Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

UNYENYEKEVU MBEGU YA KIMUNGU!




“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Machi 3, 2026
Juma la 2 la Kwaresima

Isa 1:10, 16-20;
Zab 50:8-9,16-17,21,23;
Mt 23:1-12


UNYENYEKEVU MBEGU YA KIMUNGU!


Leo nabii Isaya anawaambia wana Waisraeli wafanye uchaguzi. Wajioneshe wenyewe na waache kutenda maovu. Kwaresima ni kipindi cha neema kubwa, ni muda ambao tunapaswa kutafakari ni wapi tulipo kosea na kujaribu kurekebisha. Kama nimechukua fedha isio halali niangalie jinsi ya kurudisha. Kama nilikuwa mtu wa kuapa, niache na kubadilika. Katika hali yeyote, napaswa kufanya kitu. Naweza kuhitaji sakramenti ya kitubio au kutafuta upatanisho na mtu ambaye nilimuumiza au aliyeniumiza.

Yesu anatupa somo zuri sana katika Injili. Anatutaka sisi tuweze kutukuka! Anatutaka sisi tujulikane na wengine. Anataka mwanga wetu mzuri uangaze watu waweze kuuona na kwa mwanga huo waweze kufanya mabadiliko. Lakini anapenda hili lifanyike katika kweli sio katika hali ya kudanganya. Anataka ukweli wa “mimi” uangaze. Nao ni unyenyekevu. Unyenyekevu ni kuwa mnyofu na mwaminifu. Na wakati watu watakapo ona hali hii ndani yetu, watavutwa. Sio sana katika hali ya kidunia bali katika hali ya kibinadamu. Hawata tuangalia na kuwa na wivu bali, watatuangalia na kuona ukweli wenyewe na kuufurahia, kuutamani na kutaka kuuishi. Unyenyekevu unakusaidia ukweli kamili kuhusu wewe uweze kungaa. Na wewe ukiwa katika kweli unakuwa ndiye mtu mwingine ambaye wengine wanataka kukutana naye.

Sala: Bwana, naomba unifanye niwe mnyenyekevu. Nakuomba niweze kuwa mwaminifu na mkweli kwa jinsi nilivyo. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MACHI 3, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 3, 2026
JUMANNE, JUMA LA 2 LA KWARESIMA


SOMO 1
Isa. 1:10, 16-20

Lisikieni neno la Bwana, enyi waamuzi wa Sodoma; tegeni masikio msikie sheria ya Mungu wetu, enyi watu wa Gomora.

Jiosheni, jitakaseni; ondoeni uovu wa matendo yenu usiwe mbele za macho yangu; achene kutenda mabaya; jifunzeni kutenda mema; takeni hukumu na haki; wasaidieni walioonewa; mpatieni yatima haki yake; mteteeni mjane.

Haya, njoni, tusemezane, asema Bwana. Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji; zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa kama sufu.

Kama mkikubali na kutii mtakula mema ya nchi; bali kama mkikataa na kuasi mtaangamizwa kwa upanga; maana kinywa cha Bwana kimenena haya.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 50:8-9, 16-17, 21, 23 (K) 23

(K) Autengenezaye mwenendo wake,
Nitamwonyesha wokovu wangu.

Sitakukemea kwa ajili ya dhabihu zako,
Na kafara zako ziko mbele yangu daima.
Sitatwaa ng’ombe katika nyumba yako,
Wala beberu katika mazizi yako. (K)

Una nini wewe kuitangaza sheria yangu,
Na kuliweka agano langu kinywani mwako?
Maana wewe umechukia maonyo,
Na kuyatupa maneno yangu nyuma yako. (K)

Ndivyo ulivyofanya, nami nikanyamaza,
Ukadhani ya kuwa Mimi ni kama wewe,
Atoaye dhabihu za kushukuru, ndiye anayenitukuza.
Naye autengenezaye mwenyendo wake,
Nitamwonyesha wokovu wa Mungu. (K)



SHANGILIO
Mt. 4:17

Tubuni asema Bwana, kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.



