Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MASOMO YA MISA, MACHI 12, 2026


MASOMO YA MISA, MACHI 12, 2026
ALHAMISI, JUMA  LA 3 LA KWARESIMA


SOMO 1
Yer. 7:23-28

Naliwaamuru neno hili, nikisema, Sikilizeni sauti yangu, nami nitakuwa Mungu wenu, nanyi mtakuwa watu wangu; mkaende katika njia ile yote nitakayowaamuru, mpate kufanikiwa. Lakini hawakusikiliza, wala kutega sikio lao, bali walikwenda kw amashauri yao wenyewe, na kwa ushupavu wa mioyo yao mibaya, wakaenda nyuma wala si mbele. Tokea siku ile baba zenu walipotoka katika nchi ya Misri hata leo, nimewatuma watumishi wangu wote manabii kwenu ninyi, nikiamka mapema kila siku na kuwatuma. Lakini hawakunisikiliza, wala kutega sikio lao; bali walifanya shingo yao kuwa ngumu; walitenda mabaya kuliko baba zao. Nawe utawaambia maneno hayo yote; lakini hawatakusikiliza; nawe utawaita; lakini hawatakuitikia. Nawe utawaambia, Taifa hili ndilo lisilosikiliza sauti ya Bwana, Mungu wao, wala kupokea mafundisho; uaminifu umepotea, umekatiliwa mbali vinywa vyao.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 95:1-2, 6-9 (K) 7

(K) Ingekuwa heri leo msikie sauti yake! Msifanye migumu mioyo yenu.

Njoni, tumwimbie Bwana,
Tumfanyie shangwe mwamba wa wokovu wetu.
Tuje mbele zake kwa shukrani,
Tumfanyie shangwe kwa zaburi. (K)

Njoni, tuabudu, tusujudu,
Tupige magoti mbele za Bwana aliyetuumba.
Kwa maana ndiye Mungu wetu,
Na sisi tu watu wa malisho yake,
Na kondoo za mkono wake. (K)

Ingekuwa heri leo msikie sauti yake!
Msifanye migumu mioyo yenu;
Kama vile huko Meriba,
Kama siku ya Masa jangwani.
Hapo waliponijaribu baba zenu,
Wakanipima, wakayaona matendo yangu. (K)


SHANGILIO
Zab. 51:10, 12

Ee Mungu, uniumbie moyo safi, 
Unirudishie furaha ya wokovu wako.


INJILI
Lk. 11:14-23

Yesu alikuwa akitoa pepo bubu; ikawa pepo alipotoka, yule bubu akanena, makutano wakastaajabu. Wengine wao wakasema, Atoa pepo kwa Beelzebuli, mkuu wa pepo. Wengine walimjaribu, wakitaka ishara itokayo mbinguni. Naye akajua mawazo yao, akawaambia, Kila ufalme uliofitinika wenyewe kwa wenyewe hufanyika ukiwa; na nyumba juu ya nyumba huanguka. Basi, ikiwa Shetani naye amefitinika juu ya nafsi yake, ufalme wake utasimamaje? Kwa kuwa ninyi mnasema kwamba mimi natoa pepo kwa Beelzebuli, wana wenu je! Huwatoa kwa nani? Kwa sababu hiyo, hao ndio watakaowahukumu. Lakini, ikiwa mimi natoa pepo kwa kidole cha Mungu, basi ufalme wa Mungu umekwisha kuwajilia. Mtu mwenye nguvu aliyejifunga silaha zake, alindapo nyumba yake, vitu vyake vi salama; lakini mtu mwenye nguvu kuliko yeye atakapomwendea na kumshinda, amnyang’anya silaha zake zote alizokuwa akizitegemea, na kuyagawanya mateka yake.

Mtu ambaye si pamoja nami yu kinyume changu; na mtu asiyekusanya pamoja nami hutapanya.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

YESU: UTIMILIFU WA SHERIA



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Kwaresima
Jumatano, Machi 11, 2026 
Juma la 3 la Mwaka wa Kanisa

Kumb 4:1, 5-9
Zab 147: 12-13,15-16,19-20;
Mt 5:17-19

YESU: UTIMILIFU WA SHERIA

Masomo ya leo yanatupa picha kuhusu sheria ya Mungu. Ni za taratibu na kamilifu. Yesu alifanya kurejea “sheria na Manabii” akisema kwamba hakuja kutengua sheria za manabii bali kuzitimiza. Zilikuja kutimizwa baada ya miaka elfu na zaidi. Ilichukuwa muda kwa utimilifu wa mpango wa Mungu kujifunua. Lakini ulijifungua kwa wakati wake na kwa jinsi yake. Ni hakika, wale wote waliokuwa katika Kipindi cha Agano la Kale walikuwa na shauku ya Masiha kuja ili kutimiza vitu vyote. Nabii baada ya nabii alikuja akinyoosha kidole mbele kwa wakati ujao kwamba Masiha atakuja. Hata sheria za Agano la Kale katika hali Fulani zilikuwa ni kwa ajili ya kuwaandaa watu wa Mungu kwa ajili ya ujio wa Masiha. Lakini ilikuwa ni hali ya taratibu ya kutengeneza sheria, kuziweka kwa watu wa Israeli, kuwasaidia ili kuzielewa, na kuanza kuziishi. Hata Masiha alivyokuja, kuna wengine kwasababu ya shauku na furaha walitaka atimize yote kwa wakati mmoja. Walitaka Ufalme wao wa dunia uanzishwe na walitaka Masiha wao mpya achukue Ufalme wake.

