MASOMO YA MISA, OCTOBER 4, 2021
JUMATATU, JUMA LA 27 LA MWAKA
SOMO 1
Mdo. 1:12-14
Yesu alipokwisha kupanda mbinguni mitume
walirudi kwenda Yerusalemu kutoka mlima ulioitwa wa Mizeituni, ulio karibu na
Yerusalemu, wapata mwendo wa sabato. Hata walipoingia, wakapanda orofani,
walipokuwa wakikaa; Petro, na Yohane, na Yakobo, na, Andrea, Filipo na Tomaso, Bartholomayo
na Mathayo, Yakobo wa Alfayo, na Simoni Zelote, na Yuda wa Yakobo. Hawa wote
walikuwa wakidumu kwa moyo mmoja katika kusali, pamoja nao wanawake, na Mariamu
mama yake Yesu, na ndugu zake.
Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.
WIMBO WA KATIKATI
Lk. 1:46-55
(K) Mwenye nguvu amenitendea makuu, na
jina lake ni takatifu.
Moyo wangu wamwadhimisha Bwana,
Na roho yangu imemfurahia Mungu,
Mwokozi wangu. (K)
Kwa kuwa ameutazama
Unyonge wa mjakazi wake.
Kwa maana, tazama, tokea sasa
Vizazi vyote wataniita mbarikiwa;
Kwa kuwa Mwenye nguvu amenitendea makuu,
Na jina lake ni takatifu. (K)
Na rehema zake hudumu vizazi hata vizazi
Kwa hao wanaomcha.
Amefanya nguvu kwa mkono wake;
Amewatawanya walio na kiburi katika
mawazo ya mioyo yao; (K)
Amewaangusha wakuu katika viti vyao vya
enzi;
Na wanyonge amewakweza.
Wenye njaa amewashibisha mema,
Na wenye mali amewaondoa mikono mitupu.
(K)
SHANGILIO
Lk. 1:28
Aleluya, aleluya,
Salamu, uliyepewa neema, Bwana yu pamoja
nawe. Umebarikiwa katika wanawake.
Aleluya.
INJILI
Lk. 1:26-38
Mwezi wa sita, malaika Gabrieli alitumwa
na Mungu kwenda mpaka mji wa Galilaya, jina lake Nazareti, kwa mwanamwali
bikira aliyekuwa ameposwa na mtu, jina lake Yusufu, wa mbari ya Daudi; na jina
lake bikira huyo ni Mariamu. Akaingia nyumbani mwake akasema, Salamu, uliyepewa
neema. Bwana yu pamoja nawe.
Naye akafadhaika sana kwa ajili ya
maneno yake, akawaza moyoni, Salamu hii ni ya namna gani? Malaika akamwambia,
Usiogope, Mariamu kwa maana umepata neema kwa Mungu. Tazama, utachukua mimba na
kuzaa mtoto mwanamume; na jina lake utamwita Yesu. Huyo atakuwa mkuu ataitwa
Mwana wa Aliye juu, na Bwana Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake.
Ataimiliki nyumba ya Yakobo hata milele, na ufalme wake utakuwa hauna mwisho.
Mariamu akamwambia malaika, Litakuwaje
neno hili, maana sijui mume? Malaika akajibu akamwambia, Roho Mtakatifu
atakujilia juu yako na nguvu zake Aliye juu zitakufunika kama kivuli; kwa
sababu hiyo hicho kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu. Tena,
tazama, jamaa yako Elisabeti naye amechukua mimba ya mtoto mwanamume katika
uzee wake; na mwezi huu ni wa sita kwake yeye aliyeitwa tasa; kwa kuwa hakuna
neno lisilowezekana kwa Mungu.
Mariamu akasema, Tazama, mimi ni mjakazi
wa Bwana; na iwe kwangu kama ulivyosema. Kisha malaika akaondoka akaenda zake.
Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristu.
Copyright © 2020, "MASOMO YA
MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings
reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.
No comments:
Post a Comment