Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

KUJENGA JUMUIYA YENYE KUWA NA TAHADHARI!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumapili, Septemba 13,  2026
Juma la 24 la Mwaka wa Kanisa


YbS 27:30-28:1-7
Zab. 103:1-4, 9-12
Rum. 14:7-9
Mt. 18:21-35


KILA MKRISTU NI LAZIMA AWE TAYARI KUSAMEHE WENGINE

Ndugu Zangu, tumesikia neno la Mungu, katika masomo yote matatu. Kama nilivyowadokeza katika utangulizi wangu, kwamba masomo yote, yanaongelea jambo lilio muhimu, katika maisha yetu ya kikristu. Nalo ni kuhusu msamaha. Katika Injili tumesikia, Yesu akiwahitaji wafuasi wake, kuishi maisha ya kusameheana, hivyo nasi wakristo, tunawajibika kuyaishi maisha haya. Kila mkristu ni lazima awe tayari kusamehe wengine, wakati wo wote na bila masharti ye yote. Je, sisi nasi tupo tayari kusamehe? Ni rahisi sana kwetu kuzungumzia kuhusu neno msamaha, lakini linapokufika wewe inakuwa vigumu sana kulitekeleza.

Hebu, tusikilize tukio hili linalowahusu wanawake wawili waliokuwa marafiki wakubwa. Japo nyumba zao zilikuwa siyo karibu sana, lakini mara nyingi walikuwa pamoja. Siku moja kulitokea kutokuelewana baina yao. Kwa sababu ya mambo Fulani-Fulani waliyoyajua wao. Na tangu siku hiyo, urafiki wao ukafikia kikomo na wakawa maadui wakubwa. Viongozi wengi wa dini, waliokuwa wakiufahamu urafiki wao kindani, hasa mapadre, walijitahidi kadiri ya uwezo wao kuwapatanisha, lakini hawakufanikiwa. Ikatokea kuwa wakati wa mgogoro wao huo mimi niliamishiwa maeneo waliyoishi. Kwa vile, niliwafahamu vizuri hawa akina mama, mimi nami niliamua kujaribu bahati yangu ya kuwapatanisha. Hivyo siku moja, nilienda nyumbani kwa mmoja wao, na kuanza kuzungumzia kuhusu neno msamaha. Hususani kwa rafiki yake. Nilimsisitiza kuhusu kusamehe na kusahau tofauti zilizopo baina yao, ili urafiki wao uweze kuendelea. Mnajua alinijibu nini? He! Niko tayari kuingia katika moto wa jehanamu, lakini siyo kumsamehe.

Hivyo tunaweza kuona katika tukio hili ni jinsi gani, mwanamama huyu, alivyokuwa na hasira, na kwamba yupo tayari kwenda jehanamu, lakini siyo kumsamehe mwenzake. Kama hivyo ndivyo tulivyo, tunawezaje kuisema, ile sala aliyotufundisha BY? Ambayo ni sala ya Baba Yetu. Katika sala hii tunasema “utusamehe makosa yetu, kama tunavyowasamehe na sisi wale waliotukosea”. Hii, ina maana kwamba, tunamwomba Mungu atusamehe makosa yetu kama vile, sisi tufanyavyo kwa wenzetu. Hamna shaka NZ, ni wazi kwamba inatuwia vigumu sana kuwasamehe wale waliotusababishia matatizo katika maisha yetu. Lakini swali linabaki, tunaweza kuendelea na kinyongo chetu mpaka lini?

Katika somo la kwanza, tumesikia jinsi hasira na kinyongo vinavyoumiza. Hivyo tunasisitizwa kuwasamehe jirani zetu. Na katika Injili, Yesu anatukumbusha kuhusu kusameheana hasa pale anapomwambia Petro, samehe siyo mara saba tu, bali mara saba sabini. Hivyo na sisi, tunatakiwa kuwasamehe majirani zetu zaidi ya mara saba. Ili tuweze kufanya hivyo tunahitaji kufanya nini?

Kwanza kabisa, ni lazima tusali. Tumwombe Mungu atupe neema ya kuweza kusamehe na pia kusahau. Halafu mwombee na yule aliyekugadhabisha. Wakati Yesu anapotutia moyo wa kuwapenda adui zetu, huwa anatupa pia neema za kutenda hayo. Pili, hebu tujaribu kutafakari ni mara ngapi, Mungu ametusamehe sisi. Yeye ametusamehe mara nyingi zaidi kuliko anavyopenda, sisi kuwasamehe wenzetu. Mungu ni mwenye kusamehe, ni mwenye upendo na ni mwenye huruma kwa wale wote wanaokiuka maagizo yake. Sasa tujiulize ni kwa muda gani, sisi tutaendeleza hasira yetu kwa jirani zetu? Tatu, tujaribu kubadilisha msimamo wetu. Tujaribu kuangalia wale waliotukosea katika muonekano tofauti. Siyo kama adui zetu, bali kama wanadamu na kama tulivyo sisi. Sisi sote tuna vipaji vinavyofanana kama vile, kupenda na kutokupenda, hobi tofauti, muhono tofauti kuhusu mazuri na mabaya na mbaya zaidi tunawaumiza wenzetu, maneno na matendo yetu. Hivyo, pia jirani zetu kama tulivyo, sisi nao pia wanatuumiza kama sisi tunavyoumiza wengine. Ndiyo maana basi, sisi nasi tunahitaji kupata msamaha kutoka kwa wenzetu, kama wao wanaohitaji kutoka kwetu. Kwa hiyo ni jukumu letu kuwasamehe wale waliotukosea.

