MASOMO YA MISA, NOVEMBA 10, 2022
ALHAMISI, JUMA LA 32 LA MWAKA WA KANISA
KUMBUKUMBU YA MT. LEO MKUU (PAPA NA MWALIMU WA KANISA)
SOMO 1
Flm. 7 – 20
Nalikuwa na furaha nyingi na faraja kwa sababu ya upendo
wako, kwa kuwa mioyo ya watakatifu imeburudishwa nawe, ndugu yangu. Kwa hiyo, nijapokuwa nina ujasiri katika Kristo kukuagiza
likupasako; lakini, kwa ajili ya upendo nakusihi, kwa kuwa ni kama nilivyo,
Paulo mzee, na sasa mfungwa wa Kristo Yesu pia. Nakusihi kwa ajili ya mtoto
wangu niliyemzaa katika vifungo vyangu, yaani, Onesimo; ambaye zamani alikuwa
hakufai, bali sasa akufaa sana, wewe na mimi pia; niliyemtuma kwako, yeye
mwenyewe, maana ni moy wangu hasa; ambaye mimi nalitaka akae kwangu, apate
kunitumikia badala yako katika vifungo vya Injili.
Lakini sikutaka kutenda neno lolote isipokuwa kwa shauri
lako, ili kwamba wema wako usiwe kama kwa lazima, bali kwa hiari. Maana, labda
ndiyo sababu alitengwa nawe kwa muda, ili uwe naye tena milele; tokea sasa, si
kama mtumwa, bali zaidi ya mtumwa, ndugu mpendwa; kwangu mimi sana, na kwako
wewe zaidi sana, katika mwili na katika Bwana. Basi kama ukiniona mimi kuwa
mshirika nawe, mpokee huyu kama mimi mwenyewe. Na kama amekudhulumu, au unamwia
kitu, ukiandike ndicho juu yangu. Mimi Paulo nimeandika kwa mkono wangu
mwenyewe, mimi nitalipa. Sikuambii kwamba nakuwia hata nafsi yako. Naam, ndugu
yangu, nipate faida kwako katika Bwana; uniburudishe moyo wangu katika Kristo
Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.
WIMBO WA KATIKATI
Zab. 146:7 – 10 (K) 5
(K) Heri ambaye Mungu wa Yakobo ni msaada wake.
Bwana huishika kweli milele,
Huwafanyia hukumu walioonewa,
Huwapa wenye njaa chakula,
Hufungua waliofungwa. (K)
Bwana huwafumbua macho walopofuka,
Bwana huwainua walioinama,
Bwana huwapenda wenye haki,
Huwahifadhi wageni. (K)
Huwategemeza yatima na mjane,
Bali njia ya wasio haki huipotosha.
Bwana atamiliki milele,
Mungu wako, Ee Sayuni, kizazi hata kizazi.
Aleluya. (K)
SHANGILIO
Zab. 27:11
Aleluya, aleluya,
Ee Bwana, uifundishe njia yako, na kuniongoza katika njia
iliyonyoka.
Aleluya.
INJILI
Lk. 17:20-25
Yesu alipoulizwa na Mafarisayo, Ufalme wa Mungu utakuja
lini? Aliwajibu akawaambia, Ufalme wa Mungu hauji kwa kuuchunguza; wala
hawatasema, Tazama, upo huku, au, kule, kwa maana, tazama, ufalme wa Mungu umo
ndani yenu.
Akawaambia wanafunzi, Siku zitakuja mtakapotamani kuona
siku moja katika siku zake Mwana wa Adamu, msiione. Tena watawaambia, Tazama,
kule! Tazama, huku! Msiondoke mahali mlipo, wala msiwafuate; kwa kuwa, kama
vile umeme umulikavyo toka upande huu chini ya mbingu hata upande huu chini ya
mbingu, ndivyo atakavyokuwa Mwana wa Adamu katika siku yake. Lakini kwanza,
hana budi kupata mateso mengi, na kukataliwa na kizazi hiki.
Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.
Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA
MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright ©
1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of
Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha
ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.
No comments:
Post a Comment