Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

KUVUTWA KWA YESU!



“KUFUFUKA NA KRISTO”
Tafakari ya Pasaka
Alhamisi, Aprili 23, 2026
Juma la 3 la Mwaka

Mdo 8:26-40;
Zab 66:8-9,16-17,20 (K. 1);
Yn 6:44-51.


KUVUTWA KWA YESU!

Karl Rahner anasema, “kila ninapo ongea kuhusu mimi najikuta nikiongelea kuhusu Mungu, na kila ninapo ongelea kuhusu Mungu najikuta naongea kuhusu mimi”. Safari ya maisha yetu pia karibia ni kuvuta kila kitu na kila mtu kwangu. Katika ulimwengu huu ambao kila mtu yupo na shughuli zake ni rahisi sana kuruhusu sauti mbali mbali zituharibu. Ni rahisi kusikia kusukumwa huku na kule katika ulimwengu na mambo yake yote. Ulimwengu umekuwa mzuri sana ukiteka mipango yetu yote na kutupatia kuridhika kwa haraka lakini utatuacha bila kitu.

Lakini sauti ya Mungu na mwaliko wake ni tofauti. Unapatikana katika ukimya wa ndani. Lakini haina maana kwamba unapaswa kuwa katika monasteri ili kupata ukimya huu wa ndani. Unapatika katika uaminifu mkubwa katika sala kila siku, na tabia ya kurudi kwa Mungu kila wakati katika vitu vyote. Unapatikana tunapo jibu wito wa Mungu, na kuifuata, na kurudia tena kila mara. Hili linajenga tabia ya kuvutwa karibu, kusikia, na kuitika na kuvutwa karibu na kusikiliza na kuitika tena na tena.

Katika Injili ya leo, tunatambua kuwa tumeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, na tunavutwa daima kwa Mungu. Ndani kabisa mwa moyo wa Mwanadamu, ana mtamani Mungu. Ndio maana Yesu anasema wazi kwamba “hakuna ajaye kwangu asipovutwa na Baba yangu” (Yn 6: 44). Katika somo la kwanza tunamuona Ofisa wa Ethiopia wakati akisoma chuo cha nabii Isaya, anakutana na ukweli katika Maandiko Matakatifu kwa msaada wa Filipo, na baadae anamkubali Yesu kama Mkombozi na Bwana.

Tutenge muda tuvutwe kwa Yesu. Tenga muda mchache au zaidi kila siku wa ukimya. Funga macho na jisikilize. Msikilize Mungu akiongea na wewe. Wakati akikuvuta kwake itika kwa ukarimu. Huu ndio uchaguzi mzuri kabisa ambao waweza kufanya kila siku!

Sala: Bwana, naomba univute karibu ili niweze kutambua sauti yako. Ninapo kusikia ukiita, nisaidie niweze kukuitikia kwa ukarimu. Maisha yangu ni yako, Bwana mpendwa. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, APRILI 23, 2026




MASOMO YA MISA, APRILI 23, 2026
ALHAMISI, JUMA LA 3 LA PASAKA


SOMO 1
Mdo. 8:26-40

Malaika wa Bwana akasema na Filipo, akamwambia, Ondoka ukaende upande wa kusini hata njia ile itelemkayo kutoka Yerusalemu kwenda Gaza; nayo ni jangwa. Naye akaondoka, akaenda; mara akamwona mtu wa Kushi, towashi, mwenye mamlaka chini ya Kandake malkia wa Kushi, aliyewekwa juu ya hazina yake yote; naye alikuwa amekwenda Yerusalemu kuabudu, akawa akirejea, ameketi garini mwake akisoma chuo cha nabii Isaya. Roho akamwambia Filipo, Sogea karibu na gari hili, ukashikamane nalo. Basi Filipo akaenda mbio, akamsikia anasoma chuo cha nabii Isaya; akanena, Je! Yamekuelea haya unayosoma? Akasema, Nitawezaje kuelewa, mtu asiponiongoza? Akamsihi Filipo apande na kuketi pamoja naye. Na fungu la Maandiko alilokuwa akilisoma ni hili, Aliongozwa kwenda machinjoni kama kondoo, na kama vile mwana-kondoo alivyo kimya mbele yake amkataye manyoya, vivyo hivyo yeye naye hafunui kinywa chake. Katika kujidhili kwake hukumu yake iliondolewa. Ni nani atakayeeleza kizazi chake? Kwa maana uzima wake umeondolewa katika nchi.

