MASOMO YA MISA, DESEMBA 21, 2022
JUMATANO, JUMA LA 4 LA MAJILIO
SOMO 1
Wimb. 2:8 – 14
Sikiliza! Ni mpendwa wangu! Tazama, anakuja akiruka
milimani, akichachawa vilimani. Mpendwa wangu ni kama paa, au ayala. Tazama, asimama
nyuma ya ukuta wetu, achungulia dirishani, atazama kimiani.
Mpendwa wangu alinena, akaniambia, ondoka, mpenzi wangu,
mzuri wangu, uje zako, maana tazama, kaskazi imepita, masika imekwisha,
imekwenda zake; maua yatokea katika nchi, wakati wa kupelea umefika, na sauti
ya mwigo husikiwa kwetu. Mtini wapevusha tini zake, na mizabibu inachanua
inatoa harufu yake nzuri.
Ondoka, mpenzi wangu, mzuri wangu, uje zako. Hua wangu,
mafichoni mwa jabali, katika sitara za magenge, nitazame uso wako, nisikie
sauti yako, maana sauti yako ni tamu na uso wako mzuri.
Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.
Au.
Sef. 3:14:14 – 17
Imba, ee binti Sayuni; piga kelele, ee Israeli; furahi na
kushangilia kwa moyo wako wote, ee binti Yerusalemu. Bwana ameziondoa hukumu
zako, amemtupa nje adui yako; mfalme wa Israeli, naam, yeye Bwana, yu katikati
yako; hutaogopa uovu tena.
Katika siku ile Yerusalemu utaambiwa, usiogope, ee
Sayuni; mikono yako isilegee. Bwana, Mungu wako, yu katikati yako shujaa
awezaye kuokoa; atakushangilia kwa furaha kuu, atatulia katika upendo wake.
Atakufurahia kwa kuimba.
Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.
WIMBO WA KATIKATI
Zab. 33:2 – 3, 11 – 12, 20 – 21 (K) 1, 3
(K) Mpigieni Bwana vigelegele, enyi wenye haki: Mwimbieni
wimbo mpya.
Mshukuruni Bwana kwa kinubi,
Kwa kinanda cha nyuzi kumi mwimbieni sifa.
Mwimbieni wimbo mpya,
Pigeni kwa ustadi kwa sauti ya shangwe. (K)
Shauri la Bwana lasimama milele,
Makusudi ya moyo wake vizazi na vizazi.
Heri taifa ambalo Bwana ni Mungu wako,
Watu aliowachagua kuwa urithi wake. (K)
Nafsi zetu zinamngoja Bwana;
Yeye ndiye msaada wetu na ngao yetu.
Maana mioyo yetu itamfurahia,
Kwa kuwa tumelitumaini jina lake takatifu. (K)
SHANGILIO
Aleluya, aleluya,
Ee Utokaye Mashariki, uliye mng’ao wa mwanga wa milelel
na jua la haki, njoo kuwaangazia wakaao gizani na katika kivuli cha mauti.
Aleluya.
INJILI
Lk. 1:39 – 45
Mariamu aliondoka siku hizo, akaenda hata nchi ya
milimani kwa haraka mpaka mji mmoja wa Yuda, akaingia nyumbani kwa Zakaria
akamwamkia Elisabeti. Ikawa Elisabeti aliposikia kule kuamkia kwake Mariamu,
kitoto kichanga kikaruka ndani ya tumbo lake; Elisabeti akajazwa Roho
Mtakatifu; akapaza sauti kwa nguvu akasema,
Umebarikiwa wewe katika wanawake, naye mzao wa tumbo lako
amebarikiwa. Limenitokeaje neno hili, hata mama wa Bwana wangu anijilie mimi?
Maana sauti ya kuamkia kwako ilipoingia masikioni mwangu, kitoto kichanga
kikaruka kwa shangwe ndani ya tumbo langu. Naye heri aliyesadiki; kwa maana
yatatimizwa aliyoambiwa na Bwana.
Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.
Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA
MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright ©
1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of
Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha
ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.
No comments:
Post a Comment