Lakini mpango wa Mungu ni tofauti kabisa na hekima ya Binadamu. Njia zake zilikuwa tofauti kabisa na njia zetu. Na njia zake zikaendelea kuwa mbali kabisa na njia zetu! Yesu alitimiza kila sheria katika Agano la Kale na Manabii, na si kama vile watu walivyokuwa wanadhani. Wayahudi wakati wa Yesu walikuwa wamejikita mno katika sheria binafsi na mapokeo katika sheria ya Musa kiasi kwamba walipoteza picha halisi. Iliwawia vigumu kumtambua Yesu kwamba yeye mwenyewe ndiye mtimilifu wa sheria, kwamba alikuwa sheria ya Mungu iliochukuwa umwilisho. Kwa maneno yake na matendo yake alileta sheria katika maisha. Sio tena mlolongo wa Maandishi, sheria sasa zilikuwa kitu cha kuishi katika uhalisia na kila mtu alihisi. Tafakari kwa kujitafiti mwenyewe kama nawe ni mtu wa kuangalia tu karibu kama Wayahudi! Je, unamuona Yesu kama anayeishi na mtilifu wa sheria?

Sala: Bwana, ninakabidhi maisha yangu kwako. Nina amini kwamba una mpango kamili kwangu na kwa watoto wako wapendwa. Nipe subira niweze kukusubiri wewe na nikuache wewe ulete mapenzi yako ya Kimungu yatimie katika maisha yangu. Yesu nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MACHI 11, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 11, 2026
JUMATANO, JUMA LA 3 LA KWARESIMA

SOMO 1
Kumb. 4:1, 5-9

Musa aliwaambia makutano: Ee Israeli, zisikilizeni amri na hukumu niwafundishazo, ili mmzitende; mpate kuishi na kuingia na kuimiliki nchi awapayo Bwana, Mungu wa baba zenu.

Angalieni nimewafundisha amri na hukumu, vile vile kama Bwana, Mungu wangu, alivyoniamuru, ili mzitende katika nchi mwmingiayo ili kuimiliki. Zishikeni basi, mkazitende, maana hii ndiyo hekima yenu na akili zenu, machoni pa mataifa watakaozisikia amri hizi zote, nao watasema, Hakika taifa hili kubwa ni watu wenye hekima na akili. Kwa maana liko taifa gani kubwa, lililo na Mungu aliye karibu nao, kama Bwana, Mungu wetu, alivyo, kila tumwitapo? Tena liko taifa gani kubwa, lililo na amri na hukumu zenye haki kama torati hii yote, ninayoiweka mbele yenu leo.

Lakini, jihadhari nafsi yako, ukailinde roho yako kwa bidii, usije ukayasahau mambo yale uliyoyaona kwa macho yako, yakaondoka moyoni mwako siku zote za maisha yako; bali uwajulishe watoto wako na watoto wa watoto wako.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 147:12-13, 15-16, 19-20 (K) 12

(K) Msifu Bwana, Ee Yerusalemu.

Msifu Bwana, Ee Yerusalemu;
Msifu Mungu wako, Ee Sayuni.
Maana ameyakaza mapingo ya malango yako,
Amewabariki wanao ndani yako. (K)

Huipeleka amri yake juu ya nchi,
Neno lake lapiga mbio sana.
Ndiye atoaye theluji kama sufu,
Huimwaga barafu yake kama majivu. (K)

Humhubiri Yakobo neno lake,
Na Israeli amri zake na hukumu zake.
Hakulitendea taifa lolote mambo kama hayo,
Wala hukumu zake hawakuzijua. (K)


SHANGILIO

Mbegu neno la Mungu, 
mpanzi lakini ni Kristu; 
Yeyote ampataye, ataishi milele.


INJILI
Mt. 5:17-19

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Msidhani kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza. Kwa maana, amin, nawaambia, Mpaka mbingu na nchi zitakapoondoka, yodi moja wala nukta moja ya torati haitaondoka hata yote yatimie. Basi mtu yeyote atakayevunja amri moja katika hizi zilizo ndogo, na kuwafundisha watu hivyo, ataitwa mdogo kabisa katika ufalme wa mbinguni; bali mtu atakayezitenda na kuzifundisha, huyo ataitwa mkubwa katika ufalme mbinguni.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.


MSAMAHA



------------------------------------------------
“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Kwaresima
Jumanne, Machi 10, 2026, 
------------------------------------------------
JUMATATU, JUMA LA 3 LA KWARESIMA
------------------------------------------------

Dan 3:25,34-43;
Zab 25:4-9; 
Mt 18:21-35

MSAMAHA

Injili ya leo inatupa mfano wa jinsi ya kupokea na kutoa msamaha. Kinachovutia, ni rahisi kusamehe zaidi ya kuomba msamaha. Kwakweli katika kuomba msamaha inahitaji kuwa mwaminifu kwanza kwa kukubali kwamba nimekosa, ambapo mara nyingi ni jambo ngumu kulifanya. Ni vigumu kuchukua jukumu kwa lile tulilokosa. Katika mfano huu, huyu mtu anayeomba apewe muda ili aweze kulipa anaonekana kuwa mwaminifu. “Anapiga magoti” mbele ya Bwana wake kwa huruma na kuomba apewe muda. Na huyu Bwana wake anaonesha msamaha kwa kumsamehe deni lote ambalo lilikuwa kubwa kuliko jinsi alivyo omba.

Lakini inaonekana alikuwa muigizaji mzuri sana kwasababu mara tu ya kusamehewa deni hili kubwa, anamkimbilia mtu ambaye alikuwa anamdai tena kiasi kidogo tu, na badala ya kumuonesha huruma “anamrukia na kuanza kumpiga, akimdai, nilipe mali yangu”. Msamaha kama ni wa kweli, unapaswa uingie kila mahali katika kila kitu tufanyacho.

