Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MAMBO YA KAWAIDA YANATUFANYA TUWE TAYARI KUPOKEA YASIO YA KAWAIDA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Februari 4, 2026
JUMA LA 4 LA MWAKA

2Sam 24:2.9-17
Zab 32:1-2.5-7
Mk 6: 1-6.


MAMBO YA KAWAIDA YANATUFANYA TUWE TAYARI KUPOKEA YASIO YA KAWAIDA!


Watu waliokuwa wanamfahamu Yesu tangu akiwa kijana wanashangazwa na hekima na mambo makuu anayotenda. Walishangazwa na yote aliokuwa akisema na kutenda. Walikuwa wakimfahamu tangu alivyokuwa anakuwa, walifahamu wazazi wake na ndugu wengine, na kwa mshangao wanashangaa inawezekanaje huyu jirani yao wanaye mfahamu inawezekeanaje awavutie watu hivi na kuwa na hekima ya hali ya juu namna hii na matendo makuu. Ni wazi kwamba Yesu aliishi maisha ya kawaida kabla ya kuanza utume wake. Kiasi kwamba watu wake wa karibu hawakufahamu kwamba alikuwa mtu muhimu sana. Hili ni wazi kwasababu baada ya Yesu kuanza utume wake wa hadharani watu wake wanashangazwa na matendo yake makuu. Hawakutegemea kabisa mambo kama haya kutoka kwa Yesu wa “Nazarethi”. 

Je, sisi tunaweza kupata nini kutokana na jambo hili? Kwanza kabisa tutambue , mara nyingi mapenzi ya Mungu kwetu yanatuita kuishi maisha ya “kawaida” kabisa. Ni rahisi kuwaza kwamba tunapaswa tutende mambo makuu kwa ajili ya Mungu. Lakini vitu vikubwa ambavyo Mungu anatuitia nikuishi maisha ya kila siku ya kawaida vizuri. Hakuna wasiwasi kwamba wakati Yesu alivyokuwa akiishi maisha ya kawaida alikuwa anaishi maisha ya fadhila. Haikuwa mpango wa Mungu kwanza fadhila zake zianze kujulikana kwanza kwa wote kipindi hicho. Pili, tunaona wazi kwamba kuna wakati utume wake ulibadilika. Mapenzi ya Baba, katika maisha yake, alianza utume wake hadharani na watu wakamuona. Na wakati hili lilivyo anza watu walitambua.

Ukweli huu pia ni dhahiri pia kwetu sisi. Watu wengine wameitwa maisha ya kawaida katika hali ya kawaida kabisa. Tambua kuwa muda huu ndio muda ulioitwa ili kukuza fadhila zako, fanya mambo ya kawaida kabisa vizuri, na furahia hali ya ukimya ya maisha ya kawaida. Pia tutambue kuwa kuna uwezekano Mungu akatuita katika maisha hayo ya kawaida na kuanza kumshuhudia mbele ya watu au umati. Ufunguo ni kwamba sisi tunapaswa kumsikiliza na kuitambua sauti yake katika hali ya utulivu. Kuwa tayari na penda yeye akutumie kwa jinsi alivyopenda kwa mapenzi yake ya Kimungu.

Leo tutafakari, juu ya mapenzi ya Mungu katika maisha yetu sasa. Anataka nini kutoka kwetu? Je, anatuita kutoka katika hali yetu ya kawaida ili tuweze kuishi maisha ya kumshudia yeye mbele za watu? Au anatuita sasa tuishi maisha ya kawaida katika hali ya ukimya ya kawaida na kupalilia fadhila kwanza? Furahia mapenzi yake kwa jinsi atakavyo penda uwe na kumbatia hilo kwa moyo wote.

Sala: Bwana, nakushukuru kwa mpango wako kamili katika maisha yangu. Ninakushukuru kwa hali mbali mbali ulizoniita ili nikutumikie. Nisaidie daima niweze kuwa wazi katika mapenzi yako na daima niseme “Ndio” kwako, bila kujali unataka nifanye nini. Yesu nakuamini wewe. Amina.


.Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 4, 2026



MASOMO YA MISA, FEBRUARI 
4, 2026
JUMATANO YA JUMA LA 4 LA MWAKA


SOMO 1
2 Sam. 24:2, 9-17

Mfalme Daudi alimwambia Yoabu, jemadari wa jeshi la askari, waliokuwa pamoja naye, Zunguka sasa katikati ya kabila zote za Israeli, tangu Dani mpaka Beer-sheba, mkawahesabu watu, nipate kujua jumla ya hao watu.

Naye Yoabu akamtolea mfalme jumla ya hesabu ya watu; nao walikuwa wa Israeli mashujaa wenye kufuta panga mia nane elfu; nao wa Yuda walikuwa watu mia tano elfu.

Ndipo moyo wake Daudi ukamchoma baada ya kuwahesabu hao watu. Naye Daudi akamwambia Bwana, Nimekosa sana kwa haya niliyoyafanya lakini sasa, Ee Bwana, nakusihi uuondolee mbali uovu wa mtumishi wako; kwani nimefanya upumbavu kabisa. Na Daudi alipoondoka asubuhi, neno la Bwana likamjia nabii Gadi, mwonaji wake Daudi, kusema, Nenda, ukanene na Daudi, Bwana asema hivi, Nakuwekea mambo matatu; katika haya uchague moja, nikutendee hilo.

Basi Gadi akamwendea Daudi, akamweleza akamwambia, Basi, miaka saba ya njaa ikujie katika nchi yako? Au miezi mitatu ukimbie mbele ya adui zako, huku wakikufuatia? Au siku tatu iwe tauni katika nchi yako? Fanya shauri sasa, ufikiri, ni jawabu gani nimrudishie yeye aliyenituma. Naye daudi akamwambia Gadi, Nimeingia katika mashaka sana; basi sasa na tuanguke katika mkono wa Bwana; kwa kuwa rehema zake ni nyingi; wala nisianguke katika mkono wa wanadamu.

