Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MUNGU ANA MPANGO NASI!


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatatu, Septemba 8, 2026 
Juma la 23 la Mwaka


Sikukuu ya Kuzaliwa Bikira Maria Mtakatifu

Mik 5: 1-4 au Rum 8: 28-30; 
Zab 12: 6; 
Mt 1: 1-16, 18-23


MUNGU ANA MPANGO NASI!

Bikira Maria Mama yetu, alichukuliwa mimba kitakatifu, alizaliwa na kuishi bila dhambi, na sasa anatuombea ili hata mmoja wetu asipotee. Sisi, wanawe tunafurahi kusheherekea sikukuu yake ya kuzaliwa. Kuhusu sikukuu ya leo Mt. Andrea wa Crete anasema,"viumbe vyote vilivyo umbwa viimbe sifa na kucheza na kwa pamoja viungane kuadhimisha utukufu wa siku hii...kwani leo hekalu limejengwa kwa ajili ya Muumba wa ulimwengu". Maria alizaliwa kama hekalu la Muumba, na kwa njia ya utii wake akatimiza lengo lake ambalo alizaliwa kwa ajili yalo.

Kama Mungu alivyokuwa na mpango kwa Maria, kuzaliwa kwetu sio kwa bahati mbaya au makosa. Mungu ana mpango nasi. Kama Maria alivyotimiza lengo lake duniani, tunapaswa kutambua lengo letu katika maisha na kuwa waaminifu kwa lengo hilo. Tunapaswa kuheshimu maisha ya wengine pia, kwani Mungu naye ana mpango nao pia! Tuwaombee kwa namna ya pekee “ watoto wa kike” ambao siku hii pia ni maalumu kwa ajili yao pia

Sala: Bwana, kwa maombezi ya Bikira Maria Mama yetu, tufundishe kuheshimu kila mtu. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA SEPTEMBA 8, 2026


MASOMO YA MISA 
JUMATATU, SEPTEMBA 8, 2026
JUMA LA 23 LA MWAKA


SIKUKUU YA KUZALIWA BIKIRA MARIA MTAKATIFU

SOMO 1
Rum. 8:28 – 30

Twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake. Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi. Na wale aliowachagua tangu asili, hao akawaita; na wale aliowaita, hao akawahesabia haki; na wale aliowahesabia haki, hao akawatukuza.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 13:5 – 6 (K) Isa. 61:10

(K) Nitafurahi sana katika Bwana.

Nami nimezitumainia fadhili zako;
Moyo wangu na uufurahie wokovu wako. (K)

Naam, nimwimbie Bwana,
Kwa kuwa amenitendea kwa ukarimu. (K)



INJILI
Mt. 1:1 – 16, 18 – 23

Kitabu cha ukoo wa Yesu Kristo, mwana wa Daudi, mwana wa Ibrahimu.

Ibrahimu alimza Isaka; Isaka akamzaa Yakobo; Yakobo akamzaa Yuda na ndugu zake; Yuda akamzaa Peresi na zera kwa Tamari; Peresi akamzaa Esromu; Esromu akamzaa Aramu; Aramu akamzaa Aminadabu; Aminadabu akamzaa Nashoni; Nashoni akamzaa Salmoni; Salmoni akamzaa Boazi kwa Rahabu; Boazi akamzaa Obedi kwa Ruthu; Obedi akamzaa Yese; Yese akamzaa mfalme Daui. Daudi akamzaa Sulemani kwa yule mke wa Uria; Sulemani akamzaa Rehoboamu; Rehoboamu akamzaa Abiya; Abiya akamzaa Asa; Asa akamzaa Yehoshafati; Yehosahafati akamzaa Yoramu; Yoramu akamzaa Uzia; Uzia akamzaa Yothamu; Yothamu akamzaa Ahazi; Ahazi akamzaa Hezekia; Hezekia akamaza Yosia; Yosia akamzaa Yekonia na ndugu zake, wakati wa ule uhamisho wa Babeli. Na baada ya ule uhamisho wa Babeli, Yekonia akamzaa Shealtieli; Shealtieli akamzaa Zerubabeli; Zerubabeli akamzaa Abihudi; Abihudi akamzaa Eliakimu; Eliakimu akamzaa Azori; Azori akamzaa Sadoki; Sadoki akamzaa Akimu; Akimu akamzaa Eliudi; Eliudi akamzaa Eleazari; Eleazari akamzaa Matani; Matani akamzaa Yakobo; Yakobo akamzaa Yusufu mumewe Mariamu aliyemzaa Yesu aitwaye Kristo.