Je, waweza kuona kosa lako na kusema samahani kwa mwingine? 
Wakati unapo samehewa, jambo hili linatoa fundisho ghani? 
Je, waweza kutoa msamaha na huruma kama wewe ulivyo samehewa?

Kama huwezi kjibu “ndio” kwa maswali hayo, basi ujue mfano huu uliandikwa kwa ajili yako. Haya ni maswali magumu kukutana nayo lakini ni maswali muhimu kama tunataka kutua mizigo na kuwa huru. Tutafakari maswali hayo hapo juu na katika sala tutafiti matendo yetu. Mimi na wewe tuna deni kubwa ambalo hatuwezi kulilipa (dhambi zetu). Bwana wetu anatuita leo katika mahakama yake (Ekaristi). Kwa msaada wa Roho Mtakatifu, tujenge tena upya uhusiano wetu na kuwa vyombo vya Amani.

Sala: Bwana, ninakiri dhambi zangu. Lakini ninakiri kwa msaada wa mwanga wa neema na huruma yako. Ninapo ipokea huruma hii katika maisha yangu, ninaomba unifanye mwenye huruma kwa wengine. Nisaidie niweze kutoa msamaha kwa uhuru kamili bila kubaki na kitu. Yesu nakumini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MACHI 10, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 10, 2026
JUMANNE, JUMA LA 3 LA KWARESIMA


SOMO 1
Dan. 3:25, 34-43

Ndipo Azaria akasimama akasali hivi, akifumbua kinywa chake katikati ya moto na kusema: 

Usituache kabisa, kwa ajili ya jina lako, wala usilitangue agano lako na kutuondolea rehema zako, kwa ajili ya Ibrahimu umpendaye, na kwa ajili ya Isaka mtumishi wako, na Israeli mtakatifu wako kama nyota za mbinguni na kama mchanga wao pwani. Maana sisi, Ee Bwana, tumekuwa duni kuliko mataifa yote, na kudhulumiwa leo katika ulimwengu wote kwa sababu ya dhambi zetu. Sasa hakuna mfalme wala nabii wala kiongozi; hakuna dhabihu wala kafara wala sadaka wala uvumba; wala mahali pa kukutolea dhabihu na kuona rehema.

Lakini kwa moyo uliovunjika na kwa roho nyenyekevu tukubaliwe nawe, na sadaka yetu iwe machoni pako leo kama dhabihu za kondoo waume na ng’ombe, na kama kondoo wanono elfu kumi. Nasi tukufuate kwa unyofu, maana wanaokutumaini Wewe hawataaibika.

Na sasa tunakufuata kwa moyo wote; tunakucha na kuutafuta uso wako. Usitufedheheshe, bali ututendee kwa kadiri ya fadhili zako, sawasawa na wingi wa huruma zako. Utuokoe kwa kadiri ya maajabu yako, na kulitukuza jina lako, Ee Bwana.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 25:4-9 (K) 6

(K) Ee Bwana, kumbuka rehema zako na fadhili zako.

Ee Bwana unijulishe njia yako,
Unifundishe mapito yako, 
Uniongoze katika kweli yako,
Na kunifundisha. (K)

Ee Bwana kumbuka rehema zako na fadhili zako,
Maana zimekuwako tokea zamani.
Usiyakumbuke makosa ya ujana wangu,
Wala maasi yangu.
Ee Bwana, kwa ajili ya wema wako. (K)

Bwana yu mwema, mwenye adili,
Kwa hiyo atawafundisha wenye dhambi njia.
Wenye upole atawaongoza katika hukumu,
Wenye upole atawafundisha njia yake. (K)


SHANGILIO
Yn. 11:25, 26

Mimi ndimi ufufuo na uzima, asema Bwana; Yeye aniaminiye mimi, hatakufa kabisa na milele.


INJILI
Mt. 18:21-35

Petro alimwendea Yesu akamwambia, Bwana, ndugu yangu anikose mara ngapi nami nimsamehe? Hata mara saba? Yesu akamwambia, Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini.

Kwa sababu hii ufalme wa mbinguni umefanana na mfalme mmoja aliyetaka kufanya hesabu na watumwa wake. Alipoanza kuifanya, aliletewa mtu mmoja awiwaye talanta elfu kumi. Naye alipokosa cha kulipa, bwana wake akaamuru auzwe, yeye na mkewe na watoto wake, na vitu vyote alivyo navyo, ikalipwe ile deni. Basi yule mtumwa akaanguka, akamsujudia akisema, Bwana, nivumilie, nami nitakulipa yote pia. Bwana wa mtumwa yule akamhurumia, akamfungua, akamsamehe ile deni.

Mtumwa yule akatoka, akamwona mmoja wa wajoli wake, aliyemwia dinari mia; akamkamata, akamshika koo, akisema, Nilipe uwiwacho. Basi mjoli wake akaanguka miguuni pake, akamsihi akisema, Nivumilie, nami nitakulipa yote pia. Lakini hakutaka, akaenda, akamtupa kifungoni, hata atakapoilipa ile deni.
Basi wajoli wake walipoyaona yaliyotendeka, walisikitika sana, wakaenda wakamweleza bwana wao yote yaliyotendeka. Ndipo bwana wake akamwita, akamwambia, Ewe mtumwa mwovu, nimekusamehe wewe deni ile yoe, uliponisihi; nawe pia haikukupasa kumrehemu mjoli wako, kama mimi nilivyokurehemu wewe? Bwana wake akaghadhibika, akampeleka kwa watesaji, hata atakapolipa deni ile yote. Ndivyo na Baba yangu wa mbinguni atakavyowatenda ninyi, msiposamehekwa mioyo yenu kila mtu ndugu yake.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026 "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUINGIA KATIKA MAPENDO NA YESU!

