MASOMO YA MISA, NOVEMBA 19, 2022
JUMAMOSI, JUMA LA 33 LA MWAKA WA KANISA
SOMO 1
Ufu. 11:4 – 12
Mimi, Yohane, nilisikia sauti isemayo: Hao ndio ile
mizeituni miwili na vile vinara viwili visimamavyo mbele za Bwana wa nchi. Na
mtu akitaka kuwadhuru, moto hutoka katika vinywa vyao na kuwala adui zao. Na
mtu akitaka kuwadhuru, hivyo ndivyo impasavyo kuuawa. Hao wana amri ya
kuzifunga mbingu, ili mvua isinye katika siku za unabii wao. Na wana amri juu
ya maji kuyageuza kuwa damu, na kuipiga nchi kwa kila pigo, kila watakapo. Hata
watakapoumaliza ushuhuda wao, yule mnyama atokaye katika kuzimu atafanya vita
nao, naye atawashinda na kuwaua. Na mizoga yao itakuwa katika njia ya mji ule
mkuu, uitwao kwa jinsi ya roho Sodoma, na Misri, tena ni hapo Bwana wao
aliposulibiwa. Na watu wa hao jamaa na kabila na lugha na taifa waitazama
mizoga yao siku tatu u nusu, wala hawaiachi mizoga yao kuwekwa kaburini. Nao
wakaao juu ya nchi wafurahi juu yao na kushangilia. Nao watapelekeana zawadi
wao kwa wao, kwa kuwa manabii hao wawili waliwatesa wao wakaao juu ya nchi.
Na baada ya siku hizo tatu u nusu, roho ya uhai itokayo kwa
Mungu ikawaingia, wakasimama juu ya miguu yao; na hofu kuu ikawaangukia watu
waliowatazama. Wakasikia sauti kuu kutoka mbinguni ikiwaambia, Pandeni hata
huku. Wakapanda mbinguni katika wingu, adui zao wakiwatazama.
Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.
WIMBO WA KATIKATI
Zab. 144:1 – 2, 9 – 10 (K) 1
(K) Ahimidiwe Bwana, mwamba wangu.
Ahimidiwe Bwana, mwamba wangu,
Anifundishaye mikono yangu vita,
Vidole vyangu kupigana. (K)
Mhisani wangu na boma langu,
Ngome yangu na mwokozi wangu,
Ngao yangu niliyemkimbilia,
Huwatiisha watu wangu chini yangu. (K)
Ee Mungu, nitakuimbia wimbo mpya,
Kwa kinanda chenye nyuzi kumi nitakuimbia.
Awapaye wafalme wokovu,
Amwokoa Daudi, mtumishi wake, na upanga wa uovu. (K)
SHANGILIO
Kol. 3:16 – 17
Aleluya, aleluya,
Neno la Kristo likae kwa wingi ndani yenu katika hekima
yote, mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye.
Aleluya.
INJILI
Lk. 20:27-40
Baadhi ya masadukayo, wale wasemao ya kwamba hakuna
ufufuo, walimwendea Yesu, wakamwuliza, wakisema, Mwalimu, Musa alituandikia ya
kuwa, mtu akifiwa na dnugu yake mwenye mke, lakini hana mtoto, na amtwae huyu
mke, ampatie ndugu yake mzao. Basi, kulikuwa na ndugu saba. Wa kwanza alioa
mke, akafa hana mtoto; na wa pili akamtwaa yule mke, akafa hana mtoto; hata wa
tatu akamwoa, na kadhalika wote saba, wakafa, wasiache watoto. Mwisho akafa
yule mke naye. Basi, katika ufufuo atakuwa mke wa yupi? Maana aliolewa na wote
saba.
Yesu akawaambia, Wana wa ulimwengu huu huoa na kuolewa;
lakini, wale wahesabiwao kuwa wamestahili kuupata ulimwengu ule, na kule
kufufuka katika wafu, hawaoi wala hawaolewi; wala hawawezi kufa tena; kwa
sababu huwa sawasawa na malaika, nao ni wana wa Mungu, kwa vile walivyo wana wa
ufufuo. Lakini, ya kuwa wafu hufufuliwa, hata na Musa alionyesha katika sura ya
Kijiti, hapo alipomtaja Bwana kuwa ni Mungu wa Ibrahimu, na Mungu wa Isaka, na
Mungu wa Yakobo. Naye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai; kwa kuwa wote huishi
kwake. Waandishi wengine wakajibu wakamwambia, Mwalimu, umesema vema; wala
hawakuthubutu kumwuliza neno baada ya hayo.
Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.
Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA
MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright ©
1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of
Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha
ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.
No comments:
Post a Comment