Kuzaliwa kwake Yesu Kristo kulikuwa hivi.

Mariamu mama yake alipokuwa ameposwa na Yusufu kabla hawajakaribiana, alionekana ana mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu. Naye Yusufu, mumewe, kwa vile alivyokuwa mtu wa haki, asitake kumwaibisha, aliazimu kumwacha kwa siri. Basi alipokuwa akifikiri hayo, tazama, malaika wa Bwana alimtoke katika ndoto, akisema, Yusufu, mwana wa DAudi, usihofu kumchukua Mariamu mkeo, maana mbimba yake ni kwa uweza wa Roho Mtakatifu. Naye atazaa mwana, nawe utwamwita jina lake Yesu, maana, yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao. Hayo yote yamekuwa, ili litimie neno lililonenwa na Bwana kwa ujumbe wa nabii akisema, Tazama, bikira atachukua mimba, Naye atazaa mwana; Nao watamwita jina lake Imanueli; Yaani, Mungu pamoja nasi.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

WATU WASIO TIWA CHACHU!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumatatu, Septemba 7, 2026. 
Juma la 23 la Mwaka


1 Kor 5: 1-8; 
Zab 5: 5-7, 12; 
Lk 6: 6-11


WATU WASIO TIWA CHACHU!


“Mahusiano hayawezi kufa hivi hivi bila sababu. Yanakufa kwacsababu ya ubinafsi na kukosa uelewa”. Kukiwa na upendo na uelewa uhusiano hauwezi kufa kamwe.  Katika Injili ya Leo tunamsikia Yesu akimponya mtu aliye na mkono ulio pooza akiwa katika Sinagogi siku ya Sabato. Katika hali ya kukosa uelewa, kuwa na ubinafsi, na umimi wa viongozi wa Wayahudi, Waandishi na Mafarisayo hawakuruhusu akili zao na mioyo yao kuelewa maneno na matendo ya Yesu. Walianza kumlaumu. Viongozi hawa walikuwa wanajali zaidi kushika sheria za Sabato zaidi ya kuleta nafuu kwa wanao teseka. Waliweza kuokoa mnyama aliyeanguka shimoni siku ya sababu zaidi ya kuonesha huruma kwa mwanadamu mwenzao.

Yesu alikuwa na haki ya kumuokoa yule mgonjwa sio tu kwa kumponya mkono wake lakini hata kumsamehe makosa yake na kumpa neema, Amani na furaha. Mt. Paulo anatuonya sisi tugeuze hali zetu, tuzirekebishe. Tuadhimishe uwepo wetu na Yesu, si kwakurudia chachu ya kale, chachu ya chuki na uovu bali tukiwa donge jipya lisilochachuka ambalo Paulo anasema ni weupe wa moyo na kweli. Tusiwe watu wasio eleweka katika maisha yetu ya ufuasi, tumgeukie Yesu kweli na tuweke lengo la kuacha maisha ya kale. Achana na kiburi, wivu, kushengenya wengine, kufurahia uovu, ubinafsi, uchoyo! Kwani hizi sio sifa za mfuasi wa Yesu. Tuombe neema ya Mungu ituongoze ili daima tuweze kufurahi jirani zetu wanapofanikiwa, tusiwazibie milango tusije tukawa kama mafarisayo na waandishi. 

Sala: Ee Bwana, tusaidie tuweze kusafisha chachu ya kale na kuiondoa, tunaomba utufanye donge jipya la uaminifu na kweli. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA JUMATATU, SEPTEMBA 7, 2026



MASOMO YA MISA 
JUMATATU, SEPTEMBA 7, 2026
JUMA LA 23 LA MWAKA


SOMO 1
1Kor. 5:1 – 8

Habari imeenea ya kuwa kwenu kuna zinaa, na zinaa ya namna isiyokuwako hata katika Mataifa, kwamba mtu awe na mke wa babaye. Nanyi mwajivuna, wala hamkusikitika, ili kwamba aondolewe miongoni mwenu huyo aliyetenda jambo hilo. Kwa maana kweli, nisipokuwapo kwa mwili, lakini nikiwapo kwa roho, mimi mwenyewe, nimekwisha kumhukumu yeye aliyetenda jambo hilo, kana kwamba nikiwapo. Katika jina la Bwana wetu Yesu, ninyi mkiwa mmekusanyika pamoja na roho yangu, pamoja na uweza wa Bwana wetu Yesu; kumtolea Shetani mtu huyo, ili mwili uadhibiwe, ili na roho iokolewe katika siku ya Bwana Yesu.