 


“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Jumatatu, Machi 9, 2026
Juma la 3 la Kwaresima

2Fal 5:1–15;
Zab 42:2–3; 43:3;
LK 4: 24–30.


KUINGIA KATIKA MAPENDO NA YESU!


Ni wiki ya 3 ya kipindi cha Kwaresima, karibia nusu safari ya kipindi chetu cha Kwaresima. Upinzani juu ya Yesu na hao walio karibu naye kumpinga unazidi kukuwa. Yesu ni nabii, akitenganisha kati ya mema na mabaya, na ni nani aliye karibu naye au nani aliye mbali na ufalme aliouleta? Ni kipindi cha kufanya uchaguzi, kuitwa na kubadilika. Tunapaswa tusimame na Yesu.

Yesu anarejea habari inayo husiana na kitabu cha 2 cha Wafalme. Mfalme Aram alivyomtuma Naaman akiwa na barua akiwa na vipande kumi vya silva, vipande elfu 6 vya dhahabu, na nguo za maridadi, akiomba amponye ukoma wake. Mfalme wa Israeli alipokea barua na kurarua nguo yake, akidhani kwamba Mfalme Aram anamtaka uadui. Elisha alivyosikia kuhusu habari za Mfalme kuchana nguo yake, aliamuru amtume Naaman kwake aende na kumuonesha matendo ya Mungu, ili Wafalme na watu wote waweze kutambua kwamba yupo Mungu katika Israeli. Naaman alitii na kwenda katika nyumba ya Elisha. Pale anaambiwa akajichovye mara saba katika mto Yordani ili apone. Naaman anapatwa na hasira. Lakini mtumishi wake alifikiri pamoja naye. Hapo anatii sauti ya Elisha na hapo nyama yake inakuwa kama ya mtoto mdogo. “Naaman anakiri imani yake moja kwa moja “Hakika natambua kwa hakika hakuna Mungu duniani kote, isipokuwa Israeli”.

Katika Injili ya leo, Yesu anawakumbusha kwamba hakuna nabii katika Israeli aliyetokea kukubaliwa nyumbani kwake mwenyewe. Umati unakasirishwa na unataka kumwangamiza Yesu. Wakati alishasema vizuri kuhusu kuwaseta huru wafungwa na kuwapa nguvu waliopondeka moyo hawakuwa tayari kusikiliza sauti yake na kutubu. Mara nyingi majibu yetu yanaweza kufanana na haya ya umati. Sisi tulisafishwa dhambi zetu tulivyompokea hapo mwanzo na tukaona huruma yake. Na hivyo tunavyokaribia karibu zaidi na Mungu, Roho Mtakatifu anatuonesha sehemu ambazo hatukuwa wazi kwake. Na mara nyingi tunaweza kuishia kumkataa Yesu na kutaka kukimbia. Mungu anahitaji kile kilicho cha muhimu kwetu. Mtafute yeye, sikia neno lake, na ingia katika mapendo na Yesu tena!

Sala: Bwana, ninajitoa mwenyewe kwako. Ingia katika maisha yangu na yafanye upya kwa mapendo yako. Ninaomba pia nitoe upendo wako kwa wengine. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MACHI 9, 2026




MASOMO YA MISA, MACHI 9, 2026
JUMATATU , JUMA LA 3 LA KWARESIMA


SOMO 1
2 Fal. 5:1-15

Naamani, jemadari wa jeshi la mfalme wa Shamu, alikuwa mtu mkubwa mbele ya bwana wake, na mwenye kuheshimiwa, kwa sababu kwa mkono wake Bwana alikuwa amewapa Washami kushinda; tena likuwa mtu hodari wa vita; lakini alikuwa mwenye ukoma. Na Washami walikuwa wametoka vikosi vikosi, wakachukua mfungwa mmoja kijana mwanamke kutoka nchi ya Israeli; naye akamhudumia mkewe Naamani. Akamwambia bibi yake, Laiti bwana wangu angekuwa pamoja na yule nabii aliyeko Samaria! Maana angemponya ukoma wake. Mtu mmoja akaingia, akamwambia bwana wake, akasema, Yule kijana mwanamke aliyetoka nchi ya Israeli asema hivi na hivi. Mfalme wa Sahmu akasema, Haya! Basi, mimi nitampelekea mfalame wa Israeli waraka. Basi akaenda zake, akachukua mikononi mwake talanta kumi za fedha, na vipande vya dhahabu elfu sita, na mavazi kumi.

Akampelekea mfalme wa Israeli waraka ule, kusema, Waraka huu utakapokuwasilia, tazama, nimemtuma mtumishi wangu Naamni kwako, ili upate kumponya ukoma wake. Ikawa, mfalme wa Israeli alipousoma waraka, alirarua mavazi yake, akasema, Je! Mimi ni Mungu, niue na kuhuisha, hata mtu huyu akanipelekea mtu nimponye ukoma wake? Fahamuni, basi, nakusihini, mwone ya kuwa mtu huyu anataka kugombana nami.

Ikawa, Elisha, yule mtu wa Mungu, aliposikia kwamba mfalme wa Israeli ameyararua mavazi yake, ndipo akatuma mtu kwa mfalme, akisema, Mbona umeyararua mavazi yako? Na aje sana kwangu mimi, naye atajua ya kuwa yuko nabii katika Israeli.

