Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MASOMO YA MISA, AGOSTI 14, 2021

 

MASOMO YA MISA, AGOSTI 14, 2021

JUMAMOSI, JUMA LA 19 LA MWAKA

SOMO 1

Yos. 24:14-29

Yoshua aliwaambia makutano: Sasa mcheni Bwana, mkimtumikia kwa unyofu wa moyo na kwa kweli; na kuiweka mbali miungu ambayo baba zenu waliitumikia ng’ambo ya Mto, na huko Misri; mkamtumikie yeye Bwana. Nanyi kama mkiona ni vibaya kumtumikia Bwana, chagueni hivi leo mtakayemtumikia; kwamba ni miungu ile ambayo baba zenu waliitumikia ng’ambo ya Mto, au kwamba ni miungu ya wale Waamori ambao mnakaa katika nchi yao; lakini mimi na nyumba yangu tutamtumikia Bwana.

Hao watu wakajibu wakasema, Hasha! Tusimwache Bwana, ili kuitumikia miungu mingine; kwa maana Bwana, Mungu wetu, yeye ndiye aliyetupandisha sisi na baba zetu kutoka nchi ya Misri; kutoka nyumba ya utumwa; naye ndiye aliyezifanya ishara zile kubwa mbele ya macho yetu, na kutulinda katika njia ile yote tuliyoiendea, na kati ya watu wa mataifa yote tuliopita katikati yao. Bwana ndiye aliyewafukuza watu wa mataifa yote watoke mbele yetu, naam, Waamori waliokaa katika nchi hii; basi, kwa ksababu hiyo sisi nasi tutamtumikia Bwana; maana yeye ndiye Mungu wetu.

Yoshua akawaambia watu, Hamwezi kumtumikia Bwana; kwa kuwa yeye ni Mungu mtakatifu; yeye ni Mungu mwenye wivu; hatawasamehe makosa yenu, wala dhambi zenu. Kama mkimwacha Bwana na kuitumikia miungu migeni, ndipo atageuka na kuwatenda mabaya na kuwaangamiza, baada ya kuwatendea mema.

Lakini hao watu wakamwambia Yoshua, La! Lakini tutamtumikia bWana. Yoshua akawaambia watu, Ninyi mmekuwa mashahidi juu ya nafsi zenu, ya kuwa mmemchagua Bwana, ili kumtumikia yeye. Wakasema, Sisi tu mashahidi. Akasema, Basi sasa, iondoeni miungu migeni iliyo kati yenu, mkaielekeze mioyo yenu kwa Bwana, Mungu wa Israeli. Ndipo hao watu wakamwambia Yoshua, Bwana, Mungu wetu, ndiye tutakayemtumikia; na sauti yake ndiyo tutakayoitii.

Basi Yoshua akafanya agano na wale watu siku ile, akawapa amri na agizo huko Shekemu. Yoshua akayaandika maneno haya katika kitabu cha torati ya Mungu; kisha akatwaa jiwe kubwa, akalisimamisha huko, chini ya ule mwaloni uliokuwa karibu na patakatifu pa Bwana.

Yoshua akawaambia watu wote, Tazama, jiwe hili litakuwa shahidi juu yetu; kwa maana limesikia maneno yote ya Bwana aliyotuambia, basi litakuwa shahidi juu yenu, msije mkamkana Mungu wenu. Basi Yoshua akawaruhusu watu, wakaenda zao, kila mtu kwenye urithi wake.

Ikawa, baada ya hayo, Yoshua, mwana wa Nuni, mtumishi wa Bwana, akafa, mwenye umri wa miaka mia na kumi.

Neno la Bwana... Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI

Zab. 16:1-2, 5, 7-8, 11 (K) 5

(K) Bwana ndiye fungu la posho langu.

Mungu unihifadhi mimi,

Kwa maana nakukimbilia Wewe.

Nimemwambia Bwana, Ndiwe Bwana wangu;

Sina wema ila utokao kwako. (K)

Bwana ndiye fungu la posho langu,

Na la kikombe changu;

Wewe unaishika kura yangu.

Nitamhimidi Bwana aliyenipa shauri,

Naam, mtima wangu umenifundisha usiku. (K)

Nimemweka Bwana mbele yangu daima,

Kwa kuwa yako kuumeni kwangu, sitaondoshwa.

Utanijulisha njia ya uzima;

Mbele za uso wako ziko furaha tele;

Na katika mkono wako wa kuume

Mna mema ya milele. (K)

SHANGILIO

Yak. 1:18

Aleluya, aleluya,

Kwa kupenda kwake mwenyewe, Baba alituzaa sisi kwa neno la kweli, tuwe kama limbuko la viumbe vyake.

Aleluya.

INJILI

Mt. 19:13 – 15

Yesu aliletewa watoto wadogo ili aweke mikono yake juu yao na kuwaombea; wanafunzi wake wakawakemea. Lakini Yesu akasema, Waacheni watoto wadogo waje kwangu; wala msiwazuie; kwa maana walio mfano wa hao, ufalme wa mbinguni ni wao. Akaweka mikono yake juu yao, akatoka huko.

Neno la Bwana... Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2020, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by FurahayaKikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

 

No comments:

Post a Comment