Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

UNA KIU?



“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Jumapili, Machi 8, 2026
Juma la 3 la Kwaresima

Kut 17: 3-7;
Zab 95: 1-2, 6-9;
Rum 5: 1-2, 5-8;
Yn 4: 5-42.


UNA KIU?


 “Gods must be crazy” Ni jina la filamu na ni juu ya watu walioko katika Jangwa la Kalahari. Filamu hii inaonesha wazoefu wa jangwa. Mmoja wa watu hawa alitembelea mabubujiko ya maji ya Tungela (maporomoko makubwa ya maji Afrika), huko Afrika kusini. Alishangazwa kuona maji makubwa yanashuka kutoka juu. Alisimama pale kwa masaa akishangaa. Hawa watu waliopo Kalahari walizoea kukusanya maji kutoka katika majani (umande) au kupata maji kutoka katika aina ya mmea ambao shina lake huwa na maji, ili kupooza kiu yao. Kama ilivyo katika simulizi hilo, lirtujia ya leo ya Domini ya tatu ya Kwaresima inatuonesha kwamba sisi wote tuna kiu. Watu wana kiu ya fedha, anasa, madaraka, na mali, na hata kama akipata nyingi, bado kiu ni kubwa. Katika hali nyingine kuna “maji ya uzima” upande mwingine ndani ya Yesu Kristo. Tunapojiandaa wenyewe kuingia katika mafumbo ya mateso, kifo na ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo kipindi hiki cha Kwaresima, tunaitwa leo tutulize kiu yetu ya kiroho na kutuliza kiu ya Yesu anayezitafuta roho zetu na ana zisubiri zirudi kwake. Yesu alipata kiu ya mwanadamu kumrudia Mungu, na hivyo akasema pale msalabani “Nina kiu”.

Katika somo la kwanza tunaona Waisraeli wanao lalamika. Watu hawa hawa waliovushwa salama kutoka katika utumwani huko Misri, na waliokuwa wakitembea kwa uhuru kuelekea Nchi ya ahadi. Kwanza kabisa walilalamika kuhusu chakula, Mungu akawapa mana, mkate kutoka mbinguni. Hata baada ya kuona muujiza huu bado hawaja uamini upendo wa Mungu. Wakaanza kukusanya zaidi ya mahitaji yao, lakini yote iliharibika siku iliofuata. Alafu wakaanza kulalamika kwasababu ya maji. Pamoja na hilo Mungu akafanya muujiza mwingine akawapa maji. Lakini Israeli hakujifunza kumtuminia Mungu. Mwanadamu ni kiumbea ambaye haridhiki. Mahitaji yetu daima tunaona hayatoshi, yanaendelea kuongezeka daima. Ni kama vile kula chumvi, unahisi kiu kila wakati, alafu baadae unakula tena chumvi unahisi kiu tena.

Katika somo la Injili tunamuona huyu Mwanamke msamaria ambaye pia alikuwa akiishi maisha yake yasio pendeza. Alikuwa katika kisima ili kutuliza kiu yake ya kila siku. Alikuwa anajiribu kutuliza kiu ya mwili wake kwa kila aina ya anasa. Lakini kila siku alikuwa akirudi katika kisima kwa ajili ya maji. Yeye kama ilivyo kwa wanadamu wote ni lazima alisimama nakuuliza “hivi kuna aina ya maji ambayo nikinywa sintaona kiu tena?”. Mt. Agustino anatoa jibu anavyosema “mioyo yetu haitatulia …hadi itakapo tulia kwako Bwana Yesu”

Yesu alikuwa njiani kuelekea Yerusalemu kwa kupitia Samaria. Watu wasamaria walionekana kama Wayahudi wasio faa au Wayahudi waliochanganyika. Hawakuwa wakichukuliwa kama sehemu ya jamii ya Wayahudi. Hata tunaona Yesu anakutana na Mwanamke Msamaria. Huyu Mwanamke alikuja katika kisima kuja kuchota maji saa sita mchana. Hii ilikuwa sio kawaida kwasababu, wanawake walikuja kuchota maji wakiwa katika makundi tena ikiwa ni hasubuhi au jioni. Huyu mwanamke inaonekana alipenda kuwakwepa wenzake pengine kwasababu ya tabia ya maisha yake ambayo Yesu alimwambia baadae. Yesu akiwa ni Myahudi anamuomba maji ya kunywa. Alikuwa na mazunguzo naye ambayo yalimlenga kutoka katika mazungumzo ya maji ya kawaida hadi kwenye maji ya uzima, kutoka katika kiu ya kidunia hadi kiu ya kiroho. Anashindwa kumtambua Yesu hapo mwanzo, na Yesu anirarua dhamiri yake kwa kufunua ukweli wa maisha yake. Hili lilikuwa rahisi kwake kupokea neema ya Mungu. Yesu anamsaidia katika hali ya kukuwa na kutambua kumwadudu na hapo anamtambua Yesu kama Masiha. Baada ya kumtabua Yesu, analeta kijiji kizima kwake. Mwanamke ambaye alikuwa amekataliwa na jamii anakuwa chombo cha Mungu cha kuwaleta wanakijiji kwa Yesu. Alikuja kuchukua maji ya kawaida akarudi na maji ya uzima. Yesu hakunywa hata tone moja la maji, lakini kiu yake ilitulizwa kwa kupata roho moja kwa ajili yake.

