Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

NINANI MKUBWA KATIKA UFALME WA MUNGU?




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumanne, Agosti 11, 2026,
Tafakari ya kila siku 
Juma la 19 la Mwaka  wa Kanisa

Ez 2:8 -3:4; 
Zab 119:14, 24, 72, 103, 111, 131; 
Mt 18: 1-5, 10, 12-14


NINANI MKUBWA KATIKA UFALME WA MUNGU?


Kuna video katika mitandao inayohusu Matt Woodrum, ambayo inabeba jina la “Kijana mlemavu awavutia wengi nyakati za mwisho”. Huyu kijana Matt ilikuwa vigumu kwake kutembea, lakini alishiriki katika mashindano ya kukimbia (katika mzunguko wa duara). Wakati mashindano yalipoanza wakimbiaji wote walimpita nakukimbia nakumaliza. Wakati akiwa nusu ya mzunguko wale wakimbiaji wengine walishamaliza mzunguko mwingine nakumpita. Na wakati hajamaliza mzunguko wa kwanza wote wakamaliza mizunguko yote. Lakini Matt hakuacha kuendelea kuzunguka, hata yule kiongozi wake alivyomwambia aache yeye hakuacha. Alisema anataka kumaliza. Hakujali ni sehemu ghani yeye alitaka kumaliza. Watu kwakuona moyo wake, wakamzunguka na kuanza kumpigia makofi nakusema “songa mbele, songa mbele Matt” Matt aliwafundisha wote somo. “Kushinda haimaanishi kumaliza kwa mwendo uliopangwa”

Katika somo la Injili tunaona wafuasi wa Yesu wakimuuliza; ‘ni nani aliyemkubwa katika Ufalme wa mbinguni?’ Matt, anatupa jibu, yule mdogo, mnyonge, anayeonewa, aliyekama mtoto, asiyejiweza………Wale waliojawa na elimu ya juu kabisa, matajiri na wenye mamlaka, wakialikwa kwenye sherehe kwanza wanaangalia ni nani atakuwepo ili kusimamia shughuli zake? Pia nitakuwa katika sehemu ghani kati ya waalikwa? Je nitapewa heshima ghani? Wakati kama mtoto, au mlemavu angealikwa kwa sherehe hiyo, angejisikia mwenye bahati sana kualikwa kwenye sherehe kama hiyo. Wanatambua kwakweli hawastahili kwa mwaliko huo, lakini wamealikwa na Bwana wa sherehe.

Wafuasi nao wameanguka kwenye mtego wakudhani kwamba wanastahili kwenye Ufalme wa Mungu. Kwamba ni haki yao kuwa pale, na kuwa katika nafasi ya juu kabisa. Wakati watoto hawajui hata kama watashiriki katika Ufalme huo. Wafuasi walikosa unyenyekevu, walipoteza maana ya maisha yao nakujisahau wao ni nani. Je, mimi na wewe tupo je? Je, unafikiri una haki ya kuwa katika Ufalme wa Mbinguni? Je, unasubiria sehemu ya juu kwasababu ya utume unaofanya kwaajili ya Mungu? Kama unataka kuingia katika Ufalme wa Mungu, kuwa na moyo mnyofu kama wa watoto. Tunapaswa kuwa na moyo mnyofu uliojaa unyenyekevu ili tuyapokee vyema mapenzi ya Mungu, kwa namna hii bila hata mastahili yetu, twajuaje kama Mungu hatatukaribisha kwake? Daima tuombee neema hiyo.

Sala: Bwana, fanya moyo wangu uwe mnyenyekevu na mnyoofu kama wako. Amina.



Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, AGOSTI 11, 2026





MASOMO YA MISA, AGOSTI 11, 2026
JUMANNE, JUMA LA 19 LA MWAKA

KUMBUKUMBU YA MTAKATIFU KLARA

SOMO 1
Eze. 2:8 – 3:4

Ezekieli aliisikia sauti, ikamwambia: Mwanadamu, sikia neno hili ninalokuambia; usiwe wewe mwenye kuasi kama nyumba ile yenye kuasi; funua kinywa chako, ule nikupacho. Nami nilipotazama, mkono ulinyoshwa kunielekea; na tazama, gombo la chuo lilikuwa ndani yake. Akalikunjua mbele yangu; nalo lilikuwa limeandikwa ndani na nje; ndani yake yalikuwa yameandikwa maombolezo, na vilio, na ole!

