Everyday Saint / Maisha ya Watakatifu

MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 8, 2024


MASOMO YA MISA, SEPTEMBA 8, 2024
DOMINIKA YA 23 YA MWAKA B WA KANISA


MWANZO:
Zab. 119:137, 124

Ee Bwana, wewe ndiwe mwenye haki, na hukumu zako ni za adili. Kama zilivyo rehema zako umtendee mtumishi wako.


SOMO 1
Isa. 35:4-7

Waambieni walio na moyo wa hofu, Jipeni moyo, msiogope; tazama, Mungu wenu atakuja na kisasi, na malipo ya Mungu; atakuja na kuwaokoa ninyi. Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema atarukaruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba; maana katika nyika maji yatabubujika; na vijito jangwani. Na mchanga ung’aao mfano wa maji utakuwa ziwa la maji, na nchi yenye kiu itakuwa chemchemi za maji.

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


WIMBO WA KATIKATI
Zab. 146:7-10 (K) 1

(K) Ee nafsi yangu, umsifu Bwana.

Bwana ndiye ashikaye kweli milele,
Huwafanyia hukumu walioonewa.
Huwapa wenye njaa chakula;
Bwana hufungua waliofungwa. (K)

Bwana huwafumbua macho waliopofuka,
Huwainua walioinama.
Bwana huwapenda wenye haki,
Huwahifadhi wageni. (K)

Bwana huwategemeza yatima na mjane,
Bali njia ya wasio haki huipotosha.
Bwana atamiliki milele,
Mungu wako, Ee Sayuni, kizazi hata kizazi. (K)


SOMO 2
Yak. 2:1-5

Ndugu zangu, imani ya Bwana wetu Yesu Kristo, Bwana wa utukufu, msiwe nayo kwa kupendelea watu. Maana akiingia katika sinagogi lenu mtu mwenye pete ya dhahabu na mavzi mazuri; kisha akiingia na maskini, mwenye mavzi mabovu; nanyi mkimstahi yule aliyevaa mavzi mazuri, na kumwambia, Keti wewe hapa mahali pazuri; na kumwambia yule maskini, Simama wewe pale, au keti miguuni pangu, je! Hamkufanya hitilafu mioyoni mwenu, mkawa waamuzi wenye mawazo mabovu? Ndugu zangu wapenzi, sikilizeni, Je! Mungu hakuwachagua maskini wa dunia wawe matajiri wa imani na warithi wa ufalme aliowaahidia wampendao?

Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.


SHANGILIO
Yn. 8:12

Aleluya, aleluya.
Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, asema Bwana; Yeye anifuataye atakuwa na nuru ya uzima.
Aleluya.


INJILI
Mk. 7:31-37

Yesu alitoka katika mipaka ya Tiro, akapita katikati ya Sidoni, akaenda mpaka bahari ya Galilaya, kati ya mipaka ya Deakapoli. Wakamletea kiziwi, naye ni mwenye utasi, wakamsihi amwekee mikono. Akamtenga na mkutano faraghani, akatia vidole vyake masikioni mwake, akatema mate, akamgusa ulimi, akamtazama juu mbinguni, akaugua, akamwambia, Efatha, maana yake, Funguka. Mara masikio yake yakafunguka, kifungo cha ulimi wake kikalegea, akasema vizuri. Akawaonya wasimwambie mtu; lakini kadiri ya alivyozidi kuwaagiza, ndivyo walivyozidi kutangaza habari; wakashangaa mno kupita kiasi, wakinena, Ametenda mambo yote vema; viziwi awafanya wasikie, na bubu waseme.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.


Copyright © 2024, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

No comments:

Post a Comment