“ASALI
ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari
ya kila siku
Jumanne,
Oktoba 5, 2021,
Juma
la 27 la Mwaka
Yon
3: 1-10
Zab
130: 1-4, 7-8 (K) 3;
Lk
10: 38-42.
UWE
IMARA NA TAMBUA MIMI NI MUNGU!
Karibuni ndugu zangu katika adhimisho la
Ekaristi takatifu asubuhi ya leo. Neno la Bwana katika asubuhi ya leo tunaaanza
kwa kuliangalia somo la kwanza toka katika kitabu cha Nabii Yona. Hapa
tunamkuta Yona akihubiri toba kwa watu wa Ninawi na watu wa ninawi wanaipokea
kwa moyo mmoja na mara moja toba inaanza na Mungu anawasamehe.
Sehemu hii ya Biblia ni miongoni mwa
maeneo machache ambapo nabii ameongea na kusikilizwa mara moja. Mara nyingi
nabii alipoongea-walimuona kama kichaa, kachanganyikiwa vile-hivyo
hawakumsikiliza hata kidogo-sehemu nyingine walichapwa viboko au kufungwa
gerezani au kupigwa na mawe. Lakini hapa ni ajabu kabisa. Watu wameitikia wito
mara moja.
Tujiulize ni kwa nini? Ni kwa sababu
watu wa Ninawi hawakuwa watu wa taifa moja na Yona. Hawakuwa Wayahudi-nabii
hakubaliki katika nyumba yake-watu hawa waliuchukulia ujumbe huu kwa makini
sana na Mungu anapenda watu wa namna hii na ndiyo maana anawaondolea adhabu
yao.
Katika injili, Yesu anaonesha tena
dhahiri kwamba Yesu anawapenda watu wanaouchukulia ujumbe wa Mungu kwa
makini-hawa ni akina Maria-unakaa mguuni mwa Yesu-unauelewa kwanza ule ujumbe
halafu ndio ukautoe kwa watu ukiwa na uelewa tosha. Tofauti na Martha-yeye
alikuwa anapilikapilika tu muda wote-sasa angepata muda upi wa kuuelewa ujumbe
wa Mungu. Na kama hajaulewa atapeleka nini kwa watu, atatumikiaje watu?
Hivyo sote kama Maria lazima tukae kwa
Yesu atufunze kwanza halafu ndio tuende tukahudumie watu. Huwezi kuhudumia bila
kuwa na uelewa wa kile unachohudumu.
Somo hili linawagusa sana hasa watu
wanafunzi, au watu wote wanaojidai kuwa bize masaa 24 bila kuwa na muda wa
kukaa kwa Yesu. Mwisho wa siku wanashindwa kuelewa maana ya kile
wanachofanya-wanakata tamaa kwa haraka kwa sababu hukumshirikisha Mungu.
Utaamka asubuhi kwenda kusoma lakini kama hujakaa miguuni pa Yesu-nakwambia
unajihangaisha tu.
Kaa miguuni pa Yesu kama Maria.
Utakaanga chips na vitumbua kila siku lakini utasema kuna shetani ananiibia
fedha, utauza duka lakini ukipiga faida huoni-mwishoni utasema kuna shetani
linaniibia fedha. Au kama ni mwanafunzi utasema kuna mtu ananiibia hizi akili
zangu au kuna mtu anatuma jini lake na kuja kufyonza akili zangu na kuzimpatia
yeye ninapokuwa nimelala. Kumbe sababu ni kwamba hukai miguuni kwa Yesu na
kusikiliza neno lake. Tusiwe wachoyo wa kutafuta muda wa kukaa na Yesu.
Copyright ©2013-2021 ©FurKat,
Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.
No comments:
Post a Comment