Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

YESU KRISTO, HAZINA YANGU



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumapili, 26 Julai, 2026 
Juma la 17 la Mwaka

1 Fal 3: 5, 7-12; 
Zab 118: 57, 72, 76-77, 127-128;
Rom 8: 28-30; 
Mt 13: 44-52


YESU KRISTO, HAZINA YANGU


Mwaka 1936, Edward VI Mfalme wa England, alitokea kumpenda Valcin, msichana wa kawaida. Kadiri ya mapokeo, Mfalme alikuwa na uwezo tu wa kuoa kutoka katika familia tajiri. Alikuwa na chaguzi mbili tu. Amue kuacha ufalme wake na kumuoa Valcin au kumuacha Valcin na kubaki katika ufalme wake. Lakini wote wawili walikuwa na kitu kimoja, walikuwa watu wa ndoto.

Katika somo la kwanza tunamuona Mungu anamtokea Mfalme Sulemani na kumpa uchaguzi wa kufanya: “niombe kitu nami nitakupa”. Na wakati Sulemani alivyosema “nipe moyo wa kuelewa na hali ya kuweza kutofautisha mema na mabaya”, anaomba uelewa ili aweze kuwahudumia watu wake, aweze kutenda kwa huruma na pia aweze kutambua mema na mabaya. Sulemani anatambua vitu viwili (i) Hekima yote inatoka kwa Mungu (ii) kwa kuwa na hekima mambo yote yatakuja. Kwa kutumia lugha tunaweza kusema kwamba Sulemani aliomba “lulu” ya thamani kubwa. Na aliipata. Somo linatufunsdisha kwamba tunapo yatimiza mapenzi ya Mungu tunakuwa katika njia njema na katika mstari wa ufalme wake.

Na somo la Pili barua ya mtume Paulo inatupa mambo mawili (i) mambo yote ni mazuri kama tunatenda kwa upendo wa Mungu, tunaoitwa kwa mapenzi yake (ii) Na wote aliowaita aliwachagua na pia kuwahalalisha na pia kuwapa utukufu. Na sehemu muhimu ni kwamba Mungu anawaita watu kwa ngazi mbali mbali waweze kufurahia ufalme wake wa milele. Mungu ametuita kutuhalalisha na kutupa utukufu. Paulo anavyosema Mungu anawaita, hana maana kwamba anawaita baadhi kumtumikia na wengine kupotea. Mpango wa Mungu nikuwa wote waweze kukombolewa. Hii ina maana kwamba ni mapenzi kamili ya Mungu kwamba watu wote wakombolewe kuwaruhusu watu wakubali mapenzi yake au wakatae wenyewe kwa uhuru wao.

Katika somo la Injili Yesu anahitimisha safari ndefu ya mifano kuhusu ufalme wa Mungu kwa kuawasifu wake na waume wale wote waliokuwa werefu katika kumsikiliza na kumuelewa na kujikita katika ujumbe wake. Yesu anaendelea kufundisha kuhusu “Ufalme wa Mbinguni” kwa kutumia habari ndogo za Wagalilaya.

Yesu anatuambia kwamba Hekima ya kweli ni kutambua lulu ya thamani kubwa na kuuza vyote na kuinunua. Mifano yetu miwili katika somo la Injili, kuhusu, thamani iliofichwa na lulu-ni fundisho la kuachana na malimwengu na kujikita kwa Kristo kwa kufanya ufalme wake uweze kukuwa ulimwenguni katika hali ya kweli. Matayo mtoza ushuru huenda na yeye alitambua kitu kama hiki alivyo amua kuacha vyote na kumfuata Yesu wa Nazareth. Alivyo mtambua Yesu na hekima yake, mambo yote mengine yalikuwa ni ya ziada. Yesu pia anaweza kuja katika maisha yetu ya kila siku bila sisi kujitambua kama alivyokuja kwa Mathayo.

Mfano wa kuvua samaki kwa kutumia neti: katika Palestina kulikuwa na njia mbili za kuvua samaki, wa kwanza ilikuwa kurusha neti, katika hali ya akili kubwa na utalaamu mkubwa pia kwa wakati. Aina ya pili ilikuwa ni kulazi neti chini. Na baada ya kushika, kulikuwa na kuokota baadhi na mengine kutupa, samaki wazuri walipelekwa sokoni na wengine wabaya kutupwa. Na kama neti hii ya kulaza chini inavyo kusanya samaki wazuri na wabaya, kanisa pia lina watu wema na wabaya, watakatifu na wadhambi. Kama ilivyokuwa kwa ngano na magugu, mfano huu unatuonya na hali ya kuhukumu kabla, lakini pia inatuonya kuhusu hukumu inakayo kuja.

