Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

Tubuni na kuamini Injili.

 

“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Tafakari ya Kwaresima

Jumamosi, Febuari 21, 2021

Jumapili baada ya Jumatano ya majivu

 

Mwa. 9:8– 15

1Pet: 3:18-22

Mk: 1: 12-15

 Tubuni na kuamini Injili.

Leo ni Dominika ya Kwanza ya Kwaresima. Jumatano iliyopita wote tulikusanyika katika liturujia ya Majivu na tukapakwa Majivu kama ishara ya toba tulipokianza Kipindi hiki cha Kwaresima. Leo tunapaswa kutafakari zaidi juu ya toba yetu ya kweli dhidi ya vishawishi vinavyotuzunguka katika ulimwengu huu. Liturujia ya leo inatuonesha jinsi Yesu alivyopambana na vishawishi na alivyovishinda kwa niaba yetu. Kumbe, kitupasacho sisi kwa sasa, ni kumsikiliza Yesu katika Neno lake na hivi tushiriki ushindi wake.

Injili ya leo, inaanza kwa kutuletea picha ya mchezo wa kuigiza. Pazia linapofunguliwa, tutamwona Yesu yuko upande mmoja na Ibilisi upande wa pili. Mara Ibilisi anamchukua Yesu na kumpeleka jangwani ili amjaribu huko. Lakini ikumbukwe kuwa Yesu alikuwa amejazwa Roho Mtakatifu toka wakati wa Ubatizo wake kule Yordani. Hivi alingia katika mapambano na Ibilisi akiwa amejazwa Roho Mtakatifu. Mapambano yanayofanyika jangwani, yalimhusisha Yesu kukaa huko siku arobaini akisali, kufunga na kujaribiwa. Baada ya siku hizo arobaini, Yesu anarudi Galilaya, siyo kama mtu aliyechoka au kushindwa, bali kama mtu aliyejazwa Roho Mtakatifu, na yuko tayari kuanza kazi ya ukombozi wa mwanadamu.

Leo sisi tunaalikwa kuingia katika mapambano dhidi ya Ibilisi. Mungu anatutaka sisi tukiwa pamoja na Kristo, kwa nguvu ya Roho Mtakatifu, kupambana na vishawishi ambavyo vimo ndani yetu katika mazingira yetu, hatimaye tuvishinde vishawishi hivyo. Ni suala la kila mkristo kujitoa mhanga katika kumfuata Roho wa Kristo anayetuongoza jangwani.

Wito huo wa Mungu unatufikia sisi kwa maneno yaleyale aliyosema Yesu alipoanza kazi baada ya kurudi toka jangwani. Anasema: ‘Wakati umetimia na utawala wa Mungu umekaribia. Tubuni na kuamini Injili.

Saa ya neema

“Wakati umetimia na utawala wa Mungu umekaribia”. Kila kitu kina wakati wake. Kitabu cha Yoshua bin Sira kinatuambia: Kuna wakati wa kuzaliwa na wakati wa kufa...Wakati wa kulia na wakati wa kucheka..”. Na tunaweza kuongeza: ‘Wakati wa kutubu’. Kuna wakati ambapo neema ya Mungu inamwingia mtu bila kutegemea. Vivyo hivyo, uko wakati ambao Neno la Mungu linapenya moyoni mwa mtu na kumgusa, na hivyo kumfanya abadilike. Hata katika historia ya Kanisa, tunapata mifano ya watu ambao leo hii ni watakatifu wa na Neno la Mungu kwa wakati fulani na hivyo wakabadilika.

Mtakatifu Augustino wa Hippo, Margareta wa Kortona na wengine ni miongoni mwa watu hao. Kumbe, kwetu sisi nasi, kipindi hiki ni kipindi cha neema, ni saa ya neema, ni wakati wa kuguswa na Neno Ia Mungu na kubadilika.

Kutubu na kuamini

Kuna njia nyingi sana, na namna nyingi za kumwasi Mungu na kwenda kinyume na matakwa ya Mungu. Lakini kumrudia Mungu iko njia moja tu. nayo ni ya kutubu na kuamini juu ya uwezo wake wa kusamehe na kuponya dhambi. Unaweza ukajiona kuwa huna dhambi na wala hujatenda dhambi kama yule jirani yako au rafiki yako, lakini kumbuka kuwa unayo mapungufu yako na kasoro zako. Unayo mawazo na maneno potofu. Hayo yote ni dharnbi mbele ya Mungu. Kipindi hiki ni kipindi cha kutubu na kuamini juu ya uwezo wa Mungu wa kukusamehe hayo yote na kukuponya madhambi yako.

Ndugu zangu, kwaresima hii iwe nafasi nzuri ya kubadili mioyo yetu, fikra zetu, matendo yetu tupate kumwelekea tuliyemwacha kutokana na maelekeo yetu mabaya. Pia iwe nafasi nzuri ya kujipima jinsi gani tunamtegemea Mungu katika majaribu mbalimbali ya kiroho na yale ya kimwili.

Tumwombe Mungu basi, ili kwa njia ya Mwanae mteswa Yesu Kristo waitume zawadi yao kwetu, yaani Roho Mt atupe nguvu na uwezo wa kuwa watu wa toba.

 

------------------------

Copyright ©2013-2020 ©FurKat, FurahayaKikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

 

 

 

 

No comments:

Post a Comment