Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MAFUMBO YA UFALME WA MUNGU!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Kila siku
Alhamisi, 23 Julai, 2026, 
Juma la 16 la Mwaka



Yer 2:1-3, 7-8, 12-13
Zab 36:5-10 (K) 9
Mt 13:10-17



MAFUMBO YA UFALME WA MUNGU!


Katika maisha, mara nyingi tunadadisi, vilevile tunashangazwa na fumbo. Pale tunapopoteza hali ya fumbo katika dini ndipo Mungu anakuja kuwa kama wazo tu. Katika nyakati ya Yesu, Mungu amekuwa kama kitu kilichopo akilini mwa watu tu na si mioyoni mwao. Yesu anamnukuu nabii isaya katika injili: “maana mioyo ya watu hawa inakuwa mizito, na kwa masikio yao hawasikii vyema na macho yao wameyafumba.” Aliwaambia wanafunzi wake kwamba si kila mmoja ataelewa mifano. Yesu aliongea hayo kutokana na uzoefu. Alielewa kwamba baadhi yao ambao walisikia mifano yake walikataa kuielewa, si kwamba akilio zao hazikuweza kuelewa, bali, walifunga mioyo yao kwa yale aliyokuwa akisema Yesu. Walikuwa wameweka nia ya kutokuamini.

Mungu huweza kufunua siri za ufalme wake kwa mnyenyekevu na mtu anayemtegemea na kukiri uhitaji wa Mungu na ukweli wake. Mifano ya Yesu itatuangaza sisi kama tukiipokea kwa akili na mioyo radhi na kuwa tayari kukubali itupe changamoto. Neno la Mungu linaweza tu kuota mizizi katika moyo unaokubali na kuamini na kujitoa kwa hiari.

Sala: Bwana nakukaribisha moyoni na akilini mwangu uniangaze, unipe changamoto na unibadilishe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JULAI 23, 2026



MASOMO YA MISA, JULAI 23, 2026
ALHAMISI, JUMA LA 16 LA MWAKA


SOMO 1
Yer. 2:1-3, 7-8, 12-13

Neno la Bwana likanijia, kusema, Enenda ukalie masikioni mwa Yerusalemu, ukisema, Bwana asema hivi, Nakumbuka hisani ya ujana wako, upendo wa wakati wa uposo wako; Jinsi ulivyonifuaata huko jangwani, katika nchi isiyopandwa mbegu. Israeli walikuwa utakatifu kwa Bwana; Malimbuko ya uzao wake; Wote watakaomla watakuwa na hatia; uovu utawajilia; asema Bwana.

Nami nitawatia katika nchi ya shibe, mpate kula matunda yake na mema yake; lakini ninyi mlipoingia katika nchi ile, mliitia unajisi nchi yangu, na urithi wangu mliufanya kuwa chukizo. Makuhani hawakusema, Yuko wapi Bwana? Wala wanasheria hawakunijua; wachungaji nao waliniasi, nao manabii walitoa unabii kwa Baali, wakafuata mambo yasiyofaidia kitu.

Enyi mbingu, staajabuni kwa ajili ya jambo hili, mkaogope sana, na kuwa ukiwa sana, asema Bwana. Kwa maana watu wangu hawa wametenda maovu mawili; wameniacha mimi, niliye chemchemi ya maji ya uzima, wamejichimbia mabirika, mabirika yavunjayo, yasiyoweza kuweka maji.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 36:5 – 10 (K) 9

(K) Kwako Bwana iko chemchemi ya uzima.

Ee Bwana, fadhili zako zafika hata mbinguni,
Uaminifu wako hata mawinguni.
Haki yako ni kama milimo ya Mungu,
Hukumu zako ni vilindi vikuu. (K)

Ee Bwana, unawaokoa wanadamu na wanyama.
Ee Mungu, jinsi zilivyo na thamani fadhila zako! Wanadamu huukimbilia uvuli wa mbawa zako.
Watashibishwa kwa unono wa nyumba yako,
Nawe utawanywesha mto wa furaha zako. (K)

Maana kwako Wewe iko chemchemi ya uzima,
Katika nuru yako tutaona nuru.
Uwadumishie wakujuao fadhili zako,
Na wanyofu wa moyo uaminifu wako. (K)



SHANGILIO
Zab. 147:12, 15

Aleluya, aleluya,
Msifu Bwana, ee Yerusalemu, huipeleka amri yake juu ya nchi.
Aleluya.



INJILI
Mt. 13:10 – 17

Wanafunzi walimwambia Yesu, Kwa nini wasema nao kwa mifano? Akajibu akawaambia, Ninyi mmejaliwa kuzijua siri za ufalme wa mbinguni, bali wao hawakujaliwa. Kwa maana yeyote mwenye kitu atapewa, naye atazidishiwa tele; lakini yeyote asiye na kitu, hata kile alichonacho hata kile alicho nancho atanyang’anywa. Kwa sababu hii nasema nao kwa mifano kwa kuwa wakitazama hawaoni, na wakisikia hawasikii, wala kuelewa. Na neno la nabii Isaya linatimia kwao, likisema, Kusikia mtasikia, wala hamtaelewa; kutazama mtatazama, wala hamtaona. Maana mioyo ya watu hawa imekuwa mizito, na kwa masikio yao hawasikii vema, na macho yao wameyafumba; wasije wakaona  kwa macho yao, wakasikia kwa masikio yao, wakaelewa kwa mioyo yao, wakaongoka, nikawaponya.