Kujisifu kwenu si kuzuri. Hamjui kwamba chachu kidogo hulichachusha donge zima? Basi, jisafisheni, mkatoe ile chachu ya kale, mpate kuwa donge jipya, kama vile mlivyo hamkutiwa chachu. Kwa maana Pasaka wetu amekwisha kutolewa kuwa sadaka, yaani, Kristo; basin a tuifanye karamu, si kwa chachu ya kale, wala kwa chachu ya uovu na ubaya, bali kwa yasiyochachika, ndio weupe wa moyo na kweli.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 5:4 – 6, 11 (K) 8

(K) Bwana, uniongoze kwa haki yako.

Unawachukia wote watendao ubatili.
Utawaharibu wasemao uongo;
Bwana humzira mwuaji na mwenye hila. (K)

Maana huwi Mungu apendezwaye na ubaya;
Mtu mwovu hatakaa kwako;
Wajivunao hawatasimama mbele za macho yako. (K)

Nao wote wanaokukimbilia watafurahi;
Watapiga daima kelele za furaha.
Kwa kuwa Wewe unawahifadhi,
Walipendao jina lako watakufurahia. (K)


SHANGILIO
Zab. 19:8

Aleluya, aleluya,
Amri ya Bwana ni safi, 
huyatia macho nuru. 
Alelluya.


INJILI
Lk. 6:6 – 1

Ilikuwa siku ya sabato nyingine Yesu aliingia katika sinagogi akafundisha; na mlikuwamo mtu ambaye mkono wake wa kuume umepooza. Na waandishi na Mafarisayo walikuwa wakimvizia, ili waone kwamba ataponya siku ya sabato; kusudi wapate neno la kumshitakia. Lakini yeye atakayatambua mawazo yao, akamwambia yule mwenye mkono uliopooza, Ondoka, simama katikati; akaondoka akasimama.

Ndipo Yesu akawaambia, Nawauliza ninyi, Je! Ni halali siku ya sabato kutenda mema, au kutenda mabaya; kuponya roho au kuangamiza? Akawakazia macho wote pande zote, akamwambia yule mtu, Nyosha mkono wako. Akaunyosha; mkono wake ukawa mzima tena. Wakajawa na uchungu, wakashauriana wao kwa wao wamtendeje Yesu.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUJENGA JUMUIYA YENYE KUWA NA TAHADHARI!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila Jumapili
Jumapili, Septemba 6, 2026

Dominika ya 23 ya Mwaka

Ez 33: 7-9;
Zab 94: 1-2, 6-9;
Rom 13: 8-10;
Mt 18: 15-20


KUJENGA JUMUIYA YENYE KUWA NA TAHADHARI!

Wakati watu wameshakutana na ugumu fulani, wanakuwa wanatoa kiashirio kwa wengine kwamba muelekeo sio mzuri, viashirio vyao mara nyingi wengi hawa vitilii maanani. Lakini katika hali ya kweli, wengi hupenda kuwatazama wengine wakiwa katika njia isio faa. Mara nyingi wanawachukia, kuwatania na kuwaona wajinga. Mungu analinganisha kazi ya nabii Ezekieli na ya mlinzi. Alikuwa apewe onyo kutoka kwa Mungu naye alipeleke onyo hilo kwa kila mtu. Kazi ya Kanisa na ya kila mkristo ni sawa sawa. Ni kuwaongoza watu kwa ujumbe wa neno la Mungu. Siku hizi tunatumia teknolojia yenye nguvu kuwapa watu ishara ya hatari ya kujisahau kushika neno la Mungu. Tunachofanya leo na teknolojia kilifanyika katika Biblia, ambapo waliwaweka walinzi katika sehemu Fulani ili aweze kutoa ishara ya hatari wakati aduia anataka kukaribia.

"Mtu mmoja alikuwa akishanga shangaa aliokota ufunguo bondeni karibu na mlima mkubwa. Ulikuwa ni ufunguo wa ajabu, ufunguo ambao ulikuwa na uwezo wakufungua kila aina ya nyumba yenye hazina ulimwenguni. Kwa ufunguo huu alikusanya dhahabu na almasi kutoka katika sehemu mbali mbali alizopenda duniani. Akiwa njiani akirudi alisikia sauti ikimwambia kutoka chini ya mlima: “kabla haujatoka nje, hakikisha hausahau kitu muhimu kuliko vyote. Gafla mlango ukafunga moja kwa moja. Alikuwa amesahau kuchukua ufunguo.”

