“ASALI ITOKAYO
MWAMBANI”
Alhamisi, Januari 6, 2022,
Juma kabla ya Epifania
1Yoh. 4:19-5:4
Zab. 72:1-2, 14-15 (K)
11
Lk. 4:14-22
KUWA WATU WASIO NA
HILA!
Ndugu zangu wapendwa,
karibuni kwa adhimisho la misa takatifu asubuhi ya leo. Neno la Bwana katika
somo la kwanza Mt. Yohane anazidi kusisitiza juu ya upendo kwamba huo ndio
utambulisho, amri kuu aliyopewa Mkristo. Hivyo ahakikishe kwamba anaitii na
kuitimiza. Mt. Yohane anaendelea kusema kwamba hakuna awezaye kusema kwamba
anampenda Mungu halafu na hapohapo anamchukia ndugu yake. Hii ndivyo kanuni
ilivyo kwa sababu huu ni unafiki, kujipendekeza kwa Mungu lakini huwapendi
watoto wake, kwani Mungu huonekana kupitia watoto wake tunaokutana nao kila
siku.
Somo hili linatuchoma
wengi wetu. Kwa sababu hatuna upendo wa dhati, hata tutoapo misaada tunakuwa na
malengo yetu binafsi, tunatoa pale tunapojua kwamba tutapokea baadaye. Hatupo
tayari kutoa pale tusipopokea. Pia tunatabia ya kutoa kujitafutia jina na
umaarufu. Mara nyingi hatutoi misaada sehemu ambayo hatuonekani, au kutambuliwa.
Tutatoa pale tunapoonekana tu. Na pia tunatabia ya kutangaza tulichotoa.
Tuachane na tabia za namna hii ndugu yangu.
Siku ya leo
tujichunguze na kuona ni yupi tunayekosana naye, tusimchukie yeyote. Wote ni
watoto wa Mungu. Tutambue kwamba wanadamu sio malaika, tusitegemee wawe kamili
katika kila hali. Basi, tuwapokee katika udhaifu wao. tusimchukie yeyote.
Yesu katika somo la
injili anajitokeza katika nguvu ya Roho Mtakatifu na kuanza kuhubiri habari
njema. Anapata kuwatangazia watu wa kijijini kwake kwamba Roho wa Bwana yu juu
yake na kwa njia ya Roho huyu anaweza kutangaza uhuru kwa wafungwa na watumwa
wengi. Sisi tuombe kuwa na Roho huyu. Roho atatupatia mawazo mapya ya kufanya
shuhguli zetu. Atatupatia maneno yenye hekima ya kuwashauri wenzetu. Pia
atafanya vichwa vyetu na mioyo yetu vifikirie mawazo yenye tija kuliko mawazo
ya kushindwa shindwa kila wakati. Hakika atatupatia ukombozi toka katika
udhaifu wetu. hivyo, tumwombe Mungu siku ya leo atupe Roho huyu.
Copyright
©2013-20202 ©FurKat, FurahayaKikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.
No comments:
Post a Comment