Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

CHAGUA KULINDA MAISHA!

 


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Tafakari ya kila siku

Ijumaa, Februari 6, 2026,

Juma la 4 la Mwaka wa Kanisa

 

YbS 47: 2-11

Zab 18: 31 47, 50, 51

Mk 6: 14-29.

 

CHAGUA KULINDA MAISHA!

Leo tunaona mwisho na unyong'onyevu wa mwenye haki na asiyeogopa nabii wa kweli Yohani Mbatizaji katika mikono ya mtawala dhalimu, aliye jazwa na tamaa, na picha ya utukufu dhalimu wa uongo wa hadhi na heshima! Herode alifanya makosa makubwa matatu, ambayo mtawala mwenye kuwajibika hapaswi kufanya hivyo. Kwanza, yeye alionesha mfano mbaya, kwa kumuoa mke wa nduguye. Pili, yeye alifanya ahadi ya bila kufikiri kwa yule msichana aliyecheza. Tatu, alihofu watu watasema nini na kujaribu kuokoa heshima yake ya uongo, aliamuru mauaji ya mtu mwenye haki asiye na hatiya. Yohane Mbatizaji.

Hakuna mtu mwenye haki ya kucheza na maisha ya mtu mwingine, iwe katika gereza au katika mitaa au akiwa tumboni. Na waliopo katika madaraka, wana wajibu wa kulinda maisha, na wanalazimika kufikiri mara mbili na kufanya hakika kwamba maisha hayapo hatarini.

Tutafakari leo, kuhusu hali zetu za kila siku za maisha. Je, unapatwa na hasira na kujifanya kuielekeza kwa wengine ambao hawastahili? Tutafakari juu ya tabia hizi na tuangalie kwa undani chanzo chake. Kama ukiona chanzo cha tabia hii ambayo sio nzuri pengine ni kwasababu ya dhambi yako mwenyewe ya maisha yako, tubu kwa hakika na kuimaliza ili Bwana wetu akuweke huru kutoka katika malipo yake.

Mara moja nyuki, ambaye mwenendo wake ulikuwa mzuri na kama asali anayofanya, alikwenda kwa Mungu na kumuomba mafanikio akisema. "Naomba ninapo muuma mtu afe hapo hapo." Mungu akashtuka. Mafanikio mara moja yakabadilishwa na kuwa laana. "Mungu akasema ni sawa. Lakini yule atakayeuma ndiye atakayekufa sio yule atakayeumwa” "Mungu anapenda maisha ya endelee, sio yaharibiwe. 

Sala: Bwana, natubu dhambi zangu zote. Ninasali ili niweze kuziona dhambi zangu kwa uaminifu kabisa na kwa kweli. Ninapo ona dhambi zangu, nisaidie niweze kuziungama niweze kuwa huru na sio aliye elemewa na mzigo wa dhambi. Bwana, ninaomba niyalinde maisha ya aina zote. Ninaomba nijitahidi kuwa mjumbe wa maisha. Yesu nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com 

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 6, 2026

 


MASOMO YA MISA, FEBRUARI 6, 2026

IJUMAA YA 4 MWAKA

KUMBUKUMBU YA WAT. PAULO MIKI NA WENZAKE (Shahidi)


SOMO 1

Ybs. 47:2-11


Kama mafuta yalivyotengwa na kafara ya amani, vivyo hivyo Daudi alitengwa na wana wa Israeli. Naye alicheza pamoja na samba kana kwamba ni wana-mbuzi, pia pamoja na dubu kana kwamba ni wana-kondoo wa kundi.


Je! Hakumwua jitu katika ujana wake, Akawaondolea watu lawama; Alipouinua mkono wake na jiwe la teo, Akayashusha majivuno ya Goliathi? Kwa maana alimwita Aliye juu; Na Yeye akaitia nguvu yamini yake; Ili amwue shujaa hodari wa vita; Ili aiinue pembe ya watu wake.

Kwa hiyo binti za watu wakamtukuza wakiimbiana, na kumheshimu alivyoua makumi elfu yake; naye alipokwisha kuivaa taji ya utukufu, alipigana na adui na kuwashinda pande zote; akajenga maboma yake kati ya Wafilisti, akaivunja pembe yao vipande vipande, hata siku hii ya leo.


Katika kila kazi yake

Daudi alimshukuru Mungu Aliye juu kwa maneno matukufu; na kwa moyo wake wote akampenda Mola wake, akamhimidi kila siku daima. Pia akaweka waimbaji mbele ya madhabahu, ili watoe sauti tamu katika kuimba kwao.


Akauongeza uzuri wa sikukuu, akaziratibisha nyakati katika ukamilifu; pindi walipolihimidi jina takatifu la Bwana, hata patakatifu pakavuma sauti tokea asubuhi na mapema. Naye Bwana akamwondolea dhambi zake, akaiinua pembe yake hata milele; akampa agano la ufalme, na kiti kitakatifu cha enzi katika Israeli.


Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI

Zab. 18:30, 46, 49-50 (K) 46


(K) Atukuzwe Mungu wa wokovu wangu.


