Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

‘MJINGA’ KWA AJILI YA KRISTO?



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Ijumaa, Agosti 28, 2026, 
Juma la 21 la Mwaka wa Kanisa


KUMBUKUMBU YA MTAKATIFU AGOSTINO

1Kor 1:17-25; 
Zab 32: 1-2, 4-5, 10-11; 
Mt 25: 1-13


‘MJINGA’ KWA AJILI YA KRISTO?


“Mungu ndio, Yesu ndio, Kanisa hapana!”. Namna hii ya kufikiri imezoeleka sana kati ya wengi. Je, sisi ni mmoja wao kati ya hawa “wengi”? Je kuna wakati tunajisikia mafundisho ya kanisa ni “yakizamani, yamepitwa na wakati, yasiofikirika na hivyo hayafai kuyaishi”? Na pia hayaendani na zama zetu za sayansi ya hali ya juu? Na hasa kuhusu, maadili na mambo ya maisha ya familia? Je, inawezekana kuwa Wakristo wazuri wanaoenda kanisani kila mara na bado kubaki bila kusumbuliwa na kufuata “majibu ya haraka yanayoonekana” ambayo “wenye hekima na akili” wa ulimwengu huu wanayotoa, wakati mafundisho ya Kanisa yanoonekana kupishana na mambo hayo? 

Mafundisho ya Kanisa yanaweza kuonekana kuwa “Msalaba”- lakini hii ni kwasababu hayajajengwa katika “sayansi ya mwanadamu au hekima ya mwanadamu”, bali katika maisha ya Kristo, msulubiwa. Mt. Paulo anatuambia wazi. “ujumbe juu ya Msalaba kwao wanaopotea ni upuzi, bali sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu” (1Kor 1: 18). Ni ukuweli usiopingika kwamba, Kanisa linaoongozwa na Roho Mtakatifu, anayetufundisha kila kitu, nakutukumbusha yote aliyofundisha Kristo na kusema kwetu kama alivyotuahidi mwenyewe. ( Yn 14: 26). Je, inawezekana kwamba, “wanasayansi na wanafalsafa, watu mashuhuri na wanaojiona wenye akili sana- wanao tetea mawazo yao kwa kutoa hitimisho ya vitu vinavyoonekana –ambavyo kanisa linaona kwamba sio sahihi- kwamba wana akili na hekima zaidi kuliko Mungu aliyewaumba? 

“Kwasababu upumbavu wa Mungu una hekima zaidi ya wanadamu, na udhaifu wa Mungu una hekima zaidi ya wanadamu.”(1 Kor 1: 25). Kufuata anachosema Mama Kanisa huenda kikaonekana upumbavu katika kiwango cha ulimwengu, hii ni kwasababu Mama kanisa anafundisha kuendana na utashi wa Kristo aliyefanya jambo lilionekana kuwa la aibu kwa kufa msalabani ili kutukomboa sisi, wadhambi. Pengine kwako kuungama unaona ni upumbavu au jambo la aibu! Ujue kuungama ni kwaajili ya ukombozi wa roho yako. Sisi tuwe kama Kristo, tukubali kuonekana kuwa wajinga wa ulimwengu huu, kwakufuata mafundisho ya Kristo aliyoyasimika katika Kanisa lake.

Sala: Baba, tupe neema tuwe na utashi kama wa Kristo. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, AGOSTI 28, 2026



MASOMO YA MISA, AGOSTI 28, 2026
IJUMAA , JUMA LA 21 LA MWAKA

KUMBUKUMBU YA MTAKATIFU AGOSTINO

SOMO 1
1 Kor. 1:17 – 25

Kristo hakunituma ili nibatize, bali niihubiri Habari Njema; wala si kwa hekima ya maneno, msalaba wa Kristo usije ukabatilika. Kwa sababu neno la msalaba kwao wanaopotea ni upuzi, bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu. Kwa kuwa imeandikwa, Nitaiharibu hekima yao wenye hekima, Na akili zao wenye akili nitazikataa. 

