Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

mwombezi wa wanadamu kwa Kristo,

 

ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Tafakari ya kila siku

Jumatatu, Oktoba4, 2021,

Juma la 27 la Mwaka

 

Yon 1: 1,2:1-10

Lk 10: 25-37.

 

Karibuni ndugu zangu kwa adhimisho la Ekaristi asubuhi ya leo. Leo ni kumbukumbu ya Maria Mama wa Rozari. Neno la Bwana tunaanza kwa kuliangalia somo la kwanza linatoka katika kitabu cha Matendo ya Mitume. Hapa tunakumbana na habari ya Mama Maria akiwa amejiunga pamoja na kundi la mitume akisali-wakiwa katika maombi makubwa.

 

Walikuwa katika maombi makubwa kwa sababu walikuwa hawako na Bwana Yesu. Bwana Harusi alikuwa amekwisha ondolewa. Hivyo walikuwa wanajitahidi kusali kwa nguvu sana ili Mungu asi awaache, ili shetani asije akawashinda kwa sababu Bwana harusi wa kuwatetea hayupo tena kati yao.

 

Tunapokuja katika injili ya leo, tunakumbana na somo machachari kabisa. Hapa tunakutana na simulizi la kupashwa habari Maria. Katika simulizi hili, Maria anatajwa kwamba amejaa neema, na Bwana yupo naye kila wakati, na yeye ni mbarikiwa kuliko wanawake wote na hata kile atakachokizaa kimebarikiwa. Hapa tunaona juu ya huu ukuu wa Maria.

 

Lakini unaporudi tena katika somo la kwanza, unaona kwamba licha ya huyu Mama kuwa na cheo kikubwa, zaidi kuliko hata mitume na wanawake wenzake-yeye bado ni mnyenyekevu, bado anabakia katika sala, yeye anawatia moyo wale wanawake na mitume waliokuwa katika kukata tamaa, yeye anakuwa kwao mfano wa utii, unyenyekevu na unyofu. Anaona cheo chake kama sehemu ya huduma na si kujipatia utukufu Zaidi. Anatumia cheo chake kuwavuta watu kwa Mungu zaidi.

 

Tabia ya namna hii ndugu zangu ndiyo iliyompatia Mama Maria hata cheo cha kuwa mwombzi, mwombezi wa wanadamu kwa Kristo, kwani ni Mama aliyeungana kikamilifu na wanadamu. Pia ameungana na Mungu sawa sawa.

 

Ndugu zangu, hapa tunayomengi ya kujifunza: kwanza kati yetu wapo waliobarikiwa na Mungu, wamejazwa neema mbalimbali na Mungu: wewe unazitumiaga je? Unawafanyaga watu wamjue Mungu zaidi, Mungu atukuke zaidi kupitia kwako au unatumiaga hizo neema za Mungu kujitangaza? Nakwambia kati yetu tumezidi kutumia neema za Mungu kugandamiza wenzetu, kuwaengezea shida, kufurahisha vionjo vyetu-unakuta wewe ni mwalimu chuoni unamwambia mwanafunzi usipotoa kitu, basi nitakufelisha! ndugu yangu!

 

Unakuta mtu umebarikiwa kuwa na kampuni yako lakini kila mwanadada atakayeomba kazi kwako lazima alale nawe-nakwambia huku ni kuchezea neema za Mungu ndugu yangu na anayefanya hivyo nakwambia tubu mapema kwa sababu mambo yatakuwia mabaya sana siku moja

Neema alizokujalia Mwenyezi Mungu zifanye ziwawezeshe wengine wamjue Mungu-yaani vipaji na uwezo uliojaliwa na Mungu vimtangaze Mungu na si kumtangaza shetani. Hivi vipaji ni vya Mungu na si vya shetani. usikubali shetani atukuke katika hivi vipaji.

 

Mama Maria alijiunga na mitume ili kuwapa moyo na pia kuwafundisha kusali. Sisi nasi kama watu tuliobarikiwa na Mungu na kujawa neema, tusiwakwaze wenzetu bali waongoze wote kwa Kristo. Ameni.

 

Copyright ©2013-2021 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

No comments:

Post a Comment