Yesu alijua yote kuhusu huyu Mwanamke lakini alitaka kumpa maji ya uzima. Alitaka kuzima kiu ambayo yeye alikuwa nayo rohoni mwake. Alivyokuwa akiongea naye, na kuanza kumsikiliza kiu yake ilianza kuzimwa. Ilianza kuzimwa kwasababu ndicho alichohitaji, tunachohitaji wote, ni upendo huu kamili na kukubaliwa na Yesu, ambao Yesu anautoa mwenyewe. Alitoa kwake, na anataka kuutoa kwetu pia. Cha kushangaza Mama huyu aliondoka na kuacha “mtungi”. Hakuchukua maji aliokuwa amekuja kuchukua. Au alichukuwa? Katika hali hii ya kuacha mtungi ni alama kwamba kiu yake ilikuwa imezimwa kwa kukutana na Yesu. Hakuwa tena na kiu, Yesu alizima kiu yake.

Katika kuishi kwetu kila siku, tunajikuta tukimwacha Mungu na kutafuta mambo yanayo pita. Tunafatilia tukitafuta maana katika hivyo vitu lakini tunakuta hamna, ni utupu ndani yake. Tutafakari juu ya kiu isiopingika tulio nayo ndani mwetu. Tukisha itambua, tuelekeze dhamiri zetu kumwelekea Yesu ili azime kiu yetu kwa maji ya uzima. Tukifanya hivi, tutaacha mitungi mingi ambayo kwakweli haizimi kiu yetu.

Sala: Bwana, wewe ni maji ya uzima ambayo roho yangu inatafuta. Ninakuomba nikutane na wewe katika maisha yangu, katika aibu yangu na maumivu ya moyo. Ninaomba nikutane na upendo wako, upole wako na kukukubali sasa, ninaomba upendo wako uwe chanzo cha maisha yangu ndani yako. Yesu nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MACHI 8, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 8, 2026
JUMAPILI YA 3 YA KWARESIMA

MWANZO:
Zab. 25:15 – 16

Macho yangu humwelekea Bwana daima, naye atanitoa miguu yangu katika wavu. Uniangalie na kunifadhili, maana mimi ni mkiwa na mteswa.


SOMO 1
Kut. 17:3 – 7

Watu wakawa na kiu huko; nao wakamnung’unikia Musa, wakasema, Mbona umetupandisha kutoka Misri, kutuua sisi na watoto wetu na wanyama wetu kwa kiu? Musa akamlilia Bwana, akisema, Niwatendee nini watu hawa? Bado kidogo nao watanipiga kwa mawe.

Bwana akamwambia Musa, Pita mbele ya watu, ukawachukue baadhi ya wazee wa Israeli pamoja nawe; na ile fimbo yako ambayo uliupiga mto kwayo, uitwae mkononi mwako, ukaende. Tazama, nitasimama mbele yako huko, juu ya lile jabali katika Horebu; nawe utalipiga jabali, na maji yatatoka, watu wapate kunywa.

Musa akafanya hivyo mbele ya wazee wa Israeli. Akapaita mahali pale jina lake Masa, na Meriba; kwa sababu ya mateto ya wana wa Israeli, na kwa sababu walimjaribu Bwana, wakisema, Je! Bwana yu kati yetu au sivyo?

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 95:1 – 2, 6 – 9 (K) 8

(K) Ingekuwa heri leo msikie sauti yake!
Msifanye migumu mioyo yenu.

Njoni, tumwimbie Bwana,
Tumfanyie shangwe mwamba wa wokovu wetu.
Tuje mbele zake kwa shukrani,
Tumfanyie shangwe kwa zaburi. (K)

Njoni, tuabudu, tusujudu,
Tupige magoti mbele za Bwana aliyetuumba.
Kwa maana ndiye Mungu wetu,
Na sisi tu watu wa malisho yake,
Na kondoo za mkono wake. (K)

Ingekuwa heri leo msikie sauti yake!
Msifanye migumu mioyo yenu;
Kama vile huko Meriba,
Kama siku ya Masa Jangwani.
Hapo waliponijaribu baba zenu,
Wakanipima, wakayaona matendo yangu. (K)


SOMO 2
Ru. 5:1 – 2, 5 – 8

Basi tukiisha kuhesabiwa haki itokayo katika Imani, na tuwe na Amani kwa Mungu, kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo. Ambaye kwa yeye tumepata kwa njia ya Imani kuifikia neema hii ambayo tunasimama ndani yake; na kufurahi katika tumaini la utukufu wa Mungu.

Na tumanini halitahayarishi; kwa maana pendo la Mungu limekwisha kumiminwa katika mioyo yetu na Roho Mtakatifu tuliyepewa sisi. Kwa maana hapo tulipokuwa hatuna nguvu, wakati ulipotimia, Kristo alikufa kwa ajili ya waovu. Kwa kuwa ni shida mtu kufa kwa ajili ya mtu mwenye haki; lakini yawezekana mtu kuthubutu kufa kwa ajili ya mtu aliye mwema. Bali Mungu aonyeshe pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi.


SHANGILIO
Yn. 4:15

Bwana, hakika wewe ndiwe Mwokozi wa ulimwengu,
unipe maji yale ya uzima, nisione kiu kamwe.


