Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MASOMO YA MISA, SPTEMBA 28, 2021

 

MASOMO YA MISA, SPTEMBA 28, 2021

JUMANNE, JUMA LA 26 LA MWAKA

 

SOMO 1

Zek. 8:20-23

 

Bwana wa majeshi asema hivi, Itatokea halafu ya kwamba watakuja mataifa na wenyeji wa miji mingi; wenyeji wa mji huu watauendea mji huu, wakisema, Haya! Twendeni zetu kwa haraka tuombe fadhili za Bwana, na kumtafuta Bwana wa majeshi; Mimi nami nitakwenda. Naam, watu wa kabila nyingi na mataifa hodari watakuja Yerusalemu kumtafuta Bwana wa majeshi, na kuomba fadhili za Bwana.

Bwana wa majeshi asema hivi, Siku hizo watu kumi, wa lugha zote za mataifa, wataushika upindo wa nguo yake yeye aliye Myahudi; naam, wataushika wakisema, Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi.

 

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

 

WIMBO WA KATIKATI

Zab. 87 (K) Zek. 8:23

 

(K) Mungu yu pamoja nasi.

 

Msingi wake upo

Juu ya milima mitakatifu.

Bwana ayapenda malango ya Sayuni

Kuliko maskani zote za Yakobo.

Umetajwa kwa mambo matukufu,

Ee Mji wa Mungu. (K)

 

Nitataja Rahabu na Babeli

Miongoni mwao wanaonijua.

Tazama Filisti, na Tiro, na Kushi;

Huyu alizaliwa humo.

Naam, mintarafu Sayuni itasemwa,

Huyu na huyu alizaliwa humo. (K)

 

Na Yeye Aliye juu

Ataufanya imara.

Bwana atahesabu, awaandikapo mataifa,

Huyu alizaliwa humo.

Waimbao na wachezao na waseme,

Visiwa vyangu vyote vimo mwako. (K)

 

SHANGILIO

Zab. 119:105

 

Aleluya, Aleluya,

Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu.

Aleluya.

 

INJILI

Lk. 9:51 – 56

 

Ilikuwa, siku za kupaa kwake zilipokuwa karibu kutimia, Yesu aliukaza uso wake kwenda Yerusalemu; akatuma wajumbe kutangulia mbele ya uso wake; wakaenda wakaingia katika kijiji cha Wasamaria, ili kumtengenezea mahali. Lakini wenyeji hawakumkaribisha kwa vile alivyouelekeza uso wake kwenda Yerusalemu. Wanafunzi wake Yakobo na Yohane walipoona hayo, walisema, Bwana, wataka tuagize moto ushuke kutoka mbinguni, uwaangamize? Akawageukia akawakanya, wakaondoka wakaenda mpaka kijiji kingine.

 

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

 

-------------------------

Copyright © 2020, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

No comments:

Post a Comment