Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

KRISTO ANAONGEA NASI KWA NJIA YA FAMILIA NA MARAFIKI ZETU!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatatu, Agosti 31, 2026.
Juma la 22 la Mwaka


1 Kor 2: 10-16; 
Zab 119:97-102
Lk 4:16-30

KRISTO ANAONGEA NASI KWA NJIA YA FAMILIA NA MARAFIKI ZETU! 

Kwa ujumla tukitazama maisha yetu, inaweza kuwa vigumu kuongelea mambo ya kiroho, Biblia na Yesu na familia zetu, ndugu na marafiki tukilinganisha na kuongea na watu tusio wajua. Inaweza ikawa tena ngumu zaidi kwa sisi wenyewe kushindwa kuona jambo lolote zuri la kiroho tunalo weza kujifunza kutoka kwa wenzetu. Inaweza kuwa tunaogopa kuchekwa au kukataliwa.

Leo Yesu anasoma sehemu ya maandiko katika chuo cha nabii Isaya, hekaluni, mbele ya ndugu zake. Yesu anaendelea kusema “hakuna nabii anaye kubalika nyumbani kwake mwenyewe”. Jamaa zake walimsikiliza na walivutwa sana, lakini wakaanza kuhitimisha mara moja kwamba huyu hana kitu, si mwana wa seremala? Mwishoni wanashikwa na hasira na wanamtoa Yesu nje wakitaka kumua. 

Kama Mwana wa Mungu alipata wakati mgumu wa kukubalika katika jamaa yake mwenyewe, itakuwa vigumu pia kushirikishana Injili na wale walio karibu yetu. Lakini kilicho cha muhimu inategemea tuna fanyaje au hatumuone Kristo katika wale walio karibu yetu? Je, sisi ni mmoja wapo wa wale wasiopenda au kukataa kumuona Kristo katika ndugu zetu wa familia na wa karibu? Je, tunakuwa watu wakuhukumu wale walio karibu yetu? 

Ukweli ni kwamba ni rahisi kwetu sisi kuona makosa ya wale walio karibu yetu kuliko kuona fadhila zao. Ni rahisi zaidi kuona dhambi zao kuliko kuona uwepo wa Kristo katika maisha yao. Lakini sio kazi yetu kunyoosha kidole juu ya dhambi zao. Ni jukumu letu kumuona Mungu ndani yao. Kila mtu aliye karibu yetu bila kuwa na shaka, ana uzuri ndani yake. Watakuwa na hali ya kumtafakari Mungu kama sisi tupo tayari kuliona kwao zaidi. Kazi yetu haipaswi kuliona hilo tu bali kulitafuta ndani yao. Na tunapo kuwa karibu zaidi kati yao ndivyo tunavyopaswa kuchunguza zaidi uwepo wa Mungu ndani ya maisha yao. 

Tafakari leo, kama upo tayarii kutaka kuona unabii wa sauti ya Kristo ulio ndani ya watu walio karibu yako. Je, upo tayari kuona, kumkubali na kumpenda yeye ndani yao? 

Sala: Bwana, ninakuomba nikuone wewe kwa wale wote waliokaribu yangu kila siku. Ninakuomba nikutafute wewe zaidi katika maisha yao. Na ninapo kupata wewe ndani yao, nikupende wewe ndani yao. Yesu, nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, AGOSTI 31, 2026



MASOMO YA MISA, AGOSTI 31, 2026
JUMATATU, JUMA LA 22 LA MWAKA

SOMO 1
1 Kor. 2:1 – 5

Ndugu zangu, mimi nilipokuja kwenu, sikuja niiwahubiri siri ya Mungu kwa ufasaha wa maneno, wala kwa hekima. Maana naliazimu nisijue neno lolote kwenu ila Yesu Kristo, naye amesulibiwa. Name nalikuwako kwenu katika hali ya udhaifu na hofu na matetemeko mengi. Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu, ili Imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 119:97 – 102 (K) 97

(K) Sheria yako, Ee Bwana, naipenda mno ajabu.

Sharia yako naipenda mno ajabu,
Ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa.
Maagizo yako hunitia hekima kuliko adui zangu,
Kwa maana ninayo siku zote. (K)

Ninazo akili kuliko wakufunzi wangu wote,
Maana shuhuda zako ndizo nizifikirizo.
Ninao ufahamu kuliko wazee,
Kwa kuwa nimeyashika mausia yako. (K)

Nimeiepusha miguu yangu na kila njia mbaya,
Ili nilitii neno lako.
Sikujiepusha na hukumu zako,
Maana Wewe mwenyewe umenifundisha. (K)


SHANGILIO
Kol. 3:16, 17

Aleluya, aleluya,
Neno la Kristo likae kwa wingi ndani yenu katika hekima yote; mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye.
Aleluya.


INJILI
Lk. 4:16 – 30

Yesu alienda Nazareti, hapo alipolelewa; na siku ya sabato akaingia katika sinagogi kama ilivyokuwa desturi yake, akasimama ilia some. Akapewa chuo cha nabii Isaya, akakifungua chuo, akatafuta mahali palipoandikwa, 

Roho wa Bwana yu juu yangu, kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, na vipofu kupata kuona tena, kuwaacha huru waliosetwa, na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa.

