Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

JE, WANIPENDA




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Pasaka
Ijumaa, Mei 22, 2026
Juma la 7 la Pasaka

Mdo 25: 13-21;
Zab  103: 1-2, 11-12, 19-20 (K. 19);
Yn 21: 15-19.


JE, WANIPENDA?


Katika lugha ya Kigiriki, kuna maneno tofauti yanayo tafsiriwa kama “Upendo”. Agape ni aina ya upendo uliyo kamilika, safi, usio na ubinafsi, upo hai. Agape maana yake, kujali na kuwapenda wote, na kujali bila kuweka nafsi mbele. Kuna upendo pia ambao ni hafifu (Phileo), kumpenda mtu kwasababu yakutaka kupendwa naye au kwasababu yakutaka kupata vitu au kitu fulani kutoka kwake. 

Yesu anamuuliza Petro kwa mara zote mbili za kwanza, “je, Simoni wa Yohane, wewe wanipenda (Agape) kuliko hawa?” anasema “ndiyo Bwana, wajua nakupenda (Phileo).” Ingewezekanaje Petro aseme moja kwa moja bila wasi wasi Bwana nakupenda (Agape) baada ya kushindwa kwake kumkiri Bwana? Yesu anamuuliza mara ya tatu, Simoni mwana wa Yohane, je wanipenda (Phileo) mimi?” (angalia hapo Yesu amebadili upendo hapo kutoka Agape na kwenda Phileo). Petro “anahuzunika” si kwasababu tu Bwana alimuuliza mara ya tatu, bali ameshusha kiwango cha upendo, kutaka kumuonesha Petro upendo wake upo wapi!. Tunaweza kufikiri ni jinsi gani Petro alivyo huzunika moyoni. Isingekuwa ni kwasababu ya woga na hofu iliomkumba Petro wakati wa mateso ya Yesu, pengine kabla angeweza kusema kwanguvu zote kabisa, Bwana unaniuliza swali ghani? Bila shaka nakupenda (Agape). Lakini matendo yake yalionesha wazi ni kwa jinsi ghani alishindwa agape kwa Bwana. Alikana hata urafiki (phileo) na Bwana. Na sasa ana “huzuni” ya kweli wanavyo onana uso kwa uso na Bwana kwa yale aliyotenda.


Hili lina maana ghani kati yangu na wewe? Ina maana kwamba hatujachelewa sana. Tunaweza kuwa tumemkosea Bwana kabla, lakini kwa huzuni ya kweli, tuna nafasi nyingine yakumdhihirishia Yesu na sisi wenyewe, kwamba sisi ni Wakristo wa namna ghani. Tumejikuta tukimkana Yesu kwa kugeukia dhambi, turudi sasa na kumpenda kikamilifu (Agape). 

Yesu anamuambia Petro pia alipokuwa kijana alipenda kwenda popote pale alipopenda, pengine hata sisi tujaribu kujiuliza, sisi tukiwa bado tuna nguvu zetu tunafanya nini? Tunatumia nguvu zetu kusali au tunasubiri mpaka tuwe wazee ndio tuanze kusali? Pengine unaweza kujipa kisingizio cha kazi, je unasubiri mpaka ustaafu ndio uanze kwenda kanisani? Tujiwekee hazina tukiwa bado tuna nguvu, ili uzee wetu uwe na Baraka. Tujipatanishe na Mungu daima tukiwa bado na nguvu zetu, tusimuache Mungu kamwe.

Sala: Bwana, unafahamu kwamba nakupenda. Nafahamu unafahamu ni kwa jinsi ghani nilivyo dhaifu. Ninaomba nisikilize wito wa mwaliko wako wa kuonesha mapendo yangu kwako na hamu ya kupata huruma yako. Ninaomba nitoe upendo huu na hamu hii ya kupata huruma katika hali ya juu kabisa. Yesu, nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MEI 22, 2026



MASOMO YA MISA, MEI 22, 2026
IJUMAA YA 7 YA PASAKA

SOMO 1 
Mdo. 25 :13-21

Siku zile, Agripa mfalme na Bernike walifika Kiaisaria, wakimwamkia Festo. Na walipokuwa wakikaa huko siku nyingi, Festo akamweleza mfalme habari za Paulo, akisema, Yupo hapa mtu mmoja aliyeachwa na Feliki kifungoni; ambaye nilipokuwa Yerusalemu wakuu wa makuhani na wazee wa Wayahudi wakaniarifu habari zake, wakinitaka hukumu juu yake. Nikawajibu kwamba si desturi ya Warumi kumtoa mtu awaye yote, kabla mtu yule aliyeshitakiwa hajaonana na washitaki wake uso kwa uso, na kupewa nafasi ya kujitetea katika mashitaka yake.

