Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

NGUVU YA YESU DHIDI YA MAUTI!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatano, Julai 29,  2026 
Juma la 17 la Mwaka

KUMBUKUMBU YA FAMILIA WA MARTA, MARIA NA LAZARO

Yer 13:1-11; 
Kum 32: 18-21; 
Yn 11: 19-27 or Lk 10: 38-42


NGUVU YA YESU DHIDI YA MAUTI!

“Yesu aliwapenda, Martha, Maria na Lazaro” (Yn 11: 5). Maneno haya ya pekee katika Injili ya Yohane yanatueleza juu ya uhusiano wa pekee aliokuwa nao Yesu kati ya Martha, Maria na Lazaro. Inaonekana Yesu alikuwa mgeni wao mara nyingi katika familia hii huko Bethania, kijiji kidogo, maili mbili kutoka mji wa Yerusalemu. Tunasoma safari tatu za Yesu anazofanya ili kuwatembelea, katika Injili ya Luka 10:38-42, Yn 11: 1-53, Yn 12: 1-9. Sisi nasi tujenge Upendo kama huo na Yesu, mwana wa Mungu, tumjue Mungu. Tunaomba yeye asiwe tu mgeni wetu kila Mara katika maisha bali awe sehemu ya kiini cha familia zetu. 

Wakati Yesu alipowatembelea mara ya pili, Martha alikuwa akiomboleza na kulia juu ya kifo cha Lazaro kaka yake, na nyumba ikiwa imejawa pia na waombolezaji wengine. Lakini aliposikia Yesu amefika mahali pale, anasimama mara na kuwaacha wageni wengine na waombolezaji na anaenda kumuona Yesu. Hapa tunamuona Martha aliyebadilika. Pamoja na kwamba yupo katika hali ya majonzi na uchungu anaenda kumuona Yesu. Sasa anatambua lililo muhimu katika maisha. Katika mazungumzo yake anaanza moja kwa moja bila kuwa na wasi wasi kwamba anaamini juu ya nguvu ya Yesu, katika ufufuo wa wafu. Kwasababu ya hili analeta usemi uliomaarufu sana katika Injili ya Yohani. “MIMI (Yesu) ni ufufuo na uzima; aniaminiye mimi, hata kama anakufa ataishi na anayeishi na kuniamini hatakufa kamwe”. Baada ya hili, Martha analeta tena ungamo la Imani “ndio Bwana, ninaamini wewe ni Masiha , Mwana wa Mungu, ajaye ulimwenguni”. Na sasa Yesu anamfufua Lazaro. 

Kwa njia hii tunamuona Martha anavyoshirikiana na Neema ya Mungu katika maongezi yake na Yesu, sisi nasi tumpe Yesu nafasi aongee na sisi, sala zetu zisiwe ni sisi tu tunaongea na kueleza mambo yetu pekee, bali tumruhusu pia Mungu aongee nasi. Tumpe pia Mungu nafasi ajibu maombi yetu. Tuwe na muda wa kutafakari katika ukimya tumsikilize Mungu anataka kusema nini juu yangu? Tuwe na muda pia wa kumshukuru sio kuomba tuu, sala yetu iwe na nyanja mbali mbali. Tuwe na muda wa kumsifu, kumshukuru, kumuomba, kumsikiliza na pia kutafakari juu ya ukuu wake, na zaidi sana juu ya upendo aliotuonesha kupitia kwa Mwanaye Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwanjia yake watu wote wapo hai. 

Sala: Bwana, nina amini kwamba utanifufua siku ya mwisho, nizaliwe katika maisha ya umilele. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JULAI 29, 2026



MASOMO YA MISA, JULAI 29, 2026
JUMATANO, JUMA LA 17 LA MWAKA

KUMBUKUMBU YA FAMILIA WA MARTA, MARIA NA LAZARO


SOMO 1 
Yer. 13:1-11

Bwana aliniambia hivi, Enenda, ukajinunulie mshipi wa kitani, ukajivike viuno, wala usiutie majini. Basi nikanunua mshipi sawasawa na neno la Bwana, nikajivika viunoni. Nalo neno la Bwana likanijia mara ya pili, kusema, Twaa mshipi ule ulioununua, ulio viunoni mwako, kisha ondoka, enenda mpaka mto Frati, ukaufiche huko katika pango la jabali. Basi nikaenda, nikauficha karibu na mto Frati, kama Bwana alivyoniamuru.

Hata ikawa baada ya siku nyingi, Bwana akaniambia, Ondoka, enenda mpaka mto Frati, ukautwae ule mshipi, niliokuamuru kuuficha huko. Ndipo nikaenda mpaka mto Frati, nikachimba, nikautwaa ule mshipi katika mahali pale nilipouficha; na tazama, mshipi ulikuwa umeharibika, haukufaa tena kwa lo lote. Ndipo neno la Bwana likanijia, kusema, Bwana asema hivi, Jinsi iyo hiyo nitakiharibu kiburi cha Yuda, na kiburi kikuu cha Yerusalemu. Wata hawa waovu, wanaokataa kusikiliza maneno yangu, wanaokwenda kwa ushupavu wa mioyo yao, na kufuata miungu mingine ile kuitumikia na kuiabudu, watakuwa hali moja na mshipi huu, usiofaa kwa lo lote. Maana kama vile mshipi unavyoshikamana na viuno vya mtu, ndivyo nilivyowashikamanisha nami nyumba yote ya Israeli, na nyumba yote ya Yuda, asema Bwana; wapate kuwa watu kwangu mimi, na jina, na sifa, na utukufu; lakini hawakutaka kusikia.