Mwanadamu daima anatafuta kupata ufunguo wa furaha, Amani na kujitosheleza. Sisi wote tunatafuta ufunguo wa urafiki, kueleweka, kuwa na jina na uzuri, na kuwa na kazi nzuri yenye kuvutia na faraja. Wengine wanatafuta furaha kwa fedha, madaraka nk. Lakini hivi vyote vinatufunga na kujikuta tunapotelea huko. Vinatufunga kiasi ambacho tunasahau kitu muhimu ziadi nacho ni ufunguo wa maisha. Maisha ya Ukristo yanatufundisha kwamba dunia hii itapita, hiki ndicho tunacho paswa kuzingatia kwa macho yetu na kutazama “maisha ya umilele”. Hii inamaana kwamba maisha yetu hapa duniani yana lengo zaidi ya lengo la kawaida. Furaha tulio nayo hapa sio kitu, ni kivuli tu cha furaha halisi ambayo tutakuwa nayo huko mbinguni. Lakini ufunguo wa furaha ya maisha haya uko wapi?

Katika somo la Injili ya leo Yesu anatuonesha picha nzuri ya jumuiya ya mapendo na yenye kujali. Inatuonesha ni kwa jinsi ghani tunaweza kuanzisha jumuiya ya kweli ya Kikristo na yenye kupendana.

1. Kama mtu akikukosa, tunapaswa tumwendee kwa upendo wa Kimungu na kumrudisha kundini. Tofauti kabisa na kumlaumu na kuanza kumlaumu, tunapaswa kumfuata kwa mapendo na kumsihi katika mapendo yetu. Injili inatushauri kuwa na mazungumzo ya moja kwa moja, kwa utulivu na katika hali ya upekee, katika hali ya kurekebishana kindugu, ili kuanzisha tena urafiki uliyo vunjika. Kama hili litashindikana inashauriwa kuchukuwa watu wenye hekima na kumfuata kumuonesha kwamba jumuiya nzima inakuhitaji kurudi kundini katika mapendo yote.

2. Yesu anasisitiza nguvu ya sala. Anasema “pale wawili au watatu walipokusanyika kwa ajili yangu, Baba atakuwa katikati yao”. Huu ni uhakika anaotoa Yesu kwamba wale wanaosali yeye atakuja katikati yao na kuwa kati yao na kushiriki katika sala yao. Wayahudi walikuwa na Imani kubwa katika sala za pamoja. Iliandikwa “wawili walipo kusanyika na wanajihusisha na kujifunza Torati, utukufu wa Mungu upo katikati yao” sala za jumuiya huweka magomvi mbali na kuleta umoja. Agano, jumuiya, ukarimu, msamaha hizi ni sifa za dini ya Kibiblia. Uzoefu wa haya yote vinafanya maisha yetu kuwa na furaha, na kuishi vizuri. Haya yote yanawezekana tu pale ambapo tuna upendo. Kwa mfano,

"Mfungwa mmoja alikuwa anarudi nyumbani, kutoka katika mahabusu ya mbali akiwa kwenye treni. Alikuwa akiona aibu kwa kufungwa kwake na alikuwa akidhani familia yake itakuwa imemsamehe. Kwa ishara ya kuonesha kwamba wamemsamehe, walipaswa wafunge riboni nyeupe kwenye mti ambao ulikuwa karibu na gari nyumbani kwake. Hivyo kama hataona riboni nyeupe kwenye mti, yeye atapitiliza na treni aelekee kokote atakapo kwenda. Wakati treni ilivyofika karibu na nyumbani, akawa na wasi wasi mkubwa kiasi ambacho hakuthubutu kutazama kupitia dirishani. Marafiki zake wakaamua kubadilisha nafasi wakisema tunafahamu tu ataangalia mti uliokaribu na gari. Ghafla akanyanyua kichwa bila kujua na tazama sio roboni moja iliyowekwa kwenye mti bali mti wote ulikuwa umejaa riboni"

Amani na mshikamano unawezekana tu, pale ambapo watu wanaishi kwa roho ya upendo na msamaha. Mungu ni upendo na penye upendo Mungu yupo. Upendo wa Mungu unabeba pia upendo kwa jirani. Upendo tunaweza kuupata tu tunapo amua kuishi na wenzetu, kwa mshikamano katika jumuiya. Hili halimuumizi mtu yeyote, bali linakamilisha kila kitu na kufanya maisha yafikie katika kilele cha hali ya juu.