Mungu njia yake ni kamilifu,

Ahadi ya Bwana imehakikishwa,

Yeye ndiye ngao yao wote wanaomkimbilia. (K)


Bwana ndiye aliye hai, na ahimidiwe mwamba wangu,

Na atukuzwe Mungu wa wokovu wangu.

Bwana, nitakushukuru kati ya mataifa.

Nami nitaliimbia jina lako. (K)


Ampa mfalme wake wokovu mkuu,

Amfanyia fadhili masihi wake,

Daudi na mzao wake hata milele. (K)


SHANGILIO

Lk. 8:15


Aleluya, aleluya,

Heri wale ambao kwa unyofu na wema wa moyo hulishika neno la Mungu, kasha huzaa matunda kwa kuvumilia.

Aleluya.


INJILI

Mk. 6:14-29


Mfalme Herode alisikia habari; kwa maana jina lake lilikuwa kutangaa, akasema, Yohane Mbatizaji amefufuka katika wafu, na kwa hiyo nguvu hizi zinatenda kazi ndani yake. Wengine walisema, Ni Eliya. Wengine walisema, Huyu ni nabii, au ni kama mmoja wa manabii. Lakini Herode aliposikia, alisema, Yohane mwenyewe alikuwa amefufuka.

Kwa maana Herode mwenyewe alikuwa ametuma watu, akamkamata Yohane, akamfunga gerezani, kwa ajili ya Herodia, mkewe Filipo ndugu yake; kwa kuwa amemwoa; kwa sababu Yohane alimwambia Herode, Si halali kwako kuwa na mke wa nduguyo. Naye yule Herodia akawa akimvizia, akataka kumwua, asipate. Maana Herode alimwogopa Yohane; akimjua kuwa ni mtu wa haki, mtakatifu, akamlinda; na alipokwisha kumsikiliza alifadhaika sana; naye alikuwa akimsikiliza kwa furaha.


Hata ilipotokea siku ya kufaa, na Herode, sikukuu ya kuzaliwa kwake, alipowafanyia karamu wakubwa wake, na majemadari, na watu wenye cheo wa Galilaya; ndipo binti yake yule Herodia alipoingia, akacheza, akampendeza Herode na wale walioketi pamoja naye karamuni. Mfalme akamwambia yule kijana, Niombe lolote utakalo nitakupa, hata nusu ya ufalme wangu. Basi akatoka, akamwuliza mamaye, Niombe nini? Naye akasema, Kichwa cha Yohane Mbatizaji. Mara akaingia kwa haraka mbele ya mfalme, akaomba akisema, Nataka unipe sasa hivi katika kombe kichwa cha Yohane Mbatizaji.


Mfalme akafanya huzuni sana, lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya hao walioketi karamuni, hakutaka kumkatalia. Mara mfalme akatuma askari, akaamuru kuleta kichwa chake. Basi, akaenda, akamkata kichwa mle gerezani, akakileta kichwa chake katika kombe, akampa yule kijana, naye yule kijana akampa mamaye.


Wanafunzi wake waliposikia habari, walikwenda, wakauchukua mwili wake, wakauzika kaburini.


Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

SAFARI ISIYO HITAJI MIZIGO




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Februari 5, 2026

JUMA LA 4 LA MWAKA 

2 Falm
Nya 29:10-12
Mk 6:7-13


SAFARI ISIYO HITAJI MIZIGO


Tunapo safari mara nyingi katika maisha yetu mara nyingi huwa tunabeba mizigo. Lakini mizigo mara nyingi inatufanya tusiwe wepesi sana katika kuendelea na safari yetu bila usumbufu. Ndio hivyo Yesu anawaonya mitume wake wasibebe mizigo wala kushikamana na vitu katatika safari yao ya utume. Kilicho cha muhimu ni kuwa waminifu kwa Mungu. Kutokufungamana na mali au malimwengu ambayo yatakufanya ushindwe kuhubiri neno lake vizuri.

Ndugu yangu jiulize ni jambo gani linalo kufunga ushindwe kuhubiri neno la Mungu vizuri? Je ni pesa? Au mali? Ni mzigo gani unao chelewesha safari yako ya kumtangaza Yesu? Jiulize na muombe Yesu akusaidie kuutua na kuanza safari Upya kwa maisha ya neema.

Sala: Bwana nakuomba unisaidie niweze kushika kiaminifu wito huu wa kutangaza neno lako kama Mkristo. Nisaidie nikushuhudie daima. Amina



Copyright ©2013-2024 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 5, 2026




MASOMO YA MISA, FEBRUARI 5, 2026
ALHAMISI YA JUMA LA 4 LA MWAKA

Kumbukumbu ya Mt Agatha


SOMO 1
1 Falm. 2:1-4, 10-12

Siku ya kufa kwake Daudi ilikaribia, akamwusia Sulemani mwanawe, akasema, Mimi naenda njia ya ulimwengu wote; basi uwe hodari, ujionyeshe kuwa mwanamume; uyashike mausia ya Bwana, Mungu wako, uende katika njia zake, uzishike sheria zake, na amri zake, na hukumu zake, na shuhuda zake, sawasawa na ilivyoandikwa katika torati ya Musa, upate kufanikiwa katika kila ufanyalo, na kila utazamako; ili Bwana afanye imara neno lake alilonena kwa habari yangu, akisema, Ikiwa watoto wako wataiangalia njia yao, wakenda mbele zangu kwa kweli, kwa moyo wao wote, na kwa roho yao yote, (akasema) hutakosa mtu katika kiti cha enzi cha Israeli.

