Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

KUTAFUTA LULU YA THAMANI KUBWA

 

“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Tafakari ya kila siku

Jumatano Julai 28, 2021

Juma la 17 la Mwaka

 

Kut 34:29-35

Zab 99:5-7, 9;

Mt 13:44-46

 

 

KUTAFUTA LULU YA THAMANI KUBWA

Karibuni sana wapendwa kwa adhimisho la misa takatifu katika asubuhi ya leo. Leo katika tafakari ya neno la Bwana, katika somo la kwanza, Musa anatokea mbele ya watu, baada ya kukaa mlimani kwa siku arobaini usiku na mchana. Anapotokea mbele ya wana wa Israeli, uso wake unaonekana kungaa, na wana wa Israeli wanaoona hili, wanaogopa. Lakini Musa hakujua kwamba kwa kitendo cha uso wake kungaa, kiliwafanya wana wa Israeli waogope, yeye aliona kwamba ni jambo la kawaida, na hakujiona kungaa. Na alikuwa akienda mbele ya wana wa Israeli kama kawaida bila kujitambua kwamba kungaa kwa uso wake kuliwatisha.

Kungaa huku kulimaanisha kwamba Musa amepokea sehemu ya utukufu wa Bwana, kwa sababu alikaa na Bwana usiku na mchana juu ya mlima Sinai kwa siku arobaini mchana na usiku. Hivyo ule utukufu wa Bwana ulikuwa juu yake. Kungaa huku kulimfanya apate madaraka mbele ya wana wa Israeli, waepuke kufikiria kana kwamba hakutumwa. Hapa ni Mungu alimdhihirisha kwamba yeye ni mtume wake mpendwa hivyo asikilizwe. Musa alipaswa kutunza kungara huku kwake sura akijua kwamba yeye ni kiumbe kitakatifu cha Mungu na hivyo yafaa atimize kazi ya Bwana.

Nasi tumepokea sehemu ya utukufu wa Bwana, Bwana ametushirikisha utukufu wake, kungaa kwake kwa ubatizo wetu na baadaye kipaimara. Tuheshimu utukufu huu. Tusijichanganye au kujitoa kwa shetani. Maisha yetu yawe kwa ajili ya Bwana ili Bwana atusaidie. Ni kufuru kubwa ikiwa tutaruhusu utukufu wetu uchangamanike na maisha ya kishetani. Musa alijifunika uso wake mbele ya watu ili watu wasidharau utukufu huu, kama sehemu ya heshima. Nasi tunapaswa kufanya hivyo hivyo; tusichukulie utukufu wetu, ubatizo wetu, maisha yetu ya wakfu, kama kitu cha kawaida sana; tunapaswa kuupatia heshima zake zote. Tukiona kila kitu katika ukawaida, hakika tutashindwa kumpatia Mungu wetu sifa na heshima yake.

Katika injili, Yesu anafananisha ufalme wa mbinguni na mfanyabiashara atafutaye lulu zuri na akishajua sehemu iliyojificha, huuza yote ili kuipata lulu hiyo. Yesu ndiye mwenye kufanya sadaka ya namna hii. Yeye ndiye mwenye kukubali kutoa yote apate kuikomboa roho ya mwanadamu na kutupatia wokovu. Alikuwa tayari kutoa maisha yake kama sadaka. Nasi tuwe watu wa kukubali kuacha yote ili kujitoa kwa Yesu. Tumsifu Yesu Kristo.

------------------------

Copyright ©2013-2020 ©FurKat, FurahayaKikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

No comments:

Post a Comment