Lakini, heri macho yenu, kwa kuwa yanaona; na masikio yenu, kwa kuwa yanasikia. Kwa maana, amin, nawaambia, Manabii wengi na wenye haki walitamani kuyaona mnayoyaona ninyi, wasiyaone na kuyasikia mnayoyasikia ninyi, wasiyasikie.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 2026 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUZAMA KATIKA KRISTO!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatano, Julai 22, 2026, 
Juma la 16 la Mwaka

Sikukuu ya Mt. Maria Magdalena


Wim 3:1-4 or 2Kor 5:14-17; 
Zab 63: 1-5, 7-8; 
Yn 20:1-2, 11-18.


KUZAMA KATIKA KRISTO!

Maria Magdalena anachukuliwa kama mwanamke muhimu wa pili katika Agano Jipya baada ya Bikira Maria, Mama wa Yesu. Alisafiri na Yesu katika maisha yake ya utume na alishuhudia matukio mawili ya katika maisha ya Yesu, Mateso na ufufuko. Injili inamuelezea kama Mwanamke jasiri aliye simama na Yesu wakati wa mateso, kifo.

Maria Mgadalene ni mfano wa kweli na ulio kamili katika kuinjilisha, Mwinjilishaji wa ujumbe kamili wa furaha ya Pasaka. Mwanamke huyu “ambaye alimpenda sana Bwana na Bwana alimpenda”. Alikuwa ni mmoja wapo wa wafuasi waliomfuata Yesu, alimsindikiza hata katika safari yake ya mateso na hata bustanini alipokutana naye, alikuwa ni shuhuda wa kwanza wa “huruma ya Kimungu”. Injili ya Yohane inatuambia kuwa Maria Magdalena alilia kwasababu hakuona mwili wa Yesu (Yn 20:11); na Yesu alikuwa na huruma kwake kwa kujionesha kwake kama Mwalimu wake, na kugeuza machozi yake kuwa furaha ya Pasaka.

Alikuwa na heshima ya kuwa shuhuda wa kwanza wa ufufuko wa Yesu, wa kwanza kuona kaburi li wazi na wa kwanza kusikia habari za ufufuko. Yesu anaonesha kujali kwa namna ya pekee kwa huyu mwananmke na kumuonesha huyu mwanamke huruma ya pekee kwasababu mwanamke huyu alionesha mapendo kwa Kristo kwa kumtafuta katika bustani na hata katika mateso. Katika hali hii tunaweza kulinganisha mwanamke aliye anguka katika bustani ya Edeni na mwanamke huyu katika bustani wakati wa ufufuko. Wakwanza alileta kifo kwa mwanandamu na wa pili anatangaza uzima akiwa kaburini.

Katika bustani ya ufufuko Bwana wetu alimwambia Maria “usinishike” (Yn 20:17). Huu ni mwaliko wa kuingia katika Imani inayo zidi mambo yanayo onekana na zaidi ya akili ya mwanadamu baada ya kukutana na mafumbo ya Kimungu ambayo hayatangazwi kwa Maria tu bali kwa Kanisa zima. Huu ni mwaliko kwa kila mfuasi wa Yesu aache kutafuta utukufu binafsi au utukufu wa dunia hii, lakini kwa Imani kumtafuta Mungu anaye ishi na mfufuka.

Alikuwa shuhuda wa kwanza wakumuona Bwana mfufuka, alikuwa pia wa kwanza kutoa ushuhuda kwa mitume wake. Alitimiza amri ya Bwana mfufuka: “nenda ukawaambie ndugu zangu, napaa kwa Baba yangu na Baba yenu, kwa Mungu wangu na Mungu wenu”. Maria Magdalena aliondoka na kutangaza kwamba amemuona Bwana na kwamba amemuambia mambo haya (Yn 20:17-18). Na hivyo, akawa muinjilishaji, mjumbe anaye hubiri habari njema za ufufuko wa Bwana. Alitangaza kwa mitume kitu ambacho wangekuja kukitangaza baadae katika ulimwengu wote. Na hivyo anaitwa “Mtume kwa Mitume”. Yeye ni shuhuda wa Yesu mfufuka na ametangaza ujumbe huu kama Mitume wengine walivyofanya. Utume huu wa wamanamke huyu ni mfano kamili wa wanawake wote katika kanisa la sasa!

Tafakari tamaa ya Bwana wetu kwamba sisi siku moja tufurahi naye mbinguni. Tumsikie akituambia “Napaa kwa Baba na kualika kujiunga nami kwa moyo wako wote. Nikaribishe ndani mwako na niruhusu mimi niweze kuungana nawe. Ninakupenda Bwana na ninatamani kuwa mmoja pamoja nawe. Bwana niruhusu niingie moyoni mwako nawe uwe moyoni mwangu.

