Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

SHUHUDA WA UPENDO WA MUNGU ULIMWENGUNI



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumapili, Julai 19, 2026
Juma la 16 la Mwaka

Hek 12:13, 16-19
Zab 85:5-6,15-16;
Rom 8:26-27
Mt 13:24-43


SHUHUDA WA UPENDO WA MUNGU ULIMWENGUNI


Ulimwengu ulikuja kutoka katika uzuri mikononi mwa Mungu. Uumbaji ulianza kwa kugawa mwanga na giza(Mwa 1:4). Mungu alisema na “kuweko Mwanga katika anga kugawa usiku na mchana” (Mwa 1:14). “Mungu aliona yote aliyokuwa ameumba na tazama ilikuwa nzuri sana” (Mwa 1:31). Lakini tangia hapo mwanadamu alivyo anza, bila kujua, kuogopa utofauti imeanza kuleta mchanganyo. Alianza kutenga kati ya uzuri na ubaya, kilicho safi na kisicho safi, kitakatifu na kisicho kitakatifu. Uwepo wa ubaya ulimwenguni umebaki kuwa usumbufu kwa mwanadamu. Hakubali ukweli katika ulimwengu sehemu ambayo uzuri na ubaya upo.

Katika somo la leo kutoka katika kitabu cha Hekima, mwandishi anaandika kuhusu “Haki ya Mungu. Mungu hatumii nguvu zake kutuadhibu. Anatumia tu kwa ajili ya uzuri wa Mwanadamu. Hii ndiyo haki; kutumia hekima kwa wote. Ukuu wake ni wa mahali pote, hufunika walio wema na wabaya pia. Hawapendi tu baadhi bali anawapenda wote. Wakati watu wanatumia nguvu kuogopesha wengine na kuweka hofu kwa watu au kujiweka katika hali ya kukandamiza wengine na kuwa katika hali ya juu. Mungu pamoja na kwamba yeye mwenyewe ndiye chanzo cha nguvu yote, hatumii kutisha watu wala kutumia kuadhibu, au kurudisha kisasi, bali hata katika yote yeye huonyesha huruma kwa walio dhaifu kwa ukarimu.

Katika somo la Pili Paulo anakiri kwamba sisi hatufahamu kusali. Roho ndiye anaye tusaidia kusali na kutufundisha ni maneno ghani tutumie tuweze kupeleka maneno yetu kwa Baba. Kusali kwa Mungu ni kufungua akili na mioyo yetu kwake na kuwa tayari kupokea mapenzi yake katika maisha yetu. Sala inayotokana na Roho daima inajibiwa kwasababu inakuwa inalingana na mapenzi ya Baba. Haijaribu kujitafutia mambo yake bali inatubadilisha na kutuunganisha na mapenzi ya Mungu.

Katika somo la Injili ndani ya mifano mitatu, Yesu anatufumbulia mafumbo ya ufalme wa Mungu. Je, magugu yanatoka wapi? Chanzo cha na uwepo wa uovu unahitaji maelezo. Mathayo anayatoa kwa mfano wa Yesu. Kwanza kabisa ni mwenye shamba. Huyu anamwakilisha Mungu, yeye ambaye ndiye anaye sia mbegu na kuangalia ubora wa mbegu. Wa pili ni adui,anaye wakilishwa na kinacho onekana bora katika ulimwengu. Huyu anakuja usiku na kusia magugu ambayo yanaonekana kuwa kama ngano. Mizizi yake imesongana na ngano kiasi kwamba ni vigumu kuiondoa bila kuiondoa na ngano pia. Mhusika wa pili ni mtumishi ana mwakilisha kila mmoja wetu. Wanavyo fanya ni kama sisi tunavyo kumbana na uovu ulimwenguni, katika jumuiya zetu, au kwa kila mtu. Wanaonesha kujitoa kwao katika shamba kwa ajili ya uzalishaji. Wanakosa subira, wanavutwa na tamaa ya kutaka kuyaondoa magugu mara moja. Lakini mwenye shamba yeye ni mpole. Wala hashangazwi na hali hii. Subira ya Mungu ni kubwa na anawaambia waache magugu na ngano ziote pamoja. Katika ulimwengu huu uzuri na uovu havitengani. Vipo vitaota pamoja mpaka mwisho. Mpango wa Mungu pia anataka tutambue ulimwenguni kuna uzuri na ubaya na kwamba vipo na vinaishi ulimwenguni, na hivyo tunapaswa kupokea katika hali ya maisha yetu. Uwepo wa magugu ndani mwetu unataka kutuambia pia kwamba “Hakuna mwenye haki duniani anaye tenda mema tu na ambaye hatendi dhambi” (Ybs :20). Hapa si kuhalalisha uovu, bali Yesu anataka tufahamu hilo na kwenda katika hali ya uvumilivu tukiwa na macho ya Kimungu.

