Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

IMANI INATUONGOZA KWENYE UKWELI WA UFUFUKO!



“KUFUFUKA NA KRISTO”
Tafakari ya Pasaka
Jumamosi, Aprili 11, 2026 
Oktava ya Pasaka

Mdo 4:13-21
Zab 118:14-21
Mk 16:9-15


IMANI INATUONGOZA KWENYE UKWELI WA UFUFUKO! 

Kukosa Imani kunamfanya mtu akose ukweli mwingi katika maisha. Imani juu ya uzuri wa ndugu zetu inatufanya tujenge ulimwengu kuwa sehemu nzuri ya kuishi. Imani juu yetu wenyewe inatufanya kuachia mawimbi mbali mbali yanayokuja kwetu tusio yafahamu. Imani juu ya utume wetu inatufanya tuishi vizuri wito wetu. Imani katika mapendo kwa Mungu inatufanya sisi tusiwe watu wazama za dhambi na kuwa “washindi wa wakati huu”. Imani kwa Yesu mfufuka inatusaidia tuweze kutangaza habari za ufufuko. Zaidi ya nyakati zote, ulimwengu wa sasa unahitaji watu wenye Imani.

Kwanini mitume walishindwa kuamini kwamba Yesu amefufuka kutoka wafu? Walikuwa wameshaona miujiza mingi sana kwa Yesu kabla ya kufa. Walimsikia akifundisha kwa mamlaka makubwa na neema. Na sasa, baada ya kufufuka kutoka wafu mioyo yao imekuwa migumu na hawakuamini mara moja. Yesu alibidi kuwatokea mara nyingi na kuonesha ushuhuda huo mbele ya macho yao. Walitaka kuamini lakini hawakuweza kuruhusu wao wenyewe kuamini ufufuko kwa Imani ya kweli mpaka Yesu atoe ushuhuda. Baada ya muda walitambua hata ushuhuda waliohitaji ulikuwa ndani yao.

Mara nyingi tuna alikwa na Yesu kuwa na Imani na kumwamini yeye na kukubali mambo mengi kwa Imani. Zawadi ya Imani ni sawa na moto mdogo ndani mwetu ambao mara nyingi kwa kutojali tunaruhusu uzimwe na mambo mbali mbali bila kukuwa. Nia ya Ukristo wetu ni kuruhusu moto huo ukuwe na kufikia kilele ambacho Mungu anapenda. Inawezekana kuwasha moto huo na kuwa mkubwa na hatimaye kuchoma chochote kinacho taka kuingia ndani. Njia ya moto huu unajali sana namna tulivyoshikilia ule moto mdogo ambao tayari umeshaingia ndani mwetu. Tunapaswa kuukuza na kuulinda ili ukuwe. Hili linawezekana kwa kuacha ulegevu katika kusali. 

Sala ni ufunguo wa kumruhusu Mungu akue ndani mwetu. Yupo ndani, akiongea nasi na kutuita tuamini. Kila mara tunapo kaza macho katika moto huo, tuna uwezesha ukuwe na kuchukua nafasi. Na kama Wafuasi wangeweza kuacha tu zawadi hiyo ya Imani ikuwe wangeweza mara moja kumtambua Yesu na kumwamini mara moja, bila hata yeye kujidhihirisha kwenye macho yao. Je, unafanya nini katika maisha yako ili kuruhusu moto mdogo wa Imani uliopo ndani mwako kukuwa? Jikite daima kwenye sala, na tazama Imani yako kwa Yesu itakuwa na kungara. 

Sala: Bwana nakupenda wewe na nakuamini wewe. Ninakuomba unisaidie kukuza moto wa imani uliopandwa ndani mwangu uweze kukuwa. Nitakase moyo wangu kwa moto huu na niweke huru kutoka katika moyo wangu mgumu. Yesu nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, APRILI 11, 2026