Akaniambia, Mwanadamu, kula uonacho; kula gombo hili, kisha enenda ukaseme na wana wa Israeli. Basi nikafunua kinywa changu, naye akanilisha lile gombo. Akaniambia, Mwanadamu, lisha tumbo lako, ulijaze tumbo lako kwa hili gombo nikupalo. Ndipo nikalila, nalo kinywani mwangu lilikuwa tamu, kama utamu wa asali.

Akaniambia, Mwanadamu, haya! Waendee wana wa Israeli, ukawaambie maneno yangu.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 119:14, 24, 72, 103, 111, 131 (K) 103

(K) Mausi yako ni matamu sana kwangu.

Nimeifurahia njia ya shuhuda zako,
Kana kwamba ni mali mengi.
Shuhuda zako nazo ndizo furaha yangu,
Na washauri wangu. (K)

Sheria ya kinywa chako ni njema kwangu,
Kuliko maelfu ya dhahabu na fedha.
Mausia yako ni matamu sana kwangu,
Kupita asali kinywani mwangu. (K)

Shuhuda zako nimezifanya urithi wa milele,
Maana ndizo changamko la moyo wangu.
Nalifunua kinywa changu nikakweta,
Maana naliyatamani maagizo yako. (K)



SHANGILIO
Yn. 17:17

Aleluya, aleluya,
Neno lako ndiyo kweli, Ee Bwana, ututakase kwa ile kweli. 
Aleluya.



INJILI
Mt. 18:1 – 5, 10 , 12, 14

Wanafunzi walimwendea Yesu wakisema, Ni nani basi aliye mkuu katika ufalme wa mbinguni? Akaita mtoto mmoja, akamweka katikati yao, akasema, Amin, nawaambia, Msipoongoka na kuwa kama vitoto, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni.

Basi, yeyote ajinyenyekeshaye mwenyewe kama mtoto huyu, huyo ndiye aliye mkuu katika ufalme wa mbinguni.

Na yeyote atakayempokea mtoto mmoja mfano wa huyu kwa jina langu, anipokea mimi.

Angalieni msidharau mmojawapo wadogo hawa; kwa maana nawaambia ya kwamba malaika zao mbinguni sikuzote huutazama uso wa Baba yangu aliye mbinguni.

Mwaonaje? Mtu akiwa na kondoo mia, mmoja akampotea, je! Hawaachi wale tisa na tisini, akaenda milimani, na kumtafuta yule aliyepotea? Vivyo hivyo haipendezwi mbele za Baba yenu aliye mbinguni kwamba mmoja wa wadogo hawa apotee.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MBEGU YA IMANI!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatatu, Agosti 10, 2026 
Juma la 19 la Mwaka wa Kanisa

Sikukuu ya Mt. Laurent, Shemasi na shahidi.

2 Kor 9: 6-10;
Zab 112: 1-2, 5-9 (K) 5;
Yn 12: 24-26.

MBEGU YA IMANI!

Yesu Kristo leo anafundisha kwa kutumia mfano wa mbegu ambao tutaelewa kwa haraka zaidi. Kwakuwa ili mbegu iweze kumea ni lazima ibadilike kutoka kwenye hali yake ya mwanzo, ipokee hewa, maji, mwanga na mazingira ambayo itairuhusu kukuwa. Kama itajiruhusu yenyewe kubadilika, hapo tutaona mizizi ikichomoza, baadae majani, alafu matawi, na baadae kuwa mti nakutoa matunda au mbegu zinazofanana na mbegu ya mwanzo iliyokufa. 

Katika historia ya Ukristo, tunaambiwa ni kwasababu ya damu ya mashahidi. Kanisa la mwanzo limekuwa na kumea katika hali hii hii kwa miaka elfu mbili iliyopita. Kwakifupi, “damu ya Mashahidi ni mbegu ya Kanisa.” Wafiadini (Mashahidi) ni wale waliouwawa kwasababu ya imani yao, na hiyo ilikuwa ni kulinda Imani yao ndani ya Yesu Kristo. Wote waliomwaga damu yao kama Mt. Laurent, wamekuwa kama mbegu iliokufa nakutoa matunda. Mashahidi walikufa wakijitahidi kutetea Imani yao ndani ya Bwana wetu Yesu Kristo, na kwa njia ya vifo vyao, watu wengi wamekuja kumuamini Kristo. Leo, Yesu anatualika kujitolea maisha yetu ili kuungama Imani yetu ndani ya Kristo. Tunapaswa kuzuia yote yasio katika mpango wa Mungu, ili tuzae matunda mema na tuweze kupokea uzima wa milele na kuwa naye daima.

