Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

UFUASI MAANA YAKE UTUME

 

“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Tafakari ya kila siku

Alhamisi, Septemba  30, 2021.

Juma la 26 la Mwaka

 

Neh 8: 1-12;

Zab 18:8-11;

Lk 10: 1-12

 

UFUASI MAANA YAKE UTUME

Karibuni sana wapendwa wa Mungu kwa adhimisho la misa takatifu asubuhi ya leo. Neno la Bwana katika somo la kwanza Ezra anaisoma sheria ya Bwana, kitabu kitakatifu machoni pa wana wa Yuda waliorudi utumwani. Walipokuwa utumwani, walikosa Torati takatifu ya Musa. Hawakuwa na mtu wa kuwasomea, walisikiliza tu habari za miungu ya kipagani, na miziki ya kipagani, na hivyo mioyo yao ilikuwa tupu sana. Mioyo yao ilitamani ilishwe na neno la Mungu, na kupewa matumaini. Na leo wanaonesha kwamba yapo matumaini makubwa, ipo lishe kubwa katika neno la Mungu, yaani Biblia.

Hivyo wanapopatiwa lishe hii siku ya leo, wanafurahi na kuburudika.

 

Sisi tujifunze kulisoma neno la Mungu, hakika litatupatia maarifa, litatuonya na kutupatia maarifa. Wengi wetu tunakosa maarifa mengi kwa sababu hatusomi maandiko matakatifu. Kila tukijisikia kukosa matumaini, tujisikia hofu na ukosefu wa tumaini ni vyema kuyakimbilia maandiko matakatifu. Hakika tutapata maarifa na matumaini.

 

Hakika wengi kati yetu hatuna maarifa, tunayumbishwa na ushirikina, tamaa za kimwili, kwa sababu hatuyajui vyema maandiko matakatifu. Pia turuhusu neno la Mungu lituchome na kutuumbua. Ni kwa sababu neno la Mungu limebeba roho yenye uwezo wa kutugeuza, na kutufanya tuwe huru zaidi. Tusiache kusoma maandiko matakatifu.

 

Katika somo la injili, Bwana Yesu anawatuma wafuasi wake wakahubiri injili. Anafanya hivi kwani dunia inahitaji iletewe ukombozi na injili. Bila injili, dunia itatetereka tu. Injili ndiyo itakayoleta amani duniani, kuheshimiana, kupendana, na kufurahiana. Sisi tukubali tuwe wafuasi wa kuitangaza injili. Tukubali kutumwa.

 

Mara nyingi tunamkweza na kumtangaza shetani kuliko injili. Shetani anaonekana kuwa na nguvu zaidi kuliko injili yenyewe. Tuipende injili na hakika tutajiletea ukombozi zaidi ndani ya maisha yetu na kuishi kwa ubora zaidi. Tuipende injili kwa siku zote. Tusiiache pembeni injili ya Bwana.

 

------------------------

Copyright ©2013-2020 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

No comments:

Post a Comment