MASOMO YA MISA, APRILI 11, 2026
JUMAMOSI KATIKA OKTAVA YA PASKA


SOMO 1
Mdo. 4:13 – 21

Siku ile, makuhani na akida wa hekalu walipoona ujasiri wa Petro na Yohane, na kuwajua ya kuwa ni watu wasio na elimu, wasio na maarifa, wakastaajabu, wakatambua ya kwamba walikuwa pamoja na Yesu. Na wakimwona yule aliyeponywa akisimama pamoja nao hawakuwa na neno la kujibu. Wakawaamuru kutoka katika baraza, wakafanya shauri wao kwa wao, wakisema, Tuwafanyieni watu hyawa? Maana ni dhahiri kwa watu wote wakaao Yerusalemu ya kwamba ishara mashuhuri imefanywa nao, wala hatuwezi kuikana. Lakini neno hili lisije likaenea katika watu, na tuwatishe wasiseme tena na mtu awaye yote kwa jina hili. Wakawaita, wakawaamuru wasiseme kabisa wala kufundisha kwa jina la Yesu. Petro na Yohane wakawajibu wakawaambia, Kwamba ni haki mbele za Mungu kuwasikiliza ninyi kuliko Mungu, hukumuni ninyi wenyewe; maana sisi hatuwezi kuacha kuyanena mambo tuliyoyaona na kuyasikia. Nao walipokwisha kuwatisha tena wakawafungua, wasione njia ya kuwaadhibu, kwa sababu ya watu; kwa kuwa watu wote walikuwa wakimtukuza Mungu kwa hayo yaliyotendeka.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 118:1, 14 – 21 (K) 21

(K) Jiwe walilolikataa waashi, Limekuwa jiwe kuu la pembeni.

Aleluya,
Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema,
Kwa maana fadhili zake ni za milele.
Bwana ni nguvu zangu na wimbo wangu,
Naye amekuwa wokovu wangu.
Sauti ya furaha na wokovu,
Imo hemani mwao wenye haki. (K)

Mkono wa kuume wa Bwana hutenda makuu.
Mkono wa kuume wa Bwana umetukuzwa;
Mkono wa kuume wa Bwana hutenda makuu.
Sitakufa bali nitaishi,
Nami nitayasimulia matendo ya Bwana.
Bwana ameniadhibu sana,
Lakini hakuniacha nife. (K)

Nifungulieni malango ya haki,
Nitaingia na kumshukuru Bwana.
Lango hili ni la Bwana,
Wenye haki ndio watakaoliingia.
Nitakushukuru kwa maana umenijibu,
Nawe umekuwa wokovu wangu. (K)



SHANGILIO
Zab. 118:24

Aleluya, aleluya,
Siku hii ndiyo aliyoifanya Bwana, Tutaishangilia na kuifurahia.
Aleluya.



INJILI
Mk. 16:9 – 15

Yesu alipofufuka alfajiri siku ya kwanza ya juma, alimtokea kwanza Mariamu Magdalene, ambaye kwamba alimtoa pepo saba. Huyo akashika njia akawapasha habari wale waliokuwa pamoja naye, nao wakali wanaomboleza na kulia. Walakini hao waliposikia kama yu hai, naye amemwona, hawakusadiki.

Baada ya hayo akawatokea watu wawili miongoni mwao, ana sura nyingine; nao walikuwa wakishika njia kwenda shamba. Na hao wakaenda zao wakawapa habari wale wengine; wala hao hawakuwasadiki.

Baadaye akaonekana na wale kumi na mmoja walipokuwa wakila, akawakemea kwa kutokuamini kwao na ugumu wa mioyo yao, kwa kuwa hawakuwasadiki wale waliomwona alipofufuka katika wafu. Akawaambia, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

UFUFUKO: WITO MPYA



“KUFUFUKA NA KRISTO”
Tafakari ya Pasaka
Ijumaa, Aprili 10, 2026
Oktava ya Pasaka

Mdo 4:1-12
Zab 118:1-2,4,22-27
Yn 21:1-14


UFUFUKO: WITO MPYA

Leo, tunasikia tena habari nyingine ya ufufuko ya Bwana kuwatokea wafuasi wake. Baada ya kuona hamna namna nyingine na kuamua kurudi katika kazi yao ya uvuvi, wakiwa wamekata tamaa na kuchoka, wanarudi ufukweni mwa bahari bila kupata kitu. Mara moja wanamsikia Yesu, (hawakumtambua) akiwaambia waende kuvua tena upande mwingine. Walimtii na tazama nyavu zilijaa samaki wengi. Muujiza huu ulitosha kwa Yohane kutambua kuwa ni “Bwana”.

Hiki kitendo cha kushika samaki wengi kilikuwa kama zawadi ya Yesu kwao kuwasaidia katika kazi yao. Ilikuwa ni ishara kubwa. Ishara kubwa ni kwamba Yesu alikuwa akiwapa mitume wito mpya. Walikuwa sasa sio kuwa tena wavuvi wa samaki, bali wavuvi wa roho za watu. Na kwamba kama watajaribu kufanya haya kwa nguvu zao wenyewe, wataishia kutokupata kitu. Lakini kama watafanya kwa amri ya Bwana, watapata matunda mengi. Hata kwa jinsi wasivyo dhani. 