Kuwa Mkristo Mkristo ni sawa na kuwa kama mtu anaye itafuta lulu. Kuwa mkristo ni sawa na kuwa mtu anayewinda lulu. Inagharimu majitoleo makubwa na sadaka. Lakini pia kuna tofauti kubwa kati ya wakristo na wengine. Paulo anaonesha kwa barua yake kwa Wakorintho “wachezaji wanafanya mazoezi katika hali zote, wanafanya hivyo ili kupata lulu inayo haribika, lakini sisi tunafanya hivyo ili kupata lulu isiyo haribika” (1 Kor 9:25) hali hii ni tofauti. Lulu tunayo tafuta kama Wakristo ni lulu ya thamani isiyo haribika.

Ndio maana Injili ya leo inatoa ujumbe huu muhimu. Hakuna kitu chochote ulimwenguni kinachoweza kuchukuwa nafasi ya Mungu. Inatuambia pia kilicho na maana zaidi tutakapo kufa ni maisha tutakayo ishi, jinsi tutakavyokuwa. Mifano hii inataka kutuambia kwamba wakati mmoja anapo mgundua Yesu katika maisha, vingine vyote vinakuwa ni ziada. Na hiki ndicho Mt. Paulo anacho maanisha anavyosema “kuishi kwangu ni Kristo na ufa ni faida” (Fil 2:21). Kuwa na uhusiano binafsi na Yesu na pia na wengine wengine kumfanya Yesu kuwa ndio kioo cha maisha yao-ni kitu muhimu sana ulimwenguni humu. Yesu anavyo onekana katika maumbo ya mkate na divai, tumpe nafasi ya kwanza na ya hali ya juu.

Sala: Bwana Yesu Kristo, ninatamani kukupa thamani ya kila kitu ya maisha yangu. Ninaomba niache yote ambayo ni kikwazo cha mimi kutokuja kwako, kukupenda na kukuabudi. Ninaomba nitafute Ufalme wa Mungu katika hali zote. Yesu nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JUMAPILI, JULAI 26, 2026



MASOMO YA MISA, JUMAPILI, JULAI 26, 2026
JUMA LA 17 LA MWAKA


1 Fal. 3 : 5, 7-12

Huko Gibeoni Bwana alimtokea Sulemani katika ndoto ya usiku; Mungu akamwambia, Omba utakalo nikupe. Sulemani akasema, Ee Bwana, Mungu wangu, umenitawaza niwe mfalme mimi mtumwa wako badala ya Daudi baba yangu; nami ni mtoto mdogo tu; sijui jinsi inipasavyo kutoka wala kuingia. Na mtumwa wako yu katikati ya watu wako uliowachagua, watu wengi wasioweza kuhesabiwa, wala kufahamiwa idadi yao, kwa kuwa ni wengi. Kwa hiyo nipe mimi mtumwa wako moyo wa adili niwahukumu watu wako, na kupambanua mema na mabaya; maana ni nani awezaye kuwahukumu hawa watu wako walio wengi? Neno hili likawa jema machoni pa Bwana, ya kuwa Sulemani ameomba neno hili. Mungu akamwambia, Kwa kuwa umeomba neno hili, wala hukujitakia maisha ya siku nyingi; wala hukutaka utajiri kwa nafsi yako; wala hukutaka roho za adui zako: bali umejitakia akili za kujua kuhukumu; basi, tazama, nimefanya kama ulivyosema. Tazama, nimekupa moyo wa hekima na wa akili; hata kabla yako hapakuwa na mtu kama wewe, wala baada yako hatainuka mtu kama wewe.

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI 
Zab. 118:57, 72, 76-77, 127-130 (K) 97

(K) Sheria yako naipenda mno ajabu.

Bwana ndiye aliye fungu langu,
Nimesema kwamba nitayatii maneno yako.
Sheria ya kinywa chako ni njema kwangu,
Kuliko maelfu ya dhahabu na fedha. (K)

Nakuomba, fadhili zako ziwe faraja kwangu,
Sawasawa na ahadi yako kwa mtumishi wako.
Rehema zako zinijie nipate kuishi,
Maana sheria yako ni furaha yangu. (K)

Ndiyo maana nimeyapenda maagizo yako,
Kuliko dhahabu, naam, dhahabu iliyo safi.
Maana nayaona mausia yako yote kuwa ya adili,
Kila njia ya uongo naichukia. (K)

Shuhuda zako ni za ajabu,
Ndiyo maana roho yangu imezishika.
Kufafanusha maneno yako kwatia nuru,
Na kumfahamisha mjinga. (K)


SOMO 2 
Rum 8 : 28-30

Twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake. Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwanawake, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi. Na wale aliowachagua tangu asili, hao akawaita; na wale aliowaita, hao akawahesabia haki; na wale aliowahesabia haki, hao akawatukuza. 

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu 


SHANGILIO 
Efe. 1 :17,18

Aleluya, aleluya, Ewe Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, Uyatie nuru macho ya mioyo yetu, Ili tujue tumaini la mwito wake jinsi lilivyo. Aleluya.


