Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MASOMO YA MISA, JULAI 10, 2021

 

MASOMO YA MISA, JULAI 10, 2021

JUMAMOSI, JUMA LA 14 LA MWAKA

SOMO 1

Mwa. 48:29-33; 50:15-25

Yakobo aliwaamuru wanawe: Mimi ninakwenda kukusanywa pamoja na watu wangu; mnizike pamoja na baba zangu, katika pango iliyomo shambani mwa Efraoni, Mhiti; katika ile pango iliyomo shambani mwa Makpela, iliyo mbele ya Mamre katika nchi ya Kanaani, aliyoinunua Ibrahimu pamoja na shamba kwa Efraoni Mhiti, pawe milki yake pa kuzikia. Humo walimzika Ibrahimu, na Sara mkewe; humo wakamzika Isaka, na Rebeka mkewe; nami humo nikamzika Lea; shamba na pango iliyomo lililonunuliwa kwa bani Hethi.

Basi Yakobo alipokwisha kuwaagiza wanawe, akakunja miguu yake kitandani, akafa, akakusanywa pamoja na watu wake.

Ndugu zake Yusufu walipoona ya kwamba baba yao amekufa, walisema, Labda Yusufu atatuchukia; naye atatulipa maovu yetu tuliyomtenda. Wakapeleka watu kwa Yusufu, kunena, baba yako alitoa amri kabla ya kufa kwake, akasema, Mwambieni Yusufu hivi, Nakuomba uwaachilie ndugu zako kosa lao na dhambi yao, maana walikutenda mabaya; sasa twakuomba utuachilie kosa la watumwa wa Mungu wa baba yako. Yusufu akalia waliposema naye.

Nduguze wakaenda tena, wakamwangukia miguu, wakasema, Tazama, sisi tu watumwa wako. Yusufu akawaambia, Msiogope, je! Mimi ni badala ya Mungu? Nanyi kweli mlinikusudia mabaya, bali Mungu aliyakusudia kuwa mema, ili itokee kuokoka taifa kubwa, kama ilivyo leo. Basi sasa msiogope; mimi nitawalisha, na watoto wenu. Akawafariji, na kusema nao vema.

Akakaa yusufu katika Misri, yeye na nyumba ya babaye. Akaishi Yusufu miaka mia na kumi. Yusufu akaona wana wa Efraimu hata kizazi cha tatu; na wana wa Makiri, mwana wa Manase, alizaliwa magotini mwa Yusufu.

Yusufu akawaambia nduguze, Mimi ninakufa, lakini Mungu atawajia ninyi bila shaka, atawapandisha kutoka nchi hii, mpaka nchi aliyowaapia Ibrahimu, na Isaka, akaisema, Bila shaka Mungu atawajia ninyi, nanyi mtaipandisha huko mifupa yangu.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

WIMBO WA KATIKATI

Zab. 105: 1-4, 6-7 (K) 69:32

(K) Enyi mmtafutao Mungu, mioyo yenu ihuishwe.

Aleluya.

Mshukuruni Bwana, liitieni jina lake,

Wajulisheni watu matendo yake,

Mwimbieni, mwimbieni kwa zaburi,

Zitafakarini ajabu zake zote. (K)

Jisifuni kwa jina lake takatifu,

Na ufurahi moyo wao wamtafutao Bwana.

Mtakeni Bwana na nguvu zake,

Utafuteni uso wake siku zote. (K)

Enyi wazao wa Ibrahimu, mtumishi wake,

Enyi wana wa Yakobo wateule wake.

Yeye Bwana, ndiye Mungu wetu,

Duniani mwote mna hukumu zake. (K)

SHANGILIO

1Pet. 1:25

Aleluya, aleluya,

Neno la Bwana hudumu hata milele, na neno hilo ni neno lile jema lililohubiriwa kwenu.

Aleluya.

INJILI

Mt. 10:24 – 33

Yesu aliwafundisha mitume wake: Mwanafunzi hampiti mwalimu wake, wala mtumwa hampiti bwana wake. Yamtosha mwanafunzi kuwa kama mwalimu wake, na mtumwa kuwa kama bwana wake. Ikiwa wamemwita mwenye nyumba Beelzebuli; je! Si zaidi wale walio wa nyumbani mwake?

Basi, msiwaogope, kwa maana hakuna neno lililositirika, ambalo halitafunuliwa; wala lililofichwa, ambalo halitajulikana. Niwaambialo ninyi katika giza, lisemeni katika nuru; na msikialo kwa siri, lihubirini juu ya nyumba. Msiwaogope wauuao mwili, wasiweze kuiua na roho; afadhali mwogopeni yule awezaye kuangamiza mwili na roho pia katika jehanum. Je! Mashomoro wawili hawauzwi kwa senti moja? Wala hata mmoja haanguki chini asipojua Baba yenu; lakini ninyi, hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope basi; bora nyinyi kuliko mashomoro wengi.

Basi, kila mtu atakayenikiri mbele ya watu, nami nitamkiri mbel za Baba yangu aliye mbinguni. Basil mtu yeyote atakayenikana mbele ya watu, nami nitamkana mbele za Baba yangu aliye mbinguni.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Copyright © 2020, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by FurahayaKikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

No comments:

Post a Comment