INJILI
Mt. 23:1-12

Yesu aliwaambia makutano na wanafunzi wake, akasema, Waandishi na Mafarisayo wameketi katika kiti cha Musa; basi, yoyote watakayowaambia, myashike, na kuyatenda; lakini kwa mfano wa matendo yao, msitende; maana wao hunena lakini hawatendi. Wao hufunga mizigo mizito na kuwatwika watu mabegani mwao; wasitake wenyewe kuigusa kwa kidole chao. Tena matendo yao yote huyatenda ili kutazamwa na watu; kwa kuwa hupapanua hirizi zao, huongeza matamvua yao; hupenda viti vya mbele katika karamu, na kuketi mbele katika masinagogi, na kusalimiwa masokoni, na kuitwa na watu, Rabi.

Bali ninyi msiitwe Rabi, maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu. Wala msimwite mtu baba duniani; maana Baba yenu ni mmoja, aliye wa mbinguni. Wala msiitwe viongozi; maana kiongozi wenu ni mmoja, naye ndiye Kristo. Naye aliye mkubwa wenu atakuwa mtumishi wenu. Na yeyote atakayejikweza atadhiliwa; na yeyote atakayejidhili atakwezwa.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

USIHUKUMU!





“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Jumatatu, Machi 2, 2026.
Juma la 2 la Kwaresima

Dan 9:4-10
Zab 79:8-11,13
Lk 6:36-38


USIHUKUMU!


Ulishawahi kukutana na mtu kwa mara ya kwanza na bila hata kuongea na huyu mtu mara moja unahitimisha unayofikiri juu yake au wao? Kama sisi wenyewe ni waaminifu ni lazima tukiri kwamba ni rahisi kuhukumu watu wengine kwa haraka. Kilicho kigumu ni kubadilisha hukumu yetu tuliojiwekea kuhusu hao wengine. Ni vigumu kuwahukumu tukiwapa mafanikio na kuondoa wasi wasi wetu na kufikiri ni wazuri. 

Yesu alivyosema “usihukumu nawe hauta hukumiwa” anatualika sisi tusiwe watu wa kuwahukumu watu katika hali yeyote. Ulimwengu unahitaji watu wengi wasio hukumu na wala kulaani. Tunahitaji watu wanao fahamu kutengeneza urafiki na kuleta upendo usio na masharti. Na Mungu anataka wewe uwe mmoja wao wa hao watu. Tutafakari ni mara ngapi tumekuwa watu wakuwahukumu watu, na tutafakari ni kwa namna ghani sisi ni wazuri katika kutengeneza urafiki na wale wote walio karibu yetu. Mwishowe, kama tumekuwa watu wa kutengeneza huu urafiki, ni wazi tutapokea Baraka kutoka kwa wengine wanao tupatia na sisi urafiki kama huo. Na kwa njia hiyo sisi wote tutabarikiwa. 

Sala: Bwana, ninaomba unipe moyo usio hukumu. Ninaomba unisaidie niwapende wote ninao kutana nao kwa mapendo matakatifu na kuwakubali. Ninaomba unipe mapendo ya kweli na urafiki wa kweli kwa wengine ili niweze kuamini na kufurahia upendo unaopenda mimi niwe nao. Yesu, nakuamini wewe. Amina. 


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MACHI 2, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 2, 2026
JUMATATU, JUMA LA 2 LA KWARESIMA


SOMO 1
Dan. 9:4 – 10

Ee Bwana, Mungu mkuu, mwenye kutisha, ashikaye maagano na rehema kwao wampendao, na kuzishika amri zake; tumefanya dhambi, tumefanya ukaidi, tumetenda maovu, tumeasi, naam, hata kwa kuyaacha maagizo yako na hukumu zako; wala hatukuwasikiliza watumishi wako, manabii, ambao kwa jina lako walisema na wafalme wetu, na wakuu wetu, na baba zetu, na watu wote wa nchi.

