MASOMO YA MISA, MACHI 11, 2025
JUMANNE, JUMA LA 1 LA KWARESIMA
SOMO 1
Isa. 55:10-11
Bwana asema: Kama vile mvua ishukavyo, na
theluji, kutoka mbinguni, wala hairudi huko: bali huinywesha ardhi, na
kuizalisha na kuichipuza ikampa mtu apandaye mbegu, na mtu alaye chakula;
ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia
bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale
niliyolituma.
Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.
WIMBO WA KATIKATI
Zab. 34:3-6, 15-18 (K)17
(K) Wenye haki, Bwana anawaponya na taabu zao
zote.
Mtukuzeni Bwana pamoja nami,
Na tuliadhimishe jina lake pamoja.
Nalimtafuta Bwana akanijibu,
Akaniponya na hofu zangu zote. (K)
Wakamwelekea macho wakatiwa nuru,
Wala nyuso zao hazitaona haya.
Maskini huyu aliita, Bwana akasikia,
Akamwokoa na taabu zake zote. (K)
Macho ya Bwana huwaelekea wenye haki,
Na masikio yaje hukielekea kilio chao.
Uso wa Bwana ni juu ya watenda mabaya,
Aliondoa kumbukumbu lao duniani. (K)
Walilia, naye Bwana akasikia,
Akawaponya na taabu zao zote.
Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo,
Na waliopondeka roho huwaokoa. (K)
SHANGILIO
Zab. 95:8
Leo msifanye migumu mioyo yenu,
lakini msikie
sauti yake Bwana.
INJILI
Mt. 6:7-15
Siku ile Yesu aliwaambia wafuasi wake: Mkiwa
katika kusali, msipayuke-payuke, kama watu wa mataifa; maana wao hudhani ya
kuwa watasikiwa kwa sababu maneno yao kuwa mengi. Basi msifanane na hao; maana
Baba yenu anajua mnayohitaji kabla ninyi hamjamwomba. Basi ninyi salini hivi:
Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe,
Ufalme wako uje, Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni. Utupe
leo riziki yetu. Utusamehe deni zetu, kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu.
Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu.
Kwa maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba
yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi. Bali msipowasamehe watu makosa yao, wala
Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu.
Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.
Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA
MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright ©
1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of
Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha
ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.
No comments:
Post a Comment