Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MTAZAMENI MTU!


“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Ijumaa, Aprili 3, 2026,


IJUMAA KUU

Isa 52:13-53;
Zab 31:2,6,12-13,15-17,25
Ebr 4:14-16, 5:7-9;
Yn 18:1 - 19:42


MTAZAMENI MTU!


Ni Ijumaa kuu, siku ambayo ilikuwa muhimu sana kwa Yesu kwa lengo lake la kuja ulimwenguni. Maisha yake yote, mafundisho yake yote, kila neno la msamaha au changamoto hakuna lolote linalo leta maana kama bila msalaba. Na leo tunaitwa kujiunga na mamilioni ya watu duniani kote kwa kumtazama Mwanakondoo wa Mungu aliye sulubiwa kwa ajili ya dhambi zetu.

Kwa maneno ya Pilato. “Mtazameni mtu”, tumtazame Kristo, tukitazama na kurudi katika unyenyekevu wake wa kuzaliwa katika zizi. Tukikumbuka miaka yake aliokuwa akikuwa katika hekima na kimo. Tumuone katika unyenyekevu wake, muamini na kujikabidhi kwa Baba yake, alivyotembea na Mungu katika kila hatua ya maisha yake. Tazama aliyesali mikononi mwako naiweka roho yangu. Tazama sala hii aliyoisema wakati akivuta pumzi yake ya mwisho ilivyokuwa, lakini maisha yake yote yaliojikita ndani ya Baba yake.

Njooni na “tazama aliyesema naona kiu”, tazama aliye ona njaa, kiu, ndani ya mwili na roho. Hakuja ili kutumikiwa bali kutumikia. Aliosha miguu ya rafiki zake. Alikula chakula pamoja na wenye dhambi na kuwashika wakoma. Alitoa maisha yake siku baada ya siku kwa ajili ya watu wake. Na tazama sasa ana sulubishwa na kukataliwa. Alipigiliwa misumari msalabani na tazama anayatoa maisha yake.

Tazama mfalme wako, ametobolewa na damu inatoka miguuni, tunapiga magoti, tukitangaza siku ambayo kila mtu atapiga magoti mbele zake. Tumuangalie huyu mwalimu alivyo haribiwa, na kumuona mfalme wako wa milele, ambaye kwa njia yake vitu vyote viliumbwa. Mtazame huyu Kuhani mkuu amekaa mbinguni akikuombea kwasababu ya dhambi zako kama alivyofanya pale msalabani. Mtazame Yesu. Anga lina giza. Dunia inatetemeka. Miamba ina pasuka. Mwili wake umelala. Ukuu wake umekuwa tupu kutokana na sababu. Hapa yupo Mfalme wako.

Masomo yana andika maneno saba ya Yesu ya mwisho. Tuya tazame.

1. “Bwana, uwasamehe kwasababu hawajui watendalo”. Akiwa ametundikwa msalabani akiwa anavumilia ubaya wa wengine, Yesu aliongea maneno ya Msamaha. Alikiri kwamba hata hawa waliomsulubisha hawakuhusika asilimia zote. Hali hii ya unenyenyekevu wa Yesu unatambua undani wa huruma yake. Inaonesha kwamba hakufa akiwa na hasira au chuki, bali kama sadaka safi. Je, upo tayari kusema maneno haya? Unaweza kuvuta hisia ya watu waliokuumiza ukaita sauti ya Baba awasamehe wote?

2. “Amini, nakuambia utakuwa nami Paradiso”. Ni zawadi ilikuwa kuu namna ghani kuwa karibu na mkombozi wa Ulimwengu, kushiriki katika mateso ya Kristo katika hali halisi. Mwizi huyu alipata zawadi ya kwanza ya kufurahia ukombozi wa Yesu uliopatikana pale msalabani. Yesu anatupa sisi pia uhakika. Anatupatia ukombozi. Anatupatia sisi ukombozi huu tukiwa katikati ya mateso na dhambi zetu. Je, waweza kuisikia sauti yake ikikuita kushiriki katika maisha yake ya milele?

3. “Mama, tazama mwanao”. Hapa, Yesu kwa kufa msalabani anamkabidhi Mama yake mzazi kwa Yohane, alimkabidhi kwa kila mmoja wetu. Umoja wetu na Yesu unatufanya tuwe watu katika familia yake, na hivyo, watoto wa Mama yake mwenyewe. Je, unamkubali mama wa Yesu kama Mama yako wa kiroho?

4. “Mungu wangu, Mungu wangu, kwanini umeniacha?”. Yesu hakuwa ameachwa bali aliruhusu kuhisi kuachwa na Baba yake katika hali ya Kibinadamu. Aliruhusu mwenyewe aweze kutambua na kuelewa madhara ya dhambi. Kwahiyo, anatambua kila tunachopitia tukiwa katika uchungu. Na yupo nasi katika majaribu akitusaidia kusonga mbele kwa Imani na kumwamini Baba.

5. “Nina kiu”. Yesu alihisi kiu kwa wakati huo na alihitaji maji ili kupooza, kupoteza kwake maji mwilini. Lakini zaidi ya hayo, aliona kiu kwa ukombozi wa roho zetu. Aliona kiu ya kutuita watoto wake. Aliona kiu ya mapendo yetu. Tuliza kiu yake siku hii ya Ijumaa kuu kwa kumpa mapendo yako.

6. “Baba, mikononi Mwako naiweka roho yangu”. Haya ni maneno ya kujikabidhi kwa Mungu kabisa. Kujikabidhi maana yake, Mungu ndiye anaye endesha yote. Maana yake kuachia mapenzi yetu na kuruhusu mapenzi ya Mungu yatawale. Na ina maana kwamba Mungu ameahidi kukubali kujikabidhi kwetu na kutuongoza kwenye mpango wake mkamilifu aliyo tuandalia.

7. “Yametimia” kutimia maana yake nini? Hii ni moja wapo ya maneno ya Yesu yanayo toa maana kwamba utume wake wa ukombozi wa dunia umetimia. Ina maana kwamba upendo wake wa sadaka aliyo itoa kwa wote. Kifo chake, tunacho kikumbuka leo, ni sadaka kamili inayo ondoa dhambi za wote. Ni zawadi iliyoje!