Basi Naamani akaja na farasi wake na magari yake, akasimama mlangoni pa nyumba ya Elisha. Naye Elisha akampelekea mjumbe, akisema. Enenda ukaoge katika Yordani mara saba, na nyama ya mwili wako itakurudia nawe utakuwa safi. Lakini Naaman akakasirika, akaondoka, akasema, Tazama, nalidhania, Bila shaka atatoka kwangu, na kusimama, na kuomba kwa jina la Bwana, Mungu wake, na kupitisha mkono wake mahali penye ugonjwa, na kuniponya mimi mwenye ukoma Je! Abana na Farpari, mito ya Dameski, si bora kuliko maji yote ya Israeli? Je! Siwezi kujiosha ndani yake, na kuwa safi? Akageuka, akaondoka kwa hasira.
Watumishi wake wakamkaribia, wakamwambia, wakisema, Baba yangu, kama yule nabii angalikuambia kutenda jambo kubwa, usingalilitenda? Je! Si zaidi basi, akikuambia, Jioshe, uwe safi? Ndipo akashuka, akajichovya mara saba katika Yordani sawasawa na neno lake yule mtu wa Mungu; naye nyama ya wmili wak eikarudi ikawa kama nyam aya mwili wa mtoto mchanga, akawa safi.
Akamrudia yule mtu wa Mungu, yeye na mafuatano yake yote. Akaja, akasimama mbele yake; akasema, Sasa tazama, najua ya kwamba hakuna Mungu duniani mwote, ila katika Israeli, basi nakuomba upokee mbaraka kwa mtumwa wako.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 42:1-2, 43:3-4 (K) 42:3

(K) Nafsi yangu inamwonea kiu Mungu, Mungu aliye hai, Lini nitakapokuja nionekane mbele za Mungu.

Kama ayala aioneavyo shauku mito ya maji.
Vivyo hivyo nafsi yangu inakuonea shauku, Ee Mungu. (K)

Nafsi yangu inamwonea kiu Mungu, Mungu aliye hai,
Lini nitakapokuja nionekane mbele za Mungu? (K)

Niletewe nuru yako na kweli yako ziniongoze,
Zinifikishe kwenye mlima wako mtakatifu
Na hata maskani yako. (K)

Hivyo nitakwenda madhabahuni kwa Mungu,
Kwa Mungu aliye furaha yangu na shangwe yangu. (K)


SHANGILIO
Yn. 8:12

Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, asema Bwana, Yeye anifuataye, atakuwa na nuru ya uzima.


INJILI
Lk. 4:24-30

Yesu alifika Nazareti akawaambia makutano hekaluni: Amin, nawaambia ya kuwa, Hakuna nabii mwenye kukubaliwa katika nchi yake mwenyewe. Lakini, kwa hakika nawaambia, Palikuwa na wajane wengi katika nchi ya Israeli zamani za Eliya, wakati mbingu zilipofungwa miaka mitatu na miezi sita, njaa kuu ikaingia nchi nzima; wala Eliya hakutumwa kwa mmojawapo, ila kwa mjane mmoja wa Sarepta katika nchi ya Sidoni. Tena, palikuwa na weny eukoma wengi katika Israeli zamani za nabii Elisha, wala hapana aliyetakazwa ila Naamani, mtu wa Shamu.

Wakajaa ghadhabu wote waliokuwa katika sinagogi walipoyasikia hayo. Wakaondoka wakamtoa nje ya mji, wakampeleka mpaka ukingo wa kilima ambacho mji wao umejengwa juu yake, wapate kumtupa chini; lakini yeye alipiita katikati yao, akaenda zake.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. eadings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

UNA KIU?



“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Jumapili, Machi 8, 2026
Juma la 3 la Kwaresima

Kut 17: 3-7;
Zab 95: 1-2, 6-9;
Rum 5: 1-2, 5-8;
Yn 4: 5-42.


UNA KIU?


 “Gods must be crazy” Ni jina la filamu na ni juu ya watu walioko katika Jangwa la Kalahari. Filamu hii inaonesha wazoefu wa jangwa. Mmoja wa watu hawa alitembelea mabubujiko ya maji ya Tungela (maporomoko makubwa ya maji Afrika), huko Afrika kusini. Alishangazwa kuona maji makubwa yanashuka kutoka juu. Alisimama pale kwa masaa akishangaa. Hawa watu waliopo Kalahari walizoea kukusanya maji kutoka katika majani (umande) au kupata maji kutoka katika aina ya mmea ambao shina lake huwa na maji, ili kupooza kiu yao. Kama ilivyo katika simulizi hilo, lirtujia ya leo ya Domini ya tatu ya Kwaresima inatuonesha kwamba sisi wote tuna kiu. Watu wana kiu ya fedha, anasa, madaraka, na mali, na hata kama akipata nyingi, bado kiu ni kubwa. Katika hali nyingine kuna “maji ya uzima” upande mwingine ndani ya Yesu Kristo. Tunapojiandaa wenyewe kuingia katika mafumbo ya mateso, kifo na ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo kipindi hiki cha Kwaresima, tunaitwa leo tutulize kiu yetu ya kiroho na kutuliza kiu ya Yesu anayezitafuta roho zetu na ana zisubiri zirudi kwake. Yesu alipata kiu ya mwanadamu kumrudia Mungu, na hivyo akasema pale msalabani “Nina kiu”.

Katika somo la kwanza tunaona Waisraeli wanao lalamika. Watu hawa hawa waliovushwa salama kutoka katika utumwani huko Misri, na waliokuwa wakitembea kwa uhuru kuelekea Nchi ya ahadi. Kwanza kabisa walilalamika kuhusu chakula, Mungu akawapa mana, mkate kutoka mbinguni. Hata baada ya kuona muujiza huu bado hawaja uamini upendo wa Mungu. Wakaanza kukusanya zaidi ya mahitaji yao, lakini yote iliharibika siku iliofuata. Alafu wakaanza kulalamika kwasababu ya maji. Pamoja na hilo Mungu akafanya muujiza mwingine akawapa maji. Lakini Israeli hakujifunza kumtuminia Mungu. Mwanadamu ni kiumbea ambaye haridhiki. Mahitaji yetu daima tunaona hayatoshi, yanaendelea kuongezeka daima. Ni kama vile kula chumvi, unahisi kiu kila wakati, alafu baadae unakula tena chumvi unahisi kiu tena.