Mungu ametufanya sisi tuwe walinzi wa dunia sasa. Tunapaswa kuwa walinzi, kutangaza kwa kila mmoja, jumuiya zetu, na ulimwengu wa ukweli katika Yesu Kristo. Tunaitwa kusimama pamoja, bila kuachana katika Imani bila kuogopa kuitwa tusio na maana au mafundisho potofu, bali tutangaze kwa jirani na jumuiya zetu, ili watu wafahamu katika kutokufahamu kwao, kumuamini Yesu, na kukuwa katika neema na utakatifu. Tunapaswa kuwasaidia wengine watambue makosa yao, hasa tukiwa na kazi kama ya wazazi kwa mtoto, mwalimu kwa wanafunzi, wazee na vijana.

Tutumie njia sawa ya kuwasaidia wengine watoke katika makosa yao bila ya kuwaumiza au kuwadhalilisha na kuwaachia makovu. Badala ya kuponya tukakuza kidonda zaidi. Katika vikao vyetu tuangalie njia njema ya kumsadia mtu na kumuonya badala ya kumwanika hadharani mbele ya watu wote, kama kuna njia nzuri ya mtu mmoja kumfuata kwa hekima utamsaidia zaidi, kuliko kumkosoa mtu mbele ya watu wengi au katika kikao, hili haliponyi kwani mmoja hujisikia amedhalilishwa na utu wake kudharauliwa. Mfano tusisubiri mpaka mtu afe ndio tupate muda wa kukaa pamoja tuje kumrekebisha mtu mbele ya kikao cha ukoo, badala yake tutumie njia mbadala ya kutuma mtu mwenye hekima amsaidie na kupatana kabla ya kukaa pamoja. Kutangaza dhambi ya mtu mbele ya kikao, daima haina lengo la kuleta upatanisho wa kweli badala yake humuachia mtu maumivu na kisasi moyoni. Hakuna hata mmoja wetu angependa dhambi yake itajwe mbele ya watu. Ndio maana sakramenti ya kitubio husaidia kweli. Tumuige Yesu aliyekuwa na huruma kwa wadhambi.

Sala: Bwana, upo nasi katika jumuiya yetu, tukishikana pamoja kwa mapendo, huruma na msamaha. Tunakuomba tuwe watu wakutafuta furaha, upendo na Amani. Tunakuomba tuwe tayari kusamehe na kupatana na kila mtu. Yesu, ninakuamini wewe. Amina

------------------------
Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUMAPILI, SEPTEMBA 6, 2026



MASOMO YA MISA,
JUMAPILI, SEPTEMBA 6, 2026
JUMA LA 23 LA MWAKA
________

MWANZO
Zab. 119:137, 124

Ee Bwana, wewe ndiwe mwenye haki, na hukumu zako ni za adili. Kama zilivyo rehema zako umtendee mtumishi wako.
________

SOMO I
Eze. 33:7-9

Basi wewe, mwanadamu, nimekuweka kuwa mlinzi kwa nyumba ya Israeli; basi ulisikie neno hili kinywani mwangu, ukawape maonyo yangu. Nimwambiapo mtu mbaya, Ewe mtu mbaya, hakika utakufa, nawe husemi neno la kumwonya mtu huyo, aiache njia yake, mtu mbaya huyo atakufa katika uovu wake, lakini damu yake nitaitaka mkononi mwako. Walakini ukimwonya mtu mbaya kwa sababu ya njia yake, kusudi aiache; wala yeye asiiache; atakufa huyo katika uovu wake, lakini wewe umejiokoa roho yako.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu
________

WIMBO WA KATIKATI
Zab. 95:1-2, 6-9 (K) 7-8

(K) Ingekuwa heri leo tusikie sauti yake!

Tusifanye migumu mioyo yetu.
Njoni tumwimbie Bwana,
Tumfanyie shangwe mwamba wa wokovu wetu.
Tuje mbele yake kwa shukrani,
Tumfanyie shangwe kwa zaburi. (K)

Njoni, tuabudu, tusujudu,
Tupige magoti mbele za Bwana aliyetuumba.
Kwa maana ndiye Mungu wetu,
Na sisi tu watu wa malisho yake,
Na kondoo za mkono wake. (K)

Ingekuwa heri leo msikie sauti yake!
Msifanye migumu mioyo yenu;
Kama vile huko Meriba;
Kama siku ile ya Masa jangwani,
Hapo waliponijaribu baba zetu;
Wakanipima, wakayaona matendo yangu. (K)
________

SOMO 2
Rum. 13:8-10

Msiwiwe na mtu chochote, isipokuwa kupendana; kwa maana ampendaye mwenzake ameitimiza sharia. Maana kule kusema, Usizini, Usiue, Usiibe, Usitamani, na ikiwapo amri nyingine yoyote, inajumlishwa katika neno hili, ya kwamba, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Pendo halimfanyii jirani neno baya, basi pendo ndilo utimilifu wa sheria.