Yule towashi akamjibu Filipo, akasema, Nakuomba, nabii huyu asema maneno haya kwa habari ya nani; ni habari zake mwenyewe au za mtu mwingine? Filipo akafunua kinywa chake, naye, akakianza kwa andiko lilo hilo, akamhubiri habari njema za Yesu.

Wakawa wakiendelea njiani, wakafika mahali penye maji; yule towashi akasema, Tazama, maji haya; ni nini kinachonizuia nisibatizwe? Akaamuru lile gari lisimame; wakatelemka wote wawili majini, Filipo na yule towashi; naye akambatiza. Kisha, walipopanda kutoka majini, Roho wa Bwana akamnyakua Filipo, yule towashi asimwone tena; basi alikwenda zake akifurahi.

Lakini Filipo akaonekana katika Azoto, na alipokuwa akipita akahubiri Injili katika miji yote, hata akafika Kaisaria.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 66:8-9, 16-17, 20 (K) 1

(K) Mpigie Mungu kelele za shangwe, nchi yote.

Enyi mataifa, mtukuzeni Mungu wetu,
Itangazeni sauti ya sifa zake;
Aliyeiweka nafsi yetu katika uhai,
Wala hakuuacha mguu wetu usogezwe. (K)

Njoni sikieni, ninyi nyote mnaomcha Mungu,
Nami nitayatangaza aliyonitendea roho yangu.
Nalimwita kwa kinywa changu,
Na sifa kuu zilikuwa chini ya ulinzi wangu. (K)

Na ahimidiwe Mungu asiyeyakataa maombi yangu;
Wala kuniondolea fadhili zake. (K)



SHANGILIO
Yn. 20: 29

Aleluya, aleluya,
Wewe Toma, umesadiki kwa kuwa umeniona, wa heri wale wasioona, wakasadiki.
Aleluya.



INJILI
Yn. 6:44-51

Yesu aliwaambia Wayahudi: Hakuna mtu awezaye kuja kwangu, asipovutwa na Baba aliyenipeleka; nami nitamfufua siku ya mwisho. Imeandikwa katika manabii, Na wote watakuwa wamefundishwa na Mungu. Basi kila aliyesikia na kujifunza kwa Baba huja kwangu.

Si kwamba mtu amemwona Baba, ila yeye atokaye kwa Mungu; huyo ndiye aliyemwona Baba. Amin, amin, nawaambia, Yeye aaminiye yuna uzima wa milele.

Mimi ndimi chakula cha uzima. Baba zenu waliila mana jangwani; wakafa. Hiki ni chakula kishukacho kutoka mbinguni; mtu akila chakula hiki, ataishi milele. Na chakula nitakachotoa mimi ni mwili wangu, kwa ajili ya uzima wa ulimwengu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

JE, MATESO YANA KUVUNJA MOYO?




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Pasaka
Jumatano, Aprili 22 2026
Juma la 3 la Pasaka


Mdo 8:1-8;
Zab 66:1-7 (K. 1);
Yn 6:35-40.


JE, MATESO YANA KUVUNJA MOYO?


Kifo cha Stefano ni mwanzo wa mateso kwa jumuiya ya Kikristo. Lakini mbali na kujaribu kuupunguza ujasiri wa wanafunzi wa Yesu, kifo cha Stefano kinatia chachu na nguvu ya kuendelea kuhubiri. Kutawanyika kwa Wakristo kulikuwa na maana ya kuhubiri neno la Mungu sehemu mbali mbali na sio kukimbia kwa sababu ya hofu.

Injili ya leo inaendelea kufundisha jinsi gani Ekaristi itafanya kazi, ina maana gani, na kuna umuhimu gani kwa mpokeaji wa sakramenti kama anataka imsaidie. “hakuna hata mmoja atakaye kuja kwangu atakayeona njaa au kuona kiu” Yesu alisema. Lakini watu walikuwa na ugumu wakumuamini Yesu analalamika kwa upole “Ingawaje mmeniona hamtaki kuamini”. Sio kwamba walikuwa wamemuona tu bali walikuwa wameshaona mambo wakuu aliokuwa ametenda, kutembea juu ya maji, kuongeza mikate na samaki, kuwaponya wagonjwa na kufufua wafu. Lakini Yesu hakatishwi tamaa na mtu. Anawahakikishia; Yote alionipa Baba yatakuja kwangu, hakuna ambaye atakuja kwangu nimkatae. 

