Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

KUUTAFUTA UFALME

 

“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Tafakari ya kila siku

Alhamisi Juali  29, 2021

Juma la 17 la Mwaka

 

Kut 40:16-21, 34-38

Zab 84: 2-5, 7, 10 (K)

Mt. 13:47-53

 

 

KUUTAFUTA UFALME

Ndugu Zangu wapendwa, karibuni kwa adhimisho la misa takatifu asubuhi ya leo. Neno la Bwana katika somo la kwanza, Musa anaamriwa kutengeneza sanduku la agano na kuliweka katika hema ya kukutania. Sanduku la agano liliashiria uwepo wa Mungu katika safari ya maisha ya wana wa Israeli. Hivyo walilitegemea katika maongozi yao ya safari ya kuelekea nchi ya ahadi. Bila uwepo wa Mungu katika safari yao, wana wa Israeli wangalishindwa kuelekea katika njia salama.

Kama wana wa Israeli walivyofumbuliwa kwamba wanaongozwa na nguvu ya Mungu, nasi tutambue kwamba ni kwa namna hiyo hiyo tunavyoongozwa na nguvu ya Mwenyezi Mungu katika maisha yetu. Sisi tuwe tayari kuiruhusu nguvu ya Mungu ituongoze. Tuiruhusu ituongoze kila tuamkapo asubuhi, kila tunapotaka kufanya kazi au shughuli yoyote. Ukweli ni kwamba duniani vipo vikwazo vingi. Yupo shetani anayeleta visirani, wapo wenzetu wenye hasira na nia mbaya nasi, pia udhaifu wetu katika kufanya mambo ni mkubwa. Kuna wakati tunapatwa na vitu kama homa, woga na hasira na tunaweza kufanya mambo ya ajabu kabisa maishani, mambo ambayo hutuharibia kwa kiasi kikubwa. Lazima tuwe na utayari wa kuikaribisha nguvu ya Mungu ndani ya maisha yetu ili ituongoze kwa maisha yetu yote.

Katika somo la injili, Yesu anasisitiza kwamba ufalme wa mbinguni unafanana na juya lililotupwa baharini likakusanya samaki wa kila aina. Mfano huu waonesha utayari wa Mungu wa kuwavumilia wenye dhambi. Yupo tayari kutukubali katika udhaifu wetu, na kutuvumilia tuendelee kufanya kazi naye licha ya udhaifu wetu. Lakini anataka tusiendelee na udhaifu huu hadi mwisho, anataka tubadilike. Hizi ndizo sababu za kuwaacha wenye dhambi na wabaya waendelee kuishi pamoja kwa kila wakati. Tuwe tayari kukubali kubadilika. Tumsifu Yesu Kristo.

------------------------

Copyright ©2013-2020 ©FurKat, FurahayaKikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

 

No comments:

Post a Comment