Yesu alipokuwa pale msalabani aliwaombea watesi wake, “Baba, uwasamehe, kwa kuwa hawajui watendalo” (Lk 23/34). Yesu aliwaona hawa kuwa ni watoto wa Baba ambao wamepotea njia. Kwa hiyo, ni lazima na sisi tuanze kuwaona adui zetu kama vile Yesu alivyowaona watesi wake, na anavyotuona sisi leo hii. Anza leo kutekeleza haya. Omba neema ya kusamehe wengine, na kukumbuka huruma ya Yesu kwetu. Na muone jirani yako au mtesi wako kama ulivyo wewe. Hapo ndipo tutaweza kusamehe na kusahau kama atufanyiavyo Baba yetu wa mbinguni. Katika misa ya leo tumwombe Mungu atupe neema hii ili tuweze kuwa kielelezo bora cha ukristo wetu popote pale tutakapo kuwa.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUMAPILI, SEPTEMBA 13, 2026



MASOMO YA MISA, JUMAPILI, SEPTEMBA 13, 2026
JUMA LA 24 LA MWAKA 
________

MWANZO
YbS 36:15.16

Ee Bwana, uwape amani wakungojao, ili watu wawasadiki manabii wako; usikilize sala ya mtumwa wako, na ya taifa lako Israeli.
________

SOMO I
YbS 27:30-28:1-7

Hasira na ghadhabu, haya pia ni machukuzo na aliye mwenye dhambi yatampata. Mwenye kujilipiza kisasi ataona kisasi kutoka kwa Bwana; hakika Yeye atamfungia dhambi zake. Umsamehe jirani yako dhara alilokufanyia, hivyo nawe utasamehewa dhambi zako wakati utakaposali. Mwanadamu humkasirikia mwanadamu, je! atatafuta kuponywa na Bwana? Hamrehemu mwanadamu aliye mwenzake, je! atalalamika kwa ajili ya dhambi zake mwenyewe? Aliye mwili na damu tu huilisha hasira yake, je! ni nani atakayempatanisha yeye kwa makosa yake? Basi kumbuka mwisho wako, uuache uadui; kumbuka uozi na mauti , ujiepushe na kutenda dhambi. Kumbuka zile amri, usikasirike na jirani yako; nawe ulikumbuke agano lake Aliye juu, umwachilie ujinga wake.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu
________

WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 103:1-4, 9-12

(K) Bwana amejaa huruma na neema, 
si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa fadhili.

Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana,
Naam, vyote vilivyo ndani yangu
Vilihimidi jina lake takatifu.
Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana,
Wala usizisahau fadhili zake zote. (K)

Ndiye anayekusamehe maovu yako yote,
Akuponya magonjwa yako yote.
Akomboa uhai wako na kaburi,
Akutia taji ya fadhili na rehema. (K)

Yeye hatateta siku zote,
Wala hatashika hasira yake milele.
Hatutendei kadiri ya hatia zetu,
Wala halipi kwa kadiri ya maovu yetu. (K)

Maana vile mbingu zilivyoinuka juu ya nchi,
Kadiri ile ile rehema zake ni kuu kwa wamchao.
Kama mashariki ilivyo mbali ma magharibi,
Ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi. (K)
________

SOMO 2 
Rum. 14:7-9

Hakuna mtu miongoni mwetu aishiye kwa nafsi yake, wala hakuna afaye kwa nafsi yake. Kwa maana kama tukiishi, twaishi kwa Bwana, au kama tukifa, twafa kwa Bwana. Basi kama tukiishi au kama tukifa, tu mali ya Bwana. Maana Kristo alikufa akawa hai tena kwa sababu hii, awamiliki waliokufa na walio hai pia.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu
________

SHANGILIO
Yn. 13:34

Aleluya, aleluya,
Amri mpya nawapa, asema Bwana, 
mpendane, kama vile nilivyowapenda ninyi.
Aleluya.
________

INJILI 
Mt. 18:21-35

Petro alimwendea Yesu akamwambia, Bwana ndugu yangu anikose mara ngapi nami nimsamehe? hata mara saba? Yesu akamwambia, Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini.