Maneno ya Yesu ni muhimu kwani yanatuhakikishia sisi kwamba ni wakuaminika. Ni kweli kwamba tunaweza kuja kwake na kumuamini yeye, kumkabidhi mioyo yetu, yeye atatutendea vyema, kutujali na kututunza. Yesu anauwezo wakutujali zaidi ya hata sisi tunavyojijali wenyewe. Tunapokumbwa na dhoruba tusikate tamaa na kuogopeshwa na majaribu tukashindwa kumwamini.

Mt. Rosemaría Escriva anasema, "dhoruba ya mateso ni nzuri. Ina hasara gani? Kwani jambo ambalo limekwisha kupotezwa haliwezi kupotezwa tena. Mti ukiwa na mizizi iliyojishika chini sana, hakuna upepo uwezao kuungoa mti wa Kanisa, labda tu matawi yake makavu yataanguka”. Basi leo tuangalie maisha yetu kama tu matawi mabichi yaliojishika na kanisa au makavu yategemeayo kuanguka kutoka mtini muda wowote kutokana na upepo!

Sala: Ee Bwana, Utusaidie kuishuhudia Injili na kukubali mateso yoyote yatokanayo na shughuli hiyo. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, APRILI 22 2026



MASOMO YA MISA, 
APRILI 22 2026
JUMA LA 3 LA PASAKA, JUMATANO

SOMO 1
Mdo 8:1-8

Siku ile kulitukia adha kuu ya kanisa lililokuwa katika Yerusalemu; wote wakatawanyika katika nchi ya Uyahudi na Samaria, isipokuwa hao mitume. 

Watu watauwa wakamzika Stefano, wakamfanyia maombolezo makuu. Sauli akaliharibu kanisa, akiingia kila nyumba, na kuwaburuta wanaume na wanawake na kuwatupa gerezani.

Lakini wale waliotawanyika wakaenda huko na huko wakilihubiri neno. Filipo akatelemka akaingia mji wa Samaria, akawahubiri Kristo. Na makutano kwa nia moja wakasikiliza maneno yale yaliyosemwa na Filipo walipoyasikia na kuziona ishara alizokuwa akizifanya. Kwa maana pepo wachafu wakawatoka wengi waliopagawa nao, wakilia kwa sauti kuu; na watu wengi waliopooza, na viwete wakaponywa. Ikawa furaha kubwa katika mji ule.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 66:1-7 (K) 1

(K) Mpigie Mungu kelele za shangwe, nchi yote.

Mpigie Mungu kelele za shangwe, nchi yote, 
Imbeni utukufu wa jina lake,
Tukuzeni sifa zake.
Mwambieni Mungu, Matendo yako yatisha kama nini. (K)

Nchi yote itakusujudia na kukuimbia, 
Naam, italiimbia jina lako.
Njoni yatazameni matendo ya Mungu;
Hutisha kwa mambo awatendayo wanadamu. (K)

Aligeuza bahari ikawa nchi kavu;
Katika mto walivuka kwa miguu;
Huko ndiko tulikomfurahia.
Atawala kwa uweza wake milele;
Macho yake yawaangalia mataifa;
Waasio wasijitukuze nafsi zao. (K)



SHANGILIO
Yn. 10:27

Aleluya, aleluya,
Kondoo wangu waisikia sauti yangu, nami nawajua, nao wanifuata.
Aleluya.



INJILI
Yn. 6:35-40

Yesu aliwaambia: Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe. Lakini naliwaambia ya kwamba mmeniona wala hamwamini. Wote anipao Baba watakuja kwangu; wala yeyote ajaye kwangu sitamtupa nje kamwe. Kwa kuwa mimi sikushuka kutoka mbinguni ili niyafanye mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenipeleka. Na mapenzi yake aliyenipeleka ni haya, ya kwamba katika wote alionipa nisimpoteze hata mmjoja, bali nimfufue siku ya mwisho. Kwa kuwa mapenzi yake Baba yangu ni haya, ya kwamba kila amtazamaye Mwana na kumwamini yeye, awe na uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo. 