INJILI
Yn. 4:5 – 42

Yesu alifika kunako mji wa Samaria, uitwao Sikari, karibu na lile shamba ambalo Yakobo alimpa Yusufu, mwanawe. Na hapo palikuwa na kisima cha Yakobo. Basi Yesu, kwa sababu amechoka kwa safari yake, akaketi vivi hivi kisimani. Nayo ilikuwa yapata saa sita. Akaja mwanamke Msamaria kuteka maji. Yesu akamwambia, Nipe maji ninywe. Kwa maana wanafunzi wake wamekwenda mjini kununua chakula. Basi yule mwanamke Msamaria akamwambia, Imekuwaje wewe Myahudi kutaka maji kwangu, nami ni mwanamke Msamaria? (maana Wayahudi hawachangamani na Wasamaria).

Yesu akajibu, akamwambia, Kama ungalijua karama ya Mungu, naye ni nani akuambiaye, Nipe maji ninywe, ungalimwomba yeye, naye angalikupa maji yaliyo hai.

Yule mwanamke akamwambia, Bana, huna kitu cha kutekea, na kisima ni kirefu; basi umeyapata wapi hayo maji yaliyo hai? Je! Wewe u mkubwa kuliko baba yetu, Yakobo, aliyetupa kisima hiki, naye mwenyewe akanywa maji yake, na wanawe pia, na wanyama wake?

Yesu akajibu, akamwambia, Kila anyway maji haya ataona kiu tena; walakini yeyote atakayekunywa maji yale nitakayompa mimi hataona kiu milele; bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa milele.

Yule mwanamke akamwambia, Bwana, unipe maji hayo, nisione kiu, wala nisije hapa kuteka.

Yesu akamwambia, Nenda kamwite mumeo, uje naye hapa. Yule mwanamke akajibu, akasema, Sina mume. Yesu akamwambia, Umesema vema, Sina mume; kwa maana umekuwa na waume watano, naye uliye naye sasa siye mume wako; hapo umesema kweli. Yule mwanamke akamwambia, Bwana, naona ya kuwa u nabii! Baba zetu waliabudu katika mlima huu, nanyi husema ya kwamba huko Yerusalemu ni mahali patupasapo kuabudia. Yesu akamwambia, Mama, unisadiki, saa inakuja ambayo hamtamwabudu Baba katika mlima huu, wala kule Yerusalemu. Ninyi mnaabudu msichokijua; sisi tunaabudu tukijuacho; kwa kuwa wokovu watoka kwa Wayahudi. Lakini saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu. Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli. Yule mwanamke akamwambia, Najua ya kuwa yuaja Masihi, (aitwaye Kristo); naye atakapokuja, yeye atatufunulia mambo yote. Yesu akamwambia, Mimi ninayesema nawe, ndiye.

Mara hiyo wakaja wanafunzi wake, wakastaajabu kwa sababu alikuwa akisema na mwanamke; lakini hakuna aliyesema, Unatafuta nini? Au, Mbona unasema naye? Basi yule mwanamke akauacha mtungi wake, akaenda zake mjini, akamwambia watu, Njoni, mtazame mtu aliyeniambia mambo yote niliyoyatenda. Je! Haimkini huyu kuwa ndiye Kristo? Basi wakatoka mjini, wakamwendea.

Huko nyuma wanafunzi wakamsihi wakisema, Rabi, ule. Akawaambia, Mimi ninacho chakula msichokijua ninyi. Basi wanafunzi wake wakasemezana, Je! Mtu amemletea chakula? Yesu akawaambia, Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake. Hamsemi ninyi, Bado miezi mine, ndipo yaja mavuno? Tazama, mimi nawaambieni, Inueni macho yenu myatazame mashamba, ya kuwa yamekwisha kuwa meupe, tayari kwa mavuno. Naye avunaye hupokea mshahara, na kukusanya matunda kwa uzima wa milele, ili yeye apandaye na yeye avunaye wapate kufurahi pamoja. Kwa maana hapo neno hilo huwa kweli, Mmoja hupanda akavuna mwingine. Mimi naliwatuma myavune yale msiyoyataabikia; wengine walitaabika, nanyi mmeingia katika taabu yao.

Na katika mji ule Wasamaria wengi walimwamini kwa sababu ya neno la yule mwanamke, aliyeshuhudia kwamba, Aliniambia mambo yote niliyoyatenda. Basi wale Wasamaria walipomwendea, walimsihi akae kwao; naye akakaa huko siku mbili. watu wengi zaidi wakaamini kwa sababu ya neno lake. Wakamwambia yule mwanamke, Sasa tunaamini, wala si kwa sababu ya maneno yako tu; maana sisi tumesikia wenyewe, tena twajua ya kuwa hakika huyu ndiye Mwokozi wa ulimwengu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

KUMRUDIA MUNGU!



“ASALI ITOKAYO MWMABANI”
Tafakari ya Kwaresima
Jumamosi, Machi 7, 2026
Juma la 2 la Kwaresima

Mika 7:14-15,18-20;
Zab 103;1-4, 9-12;
Lk 15: 1-3, 11-32


KUMRUDIA MUNGU!