INJILI 
Mt. 13: 44-52

Yesu aliwaambia wafuasi wake:  Ufalme wa mbinguni umefanana na hazina iliyositirika katika shamba; ambayo mtu alipoiona, aliificha; na kwa furaha yake akaenda akauza alivyo navyo vyote, akalinunua shamba lile. Tena ufalme wa mbinguni umefanana na mfanya biashara, mwenye kutafuta lulu nzuri; naye alipoona lulu moja ya thamani kubwa, alikwenda akauza alivyo navyo vyote, akainunua.

Tena ufalme wa mbinguni umefanana na juya, lilotupwa baharini, likakusanya wa kila namna; hata lilipojaa, walilivuta pwani; wakaketi, wakakusanya walio wema vyomboni, bali walio wabaya wakawatupa Ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia; malaika watatokea, watatenga waovu mbali na wenye haki, na kuwatupa katika tanuru ya moto; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno.

Yesu aliwauliza, Mmeyafahamu hayo yote? Wakamwambia, Naam. Akawaambia, Kwa sababu hiyo, kila mwandishi mwenye elimu ya ufalme wa mbinguni amefanana na mtu mwenye nyumba atoaye katika hazina yake vitu vipya na vya kale.

Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUJITENGENEZA KATIKA KRISTO!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumamosi, 25 Julai, 2026
Juma la 16 la Mwaka 

Sikukuu ya Mt. Yakobo, Mtume

2 Kor 4: 7-15;
Zab 125: 1-6;
Mt 20: 20-28


KUJITENGENEZA KATIKA KRISTO!


Mtakatifu Yakobo, ambaye sikukuu yake tunaiadhimisha leo, alikuwa mtoto wa Zebedayo na Salome na kaka wa Yohane Mtume na Mwinjili. Alikuwa ni kati ya wale mitume watatu waliochaguliwa na Yesu ili waweze kutoa ushuhuda juu ya miujiza yake mikuu-kugeuka kwa Yesu sura na pia tukio la Gestemane. Alikuwa maarufu katika Kanisa la Yerusalemu, na alikuwa mtume wa kwanza kufa kwaajili ya Kristo. Alikufa kama shahidi, aliuwawa kwa upanga na Herodi Agrippa wa kwanza.

Injili ya leo, kweli ni neno la uzima kwetu sisi wote. Kwa kweli inaonesha njia ya Maisha Katika maisha ya Ukristo wetu. “kuwa kama Mwana wa mtu aliyekuja, si kutumikiwa bali kutumikia na kutoa maisha yake iwe fidia ya wengi”. “Kama unataka kuwa wa Kwanza, kuwa mtumishi wa wote”. Hili ni la kweli kabisa kwa watu katika, serikali, viongozi katika siasa, walimu shuleni, wafanya biashara, wazazi nyumbani, mapadre katika parokia na watu wote. Ni maneno yanayoenda kinyume kabisa na jinsi ulimwengu unavyotaka sisi tufanye. Mara nyingi tunasikia watu wakijitambulisha kwa vyeo vyao na madaraka waliyo nayo, leo maneno haya ya Yesu yanapaswa yasikike tena katika serikali, mashuleni, katika familia, Kanisani na zaidi sana katika maeneo yote ya kazi za mwanadamu. Mtazamo wa Ulimwengu unalenga kutawala watu. Ni kuwa na mamlaka ili katika mamlaka hayo aweze kufaidika. Na mwisho tutatumikiwa kwa jinsi yeyote tunavyotaka.

Lakini kwa Mkristo ni tofauti! Kuwa Mkristo maana yake nikufikiri kama Kristo, na kutenda kama Kristo. Kuishi maisha ya kweli, ikimaanisha kwamba, kuishi tofauti na malimwengu yanavyotaka tuishi. Injili ya leo inatualika kwenye furaha ya kweli, ambayo ni kutumikia. Na matokeo yake tutaitwa wana wa Mungu na tutashiriki katika karamu ya Mbinguni, hakika katika Maisha ya Mbinguni.

Sala: Bwana, nisaidie niweze kutembea katika njia za huduma yako. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.


MASOMO YA MISA, JULAI 25, 2026



MASOMO YA MISA, JULAI 25, 2026
JUMAMOSI, JUMA LA 16 LA MWAKA 
SIKUKUU YA MT. YAKOBO, MTUME


SOMO 1
2 Kor. 4:7 – 15

Tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili adhama kuu ya uwezo iwe ya Mungu, wala si kutoka kwetu. Pande zote twadhikika, bali hatusongwi; twaona shaka, bali hatukati tamaa; twaudhiwa, bali hatuachwi; twatupwa chini, bali hatuangamizwi; sikuzote twachukua katika mwili kuuawa kwake Yesu, ili uzima wa Yesu nao udhihirishwe katika miili yetu. Kwa maana sisi tulio hai, siku zote twatolewa tufe kwa ajili ya Yesu, ili uzima wa Yesu nao udhihirishwe katika miili yetu ipatikanayo na mauti. Basi hapo mauti hufanya kazi ndani yetu, bali uzima ndani yenu.