Tumezoea kuiona sadaka hii msalabani. Tunaona zawadi hii daima tunapo utazama msalaba. Lakini ni vizuri kutambua kwamba kuzoea kwetu misalaba daima inaweza kutufanya tukashindwa kuona sadaka hii juu ya msalaba. Ni rahisi kusahau kile ambacho Yesu alitufanyia. Tunaomba tendo hili Takatifu la Kimungu lizame ndani ya mioyo yetu. Kutambua sadaka ya Yesu alioitoa pale msalabani itatufanya sisi tupende kama yeye alivyo penda. Itatusadia kuwapenda wale waliotuumiza na kutuchukia. Upendo wake ni Kamili. Ni wa ukarimu wa kupita maelezo.

Sala: Bwana, ninajua umeona kiu ya roho yangu. Ulimalizia kile ambacho ulianzisha kwa kufa juu ya msalaba kwa ajili ya ukombozi wa ulimwengu. Nisaidie nitambue upendo wako na kuukubali katika maisha yangu. Ninakushukuru , Bwana mpendwa kwa zawadi ya damu yako Takatifu, iliomwagika kwa ukombozi wa Ulimwengu. Bwana, ninakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA IBAADA, IJUMAA KUU APRILI 3, 2026




MASOMO YA IBAADA, 
IJUMAA KUU APRILI 3, 2026


SOMO 1
Isa 52:13-53:12

Tazama, mtumishi wangu atatenda kwa busara, atatukuzwa, na kuinuliwa juu, naye atakuwa juu sana. Kama vile wengi walivyokustaajabia, (uso wake ulikuwa umeharibiwa sana zaidi ya mtu ye yote, na umbo lake zaidi ya wanadamu), ndivyo atakavyowasitusha mataifa mengi; wafalme watamfumbia vinywa vyao; maana mambo wasiyoambiwa watayaona; na mambo wasiyoyasikia watayafahamu.Ni nani aliyesadiki habari tuliyoileta? Na mkono wa Bwana amefunuliwa nani? Maana alikua mbele zake kama mche mwororo, Na kama mzizi katika nchi kavu; Yeye hana umbo wala uzuri; Na tumwonapo hana uzuri hata tumtamani. Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona. Sisi sote kama kondoo tumepotea; Kila mmoja wetu amegeukia njia yake mwenyewe; Na Bwana ameweka juu yake Maovu yetu sisi sote. Alionewa, lakini alinyenyekea, Wala hakufunua kinywa chake; Kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni, Na kama vile kondoo anyamazavyo Mbele yao wakatao manyoya yake; Naam, hakufunua kinywa chake. Kwa kuonewa na kuhukumiwa aliondolewa; Na maisha yake ni nani atakayeisimulia? Maana amekatiliwa mbali na nchi ya walio hai; Alipigwa kwa sababu ya makosa ya watu wangu. Wakamfanyia kaburi pamoja na wabaya; Na pamoja na matajiri katika kufa kwake; Ingawa hakutenda jeuri, Wala hapakuwa na hila kinywani mwake. Lakini Bwana aliridhika kumchubua; Amemhuzunisha; Utakapofanya nafsi yake kuwa dhabihu kwa dhambi, Ataona uzao wake, ataishi siku nyingi, Na mapenzi ya Bwana yatafanikiwa mkononi mwake; Ataona mazao ya taabu ya nafsi yake, na kuridhika. Kwa maarifa yake mtumishi wangu mwenye haki Atawafanya wengi kuwa wenye haki; Naye atayachukua maovu yao. Kwa hiyo nitamgawia sehemu pamoja na wakuu, Naye atagawanya nyara pamoja nao walio hodari; Kwa sababu alimwaga nafsi yake hata kufa, Akahesabiwa pamoja na hao wakosao. Walakini alichukua dhambi za watu wengi, Na kuwaombea wakosaji.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab 31:1, 5, 11-13a, 14-16, 24

(K)Ee Baba, mikononi mwako naiweka roho yangu.

Nimekukimbilia Wewe, Bwana,
Nisiaibike milele.
Kwa haki yako uniponye,
Mikononi mwako naiweka roho yangu;
Umenikomboa, Ee Bwana, Mungu wa kweli. (K)

Kwa sababu ya watesi wangu nimekuwa laumu,
Naam, hasa kwa jirani zangu;
Na kitu cha kutisha kwa rafiki zangu;
Walioniona njiani walinikimbia. (K)

Nimesahauliwa kama mfu asiyekumbukwa;
Nimekuwa kama chombo kilichovunjika.
Maana nimesikia masingizio ya wengi;
Hofu ziko pande zote. (K)
Lakini mimi nakutumaini Wewe, Bwana,
Nimesema, Wewe ndiwe Mungu wangu.
Nyakati zangu zimo mikononi mwako;
Uniponye na adui zangu, nao wanaonifuatia. (K)

Umwangaze mtumishi wako
Kwa nuru ya uso wako;
Uniokoe kwa ajili ya fadhili zako.
Iweni hodari, mpige moyo konde,
Ninyi nyote mnaomngoja Bwana. (K)


SOMO 2
Ebr 4:14-16, 5:7-9

Basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana maungamo yetu. Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi. Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji. Yeye, siku hizo za mwili wake, alimtolea yule, awezaye kumwokoa na kumtoa katika mauti, maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi, akasikilizwa kwa jinsi alivyokuwa mcha Mungu; na, ingawa ni Mwana, alijifunza kutii kwa mateso hayo yaliyompata; naye alipokwisha kukamilishwa, akawa sababu ya wokovu wa milele kwa watu wote wanaomtii;

