Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

KUJIFUNZA KUSAMEHE!




“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Jumanne, Februari 24, 2026
Juma la 1 la Kwaresima

Isa 55:10-11;
Zab 34: 4-7, 16-19;
Mt 6: 7-15


KUJIFUNZA KUSAMEHE!


Mara nyingi, kipindi cha kwaresima ni kipindi ambacho katika mwaka tunapima afya zetu za Kiroho, lakini pia ni wakati ambapo tunapaswa kuangalia, kama tunajiangalia zaidi nafsi zetu kuliko kumwangalia Mungu wetu anayetupenda. Kwaresima ni kipindi cha kuangalia kama Mungu anachukua nafasi ya Kwanza. 

Mt. Augustino alisema: Sala ya Baba yetu, ni kamilifu kabisa kiasi kwamba inafupisha kwa maneno machache yote ambayo mwanadamu anataka kumwomba Mungu. Mzizi wa sala hii ni MSAMAHA. Kusamehe na kusamehewa. Yote yanapaswa kutamaniwa na kutafutwa. Pengine changamoto iliopo katika kusamehe wengine ni hali ya “haki” ambayo inaonekana kupotea baada ya msamaha kutolewa. Hili ni kweli hasa kwa mtu ambaye anasamehewa ambaye ameshindwa kuomba msamaha. Katika hali nyingine wakati mmoja ameomba msamaha, na kuonesha kutubu, ni rahisi kusamehe. Lakini wakati aliyekosea haoneshi hali ya kutubu wala kujuta, hili linaacha hali ya kuoneakana kama kuna ukosefu wa haki wakati msamaha unapotolewa. Na hili linaweza kuwa ngumu sana kwetu kulishinda.

Kuwasamehe watu hakumanishi unaifuta dhambi. Msamaha haina maana kwamba dhambi haikutendwa au kwamba ni sawa tu imetokea. Bali, kumsamehe kunatenda tofauti. Kusamehe ni wazi kwamba kunaionesha dhambi yenyewe, kuikubali na kuona jinsi ya kuachana nayo. Hili ni muhimu kulielewa. Kwa kuitambua dhambi ambayo inapaswa kusamehewa, alafu na kuisamehe, haki inatendeka katika hali ya Kimungu. Haki inatendeka kwa njia ya huruma. Na huruma ina msaidia anayetoa msamaha zaidi kuliko yule anayepokea. Kwa kuona huruma kwa dhambi ya mwingine, tunakuwa huru kwa madhara ya dhambi ya mwingine. Huruma ni njia ya Mungu ya kuondoa maumivu haya katika maisha yetu na kutuweka huru tuweze kutambua huruma yake zaidi kwa msamaha wa dhambi zetu wenyewe, huruma ambayo hatuwezi kusema tunaipata kwa jitihada zetu wenyewe tu. 

Tutafakari leo, kuhusu mtu ambaye kweli unataka kumsamehe. Ni nani na alifanya nini kukuumiza? Usiogope kuwa na huruma na kumsamehe wala usisite kufanya hivyo. Na kwa huruma utakayotoa italeta haki ya Mungu katika hali ambayo kwa nguvu zako mwenyewe huwezi kuitimiza. Kwa kitendo cha kusamehe kinakufanya kikuweke huru kwa mzigo wa dhambi, na kumfanya Mungu akusamehe wewe makosa yako. 

Sala: Bwana, mimi ni mdhambi ninaye hitaji huruma yako. Ninapo tafuta huruma yako, nisaidie pia niwasamehe wengine kwa madhara walio nitendea. Yesu nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 24, 2026




MASOMO YA MISA, FEBRUARI 24, 2026
JUMANNE, JUMA LA 1 LA KWARESIMA



SOMO 1
Isa. 55:10-11

Bwana asema: Kama vile mvua ishukavyo, na theluji, kutoka mbinguni, wala hairudi huko: bali huinywesha ardhi, na kuizalisha na kuichipuza ikampa mtu apandaye mbegu, na mtu alaye chakula; ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 34:3-6, 15-18 (K)17

(K) Wenye haki, Bwana anawaponya na taabu zao zote.