Katika mfano wa Mwana mpotevu tunaona ujasiri wa huyu Mwana kwa kuchagua kurudi kwa Baba yake. Ni kweli, alitambua udhaifu wake na akaamua kurudi kwa Baba yake kuomba msamaha na kumuomba amfanye kama mmoja wa wafanyakazi wake. Alifanikiwa kurudi.! Swali la kujibu “kwanini?”

Ni vyema kusema kwamba huyu mtoto alirudi kwa Baba yake, kwanza kabisa kwasababu alitambua kutoka moyoni mwake tabia ya Baba yake. Baba alikuwa Baba mwema. Alionyesha kujali na kuwa na upendo kwa mtoto daima katika maisha yake. Ingawaje mtoto alimkimbia Baba yake, haikubadilisha ukweli kwamba yeye alitambua kuwa Baba yake alikuwa mtu mwema na kwamba anampenda. Pengine hakutambua ni kwa jinsi ghani, hadi alipo tambua mwenyewe. Ni wazi kwamba ni kwasababu ya utambuzi huu kutoka moyoni mwake unaompa ujasiri wa kurudi kwa Baba kwa matumaini ya upendo wa Baba yake.

Hili linafunua kuwa, upendo wa kweli unafanya kazi. Daima unafanya kazi. Hata kama mtu akikataa upendo mtakatifu tunaompa, lazima daima una ongeza kitu katika maisha yao. Upendo wa kweli usio na masharti ni vigumu kuukataa na kuutupilia mbali. Mwana mpotevu alitambua hili, na sisi pia tunapaswa kuwa hivyo. Huu ndio upendo alionao Baba yetu wa Mbinguni kwa kila mtu. Yeye sio Mungu mkali na mgumu. Ni Mungu anayependa kuturudisha kwake na kutupatanisha naye. Anafurahi tunapo mrudia na kuomba mahitaji yetu kwake. Ingawaje tuna wasi wasi, yeye hana wasi wasi kwa upendo wake, daima anatusubiri sisi, na sisi wenyewe kutoka ndani kabisa tunatambua hilo.

Kwaresima ni kipindi kizuri sana kwa sakramenti ya kitubio. Na sakramenti hiyo ndio ujumbe wote katika mfano huu. Ni mfano wa sisi kwenda kwa Baba yetu na dhambi zetu na atatupokea kwa huruma. Inaweza kuogopesha na kuwa na wasi wasi kwenda kwenye sakramenti ya kitubio, lakini tukiingia katika sakramenti hiyo kwa uaminifu na katika kweli, tunaona furaha tunayopata na Amani kuu. Tunajisikia Amani na kuacha mizigo iliyo tuelemea rohoni. Mungu, anatukimbilia, na kunyanyua mizigo yetu na kuitupa nyuma yetu. Usikubali kipindi hichi cha kwaresima kipite bila kuungama! Hakuna na tena, wala hakuna sehemu nyingine waweza kupata furaha hii ya kuunganika na Mungu katika kweli. Usijioneee huruma kwa kujibembeleza kwamba nitamweleza tu Mungu mwenyewe nikiwa chumbani kwangu. Nenda kaungame katika hali ya uaminifu na kweli kadiri ya Imani yetu. Mungu anakusubiri. Usikubali kubaki katika gereza la dhambi. Fanya uamuzi kama Mwana mpotevu.

Sala: Baba, nilienda kinyume na wewe na kufuata njia zangu mwenyewe. Sasa ni muda wa kurudi kwako katika hali ya uwazi na uaminifu wa moyo. Ninaomba unipe ujasiri huo ili niweze kukumbatia sakaramenti ya kitubio. Yesu nakuamini wewe. Amina.

Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

MASOMO YA MISA, MACHI 7, 2026




MASOMO YA MISA, MACHI 7, 2026
JUMAMOSI, JUMA LA 2 LA KWARESIMA

SOMO 1
Mik. 7:14-15, 18-20

Walishe watu wako kwa fimbo yako, kundi la urithi wako, wakaao peke yao, mwituni katikati ya Karmeli; na walishe katika Bashani na Gileadi, kama siku za kale. Kama katika siku zile za kutoka kwako katika nchi ya Misri nitamwonyesha mambo ya ajabu.

Ni nani aliye Mungu kama wewe, mwenye kusamehe uovu, na kuliachilia kosa la watu wa urithi wake waliosalia? Hashiki hasira yake milele, kwa maana yeye hufurahia rehema. Atarejea na kutuhurumia; atayakanyaga maovu yetu; nawe utazitupa dhambi zao zote katika vilindi yva bahari. Wewe utamtimilizia Yakobo kweli yako, na Ibrahimu rehema zako, ulizowaapia baba zetu tangu siku za kale.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 103:1-4, 9-12 (K) 8

(K) Bwana amejaa huruma na neema.

Ee nafsi yangu umhimidi Bwana.
Naam, vyote vilivyo ndani yangu
Vilihimidi jina lake takatifu.
Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana,
Wala usizisahau fadhili zake zote. (K)

Akusamehe maovu yako yote,
Akuponya magonjwa yako yote,
Aukomboa uhai wako na kaburi,
Akutia taji ya fadhili na rehema. (K)

Yeye hatateta sikuzote,
Wala hatashika hasira yake milele.
Hakututenda sawa na hatia zetu,
Wala hakutulipa kwa kadiri ya maovu yetu. (K)

Maana mbingu zilivyoinuka juu ya nchi,
Kadiri ileile rehema zake ni kuu kwa wamchao.
Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi,
Ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi. (K)


SHANGILIO
Yn. 6:64, 69

Maneno yako, Ee Bwana, ni roho, tena ni uzima; Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.