Basi Daudi akalala na babaze, akazikwa mjini mwa Daudi. Na siku alizotawala Daudi juu ya Israeli zilikuwa miaka arobaini; huko Hebraoni alitawala miaka saba, na katika Yerusalemu akatawala miaka thelathini na mitatu. 

Basi Sulemani akaketi katika kiti cha enzi cha Daudi baba yake; na ufalme wake ukawa imara sana.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Nya. 29:10-12 (K) 12

(K) Nawe watawala juu ya vyote, Ee Bwana.

Uhimidiwe, ee Bwana, Mungu wa Israeli baba yetu milele na milele.
Ee Bwana, ukuu ni wako, na uweza, na utukufu,
Na kushinda, na enzi;
Maana vitu vyote vilivyo mbinguni
Na duniani ni vyako. (K)

Ufalme ni wako, Ee Bwana, nawe umetukuzwa,
U mkuu juu ya vitu vyote.
Utajiri na heshima hutoka kwako wewe. (K)

Nawe watawala juu ya vyote;
Na mkononi mwako mna uweza na nguvu;
Mkononi mwako mna kuwatukuza 
Na kuwawezesha wote. (K)


SHANGILIO
Mk. 1:15

Aleluya, aleluya,
Ufalme wa Mungu umekaribia, tubuni na kuiamini Injili.
Aleluya.


INJILI
Mk. 6:7-13

Siku ile Yesu aliwaita wale Thenashara, akaanza kuwatuma wawili wawili, akawapa amri juu ya pepo wachafu; akawakataza wasichukue kitu cha njiani isipokuwa fimbo tu; wala mkate, wala mkoba, wala pesa za bindoni; lakini wajifungie viatu, akasema, Msivae kanzu mbili. Akawaambia, Mahali popote mtakapoingia katika nyumba, kaeni humo hata mtakapotoka mahali pale. Na mahali popote wasipowakaribisha ninyi wala kuwasikia, mtokapo huko, yakung’uteni mavumbi yaliyo chini ya miguu yenu, kuwa ushuhuda kwao. Wakatoka, wakahubiri kwamba watu watubu. Wakatoa pepo wengi, wakapaka mafuta watu wengi waliokuwa wagonjwa, wakawapoza.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MAMBO YA KAWAIDA YANATUFANYA TUWE TAYARI KUPOKEA YASIO YA KAWAIDA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Februari 4, 2026
JUMA LA 4 LA MWAKA

2Sam 24:2.9-17
Zab 32:1-2.5-7
Mk 6: 1-6.


MAMBO YA KAWAIDA YANATUFANYA TUWE TAYARI KUPOKEA YASIO YA KAWAIDA!


Watu waliokuwa wanamfahamu Yesu tangu akiwa kijana wanashangazwa na hekima na mambo makuu anayotenda. Walishangazwa na yote aliokuwa akisema na kutenda. Walikuwa wakimfahamu tangu alivyokuwa anakuwa, walifahamu wazazi wake na ndugu wengine, na kwa mshangao wanashangaa inawezekanaje huyu jirani yao wanaye mfahamu inawezekeanaje awavutie watu hivi na kuwa na hekima ya hali ya juu namna hii na matendo makuu. Ni wazi kwamba Yesu aliishi maisha ya kawaida kabla ya kuanza utume wake. Kiasi kwamba watu wake wa karibu hawakufahamu kwamba alikuwa mtu muhimu sana. Hili ni wazi kwasababu baada ya Yesu kuanza utume wake wa hadharani watu wake wanashangazwa na matendo yake makuu. Hawakutegemea kabisa mambo kama haya kutoka kwa Yesu wa “Nazarethi”. 

Je, sisi tunaweza kupata nini kutokana na jambo hili? Kwanza kabisa tutambue , mara nyingi mapenzi ya Mungu kwetu yanatuita kuishi maisha ya “kawaida” kabisa. Ni rahisi kuwaza kwamba tunapaswa tutende mambo makuu kwa ajili ya Mungu. Lakini vitu vikubwa ambavyo Mungu anatuitia nikuishi maisha ya kila siku ya kawaida vizuri. Hakuna wasiwasi kwamba wakati Yesu alivyokuwa akiishi maisha ya kawaida alikuwa anaishi maisha ya fadhila. Haikuwa mpango wa Mungu kwanza fadhila zake zianze kujulikana kwanza kwa wote kipindi hicho. Pili, tunaona wazi kwamba kuna wakati utume wake ulibadilika. Mapenzi ya Baba, katika maisha yake, alianza utume wake hadharani na watu wakamuona. Na wakati hili lilivyo anza watu walitambua.