Basi walipokutanika hapa sikukawia; bali siku ya pili nikaketi katika kiti cha hukumu nikaamuru mtu huyo aletwe. Na wale waliomshitaki waliposimama hawakuleta neno lo lote baya, kama nilivyodhani, bali walikuwa na maswali mengine mengine juu yake katika dini yao wenyewe, na katika habari ya mtu mmoja Yesu, aliyekuwa amekwisha kufa, ambaye Paulo alikaza kusema kwamba yu hai. Nami nikaona shaka jinsi ya kutafuta hakika ya habari hii, nikamwuliza kama anataka kwenda Yerusalemu ahukumiwe huko katika mambo haya. Lakini Paulo alipodai kuwekwa ahukumiwe na Kaisari, nikaamuru alindwe hata nitakapompeleka kwa Kaisari.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 103 :1-2, 11-12, 19-20 (K) 19

(K) Bwana ameweka kiti chake cha enzi mbinguni. au: Aleluya.

Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana.
Naam, vyote vilivyo ndani yangu 
Vilihimidi jina lake takatifu.
Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana,
Wala usizisahau fadhili zake zote. (K)

Maana mbingu zilivyoinuka juu ya nchi,
Kadiri ileile rehema zake ni kuu kwa wamchao.
Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi,
Ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi. (K)

Bwana ameweka kiti chake cha enzi mbinguni,
Na ufalmc wake unavitawala vitu vyote.
Mhimidini Bwana, enyi malaika zake,
Ninyi mlio hodari, mtendao neno lake,
Mkiisikiliza sauti ya neno lake. (K)



SHANGILIO 
Kol. 3 :1

Aleluya, aleluya, 
Mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu, Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu. 
Aleluya.



INJILI 
Yn. 21 :15-19

Walipokwisha kula, Yesu akamwambia Simoni Petro, Je! Simoni wa Yohane, wewe wanipenda kuliko hawa? Akamwambia, Naam, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Lisha wanakondoo wangu. Akamwambia tena mara ya pili. Simoni na Yohane wanipenda? Akamwambia, Ndiyo, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Chunga kondoo zangu.

Akamwambia mara ya tatu, Simoni wa Yohane, wanipenda? Petro alihuzunika kwa vile alivyomwambia mara ya tatu, Wanipenda? Akamwambia, Bwana, wewe wajua yote; wewe umetambua ya kuwa nakupenda. Yesu akamwambia, Lisha kondoo zangu.

Akasema, Amin, amin, nakuambia, Wakati ulipokuwa kijana, ulikuwa ukijifunga mwenyewe na kwenda utakako; lakini utakapokuwa mzee, utainyosha mikono yako, na mwingine atakufunga na kukuchukua usikotaka. Akasema neno hilo kwa kuonyesha ni kwa mauti gani atakayomtukuza Mungu. Naye akiisha kusema hayo, akamwambia, Nifuate.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo. 


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KWA NINI YESU ANASALI?

John 17:9. Jesus Prays for You - Wellspring Christian Ministries


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Pasaka
Alhamisi, Mei 21, 2026
Juma la 7 la Pasaka


Mdo 22: 30; 23: 6-11;
Zab 16: 1-2, 5-11 (K. 1);
Yn 17: 20-26


KWA NINI YESU ANASALI?


Leo tunamuona Yesu akituombea sisi tunao muamini. Ni bahati ilioje kuwa na Mungu anayetuombea? Ni furaha ilioje kuona tumepewa heshima kwa kutajwa ndani ya Injili na kuongelewa na Yesu? Yesu anawaombea wale watakao kuwa wafuasi wake baada ya kuwasikiliza mitume wake. Hapa sisi tupo kwani tunaamini waliotuachia mitume.

Wakati Yesu anavyo nyanyua macho yake mbinnguni, anasali kwa Baba yake wa mbinguni. Ukweli huu wa kunyanyua macho yake, unafunua jambo moja muhimu la uwepo wa Baba yake. Unafunua kwamba “Baba yupo juu ya yote”. Kwa hiyo kwa kuongea na Baba yake, Yesu anaonesha ishara hii kwa kumkiri kwamba Baba yupo juu ya yote. Tunapaswa pia kutambua uhusiano wa pekee na Yesu na Baba yake. Uhusiano wao ni uhsiano wa asili yote. 

Sala ya Yesu kwa Baba ilikuwa sisi wote ambao tutamwamini tuweze kushiriki umoja wa Baba na Mwana. Kwanza kwabisa tunaanza kwa kuona ukuu wa Mungu, kunyanyua macho yetu mbinguni na kuona ukweli, utukufu, ukuu, nguvu, na Mungu wa Majeshi. Tunapaswa kumuona Mungu huyu mtukufu na mkuu akishukia mioyo yetu, akiwasiliana na sisi, akitupenda sisi, akianzisha uhusiano wa karibu na sisi. Tunapaswa kukubali uwepo wake, kumwabundu akiwa anaisha ndani yetu, tukiongea naye na kumpenda yeye. 