Sala: Bwana, ninataka kuzama ndani yako. Ninatamani kuungana nawe katika hali zote. Njoo uishi moyoni mwangu na nifanye niwe mmoja nawe. Yesu, nakutumainia wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JULAI 22, 2026




MASOMO YA MISA, JUMATANO, JULAI 22, 2026
JUMA LA 16 LA MWAKA


SIKUKUU YA MT. MARIA MAGDALENA


SOMO 1
Wim. 3 :1-4

Usiku kitandani nalimtafuta mpendwa wa nafsi yangu, Nalimtafuta, nisimpate. Nikasema, Haya, niondoke nizunguke mjini, Katika njia zake na viwanjani, Nimtafute mpendwa wa nafsi yangu. Nikamtafuta, nisimpate. Walinzi wazungukao mjini waliniona; Je! mmemwona mpendwa wa nafsi yangu? Kitambo kidogo tu nikiisha kuwaondokea, Nikamwona mpendwa wa nafsi yangu.

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu

Au

SOMO 1 
2 Kor. 5 :14-17

Upendo wa Kristo watubidisha; maana tumehukumu hivi, ya kwamba mmoja alikufa kwa ajili ya wote, basi walikufa wote; tena alikufa kwa ajili ya wote, ili walio hai wasiwe hai tena kwa ajili ya nafsi zao wenyewe, bali kwa ajili yake yeye aliyekufa akafufuka kwa ajili yao.

Hata imekuwa, sisi tangu sasa hatumjui mtu awaye yote kwa jinsi ya mwili. Ingawa sisi tumemtambua Kristo kwa jinsi ya mwili, lakini sasa hatumtambui hivi tena, Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita; tazama! yamekuwa mapya.

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI
Zab 63: 1-5, 7-8 (K) 1

(K) Nafsi yangu inakuonea kiu, Ee Bwana.

Ee Mungu, Mungu wangu, nitakutafuta mapema, 
Nafsi yangu inakuonea kiu,
Mwili wangu wakuonea shauku,
Katika nchi kame na uchovu, isiyo na maji. (K)

Ndivyo nilivyokutazama katika patakatifu,
Nizione nguvu zako na utukufu wako.
Maana fadhili zako ni njema kuliko uhai;
Midomo yangu itakusifu. (K)

Ndivyo nitakavyokubariki maadamu ni hai;
Kwa jina lako nitaiinua mikono yangu.
Nafsi yangu itakinai kama kushiba mafuta na vinono; 
Kinywa changu kitakusifu kwa midomo ya furaha. (K)

Maana Wewe umekuwa msaada wangu,
Na uvulini mwa mbawa zako nitashangilia.
Nafsi yangu inakuandama sana;
Mkono wako wa kuume unanitegemeza. (K)


SHANGILIO

Aleluya, aleluya, 
Maria tuambie: sema uliyoona njiani. 
Kaburi lilimfadhi yule aliye Mzima; 
Niliona utukufu wa Kristu alipokuwa akifufuka. 
Aleluya.


INJILI 
Yn. 20 :1-2, 11-18

Siku ya kwanza ya juma Mariamu Magdalena alikwenda kaburini alfajiri, kungali giza bado; akaliona lile jiwe limeondolewa kaburini. Basi akaenda mbio, akafika kwa Simoni Petro na kwa yule mwanafunzi mwingine ambaye Yesu alimpenda, akawaambia, wamemwondoa Bwana kaburini, wala hatujui walikomweka

Lakini Mariamu alikuwa akisimama karibu na kaburi, nje yake, analia. Basi akilia hivi, aliinama na kuchungulia ndani ya kaburi. Akaona malaika wawili, wenye mavazi meupe, wameketi, mmoja kichwani na mmoja miguuni, hapo ulipolazwa mwili wake Yesu. Nao wakamwambia, Mama, unalilia nini? Akawaambia, Kwa sababu wamemwondoa Bwana wangu, wala mimi sijui walikomweka. Naye akiisha kusema hayo, akageuka nyuma, akamwona Yesu amesimama, asijue ya kuwa ni Yesu. Yesu akamwambia, Mama unalilia nini? Unamtafuta nani? Naye, huku akidhania ya kuwa ni mtunza bustani, akamwambia, Bwana, ikiwa umemchukua wewe, uniambie ulipomweka, nami nitamwondoa.

Yesu akamwambia, Mariamu. Yeye akageuka, akamwambia kwa Kiebrania, Raboni! (yaani, Mwalimu wangu). Yesu akamwambia. Usinishike; kwa maana sijapaa kwenda kwa Baba. Lakini enenda kwa ndugu zangu ukawaambie, Ninapaa kwenda kwa Baba yangu naye ni Baba yenu, kwa Mungu wangu naye ni Mungu wenu. Mariamu Magdalene akaenda, akawapasha wanafunzi habari ya kwamba, Nimemwona Bwana, na ya kwamba amemwambia hayo.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 2026 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MAPENZI YA MUNGU!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumanne, Julai 21, 2026, 
Juma la 16 la Mwaka wa Kanisa


Mik 7: 14-15, 18-20; 
Zab 85: 2-8; 
Mt 12: 46-50


MAPENZI YA MUNGU!