Basi Bwana akawaletea Israeli tauni tangu asubuhi hata wakati ulioamriwa; nao wakafa watu toka Dani mpaka Beer-sheba sabini elfu. Lakini huyo malaika aliponyosha mkono wake kuelekea Yerusalemu ili auharibu, Bwana akaghairi katika mabaya, akamwambia huyo malaika mwenye kuwaharibu watu, Yatosha, sasa ulegeze mkono wako. Naye yule malaika wa Bwana alikuwako karibu na kiwanja cha kupuria cha Arauna, Myebusi. Daudi, alipomwona malaika aliyewapiga watu, akanena na Bwana, akasema, Tazama, ni mimi niliyekosa, ni mimi niliyepotoka; lakini kondoo hawa, wamefanya nini? Mkono wako na uwe juu yangu, na juu ya nyumba ya baba yangu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 32:1-2, 5-7 (K) 5

(K) Ee Bwana, unisamehe upotovu wa dhambi yangu.

Heri aliyesamehewa dhambi,
Na kusitiriwa makosa yake.
Heri Bwana asiyemhesabia upotovu,
Ambaye rohoni mwake hamna hila. (K)

Nakujulisha dhambi yangu,
Wala sikuuficha upotovu wangu.
Nalisema, Nitayakiri maasi yangu kwa Bwana,
Nawe ukanisamehe upotovu wa dhambi yangu. (K)

Kwa hiyo kila mtu mtauwa akuombe wakati
Unapopatikana.
Hakika maji makuu yafurikapo,
Hayatamfikia yeye. (K)

Ndiwe sitara yangu, utanihifadhi na mateso,
Utanizungusha nyimbo za wokovu. (K)


SHANGILIO
Yn. 10:27

Aleluya, aleluya,
Kondoo wangu waisikia sauti yangu, asema Bwana, nami nawajua, nao wanifuata.
Aleluya.


INJILI
Mk. 6:1-6

Yesu alitoka huko, akafika mpaka nchi ya kwao, wanafunzi wake wakamfuata. Na ilipokuwa sabato, alianza kufundisha katika sinagogi; wengi waliposikia wakashangaa, wakisema, Huyu ameyapata wapi haya? Na, ni hekima gani hii aliyopewa huyu? Na, ni nini miujiza hii mikubwa inayotendeka kwa mikono yake? Huyu si yule seremala, mwana wa Mariamu, na ndugu yao Yakobo, na Yose, na Yuda, na Simoni? Na maumbu yake hawapo hapa petu? Wakajikwaa kwake. Yesu akawaambia, Nabii hakosi heshima, isipokuwa katika nchi yake mwenyewe, na kwa jaama zake, na nyumbani mwake. Wala hakuweza kufanya mwujiza wowote huko; isipokuwa aliweka mikono yake juu ya wagonjwa wachache, akawaponya. Akastaajabu kwa sababu ya kutokuamini kwao.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

IMANI YA HALI YA JUU!




“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
FEBRUARI 3, 2026
JUMA LA 4 LA MWAKA

2Sam 18:9-10,14,24-25,30 -- 19:1-3
Zab 86:1-6
Mk 5: 21-43


IMANI YA HALI YA JUU!


Katika Injili tunamuona Mwanamke aliyeteseka kwa muda wa miaka kumi na mbili kutokwa na damu. Amejaribu kutibu ugonjwa wake kwa kupitia madaktari mbali mbali na kupoteza karibu kila kitu alichokuwa nacho ili apone, lakini kwa huzuni hakufanikiwa. Inaweza kuwa kweli kwamba Mungu aliruhusu ateseke kwa miaka yote ili aweze kumpa hii nafasi ya pekee ya kudhihirisha Imani yake ili wote waweze kuiona. 

“Kama nikigusa pindo la vazi lake tu..” je alitambuaje kwamba atapona? Ni kitu ghani kilicho mwongoza mpaka awe na uhakika wa namna hii? Kwanini, baada ya kupoteza miaka yote kumi na mbili na madaktari mbali mbali na sasa anatambua sasa anaye mhitaji ni Yesu, tena aguse nguo yake apone? Jibu ni rahisi. Ni kwasababu ya zawadi ya Imani yake.

Maelezo haya kuhusu Imani yake yanafunua kwamba Imani ni zawadi ya akili ya hali ya juu ambayo ni Mungu mwenyewe aweza kuifunua. Kwa maneno mengnie, alitambua kwamba atapona, na akili ya Imani hii kwamba atapona ilikuja kwake kwa kupewa na Mungu. Baada ya kupewa alihitajika kuifanyia kazi, kwa kufanya hivyo anatoa ushuhuda wa ajabu kwao wote wanaosoma ujumbee huu siku zote katika Injili. Maisha yake, na yote aliopitia yanapaswa yatupe changamoto tutambue kwamba Mungu anaongea kwa ukweli halisi nasi, kama tutamsikiliza. Kila mara anaongea na kufunua undani wa upendo wake kwetu sisi, akituita tuingie katika maisha ya Imani ya hali ya juu. Anataka Imani yetu isiwe tu msingi wa maisha yetu, bali iwe ushuhuda wa nguvu kwa wengine. 
Mwanamke huyu alitambua kuwa Mungu atamponya na akamruhusu aongee naye. Sisi nasi tutafakari kuhusu kusikiliza kwa makini sauti ya Mungu ndani mwetu na kujaribu kuwa wazi kwenye Imani kamili ya ndani kama alivyofanya huyu mwanamke. 