Kwa sababu hii ufalme wa mbinguni umefanana na mfalme mmoja aliyetaka kufanya hesabu na watumwa wake. Alipoanza kuifanya, aliletewa mtu mmoja awiwaye talanta elfu kumi. Naye alipokosa cha kulipa, bwana wake akaamuru auzwe, yeye na mkewe na watoto wake, na vitu vyote alivyo navyo, akalipwe ile deni. Basi yule mtumwa akaanguka, akamsujudia akisema, Bwana, nivumilie, nami nitakulipa yote pia. Bwana wa mtumwa yule akamhurumia, akamfungua, akamsamehe ile deni. Mtumwa yule akatoka, akamwona mmoja wa wajoli wake, aliyemwia dinari mia; akamkamata, akamshika koo, akisema, Nilipe uwiwacho. Basi mjoli wake akaanguka miguuni pake, akamsihi, akisema, Nivumilie, nami nitakulipa yote pia. Lakini hakutaka, akaenda, akamtupa kifungoni, hata atakapoilipa deni. Basi wajoli wake walipoyaona yaliyotendeka, walisikitika sana, wakaenda wakamweleza bwana wao yote yaliyotendeka. Ndipo bwana wake akamwita, akamwambia, Ewe mtumwa mwovu, nalikusamehe wewe deni ile yote, uliponisihi; nawe, je! haikukupasa kumrehemu mjoli wako, kama mimi nilivyokurehemu wewe? Bwana wake akaghadhibika, akampeleka kwa watesaji, hata atakapoilipa deni ile yote. Ndiyo na Baba yangu wa mbinguni atakavyowatenda ninyi, msiposamehe kwa mioyo yenu kila mtu ndugu yake.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo
________

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MATUNDA MAZURI NA MSINGI MZURI!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumamosi, Septemba 12, 2026 
Juma la 23 la Mwaka

Kumbukumbu ya jumamosi ya Bikira Maria Mtakatifu

1 Kor 10: 14-22
Zab 115: 12-13, 17-18
Lk 6: 43-49


MATUNDA MAZURI NA MSINGI MZURI!

Yesu mara nyingi alitoa mfano kutoka katika mazingira ya asili na kuelezea thamani za Ufalme wa Mungu. Katika Injili ya leo tuna mifano ya tini na zabibu. Mtini ilikuwa ni alama ya rutuba, mafanikio na Amani. Zabibu zinatoa divai, alama ya furaha. Yesu anatumia mifano hii na anawaeleza wafuasi wake kwamba mti unajulikana kwa matunda yake. Ni katika hali hiyo hiyo pia mtu anatoa matunda mazuri au mabaya kulingana na mbegu iliyosiwa moyoni mwake. Na zaidi sana inategemea sana tabia ya mtu katika kuzaa matunda mema au mabaya. Wanaoishi na Roho wa Mungu wanazalisha matunda mema kama, furaha, Amani, uvumilivu, kujali, huruma, uaminifu, upole na kuweza kujizuia na kujiongoza (rej. Wagalatia 5: 22- 23). 

Wale waliyo waaminifu kwa Munguwanajua nguvu zao zipo mikononi mwa Mungu na sio kwao binafsi bali zipo kwa Mungu anayewapa neema tele za kuishi kama wafuasi wake wa kweli. Je nimatunda ghani unayozalisha ili kudhihirisha ulipozamisha mizizi yako? Kwa Mungu au mwili / Dunia?

Pengine tujaribu kujiuliza matendo yangu yanatoa ishara yeyote ya uwepo wa Kristo ndani yangu? Je matendo yangu yanaendana na Imani yangu? Au tunaishi tu na watu wanashindwa kufahamu sisi ni nani? Hatuwezi kujiita wafuasi wa Kristo wakati hatutendi kama Kristo au kama tunatenda tofauti na mapenzi ya Kristo. Matendo yetu na Imani yetu yaendane ili tuweze kuwa zabibu zinazo zaa zabibu na sio zabibu zinazo zaa mchongoma. Tuimarishe hazina njema ya mioyo yetu wenyewe ili iweze kutoa matunda mema kwa njia hii tutakuwa tumejenga msingi wetu katika Kristo na hivyo tutakuwa imara daima dhoruba ijapo tukitambua kwamba hata dhoruba iweje wa mwisho kutenda dhambi ni mimi mwenyewe, hakuna mtu anayemsaidia mtu kutenda dhambi, kwani dhambi huanzia ndani ya moyo wa mtu. Hata vingekuwepo vishawishi vya aina ghani, inabaki kwamba wa mwisho kutenda dhambi ni mtu mwenyewe. Tujenge mzingi mzuri ndani ya Yesu ili tuweze kungara kwa matunda mema.

