Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

YESU MWENYE HURUMA!

 

“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Tafakari ya kila siku

Jumamosi, Februari 6, 2021,

Juma la 4 la Mwaka wa Kanisa

 

KUMBUKUMBU YA WAT. PAULO MIKI NA WENZAKE (MASHAHIDI)

 

Ebr 13: 15-17, 20-21;

Zab 22: 1-6;

Mk 6: 30-34.

 

YESU MWENYE HURUMA!

Karibuni sana wapendwa wa Bwana kwa tafakari ya neno la Bwana katika adhimisho la Misa Takatifu. Katika zaburi yetu leo ya wimbo wa katikati, mzaburi anatueleza kwamba Bwana Mungu ni mchungaji wake. Na hakika hakuna awezaye kumshinda akiwa mikononi mwa Bwana. Hii ni zaburi iliyoimbwa na Daudi katika imani kubwa. Aliimba akiwa katika mapango akiwindwa auawe na mfalme Sauli. Daudi alimlilia Mungu kwa zaburi hii na hakika Sauli alishindwa. Daudi alipatwa na maadui wengi, alisalitiwa na wengi lakini hakuna aliyeweza kumshinda.

Leo anatutolea ushuhuda kwamba kila amtumainiye Bwana, amfanyaye Bwana kuwa mchungaji wake hakika atashinda tu. Zaburi hii inatumika leo kusisitiza ujumbe wa somo la kwanza-toka waraka kwa waebrania kwamba wakristo wanapaswa kujikabidhi kwa Yesu kwani yeye ndiye mchungaji mwema. Pia wawaheshimu viongozi wao na kuwatii. Watambue kwamba Mungu amewapatia baadhi ya wanadamu wao madaraka. Na hawa ni wachungaji kwa kundi lote. Hivyo wanapaswa kuwatii, wasijiamulie wenyewe, wasiishi bila utaratibu.

Ndugu zangu kwetu Kristo ni mchungaji mwema. Lakini shida ya sasa ni kondoo kukataa maongozi ya mchungaji, kuishi wanavyotaka. Dunia inaharibika kwa sababu ya kondoo kukataa maongozi ya wachungaji. Kristo ndiye mchungaji mkuu, lakini pia kayakabidhi madaraka hayo kwa wanadamu wenzetu na jamii. Tuishi kuendana na utaratibu, heshimu viongozi walioko ndani ya jamii. Kondoo lazima wasikie sauti ya mchungaji. Wengi wetu tunafanya vitu ovyo kwa sababu hatufuati sauti ya mchungaji.

Yesu katika injili anadhihirisha kuwa mchungaji mwema, mwenye kukubali hata kutoa muda wake wa kupumzika kwa ajili ya kondoo. Leo katika injili tunaona kwamba alikuwa wamepanga kwenda mahali pa faragha na mapumziko lakini uwepo wa watu unamsukuma kuwahudumia tu. Sisi tuache ubinafsi. Mara nyingi tukishapanga ratiba zetu tunakuwa wakali watu kutuingilia. Lakini wakati mwingine ni ubinafsi tu. Tuache ubinafsi, ratiba zetu zisitunyime tuache kuwafikia wenzetu. Amina.

 

 

 

------------------------

Copyright ©2013-2020 ©FurKat, FurahayaKikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

 

 

No comments:

Post a Comment