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


INJILI
Yn 18:1 - 19:42

Alipokwisha kusema hayo, Yesu alitoka pamoja na wanafunzi wake kwenda ng'ambo ya kijito Kedroni, palipokuwapo bustani; akaingia yeye na wanafunzi wake. Naye Yuda, yule aliyetaka kumsaliti, alipajua mahali pale; kwa sababu Yesu alikuwa akienda huko mara nyingi pamoja na wanafunzi wake. Basi Yuda, akiisha kupokea kikosi cha askari na watumishi waliotoka kwa wakuu wa makuhani na Mafarisayo, akaenda huko na taa na mienge na silaha. Basi Yesu, hali akijua yote yatakayompata, akatokea, akawaambia, Ni nani mnayemtafuta? Wao wakamjibu, Ni Yesu Mnazareti. Yesu akawaambia, Ni mimi. Yuda naye aliyemsaliti alikuwa amesimama pamoja nao. Basi alipowaambia, Ni mimi, walirudi nyuma, wakaanguka chini. Basi akawauliza tena, Mnamtafuta nani? Wakasema, Yesu Mnazareti. Yesu akajibu, Nimekwisha kuwaambieni ya kwamba ni mimi; basi ikiwa mnanitafuta mimi, waacheni hawa waende zao. Ili litimizwe lile neno alilolisema, Wale ulionipa sikumpoteza hata mmoja wao. Basi Simoni Petro alikuwa na upanga, akaufuta, akampiga mtumwa wa Kuhani Mkuu, akamkata sikio la kuume. Na yule mtumwa jina lake ni Malko. Basi Yesu akamwambia Petro, Rudisha upanga alani mwake; je! Kikombe alichonipa Baba, mimi nisikinywee? Basi wale askari na yule jemadari na wale watumishi wa Wayahudi walimkamata Yesu, wakamfunga. Wakamchukua kwa Anasi kwanza; maana alikuwa mkwewe Kayafa, yule aliyekuwa Kuhani Mkuu mwaka ule. Naye Kayafa ndiye yule aliyewapa Wayahudi lile shauri ya kwamba yafaa mtu mmoja afe kwa ajili ya watu. Wakamfuata Yesu, Petro na mwanafunzi mwingine. Na mwanafunzi huyo alikuwa amejulikana na Kuhani Mkuu, akaingia pamoja na Yesu katika behewa ya Kuhani Mkuu. Lakini Petro akasimama nje mlangoni. Basi yule mwanafunzi mwingine aliyejulikana na Kuhani Mkuu akatoka, akasema na mngoja mlango, akamleta Petro ndani. Basi yule kijakazi, aliyekuwa mngoja mlango, akamwambia Petro, Wewe nawe, je! Hu mwanafunzi mmojawapo wa mtu huyu? Naye akasema, Si mimi. Na wale watumwa na watumishi walikuwa wakisimama, wamefanya moto wa makaa; maana ilikuwa baridi; wakawa wakikota moto. Petro naye alikuwapo pamoja nao, anakota moto. Basi Kuhani Mkuu akamwuliza Yesu habari za wanafunzi wake, na habari za mafundisho yake. Yesu akamjibu, Mimi nimesema na ulimwengu waziwazi; sikuzote nalifundisha katika sinagogi na katika hekalu, wakusanyikapo Wayahudi wote; wala kwa siri mimi sikusema neno lo lote. Ya nini kuniuliza mimi? Waulize wale waliosikia ni nini niliyowaambia; wao wanajua niliyoyanena. Basi aliposema hayo, mtumishi mmojawapo aliyesimama karibu alimpiga Yesu kofi akisema, Wamjibu hivi Kuhani Mkuu? Yesu akamjibu, Kama nimesema vibaya, ushuhudie ule ubaya; bali kama nimesema vema, wanipigia nini? Basi Anasi akampeleka hali amefungwa kwa Kayafa, Kuhani Mkuu. Na Simoni Petro alikuwa akisimama huko, anakota moto. Basi wakamwambia, Wewe nawe, je! Hu mwanafunzi wake mmojawapo? Naye akakana, akasema, Si mimi. Mtumwa mmojawapo wa Kuhani Mkuu, naye ni jamaa yake yule aliyekatwa sikio na Petro, akasema, Je! Mimi sikukuona wewe bustanini pamoja naye? Basi Petro akakana tena, na mara akawika jimbi. Kisha wakamchukua Yesu kutoka kwa Kayafa mpaka Praitorio, nayo ikawa alfajiri;lakini wao wenyewe hawakuingia ndani ya ile praitorio,wasije wakanajisika,bali wapate kuila Pasaka. Basi Pilato akawatokea nje, akasema, Ni mashitaka gani mnayoleta juu ya mtu huyu? Wakajibu, wakamwambia, Kama huyu asingekuwa mtenda mabaya, tusingemleta kwako. Basi Pilato akawaambia, Haya! Mtwaeni ninyi, mkamhukumu kwa ile torati yenu! Wayahudi wakamwambia, Sisi hatuna ruhusa ya kuua mtu. Ili litimie lile neno lake Yesu alilolisema, akionyesha ni mauti gani atakayokufa. Basi Pilato akaingia tena ndani ya Praitorio, akamwita Yesu, akamwambia, Je! Wewe ni Mfalme wa Wayahudi? Yesu akamjibu, Wewe wasema hivi kwa nafsi yako, au watu wengine walikuambia habari zangu? Pilato akajibu, Ama! Ni Myahudi mimi! Taifa lako na wakuu wa makuhani ndio waliokuleta kwangu. Umefanya nini? Yesu akajibu, Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa wa ulimwengu huu, watumishi wangu wangenipigania, nisije nikatiwa mikononi mwa Wayahudi. Lakini ufalme wangu sio wa hapa. Basi Pilato akamwambia, Wewe u mfalme basi? Yesu akajibu, Wewe wasema, kwa kuwa mimi ni mfalme. Mimi nimezaliwa kwa ajili ya haya, na kwa ajili ya haya mimi nalikuja ulimwenguni, ili niishuhudie kweli. Kila aliye wa hiyo kweli hunisikia sauti yangu. Pilato akamwambia, Kweli ni nini? Naye akiisha kusema neno hilo akawatokea Wayahudi tena, akawaambia, Mimi sioni hatia yo yote kwake. Lakini kwenu kuna desturi ya mimi kuwafungulia mtu mmoja wakati wa Pasaka; basi, mwapenda niwafungulie Mfalme wa Wayahudi? Basi wakapiga kelele tena kusema, Si huyu, bali Baraba. Naye yule Baraba alikuwa mnyang'anyi.Basi ndipo Pilato alipomtwaa Yesu, akampiga mijeledi. Nao askari wakasokota taji ya miiba, wakamtia kichwani, wakamvika