Sala: Yesu nisaidiye niweze kuzaa matunda mema ya Imani, matumaini na upendo. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA JUMAMOSI, SEPTEMBA 12, 2026



MASOMO YA MISA 
JUMAMOSI, SEPTEMBA 12, 2026
JUMA LA 23 LA MWAKA


KUMBUKUMBU YA JUMAMOSI YA BIKIRA MARIA

SOMO 1
1Kor. 10:14 – 22

Wapenzi wangu, ikimbeni ibada ya sanamu. Nasema kama na watu wenye akili; lifikirini ninyi ninenalo. Kikombe kile cha Baraka tukibarikicho, je! Si ushirika wa damu ya Kristo? Mkate ule tuumegao, si ushirika wa mwili wa Kristo? Mkate ule tuumegao, si ushirika wa mwili wa Kristo? Kwa kuwa mkate ni mmoja, sisi tulio wengi tu mwili mmoja; kwa maana sisi sote twapokea sehemu ya ule mkate mmoja. Waangalieni hao waisraeli walivyokuwa kwa jinsi ya mwili; wale wazilao dhabihu, je! Hawana shirika na madhabahu?

Basi niseme nini? Ya kwamba kile kilicholewa sadaka kwa sanamu ni kitu? Au ya kwamba sanamu ni kitu? Sivyo, lakini vitu vile wavitoavyo sadaka wavitoa kwa mashetani, wala si kwa Mungu; nami sipendi ninyi kushirikiana na mashetani. Hamwezi kunywea kikombe cha Bwana na kikombe cha mashetani. Hamwezi kushirikiana katika meza ya Bwana na katika meza ya mashetani. Au twamtia Bwana wivu? Je! Tuna nguvu zaidi ya yeye?

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 116:12 – 13, 17 – 18 (K) 17

(K) Nitakutolea dhabihu ya kushukuru, Ee Bwana.

Nimrudishie Bwana nini
Kwa ukarimu wake wote alionitendea?
Nitakipokea kikombe cha wokovu;
Na kulitangaza jina la Bwana. (K)

Nitalitangaza jina la Bwana;
Nitaziondoa nadhiri zangu kwa Bwana,
Naam, mbele ya watu wake wote.
Katika nyua za nyumba ya Bwana,
Ndani yako, Ee Yerusalemu. (K)


SHANGILIO
Yn. 8:12

Aleluya, aleluya,
Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, 
asema Bwana, yeye anifuataye 
hatakwenda gizani kamwe, 
bali atakuwa na nuru ya uzima.
Aleluya.


INJILI
Lk. 6:43 – 49

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Hakuna mti mzuri uzaao matunda mabaya, wala mti mbaya uzaao matunda mazuri; kwa kuwa kila mti hutambulikana kwa matunda yake; maana, katika miiba hawachumi tini, wala katika michongoma hawachumi zabibu. Mtu mwema katika hazina njema ya moyo wake hutoa yaliyo mema, na mtu mwovu katika hazina mbovu ya moyo wake hutoa yaliyo maovu; kwa kuwa mtu, kinywa chake hunena yale yaujazayo moyo wake.

Na kwa nini mnaniita, Bwana, walakini hamtendi nisemayo?

Kila mtu ajaye kwangu, na kuyasikia maneno yangu na kuyatenda, nitawaonyesha mfano wake. Mfano wake ni mtu ajengaye nyumba, na kuchimba chini sana, na kuweka msingi juu ya mwamba; na kulipokuja gharika, mto uliishukia nyumba ile kwa nguvu, usiweze kuitikisa; kwa kuwa imejengwa vizuri. Lakini yule aliyesikia ila hakutenda, mfano wake ni mtu aliyejenga nyumba juu ya ardhi pasipokuwa na msingi, mto ukaishukia kwa nguvu, ikaanguka mara; na maangamizi yake nyumba yakawa makubwa.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

UPOFU WA KIROHO!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Ijumaa, Septemba 11, 2026 
Juma la 23 la Mwaka


1 Kor 9: 16-19, 22-27
Zab 83: 3-6, 12
Lk 6: 39-42


UPOFU WA KIROHO!

Mfano kutoka katika Injili ya leo unatukumbusha ni kwa jinsi ghani ilivyo vigumu kwa kipofu kumuongoza kipofu mwenzake. Yesu haulizii kuhusu nguvu ya roho ya mwanadamu kushinda matatizo hayo. Anatuita tutambue upofu wa roho zetu. Tuombe ili upofu wa roho zetu wenyewe uweze kuponywa. Tunahitaji neema ili tuweze kuwa waaminifu kwa nafsi zetuni katika kutambua kikomo chetu, changamoto na udhaifu wetu.

