Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

KUMTEMBELEA DAKTARI WA MIOYO YETU!

 

“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Tafakari ya Kwaresima

Jumamosi, Febuari 20, 2021

Jumamosi baada ya Jumatano ya majivu

 

Isa 58: 9-14;

Zab 86: 1-6;

Lk 5: 27-32

 

KUMTEMBELEA DAKTARI WA MIOYO YETU!

 

Karibuni sana ndugu zangu wapendwa kwa adhimisho la Misa Takatifu asubuhi ya leo. Leo masomo yetu yanatuhimiza kutambua maovu yetu, kutakatifuza siku zetu zote kwa Bwana ili tuweze kufaidi zaidi neema zitokazo kwa Bwana.

Nabii Isaya anawaeleza wana wa Yuda kwamba njia ya Bwana wanaijua, wajibu wao wanautambua lakini hawapati neema yoyote. Kosa lipo katika kuzembea na kukosa umakini katika mambo ya Bwana. Uzembe ndio unaowafanya washindwe kuvuna neema toka kwa Bwana. Walikuwa wakifanya vitu ili kutimiza ratiba tu.

Ndilo himizo tunaloambiwa sisi pia katika siku ya leo. Wengi wetu tunasali, tunahudhuria misa za dominika lakini hatupati mabadiliko. Yote haya yanasababishwa na uzembe, kutojali na kuhudhuria kwa lengo la kutimiza ratiba tu. Tujitahidi tuepuke uzembe na kufanya mambo kwa lengo la kutimiza ratiba. Haya yametufanya kuwa watu wa kupoteza muda, kwa sababu hatuvuni chochote katika sala. Tuzidishe umakini katika mambo yote ya sala. Tuepuke kumfanyia Mwenyezi Mungu maigizo.

Kwenye somo la injili, Levi anaitwa na Yesu na anapokutana na Yesu, anabadili maisha yake, anakuwa makini kuhusu mambo ya Mungu, anarudisha na alivyodhulumu. Hapa ndipo mlango wa neema ulifunguliwa juu yake na maisha yake kubalika zaidi. Nasi tutambue kwamba tutaionja neema ya Mungu maishani mwetu pale tu tutakapokuwa makini na mambo ya Mungu, kurudisha tulichodhulumu, na kumkaribisha Yesu nyumbani mwetu kama anavyofanya Levi katika injili.

Na hapa ndipo milango ya neema itakapofunguliwa juu yetu na hakika tutaweza kufurahia zaidi baraka na neema zake.

 

 

------------------------

Copyright ©2013-2020 ©FurKat, FurahayaKikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

 

 

 

No comments:

Post a Comment