Yu wapi mwenye hekima? Yu wapi mwandihsi? Yu wapi mlete hoja wa zamani hizi? Je! Mungu hakuifanya hekima ya dunia kuwa ni upumbavu? Kwa maana katika hekima ya Mungu, dunia isipopata kumjua Mungu kwa hekima yake, Mungu alipenda kuwaokoa waaminio kwa upuzi wa lile neno linalohubiriwa.

Kwa sababu Wayahudi wanataka ishara, na Wayunani wanatafuta hekima; bali sisi tunamhubiri Kristo, aliyesulibiwa; kwa Wayahudi ni kikwazo, na kwa Wayunani ni upuzi; bali kwao waitwao, Wayahudi kwa Wayunani, ni Kristo, nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu. Kwa sababu upumbavu wa Mungu una hekima zaidi ya wanadamu, na udhaifu wa Mungu una nguvu zaidi ya wanadamu.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 33:1 – 2, 4 – 5, 10 – 11 (K) 5

(K) Bwana anajaza nchi na fadhili zake.

Mpigeni Bwana vigelegele, enyi wenye haki,
Kusifu kunawapasa wanyofu wa moyo.
Mshukuruni Bwana kwa kinubi,
Kwa kinanda cha nyuzi kumi mwimbieni sifa. (K)

Kwa kuwa neno la Bwana lina adili,
Na kazi yake yote huitenda kwa uaminifu.
Huzipenda haki na hukumu,
Nchi imejaa fadhili za Bwana. (K)

Bwana huyabatilisha mashauri ya mataifa,
Huyatangua makusudi ya watu.
Shauri la Bwana lasimama milele,
Makusudi ya moyo wake vizazi na vizazi. (K)


SHANGILIO
Yn. 17:17

Aleluya, aleluya,
Neno lako ndiyo kweli, Ee Bwana, ututakase kwa ile kweli.
Aleluya.


INJILI
Mt. 25:1 – 13

Yesu aliwaambia wafuasi wake: Ndipo ufalme wa mbinguni utakapofanana na wanawali kumi, waliotwaa taa zao, wakatoka kwenda kumlaki bwana arusi. Watano wao walikuwa wapumbavu na watano wenye busara. Wale waliokuwa wapumbavu walizitwaaq taa zao, wasitwae na mafuta pamoja nao; bali wale wenye busara walitwaa mafuta katika vyombo vyao pamoja na taa zao. Hata bwana arusi alipokawia, wote wakasinzia wakalala usingizi.

Lakini usiku wa manane, pakawa na kelele, Haya, bwana arusi; tokeni mwende kumlaki. Mara wakaondoka wanawali wale wote, wakazitengeneza taa zao. Wale wapumbavu wakawaambia wenye busara, Tupeni mafuta yenu kidogo; maana taa zetu zinazimika. Lakini wale wenye busara wakawajibu, wakisema, Sivyo; hayatatutosha sisi na ninyi; afadhali shikeni njia mwende kw awauzao, mkajinunulie. Na hao walipokuwa wakienda kununua, bwana arusi akaja, nao waliokuwa wakienda kununua, bwana arusi akaja, nao waliokuwa tayari wakaingia pamoja naye arusini; mlango ukafungwa.

Halafu wakaja na wale wanawali wengine, wakasema, Bwana, Bwana, utufungulie. Akajibu akasema, Amin, nawambia, siwajui ninyi. Basi kesheni, kwa sababu hamwijui siku wala saa.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

KUWA TAYARI!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Alhamisi, Agosti 27, 2026, 
Juma la 21 la Mwaka 

Kumbukumbu ya Mt. Monika


1Kor 1:1-9; 
Zab 144:2-7; 
Mt 24:42-51


KUWA TAYARI !