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu 


WIMBO WA KATIKATI 
Kum. 32:18-21 (K) 18

(K) Humkumbuki Mwamba aliyekuzaa.

Humkumbuki Mwamba aliyekuzaa.
Mungu aliyekuzaa umemsahau.
Bwana akaona, akawachukia,
Kwa sababu ya kukasirishwa na wanawe na binti zake. (K)

Akasema, Nitawaficha uso wangu,
Nitaona mwisho wao utakuwaje;
Maana, ni kizazi cha ukaidi mwingi,
Watoto wasio imani ndani yao. (K)

Wamenitia wivu kwa kisicho Mungu, 
Wamenikasirisha kwa ubatili wao;
Nami nitawatia wivu kwa wasio watu. 
Nami nitawakasirisha kwa taifa lipumbaalo. (K)


SHANGILIO 
Kol. : 16,17

Aleluya, aleluya, Neno la Kristu likae kwa wingi ndani yenu katika hekima yote, mkimshukuru Mungu Baba kwa Yeye. Aleluya.


INJILI
Yn. 11:19 – 27

Watu wengi katika Wayahudi walikuwa wamekuja kwa Martha na Mariamu, ili kuwafariji kwa habari ya ndugu yao. Basi Martha aliposikia kwamba Yesu anakuja, alikwenda kumlaki; na Mariamu alikuwa akikaa nyumbani. Basi Martha akamwambia Yesu, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa. Lakini hata sasa najua ya kuwa yoyote utakayomwomba Mungu, Mungu atakupa. Yesu akamwambia, Ndugu yako atafufuka. Maratha akamwambia, Najua ya kuwa atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.

Yesu akamwambia, Mimi ndimi ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je! Unayasadiki hayo?

Akamwambia, Naam, Bwana, mimi nimesadiki ya kwamba wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu, yule ajaye ulimwenguni.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.

Au

INJILI
Lk. 10:38 – 42

Ikawa katika kuenenda kwao aliingia katika kijiji kimoja; mwanamke mmoja jina lake Martha akamkaribisha nyumbani kwake. Naye alikuwa na umbu lake aitwaye Mariamu, aliyeketi miguuni pake Yesu, akasikiliza maneno yake. Lakini Martha alikuwa akihangaika kwa utumishi mwingi; akamwendea, akasema, Bwana, huoni vibaya hivyo ndugu yangu alivyoniacha nitumike peke yangu? Basi mwambie anisaidie. Bwana akajibu akamwambia, Martha, Martha, unasumbuka na kufadhaika kwa ajili ya vitu vingi; lakini kinatakiwa kitu kimoja tu; na Mariamu amelichagua fungu lililo jema, ambalo hataondolewa.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUKUWA KATIKATI YA MAGUGU



“ASALI ITAKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumanne, Julai 28, 2026, 
Juma la 17 la Mwaka wa Kanisa 


Yer 14: 17-22; 
Zab 78: 8-9, 11, 13; 
Mt 13: 36-43.


KUKUWA KATIKATI YA MAGUGU

Injili ya leo inatualika kutafakari juu ya Ufalme wa Mungu. Yesu alikuja kutangaza na kuanzisha Ufalme wa Mungu. Somo la kwanza lina tukumbulisha ujumbe huu kwa kutangaza nguvu na mamlaka ya Mungu, ambaye ni mkarimu na mwenye huruma. Ingawaje ni mkuu juu ya yote anaongea na Musa uso kwa uso kama rafiki. Anatupa muda kuchagua kuwa katika ufalme wake. 

Katika mfano wa magugu na ngano, yote yanakuwa pamoja, yote yanapokea Baraka kipindi cha uhai wao, lakini mwishoni wakati wa mavuno yanatenganishwa na kila moja litaonesha matunda yake. Wengi wetu tumebarikiwa kuzaliwa katika familia ya Kikristo. Mungu ametupatia Baraka ya ubatizo hata kabla hatujauelewa maana yake. Anaendelea kutupatia Baraka kwa njia ya kanisa. Lakini Baraka za kuwa mkristo haina maana tutaenda tuu mbinguni bila kujishughulisha. Uzuri ni kwamba Mungu ametupa uhuru wa kumchagua yeye au kumkataa, wakati wa mavuno itadhihirika kama ulimchagua Mungu au la! .

