ASALI
ITOKAYO MWAMBANI”
Tafakari
ya Pasaka
Ijumaa,
Aprili 23, 2021
Juma
la 3 la Pasaka
Mdo
9:1-20;
Zab
117:1-2 (K. Mk 16:15);
Yn
6:52-59.
MAISHA
YETU YANATOKA KWA KRISTO!
Karibuni
ndugu zangu kwa adhimisho la Misa Takatifu asubuhi ya leo. Bado tunaendelea
kufurahia furaha tulizoletewa na sikukuu ya Pasaka kwa ufufuko wa Kristo Bwana
wetu.
Na
leo neno la Bwana katika injili yetu ya leo linaendelea kutufundisha juu ya
Yesu kama mkate ulioshuka kutoka mbinguni ambao kila mmoja wetu anapaswa kwenda
kwake kuula ili uweze kumpatia uzima, uweze kumsaidia apate kusafiri moja kwa
moja hadi kwenye ile nchi ya ahadi, yaani mbinguni. Yeyote atakayeukosa mkate
huu-hakika hatakaa aweze kufikia ile nchi ya ahadi.
Ndugu
zangu, ukweli ni kwamba Yesu aliamua kujishusha na kukubali kukaa katika mkate
wa Ekaristi. Hii ni namna ya kiunyenyekevu sana na ni namna aliyoamua mwenyewe
na lengo ni kutufikia sisi. Na huu ni ukweli: jinsi Ekaristi ilivyo, ipo kwa
namna ambayo inaweza kumfikia kila mtu, mkate unaotumika unampatia kila mmoja
nafasi ya kuushiriki bila ya ubaguzi au mtu yeyote kukosa.
Lakini
tukumbuke kwamba kitendo hiki cha Yesu kujishusha hivi na kukubali kukaa katika
mkate wa kawaida kama hostia tayari kimeshawafanya wengi wamdharau Yesu. Wengi
wetu tunakosa imani kwa Ekaristi-wengi wetu tunajiuliza je, kweli huu mkate ni
Yesu kweli? Unaweza kutupatia uzima wa milele? na huu uzima unatoka wapi? Sasa,
kitendo cha Yesu kuwa katika hali ya kiunyenyekevu namna hii kinamfanya
aonekane kana kwamba hana nguvu. Lakini ukweli ni kwamba unyenyekevu wa Yesu
usitufanye tusimheshimu.
Ekaristi
Takatifu ni Yesu kweli na ndugu yangu nakuomba sisi tuendelee kutoa heshima kwa
Ekaristi, tuendelee tu, hii ndio itakayotuokoa.Tuisiidhau hata kidogo.
Kishawishi cha kuidharau ni kikubwa kwani bila imani huwezi kuiona nguvu ya
Ekaristi lakini kwa walioiamini, kweli Ekaristi hutenda makubwa. Hivyo, jamani
tuiheshimu Ekaristi na kuiabudu.
Katika
somo la kwanza tumesikia jinsi nguvu ya Kristo mfufuka inavyotenda kazi. Leo
imeweza kumgeuza yule mtesaji wa kanisa na kuwa mfuasi hodari wa Yesu. Kwa
kweli jambo hili halikuwa rahisi lakini Yesu ndiye aliyependa na kwa nguvu za
Yesu, haya yamefanyika-kumgeuza mtesaji wa kanisa kuwa mfuasi wa kanisa. Paulo
anageuzwa kwa nguvu za Yesu, huyu huyu ambaye tunampokea katika Ekaristi. Sisi
tunaopokea Ekaristi, kabla ya kuipokea tumwambie Yesu ee Yesu naomba unigeuze,
nibadili mwenendo wangu. Tuache kuwa angamiza watu wema wasio na hatia labda
kwa kuwasingizia uongo, kuwaonea wivu na kuwachafua, au pengine kuacha kuuwa
kwa utoaji wa mimba. Yesu atugeuze kabisa tusiwe na hatia juu ya maisha ya mtu
mwingine. Yesu aweza. Hili liwe ombi letu leo. Tumsifu Yesu Kristo.
Copyright © 2020, "MASOMO YA MISA" published
by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya
Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.
No comments:
Post a Comment