Mtukuzeni Bwana pamoja nami,
Na tuliadhimishe jina lake pamoja.
Nalimtafuta Bwana akanijibu,
Akaniponya na hofu zangu zote. (K)

Wakamwelekea macho wakatiwa nuru,
Wala nyuso zao hazitaona haya.
Maskini huyu aliita, Bwana akasikia,
Akamwokoa na taabu zake zote. (K)

Macho ya Bwana huwaelekea wenye haki,
Na masikio yaje hukielekea kilio chao.
Uso wa Bwana ni juu ya watenda mabaya,
Aliondoa kumbukumbu lao duniani. (K)

Walilia, naye Bwana akasikia,
Akawaponya na taabu zao zote.
Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo,
Na waliopondeka roho huwaokoa. (K)



SHANGILIO
Zab. 95:8

Leo msifanye migumu mioyo yenu, 
lakini msikie sauti yake Bwana.



INJILI
Mt. 6:7-15

Siku ile Yesu aliwaambia wafuasi wake: Mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke, kama watu wa mataifa; maana wao hudhani ya kuwa watasikiwa kwa sababu maneno yao kuwa mengi. Basi msifanane na hao; maana Baba yenu anajua mnayohitaji kabla ninyi hamjamwomba. Basi ninyi salini hivi:

Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe, Ufalme wako uje, Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni. Utupe leo riziki yetu. Utusamehe deni zetu, kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu. Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu.
Kwa maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi. Bali msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

NI NANI NDUGU YANGU ALIYE MDOGO?




“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Jumatatu, Februari 23, 2026
Juma la 1 la Kwaresima

Law 19: 1-2, 11-18;
Zab 19: 8-10, 15;
Mt 25: 31- 46


NI NANI NDUGU YANGU ALIYE MDOGO?


Kwaresima ni kipindi cha kufanya yote upya, kubadili tabia zetu na kufanya mazuri zaidi na kuacha mabaya. Ni mwaliko wakwenda juu zaidi ya mtizamo wetu wa kawaida wa kibinadamu wakutazama vitu na kuangalia maisha yote na uhusiano na wengine, kwa jicho la Mungu. Mara nyingi tunajitizama wenyewe na tunadhani kwamba sisi ni watakatifu, kwasababu hatutendi dhambi kama wengine. Lakini leo tunaitwa tuende mbele zaidi ya hilo, tukuwe katika fadhila na neema.

Injili ya leo inatuambia kwamba, Yesu atatuuliza yote tulio watendea walio wadogo kwamba tuli mlinitendea Yeye. Ni ajabu kwamba Yesu anaonesha kabisa kwa kusema kwamba ni watu wadogo, pengine wale wanao onekana ni wadhambi kabisa, walio dhaifu, walio wagonjwa, wasio jiweza walio na njaa na wasio na makao, na wote wale wanao shindwa kupata mahitaji ya maisha. Jambo nzuri kabisa Yesu anajitambulisha mwenyewe kuwa na wanyonge, wadogo wa aina zote. Kwa kuwatumikia walio na mahitaji ya pekee tunakuwa tuna mtumikia Yesu. Na kwa kuonyesha muungano na wao namna hiyo, Yesu anafunua utu wao kama wanadamu.

Tutafakari juu ya utu wa kila mtu. Je, unaangalia nini kwa huyo mtu? Ni kitu ghani unakitumia kumhukumu? Ni ndani ya huyu mtu, ambapo Yesu anatusubiria sisi. Anatusubiri sisi tuweze kumpenda yeye kwa walio dhaifu na wanao onekana hawafai. Tujitoe wenyewe kuwapenda na kuwatumikia, kwani ndani yao tutampenda na kumtumikia Bwana.