Ee Bwana, haki ina wewe, lakini kwetu sisi kuna haya ya uso, kama hivi leo; kwa watu wa Yuda, na kwa wenyeji wa Yerusalemu, na kwa Israeli wote, walio karibu na hao walio mbali, katika nchi zote ulikowafukuza, kwa sababu ya makosa yao waliyokukosa. Ee Bwana, kwetu sisi kuna haya ya uso, kwa wafalme wetu, na wakuu wetu, na baba zetu, kwa sababu tumekutenda dhambi. Rehema na msamaha ni kwa Bwana Mungu wetu, ingawa tumemwasi; wala hatukuitii sauti ya Bwana, Mungu wetu, kwa kwenda katika sheria zake, alizoziweka mbele yetu kwa kinywa cha watumishi wake, manabii.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 79:8 – 9, 11, 13 (K) 103:10

(K) Usitutende sawasawa na hatia zetu, Ee Bwana.

Usikumbuke juu yetu maovu ya baba zetu,
Rehema zako zije kutulaki hima,
Kwa maana tumedhilika sana. (K)

Ee Mungu wokovu wetu utusaidie.
Kwa ajili ya utukufu wa jina lako.
Utuokoe, utughofiri dhambi zetu,
Kwa ajili ya jina lako. (K)

Kuugua kwake aliyefungwa na kuingia mbele zako.
Kwa kadiri ya uweza wa mkono wako.
Uwahifadhi wana wa mauti.
Na sisi tulio watu wako, na kondoo za malisho yako,
Tutakushukuru milele;
Tutazisimulia sifa zako kizazi kwa kizazi. (K)



SHANGILIO
Mt. 4:4
Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.



INJILI
Lk. 6:36:38

Yesu aliwaambia wafuasi wake: Iweni na huruma, kama Baba yenu alivyo na huruma. Msihukumu, nanyi hamtahukumiwa; msilaumu, nanyi hamtalaumiwa; achilieni, nanyi mtaachiliwa. Wapeni watu kitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwasukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifruani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

KWARESIMA: MUDA WA KUMFAHAMU YESU!



“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Jumapili, Machi 1, 2026.
Dominika ya 2 ya Kwaresima

Mwa 1:1-4;
Zab 33:4-5, 18-22;
2 Tim 1:8-10;
Mt 17: 1-9.



KWARESIMA: MUDA WA KUMFAHAMU YESU!



Juma la kwanza la Kwaresima linatuandaa, kufanya matendo ya kwaresima, kusali, kufunga na kutoa sadaka. Inakuwa ni hatua kwetu kutengeneza hali nzuri ya kuingia katika kipindi hichi kwa undani. Jumapili iliopita ilituandaa kuhusu majaribu, na umuhimu wa kusafisha dhambi zetu rohoni mwetu. Yesu alituanyesha njia ya kumshinda shetani na dunia na pia vishawishi vya miili yetu, alipokuwa jangwani. Leo anajifunua kwa njia ya Kugeuka sura kutualika wote kwenye utukufu alio nao na Baba yake. Kwa njia ya kungara sura tunaalikwa kwenye ufufuko wa miili, wakati tutakapo kuwa huru kuhusu dhambi. Kama mwili wa Yesu ulivyokuwa katika utukufu, ndivyo miili ya watakatifu itangaa. “Utukufu ulionipa mimi nimewapa wao” (Yn 17:22).

Uhusiano unakuwa kadiri ya muda. Tunawafahamu watu zaidi kadiri ya muda unavyo sogea. Mitume pia lazima na wao waliendelea kumfahamu Yesu kadiri ya muda ulivyokuwa ukisogea. Uhusiano wao ulianza alivyo waita hapo awali. Waliishi naye na kumsikiliza na kushuhudia miujiza na uponyaji mbali mbali. Uelewa wao lazima utakuwa ulikuwa kadiri ya muda, mpaka Petro akafikia kiwango cha kusema “Wewe ni Masiha Mwana wa Mungu aliye hai”. Lakini Petro alimpinga alivyosikia habari ya kifo chake, na Yesu alitambua kuwa Wafuasi wake hawajamfahamu vizuri bado. Walimwelewa vibaya kuwa kama Masiha wa kidunia atakaye iongoza dunia daima. Ndio, maana baada ya siku sita hivi Yesu awaliwachagua Petro, Yohane na Yakobo kwenda mlima na kushuhudia kungara kwake kwa sura inayoelezewa leo katika Injili.