Kitu cha kwanza anachoomba ni sisi tuwe na umoja (Yn 17: 21-23). Umoja wetu katika Mungu matokeo yake ni utume, kama Yesu anavyosema, “Ili ulimwengu utambue kuwa umenituma mimi” na tena “..ili ulimwengu uweze kutambua umenituma mimi na unawapenda wao kama unavyo nipenda mimi”. Zaidi na zaidi watu watakuwa na imani ndani ya Yesu, kwa uwepo wa Kanisa, na kudhihirisha kwa kutoa ushuhuda wa upendo wa Mungu ndani ya Kristo. 

Na tena Yesu anaendelea kusali “..na pia wao, ulionipa mimi, waweze kuwa nami pale nilipo, waweze kuona utukufu ulionipa, kwasababu ulinipenda mimi kabla ya kuwepo misingi ya ulimwengu.” Anaongelea maisha yetu yajayo katika maisha ya milele. Huko tutaona utukufu wake, usiofifia wala kuisha. Hapo tutakuwa naye, na tutamuona uso kwa uso.
Sala: Bwana, ninaomba unisaidie niweze kunyanyua macho yangu kuelekea mbinguni kwa sala. Ninakuomba nikugeukie wewe na Baba. Katika sala hiyo naomba nitambue kuwa upo wazi katika moyo wangu ambapo una abudiwa na kupendwa. Yesu, ninakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MEI 21, 2026



MASOMO YA MISA, MEI 21, 2026
ALHAMISI YA 7 YA PASAKA

SOMO 1 
Mdo. 22 : 30; 23 : 6-11

Wakati ule, Jemadari alitaka kujua hakika, ni kwa sababu gani Paulo ameshitakiwa na Wayahudi, akamfungua, akawaamuru wakuu wa makuhani na baraza yote wakutane. Akamleta Paulo chini, akamweka mbele yao.

Paulo alipotambua ya kuwa sehemu moja ni Masadukayo, na sehemu ya pili ni Mafarisayo, akapaza sauti yake katika ile baraza, Ndugu zangu, mimi ni Farisayo, mwana wa Farisayo; mimi ninahukumiwa kwa ajili ya tumaini la ufufuo wa wafu. Alipokwisha kunena hayo palikuwa na mashindano baina ya Mafarisayo na Masadukayo, mkutano ukafarakana. Kwa maana Masadukayo husema ya kwamba hakuna kiyama wala malaika wala roho; bali Mafarisayo hukiri yote. Pakawa na makelele mengi. Waandishi wengine wa upande wa Mafarisayo wakasimama, wakateta, w'akisema, Hatuoni uovu wo wote katika mtu huyu; bali ikiwa roho au malaika amesema naye, ni nini? Ugomvi mkubwa ulipotokea, yule jemadari akachelea Paulo asije akararuliwa nao, akaamuru askari washuke na kumwondoa kwa nguvu mikononi mwao, na kumleta ndani ya ngome.

Usiku ule Bwana akasimama karibu naye, akasema, Uwe na moyo mkuu; kwa sababu, kama ulivyonishuhudia habari zangu Yerusalemu, imeku- pasa kunishuhudia vivyo hivyo Rumi nako.
Hilo ndilo neno la Mungu.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 16:1-2, 7-11 (K) 1

(K) Mungu unihifadhi mimi, kwa maana nakukimbilia Wewe. au: Aleluya.

Mungu unihifadhi mimi,
kwa maana nakukimbilia Wewe.
Nimemwambia Bwana, Ndiwe Bwana wangu, 
sina wema ila utokao kwako. (K)

Nitamhimidi Bwana aliyenipa shauri,
Naam, mtima wangu umenifundisha usiku. 
Nimemweka Bwana mbele yangu daima,
Kwa kuwa yako kuumeni kwangu, sitaondoshwa. (K)

Kwa hiyo moyo wangu unafurahi,
Nao utukufu wangu unashangilia,
Naam, mwili wangu nao utakaa kw;a kutumaini. 
Maana hutakuachia kuzimu nafsi yangu,
Wala hutamtoa mtakatifu wako aone uharibifu. (K)

Utanijulisha njia ya uzima;
Mbele za uso wako ziko furaha tele;
Na katika mkono wako wa kuume 
Mna mema ya milele. (K)



SHANGILIO 
Yn. 16:28

Aleluya, aleluya, 
Nalitoka kwa Baba, nami nimekuja hapa ulimwenguni; tena naucha ulimwengu, na kwenda kwa Baba. 
Aleluya.



INJILI
Yn. 17 :20-26

Siku ile, Yesu alisali akisema: Wala si hao tu ninaowaombea; lakini na wale watakaoniamini kwa sababu ya neno lao. Wote wawe na umoja; kama wewe, Baba, ulivyo ndani yangu, nami ndani yako; hao nao wawe ndani yetu; ili ulimwengu upate kusadiki ya kwamba wewe ndiwe uliyenituma. Nami utukufu ule ulionipa nimewapa wao; ili wawe na umoja kama sisi tulivyo umoja. Mimi ndani yao, nawe ndani yangu, ili wawe wamekamilika katika umoja; ili ulimwengu ujue ya kuwa ndiwe uliyenituma, ukawapenda wao kama ulivyonipenda mimi. 