Tujaribu kufikiria kama Yesu alikuwa aje kesho na atawachukua wale wote wenye haki? Je, wewe utakuwa na wasiwasi? Pengine hapana. Au pengine kutakuwa na muda wa kutazama nyuma na kuwa na Amani na kuona haki inakuja. Mungu daima yupo katika kuongoza. Anatambua anafanya nini na atakuwa na utukufu juu ya vyote. 

Wakristo wanaitwa waweze kuwa kama chachu katika jamii ili ulimwengu uweze kuwa sehemu nzuri ya kukaa. Kama sisi ni mashahidi wa kweli wa Kristo, Injili itaenea daima kila mahali. Kuingia kwetu katika ufalme itategemea kuchagua wema na kuacha yale yalio machukizo mbele ya Mungu. Wito wetu kama Wakristo tumeitwa kuwa mwanga wa ulimwengu, chumvi ya ulimwengu, ngano kati ya magugu, na ushuhuda wa upendo wa Yesu ulimwenguni. Tunaomba hii iwe sala yetu kwa Yesu kwani, ili mioyo mingi iweze kutambua uwezo upendo wa Mungu na kuwa raia wa Ufalme. 

Sala: Bwana Yesu, ninakuomba unisaidie mimi niweze kukaza macho yangu kwako na katika ushindi wa mwisho. Nisaidie mimi niweze kuwa mvumilivu nikwepe maovu ya ulimwengu huu kwa neema utakazo nipatia. Ninakuomba nisisahau ahadi yako siku ya mwisho uliioongea kwetu. Yesu nakuamini
 wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JULAI 28, 2026




MASOMO YA MISA, JULAI 28, 2026
JUMANNE, JUMA LA 17 LA MWAKA


SOMO 1
Yer. 14:17-22

Macho yangu na yatiririke machozi, usiku na mchana, wala yasikome; kwa maana bikira, binti ya watu wangu, amevunjika mavunjiko makuu, kwa jeraha isiyoponyeka. Nikitoka kwenda shambani, tazama, wako huko waliouawa kwa upanga! Na nikiingia mjini, tazama, wamo humo wanaougua kwa sababu ya njaa! Maana nabii na kuhani, wote wawili, huenda huko na huko katika nchi, wala hawana maarifa.

Je! Umemkataa Yuda kabisa? Roho yako imeichukia Sayuni? Mbona umetupiga, tusiwe na dawa ya mema yoyote; tulitazamia wakati wa kupona, na tazama, kufadhaika tu!

Ee Bwana, tunakiri uovu wetu, na ubaya wa baba zetu; maana tumekutenda dhambi. Usituchukie, kwa ajili ya jina lako; usikifedheheshe kiti cha enzi cha utukufu wako; kumbuka, usilivunje agano ulilofanya nasi. Je! Katika vitu vya ubatili vya mataifa, kiko kiwezacho kuleta mvua? Je! Mbingu zaweza kutoa manyunyu! Je! Si wewe, Ee Bwana, Mungu wetu? Kwa sababu hiyo tutakungoja; kwa kuwa wewe umevifanya vitu hivi vyote. 

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 79:8-9,11, 13 (K) 9

(K) Kwa ajili ya utukufu wa jina lako, utusaidie, Ee Bwana.

Usikumbuke juu yetu maovu ya baba zetu,
Rehema zako zije kutulaki hima.
Kwa maana tumedhilika sana. (K)

Ee Mungu wa wokovu wetu, utusaidie,
Kwa ajili ya utukufu wa jina lako.
Utuokoe, utudhofiri dhambi zetu,
Kwa ajili ya jina lako. (K)

Kuugua kwake aliyefungwa na kuingia mbele zako,
Kwa kadiri ya uwezo wa mkono wako
Uwahifadhi wana wa mauti.
Na sisi tulio watu wako, na kondoo za malisho yako,
Tutakushukuru milele;
Tutazisimulia sifa zako kizazi kwa kizazi. (K)


SHANGILIO
Ebr. 4:12

Aleluya, aleluya,
Neno la Mungu li hai tena li na nguvu, li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo.
Aleluya.


INJILI
Mt. 13:36 – 43

Yesu aliwaaga makutano, akaingia nyumbani; wanafunzi wake wakamwendea, wakasema, Tufafanulie mfano wa magugu ya kondeni. Akajibu, akasema, Azipandaye zile mbegu njema ni Mwana wa Adamu; lile konde ni ulimwengu; zile mbegu njema ni wana wa ufalme; na yale magugu ni wana wa yule mwovu; yule adui aliyeyapanda ni Ibilisi; mavuno ni mwisho wa dunia; na wale wavunao ni malaika. Basi, kama vile magugu yakusanywavyo na kuchomwa motoni; ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia. Mwana wa Adamu atawatuma malaika wake machukizo yote, na hao watendao maasi, na kuwatupa katika tanuru ya moto; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno. Ndipo wenye haki watakapong’aa kama jua katika ufalme wa Baba yao. Mwenye masikio, na asikie.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

UKUBWA MACHONI MWA MUNGU

 



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatatu, 27 Julai, 2026, 
Juma la 17 la Mwaka


