Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

Hakika Mungu anao uwezo mkuu sana.

 

“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Tafakari ya Kila siku

Jumatatu, Sptemba 27, 2021,

Juma la 26 la Mwaka

 

Zek 8: 1-8;

Zab 102:16-18.19-21.29 and 22-23 (R. 17)

Lk 9: 46-50

 

Hakika Mungu anao uwezo mkuu sana.

Karibuni sana wapendwa wa Bwana kwa adhimisho la misa takatifu asubuhi ya leo. Neno la Bwana katika somo la kwanza Nabii Zekaria anatoa unabii kwa taifa la Yuda lililorudi utumwani. Lilikuta nchi yao na mji wao wa Yerusalem ukiwa katika mahame na magofu. Wengi waliuawa na miili yao kutupwa hadharani. Mwenyezi Mungu anaeleza kwamba hali itabadilika, watu watazaliwa tena wapya na kuishi muda mrefu, miji itajengwa tena upya, matajiri watatokea tena, namna ambayo itazidi ile ya mwanzoni.

 

Huu ndio unabii anaoutoa Zekaria. Hakika Mwenyezi Mungu anao uwezo mkubwa; aweza kufanya mengi bila hata ya sisi kumsaidia. Aweza kuanzisha wanadamu wengine hata bila ya sisi. Hakika Mungu anao uwezo mkuu sana. Tujifunze kumrudia na kumtukuza Mwenyezi Mungu. Kila siku wanadamu wanazaliwa upya, tena wenye uwezo kuliko sisi. Wanaojidai kuwa na uwezo sasa watashangaa kuona kwamba watazaliwa wengine wenye uwezo kutushinda sisi. Hivyo tukiwa na afya zetu, tukiwa na muda wetu, na vipaji vyetu, tumtumikie Mungu. Tusijivune au kutumia kile tupewacho na Mungu kumtesa jirani yetu.

 

Wanadamu ni kama ua lichanualo, wakati huu tunaonekana kuwa wazuri, ipo siku tutazimika. Tuwezacho kujivunia ni kwa jinsi gani tulivyoweza kuishi karibu zaidi na Mwenyezi Mungu. Ni wema gani niliompa mtoto, jirani au rafiki yangu au aliye na shida. Tujifunze kutumia muda wetu, na afya yetu vyema.

 

Pia ujumbe huu utufae na sisi ambao tumewahi kupoteza mali, kuibiwa, au kufilisika. Tutambue kwamba Mwenyezi Mungu aweza kutujaza tena mema yake, mambo yakawa tena mazuri zaidi hata kuliko zamani. Tumwombe Mwenyezi Mungu apate kubadilisha hali yetu na kuwa mpya zaidi.

 

Katika somo la injili, Yesu anatueleza kwamba aliye mdogo miongoni mwetu sote, ndiye aliye mkubwa. Mdogo ndiye anayetumikia, mara nyingi, wafalme hawatumikii bali watumwa wao, walio na cheo cha chini na kipato cha chini. Yesu anadai hawa ndio walio wakubwa mbele yake. Anayetumikia hupokea fadhila, na rehema machoni pa Bwana. Kukubali kumtumikia mwenzako ni kuonesha uaminifu kwa mambo yaliyo madogo na Mwenyezi Mungu humkabidhi yeyote anayeonesha uaminifu kwa mambo madogo hukabidhiwa mambo makubwa.

 

Tunapoonesha uaminifu kwa kuwatumikia wenzetu, Mwenyezi Mungu atatukabidhi yaliyo makubwa zaidi. Sisi tusichoke kuonesha uaminifu kwa kuwahudumia wenzetu. Tumsifu Yesu Kristo.

 

------------------------

Copyright ©2013-2020 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

No comments:

Post a Comment