Lakini kwa kuwa tuna roho ile ile ya imani; kama ilivyoandikwa, Naliamini, na kwa sababu hiyo nalinena; sisi nasi twaamini, na kwa sababu hiyo twanena; tukijua ya kwamba yeye aliyemfufua Bwana Yesu atatufufua sisi nasi pamoja na Yesu, na kutuhudhurisha pamoja nanyi. Kwa maana mambo yote ni kwa ajili yenu, ili neema hiyo ikiongezwa sana, kwa hao walio wengi shukrani izidishwe, na Mungu atukuzwe.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 126 (K) 5

(K) Wapandao kwa machozi watavuna kwa kelele za furaha.

Bwana alipowarejeza mateka wa Sayuni,
Tulikuwa kama waotao ndoto.
Ndipo kinywa chetu kilipojaa kicheko,
Na ulimi wetu kelele za furaha. (K)

Ndipo waliposema katika mataifa,
Bwana amewatendea mambo makuu.
Bwana alitutendea mambo makuu,
Tulikuwa tukifurahi. (K)

Ee Bwana, uwarejeze watu wetu waliofungwa,
Kama vijito vya Kusini.
Wapandao kwa machozi,
Watavuna kwa kelele za furaha. (K)

Ingawa mtu anakwenda zake akilia,
Azichukuapo mbegu za kupanda.
Hakika atarudi kwa kelele za furaha,
Aichukuapo miganda yake. (K)



SHANGILIO
Yn. 15:16

Aleluya, aleluya,
Ni mimi niliyewachagua ninyi nikawaweka mwende mkazae matunda, na matunda yenu yapate kukaa, asema Bwana.
Aleluya.



INJILI
Mt. 2:20 – 28

Mama yao wana wa Zebedayo alimwendea pamoja na wanawe, akamsujudia, na kumwomba neno. Akamwambia, Wataka nini? Akamwambia, Agiza kwamba hawa wanangu wawili waketi mmoja mkono wako wa kuume, na mmoja mkono wako wa kushoto, katika ufalme wako. Yesu akajibu akasema, Hamjui mnaloliomba. Je! Mwaweza kunywea kikombe nitakachonywea mimi? Wakamwambia, Twaweza. Akawaambia, Hakika mtakinywea kikombe changu; lakini kuketi mkono wangu wa kuume na mkono wangu wa kushoto sina amri kuwapa, bali watapewa waliowekewa tayari na Baba yangu.

Na wale kumi waliposikia, waliwakasirikia ndugu wawili. Lakini Yesu akawaita, akasema, Mwajua ya kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha. Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu yeyote anayetaka kuwa mkubwa kwenu, na awe mtumishi wenu; na mtu yeyote anayetaka kuwa wa kwanza kwenu na awe mtumwa wenu; kama vile Mwana wa Adamu asivyokuja kutumikiwa, bali kutumikia na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengu.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MIZIZI ILIYOJIKITA KWA KRISTO

 


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Kila siku
Ijumaa, 24 Julai, 2026 
Juma la 16 la Mwaka

Yer. 3:14-17
Yer. 31:10-13 (K) 10
Mt 13:18-18


MIZIZI ILIYOJIKITA KWA KRISTO


Injili ya leo inatualika kutafakari juu ya Yesu Kristo kama mpandaji wa neno la Mungu. Yesu anatualika tulisikilize neno la Mungu na kuongozwa nalo katika maisha yetu. Kwa kufanya hivyo mbegu iliyo pandwa mioyoni mwetu itazaa matunda. Mfano wa mpanzi unaonesha nguvu ya Neno la Mungu kwa wale wote wanao lipokea kulisikiliza na kulizamisha ndani mwao. Mfano wa mpanzi unawahusu wakristo wote hasa wale wanaopaswa kuwalisha watu neno la Mungu kama vyombo vya Kristo.

Sisi tunaona wenyewe kati yetu sisi wakristo wapo tunao jifananisha na zile mbegu zilizo anguka njiani, mbegu zilizo anguka kwenye mwamba, na mbegu zilizo pandwa katika udongo mzuri. Wakristo wote ambao hawajapandwa katika udongo mzuri ni wale ambao hawana mizizi. Wanakiri Imani ya Kristo pale tu inapo pokelewa vizuri na watu, wakati mambo ni marahisi. Lakini pale inapotoeka changamot katika kuhubiri Injili na Neno la Mungu, na wakati maisha ya kumfuata Kristo hayana umaarufu, huyu mtu huchagua njia nyingine ya tamaduni Fulani. Hili ni jambo la kweli kabisa katika maisha yetu ya sasa.Tamaduni na ulimwengu vinapingana sana na ukweli wa Imani ya Kristo. Ulimwengu unakuwa maarufu na tena wenye nguvu na kuonekana kama sehemu ya ushindi. Matatizo ya kweli yanatokana na ukosefu wa Wakristo wengi kukosa mizizi ya Imani katika maisha yao ya kila siku.