Yer. 13:1-11
Kum. 32:18-21 (K) 18
Mt 13:31-35


UKUBWA MACHONI MWA MUNGU

Yesu akiongea kuhusu Ufalme wa Mungu alisema, “Ufalme wa Mungu upo pamoja nanyi” (Lk 17:21). Tunaitwa leo kuendeleza kazi hii ya Ufalme wa Mungu. Tunaweza kuwa na ugumu tuanzie wapi. Yesu anatuambia kwamba hata mbegu ndogo kabisa ya haradali inakuwa na kuwa mti mkubwa. Ni sawa sawa na kitendo kidogo kabisa chaweza kukuza Ufalme wa Mungu. Kwasababu Ufalme wa Mungu upo kati yetu, tunapaswa kuanza kutenda kadiri yake. Tukiwa tunaacha njia za uovu, mawazo mabaya na kugeukia njia ya haki, inaweza ikawa hatua ndogo. Kitendo hiki kidogo chaweza kukuwa na kuwa mti mkubwa ambapo ndege wa angani hupata pumziko. Kitendo kidogo katika familia yangu chaweza kukuza familia yangu na kuwa sehemu kubwa ya kushuhudia kueneza Ufalme wa Mungu. Kitendo cha ukarimu kwa jamii, chaweza kubadilisha jamii nzima na kufanya Ufalme wa Mungu kuenea kama moto mkubwa.

Mara nyingi tunafikiria kwamba maisha yetu sio muhimu sana kama ya wengine. Tunaweza kuwaangalia watu wengi walio endelea na walio maarufu, “hivi kama ningekuwa na hela kama zao?” au hivi kama ningekuwa maarufu kama hao? Ni mara nyingi tumejikuta tukianguka kwenye maswali “hivi kama ningekuwa….” Mbegu ndogo yaweza kuwa msitu mkubwa. Hili linafanya tujiulize swali, Je, unafikiri wewe ni mbegu ndogo sana? Inatokea katika maisha kwamba tunajisikia tupo chini na tunahitaji zaidi. Lakini haya yote hayana tofauti na ndoto zitokanazo na tamaa za dunia. Ukweli ni kwamba kila mmoja wetu ana uwezo wa kufanya mambo makubwa katika dunia hii. Machoni pa Mungu tuna hazina ndani mwetu kubwa mno kuliko yale tunayotamani sisi wenyewe.

Nini maana ya kufanywa upya na Mungu na kuwa mti mkubwa, kama punji ya haradali ilivyo? Ni kwamba kila mmoja wetu amepewa vingi na mengi ya kutimiza ili kujenga ufalme wa Mungu na mpango wa utukufu wa Mungu alionao katika maisha yetu. Ni mpango huu utakao zaa matunda makubwa na uzima wa milele. Tunaweza tusipate jina la kutambuliwa hapa duniani. Lakini, mbinguni lilo la muhimu ni utakatifu wako na jinsi ulivyo timiza mpango wa Mungu ulivyo katika maisha yako.

Alisema Mama Teresa mara nyingi kwamba “tumeitwa ili tuweze kuwa waminifu, na sio kufanikiwa.” Ni uaminifu huu kwa Mungu wenye thamani.

Sala: Bwana, ninatambua kwamba bila wewe mimi si kitu. Bila wewe maisha yangu hayana thamani. Ninaomba niweze kukumbatia mpango wako mkamilifu na wa utukufu katika maisha yangu na katika mpango huo, niweze kupata ukuu ule ulio niandalia na kuniitia mimi. Yesu, nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JULAI 27, 2026

 



MASOMO YA MISA, JULAI 27, 2026
JUMATATU, JUMA LA 17 LA MWAKA WA KANISA


SOMO 1 
Yer. 13:1-11

Bwana aliniambia hivi, Enenda, ukajinunulie mshipi wa kitani, ukajivike viuno, wala usiutie majini. Basi nikanunua mshipi sawasawa na neno la Bwana, nikajivika viunoni. Nalo neno la Bwana likanijia mara ya pili, kusema, Twaa mshipi ule ulioununua, ulio viunoni mwako, kisha ondoka, enenda mpaka mto Frati, ukaufiche huko katika pango la jabali. Basi nikaenda, nikauficha karibu na mto Frati, kama Bwana alivyoniamuru.

Hata ikawa baada ya siku nyingi, Bwana akaniambia, Ondoka, enenda mpaka mto Frati, ukautwae ule mshipi, niliokuamuru kuuficha huko. Ndipo nikaenda mpaka mto Frati, nikachimba, nikautwaa ule mshipi katika mahali pale nilipouficha; na tazama, mshipi ulikuwa umeharibika, haukufaa tena kwa lo lote. Ndipo neno la Bwana likanijia, kusema, Bwana asema hivi, Jinsi iyo hiyo nitakiharibu kiburi cha Yuda, na kiburi kikuu cha Yerusalemu. Wata hawa waovu, wanaokataa kusikiliza maneno yangu, wanaokwenda kwa ushupavu wa mioyo yao, na kufuata miungu mingine ile kuitumikia na kuiabudu, watakuwa hali moja na mshipi huu, usiofaa kwa lo lote. Maana kama vile mshipi unavyoshikamana na viuno vya mtu, ndivyo nilivyowashikamanisha nami nyumba yote ya Israeli, na nyumba yote ya Yuda, asema Bwana; wapate kuwa watu kwangu mimi, na jina, na sifa, na utukufu; lakini hawakutaka kusikia.