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

YESU ANATOSHA KABISA



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Pasaka
Jumanne, Aprili 21, 2026
Juma la 3 la Pasaka

Mdo 7:51-8:1;
Zab 31:3-4,6-8,17,21 (K. 6);
Yn 6:30-35.


YESU ANATOSHA KABISA

Leo, Yesu anatumia njaa na kiu kutufundisha kwamba tunapaswa kuwa na njaa na kiu ya kiroho. Kuna njia moja tu ya kutuliza na kumaliza kiu hii… ni kwa njia yake tu. 

Mara nyingi tunapatwa na njaa na kiu. Tunakula na kunywa, lakini baada ya masaa kadhaa tunahisi tena njaa na kiu. Huu mzunguko hatuwezi kuukwepa. Miili yetu daima inadai chakula na kinywaji. Hii ni sawa pia katika maisha ya kiroho. Hatuwezi kusali mara moja na kusema basi inatosha na kumaliza kiu ya kiroho milele. Hatuwezi tu kusema namwamini Yesu mara moja na kubaki tu. Hii ni kwasababu sala na muunganiko na Yesu ni kitu ambacho kinapaswa kuchukua nafasi kila siku.

Ekaristi, “mkate wa uzima” unaridhisha kiu yetu na njaa yetu. Ekarisi ni zawadi ambayo tunapaswa kuitamani na kuipokea daima. Ukweli kwamba tunapaswa kuhudhuria misa na kupokea Ekaristi kila wakati ni ukweli kwamba maisha yetu ya Kikristo yanapaswa kufanywa mapya kila siku. 

Kumpenda Yesu na kumfuata yeye ni uamuzi ambao haupaswi tu kufanywa upaya kila siku, bali kufanywa upya kila wakati. Unapaswa kufanywa upya kama unavyo sikia njaa ya kimwili na kiu. Yesu ni mkate wa uzima wa Kiroho na kinywaji cha kweli cha kiroho. Yeye yupo kwa ajili yako. Muache yeye akamilishe hamu ya maisha. 

Sala: Bwana, ninakutamani wewe. Natamani umalize kiu yangu. Nisaidie nikugeukie wewe katika kila kitu. Nisaidie daima nitambue kuwa wewe ni yule ambaye namuhitaji na unatosha. Yesu, nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, APRILI 21, 2026



MASOMO YA MISA, APRILI 21, 2026
JUMA LA 3 LA PASAKA, JUMANNE

SOMO 1
Mdo. 7:51-8:1

Stefano aliwaambia Wakuu wa Makuhani: Enyi wenye shingo gumu, msiotahiriwa mioyo wala masikio, sikuzote mnampinga Roho Mtakatifu; kama baba zenu walivyofanya, na ninyi ni vivyo hivyo. Ni yupi katika manabii ambaye baba zenu hawakumwudhi? Nao waliwaua wale waliotabiri habari za kuja kwake yule Mwenye Haki; ambaye ninyi sasa mmekuwa wasaliti wake, mkamwua; ninyi mlioipokea torati agizo la malaika msiishike.

Basi waliposikia maneno haya, wakachomwa mioyo, wakamsagia meno.

Lakini yeye akijaa Roho Mtakatifu, akakaza macho yake, akitazama mbinguni, akauona utukufu wa Mungu, na Yesu akisimama upande wa mkono wa kuume wa Mungu. Akasema, Tazama, naona mbingu zimefunguka, na Mwana wa Adamu amesimama mkono wa kuume wa Mungu. Wakapiga kelele kwa sauti kuu, wakaziba masikio yao, wakamrukia kwa nia moja, wakamtoa nje ya mji, wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi wakaweka nguo zao miguuni pa kijana mmoja aliyeitwa Sauli. Wakampiga kw amawe Stefano, naye akiomba, akisema Bwana Yesu, pokea roho yangu. Akapiga magoti, akalia kwa sauti kuu, Bwana, usiwahesabie dhambi hii. Akiisha kusema haya akalala. Na Sauli alikuwa akiona vema kwa kuuawa kwake.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 31:2-3, 5, 7, 16, 20 (K) 5

(K) Mikononi mwako naiweka roho yangu, ee Bwana.