Injili ya leo inatangaza kuja sio kwa tufani bali ukombozi. Inatangaza kuja kwa Ufalme wa Mungu. Na hapo hapo tunaambiwa kwamba hatujui siku wala saa itakapokuja na kuja kwake kutakuwa kama ujio wa mwizi. Njia na silaha kubwa ya mwizi ni kuja kwakustukiza. Kuja kwa Ufalme wa Mungu hakutakuwa na kengele za tahadhari. Kuna silaha moja tuu ambayo tunaweza kuiandaa kwaujio wa ufalme wa Mungu nayo ni – kuandaa maisha yetu. Mungu ametupa sisi wanadamu uhuru wakuchagua. Kila mtu anauwezo wakuchagua jema na kutenda mema nakuishi vizuri na hapo ufalme wa Mungu ujapo atakuwa amejiandaa au mtu anauwezo wakuchagua kutenda dhambi na Mungu haingilii uhuru wake, lakini Mungu ameweka wazi njia yake kwamba kuchagua uovu sio kadiri ya sheria yake. Tuombee neema ya Mungu ili tuweze kutumia uhuru wetu vizuri tuchague kutenda mema kila wakati na tuwasaidie wengine waweze kuchagua kutenda mema ili ufalme wa Mungu ujapo kwa mara ya pili utukute tumejiandaa kila wakati.

Tuna mengi sana ya kutufundisha sisi, kila mara tunawaona vijana wadogo wanapoteza maisha wakiwa na umri mdogo kabisa, pengine kwa ajali au kwa magonjwa, tunajiuliza hivi walijua kwamba Mungu angewachukua wakiwa wadogo namna hii? Tunajiuliza hivi walikuwa wamejiandaa? Sio kazi yetu kuhukumu nakujua kuhusu wema wao lakini tunachojifuza ni kwamba siku ya mwisho ya mwanadamu hapa duniani ni Mungu mwenyewe anayepanga, lililo bora tena sana ni kuwa tayari kwa ujio wa Mungu muda wowote ule. Tukiishi kwa matumaini yetu yakiwa ndani ya Kristo, siku hiyo itakuwa ya furaha kwetu na hatutaishi kwa woga. Hofu inakuja kwasababu ya dhambi, lakini tukijipatanisha na Kristo kila mara matumaini yetu kwake ni makubwa na furaha yetu ya kuungana naye itakuwa kubwa zaidi. 

Tuwasaidie ndugu zetu wote wamrudie Kristo, tukitambua kuwa hata jani la mwisho kabisa kwenye mti ni sehemu ya mti. Mkristo au ndugu unayemuona mdhambi sana bado ni sehemu ya mwili wa Kristo. Tuwasaidie ndugu zetu kwa kuwatia moyo ili wawe karibu zaidi na Kristo ili siku yake itakapokuja tuweze kupokea neema na kumlaki Kristo. Ni furaha yetu wote kwa pamoja kuuona uso wa Mungu.

Sala: Bwana, kwakupokea sakramenti kila wakati, kwanjia ya sala zangu na ndugu zangu, kwa kutembea katika mwanga wa neno lako, naomba niwe tayari daima kukupokea wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA ALHAMISI, AGOSTI 27, 2026



MASOMO YA MISA 
ALHAMISI, AGOSTI 25, 2022
JUMA LA 21 LA MWAKA


Kumbukumbu ya Mt. Monika


SOMO 1
1 Kor. 1:1 – 9

Paulo, aliyeitwa kuwa mtume wa Yesu Kristo kwa mapenzi ya Mungu, na Sosthene ndugu yetu, kwa kanisa la Mungu lililoko Korintho, wale waliotakaswa katika Kristo Yesu, walioitwa wawe watakatifu, pamoja na wote wanaoliitia jina la Bwana wetu Yesu Kristo kila mahali, Bwana wao na wetu. Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo kwa Mungu Baba yetu, na kwa Bwana Yesu Kristo.

Namshukuru Mungu sikuzote kwa ajili yenu, kwa sababu ya neema ya Mungu mliyopewa katika Kristo yesu; kwa kuwa katika kila jambo mlitajirika katika yeye, katika maneno yote, na maarifa yote; kama ushuhuda wa Kristo ulivyothibitika kwenu; hata hamkupungukiwa na karama yoyote, mkikutazamia sana kufunuliwa kwake Bwana wetu Yesu Kristo; ambaye atawathibitisha hata mwisho, ili msilaumiwe siku ile ya Bwana wetu Yesu Kristo. Mungu ni mwaminifu ambaye mliitwa na yeye mwingine katika ushirika wa Mwanawe, Yesu Kristo Bwana wetu.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 145:2 – 7 K (1)

(K) Ee Bwana, nitalihimidi jina lako milele na milele.