Baada ya mfano huo unafuatwa na mifano mingine miwili pacha. Inaitwa mifano pacha kwasababu huleta ujumbe sawa: kwamba kulinganisha kile cha kwanza ambacho kilikuwa kidogo sana na matokeo makubwa. Mbegu ya haradali ambayo ni ndogo sana ambayo ni vigumu kuona kwa macho hukuwa na kutoa matawi makubwa, na chachu kidogo huchachusha unga wote. Ulinganishaji wake wa pekee. Mifano hii ni mwaliko wa kumtumainia Mungu.

Mifano hii ni ni mifano yetu sisi katika Jumuiya za Kikristo. Mbegu sio akili ya ulimwengu huu bali Mwana wa Mungu, Yesu. Pengine wakristo wa kwanza walipumzika mno hawakuchukulia kwa makini ahadi zao za ubatizo. Mathayo katika kuwamsha anawatikisa na kuwakumbusha kuchukulia maisha katika uhalisia. Hakufanya hivyo kuonesha kwamba ni nini kitatokea kwa wadhambi bali alitaka kuwaamsha wakristo. “Hakumtuma Mwanae ulimwenguni ili kuhukumu ulimwengu bali ulimwengu uokolewe kwa njia yake” (Yn 3:17). Je, vipi kuhusu moto? Mungu anautambua moto mmoja : Roho wa Mungu ambaye alishuka siku ya Pentekoste (Mdo 2:3). “nimekuja kuwasha moto ulimwenguni ni kwa jinsi ghani ninatamani kama umekwisha waka’? (Lk 12:49). Ni moto usiozimika utakao choma magugu yote ndani ya mioyo ya kila mmoja wetu, na kuacha tu ngano safi ambayo inahitajika katika ulimwengu ujao. Sio tangazo la kutishia na kuadhibu bali ni tangazo la kwamba siku moja Roho wa Mungu atasafisha maovu yote. Katika Ufalme wa Mungu hakutakuwa na mmoja atakayefanya kinyume.

Na mfano wa pili wa mbegu ya haradali unataka kutueleza kwamba hakuna mtu mdogo sana au mdhambi sana anayetengwa na Ufalme wa Mungu. Na pia hakuna mtu mkubwa sana anayeweza kujidai kuwa na haki zote za ufalme wa Mungu. Mungu anaweza kuvuna mavuno mengi kutoka katika moyo uliokuwa umepondeka. Mmoja anavyo jinyenyekesha kwa Bwana, na kumchagua yeye katika mambo yote, matunda huwa mengi ajabu.

Mfano wa tatu kuhusu chachu, huleta ukweli huu. Wengi wetu tunaweza kujifirikia sisi wenyewe kwamba ni wadogo sana kiasi ambacho hatuwezi kuleta mabadiliko yeyote katika jamii zetu. Chachu huwekwa katika hali ya udogo sana lakini huchachusha unga wote. Wakristo tunaitwa kuwa chachu ili tuweze kufanya ulimwengu huu sehemu nzuri ya kuishi. Kama sisi ni mashuhuda wazuri wa Injili, Neno la Mungu litaenea kila mahali. Kazi yetu kama Wakristo ulimwenguni ni muhumu sana . Tunaitwa kuwa chumvi na mwanga katika Ulimwengu huu. Kuwa ngano kati ya magugu. Kuwa kama mbegu ya haradali inayokuwa na kuleta sehemu ya kupumzika na kupata makao kwa watu, kuwa mashahidi wa upendo wa Mungu ulimwenguni. Tunaomba hali hii iweze kuwa sala yetu ya kila siku kwa Bwana, ili tuweze kubadilishwa na kuleta mabadiliko, ili Roho nyingi ziweze kupata wokovu na kufahamu upendo wa Mungu na kuwa raia wa ufalme wa Mungu.

Sala: Bwana, mimi ni mdhambi, na wewe mwenyewe ni Mtakatifu. Nipe nguvu zako na neema ili niweze kuishi maisha kadiri ya mapenzi yako. Ninaomba nisimame kwa ujasiri katikati ya uongo na uovu ambao unanizunguka. Ninaomba nikaze macho yangu daima kwako, wewe ambaye ni Mchungaji mkuu. Ninaomba niwe shahidi wa upendo wako katika familia, jirani zangu na Kanisa. Yesu, ninakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUMAPILI, JULAI 19, 2026



MASOMO YA MISA, 
JUMAPILI, JULAI 19, 2026
JUMA LA 16 LA MWAKA


MWANZO:
Zab. 54:4, 6

Tazama, Mungu ndiye anayenisaidia; Bwana ndiye anayenitegemeza nafsi yangu. Kwa ukunjufu wa moyo nitakutolea dhabihu; ee Bwana, nitalishukuru jina lako, maana ni jema.