vazi la zambarau. Wakawa wakimwendea, wakisema, Salamu! Mfalme wa Wayahudi! Wakampiga makofi. Kisha Pilato akatokea tena nje, akawaambia, Mtu huyu namleta nje kwenu, mpate kufahamu ya kuwa mimi sioni hatia yo yote kwake. Ndipo Yesu alipotoka nje, naye amevaa ile taji ya miiba, na lile vazi la zambarau. Pilato akawaambia, Tazama, mtu huyu! Basi wale wakuu wa makuhani na watumishi wao walipomwona, walipiga kelele wakisema, Msulibishe! Msulibishe! Pilato akawaambia, Mtwaeni ninyi basi, mkamsulibishe; kwa maana mimi sioni hatia kwake. Wayahudi wakamjibu, Sisi tunayo sheria, na kwa sheria hiyo amestahili kufa, kwa sababu alijifanya kuwa Mwana wa Mungu. Basi Pilato aliposikia neno hilo, akazidi kuogopa. Akaingia tena ndani ya ile Praitorio, akamwambia Yesu, Wewe umetokapi? Lakini Yesu hakumpa jibu lo lote. Basi Pilato akamwambia, Husemi nami? Hujui ya kuwa mimi nina mamlaka ya kukufungua, nami nina mamlaka ya kukusulibisha? Yesu akamjibu, Wewe hungekuwa na mamlaka yo yote juu yangu, kama usingepewa kutoka juu; kwa hiyo yeye aliyenitia mikononi mwako yuna dhambi iliyo kubwa zaidi. Na tangu hapo Pilato akatafuta kumfungua; lakini Wayahudi wakapiga makelele wakisema, Ukimfungua huyu, wewe si rafiki yake Kaisari; kila mtu ajifanyaye kuwa mfalme humfitini Kaisari. Basi Pilato, aliposikia maneno hayo, akamleta Yesu nje, akaketi juu ya kiti cha hukumu, mahali paitwapo Sakafu ya Mawe, au kwa Kiebrania, Gabatha. Nayo ilikuwa Maandalio ya pasaka, yapata saa sita. Akawaambia Wayahudi, Tazama, Mfalme wenu! Basi wale wakapiga kelele, Mwondoshe! Mwondoshe! Msulibishe! Pilato akawaambia, Je! Nimsulibishe mfalme wenu! Wakuu wa makuhani wakamjibu, Sisi hatuna mfalme ila Kaisari. Basi ndipo alipomtia mikononi mwao ili asulibiwe; nao wakampokea Yesu. Akatoka, hali akijichukulia msalaba wake, mpaka mahali paitwapo Fuvu la Kichwa, au kwa Kiebrania, Golgotha. Wakamsulibisha huko, na wengine wawili pamoja naye, mmoja huku na mmoja huku, na Yesu katikati. Naye Pilato akaandika anwani, akaiweka juu ya msalaba, imeandikwa, YESU MNAZARETI, MFALME WA WAYAHUDI. Basi anwani hiyo waliisoma wengi katika Wayahudi; maana mahali pale aliposulibiwa Yesu palikuwa karibu na mji; nayo iliandikwa kwa Kiebrania, na Kirumi, na Kiyunani. Basi wakuu wa makuhani na Wayahudi wakamwambia Pilato, Usiandike, Mfalme wa Wayahudi; bali ya kwamba yule alisema, Mimi ni mfalme wa Wayahudi. Pilato akajibu, Niliyoandika nimeyaandika. Nao askari walipomsulibisha Yesu, waliyatwaa mavazi yake, wakafanya mafungu manne, kwa kila askari fungu lake; na kanzu nayo. Basi kanzu ile haikushonwa, ilikuwa imefumwa yote pia tangu juu. Basi wakaambiana, Tusiipasue, lakini tuipigie kura, iwe ya nani. Ili litimie andiko lile linenalo, Waligawanya nguo zangu, Na vazi langu wakalipigia kura. Basi ndivyo walivyofanya wale askari. Na penye msalaba wake Yesu walikuwa wamesimama mamaye, na umbu la mamaye, Mariamu wa Klopa, na Mariamu Magdalene. Basi Yesu alipomwona mama yake, na yule mwanafunzi aliyempenda amesimama karibu, alimwambia mama yake, Mama, tazama, mwanao. Kisha akamwambia yule mwanafunzi, Tazama, mama yako. Na tangu saa ile mwanafunzi yule akamchukua nyumbani kwake. Baada ya hayo Yesu, hali akijua ya kuwa yote yamekwisha kumalizika ili andiko litimizwe, akasema, Naona kiu. Kulikuwako huko chombo kimejaa siki; basi wakatia sifongo iliyojaa siki juu ya ufito wa hisopo, wakampelekea kinywani. Basi Yesu alipokwisha kuipokea ile siki, alisema, Imekwisha. Akainama kichwa, akaisalimu roho yake. Basi Wayahudi, kwa sababu ni Maandalio, miili isikae juu ya misalaba siku ya sabato, (maana sabato ile ilikuwa siku kubwa), walimwomba Pilato miguu yao ivunjwe, wakaondolewe. Basi askari wakaenda, wakamvunja miguu wa kwanza, na wa pili, aliyesulibiwa pamoja naye. Lakini walipomjia Yesu na kuona ya kuwa amekwisha kufa, hawakumvunja miguu; lakini askari mmojawapo alimchoma ubavu kwa mkuki; na mara ikatoka damu na maji. Naye aliyeona ameshuhudia, na ushuhuda wake ni kweli; naye anajua ya kuwa anasema kweli ili ninyi nanyi mpate kusadiki. Kwa maana hayo yalitukia ili andiko litimie, Hapana mfupa wake utakaovunjwa. Na tena andiko lingine lanena, Watamtazama yeye waliyemchoma. Hata baada ya hayo Yusufu wa Arimathaya, naye ni mwanafunzi wa Yesu, (lakini kwa siri, kwa hofu ya Wayahudi), alimwomba Pilato ruhusa ili auondoe mwili wake Yesu. Na Pilato akampa ruhusa. Basi akaenda, akauondoa mwili wake. Akaenda Nikodemo naye, (yule aliyemwendea usiku hapo kwanza), akaleta machanganyiko ya manemane na uudi, yapata ratli mia. Basi wakautwaa mwili wake Yesu, wakaufunga sanda ya kitani pamoja na yale manukato, kama ilivyo desturi ya Wayahudi katika kuzika. Na pale pale aliposulibiwa palikuwa na bustani; na ndani ya bustani mna kaburi jipya, ambalo hajatiwa bado mtu ye yote ndani yake. Humo basi, kwa sababu ya Maandalio ya Wayahudi, wakamweka Yesu; maana lile kaburi lilikuwa karibu.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