Kila siku nitakuhimidi,
Nitalisifu jina lako milele na milele.
Bwana ndiye mkuu mwenye kusifiwa sana,
Wala ukuu wake hautambulikani. (K)

Kizazi kwa kizazi kitayasifu matendo yako,
Kitayatangaza matendo yako makuu.
Nitakufikiri fahari ya utukufu wa adhama yako,
Na matendo yako yote ajabu (K)

Watu watayajua matendo yako ya kutisha,
Nami nitausimulia ukuu wako.
Watalihubiri kumbukumbu la wema wako mkuu.
Wataiimba haki yako. (K)



SHANGILIO
Yn. 14:23

Aleluya, aleluya,
Mtu akinipenda, atalishika neno langu, 
na Baba yangu atampenda, 
na sisi tutakuja kwake.
Aleluya.



INJILI
Mt. 24:42 – 51

Yesu aliwambia wanafunzi wake: Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu. Lakini fahamuni neno hili; kama mwenye nyumba angaliijua ile zamu mwivi atakayokuja, angalikesha, wala asingaliiacha nyumba yake kuvunjwa. Kwa sababu hiyo ninyi nanyi jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana wa Adamu yuaja.

Ni nani basi yule mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya nyumba yake, awape watu chakula kwa wakati wake? Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo. Amin, nawaambieni, atamweka juu ya vitu vyake vyote. Lakini mtumwa yule mbaya akisema moyoni mwake, Bwana wangu anakawia; akaanza kuwapiga wajoli wake, na kula na kunywa pamoja na walevi; bwana wake mtumwa huyo atakuja siku asiyodhani, na saa asiyojua, atamkata vipande viwili, na kumwekea fungu lake pamoja na wanafiki; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUONDOA UFARISAYO NDANI MWETU!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatano, Agosti 26, 2026 
Juma la 21 la Mwaka
___________________
2 The 3: 6-10, 16-18
Zab 128: 1-2, 4-5
Mt 23: 27-32.
___________________

KUONDOA UFARISAYO NDANI MWETU!

Katika somo la Injili leo Yesu analalamika na kusema ole juu ya Mafarisayo na Waandishi kwasababu ya hali yao ya unafiki. Walikuwa wamewabebesha watu mizigo ya sheria na mambo ya njee. Waliwatesa na kuwadhulumu manabii waliokuwa wajumbe wa Mungu na kukataa kusikiliza sauti ya Mungu waliokuwa nayo ndani yao juu yao na watu wote. Wamefana na makaburi yaliopakwa chokaa, yanayo onekana mazuri kwa njee lakini ndani yamejaa mifupa na uozo. Mafarisayo na waandishi walionekana wenye haki mbele za watu lakini hawakuweza kukukutana na mwenye haki Mwenyewe-Yesu.

Kitu kimoja muhimu ni kwamba Yesu ni mwaminifu mno. Wewe je? Upo tayari kufanya kila kitu kwa uaminifu wote? Je, upo tayari kuwa mwaminifu mbele ya Mungu na juu ya roho yako mwenyewe? Tatizo ni kwamba hatuoni hivyo. Daima tunajipitisha mbele ya watu tukijifanya kwamba ni wema na kukwepa ukweli wa mifupa na kila aina ya uchafu uliyo ndani mwetu. Hili sio jambo zuri na Yesu analipinga hili katika Injili.

Leo Injili inakualika utazame ndani ya moyo wako katika hali ya kweli, na ujiulize unaona nini? Natumaini utaona wema na fadhili na kuzifurahia. Lakini pia katika hali ya kweli utaziona dhambi. Pengine sio katika hali kama ya Mafarisayo, lakini kwa hakika utaona hali ya dhambi ambazo zinapaswa kusafishwa. Tafakari leo, ni jinsi ghani waweza kuzitazama dhambi zako katika hali ya kweli na jinsi ya kuziacha.