Cha muhimu kabisa ni kuruhusu hili neno la Mungu lizamishwe ndani kabisa katika udongo wa roho zetu. Hili linapo tokea neno linakuwa na kuwa imara. Na katika ulimwengu wa mawimbi tukiwa kama wakristo tutashinda mawimbi na msuko suko wa dunia. Tutafakari kama tupo tayari kusimama ndani ya Kristo au la. Tuombe Mungu azamishe mizizi ya imani katika mioyo yetu ili tuweze kuwa imara bila kujali ina tugharimu nini.

Sala: Bwana, ninatamani neno lako lizame kabisa katika moyo wangu. Ninatamani kubaki imara katika Imani yangu bila kujali gharama. Ninatamani kuwa na Imani kubwa na katika upendo wangu kwa kila kitu. Yesu, nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2023 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JULAI 24, 2026



MASOMO YA MISA, JULAI 24, 2026
IJUMAA, JUMA LA 16 LA MWAKA

SOMO 1
Yer. 3:14 – 17

Rudini, enyi watoto wenye kuasi, asema Bwana; maana mimi ni mume wenu; nami nitatwaa mtu mmoja wa mji mmoja, na wawili wa jamaa moja, nami nitawaleta hata Sayuni; nami nitawapa ninyi wachungaji wanipendezao moyo wangu, watakaowalisha kwa maarifa na fahamu. Kisha itakuwa mtakapoongezeka na kuwa wengi katika nchi hiyo, asema Bwana, siku zile hawatasema tena, Sanduku la agano la Bwana; wala halitaingia moyoni; wala hayatafanyika hayo tena. Wakati ule watauita Yerusalemu kiti cha enzi cha Bwana; na mataifa yote watakusanyika huko Yerusalemu, kwa ajili ya jina la Bwana; wala hawatakwenda tena kwa ukaidi wa moyo wao mbaya.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Yer. 31:10 – 13 (K) 10

(K) Bwana anatulinda kama mchungaji alindavyo kundi lake.

Lisikieni neno la Bwana, enyi mataifa,
Litangazeni visiwani mbali,
Mkaseme: Aliyemtawanya Israeli atamkusanya,
Na kumlinda kama mchungaji alindavyo kundi lake. (K)

Kwa maana Bwana amemweka huru Yakobo,
Amemkomboa mkononi mwake aliyekuwa hodari kuliko yeye.
Nao watakuja na kuimba katika mlima Sayuni,
Wataukimbilia wema wa Bwana, nafaka, na divai,
Na mafuta, na wachanga wa kondoo na wa ng’ombe. (K)

Ndipo bikira atafurahi katika kucheza,
Na vijana na wazee pamoja, 
Maana nitageuza masikitiko yao kuwa furaha,
Nami nitawafariji
Na kuwafurahisha waache huzuni yao. (K)


SHANGILIO
Mt. 11:25

Aleluya, aleluya,
Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga.
Aleluya.


INJILI
Mt. 13:18 – 23

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Ninyi sikilizeni mfano wa mpanzi. Kila mtu alisikiapo neno la ufalme asielewe nalo, huja yule mwovu, akalinyakua lililopandwa moyoni mwake. Huyo ndiye aliyepandwa moyoni mwake. Huyo ndiye aliyepandwa karibu na njia. Naye aliyepandwa penye miamba, huyo ndiye alisikiaye lile neno, akalipokea mara kwa furaha; lakini hana mizizi ndani yake bali hudumu kwa muda; ikitukia dhiki au udhia kwa ajili ya lile neno, mara huchukizwa, naye aliyepandwa penye miiba, huyo ndiye alisikiaye lile neno; na shughuli za dunia, na udanganyifu wa mali hulisonga lile neno; likawa halizai. Naye aliyepandwa penye udongo mzuri, huyo ndiye alisikiaye lile neno, na kuelewa nalo; yeye ndiye azaaye matunda, huyu mia, na huyu sitini, na huyu thelathini.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MAFUMBO YA UFALME WA MUNGU!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Kila siku
Alhamisi, 23 Julai, 2026, 
Juma la 16 la Mwaka



Yer 2:1-3, 7-8, 12-13
Zab 36:5-10 (K) 9
Mt 13:10-17



MAFUMBO YA UFALME WA MUNGU!