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu 


WIMBO WA KATIKATI 
Kum. 32:18-21 (K) 18

(K) Humkumbuki Mwamba aliyekuzaa.

Humkumbuki Mwamba aliyekuzaa.
Mungu aliyekuzaa umemsahau.
Bwana akaona, akawachukia,
Kwa sababu ya kukasirishwa na wanawe na binti zake. (K)

Akasema, Nitawaficha uso wangu,
Nitaona mwisho wao utakuwaje;
Maana, ni kizazi cha ukaidi mwingi,
Watoto wasio imani ndani yao. (K)

Wamenitia wivu kwa kisicho Mungu, 
Wamenikasirisha kwa ubatili wao;
Nami nitawatia wivu kwa wasio watu. 
Nami nitawakasirisha kwa taifa lipumbaalo. (K)


SHANGILIO 
Kol. : 16,17

Aleluya, aleluya, Neno la Kristu likae kwa wingi ndani yenu katika hekima yote, mkimshukuru Mungu Baba kwa Yeye. Aleluya.



INJILI
Mt.13 : 31-35

Yesu aliwatolea mfano mwingine, akisema, Ufalme wa mbinguni umefanana na punje ya haradali, aliyoitwaa mtu akaipanda katika shamba lake; nayo ni ndogo kuliko mbegu zote; lakini ikiisha kumea, huwa kubwa kuliko mboga zote, ikawa mti, hata nyuni wa angani huja na kukaa katika matawi yake.

Akawaambia mfano mwingine; Ufalme wa mbinguni umefanana na chachu aliyoitwaa mwanamke, akaisitiri ndani ya pishi tatu za unga, hata ukachachwa wote pia. Hayo yote Yesu aliwaambia makutano kwa mifano; wala pasipo mfano hakuwaambia neno; ili litimie neno lililonenwa na nabii, akisema, Nitafumbua kinywa changu kwa mifano, Nitayatamka yaliyositirika tangu awali.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo



Copyright © 2026 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

YESU KRISTO, HAZINA YANGU



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumapili, 26 Julai, 2026 
Juma la 17 la Mwaka

1 Fal 3: 5, 7-12; 
Zab 118: 57, 72, 76-77, 127-128;
Rom 8: 28-30; 
Mt 13: 44-52


YESU KRISTO, HAZINA YANGU


Mwaka 1936, Edward VI Mfalme wa England, alitokea kumpenda Valcin, msichana wa kawaida. Kadiri ya mapokeo, Mfalme alikuwa na uwezo tu wa kuoa kutoka katika familia tajiri. Alikuwa na chaguzi mbili tu. Amue kuacha ufalme wake na kumuoa Valcin au kumuacha Valcin na kubaki katika ufalme wake. Lakini wote wawili walikuwa na kitu kimoja, walikuwa watu wa ndoto.

Katika somo la kwanza tunamuona Mungu anamtokea Mfalme Sulemani na kumpa uchaguzi wa kufanya: “niombe kitu nami nitakupa”. Na wakati Sulemani alivyosema “nipe moyo wa kuelewa na hali ya kuweza kutofautisha mema na mabaya”, anaomba uelewa ili aweze kuwahudumia watu wake, aweze kutenda kwa huruma na pia aweze kutambua mema na mabaya. Sulemani anatambua vitu viwili (i) Hekima yote inatoka kwa Mungu (ii) kwa kuwa na hekima mambo yote yatakuja. Kwa kutumia lugha tunaweza kusema kwamba Sulemani aliomba “lulu” ya thamani kubwa. Na aliipata. Somo linatufunsdisha kwamba tunapo yatimiza mapenzi ya Mungu tunakuwa katika njia njema na katika mstari wa ufalme wake.

Na somo la Pili barua ya mtume Paulo inatupa mambo mawili (i) mambo yote ni mazuri kama tunatenda kwa upendo wa Mungu, tunaoitwa kwa mapenzi yake (ii) Na wote aliowaita aliwachagua na pia kuwahalalisha na pia kuwapa utukufu. Na sehemu muhimu ni kwamba Mungu anawaita watu kwa ngazi mbali mbali waweze kufurahia ufalme wake wa milele. Mungu ametuita kutuhalalisha na kutupa utukufu. Paulo anavyosema Mungu anawaita, hana maana kwamba anawaita baadhi kumtumikia na wengine kupotea. Mpango wa Mungu nikuwa wote waweze kukombolewa. Hii ina maana kwamba ni mapenzi kamili ya Mungu kwamba watu wote wakombolewe kuwaruhusu watu wakubali mapenzi yake au wakatae wenyewe kwa uhuru wao.