Ukweli huu pia ni dhahiri pia kwetu sisi. Watu wengine wameitwa maisha ya kawaida katika hali ya kawaida kabisa. Tambua kuwa muda huu ndio muda ulioitwa ili kukuza fadhila zako, fanya mambo ya kawaida kabisa vizuri, na furahia hali ya ukimya ya maisha ya kawaida. Pia tutambue kuwa kuna uwezekano Mungu akatuita katika maisha hayo ya kawaida na kuanza kumshuhudia mbele ya watu au umati. Ufunguo ni kwamba sisi tunapaswa kumsikiliza na kuitambua sauti yake katika hali ya utulivu. Kuwa tayari na penda yeye akutumie kwa jinsi alivyopenda kwa mapenzi yake ya Kimungu.

Leo tutafakari, juu ya mapenzi ya Mungu katika maisha yetu sasa. Anataka nini kutoka kwetu? Je, anatuita kutoka katika hali yetu ya kawaida ili tuweze kuishi maisha ya kumshudia yeye mbele za watu? Au anatuita sasa tuishi maisha ya kawaida katika hali ya ukimya ya kawaida na kupalilia fadhila kwanza? Furahia mapenzi yake kwa jinsi atakavyo penda uwe na kumbatia hilo kwa moyo wote.

Sala: Bwana, nakushukuru kwa mpango wako kamili katika maisha yangu. Ninakushukuru kwa hali mbali mbali ulizoniita ili nikutumikie. Nisaidie daima niweze kuwa wazi katika mapenzi yako na daima niseme “Ndio” kwako, bila kujali unataka nifanye nini. Yesu nakuamini wewe. Amina.


.Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 4, 2026



MASOMO YA MISA, FEBRUARI 
4, 2026
JUMATANO YA JUMA LA 4 LA MWAKA


SOMO 1
2 Sam. 24:2, 9-17

Mfalme Daudi alimwambia Yoabu, jemadari wa jeshi la askari, waliokuwa pamoja naye, Zunguka sasa katikati ya kabila zote za Israeli, tangu Dani mpaka Beer-sheba, mkawahesabu watu, nipate kujua jumla ya hao watu.

Naye Yoabu akamtolea mfalme jumla ya hesabu ya watu; nao walikuwa wa Israeli mashujaa wenye kufuta panga mia nane elfu; nao wa Yuda walikuwa watu mia tano elfu.

Ndipo moyo wake Daudi ukamchoma baada ya kuwahesabu hao watu. Naye Daudi akamwambia Bwana, Nimekosa sana kwa haya niliyoyafanya lakini sasa, Ee Bwana, nakusihi uuondolee mbali uovu wa mtumishi wako; kwani nimefanya upumbavu kabisa. Na Daudi alipoondoka asubuhi, neno la Bwana likamjia nabii Gadi, mwonaji wake Daudi, kusema, Nenda, ukanene na Daudi, Bwana asema hivi, Nakuwekea mambo matatu; katika haya uchague moja, nikutendee hilo.

Basi Gadi akamwendea Daudi, akamweleza akamwambia, Basi, miaka saba ya njaa ikujie katika nchi yako? Au miezi mitatu ukimbie mbele ya adui zako, huku wakikufuatia? Au siku tatu iwe tauni katika nchi yako? Fanya shauri sasa, ufikiri, ni jawabu gani nimrudishie yeye aliyenituma. Naye daudi akamwambia Gadi, Nimeingia katika mashaka sana; basi sasa na tuanguke katika mkono wa Bwana; kwa kuwa rehema zake ni nyingi; wala nisianguke katika mkono wa wanadamu.

Basi Bwana akawaletea Israeli tauni tangu asubuhi hata wakati ulioamriwa; nao wakafa watu toka Dani mpaka Beer-sheba sabini elfu. Lakini huyo malaika aliponyosha mkono wake kuelekea Yerusalemu ili auharibu, Bwana akaghairi katika mabaya, akamwambia huyo malaika mwenye kuwaharibu watu, Yatosha, sasa ulegeze mkono wako. Naye yule malaika wa Bwana alikuwako karibu na kiwanja cha kupuria cha Arauna, Myebusi. Daudi, alipomwona malaika aliyewapiga watu, akanena na Bwana, akasema, Tazama, ni mimi niliyekosa, ni mimi niliyepotoka; lakini kondoo hawa, wamefanya nini? Mkono wako na uwe juu yangu, na juu ya nyumba ya baba yangu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 32:1-2, 5-7 (K) 5

(K) Ee Bwana, unisamehe upotovu wa dhambi yangu.

