Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

KUKUWA KATIKATI YA MAGUGU

 

“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Tafakari ya kila siku

Jumanne Julai 27, 2021

Juma la 17 la Mwaka

 

 

Kut 33:7-11;34:5-9.28

Zab 103: 6-13 (k) 8

Mt 13:36-43

 

 

KUKUWA KATIKATI YA MAGUGU

Ndugu zangu wapendwa, karibuni kwa adhimisho la misa takatifu asubuhi ya leo. Katika tafakari yetu ya neno la Bwana, leo tunakutana na habari kuhusu hema la kukutania. Hapa palikuwa sehemu maalumu kwa ajili ya kukutania na Bwana kwa wana wa Israeli. Sehemu hii ilitengwa, iliwekwa sehemu ya pekee, sehemu ya utulivu, na waliingia tu watu maalumu, mbali na zile sehemu ambazo ni nje ya makazi ya watu ya mara kwa mara, makazi yasiyokuwa na heshima. Kufanya hivi kulionesha utakatifu na ukuu wa Mungu, kwamba Mungu ni mkuu, atengewe mahali patakatifu, na mahali palipo na utulivu.

Pale walipoonesha imani hii, Bwana alikuja na kufanya makao kati yao, na kusikiliza maombi yao, na vizazi vijavyo viliweza kujifunza mambo mazuri na kujua zaidi kuhusu ukuu wa Mungu. Sisi nasi tunapaswa kuheshimu sehemu zetu takatifu, zijengwe mahali pa utulivu, zitengewe watu maalumu wa kuyatunza. Yapo maeneo ambapo makanisa yanafanyiwa usafi na kampuni, kampuni zenye watu wasio hata na imani ya Kikristo. Kwa upande mwingine hapa ni kukosea. Kanisa letu ni nyumba ya kukutania na Bwana, hata yule anayekuja kufanya usafi ndani yake awe na heshima, sehemu yako ya ibada lazima uiheshimu, vifaa vyako vya ibada lazima uviheshimu na uvitunze vyema. Ukianza kuvitapanya tu, mwishowe utashindwa kuona umuhimu wake. Wengi wetu hatuoni umuhimu wa rozari, misalaba, au sanamu kwa sababu ya kuvikosea heshima. Tuvitunze vifaa hivi.

Katika somo la injili, Yesu anaelezea kwamba ibilisi ndiye aliyepanda magugu ndani ya shamba la Bwana. Magugu haya ni nguvu ya uovu ambayo hadi sasa imekuwa ikiusumbua ulimwengu na mwanadamu anaishi kati ya nguvu hii ya uovu na wema. Sisi tutambue uwepo wa watu wa namna hii, watu wenye kupanda uovu na kusia mbegu ya chuki kwenye maisha yetu. Hawa ni wakala wa ibilisi, watakuwa wanasia mbegu hizi hadi mwisho wa maisha yetu lakini yafaa tuwe tayari kuzitambua mbegu hizi na kuziepuka ili zisichafue maisha yetu. Tumsifu Yesu Kristo

 

------------------------

Copyright ©2013-2020 ©FurKat, FurahayaKikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

No comments:

Post a Comment