Sala: Bwana mpendwa, ninaelewa na kuamini wewe upo, katika hali ya kujificha kwa walio wanyonge na dhaifu, masikini na katika wadhambi walio kati yetu. Ninaomba nikutafute wewe kwa kila mmoja nitakaye kutana naye, hasa wale walio wahitaji. Yesu nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 23, 2026





MASOMO YA MISA, FEBRUARI 23, 2026
JUMATATU, JUMA LA 1 LA KWARESIMA


SOMO 1
Law. 19:1-2, 11-18

Bwana akanena na Musa, akamwambia, Nena na mkutano wote wa wana wa Israeli, uwaambie, Mtakuwa watakatifu; kwa kuwa mimi Bwana, Mungu wenu, ni mtakatifu.

Msiibe, wala msidanganye, wala msiambiane uongo. Msiape uongo kwa jina langu, hata ukalinajisi jina la Mungu wako; Mimi ndimi Bwana. Usimdhulumu jirani yako, wala kumnyang’anya mali yake; ijara yake aliyeajiriwa isikae kwako usiku kucha hata asubuhi. Usimlaani kiziwi, wala usitie kwazo mbele ya kipofu, bali umche Mungu wako; Mimi ndimi Bwana. Msitende yasiyo haki katika hukumu, usimpendelee mtu maskini, wala kumstahi mwenye nguvu; bali utamhukumu jirani yako kwa haki. Usiende huko na huko katikati ya watu wako, kama mchongezi; wala usisimame kinyume cha damu ya jirani yako; Mimi ndimi Bwana. Usimchukie ndigu yako moyoni mwako; ni lazima kumkemea jirani yako, wala usichukue dhambi kwa ajili yake. Usifanye kisasi, wala kuwa na kinyongo juu ya wana wa watu wako; bali umpende jirani yako nafsi yako; Mimi ndimi Bwana.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 19:7-9, 14 (K) Yn. 6:64

(K) Bwana unayo maneno ya uzima wa milele.

Sheria ya Bwana ni kamilifu,
Huiburudisha nafsi.
Ushuhuda wa Bwana ni amini,
Humtia mjinga hekima. (K)

Maagizo ya Bwana ni ya adili,
Huufurahisha moyo.
Amri ya Bwana ni safi,
Huyatia macho nuru. (K)

Kicho cha Bwana ni kitakatifu,
Kinadumu milele,
Hukumu za Bwana ni kweli,
Zina haki kabisa. (K)

Maneno ya kinywa changu,
Na mawazo ya moyo wangu,
Yapate kibali mbele zake, Ee Bwana,
Mwamba wangu, na mwokozi wangu. (K)



SHANGILIO
Zab. 51:1-10, 12

Ee Mungu, uniumbie mioyo yenu; 
Unirudishie furaha ya wokovu wako.



INJILI
Mt. 25:31-46

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Hapo atakapokuja Mwana wa Adamu katika utukufu wake, na malaika watakatifu wote pamoja naye, ndipo atakapoketi katika kiti cha utukufu wake; na mataifa yote watakusanyika mbele zake; naye atawabagua kama vile mchungaji abaguavyo kondoo na mbuzi; atawaweka kodnoo mkono wake wa kuume, na mbuzi mkono wake wa kushoto.

Kisha Mfalme atawaambia wale walioko mkono wake wa kuume, Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme, mliowekewa tayari tangu kuubwa ulimwengu; kwa maana nalikuwa na njaa, mkanipa chakula; nalikuwa na kiu, mkaninywesha; nalikuwa mgeni, mkanikaribisha; nalikuwa uchi, mkanivika; nalikuwa mgonjwa, mkaja kunitazama; nalikuwa kifungoni, mkanijia.

Ndipo wenye haki watakapomjibu, wakisema, Bwana, ni lini tulipokuona una njaa, tukakulisha, au una kiu tukakunywesha? Tena ni lini tulipokuona u mgeni, tukakukaribisha, au u uchi, tukakuvika? Na Mfalme atajibu, akiwaambia, Amin, nawaambia, kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu zangu walio wadogo, mlinitendea mimi.