Heri aliyesamehewa dhambi,
Na kusitiriwa makosa yake.
Heri Bwana asiyemhesabia upotovu,
Ambaye rohoni mwake hamna hila. (K)

Nakujulisha dhambi yangu,
Wala sikuuficha upotovu wangu.
Nalisema, Nitayakiri maasi yangu kwa Bwana,
Nawe ukanisamehe upotovu wa dhambi yangu. (K)

Kwa hiyo kila mtu mtauwa akuombe wakati
Unapopatikana.
Hakika maji makuu yafurikapo,
Hayatamfikia yeye. (K)

Ndiwe sitara yangu, utanihifadhi na mateso,
Utanizungusha nyimbo za wokovu. (K)


SHANGILIO
Yn. 10:27

Aleluya, aleluya,
Kondoo wangu waisikia sauti yangu, asema Bwana, nami nawajua, nao wanifuata.
Aleluya.


INJILI
Mk. 6:1-6

Yesu alitoka huko, akafika mpaka nchi ya kwao, wanafunzi wake wakamfuata. Na ilipokuwa sabato, alianza kufundisha katika sinagogi; wengi waliposikia wakashangaa, wakisema, Huyu ameyapata wapi haya? Na, ni hekima gani hii aliyopewa huyu? Na, ni nini miujiza hii mikubwa inayotendeka kwa mikono yake? Huyu si yule seremala, mwana wa Mariamu, na ndugu yao Yakobo, na Yose, na Yuda, na Simoni? Na maumbu yake hawapo hapa petu? Wakajikwaa kwake. Yesu akawaambia, Nabii hakosi heshima, isipokuwa katika nchi yake mwenyewe, na kwa jaama zake, na nyumbani mwake. Wala hakuweza kufanya mwujiza wowote huko; isipokuwa aliweka mikono yake juu ya wagonjwa wachache, akawaponya. Akastaajabu kwa sababu ya kutokuamini kwao.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

IMANI YA HALI YA JUU!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
FEBRUARI 3, 2026
JUMA LA 4 LA MWAKA

2Sam 18:9-10,14,24-25,30 -- 19:1-3
Zab 86:1-6
Mk 5: 21-43


IMANI YA HALI YA JUU!


Katika Injili tunamuona Mwanamke aliyeteseka kwa muda wa miaka kumi na mbili kutokwa na damu. Amejaribu kutibu ugonjwa wake kwa kupitia madaktari mbali mbali na kupoteza karibu kila kitu alichokuwa nacho ili apone, lakini kwa huzuni hakufanikiwa. Inaweza kuwa kweli kwamba Mungu aliruhusu ateseke kwa miaka yote ili aweze kumpa hii nafasi ya pekee ya kudhihirisha Imani yake ili wote waweze kuiona. 

“Kama nikigusa pindo la vazi lake tu..” je alitambuaje kwamba atapona? Ni kitu ghani kilicho mwongoza mpaka awe na uhakika wa namna hii? Kwanini, baada ya kupoteza miaka yote kumi na mbili na madaktari mbali mbali na sasa anatambua sasa anaye mhitaji ni Yesu, tena aguse nguo yake apone? Jibu ni rahisi. Ni kwasababu ya zawadi ya Imani yake.

Maelezo haya kuhusu Imani yake yanafunua kwamba Imani ni zawadi ya akili ya hali ya juu ambayo ni Mungu mwenyewe aweza kuifunua. Kwa maneno mengnie, alitambua kwamba atapona, na akili ya Imani hii kwamba atapona ilikuja kwake kwa kupewa na Mungu. Baada ya kupewa alihitajika kuifanyia kazi, kwa kufanya hivyo anatoa ushuhuda wa ajabu kwao wote wanaosoma ujumbee huu siku zote katika Injili. Maisha yake, na yote aliopitia yanapaswa yatupe changamoto tutambue kwamba Mungu anaongea kwa ukweli halisi nasi, kama tutamsikiliza. Kila mara anaongea na kufunua undani wa upendo wake kwetu sisi, akituita tuingie katika maisha ya Imani ya hali ya juu. Anataka Imani yetu isiwe tu msingi wa maisha yetu, bali iwe ushuhuda wa nguvu kwa wengine. 
Mwanamke huyu alitambua kuwa Mungu atamponya na akamruhusu aongee naye. Sisi nasi tutafakari kuhusu kusikiliza kwa makini sauti ya Mungu ndani mwetu na kujaribu kuwa wazi kwenye Imani kamili ya ndani kama alivyofanya huyu mwanamke. 

Sala: Bwana, nakupenda na natamani kukusikia wewe ukiongea na mimi kila siku. Naomba uongeze Imani yangu ili niweze kukufahamu wewe na mapenzi yako katika maisha yangu. Bwana, nitumie mimi kama upendavyo niweze kuwa shuhuda wa Imani kwa wengine. Yesu, nakutumaini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, 3 FEBRUARI 2026



MASOMO YA MISA, 3 FEBRUARI 2026
JUMANNE LA JUMA LA 4 YA MWAKA


SOMO 1
2Sam. 18:9-10, 14, 24-25, 30 – 19:3

Kwa bahati Absalomu alikutana na watumishi wa Daudi. Naye Absalomu alikuwa amepanda nyumba wake, na yule nyumbu akapita chini ya matawi manene ya mwaloni mkubwa, hata kichwa chake kikakwama katika mwaloni huo, akanyakuliwa juu kati ya mbingu na nchi; na yule nyumbu aliyekuwa chini yake akaenda mbele. Basi mtu mmoja akaona hayo, akaenda akamwambia Yoabu, akasema, Tazama, mimi nalimwona Absalomu ametundikwa katika mwaloni. Yoabu akachukua vyemba vitatu mkononi mwake, akamchoma Absalomu moyoni, alipokuwa akali hai katikati ya ule mwaloni.