INJILI
Lk. 15:1-3, 11-32

Watoza ushuru wote na wenye dhambi walikuwa wakimkaribia Yesu wamsikilize. Mafarisayo na waandishi wakanung’unika, wakisema, Mtu huyu huwakaribisha wenye dhambi, tena hula nao. Akawaambia mfano huu, akisema,

Mtu mmoja alikuwa na wana wawili; yule mdogo akamwambia babaye, Baba, nipe sehemu ya mali inayoniangukia. Akawagawia vitu vyake. Hata baada ya siku si nyingi, yule mdogo akakusanya vyote, akasafiri kwenda nchi ya mbali; akatapanya mali zake huko kwa maisha ya uasherati.

Alipokuwa amekwisha tumia vyote, njaa kuu iliingia nchi ile, yeye naye akaanza kuhitaji. Akaenda akashikamana na mwenyeji mmoja wa nchi ile; naye alimpeleka shambani kwake kulisha nguruwe. Akawa akitamani kujishibisha kwa maganda waliyokula nguruwe, wala hapana mtu aliyempa kitu. Alipozingatia moyoni mwake, alisema, Ni watumishi wangapi wa baba yangu wanaokula chakula na kusaza, na mimi hapa ninakufa kwa njaa. Nitaondoka, nitakwenda kwa baba yangu na kumwambia, Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako; sistahili kuitwa mwana wako tena; nifanye kama mmoja wa watumishi wako. Akaondoka, akaenda kwa babaye.

Alipokuwa angali mbali, baba yake alimwona, akamwonea huruma, akaenda mbio akamwangukia shingoni, akambusu sana. Yule mwana akamwambia, Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako; sistahili kuitwa mwana wako tena. Lakini baba aliwaambia watumwa wake, Lileteni upesi vazi lililo bora, mkamvike; mtieni na pete kidoleni, na viatu miguuni; mleteeni ndama yule aliyenona mkamchinje nje; nasi tule na kufurahi; kw akuwa huyu mwanangu alikuwa amekufa, naye amefufuka; alikuwa amepotea, naye ameonekana. Wakaanza kushangilia.

Basi, yule mwanawe mkubwa alikuwako shamba na lipokuwa akija na kuikaribia nyumba, alisikia sauti ya nyimbo na machezo. Akaita mtumishi mmoja, akamwuliza, Mambo haya, maana yake nini? Akamwambia, Ndugu yako amekuja, na baba yako amemchinja ndama aliyenona, kwa sababu amempata tena, yu mzima. Akakasirika, akakataa kuingia ndani. Basi babaye alitoka nje, akamsihi. Akamjibu baba yake, akasema. Tazama, mimi nimekutumikia miaka mingapi hii, wala sijakosa amri yako wakati wowote, lakini hujanipa mimi mwana-mbuzi, nifanye furaha na rafiki zangu; lakini, alipokuja huyu mwana wako aliyekula vitu vyako pamoja na makahaba, umemchinjia yeye ndama aliyenona.

Akamwambia, Mwanangu, wewe u pamoja nami siku zote, na vyote nilivyo navyo ni vyako. Tena, kufanya furaha na shangwe ilipasa, kwa kuw ahuyu ndugu yako alikuwa amekufa, naye amefufuka; alikuwa amepotea, naye ameonekana.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

UPENDO UNAOTESEKA



“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Ijumaa, Machi 6, 2026
Juma la 2 la Kwaresima

Mwa 37:3-4, 12-13, 17-28;
Zab 105:16-21;
Mt 21:33-43, 45-46


UPENDO UNAOTESEKA


Katika njia nyingi, Yusufu alikuwa mwaminifu, alikuwa akilindwa katika upendo na kutendewa vyema na Baba yake. Lakini kutokuwa na hatia kulimweka mashakani mara pale alipowaambia ndugu zake kuhusu ndoto yake, na alipowaonyesha kanzu nzuri Baba yake aliyokuwa amempa. Baadaye, ingawa ndugu zake walimpiga na kumuuza utumwani, Yusufu hakuacha kuziishi amri za Mungu. Hata alipokuwa ameshtakiwa kwa uongo na kufungwa gerezani kwamba alijaribu kumwingilia mke wa bwana wake kwa nguvu, yeye aliendelea kuwa imara mbele ya Mungu. Wakati akiwa gerezani, uwezo wake wa kutafsiri ndoto ulimfikia Farao ambaye hatimaye alimweka huru na kumweka awe mkuu baada yake. Kama Yusufu alivyoamini kwamba, Mungu atamletea mema, Mungu alifanya hivyo kwa ajili yake na kuutenga uovu. Nasi pia, tusikubali kamwe kumuacha Mungu tunapokabiliana na magumu siku zote katika maisha yetu. Tumgeukia Mungu Baba yetu na kumwomba atupiganie.