Akakifunga chuo, akamtudishia mtumishi, akaketi; na watu wote waliokuwamo katika sinagogi wakamkazia macho. Akaanza kuwaambia, Leo maandiko haya yametimia masikioni mwenu. Wakamshuhudia wote, wakiyastaajabia maneno ya neema yaliyotoka kinywani mwake.

Wakasema, Huyu siye mwana wa Yusufu? Akawaambia, Hapana shaka mtaniambia mithali hii, Tabibu, jiponye nafsi yako; mambo yote tuliyosikia kwamba yametendeka Kapernaumu, yatende hapa pia katika nchi yako mwenyewe. akasema, Amin, nawaambia ya kuwa, Hakuna nabii mwenye kukubalika nchi yake mwenyewe.

Lakini, kwa hakika nawaambia, Palikuwa na wajane wengi katika nchi ya Israeli zamani za Eliya, wakati mbingu zilipofungwa miaka mitano na miezi sita, njaa kuu ikaingia nchi nzima; wala Eliya hakutumwa kwa mmojawapo, ila kwa mjane mmoja wa Sarepta katika nchi ya Sidoni. Tena, palikuwa na wenye ukoma wengi katika Israeli zamani za nabii Elisha, wala hapana aliyetakaswa ila Naamani, mtu wa Shamu.

Wakajaa ghadhabu wote waliokuwa katika sinagogi walipoyasikia hayo. Wakaondoka wakamtoa nje ya mji, wakampeleka mpaka ukingo wa kilima ambacho mji wao umejengwa juu yake, wapate kumtupa chini; lakini yeye alipita katikati yao, akaenda zake.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

YATOE MAISHA KAMA HUTAKI KUYAPOTEZA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumapili, Agosti 30, 2026 
Juma la 22 la Mwaka
___________________

Yer 20:7-9; 
Zab 62:2-6, 8-9; 
Rum 12;1-2; 
Mt 16:21-27
___________________

YATOE MAISHA KAMA HUTAKI KUYAPOTEZA!

“Mbegu ya ngano isipo anguka katika ardhi na kufa, inabaki kuwa hivyo hivyo, lakini ikifa, inazaa matunda zaidi” (Yn 12:24). Mungu alimwahidia Abrahamu mafanikio na kuwa na watoto kama nyota za Mbinguni, alimwambia pia amtoe sadaka mwanae wa pekee Isaka, ambaye ndiye aliyekuwa afanye ahadi yake itimie. Jaribio kama hili linaweza kukabiliwa na mtu mwenye kuamini kama Abraham. Leo Yesu ana ahidi kuwatambulisha wafuasi katika maisha “atakaye nifuata mimi atakuwa na nuru ya uzima…hataona kifo…hatakufa.” (Yn 8:12, 51-52)

“Mungu ni mwema kwa walio na haki, kwa watu walio na mioyo safi” (Zab 73:1). “Mwamini yeye na mruhusu yeye afanye kazi atakuwa sababu ya wewe kungaa kama jua”. (Zab 37:5-6). Mungu alimwita Yeremia “Nenda utume wowote nitakao kupa, na utasema chochote kile nitakacho kuamuru useme,” wakati alivyo kuwa na woga, akilalamika kwamba yeye ni mdogo na kwamba hafahamu kuongea, Bwana alimhakikishia: “usiogope..nitakuwa nawe kukulinda…watapigana nawe lakini hawatakushinda kwani nitakuwa nawe kukuokoa” (Yer 1:7-8, 19). Yeremia alikubali, watu hawakumuelewa, aliambiwa akae kimya na hata alipigwa na kufungwa gerezani. Katika hali hii Yeremia akapaza kilio chake kwa Mungu, ambapo kinasikika katika somo la kwanza “Yahweh, uliniita mimi nami nikaitika”. Nabii anafananisha wito wake kama vile mvulani anavyo mchumbia mwanamke kwa maneno mazuri, na baada ya kukubali maneno yake, na kutimiza haja ya moyo wake, anaachwa. Hivyo anajikuta akilaani kwanini alianguka kwenye upendo wa uongo. Katika hali hiyo ya taabu, Yeremia anajazwa na hasira kwa mpendwa wake na anasema “sintamfikiria tena Mungu na wala sintaongea tena juu ya jina la Mungu”. Lakini kwasababu alisha uonja upendo wa Mungu, Yeremia anashindwa kujinasua yeye ambaye alishaitika wito wake. Ndani ya moyo wake kuna waka moto ambao hawezi kuuzima. Pamoja na mateso anayopata na wakati mgumu alionayo hawezi kuacha utume wake.

Katika somo la pili Paulo anawaasa wakristo wasije wakashikamana na mtazamo wa “ulimwengu huu”, namna ya kuwaza na jinsi dunia inavyo dhani ni hekima kwa wote. Mkristo hapaswi kuwaza na kujiingiza kwenye maadili ambayo dunia inadhani ni sawa tu kwa wote. Mkristo anapaswa kutambua, kuwa mtulivu, na kuwa na akili ya upya muda wote, tabia ambayo inakubalika kwa Mungu hata kama watu hawaitaki au haionekani yenye maana kwa watu.