Sala: Bwana, nisaidie mimi niweze kuchukua hatua ya kujitazama mimi mwenyewe maisha yangu. Nisaidie nisione tuu fadhila nzuri ulizoweka ndani yangu, lakini pia nisaidie niweze kuona uovu au dhambi zilizo ndani ya moyo wangu. Ninakuomba unisafishe kutoka katika dhambi hiyo ili niweze kukupenda wewe zaidi. Yesu, nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUMATANO, AGOSTI 26, 2026

 


MASOMO YA MISA, JUMATANO, AGOSTI 26, 2026
JUMA LA 21 LA MWAKA 

________

SOMO I

2 The 3: 6-10, 16-18

 

Ndugu, twawaagiza katika jina la Bwana Yesu Kristo, jitengeni nafsi zenu na kila ndugu aendaye bila utaratibu, wala si kwa kufuata mapokeo mliyoyapokea kwetu.

 

Mwajua wenyewe jinsi iwapasavyo kutufuata; kwa sababu hatukuenda bila utaratibu kwenu; wala hatukula chakula kwa mtu ye yote bure; bali kwa taabu na masumbufu, usiku na mchana tulitenda kazi, ili tusimlemee mtu wa kwenu awaye yote. Si kwamba hatuna amri, lakini makusudi tufanye nafsi zetu kuwa kielelezo kwenu, mtufuate.

 

Kwa kuwa hata wakati ule tulipokuwapo kwenu tuliwaagiza neno hili, kwamba ikiwa mtu hataki kufanya kazi, basi, asile chakula.

 

Sasa, Bwana wa amani mwenyewe na awape amani daima kwa njia zote. Bwana awe pamoja nanyi nyote.

 

Salamu zangu mimi Paulo, kwa mkono wangu mwenyewe. Hii ndiyo alama katika kila waraka, ndio mwandiko wangu. Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo na iwe pamoja nanyi nyote.

 

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu
________

WIMBO WA KATIKATI 

Zab 128: 1-2, 4-5 (K) 1


(K) Heri kila mtu amchaye Bwana.


Taabu ya mikono yake hakika utaila;

Utakuwa heri, na kwako kwema.

Mkeo atakuwa kama mzabibu uzaao,

Vyumbani mwa nyumba yako. (K)


Tazama, atabarikiwa hivyo, yule amchaye Bwana. 

Bwana akubariki toka Sayuni,

Uone uheri wa Yerusalemu siku zote za maisha yako. (K)

________

SHANGILIO
Yn 10: 27

Aleluya, aleluya,
Kondoo wangu waisikia sauti yangu,
nami nawajua, nao wanifuata.
Aleluya.

________

INJILI 
Mt. 23: 27-32

Yesu alisema, Ole wenu, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! kwa kuwa mmefanana na makaburi yaliyopakwa chokaa, nayo kwa nje yaonekana kuwa mazuri, bali ndani yamejaa mifupa ya wafu, na
uchafu wote. Vivyo hivyo ninyi nanyi, kwa nje mwaonekana na watu kuwa wenye haki, bali ndani mmejaa unafiki na maasi.

Ole wenu, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! kwa kuwa mnayajenga makaburi ya manabii, na kuyapamba maziara ya wenye haki, na kusema, Kama sisi tungalikuwako zamani za baba zetu, hatungalishirikiana nao katika damu ya manabii. Hivi mwajishuhudia wenyewe, ya kwamba ninyi ni wana wao waliowaua manabii. Kijazeni basi kipimo cha baba zenu.


Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo
________

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

UHURU KWAKUACHANA NA UNAFIKI!


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumanne, Agosti 25, 2026, 
Tafakari ya kila siku
Juma la 21 la Mwaka wa Kanisa


2Thes 2:1-3, 14-17; 
Zab 95:10-13; 
Mt 23:23-26


UHURU KWAKUACHANA NA UNAFIKI!