Muujiza huu wa Yesu unaanza kufunua kwa mitume na kwetu pia juu ya wito wa kuhubiri habari njema ulimwenguni. Ufunuo huu ulikuja baada ya ufufuko, ambapo Yesu anawapa mitume maelezo wa kuchukua ujumbe wa ukombozi. Tunapaswa kuona katika muujiza huu juu ya wito wetu wa kuhubiri habari njema. Na tunapaswa kuona katika muujiza huu kutangaza habari njema kwa amri ya Yesu, katika hali yake na ndani ya mapenzi yake.

Mara nyingi wakristo wanakuja na mawazo mazuri ya jinsi ya kuhubiri Injili. Lakini ufunguo ni kujinyenyekesha sisi wenyewe mbele za Mungu na kutambua kwamba sisi hatuwezi kuhubiri habari njema bila kuongozwa na Yesu katika muelekeo sahihi. Tunapaswa kuisikiliza sauti yake na kuitika wakati anaelekeza. Kuhubiri habari njema ni jibu zuri la kuitika wito wa Yesu zaidi ya kitu chochote ambacho twaweza kufanya. Tunapo endelea na kipindi cha pasaka ni vizuri kila mtu akatafakari juu ya jukumu lake la kuhubiri habari njema. Tumuache Bwana aongee na sisi nasi tufuate muelekeo wake. Mungu anapenda kututumia sisi, tumpe nafasi.

Sala: Bwana, nipo tayari unitumie kuhubiri habari njema. Nisaidie kwa ujasiri niweze kuitika wito, na nisaidie nifuate kwa uaminifu muelekeo unao niongoza. Yes, nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, APRILI 10, 2026


MASOMO YA MISA, APRILI 10, 2026
OKTAVA YA PASAKA, IJUMAA


SOMO 1
Mdo 4:1-12

Petro na Yohane walipokuwa wakisema na watu wale, makuhani na akida wa hekalu na Masadukayo wakawatokea, wakifadhaika sana kwa sababu wanawafundisha watu na kuhubiri katika Yesu ufufuo wa wafu. Wakawakamata, wakawaweka gerezani hata asubuhi; kwa kuwa imekwisha kuwa jioni. Lakini wengi katika hao waliosikia lile neno waliamini; na hesabu ya watu waume ikawa kama elfu tano. Hata asubuhi wakubwa na wazee na waandishi wakakusanyika Yerusalemu, na Anasi Kuhani Mkuu, na Kayafa pia, na Yohane na Iskanda, na wote wale waliokuwa jamaa zake Kuhani Mkuu. Walipowaweka katikati wakawauliza, Kwa nguvu gani na kwa jina la nani ninyi mmefanya haya? Ndipo Petro, akijaa Roho Mtakatifu, akawaambia, Enyi wakubwa wa watu na wazee wa Israeli, kama tukiulizwa leo habari ya jambo jema alilofanyiwa yule mtu dhaifu, jinsi alivyoponywa, jueni ninyi nyote na watu wote wa Israeli ya kuwa kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, ambaye ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu, kwa jina hilo mtu huyu anasimama ali mzima mbele yenu. Yeye ndiye jiwe lile lililodharauliwa na ninyi waashi, nalo limewekwa kuwa jiwe kuu la pembeni. Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab 118:1-2, 4, 22-27

(K) Jiwe walilolikataa waashi, Limekuwa jiwe kuu la pembeni.

Haleluya. Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema,
Kwa maana fadhili zake ni za milele.
Israeli na aseme sasa,
Ya kwamba fadhili zake ni za milele.
Wamchao Bwana na waseme sasa,
Ya kwamba fadhili zake ni za milele.

Jiwe walilolikataa waashi
Limekuwa jiwe kuu la pembeni.
Neno hili limetoka kwa Bwana,
Nalo ni ajabu machoni petu.
Siku hii ndiyo aliyoifanya Bwana,
Tutashangilia na kuifurahia.

Ee Bwana, utuokoe, twakusihi;
Ee Bwana, utufanikishe, twakusihi.
Na abarikiwe yeye ajaye kwa jina la Bwana;
Tumewabarikia toka nyumbani mwa Bwana.
Bwana ndiye aliye Mungu, Naye ndiye aliyetupa nuru.