Baba, hao ulionipa nataka wawe pamoja nami po pote nilipo, wapate na kuutazama utukufu wangu ulionipa; kwa maana ulinipenda kabla ya kuwekwa msingi ulimwengu. Baba mwenye haki, ulimwengu haukukujua; lakini mimi nalikujua, na hao wamejua ya kuwa ndiwe uliyenituma. Nami naliwajulisha jina lako, tena nitawajulisha hilo; ili pendo lile ulilonipenda mimi liwe ndani yao, nami niwe ndani yao.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo. 


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

SALA YA KUWAOMBEA WANAFUNZI


 

“KUFUFUKA NA KRISTO”

Tafakari ya Pasaka

Jumatano, Mei 20, 2026,

Juma la 7 la Pasaka

 

Mdo 20 : 28-38

Yn. 17:11-19

  

SALA YA KUWAOMBEA WANAFUNZI

 

Ndugu wapendwa, karibuni tena kwa tafakari ya neno la Bwana leo. Bado tupo katika kipindi cha Novena tukimuomba Roho Mtakatifu na tunazidi kumshukuru kwa neema zake kwani kwa hakika hata mimi (labda hata na wewe) umekwisha kuanza kuona matunda ya hizi neema zipatikanazo kwa kusali novena kipindi hiki. Tuzidi kumwomba Mungu azidi kutubariki.

 

Katika neno la Bwana leo, tukianza na injili yetu, tunakutana na Yesu akiendelea kutoa sala ya kuwaombea wanafunzi wake hali akijiandaa kuagana nao. Anaomba Mungu awalinde ili wabakie katika umoja. Yesu mwenyewe anasema kwamba yeye alipokuwa pamoja nao aliwalinda na kuwaongoza vyema. Alihakikisha kwamba hawadumbukii shimoni na alijitahidi kweli lakini mmoja wao alikataa huu mwongozo wa Yesu na kuona kwamba hauhitaji na hivyo akachagua njia yake mwenyewe na huko alikamatwa na shetani aliyempotosha. Huyu ndiye Yuda Iscariot. Wale waliofuata mwongozo wake angalau kidogo tu Yesu anaomba kwamba Mungu awalinde na yule mwovu na kuwatakasa katika kweli.

 

Katika injili hii Yesu anakuwa mfano kwetu kwamba kila aliyekabidhiwa na kundi, lazima ajiandae kujitoa sadakaa kwa ajili yake na kuliongoza katika mwongozo sahihi. Sio kuliacha ili liangamie. Hili linakuwa somo hasa kwa baadhi yetu ambao ni viongozi; uongozi ni kujitoa sadaka, ni utayari wa kuhakikisha kwamba wenzangu wanakula kwanza, wanapata mahitaji yao kwanza halafu mimi baadaye. Furaha yangu ni pale wenzangu wanaposhiba kwanza na sio mimi nishibe. Kama mambo ndio yako hivi, basi wengi wetu hapa kwa kweli tunahitaji tumwombe Mungu msamaha kwanza. Hii ni kwa sababu wengi tunachukuliaga nafasi za cheo kama sehemu za sisi kufaidi juu ya vichwa vya wengine. Hapa ni kutenda kinyume cha alivyotenda Bwana wetu Yesu Kristo ambaye tunasema tunamwamini. Somo hili tena linatoa onyo kali kwa wale akina baadhi yetu ambao tunatabia za kufanya mahusiano ya kimapenzi hasa nje ya ndoa zetu. Unapofanya mapenzi na mtu, jua kwamba kuna uwezekano wa kiumbe kuzaliwa. Wasichana wanaofanya mapenzi na wanaume wengi wameishia kuzaa watoto ambao hata baba zao hawajulikani. Watoto wa namna hii huishia kutekelekezwa. Najua ni kweli wengi wetu tunaudhaifu wa kutenda dhambi hizi za kufanya mapenzi nje ya ndoa. Hii ni dhambi. Lakini dhambi inaongezeka Zaidi pale ninapofanya mapenzi bila kutambua kwamba kile kitendo changu chaweza kuzalisha tunda gani. Na je, huwa ninakuwa tayari kufuatilia kilichotokea baada ya dhambi yangu ili niwe tayari kumtunza huyo mtoto. Jamani, kama umetenda dhambi ya uzinzi/uasherati, basi fuatilia pia na yule mtoto atakayezaliwa ili umtunze ili dhambi zisiongezeke zaidi kuliko kuacha yule mtoto azaliwe kama asiyekuwa na Baba (kwa sababu labda mama atakuwa ametembea na wengi) na hivyo yule mtoto kuteseka zaidi. Na kwa wale wazazi tunaowatelekezaga watoto tuache tabia hizi. Tuige mfano wa Yesu.