Katika somo la Injii Yesu ameamua kurarua matarajio ya wafuasi. Mawazo ya mitume yalikuwa ni kupata sehemu nzuri ya heshima kwasababu ya mawazo yaliyo kuwa yameshasemwa na vongozi wa Wayahudi, kuwa na Amani na ulimwengu mpya wenye haki. Waliamini kwamba mwisho wa ulimwengu ulikuwa karibu na mkuu wao alikuwa ni Kristo, Masiha anaye subiriwa “Mwana wa Daudi”. Tangu kungara sura, na kumpa Petro funguo, walimfuata Yesu ili waweze kushuhudia uhalisia wa ndoto zao za utukufu. 

Yesu akijua hali hii ya mtazamo mbaya kuhusu yeye, anaamua kubadilisha mitizamo yao. Anasema kwa wazi kwamba yeye hatembei kuuendea utukufu huo, bali kwenda Yerusalemu kuteswa, kuuwawa na siku ya tatu atafufuka. Mitume hawakuweza kulielewa hili., kwasababu walikuwa wameshajifunza kutoka kwa Marabi kwamba Masiha hawezi kufa, na kwamba waliowema watafufuka na kuingia katika utawala wa huyu Masiha atakaye kuja, na hivyo Petro anamjibu. Petro hataki kusimama katika barabara inayo ongoza katika kutofanikiwa. Anajaribu kumbadilisha Yesu abadilishe mtazamo wake.

Jibu la Yesu “rudi nyuma yangu shetani”. Petro hakuwa anatenda kosa dogo. Alikuwa anafuata njia inayo pingana na Bwana. Alikuwa akitenda kama zile tabia za shetani aliye jaribu kumshawishi Yesu aelekeze mawazo yake katika ufalme wa kidunia, na kuwa na mamlaka ya kuangamiza. Alimuongoza katika mlima mkubwa nakumuonesha falme zote kwa mara moja na utukufu wa ulimwengu na kumwambia “yote haya nitakupa, kama utapiga goti na kunisujudia mimi” lakini Yesu akajibu “nenda zako shetani” (Mt 4:8-10). Sasa kishawishi hiki hiki –katika hali ya juu pia na Petro-hawezi kuacha bali kujibu kwa ukali ule ule.

Katika Injili ya jumapili iliyopita, Simoni Petro alikuwa ameitwa na Yesu kwamba yeye ni jiwe linaloishi la kanisa lake kwasababu alikuwa amepokea ufunuo wa Baba yake, alipokea Imani na mpango wake na amekiri Imani juu ya Mwana wa Mungu aliye hai. Sasa anajikuta yeye mwenyewe akianguka kwani aliruhusu akili ya kibinadamu imtawale. Baada ya kumkemea Petro anawageukia pia na wengine na kuwaeleza wazi.

Mambo matatu muhimu katika kubadilika “Jikane mwenyewe uchukue msalaba wako unifuate”. Kwanza, kujikana mwenyewe maana yake kila mfuasi aache kujifikiria mwenyewe kwanza. Neno hili ni ni muhimu sana katika ulimwenu wetu wa ubinafsi na umimi. Hali ya kujali mambo binafsi zaidi yanazingatiwa hata katika jambo dogo la upendo kwa wengine. Mfuasi yeyote wa Kristo anaitwa kwanza kabisa kuacha mambo yeyote ya ubinafsi, hata kujipendelea mwenyewe kiroho bila kuwaombea wengine. Daima anapaswa kutenda mapenzi ya Mungu. 

Pili, “kuchukua msalaba” haina maana ya kuvumilia mateso kidogo au makubwa ya maisha kama sehemu ya kumfurahisha Mungu. Mkristo hatafuti mateso bali upendo. Msalaba ni ishara ya upendo na zawadi kuu. Kuubeba na kumfuata Kristo maana yake umeamua kufuata ile njia yake ya upendo kwa ajili ya wanadamu. Kutoa maisha kwa ajili ya wengine, kufariji, hata kifo na mateso kwa ajili ya kubaki katika kuishika injili yake. 

Na hatimaye, “Nifuate mimi” maana yake kushiriki’ kuchagua kumfuata, kwa mapendo na kukabidhi maisha yote kwa Mungu. Kutoa maisha yako kwa mapendo na kuwa naye.

Yesu anamalizia na sababu tatu za kuwasihi wafuasi wake wapokee hayo maelekezo: kwanza, anaye toa maisha yake kwa ajili ya mwingine hayapotezi bali anayapokea. Ni yule tuu mwenye ujasiri wa kupoteza mbegu ya uzima wa maisha yake, kutupwa ardhini, “kuilinda” “ataipokea”. Pili, maisha ya ulimwengu huu yanaisha mara moja. Ni ya kupita, ni hafifu, na sio vizuri kuyategemea kama vile ni ya milele. Tatu, ni zawadi ya mwisho, Mungu hataangalia majina au mangapi tumejitengenezea mbele za watu au kwa jina letu, bali ni kazi ngapi za mapendo zinazo toka katika majina yetu. Kwa njia hiyo utakatifu wetu haupimwi na sifa wanazo sema watu juu yetu bali kazi njema za mapendo na muonekano wetu mbele ya Mungu.