INJILI
Yn 21:1-14

Baada ya hayo Yesu alijidhihirisha tena kwa wanafunzi wake, penye bahari ya Tiberia, naye alijidhihirisha hivi. Simoni Petro, na Tomaso aitwaye Pacha, na Nathanaeli wa Kana ya Galilaya, na wana wa Zebedayo, na wengine wawili wa wanafunzi wake, walikuwapo pamoja. Simoni Petro aliwaambia, Naenda kuvua samaki. Nao wakamwambia, Sisi nasi tutakwenda nawe. Basi wakaondoka, wakapanda chomboni; ila usiku ule hawakupata kitu. Hata asubuhi kulipokucha, Yesu alisimama ufuoni; walakini wanafunzi hawakujua ya kuwa ni Yesu. Basi Yesu akawaambia, Wanangu, mna kitoweo? Wakamjibu, La. Akawaambia, Litupeni jarife upande wa kuume wa chombo, nanyi mtapata. Basi wakatupa; wala sasa hawakuweza kulivuta tena kwa sababu ya wingi wa samaki. Basi yule mwanafunzi ambaye Yesu alimpenda akamwambia Petro, Ndiye Bwana. Naye Simoni Petro, aliposikia ya kwamba ni Bwana, akajifunga vazi lake, (maana alikuwa uchi), akajitupa baharini. Na hao wanafunzi wengine wakaja katika mashua; maana hawakuwa mbali na nchi kavu; ila yapata dhiraa mia mbili; huku wakilikokota lile jarife lenye samaki. Basi waliposhuka pwani, wakaona huko moto wa makaa, na juu yake pametiwa samaki, na mkate. Yesu akawaambia, Leteni hapa baadhi ya samaki mliowavua sasa hivi. Basi Simoni Petro akapanda chomboni, akalivuta jarife pwani, limejaa samaki wakubwa, mia hamsini na watatu; na ijapokuwa ni wengi namna hiyo, jarife halikupasuka. Yesu akawaambia, Njoni mfungue kinywa. Wala hakuna mtu katika wale wanafunzi aliyethubutu kumwuliza, U nani wewe? Wakijua ya kuwa ni Bwana. Yesu akaenda akautwaa mkate, akawapa, na samaki vivyo hivyo. Hiyo ndiyo mara ya tatu ya Yesu kuonekana na wanafunzi wake baada ya kufufuka katika wafu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, APRILI 9, 2026



MASOMO YA MISA, APRILI 9, 2026
OKTAVA YA PASAKA, ALHAMISI

SOMO 1
Mdo 3:11-26

Siku zile, kiwete yule aliyeponywa alipokuwa akiwashika Petro na Yohane, watu wote wakawakusanyikia mbio katika tao lile lililoitwa tao la Sulemani, wakishangaa sana. Hata Petro alipoyaona haya akawajibu wale watu, Enyi Waisraeli, mbona mnastaajabia haya, au mbona mnatukazia macho sisi, kana kwamba tumemfanya huyu aende kwa nguvu zetu sisi, au kwa utauwa wetu sisi? Mungu wa Ibrahimu na wa Isaka na wa Yakobo, Mungu wa baba zetu, amemtukuza mtumishi wake Yesu, ambaye ninyi mlimsaliti na kumkana mbele ya Pilato, alipokuwa ametoa hukumu yake afunguliwe. Bali ninyi mlimkana yule Mtakatifu, yule Mwenye haki, mkataka mpewe mwuaji; mkamwua yule Mkuu wa uzima, ambaye Mungu amemfufua katika wafu; na sisi tu mashahidi wake. Na kwa imani katika jina lake, jina lake limemtia nguvu mtu huyu mnayemwona na kumjua; na imani ile iliyo kwake yeye imempatia huyu uzima huu mkamilifu mbele yenu ninyi nyote. Basi sasa, ndugu, najua ya kuwa mliyatenda haya kwa kutokujua kwenu, kama na wakuu wenu walivyotenda. Lakini mambo yale aliyohubiri Mungu tangu zamani kwa kinywa cha manabii wake wote, ya kwamba Kristo wake atateswa, ameyatimiza hivyo. Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake Bwana; apate kumtuma Kristo Yesu mliyewekewa tangu zamani; ambaye ilimpasa kupokewa mbinguni hata zije zamani za kufanywa upya vitu vyote, zilizonenwa na Mungu kwa kinywa cha manabii wake watakatifu tokea mwanzo wa ulimwengu. Kwa maana Musa kweli alisema ya kwamba, Bwana Mungu wenu atawainulieni nabii, katika ndugu zenu, kama mimi; msikieni yeye katika mambo yote atakayonena nanyi. Na itakuwa ya kwamba kila mtu asiyemsikiliza nabii huyo ataangamizwa na kutengwa na watu wake. Naam, na manabii wote tangu Samweli na wale waliokuja baada yake, wote walionena, walihubiri habari za siku hizi. Ninyi mmekuwa watoto wa manabii na wa maagano yale, ambayo Mungu aliagana na baba zenu, akimwambia Ibrahimu, Katika uzao wako kabila zote za ulimwengu zitabarikiwa. Mungu, akiisha kumfufua mtumishi wake Yesu, alimtuma kwenu ninyi kwanza, ili kuwabarikia kwa kumwepusha kila mmoja wenu na maovu yake.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab 8:1, 4-8 

(K)Ee, Mungu, Bwana wetu; jinsi lilivyo tukufu jna lako duniani mwote.