Sala: Bwana, nakupenda na natamani kukusikia wewe ukiongea na mimi kila siku. Naomba uongeze Imani yangu ili niweze kukufahamu wewe na mapenzi yako katika maisha yangu. Bwana, nitumie mimi kama upendavyo niweze kuwa shuhuda wa Imani kwa wengine. Yesu, nakutumaini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, 3 FEBRUARI 2026



MASOMO YA MISA, 3 FEBRUARI 2026
JUMANNE LA JUMA LA 4 YA MWAKA


SOMO 1
2Sam. 18:9-10, 14, 24-25, 30 – 19:3

Kwa bahati Absalomu alikutana na watumishi wa Daudi. Naye Absalomu alikuwa amepanda nyumba wake, na yule nyumbu akapita chini ya matawi manene ya mwaloni mkubwa, hata kichwa chake kikakwama katika mwaloni huo, akanyakuliwa juu kati ya mbingu na nchi; na yule nyumbu aliyekuwa chini yake akaenda mbele. Basi mtu mmoja akaona hayo, akaenda akamwambia Yoabu, akasema, Tazama, mimi nalimwona Absalomu ametundikwa katika mwaloni. Yoabu akachukua vyemba vitatu mkononi mwake, akamchoma Absalomu moyoni, alipokuwa akali hai katikati ya ule mwaloni.

Basi Daudi alikuwa ameketi kati ya malango mawili; mlinzi akapanda juu hata dari ya lile lango hata ukutani, akainua macho yake, akaangalia, na tazama, mtu anakuja mbio peke yake. Mlinzi akalia, akamwambia mfalme, Naye mfalme akasema, Kama yup eke yake, ana habari kinywani mwake. Akaja mbio, akakaribia. Naye mfalme akasema, Geuka, usimame hapa, Akageuka, akasimama.

Na tazama, yule Mkushi akafika; Mkushi akasema, Nina habari kwa bwana wangu mfalme; kwa maana Bwana amekulipizia kisasi leo juu ya hao wote walioinuka kupigana nawe. Naye mfalme akamwambia yule Mkushi, Yule kijana, Absalomu, je! Yu salama? Yule Mkushi akajibu, Adui za bwana wangu mfalme, na wote wainukao ili kukudhuru, na wawe kama alivyo yule kijana.

Naye mfalme akataabika sana, akapanda juu, akaingia kile chumba kilichokuwa juu ya lango, akalia; na katika kwenda kwake alisema hivi, Mwanangu Absalomu! Ee mwanangu! Mwangu Absalomu! Laity ningalikufa badala yako, Absalomu, mwanangu, mwanangu!

Kisha Yoabu akaambiwa, Angalia, mfalme anamlilia Absalomu na kumwomboleza. Na kushinda kwao vitani siku ile kukageuzwa kuwa maombolezo kwa watu wote; maana watu walisikia siku ule ya kwamba, Mfalme anahuzunika kwa ajili ya mwanawe. Watu wakajificha siku ile, wakaingia mjini kama vile watu waonao fedheha wajifichavyo, hapo wakimbiapo vitani.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 86:1-6 (K) 1

(K) Ee Bwana, utege sikio lako, unijibu.

Ee Bwana, utege sikio lako unijibu,
Maana mimi ni maskini na mhitaji.
Unihifadhi nafsi yangu, maana mimi ni mcha Mungu,
Wewe uliye Mungu wangu,
Umwokoe mtumishi wako anayekutumaini. (K)

Wewe, Bwana, unifadhili, 
Maana nakulilia mchana kutwa.
Uifurahishe nafsi ya mtumishi wako,
Maana nafsi yangu nakuinulia wewe, Bwana. (K)

Kwa maana, Bwana, u mwema,
Umekuwa tayari kusamehe,
Na mwingi wa fadhili kwa watu wote wakuitao,
Ee Bwana, uyasikie maombi yangu,
Uisikilize sauti ya dua zangu. (K)



SHANGILIO
Mt. 8:17

Aleluya, aleluya,
Mwenye aliutwaa udhaifu wetu, na kuyachukua magonjwa yenu.
Aleluya.


INJILI
Mk. 5:21 – 43

Yesu alipokwisha kuvuka kurudia ng’ambo katika kile chombo, wakamkusanyikia mkutano mkuu; naye alikuwa kando ya bahari. Akaja mtu mmoja katika wakuu wa sinagogi, jina lake Yairo; hata alipomwona, akaanguka miguuni pake, akimsihi sana, akisema, Binti yangu mdogo yu katika kufa; nakuomba uje, uweke mkono wako juu yake, apate kupona, na kuishi. Akaenda pamoja naye. Mkutano mkuu wakamfuata, wakimsong-songa.

Na mwanamke mmoja mwenye kutoka damu muda wa miaka kumi na miwili, na kuteswa mengi kwa mikono ya matabibu wengi, amegharimiwa vitu vyote alivyo navyo, kusimfae hata kidogo, bali hali yake ilizidi kuwa mbaya; aliposikia habari za Yesu, alipita katiak mkutano kwa nyuma, akaligusa vazi lake; maana, alisema, Nikiyagusa mavazi yake tu, nitapona. Mara chemchemi ya damu yake ikakauka, anaye akafahamu mwilini mwake kwamba amepona msiba ule.