 

Katika somo la kwanza Paulo naye anatoa hotuba yake ya mwisho ambaye anajionyesha pia kama askari mwaminifu aliyepigana kwa ajili ya Kristo huko Efeso. Hivyo anaondoka akijisifia historia nzuri ya imani na mfano wa maisha. Hivyo anawaambia wale wa Efeso kwamba ni kazi kwao. Kila linalohitajika alikwisha waonesha mfano. Hivyo wanatakiwa watende kwa kadiri walichoona toka kwake na sio toka kwa waalimu wa uongo ambao Paulo anasema kwamba wangeivamia Efeso. Hili ni somo kubwa kwetu. Sisi tulipokeaga mfano mzuri toka kwa wazazi, waalimu wetu na wazee wetu. Tujiulize, je hivi sasa ninatenda kuendana na kile alichonifundisha mama yangu? Hivi kweli haya maisha ninayoishi sasa niliyajifunza au ninamuiga nani. Je, ukataji wangu wa nywele unafanana na ule wa baba au mama yangu? Maneno yangu, uvaaji wangu unafanana na ule wa mwalimu wangu? Hivi vimini ninaviiga kwa mama yangu? Jiulize. Mara nyingi tunashindwa kwa sababu huwa hatuwaigi wale mifano yetu ya kiimani. Tunaishia kuiga wanamuziki, wachezaji mpira, kila kitu tunaiga kwao. Ukataji wa nywele wa wachezaji kama akina Balotel, jinsi wanavyochukuaga wasichana mbalimbali, namna wanavyovaa, jinsi wanavyovaaga vimini, jinsi wanavyofuga nywele, wanavyoongea, yote hayo. Hata akifukuza mke na wewe unafukuza. Tambua tunu njema za imani kutoka kwa wazee wako walio kurithisha imani. Tutafakari haya

------------------------

Copyright ©2013-2025 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MEI 20, 2026


MASOMO YA MISA, MEI 20, 2026
JUMATANO YA 7 YA PASAKA

SOMO 1 
Mdo 20 : 28-38

Paulo aliwaambia wakuu wa kanisa ya Efeso: Jitunzeni nafsi zenu, na lile kundi lote nalo, ambalo Roho Mtakatifu amewaweka ninyi kuwa waangalizi ndani yake, mpate kulilisha kanisa lake Mungu, alilolinunua kwa damu yake mwenyewe. Najua mimi ya kuwa baada ya kuondoka kwangu mbwamwitu wakali wataingia kwenu, wasilihurumie kundi; tena katika ninyi wenyewe watainuka watu, wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao. Kwa hiyo kesheni, mkikumbuka ya kwamba miaka mitatu, usiku na mchana, sikuacha kumwonya kila mtu kwa machozi. Basi, sasa nawaweka katika mikono ya Mungu, na kwa neno la neema yake, ambalo laweza kuwajenga na kuwapa urithi pamoja nao wote waliotakaswa. Sikutamani fedha wala dhahabu, wala mavazi ya mtu. Ninyi wenyewe mnajua ya kuwa mikono yangu hii imetumika kwa mahitaji yangu na ya wale waliokuwa pamoja nami. Katika mambo yote nimewaonyesha ya kuwa kwa kushika kazi hivi imewapasa kuwasaidia wanyonge, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, jinsi alivyosema mwenyewe, Ni heri kutoa kuliko kupokea. Alipokwisha kunena haya akapiga magoti, akaomba pamoja nao wote. Wakalia sana wote, wakamwangukia Paulo shingoni, wakambusu-busu, wakihuzunika zaidi kwa sababu ya neno lile alilosema, ya kwamba hawatamwona uso tena. Wakamsindikiza hata merikebuni. 

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 68:28-29, 32-35 (K) 32

(K) Enyi falme za dunia, mwimbieni Mungu. 
Au: Aleluya.

Ee Mungu, uziamuru nguvu zako;
Ee Mungu, uwe hodari uliyetufanyia makuu.
Kwa ajili ya hekalu lako Yerusalemu 
Wafalme watakuletea hedaya. (K)

Enyi falme za dunia, mwimbieni Mungu,
Msifuni Bwana kwa nyimbo.
Apandaye mbingu za mbingu za tangu milele;
Aitoa sauti yake, sauti ya nguvu.
Mhesabieni Mungu nguvu; (K)

Enzi yake i juu ya Israeli;
Na nguvu zake zi mawinguni.
Mungu ni mwenye kutisha Kutoka patakatifu pako.
Ndiye Mungu wa Israeli;
Yeye huwapa watu wake nguvu na uwezo.
Na ahimidiwe Mungu. (K)


SHANGILIO 
Yn. 14 : 26

Aleluya, aleluya, 
Roho Mtakatifu atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia. 
Aleluya.


INJILI 
Yn. 17:11-19

Siku ile, Yesu alisali akisema: Baba mtakatifu, kwa jina lako ulilonipa uwalinde hawa; ili wawe na umoja kama sisi tulivyo. Nilipokuwapo pamoja nao, mimi naliwalinda kwa jina lako ulilonipa, nikawatunza; wala hapana mmojawapo wao aliyepotea, ila yule mwana wa upotevu, ili andiko litimie.