Wewe, Mungu, Bwana wetu 
Jinsi lilivyo tukufu jina lako duniani mwote! 
Wewe umeuweka utukufu wako mbinguni; 
Mtu ni kitu gani hata umkumbuke, 
Na binadamu hata umwangalie? (K)

Umemfanya mdogo punde kuliko Mungu; 
Umemvika taji ya utukufu na heshima;
Umemtawaza juu ya kazi za mikono yako; 
Umevitia vitu vyote chini ya miguu yake. (K) 

Kondoo, na ng'ombe wote pia; 
Naam, na wanyama wa kondeni; 
Ndege wa angani, na samaki wa baharini; 
Na kila kipitacho njia za baharini. (K)


INJILI
Lk 24:35-48

Wanafunzi waliwapa habari ya mambo yale ya njiani, na jinsi alivyotambulikana nao katika kuumega mkate. 

Na walipokuwa katika kusema habari hiyo, yeye mwenyewe alisimama katikati yao, akawaambia, Amani iwe kwenu. 

Wakashituka, wakaogopa sana, wakidhani ya kwamba wanaona roho. Akawaambia, Mbona mnafadhaika? Na kwa nini mnaona shaka mioyoni mwenu? Tazameni mikono yangu na miguu yangu, ya kuwa ni mimi mwenyewe. Nishikenishikeni, mwone; kwa kuwa roho haina mwili na mifupa kama mnavyoniona mimi kuwa nayo. Na baada ya kusema hayo aliwaonyesha mikono yake na miguu yake. Basi walipokuwa hawajaamini kwa furaha, huku wakistaajabu, aliwaambia, Mna chakula cho chote hapa? Wakampa kipande cha samaki wa kuokwa. Akakitwaa, akala mbele yao. 

Kisha akawaambia, Hayo ndiyo maneno yangu niliyowaambia nilipokuwa nikali pamoja nanyi, ya kwamba ni lazima yatimizwe yote niliyoandikiwa katika Torati ya Musa, na katika Manabii na Zaburi. Ndipo akawafunulia akili zao wapate kuelewa na maandiko. Akawaambia, Ndivyo ilivyoandikwa, kwamba Kristo atateswa na kufufuka siku ya tatu; na kwamba mataifa yote watahubiriwa kwa jina lake habari ya toba na ondoleo la dhambi, kuanza tangu Yerusalemu. Nanyi ndinyi mashahidi wa mambo haya.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

UFUFUKO: YESU YUPO HAI KATIKA EKARISTI TAKATIFU.



“KUFUFUKA NA KRISTO”
Tafakari ya Pasaka
Jumatano, Aprili 8, 2026
Oktava ya Pasaka

Mdo 3:1-10
Zab 105:1-4,6-9
Lk 24:13-35


UFUFUKO: YESU YUPO HAI KATIKA EKARISTI TAKATIFU.


Kutokea kwa Yesu kwa wafuasi wake wawili inaonekana kuleta hisia. Walikuwa wameshakuwa na matumaini kwamba yeye ni Masiha lakini aliuawa. Na tazama kuna wengine wanasema kaburi lake liko wazi. Kadiri ujumbe unapo endelea, Yesu “anawaelezea yote yaliosemwa kuhusu yeye katika maandiko”. Kwa njia hiyo wale wafuasi wakatambua huyu mtu wanaye ongea naye ana uelewa wa juu na hekima ya hali ya juu, hivyo wanamualika akae nao. Yesu alikaa na kuketi nyumbani kwao. Wakiwa pale, maandiko yanasema “alichukua mkate, akaubariki, akaumega na kuwapa. Kwa njia hiyo macho yao yalifumbuliwa, wakamtambua na ghafla akaondoka machoni mwao”. Kwanini Yesu, alificha wafuasi wake wasimtambue alikuwa nani, na kuwaruhusu wamtambue tu, na ghafla akaondoka machoni mwao?

Yesu alipenda wale wafuasi na sisi wote pia, kwamba huyu ambaye amefufuka kutoka wafu yupo hai kweli na kwamba tutamtambua katika kuumega mkate. Tutamtambua katika Ekaristi Takatifu. Kutokea kwa Yesu kwa wafuasi wake, ni wazi, kwamba Yesu anakuwa wazi katika Ekaristi Takatifu. Yesu yupo hai katika Ekaristi! Lakini inatuambia kuwa amejificha ndani ya Ekaristi Takatifu. Muunganiko huu wa kujificha na uwepo wake kweli unatupa muongozo mzuri wa Imani yetu.

