MASOMO YA MISA, AGOSTI 10, 2026
JUMATATU , JUMA LA 19 LA MWAKA
SIKUKUU YA MT. LAURENT
SOMO 1
2Kor 9:6-10
Apandaye haba atavuna haba; apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu. Kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu. Na Mungu aweza kuwajaza kila neema kwa wingi, ili ninyi, mkiwa na riziki za kila namna sikuzote, mpate kuzidi sana katika kila tendo jema; kama ilivyoandikwa, Ametapanya, amewapa maskini, Haki yake yakaa milele.
Na yeye ampaye mbegu mwenye kupanda, na mkate uwe chakula, atawapa mbegu za kupanda na kuzizidisha, naye atavaongeza mazao ya haki yenu.
Neno la Mungu...Tumshukuru Mungu
WIMBO WA KATIKATI
Zab. 112: 1-2, 4, 9 (K) 5
(K) Heri atendaye fadhali na kukopesha.
Heri mtu yule amchaye Bwana,
Apendezwaye sana na maagizo yake.
Wazao wake watakuwa hodari duniani;
Kizazi cha wenye adili kitabarikiwa. (K)
Nuru huwazukia wenye adili gizani;
Ana fadhili na huruma na haki. (K)
Amekirimu, na kuwapa maskini,
Haki yake yakaa milele,
Pembe yake itatukuzwa kwa utukufu. (K)
SHANGILIO
Yn 8: 12
Aleluya, aleluya,
Yeye anifuataye, asema Bwana, hatakwenda gizani kamwe, bali atakuwa na nuru ya uzima.
Aleluya.
INJILI
Yn 12: 24-26
Yesu aliwaambia wanafunzi wake: Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi. Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele. Mtu akinitumikia, na anifuate; nami nilipo, ndipo na mtumishi wangu atakapokuwapo. Tena mtu akinitumikia, Baba atamheshimu.
Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo
Copyright © 2026, "MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com

No comments:
Post a Comment