Sala: Bwana, nakupenda wewe. Ninakuomba nisiogope kujikana mwenyewe, kuchukua msalaba wangu, nakukufuata wewe. Ninakuomba nikuwe katika upendo na wewe, ili niweze kuishi maisha yangu kwa upendo wako. Ninakuomba matendo ya maisha yangu yalindwe na uhusiano wangu na wewe. Ninakuomba nifuate sadaka yako ya kujitoa bila kujibakiza, na kuwa sadaka kwa watu wote. Yesu, nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUMAPILI, AGOSTI 30, 2026


MASOMO YA MISA, 
JUMAPILI, AGOSTI 30, 2026
JUMA LA 22 LA MWAKA 
________

MWANZO
Zab. 86:3, 5

Ee Bwana, unifadhili maana nakulilia wewe mchana kutwa. Kwa maana wewe, Bwana, u mwema, umekuwa tayari kusamehe, na mwingi wa fadhili kwa watu wote wakuitao.
________

SOMO I
Jer. 20:7-9

Ee Bwana, umenihadaa, nami nimehadaika; wewe una nguvu kuliko mimi, ukashinda; nimekuwa kitu cha kuchekesha, mchana kutwa; kila mtu hunidhihaki. Maana kila ninenapo napiga kelele; nalia, Dhuluma na uharibifu! Kwa kuwa neno la Bwana limefanywa shutumu kwangu, na dhihaka, mchana kutwa. Nami nikisema, Sitamtaja wala sitasema tena kwa jina lake; ndipo moyoni mwangu kumekuwamo kama moto uwakao, uliofungwa ndani ya mifupa yangu, nami nimechoka kwa kustahimili, wala siwezi kujizuia.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu
________

WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 63:1-5, 7-8 (K) 1

(K) Ee Bwana, Mungu wangu, nafsi yangu inakuonea kiu.

Ee Mungu, Mungu wangu, nitakutafuta mapema,
Nafsi yangu inakuonea kiu.
Mwili wangu wakuonea shauku,
Katika nchi kame na chovu, isiyo na maji. (K)

Ndivyo nilivyokutazama katika patakatifu,
Nizione nguvu zako na utukufu wako.
Maana fadhili zako ni njema kuliko uhai,
Midomo yangu itakusifu. (K)

Ndivyo nitakavyokubariki maadamu ni hai,
Kwa jina lako nitaiinua mikono yangu.
Nafsi yangu itakinai kama kushiba mafuta na vinono,
Kinywa changu kitakusifu kwa midomo ya furaha. (K)

Maana Wewe umekuwa msaada wangu,
Na uvulini mwa mbawa zako nitashangilia.
Nafsi yangu imekuandama sana,
Mkono wako wa kuume unanitegemeza. (K)
________

SOMO 2 
Rum 12: 1-2

Basi ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana. Wala msifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu
________

SHANGILIO
Lk 21: 36

Aleluya, aleluya,
Kesheni kila wakati, ili mpate kuokoka, 
na kusimama mbele ya Mwana wa Adamu.
Aleluya
________

INJILI 
Mt 16:21-27

Tangu wakati huo Yesu alianza kuwaonya wanafunzi wake ya kwamba imempasa kwenda Yerusalemu, na kupata mateso mengi kwa wazee na wakuu wa makuhani, na waandishi, na kuuawa, na siku ya tatu kufufuka. Petro akamchukua, akaanza kumkemea, akisema. Hasha, Bwana, hayo hayatakupata. Akageuka, akamwambia Petro, nenda nyuma yangu, Shetani; u kikwazo kwangu; maana huyawazi yaliyo ya Mungu, bali ya wanadamu.

Wakati huo Yesu aliwaambia wanafunzi wake, Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake, anifuate. Kwa kuwa mtu atakaye kuiokoa nafsi yake, ataipoteza; na mtu atakayeipoteza nafsi yake kwa ajili yangu, ataiona. Kwani atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote, na kupata hasara ya nafsi yake? Au mtu atatoa nini badala ya nafsi yake? Kwa sababu Mwana wa Adamu atakuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika zake; ndipo atakapomlipa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo
________

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

TUSIMAME KWA UKWELI!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumamosi, Agosti 29, 2026
Juma la 21 la Mwaka

Kumbukumbu ya Kukatwa kichwa kwa Yohane Mbatizaji

Yer1: 2 17-19;
Zab 96:10-13
Mk 6:17-29


TUSIMAME KWA UKWELI!


Ushahidi wa Mt. Yohane Mbatizaji unatukumbusha kwamba wito wa muhimu katika Ukristo wetu kuliko yote ni kuishi Injili. Hatuna wasi wasi kwamba Yohane aliteseka gerezani na kifungo kama shahidi wa mkombozi, yeye alikuwa ndio mtangulizi. Mtesi wake, mfalme Herode na Herodia hawakumuhukumu ili amkane Kristo, bali walitaka akae kimya kuhusu ukweli, afiche ukweli. Lakini hakuweza kukaa kimya. Na matokeo yake ilimbidi kukatwa kichwa chake na watesi wake. Alikufa kwasababu ya ukweli, alikufa kwa ajili ya Kristo. Je, Yesu hakusema “mimi ni ukweli!” kwa hiyo kwasababu Yohane alimwaga damu yake kwasababu ya ukweli ni wazi na hakika kwamba alikufa kwa ajili ya Kristo. 