Kisha atawaambia na wale walioko mkono wake wa kushoto, Ondokeni kwangu, mliolaaniwa, mwende katika moto wa milele, aliowekewa tayari Ibilisi na malaika zake; kwa maana nalikuwa na njaa, msinipe chakula; nalikuwa na kiu, msininyweshe; nalikuwa mgeni, msinikaribishe; nalikuwa uchi, msinivike; nalikuwa mgonjwa na kifungoni, msije kunitazama.

Ndipo hao pia watajibu, wakisema, Bwana, ni lini tulipokuona wewe una njaa, au una kiu, au u mgeni, au u uchi, au u mgonjwa, au u kifungoni, tusikuhudumie? Naye atawajibu, akisema, Amin, nawaambia, Kadiri msivyomtendea mmojawapo wa hao walio wadogo, hamkunitendea mimi. Na hao watakwenda zao kuingia katika adhabu ya milele; bali wenye haki watakwenda katika uzima wa milele.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

VISHAWISHI-NAFASI YA KUKUWA!



“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Jumapili, Februari 22, 2026
Jumapili ya 1 ya Kwaresima

Mwa 2:7-9; 3:1-7; 
Zab 51:3-6, 12-14, 17; 
Rum 5: 12-19;
Mt 4: 1-11.


VISHAWISHI-NAFASI YA KUKUWA! 


Kushawishiwa , maana yake ni kuvutwa kwenye kitu kisichoruhusiwa. Injili ya Leo inatuambia Yesu alijaribiwa “Kristo kuhani Mkuu, alijaribiwa kwa kila namna kama tulivyo lakini hakutenda dhambi” (Ebr 4:15). Biblia inatualika tutazame vishawishi kama nafasi ya kujipima uchaguzi wetu, nafasi ya kukuwa. Uchaguzi upo kati ya kukubali mpango wa Mungu au kuukataa. Adamu aliamua kuchagua njia isiofaa/hukumu yake mwenyewe; Kristo daima alirejea neno la Mungu daima. Adamu alinyoosha mkono wake juu ya tunda la kifo; Yesu amekuwa chanzo cha uhai. 

Kitabu cha Mwanzo kinamuonesha mwanadamu akiwa katika bustani ya Edeni, ambapo katikati yake kulikuwa na mti wa “uhai” na “maarifa” mema na mabaya. Ni kwa ajili ya Mungu na unawakilisha vizuizi viwili ambavyo havipaswi kuvukwa. Kwanza unawakilisha alama ya Mungu, mtoa uhai, na asiyeweza kufa. Mwanadamu kunyoosha mkono juu ya mti huu ni sawa na kukataa hali yake ya kibinadamu. Pia mti ni wa maarifa ya mema na mabaya. Kunyoosha mkono juu ya mti huu ni kutaka kuwa mkuu wa maamuzi yako na matendo yako mwenyewe. Ni jambo kubwa la kutaka kujianzilishia ukuu-kuanza kumpinga Mungu au kukataa maneno yake ya Kibaba ambayo ni maneno ya maadili mema ya kuchagua. Wakati mwanadamu anasahau kwamba yeye ni kiumbe aliyeumbwa na kujaribu kujifanya Mungu, mjuaji wa mema na mabaya anajimaliza mwenyewe. Ni wazi kwamba anaanza kuita “ubaya kuwa ni wema na kuita wema ni ubaya: kubadili giza kuwa mwanga na mwanga kuwa giza, vitu vichungu na kusema vitamu, au kusema vitamu kuwa vichungu” (Isa 5:20). 

