Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MASOMO YA MISA, OKTOBA 2, 2024

 

_____________

MASOMO YA MISA OKTOBA 2, 2024
JUMATANO, JUMA LA 26 LA MWAKA

Kumbukumbu ya Watakatifu Malaika Walinzi wetu
_____________

SOMO 1
Kut. 23:20-23


Bwana asema hivi: Tazama, mimi namtuma malaika aende mbele yako, ili akulinde njiani na kukupeleka mpaka mahali pale nilipokutengezea. Jitunzeni mbele yake, mwisikize sauti yake; wala msimtie kasirani; maana, hatawasamehe makosa yenu; kwa kuwa jina langu limo ndani yake. Lakini ukiisikiza sauti yake kweli, na kuyatenda yote ninenayo mimi; ndipo mimi nitakuwa ni adui wa adui zako, na mtesi wa hao wakutesao. Kwa kuwa malaika wangu atatangulia mbele yako, na kukufikisha kwenye Mwamori, na Mhiti, na Mperizi, na Mkanaani, na Mhivi, na Myebusi; nami nitawakatilia mbali.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.
_____________

WIMBO WA KATIKATI
Zab. 91:1-6.10-11  (K) 11

(K) Amekuagizia malaika zake wakulinde katika njia zako zote.

Aketiye mahali pa siri pake aliye juu,
Atakaa katika uvuli wake Mwenyezi.
Nitasema, Bwana ndiye kimbilio langu na ngome yangu,
Mungu wangu nitakayemtumaini. (K)

Maana Yeye atakuokoa na mtego wa mwindaji,
Na katika tauni iharibuyo.
Kwa manyoya yake atakufunika, 
Chini ya mbawa zake utapata kimbilio. (K)

Hutaogopa hofu ya usiku,
Wala mshale urukao mchana,
Wala tauni ipitayo gizani.
Wala uele uharibuo adhuhuri, (K)

Mabaya hayatakupata wewe,
Wala tauni haitaikaribia hema yako.
Kwa kuwa atakuagizia malaika zake
Wakulinde katika njia zako zote. (K)
_____________

SHANGILIO
Yn 14:5

Aleluya, aleluya, 
Mhimidini Bwana, enyi majeshi yake yote, ninyi watumishi wake mfanyao mapenzi yake.
Aleluya.
_____________

INJILI
Mt. 18:1-5.10

Wanafunzi walimwendea Yesu wakisema, Ni nani basi aliye mkuu katika ufalme wa mbinguni? Akaita mtoto mmoja, akamweka katikati yao, akasema, Amin, nawaambia, Msipoongoka na kuwa kama vitoto, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni. Basi, yeyote ajinyenyekeshaye mwenyewe kama mtoto huyu, huyo ndiye aliye mkuu katika ufalme wa mbinguni.

Na yeyote atakayempokea mtoto mmoja mfano wa huyu kwa jina langu, anipokea mimi.

Angalieni msidharau mmojawapo wadogo hawa; kwa maana nawaambia ya kwamba malaika zao mbinguni sikuzote huutazama uso wa Baba yangu aliye mbinguni.


Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.
_____________

Copyright © 2024, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

No comments:

Post a Comment