Katika somo la Injili Yesu anahitimisha safari ndefu ya mifano kuhusu ufalme wa Mungu kwa kuawasifu wake na waume wale wote waliokuwa werefu katika kumsikiliza na kumuelewa na kujikita katika ujumbe wake. Yesu anaendelea kufundisha kuhusu “Ufalme wa Mbinguni” kwa kutumia habari ndogo za Wagalilaya.

Yesu anatuambia kwamba Hekima ya kweli ni kutambua lulu ya thamani kubwa na kuuza vyote na kuinunua. Mifano yetu miwili katika somo la Injili, kuhusu, thamani iliofichwa na lulu-ni fundisho la kuachana na malimwengu na kujikita kwa Kristo kwa kufanya ufalme wake uweze kukuwa ulimwenguni katika hali ya kweli. Matayo mtoza ushuru huenda na yeye alitambua kitu kama hiki alivyo amua kuacha vyote na kumfuata Yesu wa Nazareth. Alivyo mtambua Yesu na hekima yake, mambo yote mengine yalikuwa ni ya ziada. Yesu pia anaweza kuja katika maisha yetu ya kila siku bila sisi kujitambua kama alivyokuja kwa Mathayo.

Mfano wa kuvua samaki kwa kutumia neti: katika Palestina kulikuwa na njia mbili za kuvua samaki, wa kwanza ilikuwa kurusha neti, katika hali ya akili kubwa na utalaamu mkubwa pia kwa wakati. Aina ya pili ilikuwa ni kulazi neti chini. Na baada ya kushika, kulikuwa na kuokota baadhi na mengine kutupa, samaki wazuri walipelekwa sokoni na wengine wabaya kutupwa. Na kama neti hii ya kulaza chini inavyo kusanya samaki wazuri na wabaya, kanisa pia lina watu wema na wabaya, watakatifu na wadhambi. Kama ilivyokuwa kwa ngano na magugu, mfano huu unatuonya na hali ya kuhukumu kabla, lakini pia inatuonya kuhusu hukumu inakayo kuja.

Kuwa Mkristo Mkristo ni sawa na kuwa kama mtu anaye itafuta lulu. Kuwa mkristo ni sawa na kuwa mtu anayewinda lulu. Inagharimu majitoleo makubwa na sadaka. Lakini pia kuna tofauti kubwa kati ya wakristo na wengine. Paulo anaonesha kwa barua yake kwa Wakorintho “wachezaji wanafanya mazoezi katika hali zote, wanafanya hivyo ili kupata lulu inayo haribika, lakini sisi tunafanya hivyo ili kupata lulu isiyo haribika” (1 Kor 9:25) hali hii ni tofauti. Lulu tunayo tafuta kama Wakristo ni lulu ya thamani isiyo haribika.

Ndio maana Injili ya leo inatoa ujumbe huu muhimu. Hakuna kitu chochote ulimwenguni kinachoweza kuchukuwa nafasi ya Mungu. Inatuambia pia kilicho na maana zaidi tutakapo kufa ni maisha tutakayo ishi, jinsi tutakavyokuwa. Mifano hii inataka kutuambia kwamba wakati mmoja anapo mgundua Yesu katika maisha, vingine vyote vinakuwa ni ziada. Na hiki ndicho Mt. Paulo anacho maanisha anavyosema “kuishi kwangu ni Kristo na ufa ni faida” (Fil 2:21). Kuwa na uhusiano binafsi na Yesu na pia na wengine wengine kumfanya Yesu kuwa ndio kioo cha maisha yao-ni kitu muhimu sana ulimwenguni humu. Yesu anavyo onekana katika maumbo ya mkate na divai, tumpe nafasi ya kwanza na ya hali ya juu.

Sala: Bwana Yesu Kristo, ninatamani kukupa thamani ya kila kitu ya maisha yangu. Ninaomba niache yote ambayo ni kikwazo cha mimi kutokuja kwako, kukupenda na kukuabudi. Ninaomba nitafute Ufalme wa Mungu katika hali zote. Yesu nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUMAPILI, JULAI 26, 2026



MASOMO YA MISA, JUMAPILI, JULAI 26, 2026
JUMA LA 17 LA MWAKA


1 Fal. 3 : 5, 7-12

Huko Gibeoni Bwana alimtokea Sulemani katika ndoto ya usiku; Mungu akamwambia, Omba utakalo nikupe. Sulemani akasema, Ee Bwana, Mungu wangu, umenitawaza niwe mfalme mimi mtumwa wako badala ya Daudi baba yangu; nami ni mtoto mdogo tu; sijui jinsi inipasavyo kutoka wala kuingia. Na mtumwa wako yu katikati ya watu wako uliowachagua, watu wengi wasioweza kuhesabiwa, wala kufahamiwa idadi yao, kwa kuwa ni wengi. Kwa hiyo nipe mimi mtumwa wako moyo wa adili niwahukumu watu wako, na kupambanua mema na mabaya; maana ni nani awezaye kuwahukumu hawa watu wako walio wengi? Neno hili likawa jema machoni pa Bwana, ya kuwa Sulemani ameomba neno hili. Mungu akamwambia, Kwa kuwa umeomba neno hili, wala hukujitakia maisha ya siku nyingi; wala hukutaka utajiri kwa nafsi yako; wala hukutaka roho za adui zako: bali umejitakia akili za kujua kuhukumu; basi, tazama, nimefanya kama ulivyosema. Tazama, nimekupa moyo wa hekima na wa akili; hata kabla yako hapakuwa na mtu kama wewe, wala baada yako hatainuka mtu kama wewe.