Nyoka anaingia katikati na anawaalika Adamu na Eva kula tunda lililokatazwa. Kitabu cha Hekima kinanyambulisha kuwa ni muovu. (Hek 2:23-24). Kinatufanye tushangae ni muovu yupi anaye shawishi na kudanganya. Nyoka ni mnyama , mwerevu kuliko wanyama wote aliyeumbwa na Mungu. Ni kilele cha kazi ya Mungu aliofanya. Ndio, nyoka si mwingine isipokuwa mwanadamu mwenyewe ambaye, kwa kufikia kilele cha majivuno yake, anatambua mwisho wa uwezo wake. Anajitengenezea maadili yake mwenyewe, akijifanya kutenda mambo katika hali ya kipekee. Nyoka anawakilisha hali yetu ya kupenda mapenzi yetu yawe zaidi ya mapenzi ya Mungu, kujiona wenyewe kuwa Mungu. Ndio sehemu hii ya mwanadamu inatufanya tutende pasipo Mungu. Maneno ya nyoka si kitu kingine zaidi ya mawazo yetu ya ndani ambayo ndipo dhambi inapo anzia. Kitu kingine ni dhambi. Dhambi inazaliwa kwa kutafuta vitu vizuri na vya furaha. Uharibifu ni kwamba, kutokumwamini Mungu, mwanadamu anachagua sehemu mbaya, kupoteza lengo na kujiangamiza mwenyewe. Baada ya dhambi hawaukubali ukweli. Wanajaribu kujificha na kujisikia kukata majani na kujifunika wenyewe. 

Katika somo la pili, Paulo najaribu kuonesha kwamba Adamu ni wazi anajukumu la maovu yote. Anatumia ulinganishaji, kati ya Adamu na Kristo kuelezea kazi ya ukombozi alioitimiza Yesu. Adamu alitaka kuwa bwana wa mema na mabaya, na badala yake akapata kifo kama mshahara wake. Kristo, kinyume na Adamu, alitambua utegemezi wake na Mungu. Alikuwa daima mwaminifu kwa Baba, akawa Bwana wa uhai. Wote wanaomfuata na kuiga utii wake kwa Baba watafanywa wenye haki. 

Katika somo la Injili, “Yesu alikaa jangwani kwa siku arobaini na alijaribiwa na shetani” (Mk 1:12-13). Kwa kutumia lugha ya Biblia na lugha ya picha, alimaanisha maisha yote ya Yesu yalikuwa kati yake na huku shetani akimjaribu. Majibu ya Yesu kwa shetani yanawakilisha matukio matatu ya wana Waisraeli katika kitabu cha kutoka: manunguniko ya chakula na zawadi ya manna (Kut 16), kugoma kwasababu ya maji (Kut 17), kuabudu ndama wa shaba (kut 32) hivyo Yesu anayaishi tena maisha ya watu wake. Yeye anapatwa na majaribu yale yale, lakini anayashinda. Ni wale tu, wanaothamini maisha yao katika mwanga wa neno la Mungu wanaoweza kutoa ushuhuda wa kweli Ulimwenguni. 

Vishawishi vipo. Ni matokeo ya maanguko ya wanadamu wa kwanza. Yanatoka katika udhaifu wetu lakini pia kutoka katika yule muovu. Yesu hakukubali kuanguka katika vishawishi alivyokuwa jangwani na wala hakuanguka katika kishawishi katika maisha yake yote. Aliyashinda na kuteseka kwa ajili ya hayo. Hili linatuambia kwamba anaweza kuwa kiongozi wetu na mfano wetu wa kuiga wakati tukiwa katikati ya vishawishi kila mara na kila siku. Wakati mwingine tunaweza kujisikia wa pweke tuliotengwa katika jangwa la dhambi zetu. Tunaweza kujisikia kama vile mnyama mkali wa tamaa zetu unatushinda. Tunaweza kujisikia yule muovu anatunyemelea. Sawa, Yesu alipatwa na haya pia. Aliruhusu kupitia haya kwa kushiriki ubinadamu wetu. Kwa njia hii ni Yesu anayeweza kukutana nasi katika jangwa letu. Yupo tayari anatusubiri, akitutafuta, akituita sisi. Ni huyu alieyeshinda vishawishi vya muovu jangwani, ndiye atakaye tuongoza kuepuka. Kwahiyo, kama jangwa lako ni mahangaiko ya maisha sasa, au ni majaribu mbali mbali, Yesu anataka kukutana nawe akuongoze katika njia iliyo njema. Alimshinda yule wa jangwani na jinsi alivyokuwa, hivyo anauwezo wakushinda jangwa lolote lile katika maisha yako.