Na sasa naja kwako; na maneno haya nayasema ulimwenguni, ili wawe na furaha yangu imetimizwa ndani yao. Mimi nimewapa neno lako; na ulimwengu umewachukia; kwa kuwa wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.

Mimi siombi kwamba uwatoe katika ulimwengu; bali uwalinde na yule mwovu. Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu. Uwatakase kwa ile kweli; neno lako ndiyo kweli. Kama vile ulivyonituma mimi ulimwenguni, nami vivyo hivyo naliwatuma hao ulimwenguni. Na kwa ajili yao najiweka wakfu mwenyewe, ili na hao watakaswe katika kweli.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo. 

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

UTUME WA KUTIMIZA!




“KUFUFUKA NA KRISTO”
Tafakari ya Pasaka
Jumanne, Mei 19, 2026
Juma la 7 la Pasaka


Mdo  20: 17-27;
Zab 68: 10-11, 20-21(K. 33);
Yn 17: 1-11.


UTUME WA KUTIMIZA!


Paulo anauacha moyo wake uweze kuzungumza na wakubwa wa Kanisa. Kanisa lilikuwa katika hali ya uchanga, na lilihitaji watu watakao jitolea kweli kwaajili ya kulihudumia. Yesu mwenyewe alimchagua Paulo kuwa mmoja wa wahudumu wa kanisa. Kwakweli, Paulo, hakuishi uongo, hakuwa mtu wakutafuta faida binafsi. Alikuwa muhubiri wa kweli na muwazi, ambaye aliongea vizuri ujumbe wake ili aeleweke hata na wale wadogo kabisa. Alikuwa mhubiri maarufu, alihubiri Injili, alihubiri injili kama ushuhuda kwao wakipokea, na kama ushahidi juu yao kama watakataa. Alikuwa mhubiri aliyejiamini, aliyekuwa na lengo sio la kujulisha akili zao bali mioyo yao na maisha yao. Alikuwa mhubiri aliyefanya kazi kweli, mwenye utajiri mwingi kwa maneno yake, hakuchoka wala kuboreka. Alikuwa mhubiri mwaminifu. Hakuacha kukemea pale mambo yalipoenda tofauti, na kwa ujasiri akatangaza fumbo la msalaba.

Alikuwa mkristo wa kweli, hakuhubiri misemo yenye mashaka wala kufundisha falsafa ya juu yenye kupotosha, wala hakuingilia mambo ya nchi, au njia za kuongoza, lakini alihubiri Imani na toba kama alivyofanya mwalimu wake ambaye ni Yesu. Paulo alichukulia wito wake kama utume aliopewa na Bwana wake Yesu Kristo. Kwanjia hii aliuchukulia kuwa ni mtakatifu na wamamlaka kutoka juu. Kama Paulo sisi nasi tuna bado mbio za kukimbia, kazi ya kufanya. Tuna kazi maalumu tuliopangiwa. Tupo katika hali mbaya kama tutakataa na kuacha kazi yetu.

“Saa” anao ongelea Yesu ni muda wa kusulubiwa kwake ambao waweza kuonekana kama muda wa huzuni. Lakini katika hali ya Kimungu ni muda wa utukufu. Ni muda wa kutukuzwa na Baba yake wa Mbinguni kwasababu alitimiza mapenzi ya Baba yake katika ukamilifu wote. Alipokea kifo chake kwa ajili ya wokovu wa Ulimwengu. Wasaa wa Yesu ni muda ambao tunapaswa kuuishi kila wakati, kwa kubeba misalaba yetu ya kila siku. Kwa kufanya hivyo misalaba yetu inatakatifuzwa kwa nguvu za Kimungu na kuwa sehemu ya kupata neema za Mungu. Uzuri wa Injili ni kwamba kila msalaba tunao vumilia au kubeba, ni muda wa kudhihirisha msalaba wa Yesu. Tunaitwa na yeye kwa kumpa utukufu kwa kuishi mateso yetu na kifo chetu siku zote za maisha yetu. Kufa katika dhambi na kufufuka katika neema.

Sala: Bwana Yesu, tupe nguvu tuweze kuvumilia katika magumu yetu yote ya maisha. Tunaomba yote yawe sehemu ya kukupa utukufu. Tunaomba tuwe kama Mt. Paulo, kwa kuwa waaminifu katika utume uliotupatia sisi. Yesu, nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MEI 19, 2026



MASOMO YA MISA, MEI 19, 2026
JUMANNE, JUMA LA 7 LA PASAKA



SOMO 1
Mdo. 20 :17-27

Siku zile, toka Mileto Paulo alituma watu kwenda Efeso, akawaita wazee wa kanisa. Walipofika

kwake, akawaambia, Ninyi wenyewe mnajua tangu siku ya kwanza nilipokanyaga hapa Asia, jinsi nilivyokuwa kwenu wakati wote, nikimtumikia Bwana kwa unyenyekevu wote, na kwa machozi na majaribu yaliyonipata kwa hila za Wayahudi; ya kuwa sikujiepusha katika kuwatangazia neno lo lote liwezalo kuwafaa, bali naliwafundisha waziwazi, na nyumba kwa nyumba, nikiwashuhudia Wayahudi na Wayunani wamtubie Mungu, na kumwamini Bwana wetu Yesu Kristo.