Ipo wazi kutoka katika maisha ya Yesu na mifano kwamba hakulaumu yeyote; alilaumu dhambi yenyewe si mdhambi. Hata leo katika Injili ya leo, analaumu njia ambayo Mafarisayo na Walimu wa sheria, wametumia dini na matendo ya dini vibaya kwaajili ya manufaa ya wao binafsi. Yesu analaumu unafiki wa watu. Katika uhalisia unafiki maana yake ni mtu kujifanya kuwa na kitu ambacho katika hali ya kweli hana. Kusema uongo na unafiki huwa vinaenda sambamba. Yesu hapendi maisha ya namna hii. Katika hali ya maisha ya unafiki maana halisi ya dini inapotea, na hapo dini inakuwa inafanywa kwa njia zisizo eleweka. Yesu aliweza kutambua mara moja waliokuwa waaminifu na wale walikuwa wanafiki. Kwa hiyo alilaumu unafiki wao kwa ujasiri kabisa. Wanafiki walijaribu kwa njia zote ili kupata wafuasi. Walipopata mfuasi, maisha yake yanafanywa kuwa maguu kwa kumtambulishia sheria nyingi, mila nyingi za njee na mambo mengi yakufanya. Kwahiyo Watu walipoteza muelekeo kamili wa yaliokuwa ya muhimu katika dini, na kushikilia mambo yasio ya lazima.

 Mambo yote, mila na tamaduni za kidini yanapaswa yatuongoze kwa Mungu. Ni njia zinazo tumika katika dini ili kutuleta karibu na Mungu. Ni njia zinazotumika katika dini ili kutuleta karibu zaidi na Mungu, na mambo hayo sio mwisho wa kila kitu, mwisho unapaswa kuwa Mungu. Yesu analaumu aina zote za unafiki zinazomfanya Mungu awe mbali nasi katika matendo yetu ya Imani (dini). 
 
Sala: Mungu Baba yetu wa Mbinguni tuweke huru kutoka katika tabia ya unafiki wetu katika kumfuata Mwanao. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, AGOSTI 25, 2026




MASOMO YA MISA, AGOSTI 25, 2026
JUMANNE, JUMA LA 21 LA MWAKA

SOMO 1
2The. 2:1 – 3, 14 – 17

Tunakusihini ndugu, kwa habari ya kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo, na kukusanyika kwetu mbele zake, kwamba msifadhaishwe upesi hata kuiacha nia yenu, wala msisitushwe, kwa roho, wala kwa neno, wala kwa waraka unaodhaniwa kuwa ni wetu, kana kwamba siku ya Bwana imekwisha kuwapo. Mtu awaye yote asiwadanganye kwa njia yoyote; maana haiji, usipokuja kwanza ule ukengeufu; akafunuliwa yule mtu wa kuasi, mwana wa uaharibifu.

Bwana aliwaita ninyi kwa injili yetu, ili kuupata utukufu wa Bwana wetu Yesu Kristo. Basi, ndugu, simameni imara, mkayashike mapokeo mliyofundishwa, ama kwa maneno, ama kwa waraka wetu. Na Bwana wetu Yesu Kristo mwenyewe, na Mungu Baba yetu, aliyetupenda akatupa faraja ya milele na tumaini jema, katika neema, awafariji mioyo yenu, na kuwafanya imara katika kila neno na tendo jema.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 96:10 – 13 (K) 13

(K) Bwana anakuja aihukumu nchi.

Semeni katika mataifa, Bwana ametamalaki,
Naam, ulimwengu umethibitika usitikisike,
Atawahukumu watu kwa adili. (K)

Mbingu na zifurahi, nchi na ishangilie,
Bahari na ivume na vyote viijazavyo.
Mashamba na yashangilie, na vyote vilivyomo,
Ndipo miti yote ya mwituni iimbe kwa furaha;
Mbele za Bwana, kwa maana anakuja.
Kwa maana anakuja aihukumu nchi. (K)

Atahukumu ulimwengu kwa haki,
Na mataifa kwa uaminifu wake. (K)


SHANGILIO
Lk. 8:15

Aleluya, aleluya,
Wanabarikiwa wale ambao kwa unyofu na wema wa mioyo yao hulisikia neno la Mungu, na kulishika. 
Aleluya.