Sala: Bwana, ninakubali upendo wako mkamilifu kwangu. Nina amini kwamba unanipenda mimi kiasi kwamba nitaweza kuvumilia mateso, kuelewa mateso yote. Ninakuomba nikutane nawe katika jangwa la maisha yangu. Ninakuomba nikuruhusu wewe uniongoza katika sehemu tulivu na yenye maji. Yesu nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 22, 2026



MASOMO YA MISA, FEBRUARI 22, 2026
DOMINIKA YA 1 YA KWARESIMA



SOMO 1
Mwa. 2:7 – 9, 3:1 – 7

Bwana Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai. Bwana Mungu akampanda bustani upande wa mashariki wa Edeni, akamweka ndani yake huyo mtu aliyemfanya. Bwana Mungu akachipusha katika ardhi kila mti unaotamanika kwa macho na kufaa kwa kuliwa; na mti wa uzima katikati ya bustani, na mti wa ujuzi wa mema na mabaya.

Basi nyoka alikuwa mwerevu kuliko wanyama wote wa mwitu aliowafanya Bwana Mungu. Akamwambia mwanamke, Ati! Hivi ndivyo alivyosema Mungu, Msile matunda ya miti yote ya bustani?
Mwanamke akamwambia nyoka, Matunda ya miti ya bustanini twaweza kula; lakini matunda ya mti ulio katikati ya bustani Mungu amesema, Msiyale wala msiyaguse, msije mkafa.

Nyoka akamwambia mwanamke, Hakika hamtakufa, kwa maana Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.

Mwanamke alipoona ya kuwa ule mti wafaa kwa chakula, wapendeza macho, nao ni mti wa kutamanika kwa maarifa, basi alitwaa katika matunda yake akala, akampa na mumewe, naye akala. Wakafumbuliwa macho wote wawili wakajijua kuwa wa uchi, wakashona majani ya mtini, wakajifanyia nguo.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 51:1 – 4, 10 – 12, 15

(K) Uturehemu, ee Bwana, kwa kuwa tumetenda dhambi.

Ee Mungu unirehemu,
Sawasawa na fadhili zako.
Kiasi cha wingi wa rehema zako,
Uyafute makosa yangu.
Unioshe kabisa na uovu wangu,
Unitakase dhambi zangu. (K)

Maana nimejua mimi makosa yangu,
Na dhambi yangu I mbele yangu daima.
Nimekutenda dhambi Wewe peke yako,
Na kufanya maovu mbele ya macho yako. (K)

Ee Mungu, uniumbie moyo safi,
Uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu.
Usinitenge na uso wako,
Wala roho yako mtakatifu usiniondolee. (K)

Unirudishie furaha ya wokovu wako;
Unitegemeze kwa roho ya wepesi.
Ee Bwana, uifumbue midomo yangu,
Na kinywa changu kitazinena sifa zako. (K)



SOMO 2
Rum. 5:12 – 19

Kama kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.

Maana kabla ya sheria dhambi ilikuwamo ulimwenguni, lakini dhambi haihesabiwi isipokuwapo sheria; walakini mauti ilitawala tangu Adamu mpka Musa, nayo iliwatawala hata wao wasiofanya dhambi ifananayo na kosa la Adamu, aliye mfano wake yeye atakayekuja. Lakini karama ile haikuwa kama lile kosa; kwa maana ikiwa kwa kukosa kwake yule mmoja wengi walikufa, zaidi sana neema ya Mungu, na kipawa kilicho katika neema yake mwanadamu mmoja Yesu Kristo kimezidi kwa ajili ya wale wengi. Wala kadiri ya yule mtu mmoja aliyefanya dhambi si kadiri ya kile kipawa; kwa maana hukumu ilikuja kwa njia ya mtu mmoja ikaleta adhabu; bali karama ya neema ilikuja kwa ajili ya makosa mengi, ikaleta kuhesabiwa haki.