Somo la Injili ya leo linatoa nafasi ya kuongea kuhusu Bikira Maria. Wengi wanaosoma sehemu hii ya injili hudhani kwamba Yesu alikuwa akijiweka mbali na Mama yake au kumtenga Mama yake. Lakini ukweli ni kwamba maneno ya Yesu yanatangaza ukweli zaidi kuliko maneno mengine. Kwasababu yanaeleza ni kwa jinsi gani mmoja anaweza kuwa mmoja katika familia yake. Na hili linatokea pale mmoja “anapofanya mapenzi ya Baba yake”. Ni nani aliyefanya mapenzi ya Mungu kama Bikira Maria? Ni nani aliyekuwa mtii kwa Mungu zaidi ya Bikira Maria? Hakuna hata mmoja. Alitenda kwa utii mkamilifu siku zote za maisha yake, na hivyo alitimiza vigezo vyakuwa mmoja katika familia ya Yesu. Maria ni Mwanadamu pekee aliyeshiriki moja kwa moja kwenye Mwili wa Kristo. Lakini Yesu anatutaka sisi wote tuweze kuwa katika familia yake. Tunaweza kuwa kaka zake, dada zake, baba zake na Mama zake kwa kufanya mapenzi ya Mungu. 

Tafakari leo juu ya kazi aliyonayo Mama Maria katika maisha yetu. Mungu anakutaka wewe umuheshimu, kumuiga na kumfanya mmoja wa familia yako. Anataka wewe umpokee kama mama yako wa kiroho kwasababu wewe ni mmoja katika familia yake. Kama unajitahidi kuwa mtii kwa Mungu na kutenda mapenzi yake utashiriki pia katika baraka za maisha yake. Moja wapo wa hizo baraka ni Bikira Maria kuwa Mama yako. Huwezi kuwa mmoja wa Familia ya Yesu alafu umkatae mama yake.

Sala: Bwana, ninatamani kuwa mtii kwako na kutenda mapenzi yako katika kila kitu. Ninatamani kukumbatia daima mapenzi kamili ya Mungu katika maisha yangu. Katika kutenda mapenzi haya Matakatifu, nisaidie niweze kushiriki kikamili na kuwa mmoja wa familia yako kikamilifu. Yesu, nakuamini wewe. Maria Mtakatifu Mama wa Mungu tunakuomba sisi tuweze kuwa karibu na Mwanao Yesu, kwa kutenda mapenzi yake muda wote. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JULAI 21, 2026




MASOMO YA MISA, JULAI 21, 2026
JUMANNE, JUMA LA 16 LA MWAKA


SOMO 1
Mik. 7:14 – 15, 18 – 20

Walishe watu wako kwa fimbo yako, kundi la urithi wako, wakaao peke yao, mwituni katikati ya Karmeli; na walishe katika Bashani na Gileadi, kama siku za kale. Kama katika siku zile za kutoka kwako katika nchi ya Misri nitamwonyesha mambo ya ajabu.

Ni nani aliye Mungu kama wewe, mwenye kusamehe uovu, na kuliachilia kosa la watu wa urithi wake waliosalia? Hashiki hasira yake milele, kwa maana yeye hufurahia rehema. Atarejea na kutuhurumia; atayakanyaga maovu yetu; nawe utazitupa dhambi zao zote katika vilindi vya bahari. Wewe utamtimilizia Yakobo kweli yako, na Ibrahimu rehema zako, ulizowaapia baba zetu tangu siku za kale.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 85:1 – 7 (K) 7

(K) Ee Bwana, utuonyeshe rehema zako.

Bwana, umeiridhia nchi yako,
Umewarejeza mateka wa Yakobo.
Umeusamehe uovu wa watu wako,
Umezisitiri hatia zao zote.
Umeiondoa ghadhabu yako yote,
Umerudi na kuuacha ukali wa hasira yako. (K)

Mungu wa wokovu wetu, uturudishe,
Uikomeshe hasira uliyo nayo juu yetu.
Je! Utatufanyia hasira hata milele?
Utadumisha ghadhabu kizazi hata kizazi. (K)

Je! Hutaki kurudi na kutuhuisha,
Watu wako wakufurahie?
Ee Bwana, utuonyeshe rehema zako,
Utupe wokovu wako. (K)



SHANGILIO
2 Kor. 5:19

Aleluya, aleluya,
Mungu alikuwa ndani ya Kristu, akiupatanisha ulimwengu na nafsi yake. Ametia ndani yetu neno la upatanisho.
Aleluya.



INJILI
Mt. 12:46 – 50

Yesu alipokuwa katika kusema na makutano, tazama, mama yake na ndugu zake walikuwa wakisimama nje wataka kusema naye. Mtu mmoja akamwambia, Tazama, mama yako na ndugu zako wamesimama nje, wanataka kusema nawe. Akajibu, akamwambia yule aliyempasha habari, Mama yangu ni nani? Na ndugu zangu ni akina nani? Akawanyoshea mkono wanafunzi wake, akasema, Tazama, Mama yangu na ndugu zangu! Kwa maana yeyote atakayeyafanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni, huyu ndiye ndugu yangu, na umbu langu, na mama yangu.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MKUBWA KULIKO YONA



ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatatu, Julai 20, 2026
Juma la 16 la Mwaka

Mik 6: 1-4, 6-8
Zab 49: 5-6, 8-9, 16-17, 21, 23; 
Mt 12: 38-42


MKUBWA KULIKO YONA 


Kuna watu kati yetu ambao daima hawana furaha, haijalishi umewatendea nini, daima hawana raha na wanalalamika daima. Licha ya makubwa ambayo Bwana amewatendea bado hawaridhiki. Daima Wayahudi walitaka ishara ili kuhakiki ukweli wa unabii. Hawakumtambua Yesu na hivyo wanahitaji ishara zaidi ili waweze kumkubali Yesu. Lakini ukweli ni kwamba hata Yesu angefanya ishara nyingine zaidi bado wasingebadilika. Hata alivyo mponya yule mgonjwa aliyekuwa bubu na kipofu (Mt 12:22), walimlaumu kwa kufanya ishara hizi kwa kutumia mkuu wa pepo. 