Uwe kwangu mwamba wa nguvu,
Nyumba yenye maboma ya kunionkoa.
Ndiwe genge langu na ngome yangu;
Kwa ajili ya jina lako uniongoze, unichunge. (K)

Mikononi mwako naiweka roho yangu; 
Umenikomboa, Ee Bwana, Mungu wa kweli.
Bali mimi namtumaini Bwana.
Na nishangilie, nizifurahie fadhili zako. (K)

Umwangaze mtumishi wako,
Kwa nuru ya uso wako;
Uniokoe kwa ajili ya fadhili zako.
Utawaficha katika hema
Na mashindano ya ndimi. (K)


SHANGILIO
Yn. 10:14

Aleluya, aleluya, 
Mimi ndimi mchungaji mwema,
nao walio wangu nawajua,
nao walio wangu wanijua mimi.
Aleluya.


INJILI
Yn. 6:30-35

Siku ile, Wayahudi walimwambia Yesu: Unafanya ishara gani basi, ili tuione tukakuamini? Unatenda kazi gani? Baba zetu waliila mana jangwani, kama vile ilivyoandikwa, Aliwapa chakula cha mbinguni ili wale.

Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Siye Musa aliyewapa chakula kile cha mbinguni, bali Baba yangu anawapa ninyi chakula cha kweli kitokacho mbinguni. Kwa maana chakula cha Mungu ni kile kishukacho kutoka mbinguni na kuupa ulimwengu uzima.
Basi wakamwambia, Bwana, sikuzote utupe chakula hiki. Yesu akawaambia, Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo 


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUKUTANA NA MCHUNGAJI MWEMA ANAYETAKATISHA ROHO ZETU




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Pasaka
JUMATATU, JUMA LA 3 LA PASAKA
Aprili 20, 2026

KUKUTANA NA MCHUNGAJI MWEMA ANAYETAKATISHA ROHO ZETU

Shangwe za Pasaka zinaendelea kutupa msingi hasa tunapo ingia katika juma la tatu la Pasaka. Mchungaji mwema amefufuka. Yeye ambaye alitoa maisha yake kwa ajili ya kondoo wake, amefufuka. Yeye ambaye anatupenda na kulinda kundi lake hakuweza kufungwa na kifo. Kilicho cha muhimu anaendelea kuwa mchungaji wetu mwema.

Shemasi Stefano alifanya kazi muhimu sana katika kanisa la mwanzo. Maisha yake ya kujitoa kabisa kwa Yesu, utayari wake wa kufa kwa ajili yake, Stefano anakuwa mfano kwa Wafiadini wote waliokuja baadae, na hata kwa wakristo wote wa nyakati zote. Leo tutasikia yupo katika kujaribiwa na kesho tutasikia kuuwawa kwake. “Wana heri ambao maisha yao hayana hatia”.

Mafundisho ya Yesu leo ni muhimu sana katika kuelewa kwetu juu ya asili ya Ekaristi na jinsi anavyotaka sisi tuijongee. Kundi lile ambalo lililishwa kwa mikate na samaki wawili sasa wapo katika kumtafuta. Kumtafuta Yesu ni muhimu sana, lakini cha muhimu yule mtafutaji lazima atambue nia yake mathubuti. Yesu anawambia, “hakika nawaambia hamnitafuti mimi kwasababu mliona miujiza, lakini kwasababu mlikula mikate na kushiba”.

Kumtafuta huku hakukuwa kwasababu ya upendo kwake, bali kufaidika naye. Sisi mara nyingi tunamtafuta Yesu kwa faida zetu, pengine kwasababu ya gari, nyumba, mchumba mwema, kuponywa kutoka katika magonjwa. Yesu aliwaonya watu wasitafute vitu viharibikavyo bali vya milele (Yesu mwenyewe). Tatizo ni hili sisi kama lile kundi, hatumtafuti Yesu zaidi ya chakula na mahitaji ya kimwili, hatumtambui kwamba yeye anafanya mioyo yetu safi kwa chakula cha milele anachotupa.

