Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MSAMAHA

 

“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Tafakari ya Kwaresima

Jumanne, Machi 9, 2021,

Juma la 3 la Kwaresima

 

Dan 3:25,34-43;

Zab 25:4-9;

Mt 18:21-35

 

MSAMAHA

Karibuni sana wapendwa kwa adhimisho la Misa Takatifu asubuhi ya leo. Neno la Bwana katika somo la kwanza tunakutana na sala aliyoisali Azariah akiwa katika tanuru la moto baada ya kutupwa huko na mfalme Nebuchadnezer kwa sababu ya kumtukuza Bwana Mungu wa Israeli.

Azariah alimtumikia na kumwamini Bwana Mungu na leo anashuhudia ulinzi wake maishani, anamfanya asiaibike machoni pa adui zake. Kwa Azariah, huu ulikuwa wakati mgumu wa kujaribiwa lakini alilia na Bwana na Bwana alimuokoa.

Sisi tujiombee ili tuwe na imani kama ya Azariah kila tukumbanapo na vishawishi au adui maishani mwetu. Vishawishi vinatukumba kila siku na kuishia kutushinda. Ni jambo la fedheha kuanguka mikononi mwa adui zako. Wengi wetu tumekuwa tukiabika kwa kushindwa na adui zetu. Tumwombe Mungu ili tusiaibike, tutoke kifua mbele.

Katika somo la injili, Yesu anaelezea habari za mtumishi aliyesamehewa deni kubwa na baadaye kukataa kusamehe mwenzake deni dogo. Huyu mtumishi wa kwanza aliyesamehewa deni kubwa yaonekana alikuwa na deni kubwa ajabu. Hili deni inaonekana kwamba alilirithi toka kwa ndugu au wazazi wake. Hivyo likamuangukia yeye kulipa. Ndio sababu za hili deni kuwa kubwa hivi. Lakini alipoomba msamaha alisamehewa na hivyo alipaswa kuonesha kwa mwenzake huruma kama iliyomtokea na kwake pia.

Yesu anatumia mfano huu kuelezea hali yetu kama wanadamu kwamba tunapaswa kusamehe kwani sisi ndio tuliosamehewa deni kubwa na Mungu. Sisi tulirithi deni la dhambi toka kwa wazazi wetu wa mwanzo-Yesu ndiye aliyekufa msalabani kutufutia deni hili. Bei ya deni hili lilikuwa kubwa sana kiasi kwamba sisi kama sisi hata kama tungalifanya nini hakika hatungaliweza kulipa. Yesu ametulipia deni hili. Sisi ndio tuliosamehewa deni kubwa na hivyo yatupasa kuwasamehe wenzetu.

Wapo wenzetu wenye mtindo mbaya wa kudai, tunadai hadi senti ya mwisho. Tunatumia lugha mbaya katika kudai, leo tunakumbushwa kwamba tutambue kwamba sisi nasi tumewahi kusamehewa madeni tena makubwa kabisa. Hivyo tuwe na utayari wa kuwasamehe wenzetu. Yesu anadhihirisha kwamba tunapokosa utayari wa kuwasamehe wenzetu-ni hasara kwetu kwani tunajifufulia tena ile adhabu tuliyostahili kutokana na madhambi yetu. Sisi tusiache kuwasamehe wenzetu.

Tunapojisikia hali ya kutokusamehe-ni lazima kutambua kwamba ni shetani ametuingilia, na lengo lake ni kutuvika kiburi ili aturudishe katika utumwa wa lile kosa la mwanzo. Shetani anatafuta watumwa, sisi tusikubali tena kuwa watumwa wake kwakushindwa kuwasamehe wenzetu.

Ukweli ni kwamba ulimwenguni bila kusamehe hatutaweza kuendelea na maisha. Wanadamu ni dhaifu mno, hata yule tunayemtegemea kwamba hawezi kutenda dhambi fulani atatenda. Baadhi ni wadhaifu ajabu-unaweza kusema ni nini kipo vichwani mwao? Ni nini kimeingia huko .

Copyright ©2013-2020 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

No comments:

Post a Comment