Katika maisha, mara nyingi tunadadisi, vilevile tunashangazwa na fumbo. Pale tunapopoteza hali ya fumbo katika dini ndipo Mungu anakuja kuwa kama wazo tu. Katika nyakati ya Yesu, Mungu amekuwa kama kitu kilichopo akilini mwa watu tu na si mioyoni mwao. Yesu anamnukuu nabii isaya katika injili: “maana mioyo ya watu hawa inakuwa mizito, na kwa masikio yao hawasikii vyema na macho yao wameyafumba.” Aliwaambia wanafunzi wake kwamba si kila mmoja ataelewa mifano. Yesu aliongea hayo kutokana na uzoefu. Alielewa kwamba baadhi yao ambao walisikia mifano yake walikataa kuielewa, si kwamba akilio zao hazikuweza kuelewa, bali, walifunga mioyo yao kwa yale aliyokuwa akisema Yesu. Walikuwa wameweka nia ya kutokuamini.

Mungu huweza kufunua siri za ufalme wake kwa mnyenyekevu na mtu anayemtegemea na kukiri uhitaji wa Mungu na ukweli wake. Mifano ya Yesu itatuangaza sisi kama tukiipokea kwa akili na mioyo radhi na kuwa tayari kukubali itupe changamoto. Neno la Mungu linaweza tu kuota mizizi katika moyo unaokubali na kuamini na kujitoa kwa hiari.

Sala: Bwana nakukaribisha moyoni na akilini mwangu uniangaze, unipe changamoto na unibadilishe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JULAI 23, 2026



MASOMO YA MISA, JULAI 23, 2026
ALHAMISI, JUMA LA 16 LA MWAKA


SOMO 1
Yer. 2:1-3, 7-8, 12-13

Neno la Bwana likanijia, kusema, Enenda ukalie masikioni mwa Yerusalemu, ukisema, Bwana asema hivi, Nakumbuka hisani ya ujana wako, upendo wa wakati wa uposo wako; Jinsi ulivyonifuaata huko jangwani, katika nchi isiyopandwa mbegu. Israeli walikuwa utakatifu kwa Bwana; Malimbuko ya uzao wake; Wote watakaomla watakuwa na hatia; uovu utawajilia; asema Bwana.

Nami nitawatia katika nchi ya shibe, mpate kula matunda yake na mema yake; lakini ninyi mlipoingia katika nchi ile, mliitia unajisi nchi yangu, na urithi wangu mliufanya kuwa chukizo. Makuhani hawakusema, Yuko wapi Bwana? Wala wanasheria hawakunijua; wachungaji nao waliniasi, nao manabii walitoa unabii kwa Baali, wakafuata mambo yasiyofaidia kitu.

Enyi mbingu, staajabuni kwa ajili ya jambo hili, mkaogope sana, na kuwa ukiwa sana, asema Bwana. Kwa maana watu wangu hawa wametenda maovu mawili; wameniacha mimi, niliye chemchemi ya maji ya uzima, wamejichimbia mabirika, mabirika yavunjayo, yasiyoweza kuweka maji.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 36:5 – 10 (K) 9

(K) Kwako Bwana iko chemchemi ya uzima.

Ee Bwana, fadhili zako zafika hata mbinguni,
Uaminifu wako hata mawinguni.
Haki yako ni kama milimo ya Mungu,
Hukumu zako ni vilindi vikuu. (K)

Ee Bwana, unawaokoa wanadamu na wanyama.
Ee Mungu, jinsi zilivyo na thamani fadhila zako! Wanadamu huukimbilia uvuli wa mbawa zako.
Watashibishwa kwa unono wa nyumba yako,
Nawe utawanywesha mto wa furaha zako. (K)

Maana kwako Wewe iko chemchemi ya uzima,
Katika nuru yako tutaona nuru.
Uwadumishie wakujuao fadhili zako,
Na wanyofu wa moyo uaminifu wako. (K)



SHANGILIO
Zab. 147:12, 15

Aleluya, aleluya,
Msifu Bwana, ee Yerusalemu, huipeleka amri yake juu ya nchi.
Aleluya.



INJILI
Mt. 13:10 – 17

Wanafunzi walimwambia Yesu, Kwa nini wasema nao kwa mifano? Akajibu akawaambia, Ninyi mmejaliwa kuzijua siri za ufalme wa mbinguni, bali wao hawakujaliwa. Kwa maana yeyote mwenye kitu atapewa, naye atazidishiwa tele; lakini yeyote asiye na kitu, hata kile alichonacho hata kile alicho nancho atanyang’anywa. Kwa sababu hii nasema nao kwa mifano kwa kuwa wakitazama hawaoni, na wakisikia hawasikii, wala kuelewa. Na neno la nabii Isaya linatimia kwao, likisema, Kusikia mtasikia, wala hamtaelewa; kutazama mtatazama, wala hamtaona. Maana mioyo ya watu hawa imekuwa mizito, na kwa masikio yao hawasikii vema, na macho yao wameyafumba; wasije wakaona  kwa macho yao, wakasikia kwa masikio yao, wakaelewa kwa mioyo yao, wakaongoka, nikawaponya.