Basi Daudi alikuwa ameketi kati ya malango mawili; mlinzi akapanda juu hata dari ya lile lango hata ukutani, akainua macho yake, akaangalia, na tazama, mtu anakuja mbio peke yake. Mlinzi akalia, akamwambia mfalme, Naye mfalme akasema, Kama yup eke yake, ana habari kinywani mwake. Akaja mbio, akakaribia. Naye mfalme akasema, Geuka, usimame hapa, Akageuka, akasimama.

Na tazama, yule Mkushi akafika; Mkushi akasema, Nina habari kwa bwana wangu mfalme; kwa maana Bwana amekulipizia kisasi leo juu ya hao wote walioinuka kupigana nawe. Naye mfalme akamwambia yule Mkushi, Yule kijana, Absalomu, je! Yu salama? Yule Mkushi akajibu, Adui za bwana wangu mfalme, na wote wainukao ili kukudhuru, na wawe kama alivyo yule kijana.

Naye mfalme akataabika sana, akapanda juu, akaingia kile chumba kilichokuwa juu ya lango, akalia; na katika kwenda kwake alisema hivi, Mwanangu Absalomu! Ee mwanangu! Mwangu Absalomu! Laity ningalikufa badala yako, Absalomu, mwanangu, mwanangu!

Kisha Yoabu akaambiwa, Angalia, mfalme anamlilia Absalomu na kumwomboleza. Na kushinda kwao vitani siku ile kukageuzwa kuwa maombolezo kwa watu wote; maana watu walisikia siku ule ya kwamba, Mfalme anahuzunika kwa ajili ya mwanawe. Watu wakajificha siku ile, wakaingia mjini kama vile watu waonao fedheha wajifichavyo, hapo wakimbiapo vitani.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 86:1-6 (K) 1

(K) Ee Bwana, utege sikio lako, unijibu.

Ee Bwana, utege sikio lako unijibu,
Maana mimi ni maskini na mhitaji.
Unihifadhi nafsi yangu, maana mimi ni mcha Mungu,
Wewe uliye Mungu wangu,
Umwokoe mtumishi wako anayekutumaini. (K)

Wewe, Bwana, unifadhili, 
Maana nakulilia mchana kutwa.
Uifurahishe nafsi ya mtumishi wako,
Maana nafsi yangu nakuinulia wewe, Bwana. (K)

Kwa maana, Bwana, u mwema,
Umekuwa tayari kusamehe,
Na mwingi wa fadhili kwa watu wote wakuitao,
Ee Bwana, uyasikie maombi yangu,
Uisikilize sauti ya dua zangu. (K)



SHANGILIO
Mt. 8:17

Aleluya, aleluya,
Mwenye aliutwaa udhaifu wetu, na kuyachukua magonjwa yenu.
Aleluya.


INJILI
Mk. 5:21 – 43

Yesu alipokwisha kuvuka kurudia ng’ambo katika kile chombo, wakamkusanyikia mkutano mkuu; naye alikuwa kando ya bahari. Akaja mtu mmoja katika wakuu wa sinagogi, jina lake Yairo; hata alipomwona, akaanguka miguuni pake, akimsihi sana, akisema, Binti yangu mdogo yu katika kufa; nakuomba uje, uweke mkono wako juu yake, apate kupona, na kuishi. Akaenda pamoja naye. Mkutano mkuu wakamfuata, wakimsong-songa.

Na mwanamke mmoja mwenye kutoka damu muda wa miaka kumi na miwili, na kuteswa mengi kwa mikono ya matabibu wengi, amegharimiwa vitu vyote alivyo navyo, kusimfae hata kidogo, bali hali yake ilizidi kuwa mbaya; aliposikia habari za Yesu, alipita katiak mkutano kwa nyuma, akaligusa vazi lake; maana, alisema, Nikiyagusa mavazi yake tu, nitapona. Mara chemchemi ya damu yake ikakauka, anaye akafahamu mwilini mwake kwamba amepona msiba ule.

Mara yesu, ahali akifahamu nafsi ni mwake kwamba nguvu zimemtoka, akageuka kati ya mkutano, akasema, Ni nani aliyenigusa mavazi yangu? Wanafunzi wake wakambwambia, Je! Wawaona makutano wanavyokusonga-songa, nawe wasema, Ni nani aliyenigusa? Akatazama pande zote ili amwone yule aliyelitenda neno hilo. Na yule mwanamke akaingiwa na hofu na kutetemeka, akijua lililompata, akaja akamwangukia, akamweleza kweli yote. Akamwambia, Binti, Imani yako imekuponya, enenda zako kwa Amani, uwe mzima, usiwe na msiba wako tena.