Sala: Bwana, nakuomba niwe mbegu ya Imani. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, AGOSTI 10, 2026



MASOMO YA MISA, AGOSTI 10, 2026
JUMATATU , JUMA LA 19 LA MWAKA 

SIKUKUU YA MT. LAURENT

SOMO 1 
2Kor 9:6-10

Apandaye haba atavuna haba; apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu. Kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu. Na Mungu aweza kuwajaza kila neema kwa wingi, ili ninyi, mkiwa na riziki za kila namna sikuzote, mpate kuzidi sana katika kila tendo jema; kama ilivyoandikwa, Ametapanya, amewapa maskini, Haki yake yakaa milele.

Na yeye ampaye mbegu mwenye kupanda, na mkate uwe chakula, atawapa mbegu za kupanda na kuzizidisha, naye atavaongeza mazao ya haki yenu.

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 112: 1-2, 4, 9  (K) 5 

(K) Heri atendaye fadhali na kukopesha.

Heri mtu yule amchaye Bwana,
Apendezwaye sana na maagizo yake.
Wazao wake watakuwa hodari duniani;
Kizazi cha wenye adili kitabarikiwa. (K)

Nuru huwazukia wenye adili gizani;
Ana fadhili na huruma na haki. (K)

Amekirimu, na kuwapa maskini,
Haki yake yakaa milele,
Pembe yake itatukuzwa kwa utukufu. (K)


SHANGILIO
Yn 8: 12

Aleluya, aleluya,
Yeye anifuataye, asema Bwana, hatakwenda gizani kamwe, bali atakuwa na nuru ya uzima.
Aleluya.


INJILI 
Yn 12: 24-26

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi. Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele. Mtu akinitumikia, na anifuate; nami nilipo, ndipo na mtumishi wangu atakapokuwapo. Tena mtu akinitumikia, Baba atamheshimu.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

USIOGOPE




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumapili, Agosti 9 2026
Juma la 19 la Mwaka

1 Fal. 19:9, 11-13
Zab. 85 :8-13, (K)7
Rum 9: 1-5
Mt 14:22-33


USIOGOPE

Upo msemo usemao “bahari shwari haitoi wanamaji stadi.” Bahari yenye mawimbi mazito huwaimarisha wanamaji wake. Matatizo kama mawimbi yanaweza kukuimarisha. Tuwe tayari kuyapokea mawimbi yanayojitokeza ndani ya maisha yetu. Kuwa na mtazamo hasi dhidi ya matatizo ni kama kupambana na ukuta. “Wavuvi wanajua kuwa bahari ni hatari na ina dhoruba za kuogopesha, lakini hawajawahi kuona hatari hizi kama sababu tosha za kubaki kandokando ya bahari au ufukweni,” alisema Vincent van Goth. Wavuvi hujitosa kwenye maji marefu. Wavuvi ni mfano wa kuigwa tunapokumbana na mawimbi ya matatizo katika bahari ya maisha. Kuna mtu aliyemwambia mvuvi hivi: “wewe hauogopi kwenda baharini kuvua samaki? Mjomba wako, kaka yako na babu yako wote walikufa maji, kwa nini hauogopi?” Mvuvi alijibu hivi: “watu wengi hufa wakiwa vitandani lakini watu hawaachi kulala vitandani.” “Kuna mambo ambayo unajifunza vizuri sana wakati kuna utulivu na mengine wakati kuna dhoruba,” alisema Willa Cather

Kwa Yesu si kila mara mawingu yalibaki bluu. Kuna wakati wingu lilikuwa jeusi likiashiria dhoruba na matatizo. Alikataliwa na wasamaria katika kijiji cha Wasamaria (Lk 9:51-56). Pia kwa Ayubu mawingu hayakuwa kila mara ya bluu. Katikati ya mawimbi ya matatizo, Ayubu alizidi kuimarika. Ni kama jani la chai linapata nguvu ya kugeuza rangi ya maji likiwa kwenye maji moto. Ukiwa kwenye mawimbi ya matatizo kumbuka ukweli huu: Kwanza, tuko salama kwenye mawimbi ya matatizo tukiwa na Mungu kuliko tukiwa pasipokuwa na mawimbi ya matatizo bila Mungu. Mungu anaweza kutuliza mawimbi au akayaacha mawimbi akamtuliza binadamu. Pili, maisha bila mawimbi ya matatizo hufanya uwezekano wa mazuri kuwa sifuri. Tatu, tukumbuke kwamba joto likizidi, kutanuka kunazidi-matatizo makubwa yanaweza kukufanya uwe mkubwa. Kuna methali isemayo: “anayesema sijawahi kuliona jambo hili, si mkubwa kiumri.” Nne, ukiomba mvua inyeshe-kuwa tayari kukanyaga matope. Tano, tambua kwamba mawimbi ya matatizo yanakujia ili kukuimarisha na si kukudhoofisha.