Mara yesu, ahali akifahamu nafsi ni mwake kwamba nguvu zimemtoka, akageuka kati ya mkutano, akasema, Ni nani aliyenigusa mavazi yangu? Wanafunzi wake wakambwambia, Je! Wawaona makutano wanavyokusonga-songa, nawe wasema, Ni nani aliyenigusa? Akatazama pande zote ili amwone yule aliyelitenda neno hilo. Na yule mwanamke akaingiwa na hofu na kutetemeka, akijua lililompata, akaja akamwangukia, akamweleza kweli yote. Akamwambia, Binti, Imani yako imekuponya, enenda zako kwa Amani, uwe mzima, usiwe na msiba wako tena.

Hata laipokuwa katika kunena, wakaja watu kutoka kwa yule mkuu wa sinagogi, wakisema, Binti yako amekwisha kufa; kwani kuzidi kumsumbua mwalimu? Lakini Yesu, alipolisikia lile neno likinenwa, akamwambia mkuu wa sinagogi, Usiogope, amini tu. Wala hakumruhusu mtu afuatane naye, ila Petro, na Yakobo, na Yohane nduguye Yakobo. Wakafika nyumbani kwa yule mkuu wa sinagogi, akaona ghasia, na watu wakilia, wakifanya maombolezo makuu. Alipokwisha kuingia, akawaambia, Mbona mnafanya ghasia na kulia? Kijana hakufa, bali amelala tu. Wakamcheka sana.

Naye alipokwisha kuwatoa nje wote, akamtwaa babaye yule kijana na mamaye, na wale walio pamoja naye, akaingia ndani alimokuwamo yule kijana. Akamshika mkono kijana, akamwambia, Talitha, kumi; tafsiri yake, Msichana, nakuambia, Inuka. Mara akasimama yule kijana, akaenda; maana laikuwa amepata umri wa miaka kumi na miwili. Mara wakashangaa mshangao mkuu. Akawaonya sana, mtu asijue habari ile; akaamuru apewe chakula.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo 


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUJIWEKA WAKFU KWA BWANA!



“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari ya kila siku
Jumatatu, Februari 2, 2026, 
Juma la 4 la Mwaka wa Kanisa

Sherehe ya Kutolewa Bwana hekaluni. 

Mal 3: 1-4;
Zab 24: 7-10;
Ebr 2: 14-18
Lk 2: 22-40.


KUJIWEKA WAKFU KWA BWANA!


Katika somo la Injili, Luka anaeleza taratibu tatu za sheria ambazo Maria na Yesu walijiweka. Siku nane baada ya kuzaliwa kwake, Yesu alitahiriwa. Alafu siku 33 baadae, Mama yake alimchukua Yesu Hekaluni kwa kazi mbili. Kwanza, kumtolea mtoto Yesu kwa Mungu, na alimtolea tena kwa kutoa shekeli tano. Hii ni mila ambayo ilikumbusha yote kuhusu kutolea sadaka kwa ajili ya kuokoa watoto wa kwanza wa kiume wa Israeli kutoka katika yule malaika wa kifo katika usiku wa Pasaka ya kwanza huko Misri. Pili, Maria alitolea sadaka ya mila yao ya kumtakasa na damu ya mama wakati wa kuzaliwa kwa mtoto.

Mila hizi tatu-kutahiriwa, kutakaswa baada ya mtoto kuzaliwa na sadaka ya kumuokoa mtoto wa kwanza wa kiume-vinaelekeza jinsi Mwanadamu hali yake ilikuwa ya dhambi. Kwasababu ya dhambi, Mwanadamu aliye anguka alijitenga na Mungu na alistahili tu baada ya kuhukumiwa na Mungu. Mila hizi zilionesha ulazima wa kukombolewa na kutakaswa. Mkombozi wetu alipitishwa katika mila hizi ingawaje hakutenda dhambi wala hakuwa na dhambi. Aliingia katika mila hizi kama mtoto, kama alivyokuwa mtu mzima na akaruhusu kujikabidhi kwaYohane Mbatizaji abatizwe ingawaje hakuwa na dhambi. Alifanya haya si kwasababu alihitaji utakaso wake mwenyewe bali alionyesha mshikamano wake na wadhambi ambao amekuja kuwakomboa. Kwa kufanya haya, Yesu alichukua udhaifu wetu juu ya nafsi yake mwenyewe kwa ajili ya wale aliokuja kuwakomboa. “Kwasababu alimfanya Yeye ambaye hakujua dhambi kuwa dhambi kwa ajili yetu, ili tuweze kuwa watakatifu wa Mungu kwa njia yake” (2 Kor 5:21). Wakati Maria anatolea “sadaka ya dhambi” na sadaka ya kuteketezwa kwa ajili ya utakaso, alileta sadaka ya mtu maskini njiwa wawili. Hili pia ni jambo jingine la kazi ya Yesu ya kutukomboa. Kama inavyosema “Unatambua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba alikuwa tajiri, lakini kwa niaba yetu amekuwa maskini, ili kwa njia ya umaskini wake tuweze kuwa tajiri” (2 Cor 8:9).

Simeoni alikuwa mtu mwenye haki na aliyejitoa. Roho Mtakatifu alikuwa juu yake na alimpa ufunuo wa kinabii. Alikuwa akitarajia faraja ya Isaeli, ambayo ni alama ya rafaja ya Israeli ambayo wanapokea Waisraeli kwa njia ya Masiha. Anna kwa upande mwingine alikuwa nabii. Baada ya kumuona mtoto Yesu, aliongelea kuhusu Yesu kwao wote waliokuwa wakitarajia ukombozi ambao Masiha angeleta. Siku hii ya leo tukumbuke pia kujitolea kwetu kwa Bwana kwa njia ya Ubatizo. Tujitoe wenyewe kwa Bwana na ufalme wake bila kuwa na mioyo iliogawanyika. 