Kwa maana ikiwa kwa kusa mtu mmoja mauti ilitawala kwa sababu ya yule mmoja, zaidi sana wao wapokeao wingi wa neema, na kile kipawa cha haki, watatawala katika uzima kwa yule mmoja, Yesu Kristo. Basi tena, kama kwa kosa moja watu wote walihukumiwa adhabu, kadhalika kwa tendo moja la haki watu wote walihesabiwa haki yenye uzima. Kwa sababu kama kwa kuasi kwake mtu mmoja watu wengi waliingizwa katika hali ya wenye dhambi, kadhalika kwa kutii kwake mmoja watu wengi wameingizwa katika hali ya wenye haki.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



SHANGILIO
Mt. 4:4

Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.



INJILI
Mt. 4:1 – 11

Kisha Yesu alipandishwa na Roho nyikani, ili ajaribiwe na Ibilisi. Akafunga siku arobaini mchana na usiku, mwisho akaona njaa. Mjaribu akamjia akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, amuru kwamba mawe haya yawe mikate. Naye akajibu akasema, Imeandikwa, Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa ila neno litokalo katika kinywa cha Mungu. Kisha Ibilisi akamchukua mpaka mji mtakatifu, akamweka juu ya kinara cha hekalu, akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu jitupe chini; kwa maana imeandikwa, Atakuagizia malaika zake; na mikononi mwao watakuchukua; Usije ukajikwaa mguu wako katika jiwe.

Yesu akamwambia, Tena imeandikwa, Usimjaribu Bwana Mungu wako. Kisha Ibilisi akamchukua mpaka mlima mrefu mno, akamwonyesha milki zote za ulimwengu, na fahari yake, akamwambia, Haya yote nitakupa, ukianguka kunisujudia. Ndipo Yesu alipomwambia, Nenda zako, Shetani; kwa maana imeandikwa, Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake. Kisha Ibilisi akamwacha; na tazama, wakaja malaika wakamtumikia.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUMTEMBELEA DAKTARI YA MIOYO YETU!



“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Jumamosi, Februari 21, 2026
Jumamosi baada ya Jumatano ya majivu

Isa 58: 9-14;
Zab 86: 1-6;
Lk 5: 27-32


KUMTEMBELEA DAKTARI YA MIOYO YETU!


Roho ya kweli ya Kwaresima ni, kufunga, kutoa sadaka na sala, yote haya yamejengwa juu ya kwenda kinyume na matamanio yetu, na kutamani kuwa na Mungu katika Ufalme wake. Hii haina maana kwamba mmoja anapaswa kuacha kwa muda wa siku 40 ili awasaidie maskini wakati wa Kwaresima tu. Tunapaswa kuelewa nafasi mbali mbali zinazokuja katika maisha yetu ya kila siku. Ni muda pia wa kuacha dhambi na kupokea uponyaji kutoka kwa mganga mtakatifu.

Yesu aliwahitaji wadhambi. Yeye ni mkombozi, na mkombozi aliwahitaji wadhambi ili awakomboe! Kuja kwa Yesu tukiwa na mizigo ya dhambi zetu, inampa furaha katika moyo wake. Anafurahi kwasababu anatimiza ule utume aliotumwa na Baba yake, akionesha kuruma yake kama Mkombozi pekee. Muacha akupe huruma yake! Unafanya hivi kwa kuja kwake katika hali yako ya dhambi na kujinyenyekesha mbele kama asiestahili huruma yake, na ambaye unastahili tu hukumu. Kuja kwa Yesu inamfanya yeye aweze kuonesha huruma yake kutoka katika chemchemi ya huruma yake.

Angalia katika hali ya kwamba Yesu ni Mganga Mtakatifu anayekusubiri ili aweze kutimiza wajibu wake wa kuponya. Anakuhitaji wewe ukubali dhambi zako na kuwa wazi kwa uponyaji wake. Kwa kufanya hivyo, unaruhusu mlango wa huruma yake ufunguke na kumimina baraka kwako na katika kipindi chetu.
               