FANYENI HIVI KWA KUNIKUMBUKA MIMI!



“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Alhamisi, Aprili 2, 2026
Juma Kuu

ALHAMISI KUU

Kut 12: 1-8,11-14;
Zab116: 12-13,15-18;
1 Kor: 11:23-26;
Yn 13: 1-15


FANYENI HIVI KWA KUNIKUMBUKA MIMI!


Leo tunaanza siku tatu, muhimu katika Pasaka-maadhimisho matatu makuu ya Imani yetu Katoliki. Leo tunaanza na zawadi ya Bwana wetu ya Ekaristi Takatifu tuliopewa kwa ukuhani aliosimika. Kesho tunaingia katika fumbo la Msalaba. Na Jumamosi jioni tunaingia katika utukufu wa ufufuko wake.

Alhamisi kuu jioni, tuna adhimisha siku ambayo Yesu aliweka Ekaristi Takatifu, kwa kusema “fanyeni hivi kwa kunikumbuka mimi” Tangu siku hiyo Misa Takatifu imekuwa ikiadhimishwa mara nyingi sana katika kila pembe ya dunia kwa kutii amri ya Yesu.

Kama tungeelewa thamani na zawadi hii Takatifu, Ekaristi Takatifu! Ekaristi Takatifu ni Mungu mwenyewe katika ulimwengu huu, tuliopewa sisi kutugeuza na kutufanya tuwe tunachopokea. Ekaristi Takatifu katika ukweli halisi, inatubadilisha sisi tuwe kama Kristo mwenyewe. Tukipokea Ekaristi Takatifu tunavutwa kwenye maisha ya Kimungu ya Utatu Mtakatifu. Tunaungana na Mungu na tunapewa chakula cha uzima wa milele.

Yesu pia alioonesha mfano wa unyenyekevu wa hali ya juu na huduma ambayo tunapaswa kuitoa na kuiiga tunapo amua kumfuata na kuwa wamoja pamoja naye. Aliwaosha miguu mitume ili kuwafundisha wao na sisi kwamba mwili na damu yake tumepewa ili tuweze kupenda kama yeye alivyo penda. Ekaristi inatugeuza kuwa watumishi wa unyenyekevu wa kweli. Tunaitwa tuwahudumie ndugu zetu. Huduma hii inachukua hali mbali mbali lakini ndicho tulichoitiwa kufanya. Huduma katika unyenyekevu ni muonekano mzuri wa kueleza muunganiko wetu na Mwana wa Mungu. Ukuu unaonekana katika hali ya dunia kama kitu kizuri na cha kutamanika. Lakini leo Yesu anatupa aina nyingine ya ukuu. Alhamisi kuu, anaonesha kwamba ukuu huu katika unyenyekevu unapatikana katika huduma hii. Ili kumuiga yeye inatupasa kuacha majivuno yetu kwanza. Na hili linawezekana tunapopokea Ekaristi Takatifu tukiwa safi na wenye Imani. Ekaristi inatusaidia kuwapenda na kuwatumikia namna hii. Na kitendo hichi cha upendo na huduma kitashinda katika mioyo yetu kwa ajili ya Ufalme wa Mungu. Tukiwa tuna adhimisha Alhamisi kuu, tunapata changamoto ya kuangalia unyenyekevu wetu, na kubadilika na kujikita katika kuwahudumia wengine.

Juu ya Msalaba, alitoa maisha yake kwasababu ya dhambi zetu na kutupatanisha na Baba. Lakini kifo chake msalabani haina maana kwamba tutakwenda Mbinguni moja kwa moja. Tunapaswa kushirikiana na neema yake aliotoa pale msalabani. Na hii ndio Ekaristi iliotoka ndani yake. Yesu aliyekufa juu ya Msalaba ndiye Yesu yule yule aliye aliye juu ya altare wakati wa misa. Ambaye alilipia dhambi zetu pale msalabani ndiye yule yule anaye tupa neema zake na ukombozi juu ya altare wakati wa misa. Juu ya Msalaba Yesu alitoa sadaka kamili ambayo haina haja ya kurudiwa tena. Katika altare sadaka ile ile ya Yesu alioitoa inawekwa wazi tena kwa ajili ya ukombozi wetu. Si kwamba inarudiwa tena bali ni sadaka ile ile ya Yesu alioitoa msalabani. Inawezekana je? Ni kwasababu Mungu hafungwi na sehemu wala wakati wala historia, ndio maana sadaka inakuwa ileile. Yeye anayafanya yaliotokea wakati ule yawe tena wazi juu ya altare. Kwahiyo juu ya altare anatupa tena nguvu ya kukabili madimbwi ya dhambi na kuingia katika uwepo wake katika hali kamili. Kwa hiyo, kilicho tokea pale msalabani ndicho kinacho tokea altareni.

Ndivyo Yesu alivyo jikita katika kuleta ufalme wake kwetu. Hivyo, tutakavyo kwenda kanisani leo, tuangalie kwa makini katika hostia Takatifu na kumuona Yesu akiwa mbele yetu. Na kumuona yeye akitupa huruma yake. Tumuone yeye akitoa upendo wake.

Sala: Bwana, nisaidie niweze kuwaza jinsi ya kuwa mtumishi. Nisaidie niweze kuishi unyenyekevu huu kwa matendo yangu. Ninaomba zawadi ya mwili wako Mtakatifu na damu yako vinibadilishe niweze kuwa mtu yule ambaye unapenda niwe. Yesu, nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, APRILI 2, 2026



MASOMO YA MISA, APRILI 2, 2026
ALHAMISI KUU


SOMO 1
Kut 12:1-8, 11-14

Bwana akanena na Musa na Haruni katika nchi ya Misri, akawaambia, Mwezi huu utakuwa mwanzo wa miezi kwenu; utakuwa ni mwezi wa kwanza wa mwaka kwenu. Semeni na mkutano wote wa Israeli, mkawaambie, Siku ya kumi ya mwezi huu kila mtu atatwaa mwana-kondoo, kwa hesabu ya nyumba ya baba zao, mwana-kondoo kwa watu wa nyumba moja; na ikiwa watu wa nyumba ni wachache kwa mwana-kondoo, basi yeye na jirani yake aliye karibu na nyumba yake na watwae mwana-kondoo mmoja, kwa kadiri ya hesabu ya watu; kwa kadiri ya ulaji wa kila mtu, ndivyo mtakavyofanya hesabu yenu kwa yule mwana-kondoo. Mwana-kondoo wenu atakuwa hana ila, mume wa mwaka mmoja; mtamtwaa katika kondoo au katika mbuzi. Nanyi mtamweka hata siku ya kumi na nne ya mwezi ule ule; na kusanyiko lote la mkutano wa Israeli watamchinja jioni.Nao watatwaa baadhi ya damu yake na kuitia katika miimo miwili na katika kizingiti cha juu, katika zile nyumba watakazomla. Watakula nyama yake usiku ule ule, imeokwa motoni, pamoja na mkate usiotiwa chachu; tena pamoja na mboga zenye uchungu. Tena mtamla hivi; mtakuwa mmefungwa viuno vyenu, mmevaa viatu vyenu miguuni, na fimbo zenu mikononi mwenu; nanyi mtamla kwa haraka; ni pasaka ya Bwana. Maana nitapita kati ya nchi ya Misri usiku huo, nami nitawapiga wazaliwa wa kwanza wote katika nchi ya Misri, wa mwanadamu na wa mnyama; nami nitafanya hukumu juu ya miungu yote ya Misri; Mimi ndimi Bwana. Na ile damu itakuwa ishara kwenu katika zile nyumba mtakazokuwamo; nami nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu, lisiwapate pigo lo lote likawaharibu, nitakapoipiga nchi ya Misri. Na siku hii itakuwa ukumbusho kwenu, nanyi mtaifanya iwe sikukuu kwa Bwana; mtaifanya iwe sikukuu katika vizazi vyenu vyote, kwa amri ya milele

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab 116:12-13, 15-18

(K)Kikombe kile cha baraka tukibarikicho, Je, !Si ushirika wa damu ya Kristo?