Yona alikuwa ishara. Alikaa muda wa siku tatu katika tumbo la nyangumi. Ni wazi kwamba walidhani ameshakufa. Lakini nyangumi huyu alitumika kama chombo cha kumfanya Yona atubu na kwenda kupeleka ujumbe Ninawi ili watubu. Walitubu kweli na kubadili maisha yao. Giza ndani ya tumbo la nyangumi, mwishoni limekuwa ni baraka na ishara ya daima. Ishara ya Yona ilikuwa ni ishara ya kifo cha Yesu, mwili wake kukaa siku tatu katika ardhi na baadae kufufuka. Hii ndio ishara ambayo Yesu anatoa na ambayo ataendelea kutoa. Ni ishara ya matumaini makubwa tukiitazama vizuri. 

Sisi mara nyingi twaweza kuanguka katika kishawishi hicho hicho. Mara nyingi tunahitaji ishara licha ya ishara mbali mbali ambazo Yesu anazotupatia. Mara nyingi tunataka ishara kutoka kwa Mungu. Tunamtaka yeye aongee kwa sauti na kwa ufasaha. Yesu Kristo yupo nasi daima, akituponya sisi na magonjwa yetu. Yesu yupo ndani ya jirani tunayekutana naye. Ishra kubwa kabisa ni Mungu kuwa Mwanadamu na neno kuwa mwili/chakula kwa ajili ya uhai wa ulimwengu.

Yesu anatukumbusha kwamba tunapaswa kuamini yale yote anayotuambia hata kama tunajisikia tupo kwenye giza na taabu katika tumbo la samaki au kaburini na matumaini yamepotea. Mungu yupo katika kila kitu. Mungu yupo katika kila kitu na yupo kati yetu hata pale tunapohisi yupo kimya. Anaongea na wewe muda wote. Jifunze kutambua sauti yake. 

Sala: Bwana nisaidie mimi nikuamini wewe hata pale ambapo sioni ishara na miujiza kutoka mbinguni. Nisaidie mimi nikuamini wewe hata pale ninapokuwa na wasi wasi na mashaka na udhaifu wangu katika maisha. Ninaomba unipe Imani thabiti niweze kujibu wito wako katika maisha yangu. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JULAI 20, 2026



MASOMO YA MISA, JULAI 20, 2026
JUMATATU, JUMA LA 16 LA MWAKA


SOMO 1
Mik. 6:1-4, 6-8

Sikieni asemavyo Bwana; Simama, ujitetee mbele ya milima, vilima navyo na visikie sauti yako. Sikieni, enyi milima, mateto ya Bwana, na ninyi, enyi misingi ya dunia iliyo imara; kwa maana Bwana ana mateto na watu wake, naye atahujiana na Israeli. Enyi watu wangu, nimewatenda nini? Nami nimewachosha kwa habari gani? Shuhudieni juu yangu. Kwa maana nalikupandisha kutoka nchi ya Misri, na kukukomboa utoke katika nyumba ya utumwa, nami naliwapeleka Musa, na Haruni, na Miriamu, watangulie mbele yako.
Nimkaribie Bwana na kitu gani, na kuinamana mbele za Mungu aliye juu? Je! Nimkaribie na sadaka za kuteketezwa, na ndama za umri wa mwaka mmoja? Je! Bwana atapendezwa na elfu za kondoo waume, au na elfu kumi za mito ya mafuta? Je! Nimtoe mzaliwa wangu wa kwanza kwa kosa langu, mzao wa mwili wangu kwa dhambi ya roho yangu? Ee mwanadamu, yeye amekuonyesha yaliyo mema; na Bwana anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 50:5 – 6, 8 – 9, 16 – 17, 21, 23 (K) 23

Nikusanyieni wacha Mungu wangu, 
Waliofanya agano nami kwa dhabihu.
Na mbingu zitatangaza haki yake, 
Kwa maana Mungu ndiye aliye hakimu. (K)

Sitakukemea kwa ajili ya dhabihu zako,
Na kafara zako ziko mbele zangu daima.
Sitatwaa ng’ombe katika nyumba yako,
Wala beberu katika mazizi yako. (K)

Mtu asiye haki, Mungu amwambia,
Una nini wewe kuitangaza sheria yangu.
Maana wewe umechukia maonyo,
Na kuyatupa maneno yangu nyuma yako. (K)

Ndivyo ulivyofanya, nami nikanyamaza,
Ukadhani ya kuwa Mimi ni kama wewe.
Atoaye dhabihu za kushukuru ndiye anayenitukuza,
Nitamwonyesha wokovu wa Mungu. (K)



SHANGILIO
Yn. 17:17

Aleluya, aleluya,
Neno lako ndiyo kweli, ee Bwana, ututakase kwa ile kweli.
Aleluya.