Wafuasi walikuwa mbele ya Yesu lakini hawakuweza kumtambua. Pengine na sisi ni wazi pia. Hili ni kweli hasa wakati tukiwa kanisani wakati wa misa lakini pia kwa upande mwingine tunamtambua. Tunapaswa kujikita katika kumuona yeye, kumtumbua na kumwabudu. Tunapaswa kutambua uwepo wa Yesu mfufuka kati yetu. Yupo nasi sasa, anatupenda sisi, anaongea na sisi, na anatuita tumpende. Tumtafute na kusikiliza sauti yake. Unaweza kushangazwa ni kwa jinsi ghani anaweza kuwa.

Sala: Bwana, ninakushukuru kwa kunipenda mimi kila wakati. Ninaomba unipe macho ya Imani niweze kukuona daima katika Ekaristi Takatifu, na naomba unisaidie niweze kutambua uwepo wako katika kila tukio la maisha yangu. Ninakupenda, Bwana mpendwa.  Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, APRILI 8, 2026




MASOMO YA MISA, APRILI 8, 2026
OCTAVA YA PASAKA, JUMATANO

SOMO 1
Mdo 3:1-10

Petro na Yohane walikuwa wakikwea pamoja kwenda hekaluni, saa ya kusali, saa tisa.

Na mtu mmoja aliyekuwa kiwete toka tumboni mwa mamaye alichukuliwa na watu, ambaye walimweka kila siku katika mlango wa hekalu uitwao Mzuri, ili aombe sadaka kwa watu waingiao ndani ya hekalu. Mtu huyu akiwaona Petro na Yohane wakiingia hekaluni aliomba apewe sadaka. Na Petro, akimkazia macho, pamoja na Yohane, akasema, Tutazame sisi. Akawaangalia, akitaraji kupata kitu kwao. Lakini Petro akasema, Mimi sina fedha, wala dhahabu, lakini nilicho nacho ndicho nikupacho. Kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, simama uende. Akamshika mkono wa kuume, akamwinua, mara nyayo zake na vifundo vya miguu yake vikatiwa nguvu. Akaondoka upesi akasimama, akaanza kwenda; akaingia ndani ya hekalu pamoja nao, akienda, akiruka-ruka, na kumsifu Mungu.

Watu wote wakamwona akienda, akimsifu Mungu. Wakamtambua, ya kuwa yeye ndiye aliyekuwa akiketi na kuomba sadaka penye mlango Mzuri wa hekalu; wakajaa ushangao wakastaajabia mambo yale yaliyompata.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab 105:1-4, 6-9

(K)Bwana anajaza nchi na fadhili zake.
Au Aleluya
           
Mshukuruni Bwana,liitieni jina,
Wajulisheni watu matendo yake.
Mwimbieni, mwimbieni kwa zaburi,
Zitafakarini ajabu zake zote. (K)

Jisifuni kwa jina lake takatifu,
Na ufurahi moyo wao wamtafutao Bwana.
Mtakeni Bwana na nguvu zake,
Utafuteni uso wake sikuzote. (K)

Enyi wazao wa Ibrahimu, mtumishi wake;
Enyi wana wa Yakobo, wateule wake.
Yeye, Bwana, ndiye Mungu wetu;
Duniani mwote mna hukumu zake. (K)

Analikumbuka agano lake milele;
Neno lile aliloviamuru vizazi elfu.
Agano alilofanya na Ibrahimu,
Na uapo wake kwa Isaka.  (K)


SHANGILIO
Zab. 118:24

Aleluya, aleluya,
Siku hii ndiyo aliyoifanya Bwana, Tutashangilia na kuifurahia.
Aleluya.


INJILI
Lk 24:14-35

Siku ile ile watu wawili miongoni mwao walikuwa wakienda kijiji kimoja, jina lake Emau, kilichokuwa mbali na Yerusalemu kama mwendo wa saa mbili. Nao walikuwa wakizungumza wao kwa wao habari za mambo hayo yote yaliyotukia. YesuIkawa katika kuzungumza na kuulizana kwao, Yesu mwenyewe alikaribia, akaandamana nao. Macho yao yakafumbwa wasimtambue. Akawaambia, Ni maneno gani haya mnayosemezana hivi mnapotembea? Wakasimama wamekunja nyuso zao.