Nimrudishie Bwana nini
Kwa ukarimu wake wote alionitendea?
Nitakipokea kikombe cha wokovu;
Na kulitangaza jina la Bwana. (K)

Ina thamani machoni pa Bwana
Mauti ya wacha Mungu wake.
Ee Bwana, hakika mimi ni mtumishi wako,
Mtumishi wako, mwana wa mjakazi wako,
Umevifungua vifungo vyangu. (K)

Nitakutolea dhabihu ya kushukuru;
Na kulitangaza jina la Bwana;
Nitaziondoa nadhiri zangu kwa Bwana,
Naam, mbele ya watu wake wote. (K)



SOMO 2
1Kor 11:23-26

Kwa maana mimi nalipokea kwa Bwana niliyowapa nanyi, ya kuwa Bwana Yesu usiku ule aliotolewa alitwaa mkate, naye akiisha kushukuru akaumega, akasema, Huu ndio mwili wangu ulio kwa ajili yenu; fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu. Na vivi hivi baada ya kula akakitwaa kikombe, akisema, Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu; fanyeni hivi kila mnywapo, kwa ukumbusho wangu. Maana kila mwulapo mkate huu na kukinywea kikombe hiki, mwaitangaza mauti ya Bwana hata ajapo.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



INJILI
Yn 13:1-15

Basi, kabla ya sikukuu ya Pasaka, Yesu, hali akijua ya kuwa saa yake imefika, atakayotoka katika ulimwengu kwenda kwa Baba, naye ali amewapenda watu wake katika ulimwengu, aliwapenda upeo. Hata wakati wa chakula cha jioni; naye Ibilisi amekwisha kumtia Yuda, mwana wa Simoni Iskariote, moyo wa kumsaliti; Yesu, hali akijua ya kuwa Baba amempa vyote mikononi mwake, na ya kuwa alitoka kwa Mungu naye anakwenda kwa Mungu, aliondoka chakulani; akaweka kando mavazi yake, akatwaa kitambaa, akajifunga kiunoni. Kisha akatia maji katika bakuli, akaanza kuwatawadha wanafunzi miguu, na kuifuta kwa kile kitambaa alichojifunga. Hivyo yuaja kwa Simoni Petro. Huyo akamwambia, Bwana! Wewe wanitawadha miguu mimi? Yesu akajibu, akamwambia, Nifanyalo wewe hujui sasa; lakini utalifahamu baadaye. Petro akamwambia, Wewe hutanitawadha miguu kamwe. Yesu akamwambia, Kama nisipokutawadha, huna shirika nami. Simoni Petro akamwambia, Bwana, si miguu yangu tu, hata na mikono yangu na kichwa changu pia. Yesu akamwambia, Yeye aliyekwisha kuoga hana haja ila ya kutawadha miguu, bali yu safi mwili wote; nanyi mmekuwa safi, lakini si nyote. Kwa maana alimjua yeye atakayemsaliti; ndiyo maana alisema, Si nyote mlio safi. Basi alipokwisha kuwatawadha miguu, na kuyatwaa mavazi yake, na kuketi tena, akawaambia, Je! Mmeelewa na hayo niliyowatendea? Ninyi mwaniita, Mwalimu, na, Bwana; nanyi mwanena vema, maana ndivyo nilivyo. Basi ikiwa mimi, niliye Bwana na Mwalimu, nimewatawadha miguu, imewapasa vivyo kutawadhana miguu ninyi kwa ninyi. Kwa kuwa nimewapa kielelezo; ili kama mimi nilivyowatendea, nanyi mtende vivyo.

Injili ya Bwana.........Sifa Kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUBEBA MISALABA YETU!


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Kwaresima
Jumatano, Aprili 1, 2026 
Juma Kuu

Isa 50: 4-9; 
Zab 68: 8-10, 21-22, 31, 33-34; 
Mt 26: 14-25.


KUBEBA MISALABA YETU!

“Naliwatolea wapigao mgongo wangu, na wang'oao ndevu mashavu yangu; sikuficha uso wangu usipate fedheha na kutemewa mate." Mstari huu kutoka kitabu cha nabii Isaya unatukumbusha juu ya uchungu wa Yesu. Lakini, tunaweza kufikiria tu kile alichokihisi Yesu aliposoma maneno haya ya Isaya. Je, unafikiri maneno haya yalimpelekea awe na hofu? Au labda kwa sababu yeye alikuwa mwana wa Mungu, jambo hili halikumsumbua yeye kabisa? Pangine ukweli upo sehemu fulani kati ya hayo. Kuwa binadamu, Yesu kiasili alihisi matatizo makubwa juu ya kile kilichokuwa kikimngojea yeye. Lakini katika Umungu wake, aliweza kutamka kwa kujiamini sana, Bwana Mungu ndiye msaada wangu hivyo sina mashaka. Hivyo hakika alikuwa na hofu kubwa juu ya majaribu yaliopo mbele yake, vilevile Yeye alijawa na nguvu akijua kuwa Baba yake alikuwa pamoja naye na kamwe asinge mwacha. 

Kuna uwiano hapa kwa maisha yetu. Hatuwezi kuona wakati ujao, lakini tunatambua kuwa tuna ugumu fulani waweza kuja katika maisha yetu na tunapaswa kuushughulikia. Pengine hatupo katika hali ambayo dhambi yetu inatuonesha tuna mkana Yesu moja kwa moja, lakini kila mmoja anaweza kuona aina fulani ya dhambi katika maisha yake. Tumia juma hili kwa uaminifu na kweli. Huruma ya Mungu ni ya ndani sana na njema mno, kiasi kwamba ungeielewa, kusingekuwa na haja ya kubaki na dhambi zako ukifikiria niungame namna ghani. Hali halisi haipo kama tunavyo ifikiria sisi wenyewe. Kama Yesu, tunajikabidhi kwa upendo na msaada wa Baba yetu wa Mbinguni. Tukiwa naye, ni hakika kwamba tunashinda tatizo lolote lile, kwani hawezi kuwatupa watoto wake.