“Ewe mwenye imani haba mbona uliona shaka” (Mathayo 14:31) Maisha ni kigeugeu. Mambo yalimgeuka mtume Petro. Petro alikuwa mtu wa kufanya maamuzi kwa ghafla na haraka. Hakufikiri sana kabla ya kutenda. Jambo hili pengine ni busara likilinganishwa na mtu ambaye anafikiri sana mwishowe hatendi lolote. Katika nafsi ya Petro, kuna mchanganyiko wa mambo. Anatamani kuwa na Yesu. Pia anatamani kuonesha kuwa anaweza kutenda analolitenda Yesu: kutembea juu ya maji. Kuna upendo na majivuno kama ilivyo kwa kila mmoja wetu. Petro ana ujasiri na woga. Anaanza vizuri, anaona dhoruba na kuogopa. Anakosa imani.

Sababu kubwa ya kupotea kwa imani ya Petro ni kwa kuwa macho yake, mawazo yake na moyo wake alivielekeza kwenye dhoruba badala ya Kristu. Alipomtazama Yesu Kristu, imani ilipatikana akalia kwa sauti, “ Bwana, niokoe!” (Mt 14; 30). Licha ya Petro kuwa na imani haba, Yesu alimuokoa. “Hapo, Yesu akanyosha mkono wake, akamshika … wakapanda mashuani, na upepo ukakoma” (Mt 14: 31-32). Nasi tunapambana na matatizo. Matatizo ya siku hizi ni kama: umasikini, makazi duni, ukosefu wa kazi, magonjwa yasiyo na tiba, ukosefu wa riziki, uzinifu, uzazi kwa namna isiyo halali, ukatili na vita, ukabila- damu inakuwa nzito kuliko maji ya ubatizo. Tumwombe Yesu atuokoe.

Katika kilele cha dhoruba, Yesu alijitokeza. Katika kilele cha hatari, katika upeo wa wasiwasi, Yesu alijitokeza. Anakuja wakati ambapo hategemewi kabisa. Mitume walifikiri ni mzuka wakauotea mbali. Yesu ni Mkombozi tunayeweza kumkimbilia. Alifanya kile ambacho binadamu hawezi kufanya. Alitembea juu ya maji. Vile ambavyo hatuwezi kufanya tumuachie yeye. Wakati tunapozama kwenye bahari ya matatizo, tulie kwa sauti: “Bwana utuokoe !” Shibisha imani yako na mashaka yako. Imani ikiongezeka, mashaka yanapungua na kinyume chake ni kweli. “Imani si kujaribu kuamini jambo bila ya kuzingatia ushahidi: imani ni kujaribu kufanya jambo bila kuzingatia matokeo,” alisema Sherwood Eddy. “Wanashinda wale wanaoamini wanaweza,” alisema Virgil. Ni katika mtazamo huo Erasmus alisema, “Amini kuwa unacho na unakuwa nacho.” Swali kubwa hapa si kuwa una imani au hauna imani. Jambo la msingi ni imani katika nini na imani katika nani. Ili kufanikiwa na kushinda, unahitaji kuwa na imani katika Mungu na kujiamini hata ikiwa imani ndogo au haba inatosha kukuondolea vikwazo, vihunzi na vizingiti. Tunasoma hivi katika Biblia, mitume wakamwambia Bwana, Tuongezee imani. Bwana akasema, Kama mngekuwa na imani kiasi cha chembe ya haradali, mngeuambia mkuyu huu, Ng’oka, ukapandwe baharini, nao ungewatii” (Luka 17: 5-6).

Kifungu cha Biblia hicho kinabainisha ukweli huu, imani kidogo yaweza kufanya mambo makubwa. Ni ukweli unaoendana na ujumbe wa methali ya Kiswahili, “Kidogo kidogo kamba ukatika.” Nguvu ya mbegu haitegemei ukubwa au udogo wake inategemea uhai uliofichwa katika mbegu hiyo. Kuna nguvu ambayo imefichwa ndani mwako. Kama ni hivyo unahitaji kujiamini kuwa utaweza kufanikiwa katika maisha. Kwa imani na kujiamini ndege imevumbuliwa. Kwa imani na kujiamini, simu za mkononi zimegunduliwa. Kwa imani na kujiamini utalaamu wa kutengeneza runinga umefunuliwa.