Katika hali zote za kuchukiwa na kukataliwa kwa karne zote, kuna mmoja tu aliyesimama imara kuliko wengine wote. Kukataliwa kwa Mwana wa Mungu. Yesu hakuwa na kitu kingine isipokuwa upendo kamili moyoni mwake. Alipenda ubora wa kila aliyekutana naye. Na alikuwa tayari kumpa upendo yeyote aliyekuwa tayari kuupokea. Ingawaje wengi waliupokea lakini pia wengi waliukataa. Ni vizuri kutambua kuwa kukataliwa kwa Yesu kuliacha maumivu ya ndani na mateso. Ni wazi kwamba mateso ya Msalabani ndio yaliokuwa ya hali ya juu kabisa. Lakini kidonda alichohisi moyoni mwake kwa kukataliwa kilisababisha mateso makubwa. Kuteseka namna hii ilikuwa ni kitendo cha upendo, sio kitendo cha udhaifu. Yesu hakuteseka ndani kwasababu ya majivuno au kwasababu ya ubinafsi wake. Bali moyo wake uliumia kwasababu alipenda kutoka ndani. Na pale upendo huo ulipo kataliwa, ulimjaza yeye huzuni kuu (Mt 5:4).

Jaribu kufikiria kama Yesu ange amua kukata tamaa. Jaribu kufikiria, kama kipindi cha kukamatwa kwake Yesu angeita malaika kama jeshi kutoka mbinguni kumwokoa. Ingekuwaje kama angefanya kitendo hichi cha kufikirika “watu hawa hawastahili!”. Matokeo yake yangekuwa tusinge pokea zawadi ya ukombozi wa milele kwa njia ya mateso, kifo na ufufuko. Mateso yasinge badilika kwenda kwenye upendo.

Yesu alijibu kwa mapendo kamili pale alipolia kwa sauti kuu “Baba, wasamehe, hawajui watendalo.” Kitendo hiki cha upendo katikati ya mateso yake na kukataliwa kwake kilimfanya awe “jiwe kuu la msingi” la Kanisa, na hivyo kuwa jiwe kuu la maisha mapya! Tunaitwa kuiga mapendo haya na kushiriki sio tu kwakusamehe, bali pia kutoa mapendo matakatifu ya huruma. Tukifanya hivyo, sisi pia tunakuwa jiwe la msingi la upendo na neema kwa wote wanao hitaji zaidi.

Sala: Bwana, nisaidie mimi niweze kuwa jiwe la pembeni. Nisaidie mimi sio nisamehe tu kila mara ninapokosewa bali pia nitoe upendo na huruma kwao. Wewe ni Mungu na mfano kamili wa upendo huu. Ninaomba nishiriki katika upendo huu, nikilia kwa sauti kuu pamoja nawe “Baba wasamehe, hawajui watendalo”. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MACHI 6, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 6, 2026
IJUMAA, JUMA LA 2 LA KWARESIMA


SOMO 1
Mwa. 37:3-4, 12-13, 17-28

Israeli akampenda Yusufu kuliko wanawe wote, maana ni mwana wa uzee wake, akamfanyia kanzu ndefu. Ndugu zake wakaona ya kuwa baba yao anampenda kuliko ndugu zake wote, wakamchukia, na hawakuweza kusema naye kwa amani.

Ndugu zake wakaenda kuchunga kondoo za baba yao huko Shekemu. Israeli akamwambia Yusufu, Je! Ndugu zako hawachungi kondoo katika Shekemu? Njoo, nikutume kwao.

Basi Yusufu akawafuata ndugu zake akawakuta huko Dothani. Wakamwona toka mbali, na kabla hajawakaribia, wakafanya shuri juu yake ili wamwue. Wakasemezana wao kwa wao, Tazama, yule bwana wa ndoto anakuja. Haya, twende, tukamwue na kumtupa katika birika mojawapo, nasi tutasema, Mnyama mkali amemla; kisha tutaona zitakuwaje ndoto zake. Reubeni akasikia akamwokoa katika mikono yao, akasema, Tusimwue. Reubeni akawaambia, Msimwage damu; mtupeni katika birika iliyopo nyikani, wala msimguse; ili apate kumwokoa katika mikono yao, akamrudishe kwa baba yake. Ikawa Yusufu alipofika kwa ndugu zake, wakamvua Yusufu kanzu yake, kanzu ile ndefu aliyoivaa, wakamtwaa wakamtupa katika birika; na hiyo birika ilikuwa tupu, hamna maji. Nao wakakaa kitako kula chakula.

Wakainua macho yao, wakaona, msafara wa Waishmaeli wanakuja wakitoka Gileadi na ngamia zao, wakichukua ubani na zeri na manemane, wakisafiri kuvichukua mpaka Misri. Yuda akawaambia ndugu zake, Kwafaa nini kumwua ndugu yetu, na kuificha damu yake? haya, na tumwuze kwa hawa Waishmaeli, wala mikono yenu isimdhuru, maana yeye ni ndugu yetu, na damu yetu. Ndugu zake wakakubali.

Wakapita wafanyabiashara Wamidiani; basi wakamtoa Yusufu, wakampandisha kumtoa katika birika wakamwuza Yusufu kwa Waishmaeli kwa vipande vya fedha ishirini; nao wakamchukua Yusufu mpaka Misri.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 105:16-21 (K) 5

(K) Zikumbukeni ajabu zake Bwana alizozifanya.