Lakini, heri macho yenu, kwa kuwa yanaona; na masikio yenu, kwa kuwa yanasikia. Kwa maana, amin, nawaambia, Manabii wengi na wenye haki walitamani kuyaona mnayoyaona ninyi, wasiyaone na kuyasikia mnayoyasikia ninyi, wasiyasikie.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 2026 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUZAMA KATIKA KRISTO!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatano, Julai 22, 2026, 
Juma la 16 la Mwaka

Sikukuu ya Mt. Maria Magdalena


Wim 3:1-4 or 2Kor 5:14-17; 
Zab 63: 1-5, 7-8; 
Yn 20:1-2, 11-18.


KUZAMA KATIKA KRISTO!

Maria Magdalena anachukuliwa kama mwanamke muhimu wa pili katika Agano Jipya baada ya Bikira Maria, Mama wa Yesu. Alisafiri na Yesu katika maisha yake ya utume na alishuhudia matukio mawili ya katika maisha ya Yesu, Mateso na ufufuko. Injili inamuelezea kama Mwanamke jasiri aliye simama na Yesu wakati wa mateso, kifo.

Maria Mgadalene ni mfano wa kweli na ulio kamili katika kuinjilisha, Mwinjilishaji wa ujumbe kamili wa furaha ya Pasaka. Mwanamke huyu “ambaye alimpenda sana Bwana na Bwana alimpenda”. Alikuwa ni mmoja wapo wa wafuasi waliomfuata Yesu, alimsindikiza hata katika safari yake ya mateso na hata bustanini alipokutana naye, alikuwa ni shuhuda wa kwanza wa “huruma ya Kimungu”. Injili ya Yohane inatuambia kuwa Maria Magdalena alilia kwasababu hakuona mwili wa Yesu (Yn 20:11); na Yesu alikuwa na huruma kwake kwa kujionesha kwake kama Mwalimu wake, na kugeuza machozi yake kuwa furaha ya Pasaka.

Alikuwa na heshima ya kuwa shuhuda wa kwanza wa ufufuko wa Yesu, wa kwanza kuona kaburi li wazi na wa kwanza kusikia habari za ufufuko. Yesu anaonesha kujali kwa namna ya pekee kwa huyu mwananmke na kumuonesha huyu mwanamke huruma ya pekee kwasababu mwanamke huyu alionesha mapendo kwa Kristo kwa kumtafuta katika bustani na hata katika mateso. Katika hali hii tunaweza kulinganisha mwanamke aliye anguka katika bustani ya Edeni na mwanamke huyu katika bustani wakati wa ufufuko. Wakwanza alileta kifo kwa mwanandamu na wa pili anatangaza uzima akiwa kaburini.

Katika bustani ya ufufuko Bwana wetu alimwambia Maria “usinishike” (Yn 20:17). Huu ni mwaliko wa kuingia katika Imani inayo zidi mambo yanayo onekana na zaidi ya akili ya mwanadamu baada ya kukutana na mafumbo ya Kimungu ambayo hayatangazwi kwa Maria tu bali kwa Kanisa zima. Huu ni mwaliko kwa kila mfuasi wa Yesu aache kutafuta utukufu binafsi au utukufu wa dunia hii, lakini kwa Imani kumtafuta Mungu anaye ishi na mfufuka.

Alikuwa shuhuda wa kwanza wakumuona Bwana mfufuka, alikuwa pia wa kwanza kutoa ushuhuda kwa mitume wake. Alitimiza amri ya Bwana mfufuka: “nenda ukawaambie ndugu zangu, napaa kwa Baba yangu na Baba yenu, kwa Mungu wangu na Mungu wenu”. Maria Magdalena aliondoka na kutangaza kwamba amemuona Bwana na kwamba amemuambia mambo haya (Yn 20:17-18). Na hivyo, akawa muinjilishaji, mjumbe anaye hubiri habari njema za ufufuko wa Bwana. Alitangaza kwa mitume kitu ambacho wangekuja kukitangaza baadae katika ulimwengu wote. Na hivyo anaitwa “Mtume kwa Mitume”. Yeye ni shuhuda wa Yesu mfufuka na ametangaza ujumbe huu kama Mitume wengine walivyofanya. Utume huu wa wamanamke huyu ni mfano kamili wa wanawake wote katika kanisa la sasa!

Tafakari tamaa ya Bwana wetu kwamba sisi siku moja tufurahi naye mbinguni. Tumsikie akituambia “Napaa kwa Baba na kualika kujiunga nami kwa moyo wako wote. Nikaribishe ndani mwako na niruhusu mimi niweze kuungana nawe. Ninakupenda Bwana na ninatamani kuwa mmoja pamoja nawe. Bwana niruhusu niingie moyoni mwako nawe uwe moyoni mwangu.