Je, tumekuwa waoga kufanya jambo sahihi au kutoa ushuhuda wa Imani yetu au kusimama kwa ajili ya ukweli kwasababu tulikuwa tunaogopa wengine wanatufikiriaje au watatuambia nini? Nina Imani kwamba wengi wetu tulishakuwa hivyo, ni kitu ambacho tunapigana nacho kila wakati. Vijana wanateseka kupita katika makundi mbali mbali na hujikuta wakiingia katika tabia mbali mbali zisizo nzuri, wakati mwingine hujikuta wanahatarisha maisha yao, chanzo ikiwa nikuogopa kusimamia ukweli. Wafanyakazi wanagoma kwa kutoa sababu za kupinga rushwa au tamaduni mbali mbali zisizo jali utu wa watu. Sisi Wakristo tunakuwa Wakristo wa jina tu sio wa matendo yetu. Ni kitendo cha vita kati ya dhamiri zetu na vionjo vyetu. Tuna mfano wa mfalme Herode, aliyejua kwamba kitu cha kweli cha kufuata ni kumsikiliza Yohane Mbatizaji na kumwachia huru, lakini alikuwa anaogopa wageni wake watamfikiriaje. Kinyume na nia yake nzuri, anamtoa Yohane auwawe. Yohane alitoa thamani ngumu, kwasababu alifanya uchaguzi sahihi wa kuwa mwaminifu kwa Bwana na akasimama kadiri ya ukweli wa dhamiri yake. Ushuhuda wa Yohane ni mfano kwetu wakusimama imara kila mara kwa kuchagua lililo sahihi kila mara na kulifanya. Ni wazi mbele ya macho ya watu tunaweza kuonekana wajinga, lakini mbele ya Mungu tutaonekana kama watakatifu. 

Sala: Bwana, tufanye waenezaji wa ukweli kwa maneno na matendo yetu. Bwana ninakuomba niwe na ujasiri wa Mwana wako na nguvu kama ya Yohane Mbatizaji katika kubeba misalaba yangu katika maisha. Ninakuomba nibaki imara katika sala nikiwa nimejazwa matumaini ninapo kusikia wewe ukiniita mimi kubeba msalaba wangu. Yesu, nakutumainia wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, AGOSTI 29, 2026



MASOMO YA MISA, AGOSTI 29, 2026
JUMAMOSI, JUMA LA 21 LA MWAKA

KUMBUKUMBU YA KUFA SHAHIDI MT. YOHANE MBATIZAJI

SOMO 1
Yer 1:17-19

Neno la Bwana lilinijia, Haya basi, wewe jifunge viuno, ukaondoke, ukawaambie maneno yote niliyokuamuru; usifadhaike kwa ajili yao, nisije nikakufadhaisha wewe mbele yao. Maana, tazama, nimekufanya leo kuwa mji wenye boma, na nguzo ya chuma, na kuta za shaba, juu ya nchi yote; juu ya wafalem wa Yuda, na juu ya wakuu wake, na juu ya makuhani wake, na juu ya watu wa nchi hii. Nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, asema Bwana, ili nikuokoe.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI
Zab. 71:1-6,15,17 (K) 15

(K) Kinywa changu kitasimulia haki yako.

Nimekukimbilia Wewe, Bwana,
Nisiaibike milele.
Kwa haki yako uniponye, uniopoe,
Unitegee sikio lako, uniokoe. (K)

Uwe kwangu mwamba wa makazi yangu,
Nitakakokwenda sikuzote.
Umeamuru niokolewe,
Ndiwe genge langu na ngome yangu.
Ee Mungu wangu, uniopoe mkononi mwa mkorofi. (K)

Maana ndiwe taraja langu, Ee Bwana Mungu,
Tumaini langu tokea ujana wangu.
Nimekutegemea Wewe tangu kuzaliwa,
Ndiwe uliyenitoa tumboni mwa mama yangu,
Ninakusifu Wewe daima. (K)

Kinywa changu kitasimulia haki na wokovu wako,
Mchana kutwa; maana sijui hesabu yake.
Ee Mungu, umenifundisha tokea ujana wangu,
Nimekuwa nikitangaza miujiza yako hata milele. (K)

SHANGILIO

Aleluya, aleluya,
Heri wenye kuudhiwa kwa ajili ya haki, maana ufalme wa mbinguni ni wao.
Aleluya.

INJILI
Mk. 6:17-29

Herode mwenyewe alikuwa ametuma watu, kumkamata Yohane, akamfunga gerezani, kwa ajili ya Herodia, mkewe Filipo ndugu yake; kwa kuwa amemwoa; kwa sababu Yohane alimwambia Herodi, Si halali kwako kuwa na mke wa nduguyo.

Naye yule Herodia akawa akimvizia, akataka kumwua, asipate. Maana Herodi alimwogopa Yohane; akimjua kuwa ni mtu wa haki, mtakatifu, akamlinda; na alipokwisha kumsikiliza alifadhaika sana, naye alikuwa akimsikiliza kwa furaha.