Yesu anaendelea kuwa mchungaji wetu mwema sasa. Anafanya hivi kwakutufundisha ni kitu gani tunachohitaji hasa kwa ajili ya maisha yetu, ambacho ni Ekaristi. Ni sakramenti kubwa kuliko zote, ambayo tunapaswa kuwa tumejiandaa, ili tuweze kukutana na Yesu mfufuka.

Sala: Mungu Baba yetu mwanga wako wa ukweli unatuangaza kwenye njia za Yesu Kristo. Bwana tunakuomba utuimarishe kwa sakramenti hii ya Ekaristi, ili tuweze kupata Amani, upendo, na kumjali Yesu Mchungaji wetu mwema.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, APRILI 20 2026





MASOMO YA MISA, APRILI 20  2026
JUMA LA 3 LA PASAKA, JUMATATU


SOMO 1
Mdo. 6:8-15

Stefano, akijaa neema na uwezo, alikuwa akifanya maajabu na ishara kubwa katika watu. Lakini baadhi ya watu wa sinagogi lililoitwa sinagogi la Mahuru, na la Wakirene, na la Waiskanderia, na la wale wa Kilikia na Asia, wakaondoka na kujadiliana na Stefano; lakini hawakuweza kushindana na hiyo hekima na huyo Roho aliyesema naye. Hata wakashawishi watu waliosema, tumemsikia mtu huyu akinena maneno ya kumtukana Musa na Mungu.

Wakawataharakisha watu na wazee na waandishi; wakamwendea, wakamkamata, wakampeleka mbele ya baraza. Wakasimamisha mashahidi wa uongo waliosema, Mtu huyu haachi kusema maneno ya kufuru juu ya mahali hapa patakatifu na juu ya torati; maana tumemsikia akisema kwamba Yesu huyo Mnazareti atapaharibu mahli hapa, na kuzibadili desturi tulizopewa na Musa.

Watu wote walioketi katika ile baraza wakamkazia macho yao, wakamwona uso wake kuwa kama uso wa malaika.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 119: 23-24, 26-27, 29-30 (K)

(K) Heri walio kamili njia zao.

Wakuu nao waliketi wakaninena,
Lakini mtumishi wako atazitafakari amri zako.
Shuhuda zako ndizo furaha yangu,
Na washauri wangu. (K)

Nalizisimulia njia zangu ukanijibu,
Unifundisha amri zako.
Unifahamishe njia ya mausia yako,
Nami nitayatafakari maajabu yako. (K)

Uniondolee njia ya uongo,
Unineemesha kwa sheria yako.
Nimeichagua njia ya uaminifu,
Na kuziweka hukumu zako mbele yangu. (K)


SHANGILIO
Lk. 24:25-26

Aleluya, aleluya,
Ilimpasa Kristu kupata mateso haya, na kuingia katika utukufu wake.
Aleluya.

INJILI
Yn. 6:22-29

Siku ya pili yake mkutano waliosimama ng’ambo ya bahari waliona ya kuwa hakuna mashua nyingine huko ila moja; tena ya kuwa Yesu hakuingia katika mashua ile pamoja na wanafunzi wake, bali wanafunzi wake walikwenda peke yao. Walakini zikaja mashua nyingine kutoka Tiberia mpaka karibu na mahali pale walipokula mikate, wakati Bwana aliposhukuru. Basi mkutano, walipoona ya kuwa Yesu hayuko huko wala wanafunzi wake, waliingia mashuani wenyewe, wakaenda Kapernaumu wakimtafuta Yesu. Hata walipomwona ng’ambo ya bahari, walimwambia, Rabi, wewe umekuja lini hapa?

Yesu akawajibu, akasema, Amin, amin, nawaambieni, Ninyi mnanitafuta, si kwa sababu mliona ishara, bali kwa sababu mlikula ile mikate mkashiba. Msikitendee kazi chakula chenye kuharibika, bali chakula kidumucho hata uzima wa milele; ambacho Mwana wa Adamu atawapa, kwa sababu huyo ndiye aliyetiwa muhuri na Baba, yaani, Mungu. Basi wakamwambia, Tufanyeje ili tupate kuzitenda kazi za Mungu? Yesu akajibu, akawaambia, Hii ndiyo kazi ya Mungu, mmwamini yeye aliyetumwa na yeye.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com