Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MASOMO YA MISA, OKTOBA 29, 2022


MASOMO YA MISA, OKTOBA 29, 2022
JUMAMOSI, JUMA LA 30 LA MWAKA WA KANISA

SOMO 1
Flp. 1:18 – 26

Kristo anahubiriwa; na kwa hiyo nafurahi, naam, nami nitafurahi. Maana najua ya kuwa haya yatanigeukia kuwa wokovu wangu, kwa sababu ya kuomba kwenu, na kuruzukiwa Roho wa Yesu Kristo; kama vile nilivyotazamia sana, na kutumaini, kwamba sitaaibika kamwe, bali kwa uthabiti wote, kama siku zote, na sasa vivyo hivyo Kristo ataadhimishwa katika mwili wangu; ikiwa kwa maisha yangu, au ikiwa kwa mauti yangu.

Kwa maana kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida. Ila ikiwa kuishi katika mwili, kwangu mimi ni matunda ya kazi; basi nitakalolichagua silitambui. Ninasongwa katikati ya mambo mawili; ninatamani kwenda zangu nikae na Kristo; maana ni vizuri zaidi sana; bali kudumu katika mwili kwahitajiwa zaidi kwa ajili yenu. Nami nikitumaini hayo, najua ya kuwa nitakaa na kudumu pamoja nanyi, ili mpate kuendelea na kufurahi katika Imani; hata mzidi kuona fahari katika Kirso Yesu juu yangu kwa sababu ya kuwapo kwangu pamoja nanyi tena.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 42:1 – 2, 4 (K) 2

(K) Nafsi yangu inamwonea kiu Mungu.

Kama ayala aioneavyo shauku mito ya maji.
Vivyo hivyo nafsi yangu inakuonea shauku, Ee Mungu. (K)

Nafsi yangu inamwonea kiu Mungu, Mungu aliye hai,
Lini nitakapokuja nionekane mbele za Mungu? (K)

Jinsi nilivyokuwa nikienda na mkutano,
Na kuwaongoza nyumbani kwa Mungu,
Kwa sauti ya furaha na kusifu. (K)


SHANGILIO
Zab. 19:8

Aleluya, aleluya,
Amri ya Bwana ni safi, huyatia macho nuru.
Aleluya.


INJILI
Lk. 14:1, 7-11

Yesu alipoingia ndani ya nyumba ya mtu mmoja miongoni mwa wakuu wa Mafarisayo siku ya sabato, ale chakula, walikuwa wakimvizia.

Akawaambia mfano wale walioalikwa, alipoona jinsi walivyochagua viti vya mbele; akisema, Ukialikwa na mtu arusini, usiketi katika kiti cha mbele; isiwe kwamba amealikwa mtu mwenye kustahiwa kuliko wewe, akaja yule aliyewaalika wewe na yeye, na kukuambia, Mpishe huyu! Ndipo utakapoanza kwa haya kushika mahali pa nyuma, ili ajapo yule aliyekualika akuambie, Rafiki yangu, njoo huku mbele Zaidi; ndipo utakapokuwa na utukufu mbele ya wote walioketi pamoja nawe. Kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright © 1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.         

No comments:

Post a Comment