Hata ilipotokea siku ya kufaa, na Herode, sikukuu ya kuzaliwa kwake, alipowafanyia karamu wakubwa wake, na majemadari, na watu wenye cheo wa Galilaya; ndipo binti yake yule Herodia alipoingia, akacheza, akampendeza Herode na wale walioketi pamoja naye karamuni. Mfalame akamwambia yule kijana, Niombe lolote utakaloniomba nitakupa, hata nusu ya ufalme wangu. Basi akatoka, akamwuliza mamaye, Niombe nini? Naye akasema, Kichwa cha Yohane Mbatizaji. Mara akaingia kwa haraka mbele ya mfalme, akaomba akisema, Nataka unipe sasa hivi katika kombe kichwa cha Yohane Mbatizaji. Mfalme akafanya huzuni sana lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya hao walioketi karamuni, hakutaka kumkatalia. Mara mfalme akatuma askari, akaamuru kuleta kichwa chake.

Basi, akaenda, akamkata kichwa mle gerezani, akakileta kichwa chake katika kombe, akampa yule kijana, naye yule kijana akampa mamaye. Wanafunzi wake waliposikia habari, walikwenda wakauchukua mwili wake, wakauzika kaburini.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

‘MJINGA’ KWA AJILI YA KRISTO?



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Ijumaa, Agosti 28, 2026, 
Juma la 21 la Mwaka wa Kanisa


KUMBUKUMBU YA MTAKATIFU AGOSTINO

1Kor 1:17-25; 
Zab 32: 1-2, 4-5, 10-11; 
Mt 25: 1-13


‘MJINGA’ KWA AJILI YA KRISTO?


“Mungu ndio, Yesu ndio, Kanisa hapana!”. Namna hii ya kufikiri imezoeleka sana kati ya wengi. Je, sisi ni mmoja wao kati ya hawa “wengi”? Je kuna wakati tunajisikia mafundisho ya kanisa ni “yakizamani, yamepitwa na wakati, yasiofikirika na hivyo hayafai kuyaishi”? Na pia hayaendani na zama zetu za sayansi ya hali ya juu? Na hasa kuhusu, maadili na mambo ya maisha ya familia? Je, inawezekana kuwa Wakristo wazuri wanaoenda kanisani kila mara na bado kubaki bila kusumbuliwa na kufuata “majibu ya haraka yanayoonekana” ambayo “wenye hekima na akili” wa ulimwengu huu wanayotoa, wakati mafundisho ya Kanisa yanoonekana kupishana na mambo hayo? 

Mafundisho ya Kanisa yanaweza kuonekana kuwa “Msalaba”- lakini hii ni kwasababu hayajajengwa katika “sayansi ya mwanadamu au hekima ya mwanadamu”, bali katika maisha ya Kristo, msulubiwa. Mt. Paulo anatuambia wazi. “ujumbe juu ya Msalaba kwao wanaopotea ni upuzi, bali sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu” (1Kor 1: 18). Ni ukuweli usiopingika kwamba, Kanisa linaoongozwa na Roho Mtakatifu, anayetufundisha kila kitu, nakutukumbusha yote aliyofundisha Kristo na kusema kwetu kama alivyotuahidi mwenyewe. ( Yn 14: 26). Je, inawezekana kwamba, “wanasayansi na wanafalsafa, watu mashuhuri na wanaojiona wenye akili sana- wanao tetea mawazo yao kwa kutoa hitimisho ya vitu vinavyoonekana –ambavyo kanisa linaona kwamba sio sahihi- kwamba wana akili na hekima zaidi kuliko Mungu aliyewaumba? 

“Kwasababu upumbavu wa Mungu una hekima zaidi ya wanadamu, na udhaifu wa Mungu una hekima zaidi ya wanadamu.”(1 Kor 1: 25). Kufuata anachosema Mama Kanisa huenda kikaonekana upumbavu katika kiwango cha ulimwengu, hii ni kwasababu Mama kanisa anafundisha kuendana na utashi wa Kristo aliyefanya jambo lilionekana kuwa la aibu kwa kufa msalabani ili kutukomboa sisi, wadhambi. Pengine kwako kuungama unaona ni upumbavu au jambo la aibu! Ujue kuungama ni kwaajili ya ukombozi wa roho yako. Sisi tuwe kama Kristo, tukubali kuonekana kuwa wajinga wa ulimwengu huu, kwakufuata mafundisho ya Kristo aliyoyasimika katika Kanisa lake.

Sala: Baba, tupe neema tuwe na utashi kama wa Kristo. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, AGOSTI 28, 2026



MASOMO YA MISA, AGOSTI 28, 2026
IJUMAA , JUMA LA 21 LA MWAKA

KUMBUKUMBU YA MTAKATIFU AGOSTINO

SOMO 1
1 Kor. 1:17 – 25

Kristo hakunituma ili nibatize, bali niihubiri Habari Njema; wala si kwa hekima ya maneno, msalaba wa Kristo usije ukabatilika. Kwa sababu neno la msalaba kwao wanaopotea ni upuzi, bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu. Kwa kuwa imeandikwa, Nitaiharibu hekima yao wenye hekima, Na akili zao wenye akili nitazikataa. 