Akaiita njaa iijilie nchi,
Akakiharibu chakula chote walichokitegemea.
Alimpeleka mtu mbele yao,
Yusufu utumwani. (K)

Walimwumiza miguu yake kwa pingu,
Akatiwa katika minyororo ya chuma.
Hata wakati wa kuwadia neno lake,
Ahadi ya Bwana ilimjaribu. (K)

Mfalme alituma watu akamfungua,
Mkuu wa watu akamwachia.
Akamweka kuwa bwana wa nyumba yake,
Na mwenye amri juu ya mali zake zote. (K)



SHANGILIO
Yn. 3:16

Jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe wa pekee; Kila mtu amwaminiye huwa na uzima wa milele.



INJILI
Mt. 21:33-43; 45-46

Yesu aliwaambia wakuu wa makuhani na wazee wa watu, Sikilizeni mfano mwingine. Kulikuwa na mtu mwenye nyumba, naye alipanda shamba la mizabibu, akalizungusha ugo, akachimba shimo la shinikizo ndani yake, akajenga mnara, akapangisha wakulima, akasafiri. Wakati wa matunda ulipokuwa karibu, akawatuma watumwa wake kwa wale wakulima, wapokee matunda yake. Wale wakulima wakawakamata watumwa wake, huyu wakampiga, na huyu wakamwua, na huyu wakampiga kwa mawe. Akawatuma tena watumwa wengine wengi kuliko wa kwanza, wakawatenda vile vile.
Mwishowe akamtuma mwanawe kwao, akisema, Watamstahi mwanangu. Lakini wale wakulima walipomwona yule mwana, wakasemezana wao kwa wao, Huyu ni mrithi; haya na tumwue, tuutwae urithi wake. Wakamkamata, wakamtupa nje ya shamba la mizabibu, wakamwua. Basi atakapokuja yule bwana wa shamba la mizabibu, atawatendaje wale wakulima? Wakamwambia, Ataangamiza vibaya wale wabaya; na shamba la mizabibu atawapangisha wakulima wengine, watakaomlipa matunda kwa wakati wake.

Yesu akawaambia, Hamkupata kusoma katika maandiko, Jiwe walilolikataa waashi, hilo limekuwa jiwe kuu la pembeni; neno hili limetoka kwa Bwana, nalo ni ajabu machoni petu? Kwa sababu hiyo nawaambia, Ufalme wa Mungu utaondolewa kwenu, nao watapewa taifa, linguine lenye kuzaa matunda yake.

Wakuu wa makuhani na Mafarisayo, waliposikia mifano yake, walitambua ya kuwa anawanenea wao. Nao walipotafuta kumkamata waliogopa makutano, kwa maana wao walimwona kuwa nabii.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

UPENDO WA MUNGU KWA MASKINI



“KWARESIMA YA UKARIMU”
Tafakari ya Kwaresima
Alhamisi, 5 Machi 2026
Juma la 2 la Kwaresima

Yer 17:5-10;
Zab 1:1-4, 6;
Lk 16:19-31


UPENDO WA MUNGU KWA MASKINI


Katika mfano wa Injili ya Leo tuna mtu mmoja ambaye ametajwa kwa jina, Lazaro. Mfano wa tajiri na Lazaro ni mfano ambao unabaki kuwa maarufu. Ni Lazaro tu anayetambulika katika hali hii? Kwanini Lazaro? Inawezekana ni kwasababu ya nafasi walio nayo maskini machoni pa Mungu. Mfano huu unatuonyesha ni kwa jinsi ghani Mungu anavyo chukizwa na ukosefu wa haki wa kuwafanya wana wake kuwa waombaji na kuwafanya kula makombo yanayotoka katika viti vya jirani zao walio na Mafanikio. Yesu anatuita kutoka moyoni mwake kwa ajili ya maskini. Anatuita tumuone kila mmoja hata wale maskini kabisa na walio katika hali ya mwisho kabisa, na kuwahudumia katika hali ya utu na heshima wanayostahili kama wanadamu wenzetu na watoto wa Mungu.

Kama ilikuwa ni kuchagua ungechagua nini? Kuwa tajiri na kuponda maisha kila siku, ukivaa mavazi ya kitani, kuwa na kila kitu unachopenda ulimwenguni? Au kuwa maskini uliye mwombaji, uliyefunika vidonda vyako, kuishi katika njia ya milango, ukihisi njaa?. Ni swali rahisi sana kujibu katika hali ya kawaida. Maisha ya utajiri na mafanikio yanavutia katika hali ya kwanza kabisa. Lakini swala ni kwamba hayapaswa kuchukuliwa katika hali ya kawaida, tunapaswa kuzama ndani kabisa na kulinganisha watu hawa wawili na matokeo ya maisha yao ya ndani ya roho yao ya milele.

Kwa maskini alivyokufa, “alichukuliwa na malaika katika kifua cha Abraham”. Na kwa tajiri, maandiko yanasema kwamba “alikufa na kuzikwa” na kwenda kwenye “ulimwengu mwingine ambapo alikuwa akiteseka” Sasa ni yupi unayependa kuchagua? Lengo la mfano huu ni rahisi kabisa, tukiwa hapa duniani tunapaswa kutubu, kuacha dhambi, kusikiliza Maandiko Matakatifu, kuamini na kuweka mioyo yetu kuelekea lengo letu la utajiri wa mbinguni.