INJILI
Mt. 25:23 – 26

Yesu alisema, Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnalipa zaka na mnanaa na bizari na jira, lakini meacha mambo makuu ya sheria, yaani, adili, na rehema, na imani; hayo imewapasa kuyafanya, wala yale mengine msiyaache. Viongozi vipofu, wenye kuchuja mbu na kumeza ngamia.
Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnasafisha nje ya kikombe na chano, na ndani yake vimejaa unyang’anyi na kutokuwa na kiasi. Ewe Farisayo kipofu, safisha kwanza ndani ya kikombe, ili nje yake nayo ipate kuwa safi.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

NJOO NA UONE: KUKUTANA NA YESU!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatatu, Agosti 24, 2026, 
Tafakari ya kila siku
Juma la 21 la mwaka wa Kanisa

Sikukuu ya Mt. Bartolomayo, Mtume

Uf 21: 9-14; 
Zab 144: 10-13, 17-18;
Yn 1: 45-51


NJOO NA UONE: KUKUTANA NA YESU!


Leo kanisa linafurahia kwa kuadhimisha sikukuu ya Mt. Bartolomayo Mtume. Anajulikana pia kwa jina la Nathanael na alikuwa mmoja wao wa mitume kumi na mbili wa Bwana wetu Yesu Kristo. Alikuwa ni mmisionari akiwa na Philipo na Tomas. Inasemakana alihubiri Injili katika maeneo haya ya, Armenia, India, Persia na Phrygia.

Katika Injili ya leo tunamuona jinsi Philipo anampeleka Nathanaeli kwa Yesu ili aweze naye kukutana na Masiha. Kwahiyo Philipo anatoa ushuhuda ghani kwa Nathanaeli? Badala ya kuchukua muda wakubishana na rafiki yake, Philipo anaamua kuchukua uamuzi wa hekima wa “Kumpele na kumuona” Yesu kwa macho yake mwenyewe, Yesu huyu anayezungumzwa na watu. Philipo alitambua kwamba kukutana na Yesu mtu binafsi inaweza ikabadilisha maisha ya mtu kabisa. Wakati watu wanapopokea neno la Kristo, na wanapoona upendo wake katika matendo, Yesu mwenyewe, kwa njia ya Roho Mtakatifu, anagusa mioyo yao na kufungua mioyo na akili zao kwenye ufunuo wa Mungu. 

Wakati Philipo alivyomleta Nathanaeli kwa Yesu, Yesu alifanya kitu ambacho ni Mungu mwenyewe tu anaweza kufanya! Alifungua moyo wa Nathanaeli na mawazo yake ya ndani ukaweza kutamani ufunuo wa Mungu. Nathanaeli aliyatambua maandiko, alisoma Torati na Manabii na alikuwa akitazamia ahadi ya Mungu itimizwe kwaajili ya watu wa Israeli. Nathanaeli alikuwa ni mtu anayemtafuta Mungu kutoka moyoni. Hakufikiri tu kukua katika akili ya elimu ya Mungu bali alifikiri kuhusu jinsi ya kuungana na Mungu pia. Ndio maana alikuwa tayari kukutana na Yesu, na kuona kama huyu mtu anayefanya miujiza kutoka Galilaya kuwa anaweza kuwa Masiha anayesubiriwa. 

Mungu ameweka katika kila moyo wa Mwanadamu hamu na tamaa ya kumtafuta, yeye aliyetuumba wote kwa upendo wake. Sisi pia tunaalikwa tuweze kuwa na uhusiano mzuri na Yesu binafsi. Pia tujitahidi kuwaelekeza wengine waweze kukutana na Yesu. Tusiwe chanzo cha kuwapeleka wenzetu kwenye uovu unaowaweka mbali na Yesu. Tuwafariji wale waliokata tamaa, tuwapeleke kwa Yesu kwenye matumaini ya kweli, tuwapeleke wakakutane na Mungu ili aweze kugusa maisha yao. Sisi wenyewe tuimarishe uhusiano wetu na Mungu ili kwa uthabiti wetu tuweze kuwavuta wengine kwa Yesu. Tujaribu kuwa na Yesu daima katika maisha yetu ya kila siku na tuwe mashaidi wake wa kweli.