Sala: Bwana, ninataka kuzama ndani yako. Ninatamani kuungana nawe katika hali zote. Njoo uishi moyoni mwangu na nifanye niwe mmoja nawe. Yesu, nakutumainia wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JULAI 22, 2026




MASOMO YA MISA, JUMATANO, JULAI 22, 2026
JUMA LA 16 LA MWAKA


SIKUKUU YA MT. MARIA MAGDALENA


SOMO 1
Wim. 3 :1-4

Usiku kitandani nalimtafuta mpendwa wa nafsi yangu, Nalimtafuta, nisimpate. Nikasema, Haya, niondoke nizunguke mjini, Katika njia zake na viwanjani, Nimtafute mpendwa wa nafsi yangu. Nikamtafuta, nisimpate. Walinzi wazungukao mjini waliniona; Je! mmemwona mpendwa wa nafsi yangu? Kitambo kidogo tu nikiisha kuwaondokea, Nikamwona mpendwa wa nafsi yangu.

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu

Au

SOMO 1 
2 Kor. 5 :14-17

Upendo wa Kristo watubidisha; maana tumehukumu hivi, ya kwamba mmoja alikufa kwa ajili ya wote, basi walikufa wote; tena alikufa kwa ajili ya wote, ili walio hai wasiwe hai tena kwa ajili ya nafsi zao wenyewe, bali kwa ajili yake yeye aliyekufa akafufuka kwa ajili yao.

Hata imekuwa, sisi tangu sasa hatumjui mtu awaye yote kwa jinsi ya mwili. Ingawa sisi tumemtambua Kristo kwa jinsi ya mwili, lakini sasa hatumtambui hivi tena, Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita; tazama! yamekuwa mapya.

Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu


WIMBO WA KATIKATI
Zab 63: 1-5, 7-8 (K) 1

(K) Nafsi yangu inakuonea kiu, Ee Bwana.

Ee Mungu, Mungu wangu, nitakutafuta mapema, 
Nafsi yangu inakuonea kiu,
Mwili wangu wakuonea shauku,
Katika nchi kame na uchovu, isiyo na maji. (K)

Ndivyo nilivyokutazama katika patakatifu,
Nizione nguvu zako na utukufu wako.
Maana fadhili zako ni njema kuliko uhai;
Midomo yangu itakusifu. (K)

Ndivyo nitakavyokubariki maadamu ni hai;
Kwa jina lako nitaiinua mikono yangu.
Nafsi yangu itakinai kama kushiba mafuta na vinono; 
Kinywa changu kitakusifu kwa midomo ya furaha. (K)

Maana Wewe umekuwa msaada wangu,
Na uvulini mwa mbawa zako nitashangilia.
Nafsi yangu inakuandama sana;
Mkono wako wa kuume unanitegemeza. (K)


SHANGILIO

Aleluya, aleluya, 
Maria tuambie: sema uliyoona njiani. 
Kaburi lilimfadhi yule aliye Mzima; 
Niliona utukufu wa Kristu alipokuwa akifufuka. 
Aleluya.


INJILI 
Yn. 20 :1-2, 11-18

Siku ya kwanza ya juma Mariamu Magdalena alikwenda kaburini alfajiri, kungali giza bado; akaliona lile jiwe limeondolewa kaburini. Basi akaenda mbio, akafika kwa Simoni Petro na kwa yule mwanafunzi mwingine ambaye Yesu alimpenda, akawaambia, wamemwondoa Bwana kaburini, wala hatujui walikomweka

Lakini Mariamu alikuwa akisimama karibu na kaburi, nje yake, analia. Basi akilia hivi, aliinama na kuchungulia ndani ya kaburi. Akaona malaika wawili, wenye mavazi meupe, wameketi, mmoja kichwani na mmoja miguuni, hapo ulipolazwa mwili wake Yesu. Nao wakamwambia, Mama, unalilia nini? Akawaambia, Kwa sababu wamemwondoa Bwana wangu, wala mimi sijui walikomweka. Naye akiisha kusema hayo, akageuka nyuma, akamwona Yesu amesimama, asijue ya kuwa ni Yesu. Yesu akamwambia, Mama unalilia nini? Unamtafuta nani? Naye, huku akidhania ya kuwa ni mtunza bustani, akamwambia, Bwana, ikiwa umemchukua wewe, uniambie ulipomweka, nami nitamwondoa.

Yesu akamwambia, Mariamu. Yeye akageuka, akamwambia kwa Kiebrania, Raboni! (yaani, Mwalimu wangu). Yesu akamwambia. Usinishike; kwa maana sijapaa kwenda kwa Baba. Lakini enenda kwa ndugu zangu ukawaambie, Ninapaa kwenda kwa Baba yangu naye ni Baba yenu, kwa Mungu wangu naye ni Mungu wenu. Mariamu Magdalene akaenda, akawapasha wanafunzi habari ya kwamba, Nimemwona Bwana, na ya kwamba amemwambia hayo.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 2026 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.