Katika somo la kwanza Paulo anatuhimiza tupige mbio kila wakati tukililenga lile taji alilotuandalia Kristo mwenyewe kwani huo ndio ushindi wetu. Anatuhimizi tujifunze pia kuishi na wanyonge ili kwa hilo tuwapate wanyonge. Anatufundisha unyenyekevu katika maisha ya kumtangaza Kristo. Kwakufanya hivyo Injili tunayoihubiri italeta mafanikio kwa watu na zaidi sana kwetu sisi wenyewe. Paulo aliona pia hatari yakuweza kuwafundisha watu maneno ya Yesu na kuwasaidia lakini binafsi ukajisahau. Mhubiri wa kweli anajihubiria mwenyewe kwanza na baadae inatoka kwake na kuwagusa wengine. Kwahiyo Paulo anatuhimiza leo pia tuchunguze nafsi zetu kabla hatujaenda kwa wengine. 

Sala: Bwana, tusaidie tuweze kuwa Wafuasi wazuri. Tusaidie tuweze kujifunza jinsi ya kurekebisha maisha yetu wenyewe kabla hatuja angalia matendo ya wengine. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA IJUMAA, SEPTEMBA 11, 2026




MASOMO YA MISA 
IJUMAA, SEPTEMBA 11, 2026
JUMA LA 23 LA MWAKA


SOMO 1
1Kor. 9:16-19, 22-27

Ijapokuwa naihubiri Injili, sina la kujisifia; maana nimewekewa sharti; tena ole wangu nisipoihubiri Injili! Maana nikiitenda kazi hii kwa hiari yangu nina thawabu; ila ikiwa si kwa hiari yangu, nimeaminiwa uwakili. Basi thawabu yangu ni nini? Ni hii, ya kuwa nihubiripo, nitaitoa Injili bila gharama, bila kutumia kwa utimilifu uwezo wangu nilio nao katika Injili.

Maana, ingawa nimekuwa huru kwa watu wote, nalijifanya mtumwa wa wote, ili nipate watu wengi zaidi. Kwa unyonge nalikuwa mnyonge, ili niwapate wanyonge. Nimekuwa hali zoTe kwa watu wote, ili kwa njia zote nipate kuwaokoa watu. Nami nafanya mambo yote kwa ajili ya Injili ili kuishiriki pamoja na wengine.

Je! Hamjui, ya kuwa wale washindanao kwa kupiga mbio, hupiga mbio wote lakini apokeaye tuzo ni mmoja? Pigeni mbio namna hiyo, ili mpate. Na kila ashindanaye katika michezo hujizuia katika yote; basi hao hufanya hivyo kusudi wapokee taji iharibikayo; bali sisi tupokee taji isiyoharibika. Hata mimi napiga mbio vivyo hivyo, si kama asitaye; napiga ngumi vivyo hivyo, si kama apigaye hewa; bali nautesa mwili wangu na kuutumikisha; Isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 84:2 – 5, 7, 11 (K) 1

(K) Maskani zao zapendeza kama nini, Ee Bwana wa majeshi.

Nafsi yangu imeziona shauku nyua za Bwana,
Naam, na kuzikondea.
Moyo wangu na mwili wangu
Ninamlilia Mungu aliye hai. (K)

Shomoro naye ameona nyumba,
Na mbayuwayu amejipatia kioto,
Alipoweka makinda yanke,
Kwenye madhabahu zako, Ee Bwana wa majeshi,
Mfalme wangu na Mungu wangu. (K)

Heri wakaao nyumbani mwako,
Wanakuhimidi daima.
Heri ambaye nguvu zake zatoka kwako,
Na njia ziendazo Sayuni zimo moyoni mwake.
Huendelea toka nguvu hata nguvu,
Huonekana Sayuni kila mmoja mbele za Mungu. (K)

Kwa kuwa Bwana, Mungu, ni jua na ngao,
Bwana atatoa neema na utukufu.
Hatawanyima kitu chema
Hao waendao kwa ukamilifu. (K)


SHANGILIO
Mt. 11:25

Aleluya, aleluya,
Nakushukuru Baba, Bwana wa mbingu na nchi, 
kwa kuwa mambo haya uliwaficha
wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga.
Aleluya.


