MASOMO YA MISA, APRILI 10, 2023
JUMATATU KATIKA OKTAVA YA PASKA
SOMO 1
Mdo. 2:14, 22 – 32
Petro alisimama pamoja na wale kumi na mmoja,
akapaza sauti yake, akawaambia, Enyi watu wa Uyahudi, na ninyi nyote mkaao
Yerusalemu, lijueni jambo hili, mkalisikilize maneno yangu.
Enyi waume wa Israeli, sikilizeni maneno haya;
Yesu wa Nazareti, mtu aliyedhihirishwa kwenu na Mungu kwa miujiza na ajabu na
ishara, ambazo Mungu alizifanya kwa mkono wake kati yenu, kama ninyi wenyewe
mnavyojua; mtu huyu alipotolewa kwa shauri la Mungu lililokusudiwa, na kwa
kujua kwake tangu zamani, ninyi mkamsulibisha kwa mikono ya watu wabaya,
mkamwua; ambaye Mungu alimfufua, akaufungua uchungu wa mauti, kwa sababu
haikuwezekana ashikwe nao. Maana Daudi ataja habari zake.
Nalimwona Bwana mbele yangu sikuzote, kwa kuwa
yuko upande wa mkono wangu wa kuume, nisitikisike. Kwa hiyo moyo wangu
ukapendezewa, ulimi wangu ukafurahi; tena mwili wangu nao utakaa katika
matumaini. Kwa maana hutaiacha roho yangu katika kuzimu; wala hutamtoa
Mtakatifu wako aone uharibifu. Umenijulisha njia za uzima; utanijaza furaha kwa
uso wako.
Waume, ndugu zangu, mniwie radhi, niseme kwa
ujasiri mbele yenu habari za baba yetu mkuu, Daudi, ya kuwa alifariki akazikwa,
na kaburi lake liko kwetu hata leo. Basi kwa kuwa ni nabii, akijua ya kuwa
alifariki akazikwa, na kaburi lake liko kwetu hata leo. Basi kwa kuwa ni nabii,
akijua ya kuwa Mungu amemwapia kwa kiapo, ya kwamba katika uzao wa viuno vyake
akamketisha mmoja katika kiti chake cha enzi; yeye mwenyewe akitangulia kuyaona
haya, alitaja habari za kufufuka kwake Kristo, ya kwamba roho yake haikuachwa
kuzimu, wala mwili wake haukuona uharibifu. Yesu huyo Mungu alimfufua, na sisi
sote tu mashahidi wake.
Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.
WIMBO WA KATIKATI
Zab. 16:1 – 2, 5, 7 – 11 (K) 1
(K) Mungu unihifadhi mimi, kwa maana
nakukimbilia wewe.
Mungu unihifadhi mimi,
Kwa maana nakukimbilia Wewe.
Nimemwambia Bwana, Ndiwe Bwana wangu;
Bwana ndiye fungu la posho langu, na la kikombe
changu;
Wewe unaishika kura yangu. (K)
Nitamhimidi Bwana aliyenipa shauri,
Naam, mtima wangu umenifundisha usiku.
Nimemweka Bwana mbele yangu daima,
Kwa kuwa yako kuumeni kwangu, sitaondoshwa. (K)
Kwa hiyo moyo wangu unafurahi,
Nao utukufu wangu unashangilia,
Naam, mwili wangu nao utakaa kwa kutumaini.
Maana hutaiachaia kuzimu nafsi yangu.
Wala hutamtoa mtakatifu wako aone uharibifu. (K)
Utanijulisha njia ya uzima;
Mbele za uso wako ziko furaha tele;
Na katika mkono wako wa kuume mna mema ya
milele. (K)
SHANGILIO
Zab. 118:24
Aleluya, aleluya,
Siku hii ndiyo aliyoifanya Bwana, tutaishangilia
na kuifurahia.
Aleluya.
INJILI
Mt. 28:8 – 15
Wanawake waliondoka upesi kutoka kaburini, kwa
hofu na furaha nyingi, wakaenda mbio kuwapasha wanafunzi wake habari.
Na tazama, Yesu akakutana nao, akisema, Salamu!
Wakakaribia wakamshika miguu, wakamsujudia. Kisha Yesu akawaambia, Msiogope;
enendeni, mkawaambie ndugu zangu waende Galilaya, ndiko watakakoniona.
Nao wale walipokuwa wakienda, tazama, baadhi ya
askari waliingia mjini, wakawapasha wakuu wa makuhani habari za mambo yote
yaliyotendeka. Wakakusanyika pamoja na wazee, wakafanya shauri, wakawapa askari
fedha nyingi, wakisema, Semeni, ya kwamba wanafunzi wake walikuja usiku,
wakamwiba, sisi tulipokuwa tumelala. Na neno hili likisikilikana kwa liwali,
sisi tutasema naye, nanyi tutawaondolea wasiwasi. Basi wakazitwaa zile fedha,
wakafanya kama walivyofundishwa. Na neno hilo likaenea kati ya Wayahudi hata
leo.
Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.
Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA
MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright ©
1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of
Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha
ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.
No comments:
Post a Comment