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 118:57, 72, 76-77, 127-130 (K) 97

(K) Sheria yako naipenda mno ajabu.

Bwana ndiye aliye fungu langu,
Nimesema kwamba nitayatii maneno yako.
Sheria ya kinywa chako ni njema kwangu,
Kuliko maelfu ya dhahabu na fedha. (K)

Nakuomba, fadhili zako ziwe faraja kwangu,
Sawasawa na ahadi yako kwa mtumishi wako.
Rehema zako zinijie nipate kuishi,
Maana sheria yako ni furaha yangu. (K)

Ndiyo maana nimeyapenda maagizo yako,
Kuliko dhahabu, naam, dhahabu iliyo safi.
Maana nayaona mausia yako yote kuwa ya adili,
Kila njia ya uongo naichukia. (K)

Shuhuda zako ni za ajabu,
Ndiyo maana roho yangu imezishika.
Kufafanusha maneno yako kwatia nuru,
Na kumfahamisha mjinga. (K)


SOMO 2 
Rum 8 : 28-30

Twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake. Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwanawake, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi. Na wale aliowachagua tangu asili, hao akawaita; na wale aliowaita, hao akawahesabia haki; na wale aliowahesabia haki, hao akawatukuza. 

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu 


SHANGILIO 
Efe. 1 :17,18

Aleluya, aleluya, Ewe Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, Uyatie nuru macho ya mioyo yetu, Ili tujue tumaini la mwito wake jinsi lilivyo. Aleluya.


INJILI 
Mt. 13: 44-52

Yesu aliwaambia wafuasi wake:  Ufalme wa mbinguni umefanana na hazina iliyositirika katika shamba; ambayo mtu alipoiona, aliificha; na kwa furaha yake akaenda akauza alivyo navyo vyote, akalinunua shamba lile. Tena ufalme wa mbinguni umefanana na mfanya biashara, mwenye kutafuta lulu nzuri; naye alipoona lulu moja ya thamani kubwa, alikwenda akauza alivyo navyo vyote, akainunua.

Tena ufalme wa mbinguni umefanana na juya, lilotupwa baharini, likakusanya wa kila namna; hata lilipojaa, walilivuta pwani; wakaketi, wakakusanya walio wema vyomboni, bali walio wabaya wakawatupa Ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia; malaika watatokea, watatenga waovu mbali na wenye haki, na kuwatupa katika tanuru ya moto; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno.

Yesu aliwauliza, Mmeyafahamu hayo yote? Wakamwambia, Naam. Akawaambia, Kwa sababu hiyo, kila mwandishi mwenye elimu ya ufalme wa mbinguni amefanana na mtu mwenye nyumba atoaye katika hazina yake vitu vipya na vya kale.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUJITENGENEZA KATIKA KRISTO!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumamosi, 25 Julai, 2026
Juma la 16 la Mwaka 

Sikukuu ya Mt. Yakobo, Mtume

2 Kor 4: 7-15;
Zab 125: 1-6;
Mt 20: 20-28


KUJITENGENEZA KATIKA KRISTO!


Mtakatifu Yakobo, ambaye sikukuu yake tunaiadhimisha leo, alikuwa mtoto wa Zebedayo na Salome na kaka wa Yohane Mtume na Mwinjili. Alikuwa ni kati ya wale mitume watatu waliochaguliwa na Yesu ili waweze kutoa ushuhuda juu ya miujiza yake mikuu-kugeuka kwa Yesu sura na pia tukio la Gestemane. Alikuwa maarufu katika Kanisa la Yerusalemu, na alikuwa mtume wa kwanza kufa kwaajili ya Kristo. Alikufa kama shahidi, aliuwawa kwa upanga na Herodi Agrippa wa kwanza.

Injili ya leo, kweli ni neno la uzima kwetu sisi wote. Kwa kweli inaonesha njia ya Maisha Katika maisha ya Ukristo wetu. “kuwa kama Mwana wa mtu aliyekuja, si kutumikiwa bali kutumikia na kutoa maisha yake iwe fidia ya wengi”. “Kama unataka kuwa wa Kwanza, kuwa mtumishi wa wote”. Hili ni la kweli kabisa kwa watu katika, serikali, viongozi katika siasa, walimu shuleni, wafanya biashara, wazazi nyumbani, mapadre katika parokia na watu wote. Ni maneno yanayoenda kinyume kabisa na jinsi ulimwengu unavyotaka sisi tufanye. Mara nyingi tunasikia watu wakijitambulisha kwa vyeo vyao na madaraka waliyo nayo, leo maneno haya ya Yesu yanapaswa yasikike tena katika serikali, mashuleni, katika familia, Kanisani na zaidi sana katika maeneo yote ya kazi za mwanadamu. Mtazamo wa Ulimwengu unalenga kutawala watu. Ni kuwa na mamlaka ili katika mamlaka hayo aweze kufaidika. Na mwisho tutatumikiwa kwa jinsi yeyote tunavyotaka.