Katika somo la Injili tunamuona huyu Mwanamke msamaria ambaye pia alikuwa akiishi maisha yake yasio pendeza. Alikuwa katika kisima ili kutuliza kiu yake ya kila siku. Alikuwa anajiribu kutuliza kiu ya mwili wake kwa kila aina ya anasa. Lakini kila siku alikuwa akirudi katika kisima kwa ajili ya maji. Yeye kama ilivyo kwa wanadamu wote ni lazima alisimama nakuuliza “hivi kuna aina ya maji ambayo nikinywa sintaona kiu tena?”. Mt. Agustino anatoa jibu anavyosema “mioyo yetu haitatulia …hadi itakapo tulia kwako Bwana Yesu”

Yesu alikuwa njiani kuelekea Yerusalemu kwa kupitia Samaria. Watu wasamaria walionekana kama Wayahudi wasio faa au Wayahudi waliochanganyika. Hawakuwa wakichukuliwa kama sehemu ya jamii ya Wayahudi. Hata tunaona Yesu anakutana na Mwanamke Msamaria. Huyu Mwanamke alikuja katika kisima kuja kuchota maji saa sita mchana. Hii ilikuwa sio kawaida kwasababu, wanawake walikuja kuchota maji wakiwa katika makundi tena ikiwa ni hasubuhi au jioni. Huyu mwanamke inaonekana alipenda kuwakwepa wenzake pengine kwasababu ya tabia ya maisha yake ambayo Yesu alimwambia baadae. Yesu akiwa ni Myahudi anamuomba maji ya kunywa. Alikuwa na mazunguzo naye ambayo yalimlenga kutoka katika mazungumzo ya maji ya kawaida hadi kwenye maji ya uzima, kutoka katika kiu ya kidunia hadi kiu ya kiroho. Anashindwa kumtambua Yesu hapo mwanzo, na Yesu anirarua dhamiri yake kwa kufunua ukweli wa maisha yake. Hili lilikuwa rahisi kwake kupokea neema ya Mungu. Yesu anamsaidia katika hali ya kukuwa na kutambua kumwadudu na hapo anamtambua Yesu kama Masiha. Baada ya kumtabua Yesu, analeta kijiji kizima kwake. Mwanamke ambaye alikuwa amekataliwa na jamii anakuwa chombo cha Mungu cha kuwaleta wanakijiji kwa Yesu. Alikuja kuchukua maji ya kawaida akarudi na maji ya uzima. Yesu hakunywa hata tone moja la maji, lakini kiu yake ilitulizwa kwa kupata roho moja kwa ajili yake.

Yesu alijua yote kuhusu huyu Mwanamke lakini alitaka kumpa maji ya uzima. Alitaka kuzima kiu ambayo yeye alikuwa nayo rohoni mwake. Alivyokuwa akiongea naye, na kuanza kumsikiliza kiu yake ilianza kuzimwa. Ilianza kuzimwa kwasababu ndicho alichohitaji, tunachohitaji wote, ni upendo huu kamili na kukubaliwa na Yesu, ambao Yesu anautoa mwenyewe. Alitoa kwake, na anataka kuutoa kwetu pia. Cha kushangaza Mama huyu aliondoka na kuacha “mtungi”. Hakuchukua maji aliokuwa amekuja kuchukua. Au alichukuwa? Katika hali hii ya kuacha mtungi ni alama kwamba kiu yake ilikuwa imezimwa kwa kukutana na Yesu. Hakuwa tena na kiu, Yesu alizima kiu yake.

Katika kuishi kwetu kila siku, tunajikuta tukimwacha Mungu na kutafuta mambo yanayo pita. Tunafatilia tukitafuta maana katika hivyo vitu lakini tunakuta hamna, ni utupu ndani yake. Tutafakari juu ya kiu isiopingika tulio nayo ndani mwetu. Tukisha itambua, tuelekeze dhamiri zetu kumwelekea Yesu ili azime kiu yetu kwa maji ya uzima. Tukifanya hivi, tutaacha mitungi mingi ambayo kwakweli haizimi kiu yetu.

Sala: Bwana, wewe ni maji ya uzima ambayo roho yangu inatafuta. Ninakuomba nikutane na wewe katika maisha yangu, katika aibu yangu na maumivu ya moyo. Ninaomba nikutane na upendo wako, upole wako na kukukubali sasa, ninaomba upendo wako uwe chanzo cha maisha yangu ndani yako. Yesu nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MACHI 8, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 8, 2026
JUMAPILI YA 3 YA KWARESIMA

MWANZO:
Zab. 25:15 – 16

Macho yangu humwelekea Bwana daima, naye atanitoa miguu yangu katika wavu. Uniangalie na kunifadhili, maana mimi ni mkiwa na mteswa.


SOMO 1
Kut. 17:3 – 7

Watu wakawa na kiu huko; nao wakamnung’unikia Musa, wakasema, Mbona umetupandisha kutoka Misri, kutuua sisi na watoto wetu na wanyama wetu kwa kiu? Musa akamlilia Bwana, akisema, Niwatendee nini watu hawa? Bado kidogo nao watanipiga kwa mawe.