Sala: Bwana Yesu, jifunue mwenyewe ndani yangu ili niweze kuwa nawe daima katika maisha yangu. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, AGOSTI 24, 2026



MASOMO YA MISA, AGOSTI 24, 2026
JUMATATU, JUMA LA 21 LA MWAKA

SIKUKUU YA MT. BARTOLOMEO, MTUME


SOMO 1 
Ufu 21: 9-14

Malaika alinijia akanena nami, akisema, Njoo huku, nami nitakuonyesha yule Bibi-arusi, mke wa Mwana-Kondoo. Akanichukua katika Roho mpaka mlima mkubwa, mrefu, akanionyesha ule mji mtakatifu, Yerusalemu, ukishuka kutoka mbinguni kwa Mwenyezi Mungu; wenye utukufu wa Mungu, na mwangaza wake ulikuwa mfano wa kito chenye thamani nyingi kama kito cha yaspi, safi kama bilauri; ulikuwa na ukuta mkubwa, mrefu, wenye milango kumi na miwili, na katika ile milango malaika kumi na wawili; na majina yameandikwa ambayo ni majina ya kabila kumi na mbili za Waisraeli. Upande wa mashariki milango mitatu; na upande wa kaskazini milango mitatu; na upande wa kusini milango mitatu; na upande wa magharibi milango mitatu. Na ukuta wa mji ulikuwa na misingi kumi na miwili, na katika ile misingi majina kumi na mawili ya wale mitume kumi na wawili wa Mwana-Kondoo.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 145: 10-13, 17-18 (K) 11 

(K) Wacha Mungu wataunena, utukufu wa ufalme wako, Ee Bwana.

Ee Bwana, kazi zako zote zitakushukuru, 
na wacha Mungu wako watakuhimidi.
Wataunena utukufu wa ufalme wako, 
na kuuhadithia uweza wako.

Ili kuwajulisha watu matendo yake makuu,
Na utukufu wa fahari ya ufalme wake.
Ufalme wako ni ufalme wa zamani zote,
Na mamlaka yako ni ya vizazi vyote. (K)

Bwana ni mwenye haki katika njia zake zote,
Na mwenye fadhili juu ya kazi zake zote.
Bwana yu karibu na wote wamwitao,
Wote wamwitao kwa uaminifu. (K)


SHANGILIO
Yn 1: 49

Aleluya, aleluya,
Rabi, wewe u Mwana wa Mungu, ndiwe Mfalme wa Israeli.
Aleluya.


INJILI 
Yn 1: 45-51

Filipo alimwona Nathanaeli, akamwambia, Tumemwona yeye aliyeandikiwa na Musa katika torati, na manabii, Yesu, mwana wa Yusufu, mtu wa Nazareti. Nathanaeli akamwambia, Laweza neno jema kutoka Nazareti? Filipo akamwambia, Njoo uone.

Basi Yesu, akamwona Nathanaeli anakuja kwa- ke, akanena habari zake, Tazama, Mwisraeli kweli kweli, hamna hila ndani yake. Nathanaeli akamwambia, Umepataje kunitambua? Yesu akajibu, akamwambia, Kabla Filipo hajakuita, ulipokuwapo chini ya mtini nilikuona. Nathanaeli akamjibu, Rabi, wewe u Mwana wa Mungu, ndiwe Mfalme wa Israeli. Yesu akajibu, akamwambia, Kwa sababu nilikuambia, Nilikuona chini ya mtini, waamini? Utaona mambo makubwa kuliko haya. Akawaambia, Amin, amin, nawaambia, Mtaziona mbingu zimefunguka na malaika wa Mungu waki- kwea na kushuka juu ya Mwana wa Adamu.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com