Kungara sura kwa Yesu kunatokea wakiwa juu ya milima. Mlimani palijulikna kama sehemu ya kukutana na Mungu. Wakati Yesu anageuka sura mavazi yake yalingaa sana na uso wake ulingara. Taswira hii alioionyesha Yesu ni hali ya utukufu ambayo itakuja baada ya maisha ya ulimwengu huu. Musa na Elia ambao katika tamaduni ya Wayahudi waliwakilisha mambo mawili muhimu ya Wayahudi. Sheria na Manabii. Musa na Elia walikuwa ni watu ambao walipata kuwasiliana na Mungu wakiwa katika milima. Na waliwaongoza watu wa Israeli kumrudia Mungu.

Kwa kuangalia hali hii ya kugusa na kuogopesha, Petro anaomba kujengwe vibanda vitatu kimoja cha Yesu, kimoja cha Elia na kimoja cha Musa. Petro alipenda hii hali iendelee kuwapo. Mungu anaingia kati na kumfunua mwanae (Mwana wa Mungu) kwa wafuasi “Huyu ndiye Mwanangu mpendwa…” Mitume wanaogopa na wanainamisha nyuso zao. Walivyo nyanyuka walikuta kila kitu kikiwa katika hali yakawaida. Tukio hili ni lazima lilikuwa ni la nguvu sana kuliko tukio lolote lile ambalo mitume hawa watatu waliweza kulishuhudia. Katika tukio hili la kungara sura, Umungu wa Yesu ulifunuliwa kwao. Waliweza kufahamu Yesu ni nani na kwanini Yesu alikuwa akiongelea kuhusu kifo na ufufuko . wafuasi waliweza kuja kumfahamu Yesu vizuri zaidi wakati wa Karamu ya mwisho, mateso yake alivyokuwa pale Getsemane, mateso yake, kifo na kufufuka. Muda wote waliokuwa na Yesu waliweza kuja kumfahamu Yesu na kutambua nini maana ya kuwa wafuasi. Nasi ni hivyo hivyo.

Katika somo la kwanza tunasikia kuhusu kuitwa kwa Abrahamu. Abrahamu anajibu wito wa kwanza kabisa wa Mungu. Na ni baada ya muda tu alikuja kumfahamu Mungu vizuri na utume wake kwa ajili yake. Hivyo, tunavyopata muda wa kuwa na Mungu zaidi ndivyo tunavyozidi kuendelea kumfahamu zaidi, na kadiri tunayo endelea kumfahamu Mungu, ndivyo tunavyo fahamu mpango wake kwetu.

Kwaresima ni kipindi cha kutafakari na kukaribisha neema ya Mungu katika maisha yetu. Sio muda tu wakuachia vitu, bali pia ni muda wakupokea zawadi kubwa kutoka kwa Mungu. Mungu hajatusahau sisi watoto wake ila ni sisi tuliomsahau yeye na kukimbia uso wake. Leo, upendo unafunuliwa kwetu kwa njia ya Yesu. Yesu kwa njia ya ufufuko anatufanya sisi kuwa sehemu ya mpango wa Mungu tangu milele, kuwa watakatifu na kupendwa na Mungu kwa kuwa daima mbele zake. Ufufuko unaleta kwetu mwanga katika maisha yetu kama wa kungara sura kwa Yesu, kiasi kwamba hakuna giza linalo baki.