Sala: Mpendwa Mkombozi na Mganga Mtakatifu, ninakushukuru kwa kuja kutukomboa na kutuponya. Ninakushukuru kwa tamaa yako ya kuonesha huruma yako katika maisha yangu. Naomba uninyenyekeshe niweze kuwa wazi kwa uponyaji wako. Yesu nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 21, 2026





MASOMO YA MISA, FEBRUARI 21, 2026
JUMAMOSI BAADA YA MAJIVU


SOMO 1
Isa. 58:9-14

Bwana asema hivi: Kama ukiiondoa nira; isiwepo kati yako, wala kunyosha kidole, wala kunena maovu; na kama ukimkunjulia mtu mwenye njaa nafsi yako, na kuishibisha nafsi iliyoteswa; ndipo nuru yako itakapopambazuka gizani; na kiwi chako kitakuwa kama adhuhuri.

Naye Bwana atakuongoza daima, ataishibisha nafsi yako mahali pasipokuwa na maji, na kuitia nguvu mifupa yako; nawe utakuwa kama bustani iliyotiwa maji, na kama chemchemi ambayo maji yake hayapungui.

Na watu wako watapajenga mahali palipokuwa ukiwa; utaiinua misingi ya vizazi vingi; nawe utaitwa, Mwenye kutengeneza mahali palipobomoka; na, Mwenye kurejeza njia za kukalia.

Kama ukigeuza mguu wako usiihalifu sabato, usifanye anasa yako siku ya utakatifu wangu; ukiita sabato siku ya furaha, na siku takatifu ya Bwana yenye heshima; ukiitukuza, kwa kutokuzifanya njia zako mwenyewe, wala kuyatafuta yakupendezayo wala kusema maneno yako mwenyewe; ndipo utakapojifurahisha katika Bwana; nami nitakupandisha mahali pa nchi palipoinuka; nitakulisha urithi wa Yakobo baba yako; kwa maana kinywa cha Bwana kimenena hayo.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 86:1-2, 3-4, 5-6 (K) 11

(K) Ee Bwana, unifundishe njia yako;
Nitakwenda katika kweli yako.

Ee Bwana, utege sikio lako unijibu,
Maana mimi ni maskini na mhitaji,
Unihifadhi nafsi yangu,
Maana mimi ni mcha Mungu.
Wewe uliye Mungu wangu,
Umwokoe mtumishi wako anayekutumaini. (K)

Wewe, Bwana, unifadhili,
Maana nakulilia Wewe mchana kutwa.
Uifurahishe nafsi ya mtumishi wako,
Maana nafsi yangu nakuinulia Wewe, Bwana. (K)

Kwa maana Wewe, Bwana, U mwema,
Umekuwa tayari kusamehe,
Na mwingi wa fadhili,
Kw awatu wote wakuitao.
Ee Bwana, uyasikie maombi yangu;
Uisikilize sauti ya dua zangu. (K)



SHANGILIO
Eze. 33:11

Waambie, kama mimi niishivyo, asema Bwana Mungu, Sikufurahii kufa kwake mtu mwovu; Bali aghairi mtu mwovu, na kuiacha njia yake akaishi.



INJILI
Lk. 5:27-32

Siku ile: Yesu akaona mtoza ushuru, jina lake Lawi, ameketi forodhani, akamwambia, Nifuate. Akaacha vyote, akaondoka, akamfuata.

Na Lawi akamfanyia karamu kubwa nyumbani mwake; palikuwa na mkutano mkuu wa watoza ushuru na watu wengineo waliokuwa wameketi chakulani pamoja nao. Ikawa Mafarisayo na waandishi wao kuwanung’unukia wanafunzi wake, wakisema, Mbona mnakula na kunywa pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi? Yesu akajibu akawaambia, Wenye afya hawana haja na tabibu, isipokuwa walio hawawezi. Sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.