INJILI
Mt. 12: 38 – 42

Baadhi ya waandishi wa Mafarisayo walimjibu Yesu wakasema, Mwalimu, twataka kuona ishara kwako. Akajibu, akawaambia, Kizazi kibaya na cha zinaa chatafuta ishara, wala hakitapewa ishara, ila ishara ya nabii Yona. Kwani kama vile Yona alivyokuwa siku tatu mchana na usiku katika tumbo la nyangumi, hivyo ndivyo Mwana wa Adamu atakavyokuwa siku tatu mchana na usiku moyo wa nchi. Watu wa Ninawi watasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, nao watawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu wao walitubu kwa mahubiri ya Yona; na hapa yupo aliye mkuu kuliko Yona. Malkia wa kusini atasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu yeye alikuja kutoka pande za mwisho za dunia ili asikie hekima ya Sulemani, na hapa yupo aliye mkuu kuliko Sulemani.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

SHUHUDA WA UPENDO WA MUNGU ULIMWENGUNI



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumapili, Julai 19, 2026
Juma la 16 la Mwaka

Hek 12:13, 16-19
Zab 85:5-6,15-16;
Rom 8:26-27
Mt 13:24-43


SHUHUDA WA UPENDO WA MUNGU ULIMWENGUNI


Ulimwengu ulikuja kutoka katika uzuri mikononi mwa Mungu. Uumbaji ulianza kwa kugawa mwanga na giza(Mwa 1:4). Mungu alisema na “kuweko Mwanga katika anga kugawa usiku na mchana” (Mwa 1:14). “Mungu aliona yote aliyokuwa ameumba na tazama ilikuwa nzuri sana” (Mwa 1:31). Lakini tangia hapo mwanadamu alivyo anza, bila kujua, kuogopa utofauti imeanza kuleta mchanganyo. Alianza kutenga kati ya uzuri na ubaya, kilicho safi na kisicho safi, kitakatifu na kisicho kitakatifu. Uwepo wa ubaya ulimwenguni umebaki kuwa usumbufu kwa mwanadamu. Hakubali ukweli katika ulimwengu sehemu ambayo uzuri na ubaya upo.

Katika somo la leo kutoka katika kitabu cha Hekima, mwandishi anaandika kuhusu “Haki ya Mungu. Mungu hatumii nguvu zake kutuadhibu. Anatumia tu kwa ajili ya uzuri wa Mwanadamu. Hii ndiyo haki; kutumia hekima kwa wote. Ukuu wake ni wa mahali pote, hufunika walio wema na wabaya pia. Hawapendi tu baadhi bali anawapenda wote. Wakati watu wanatumia nguvu kuogopesha wengine na kuweka hofu kwa watu au kujiweka katika hali ya kukandamiza wengine na kuwa katika hali ya juu. Mungu pamoja na kwamba yeye mwenyewe ndiye chanzo cha nguvu yote, hatumii kutisha watu wala kutumia kuadhibu, au kurudisha kisasi, bali hata katika yote yeye huonyesha huruma kwa walio dhaifu kwa ukarimu.

Katika somo la Pili Paulo anakiri kwamba sisi hatufahamu kusali. Roho ndiye anaye tusaidia kusali na kutufundisha ni maneno ghani tutumie tuweze kupeleka maneno yetu kwa Baba. Kusali kwa Mungu ni kufungua akili na mioyo yetu kwake na kuwa tayari kupokea mapenzi yake katika maisha yetu. Sala inayotokana na Roho daima inajibiwa kwasababu inakuwa inalingana na mapenzi ya Baba. Haijaribu kujitafutia mambo yake bali inatubadilisha na kutuunganisha na mapenzi ya Mungu.

Katika somo la Injili ndani ya mifano mitatu, Yesu anatufumbulia mafumbo ya ufalme wa Mungu. Je, magugu yanatoka wapi? Chanzo cha na uwepo wa uovu unahitaji maelezo. Mathayo anayatoa kwa mfano wa Yesu. Kwanza kabisa ni mwenye shamba. Huyu anamwakilisha Mungu, yeye ambaye ndiye anaye sia mbegu na kuangalia ubora wa mbegu. Wa pili ni adui,anaye wakilishwa na kinacho onekana bora katika ulimwengu. Huyu anakuja usiku na kusia magugu ambayo yanaonekana kuwa kama ngano. Mizizi yake imesongana na ngano kiasi kwamba ni vigumu kuiondoa bila kuiondoa na ngano pia. Mhusika wa pili ni mtumishi ana mwakilisha kila mmoja wetu. Wanavyo fanya ni kama sisi tunavyo kumbana na uovu ulimwenguni, katika jumuiya zetu, au kwa kila mtu. Wanaonesha kujitoa kwao katika shamba kwa ajili ya uzalishaji. Wanakosa subira, wanavutwa na tamaa ya kutaka kuyaondoa magugu mara moja. Lakini mwenye shamba yeye ni mpole. Wala hashangazwi na hali hii. Subira ya Mungu ni kubwa na anawaambia waache magugu na ngano ziote pamoja. Katika ulimwengu huu uzuri na uovu havitengani. Vipo vitaota pamoja mpaka mwisho. Mpango wa Mungu pia anataka tutambue ulimwenguni kuna uzuri na ubaya na kwamba vipo na vinaishi ulimwenguni, na hivyo tunapaswa kupokea katika hali ya maisha yetu. Uwepo wa magugu ndani mwetu unataka kutuambia pia kwamba “Hakuna mwenye haki duniani anaye tenda mema tu na ambaye hatendi dhambi” (Ybs :20). Hapa si kuhalalisha uovu, bali Yesu anataka tufahamu hilo na kwenda katika hali ya uvumilivu tukiwa na macho ya Kimungu.

