Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

ROHO MTAKATIFU ANAFUMBUA MAFUMBO YA IMANI!

 

“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Tafakari ya kila siku

Jumamosi, Septemba 25, 2021.

Juma la 25 la Mwaka

 

 

Zek 2: 5-9, 14-15;

Yer 31: 10-12, 13;

Lk 9: 43-45

 

 

ROHO MTAKATIFU ANAFUMBUA MAFUMBO YA IMANI!

 

Ndugu zangu wapendwa, karibuni kwa adhimisho la misa takatifu asubuhi ya leo. Neno la Bwana katika somo la kwanza Nabii Zekaria anaelezea juu ya utukufu utakaolipata taifa la Israeli. Anatangaza kuja na kukaa kati yao na mataifa mengi yataujia mji wa Yerusalemu na kuupatia utukufu. Na Bwana atakuwa mlinzi na ukuta wa moto kwa taifa hili. Hivyo Yerusalemu haitalindwa na ukuta wa mwanadamu bali na ulinzi wa malaika wa Mungu.

 

Maneno haya yawe kwetu maneno ya kutuhamasisha juu ya kuutumainia ulinzi wa Bwana. Baadhi yetu tunalindwa na mbwa wakali, au silaha kali, au kampuni thabiti za ulinzi na kukaa katika majengo yaliyowekewa uzio mkali wa umeme. Lakini tusipokuwa makini katika kumtumainia Bwana, katika kumkaribisha Bwana alinde kila tulichonacho, hakika hatuwezi kuwa salama. Tunakuwa salama kwa pale tu Bwana anapokuja na kufanya makao katika miji na nyumba zetu. Kwani waweza kuwa hata na ulinzi wa ukuta mkali lakini adui akaishia kutuvamia tu. Magonjwa mbalimbali yanawasumbua hata walio katika ulinzi mkali. Haya hayawezi kukomeshwa kwa silaha tulizo nazo au pesa zetu.

 

Tunahitaji ulinzi wa Mungu. Shetani huzungukazunguka kama simba angurumaye akitafuta mawindo. Hivyo yafaa tuwe imara. Tujifunze kumkaribisha Mwenyezi Mungu ili achukue madaraka na ulinzi wa maisha yetu. Nguvu za mwanadamu hazitoshi.

 

Katika somo la injili, Yesu anawaeleza wanafunzi wake ukweli wa mambo yatakayotukia maishani mwake kwamba atateswa na kufa na siku ya tatu atafufuka. Lakini neno hili linakuwa vigumu kupokelewa na wanafunzi wa Yesu. Na pia wanaogopa hata kumuuliza. Haya yalitokea kwa sababu Yesu aliongea kuhusu ukweli wa maisha yake jinsi ulivyo, uhalisia wa mambo yatakavyokuwa kwamba itambidi kuteswa. Lakini inakuwa vigumu kwa uhalisia huu kupokelewa. Na ikiwa Yesu angeukataa uhalisia huu, kwa hakika angalishindwa kutekeleza wajibu wake, na hata kutimiza lengo liliomleta.

 

Sisi tuwe watu wenye kukubali, wenye kukubali uhalisia wa maisha yetu. Tuzikubali hali zetu, kama tunataka kweli kuwa wafuasi wa Bwana. Tusinganganie kile wanachotaka wenzetu bali tutimize kile kinachotakiwa na uhalisia wa maisha yetu. Tuishi sisi kama sisi, tuishi utume na majukumu ya Bwana.

------------------------

Copyright ©2013-2020 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

No comments:

Post a Comment