Mitume walipoomba kuongezewa imani, Yesu hakusema nimewaongezea imani. Hakuahidi kuwaongezea imani. Ni kama aliwaambia anza na mlicho nacho, kidogo huvuta kikubwa, kidogo huzaa kikubwa, laini huzaa ngumu. Walikuwa kama mfanyabiashara asemaye nina pesa kidogo sana ngoja iwe nyingi ndipo nianze kufanya biashara. Je, itaongezekaje bila kuzalisha, kuuza na kununua? Walikuwa kama mkulima asemaye ‘nina mbegu lakini hazitoshi nitalima nikiwa na mbegu za kutosha.’ Anza na ulicho nacho. Hawezi kusema sina pesa yote ya kujenga na kumalizia nyumba. Anza kujenga na pesa uliyo nayo. Ili kuwa na zaidi, anza na ulicho nacho. Aliyenacho ataongezewa-ndivyo Bwana Yesu alivyofundisha.

Imani ni ufunguo wa mafanikio. Na sifa ya mtu anayefanikiwa ni kuwa ana imani. Imani kamili ndiyo kumtegemea Mungu na kumtumaini na kumtii. Tukiwa na imani kwa Mungu twaweza kusema, “Bwana ndiye anisaidiaye, sitaogopa” (Waebrania 13:6). Hatuna budi kuwa na imani na uwezo Mungu aliotujalia yaani kujiamini. Kuna hadithi juu ya wakristu ambao walimuomba mchungaji wakati wa ibada ya Jumapili iliyokuwa inafuata waombe kupata mvua baada ya mvua kutonyesha kwa kipindi cha muda mrefu. Walishangaa siku hiyo ya maombi ya Jumapili mchungaji aliposema hayuko tayari kuomba kupata mvua maana watu hawaonyeshi imani kwa vile hawakwenda na miavuli ya kujikinga mvua. Imani lazima ionekane katika matendo. Mungu anasaidia na wewe unaweka juhudi na maarifa. Henry Ford alisema, “Kama unaamini unaweza kufanya jambo fulani au hauamini kama unaweza kufanya jambo fulani, uko sawa.” Usipoamini kwamba jambo fulani linaweza kufanyika, halitafanyika. Ukiamini, litafanyika. Imani inafukuza mashaka kama mwanga ufukuzavyo giza. Mashaka yakibisha hodi mlangoni mwako, itume imani-ijibu mashaka. Sala yetu iwe kama ya kijana mmoja kwenye Biblia, “Naamini, nisaidie kutokuamini kwangu” (Marko 9: 24).

Dunia ni bahari yenye mawimbi-inahitaji wanamaji stadi. Duniani kuna mengi sawasawa na bahari. Kuna papa na nyangumi tena wale wa hatari. Lakini ukweli unabaki: Bahari shwari haitoi wana maji stadi. Bahari iliyotulia haiwezi kuwatoa wanamaji hodari. Kuna methali ya Kiswahili isemayo: Bahari haishi zinge. Zinge ni machafuko ya mara kwa mara (mabadiliko ya ghafla). Bahari daima imo katika mabadiliko wala haitabiriki. Maisha kama vile bahari yamejawa na mema na maovu na yanapotujia sharti tuwe tayari kuyakabili. Tukabili mawimbi kwa utulivu bila hofu. Tukabili mawimbi ya mawazo mabaya, mahusiano mabaya na kushindwa.

Sala: Ee Bwana ninakuomba unipe imani niweze kupambana na dhoruba za maisha nikitambua kwamba hakuna mawimbi yasiyokuwa na Mwisho. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUMAPILI, AGOSTI 9, 2026



MASOMO YA MISA, JUMAPILI, AGOSTI 9, 2026
JUMA LA 19 LA MWAKA 


SOMO 1
1 Fal. 19:9, 11-13

Eliya alifika kunako pango, akalala ndani yake. Na tazama, neno la Bwana likamjia. Akasema, Toka, usimame mlimani mbele za Bwana. Na tazama, Bwana akapita; upepo mwingi wa nguvu ukaipasua milima, ukaivunjavunja miamba mbele za Bwana; lakini Bwana hakuwamo katika upepo ule; na baada ya upepo, tetemeko la nchi; lakini Bwana hakuwamo katika lile tetemeko la nchi: na baada ya tetemeko la nchi kukawa na moto; lakini Bwana hakuwamo katika moto ule; na baada ya moto sauti ndogo, ya utulivu. Ikawa, Eliya alipoisikia, alijifunika uso wake katika mavazi vake, akatoka, akasimama mlangoni mwa pango.