Neno la Bwana...Tumshukuru Mungu
________

SHANGILIO
Yn. 14:23

Aleluya, aleluya,
Mtu akinipenda, atalishika neno langu;
Na baba yangu atampenda; Nasi tutakuja kwake.
Aleluya.
________

INJILI
Mt. 18:15-20

Siku ile Yesu aliwaambia wafuasi wake: Ndugu yako akikukosa, enenda ukamwonye, wewe na yeye peke yenu; akikusikia, umempata nduguyo. La, kama hasikii, chukua pamoja nawe tena mtu mmoja au wawili, ili kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila neno lithibitike. Na asipowasikiliza wao, liambie kanisa; na asipolisikiliza kanisa pia, na awe kwako kama mtu wa mataifa na mtoza ushuru. Amin, nawaambieni, yoyote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni; na yoyote mtakayoyafungua duniani yatakuwa yamefunguliwa mbinguni.



Tena nawaambia, ya kwamba wawili wenu watakapopatana duniani katika jambo lolote watakaloliomba, watafanyiwa na Baba yangu aliye mbinguni. Kwa kuwa walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo
________

-------------------------
Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUFANYA LISILO HALALI SIKU YA SABATO?



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumamosi, Septemba 5, 2026 
Juma la 22 la Mwaka


1 Kor 4: 6-15; 
Zab 144: 17-21; 
Lk 6: 1-5


KUFANYA LISILO HALALI SIKU YA SABATO?

Sabato ilikuwepo hata kabla Torati haijatolewa katika Mlima Sinai (Kut 19). Wayahudi walifundishwa “kukumbuka siku ya Sabato” na kuifanya takatifu. Siku ya sabato ilitegemewa kuwa siku ya mapumziko na siku ya kuabudu, muda wa kukumbuka siku aliyo pumzika Mungu baada ya kazi ya uumbaji, siku ya saba. Mafarisayo walichukulia kitendo walichofanya wafuasi kwenye Injili kuwa ni kufuru kuhusu Sabato. Walivyomlaumu Yesu kuwa ameikufuru Sabato, Yesu aliwajjibu vyema. Yesu alimtumia Daudi kama mfano, wakati Daudi akimkimbia Sauli alikula mikate ile ya Wonyesho (iliobarikiwa) inayotumika tu pale Mahali Patakatifu (tabernacle) ambayo ililiwa na makuhani pekee. (Sam 21: 1-6). Yesu anasema wazi kwamba Sabato sio Bwana, bali Mwana wa mtu (Yesu mwenyewe) ndiye. Ni yeye mwenyewe mwenye mamlaka ya kubadili torati na sheria ya Sabato. 

Yesu anatufundisha tusifungwe mno na sheria tushindwe kuonesha upendo kwa jirani zetu. Pamoja na kutimiza majukumu yetu, tusisahau kwamba sisi tunayo sheria ya Kristo ambayo ni upendo, sheria isiyo na upendo si sheria ya Kristo. Mt. Greogori mkuu, alitambua hilo ndio maana alitoa huduma bora katika kanisa, na zaidi sana upendo wake kwa fukara uliomdhihirisha kuwa yeye ni kiongozi na mchungaji wa kweli. Tumuombe atuombee kwa Mungu ili nasi tuweze kuwa na roho ya kuwapenda wote wasiojiweza tuwe na moyo wakuwahudumia kwa upendo bila kujali jamii inaniona je. Ndugu zangu sisi tunalo deni, na deni letu ni Upendo kwa Mungu na jirani zetu, tujaribu kulilipa kila siku tuwapo hapa duniani.

