MASOMO YA MISA, FEBRUARI 21, 2024
JUMATANO, JUMA
LA 1 LA KWARESIMA
SOMO 1
Yon. 3:1-10
Neno la Bwana likamjia Yona mara ya pili,
kusema, Ondoka, uende Ninawi, mji ule mkubwa, ukaihubiri habari
nitakayokuamuru.
Basi Yona akaondoka, akaenda Ninawi, kama Bwana
alivyonena. Basi Ninawi ulikiuwa mji mkubwa mno, ukubwa wake mwendo wa siku
tatu, Yona akaanza kuuingia mji mwendo wa siku moja, akapaza sauti yake,
akasema, Baada ya siku arobaini Ninawi utaangamizwa.
Basi watu wa Ninawi wakamsadiki Mungu;
wakatangaza kufunga, wakajivika nguo za magunia, tangu yeye aliye mkubwa hata
aliye mdogo. Habari ikamfikia mfalme wa Ninawi, naye akaondoka katika kiti
chake cha enzi, akavua vazi lake, akajivika nguo za magunia, na kuketi katika
majivu. Naye akapiga mbiu, akatangaza habari katika mji wa Ninawi, kwa amri ya
mfalme na wakuu wake; kusema. Mwanadamu asionje kitu, wala mnyama wala makundi
ya ng’ombe, wala makundi ya kondoo; wasile, wala wasinywe maji; bali na
wafunikwe nguo za magunia, mwanadamu na mnyama pia, nao wakamlilie Mungu kwa
nguvu, naam, na wageuke, kila mtu akaache njia yake mbaya, na udhalimu ulio
mikononi mwake. Ni nani ajuaye kwamba Mungu hatageuka na kughairi, na kuiacha
hasira yake kali, ili tusiangamizwe?
Mungu akaona matendo yao, ya kuwa wameiacha njia
yao mbaya. Basi Mungu akalighairi neno lile baya, ambalo alisema atawatenda;
asilitende.
Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.
WIMBO WA KATIKATI
Zab. 51:1-2, 10-11, 16-17 (K) 17
(K) Moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu,
hutaudharau.
Ee Mungu, unirehemu,
Sawa na fadhili wako.
Kiasi cha wingi wa rehema zako,
Uyafute makosa yangu. (K)
Ee Mungu, uniumbie moyo safi,
Uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu.
Usinitenge na uso wako,
Wala roho yako mtakatifu usiniondolee. (K)
Maana hupendezwi na dhabihu, au ningeitoa,
Wewe huridhii sadaka ya kuteketezwa.
Dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika,
Moyo uliyovunjika na kupondeka. (K)
SHANGILIO
Eze. 18:31
Tupilieni mbali nanyi makosa yenu yote
mliyoyakosea, Asema Bwana. Jifanyeni moyo mpya na roho mpya.
INJILI
Lk. 11:29-32
Makutano walipokuwa wakimkusanyikia, Yesu
alianza kusema, Kizazi hiki ni kizazi kibaya; kinatafuta ishara, wala
hakitapewa ishara, ila ishara ya Yona. Maana, kama vile Yona alivyokuwa ishara
kwa Waninawi, ndivyo atakavyokuwa Mwana wa Adamu kwa kizazi hiki. Malkia wa
Kusini ataondoka siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu
kuwa na hatia; kwa sababu yeye alikuja kutoka nchi za dunia aisikie hekima ya
Sulemani; na hapa pana mkubwa kuliko Sulemani. Watu wa Ninawi watasimama siku
ya hukumu pamoja na kizazi hiki, nao watakihukumu kuwa na hatia; kwa sababu wao
walitubu kwa mahubiri ya Yona, na hapa pana mkubwa kuliko Yona.
Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.
Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA
MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright ©
1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of
Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha
ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.
🙏🙏
ReplyDelete