Bwana akamwambia Musa, Pita mbele ya watu, ukawachukue baadhi ya wazee wa Israeli pamoja nawe; na ile fimbo yako ambayo uliupiga mto kwayo, uitwae mkononi mwako, ukaende. Tazama, nitasimama mbele yako huko, juu ya lile jabali katika Horebu; nawe utalipiga jabali, na maji yatatoka, watu wapate kunywa.

Musa akafanya hivyo mbele ya wazee wa Israeli. Akapaita mahali pale jina lake Masa, na Meriba; kwa sababu ya mateto ya wana wa Israeli, na kwa sababu walimjaribu Bwana, wakisema, Je! Bwana yu kati yetu au sivyo?

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 95:1 – 2, 6 – 9 (K) 8

(K) Ingekuwa heri leo msikie sauti yake!
Msifanye migumu mioyo yenu.

Njoni, tumwimbie Bwana,
Tumfanyie shangwe mwamba wa wokovu wetu.
Tuje mbele zake kwa shukrani,
Tumfanyie shangwe kwa zaburi. (K)

Njoni, tuabudu, tusujudu,
Tupige magoti mbele za Bwana aliyetuumba.
Kwa maana ndiye Mungu wetu,
Na sisi tu watu wa malisho yake,
Na kondoo za mkono wake. (K)

Ingekuwa heri leo msikie sauti yake!
Msifanye migumu mioyo yenu;
Kama vile huko Meriba,
Kama siku ya Masa Jangwani.
Hapo waliponijaribu baba zenu,
Wakanipima, wakayaona matendo yangu. (K)


SOMO 2
Ru. 5:1 – 2, 5 – 8

Basi tukiisha kuhesabiwa haki itokayo katika Imani, na tuwe na Amani kwa Mungu, kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo. Ambaye kwa yeye tumepata kwa njia ya Imani kuifikia neema hii ambayo tunasimama ndani yake; na kufurahi katika tumaini la utukufu wa Mungu.

Na tumanini halitahayarishi; kwa maana pendo la Mungu limekwisha kumiminwa katika mioyo yetu na Roho Mtakatifu tuliyepewa sisi. Kwa maana hapo tulipokuwa hatuna nguvu, wakati ulipotimia, Kristo alikufa kwa ajili ya waovu. Kwa kuwa ni shida mtu kufa kwa ajili ya mtu mwenye haki; lakini yawezekana mtu kuthubutu kufa kwa ajili ya mtu aliye mwema. Bali Mungu aonyeshe pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi.


SHANGILIO
Yn. 4:15

Bwana, hakika wewe ndiwe Mwokozi wa ulimwengu,
unipe maji yale ya uzima, nisione kiu kamwe.


INJILI
Yn. 4:5 – 42

Yesu alifika kunako mji wa Samaria, uitwao Sikari, karibu na lile shamba ambalo Yakobo alimpa Yusufu, mwanawe. Na hapo palikuwa na kisima cha Yakobo. Basi Yesu, kwa sababu amechoka kwa safari yake, akaketi vivi hivi kisimani. Nayo ilikuwa yapata saa sita. Akaja mwanamke Msamaria kuteka maji. Yesu akamwambia, Nipe maji ninywe. Kwa maana wanafunzi wake wamekwenda mjini kununua chakula. Basi yule mwanamke Msamaria akamwambia, Imekuwaje wewe Myahudi kutaka maji kwangu, nami ni mwanamke Msamaria? (maana Wayahudi hawachangamani na Wasamaria).

Yesu akajibu, akamwambia, Kama ungalijua karama ya Mungu, naye ni nani akuambiaye, Nipe maji ninywe, ungalimwomba yeye, naye angalikupa maji yaliyo hai.

Yule mwanamke akamwambia, Bana, huna kitu cha kutekea, na kisima ni kirefu; basi umeyapata wapi hayo maji yaliyo hai? Je! Wewe u mkubwa kuliko baba yetu, Yakobo, aliyetupa kisima hiki, naye mwenyewe akanywa maji yake, na wanawe pia, na wanyama wake?

Yesu akajibu, akamwambia, Kila anyway maji haya ataona kiu tena; walakini yeyote atakayekunywa maji yale nitakayompa mimi hataona kiu milele; bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa milele.

Yule mwanamke akamwambia, Bwana, unipe maji hayo, nisione kiu, wala nisije hapa kuteka.

Yesu akamwambia, Nenda kamwite mumeo, uje naye hapa. Yule mwanamke akajibu, akasema, Sina mume. Yesu akamwambia, Umesema vema, Sina mume; kwa maana umekuwa na waume watano, naye uliye naye sasa siye mume wako; hapo umesema kweli. Yule mwanamke akamwambia, Bwana, naona ya kuwa u nabii! Baba zetu waliabudu katika mlima huu, nanyi husema ya kwamba huko Yerusalemu ni mahali patupasapo kuabudia. Yesu akamwambia, Mama, unisadiki, saa inakuja ambayo hamtamwabudu Baba katika mlima huu, wala kule Yerusalemu. Ninyi mnaabudu msichokijua; sisi tunaabudu tukijuacho; kwa kuwa wokovu watoka kwa Wayahudi. Lakini saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu. Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli. Yule mwanamke akamwambia, Najua ya kuwa yuaja Masihi, (aitwaye Kristo); naye atakapokuja, yeye atatufunulia mambo yote. Yesu akamwambia, Mimi ninayesema nawe, ndiye.

Mara hiyo wakaja wanafunzi wake, wakastaajabu kwa sababu alikuwa akisema na mwanamke; lakini hakuna aliyesema, Unatafuta nini? Au, Mbona unasema naye? Basi yule mwanamke akauacha mtungi wake, akaenda zake mjini, akamwambia watu, Njoni, mtazame mtu aliyeniambia mambo yote niliyoyatenda. Je! Haimkini huyu kuwa ndiye Kristo? Basi wakatoka mjini, wakamwendea.