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 85 :8-13, (K)7

(K) Ee Bwana, utuonyeshe rehema zako, Utupe wokovu wako.

Nisikie atakavyosema Mungu Bwana,
Maana atawambia watu wake amani.
Hakika wokovu wake u karibu na wamchao,
Utukufu ukae katika nchi yetu. (K)

Fadhili na kweli zimekutana,
Haki na amani zimebusiana.
Kweli imechipuka katika nchi,
Haki imechungulia kutoka mbinguni. (K)

Naam, Bwana atatoa kilicho chema,
Na nchi yetu itatoa mazao yake.
Haki itakwenda mbelc zake,
Nayo itazifanya hatua zake kuwa njia. (K)


SOMO 2 
Rum 9: 1-5

Nasema kweli katika Kristo, sisemi uongo, dhamiri yangu ikinishuhudia katika Roho Mtakatifu, ya
kwamba nina huzuni nyingi  na maumivu yasiyokoma moyoni mwangu. Kwa maana ningeweza kuomba mimi mwenyewe niharimishwe na kutengwa na Kristo kwa ajili ya ndugu zangu, jamaa zangu kwa jinsi ya mwili; ambao ni Waisraeli, wenye kule kufanywa wana, na ule utukufu, na maagano, na kupewa torati, na ibada ya Mungu, na ahadi zake; ambao mababu ni wao, na katika hao alitoka Kristo kwa jinsi ya mwili. Ndiye aliye juu ya mambo yote, Mungu, mwenye kuhimidiwa milele. Amina.

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu 


SHANGILIO 
Lk. 19:38

Aleluya, aleluya, 
Abarikiwe Mfalme ajaye kwa jina la Bwana;
Aleluya.


INJILI 
Ml 14:22-33

Yesu aliwalazimisha wanafunzi wake wapande chomboni na kutangulia mbele yake kwenda ng'ambe. wakati yeye alipokuwa akiwaaga makutano. Nave alipokwisha kuwaaga makutano, alipanda mlimani faraghani, kwenda kuomba. Na kulipokuwa jioni, alikuwako huko peke yake. Na kile chombo kimekwisha kufika katikati ya bahari, kinataabika sana na mawimbi; maana upepo ulikuwa wa mbisho. Hata wakati wa zamu ya nne ya usiku Yesu akawaendea. akienda kwa miguu juu ya bahari. Wanafunzi walipomwona akienda juu ya bahari, wakafadhaika, wakisema, Ni kivuli, wakapiga yowe kwa hofu. Mara Yesu akanena, akawaambia, Jipeni movo; ni mimi; msiogope. Petro akamjibu, akasema, Bwana, ikiwa ni wewe, niamuru nije kwako juu ya maji. Akasema, Njoo. Petro akashuka chomboni, akaenda kwa miguu juu ya maji, ili kumwendea Yesu. Lakini alipouona upepo, akaogopa; akaanza kuzama, akapiga yowe akisema, Bwana, niokoe. Mara Yesu akanyosha mkono wake, akamshika, akamwambia, Ewe mwenye imani haba, mbona uliona shaka? Nao walipopanda chomboni, upepo ulikoma. Nao waliokuwamo ndani ya chombo wakamsujudia wakisema, Hakika wewe ni Mwana wa Mungu.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

IMANI KUBWA!

 

“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumamosi, Agosti 8 2026
Juma la 18 la Mwaka
 
Hab. 1: 12 - 2: 4;
Zab. 9 : 7-12 (K) 10;
Mt 17: 14-20.
 
 
IMANI KUBWA!

 

Katika Injili ya leo, baada ya wanafunzi wa Yesu kurudi katika utume wao, walishangaa kwanini hawakuweza kumponya kijana aliyekuwa ana pepo mchafu. “kasababu ya Imani yenu ndogo” Yesu aliwaambia. Mngekua na Imani ndogo kama chembe ya haradani” aliwaambia, “hakuna chochote ambacho kingeshindikana kwenu”.Mwaliko huu wa Yesu sio kiingiilio cha kumpa rushwa Mungu atafanyie maajabu, bali ni mwito wa kuweka matumaini yetu yote kwake kwa chochote kitokeacho kwetu, yeye tayari ajua lipi bora kwetu kulingana na mapenzi yake.Imani hii ikiwa ndani ya upendo mkuu, ndio iletayo furaha na amani katika maisha yetu, hata katika kipindi kigumu cha maisha yake.

 

Sala: Ee Bwana, Nakutumainia wewe. Amina.