Lakini kwa Mkristo ni tofauti! Kuwa Mkristo maana yake nikufikiri kama Kristo, na kutenda kama Kristo. Kuishi maisha ya kweli, ikimaanisha kwamba, kuishi tofauti na malimwengu yanavyotaka tuishi. Injili ya leo inatualika kwenye furaha ya kweli, ambayo ni kutumikia. Na matokeo yake tutaitwa wana wa Mungu na tutashiriki katika karamu ya Mbinguni, hakika katika Maisha ya Mbinguni.

Sala: Bwana, nisaidie niweze kutembea katika njia za huduma yako. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.


MASOMO YA MISA, JULAI 25, 2026



MASOMO YA MISA, JULAI 25, 2026
JUMAMOSI, JUMA LA 16 LA MWAKA 
SIKUKUU YA MT. YAKOBO, MTUME


SOMO 1
2 Kor. 4:7 – 15

Tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili adhama kuu ya uwezo iwe ya Mungu, wala si kutoka kwetu. Pande zote twadhikika, bali hatusongwi; twaona shaka, bali hatukati tamaa; twaudhiwa, bali hatuachwi; twatupwa chini, bali hatuangamizwi; sikuzote twachukua katika mwili kuuawa kwake Yesu, ili uzima wa Yesu nao udhihirishwe katika miili yetu. Kwa maana sisi tulio hai, siku zote twatolewa tufe kwa ajili ya Yesu, ili uzima wa Yesu nao udhihirishwe katika miili yetu ipatikanayo na mauti. Basi hapo mauti hufanya kazi ndani yetu, bali uzima ndani yenu.

Lakini kwa kuwa tuna roho ile ile ya imani; kama ilivyoandikwa, Naliamini, na kwa sababu hiyo nalinena; sisi nasi twaamini, na kwa sababu hiyo twanena; tukijua ya kwamba yeye aliyemfufua Bwana Yesu atatufufua sisi nasi pamoja na Yesu, na kutuhudhurisha pamoja nanyi. Kwa maana mambo yote ni kwa ajili yenu, ili neema hiyo ikiongezwa sana, kwa hao walio wengi shukrani izidishwe, na Mungu atukuzwe.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 126 (K) 5

(K) Wapandao kwa machozi watavuna kwa kelele za furaha.

Bwana alipowarejeza mateka wa Sayuni,
Tulikuwa kama waotao ndoto.
Ndipo kinywa chetu kilipojaa kicheko,
Na ulimi wetu kelele za furaha. (K)

Ndipo waliposema katika mataifa,
Bwana amewatendea mambo makuu.
Bwana alitutendea mambo makuu,
Tulikuwa tukifurahi. (K)

Ee Bwana, uwarejeze watu wetu waliofungwa,
Kama vijito vya Kusini.
Wapandao kwa machozi,
Watavuna kwa kelele za furaha. (K)

Ingawa mtu anakwenda zake akilia,
Azichukuapo mbegu za kupanda.
Hakika atarudi kwa kelele za furaha,
Aichukuapo miganda yake. (K)



SHANGILIO
Yn. 15:16

Aleluya, aleluya,
Ni mimi niliyewachagua ninyi nikawaweka mwende mkazae matunda, na matunda yenu yapate kukaa, asema Bwana.
Aleluya.



INJILI
Mt. 2:20 – 28

Mama yao wana wa Zebedayo alimwendea pamoja na wanawe, akamsujudia, na kumwomba neno. Akamwambia, Wataka nini? Akamwambia, Agiza kwamba hawa wanangu wawili waketi mmoja mkono wako wa kuume, na mmoja mkono wako wa kushoto, katika ufalme wako. Yesu akajibu akasema, Hamjui mnaloliomba. Je! Mwaweza kunywea kikombe nitakachonywea mimi? Wakamwambia, Twaweza. Akawaambia, Hakika mtakinywea kikombe changu; lakini kuketi mkono wangu wa kuume na mkono wangu wa kushoto sina amri kuwapa, bali watapewa waliowekewa tayari na Baba yangu.

Na wale kumi waliposikia, waliwakasirikia ndugu wawili. Lakini Yesu akawaita, akasema, Mwajua ya kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha. Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu yeyote anayetaka kuwa mkubwa kwenu, na awe mtumishi wenu; na mtu yeyote anayetaka kuwa wa kwanza kwenu na awe mtumwa wenu; kama vile Mwana wa Adamu asivyokuja kutumikiwa, bali kutumikia na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengu.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.