Sala: Bwana nilizaliwa katika hali ya dhambi. Pokea sadaka yangu mwenyewe ya unyenyekevu na naomba unifanye nistahili ufalme wako. Yesu anakuamini wewe. Amina



Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 2, 2025



MASOMO YA MISA, FEBRUARI 2, 2025
JUMATATU, JUMA LA 4 LA MWAKA

SIKUKUU YA KUTOLEWA BWANA HEKALUNI


SOMO 1
Mal. 3:1-4

Bwana Mungu asema hivi: Angalieni, namtuma mjumbe wangu, naye ataitengeneza njia mbele yangu; naye Bwana mnayemtafuta atalijilia hekalu lake ghafula; naam yule mjumbe wa agano mnayemfurahia, angalieni, anakuja, asema Bwana wa majeshi. Lakini ni nani atakayestahimili siku ya kuja kwake? Au ni nani atakayesimama atakapoonekana yeye? Kwa maana yeye ni mfano wa moto wa mtu asafishaye fedha, ni mfano wa sabuni ya mtu afuaye nguo; naye ataketi kama asafishaye fedha na kuitakasa, naye atawatakasa wana wa Lawi, atawasafisha kama dhahabu na fedha; nao watamtolea Bwana dhabihu katika haki. Wakati ule ndipo dhabihu za Yuda na Yerusalemu zitakapopendeza mbele za Bwana, kama katika siku za kale, na kama katika miaka ya zamani.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
ZAB. 24:7-10 (K) 8

(K) Ni nani Mfalme wa utukufu? Ni Bwana.

Inueni vichwa vyenu, enyi malango,
Inukeni, enyi malango ya milele, 
Mfalme wa utukufu apate kuingia. (K)

Ni nani Mfalme wa utukufu?
Bwana mwenye nguvu, hodari,
Bwana hodari wa vita. (K)

Inueni vichwa vyenu, enyi malango,
Naam, viinueni, enyi malango ya milele
Mfalme wa utukufu apate kuingia. (K)

Ni nani huyu Mfalme wa utukufu?
Bwana wa majeshi,
Yeye ndiye Mfalme wa utukufu. (K)


SOMO 2
Ebr. 2:14-18

Basi, kwa kuwa watoto wameshiriki damu na mwili, yeye naye vivyo hivyo alishiriki yayo hayo, ili kwa njia ya mauti amharibu yeye aliyekuwa na nguvu za mauti, yaani, Ibilisi, awaache huru wale ambao kwamba maisha yao yote kwa hofu ya mauti walikuwa katika hali ya utumwa. Maana ni hakika, hatwai asili ya malaika, ila atwaa asili ya mzao wa Ibrahimu. Hivyo ilimpasa kufananishwa na ndugu zake katika mambo yote, apate kuwa kuhani mkuu mwenye rehema, mwaminifu katika mambo ya Mungu, ili afanye suluhu kwa dhambi za watu wake. Na kwa kuwa mwenyewe aliteswa alipojaribiwa, aweza kuwasaidia wao wanaojaribiwa.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


SHANGILIO
Lk. 2:32

Aleluya, aleluya!
Nuru ya kuwa mwangaza wa Mataifa, Na kuwa utukufu wa watu wako Israeli.
Aleluya!


INJILI
Lk. 2:22-40

Zilipotimia siku za kutakasika kwao, kama ilivyo torati ya Musa, wazee wa Yesu walikwenda naye hata Yerusalemu, wamweke kwa Bwana, (kama ilivyoandikwa katika sheria ya Bwana, Kila mtoto mwanamume aliye kifungua mimba ya mamaye na aitwe mtakatifu kwa Bwana), wakatoe na sadaka, kama ilivyonenwa katika sheria ya Bwana, Huwa wawili au makinda ya njiwa wawili. Na tazama, pale Yerusalemu palikuwa na mtu, jina lake Simeoni, naye ni mtu mwenye haki, mcha Mungu, akiitarajia faraja ya Israeli; na Roho Mtakatifu alikuwa juu yake. Naye alikuwa ameonywa na Roho Mtakatifu ya kwamba hataona mauti kabla ya kumwona Kristo wa Bwana. Basi akaja hekaluni ameongozwa na Roho; na wale wazazi walipomleta mtoto Yesu ndani, ili wamfanyie kama ilivyokuwa desturi ya sheria, yeye mwenyewe alimpokea mkononi mwake, akamshukuru Mungu, akisema, Sasa, Bwana, wamruhusu mtumishi wako, kwa amani, kama ulivyosema; kwa kuwa macho yangu yameuona wokovu wako, uliouweka tayari machoni pa watu wote; nuru ya kuwa mwangaza wa mataifa, na kuwa utukufu wa watu wako Israeli.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MAISHA YA FURAHA!



“MBEGU ZA UZIMA”
Tafakari ya kila Jumapili
Jumapili, Februari 1, 2026 
Juma la 4 la Mwaka A wa Kanisa

Sef 2: 3; 3: 12-13; 
Zab 146: 6-10; 
1Kor 1: 26-31; 
Mt 5: 1-12.


MAISHA YA FURAHA!

Sisi wote tunapenda kuwa na furaha, na huwa tunajishughulisha kwa hatima hii katika hali mbali mbali. Masomo ya leo yanatuonesha jinsi ya kuwa na maisha ya furaha. Lakini ni kinyume na jinsi tunavyo fikiria. Huwa tunajua kuwa maskini, kuwa mpole na kuonewa haviongozi kwenda kwenye maisha ya furaha. Ila kujiinua kwa ukuu wetu, mafanikio yetu, maisha yanayo zalisha, majivuno yanaongoza kwenye maisha ya furaha.