INJILI
Lk. 6:39 – 42

Yesu aliwaambia wanafunzi wake mithali, Je! Aliye kipofu aweza kuongoza kipofu? Hawatatumbukia shimoni wote wawili? Mwanafunzi hawi mkuu kuliko mwalimu wake, lakini kila mtu ambaye amehitimu hulingana na mwalimu wake. Basi, mbona wakitazama kibanzi kilicho ndani ya jicho la ndugu yako, na boriti iliyo ndani ya jicho lako mwenye huiangalii? Au, utawezaje kumwambia ndugu yako, Ndugu yangu, niache nikitoe kibanzi kilicho ndani ya jicho lako, nawe huiangalii boriti iliyo ndani ya jicho lako mwenyewe? Mnafikiri wewe, itoe kwanza ile boriti katika jicho lako mwenyewe, ndipo utakapoona vema kukitoa kile kibanzi kilichomo katika jicho la ndugu yako.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

WAPENDE MAADUI



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Alhamisi, Septemba 10,  2026, 
Juma la 23 la Mwaka

1Kor 8: 1-7, 11-13; 
Zab 139: 1-3, 13-14, 23-24; 
Lk 6: 27-38


WAPENDE MAADUI 

Yesu aliwaambia wafuasi wake: “kwenu sikieni wapendeni maadui zenu, watendeeni mema wanao wachukia, wabarikini wanao walaani, waombeeni wanao watenda vibaya.” - Luka 6:27-28

Maneno haya ni marahisi sana kuyasema kuliko kuyatenda. Wakati watu wamekutendea vibaya kwa kukutenda vibaya unachopaswa kufanya ni kuwapenda na kuwaombea. Na Yesu anasema kwa uhakika kwamba hichi ndicho tulichoitwa kufanya. 

Katikati ya mateso na vita inayofanywa juu yetu ni rahisi kuumia. Na huku kuumia kunaweza kutufanya tupatwe na hasira na kutaka kurudisha kisasi na hata chuki. Kama tutakubali kuingia katika kishawishi hichi tutakuwa sisi wenyewe tumeamua kujiumiza. Ukweli ni kwamba kuwachukia wale waliotuumiza hufanya mambo yawe mbaya zaidi. 

Lakini tutakuwa waongo kusema ukweli kuhusu nguvu inayotusukuma kutoka ndani mwetu hasa pale tunapokosewa na inavyokuwa vigumu kutimiza maneno ya Yesu ya kurudisha kwa upendo. Ili kuwa waaminifu ni vizuri tukubali ukweli huu kwanza. Nguvu hii huondoka ndani pale tunapojaribu kushika upendo licha ya hasira na hisia tulizo nazo. 

Hisia hizi zinatujulisha kwamba Mungu anahitaji mengi zaidi kutoka kwetu na sio kuongozwa na hisia hizi. Kuwa na hasira au chuki sio kitu cha kufurahisha. Ukweli ni kwamba kinaweza kuwa ni kitendo cha mateso makubwa, lakini haipaswi kuwa hivyo. Kama tumeeelewa ujumbe huu wa Yesu njia yake ni njia nzuri ya kukwepa mateso haya. Tutatambua kwamba kulipiza kisasa hufanya kidonda kiwe kikubwa zaidi na zaidi. Tukijifunza kupenda pale mahali ambapo tumetendewa vibaya tunatambua kwamba upendo katika hali hii huwa na nguvu sana. Ni upendo ndio unaoenda zaidi ya hisia. Upendo huu tumepewa kama zawadi kutoka kwa Mungu. Ni upendo na ukarimu ndio unatufanya tuwe na furaha ya kweli..

Tafakari leo juu ya kidonda chochote kile unachokibeba ndani mwako. Tambua kwamba vidonda hivi vinaweza kuwa sababu ya utakatifu wako na furaha yako kama utamruhusu Mungu akubadilishe na kuanza kuwatendea kwa upendo wale waliokutenda mabaya. 

Sala: Bwana, ninatambua kwamba nimeitwa niwapende maadui wangu. Ninatambua kwamba nimeitwa niwapende wale wote walionitenda mabaya. Nisaidie niweze kukabidhi kwako hisia zote za chuki au hasira naomba uvibadilishe kwa upendo wa kweli. Yesu nakuamini wewe. Amina


.Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 10, 2026



MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 10, 2026
ALHAMISI, JUMA LA 23 LA MWAKA

SOMO 1
1Kor. 8:1-7, 11-13

Twajua ya kuwa sisi sote tuna ujuzi. Ujuzi huleta majivuno, bali upendo hujenga. Mtu akidhani ya kuwa anajua neno, hajui neno lolote bado, kama impasavyo kujua. Lakini mtu akimpenda Mungu, huyo amejulikana naye. Basi kwa habari ya kuvila vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu; twajua ya kuwa sanamu si kitu katika ulimwengu, nay a kuwa hakuna Mungu ila mmoja tu. Kwa maana ijapokuwa wako waitwao miungu, ama mbinguni ama duniani, kama vile walivyoko miungu mingi na mabwana wengi; lakini kwetu sisi Mungu ni mmoja tu, aliye Baba, ambaye vitu vyote vimetoka kwake, nasi tunaishi kwake; yuko na Bwana mmoja Yesu Kristo, ambaye kwake vitu vyote vimekuwapo, na sisi kwa yeye huyo.