Sala: Bwana, ninaomba unisadie katika juma hili niweze kukabili dhambi zangu na udhaifu wangu. Mimi ni mdhambi, Bwana mpendwa, lakini inaweza kuwa vigumu sana kwangu kukubali ukweli huu. Ninaomba nikabidhi dhambi zangu kwako, ili niweze kuwa huru, na kupokea nafasi katika huruma yako kuu. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, APRILI 1, 2026




MASOMO YA MISA, APRILI 1, 2026
JUMATANO YA JUMA KUU

SOMO 1
Isa. 50:4-9

Bwana Mungu amenipa ulinzi wa hao wafundishwao, nipate kujua jinsi ya kumtegemea kwa maneno yeye aliyechoka, huniamsha asubuhi baada ya asubuhi; huniamsha, sikio langu lipate kusikia kama watu wafundishwao. Bwana Mungu amenizibua sikio langu, wala sikuwa mkaidi, wala sikurudi nyuma.

Naliwatolea wapigao mgongo wangu, na wang’oao ndevu mashavu yangu; sikuficha uso wangu usipate fedheha na kutemewa mate.
Maana Bwana Mungu atanisaidia; kwa sababu hiyo sikutahayari, kwa sababu hiyo nimekaza uso wangu kama gumegume, nami najua ya kuwa sitaona haya.

Yeye anipatiaye haki yangu yu karibu; ni nani atakayeshindana nami? Na tusimame pamoja; ni nani aliye hasimu yangu? Na anikaribie basi.

Tazama, Bwana Mungu atanisaidia; ni nani atakayenihukumu kuwa mkosa?

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 69:7-9, 20-21, 30, 32-33 (K) 13

(K) Kwa wingi wa fadhili zako unijibu, ee Bwana.

Kwa ajili yako nimestahimili laumu,
Fedheha imenifunika uso wangu.
Nimekuwa mgeni kwa ndugu zangu,
Na msikwao kwa wana wa mama yangu.
Maana wivu wa nyumba yako umenila,
Na laumu zao wanaokulaumu zimenipata. (K)

Laumu imenivunja moyo, 
Nami ninaugua sana.
Namngoja aje wa kunihurumia, wala hakuna; 
Na wa kunifariji, wala sikumwona mtu.
Wakanipa uchungu kuwa chakula changu;
Nami nilipokuwa na kiu wakaninywesha siki. (K)

Nitalisifu jina la Mungu kwa wimbo,
Nami nitamtukuza kwa shukrani.
Walioonewa watakapoona watafurahi;
Enyi mmtafutao Mungu, mioyo yenu ihuishwe.
Kwa kuwa Bwana huwasikia wahitaji,
Wala hawadharau wafunga wake. (K)


SHANGILIO
Yn. 3:16

Jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe wa pekee, kila mtu amwaminiye huwa na uzima wa milele.


INJILI
Mt. 26:14-25

Wakati huo mmoja wa wale Thenashara, jina lake Yuda Iskariote, aliwaendea wakuu wa makuhani, akasema, Ni nini mtakachonipa, nami nitamsaliti kwenu? Wakampimia vipande thelathini vya fedha. Tokea wakati huo akawa akitafuta nafasi apate kumsaliti.

Hata siku ya kwanza ya mikate isiyotiwa chachu, wanafunzi wake wakamwendea Yesu, wakamwambia, Ni wapi utakapo tukuandalie uile Pasaka? Akasema, Enendeni mjini kwa mtu Fulani, mkamwambie, Mwalimu asema, Majira yangu ni karibu; kwako nitafanya Pasaka pamoja na wanafunzi wangu. Wanafunzi wakafanya kama Yesu alivyowaagiza, wakaiandaa Pasaka.

Basi kulipokuwa jioni aliketi chakulani pamoja na wale Thenashara. Nao walipokuwa wakila, alisema, Amin, nawaambia, Mmoja wenu atanisaliti. Wakahuzunika sana, wakaanza kumwuliza mmoja mmoja, Ni mimi, Bwana? Akajibu akasema, Yeye aliyetia mkono wake pamoja nami katika kombe, ndiye atakayenisaliti. Mwana wa Adamu aenda zake, kama alivyoandikiwa; lakini ole wake mtu yule ambaye amsaliti Mwana wa Adamu! Ingekuwa heri kwake mtu yule kama asingalizaliwa. Yuda, yule mwenye kumsaliti, akajibu, akasema, Ni mimi, Rabi? Akamwambia, Wewe umesema.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUWA HURU KUMCHAGUA YESU!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya Kwaresima
Jumanne, Machi 31, 2026 
Juma Kuu

Isa 49: 1-6; 
Zab 71: 1-6, 15, 17; 
Yn 13: 21-33, 36-38.


KUWA HURU KUMCHAGUA YESU!

Ni juma la mwisho Yesu yupo na wafuasi wake kabla ya kufa. Wote kumi na tatu wanakula mlo wa Pasaka na ni muda muhimu. Yesu anaeleza kuhusu yule atakaye msaliti “amin nawaambieni mmoja wenu atanisaliti”. Hakuna aliye amini kwamba atakuwa yeye, “hakika sio mimi”. Majivuno ni kitu ambacho kinatufanya tusikubali makosa yetu na hili ndilo linalo tokea wakati wa mlo huu. “Mtanipa nini kama nikimtoa kwenu?” ndivyo Yuda anavyomsaliti kwasababu ya tamaa. Petro anamkana kwasababu ya woga wa maisha yake mwenyewe, anasema uongo ili aweze kukwepa hatari. 

Yesu alikuwa na moyo wa Kibinadamu na alimpenda Yuda kwa mapendo ya Kimungu kwa njia ya moyo wake wa kibinadamu. Kwa matokeo ya upendo huu mkamilifu wa Yesu kwa Yuda, moyo wa Yesu unasumbuka.  Si kwamba Yesu mwenyewe aliumizwa au kuwa na hasira kwa usaliti wa Yuda. Bali, ni kwamba moyo wa Yesu ulichomwa kwa uchungu kwamba Yuda anapotea, ambaye alikuwa anampenda kwa mapendo kamili. Yuda alikuwa na uhuru kamili, lakini alichagua kumsaliti Yesu. Hili ni kweli hata kwetu pia. Sisi tuna uhuru kamili na tumepewa uwezo huo huo ambayo Yuda alikuwa nao kumpenda Yesu kwa mapendo kamili au kumsaliti. Tunaweza kuruhusu zawadi yake ya ukombozi iingie katika maisha yetu au kuikataa. Ni juu ya uwezo wetu kamili. 