Katika somo la kwanza tunasikia kuishi katika maisha ya umaskini wa roho maana yake kuishi kwa unyenyekevu itatuongoza kwenda kwenye furaha. Na katika somo la pili tunasikia Mt. Paulo akitujulisha kwamba uchaguzi wa Mungu ni tofauti na uchaguzi wa Mwanadamu wanaofanya. Mungu anachagua wale wanyonge katika jamii na dhaifu mbele ya uso wa Ulimwengu ili kuwanyenyekesha wenye majivuno. Leo katika injili tunamuona Yesu akihutubia mlimani, akitupa njia za kuwa na furaha. Yesu kwa kupitia “heri” anatupa njia sahihi za kuingia kwenye furaha. Zinatuongoza kwanza, katika uhusiano na Mungu na hapo ni Mungu atakaye tubariki ili tuwe na maisha ya furaha. Zinaonesha wazi kwamba sio mwanadamu anaye ongoza kwenye furaha bali ni Mungu na hali zetu kumwelekea yeye. 

Katika masomo ya Noeli, Yesu alifunuliwa kama Mwana wa Kifalme wa Daudi na Mwana wa Mungu. Kama Musa alivyowaongoza Waisraeli kupitia bahari ya Shamu na kuwapa sheria ya Mungu katika mlima Sinai, Yesu pia amepita katika maji ya ubatizo na sasa katika Injili, anaenda Mlimani kutangaza sheria mpya- sheria ya ufalme wake. Heri hizi zina ashiria ukamilifu wa Agano la Mungu alilo mwahidia Abrahamu- kwamba kupitia uzao wake mataifa yote yatapokea Baraka za Mungu (Mwa 12:3; 22:18).

Heri hizi sinatufunulia njia ya Kimungu na malengo ya maisha yetu. Kujitahidi kwetu kote kunapaswa kuwa kwa fadhila hizi-kwa maskini wa roho; wanyenyekevu na wenye moyo safi; wenye huruma na watengenezaji wa Amani, watafuta haki inayotoka katika sheria ya Ufalme wa Mungu. Njia ambayo Mungu ameiweka mbele yetu leo ni njia yenye majaribu na mateso. Lakini ana ahidi kutufariji katika huzuni na kutupa thawabu kubwa. 

Heri hizi zipo katika mtiririko wa pekee, kuanzia heri ya kwanza ambayo heri maskini wa roho. Ni kwa kuanza kwa kuwa mnyenyekevu mbele ya Mungu na kuruhusu upendo wa Mungu uingie katika maisha yetu. Kwani kwa unyenyekezu wa roho utatufanya tuvumilie yote, kuonewa na kuteswa na kujitahidi katika maisha yetu. Na mwisho wa yote tutapata raha na kuridhika. Mungu amechagua kuwabariki wanyonge na wadogo, wale wanao onekana wajinga na wasiopendwa katika macho ya dunia, kama anavyosema Paulo katika somo la pili. Wale maskini wa roho ni wale wanao fahamu kwamba hawawezi kufanya chochote na kufanikiwa pasipo huruma na neema ya Mungu. 

Sisi tupo katika kipindi ambacho tunavutwa sana na raha na kujiridhisha kwa starehe za dunia, kuwa na mali nyingi na mafanikio makubwa. Haya yote yanatupa hali ya shauku kubwa. Lakini ukweli ni kwamba hatujawahi kuridhika na kila kukicha tunatafuta zaidi na zaidi. Tajiri mkubwa, bado anahitaji zaidi, ana kila kitu katika maisha lakini bado hana raha ya maisha. Tumeona maisha ya matajiri wengi katika dunia, hawajawahi kuridhika, daima wanatafuta ili aweze kuwa juu ya wengine na kwa hili hana raha anahangaika daima. 

Jumapili iliopita masomo yaliongelea kuhusu wito wetu wa pamoja wa kuwa wafuasi. Tumepewa wito wa kuwa mwanga kwa ulimwengu. Na leo Yesu, anatupa mwanga-maneno ya uzima wa milele. Yesu anatuonesha sisi njia ambayo tunaweza kuiishi sio maneno matupu pekee. Kwasababu yeye mwenyewe aliishi heri zote tangu kuzaliwa mpaka ufufuko wake. Ni njia ya kuelekea kwenye maisha ya furaha ambayo ni maisha ya uzima wa milele. Sio safari rahisi, kwani twaweza kukumbana na umaskini katika maisha, kuumizwa, kuteseka kwa sababu ya haki na kuuonewa. Lakini, ni pale ambapo tutafungua mioyo yetu kwa Yesu tunaweza kupata furaha na kuridhika katika maisha ambayo anatupa sisi kutoka katika upendo wake usio na mwisho. 

Heri ni kipimo kamili cha maisha ya furaha na zaidi sana maisha yetu ya Kikristo. Zinatuita kwenda sehemu yenye faraja kamili. Tunapaswa kuwa jasiri na kuwa tayari kwenda kinyume na yale mambo ya wakati huu yanayo pingana na “heri”, tuwe tayari kusema “hapana” kwa maisha ya raha za muda tu na kutupilia mbali tamaduni mbaya, ambazo kwa ukweli zinatupa raha ya muda tu katika maisha. 

Sala: Bwana, ninaomba niweze kukumbatia “heri” zote ulizo tupatia sisi. Ninasali, zaidi sana , moyo wangu uweze kukua katika unyenyekevu. Ninaomba ukue katika kuwaonea huruma wanao onewa, wanao umizwa, waliochanganyikiwa na waliobanwa na maisha ya dhambi. Ninakushukuru kwa Baraka unazoendelea kunipa. Yesu, nakuamini wewe. Amina


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 1, 2026



MASOMO YA MISA, FEBRUARI 1, 2026
DOMINIKA YA 4 YA MWAKA A


MWANZO:
Zab. 106:47

Ee Bwana Mungu wetu, utuokoe, utukusanye kwa kututoa katika mataifa, tulishukuru jina lako takatifu, tuzifanyie shangwe sifa zako.