SOMO 1 
Hek. 12 :13.16-19

Hakuna Mungu mwingine ye yote ila Wewe, unayewaangalia watu wote, hata umwonyeshe huyo ya kuwa hukuhukumu bila haki. Madhali ndio uweza wako ulio asili ya haki, na kwa sabiki ya milki yako juu ya mambo yote unawaachilia wote. Kwa kuwa iwapo wanadamu hawasadiki ya kuwa umekamilika katika uweza wako, Wewe wazidhirisha nguvu zako; tena ukijishughulisha na wale wasioikiri kweli hiyo, waifadhaisha jeuri yao. Walakini desturi yako unauzuia hata uweza wako, na kuhukumu kwa upole, na kututawala kwa uvumilivu mwingi. Yaani uweza unao, wakati wo wote utakapo kuutumia.

Pamoja na hayo, uliwafundisha watu wako kwa matendo yako ya namna hiyo ya kwamba imempasa mwenye haki kuwa mpenda wanadamu; tena ukawatilia wanao tumaini jema, kwa sababu, endapo watu wametenda dhambi, unawajalia toba.

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 86:5-6, 9-10, 15-16 (K) 5

(K) Kwa maana Wewe, U mwema, Umekuwa tayari kusamehe.

Wewe, Bwana, U mwema,
Umekuwa tayari kusamehe.
Na mwingi wa fadhili,
Kwa watu wote wakuitao.
Ee Bwana, uyasikie maombi yangu;
Uisikilize sauti ya dua zangu. (K)

Mataifa yote uliowafanya watakuja;
Watakusujudia Wewe, Bwana.
Watalitukuza jina lako;
Kwa kuwa ndiwe uliye mkuu.
Wewe ndiwe mfanya miujiza,
Ndiwe Mungu peke yako. (K)

Lakini Wewe, Bwana,
U Mungu wa rehema na neema.
Mvumilivu, mwingi wa fadhili na kweli.
Unielekee na kunifadhili mimi. (K)


SOMO 2 
Rum 8 : 26-27

Roho hutusaidia udhaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo; lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa. Na yeye aichunguzaye mioyo aijua nia ya Roho ilivyo, kwa kuwa huwaombea watakatifu kama apendavyo Mungu.

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu


SHANGILIO 
Yn. 17:17

Aleluya, aleluya, 
Neno lako ndiyo kweli, 
Ee Bwana, Ututakase sisi kwa ile kweli. 
Aleluya.


INJILI 
Mt. 13:24-43

Yesu aliwatolea mfano, akisema, Ufalme wa mbinguni umefanana na mtu aliyepanda mbegu njema katika konde lake; lakini watu walipolala, akaja adui yake akapanda magugu katikati ya ngano, akaenda zake. Baadaye majani ya ngano yalipomea na kuzaa, yakaonekana na magugu. Watumwa wa mwenye nyumba wakaenda wakamwambia, Bwana, hukupanda mbegu njema katika konde lako? limepata wapi basi magugu? Akawaambia, Adui ndiye aliyetenda hivi. Watumwa wakamwambia, Basi, wataka twende tukayakusanye? Akasema, La; msije mkakusanya magugu, na kuzing’oa ngano pamoja nayo. Viacheni vyote vikue hata wakati wa mavuno; na wakati wa mavuno nitawaambia wavunao, Yakusanyeni kwanza magugu, myafunge matita matita mkayachome; bali ngano ikusanyeni ghalani mwangu.

Akawatolea mfano mwingine, akisema, Ufalme wa mbinguni umefanana na punje ya haradali, aliyoitwaa mtu akaipanda katika shamba lake; nayo ni ndogo kuliko mbegu zote; lakini ikiisha kumea, huwa kubwa kuliko mboga zote, ikawa mti, hata nyuni wa angani huja na kukaa katika matawi yake.

Akawaambia mfano mwingine; Ufalme wa mbinguni umefanana na chachu aliyoitwaa mwanamke. akaisitiri ndani ya pishi tatu za unga, hata ukachachwa wote pia. Hayo yote Yesu aliwaambia makutano kwa mifano; wala pasipo mfano hakuwaambia neno; ili litimie neno lililonenwa na nabii, akisema, Nitafumbua kinywa changu kwa mifano, Nitayatamka yaliyositirika tangu awali.

Kisha Yesu akawaaga makutano, akaingia nyumbani; wanafunzi wake wakamwendea, wakasema, Tufafanulie mfano wa magugu ya kondeni. Akajibu, akasema, Azipandaye zile mbegu njema ni Mwana wa Adamu; lile konde ni ulimwengu; zile mbegu njema ni wana wa ufalme; na yale magugu ni wana wa yule mwovu; yule adui aliyeyapanda ni Ibilisi; mavuno ni mwisho wa dunia; na wale wa wavunao ni malaika. Basi, kama vile magugu yakusanywavyo na kuchomwa motoni; ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia. Mwana wa Adamu atawatuma malaika zake; nao watakusanya kutoka katika ufalme wake machukizo yote, na hao watendao maasi, na kuwatupa katika tanuru ya moto; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno. Ndipo wenye haki watakapong’aa kama jua katika ufalme wa Baba yao. Mwenye masikio, na asikie.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

UTUMISHI WA YESU!