 

------------------------

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, FurahayaKikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

 

MASOMO YA MISA, JUMAMOSI, AGOSTI 8, 2026





MASOMO YA MISA, JUMAMOSI, AGOSTI 8, 2026
JUMA LA 18 LA MWAKA

SOMO 1
Hab. 1: 12 - 2: 4

Ee Bwana, Mungu wangu, mtakatifu wangu, wewe si wa milele? hatutakufa. Ee Bwana, umemwandikia hukumu, nawe, Ee Jabali, umemweka imara ili aadhibishwe.

Wewe uliye na macho safi hata usiweze kuangalia uovu. wewe usiyeweza kutazama ukaidi, mbona unawaangalia watendao kwa hila; na kunyamaza kimya. hapo mtu mwovu ammezapo mtu aliye mwenye haki kuliko yeye; na kufanva wanadamu kuwa kama samaki wa baharini, kama vitu vitambaavyo. ambavyo havina mtawala?

Yeye huwatoa wote kwa ndoana yake, huwakamata katika wavu wake, na kuwakusanya katika
juya lake: ndiyo sababu afurahi na kupendezwa. 

Kwa sababu hiyo huutolea wavu wake sadaka, na kulifukizia uvumba juya lake; kwa sababu kwa vitu vile fungu lake limenona, na chakula chake kimekuwa tele.

Je! atawatoa walio katika wavu wake, asiache kuwaua watu wa mataifa daima? Mimi nitasimama katika zamu yangu, nitajiweka juu ya mnara. nitaangalia ili nione atakaloniambia, na jinsi nitakavyojibu katika habari ya kulalamika kwangu. Bwana akanijibu, akasema, Iandike njozi ukaifanye iwe wazi sana katika vibao, ili aisomave apate kuisoma kama maji. Maana njozi hii bado ni kwa wakati ulioamriwa, inafanya haraka ili kuufikilia mwisho wake, wala haitasema uongo; ijapokawia. ingojee: kwa kuwa haina budi kuja, haitakawia. Tazama. roho yake hujivuna, haina unyofu ndani yake; lakini mwenye haki ataishi kwa imani yake.

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 9 : 7-12 (K) 10

(K) Wewe Bwana, hukuwaacha wakutafutao.

Bwana atakaa milele,
Ameweka kiti chake tayari kwa hukumu.
Nave atauhukumu ulimwengu kwa haki;
Atawaamua watu kwa adili. (K)

Bwana atakuwa ngome kwake aliyeonewa,
Naam, ngome kwa nyakati ya shida.
Nao wakujuao jina lako wakutumaini Wewe,
Maana Wewe, Bwana, hukuwaacha wakutafutao. (K)

Mwimbieni Bwana akaaye Sayuni,
Yatangazeni kati ya watu matendo yake.
Maana mlipiza kisasi cha damu awakumbuka,
Hakukisahau kilio cha wanyonge. (K)


SHANGILIO 
Yn. 10: 27

Aleluya, aleluya,
Kondoo wangu waisikia sauti yangu, nami nawajua, nao wanifuata.
Aleluya.



INJILI

Mt. 17: 14-20

 

Mtu mmoja alimjia Yesu, akampigia magoti, akisema, Bwana, umrehemu mwanangu, kwa kuwa ana kifafa, na kuteswa vibaya; maana mara nyingi huanguka motoni, na mara nyingi majini. Nikamleta kwa wanafunzi wako, wasiweze kumponva. Yesu akajibu, akasema. Envi kizazi kisichoamini, kilichopotoka, nitakaa pamoja nanyi hata lini? Nitachukuliana nanyi hata lini? Mleteni huku kwangu. Yesu akamkemea pepo, naye akamtoka; yule kijana akapona tangu saa ile.

 

Kisha wale wanafunzi wakamwendea Yesu kwa faragha wakasema, Mbona sisi hatukuweza ku- mtoa? Yesu akawaambia, Kwa sababu va upungufu wa imani yenu. Kwa maana, amin, nawaambia, Mkiwa na imani kiasi cha punje ya haradali mtauambia mlima huu, Ondoka hapa uende kule; nao utaondoka; wala halitakuwako neno lisilowezekana kwenu. 


Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo


Copyright © 2026 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUPOTEZA MAISHA YA NAFSI ILI KUPATA YOTE!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Ijumaa, Agosti 7, 2026, 
Juma la 18 la Mwaka

Nah 2:1, 3:1-3, 6-7; 
Kumb 32:35, 39, 41; 
Mt 16:24-28


KUPOTEZA MAISHA YA NAFSI ILI KUPATA YOTE!