Sala: Bwana, naomba nikuheshimu katika kazi yangu na katika mapumziko yangu na niwatendee jirani zangu kwa heshima na upendo. Niweke mbali na roho ya mabishano na ubinafsi ili niweze kutafuta uzuri wa jirani zangu katika hali zote. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 5, 2026




MASOMO YA MISA 
JUMAMOSI, SEPTEMBA 5, 2026
JUMA LA 22 LA MWAKA


SOMO 1
1Kor. 4:6 – 15

Ndugu zangu, mambo hayo nimeyafanya kuwa mfano wa mimi na Apolo kwa ajili yenu, ili kwamba kwa mfano wetu mpate kujifunza kutokupita yale yaliyoandikwa; ili mmoja wenu asijivune kwa ajili ya huyu, kinyume cha mwenziwe. Maana ni nani anayekupambanua na mwingine? Nawe una nini usichokipokea? Lakini iwapo ulipokea, wajisifia nini kana kwamba hukupokea? Mmekwisha kushiba, mmekwisha kupata utajiri, mmemiliki pasipo sisi. Naam, laity mngemiliki, ili sisi nasi tumiliki pamoja nanyi! Maana nadhani ya kuwa Mungu ametutoa sisi mitume mwisho, kama watu waliohukumiwa wauawe; kwa sababu tumekuwa tamasha kwa dunia; kwa malaika na wanadamu.

Sisi tu wapumbavu kwa ajili ya Kristo, lakini ninyi ni wenye akili katika Kristo; sisi tu dhaifu, lakini ninyi mna nguvu; ninyi mna utukufu, lakini sisi hatupati heshima. Hata saa hii ya sasa, tuna njaa na kiu, tu uchi, twapigwa ngumi, tena hatuna makao; kasha twataabika tukifanya kazi kwa mikono yetu wenyewe. Tukitukanwa twabariki, tukiudhiwa twastahimili; tukisingiziwa twasihi; tumefanywa kama takataka za dunia, na tama ya vitu vyote hata sasa.

Siyaandiki hayo ili kuwatahayarisha; bali kuwaonya kama watoto niwapendao. Kwa kuwa ijapokuwa mna waalimu kumi elfu katika Kristo, walakini hamna baba wengi. Maana mimi ndimi niliyewazaa katika Kristo Yesu kwa njia ya Injili.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 145:17 – 21 (K0 18

(K) Bwana yu karibu na wote wamwitao.

Bwana ni mwenye haki katika njia zake zote,
Na mwenye fadhili juu ya kazi zake zote.
Bwana yu karibu na wote wamwitao,
Wote wamwitao kwa uaminifu. (K)

Atawafanyia wamchao matakwa yao,
Nay atakisikia kilio chao na kuwaokoa.
Bwana huwahifadhi wote wammpendao,
Na wote wasio haki atawaangamiza. (K)

Kinywa change kitazinena sifa za Bwana;
Wote wenye mwili na walihimidi jina lake takatifu
Milele na milele. (K)


SHANGILIO
Zab. 119:18

Aleluya, aleluya, 
Unifumbue macho yangu niyatazame 
maajabu yatokayo katika sharia yako.
Aleluya.


INJILI
Lk. 6:1 – 5

Ilikuwa siku ya sabato moja Yesu alikuwa akipita katika mashamba, wanafunzi wake wakawa wakivunja masuke na kuyala, wakiyapukusa-pukusa mikononi mwao. Basi baadhi ya Mafarisayo wakawaambia, Mbona mnafanya lisilo halali siku ya sabato? Yesu akawajibu akawaambia, Hamkulisoma, hata hilo alilolifanya Daudi, alipokuwa na njaa, nay eye na wale aliokuwa nao? Jinsi alivyoingia katika nyumba ya Mungu, akaitwaa mikate ile ya Wonyesho, akaila akawapa na hao wenziwe, ambayo si halali kuila ila kwa makuhani peke yao. Akawaambia, Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

HAKUNA KIRAKA; HAKUNA KUCHANGANYA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Ijumaa, Septemba 4, 2026, 
Juma la 22 la Mwaka wa Kanisa

1Kor 4: 1-5; 
Zab 36: 3-6, 27-28, 39-40; 
Lk 5: 33-39

HAKUNA KIRAKA; HAKUNA KUCHANGANYA!

Leo Yesu anatumia mfano wa viriba vinavyotumika kuhifadhia divai ili atufundishe lengo letu la kuja Ulimwenguni. Kama ilivyo vigumu kwa divai mpya kukaa kwenye viriba vikukuu, mafundisho ya Yesu hayawezi kuendana na namna yetu ya maisha ya dhambi na jinsi ya kufikiri kama zamani. Kumkubali Yesu na mafundisho yake ina maana kwamba kuanza maisha mapya. Hakuna kuchanganya maisha ya zamani na maisha mapya, lazima kuacha maisha ya dhambi na kuanza maisha mapya. Unavyoitwa na Yesu kuna labda uitike “NDIYO” au “HAPANA”. Ndiyo ikimanisha kwamba unafanywa kiumbe kipya kabisa na kuanza maisha mapya au Hapana ukimanisha umekataa na umeamua kuishi katika maisha ya zamani ya dhambi na kubaki katika hali mbaya. Tuombe neema ya Roho Mtakatifu ili sisi tuliosema ndio tusichanganye tena maisha haya mapya na maisha ya dhambi, maisha ya kale.