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumamosi, 18 Julai, 2026
Tafakari ya Kila siku
Juma la 15 la Mwaka

Kut 12:37-41
Zab 136:1-10
Mt: 12:14-21


UTUMISHI WA YESU! 

 
Neno kuu katika injili ya leo ni ‘tazama mtumishi wangu niliyemchagua.’ Kama Yesu alivyosema, hakuna ushahidi mkubwa kuliko ule wa Mungu baba kumshuhudia mwana; na huu ndio ushuhuda, kama ilivyoandikwa kwanza na nabii isaya, na kutafsiriwa na mwinjili mathayo. Lakini mtumishi mwaminifu wa Mungu anahukumiwa na watumishi wa uongo. Tunaona kuna mwendelezo katika hali ya taifa la israeli kumkataa Kristo. kuna mashaka, kupinga, kutojali na hatimaye kumkataa. Haya yote yanaongozwa na mafarisayo na waandishi wanaochukuliwa kuwa viongozi wa dini katika yerusalemu na Israeli. Tofauti na suluhisho lao baada ya baraza waliyokaa na kuamua kupanga namna ya kumwangamiza, roho wa Mungu alionesha maajabu na uzuri wa Kristo. Ndio kusema kuwa Mungu anamzungumzia Kristo toauti kabisa na ulimwengu unavyomzungumzia. Yesu angeweza kufanya chochote kujilinda dhidi ya washitaki wake, lakini huo haukuwa mpango wa Mungu. Alijitoa kabisa kufanya mapenzi ya baba yake. Akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Hicho ndicho kiini cha utumishiwake.

Sala: Ee Bwana, nisaidie kukabiliana na upinzani na maadui zangu kwa upendo badala ya chuki na vita. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JULAI 18, 2026




MASOMO YA MISA, JULAI 18, 2026
JUMAMOSI YA 15 YA MWAKA



SOMO YA 1
Mik. 2:1 – 5

Ole wao wakusudiao mambo maovu, na kutenda mabaya vitandani mwao! Kunapopambazuka asubuhi huyafanya, kwa sababu ya katika uwezo wa mikono yao. Nao hutamani mashamba, na kuyashika; na nyumba pia, nao huzichukua; nao humwonea mtu na nyumba yake, naam, mtu na urithi wake. Basi Bwana asema hivi, Angalia, nakusudia jambo baya juu ya jamaa hii, ambalo hamtazitoa shingo zenu, wala hamtakwenda kwa kiburi; kwa maana ni wakati mbaya. Siku hiyo watatunga mithali juu yenu, na kuomboleza kwa maombolezo ya huzuni nyingi, na kusema, Sisi tumenyang’anyiwa kabisa; Yeye analibadili fungu la watu wangu; Jinsi anavyoniondolea hilo!

Awagawia waasi mashamba yetu. Kwa hiyo hutakuwa na mtu atakayeitupa Kamba kwa kura katika mkutano wa Bwana.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 10:1 – 4, 7 – 8, 14 (K) 12

(K) Usiwasahau wanyonge, Ee Bwana.

Ee Bwana, kwa nini wasimama mbali?
Kwa nini kujificha nyakati za shida?
Kwa kiburi chake asiye haki
Mnyonge anafuatiwa kwa ukali;
Na wanaswe kwa hila zizo hizo walizoziwaza. (K)

Maana mdhalimu hujisifia tamaa ya nafsi yake,
Na mwenye choyo humkana Bwana na kumdharau.
Mdhalimu kwa kiburi cha uso wake
Asema, Hatapatiliza.
Jumla ya mawazo yake ni, Hakuna Mungu. (K)

Kinywa chake kimejaa laana,
Na hila na dhuluma.
Chini ya ulimi wake kuna madhara na uovu,
Hukaa katika maoteo ya vijivi.
Mahali pa siri humwua asiye na hatia,
Macho yake humvizia mtu duni. (K)

Umeona, maana unaangalia madhara na jeuri,
Uyatwae mkononi mwako.
Mtu duni hukuachia nafsi yake,
Maana umekuwa msaidizi wa yatima. (K)



SHANGILIO
Yn. 14:23

Aleluya, aleluya,
Mtu akinipenda, atalishika neno langu, na Baba yangu atampenda, na sisi tutakuja kwake.
Aleluya.



INJILI
Mt. 12:14 – 21

Mafarisayo walitoka wakafanya shauri juu ya Yesu jinsi ya kumwangamiza. Naye Yesu hali akiyafahamu hayo akaondoka huko; na watu wengi wakamfuata; akawaponya wote, akawakataza wasimdhihirishe; ili litimie neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema,
Tazama, mtumishi wangu niliyemteua; mpendwa wangu, moyo wangu uliyependezwa naye; nitatia roho yangu juu yake, naye atawatangazia Mataifa hukumu. Hatateta wala hatapaza sauti yake; wala mtu hatasikia sauti yake njiani. Mwanzi uliopondeka hatauvunja, wala utambi utokao moshi hatauzima, hata ailetapo hukumu ikashinda. Na jina lake Mataifa watalitumainia.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

KUSHIKA SIKU TAKATIFU YA SABATO!




ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Ijumaa, Julai 19, 2024
Juma la 15 la Mwaka


Isa. 38:1 – 6, 21 – 22, 7 – 8
Isa. 38:10 – 12, 16 (K) 17
Mt 12:1-8


KUSHIKA SIKU TAKATIFU YA SABATO!


Mitume wa Yesu walikuwa na njaa wakaanza kuvunja masuke ya ngano na kula ili kupooza njaa yao. Mafarisayo walianza kuwalaumu mitume wa Yesu kwani wanafanya kitu ambacho wao walikiita “kinyume na sheria” ya Sabato. Walisema kwamba kitendo cha mitume kukata masuke ya ngano na kula kilionekana ni “kazi” kiasi ambacho kinavunja sheria ya sabato ambayo watu hawapaswi kufanya kazi. Mitume hawakufanya kitu chochote kibaya ila walilaumiwa. Walikuwa watu wasio na kosa kama Yesu anavyosema. Yesu anawajibu Mafarisayo na hali yao yakutokufikiri vizuri kwa kuwakumbusha maandiko “nataka rehema na sio sadaka”. Anasema kwamba mitume wameonewa kwasababu mafarisayo hawakuelewa maandiko haya juu ya Huruma ya Mungu.

Sheria ya Sabato ya kupumzika ilikuwa imetoka kwa Mungu. Lakini sheria ya kupumzika haikuwa kwa ajili yake yenyewe. Siku ya sabato ya kupumzika ilikuwa zawadi kwa wanadamu kwani Mungu alijua Mwanadamua anahitaji siku ya kupumzika. Alitambua tunahitaji muda wa kupumzika katika wiki, kumwabudu Mungu na kuwa na wengine. Lakini mafarisayo waliigeuza siku ya sabato kuwa mzigo mkubwa. Waliifanya kuwa mzigo na hivyo kushindwa kuifanya iwe siku ya kumwabudu Mungu na kukutana na wengine.

Sisi huwa tunafanya hali yetu ya kujiona tumeelimika na kuwafanya watu waone kazi yangu au biashara yangu ndio maisha yote. Hali hiyo inakataliwa na kupingwa na siku ya Sabato. Kila siku ya sabato inatuambia kwamba sisi sio, vifaa bali ni watu. Hatupo ulimwenguni huku kutengeneza vitu na pesa, tupo ulimwenguni kujielimisha katika uzuri na urafiki na kumjua Mungu. Sabato inatukumbusha kwamba sisi sio mashine bali ni viumbee pekee vya kumtumikia Mungu. Sisi sio watu wabinafsi, bali watu tunaoshirikiana na kupendana. Hivyo katika siku hii tumkumbuke Muumba wetu na viumbe vyote katika siku hii. Tujiunge na viumbe vyote tumwimbie Mungu na kuifanya siku hii TAKATIFU!

SALA: Bwana, nisaidie kupenda sheria yako. Nisaidie mimi niweze kuiona katika huruma na neema. Ninaomba niburudishwe kwa amri zako na kunyanyuliwa katika mapenzi yako. Yesu nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JULAI 17, 2026




MASOMO YA MISA, JULAI 17, 2026
IJUMAA YA 15 YA MWAKA


SOMO 1
Isa. 38:1 – 6, 21 – 22, 7 – 8

Siku hizo Hezekia aliugua, akawa katika hatari ya kufa; na Isaya nabii, mwana wa Amozi, akaenda kwa mfalme, akamwambia, Bwana asema hivi, Tengeneza mambo ya nyumba yako; maana utakufa, wala hutapona. Basi Hezekia akajigeuza, akaelekeza uso wake ukutani, akamwomba Bwana, akasema, Ee Bwana, kumbuka haya, nakusihi kwamba nimekwenda mbele zako katika kweli na kwa moyo mkamilifu, na kutenda yaliyo mema machoni pako. Hezekia akalia sana sana.

Kisha neno la Bwana likamjia Isaya, kusema, Enenda ukamwambie Hezekia, Bwana, Mungu wa Daudi, baba yako, asema hivi, Mimi nimeyasikia maombi yako, nimeyaona machozi yako; tazama nitaziongeza siku zako, kiasi cha miaka kumi na mitano. Nami nitakuokoa wewe, na mji huu, na mkono wa mfalme wa Ashuru, name nitaulinda mji huu.