Maandiko matakatifu yanatuonesha njia ya kwenda katika muelekeo huu. Kwanza kabisa, kuwa na muda wa kusali kama Yesu. Pili ni kumfahamu Yesu, na hili linafanyika kwa kutafakari Maandiko Matakatifu, Mungu aliwaambia wafuasi kwamba “Msikilizeni yeye” pia Neno la Mungu linafunua nafsi ya Yesu kwetu sisi kila siku. Tatu, tuwe tumeungana katika jumuiya zetu. Kama mitume watatu walivyo pata kumshuhudia Yesu, na kushiriki katika mwanga uliofunuliwa na Mungu. Hili linawezekana daima tunavyo shiriki katika Ekaristi Takatifu, tunaitwa wote kuunganika katika kungara kwa Yesu katika Ekaristi takatifu. Na mwisho kabisa, kushiriki katika mahusiano mazuri na wenzetu. Mitume hawakuweza kushirikisha walio yaona muda ule, bali walishirikisha baada ya ufufuko wakati wamesha elewa maana kamili ya kungara kwake sura, walishirikisha wengine kwa kuhubiri habari Njema. Sisi pia tunaitwa kutangaza kungara kwa sura kwa Yesu kwa kuwatangazia wale wote waliotengwa. Tunaitwa kutambua matendo ya roho na matendo ya nje ya huruma: kuwalisha maskini, kuwapa maji walio na kiu, kuwavisha wasio na nguo, kuwakaribisha wasio na makao, kuwaponya wagonjwa, kutembelea wafungwa, kuwazika wafu, , kuwasaidia walio na mashaka, kuwaelekeza walio wajinga, kuwa elekeza wadhambi warudi, kuwafariji wenye matatizo, kuwasamehe walio tukosea, kuchukuliana kwa huruma wale wote wanao tuumiza na kuwaombea walio wazima na wafu.

Sala: Bwana, ninaomba nifarijike kwa utukufu wako na ukweli wako. Ninaomba nikumbuke utukufu huu ninapo tembea katika changamoto mbali mbali katika maisha. Utatembea mbele yangu na kunitangulia nikikuamini wewe. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MACHI 1, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 1, 2026
JUMAPILI YA 2 YA KWARESIMA



SOMO 1
Mwa. 12:1 – 4a

Bwana akamwambia Abramu, Toka wewe katika nchi yako, na jamaa zako, na nyumba ya baba yako, uende mpaka nchi nitakayokuonyesha; nami nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa, na kukubariki, na kulitukuza jina lako; nawe uwe Baraka; nami nitawabariki wakubarikio, naye akulaaniye nitamlaani; na katika wewe jamaa zote za dunia watabarikiwa.

Basi Abramu akaenda, kama Bwana alivyomwamuru.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 33:4 – 5, 18 – 20, 22 (K) 22

(K) Ee Bwana, fadhili zako zikae nasi,
Kama vile tulivyokungoja Wewe.

Kwa kuwa neno la Bwana lina adili,
Na kazi yake yote huitenda kwa uaminifu.
Huzipenda haki na hukumu,
Nchi imejaa fadhili za Bwana. (K)

Tazama, jicho la Bwana li kwao wamchao,
Wazingojeao fadhili zake.
Yeye huwaponya nafsi zao na mauti,
Na kuwahuisha wakati wa njaa. (K)

Nafsi zetu zinamngoja Bwana;
Yeye ndiye msaada wetu na ngao yetu.
Ee Bwana, fadhili zako zikae nasi,
Kama vile tulivyokungoja Wewe. (K)



SOMO 2
2Tim. 1:8b – 10

Uvumilie mabaya pamoja nami kwa ajili ya Injili, kwa kadiri ya nguvu ya Mungu; ambaye alituokoa akatuita kwa mwito mtakatifu, si kwa kadiri ya matendo yetu sisi, bali kwa kadiri ya makusudi yake yeye na neema yake. Neema hiyo tulipewa katika Kristo Yesu tangu milele, na sasa inadhihirishwa kwa kufunuliwa kwake Mwokozi wetu Kristo Yesu; aliyebatili mauti, na kuufunua uzima na kutokuharibika, kwa ile Injili.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



SHANGILIO
Mt. 17:5

Sauti ya Baba ilitoka katika wingu jeupe: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, msikieni yeye.”