Baada ya mfano huo unafuatwa na mifano mingine miwili pacha. Inaitwa mifano pacha kwasababu huleta ujumbe sawa: kwamba kulinganisha kile cha kwanza ambacho kilikuwa kidogo sana na matokeo makubwa. Mbegu ya haradali ambayo ni ndogo sana ambayo ni vigumu kuona kwa macho hukuwa na kutoa matawi makubwa, na chachu kidogo huchachusha unga wote. Ulinganishaji wake wa pekee. Mifano hii ni mwaliko wa kumtumainia Mungu.

Mifano hii ni ni mifano yetu sisi katika Jumuiya za Kikristo. Mbegu sio akili ya ulimwengu huu bali Mwana wa Mungu, Yesu. Pengine wakristo wa kwanza walipumzika mno hawakuchukulia kwa makini ahadi zao za ubatizo. Mathayo katika kuwamsha anawatikisa na kuwakumbusha kuchukulia maisha katika uhalisia. Hakufanya hivyo kuonesha kwamba ni nini kitatokea kwa wadhambi bali alitaka kuwaamsha wakristo. “Hakumtuma Mwanae ulimwenguni ili kuhukumu ulimwengu bali ulimwengu uokolewe kwa njia yake” (Yn 3:17). Je, vipi kuhusu moto? Mungu anautambua moto mmoja : Roho wa Mungu ambaye alishuka siku ya Pentekoste (Mdo 2:3). “nimekuja kuwasha moto ulimwenguni ni kwa jinsi ghani ninatamani kama umekwisha waka’? (Lk 12:49). Ni moto usiozimika utakao choma magugu yote ndani ya mioyo ya kila mmoja wetu, na kuacha tu ngano safi ambayo inahitajika katika ulimwengu ujao. Sio tangazo la kutishia na kuadhibu bali ni tangazo la kwamba siku moja Roho wa Mungu atasafisha maovu yote. Katika Ufalme wa Mungu hakutakuwa na mmoja atakayefanya kinyume.

Na mfano wa pili wa mbegu ya haradali unataka kutueleza kwamba hakuna mtu mdogo sana au mdhambi sana anayetengwa na Ufalme wa Mungu. Na pia hakuna mtu mkubwa sana anayeweza kujidai kuwa na haki zote za ufalme wa Mungu. Mungu anaweza kuvuna mavuno mengi kutoka katika moyo uliokuwa umepondeka. Mmoja anavyo jinyenyekesha kwa Bwana, na kumchagua yeye katika mambo yote, matunda huwa mengi ajabu.

Mfano wa tatu kuhusu chachu, huleta ukweli huu. Wengi wetu tunaweza kujifirikia sisi wenyewe kwamba ni wadogo sana kiasi ambacho hatuwezi kuleta mabadiliko yeyote katika jamii zetu. Chachu huwekwa katika hali ya udogo sana lakini huchachusha unga wote. Wakristo tunaitwa kuwa chachu ili tuweze kufanya ulimwengu huu sehemu nzuri ya kuishi. Kama sisi ni mashuhuda wazuri wa Injili, Neno la Mungu litaenea kila mahali. Kazi yetu kama Wakristo ulimwenguni ni muhumu sana . Tunaitwa kuwa chumvi na mwanga katika Ulimwengu huu. Kuwa ngano kati ya magugu. Kuwa kama mbegu ya haradali inayokuwa na kuleta sehemu ya kupumzika na kupata makao kwa watu, kuwa mashahidi wa upendo wa Mungu ulimwenguni. Tunaomba hali hii iweze kuwa sala yetu ya kila siku kwa Bwana, ili tuweze kubadilishwa na kuleta mabadiliko, ili Roho nyingi ziweze kupata wokovu na kufahamu upendo wa Mungu na kuwa raia wa ufalme wa Mungu.

Sala: Bwana, mimi ni mdhambi, na wewe mwenyewe ni Mtakatifu. Nipe nguvu zako na neema ili niweze kuishi maisha kadiri ya mapenzi yako. Ninaomba nisimame kwa ujasiri katikati ya uongo na uovu ambao unanizunguka. Ninaomba nikaze macho yangu daima kwako, wewe ambaye ni Mchungaji mkuu. Ninaomba niwe shahidi wa upendo wako katika familia, jirani zangu na Kanisa. Yesu, ninakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUMAPILI, JULAI 19, 2026



MASOMO YA MISA, 
JUMAPILI, JULAI 19, 2026
JUMA LA 16 LA MWAKA


MWANZO:
Zab. 54:4, 6

Tazama, Mungu ndiye anayenisaidia; Bwana ndiye anayenitegemeza nafsi yangu. Kwa ukunjufu wa moyo nitakutolea dhabihu; ee Bwana, nitalishukuru jina lako, maana ni jema.