Basi Isaya akasema, Na watwae mkate wa tini, wakauweke juu ya jipu, naye atapona. Tena Hezekia alikuwa amesema, Iko ishara gani ya kunionyesha ya kuwa nitapanda niingie nyumbani mwa Bwana? Jambo hili liwe ishara kwako itokayo kwa Bwana, ya kuwa Bwana atalitimiza jambo hili alilolisema; Tazama, nitakirudisha nyuma kivuli madaraja kumi, ambayo kilishuka juu ya duara ya Ahazi kwa sababu ya jua. Basi jua likarudi madaraja kumi katika hiyo duara, ambayo limekwisha kushuka.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Isa. 38:10 – 12, 16 (K) 17

(K) Umeniokoa na shimo la uharibifu, Ee Bwana.

Nalisema, katika usitawi wa siku zangu
Nitakwenda kuingia malango ya kuzimu;
Nimenyimwa mabaki ya miaka yangu. (K)

Nalisema, Sitamwona Bwana, yeye Bwana,
Katika nchi ya walio hai;
Sitamwona mwanadamu tena pamoja na hao
Wakaao duniani. (K)

Kao langu limeondolewa kabisa,
Limechukuliwa kama hema ya mchungaji;
Nimekunja maisha yangu kama mfumaji;
Atanikatilia mbali na kitanda cha mfumi;
Tangu mchana hata usiku wanimaliza. (K)

Ee Bwana, kwa mambo hayo watu huishi;
Na uhai war oho yangu u katika hayo yote;
Kwa hiyo uniponye na kunihuisha. (K)



SHANGILIO
Yn. 10:27

Aleluya, aleluya,
Kondoo wangu waisikia sauti yangu, name nawajua, nao wanifuata.
Aleluya.



INJILI
Mt. 12:1 – 8

Wakati ule Yesu alipita katika mashamba siku ya sabato; wanafunzi wake wakaona njaa, wakaanza kuvunja masuke, wakala. Na Mafarisayo walipoona, walimwambia, Tazama! Wanafunzi wako wanafanya neno ambalo si halali kulifanya siku ya sabato.

Akawaambia, Hamkusoma alivyotenda Daudi, alipokuwa na njaa, yeye na wenziwe? Jinsi alivyoingia katika nyumba ya Mungu, akaila mikate ile ya wonyesho, ambayo si halali kwake kuila wala kwa wale wenziwe, ila kwa makuhani peke yao? Wala hamkusoma katika torati, kwamba siku ya sabato makuhani hekaluni huinajisi sabato wasipate hatia? Lakini nawaambieni, kwamba hapa yupo aliye mkuu kuliko hekalu. Lakini kama mngalijua maana yake maneno haya, Nataka rehema, wala si sadaka, msingaliwalaumu wasio na hatia. Kwa maana Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MWALIKO KUTOKA KWA YESU




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Alhamisi, Julai 16, 2026
Juma la 15 la Mwaka

Isa. 26:7 – 9, 12, 16 – 19
Zab. 102:12 – 20 (K) 19
Mt 11:28-30


MWALIKO KUTOKA KWA YESU


“Kuna kitu zaidi katika maisha” “Bwana lazima atakuwa na mpango na mimi”. Maneno haya tumeyazoea katika maisha yetu, maneno ambayo huonekana mara nyingi kwa wale ambao huonekana kutokuwa na furaha katika maisha. Ni maneno ya wale wanaotafuta maana ya maisha yao.

Mwaliko kutoka kwa Yesu, “njooni kwangu ninyi nyote mnao sumbuka na kuelemewa na mizigo nami nitawapumzisha”, ni maneno ambayo tunayasikia daima. Ni maneno ya faraja yenye kutualika tumkaribishe Yesu aangaze maisha yetu ya kila siku, achukue hofu zetu, kuchanganyikiwa kwetu, na yote tuliobeba ambayo yanatuangusha chini. Ni mwaliko wa upendo na huruma na ni mwaliko ambao tunapaswa kuukubali kila siku.

Ni kitu gani kinacho kuelemea? Ni kitu ghani kinacho kufanya uzidiwe na mizigo kiasi ambacho kinakuweka daima katika machungu, kukosa Amani na uwa na hofu nyingi? Je, kuna kitu ambacho unakifikiria sana? Je, kuna kitu ambacho unaona kabisa huwezi hata kukigusa? Chochote kile ambacho kina sumbua moyo wako, Yesu anataka kukinyanyua. Mara nyingi tunabeba mizigo mingi katika maisha ambayo hatutaki kuiachia iondoke. Tunakuwa na hofu ya kumkaribisha Yesu aingie ndani mwetu. Kuja kwa Yesu inamaana kwamba kuwa tayari kuyakabili yote katika hali ya kweli na uawazi na kukabili mizigo yetu mbele ya Yesu. Lakini kitu kikubwa ambacho tunapaswa kufahamu ni kwamba Yesu ni mpole, mwenye huruma, mkarimu katika kusamehe na neema. Yeye anatamani kubeba mizigo yetu juu zaidi hata zaidi ya jinsi tunavyopenda yeye ainyanyue. Yeye anaona ukandamizaji wote na anatamani daima kuuondoa.