INJILI
Mt. 17:1 – 9

Yesu akawatwaa Petro, na Yakobo, na Yohane nduguye, akawaleta juu yam lima mrefu faraghani; akageuka sura yake mbele yao; uso wake ukang’aa kama jua, mavazi yake yakawa meupe kama nuru. Na tazama, wakatokewa na Musa na Eliya, wakizungumza naye.

Petro akajibu akamwambia Yesu, Bwana, ni vizuri sisi kuwapo hapa; ukitaka, nitafanya hapa vibanda vitatu, kimoja chako wewe, na kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya.

Alipokuwa katika kusema, tazama, wingu jeupe likawatia uvuli; na tazama, sauti ikatoka katika lile wingu, ikasema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye; msikieni yeye. Na wale wanafunzi waliposikia, walianguka kifulifuli, wakaogopa sana.

Yesu akaja, akawagusa, akasema, Inukeni, wala msiogope. Wakainua macho mlimani, Yesu aliwaagiza, akasema, Msimwambie mtu yeyote habari ya maono hayo, hata Mwana wa Adamu atakapofufuka katika wafu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUTAMANI KUWA MKAMILIFU!





“KWARESIMA YA UKARIMU”
Jumamosi, Februari 28, 2026,
Juma la 1 la Kwaresima


Kumb 26: 16-19;
Zab 119: 1-2, 4-5, 7-8;
Mt 5: 43-48



KUTAMANI KUWA MKAMILIFU!


Liturujia ya leo inalenga katika Sheria ya Mungu, ambayo Mungu ametupa kwa njia ya Musa ili kuifuata kwa moyo na nafsi nzima. Katika Injili, tunaona Yesu, analeta upendo wenye athari kubwa, zaidi kuliko wowote ule ambao waliutenda kabla. Kumpenda kila mtu, bila kuwa na fikra au sababu yeyote ile, bila kujali kama wao wanatupenda sisi au la, bila kufikiria wanatuwazia mabaya au mazuri?

Yesu wakati alipokuwa dunia hii, alikabiliwa na upinzani sana, kutoka kwa mamlaka ya kidini, kutoka kwenye mamlaka ya kisiasa, kutoka mji wake mwenyewe, kutoka kwa baadhi ya wanafunzi wake mwenyewe. Hata hivyo, yeye amewapenda daima wote. Ujumbe wake wa huruma au wa kubadilika mara zote ulijawa na upendo mkuu. Hata juu ya Msalaba, aliwatazama kwa huruma watesi wake. Upendo kwa Mungu na kwa jirani huenda pamoja, na hauwezi kutenganishwa. Mt. Yohane anaweka wazi kwamba, “Mtu akisema, “Nampenda Mungu,” naye anamchukia ndugu yake, ni mwongo (1Yoh 4:20). 

Leo tunapewa changamoto na upendo huu wa Yesu Kristo. Tumekuwa mara nyingi sana watu ambao tunabagua wengine, juu ya rangi, dini, jinsia, kabila, juu ya tabaka, utaifa, juu ya hadhi ya jamii, utamaduni, elimu, kiasi cha mali ulicho nacho nk, Je, tunaweza kuamua kumwiga Yesu kuanzia sasa na kuendelea? Je, tunaweza kuwapenda wale wote ambao wametuumiza katika maisha yetu? Wale wanaotutesa kwasababu ya utamaduni wetu, dini yetu,au mawazo yetu? Yesu alishinda haya yote kwa upendo wake, Je, sisi twaweza kufanya hivyo tushinde kwa njia ya upendo?

Sala: Bwana, ninataka kuwa mtakatifu. Ninataka kuwa mtakatifu kama wewe ulivyo mtakatifu. Nisaidie niishi kila wakati kwa ajili yako. Ninatoa muda wangu wote kwa ajili yako. Yesu, nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com