Bali ujuzi huu haumo ndani ya watu wote; ila wengine kwa kuizoelea ile sanamu hata sasa hula kana kwamba ni kitu kilichotolewa sadaka kwa sanamu; na dhamiri zao, kwa kuwa dhaifu, hunajisika. Na yule aliye dhaifu aangamizwa kwa ujuzi wako, naye ni ndugu ambaye Kristo alikufa kwa ajili yake. Hivyo, mkiwatenda dhambi ndugu zenu na kuitia jeraha dhambiri iliyo dhaifu, mnamtenda dhambi Kristo. Kwa hiyo, chakula kikimkwaza ndugu yangu, hakika sitakula nyama hata milele, nisije nikamkwaza ndugu yangu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 139:1-3, 13-14, 23-24 (K) 24

(K) Uniongoze, Bwana, katika njia ya milele.

Ee Bwana umenichunguza na kunijua.
Wewe wajua kuketi kwangu na kuondoka kwangu;
Umelifahamu wazo langu tokea mbali.
Umepepeta kwenda kwangu na kulala kwangu,
Umeelewa na njia zangu zote. (K)

Maana Wewe ndiwe uliyeniumba mtima wangu,
Uliniunga tumboni mwa mama yangu.
Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa
Kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. (K)

Ee Mungu, unichunguze, uujue moyo wangu,
Unijaribu, uyajue mawazo yangu;
Uone kama iko njia iletayo majuto ndani yangu,
Ukaniongoze katika njia ya milele. (K)


SHANGILIO
Zab. 147:12,15

Aleluya, aleluya,
Msifu Bwana, Ee Yerusalemu, huipeleka amri yake juu ya nchi.
Aleluya.


INJILI
Lk. 6:27-38

Yesu aliwaambia wafuasi wake: Nawaambia ninyi mnaosikia, Wapendeni adui zenu, watendeeni mema wale ambao wawachukia ninyi, wabarikieni wale ambao wawalaani ninyi, waombeeni wale ambao wawaonea ninyi. Akupigaye shavu moja, mgeuzie la pili, naye akunyang’anyaye joho yako, usimzuilie na kanzu. Mpe kila akuombaye, na akunyang’anyaye vitu vyako, usitake akurudishie. Na kama mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni vivyo hivyo.

Maana mkiwapenda wale wawapendao ninyi, mwaonyesha fadhili gani? Kwa kuwa hata wenye dhambi huwapenda wale wawapendao. Nanyi mkiwatendea mema wale wawatendao mema, mwaonyesha fadhili gani? Hata wenye dhambi hufanya vivyo hivyo. Na mkiwakopesha watu huku mkitumaini kupata kitu kwao, mwaonyesha fadhili gani? Hata wenye dhambi huwakopesha wenye dhambi, ili warudishiwe vile vile.

Bali wapendeni adui zenu, tendeni mema, na kukopesha msitumaini kupata malipo, na thawabu yenu itakuwa nyingi; nanyi mtakuwa wana wa Aliye juu, kwa kuwa yeye ni mwema kwa wasiomshukuru, na waovu.

Basi, iweni na huruma, kama Baba yenu alivyo na huruma. Msihukumu, nanyi hamtahukumiwa; msilaumu, nanyi hamtalaumiwa; achilieni, nanyi mtaachiliwa. Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwasukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

KIU YA KUTAKA FURAHA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatano, Septemba 9, 2026
Juma la 23 la Mwaka


1 Kor 7: 25-31; 
Ps 44: 11-12, 14-17; 
Lk 6: 20-26


KIU YA KUTAKA FURAHA!

Kila moyo wa mwanadamu umeumbwa kwa ajili ya furaha. Mungu mwenyewe, katika Utatu Mtakatifu, ndiye Furaha Kuu, ndiye Furaha yote. Masomo yetu ya leo yanatuambia kwamba maskini wapo katika hali salama zaidi kuliko matajiri. Moyo wa Mwanadamu, na uzuri wake na uwezo wake wakupata utakatifu, unachafuliwa, unazimwa na kuharibiwa kwa kuwa mtumwa wa mali na anasa. Tamaa isiyo na mpangilio ya fedha, nyumba, ardhi na vitu vimechafua furaha ya watu wengi na pia furaha ya familia mbali mbali. 

Leo Injili inaongelea pia kitu kingine kinachochafua roho nyingi: tamaa ya anasa na kusifiwa (kijenga jina). “Ole wenu ninyi watu wote watakapo wasifu, kwakuwa baba zao waliwatenda manabii wa uongo mambo kama hayo” (Lk 6: 26). “heri yenu ninyi watu watakapo wachukia, na kuwatenga, na kuwashutumu, na kulitupa nje jina lenu kama neno ovu, kwa ajili ya Mwana wa Adamu. Furahini na kuruka-ruka, kwakuwa, tazama, thawabu yenu ni kubwa mbinguni, maana, baba zao waliwatenda manabii vivyo hivyo.” (Lk 6: 22-23). 