Tajiri huyu angeweza kumuona Lazaro na kujali utu wake na thamani yake, yeye aliyekuwa amelala katika mlango wake, na kumuona kwa mapendo na huruma. Lakini hakufanya hivyo. Alikuwa amejikita sana juu ya nafsi yake. Dhambi zilimfunika macho akashindwa kumuona Lazaro. Tutafakari leo, kama unaona dhambi yeyote ndani yako inayo fanana na huyu tajiri katika maisha yako, ungama dhambi leo na kuziacha. Na kama umezoea kujikita katika ubinafsi, ukijiingiza katika anaasa za hali ya juu, kumbatia umaskini wa roho, na kujitahidi kuunganika na Mungu tu na baraka nyingi zinazokuja kwetu kwa kukumbatia yote yale aliyo yafunua kwetu.

Sala: Bwana, niweke huru kutoka katika hali isio faa. Nisaidie mimi niweze kubaki katika heshima ya kuwaheshimu watu wote, na kujitoa mwenyewe kuwahudumia. Yesu, nakuamini wewe. Amina.


Copyright ©2013-2026 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

MASOMO YA MISA, MACHI 5, 2026



MASOMO YA MISA, MACHI 5, 2026
ALHAMISI JUMA LA 2 LA KWARESIMA

SOMO 1
Yer. 17:5-10

Bwana asema hivi: Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu, amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake, na moyoni mwake amemwacha Bwana. Maana atakuwa kama fukara nyikani, hataona yatakapotokea mema; bali atakaa jangwani palipo na ukame, katika nchi ya chumvi isiyokaliwa na watu.

Amebarikiwa mtu yule anayemtegemea Bwana, ambaye Bwana ni tumaini lake. Maana atakuwa kama mti uliopandwa kando ya maji, uenezao mizizi yake karibu na mto; hautaona hofu wakati wa hari ujapo, bali jani lake litakuwa bichi; wala hautahangaika mwaka wa uchache wa mvua, wala hautaacha kuzaa matunda.

Moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha; nani awezaye kuujua? Mimi, Bwana, nauchunguza moyo, navijaribu viuno, hata kumpa kila mtu kiasi cha njia zake, kiasi cha matunda ya matendo yake.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.



WIMBO WA KATIKATI
Zab. 1:1-4, 6 (K) 40:4

(K) Heri aliyemfanya Bwana kuwa tumaini lake.

Heri mtu yule asiyekwenda
Katika shauri la wasio haki;
Wala hakusimama katika njia ya wakosaji;
Wala hakuketi barazani pa wenye mizaha.
Bali sheria ya Bwana ndiyo impendezayo,
Na sheria yake huitafakari mchana na usiku. (K)

Naye atakuwa kama mti uliopandwa
Kandokando ya vijito vya maji,
Uzaao matunda yake kwa majira yake,
Wala jani lake halinyauki;
Na kila alitendalo litafanikiwa. (K)

Sivyo walivyo wasio haki;
Hao ni kama makapi yapeperushwayo na upepo.
Kw akuwa Bwana anaijua njia ya wenye haki,
Bali njia ya wasio haki itapotea. (K)



SHANGILIO

Nitaondoka, nitakwenda kwa baba yangu na kumwambia, Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako.



INJILI
Lk. 16:19-31

Yesu aliwaambia Mafarisayo: Palikuwa na mtu mmoja, tajiri, aliyevaa nguo za rangi ya zambarau na kitani safi, na kula sikuzote kwa anasa. Na maskini mmoja, jina lake Lazaro, huwekwa mlangoni pake, ana vidonda vingi, naye alikuwa akitamani kushibishwa kwa makombo yaliyoanguka katika meza ya yule tajiri; hata mbwa wakaja wakamramba vidonda vyake. Ikawa yule maskini alikufa, akachukuliwa na malaika mpaka kifuani kwa Ibrahimu. Yule tajiri naye akafa, akazikwa.

Basi, kule kuzimu aliyainua macho yake, alipokuwa katika mateso, akamwona Ibrahimu kwa mbali, na Lazaro kifuani mwake. Akalia, akasema, Ee baba Ibrahimu, nihurumie, umtume Lazaro achovye ncha ya kidole chake majini, auburudishe ulimi wangu; kwa sababu ninateswa katika moto huu. Ibrahimu akasema, Mwanangu, kumbuka ya kwamba wewe uliyapokea mambo mema yako katika maisha yako, na Lazaro vivyo alipata mabaya; na sasa yeye yupo hapa anafarijiwa, na wewe unaumizwa. Na zaidi ya hayo, kati yetu sisi na ninyi kumewekwa shimo kubwa, ili wale watakao kutoka huku kwenda kwenu wasiweze; wala watu wa kwenu wasivuke kuja kwetu.

Akasema, Basi, baba, nakuomba, umtume nyumbani kwa baba yangu, kwa kuwaninao ndugu watano, ili awashuhudie, wasije wao piawakafika mahali hapa pa mateso. Ibrahimu akasema, Wanao Musa na manabii; na wawasikilize wao. Akasema, La, baba Ibrahimu, lakini kama akiwaendea atokaye kwa wafu, watatubu. Akamwambia wasipowasikia Musa na manabii, hawatashawishwa hata mtu akifufuka katika wafu.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.



Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.