Akajibu mmoja wao, jina lake Kleopa, akamwambia, Je! Wewe peke yako u mgeni katika Yerusalemu, hata huyajui yaliyotukia humo siku hizi? Akawauliza, Mambo gani? Wakamwambia, Mambo ya Yesu wa Nazareti, aliyekuwa mtu nabii, mwenye uwezo katika kutenda na kunena mbele za Mungu na watu wote; tena jinsi wakuu wa makuhani na wakubwa wetu walivyomtia katika hukumu ya kufa, wakamsulibisha. Nasi tulikuwa tukitumaini ya kuwa yeye ndiye atakayewakomboa Israeli. Zaidi ya hayo yote, leo ni siku ya tatu tangu yalipotendeka mambo hayo; tena, wanawake kadha wa kadha wa kwetu walitushitusha, waliokwenda kaburini asubuhi na mapema, wasiuone mwili wake; wakaja wakasema ya kwamba wametokewa na malaika waliosema kwamba yu hai. Na wengine waliokuwa pamoja nasi walikwenda kaburini wakaona vivyo hivyo kama wale wanawake walivyosema, ila yeye hawakumwona.

Akawaambia, Enyi msiofahamu, wenye mioyo mizito ya kuamini yote waliyoyasema manabii! Je! Haikumpasa Kristo kupata mateso haya na kuingia katika utukufu wake? Akaanza kutoka Musa na manabii wote, akawaeleza katika maandiko yote mambo yaliyomhusu yeye mwenyewe.

Wakakikaribia kile kijiji walichokuwa wakienda, naye alifanya kama anataka kuendelea mbele. Wakamshawishi wakisema, Kaa pamoja nasi, kwa kuwa kumekuchwa, na mchana unakwisha. Akaingia ndani kukaa nao. Ikawa alipokuwa ameketi nao chakulani, alitwaa mkate, akaubariki, akaumega, akawapa. Yakafumbuliwa macho yao, wakamtambua; kisha akatoweka mbele yao. Wakaambiana, Je! Mioyo yetu haikuwaka ndani yetu hapo alipokuwa akisema nasi njiani, na kutufunulia maandiko? Wakaondoka saa ile ile, wakarejea Yerusalemu, wakawakuta wale kumi na mmoja wamekutanika, wao na wale waliokuwa pamoja nao, wakisema, Bwana amefufuka kweli kweli, naye amemtokea Simoni. Nao waliwapa habari ya mambo yale ya njiani, na jinsi alivyotambulikana nao katika kuumega mkate.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania. These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

UFUFUKO: WITO WA KUKUWA KATIKA MAHUSIANO NA YESU!



“KUFUFUKA NA KRISTO”
Tafakari ya Pasaka
Jumanne, Aprili 7, 2026 
Oktava ya Pasaka

Mdo 2:36-41
Zab 33:4-5,18-20,22
Yn 20:11-18.


UFUFUKO: WITO WA KUKUWA KATIKA MAHUSIANO NA YESU!


Leo Maria Magdalena anarudi Kaburini baada ya Simoni Petro na Yohane wameshaondoka. Akili ya ufufuko inaonekana haijaingia katika akili yake, ingawaje yeye mwenyewe alikuwa amefufuka katika kaburi katika kufungwa na pepo saba (Lk 8:2). Baada ya kuona kaburi li wazi anabubujika machozi. Uwepo wa malaika haukumuogopesha, kwasababu alikuwa na huzuni kubwa kwasababu ya kupotelewa na mkombozi wa roho yake. Yesu anamtokea ghafla katika huzuni yake na kwa furaha, anasema “Rabi!” Mwalimu!. Yesu anamwambia asimshike.

Huu ulikuwa ni wakati ambao Maria alikuwa na hisia. Alikuwepo alipokuwa akitazama msalaba. Alimfahamu Yesu vizuri na alimpenda sana. Alimtazama akifa na ghafla sasa anamtamzama akiwa amefufuka amesimama mbele yake. Ni wazi kwamba alipatwa na furaha kubwa. Yesu hakuwa mkali kwa Maria kwa kumwambia kwamba asimshike. Alikuwa anampa ushauri mzuri na muelekeo wa safari ya maisha yake ya kiroho na Yesu. Alikuwa anamwambia kwa hakika kwamba, hali yetu sasa inabadilika, na kuwa katika hali ya ndani zaidi. Alimwambia usinishike kwasababu ‘hajapaa kwenda kwa Baba bado’.

Kwa wakati huo uhusiano wa Maria ulikuwa katika ngazi ya kibinadamu. Alipata muda wa kuwa na Yesu, kuwa karibu na Yesu na kumsikiliza, na alimpenda kwa moyo wote wa kibinadamu. Lakini Yesu alipenda yeye na sisi wote, tumpende sasa katika ngazi ya Kimungu. Akiwa katika kiti chake cha enzi Mbinguni anaweza sasa kuingia katika mioyo yetu. Anaweza kuingia ndani ya moyo wa Maria na sisi wote. Anaweza kuishi ndani yetu nasi ndani yake. Na yeye kuwa mmoja pamoja nasi. 