Hata laipokuwa katika kunena, wakaja watu kutoka kwa yule mkuu wa sinagogi, wakisema, Binti yako amekwisha kufa; kwani kuzidi kumsumbua mwalimu? Lakini Yesu, alipolisikia lile neno likinenwa, akamwambia mkuu wa sinagogi, Usiogope, amini tu. Wala hakumruhusu mtu afuatane naye, ila Petro, na Yakobo, na Yohane nduguye Yakobo. Wakafika nyumbani kwa yule mkuu wa sinagogi, akaona ghasia, na watu wakilia, wakifanya maombolezo makuu. Alipokwisha kuingia, akawaambia, Mbona mnafanya ghasia na kulia? Kijana hakufa, bali amelala tu. Wakamcheka sana.

Naye alipokwisha kuwatoa nje wote, akamtwaa babaye yule kijana na mamaye, na wale walio pamoja naye, akaingia ndani alimokuwamo yule kijana. Akamshika mkono kijana, akamwambia, Talitha, kumi; tafsiri yake, Msichana, nakuambia, Inuka. Mara akasimama yule kijana, akaenda; maana laikuwa amepata umri wa miaka kumi na miwili. Mara wakashangaa mshangao mkuu. Akawaonya sana, mtu asijue habari ile; akaamuru apewe chakula.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo 


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUJIWEKA WAKFU KWA BWANA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatatu, Februari 2, 2026, 
Juma la 4 la Mwaka wa Kanisa

Sherehe ya Kutolewa Bwana hekaluni. 

Mal 3: 1-4;
Zab 24: 7-10;
Ebr 2: 14-18
Lk 2: 22-40.


KUJIWEKA WAKFU KWA BWANA!


Katika somo la Injili, Luka anaeleza taratibu tatu za sheria ambazo Maria na Yesu walijiweka. Siku nane baada ya kuzaliwa kwake, Yesu alitahiriwa. Alafu siku 33 baadae, Mama yake alimchukua Yesu Hekaluni kwa kazi mbili. Kwanza, kumtolea mtoto Yesu kwa Mungu, na alimtolea tena kwa kutoa shekeli tano. Hii ni mila ambayo ilikumbusha yote kuhusu kutolea sadaka kwa ajili ya kuokoa watoto wa kwanza wa kiume wa Israeli kutoka katika yule malaika wa kifo katika usiku wa Pasaka ya kwanza huko Misri. Pili, Maria alitolea sadaka ya mila yao ya kumtakasa na damu ya mama wakati wa kuzaliwa kwa mtoto.

Mila hizi tatu-kutahiriwa, kutakaswa baada ya mtoto kuzaliwa na sadaka ya kumuokoa mtoto wa kwanza wa kiume-vinaelekeza jinsi Mwanadamu hali yake ilikuwa ya dhambi. Kwasababu ya dhambi, Mwanadamu aliye anguka alijitenga na Mungu na alistahili tu baada ya kuhukumiwa na Mungu. Mila hizi zilionesha ulazima wa kukombolewa na kutakaswa. Mkombozi wetu alipitishwa katika mila hizi ingawaje hakutenda dhambi wala hakuwa na dhambi. Aliingia katika mila hizi kama mtoto, kama alivyokuwa mtu mzima na akaruhusu kujikabidhi kwaYohane Mbatizaji abatizwe ingawaje hakuwa na dhambi. Alifanya haya si kwasababu alihitaji utakaso wake mwenyewe bali alionyesha mshikamano wake na wadhambi ambao amekuja kuwakomboa. Kwa kufanya haya, Yesu alichukua udhaifu wetu juu ya nafsi yake mwenyewe kwa ajili ya wale aliokuja kuwakomboa. “Kwasababu alimfanya Yeye ambaye hakujua dhambi kuwa dhambi kwa ajili yetu, ili tuweze kuwa watakatifu wa Mungu kwa njia yake” (2 Kor 5:21). Wakati Maria anatolea “sadaka ya dhambi” na sadaka ya kuteketezwa kwa ajili ya utakaso, alileta sadaka ya mtu maskini njiwa wawili. Hili pia ni jambo jingine la kazi ya Yesu ya kutukomboa. Kama inavyosema “Unatambua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba alikuwa tajiri, lakini kwa niaba yetu amekuwa maskini, ili kwa njia ya umaskini wake tuweze kuwa tajiri” (2 Cor 8:9).

Simeoni alikuwa mtu mwenye haki na aliyejitoa. Roho Mtakatifu alikuwa juu yake na alimpa ufunuo wa kinabii. Alikuwa akitarajia faraja ya Isaeli, ambayo ni alama ya rafaja ya Israeli ambayo wanapokea Waisraeli kwa njia ya Masiha. Anna kwa upande mwingine alikuwa nabii. Baada ya kumuona mtoto Yesu, aliongelea kuhusu Yesu kwao wote waliokuwa wakitarajia ukombozi ambao Masiha angeleta. Siku hii ya leo tukumbuke pia kujitolea kwetu kwa Bwana kwa njia ya Ubatizo. Tujitoe wenyewe kwa Bwana na ufalme wake bila kuwa na mioyo iliogawanyika. 

