Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MASOMO YA MISA, FEBRUARI 7, 2026



MASOMO YA MISA, FEBRUARI 7, 2026
JUMAMOSI YA WIKI YA 4 MWAKA

SOMO 1
1 Fal. 3:4-13

Mfalme Sulemani alienda Gibeoni, ilia toe dhabihu huko; kwa kuwa ndipo mahali pa juu palipo pakuu. Sulemani akatoa sadaka elfu za kuteketezwa juu ya madhabahu ile. Na huko Gibeoni Bwana akamtokea Sulemani katika ndoto ya usiku; Mungu akamwambia, Omba utakalo nikupe. Sulemani akasema, Umemfanyia mtumwa wako Daudi baba yangu fadhili kuu, kadiri alivyoenenda mbele zako katika kweli, na katika haki, na katika unyofu wa moyo pamoja nawe; nawe umemwekea na fadhili hii kubwa, maana umempa mwana wa kuketi kitini pake kama ilivyo leo.

Na sasa, Ee Bwana, Mungu wangu, umenitawaza niwe mfalme mimi mtumwa wako badala ya Daudi baba yangu; nami ni mtoto mdogo tu; sijui jinsi inipasavyo kutoka wala kuingia. Na mtumwa wako yu katikati ya watu wako uliowachagua, watu wengi wasioweza kuhesabiwa, wala kufahamiwa idadi yao, kwa kuwa ni wengi. Kwa hiyo nipe mimi mtumwa wako moyo wa adili niwahukumu watu wako, na kupambanua mema na mabaya; maana ni nani awezaye kuwahukumu hawa watu wako walio wengi?

Neno hili likawa jema machoni pa Bwana, ya kuwa Sulemani ameomba neno hili. Mungu akamwambia, Kwa kuwa umeomba neno hili, wala hukujitakia maisha ya siku nyingi; wala hukutaka utajiri kwa nafsi yako; wala hukutaka roho za adui zako; bali umejitakia akili za kujua kuhukumu; basi, tazama, nimefanya kama ulivyosema. Tazama, nimekupa moyo wa hekima na wa akili; hata kabla yako hapakuwa na mtu kama wewe. Na mambo yale usiyoyaomba nimekupa, mali na fahari, hata hapatakuwa na mtu katika wafalme kama wewe, siku zako zote.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 119:9-14 (K) 12

(K) Unifundishe amri zako, ee Bwana.

Jinsi gani kijana aisafishe njia yake?
Kwa kutii akilifuata neno lako.
Kwa moyo wangu wote nimekutafuta,
Usiniache nipotee mbali na maagizo yako. (K)

Moyoni mwangu nimeliweka neno lako,
Nisije nikakutenda dhambi.
Ee Bwana umehimidiwa,
Unifundishe amri zako. (K)

Kwa midomo yangu nimezisimulia
Hukumu zote za kinywa chako.
Nimeifurahia njia ya shuhuda zako
Kana kwamba ni mali mengi. (K)


SHANGILIO
Zab. 119:28, 33

Aleluya, aleluya,
Unitie nguvu sawasawa na neno lako,
Ee Bwana, unifundishe njia ya amri zako.
Aleluya.


INJILI
Mk. 6:30-34

Mitume walikusanyika mbele ya Yesu; wakampa habari za mambo yote waliyoyafanya, na mambo yote waliyoyafundisha. Akawaambia, Njoni ninyi peke yenu kwa faragha; mahali pasipokuwa na watu, mkapumzike kidogo. Kwa sababu walikuwako watu wengi, wakija, wakienda, hata haikuwako nafasi ya kula. Wakaenda zao faragha mashuani, mahali pasipokuwa na watu. Watu wakawaona wakienda zao, na wengi wakatambua, wakaenda huko mbio kwa miguu, toka miji yote, wakatangulia kufika. Naye aliposhuka mashuani, akaona mkutano mkuu, akawahurumia; kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji; akaanza kuwafundisha mambo mengi.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

No comments:

Post a Comment