Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MOYO WA UKARIMU!

 “ASALI ITOKAYO MWAMBANI”

Tafakari ya Kila siku

Jumatatu, Novemba 23, 2020.

Juma la 34 la Mwaka

 

Uf 14: 1-5;

Zab 24: 1-6

Lk 21: 1-4.

 

MOYO WA UKARIMU!

 

Leo Yesu anaona wema na ukarimu wa mama mjane, hakuhitaji kujitangaza au kutangaza alichokuwa anafanya, na huenda pia alikuwa na aibu juu ya wale matajiri, ambao walitoa kwa wingi wa vitu, na kuwafanya watu wengine watamani uhuru wao. Lakini Mama huyu katika moyo wake usiojaa majivuno, alitoa kile alichokuwa nacho kama sadaka yake, na anasatahili sifa alizotoa Kristo. Alitoa kila kitu alichokuwa nacho kwani alikuwa na Mungu ndani ya moyo wake. Ni vizuri sana kuwa na Mungu ndani ya mioyo yetu kuliko kuwa na dhahabu katika makabati yetu.

 

Tazama baadhi ya watakatifu wengi walioishi bila kujionesha. Mfano Mt. Thérèsa wa Lisieux, alijotoa kwa Kristo katika hali ya vitu vidogo. Aliishi ndani ya nyumba yao ya kitawa kwa muda bila hata ya kuhangaika na malimwengu. Kwahiyo katika mtazamo wa ulimwengu anaonekana amechangia kidogo sana katika ulimwengu. Lakini leo hii ni Mwalimu wa Kanisa tunashukuru kwa zawadi ya maisha yake ya kiroho na ushuhuda wa maisha yake.

 

Yanaweza yakasemwa haya kwako pia. Pengine unajihangaisha na kitu ambacho ulimwengu unaona hakina thamani. Pengine, kupika, kuosha vyombo na kuhudumia familia na shughuli za kila siku. Swali la kujiuliza ni Mungu ananiona je?, sio ulimwengu unanionaje.

Tafakari leo juu ya maisha yako. Pengine hujaitwa ili uende ukafanyea mambo makubwa katika hali ya kuonekana na watu au katika hali ya Ulimwengu. Au pengine haukufanya kitu kikubwa kinacho onekana katika kanisa. Lakini anacho ona Mungu ni ule upendo wako unaonekana katika mambo hayo madogo unayotenda kutimiza majukumu yako ya kila siku, kuwapenda familia yako, kusali kila siku nk, ni baadhi ya sadaka unayompa Mungu kila siku. Anaona hili na muhimu kabisa, anaona upendo na majitoleo ambayo unayofanya. Fanya mambo hayo madogo kwa upendo mkubwa na utakuwa ukimpa Mungu mengi kabisa katika kutimiza mapenzi yake.

 

Sala: Bwana, ninajitoa mimi mwenyewe kwako na kwa huduma yako kila siku. Ninaomba nifanye yanayo nipasa kutenda kwa upendo mkubwa. Ninaomba uendelee kunionesha mimi majukumu yangu na ninaomba unisaidie mimi niweze kujikita katika majukumu hayo kadiri ya mapenzi yako matakatifu. Bwana Yesu nakuamini wewe. Amina

 

Copyright ©2013-2020 ©FurKat, FurahayaKikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.

No comments:

Post a Comment