Yu wapi mwenye hekima? Yu wapi mwandihsi? Yu wapi mlete hoja wa zamani hizi? Je! Mungu hakuifanya hekima ya dunia kuwa ni upumbavu? Kwa maana katika hekima ya Mungu, dunia isipopata kumjua Mungu kwa hekima yake, Mungu alipenda kuwaokoa waaminio kwa upuzi wa lile neno linalohubiriwa.

Kwa sababu Wayahudi wanataka ishara, na Wayunani wanatafuta hekima; bali sisi tunamhubiri Kristo, aliyesulibiwa; kwa Wayahudi ni kikwazo, na kwa Wayunani ni upuzi; bali kwao waitwao, Wayahudi kwa Wayunani, ni Kristo, nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu. Kwa sababu upumbavu wa Mungu una hekima zaidi ya wanadamu, na udhaifu wa Mungu una nguvu zaidi ya wanadamu.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 33:1 – 2, 4 – 5, 10 – 11 (K) 5

(K) Bwana anajaza nchi na fadhili zake.

Mpigeni Bwana vigelegele, enyi wenye haki,
Kusifu kunawapasa wanyofu wa moyo.
Mshukuruni Bwana kwa kinubi,
Kwa kinanda cha nyuzi kumi mwimbieni sifa. (K)

Kwa kuwa neno la Bwana lina adili,
Na kazi yake yote huitenda kwa uaminifu.
Huzipenda haki na hukumu,
Nchi imejaa fadhili za Bwana. (K)

Bwana huyabatilisha mashauri ya mataifa,
Huyatangua makusudi ya watu.
Shauri la Bwana lasimama milele,
Makusudi ya moyo wake vizazi na vizazi. (K)


SHANGILIO
Yn. 17:17

Aleluya, aleluya,
Neno lako ndiyo kweli, Ee Bwana, ututakase kwa ile kweli.
Aleluya.


INJILI
Mt. 25:1 – 13

Yesu aliwaambia wafuasi wake: Ndipo ufalme wa mbinguni utakapofanana na wanawali kumi, waliotwaa taa zao, wakatoka kwenda kumlaki bwana arusi. Watano wao walikuwa wapumbavu na watano wenye busara. Wale waliokuwa wapumbavu walizitwaaq taa zao, wasitwae na mafuta pamoja nao; bali wale wenye busara walitwaa mafuta katika vyombo vyao pamoja na taa zao. Hata bwana arusi alipokawia, wote wakasinzia wakalala usingizi.

Lakini usiku wa manane, pakawa na kelele, Haya, bwana arusi; tokeni mwende kumlaki. Mara wakaondoka wanawali wale wote, wakazitengeneza taa zao. Wale wapumbavu wakawaambia wenye busara, Tupeni mafuta yenu kidogo; maana taa zetu zinazimika. Lakini wale wenye busara wakawajibu, wakisema, Sivyo; hayatatutosha sisi na ninyi; afadhali shikeni njia mwende kw awauzao, mkajinunulie. Na hao walipokuwa wakienda kununua, bwana arusi akaja, nao waliokuwa wakienda kununua, bwana arusi akaja, nao waliokuwa tayari wakaingia pamoja naye arusini; mlango ukafungwa.

Halafu wakaja na wale wanawali wengine, wakasema, Bwana, Bwana, utufungulie. Akajibu akasema, Amin, nawambia, siwajui ninyi. Basi kesheni, kwa sababu hamwijui siku wala saa.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

KUWA TAYARI!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Alhamisi, Agosti 27, 2026, 
Juma la 21 la Mwaka 

Kumbukumbu ya Mt. Monika


1Kor 1:1-9; 
Zab 144:2-7; 
Mt 24:42-51


KUWA TAYARI !

Injili ya leo inatangaza kuja sio kwa tufani bali ukombozi. Inatangaza kuja kwa Ufalme wa Mungu. Na hapo hapo tunaambiwa kwamba hatujui siku wala saa itakapokuja na kuja kwake kutakuwa kama ujio wa mwizi. Njia na silaha kubwa ya mwizi ni kuja kwakustukiza. Kuja kwa Ufalme wa Mungu hakutakuwa na kengele za tahadhari. Kuna silaha moja tuu ambayo tunaweza kuiandaa kwaujio wa ufalme wa Mungu nayo ni – kuandaa maisha yetu. Mungu ametupa sisi wanadamu uhuru wakuchagua. Kila mtu anauwezo wakuchagua jema na kutenda mema nakuishi vizuri na hapo ufalme wa Mungu ujapo atakuwa amejiandaa au mtu anauwezo wakuchagua kutenda dhambi na Mungu haingilii uhuru wake, lakini Mungu ameweka wazi njia yake kwamba kuchagua uovu sio kadiri ya sheria yake. Tuombee neema ya Mungu ili tuweze kutumia uhuru wetu vizuri tuchague kutenda mema kila wakati na tuwasaidie wengine waweze kuchagua kutenda mema ili ufalme wa Mungu ujapo kwa mara ya pili utukute tumejiandaa kila wakati.