Yesu anatuambia katika Injili kwamba, ni lazima kujikana nafsi ili kumfuata. Kujikana maana yake ni, kutokujibakiza, kutokujijengea heshima, kukataa, kujiachia, kujiweka huru kutoka mambo ya vionjo binafsi. Ni kusema “Ndio” kwa Kristo na kusema “Hapana” kwa nafsi. Sababu ya kujikana ni kwamba mioyo yetu ni muhimu zaidi kuliko ulimwengu mzima. Mwanadamu akishapoteza roho yake, imepotea haiwezi kununuliwa popote nakurudishwa. Mwanadamu atakaye ipoteza, ameipoteza milele. Msalaba unaonekana katika hali ya kawaida kama mateso na kupoteza, lakini kwa kweli ni faida. Sadaka ya Kristo Msalabani imekuwa fidia kubwa kwetu na kuleta wokovu. Je nipo tayari kujikana mwenyewe, kuchukua msalaba wangu na kumfuata Kristo? 

Sala: Mungu wangu, Mungu wangu, chukua yote kwangu yanayoniweka mbali nawe, Mungu wangu, Mungu wangu, nipe yote yanayo nileta karibu nawe, Mungu wangu, Mungu wangu, chukua ubinafsi ndani yangu na unipe yote katika wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, IJUMAA, AGOSTI 7, 2026




MASOMO YA MISA, IJUMAA, AGOSTI 7, 2026
JUMA LA 18 LA MWAKA

SOMO 1
Nah. 1:15; 2:2; 3:1-3, 6-7

Tazama juu ya milima iko miguu yake aletaye habari njema, atangazaye Amani. Zishike sikukuu zako, Ee Yuda, uziondoe nadhiri zako; kwa maana yule asiyefaa kitu hatapita kati yako tena kamwe; amekwisha kukatiliwa mbali.

Kwa maana Bwana anairudisha fahari ya Yakobo, kama fahari ya Israeli; maana watekao nyara wamewateka, na kuyaharibu matawi ya mizabibu yao.

Ole wake mji wa damu! Umejaa mambo ya uongo na unyang’anyi; mateka hayaondoki. Kelele za mjeledi, kelele za magurudumu yafanyayo kishindo; na farasi wenye kupara-para, na magari ya vita yenye kuruka-ruka; mpanda farasi akipanga, na upanga ukimeta-meta, na mkuki ukimemetuka; na wingi wa waliouawa, na chungu kubwa ya mizoga; mizoga haina mwisho; wanajikwaa juu ya mizoga yao. Nani nitatupa uchafu uchukizao juu yako, kukufanya uwe mchafu, nami nitakufanya kuwa kitu cha kutazamwa kwa dahrau. Hata itakuwa, wote wakutazamao watakukimbia, wakisema, Ninawi umeharibika; ni nani atakayeuhurumia? Nikutafutie wapi wafariji?

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


WIMBO WA KATIKATI
Kum. 32: 35 – 36, 39, 41 (K) 39

(K) Naua Mimi, nahuisha Mimi.

Maana siku ya msiba wao imekaribia,
Na mambo yatakayowapata yatafanya haraka.
Kwa kuwa Bwana atawaamua watu wake,
Atawahurumia watumwa wake. (K)

Fahamu sasa ya kuwa Mimi, naam, Mimi ndiye.
Wala hapana Mungu mwingine ila Mimi;
Naua Mimi, nahuisha Mimi,
Nimejeruhi, tena naponya. (K)

Nikiuonoa upanga wangu wa umeme,
Mkono wangu ukishika hukumu,
Nitawatoza kisasi adui zangu,
Nitawalipa wanaonichukia. (K)


SHANGILIO
Lk. 8:15

Aleluya, aleluya,
Wanabarikiwa wale ambao kwa unyofu na wema wa mioyo yao hulisikia neno la Mungu, na kulishika.
Aleluya.


INJILI
Mt. 16:24-28

Wakati huo Yesu aliwaambia wanafunzi wake, Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake, anifuate. Kwa kuwa mtu atakaye kuiokoa nafsi yake, ataipoteza; na mtu atakayepoteza nafsi yake kwa ajili yangu, ataiona. Kwani atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote, na kupata hasara ya nafsi yake? Au mtu atatoa nini badala ya nafsi yake? 

Kwa sababu Mwana wa Adamu atakuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika zake; ndipo atakapomlipa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake. Amin, nawaambieni, Pana watu katika hawa wasimamao hapa, ambao hawataonja mauti kabisa, hata watakapomwona Mwana wa Adamu akija katika ufalme wake. 

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo


Copyright © 2026 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.