SOMO 1
Sef. 2:3, 3:12 – 13

Mtafuteni Bwana, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya Bwana.

Lakini nitasaza ndani yako watu walioonewa na masikini, nao watalitumainia jina la Bwana. Mabaki ya Israeli hawatatenda uovu, wala kusema uongo; wala ulimi wa hadaa hautaonekana kinywani mwao; kwa maana watakula na kulala, wala hapana mtu atakayewaogofya.

Neno la Mungu… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 146:6b – 10 (K) Mt. 5:3

(K) Heri walio maskini wa roho; Maana ufalme wa mbinguni ni wao.

Huishika kweli milele.
Huwafanyia hukumu walioonewa,
Huwapa wenye njaa chakula;
Bwana hufungua waliofungwa. (K)

Bwana huwafumbua macho waliopofuka;
Bwana huwainua walioinama;
Bwana huwapenda wenye haki;
Bwana huwahifadhi wageni. (K)

Huwategemeza yatima na mjane;
Bali njia ya wasio haki huipotosha.
Bwana atamiliki milele,
Mungu wako, Ee Sayuni, kizazi hata kizazi. (K)



SOMO 2
1Kor. 1:26 – 31

Ndugu zangu, angalieni mwito wenu, ya kwamba si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheo walioitwa; bali Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima; tena Mungu alivichagua vitu dhaifu vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu; tena Mungu alivichagua vitu vinyonge vya dunia na vilivyodharauliwa, naam, vitu ambavyo haviko, ili avibatilishe vile vilivyoko; mwenye mwili awaye yote asije akajisifu mbele za Mungu. Bali kwa yeye ninyi mmepata kuwa katika Kristo Yesu, aliyefanywa kwetu hekima itokayo kwa Mungu, na haki, na utakatifu, na ukombozi; kusudi, kama ilivyoandikwa, Yeye aonaye fahari na aone fahari juu ya Bwana.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



SHANGILIO
Yn. 14:5

Aleluya, aleluya,
Tomaso akamwambia Bwana, Sisi hatujui uendako, nasi twaijuaje njia?
Aleluya.



INJILI
Mt. 5:1-12

Yesu alipowaona makutano, alipanda mlimani; na alipokwisha kuketi, wanafunzi wake walimjia; akafumbua kinywa chake, akawafundisha, akisema,
Heri walio maskini war oho; Maana ufalme wa mbinguni ni wao.
Heri wenye huzuni; maana hao watafarijika.
Heri wenye upole; maana hao watairithi nchi.
Heri wenye njaa na kiu ya haki;
Maana hao watashibishwa.
Heri wenye rehema; maana hao watapata rehema.
Heri wenye moyo safi; maana hao watamwona Mungu.
Heri wapatanishi; maana hao wataitwa wana wa Mungu.
Heri wenye kuudhiwa kwa ajili ya haki; maana ufalme wa mbinguni ni wao.
Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUMWAMINI YESU KWA MAISHA YETU!



ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Jumamosi, Januari 31, 2026
JUMA LA 3 LA MWAKA 

2 Sam 12:1-7.10-17;
Zab 51:10-15
Mk 4: 35-41

KUMBUKUMBU YA MT. YOHANE BOSCO


KUMWAMINI YESU KWA MAISHA YETU!


Bahari na mawimba yana mtii Mungu kwasababu ni sehemu ya uumbaji wake. Na wala hakuna tatizo kubwa sana kwa Mungu ambalo anashindwa kulitatua. Hofu zetu hazina mwisho, matatizo yetu yanatusumbua, kwasababu sisi wenyewe tumechagua kuyakabili wenyewe kwa nguvu zetu. Wafuasi walikuwa ni watu wa kawaida kama sisi. Hata wakiwa kati ya Yesu wana ogopeshwa na gharika! Laiti kama Mwanadamu angelijua kukabidhi hofu zake na maumivu yake kwa Mungu! 

Ni rahisi sana kukata tamaa katika maisha. Ni rahisi zaidi kuelekeza mwelekeo wote kwenye matatizo na kuacha mengine yanayo tuzunguka. Hata kama ingekuwa ni maneno ya hasira na ya kuumiza kutoka kwa wengine, matatizo ya kifamilia, matatizo ya umma, ukosefu wa fedha nk. Kuna kila sababu ya kila mmoja wetu kuanguka kwenye mtego wa hofu, kuchanganyikiwa, kuumia na kuwa na shauku. Lakini ilikuwa ni kwasababu ya sababu hizi Yesu aliruhusu tukio hili litokee akiwa na wafuasi wake. Alikuwa kwenye boti na wafuasi wake akaruhusu wafuasi wakumbwe na gharika kuu, wakati yeye akiwa amelala, ili aweze kuleta ujumbe wa kufaa kwetu sisi wote. 

Katika habari hii, wafuasi walilenga kwenye kitu kimoja tuu: walikuwa waangamie! Bahari ilikuwa ikiwasukasuka na waliogopa maangamizi makubwa! Lakini kwa kupitia yote hayo, Yesu alikuwa pale akionekana amelala, akiwasubiri waweze kumwamsha. Na walipo mwamsha, alikemea gharika na hali ikawa shwari. Hili ni kweli pia katika maisha yetu. Sisi mara nyingi tunaruhusu matatizo mengi tunayopata yatutese na kutusukasuka. Ufunguo ni kwamba tunapaswa kugeuza macho yetu na kumwelekea Yesu. Muone mbele yako amelala, anakusubiri umwamshe. Yupo daima, akikusubiri na yupo tayari daima. Kumwamsha Bwana wetu ni rahisi kama ilivyo rahisi kugeuza macho yetu kutoka katika gharika na kusadiki uwezo wake wa Kimungu. Yote ni kuwa na Imani kwake tu. Imani kamili. Je, una mwamini yeye? Tumwache Yesu achukue nafasi ya kila kitu katika maisha yetu tuliopo. Anatupenda na kweli atatujali wote. 