Sala: Bwana nilizaliwa katika hali ya dhambi. Pokea sadaka yangu mwenyewe ya unyenyekevu na naomba unifanye nistahili ufalme wako. Yesu anakuamini wewe. Amina



Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 2, 2025



MASOMO YA MISA, FEBRUARI 2, 2025
JUMATATU, JUMA LA 4 LA MWAKA

SIKUKUU YA KUTOLEWA BWANA HEKALUNI


SOMO 1
Mal. 3:1-4

Bwana Mungu asema hivi: Angalieni, namtuma mjumbe wangu, naye ataitengeneza njia mbele yangu; naye Bwana mnayemtafuta atalijilia hekalu lake ghafula; naam yule mjumbe wa agano mnayemfurahia, angalieni, anakuja, asema Bwana wa majeshi. Lakini ni nani atakayestahimili siku ya kuja kwake? Au ni nani atakayesimama atakapoonekana yeye? Kwa maana yeye ni mfano wa moto wa mtu asafishaye fedha, ni mfano wa sabuni ya mtu afuaye nguo; naye ataketi kama asafishaye fedha na kuitakasa, naye atawatakasa wana wa Lawi, atawasafisha kama dhahabu na fedha; nao watamtolea Bwana dhabihu katika haki. Wakati ule ndipo dhabihu za Yuda na Yerusalemu zitakapopendeza mbele za Bwana, kama katika siku za kale, na kama katika miaka ya zamani.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
ZAB. 24:7-10 (K) 8

(K) Ni nani Mfalme wa utukufu? Ni Bwana.

Inueni vichwa vyenu, enyi malango,
Inukeni, enyi malango ya milele, 
Mfalme wa utukufu apate kuingia. (K)

Ni nani Mfalme wa utukufu?
Bwana mwenye nguvu, hodari,
Bwana hodari wa vita. (K)

Inueni vichwa vyenu, enyi malango,
Naam, viinueni, enyi malango ya milele
Mfalme wa utukufu apate kuingia. (K)

Ni nani huyu Mfalme wa utukufu?
Bwana wa majeshi,
Yeye ndiye Mfalme wa utukufu. (K)


SOMO 2
Ebr. 2:14-18

Basi, kwa kuwa watoto wameshiriki damu na mwili, yeye naye vivyo hivyo alishiriki yayo hayo, ili kwa njia ya mauti amharibu yeye aliyekuwa na nguvu za mauti, yaani, Ibilisi, awaache huru wale ambao kwamba maisha yao yote kwa hofu ya mauti walikuwa katika hali ya utumwa. Maana ni hakika, hatwai asili ya malaika, ila atwaa asili ya mzao wa Ibrahimu. Hivyo ilimpasa kufananishwa na ndugu zake katika mambo yote, apate kuwa kuhani mkuu mwenye rehema, mwaminifu katika mambo ya Mungu, ili afanye suluhu kwa dhambi za watu wake. Na kwa kuwa mwenyewe aliteswa alipojaribiwa, aweza kuwasaidia wao wanaojaribiwa.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


SHANGILIO
Lk. 2:32

Aleluya, aleluya!
Nuru ya kuwa mwangaza wa Mataifa, Na kuwa utukufu wa watu wako Israeli.
Aleluya!


INJILI
Lk. 2:22-40

Zilipotimia siku za kutakasika kwao, kama ilivyo torati ya Musa, wazee wa Yesu walikwenda naye hata Yerusalemu, wamweke kwa Bwana, (kama ilivyoandikwa katika sheria ya Bwana, Kila mtoto mwanamume aliye kifungua mimba ya mamaye na aitwe mtakatifu kwa Bwana), wakatoe na sadaka, kama ilivyonenwa katika sheria ya Bwana, Huwa wawili au makinda ya njiwa wawili. Na tazama, pale Yerusalemu palikuwa na mtu, jina lake Simeoni, naye ni mtu mwenye haki, mcha Mungu, akiitarajia faraja ya Israeli; na Roho Mtakatifu alikuwa juu yake. Naye alikuwa ameonywa na Roho Mtakatifu ya kwamba hataona mauti kabla ya kumwona Kristo wa Bwana. Basi akaja hekaluni ameongozwa na Roho; na wale wazazi walipomleta mtoto Yesu ndani, ili wamfanyie kama ilivyokuwa desturi ya sheria, yeye mwenyewe alimpokea mkononi mwake, akamshukuru Mungu, akisema, Sasa, Bwana, wamruhusu mtumishi wako, kwa amani, kama ulivyosema; kwa kuwa macho yangu yameuona wokovu wako, uliouweka tayari machoni pa watu wote; nuru ya kuwa mwangaza wa mataifa, na kuwa utukufu wa watu wako Israeli.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.