Juma kuu ni kipindi cha kuzama ndani kabisa na kujitazama upo katika barabara ipi. Kila wakati na kila siku unaitwa na Mungu kumchagua yeye kwa upendo wako wote. Lakini kama ilivyokuwa kwa Petro na Yuda, mara nyingi tunamkana na kumsaliti. Tunashindwa kabisa kutoa maisha yetu katika hali ya sadaka na kwa ukarimu kama alivyo fanya Bwana. Katika juma hili kuu, tujitafiti kwa undani kabisa, kama nipo tayari kutafuta msamaha kwa Yesu wa Huruma? Tumrudie Yesu na tumfuate na msalaba katika juma hili. 

Sala: Bwana, ninakupenda wewe, lakini ninatambua kuwa nina kuhuzunisha moyo wako kwa kukusaliti kwangu. Nisaidie niweze kuona dhambi yangu katika kweli juma hili. Kwa kuiona ninaomba niachane na kile kinacho nifanya daima niwe mbali nawe katika kukupenda, ili niweze kutembea nawe katika msalaba na kushiriki utukufu wako. Yesu, ninakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2024 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MACHI 31, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 31, 2026
JUMANNE YA JUMA KUU

SOMO 1
Isa. 49:1-6

Nisikilizeni, enyi visiwa; tegeni masikio yenu, enyi kabila za watu mlio mbali sana; Bwana ameniita tangu tumboni; toka tumbo la mama yangu amenitaja jina langu.

Naye anifanya kinywa changu kuwa kama upanga mkali; katika kivuli cha mkono wake amenisitiri; naye amenifanya kuwa mshale uliosuguliwa; katika podo lake amenificha.

Akaniambia; Wewe u mtumishi wangu, Israeli, ambaye katika wewe nitatukuzwa. Lakni nikasema, Nimejitaabisah bure, nimetumia nguvu zangu bure bila faida; lakni hakika hukumu yangu ina Bwana, na thawabu yangu ina Mungu wangu.

Na sasa Bwana asema hivi, yeye aliyeniumba tangu tumboni niwe mtumishi wake, ili nimletee Yakobo tena, na Israeli wakusanyike mbele zake tena.

Ni neno dogo sana wewe kuwa mtumishi wangu ili kuziinua kabila za Yakobo, na kuwarejeza watu wa Israeli waliohifadhiwa; zaidi ya hayo nitakutoa uwe nuru ya mataifa, upate kuwa wokovu wangu hata miisho ya dunia.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 71:1-6, 15, 17 (K) 15

(K) Kinywa changu kitasimulia haki na wokovu wako.

Nimekukimbilia Wewe, Bwana,
Nisiaibike milele.
Kwa haki yako uniponye, uniopoe,
Unitegee sikio lako, uniokoe. (K)

Uwe kwangu mwamba wa makazi yangu,
Nitakakokwenda siku zote.
Umeamuru niokolewe,
Ndiwe genge langu na ngome yangu.
Ee Mungu wangu, uniopoe mkononi mwa mkorofi,
Katika mkono wake mwovu, mdhalimu. (K)

Maana ndiwe taraja langu, Ee Bwana Mungu,
Tumaini langu tokea ujana wangu.
Nimekutegemea Wewe tangu kuzaliwa,
Ndiwe uliyenitoa tumboni mwa mama yangu,
Ninakusifu Wewe daima. (K)

Kinywa changu kitasimulia haki na wokovu wako.
Mchana kutwa; maana sijui hesabu yake.
Ee Mungu, umenifundisha tokea ujana wangu;
Nimekuwa nikitangaza miujiza yako hata leo. (K)


SHANGILIO
Amo. 5:14

Tafuteni mema, wala si mabaya, mpate kuishi, hivyo Bwana, atakuwa pamoja nanyi.


INJILI
Yn. 13:21-33, 36-38

Pale alipokuwa na mitume wake mezani Yesu alifadhaika rohoni, akashuhudia akisema, Amin, amin, nawaambieni, Mmoja wenu atanisaliti. Wanafunzi wakatazamana, huku wakiona shaka ni nani amtajaye.

Na palikuwapo mmoja wa wanafunzi wake, ameegama kifuani pa Yesu, ambaye Yesu alimpenda. Basi Simoni Petro akampungia mkono, akamwambia, Uliza, ni nani amtajaye? Basi yeye, hali akimwelekea Yesu kifua chake, akamwambia, Bwana, ni nani? Basi Yesu akajibu, Ndiye mtu yule nitakayemtowelea tonge na kumpa. Akatowelea tonge, akalitwaa akampa Yuda, mwana wa Simoni Iskariote. Na baada ya hilo tonge Shetani alimwingia. Basi Yesu akamwambia, Uyatendayo yatende upesi. Wala hakuna mtu katika wale walioketi chakulani aliyeijua sbabu ya kumwambia hivyo. Kwa maana wengine walidhania, kwa kuwa Yuda huchukua mfuko, ya kwamba Yesu alimwambia kama, Nunua tunavyohitaji kwa sikukuu; au kwamba awape maskini kitu. Basi huyo, akiisha kulipokea lile tonge, akatoka mara hiyo. Nako kulikuwa ni usiku.

Basi huyo alipokwisha kutoka, Yesu alisema, Sasa ametukuzwa Mwana wa Adamu, naye Mungu ametukuzwa ndani yake. Mungu naye atamtukuza ndani ya nafsi yake; naye atamtukuza mara.

Enyi watoto wadogo, bado kitambo kidogo sitakuwa pamoja nayi; mtanitafuta; na kama vile nilivyowaambia WAyahudi ya kwamba, Mimi niendako ninyi hamwezi kuja; kadhalika sasa nawaambia ninyi.

Simoni Petro akamwambia, Bwana, unakwendapi? Yesu akamjibu, Niendako huwezi kunifuata sasa lakini utanifuata baadaye. Petro akamwambia Bwana, kwa nini mimi nisiweze kukufuata sasa. Mimi nitautoa uhai wangu kwa ajili yako. Yesu akamjibu, Je! Wewe utautoa uhai wako kwa ajili yangu? Amin, amin, nakuambia, Jimbi hatawika hata wewe utakapokuwa umenikana mara tatu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.