Tafakari leo kuhusu huu wito wa Yesu wa upole “Njoo kwangu” bila kuwa na hofu na wasi wasi. Mgeukie yeye na muache yeye aweze kuchambua vitu peke yake. Yeye Anakupenda zaidi ya jinsi unavyo dhani na yeye ataiweka miguu yako katika njia iliyo sawa. Fungua moyo wako kwa Yesu. Tembea katika kiini cha Bwana katika sala na kutana naye katika Ekaristi. Sikiliza wito wake.

Sala: Bwana, ninakuja kwako na ninaleta kila mzigo wangu kwako. Ninakupa maisha yangu, matumaini yangu, hofu zangu, wakati wangu wote wa sasa na ujao, na hofu zote katika maisha. Yesu ninakupa kila kitu. Yesu, nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JULAI 16, 2026




MASOMO YA MISA, JULAI 16, 2026
ALHAMISI YA 15 YA MWAKA

KUMBUKUMBU YA BIKIRA MARIA WA MLIMA KARMELI


SOMO 1
Isa. 26:7 – 9, 12, 16 – 19

Njia yake mwenye haki ni unyofu; wewe uliye mnyofu wainyosha njia ya mwenye haki. Naam, katika njia ya hukumu zako sisi tumekungoja, Ee Bwana; shauku ya nafsi zetu inaelekea Jina lako na ukumbusho wako.

Kwa nafsi yangu nimekutamani wakati wa usiku; naam, kwa nafsi yangu ndani yangu nitakutafuta mapema; maana hukumu zako zikiwapo duniani, watu wakaao duniani hujifunza haki.
Bwana, utatuamuria Amani; maana ni wewe pia uliyetutendea kazi zetu zote. Bwana, katika taabu zao walikwenda kwako; waliomba maombi mengi wakati adhabu ayko ilipokuwa juu yao.

Kama vile mwanamke mwenye mimba anayekaribia wakati wake wa kuzaa, alivyo na utungu na kulia kwa sababu ya maumivu yake, ndivyo tulivyokuwa sisi mbele zako, Ee Bwana. Tumekuwa na mimba, tumekuwa na utungu, tumekuwa kana kwamba tumeza upepo; hakutkufanya wokovu wowote duniani, wala hawakuanguka wakaao duniani.

Wafu wako wataishi, maiti zangu zitafufuka; amkeni, kaimbeni, ninyi mnaokaa mavumbini, kwa maana umande wako ni kama umande wa mimea, nayo ardhi itawatoa waliokufa.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 102:12 – 20 (K) 19

(K) Toka mbinguni Bwana ameangalia nchi.

Wewe, Bwana, utaketi ukimiliki milele,
Na kumbukumbu lako kizazi hata kizazi.
Wewe mwenyewe utasimama,
Na kuirehemu Sayuni,
Kwa maana ndio wakati wa kuihurumia,
Naam, majira yaliyoamriwa yamewadia.
Maana watumishi wake wameyaridhia mawe yake;
Na kuyaonea huruma mavumbi yake. (K)

Kisha mataifa wataliogopa jina la Bwana,
Na wafalme wote wa dunia utukufu wake.
Bwana atakapokuwa ameijenga Sayuni,
Atakapoonekana katika utukufu wake.
Atakapoyaelekea maombi yake aliye mkiwa,
Asiyadharau maombi yao. (K)

Kizazi kitakachokuja kitaandikia hayo,
Na watu watakaoumbwa watamsifu Bwana.
Maana ametazama toka patakatifu pake pa juu,
Toka mbinguni Bwana ameangalia nchi.
Ili akusikie kuugua kwake aliyefungwa,
Na kuwafungua walioandikiwa kufa. (K)



SHANGILIO
Zab. 111:7, 8

Aleluya, aleluya,
Maagizo yako yote, ee Bwana, ni amini, yamethibitika milele na milele.
Aleluya.



INJILI
Mt. 11:28 – 30

Yesu aliwaambia makutano: Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, name nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

SIRI YA UFALME WA MUNGU ILIYO FUNULIWA KWA WATOTO!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatano, Julai 15, 2026
Juma la 15 la Mwaka

Isa. 10: 5 – 7, 13 – 16
Zab. 94: 5 – 10, 14 – 15 (K) 14
Mt 11:25-27


SIRI YA UFALME WA MUNGU ILIYO FUNULIWA KWA WATOTO!


Tunatambua sisi wote kwamba watoto wadogo wapo makini sana. Hasa wanapo kutana na watu wakarimu na wenye upendo, wana hisi mara moja na wanavutiwa kwao. Watoto wana waamini wakubwa. Kwahiyo kutoka katika hali hii ya watoto, uhusiano wetu na Mungu unapaswa kujikita katika hali hii na sio kumweka katika majaribu! Katika Injili Yesu anasema, vitu vyote amekabidhiwa na Baba yake. Ni kwasababu ana mwamini Baba yake bila kujibakiza.