Yesu anataka kutuambia kwamba watu wakweli wanaomfuata watapata mateso mengi, haitakuwa rahisi njia ya Yesu, mtu anapaswa kusema ukweli hata pale inapo hatarisha maisha yake, kama vile manabii wa ukweli walivyoteseka zamani. Sifa za nabii wa ukweli ni kwamba hakuambii kile ambacho unachotaka kusikia bali anasema ukweli kwasababu ni ukweli. Manabii wengi walipoteza maisha yao kwasababu waliitwa na wafalme ili kutoa unabii juu ya jambo Fulani, lakini wao kwa ujasiri walisema ukweli hata kumrekebisha mfalme na hapo maisha yao yakawa hatarini. Mfalme alitegemea kusikia akisifiwa tu, lakini manabii wa kweli walisema ukweli, huu ndio wito anaotuambia Yesu. Tusiwe kama nmanabii wa uongo wanaopenda kuongea tu kile ambacho watu wanapenda kusikia bali tuseme ukweli kwasababu ni jambo la kweli. 

Sala: “Umetuumba kwa ajili yako mwenyewe, ee Bwana! Na roho zetu hazitatulia mpaka zitakapo tulia kwako.” (Mt. Agustino)  Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA JUMATANO, SEPTEMBA 9, 2026



MASOMO YA MISA 
JUMATANO, SEPTEMBA 9, 2026
JUMA LA 23 LA MWAKA


SOMO 1
1Kor. 7:25 – 31

Kwa habari za wanawali sina amri ya Bwana, lakini natoa shauri langu, mimi niliyejaliwa kwa rehema za Bwana kuwa mwaminifu. Basi, naona hili kuwa jema, kwa ajili ya shida iliyopo, kwamba ni vema mtu akae kama alivyo. Je! Umefungwa kwa mke? Usitake kufunguliwa. Umefunguliwa? Usitafute mke. Lakini, kama ukioa, huna hatia; wala mwanamwamli akiolewa, hana hatia; lakini watu kama hao watakuwa na dhiki katika mwili; name nataka kuwazuilia hayo.

Lakini, ndugu, nasema hivi, muda ubakio si mwingi; basi tokea sasa wale walio na wake na wawe kama hawana; na wale waliao kama hawalii; na wale wafurahio kama hawafurahi; na wale wanunuao, kama hawana kitu. Na wale wautumiao ulimwengu huu, kama hawautumii sana; kwa maana mambo ya ulimwengu huu yanapita.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 45:10 – 11, 13 – 16 (K) 10

(K) Sikia, binti, utazame, utege sikio lako.

Sikia, binti, utazame, utege sikio lako, 
Uwasahau watu wako na nyumba ya baba yako.
Naye mfalme atautamani uzuri wako,
Maana ndiye bwana wako, nawe umsujudie. (K)

Binti mfalme yumo ndani ana fahari tupu, 
Mavazi yake ni nyuzi za dhahabu.
Atapelekwa kwa mfalme
Wanawali wenzake wanaomfuata. (K)

Watapelekwa kwa furaha na shangwe,
Na kuingia katika nyumba ya mfalme.
Badala ya baba zako watakuwapo watoto wako, 
Utawafanya kuwa wakuu katika nchi zote. (K)


SHANGILIO
Zab. 119:105

Aleluya, aleluya,
Neno lako ni taa ya miguu yangu, 
na mwanga wa njia yangu.
Aleluya.


INJILI
Lk. 6:20 – 26

Yesu aliinua macho yake akawatazama wanafunzi wake, akasema,
Heri ninny imlio maskini, kwa sababu ufalme wa Mungu ni wenu.
Heri ninyi mlio na njaa sasa, kwa sababu mtashiba.
Heri ninny mliao sasa, kwa sababu mtacheka.

Heri ninyi watu watakapowachukia na kuwatenga, na kuwashutumu, na kulitupa nje jina lenu kama neno ovu, kwa ajili ya Mwana wa Adamu.

Furahiwani siku ile na kuruka-ruka, kwa kuwa, tazama, thawabu yenu ni kubwa mbinguni; maana, baba zao waliwatenda manabii vivyo hivyo.

Lakini, ole wenu ninyi mlio na mali, kwa kuwa faraja yenu mmekwisha kuipata.

Ole wenu ninyi ambao mmeshiba sasa, kwa kuwa mtaona njaa.
Ole wenu ninyi mnaocheka sasa, kwa kuwa mtaomboleza na kulia.
Ole wenu ninyi watu wote watakapowasifu, kwa kuwa baba zao waliwatenda manabii wa uongo mambo kama hayo.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.