Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

Kutokana na mahangaiko

“ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Tafakari ya kila siku

Jumapili, Februari 7, 2021,

Juma la 5 la Mwaka wa Kanisa

 

 

Yob 7: 1-4,6-7

Zab 146: 1-6;

1 Cor: 9: 16-19,22-23

Mk 1: 29-39

 

Kutokana na mahangaiko

 

Mara nyingi katika maisha ya kila siku, huwa tunashuhudia watu wengi wakipatwa na shida mbalimbali. Kwa mfano; magonjwa, vita, njaa n.k. Matatizo hayo huwa yanawakumba watu wote; wadogo kwa wakubwa, matajiri kwa fukara, wacha Mungu na wasiomcha Mungu. Kutokana na mahangaiko, shida, mateso na taabu hizo, watu wengi huwa wanajiuliza:“Hivi kwa nini dunia imejawa na mateso, mahangaiko na shida mbali mbali?’’

Cha kushangaza zaidi ni pale watu waonapo hata wacha Mungu, kwa mfano: Viongozi wa dini na wafuasi wengine wa dini ambao kwa namna moja au nyingine hujitahidi sana kushika maongozi ya Mungu, nao hupatwa na mateso zaidi ya wale ambao jamii inawaona kuwa ni watenda dhambi zaidi. Kama vile wezi, majambazi, malaya n.k.

Jibu la maswali kama haya, ni kwamba mateso, shida na mahangaiko kweli yapo. Haya yote ni sehemu ya maisha ya mwanadamu. Jambo la msingi ni namna ya kuyapokea na kuyakabili hayo mateso na taabu zote. Masomo yetu ya leo, yanatupa mwongozo mzuri na bora wa namna ya kuyapokea na kukabiliana na mateso na taabu za hapa duniani.

Katika somo la Kwanza, tunamkuta Ayubu, mtu ambaye alikuwa mcha Mungu sana akiwa katika mateso makali ya magonjwa na pia mateso ya kufiwa na wanawe wote pamoja na upotevu wa mali yake yote. Matatizo haya yana mfanya Ayubu awe mtu wa mateso na maumivu makali sana, ingawa hapo mwanzo alikuwa mtu mwenye furaha tele. Ayubu anafananisha mateso yake na mateso ya watumwa ambao hufanyishwa kazi nzito kila siku toka asubuhi hadi usiku. Kwake yeye, anaona mateso yake ni magumu mno, kwani mateso yake hayana muda wa mapumziko.

Pamoja na mateso na mahangaiko hayo yote, Ayubu anabaki katika msimamo wake wa kuwa na imani kwa Mungu. Baadhi ya rafiki na jamaa zake walimshauri amwasi Mungu (amtukane tu Mungu) ili aweze kuachana na mateso na magumu hayo. Lakini kwa ushujaa wote Ayubu alikataa kufanya hivyo na akaendelea na msimamo wake wa kubaki katika imani kwa Mungu. Hatimaye Mungu hakumwacha mtupu.

Katika somo la Injili, tunamkuta Bwana wetu Yesu Kristo akijionesha bayana kuwa yeye ana nguvu au uwezo wa kuponya au kuondoa mateso na shida ambazo mwanadamu anakabiliwa nazo.Yeye anamponya mama mkwe wa Petro, ambaye alikuwa ameshikwa na homa kali, kwa kumshika mkono na kumwinua.

Kadiri ya desturi za Kiyahudi, ugonjwa wa namna hii ulitibiwa kwa kufunga nywele, toka katika kichwa cha mgonjwa, na kisu cha chuma kwa pamoja, na kisha kifurushi hicho kiliwekwa kichakani. Baadaye, mtaalamu/mganga alifanya matambillo fulani ambayo yaliambatana na maneno ya pekee kwa ajili ya kumtibu mgonjwa huyo. Baadhi ya wagonjwa, walibahatika kupona, lakini wengine ilishindikana. Kumbe, Yesu anamponya mama Mkwe wa Petro, kwa namna isiyo ya kawaida kabisa kwa Wayahudi. Kutokana natukio hilo, watu wengi walimwamini Yesu na hivi walianza kutangaza habari zake katika kijiji chao cha Kapernaumu.

Ilipokuwa jioni, watu wengi, toka katika kila kona ya kijiji, walifika kwa Yesu wakimletea wagonjwa wao ili awaponye. Yesu alifanya kazi hiyo kubwa kwa muda mrefu. Na ilipofika asubuhi alijitenga kidogo ili kusali. Watu wakawa wana mtafuta, kwani walifahamu fika kwamba Yesu ana nguvu za kimungu na hivi ana uwezo wa kuponya maradhi, shida na mateso yanayowakabili. Lakini Bwana wetu Yesu Kristo aliwaambia wanafunzi wake waondoke na kwenda mahali pengine ili kuhubiri habari za ufalme wa Mungu huko.

Mateso, NDW, ni sehemu ya maisha ya mwanadamu. Ni vigumu kwa mwanadamu kuondokana na matatizo au shida ambazo humpelekea katika kupata mateso au maumivu makali. Matatizo katika maisha ya mwanadamu ni jambo la kawaida. Jambo la msingi kwetu sisi, ambao ni wafuasi wa Kristo ni kuyapokea na kuyakabili katika jicho la imani kwa Mungu na Yesu Kristo ambaye ni Mkombozi wetu. Katika matatizo na shida zetu mbali mbali hatupaswi kukimbilia kwa waganga wa kienyeji ili kuagua au kupata tiba zisizo za kweli. Bali yatupasa kumkimbilia Bwana wetu Yesu Kristo.

 

------------------------

Copyright ©2013-2020 ©FurKat, FurahayaKikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

 

 

No comments:

Post a Comment