Tuna mengi sana ya kutufundisha sisi, kila mara tunawaona vijana wadogo wanapoteza maisha wakiwa na umri mdogo kabisa, pengine kwa ajali au kwa magonjwa, tunajiuliza hivi walijua kwamba Mungu angewachukua wakiwa wadogo namna hii? Tunajiuliza hivi walikuwa wamejiandaa? Sio kazi yetu kuhukumu nakujua kuhusu wema wao lakini tunachojifuza ni kwamba siku ya mwisho ya mwanadamu hapa duniani ni Mungu mwenyewe anayepanga, lililo bora tena sana ni kuwa tayari kwa ujio wa Mungu muda wowote ule. Tukiishi kwa matumaini yetu yakiwa ndani ya Kristo, siku hiyo itakuwa ya furaha kwetu na hatutaishi kwa woga. Hofu inakuja kwasababu ya dhambi, lakini tukijipatanisha na Kristo kila mara matumaini yetu kwake ni makubwa na furaha yetu ya kuungana naye itakuwa kubwa zaidi. 

Tuwasaidie ndugu zetu wote wamrudie Kristo, tukitambua kuwa hata jani la mwisho kabisa kwenye mti ni sehemu ya mti. Mkristo au ndugu unayemuona mdhambi sana bado ni sehemu ya mwili wa Kristo. Tuwasaidie ndugu zetu kwa kuwatia moyo ili wawe karibu zaidi na Kristo ili siku yake itakapokuja tuweze kupokea neema na kumlaki Kristo. Ni furaha yetu wote kwa pamoja kuuona uso wa Mungu.

Sala: Bwana, kwakupokea sakramenti kila wakati, kwanjia ya sala zangu na ndugu zangu, kwa kutembea katika mwanga wa neno lako, naomba niwe tayari daima kukupokea wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA ALHAMISI, AGOSTI 27, 2026



MASOMO YA MISA 
ALHAMISI, AGOSTI 25, 2022
JUMA LA 21 LA MWAKA


Kumbukumbu ya Mt. Monika


SOMO 1
1 Kor. 1:1 – 9

Paulo, aliyeitwa kuwa mtume wa Yesu Kristo kwa mapenzi ya Mungu, na Sosthene ndugu yetu, kwa kanisa la Mungu lililoko Korintho, wale waliotakaswa katika Kristo Yesu, walioitwa wawe watakatifu, pamoja na wote wanaoliitia jina la Bwana wetu Yesu Kristo kila mahali, Bwana wao na wetu. Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo kwa Mungu Baba yetu, na kwa Bwana Yesu Kristo.

Namshukuru Mungu sikuzote kwa ajili yenu, kwa sababu ya neema ya Mungu mliyopewa katika Kristo yesu; kwa kuwa katika kila jambo mlitajirika katika yeye, katika maneno yote, na maarifa yote; kama ushuhuda wa Kristo ulivyothibitika kwenu; hata hamkupungukiwa na karama yoyote, mkikutazamia sana kufunuliwa kwake Bwana wetu Yesu Kristo; ambaye atawathibitisha hata mwisho, ili msilaumiwe siku ile ya Bwana wetu Yesu Kristo. Mungu ni mwaminifu ambaye mliitwa na yeye mwingine katika ushirika wa Mwanawe, Yesu Kristo Bwana wetu.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 145:2 – 7 K (1)

(K) Ee Bwana, nitalihimidi jina lako milele na milele.

Kila siku nitakuhimidi,
Nitalisifu jina lako milele na milele.
Bwana ndiye mkuu mwenye kusifiwa sana,
Wala ukuu wake hautambulikani. (K)

Kizazi kwa kizazi kitayasifu matendo yako,
Kitayatangaza matendo yako makuu.
Nitakufikiri fahari ya utukufu wa adhama yako,
Na matendo yako yote ajabu (K)

Watu watayajua matendo yako ya kutisha,
Nami nitausimulia ukuu wako.
Watalihubiri kumbukumbu la wema wako mkuu.
Wataiimba haki yako. (K)



SHANGILIO
Yn. 14:23

Aleluya, aleluya,
Mtu akinipenda, atalishika neno langu, 
na Baba yangu atampenda, 
na sisi tutakuja kwake.
Aleluya.



INJILI
Mt. 24:42 – 51

Yesu aliwambia wanafunzi wake: Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu. Lakini fahamuni neno hili; kama mwenye nyumba angaliijua ile zamu mwivi atakayokuja, angalikesha, wala asingaliiacha nyumba yake kuvunjwa. Kwa sababu hiyo ninyi nanyi jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana wa Adamu yuaja.

Ni nani basi yule mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya nyumba yake, awape watu chakula kwa wakati wake? Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo. Amin, nawaambieni, atamweka juu ya vitu vyake vyote. Lakini mtumwa yule mbaya akisema moyoni mwake, Bwana wangu anakawia; akaanza kuwapiga wajoli wake, na kula na kunywa pamoja na walevi; bwana wake mtumwa huyo atakuja siku asiyodhani, na saa asiyojua, atamkata vipande viwili, na kumwekea fungu lake pamoja na wanafiki; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.