Tukienenda katika “NDIYO” yetu ndani ya maisha mapya ndani ya Kristo, kama Mt. Paulo anavyosema katika somo la kwanza, watu watatuhesabu kuwa watumishi wa Kristo, na mawakili wa siri ya Mungu. Na furaha yetu haitakuwa kwasababu watu wametuhesabu kuwa watumishi wa Kristo bali ni kwasababu Mungu atatuhesabu kuwa mawakili wake hapa duniani. Kwani hata hivyo Mungu akituhesabia haki ninani tena awezaye kutuhukumu? Hakuna yeyote wala nafsi zetu wala mwanadamu yeyote. Kwakuwa furaha yetu itakuwa katika Bwana daima.

Sala: Bwana Yesu, nisaidiye kubadili maisha yangu kwa mwanga wa Neno lako. Amina



Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 4, 2026



MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 4, 2026
IJUMAA, JUMA LA 22 LA MWAKA


SOMO 1
1Kor. 4:1 – 5

Mtu na atuhesabu hivi, kuwa tu watumishi wa Kristo, na mawakili wa siri za Mungu. Hapo tena inayohitajiwa katika mawakili, ndiyo mtu aonekane kuwa mwaminifu. Lakini, kwangu mimi, si kitu kabisa nihukumiwe na ninyi, wala kwa hukumu ya kibinadamu, wala sijihukumu hata nafsi yangu. Maana sijui sababu ya kujishitaki nafsi yangu, lakini sihesabiwi haki kwa ajili hiyo; ila anihukumuye mimi ni Bwana. Basi ninyi msihukumu neno kabla ya wakati wake, hata ajapo Bwana; ambaye atayamulikisha yaliyositirika ya giza, na kuyadhihirisha mashauri ya mioyo; ndipo kila mtu atakapoipata sifa yake kwa Mungu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 37:3 – 6, 27, 28, 39 – 40 (K) 39

(K) Wokovu wa wenye haki una Bwana.

Umkabishi Bwana njia yako,
Pia umtumaini, naye atafanya.
Atajitokeza haki yako kama nuru,
Na hukumu yako kama adhuhuri. (K)

Umtumaini Bwan aukatende mema,
Ukae katika nchi, upendezwe na uaminifu.
Nawe utajifurahisha kwa Bwana,
Naye atakupa haja za moyo wako. (K)

Jiepue na uovu, utende mema, 
Na kukaa hata milele.
Kwa kuwa Bwana hupenda haki,
Wala hawaachi watauwa wake. (K)

Na wokovu wa wenye haki una Bwana;
Yeye ni ngome yao wakati wa taabu.
Naye Bwana huwasaidia na kuwaopoa;
Huwaopoa na wasio haki na kuwaokoa;
Kwa kuwa wamemtumaini Yeye. (K)


SHANGILIO
Zab. 25:4, 5

Aleluya, aleluya,
Ee Bwana, unijulishe njia zako, unifundishe mapito yako.
Aleluya.


INJILI
Lk. 5:33 – 39

Mafarisayo na waandishi walimwambia Yesu, Wanafunzi wa Yohane hufunga mara nyingi, na kuomba dua; na kadhalika wanafunzi wa Mafarisayo; lakini wanafunzi wako hula na kunywa! Lakini Yesu akawaambia, Je! Mwaweza kuwafanya wafunge walioalikwa arusini, akiwapo bwana arusi pamoja nao? Lakini siku zitakuja watakapoondolewa bwana arusi, ndipo watakapofunga siku zile. Akawaambia na mithali, Hakuna akataye kiraka cha vazi jipya na kukitia katika vazi kuukuu; na kama akitia, amelikata lile jipya, na kile kiraka cha vazi jipya hakilingani na lile vazi kuukuu.

Wala hakuna mtu atiaye divai mpya katika viriba vikuukuu; na kama akitia, ile divai mpya itavipasua vile viriba, divai yenyewe itamwgika, na viriba vitaharibika. Lakini divai mpya sharti kutiwa katika viriba vipya. Wala hakuna anyway divai ya kale akatamani divai mpya; kwa kuwa asema, Ile ya kale ndiyo iliyo njema.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com