Yesu anashuhudia kwamba Baba anawafunulia mambo yake wale walio kama watoto wachanga. Chakushangaza ni kwamba anasema, Baba amewaficha mambo haya wale wenye hekima na akili”. Lakini hii ina maana kwamba sio vizuri kujiona watu ambao tunafahamu kila kitu na kwamba tuna kila kitu. Sio vizuri kujazwa na majivuno na kujiona una majibu yote. Hatupaswi kusahau nini maana ya kuwa kama watoto wachanga. Haijalishi ni msomi namna ghani lakini twaweza kuwa wajinga sana. Hekima na akili haina thamani kama hatuna Imani kwa Mungu kama watoto wachanga wanavyo waamini wazazi wazuri. Haijalishi nina elimu namna ghani, hatuwezi kumpita Mungu. Mungu daima ni mwenye hekima, mwenye nguvu, na mwaminifu daima! Maisha hayapaswi kuchanganywa, yanapaswa kuwa ya kawaida.

Tafakari leo, ni kwa jinsi ghani ulivyo tayari kumrudia Mungu kwa moyo wa unyenyekevu hasa kwa maswali magumu katika maisha. Tafakari ni kwa jinsi ghani ulivyo tayari kumgeukia kwa Imani na matumaini ukifahamu kwamba Mungu daima ana majibu katika maisha yetu ya kila siku.

Sala: Bwana, ninakuja tena kwako kwa kukuamini. Nisaidie mimi nitambue kuwa hekima yote inatoka kwako Baba na sio kwangu. Nisaidie mimi nikugeukie wewe daima kama mtoto na nisaidie maisha yangu yabaki ya kawaida kama unavyo tamani. Yesu, nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, JULAI 15, 2026




MASOMO YA MISA, JULAI 15, 2026\
KUMBUKUMBU YA MTAKATIFU BONAVENTURI
JUMATANO YA 15 YA MWAKA


SOMO 1
Isa. 10: 5 – 7, 13 – 16

Bwana asema hivi: Ole wake Ashuru! Fimbo ya hasira yangu, ambaye gongo lililo mkononi mwake ni ghadhabu yangu! Nitamtuma juu ya taifa lenye kukufuru, nitampa maagizo juu ya taifa lenye kukufuru, nitampa maagizo juu ya watu wa ghadhabu yangu, ateke nyara, na kuchukua mateka, na kuwakanyaga kama matope ya njiani. Lakini hivyo sivyo akusudiavyo mwenyewe, wala sivyo moyo wake uwazavyo; maana katika moyo wake akusudia kuharibu, na kukatilia mbali mataifa, wala si mataifa machache.

Kwa maana amesema, Kwa nguvu za mkono wangu nimetenda jambo hili, na kwa hekima yangu; maana mimi nina busara; name nimeiondoa mipaka ya watu, nikaziteka akiba zao, nikawaangusha waketio juu ya viti vya enzi kama afanyavyo shujaa. Na mkono wangu umezitoa maji za mataifa kama katika kioto cha ndege; na kama vile watu wakusanyavyo mayai yaliyoachwa, ndivyo nilivyokusanya dunia yote; wala hapana aliyetikisa bawa, wala kufumbua kinywa, wala kulia.

Je! Shoka lijisifu juu yake alitumiaye? Je! Msumeno ujitukuze juu yake auvutaye? Ingekuwa kana kwamba bakora ingewatikisa waiinuao, au fimbo ingemwinua yeye ambaye si mti.

Kwa hiyo Bwana, Bwana wa majeshi, atawapekelea kukonda watu wake walionona; na badala ya utukufu wake kutawashwa kuteketea kama kuteketea kwa moto.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 94: 5 – 10, 14 – 15 (K) 14

(K) Bwana hatawatupa watu wake.

Ee Bwana, wanawaseta watu wako;
Wanauseta urithi wako;
Wanamwua mjane na mgeni;
Wanawafisha yatima. (K)

Nao husema, Bwana haoni;
Mungu wa Yakobo hafikiri.
Enyi wajinga miongoni mwa watu fikirini;
Enyi wapumbavu, lini mtakapopata akili? (K)

Aliyelitia sikio mahali pake asisikie?
Aliyelifanya jicho asilione?
Awaadhibuye mataifa asikemee?
Amfundishaye mwanadamu asijue? (K)

Kwa kuwa Bwana hatawatupa watu wake.
Wala hutauacha urithi wake,
Maana hukumu itairejea haki,
Na wote walio wanyofu wa moyo wataifuata. (K)



SHANGILIO
Zab. 27:11

Aleluya, aleluya,
Ee Bwana, unifundishe njia yako, na kuniongoza katika njia iliyonyoka.
Aleluya.



INJILI
Mt. 11:25 – 27

Wakati ule Yesu alijibu akasema, Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga. Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyopendeza mbele zako. Akasema, Nimekabidhiwa vyote na baba yangu; wala hakuna amjuaye Mwana, ila Baba; wala hakuna amjuaye Baba, ila Mwana, na yenyote ambaye Mwana apenda kumfunulia.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com