Basi sasa, angalieni, nashika njia kwenda Yerusalemu hali nimefungwa rohoni, nisiyajue mambo yatakayonikuta huko; isipokuwa Roho Mtakatifu mji kwa mji hunishuhudia akisema, ya kwamba vifungo  na dhiki vyaningoja. Lakini siyahesabu maisha yangu kuwa kitu cha thamani kwangu kama kuumaliza mwendo wangu na huduma ile niliyopokea kwa Bwana Yesu, kuishuhudia Habari njema ya neema ya Mungu. Na sasa, tazameni, mimi najua ya kuwa ninyi nyote niliowahubiria ufalme wa Mungu, nikienda huko na huko, hamtaniona uso tena. Kwa hiyo nawashuhudia wote siku hii ya leo, ya kuwa mimi sina hatia kwa damu ya mtu awaye yote. Kwa maana sikujiepusha na kuwahubiria habari ya kusudi lote la Mungu.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 68 : 9-10, 19-20 (K) 32

K. Enyi falme wa dunia, mwimbieni Mungu. Au: K. Aleluya.

Ee Mungu, ulinyesha mvua ya neema;
Urithi wako ulipochoka uliutia nguvu.
Kabila yako ilifanya kao lake huko;
Ee Mungu, kwa wema wako uliwaruzuku walioonewa. (K)

Na ahimidiwe Bwana,
Siku kwa siku hutuchukulia mzigo wetu;
Mungu ndiye wokovu wetu.
Mungu kwetu sisi ni Mungu wa kuokoa;
Na njia za kutoka mautini. (K)



SHANGILIO
Yn. 14:16

Aleluya, aleluya,
Nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele.
Aleluya.



INJILI
Yn. 17:1-11

Siku ile, Yesu aliinua macho yake kuelekea mbinguni, akasema, Baba, saa imekwisha kufika. Mtukuze Mwanao, ili Mwana wako naye akutukuze wewe. Kama vile ulivyompa mamlaka juu ya wote wenye mwili, ili kwamba wote uliompa awape uzima wa milele. Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma. Mimi nimekutukuza duniani, hali nimeimaliza kazi ile uliyonipa niifanye.

Na sasa, Baba, unitukuze mimi pamoja nawe, kwa utukufu ule niliokuwa nao pamoja nawe kabla ya ulimwengu kuwako. Jina lako nimewadhihirishia watu wale ulionipa katika ulimwengu; walikuwa wako, ukanipa mimi, na neno lako wamelishika. Sasa wamejua ya kuwa yote uliyonipa yatoka kwako. Kwa kuwa maneno uliyonipa nimewapa wao; nao wakayapokea, wakajua hakika ya kuwa nalitoka kwako, wakasadiki ya kwamba wewe ndiwe uliyenituma. Mimi nawaombea hao; siuombei ulimwengu; bali hao ulionipa, kwa kuwa hao ni wako; na wote walio wangu ni wako, na walio wako ni wangu; nami nimetukuzwa ndani yao. Wala mimi simo tena ulimwenguni, lakini hawa wamo ulimwenguni, nami naja kwako.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

WAKRISTO WENYE KUTOA USHUHUDA!




“KUFUFUKA NA KRISTO”
Tafakari ya Pasaka
Jumatatu, Mei 18, 2026
Juma la 7 la Pasaka

Mdo 19: 1-8;
Zab 67: 2-7 (R. 33);
Yn 16: 29-33.


WAKRISTO WENYE KUTOA USHUHUDA!


Ni rahisi kuwa mkristu na kumfuata Yesu wakati ukiwa na watu wengi na wakati wengine wakifanya hivyo. Lakini je, inakuwaje kuhusu wakati ambapo Imani yako inapo vamiwa au inazuiwa na kupingwa? Au wakati ambapo inakubidi kufanya uchaguzi wa kutoka katika utamaduni mbaya uliozoeleka na jamii yako na kusimama kwenye Imani yako? Kuna changamoto nyingi katika ufuasi wetu wa kumfuata Kristo. Katika Injili ya leo kuna watu ambao walikuwa wakiongelea mafundisho ya Yesu wakimsikiliza na kuongea kuhusu yeye. Wengi waliishia pia kuamini alikuwa Masiha. Walimsikiliza na kumwamini kwamba alitoka kwa Mungu. Yesu aliwongelea hao mara moja na kwamba ingawaje wanaamini sasa, kutakuwa na muda ambapo watamkataa na kumwacha peke yake. Moja ya jaribio kubwa la Imani yetu ni kuangalia ni kwa jinsi ghani tulivyo waaminifu katika Imani yetu tunapo mfuata Yesu bila kuwa na umati. Ni katika wakati huu, tunakuwa na muda wa kudhihirisha Imani yetu na kuzamisha maana yetu ya kuwa Wakristo.

