikiliza maneno yangu, wanaokwenda kwa ushupavu wa mioyo yao, na kufuata miungu mingine ile kuitumikia na kuiabudu, watakuwa hali moja na mshipi huu, usiofaa kwa lo lote. Maana kama vile mshipi unavyoshikamana na viuno vya mtu, ndivyo nilivyowashikamanisha nami nyumba yote ya Israeli, na nyumba yote ya Yuda, asema Bwana; wapate kuwa watu kwangu mimi, na jina, na sifa, na utukufu; lakini hawakutaka kusikia.

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu 


WIMBO WA KATIKATI 
Kum. 32:18-21 (K) 18

(K) Humkumbuki Mwamba aliyekuzaa.

Humkumbuki Mwamba aliyekuzaa.
Mungu aliyekuzaa umemsahau.
Bwana akaona, akawachukia,
Kwa sababu ya kukasirishwa na wanawe na binti zake. (K)

Akasema, Nitawaficha uso wangu,
Nitaona mwisho wao utakuwaje;
Maana, ni kizazi cha ukaidi mwingi,
Watoto wasio imani ndani yao. (K)

Wamenitia wivu kwa kisicho Mungu, 
Wamenikasirisha kwa ubatili wao;
Nami nitawatia wivu kwa wasio watu. 
Nami nitawakasirisha kwa taifa lipumbaalo. (K)


SHANGILIO 
Kol. : 16,17

Aleluya, aleluya, Neno la Kristu likae kwa wingi ndani yenu katika hekima yote, mkimshukuru Mungu Baba kwa Yeye. Aleluya.


INJILI
Yn. 11:19 – 27

Watu wengi katika Wayahudi walikuwa wamekuja kwa Martha na Mariamu, ili kuwafariji kwa habari ya ndugu yao. Basi Martha aliposikia kwamba Yesu anakuja, alikwenda kumlaki; na Mariamu alikuwa akikaa nyumbani. Basi Martha akamwambia Yesu, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa. Lakini hata sasa najua ya kuwa yoyote utakayomwomba Mungu, Mungu atakupa. Yesu akamwambia, Ndugu yako atafufuka. Maratha akamwambia, Najua ya kuwa atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.

Yesu akamwambia, Mimi ndimi ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je! Unayasadiki hayo?

Akamwambia, Naam, Bwana, mimi nimesadiki ya kwamba wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu, yule ajaye ulimwenguni.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.

Au

INJILI
Lk. 10:38 – 42

Ikawa katika kuenenda kwao aliingia katika kijiji kimoja; mwanamke mmoja jina lake Martha akamkaribisha nyumbani kwake. Naye alikuwa na umbu lake aitwaye Mariamu, aliyeketi miguuni pake Yesu, akasikiliza maneno yake. Lakini Martha alikuwa akihangaika kwa utumishi mwingi; akamwendea, akasema, Bwana, huoni vibaya hivyo ndugu yangu alivyoniacha nitumike peke yangu? Basi mwambie anisaidie. Bwana akajibu akamwambia, Martha, Martha, unasumbuka na kufadhaika kwa ajili ya vitu vingi; lakini kinatakiwa kitu kimoja tu; na Mariamu amelichagua fungu lililo jema, ambalo hataondolewa.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUKUWA KATIKATI YA MAGUGU



“ASALI ITAKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumanne, Julai 28, 2026, 
Juma la 17 la Mwaka wa Kanisa 


Yer 14: 17-22; 
Zab 78: 8-9, 11, 13; 
Mt 13: 36-43.


KUKUWA KATIKATI YA MAGUGU

Injili ya leo inatualika kutafakari juu ya Ufalme wa Mungu. Yesu alikuja kutangaza na kuanzisha Ufalme wa Mungu. Somo la kwanza lina tukumbulisha ujumbe huu kwa kutangaza nguvu na mamlaka ya Mungu, ambaye ni mkarimu na mwenye huruma. Ingawaje ni mkuu juu ya yote anaongea na Musa uso kwa uso kama rafiki. Anatupa muda kuchagua kuwa katika ufalme wake. 

Katika mfano wa magugu na ngano, yote yanakuwa pamoja, yote yanapokea Baraka kipindi cha uhai wao, lakini mwishoni wakati wa mavuno yanatenganishwa na kila moja litaonesha matunda yake. Wengi wetu tumebarikiwa kuzaliwa katika familia ya Kikristo. Mungu ametupatia Baraka ya ubatizo hata kabla hatujauelewa maana yake. Anaendelea kutupatia Baraka kwa njia ya kanisa. Lakini Baraka za kuwa mkristo haina maana tutaenda tuu mbinguni bila kujishughulisha. Uzuri ni kwamba Mungu ametupa uhuru wa kumchagua yeye au kumkataa, wakati wa mavuno itadhihirika kama ulimchagua Mungu au la! .

Tujaribu kufikiria kama Yesu alikuwa aje kesho na atawachukua wale wote wenye haki? Je, wewe utakuwa na wasiwasi? Pengine hapana. Au pengine kutakuwa na muda wa kutazama nyuma na kuwa na Amani na kuona haki inakuja. Mungu daima yupo katika kuongoza. Anatambua anafanya nini na atakuwa na utukufu juu ya vyote. 

Wakristo wanaitwa waweze kuwa kama chachu katika jamii ili ulimwengu uweze kuwa sehemu nzuri ya kukaa. Kama sisi ni mashahidi wa kweli wa Kristo, Injili itaenea daima kila mahali. Kuingia kwetu katika ufalme itategemea kuchagua wema na kuacha yale yalio machukizo mbele ya Mungu. Wito wetu kama Wakristo tumeitwa kuwa mwanga wa ulimwengu, chumvi ya ulimwengu, ngano kati ya magugu, na ushuhuda wa upendo wa Yesu ulimwenguni. Tunaomba hii iwe sala yetu kwa Yesu kwani, ili mioyo mingi iweze kutambua uwezo upendo wa Mungu na kuwa raia wa Ufalme. 

Sala: Bwana Yesu, ninakuomba unisaidie mimi niweze kukaza macho yangu kwako na katika ushindi wa mwisho. Nisaidie mimi niweze kuwa mvumilivu nikwepe maovu ya ulimwengu huu kwa neema utakazo nipatia. Ninakuomba nisisahau ahadi yako siku ya mwisho uliioongea kwetu. Yesu nakuamini
 wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com