Kwa kuacha ngazi ya upendo wa kibinadamu tu na Yesu, Maria aliweza sasa kumpenda katika ngazi ya juu ambayo asingeweza kama alikuwa katika ngazi ya Kibinadamu. Huu ni muunganiko wa Kimungu, ambao kila mmoja wetu anaitwa. Yesu sasa ameshafufuka na sasa tunaweza kushiriki matunda ya ufufuko wake. Sisi, na Maria, tunaweza sasa kumuweka ndani ya mioyo yetu, kwasababu ndiye anaye tutegemeza sisi. 

Sala: Bwana, ninaomba niungane nawe kama wewe ulivyo ungana na mimi. Ninaomba akili, moyo na utashi wangu wote uwe wako. Ninaomba uje uishi ndani ya moyo wangu nami niishi ndani ya moyo wako. Nayatoa maisha yangu kwako, Bwana mpendwa, ninakuomba nikupe yote niliyo nayo na jinsi nilivyo. Yesu, nakuamini wewe. Amina

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, APRILI 7, 2026

MASOMO YA MISA, APRILI 7, 2026
OCTAVA YA PASAKA, JUMANNE

SOMO 1
Mdo 2:36-41

Petro aliwaambia Wayahudi: Nyumba yote ya Israeli na wajue yakini ya kwamba Mungu amemfanya Yesu huyo mliyesulibisha kuwa Bwana na Kristo. Walipoyasikia haya wakachomwa mioyo yao, wakamwambia Petro na mitume wengine, Tutendeje, ndugu zetu? Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu. Kwa kuwa ahadi hii ni kwa ajili yenu, na kwa watoto wenu, na kwa watu wote walio mbali, na kwa wote watakaoitwa na Bwana Mungu wetu wamjie. Akawashuhudia kwa maneno mengine mengi sana na kuwaonya, akisema, Jiokoeni na kizazi hiki chenye ukaidi. Nao waliolipokea neno lake wakabatizwa; na siku ile wakaongezeka watu wapata elfu tatu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab 33:4-5, 18-20, 22

(K)Nchi imejaa fadhili za Bwana (au) Aleluya.

Kwa kuwa neno la Bwana lina adili,
Na kazi yake yote huitenda kwa uaminifu.
Huzipenda haki na hukumu,
Nchi imejaa fadhili za Bwana.

Tazama, jicho la Bwana li kwao wamchao,
Wazingojeao fadhili zake.
Yeye huwaponya nafsi zao na mauti,
Na kuwahuisha wakati wa njaa.

Nafsi zetu zinamngoja Bwana;
Yeye ndiye msaada wetu na ngao yetu.
Ee Bwana, fadhili zako zikae nasi,
Kama vile tulivyokungoja Wewe.



SHANGLIO
Zab. 118:24

Aleluya, aleluya,
Siku hii ndiyo aliyoifanya Bwana, Tutashangilia na kuifurahia.
Aleluya.


INJILI
Yn 20:11-18

Mariamu alikuwa akisimama karibu na kaburi, nje yake, analia. Basi akilia hivi, aliinama na kuchungulia ndani ya kaburi. Akaona malaika wawili, wenye mavazi meupe, wameketi, mmoja kichwani na mmoja miguuni, hapo ulipolazwa mwili wake Yesu. Nao wakamwambia, Mama, unalilia nini? Akawaambia, Kwa sababu wamemwondoa Bwana wangu, wala mimi sijui walikomweka. Naye akiisha kusema hayo, akageuka nyuma, akamwona Yesu amesimama, asijue ya kuwa ni Yesu. Yesu akamwambia, Mama, unalilia nini? Unamtafuta nani? Naye, huku akidhania ya kuwa ni mtunza bustani, akamwambia, Bwana, ikiwa umemchukua wewe, uniambie ulipomweka, nami nitamwondoa. Yesu akamwambia, Mariamu. Yeye akageuka, akamwambia kwa Kiebrania, Raboni! (Yaani, Mwalimu wangu). Yesu akamwambia. Usinishike; kwa maana sijapaa kwenda kwa Baba. Lakini enenda kwa ndugu zangu ukawaambie, Ninapaa kwenda kwa Baba yangu naye ni Baba yenu, kwa Mungu wangu naye ni Mungu wenu. Mariamu Magdalene akaenda, akawapasha wanafunzi habari ya kwamba, Nimemwona Bwana, na ya kwamba amemwambia hayo.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.