MASOMO YA MISA NOVEMBA 30, 2022
JUMATANO, JUMA LA 1 LA MAJILIO
SIKUKUU YA MT. ANDREA, MTUME
SOMO 1
Rum. 10:9-18
Ukimkiri Yesu kw akinywa chako ya kuwa ni Bwana, na
kuamini moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka. Kwa maana
kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kwa kinyw ahukiri hata kupata wokovu.
Kwa maana andiko lanena, Kila amwaminiye hatatahayarika. Kwa maana hakuna
tofauti ya Myahudi na Myunani; maana yeye yule ni Bwana wa wote, mwenye utajiri
kwa wote wamwitao; kwa kuwa, Kila atakayeliitia Jina la Bwana ataokoka.
Basi wamwiteje yeye wasiyemwamini? Tena wamwaminije yeye
wasiyemsikia? Tena wamsikieje pasipo mhubiri? Tena wasipopelekwa? Kama
ilivyoandikwa, Ni mizuri kama nini miguu yao wahubirio habari ya mema! Lakini
si wote walioitii ile habari njema. Kwa maana Isaya asema, Bwana, ni nani
aliyeazimia habari zetu? Basi Imani, chanzo chake ni kusikia; na kusikia huja
kwa neno la Kristo. Lakini nasema, Je! Wao hawakusikia? Naam, wamesikia, Sauti
yao imeenea duniani mwote, na maneno yao hata miisho ya ulimwengu.
Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.
WIMBO WA KATIKATI
Zab. 19:1-4 (K)
(K) Sauti yao imeenea duniani mwote.
Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu,
Na anga laitangaza kazi ya mikono yake.
Mchana husemezana na mchana,
Usiku hutolea usiku maarifa. (K)
Hakuna lugha wala maneno,
Sauti yao haisikilikani.
Sauti yao imeenea duniani mwote,
Na maneno yao hata miisho ya ulimwengu. (K)
SHANGILIO
Mt. 4:18
Aleluya, aleluya,
Bwana asema, Nifuateni, nitawafanya kuwa wavuvi wa watu.
Aleluya.
INJILI
Mt. 4:18-22
Yesu alipokuwa akitembea kando ya bahari ya Galilaya,
aliona ndugu wawili, Simoni aitwaye Petro, na Andrea nduguye, wakitupa jarife
baharini; kwa maana walikuwa wavuvi. Akawaambia, Nifuateni, nami nitawafanya
kuwa wavuvi wa watu. Mara wakaziacha nyavu zao, wakamfuata.
Akaendelea mbele, akanona ndugu wengine wawili, Yakobo wa
Zebedayo, na Yohane nduguye, ambao walikuwamo chomboni pamoja na Zebedayo baba
yao, wakizitengeneza nyavu zao; akawaita. Mara wakakiacha chombo na baba yao,
wakamfuata.
Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.
Copyright © 1993 T.M.P. Book Department, Tabora - Tanzania: see MASOMO YA
MISA. Scripture readings from ‘Biblia Takatifu’are published and copyright ©
1975, 1993 by T.M.P. Book Department, Tabora – Tanzania.© Bible Society of
Kenya, © Bible Society of Tanzania.These readings are a reproduction by Furaha
ya Kikatoliki: see www.fur-kat.blogspot.com.
No comments:
Post a Comment