Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

UFALME WA MUNGU UPO KATI YETU.


“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”
Alhamisi, Novemba 10, 2022
Juma la 32 la Mwaka wa Kanisa

Kumbukumbu ya Mt. Leo Mkuu, Papa na Mwalimu wa Kanisa. 

Flm1:7-20; 
Zab 145:7-10; 
Lk 17:20-25


UFALME WA MUNGU UPO KATI YETU

Barua ya Mt. Paulo kwa Filemoni, ni barua fupi sana, ina aya tu, lakini ni barua ilioandikwa kwa utaalamu mkubwa. Mt. Paulo anaianza kwa kukiri uzuri wa Filemoni na kwa jinsi alivyo wawekea na kuwaonesha wema jumuiya ya Kikristo. Mt. Paulo anasisitiza juu ya Onesimo, ambaye alikuwa mtumwa wa Filemoni, na anamuomba amchukue Onesimo kama ndugu katika Kristo. Na anamuomba Filemoni amsamehe Onesimo kwa kosa lolote alilotenda kabla. Unaweza kuona ni kwa jinsi ghani Ufalme wa Mungu ulivyowekwa wazi na Paulo. Ufalme wa Mungu ambao upo wazi kwa kila mtu. Kazi yetu ni kuutambua ufalme huo ndani yetu. 

Tunapokuwa tayari kutangaza msamaha tunakuwa tunaonesha tunu za ufalme wa Mungu tungali hapa duniani. Kushindwa kusamehe na kubeba watu moyoni pengine limekuwa tatizo la wengi. Leo nasi tunaalikwa tusiwabebe watu na wala tusikubali kujiumiza wenyewe kwa kubeba chuki kwani chuki ni sumu ndani wa mwili wa mtu mwenyewe. 

Sala: Bwana Yesu nisaidie mimi niweze kueneza Ufalme wako kwa njia ya maneno na matendo yangu.


Copyright ©2013-2022 ©FurKat, Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com


No comments:

Post a Comment