MASOMO YA MISA OKTOBA
30, 2025
ALHAMISI, JUMA LA 30 LA
MWAKA
_____________
SOMO 1
Rum. 8:31-39
Mungu akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu? Yeye asiyemwachilia Mwana wake mwenyewe, bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, atakosaje kutukirimia na mambo yote pamoja naye? Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na Zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.
Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! Ni dhiki, au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga? Kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Kwa ajili yako tunauawa mchana kutwa, tumehesabiwa kuwa kama kondoo wa kuchinjwa. Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na Zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda.
Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.
Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.
WIMBO WA KATIKATI
Zab. 109:21-22, 26-27
(K) Ee Bwana, uniokoe sawasawa na fadhili zako.
Na wewe, Mungu, Bwana,
Unitendee kwa ajili ya jina lako,
Kwa kuwa fadhili zako ni njema uniokoe.
Kwa maana mimi ni mnyonge na mhitaji,
Na moyo wangu umejeruhi ndani yangu. (K)
Ee Bwana, Mungu wangu, unisaidie,
Uniokoe sawasawa na fadhili zako.
Nao wakajue ya kuwa ndio mkono wako;
Wewe, Bwana, umeyafanya hayo. (K)
Nitamshukuru Bwana kwa kinywa changu,
Naam, nitamsifu katikati ya mkutano.
Maana atasimama mkono wa kuume wa mhitaji,
Amwokoe na wanaoihukumu nafsi yake. (K)
SHANGILIO
Zab. 25:4,5
Aleluya, aleluya,
Ee Bwana, unijulishe njia zako, unifundishe mapito yako.
Aleluya.
INJILI
Lk. 13:31-35
Siku moja, Mafarisayo kadha wa kadha walimwendea Yesu, wakamwambia, Toka hapa, uende mahali pengine, kwa sababu Herode anataka kukuua. Akawaambia, Nendeni, mkamwambie yule mbweha, Tazama, leo na kesho natoa pepo na kuponya wagonjwa, siku ya tatu nakamilika. Pamoja na hayo imenipasa kushika njia yangu leo na kesho na kesho kutwa; kwa kuwa haimkini nabii aangamie nje ya Yerusalemu.
Ee Yerusalemu, Yerusalemu, uwauaye manabii na kuwapiga kwa mawe waliotumwa kwako, mara ngapi nimetaka kuwakusanya watoto wako kama vile kuku avikusanyavyo vifaranga vyake chini yambawa zake.
Neno la Bwana...Sifa kwako, ee Kristo
_____________
Copyright © 2025,
"MASOMO YA MISA" published by T.M.P. Book Department, Tabora –
Tanzania. Readings reproduced by Furaha ya Kikatoliki: see
www.fur-kat.blogspot.com.

No comments:
Post a Comment