MASOMO YA MISA, NOVEMBA 12, 2022
JUMAMOSI, JUMA LA 32 LA MWAKA WA KANISA
KUMBUKUMBU YA MT. JOSAFATI (ASKOFU NA SHAHIDI)
SOMO 1
3Yoh. 1:5 – 8
Mpenzi, kazi ile ni ya uaminifu uwatendeayo hao ndugu na
hao wageni nao, waliokushuhudia upendo wako mbele ya kanisa; utafanya vizuri
ukiwasafirisha kama ipasavyo kwa Mungu. Kwa maana, kwa ajili ya Jina hilo,
walitoka, wasipokee kitu kwa Mataifa. Basi imetupasa sisi kuwakaribisha watu
kama hao, ili tuwe watenda kazi pamoja na kweli.
Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.
WIMBO WA KATIKATI
Zab. 112:1 – 6 (K) 1
(K) Heri mtu yule amchaye Bwana.
Aleluya.
Heri mtu yule amchaye Bwana,
Apendezwaye sana na maagizo yake
Wazao wake watakuwa hodari duniani;
Kizazi cha wenye adili kitabarikiwa. (K)
Nyumbani mwake mna utajiri na mali,
Na haki yake yakaa milele.
Nuru huwazukia wenye adili gizani;
Ana fadhili na huruma na haki. (K)
Heri atendaye fadhili na kukopesha;
Atengenezaye mambo yake kwa haki.
Kwa maana hataondoshwa kamwe;
Mwenye haki atakumbukwa milele. (K)
SHANGILIO
Zab. 130:5
Aleluya, aleluya,
Roho yangu inamngoja Bwana, na neno lake nimelitumainia.
Aleluya.
INJILI
Lk. 18:1-8
Yesu aliwaambia wanafunzi wake mfano, ya kwamba imewapasa
kumwomba Mungu sikuzote, wala wasikate tamaa. Akasema, Palikuwa na kadhi katika
mji Fulani, hamchi Mungu, wala hajali watu. Na katika mji huo palikuwa na
mwanamke mjane, aliyekuwa akimwendea-endea, akisema, Nipatie haki na adui
wangu. Naye kwa muda alikataa; halafu akasema moyoni mwake, Ijapokuwa simchi
Mungu wala sijali watu, lakini, kwa kuwa mjane huyu ananiudhi, nitampatia haki
yake, asije akanichosha kwa kunijia daima.
Bwana akasema, Sikilizeni asemavyo yule kadhi dhalimu. Na
Mungu, je! Hatawapatia haki wateule wake wanaomlilia mchana na usiku, naye ni
mvumilivu kwao? Nawaambia, atawapatia haki upesi; walakini, atakapokuja Mwana
wa Adamu, je! Ataiona Imani duniani?
Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.
Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA
MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright ©
1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of
Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha
ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.
No comments:
Post a Comment