Sala: Bwana, ninakugeukia katikati ya changamoto za maisha na ninatamani kukuamsha uje katika maisha na kunisaidia. Ninatambua upo daima karibu yangu, ukinisubiri mimi nikuamini wewe kwa kila kitu. Nisaidie nielekeze macho yangu kwako na kuwa na Imani kamili katika mapendo yako. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, JANUARI 31, 2026







MASOMO YA MISA, JANUARI 31, 2026
JUMAMOSI YA JUMA LA 3 LA MWAKA

KUMBUKUMBU YA MT. YOHANE BOSCO


SOMO 1
2 Sam. 12:1-7, 10-17

Bwana alimtuma Nathani aende kwa Daudi. Naye akamwendea, akamwambia, Palikuwa na watu wawili katika mji mmoja; mmoja wao alikuwa tajiri, wa pili maskini. Yule tajiri alikuwa na kondoo na ng’ombe wengi sana; bali yule maskini hakuwa na kitu, ila mwana-kondoo mmoja, mdogo, ambaye amemnunua na kumlea; naye akakua pamoja naye, na pamoja na wanawe; hula sehemu ya posho lake, na kukinywea kikombe chake, na kulala kifuani mwake, akawa kwake kama binti. Hata msafiri mmoja akamfikilia yule tajiri, naye akaacha kutwaa mmoja wa kondoo zake mwenyewe au mmoja wa ng’ombe zake mwenyewe, ili kumwandalia yule msafiri aliyemfilia, bali alimnyang’anya yule maskini mwana-kondoo wake, akamwandalia yule mtu aliyemfikilia. 

Ndipo hasira ya Daudi ikawaka sana juu ya mtu yule; akamwambia Nathani, Aishivyo Bwana, mtu huyo aliyetenda jambo hili, hakika yake astahili kufa; naye atamrudishia yule mwana-kondoo mara nne, kwa sababu ametenda neno hili, na kwa sababu hakuwa na huruma. 
Basi, Nathani akamwambia Daudi, Wewe ndiwe mtu huyo. Basi, sasa upanga hautaondoka nyumbani mwako, kwa sababu umenidharau, ukamtwaa mkewe Uria, Mhiti, kuwa mke wako.

Bwana asema hivi, Angalia, nitakuondokeshea uovu katika nyumba yako, anmi nitawatwaa wake zako mbele ya macho yako, na kumpa jirani yako, naye atalala na wake zako mbele ya jua hili. Maana wewe ulifanya jambo lile kwa siri; bali mimi nitalifanya jambo hili mbele ya Israeli wote na mbele ya jua.

Daudi akamwambia Nathani, Nimemfanyia Bwana dhambi. Nathani akamwambia Daudi, Bwana naye ameiondoa dhambi yako; hutakufa. Lakini, kwa kuwa kwa tendo hili umewapa adui za Bwana nafasi kubwa ya kukufuru, mtoto atakayezaliwa kwako hakika yake atakufa. Naye Nathani akatoka kwenda nyumbani kwake.

Basi Bwana akampiga yule mtoto ambaye mkewe Uria alimzalia Daudi, naye akawa hawezi sana. Basi Daudi akamwomba Mungu kwa ajili ya mtoto; Daudi akafunga, akaingia, akalala usiku kucha chini. Nao wazee wa nyumba yake wakondoka, wakasimama karibu naye, ili wamwinue katika nchi; lakini hakukubali, wala hakula chakula pamoja nao.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 51:10-15 (K) 12

(K) Ee Mungu, uniumbie moyo safi.

Ee Mungu, uniumbie moyo safi,
Uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu.
Usinitenge na uso wako,
Wala roho yako takatifu usiniondolee. (K)

Unirudishie ya wokovu wako,
Unitegemeze kwa roho ya wepesi.
Nitawafundisha wakosaji njia zako,
Na wenye dhambi watarejea kwako. (K)

Ee Mungu, Mungu wa wokovu wangu,
Uniponye na damu za watu,
Na ulimi wangu utaiimba haki yako.
Ee Bwana, uifumbue midomo yangu,
Na kinywa changu kitazinena sifa zako. (K)


SHANGILIO
Yn. 3:16

Aleluya, aleluya,
Jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe wa pekee, ili kila mtu aaminiye awe na uzima wa milele.
Aleluya.


INJILI
Mk. 4:35-41

Siku ile kulipokuwa jioni, Yesu akawambia, Na tuvuke mpaka ng’ambo. Wakauacha mkutano, wakamchukua vile vile alivyo katika chombo. Na vyombo vingine vilikuwako pamoja naye. Ikatokea dhoruba kuu ya upepo, mawimbi yakakipiga chombo hata kikaanza kujaa maji. Naye mwenyewe alikuwapo katika shetri, amelala juu ya mto; wakamwamsha, wakamwambia, Mwalimu, si kitu kwako kuwa tunaangamia? Akaamka, akaukemea upepo, akaiambia bahari, Nyamaza, utulie. Upepo ukakoma, kukawa shwari kuu. Akawaambia, Mbona mmekuwa waoga? Hamna Imani bado? Wakaingiwa na hofu kuu, wakaambiana, Ni nani huyu, basi, hata upepo na bahari humtii?

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.