Siku hizi tunaongea mara nyingi juu ya “uinjilishaji mpya” . Uinjilishaji huu hauwezi kufanya kazi tu kwa njia ya vyombo vya habari. Watu hawataguswa na maneno yetu: kwa njia ya tweeter, kuandika ujumbe, redio wala katika websites, bali ni njia ya mwanadamu kwa mwanadamu kushuhudia nguvu ya Roho ambayo itabadili maisha yetu na tabia zetu kama vile Roho alivyo mbadili Paulo kutoka katika hali ya kulitesa kanisa na kuwa mtangazaji mkubwa wa habari njema. Watu wa siku hizi na hasa wale waliyo batizwa na wameamua kuliacha kanisa wana hangaika kutafuta ishara ya Roho wa Mungu. Kama tunataka watu wasikilize habari njema, tunapaswa kufanywa upya na Roho Mtakatifu. Baba Mtakatifu Fransisko alipendekeza kwamba wengi wetu tunaogopa kufanya mabadiliko, kwasababu hatuweze kukaa na Roho-kwasababu Roho anaweza kutupeleka sehemu ambayo hatupendi kwenda, kwa mtu binafsi na hata kwa pamoja. Tumuombe Mungu atujaze upya Roho Mtakatifu na tumruhusu Roho Mtakatifu atupe changamoto!

Sala: Bwana, naamini. Nisaidie Imani hiyo juu yako ibaki imara daima. Yesu, nakuamini wewe. Ee Roho Mtakatifu wa mapendo, shuka kwangu ili niweze kushuhudia ukweli wako. Roho Mtakatifu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MEI 18, 2026



MASOMO YA MISA, MEI 18, 2026
JUMATATU, JUMA LA 7 LA PASAKA


SOMO 1
Mdo. 19:1-8

Ikawa, Apolo alipokuwa Korintho, Paulo, akiisha kupita kati ya nchi za juu, akafika Efeso; akakutana na wanafunzi kadha wa kadha huko; akawauliza, Je! mlipokea Roho Mtakatifu mlipoamini? Wakamjibu, La, hata kusikia kwamba kuna Roho Mtakatifu hatukusikia. Akawauliza, basi mlibatizwa kwa ubatizo gani? Wakasema, kwa ubatizo wa Yohane. Paulo akasema, Yohane alibatiza kwa ubatizo wa toba, akiwaambia watu wamwamini yeye atakayekuja nyuma yake, yaani, Yesu.

Waliposikia haya wakabatizwa kwa jina la Bwana Yesu. Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao; wakaanza kunena kwa lugha, na kutabiri. Na jumla yao walipata wanaume kumi na wawili. Akaingia ndani ya sinagogi, akanena kwa ushujaa kwa muda wa miezi mitatu, akahojiana na watu, na kuwavuta katika mambo ya ufalme wa Mungu.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATI KATI
Zab. 68 :1-6 (K) 32

(K) Enyi falme za dunia, mwimbieni Mungu. au: Aleluya.

Mungu huondoka, adui zake wakatawanyika,
Nao wamchukiao huukimbia uso wake.
Kama moshi upeperushwavyo,
Ndivyo uwapeperushavyo wao;
Kama nta iyeyukavyo mbele ya moto,
Ndivyo waovu wapoteavyo usoni pa Mungu. (K)

Bali wenye haki hufurahi,
Na kuushangilia uso wa Mungu,
Naam, hupiga kelele kwa furaha.
Mwimbieni Mungu, lisifuni jina lake,
Shangilieni mbele zake. (K)

Baba wa yatima na mwamuzi wa wajane,
Mungu katika kao lake takatifu.
Mungu huwakalisha wapweke nyumbani;
Huwatoa wafungwa wakae hali ya kufanikiwa;
Bali wakaidi hukaa katika nchi kavu. (K)



SHANG1LIO
Mt. 28 :19, 20

Aleluya, aleluya,
Enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, hata ukamilifu wa dahari.
Aleluya.



INJILI
Yn. 16:29-33

Wanafunzi walimwambia Yesu: Tazama, sasa wasema waziwazi, wala huneni mithali yo yote. Sasa tumejua ya kuwa wewe wafahamu mambo yote wala huna haja ya mtu akuulize; kwa hiyo twasadiki ya kwamba ulitoka kwa Mungu.

Yesu akawajibu, Je! mnasadiki sasa? Tazama. saa yaja, naam, imekwisha kuja ambapo mtatawanyika kila mmoja kwao kwao, na kuniacha mimi peke yangu; walakini mimi si peke yangu, kwa kuwa Baba yupo pamoja nami. Hayo nimewaambieni mpate kuwa na amani ndani yangu. Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.