Huko nyuma wanafunzi wakamsihi wakisema, Rabi, ule. Akawaambia, Mimi ninacho chakula msichokijua ninyi. Basi wanafunzi wake wakasemezana, Je! Mtu amemletea chakula? Yesu akawaambia, Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake. Hamsemi ninyi, Bado miezi mine, ndipo yaja mavuno? Tazama, mimi nawaambieni, Inueni macho yenu myatazame mashamba, ya kuwa yamekwisha kuwa meupe, tayari kwa mavuno. Naye avunaye hupokea mshahara, na kukusanya matunda kwa uzima wa milele, ili yeye apandaye na yeye avunaye wapate kufurahi pamoja. Kwa maana hapo neno hilo huwa kweli, Mmoja hupanda akavuna mwingine. Mimi naliwatuma myavune yale msiyoyataabikia; wengine walitaabika, nanyi mmeingia katika taabu yao.

Na katika mji ule Wasamaria wengi walimwamini kwa sababu ya neno la yule mwanamke, aliyeshuhudia kwamba, Aliniambia mambo yote niliyoyatenda. Basi wale Wasamaria walipomwendea, walimsihi akae kwao; naye akakaa huko siku mbili. watu wengi zaidi wakaamini kwa sababu ya neno lake. Wakamwambia yule mwanamke, Sasa tunaamini, wala si kwa sababu ya maneno yako tu; maana sisi tumesikia wenyewe, tena twajua ya kuwa hakika huyu ndiye Mwokozi wa ulimwengu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUMRUDIA MUNGU!



“ASALI ITOKAYO MWMABANI”
Tafakari ya Kwaresima
Jumamosi, Machi 7, 2026
Juma la 2 la Kwaresima

Mika 7:14-15,18-20;
Zab 103;1-4, 9-12;
Lk 15: 1-3, 11-32


KUMRUDIA MUNGU!


Katika mfano wa Mwana mpotevu tunaona ujasiri wa huyu Mwana kwa kuchagua kurudi kwa Baba yake. Ni kweli, alitambua udhaifu wake na akaamua kurudi kwa Baba yake kuomba msamaha na kumuomba amfanye kama mmoja wa wafanyakazi wake. Alifanikiwa kurudi.! Swali la kujibu “kwanini?”

Ni vyema kusema kwamba huyu mtoto alirudi kwa Baba yake, kwanza kabisa kwasababu alitambua kutoka moyoni mwake tabia ya Baba yake. Baba alikuwa Baba mwema. Alionyesha kujali na kuwa na upendo kwa mtoto daima katika maisha yake. Ingawaje mtoto alimkimbia Baba yake, haikubadilisha ukweli kwamba yeye alitambua kuwa Baba yake alikuwa mtu mwema na kwamba anampenda. Pengine hakutambua ni kwa jinsi ghani, hadi alipo tambua mwenyewe. Ni wazi kwamba ni kwasababu ya utambuzi huu kutoka moyoni mwake unaompa ujasiri wa kurudi kwa Baba kwa matumaini ya upendo wa Baba yake.

Hili linafunua kuwa, upendo wa kweli unafanya kazi. Daima unafanya kazi. Hata kama mtu akikataa upendo mtakatifu tunaompa, lazima daima una ongeza kitu katika maisha yao. Upendo wa kweli usio na masharti ni vigumu kuukataa na kuutupilia mbali. Mwana mpotevu alitambua hili, na sisi pia tunapaswa kuwa hivyo. Huu ndio upendo alionao Baba yetu wa Mbinguni kwa kila mtu. Yeye sio Mungu mkali na mgumu. Ni Mungu anayependa kuturudisha kwake na kutupatanisha naye. Anafurahi tunapo mrudia na kuomba mahitaji yetu kwake. Ingawaje tuna wasi wasi, yeye hana wasi wasi kwa upendo wake, daima anatusubiri sisi, na sisi wenyewe kutoka ndani kabisa tunatambua hilo.

Kwaresima ni kipindi kizuri sana kwa sakramenti ya kitubio. Na sakramenti hiyo ndio ujumbe wote katika mfano huu. Ni mfano wa sisi kwenda kwa Baba yetu na dhambi zetu na atatupokea kwa huruma. Inaweza kuogopesha na kuwa na wasi wasi kwenda kwenye sakramenti ya kitubio, lakini tukiingia katika sakramenti hiyo kwa uaminifu na katika kweli, tunaona furaha tunayopata na Amani kuu. Tunajisikia Amani na kuacha mizigo iliyo tuelemea rohoni. Mungu, anatukimbilia, na kunyanyua mizigo yetu na kuitupa nyuma yetu. Usikubali kipindi hichi cha kwaresima kipite bila kuungama! Hakuna na tena, wala hakuna sehemu nyingine waweza kupata furaha hii ya kuunganika na Mungu katika kweli. Usijioneee huruma kwa kujibembeleza kwamba nitamweleza tu Mungu mwenyewe nikiwa chumbani kwangu. Nenda kaungame katika hali ya uaminifu na kweli kadiri ya Imani yetu. Mungu anakusubiri. Usikubali kubaki katika gereza la dhambi. Fanya uamuzi kama Mwana mpotevu.

Sala: Baba, nilienda kinyume na wewe na kufuata njia zangu mwenyewe. Sasa ni muda wa kurudi kwako katika hali ya uwazi na uaminifu wa moyo. Ninaomba unipe ujasiri huo ili niweze kukumbatia sakaramenti ya kitubio. Yesu nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com