SOMO 1 
Hek. 12 :13.16-19

Hakuna Mungu mwingine ye yote ila Wewe, unayewaangalia watu wote, hata umwonyeshe huyo ya kuwa hukuhukumu bila haki. Madhali ndio uweza wako ulio asili ya haki, na kwa sabiki ya milki yako juu ya mambo yote unawaachilia wote. Kwa kuwa iwapo wanadamu hawasadiki ya kuwa umekamilika katika uweza wako, Wewe wazidhirisha nguvu zako; tena ukijishughulisha na wale wasioikiri kweli hiyo, waifadhaisha jeuri yao. Walakini desturi yako unauzuia hata uweza wako, na kuhukumu kwa upole, na kututawala kwa uvumilivu mwingi. Yaani uweza unao, wakati wo wote utakapo kuutumia.

Pamoja na hayo, uliwafundisha watu wako kwa matendo yako ya namna hiyo ya kwamba imempasa mwenye haki kuwa mpenda wanadamu; tena ukawatilia wanao tumaini jema, kwa sababu, endapo watu wametenda dhambi, unawajalia toba.

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 86:5-6, 9-10, 15-16 (K) 5

(K) Kwa maana Wewe, U mwema, Umekuwa tayari kusamehe.

Wewe, Bwana, U mwema,
Umekuwa tayari kusamehe.
Na mwingi wa fadhili,
Kwa watu wote wakuitao.
Ee Bwana, uyasikie maombi yangu;
Uisikilize sauti ya dua zangu. (K)

Mataifa yote uliowafanya watakuja;
Watakusujudia Wewe, Bwana.
Watalitukuza jina lako;
Kwa kuwa ndiwe uliye mkuu.
Wewe ndiwe mfanya miujiza,
Ndiwe Mungu peke yako. (K)

Lakini Wewe, Bwana,
U Mungu wa rehema na neema.
Mvumilivu, mwingi wa fadhili na kweli.
Unielekee na kunifadhili mimi. (K)


SOMO 2 
Rum 8 : 26-27

Roho hutusaidia udhaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo; lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa. Na yeye aichunguzaye mioyo aijua nia ya Roho ilivyo, kwa kuwa huwaombea watakatifu kama apendavyo Mungu.

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu


SHANGILIO 
Yn. 17:17

Aleluya, aleluya, 
Neno lako ndiyo kweli, 
Ee Bwana, Ututakase sisi kwa ile kweli. 
Aleluya.


INJILI 
Mt. 13:24-43

Yesu aliwatolea mfano, akisema, Ufalme wa mbinguni umefanana na mtu aliyepanda mbegu njema katika konde lake; lakini watu walipolala, akaja adui yake akapanda magugu katikati ya ngano, akaenda zake. Baadaye majani ya ngano yalipomea na kuzaa, yakaonekana na magugu. Watumwa wa mwenye nyumba wakaenda wakamwambia, Bwana, hukupanda mbegu njema katika konde lako? limepata wapi basi magugu? Akawaambia, Adui ndiye aliyetenda hivi. Watumwa wakamwambia, Basi, wataka twende tukayakusanye? Akasema, La; msije mkakusanya magugu, na kuzing’oa ngano pamoja nayo. Viacheni vyote vikue hata wakati wa mavuno; na wakati wa mavuno nitawaambia wavunao, Yakusanyeni kwanza magugu, myafunge matita matita mkayachome; bali ngano ikusanyeni ghalani mwangu.

Akawatolea mfano mwingine, akisema, Ufalme wa mbinguni umefanana na punje ya haradali, aliyoitwaa mtu akaipanda katika shamba lake; nayo ni ndogo kuliko mbegu zote; lakini ikiisha kumea, huwa kubwa kuliko mboga zote, ikawa mti, hata nyuni wa angani huja na kukaa katika matawi yake.

Akawaambia mfano mwingine; Ufalme wa mbinguni umefanana na chachu aliyoitwaa mwanamke. akaisitiri ndani ya pishi tatu za unga, hata ukachachwa wote pia. Hayo yote Yesu aliwaambia makutano kwa mifano; wala pasipo mfano hakuwaambia neno; ili litimie neno lililonenwa na nabii, akisema, Nitafumbua kinywa changu kwa mifano, Nitayatamka yaliyositirika tangu awali.

Kisha Yesu akawaaga makutano, akaingia nyumbani; wanafunzi wake wakamwendea, wakasema, Tufafanulie mfano wa magugu ya kondeni. Akajibu, akasema, Azipandaye zile mbegu njema ni Mwana wa Adamu; lile konde ni ulimwengu; zile mbegu njema ni wana wa ufalme; na yale magugu ni wana wa yule mwovu; yule adui aliyeyapanda ni Ibilisi; mavuno ni mwisho wa dunia; na wale wa wavunao ni malaika. Basi, kama vile magugu yakusanywavyo na kuchomwa motoni; ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia. Mwana wa Adamu atawatuma malaika zake; nao watakusanya kutoka katika ufalme wake machukizo yote, na hao watendao maasi, na kuwatupa katika tanuru ya moto; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno. Ndipo wenye haki watakapong’aa kama jua katika ufalme wa Baba yao. Mwenye masikio, na asikie.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.